Wakiwa kitandani mama na baba yao kina Sera, mama akaanza njama zake kwa kuanza kumdanganya mumewe. Akaanza kumwambia juu ya mipango mizuri anayofikiria juu ya Tunda mpaka akamshangaza na mumewe. “Mbona umebadilika gafla!?” “Hata nifanye nini Tunda ni damu yangu. Nimeona heri tumsaidie tu. Nitamsomesha, hata kama ni mafunzo ya muda mfupi kisha nimtafutie kazi.” Baba yake Sera akacheka. “Ingekuwa hatujatoka kwa walokole, ningesema umelewa!” Mama Sera akacheka sana.
“Au yale maji mwenzangu uliyokuwa ukinywa ilikuwa konyagi?” Mama yake Sera akaendelea kucheka. “Pale napo kazi ipo! Nyumba imepooza, haina hata wine! Khaa! Balaa gani hili?” “Hawamalizi kuomba! Mimi niliamua kufunga macho kukubali yaishe.” Walizidi kucheka kwa sauti. “Lakini yule mama ni mtanzania kabisaa, imekuaje awe na mtoto mzungu!?” “Huwajui walokole wewe! Wanahangaika hukooo, wakishindwa maisha, ndio wanarudi kwa Mungu wanajidai wameokoka. Wanafiki tu.” Mama Sera na mumewe waliendelea kukashifu na kucheka sana, mpaka walipolala.
Jumapili ambayo Net aliomba kufika jioni ili azungumze na Tunda.
Waliamka siku inayofuata ilikuwa siku ya jumapili. Familia hiyo hawakuwa wakiacha kwenda kanisani. Kwa hiyo Tunda na Nyange walikuwa wakiamka alfajiri kama kawaida yao kuwaandalia kifungua kinywa, na kunyoosha nguo zao ili wawahi misa ya kwanza ya lugha ya kingereza. Tunda alijitahidi kuandaa meza vizuri sana, ili kuepuka ugomvi wa asubuhi asubuhi.
Lakini ghafla hali ya hewa ikatibuka. Shangazi yake alianza kwa kuulizia mkufu wake wa dhahabu aliokuwa amenunuliwa na watoto wake siku ya mother’s day. Ikaanza kazi ya kusakwa huo mkufu. “Kwani uliweka wapi?” Mumewe akahoji huku akiendelea kusaidia kutafuta. “Jana wakati naenda kwenye shuguli ya Net nyumbani kwao, niliuacha hapa mezani! Tena nilitaka kuvaa dhahabu, lakini nikaona nivae tu silver. Yaani nilinyanyua kabisa nikitaka kuuvaa, tena niliweka mpaka shingoni, nikarudisha hapa mezani na kuamua kuvaa silver. Tena moyo ulisita kabisa! Najuta kupuuzia hisia zangu!” Shangazi akalalamika kwa majuto.
“Basi muulize Tunda na mwenzie tuliowaacha hapa ndani.” Ndicho alichokuwa akisubiria. Mumewe alipoweka tu kituo, akatoka na kuwaita wote. Watoto wake wote walisema waliuona huo mkufu mara ya mwisho mezani kwa mama yao. Ndipo baba mwenye nyumba na yeye akapandwa na hasira . “Sasa sikilizeni mabinti. Nautaka huo mkufu wa mke wangu sasa hivi kabla sijawang’oa meno. Sitaki mchezo.” Tunda na Nyange walibaki wametoa macho.
“Mmesikia?” “Mimi sijaingia tena chumbani kwenu baba. Ni vile asubuhi tu wakati nasafisha. Sijarudi huko tena.” Nyangeta akajitetea, lakini Tunda alibaki kimya kama hakuwepo pale kimawazo. “Na wewe Tunda?” Kama aliyeshtuliwa kutoka usingizini. “Abee!” “Mkufu wa shangazi yako uko wapi?” Kabla hajajibu shangazi yake akamnasa kofi kubwa sana la usoni. Tunda alipepesuka akarudi nyuma. “Aaaaahh!” Tunda alisikika akigugumia maumivu huku ameshikilia uso kama unaotaka kuanguka!
“Jizi hili mama! Ndiye atakuwa amekuchukulia mkufu wako. Maana Nyange tumeishi naye miaka yote hapa, mbona kusiibiwe kitu iwe sasa hivi yeye akiwepo?” Samatha akadakia. “Nyange kalete mifuko yake tuangalie ndani.” Shangazi akatoa amri. Nyange alikwenda na kuleta mifuko ya Tunda. Mfuko wa kwanza ulipomiminwa tu, ule mkufu ukaanguka chini mbele ya macho yao wote. “Haaa!” Kila mtu akashtuka mpaka Tunda mwenyewe.
Yule Mzee hakupoteza muda. Alichomoa mkanda kiunoni mwake, nakuanza kumpiga Tunda kila mahali huku akimpiga mateke kama mbwa na kumtukana sana. Alimpiga mpaka jasho lilikuwa likimtoka huku akimwambia jinsi alivyolaaniwa na hana bahati kwenye maisha. Kwa kuwa ndio shangazi yake alikuwa anataka kumpeleka shule lakini ameharibu kwa kumwibia.
Tunda alikuwa kigaragazwa pale chini kama tambara bovu mpaka Nyange alipoanza kupiga yoe akikimbia nje kama mwehu akiomba msaada kwa majirani, ndipo yule mzee alipomuachia na kuanza kumkimbiza sasa Nyange, kumrudisha ndani. Nyange alimnyanyua pale chini na kumpeleka chumbani kwao. “Na asitoke huko ndani mpaka baba yake atakapokuja kumchukua. Hatuwezi kukaa na jizi humu ndani.” Shangazi akaweka msisitizo.
Baba yake alipigiwa simu palepale, huku akitishiwa kuwa akichelewa kidogo tu, atamkuta mwanae kituo cha polisi. Baada ya muda mfupi sana baba yake Tunda alifika pale. Alielezwa mabaya mengi ya Tunda, na jinsi walivyomvumilia kwa muda mrefu, lakini wamefika mwisho. Yule baba hakusema chochote katika hizo shutuma ila kumuulizia mwanae. “Yuko wapi Tunda mwenyewe?” “Huko chumbani, amejifungia kwa aibu.” “Nimewasikia na ninaomba radhi kwa yote aliyofanya. Naomba mniitie, tuondoke.” Aliitwa Nyange, nakuambiwa akamwite Tunda.
Baada ya muda Nyange alirudi huku akilia kwa hofu. “Hawezi hata kunyanyuka kitandani.” Baba yake akasimama kwa haraka na wasiwasi. “Kwani nimgonjwa?” Baba yake akauliza huku akimtizama Nyange. Nyange alishindwa kujibu akakimbilia jikoni. “Kuna nini dada? Tunda ni mgonjwa?” “Kwani huwa wezi wanafanywaje?” Mama Sera akamuuliza mdogo wake kwa jeuri sana. Baba yake Tunda akaonelea aende akajionee yeye mwenyewe. Alishtuka na kurudi nyuma mara baada yakuingia mle ndani na kumkuta Tunda hatizamiki. Alikuwa amepasuka sehemu ya juu ya jicho iliyosababisha kuvuja kwa damu na kulowesha uso mzima mpaka mto aliokuwa amelalia. Midomo yake ilikuwa imepasuka juu na chini, kila alipotoa pumzi nje, damu zilitoka puani.
“Mungu wangu dada! Unauwa mtoto wangu sababu ya mkufu!? Mmekosa utu kiasi cha kuweka mali mbele kuliko binadamu?!” “Unatetea tabia chafu kama hiyo kwa kuwa na wewe ni mwizi.” Shemeji yake akadakia. “Naomba muondoke sasa hivi ndani kwangu, na sitaki kukuona wewe wala mtoto wako tena mkikanyaga hapa nyumbani kwangu. Nikiiona sura yako hapa, baada ya dakika tano zijazo, nakupiga risasi ya mguu. Toa mzoga wako uondoke.” “Mungu atakulipa shemeji. Ipo siku mtajutia unyama mliofanya kwa mwanangu.” Yohana akambeba mwanae, Tunda na kuondoka naye.
Hakuna Msiba Usiekuwa na Mwenzie.
Tunda alishtuka akiwa wodini na baba yake pembeni. “Sikuiba baba. Wamenisingizia.” Tunda aliongea kwa shida sana. “Nasikia maumivu makali sana.” Tunda aliendelea kutokwa na machozi. “Usiongee. Wamekushona shona sana huko usoni. Pumzika tu.” “Wamenising..” “Nafahamu Tunda. Nyange ameniambia kila kitu. Mungu atalipa mwanangu. Pole sana.” Tunda alipumua taratibu akigugumia maumivu, kisha akalala kwa faraja yakujua safari hii baba yake amemuamini.
Alikuwa amevunjwa mbavu na damu ilikuwa ikivuja kwa ndani. Mkono wake wakushoto pia ulikuwa umevunjika kabisa mpaka ulitengana na kuonekana mfupa kwa nje kuwa imetengana. Na bega hilohilo la kushoto, lilitenguliwa. Matibabu yakaanza baada yakufanyiwa x-ray. Akatobolewa na kuwekewa vyuma vilivyotokeza nje kama mshikaki. Waliambiwa sio wakutoka pale siku za karibuni. Hilo likawa sio jambo baya.
Zikawa habari njema zaidi kwa baba yake ambaye hakujua atampeleka wapi binti huyo aliyekuwa anakaribia miaka 20. Akaanza matibabu. Baba yake peke yake ndiye aliyekuwa akimuuguza bila kuchoka asubuhi na jioni alirudi pale hospitalini kumuona mwanae. Alimletea vyakula vyakawaida. Wakati mwingine uji, wakati mwingine Tunda alijua kabisa amemletea chakula alichonunua kwa mama Lishe. Lakini hakuacha kufika hapo. Alileta juice za kuongeza damu na kumsisitiza awe anakunywa. Na kabla hajaondoka jioni, alihakikisha angalau anamnywesha hiyo juisi, ndipo anamuacha mpaka kesho yake anapomletea uji. Napo pia alikuwa akiwahi sana. Anahakikisha anamsaidia kumpigisha mswaki, anamsaidia kunywa uji. Akiona ameshiba vizuri, anamuongezea tena juisi ya kuongeza damu, ndipo anamuachia nyingine pembeni na kumsihi awe anakunywa kila wakati. “Itakusaidia kuongeza damu.” Alisisitiza baba yake.
Wakati mwingine alimletea juisi za majani ambayo alisema ameambiwa na watu inaongeza damu kwa haraka. Rosella. Au matembele. Ikawa basi tu, anamuona vile baba yake anavyohangaika kumuuguza na hakuwahi kuzungumzia habari za ujauzito aliokuwa amepata wakati anaishi na mama yake, ila tu kumuuguza kwa juhudi zake zote.
Siku zilikwenda, madaktari akiridhishwa na upataji wake nafuu. Swali la akitoka hapo atakwenda wapi, sio kuwa lilimsumbua Tunda peke yake, hata baba yake pia. Anampeleka wapi binti huyo! Elimu yake ni ya darasa la pili. Ndugu aliyebaki ni yeye tu. Hata Tunda mwenyewe alizidi kukosa raha kila alipoambiwa anaendelea vizuri. Akakumbuka kuwa kwa ndugu wote amezuiliwa kwenda kuishi. Hana ujuzi wowote ule, na baba yake hakuonekana kama anazo pesa zakumtafutia chumba kama alivyokuwa ameahidiwa na baba Tom.
Ilimbidi baba yake azungumze na uongozi wa hospitali kuomba Tunda aendelee kuwepo hapo mpaka atakapopona kabisa. Alieleza hali yake na maisha ya Tunda kwa ujumla, ndipo akaruhusiwa kuendelea kuugulia pale akiwa anapewa chakula cha bure bila kutakiwa kuondoka, kwa sababu kwa taratibu za kihospitali alitakiwa akishawekewa vile vyuma, baada ya juma moja, arudi nyumbani. Ila kurudi hospitalini hapo kwa siku maalumu atakazokuwa amepangiwa na daktari kuwa akifika kuonana na wataalamu na baadaye kufanyiwa lazoezi. Lakini ndipo uongozi ukamruhusu kubakia hospitalini hapo.
Ndipo maisha ya Tunda yakaendelea hapo hospitalini akiuguzwa kwa utulivu, huku akifikiria pakwenda baada yakutoka hapo. Hakuwahi kumsahau baba Tom na ahadi zake nzuri alizokuwa akimpa kila akimtumia. Ni kweli hakutegemea kama angemtelekeza na kutomtafuta hata kujua anaendeleaje! Akazidi kuumia kujikuta yeye ndiye aliyebaki akilaumiwa wala si baba Tom. “Mama ameweza kumsamehe mumewe, lakini sio mimi!” Tunda alizidi kuumia.
Lakini hakumshangaa sana mama yake. Alijulikana hata na ndugu zake pamoja na wazazi wake kuwa ana roho mbaya na ni mbinafsi wakupitiliza. Tokea anakuwa pale kijijini kwa bibi yake, alikuwa akisikia aliyedhani wakimsema ni dada yake anayemfuata, kumbe mama! Baba yake akaendelea kumuuguza bila kuchoka. Hakukosa kila siku asubuhi na jioni pia.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Akiwa bado hapohapo hospitalini, siku hiyo asubuhi Tunda alimuona baba yake akiingia na chupa ya uji lakini hakuwa na furaha kabisa ila wasiwasi mwingi usoni mpaka akamshtua Tuna. “Kuna nini?” Tunda akamuuliza. “Nilipata matatizo kazini. Wakanikamata na kunifunga. Hapa nipo nje kwa dhamana. Lakini leo ndio siku ya hukumu.” “Lakini si utashinda hiyo kesi?” Tunda aliuliza akionyesha na yeye ameingiwa hofu. “Sijui mwanangu! Lakini nikihukumiwa jela..” Yule baba akasita. “Nitafanyaje baba?!” Tunda naye akazidi kumchanganya baba yake. “Nitahudumiwa na nani? Nikitoka hapa nitaenda wapi mimi!? Naomba wasikufunge.” “Usiponiona mpaka jioni usifikiri nimekukimbia, ujue nimefungwa Tunda. Na lazima niondoke sasa hivi niwahi mahakamani..” Tunda akazidi kulia.
“Hata kama hutakaa ukaniona tena maishani, nataka ujue wewe sio mtoto wa bahati mbaya. Mama yako alinikimbia akiwa na ujauzito wako, kwa sababu zake mwenyewe. Akaenda kumdanganya mwanaume mwingine kuwa ile mimba ni yake. Ulipozaliwa na rangi hiyo na yule jamaa yake alikuwa akijua wazi mahusiano yangu na mama yako, ila walikuwa wakiiba tu, ndipo akamuacha mama yako na mama yako akaamua kwenda kukuacha kwa wazazi wake. Siku ya kwanza kuniona ndio na mimi ilikuwa mara yangu ya kwanza hata kujua kama mimba yako ilitungwa.” Hofu iliyokuwa imemuingia Tunda, hakuweza hata kuongea ila kulia tu.
“Na wakati ule tunaishi wote, unakumbuka uliondoka nikiwa safarini? Nilimpigia simu mama yako maana niliambiwa na mke wangu ulitoroka nyumbani. Mama yako akasema nisiwahi kumpigia simu kamwe kukuulizia kwa unyama niliokufanyia mimi na mke wangu. Tena alinitishia na kuniambia alikupiga picha zote wakati unamajeraha tuliyokusababishia wakati tukiishi wote. Kwa hiyo ikitokea tu nakutafuta tena, hatasita kuniripoti polisi. Nikaamua kunyamaza, mpaka tena siku ile alipokuja nyumbani kwangu tena na kuanza kuongea kama mwehu kuwa hakutaki tena kwa kuwa unamahusiano na mumewe, na ulitaka kuzaa naye pia. Aliniambia upo hospitalini amekutoa ile mimba hataki nikupokee tena.” Baba yake aliendelea kuongea kinyonge.
“Nilitamani urudi nyumbani, lakini ndoa yangu ilishaanza kuwa kwenye misukosuko sana. Nilisimamishwa kazi, nikawekwa kwenye uchunguzi. Yule mama ndiye anatunza familia kwa sasa. Niseme ndiye anayenilisha. Nilijua wazi asingekubali atulishe mimi na wewe. Nilimomba dada akae na wewe nikijua kibiashara ambacho nilikuwa nimekianza kukifanya, kingenilipa kidogo, ili nikutafutie angalau chumba uanze maisha, lakini nimesumbuka mpaka hivi leo sijafanikiwa. Kwa hiyo Tunda, sijawahi kukuona wewe ni mzigo, mwanangu. Ni hivyo maisha yangu yamekuwa kama nina laana, lakini ningekutunza mama.” Tunda alikuwa akilia sana.
“Lazima niondoke sasa hivi, lasivyo nisipotokea mahakamani nitaonekana nimekimbia kesi, au nimetoroka. Kila la kheri mwanangu. Chukua hii bahasha ina pesa kidogo, angalau utapata pakuanzia ukitoka hapa.” Baba yake aliondoka na kumuacha Tunda akiwa amechanganyikiwa kabisa.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Siku zilizidi kwenda akiwa pale hospitalini bila baba yake kutokea, akazidi kuamini ni kweli baba yake amefungwa. Kosa alilojiapia kutofanya nikukubali kuondoka pale kwa haraka, mpaka atakapopona kabisa. Na kwa kuwa hakuna mtu mwingine aliyetokea hapo hata kumjulia hali, uongozi wa hospitali ukamkubalia kuendelea kukaa pale. Akaanza kula chakula cha pale hospitalini, na kwa kuwa alikaa pale muda mrefu kidogo, manesi wengine walianza kumfahamu. Walimletea vitu vidogo vidogo vyakula.
Kwake yale yalikuwa mapumziko makubwa sana. Alipata muda mtulivu wakula na kushiba, huku akiwaza kitu cha kufanya akitoka pale. Mbali na lugha ya kingereza aliyoweza kuiongea kifasaha, hakuwa na elimu yeyote ile. Kifaransa hakuwa mzuri sana, lakini aliweza kuongea japo chakuombea maji. Alijaliwa mwandiko mzuri sana. Ndio hatua ya mwisho aliyofanya kwa makini alipokuwa shuleni wakati akili zake zimetulia akiwa kwa bibi yake. Darasa la kwanza na la Pili. Aliishia kwenye kujifunza kuumba herufi na kusoma, ndipo akapelekwa mjini na mikasa yake ya maisha ikafuata.
“Nani ataniajiri sababu ya mwandiko?” Tunda aliendelea kuwaza akiwa pale hospitalini akiendelea kupona na madaktari wakimpa habari walizodhani ni njema kwake. Kuwa karibuni sana, watamruhusu. “Lazima kujua kitu chakufanya mara baada ya kutoka hapa.” Tunda aliendelea kuwaza wakati wanamtoa vyuma vya mkono baada ya mifupa yote kuunga vizuri.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Mwenge nako hapakuwa mbali kwa mida hiyo ambayo hapakuwa na foleni, alisikia konda akitangaza wamefika mwisho, na hakuwa hata amepata jibu la wapi pakwenda. Ikabidi tu kushuka na kuamua kutafuta sehemu ya kula. Alikuwa na pesa kidogo aliyokuwa ameachiwa na baba yake. Akasogea mpaka kwenye vibanda vya chips. Akaagiza chips yai. Alikuwa hajala hicho chakula kwa muda mrefu sana. Tokea akiishi kwa mama yake. Akajicheka akiwa amekaa anasubiria. Kumbukumbu ya vile baba Tom alivyokuwa akimuhonga aina hiyo ya chakula ikamjia. Alichokuwa akimfanyia ni kubadili tu. Kama sio chips yai na firigisi, basi alimnunulia kuku wakukaanga. Atamfungia kwenye mifuko na kumpelekea nyumbani. Mpaka na yeye akajenga mazoea. Akibakia nyumbani peke yake, basi ataagiza chips yai. Chuki ikazidi kujengeka kila alipokuwa akimfikiria baba Tom kituoni hapo, peke yake hajui pakwenda.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Tunda anatakiwa aanze maisha mapya yakujitegemea akiwa anahesabika ni tatizo la jamii. Ndugu hawamtaki, shule hana, ujuzi aliyonayo ni wa mapenzi tu. Endelea kuwa na Tunda kujua ni nini atafanya huko mtaani baada yakutoka hospitalini!?
Usikose Sehemu ya 8
0 Comments:
Post a Comment