Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Nilipotea! – Sehemu ya 31 - Naomi Simulizi

Nilipotea! – Sehemu ya 31

 

Jumatatu.

N

et alifika ofisini kwa Tunda kumchukua, wakaelekea mpaka kwenye ofisi ya mwanasheria waliyezungumza naye siku iliyopita. Aliwakaribisha kwa kuchangamka. Akawaambia wakimlipa vizuri atawaandalia kila kitu. Watakachohitajika kupeleka pale ni copy ya passport ya Net, na picha zao, basi. Yeye atawafanyia kila kitu. Hilo nalo likawa jambo jema sana. Wakapanga mipango yao na kuwa ijumaa ndio harusi.

          Net na Tunda walitoka pale wakiwa wamejawa cheko. Hawakuwa wakiamini kile kinachotaka kuwatokea. Kutoka kusubiri siku 21 ndipo waoane mpaka kuweza kufunga ndoa yao ndani ya week! Mungu awape nini! Wakampigia simu mama Penny wakamweleza kila kitu na kumtaka asimwambie mtu yeyote. Tunda alimwambia anamfuata ili wakatafute nguo zao na kina Penny watakao simamia, halafu Net atamtafuta mchungaji wapange mipango yao, lakini ijumaa harusi. Vilijaa vicheko tu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Vipi sasa mama Cote?” Tunda akamuuliza Net. “Huyo nitamtaarifu siku yenyewe ya harusi, nikiwa nimehakikisha wewe upo sehemu ya tukio, na mfungishaji yupo.” “Net!” “Kweli Tunda. Nashindwa kabisa kumuamini mama kwa sasa, hasa katika hili. Lolote laweza kutokea.” “Bibi yako?” “Nana nitamwambia. Na hivi anataka niondoke naye jumamosi, itakuwa sababu nzuri sana. Atajua nipo kwenye honeymoon na mke wangu.” Tunda akacheka, asiamini kama ijumaa atakuwa mke wa Net.

“Siamini Net!” “Mimi mwenyewe siamini! Naona siku zinachelewa. Nawahi kuchukua passport yangu, nikatoe copy, nipige picha nimpelekee leo leo. Naomba na wewe usinicheleweshe Tunda.” “Mimi naona twende tukapige picha, ukae nazo tu. Ukienda kumpelekea hivyo vitu, umpelekee kila kitu kwa pamoja.” Wakakubaliana.

Maandalizi ya Harusi ya

Net & Tunda.

H

iyo week ikajaa hekaheka kweli kwa Net, Tunda, mama Penny na familia yake ili kuweza kukamilisha kila kitu kwa wakati. Mama Penny yeye alikuwa atafute wapambaji, mtu wa vyakula na vinywaji pamoja na keki. Tunda alikuwa na kazi zake za kupamba juma hilo, ambazo alishawakubalia watu, asingeweza kuahirisha tena. Katikati ya juma alimwambia mama Penny atapamba mwenyewe, ila jumamosi ndio kazi zote akamuhamishia mama Penny akijua yeye atakuwa kwenye fungate.

Ikawa tena kuna shuguli nyingine yakutafuta nguo ya harusi itakayompendeza yeye kwanza kama bibi harusi, na wasimamizi wake, ndani ya siku hizo hizo chache. Na juma hilo hilo tena alitakiwa kuhama pale alipokuwa akiishi, kuhamisha baadhi ya vitu vyake kwa mama Penny. Kukajaa heka heka, hata safari ya kwenda kwa shangazi yake ya kuwaringishia Net, na kujua yaliyojiri baada ya kuwatumia picha za fumanizi la mjomba wake ikasaulika.

 

Mama Cote akashangaa haulizwi chochote. Net anafika kazini asubuhi kama kawaida, mchana anatoka kwa lisaa au zaidi, kisha anarudi kazini kama kawaida. Salamu kama kawaida. Hakuna tofauti hata hapakuwa na hasira usoni kwa Net. Ritha alikumbuka maneno makali na kashfa aliyomtupia Net. Akakumbuka ugomvi aliouacha kati yake na Bethy, lakini hakuuliza chochote! Na kitendo cha Tunda kufika kwenye miahadi yao na mama Penny, wazi mama yake alijua Net anajua. ‘Lakini ni nini kinaendelea?’ Mama Cote akaendelea kujiuliza.

Alitegemea Maya kugeuka kisirani mara baada ya kusikiliza akimgombesha kaka yake, lakini akashangaa na yeye ametulia tu. Bibi Cote naye kama vile alivyokuwa akishangaa siku ya ugomvi, kuashiria hakuwa anaelewa maneno yale makali yaliyokuwa yakimtoka Ritha kwa kijana wao, basi akaendelea kujidai kama haelewi chochote na kama amepuuza. Hakuulizia lolote. Akaendelea kuzunguka kwenye sehemu wanazouza vitu vya asili yeye na Maya, wakinunua zawadi. Wakati mwingine Net aliwatoa. Basi pakatulia.

Jumatano.

Bibi Cote kwa Tunda.

N

et alikuwa amemwambia Tunda kuwa bibi yake anataka kuzungumza naye. Siku nzima Tunda hakuwa na raha. Tumbo lilikuwa likimuuma, alishindwa hata kutulia kwa wasiwasi. Alikuwa na kazi ya kupamba ukumbi wa tamasha. Alipamba zaidi ya alivyolipwa kwa wasiwasi. Net alimwambia atamfikisha huyo bibi nyumbani kwake mida ya saa 12 jioni ili awahi kurudi kumchukua kwa kwenda kulala. Tunda aliwahi kurudi nyumbani kwake, ili kupika chakula chakumkaribisha huyo bibi. Mama Penny alikuwa kwenye simu muda wote akimtuliza.

Kama kawaida ya Net, hakuchelewa. Kumi na mbili kamili, anagonga mlango akiwa na bibi yake na Maya. Net alianza kucheka pale Tunda alipofungua mlango. “Sasa unacheka nini bwana? Pisha mlangoni wageni waingie.” “Unaonekana una hali mbaya kweli bibi harusi wangu. Ndoa ipo kweli?” Tunda akacheka na kumsukuma Net pembeni kidogo, akampa mkono Maya, na kumkumbatia. Maya akaingia ndani, akamsogelea bibi Net. “Net aliniambia unajua shikamoo.” Tunda alimwambia bibi Cote na tabasamu la wasiwasi usoni. “Najua.” Akajibu yule bibi wa kizungu kwa kiswahili na kumshtua sana Tunda. “Sasa ukimsema huyo, ujue anasikia.” Net akaongeza na kuingia ndani akawaacha Tunda na bibi yake hapo nje wakishangaana.

“Shikamoo.” Tunda akasalimia. “Marahaba Tunda.” Aliitika vizuri tu, kwa kiswahili chenye lafudhi ya kigeni kisha akaendelea kuzungumza kwa kingereza. “Nina swali kabla hatujaingia ndani.” Moyo wa Tunda ulipasuka. “Huyu bibi anataka kuniuliza nini tena!?” Kwa haraka Tunda akajiuliza huku akimeza mate. “Karibu.” Tunda akajibu kwa upole, na wasiwasi usoni. Akaangalia mlango kama anayetamani Net atoke ili amsaidie kwenye kujibu hilo swali.

“Funga huo mlango vizuri.” Alimwambia Tunda kwa lugha ya kingereza fasaha na chepesi tu. Tunda akafunga na kurudi pale pale alipokuwa amesimama na bibi Cote. “Hataki Net asikie!?” Tunda alizidi kupatwa na wasiwasi.

Alikuwa bibi wa kizungu bila kuchanganya hata kidogo. Alionekana ni mwanamke aliyesoma. Na kwa kuwa hakuwepo Net wala Maya, hakuweka ile sura yake ya utani. Akavaa sura ya kimama, yenye jukumu kwa kijana wake. Hakuwa na umbile kubwa. Alikuwa na mwili wa kiasi unaonekana unafanyiwa juhudi za makusudi, kutunzwa vizuri, japo usoni alionekana umri umeshakwenda, ila ipo neema yakifedha.

“Why Net?” Akauliza swali la moja kwa moja, nakumuacha Tunda ametoa macho. “Umenielewa?” “Ndiyo.” Tunda akajibu kwa upole kama anayetafuta sehemu yakuanzia kujibu swali hilo fupi tu. “Kwa nini iwe Net?” Akarudia swali lake tena, bila maneno mengi. Lakini kwa muonekano wa yule bibi, hakuwa mtu wakudanganyika au kupewa majibu mepesi.

Tunda akabaki ametulia tu kama anayefikiria, akiwa ameinama. “Ninakuuliza hivyo kwa makusudi kwa ile garama anayotaka kulipa Net kwa ajili yako. Wewe unaonekana ni binti mzuri kabisa. Hilo halina swali. Nikiwa na maana kuwa, unaweza kuolewa na mtu yeyote unayemtaka. Najua kwa sehemu pale alipo kwa sasa Gabriel juu yako, lakini umeamua kuolewa na Net. Sasa swali langu nataka kujua, ni kwa nini umemchagua Net, wakati ulishakuwa na mahusiano na Gabriel, na yeye anaonekana bado anakupenda na anakuhitaji?” Bibi Cote akaendelea taratibu tu akimuelewesha Tunda ili ampe majibu yatakayomridhisha.

“Kwa sababu kama ni pesa.” Akatoa kijitabu cha hundi kwenye mkoba aliokuwa amebeba. Tunda aliweza kujua aina ya ule mkoba. Ni wa Gucci ile ya bei kubwa. “Naweza kukulipa bila ya yeyote yule kujua. Nitajie tu kiasi unachotaka, nitakupa bila kukuuliza mara mbili ili umuache Net.” Yule bibi akaendelea, lakini Tunda akabaki kama amepigwa na bumbuwazi. “Na wala usifikiri huu ni mtego. Sikutegi ni kutaka kurahisisha mambo tu.” Yule bibi akaongeza.

 “Labda hujajua pale alipo Net. Hajawahi kuwa na tatizo na yeyote mpaka ulipokuja kwenye maisha yake. Alikuwa ni kijana mwenye furaha na amani na kila mtu mpaka alipotokea Tunda kwenye maisha yake. Ndipo kila kitu cha Net kimebadilika. Sasa hivi hayupo kwenye maelewano na mama yake sababu yako. Sasa kama wewe upo kwa ajili ya pesa tu, naweza kukulipa pesa yeyote unayotaka ili tu, tuachane kwa amani na Net aendelee na maisha yake.” Yule bibi akamkazia macho Tunda.

“Hata mimi natamani ingekuwa ni pesa tu, pengine hata kwangu ingekuwa rahisi.” Tunda akaanza taratibu huku akimtizama bibi Cote. “Kwa sababu ya Net, hata mimi maisha yangu yamebadilika. Sivyo kama nilivyokuwa zamani. Kabla sijaamua kutulia kwa Mungu, hata baada ya kutulia kwa Mungu, Net amebadili maisha yangu. Ile amani na utulivu niliyokuwa nayo siku chache kabla Net hajaja na kuniambia alikuwa ananipenda anataka anioe, imeisha kabisa. Niliweza kurudisha heshima kwenye jamii, na watu wakamtizama Tunda ambaye ametulia kanisani, lakini sasa hivi nalipa garama kubwa sana ambayo hailipiki kwa pesa, kwa kuwa kwenye mahusiano tu na Net.” Tunda akaendelea.

“Nimejitengenezea maadui ambao sikuwa hata nikifikiria kama wanaweza kuwa adui. Mbaya zaidi wanatokea kanisani ambako mimi kumenisaidia kunipa heshima. Na sikuwa nimejiandaa wala sikuwa nimetegemea.” Tunda akacheka kidogo, kisha akaendelea.

“Nilikuwa nikimwambia mtu fulani aliyekuwa akinilalamikia ni kwa nini sikuwa nimemwambia kabla kama yupo mtu kama Net kwenye maisha yangu, nimekuja kumshtukiza tu baada ya Net kutokea! Nikamjibu kuwa hata mimi sikujua kama Net yupo, japo alikuwepo. Nakwambia kweli Ms Cote, siku chache zilizopita, kama ungeniambia kama Net anaweza kunipenda na kutaka niwe mke wake, nisingekubali wala kudhania.”

“Hakika sikuwahi kumfikiria japo nilishaishi naye kwa kipindi fulani, Arusha. Tena tulikuwa karibu sana tu, lakini hata sikujua kama anazo hisia zozote za kimapenzi kwangu na wala mawazo yangu hayakuwahi kumfikiria Net kuja kunipenda niwe mke wake. Hata kama dunia nzima tungebaki mimi na Net tu, pia nisingeweza hata kudhania kama Net, anayenifahamu Tunda mimi angeweza kunichagua na kunitaka niwe mke wake. Bado siamini.” Tunda akaendelea.

“Kipindi Net ananifuata kunitaka nije niwe mke wake, nilikuwa nina kijana ambaye alitaka kunioa kama hivi Net. Yeye naweza kusema anauwezo, sio kama Net ninayesikia kutoka kwa mama yake kuwa anapesa. Naweza kusema yule kijana alikuwa na pesa, zakuzishuhudia. Za Net nazisikia tu kutoka kwenu. Hatuongelei pesa za Net tukiwa naye. Hapa naishi kwa jasho langu. Anyways, turudi kwenye jambo la muhimu. Yule kijana alikuwa akiitwa Julius. Na sio kwamba ni yeye tu aliyetaka kunioa, ila yeye ndiye anayefanana na Gabriel ambaye nimeshawahi kuchezea pesa yake, lakini nilishindwa kusema ndiyo kwao, hata Gabriel kwa sasa nimemwambia hapana, kwa kuwa hawamfahamu Tunda hata kidogo. Ni Net tu ndiye anayenifahamu. Angalia kiganja chako cha mkono.” Tunda alimwambia bibi Cote.

Yule bibi akaangalia. “Huo mkono unapokuwa mchafu si unauosha?” Tunda akamuuliza bibi Cote, kimya. “Unapokuwa mkavu si unaupaka mafuta?” Tunda akamuuliza tena. “Kwani huo mkono huwa unaongea na wewe mpaka unaufanyia hayo yote?” Kimya. “Jibu ni hapana. Uwe umechafuka kwa bahati mbaya au makusudi, huwa unauosha. Uwe mkavu wakati wa baridi au joto. Usiku au mchana, huwa unajua na kuupaka mafuta zaidi ya mara moja na huwa huchoki wala hakuna mahali unakolalamikia jinsi unavyouhangaikia huo mkono na kutamani ukatwe.” Tunda akaendelea.

“Hivyo ndivyo Tunda huyu aliyesimama na wewe hapa, ndivyo nilivyo mkono kwa Net. Ananifahamu, ananisafisha na hajawahi kuchoka kuyasaka yale mazuri yaliyopo ndani yangu na kuyatoa nje yale ambayo hakuna mwanadamu ambaye amewahi kuyaona, hata mama yangu mzazi alishindwa, ila Net ameweza. Kwa kunisifia, na kunihimiza niyaishi. Sijawahi kuwa mchafu kwa Net kiasi chakushindwa kunisafisha.” Tunda akaanza kutokwa na machozi.

“Gabriel alishakuwa na mahusiano na Nancy, aliyekuwa akiishi hapa, akitumia huu mwili wangu kama mpenzi wake. Tunda ambaye alijigeuza Nancy alimtumikia Gabriel mchana na usiku bila kuchoka, lakini Gabriel alimuacha Nancy akiwa anamlilia hana pakwenda. Ilikuwa usiku. Mvua ikimnyeshea. Net. Nathaniel Cote..” Tunda akakwama kwa muda. Akajaribu kutulia. Akafuta machozi mbele ya yule bibi.

“Usiku ule, nikiwa nimeachwa peke yangu. Pengine kila mtu angefurahia kupatwa na kile kilichokuwa kikinipata kwa wakati ule. Wakifurahia nisulubishwe kwa maisha mabaya niliyokuwa nikiishi wakati ule. Lakini Net hakunihukumu. Alimchukua Nancy, akijua wazi yupo Tunda ndani ya huyo Nancy, akamhifadhi usiku ule, akanilisha, akanilipia madeni ya wakati ule, akanipeleka kanisani. Alihakikisha kila aina ya Nancy, na wengine ndani yangu, wanaondoka ili tu, Tunda aliyemjua Net, ambaye hata mimi sikujua kama Tunda anaweza kuwa hivi, ila Net. Alihakikisha anawatoa kina Nancy wote, na kumbakiza Tunda huyu.” Tunda akaendelea.

“Mwanamke anayemtaka sasa hivi Gabriel, hayupo. Mungu alimtoa na kumbakisha Tunda mbaye ni Net tu anamfahamu na kumjua, na bado anampenda. Kwa mwanaume yeyote yule anayekuja sasa hivi, akimtaka Tunda, halafu akaja kujua habari za kina Nancy ambao walishaishi zamani kwenye mwili wa Tunda, hakuna anayeweza kunitizama kama Net, Ms Cote. HAKUNA. Nalijua hilo kwa hakika kwani hata Julius alipojua historia yangu ya nyuma, alishindwa kunitizama kama zamani, ila Net.”

“Nimekula na kuichezea pesa ya Gabriel kuliko Net. Ila sijawahi kulala usingizi mzuri, kama ninaoupata sasa hivi ambapo nipo na Net, nikifanya kazi kwa bidii kujiingizia kipato kwa jasho langu. Na ndio maana kwa sasa hivi ambapo Mungu amenipa uwezo wakutengeneza pesa mimi mwenyewe, hata sihitaji pesa ya Net. Net alinisaidia kunitoa kwenye madeni, akanipa akili ya kuzitafuta pesa. Sasa hivi sina shida na pesa yako, wala pesa ya mama yake, au hata yeye Net mwenyewe. Isipokuwa Net mwenyewe. Mimi namtaka Net.” Tunda akaendelea taratibu tu kama kawaida yake.

“Nitakudanganya nikikwambia eti habari za Net kuwa na pesa nyingi eti sio habari njema kwangu. Nitakudanganya. Nimeishi kwenye shida, na ni kweli nimejiapia sitaolewa na mwanaume ambaye hana pesa au akili ya maendeleo, labda awe Net. Net atanioa hata kama ni masikini ila mapenzi yatanitosha. Nitakuwa radhi hata kumuweka ndani nimlishe kama mtoto mdogo, lakini sio mwanaume mwingine. Nimeteseka sana maishani. Sitaki kuja kuanza kupata tena shida nikiwa na umri huu. Hapana. Sitaki kurudi nyuma labda na Net. Sasa nikisikia kuwa anazo pesa, nafurahia naona ni kweli Mungu amekusudia kunipumzisha.” Tunda akamuona yule bibi anatabasamu.

“Net ameniambia umenitayarishia chakula cha kitanzania. Naona nipo tayari kula.” Tunda akacheka huku anavuta pumzi kwa nguvu mpaka akainama kwa kushika magoti yake. Hata yeye hakujua ni wapi aliupata ule ujasiri wakuzungumza na yule bibi. Tena kwa kingereza kizuri tu. Akamsikia yule bibi anacheka. Akajua anacheka vile alivyofanya mbele yake bila kutarajia. Tunda akasimama na kumwangalia na tabasamu la ushindi. “Karibu ndani.” Tunda akamkaribisha na kumfungulia mlango, wakaingia.

 

Kwa muonekano wa bibi yake tu, akajua mambo yalienda vizuri na amempenda Tunda. Hakuna aliyeondoka. Wote walikaa jioni hiyo hapo kwa Tunda, vicheko vikaanza. Ile sura ya yule bibi alipokuwa na Tunda nje, sio hii aliyokuwa nayo alipokuwa na Net pamoja na Maya, hapo ndani. Tunda akaamini ni kweli anawapenda na kuwadekeza hao watoto.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wasiwasi ulikuwa umemwingia huyo bibi baada yakugundua ugomvi mkubwa uliokuwepo kati ya Net na mama yake. Japokuwa alimfahamu Ritha, lakini hakutaka kumpuuza. Akaona na yeye apate muda na Tunda kabla hajaolewa na Net na kuingia kwenye familia yake. Kwa kuwa yule bibi alikuwa msomi, na kazi zake nyingi anakutana na watu aina tofauti tofauti.

Alijua kwa kukaa na Tunda kwa muda mfupi tu, atamjua kama ni mkweli au la. Na kweli, kwa muda mfupi sana aliozungumza na Tunda, akajua moyo wake. Si kwa yale tu maneno, lakini aliweza kusoma mpaka moyo wake. Hiyo nayo ni karama yake ambayo Mungu alimjalia huyo bibi na kufanikiwa kufanya anachokifanya huko kwao na ulimwenguni.

 

Alhamisi.

Tunda kwa baba yake.

S

iku ya alhamis Tunda akaamua kwenda kwa baba yake kabla ya siku ya harusi. Alishatoka hospitalini. Alilazwa siku tatu tu, akarudishwa gerezani. Ilibidi kuomba kibali maalumu kumuona kwani haikuwa siku ya kutembelea wafungwa. Alikwenda na mwanasheria wake akamsaidia kumuombea, alipofanikiwa, yeye akaondoka na kumuacha Tunda akimsubiria baba yake hapo.

“Unajisikiaje?” “Nashukuru angalau. Japo bado mwili hauna nguvu. Kuna dawa bado natumia.” “Pole  baba.” “Asante. Nakushukuru sana Tunda mwanangu. Naona mwanasheria uliyenitafutia anahangaika kweli! Najua inakugarimu.” “Nahangaika utoke baba. Hata yeye anasema anaona atafanikiwa. Ameanza upelelezi wa chinichini, anasema ameshapata watu wawili ambao walimwambia ni mpango walikufanyia pale ofisini ili utolewe. Wanasema walipokuwa wakitaka upitishe malipo yao kama ni ya uongo, ulikuwa ukiwakatalia ndio maana walikubambikizia receipt ya uongo, wao wakala pesa, uonekane wewe ndio uliiba. Sasa anasema anataka kumtega mmoja wao. Amrikodi, ndipo awapelekee wale wenye kampuni wajue ubaya wa wafanyakazi wao. Na anasema wakikubali kufuta tu kesi, anafungua ya madai ili ulipwe fidia zote.”

“Ameniambia na mimi hivyo hivyo. Ila amenisisitiza wakinilipa na kuniomba nirudi kazini, nisikubali.” Tunda akashangaa kidogo. “Kwa nini tena?” “Anasema hakuna mtu anafuraia kuingia hasara. Kwa kunilipa mimi fidia, nikuwaingiza wao hasara. Sasa kuja kurudi tena pale, wanaweza kunitega kokote. Amenishauri nianze kufikiria kujiajiri.” Baba Chale yaani baba yake Tunda akacheka kidogo kama anayefikiria.

“Nini?” Tunda akamuuliza. “Anajiamini huyo! Anasema hajawahi kushindwa kesi. Kwa hiyo anasisitiza niendelee kufikiria biashara yakufanya, pesa inakuja.” Tunda akacheka kidogo. “Kuwa na imani baba.” “Aaaha!” “Nini? Usikate tamaa.” “Tusubiri tuone.” Akajibu kama anayefikiria. “Najuta kuacha kazi wizarani nakuhamia kampuni ya watu binafsi. Najuta mengi tu.” “Pole baba. Naamini kila kitu kitakuwa sawa. Anza kufikiria chakufanya baada ya kutoka hapa.” Wakatulia kidogo.

“Naolewa kesho.” “Net ameniambia. Mbona huna furaha sasa?” Baba yake akamuuliza. “Kwanza wameshakulipa mahari?”  Baba yake akaanza kucheka. “Au umesamehe mahari?” “Huko kukupenda tu ni mahari tosha. Ningepata wapi mtu wa kukupenda hivyo? Nimemwambia ahakikishe tu anakuheshimu.” Tunda akajifuta machozi. “Net ananipenda sana, baba.” “Sasa tatizo liko wapi!?” Baba yake akamuuliza.

“Kuna kitu nilikuwa sijakwambia baba na hata Net siku ya kwanza kuja naye hapa aligusia, lakini najua hukuwa umeelewa vizuri.” “Juu ya nini tena?” Baba yake akauliza. “Kipindi kile uliponiacha hospitalini nikiwa mgonjwa, ndio wakakufunga. Nikatoka lakini nikashindwa kuja kukuona, ni kwa kuwa nilikuwa nakuogopa.” Baba yake akakunja uso.

“Kwa nini!?” “Nilikuwa nikiishi maisha mabaya sana. Nilijua ungeniona tu, na vile nilivyokuwa nimefanikiwa, ungeniuliza maswali ambayo ningeshindwa kukujibu, na mimi sikutaka kukudanganya.” Baba yake kimya. Akainama kama anayefikiria. “Niliishi maisha machafu sana baba. Nilionekana nimefanikiwa kwa nje, lakini hayakuwa maisha mazuri mpaka Net aliponitoa huko nakunipeleka kanisani. Huko nako nikapona roho, lakini imekua ndio chanzo cha matatizo yangu.” Baba yake akawa haelewi.

“Kanisani tena!?”  Akamuuliza. “Ilibidi kutubu dhambi zangu. Nilikuwa na mashetani ambayo mengine yaliongea uchafu waliokuwa wakinitumia niufanye, mengine nilikiri mwenyewe. Nilikuwa nimefika mwisho baba. Nilikuwa nimechoka. Nikajua nimepata sehemu yakutoa matatizo yangu. Lakini hata Net aliniambia pale ni sehemu sahihi naweza kuongea chochote. Sasa kama nilivyokwambia. Nilikuwa nimefika mwisho, nataka kupumzika. Na kama unavyojua, uliniacha peke yangu nikiwa nimefungiwa milango na ndugu wote. Nikajikuta nakiri kila kitu.” “Hukukosea Tunda. Ulifanya vizuri kukiri kanisani. Si ndio umepata msaada sasa? Nakupongeza.” Baba yake alijaribu kumsifia.

“Na mimi ndivyo nilivyofikiria baba. Lakini imekuwa tofauti. Badala yake nimekuwa ni kama nimetengeneza mwiba wakunichoma. Moja ya wanaume niliokwisha kuwa na mahusiano nao, alitaka kumuoa mama yake Net.” Baba yake alishtuka mpaka Tunda akamuona. Tunda akainama. “Net anafahamu hilo!?” “Anafahamu baba. Na mwingine alikuwa rafiki kipenzi, kama ndugu kwa Net.” Tunda akaendelea huku anafuta machozi.

“Siku nimeenda kukiri pale kanisani, huyo baba aliyekuwa amuoe mama yake Net, alikuwepo na mama yake Net alikuwepo. Net hakuwa akijua kama mama yake alitaka kuolewa na yule mzee. Na mimi nilipaniki nilipomkuta yule mzee pale ofisini kwa mchungaji. Kwa kuwa nilitaka kuanza maisha mapya, Net akaniambia amenipeleka pale kwa watu wacha Mungu, nafika pale nakutana na yule Mzee, nilipaniki sana. Mbele yao, nikapaniki. Nikamwambia Net mbona anataka kunirudisha kule kule kubaya? Mimi sikujua kama yule mzee ni wa kanisani. Maana alishawahi kunilipa mara mbili japo kanisani alisema ni mara moja tu. Basi, ndio uadui umeanza. Mama yake Net hanitaki kabisa.” “Na Net mwenyewe!?” Baba yake akiwa kwenye mshangao, akauliza.

“Huna utakachomwambia Net juu yangu, mbali ya kunioa mkaelewana baba. Na hivi ninavyokwambia sio kwamba alisikia siku nakiri kanisani! Alishanifumania zaidi ya mara tatu. Hata huyo rafiki yake, anaitwa Gabriel, alishanifumania naye. Mimi mwenyewe sikuwahi kujua kama Net anaweza kuja kunifikiria mimi kama mwanamke wakuoa.” Yule baba alivuta pumzi kwa nguvu, akatulia kidogo.

“Utafanyaje?” Mwishowe akamuuliza. “Sijui baba. Ila ninachojua kesho naolewa naye. Japo ni kwenye mazingira hatarishi sana. Mama yake anatafuta kila mbinu yakuniangamiza. Hataki hata kuniona, na ametengeneza watu ambao wanatugeuka. Huyo Gabriel, amemgeka Net, anamtisha kuwa asinioe kwa kuwa mimi ni mwanamke wake na bado ananipenda ni kama amempokonya mkewe.” Tunda alimuelezea baba yake kila kitu bila kumfisha mpaka maswala ya nyumba.

Alimuacha baba yake haelewi huyo Net anatakaje bado kumuoa binti yake. Tunda aliondoka akiwa amempa baba yake habari chungu na tamu. Tamu kwa kuwa anajua Net anampenda kwa dhati. Chungu akiwaza mwisho wake ni nini!? Maana anaingia kwenye ndoa akiwa na vita na mwanamke mwenye jina kubwa na pesa hapo nchini. Mbaya zaidi, ni mama yake Net, na ndiye anayemuweka Net mjini

Ijumaa.

Harusi ya Net na Tunda.

S

iku hiyo Tunda aliamkia saluni akiwa na mama Penny pamoja na watoto wake. Mama yake alifika hapo saluni akitokea hotelini akiwa na Aneti. Wote Tunda alitaka watengenezwe. Tunda mpenda nywele, alishashonewa nywele nzuri sana siku iliyopita kabla ya kwenda kwa baba yake. Siku hiyo ilikuwa kupambwa tu, na ile nywele kutengenezwa muundo wa kuweza kubeba shela na maua. Net, mchungaji na Tom walikuwa saluni yao. Kulikuwa na hekaheka wakitaka kumaliza mapema, ili harusi ifungwe mapema kabla ya giza kuingia. Bibi Cote alikuwa akiondoka kesho yake, yeye na Maya kurudi nchini Canada.

Mama Penny na baadhi ya vijana wa pale kanisani, walishapamba nje ya nyumba ya Net, ambako kwa wakati huo kisheria ilikuwa nyumbani kwa Tunda. Hawakutaka kufunga hiyo ndoa kokote ila hapo. Mama Penny alikuwa ameshamsaidia Net kutafuta wapishi wazuri na waliahidi kuja na vinywaji. Na akawataka wafike hapo mapema tu. Wakakubaliana na mama Penny. Net alishamkabidhi mama Penny pesa yote bila maswali. Akabaki mama Penny kufanya mipango yote. Yeye peke yake akipiga simu huku na kule. Mpaka inafika ijumaa, mama Penny akiwa saluni bado alikuwa kwenye simu akihakikisha jambo haliharibiki. Alitulia mida ya saa 9 mchana wakiwa bado wapo saluni, alipopata simu kuwa watu wa chakula, vinywaji, Dj na keki wameshafika nyumbani kwa Tunda na Net.

Hapo mama Penny akawa amebakisha kumpelekea Net mke tu. Na Net naye akawa ametulia kuona kila kitu kinaenda sawa mpaka muda huo. Na yule mwanasheria aliwahakikishia kila kitu kitakuwa sawa, wakalipia garama zote za mtu wakufika pale kufungisha hiyo ndoa yao. Na kweli na yeye akafika kwa wakati.

Kama kawaida Tunda hakujikosea. Alivaa shela nyeupee, kama asiyemjua mwanaume. Akatengenezwa vizuri, na ile rangi yake ya weusi, usingechoka kupiga vigelegele. Japokuwa walikuwa wachache lakini palitengenezwa kupendezea wachache hao. Hakutaka kuhusisha watu wa kanisani kabisa. Wao walikuwa wachungaji, halafu ndoa inafanyika nyumbani na ni ya serikali! Wanawaambiaje watu? Hata hivyo walifanya kwa kuwa ni Tunda. Na alishamwingia mama Penny mpaka rohoni.

Mama Penny alimuona Tunda kama mdogo wake wakuzaliwa na rafiki haswa. Penny hakuacha kujisifia. Furaha yake ilitimia pale alipoambiwa ataanza kuingia yeye na mdogo wake pamoja na Aneti. “Wataniona mimi kabla ya aunt Tunda.” Hakuacha kujisifia.

Net, Tom na Mchungaji walishafika hapo kutokea saluni. Bibi Cote na Maya walikuwepo hapo nyumbani kwa Net mapema tu. Wakati Tunda anakaribia na hapo nyumbani ndipo Net akampigia simu mama yake kumtaka afike nyumbani kwake. Akiwa na mshangao kwani hawakuwa wakizungumza mbali ya salamu. Akakubali kufika. Lakini akitaka kujua kuna nini na kama ni mazungumzo kwa nini wasizungumzie tu ofisini, Net akamwambia anamuomba afike nyumbani kwake, hatamuweka muda mrefu.

          Gari hiyo ya Limousine iliyokuwa imembeba bibi harusi na wasimamizi wake pamoja na mama yake Tunda, iliwasili nyumbani hapo saa 10 kamili jioni. Net alimpigia simu mama Penny akimuomba wasubiri kwenye gari mpaka atakapowaambia washuke. Mama Penny akashangaa ni kwa nini wasubiri nje!

Mama Cote alifika nyumbani kwa Net bila kuchelewa. Akashangaa kukuta shamrashamra na nyimbo za taratibu zikipigwa na pameandaliwa kama kwenye sherehe. Net akamfuata pale alipoegesha gari. “Ni nini kinaendelea?” “Tunaweza kuzungumza pale kwenye meza aliyokaa bibi?” “No.” Yule mama alikataa bila kupepesa macho. “Niambie ni nini kinaendelea Net?” “Leo, namuoa Tunda.” Mama Cote alibaki akimtizama mwanae kwa sekunde kadhaa bila kujibu kitu.

“Nampenda Tunda, mama. Na nilikwambia lazima nimuoe.” “Kwa shida zote nilizopata na wewe Net, leo, sasa hivi ndio unaniambia unaoa!? Unaniambia kama mpitaji tu? Unanitoa ofisini kuja kwenye harusi yako!?” Net alimuona vile mama yake alivyobadilika. Alipandisha hasira mpaka midomo ilikuwa inacheza.

Ritha amtangazia Vita iliyo ramsi Mwanae, Siku ya harusi yake.

“Unanidharau mimi Net!? Unapanga mipango yako na bibi yako mimi nakuwa kama mtu wa kando tu?” “Naomba utulie mama. Hii mipango nimepanga mimi mwenyewe. Bibi hausiki.” “Na yeye bibi yako umetoka kumpigia simu sasa hivi?” Mama yake akauliza akionekana amekasirika kupita kiasi.

“Mama!” Net alitaka kumshika, mama Cote akarudi nyuma. “Niambie ukweli Net. Na yeye bibi yako ndio anajua leo kama unamuoa Tunda, mwanamke malaya huyo, aliyetembea na kama baba yako na kaka yako pia!?” “Anajua mama. Maya alikusikia ukiwa unagomba siku ile. Tuliposhindwa kumjibu ni nini tunaongea, akaja kumuuliza Maya kesho yake, ndipo Maya akamwambia kile alichokusikia ukisema. Akaja kuniuliza kama ni kweli juu ya Tunda. Ni kamwambia ni kweli.” “Kwa hiyo yeye anaona ni sawa umuoe malaya yule!?” Mama Cote akauliza.

“Kwanza nakusihi mama yangu, usimtukane Tunda. Masaa machache sana, anakuwa mke wangu, yaani mwili mmoja na mimi. Pili, Nana anaamini kwenye kukosa na kusamehewa dhambi. Nakuomba..” “Kwa hiki ulichonifanyia leo, ni kunikana hadharani mbele za watu. Umemchagua Tunda, dhidi yangu. Umemthamini bibi yako anayekupa mali zao, umenidharau mimi mama yako niliyekubeba tumboni miezi 9, na kukunyonyesha.” “Mama!” Net akaishiwa nguvu.

“Sasa kuanzia leo, utakapofanyika mwili mmoja na Tunda tu, sahau kabisa kama mimi ni mama yako. Nisikuone nyumbani kwangu wala ofisini.” “Mama Please!” Net alishakuwa mwekundu akatamani kulia. “Sikutanii Net. Ukimuoa tu Tunda. Leo au kesho, ujue wazi wewe sio mtoto wangu tena. Usiwahi kuja kuniita mama tena maishani. Hata ukisikia mimi nimekufa leo, usije kwenye mazishi yangu. Usisogee kwenye chochote nilichokitafuta kwa jasho langu. Wewe sio mwajiriwa wangu.” Ritha alikuwa akitetemeka kwa hasira. Akaendelea.

“Yaani kwa kifupi nataka ujue, tokea siku ulipouza mali ya kampuni yangu kwa Tunda, yaani hii nyumba, ulijifukuzisha kazi, na ujue wazi, umefanya kosa kisheria.” “Hii nyumba ni yangu mama. Nipo huru kufanya ninachotaka.” Net alimshangaa mama yake.

“Ilikuwa kwa jina gani?” Mama yake akamuuliza huku amemtolea macho. “Cote LTD kwa kuwa..” “Exactly! Ilikuwa chini yangu. Mali yangu kisheria, wewe ni mfanyakazi wangu. Umeuza mali ya kampuni kwa mwanamke wako. Wewe ni mwizi. Nimekuleta nchini kama mfanyakazi, umeniibia. Ujue ninapoondoka hapa, nakwenda kukushitaki kwa watu wa usalama na uhamiaji. Kitakachokupata, ndipo utajua mimi ni nani! Na ukumbuke nilikuonya. Usinijaribu. Kama unadhani nakutania, muoe huyo malaya.”

 “Mama! Nimejenga hii nyumba kwa pesa yangu, ni jasho langu!” Bibi Cote akasogea. “Kuna nini?” Bibi Cote akauliza. “Na umwambie bibi yako, kuanzia leo, asinitafute tena, na jina lenu namwachia Tunda. Nitabadilisha jina la kampuni yangu nirudishe la baba yangu. Mwambie mtoto wake hakuniokota. Alinikuta Canada sababu baba yangu alinilipia pesa yakuishi huko. Mizigo yake yote itamfuata hapa kwenye hii nyumba mliyoniibia. Na umwambie Maya, ana siku ya leo tu kuchagua. Awe mtoto wangu, au anikane kama wewe utakavyonikana leo, endapo utamuoa Tunda. Uamuzi ni wako. Tunda au mimi.” Mama Cote akamalizia kwa lugha ya kiswahili, akapanda gari yake, akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Net maji yamezidi unga. Anamwaga ili asonge ugali? Usikose mwendelezo. Vita yake ndio inaanza rasmi endapo anamuoa Tunda. Usikose muendelezo kujua kama ameamua kusuka au kunyoa! Kama Tunda alivyompokonya ndoa yake kwa kutembea na mwanaume wake, ndivyo anavyotaka kumpokonya na yeye ndoa. Yupo garini, ameshapambwa, anasubiri harusi. Je, ndoa ipo? Usipitwe.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment