Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Nilipotea! – Sehemu ya 30 - Naomi Simulizi

Nilipotea! – Sehemu ya 30

 

T

unda alicheka sana vile Net alivyomtizama, akajua ameropoka akamuuliza swali kubadili mazungumzo. “Sasa nyinyi mkamshaurije huyo Gabriel na mkewe?” “Waliitwa na wachungaji na wazee wakanisa. Wakasikilizwa na kupewa ushauri. Lakini Gab akasisitiza anachotaka ni talaka, akuoe wewe.” “Sio mimi. Amuoe Nancy ambaye alishaondoka.” Tunda alijaribu kumrekebisha Net huku akiendelea kucheka.

“Mimi naona nikuchukue tu twende wote ndio akili yangu itatulia. Nikikuacha hapa naweza kuchanganyikiwa huko bure! Kwa jinsi unavyomfahamu Gabriel na yeye anavyo kulilia! Mimi naona twende tu.” Tunda alizidi kucheka. “Anamfahamu Nancy. Hamjui Tunda hata kidogo. Net wangu ndiye anayemjua Tunda mwenyewe.” “Wewe ni poze tu!” “Mimi na wewe Net?” “Bado kabisa Tunda. Naona mpaka nikuoe.” Tunda alizidi kucheka.

“Sasa kuna jambo la mwisho linalonisumbua. Maana sasa hivi inabidi nikwambie kila kitu ili ujue.” Tunda akatulia.

 

“Si na mimi sasa hivi unanifahamu kama Gabriel?” Tunda akaanza kucheka tena. “Ujue uache kujifananisha na Gabriel wewe Net! Yule sio na wala hatakaa akawa mpinzani wako hata siku moja.” “Kweli Tunda?” “Kabisa. Wewe wala usimsikilize Gab. Na wala usimuwekee mazingira yakumuonyesha unawasiwasi au mpo wapinzani. Yeye anamjua Nancy, wewe unammiliki Tunda.” Net akacheka.

“Haya Tunda.” “Kweli Net. Mimi sikupambi. Hakuna jinsi ikatokea nikarudiana na Gabriel tena. Yale ni maisha ninayojutia kuyaishi. Wala sifurahii hapa na kutamani kurudi. Yote niliyafanya kwake ili kufikia pesa yake. Sasa wewe unafikiri bila kuwa vile, angefikia kuniachia kadi za benki na cheki?” Net alibaki akimtizama. “Ilikuwa lazima niwe kinyume kabisa na alivyo Bethy ili kufanikisha malengo yangu. Nancy alikuwa tapeli wa mapenzi. Acha hata kufikiria hilo, ni kama unanirudisha huko. Naomba sisi tuendelee na yetu Net.” Tunda akamtuliza.

“Unajua tukisita sita na kuwasikiliza wanachoongea juu yetu, tutajikuta tunakwama kwenye njia mbili na hatutaweza kwenda mbele. Tunaishi nyuma, na utashindwa kunisaidia kama ulivyoniahidi kunisaidia kuishi maisha haya. Tutajikuta tunaishi nyuma na sasa. Mbele hatuendelei. Tafadhali usiyumbishwe Net. Wewe ndio nguzo yangu. Ukianza kuangalia nyuma na kusikiliza watu kama Gab, ujue utanipoteza na mimi. Tafadhali Net, tulia.” Net akavuta nguvu kwa nguvu na kukaa wima.

Tunda akasimama na kwenda kumbusu shavuni. “Nakupenda Net.” Akamnong’oneza sikioni. Net akacheka akionekana ametulia. Akamshika vizuri, akambusu mdomoni kwa muda tu. Net akiwa amekaa, Tunda amemuinamia. Akambusu tena na tena. Tunda akafurahia. Maana alilipata busu kama hilo mara ya mwisho ilikuwa jumapili. “Nakupenda Tunda.” “Nashukuru Net. Nikwawambie siri yangu ndipo tuendelee na mipango yetu?” Tunda akarudi kukaa.

“Niambie.” “Nimekuwa na Gab na wanaume wengine wengi tu. Lakini katika yote niliyofanya, nilitunza busu langu.” Net akashangaa kidogo. “Kwamba ulikuwa hubusu midomo au!?” “Hata mmoja.” Net akakunja uso. “Hata Gabriel!?” Net akauliza kama asiyeamini. “Hata yeye.” “Sadiki!?”  Akaendelea kuhoji kwa mshangao zaidi. Tunda akatingisha kichwa kukataa. “Kwa nini!?” Tunda akacheka kidogo.

“Nilijua watu wote wananitumia tu. Hakuna anayenipenda mimi kama mimi Tunda. Na mimi nilijua nawaibia. Nikaogopa kwenye huo wizi, nisije nika fall in love, au niseme nikapenda halafu nikaja kukimbiwa. Namaanisha ni kitu nilichokuwa nimejiwekea makusudi ili kujikumbusha kila wakati ni nini nafanya ili nisipitilize na kuumia kihisia na kiafya. Sijui unanielewa?” Tunda akamuuliza Net.

“Gabriel ni mmoja wa walio jaribu sana kunishawishi katika hilo lakini hapo nilichora mstari hata kwake Gab. Nilikataa kabisa. Nilitaka siku nitakapo kubali kumbusu mtu mdomoni, iwe nimefika mwisho wa kila kitu. Iwe ni ishara kuwa nimejiachia kwake kwa asilimia zote. Yaani kwa mara ya kwanza niwe nimejifunga kwa huyo mtu ambaye atanikubali mimi Tunda. Ni wewe Net. Nimekubali kujifunga kwako kwa ile garama kubwa ambayo umelipa kwangu. Sina jinsi nitakuwa na furaha na mtu mwingine isipokuwa wewe. Kwako sijifichi. Kwa hiyo naomba uwe na uhakika na mapenzi yangu. Nakuahidi nitatulia kwako tu.” Ilimgusa sana Net.

“Nashukuru Tunda.” “Hii nimekwambia makusudi pengine itakusaidia kwa upande mmoja na yale yanayokukabili sasa hivi kwa Gab. Tafadhali usije wahi kujifananisha naye. Tupange mipango yetu au upange mipango yetu bila kutishwa na yeyote juu yangu. Nakupenda nikiwa nahitaji mapenzi tu kwako, sio pesa zako Net. Nakuhitaji wewe Net.” “Hilo najua Tunda. Ila uliloniambia ni kweli limeniongezea ujasiri.” Tunda akacheka.

 

“Basi tuendelee na mipango yetu.” “Nyumba niliyonayo nimeshakusimulia. Nimejenga kwa pesa yangu, lakini kwa kuwa mimi sio mzawa, imenibidi kuiweka chini ya jina la kampuni ya mama. Hati inaonyesha ni ya kampuni ya mama na ninayo. Sasa naomba nikuuzie ili ikitokea mama anataka kuninyang’anya niwe nimeshauza nyumba yangu.” “Hapana Net! Sio kwa jina langu mimi. Unataka mama yako aje aniue!? Hapana Net.” Tunda alikataa kabisa.

“Nisikilize Tunda. Tanzania ni nyumbani, lazima kurudi. Tukirudi tutaishi wapi? Nataka ibakie kwa jina lako ili tuwe na kwetu hata hapa.” “Uwiii Net! Unataka kuniingiza matatizoni wewe!” “Sina jinsi. Sina mtu ninayemuamini ambaye najua hatakuja kunibadilikia baadaye. Watu wanabadilika Tunda. Na mimi shida yangu sio pesa, ni ile nyumba. Nilishaona watoto wangu wakicheza mle ndani. Nilishaona jinsi tunavyoishi mle ndani. Sitaki siku moja mama aje aiuze kwa hasira au waje wamfilisi na kuichukua nyumba yangu.” “Unahisi wanaweza kuja kumfilisi?” Tunda akauliza.

“Mama ameruhusu hasira zimtawale hataki kufikiria. Ile kampuni anasahau kuwa namsaidia kuiendesha kwa asilimia kubwa sana. Nina uhakika itachukua muda mfupi sana kuharibikiwa baada ya kunifukuza mimi kama alivyokufanyia wewe Arusha. Nimeona hapa kuna watu wachache sana wachapakazi, wanaojituma na waaminifu. Kumpata mtu wa hivyo kwenye kampuni yako! Akakufanyia kazi nzuri, sio kitu rahisi. Unaweza kumpata mchapakazi, lakini baadaye anaingiwa tamaa, anaanza kuiba. Mama hilo analisahau wakati limeshamtokea.” Net akaendelea.

“Na kwa maneno aliyozungumza jana, najua atatekeleza nia yake kwa haraka.” “Nia gani?” Tunda akaendelea kuuliza kutaka kujua kila kitu. “Aliongea kwa kuropoka sababu ya hasira kuwa, anaweza kunipokonya kibali cha mimi kuishi hapa nchini.” “Hivi anao huo uwezo!?” “Kabisa. Kumbuka kisheria yeye ndiye anayeonyesha ananiweka hapa nchini. Kwamba ni mwajiri wake. Ni kiasi cha kunifukuza kazi kwa maandishi na kuniripoti kuwa amenifukuza kazi, basi. Itanilazimu kuondoka ili niwe mbali na wewe.” Tunda akanyamaza.

“Ndio ujue changamoto zinazotukabili na wewe usaidie sio kulinda nafsi yako.” “Ninavyojitahidi kujiweka mbali na hizo mali ambazo mama yako anazonihubiria kila akiiona sura yangu!” “Kwa hiyo na wewe unataka tuwe na ndoa kama ya Gabriel na Bethy?” “Hapana Net.” “Sasa mbona hutaki hata nikusaidie hata shilingi wakati umeshasikia ninazo pesa.” Tunda akaanza kucheka.

“Kumbe kweli unazo pesa?” “Sasa wewe unafikiri kwa nini mama anahangaika hivyo?” Tunda alizidi kucheka. “Lakini wakati wote wewe umekuwa kunionyesha kwa vitendo vile unavyofanya kazi kwa bidii Net. Sijawahi kukutana na wewe popote kama haupo kikazi. Mimi nikajua ndivyo unavyoingiza pesa yako. Kwa jasho lako.” “Nisikilize Tunda. Ni kweli nimekuzwa kwenye mazingira ya kitajiri sana. Lakini kila pesa ninayomiliki, babu alihakikisha tokea napata akili yangu, naifanyia kazi.” Tunda akatulia.

          “Hajawahi kunipa pesa kama kunipa tu. Hata nilipokuwa na shida, alinipa kazi ndipo ananilipa. Nakiri wakati mdogo alikuwa ananipa kazi zisizoendana na malipo, lakini nimekuja kuelewa alikuwa akinifundisha. Nimekuja kukua hivyo hivyo. Hakuna pesa kwenye akaunti yangu ambayo sio jasho langu. Kufanya kazi kwa bidii ndicho ninachojua tokea mtoto. Na mimi sio kama Maya. Ukimwangalia Maya na mimi, unaweza kufikiri tumelelewa na watu wawili tofauti. Lakini ni watu hao hao.”

“Maya alikuwa akipewa pesa ya matumizi kila week, na akitaka nyingine anapewa bila kuulizwa swali. Lakini sio mimi. Kwanza babu alinikuza kutoomba pesa ila kazi ili kupata pesa. Kwa kifupi ninazo pesa kwa kufanya kazi. Nikiwa hapa Tanzania, namfanyia mama kwenye kampuni yake. Nikiwa Canada, nafanya kazi kwenye kampuni ya Cote ya Canada, na huko pia nalipwa.” “Basi ndio maana naona kama wewe unaweza kufanya kazi kwa bidii ukapata pesa, basi na mimi nifanye.” Net akacheka.

“Sasa wewe sio mimi. Mimi mwenzio pesa yangu ni yangu tu. Haiombwi na ndugu yeyote labda niamue kumnunulia mtu zawadi. Nina uhakika nina kazi nyingi zinazoniingizia pesa nyingi kuliko wewe. Nikikaa pale ofisini, nakuwa nafanya kazi mbili au tatu kwa wakati mmoja na zote ninalipwa.” “Kivipi?” Tunda akauliza.

“Kampuni ya Cote hapa nchini ni ya mama. Cote ya Canada ni ya bibi na babu. Imesambaa nchi na miji mingi sana. Babu alihakikisha nafundishwa lugha tano muhimu tokea mtoto. Nina uwezo wakuziongea hizo lugha, na hii ya kiswahili, kama mzawa.” “Net!” Tunda akashangaa. Net akacheka.

“Nilifundishwa Tunda.” “Lakini na wewe unayo akili.” “Nikipaji. Babu alikuwa anasema hivyo. Unajua kuna watu wanakipaji cha lugha tu. Uwezo wakuongea lugha nyingi bila shida. Na pia kufundishwa. Sasa turudi kwenye swali lako.” Tunda akacheka.

“Babu naye alikuwa akizungumza lugha nyingi sana. Yule hata ukimtupa kwenye kijiji chochocte hapa Tanzania, angeweza kuongea kilugha chao.” Tunda akacheka. “Na wewe unajua kilugha gani?” Net akacheka. “Nimekupita mbali sana kwenye kilugha Tunda. Nikianza hapa! Utaona aibu unaweza kufikiri wewe ndio mgeni, mimi mzawa.” “No way! Kilugha gani unazungumza Net?” Tunda akabisha kwa mshangao. Maana aliuliza akijua wazi Net hajui kilugha chochote kutoka kabila lolote Tanzania.

“Wewe si unakijua kipogolo?” Tunda akaanza kucheka. “Net unanitania!” “Kama unabisha,  ongea neno la kipogolo kisha nitakwambia maana.” Tunda hakuamini. “Net! Kwanza kwa nini Kipogolo?” “Kwa ajili yako.” Tunda akakunja uso kama ambaye hajaelewa. “Unakumbuka uliniambia ulikuja mjini ulikuwa hujui kuzungumza kiswahili ila kipogolo tu?” “Net!” Net akacheka sana.

“Sasa huwa nina mtindo wa kuchangamsha akili. Just for fun. Kujichangamsha tu. Hilo neno la ‘kipogolo’ likanisumbua sana. Nikaona isiwe shida. Sekretari wa mama ni mtu wa huko huko. Nikaanza kumwambia anifundishe. Na nikamuomba aniandikie maana ya maneno 100 kwa kipogolo. Nikamwandikia  hayo maneno 100 kwa kingereza na kiswahili, na kumuomba aandike hayo maneno kwa kipogolo. Nikayaweza hayo 100 mpaka na jinsi ya kuweka ulimi. Nikaongeza mengine 100. Kisha nikaanza kutengeneza sentensi. Yeye mwenyewe hakuamini. Akabaki kutoa macho kama wewe.” Tunda akashangaa sana.

“Kweli sikufahamu Net.” Net akacheka tena. “Turudi swali lako la mwanzoni, kisha tuendelee na mambo yetu. Kwa hiyo. Kama nilivyokwambia, hiyo kampuni ya Cote huko Canada, inayo matawi mengi tu, nchi mbali mbali. Sasa huwa nafanya kazi kwenye upande wa mawasiliano na masoko. Nikiwa nimekaa hapa, nakuwa pia mfanyakazi wao. Nawasiliana kwenye hizo nchi Papa au tuseme Nana anazokuwa ananichagulie nifanye mwenzi huo. Matawi yake. Nafanya kazi nao kwa simu, na kompyuta. Namtafutia na bibi masoko kama hivi mama. Namtumia hizo kazi, nalipwa.” Tunda akabaki ametoa macho.

“Kwa hiyo ndio hivyo ninavyoingiza pesa. Usijifananishe na mimi. Kubali nikusaidie kila unapohitaji msaada. Umenielewa?” “Sasa hivi nimekuelewa Net. Lakini acha nifanye kidogo. Na mimi nijione naweza kufanya kitu hapa duniani. Wewe umenifundisha. Mungu amenipa uwezo, naona nitumike kidogo. Nakuahidi nikikwama kabisa nitakwambia.” Net akacheka.

“Kweli Net. Niamini bado sijakwama. Najua unasema ni msemo ninaokwambia kila wakati. Lakini ni kweli sijakwama. Kila kitu kinachonikabili. Wazazi na mimi mwenyewe, vipo ndani ya uwezo wangu. Na ninataka kujiona ni mimi ndiye nimefanya.” “Nimekuelewa Tunda. Ila na mimi naomba niongezeke kwenye orodha ya wanaotaka msaada wako. Fikiria jinsi yakunisaidia mimi na wanangu, wewe kama mama wa familia.” Tunda akacheka sana.

“Haya Nethaniel Cote, baba watoto wangu, at your service.” Net akacheka sana. “Nyumba unauza kwa kiasi gani? Mwenzio sina hela ya kununua nyumba sasa hivi. Kodi tu yenyewe inanitoa jasho!” “Wala usijali. Hiyo pesa itakuwa ya makaratasi tu. Hunipi pesa yeyote ile. Ninachofanya ni kukumilikisha wewe. Kutoka Cote Ltd kuwa Tunda.” “Natamani ingekuwa Tunda Cote tayari!” Net alicheka sana.

“Ndio twende Canada tukafunge ndoa.” “Kwa nini tusifunge hapa ndio twende?” “Hapa kuna sheria nyingi Tunda. Mpaka itangazwe na kusiwe na vipingamizi.” “Na tayari tuna vipingamizi tena vya msingi sana!” Tunda akaongeza. “Umeona eeh! Naona sasa unaelewa ninakopitia.” Net na Tunda walizungumza wakiweka mipango yao. Mpaka wakafikia mwafaka.

Kwa mara ya kwanza walitoka pale wakiwa wapo ukurasa mmoja.  Kama watu wenye mipango inayo fanana. Wanania mamoja kama wanaotaka kujenga familia yao kiukweli. Na kwa mara ya kwanza, Net alijifungua kwa Tunda, Tunda akamfahamu japo kwa kiasi. Akaweza kumfariji na kama kawaida ya Tunda, Mungu alimpa na yeye lugha ya ushawishi na alikuwa na uwezo wa kufikiria kwa haraka. Ndivyo alivyoweza kuwatapeli kina Gabriel, Kinny, Mbawala na wengine wengi. Sasa akampanga na Net. Akatoka pale kama Nathaniel Cote wa zamani sio anayetishwa na mama yake na Gabriel.

 

Mipango Kabambe Yaanza.

Tunda Kwa Mama yake.

T

unda alitoka pale akiwa ameshakubali kuwa maisha yake sio Tanzania tena, kwa hiyo akaanza kujiandaa kuacha familia yake vizuri. Na Net hivyo hivyo ila walikubaliana wasiwaambie watu kwanza. Tunda alirudi hotelini kwa mama yake akamwambia aende naye akamuonyeshe kitu. Alitoka hapo na wadogo zake, mpaka ofisini kwake. Mama yake alishangaa maendeleo ya mwanae. “Hongera Tunda.” “Asante mama. Unapenda niwe nakuchukua kwenda kupamba? Nitakulipa.” Mama yake akacheka.

“Kweli.” “Nitashukuru Tunda. Sina pesa kabisa. Nitaanza hata kukusaidia kusafisha.” Wakacheka.

“Mimi mwenyewe nilifundishwa hivyo hivyo. Utaweza tu na utafurahia. Lakini inabidi kutafuta pakuishi mama. Yule mwanasheria ambaye nimekwambia nitakupeleka kwake amesema mambo ya kesi huwa yanachukua muda. Lazima kina Tom warudi shule. Na pale nilipowakuta, mlipokuwa mkiishi na baba yao, sio mazingira mazuri kwao kuendelea na masomo.” “Naelewa Tunda. Lakini hata sijui nafanyaje! Unajua kazi nilifukuzwa?” “Kwa nini!?”  Akasita kumwambia ukweli Tunda.

Tunda akaona asilazimishie kujua yasiyo muhusu, yeye afanye anachoweza. “Sababu ya wizi.” Tom akadakia, wote wakamgeukia Tom. Tunda akakunja uso na kumgeukia mama yake. “Na wewe walikusingizia!?” Akahisi wazazi wake wote wamepata tatizo linalofanana. “Mambo yalikuwa magumu sana. Nilianza kuchukua madawa, na kuwauzia watu. Hasa ya usingizi. Wakanitega na kunikamata. Hivi ninavyokwambia nimefukuzwa kwa barua kutoka wizarani. Niliponea kufungwa. Nimejiharibia, hakuna ninakoweza kuajirika tena kwa kazi hii ya uuguzi.” “Pole.”

“Mambo yalikuwa magumu sana. Lakini najua sikutakiwa kuiba.” Tunda hakuwahi kumuona mama yake akiwa mnyenyekevu vile. Alijirudi kama sio yeye. “Basi biashara itakusaidia.” Wakazungumza hapo na mama yake, akimuonyesha anachofanya.

 Kwa Net.

N

et yeye akaondoka pale akiwa amejawa furaha na ujasiri. Mambo yalikuwa yanakwenda vizuri kwa upande wake na Tunda. Wapo ukurasa mmoja. Walishakubaliana waendelee na mipango yao, wasiwajali mama Cote na Gabriel.

Kimya kimya bila kumshirikisha yoyote akaanza kushugulikia karatasi ambazo alijua Tunda angehitaji kuombea Visa ya Canada. Na kutafuta ushauri wa kisheria jinsi anavyoweza kumkabidhisha Tunda ile nyumba kisheria na kuhakikisha hakuna mtu anayeweza kumnyang’anya tena. Ibakie kwa jina la Tunda tu. Siku hiyo hakurudi ofisini. Akawa na hekaheka nyingi karibia siku nzima.

Ijumaa.

K

ila mmoja alikuwa kwenye mikakati yake kwa nafasi yake. Net na Tunda kivyao, kukamilisha yao ambayo ni wao tu wawili walikuwa wakiyajua. Na Ritha naye akawa kwenye mikakati yake, akiwatumia wanandoa hao. Gabriel na mkewe. Ritha kama kawaida yake. Alishawasoma wote wawili. Gab na Bethy. Akajua udhaifu wa wanandoa hao. Akawapigia mahesabu. Akawapanga vizuri akabadili utaratibu. Akaamua awe anakutana na wana ndoa hao tofauti tofauti na kila mmoja alifanya nao makubaliano tofauti tofauti. Akiwa na Bethy lengo ni kumuangamiza kabisa Tunda, lakini anapokuwa na Gabriel lengo linakuwa ni kumtenganisha Net na Tunda. Kote, yeye ndiye alinufaika bila wengine kujua.

Net alijitahidi kumkamilishia Tunda vitu vyote ambavyo walitakiwa kuwa navyo ili kuhakikisha Tunda anapata Visa ya Canada. Ilikuwa ni siku ya ijumaa ambapo walikutana jioni nyumbani kwa Tunda ili kuanza kutuma maombi hayo ya Visa kwenye ubalozi wa Canada. Simu ya Tunda iliyokuwa karibu na Net, ikaanza kuita. Net akaichukua ili kumpa. Akashtuka kuona namba ya mama yake. “Nini?” Tunda akauliza baada yakumuona Net ameshtuka. Net yeye ndiye aliyekuwa akijaza kwenye laptop yake, kumuombea Tunda Visa, online. “Mama huyu!” Tunda akakunja uso.“Amepata wapi namba yangu!?” Tunda akauliza. “Pokea tumsikilize.” Net akashauri.

Tunda akapokea na kubonyeza kwenye speaker ili na Net asikie. “Upo sehemu tunayoweza kuzungumza?” “Ndiyo. Shikamoo.” “Upo peke yako?” Mama Cote akauliza. “Ndiyo sababu uliyonipigia simu?” Tunda akamuhoji akimtaka asimpotezee muda. “Hapana. Naona ni kama tumeanza vibaya Tunda. Nataka amani na wewe. Net ni mtoto wangu najua na wewe utakuwa kwenye familia. Lazima tuwe pamoja na tupatane.” Tunda alibaki kimya akimsikiliza. “Upo Tunda?” “Nipo na ninakusikiliza.” “Ndio nilikuwa nataka nikukaribishe kwa chakula cha mchana, pale Paz city. Tupate muda wa kuzungumza.” Net akakunja uso.

“Lini na saa ngapi?” “Kesho, saa saba mchana.” “Kesho ndio siku yangu kubwa ya kazi. Kuanzia asubuhi mpaka usiku.” Tunda akajibu. “Jumapili je?” Mama Cote akauliza. “Nakuwa kanisani.” “Ukitoka kanisani, je?” “Nitazungumza na Net, kisha nitakujulisha.” “Sio kila jambo letu tunalofanya mimi na wewe, Net ajue! Kuna mambo ya wanawake yanayotuhusu sisi tu. Wala Net haihitaji kujua.” Mama Cote alizungumza kirafiki. “Naomba nikujibu baadaye kama nitaweza  kwa siku hiyo ya jumapili au tufanye wakati mwingine. Asante na usiku mwema.” Tunda akakata.

“Kuna jambo linaendelea Tunda. Kuna mtego tu. Kama kweli mama angekuwa na nia ya kutaka amani na wewe, kwanza asingeficha kukutana kwenu, na angekualika nyumbani kwake alipo Nana. Mara ya mwisho alikuwa akigomba na Nana alijua kuna tatizo. Na anajua kabisa vile Nana anavyonipenda na kuniheshimu. Hajawahi hata kunipazia sauti mbele yake. Kama angetaka kulisawazisha hilo, angeanzia alipo Nana ambako ameharibu.”

“Kwa kuwa Nana alishtuka sana, alipotoka na kumkuta mama akinifokea, mimi nimetulia tu. Alitaka kujua tatizo ni nini, lakini sikutaka kuharibu zaidi, ila najua Maya atakuwa ameshaanza kuhisi. Alishangaa siku ile ya kukuvalisha pete vile ulivyoondoka bila kuaga na kutokurudi tena pale wakati bado yeye Nana yupo. Tena akiwa amekuonyesha amekukubali!” Tunda akajua aliharibu kuondoka bila kuaga. Ila akaona anyamaze tu, Net aendelee.

“Na Nana aliposema wakati namrudisha Canada na wewe twende wote, mama alikataa mbele yetu wote bila kufikiria kitu kilichoamsha maswali kwa Nana na Maya, wakimuhoji ni kwa nini hataki wewe ufike nyumbani, Canada! Akatoa sababu ambazo hata bibi alijua anadanganya maana alimuuliza maswali ambayo hakuwa na utetezi mzuri. Liko jambo Tunda. Na sijui ni nini anataka?” Net alibadilika mpaka sura.

“Nitafanyaje Net? Naogopa. Akija kunidhuru je?” “Na mimi hilo ndilo linalonitia wasiwasi. Mama amefika pabaya. Na sasa hivi atafanya chochote ili kushinda. Mbaya zaidi, sidhani kama atafurahia matunda ya anachopanda sasa hivi. Huwa namjua kuwa anahasira sana. Sasa najiuliza hiyo hasira ikimwisha, akajikuta katikati ya huo uharibifu, sijui atajitoaje!? Hakika sijui! Mimi nimemuonya sana. Na mbaya zaidi ameingia kwenye ndoa ya Gabriel, anawachanganya wale watu, nahisi mwisho wake hautakuwa mzuri.” Net aliendelea kulalamika.

“Turudi kwangu Net. Nifanyaje?” “Nenda. Lakini usiende peke yako. Muombe mama Penny akusindikize. Ila usimwambie mama kama utakwenda na mama Penny. Ashtukie tu unafika pale na mama Penny. Na mimi nitakuwa karibu. Kwa lolote watakalopanga kukufanyia, niwepo karibu.” “Hapo sawa.” Wakakubaliana.

Tunda akampigia simu mama Penny. Akamuelezea kwa kifupi, na hofu yake na Net juu ya kikao hicho, mama Penny akakubali kumsindikiza. Akamtumia ujumbe mama Cote kuwa itakuwa jioni ya saa 9 sio saa saba mchana. Mama Cote akakubali. Net na Tunda wakatuma yale maombi ya Tunda kwenye ubalozi wa Canada, wakabaki wakipanga mipango yao.

Jumapili!

N

et alikwenda kumchukua Tunda nyumbani kwake wakaenda naye ibadani, kanisani kwa kina mama Penny. Walikaa pamoja. Baada ya ibada wao walikwenda kukaa kwenye gari wakimsubiria mama Penny amalize mambo yake pale kanisani, waongozane na Tunda. “Nilitamani kwenda kwa baba leo.” Tunda alianza baada ya muda mfupi kuingia kwenye gari. “Kama ukiwahi kumaliza, tunaweza kwenda.” Tunda akamtizama Net.

          “Vipi?” “Nina wasiwasi Net. Naomba chochote kikinipata, usiache kumfuatilia baba yangu na kuhakikisha anatolewa jela.” “Tunda!” “Kweli Net. Chochote kinaweza kutokea. Nililala nikiwaza. Mama Cote nimempokonya watu wawili muhimu sana kwenye maisha yake. Nakumbuka chuki aliyokuwa nayo tulipokuwa Arusha! Ile ilikuwa kwa mchumba wake tu. Sasa, sasa hivi itakuwa zaidi kwa kuwa nimeingia kwenye familia yake yote. Maya na bibi pia wanaonekana wapo upande wangu. Hawezi kukubali hivi hivi.” Net akanyamaza.

“Au usiende?” Hofu ikawa imeshamwingia Net. “Siwezi kuacha kutokwenda. Ikiwa ni kweli anataka amani je? Nitakuwa nimekimbia kitu cha msingi sana kwetu.” Net kimya. “Tunamuhitaji Net. Hatuwezi kumpuuza. Katika lolote lile analotaka kufanya, nia nikulinda kilicho chake.” Net kimya, alimjua mama yake.

Tunda naye akanyamaza mpaka mama Penny alipokuja kuwagongea kioo. “Mbona mpo kama mko msibani!?” Wote wakacheka. “Twende Tunda.” Mama Penny akaelekea kwenye gari yake. Tunda akambusu shavuni Net na kutaka kuondoka. Net akamuwahi tena kupata busu la mdomoni. Akambusu kwa muda kidogo, akamuachia midomo lakini akabaki amemshilia pale pale pembeni ya shingo alipokuwa amemshika wakati akimbusu.

“Nakupenda Tunda. Na nina kuombea.” Angalau Tunda akatabasamu.“Asante Net. Na mimi ukumbuke nakupenda.” “Siwezi kusahau Tunda. Asante.”  Tunda akampa busu la juu ya midomo, akashuka kwenye gari ya Net, akaingia kwenye gari ya mama Penny. Wakaondoka,  Net akiwafuata nyuma kwa gari yake.

 ~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Acha wasiwasi wewe Tunda!” “Sijui mama Penny, moyo wangu umekosa amani kabisa!” “Sasa mimi si nipo na Net naye amesema hatakuwa mbali?” Tunda akavuta pumzi mara kadhaa na kuzishusha. Wakatulia hapo garini. Mama Penny akaendesha moja kwa moja mpaka Paz City. Kwa kuwa ilikuwa siku ya jumapili, hamna magari mengi barabarani, iliwachukua muda mfupi kufika. Akaegesha gari, wote wawili wakashuka.

          Akajaribu kumchokoza kidogo, Tunda akaanza kucheka huku wanaingia ndani. Kuingia tu, akawaona mama Cote na Bethy wamekaa wakimsubiria. Wote walionekana kushtuka. Kicheko cha Tunda kiliisha gafla baada yakumkuta na Bethy aliyekuwa ameonyeshwa picha zake na Gabriel na yeye yupo pale. Moja kwa moja akajua lipo jambo. Na mama Cote naye aliduwaa wazi baada yakumuona mama Penny.

Wakatembea mpaka kufikia meza. “Karibuni.” Bethy yeye akajikaza kuvunja ukimya maana yeye Ritha ni kama alibaki ameduaa tu. “Naona umeamua kuleta mtu mwingine!” Ritha akajikuta anaropoka.  “Huyu ni mama Penny, ni dada yangu. Sidhani kama anashida kuwepo kwenye kikao chetu chakuleta amani, kama ambavyo na Bethy yupo hapa.” Tunda akamjibu taratibu tu.

“Kumbe mnafahamiana na Bethy?” Ritha akauliza kwa mshangao. “Ataacha kunifahamu vipi wakati alikuwa mke mwenzangu?” Bethy akajibu. “Ulikuwa mke mwenza na Nancy, wala sio Tunda. Na Nancy alishaondoka muda mrefu sana, anayeishi sasa hivi ni Tunda.”  Tunda akajibu bila kubabaika au kuonyesha hofu. “Akijakurudi Nancy tena itakuaje?” Akauliza Ritha. Tunda akacheka. “Nilijua tu kama hukuwa na nia ya amani mama Cote. Ila kwa kuwa nimeshafika mpaka hapa, naomba uniambie ulichoniitia.” “Ni mazungumzo tu ili kuwekana sawa. Una wasiwasi gani?” “Sina wasiwasi wowote.” Tunda akajibu.

“Basi niseme haraka.” Ritha akaongeza. Tunda akanyamaza akabaki akimtizama, muhudumu akafika. “Naona wageni wenu wamefika. Mpo tayari kuagiza vinywaji sasa?” Muhudumu akauliza na tabasamu akimtizama mama Cote na Bethy. “Naomba red wine.” Bethy akamwambia muhudumu. “Kama tukipata chupa ya champaign ingetufaa. Isio na kileo lakini. Tunataka kusherehekea. Lete na glass 3.” “Mimi sitakunywa champ…” Tunda akataka kukataa, Ritha akamuwahi kwa swali la kejeli. “Hutaki kusherehekea kumilikishwa nyumba ya Cote?” Kimya.

Tunda akajua tayari yule mama ameshajua. “Ulifikiri itakuwa siri mpaka lini?” Ritha akauliza huku akicheka wazi akionekana na maumivu moyoni. “Ulifikiri sitajua kama umeshaanza kuchukua mali zangu?” Akauliza tena. Tunda na mama Penny kimya. “Hakuna kitu cha Cote kinaendelea hapa mjini, mimi nisijue. Umefanikiwa kuingia kwenye akili za Net, kwa akili kubwa sana, kuliko shule aliyosoma yeye! Tena umehakikisha umefanya mambo yako kisomi sana, hakuna penye swali, wala utata. Sasa hivi wewe ndio mmiliki halali wa nyumba ya Net, iliyokuwa ipo chini ya kampuni yangu. Alikwambia hayo yote?” Tunda kimya.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

       Akakumbuka siku ya alhamisi Net alipomfuata ofisini na makaratasi kutoka kwa mwanasheria akimuomba aweke saini kwenye hizo fomu, ili kukamilisha utaratibu wa kumiliki hiyo nyumba na kutuma maombi ya kubadili jina lililopo kwenye hati. Kutoka Cote, kuwa Tunda. Net alimwambia ameshakamilisha kila kitu. Na baada ya yeye kuweka saini tu, ile nyumba ni yake kihalali, na akampa milioni 3 taslimu, kisha akamuomba yeye Tunda, amwandikie hundi ya milioni tatu kama malipo ya kununua nyumba kwa kina Cote.

       Akiwa na wasiwasi, bila amani, huku Net akimsisitiza kuwa ile nyumba ni jasho lake, hawezi kuacha ikapotea bure, Tunda alisaini. Akaandika na hundi ya milioni 3 tu, inayoonyesha jina la mlipaji kuwa ni yeye Tunda, akamkabidhi Net. Net aliondoka akimwambia yeye mwenyewe atamalizia kila kitu.

 

Akasahau hata kumuuliza iliendaje. Alhamisi jioni yake hakumuona Net, alimtoa bibi yake na Maya kwa chakula cha jioni. Ijumaa walikutana wakiwa na lengo lakutuma maombi ya Visa. Kila mtu akili ikazama huko kwenye kuhakikisha hawakosei kutuma hayo maombi. Tunda akimsaidia kumpa Net baadhi ya taarifa zinazomuhusu yeye tokea anazaliwa, Net anazijaza kwenye kwenye hizo fomu za maombi, mtandaoni. Ndipo simu ya mama Cote ikaingia kumtaka wakutane. Mambo yakavurugana. Net akaondoka kwenda kulala kwa makubaliano ataenda kumsaidia mpenzi wake kupamba siku inayofuata jumamosi.

Tunda aliamka siku ya jumamosi akiwa na mawazo ya kazi na hofu yakukutana na Ritha hiyo siku ya jumapili. Alianzia hotelini alikokuwepo mama yake na wadogo zake. Akamchukua mama yake. Ilikuwa saa 11 asubuhi ya siku hiyo ya jumamosi wakati Tunda alipowasili ukumbini na mama yake ili waanze kupamba. Net hakuchelewa, na vijana wa kazi nao hawakuchelewa. Wakaanza kazi. Kufika saa tano asubuhi, wakawa wamemaliza ukumbi wa kwanza, kwenda wa pili.

          Kwa kuwa kazi zilikuwa mbili tu jumamosi hiyo, wakaambiana wapumzike kidogo, wakutane saa 6 na nusu kwenye ukumbi mwingine. Mama yake aliondoka kwenda kukutana na dalali, Tunda na Net wakaelekea ukumbi mwingine. Tunda alirudi nyumbani saa mbili usiku akiwa hoi, hata wazo la kuuliza juu mipango ya Net na nyumba yake hakuwa nalo ila wasiwasi wa kukutana na mama Cote kesho yake ndio uliokuwa umebaki.

          Makubaliano na mama yake ilikuwa ni atafute chumba hata kimoja, aishi hapo kwa muda wakati anafuatilia mambo ya mali zake na mumewe. Tunda alimuahidi kumlipia kodi ya mwaka mzima, wakati anatafuta kitu chakumwingizia kipato na wadogo zake warudi shule. Aneti alishaanza kupata nafuu kubwa tu. Hapo ndipo mama Cote ndio anamkumbusha maswala ya hiyo nyumba ambayo hata hawakuwa wameongea itakuje baada ya nyumba hiyo kuwa yake kihalali.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Kwa hiyo nyumba ishakuwa yako kihalali sasa! Bado tu hati, ni nini kinafuata Tunda? Hebu tuambie.” Ritha akamtoa Tunda mawazoni.  “Hilo swali ni la msingi sana. Lakini hata sijafikiria kinachofuata.” Tunda alijibu ukweli wa mambo, lakini wao wakachukulia wanabezwa. “Labda kuhamisha kampuni yako mama Cote iwe kwa jina lake.” Bethy akaongenza kwa kejeli. “Hapana. Mnafanya biashara ambazo sina nia wala mpango wa kuzifanya. Kwa hiyo katika hilo usiwe na wasiwasi. Mimi nipo na Net, wala nyinyi msiwe na wasiwasi na vyenu.” Tunda akajibu akiwa ametulia tu.

“Ni kweli. Una haja gani yakufanya kazi wakati pesa yote ninayoitolea jasho na niliyoitolea jasho inaingia mfukoni mwako?” Ritha akaongeza. “Mama Penny, naomba twende dada yangu. Naona kikao kimeisha.” Tunda akasukuma kiti nyuma, akasimama. “Huyo ndio mlinzi wako?” Bethy akauliza kwa kejeli. “Kama ulivyo wewe kwa mama Cote.” Akajibu Tunda, wakaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alipoingia tu kwenye gari, mama Penny akampigia simu Net na mumewe akawaomba warudi kanisani wakazungumze. Hakuna aliyekataa. Tunda akamuona mama Penny amebadilika. Lakini hakutaka kumuuliza. Akanyamaza tu, alijua ataongea tu. Mama Penny hawezi kuweka jambo moyoni. Akaamua ampe muda ayapange maneno yake mpaka atakapokuwa tayari kuongea ambapo pengine itakuwa kwenye hicho kikao. Wakaendesha kimya kimya mpaka kanisani.

Wakamkuta na mchungaji naye ndio anashuka kwenye gari yake. “Njaa inaniuma mama! ” Mchungaji akamlalamikia mkewe. “Wote hatujala baba Penny. Pole. Lakini hili ni la muhimu. Umewarudisha kina Penny?” “Ndio nimeingia tu ndani na wewe ukapiga kunitaka nirudi hapa, kwema?” “Twende tukazungumzie ofisini.” Net naye akafika, wote wakaingia ofisini.

“Ni nini kinaendelea Tunda na Net!?” Mama Penny akauliza. “Labda ufafanue zaidi mama Penny.” Net akaongea kiungwana. “Tuanzie swala la nyumba. Ni nyumba gani anayolalamikia mama yako?” Net akaeleza kwa kifupi mwanzo mpaka mwisho na kumuacha mama Penny na mumewe wametoa macho.

“Nia ni nzuri Net, lakini huoni kama unamwingiza mwenzio matatizoni?” Mchungaji akauliza. Net kimya. Mchungaji akaendelea. “Kwa historia ya Tunda, na hiki ulichokifanya wewe, watu wote watajua nia ya Tunda kwako ni kweli ni mali.” “Sina jinsi baba Penny. Sina namna nyingine. Tunda atakuwa mke wangu. Hiyo nyumba ikiwa chini ya Tunda, nitakuwa sijapoteza.” Net akaendelea kutetea lakini akaona kila mtu kimya. Wazi usoni walionyesha kutoridhika. Tunda alibaki ameinama tu.

“Jamani, hiyo nyumba ni jasho langu. Nimetengeneza kwa jasho langu mimi bila msaada hata shilingi kutoka kwa mtu yeyote yule na Mungu wangu ni shahidi. Sio nyumba ya ajabu sana, lakini ni yangu. Nimeijenga mchana na usiku, kwa kujinyima. Kwa maombi mpaka nikamaliza. Siwezi kuruhusu hasira ya mama ikafanya ipotee bure.” Net akaendelea kuweka utetezi wake.

“Babu mwenyewe kabla ya kufariki alitaka kunisaidia kwa kuwekeza pesa, lakini nilikataa. Ile nyumba nimejenga nikiwa mwanafunzi, huku nikiwafanyia kazi babu na Nana. Niliwaambia msaada ninaotaka kutoka kwao, ni kazi. Wakaniajiri kwenye kampuni yao. Nilikuwa nikifanya kazi huku nasoma, ili tu nijenge kitu changu kisichokuwa na mkono wa mtu. Sikatai kuwa mama ndiye alihusika kunitafutia kiwanja.”

“Sijui alifanyaje kukipata, ila pia nilikilipia mimi mwenyewe kwa pesa niliyoipata kwa kufanya kazi. Kuanzia msingi mpaka vigae, ni pesa yangu. Hakika siwezi kuruhusu ikapotea bure. Babu alishawahi kuja kabla hata hajaanza kuugua na kuiona. Natamani mngeona furaha iliyokuwepo usoni mwake baada yakuiona ile nyumba. Alijivunia sana na ikawa ni kitu anachojisifia kwa wenzake mpaka anakufa.”

“Babu alikuwa na mtoto mmoja tu, ambaye ni baba yangu. Baba naye akafariki na kuniacha mimi nikilelewa na babu. Babu naye alizaliwa peke yake. Mimi na Maya ndio ukoo kwa babu. Alinilea mimi na Maya kama watoto sio wajukuu. Chochote nilichofanya, kilimgusa babu moja kwa moja. Ile kuona nimebadili udogo kuwa jengo vile, kwake ni kitu amekisema mpaka anaingia kaburini anasimulia mpaka madaktari na manesi waliokuwa wakimtibu, tena kwa kurudia rudia.”

“Alikuwa akiwaambia kuwa, ‘Net amejenga nyumba kutoka kwenye msingi. Amebadili vumbi kuwa jengo, msitu kuwa mahali pamakazi.’ Ndio usemi babu yangu alisema na kujivunia mpaka kifo chake. Leo niache mtu baki tu aje aishi kwenye ile nyumba! Hapana jamani. Ni garama ambayo nimemuomba Tunda anisaidie kulipa ili hiyo nyumba ibaki kuwa yetu na watoto wetu.” Hata Tunda hakujua kwa mapana kiasi hicho.

Yeye Tunda alijua ni nyumba tu ambayo inamuhangaisha mtoto huyo wa kizungu. Alishatamani kumwambia wajenge kwenye kiwanja chake nyumba kama ile, lakini kumbe nyumba yenyewe ina historia nzito sana kwa Net. “That’s my legacy! Tafadhali naomba mnielewe.” Net alimalizia hivyo akiweka msisitizo, nakuwaacha wote wanavuta pumzi kwa nguvu.

“Mimi narudia pale pale Net. Nia ni nzuri. Lakini unamwingiza au tuseme unahalalisha vita inayoendelea kwa Tunda.” “Ningefanyaje baba Penny? Rafiki au familia ya pekee mbali na mama yangu ninayoifahamu na ambao nipo karibu nao ni ya Gabriel ambaye kama tulivyowaambia, ndio wako kinyume nasi kwa sasa. Nikisema niende kwa wazazi wake Gabriel ndio nitakuwa naharibu kabisa. Gabriel ni zaidi ya alumasi kwa mama yake. Hakuna mtu mkamilifu hapa duniani kama Gabriel kwa mama yake.”

“Ni vile tu yule mama si mtu wa mbele mbele kwenye mambo, najua hili ambalo Gabriel analalamika nalo, atakuwa anajua kabisa, na kunilaumu. Kwa kuwa ninauhakika ni sisi tu ndio tulikuwa hatujui kama Gabriel anamatatizo ya ndoa, lakini si yule mama. Anamjua mwanae kwa kumtizama tu. Furaha ya Gabriel ndio ya yule mama. Hajui kusema hapana kwa Gabriel, mpaka baba yake alikuwa akihofia atamuharibu. Kwa kifupi nilikuwa sina wa kumkimbilia ila Tunda.” Kimya.

“Tunda amesema unamrudisha bibi yako Canada. Ukumbuke utamuacha hapa peke yake. Na kwa baya lolote litakalompata Tunda, ujue limeathiri watu wanne wanao mtegemea kwa karibu sana Tunda.” “Naelewa mama Penny. Nimeshaongea na bibi, amekubali arudi tu na Maya. Sisi tumfuate tutakapokuwa tayari. Japo alitoa ushauri mgumu kidogo. Najua kwa desturi ya hapa ni ngumu. Sikumjibu ndio au hapana, nilinyamaza kwa kuwa nilijua haiwezekani.” “Ni nini?” Tunda akauliza. Net akabaki kama anafikiria.

“Net?” Tunda akauliza tena kwa upole. Akamshika mkono. “Ni ushauri gani bibi amekupa?” “Nilimweleza kwa kifupi, kwa kuwa yeye pia anajua ni kwa nini nipo hapa na ninaishi hapa kwa kibali cha kazi. Akashauri kwa kuwa mambo ya kanisani yanaweza kuchukua muda mrefu kabla ya ndoa, akatoa ushauri nimuoe Tunda mahakamani, tukitulia ndio tufanye kanisani. Lakini nika..” “Sawa.” Tunda akakubali kwa haraka bila hata Net kumaliza. Net hakutegemea.

Wote wakamgeukia Tunda. “Tunda!” Mchungaji na mkewe wakajikuta wakimshangaa kwa pamoja. Tunda akamgeukia Net vizuri. “Nisikilize Net. Kama itakusaidia kwenye mambo yako yakuwa hapa Tanzania bila shida na maswala mengine kama hiyo nyumba. Angalau ikijulikana ipo kwa jina langu, na mimi ni mkeo, itapunguza maswali na makali ya hilo jambo. Tufanye tu hivyo.” Kimya.

“Kwani ndoa ni nini?” Tunda akamgeukia mchungaji na mkewe. “Binafsi nina amani. Ndoa ni makubaliano ya mume na mke. Kama mimi na wewe tumekubaliana, sidhani kama kuna shida.” Net akaongeza akionekana kulifurahia hilo. Mama Penny na mumewe wakaangaliana.

“Kweli safari hii tumejaribiwa pabaya!” Baba Penny alisikika Tunda akacheka. “Mimi naombeni mfikirie baba Penny. Hii ndoa yetu mtatangaza lakini wote tunajua mtagonga tu mwamba, hamtafika popote. Mimi na Net wote tuna vipingamizi ambavyo hatuwezi kukwepa. Watawapinga kwenye kila tangazo na kila eneo. Na wote watakuwa na sababu zakueleweka.” “Nakushukuru Tunda.” Net akamgeukia na kumbusu. Furaha ikawajaa gafla.

“Naomba msubiri kwanza.” Mama Penny akawakatiza. “Hivi wewe Tunda unajua harusi za mahakamani?” Akamuuliza Tunda. “Kwanza ujue ni ndoa halali tu, hakuna watu zaidi yenu na mashahidi. Huwezi kutokea pale na mashela kama maharusi wengine na kelele za vigelegele. Ni kimya kimya!” “Lakini Net si atakuwepo?” Tunda akauliza.

“Tunda! Naomba ufikirie.” “Baba Penny, najua maisha niliyoishi, najua nilipo na ninapokwenda. Hakuna mwanaume atakuja kunipenda na kuniheshimu ila Net. Sitakubali apande ndege, hata kwa ahadi ya kurudi, bila kunioa. Iwe kanisani, iwe mahakamani. Sijali. Na kama Net mwenyewe anaona nisawa, nataka ndoa.” Ilikuwa faraja kubwa sana kwa Net.

“Binafsi itanirahisishia mambo mengi sana. Hata ukaaji wangu hapa nchini, hautakuwa wa shida kama hivi sasa ambavyo nahangaika kuombewa vibali vya kazi kila wakati, na zaidi sasa hivi inavyojulikana nafanya kazi chini ya kampuni ya mama, ambaye ndio ananitishia . Najua ni garama kubwa analipa Tunda, lakini sina jinsi.” “Mimi nipo tayari Net. Naombeni baraka zenu mama Penny na mchungaji. Tafadhali sana. Nawahitaji sasa hivi kuliko mtakavyofikiria.” “Mmmh! Kazi ipo!” Alisikika mama Penny. Tunda na Net wakabaki wakiwaangalia kwa zamu.

“Labda ni hivyo pia ambavyo hata bado hatujaitangaza kanisani. Lasivyo watu wasingeelewa. Kutoa harusi kanisani kupeleka mahakamani!” “Sio hivyo tu baba Penny, na sisi ndio wasimamizi!” Akaongeza mama Penny. “Tutabariki kanisani mambo yakitulia. Hata Nana amesema hivyo. Nana mwenyewe alikuwa anategemea harusi kubwa ya kanisani, lakini hatuna jinsi. Amesema tutafanya tena nyingine. Nawaomba mtusaidie mama Penny. Tafadhali.” “Lini?” Akauliza mchungaji.

Net akamgeukia Tunda. “Wewe ulitaka iwe lini?” Tunda akamuuliza Net. “Utajali tukifanya kabla ya bibi kuondoka?” “Inamaana iwe week hii inayoanza kesho!?” Tunda akauliza kwa kushtuka kidogo. “Unafikiri itawezekana?” Net akauliza tena, Tunda akamgeukia mama Penny. Mama Penny akavuta pumzi kwa nguvu. Akarudi kumtizama Net. Akajiweka tena sawa kama anayefikiria.

“Maswala ya mahari! Unaelewa mambo ya mahari Net?” Mchungaji akamuuliza Net. “Sidhani kama nilazima.” Akawahi kujibu Tunda. “Hapana Tunda. Baba yupo hai. Lazima kumuuliza yeye.” “Sawa. Nitakwenda kuzungumza naye mimi mwenyewe na kumwambia nia yangu yakutaka tufunge ndoa kwa haraka. Akitoka, atashuhudia harusi yetu ya kanisani.” “Hapo sawa.” Mchungaji akaridhika.

“Sasa mtatusimamia au kwa kuwa ni ya mahakamani hamtaki tena.” Mama Penny wakaangaliana na mumewe. “Msibadili mawazo bwana!” Tunda akabembeleza. “Ni hivyo nakupenda tu Tunda, lakini…” Tunda akaanza kucheka. “Unacheka nini wakati mnatuingiza matatizoni?” “Heri niwe na wewe matatizoni mama Penny, naona nitashinda kuliko niwe peke yangu.” Mchungaji na Net wakacheka. “Unaakili mbovu wewe!” “Kweli tena mama Penny. Sasa unafikiri nitafanyaje?” “Haya, nendeni mkapange mambo yenu mkiwa mmetulia, halafu kesho mtatujulisha.” Net na Tunda wakashukuru, nakutoka.

Wakiwa njiani Net akampigia simu mmoja wa mwanasheria ambaye wanamtumia sana kwenye mambo ya kampuni yao kumuomba muongozo. Yule mwanasheria akampa namba ya simu ya mtu ambaye alijua anaweza kumsaidia kumpa taratibu zote. Alipompigia tu simu, akapokea bila kuchelewa.  Moja kwa moja Net akamweleza nia yao yakutaka kuoana. Akamwambia kuwa yeye hakuwa mzawa, lakini alitaka kufunga ndoa ambayo itatambulika kimataifa.

Akamwambia inawezekana kabisa, lakini kwa kuwa yeye hakuwa raia wa Tanzania, ili kufunga ndoa nchini anatakia kwanza kuwa na ‘Certificate of No impediment’ , kutoka nchini kwao. Ili kuonyesha kuwa hujawahi kuoa kabla. Na iambatanishwe na cheti chake cha kuzaliwa. Aliendelea kuwaeleza pia lazima kwenda kwenye ofisi za Msajili wa ndoa ili kujaza fomu ambazo utalipia pesa. Kisha ndipo waombe cheti cha ndoa maalumu kinachoweza kufahamika kimataifa ambacho watalipia pesa zaidi kwa kuwa watajaza fomu tofauti na zile za kuombea cheti cha kawaida cha ndoa.

           Aliwaambia watakapofika pale waombe fomu zinazojulikana kama RGM 111, kwa ajili ya ‘International Certificate of Marriege’. Kwa hiyo akamwambia lazima akienda kwenye ofisi hizo za msajili wa ndoa, awe na copy ya passport yake, na hiyo Certificate of No Imediment,  atakayokuwa ameipata kutoka nchini kwao, na picha mbili za passport size. Kisha unasubiri siku 21 ili kama kuna mtu anakipingamizi chochote aweze kufika na kuweza kuwasiliana na ofisi hizo.

Tunda na Net wakaangaliana. Maana Net aliweka kwenye speaker kwa hiyo Tunda alikuwa akisikiliza. “Mmmh!” Tunda akaguna. “Hakuna jinsi yakufupisha hayo mambo yote?” Net akauliza. “Upo uwezekano wakufupisha hizo siku 21.” Net na Tunda wakajiweka sawa kusikiliza. “Mnaweza kuomba kwenye hizo hizo ofisi, lakini itabidi kulipia zaidi.” “Hamna shida.” Net alijibu kwa haraka sana.

“Okay. Basi mtakapofika pale, muombeSpecial Marriage License’. Mtakapomaliza kujaza hizo fomu na kulipia garama zake, mtapewa cheti chenu, kisha mnaweza kufunga hiyo ndoa popote mnapotaka ambapo Msajili wa ndoa akawafuata mtakapo lakini itabidi kugaramia zaidi. Mtalipia na usafiri wake pia. Na kama mtataka mfungie pale pale, mnaweza kuulizia kwa siku yenu mtakayokuwa mmepanga kama wanaweza kuwafungisha. Lakini mjue itakuwa siku na muda wa kazi.” Yule mwanasheria akaendelea.

“Siku yakufungishwa hiyo ndoa nilazima kuwepo na mashahidi wasiopungua wawili. Haijalishi kama ni wa zawa au sio wazawa wa nchi. Lakini ni lazima kuwepo na hao mashahidi. Baada ya kufunga ndoa, ndipo mtakapo ka bidhiwa vyeti viwili vya ndoa.” Yule mwanasheria akawa amemaliza.

“Sasa na hiyo ‘Certificate of No impediment’  utaipata wapi Net? Hayo sio mambo ya leo wala kesho. Hiyo kitu ishakuwa ngumu.” “Naomba tusikate tamaa mapema Tunda.” Bado yule wakili alikuwa akiwasikiliza.

          “Lakini kila kitu kinawezekana.” Wakamsikia yule mwanasheria akionea. Wote wakatulia. “Mnanisikiliza?” “Tupo.” Net akaitika. “Njooni kesho ofisini, tutazungumza zaidi. Naweza kuwasaidia hata ijumaa mkafunga ndoa.” Hiyo ikawa habari njema sana kwao. Wakaagana kwa makubaliano wakutane kesho yake.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mipango kabambe, inayosukwa kisomi na kwa makini inaendelea. Mpango upi utafanikiwa? Endelea kufuatilia.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment