Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA! - SEHEMU YA 1. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA! - SEHEMU YA 1.

 

Kila mtu alimfahamu kwa unadhifu wake. Mavazi mazuri, vile alivyojibeba na kujithamini. Hakuna kitu kingekuwa mwilini mwake kisivutie machoni kwa yeyote aliyebahatika kumuona. Kuanzia aina za nguo, viatu, hereni zinazokuwa zikiendana na aina ya nywele anazokuwa akitengeneza kichwani kwake. Inavutia zaidi jinsi anavyoweza kubadili muundo wa hizo nywele kila wakati kutegemeana na nguo anayokuwa anavaa siku hiyo. Aina ya simu anazobadili, unaweza kusema ni mfanyabiashara aliyefaniki sana. Kila toleo jipya ya aina ya simu za Iphone zinazotoka, basi Naya alikuwa nayo. Aina ya begi alilokuwa akibebea laptop yake ya Mac, ambazo nazo hizo begi pia alibadilisha mara kwa mara kutokana na nguo anayovaa siku hiyo kuingia kwenye kipindi hapo chuoni, nayo iliendana na mavazi yake. Akipita sehemu, lazima utajua Naya amepita pia kwa aina ya manukato yake yaliyotulia lakini pia kudumu kwa muda. Ukweli Naya alikuwa nadhifu kama mwanamitindo wa nchi za walioendelea.

Aina ya mahusiano ya kimapenzi aliyokuwa nayo yalimfanya kujikuta akiishi kwa kukwepa watu zaidi wasichana waliodhani ni maringo wasijue kinachomkabili mrembo huyo aliyejaliwa na urefu wa kike uliomfanya avutie kwenye kila aina ya mavazi anayoweka mwilini. Usingemkuta Naya akisalimia wala kumtizama mtu. Hakujulikana ni wapi analala. Chuoni au nje ya chuo kwa mpenzi wake. Wanachuo karibu wote walishamfahamu na wengine kumjua mmiliki wa gari iliyokuwa ikimshusha Naya hapo chuoni. Alikuwa kijana wa hapohapo jijini Morogoro. Alijulikana kwa pesa, hata aina hiyo ya gari iliyokuwa ikimfuata na kumrudiaha Naya ilitangaza utajiri wa Malon. Ilikuwa nzuri na ya thamani sana. Kubwa, SUV ya silver iliyovimba vizuri na kuzungushiwa vioo vyeusi. Akishuka Naya ndani ya hiyo gari, ungesema ni mwanamtindo maarufu kutoka nchini Marekani, Los Angelas.

Kila mtu alikuwa akitamani kumuona anaposhuka garini akiwa anarudi chuoni. Mwendo wake akiwa anatokea kwenye hiyo gari kuelekea chumbani kwake au darasani kuhudhuria vipindi, ungependa kuwepo na kumtizama.

Hakuwa akikosa kipindi hata kimoja kitu kilichowashangaza wengi. Nidhamu ya shule ilikuwepo kwa hali ya juu. Alichukua chumba na wasichana wengine wawili hapohapo chuoni Mzumbe na kukitumia mara chache sana, zaidi kuweka madaftari yake na baadhi ya vitu vyake vichache. Kilikuwa chumba cha watu watatu tu na yeye akiwemo humo.

Wenzake walio bahatika kuwa na Naya chumba kimoja, wao walisema huwa anawasalimia. Na endapo ni zamu yake ya usafi, alikuwa na mtu ambaye alimlipa kumfanyia usafi, msichana aliyekuwa akitokea mtaani na kuja hapo kwenye hosteli zao. Basi atafanya majukumu ya Naya yote, ndipo anaondoka na yeye.

Usingemkuta akibishana au kugombana na mtu. Kwanza hakuwa na huo muda. Mambo yake aliyafanya kwa utulivu na hakuwa na muda na mtu yeyote isipokuwa salamu tu au jambo lihusulo masomo awapo darasani na wenzie, basi. Akawa hivyo tokea anafika hapo mwaka wa kwanza. Naya akawa gumzo kwenye chuo hicho cha Mzumbe. Alikuwa akisomea mambo ya masoko. Markerting. Watu waliokuwa wakitaniwa ni wauza sura. Basi hilo jina likaendana kabisa na Naya.

Bila kufungua mdomo, alilipa kumtizama. Na ungetaka kumsogelea kununua chochote anachotaka kukuuzia. Lakini napo ilikuwa shida kuisikia sauti yake. Hakujibu swali wala kuuliza swali darasani. Atatulia kwenye kiti chake kuanzia anaingia mpaka anatoka labda wapangiwe kazi yakufanya kama kundi nakutakiwa kuiwakilisha mbele ya wenzao darasani, hapo atatoa ushirikiano wote na akitoa mchango wake ndipo utajua si mjinga kwenye masomo, anao uelewa mkubwa sana kwa kilichowapeleka hapo chuoni.

Muhula wa kwanza alikuwa anachumba, lakini kila siku jioni alikuwa anakuja kuchukuliwa na kurudishwa asubuhi. Hakuwa akichukua mkopo wa serikali. Alijilipia ada yeye mwenyewe. Japokuwa Malon mpenzi wake alishajulikana hapo chuoni hata kwa wasio wazawa wa huo mji kasoro bahari, Morogoro, lakini wengine walijua lazima Naya mwenyewe pia atakuwa mtoto wa milionea mmoja mkubwa sana huko jijini Dar. Hakuonekana kama msichana aliyezikuta pesa kwa Malon. Alionekana kama aliyezaliwa kwenye pesa, na kukulia kwenye pesa ndipo akakutana na huyo mwenye pesa, Malon. Ikawa kukisia kwingi na kubashiri kwa hali ya juu. Lakini hakuna aliyejua ukweli juu ya Naya kwa kuwa hakutengeneza rafiki hata mmoja hapo chuoni.

Muhula huo wa kwanza kwa mwaka wa kwanza ukaendelea kila mtu akitamani ukaribu naye na kumfahamu kwa karibu. Lakini akajitahidi kujitenga haswa. Wakatafuta kujua maendeleo yake darasani. Ikabidi kumfuatilia hata kujua alama anazopata kama zinaendana na muonekano wake. Lakini wakaja gundua ni msichana aliyekuwa akifanya kawaida. Hakuwa akipata alama za juu sana, lakini pia hakuwa akifeli.

Mwisho wa muhula wa kwanza, alipotoka kwenye mtihani wake wa mwisho, hata hakukaa hapo chuoni. Gari lilelile lililokuwa likija kumchukua kila siku chuoni, lilikuwa likimsubiria nje ya hosteli yao. Alitoka kwenye mitihani, akachukua baadhi ya vitu vyake, na kuchukua baadhi ya vitu vyake, nakuondoka hapo chuoni. Baadhi ya watu walimsikia akizungumza kwenye simu akisema, “Sio jumamosi hii. Ni ile ingine ndio tutakwenda.” Kimya kwa muda. “Siku 8 tu ndio Dubai.” Alisikika tu hivyo wakati anatoka hapo kwenye chumba chao, akiondoka bila yakumuaga mtu. 

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

 Muhula wa pili watu walianza kuingia hosteli kuanzia siku ya ijumaa. Wengine jumamosi. Hakuna aliyemtegemea Naya mpaka jumatatu siku ya darasani. Lakini chakushangaza, jumapili asubuhi Naya aliingia hapo chuoni na masanduku ya maana matupu akionyesha ni kama anahamia kwenye chumba chake ramsi. Alishushwa na taksii.

Dereva alimsaidia kuingiza mizigo yote ndani. Kuanzia masanduku makubwa mpaka madogo, yalikuwa ya thamani sana. Walioshuhudia akiingia, walisimama kukodoa macho.  Hakugusa chochote kwani wakati wote alikuwa na kucha ndefu na nadhifu. Pengine alihofia kuvunja kucha zake! Lakini dereva taksii alimsaidia kumshushia vitu vyake vyote na kumwingizia mpaka ndani chumbani kwao, Naya akimwelekeza.

Maisha ya muhula wa pili yakaanza watu wakishangaa harudi tena nyumbani wala haji kuchukuliwa jioni. Mpaka siku ya ijumaa gari lilelile lilirudi tena hapo chuoni. Walimuona Naya ametoka. Badala yakupanda, walimuona amesimama upande wa dereva. Akaonekana akizungumza kidogo na dereva, kisha Naya akaondoka. Lile gari lilisimama hapo kama nusu saa mbeleni, baadaye likaondoka bila Naya.

Naya alikaa hapo chuoni mpaka jumapili tena asubuhi. Gari ileile ikasimama pale pale. Safari hii akashuka kaka mtanashati haswa. Watu wakaanza kuitana. Kwa mara ya kwanza kushuka mtu. Kijana mzuri na alioonekana hata mambo yake ni mazuri. Misuli iliyovuta macho ya wadada zaidi na kuzidi kuitana mpaka madirishani. “Ndiye  atakuwa huyo Malon bwana wake Naya!” “Mimi namjua Malon, ndiye huyo.” Mwingine akaongeza kishabiki. “Anakuja. Tuondokeni.” “Kwa nini? Tusubirini tuone.” Mwingine akawakataza wenzie waliokuwa wamesimama nje ya hosteli nyingine.

“Habari zenu?” Akasalimia yule kijana aliyeshuka kwenye gari. “Salama tu. Karibu.” “Namuulizia Naya. Sijui mnamfahamu?” “Chumba chao ni jengo lile pale nyuma ya ulipoegesha gari yako. Chumba cha pili kulia ukiingia tu.” “Asante.” Akaondoka na kuacha manukano mazuri pale. “Ooooh! Atakuwa bwana ake. Ndio maana Naya ananyodo!” Wakaanza kumteta wakati Malon akiondoka kuelekea alipoelekezwa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Hodi ilisikika kwenye chumba cha kina Naya na wenzake. Wote walikuwa wamejilaza kitandani mida hiyo. Naya ndio alikuwa amelala kabisa. Mmoja wao akasimama kwenda kufungua mlango. “Karibu.” “Asante. Namuulizia Naya.” “Yule pale amelala.” Malon akapitiliza na kwenda kusimama kwenye kitanda alichokuwa amelala Naya. Ilikuwa double decker. Naya alichukua kitanda cha juu. Hayo matandiko tu, ungependa kugusa. Mazuri ya Chuichui safi lakini rangi ya dhahabu ilipendeza na kuvutia haswa. Silk nzuri Ungependa kutizama. Hata foronya za mito ilikuwa silk ya dhahabu yenye chui chui pia.

“Naya!” Aliita Malon akiwa amesimama pembeni ya kitanda alichokuwa amelala Naya. “Malo!” Akashtuka Naya alipomuona mgeni wake. “Vipi?” Malon akauliza. “Nilikuwa nimelala.” “Mzima lakini?” “Mzima. Nilikuwa nasoma, nikapitiwa na usingizi.” “Naomba twende.” “Hapana Malo.” Naya akakataa taratibu.

“Unataka nikwambie nini ujue nimekosa na kujutia?” “Leo ni jumapili Malo. Kesho nina vipindi kuanzia asubuhi. Siwezi kuondoka leo.” “Nitakurudisha usiku. Mimi mwenyewe.” Kimya. “Naya!” Kimya. “Si unajua leo sitaondoka hapa bila wewe?” “Naomba muda Malo.” Wenzake Naya wakasikia akijibu.

“Mpaka lini? Nimekuacha muda wote huo, bado unataka muda! Naomba twende tukazungumze.” “Nitakuja ijumaa.” “Hapana. Nataka twende sasa hivi.” Malon akasikika akiamrisha, sio kuomba tena. Naya akakunja uso kwa kumshangaa kidogo. Alipoona sura ya Malon inazidi kubadilika, akaanza kukusanya vitu vyake taratibu. Akashuka hapo kitandani. Wazi ni kama amelazimika. Akafungia vitu vyake vyote kwenye upande wake wa kabati au loka, akatoka bila kuaga. Malo akamfuata nyuma kimya kimya.

“Kwa nini unafanya ubabe wakati umekosa, Malo?” Naya aliuliza mara baada yakuingia tu kwenye gari.” “Utakumbushia kosa moja mpaka lini? Jambo moja haliishi daima!?” “Kwa hiyo wewe unafikiria ni jambo dogo?” “Sasa ulitaka nifanyaje? Nilishakwambia nilipaniki ndio maana nikakupiga kibao. Nimekwambnia nimekosa, ni nini usichoweza kusamehe?” Naya akashangaa sana.

“Mbona kosa unalozungumzia ni moja tu, Malo! Kwa nini huzungumzii usaliti wako?” “Acha mambo ya kitoto Naya! Nimekwambia kabisa yule sio mwanamke wangu. Imetokea mara moja, basi. Unataka kujiliza mpaka lini! Kwa nini unashindwa kuwa muelewa?” “Unataka nielewe nini Malo? Nimekufumania kabisa! Upo naye mnafanya mapenzi! Badala uniombe msamaha, ukanipiga. Ulitaka nifanye nini?” Naya akaanza kulia.

“Nimekwambia nilipaniki Naya. Sikujua kama ungerudi nyumbani siku ile.” “Malo! Sasa hiyo ndio inatakiwa inifariji?” “Acha utoto Naya. Nishakuomba msamaha na nimekwambia yule sio mwanamke wangu. Ilitokea mara moja tu, na nimekwambia haitatokea tena. Unachotaka kusikia kutoka kwangu ni nini!? Kwa nini unataka tukae kwenye jambo moja wakati wote? Kwa nini unapenda kubeba mambo moyoni? Unafikiri au unataka nini kitokee? Niambie Naya.” “Sijui Malo.” “Lazima ujue na uniambie. Mimi mtindo wa kuzungumzia mambo zaidi ya mara moja au mbili unajua wazi siwezi. Jambo likitokea naomba tulizungumze na liishe. Unanielewa Naya?” Kimya.

“NAYA!” Malo akaita kwa ukali mpaka Naya akashtuka na kumtizama . “Nimeuliza kama umeelewa?” “Nimekusikia.” Naya akajibu kwa upole, kisha akageukia dirishani, kimya. Malo akaendelea kukanyaga mafuta mpaka nyumbani kwake alipokuwa akiishi na Naya.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Malo alikuwa kijana mdogo tu, lakini alikuwa amejijenga haswa. Maisha yake yalikuwa hapo hapo mjini Morogoro. Mji ulionekana wakushoto au duni kuishi, lakini sio kwa Malo. Alistawi na kutajirika kwenye huo mji. Biashara alizokuwa akifanya, Naya hakuwa akizijua, lakini alijua Malo anazo pesa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Kesho nina vipindi asubuhi Malo.” “Nakumbuka. Nilitaka uje kuchukua zawadi niliyokununulia. Ujue ndio nakuomba msamaha.” Naya akanyamaza, akapitiliza chumbani. Malo akaja nyuma yake. “Ipo hapo mezani.” Naya akasogelea meza. Alianza kuhisi ni nini. Ulikuwa mkebe mzuri mezani. Akatizama na kuacha bila hata kugusa, akaenda kukaa kitandani, kimya.

“Kaa hapo kitandani nikuvalishe mwenyewe.” Malo alifuata ule mkebe pale mezani, akaenda akamsogelea Naya pale alipokuwa amekaa kitandani. Akapiga magoti. Naomba mguu. Naya akanyoosha huku akimtizama machoni akiwa ametulia tu. Akafungua ule mkebe, akatoa cheni ya mguuni, nzito ya dhahabu.

Akamvalisha na kuanza kumbusu kuanzia mguuni kupanda juu taratibu huku mikono ikimpapasa. Akaendelea kumbusu taratibu mpaka mapajani. Naya akajilaza. Alimjua Malo akikosa, msamaha wake utaupata kwenye zawadi atakayompa na mapenzi.

Hata kama Naya anakuwa amekasirika na akili hazipo pale. Huwa anahangaika kumtuliza kwa kumchezea. Basi hapo atahakikisha Naya anaridhika kweli kweli. Hata kama yeye atamfikisha mara tatu, atahangaika mpaka ahakikishe ameridhika ndipo na yeye anaweza hata kuambulia bao moja. Ndio msamaha wake, lakini sio maneno.

 ~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alimjua jinsi alivyo mbaya wa maneno. Malo alijawa kashifa. Jeuri na hasira za kupitiliza. Na anapokasirika huwa anapoteza uwezo wa kufikiria kabisa. Anaweza kufanya jambo, mpaka yeye mwenyewe huwa anajishangaa. Naya hakuwahi kumuona akivuta bangi, lakini hakushindwa kumfananisha na mvuta bangi.

Mkono mwepesi kupiga hata wafanyakazi wake. Ukimuudhi popote na mbele ya yeyote, hakuwa akiweza kujisaidia. Kijana mdogo aliyekuwa amefanikiwa sana, na kuogopewa mno hata na rafiki zake. Usimwibie wala kujaribu kumzunguka kwenye biashara zake, kudhuru haikuwa shida. Naya alishamshuhudia akimpiga ngumi za usoni mmoja wa wafanyakazi wake, akashangaa kama ipo roho ya kibinadamu ndani yake! Alimpiga mfululizo karibu ya kumuua na kumfukuza kama takataka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Malo kijana wa Moro. Alizaliwa hapo Moro mjini, na mama muuguzi aliyekuwa ngazi ya chini kabisa kwenye hospitali kuu ya serikali na baba akiwa dereva kwenye magari ya hapo hospitalini, hapohapo jijini Morogoro. Malon kama ndugu zake wengine walisomesha na wazazi wao hapohapo Morogoro kwenye shule za kata tu. Kwa kifupi ni mtoto wa Mji kasoro bahari. Hakuna asilolijua kwenye mji huo. Hakuna asiyemjua. Na kwa kuwa alishakaa sana mtaani baada ya kufeli kidato cha nne na kukataa kuendelea na masomo, hakuna asilolijua hapo mjini. Kuanzia maovu mpaka mazuri yanayoendelea mtaani, Malon aliyajua.

Alifahamika hata na watoto wadogo wa mtaani. Ila Hakuna aliyejua siri ya nafanikio yake ya haraka. Ilikuwa ni kufunga na kufungua, Malo akawa anamiliki thamani nyingi sana. Wengine walisema ni madawa ya kulevya, lakini hakuna aliyemkamata nayo.

 Alibadilisha maisha ya nyumbani kwao kwa haraka sana. Wazazi wake wakawa na maisha mazuri kutoka kwa Malo aliyekuwa amekataa shule na kumuumiza sana baba yake ambaye alikuwa na uwezo mdogo, ila alikuwa tayari kusomesha watoto wake. Mambo yalipombadilikia, hata dada zake waliomtangulia walinufaika. Waliotaka kusoma aliwasomesha na kuwafungulia biashara. Kwa ujumla Malo akawa msaada mkubwa sana wa familia.

Ndipo akaangukia kwa Naya aliyempenda kufa. Kila mtu alijua ukitaka maneno na Malon, msogelee Naya. Alikuwa kama pumzi yake. Alimpenda kupitiliza kasoro umalaya ndio ilikuwa tatizo la Malon. Alimtunza Naya na kumpa kila atakalo, lakini tatizo ni mahusino ya hovyo aliyokuwa nayo kwa wanawake mbali mbali. Rafiki yake wa karibu sana waliyekuwa naye tokea utotoni, Chezo kama wengi walivyozoea kumwita, alishindwa kujua tatizo la Malon.

“Shida ni nini Malo!? Unataka nini na kwa nani!?” “Swala la nani ni Naya tu.” “Sasa kwa nini hutulii naye!?” “Nani amekwambia sijatulia na Naya!?” Hapo anacheka kama mazuri. “Acha kunitazama hivyo Chezo!  Kuonja mboga sio kula, baba! Na hata nipewe vipi na nani, lazima nikamalizie kwa Naya, ndio naridhika. Hata wewe unajua.” Chezo hubaki akimtizama na kushindwa kumuelewa. “Mbona wewe hutosheki na bia moja, kaka?” Malo hakuacha kumuuliza hivyo. “Usilinganishe pombe na wanawake Malo! Unamuumiza sana Naya.” “Naya mwenyewe anajua yeye ndio mwenyewe, hana mpinzani.” “Muonyeshe kwa vitendo basi!” “Ulitaka nimfanyeje? Wewe Ni shahidi. Naya anamiliki mpaka roho yangu! Natakiwa kufanya nini tena?!” Hapo huwezi kumshinda Malon. Na Chezo alimjua. Ukiendelea zaidi, ni ugomvi. Heri yeye ashinde.

 ~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

     Baada ya mapenzi hayo mazito, Naya akapitiwa na usingizi. Malon akamfunika, nakujilaza pembeni yake mpaka na yeye akapitiwa na usingizi. Alifungua macho akakuta Malon akimtizama. Akajiweka sawa akiwa palepale kitandani, akatulia. “Vipi?” Malon akaanza kumchezea nyusi taratibu. Naya akabaki kimya. “Nije kukuchukua kesho saa ngapi?” Malon akauliza tena akionyesha penzi na usingizi aliopata, umemtuliza. Kimya. “Au leo tunalala? Nitakupeleka asubuhi.” Kimya. “Mbona hunijibu Naya!? Unaniacha nazungumza peke yangu tu? Au bado umekasirika?” “Huwa unatafuta nini Malo?” “Kwa nani?” “Najua unanielewa Malo.” Malon akaanza kucheka.

“Naya kwa kupenda kubeba mambo! Ni nini kisichoisha? Mbona mwenzio siweki mambo moyoni? Nakuhakikishia hao wote hawana maana Naya. Ila wewe tu. Au hilo unamashaka nalo?” Naya akanyamaza. Alijua Malo anampenda sana, lakini hakujua ni nini kinachomsumbua. “Mapenzi ninayokumbuka ni yako tu Naya wangu. Wote wapuuzi. Wala wasikusumbue kichwa chako.” “Sasa kwa nini hutulii Malo? Utaniua na UKIMWI.” “Hakuna ninayelala naye bila kondomu.” “Kweli Malo! Unaniambia bila kunifikiria nafsi yangu? Unajua na mimi ni binadamu? Nina hisia!” Malo akazidi kucheka na kumuumiza Naya zaidi. Akataka kutoka pale kitandani lakini Malon akamvuta mkono kwa nguvu na kumrudisha palepale kitandani.

“Acha hasira Naya. Ninachojaribu kukwambia nipo makini. Nakulinda sana mpenzi wangu. Katika kila jambo ninalofanya nakufikiria. Kwamba kabla ya kufa wewe, ujue na mimi nitakufa.” “Kwa hiyo hata unapokuwa unafanya nao mapenzi unakuwa ukinifikiria?” “Unapenda kufikiria mbali wewe!” “Acha kucheka Malo! Utajisikiaje na mimi nikifanya kama unavyofanya wewe?” Kicheko cha Malon kikakata ghafla na kukaa.

“Na mwanaume gani huyo asiyependa nafsi yake!? Nitamtahiri bila ganzi.” Naya akamtizama, akasimama. “Rudi Naya.” “Naenda kuoga niondoke.” Malon akaruka pale alipokuwa amekaa akamfuta kwa haraka. “Nakuonya Naya! Usithubutu.” “Mbona wewe unafanya? Kitakachonizuia mimi ni nini?” “Nakuonya Naya. Usishindane na mimi.” “Niache Malo. Acha kunitolea macho na kunishika mkono wangu kwa nguvu.” Alimuona ameshabadilika kabisa.

“Unataka kunipiga tena?” Naya akamuuliza. “Nipige tu, umalizie hasira zako.” Malon akamuachia. “Nimekuonya Naya.” “Mbona mimi nakuonya na huachi? Mara ngapi umelala na wanawake na mimi nikiwa nipo hapa nakusubiria? Mbaya zaidi unalala nao, halafu unakuja kulala na mimi! Unanichafua tu.” “Wewe ndio unakuwa unanihisi nimetoka kwa wanawake wengine wakati sio kweli.” “Mara ngapi nimekufumania Malo? Mara ngapi?” “Kwa nini unapenda kutunza mambo!? Unataka litokee nini!?” Naya akaondoka na kuingia bafuni akajifungia.

“Naya!” Akamsikia akiita nje ya mlango. “Nitavunja huu mlango Naya wewe fungua!” “Vunja. Kwani ndio itakuwa mara yako ya kwanza?” Naya akajibu huku akifungulia maji ili aoge. “Naya!” Malo akaita tena kama anayemtisha lakini Naya hakumjibu tena. Akamsikia ametulia. Akaendelea kuoga mpaka akamaliza. Akatoka akiwa amejikausha kabisa, akamkuta akimsubiri nje ya mlango. Akampita.

“Umeanza mahusiano huko chuo?” “Mimi sio kama wewe Malo.” “Nani amekwambia nimeanzisha mahusiano? Sina mahusiano na yeyote ila wewe tu.” Naya akanyamaza akaendea ilipokuwa meza yake ya vipodozi. “Nimekuuliza Naya. Maana mimi nimekujibu. Sina mahusiano na mwanamke yeyote ila wewe.” “Kwa hiyo unaita nini kile ninachokuona ukifanya na wanawake wengine?” “Ujue uwe unatumia akili Naya wewe. Nani umemuona analalia kitanda changu isipokuwa wewe peke yako?” “Kwa hiyo ukiwa unalala na wanawake zako hapo nje ya hiki chumba ni sawa, mbaya isiwe hapa kitandani?” “Naya!” “Basi usiwe na wasiwasi, na mimi watakuwa wakinilala kwenye vitanda vyao sio hapa kwenye kitanda chako.” Malo alipiga ngumi kwenye ile meza aliyokuwa amesimama Naya akijipaka lotion. Naya alishtuka mpaka akaruka. Kila kitu kilianguka sakafuni na kuzagaa kila mahali pale chumbani kulikokuwa kuna sakafu yenye marumaru nyeupe na kapeti chini ya kitanda.

Akamuona anavaa nguo zake nakutoka. Akajua hapo ndio amekasirika mpaka mwisho anakaribia kurukwa akili. Naya akahema kwa nguvu. Hakujisumbua kuokota kitu hata kimoja. Akavaa nguo zake, akampigia moja wa dereva wa Malon, akafika pale akamchukua usiku huo na kumrudisha chuoni.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

     Naya akashangaa kumekuwa kimya juma zima. Ila jumbe tu za kumtakia usiku mwema. Tena kwa kifupi tu. Naya akawa anamcheka. ‘Usiku mwema.’ ‘Asante na wewe.’ Naya alibaki kujibu tu hivyo bila nyongeza. Jumatatu mpaka ijumaa. Naya akamuhurumia. Alijua wazi anateseka bila kumuona. Lakini alikusudia amwache kwanza. Juma hilo likapita. Ikaanza jumatatu tena mpaka ijumaa. Lakini ilipofika jumatano, Naya akaacha kujibu jumbe za kutakiana usiku mwema.

Kwa muda huo alipokuwepo hapo chuoni alikuwa akijisomea maktaba ya chuo, au chumbani kama wenzake hawapo au wamelala. Hawakuamini vile Naya alivyokuwa akisoma. Hata usiku alikuwa akiamka kusoma kitu kilichowashangaza. Walijua ni urembo tu ndio unaoendelea kwenye kichwa chake, kumbe na shule pia!

Ijumaa wakati anatoka kwenye kipindi cha mwisho kabisa akiwa anaelekea chumbani kwao, akaona gari ya Chezo nje ya hosteli yao. Akashtuka kidogo. Akaongeza mwendo mpaka pale. Alimkuta Chezo ametulia tu garini.

“Kwema Chezo!?” “Kwema. Ila nimekuja kukuchukua.” “Kwenda wapi!?” Naya akashangaa. “Malo atachanganyikiwa, Naya.” “Anachanganywa na nini?” “Acha utani Naya.” “Sikutanii Chezo, kwanza yuko wapi?” “Kwake. Yupo kama mgonjwa. Nikaona nije tu kukufuata.” Naya akaingia ndani ya gari.

“Naomba tuzungumze Chezo.” “Nini tena?” “Hivi unajua alichokifanya Malo?” “Hajaniambia kabisa. Ila ameniambia kwa mara ya kwanza umemtamkia upo huru kufanya mapenzi na mwanaume mwingine kama kumlipiza kisasi wakati alishakuomba msamaha na amekiri kosa.” Naya akashangaa sana maelezo aliyonayo Chezo. “Wewe amekwambia amekosa nini?” “Nilimuuliza hivyo, hakujibu.” “Kwa kuwa anakujua Chezo, ndio maana ameshindwa kukujibu.” “Amefanya nini tena?” Naya akaguna.

“Nini?” “Unakumbuka nilikuwa likizo, nikamwambia lazima niende nyumbani, baba ananiulizia?” “Nakumbuka. Si tulikuwa wote baa.” “Sawa sawa. Sasa baada ya kama siku mbili mbeleni, Malo akanirudisha mpaka karibu kabisa na nyumbani. Akaniuliza lini nategemea kurudi, nikamwambia inategemea na hali ya nyumbani, sina uhakika. Nimekaa nyumbani kama baada ya siku kumi nikapanda basi asubuhi, nikajiambia nikae naye mpaka jioni, nirudi nyumbani. Nilikaa pale mpaka jioni, Malo hayupo, hapokei simu na hakuwa safari.” “Wewe ulijuaje?” Chezo akauliza.

“Kumbuka nilikuwa naye Dubai? Baada yakupokea mzigo wake kutoka Brazil na kuusambaza pale, tukarudi naye Dar. Tukakaa Dar kama siku mbili ndio tukarudi huku Moro. Aliniambia ratiba zake zote. Akataka kukutana na mwanamke fulani hivi. Akaniambia ni mambo ya biashara kwa kuwa alitaka yule mwanamke sijui nikwambie msichana aje pale hotelini. Yule dada akaja, alitukuta tunakula chakula cha usiku sehemu ya mgahawani. Wakazungumza kidogo, kisha wakahama meza.”

“Mimi sikujali kwa kuwa nilijua ni mambo ya biashara. Wakazungumza baada ya muda wakarudi pale mezani wakiwa wanacheka. Malo mimi namfahamu Chezo. Namfahamu vizuri tu. Jinsi alivyokuwa akimtizama yule dada kabla na baada, nikajua tayari lipo jambo.” “Umeanza Naya.” “Subiri Chezo. Yule dada akaropoka, ‘tutaonana basi hiyo jumamosi’. Nikashtuka, nikamtizama Malo. Malo akapotezea. Yule dada akaondoka. Nikamuuliza Malo, mnaonana wapi hiyo jumamosi? Kama unavyomjua Malo, akaanza kucheka, akasema kama hivi ulivyosema wewe. ‘Umeanza Naya. Huyu dada mtumzima nataka nini? Ni mambo ya biashara tu.’ Akanijibu hivyo, nikanyamaza.”

“Si ndio tukarudi Moro, tukawa wote! Mimi sikuondoka kwa haraka kama nilivyomwambia Malo kuwa tukirudi tu Moro sitakaa itanibidi kurudi nyumbani. Inamaana na ile jumamosi yule dada aliyosema angekutana na Malo, mimi nilikuwepo na Malo, nafikiri wakashindwa kuonana. Nikaja kuondoka baada siku ile kuwaaga pale baa. Sasa turudi niliporudi na kumkosa pale nyumbani nikijua hana safari. Nikamuuliza Side. Tena kwa kumpigia. Nikamuuliza Malo yuko wapi? Akasema yeye alijua yupo na mimi Dar. Maana  alimuaga anakwenda Dar. Basi, mimi nikarudi Dar. Nikatulia. Alikuja kunitafuta kesho yake, kwa uongo kuwa alikuwa amepoteza simu, hakujua wapi alikuwa ameiacha.” Chezo mwenyewe akacheka.

“Umeona eeh! Hata wewe unajua ni uongo. Malo hawezi kupoteza simu.” “Kupoteza simu kwa Malo ni kama amepoteza pumzi.” Chezo akaongeza. “Sawa sawa. Sasa mimi nikajua tayari. Ila sikujua ni nani.  Nikamtega bila yeye kujua, nikamwambia huko unakoegesha gari mchana kutwa, wanamuona. Wewe unamjua Malo nikimfumania anavyokuwa mwema. Akaongea mengi wee, mimi namsikiliza tu. Mwishoe nikaona nikate simu.”

“Nikatulia kama siku 4 hivi, nikarudi  tena kwake. Huwezi amini Chezo, nilimkuta Malo na yuleyule dada aliyetufuata kule hotelini Dar, sebuleni. Sebuleni Chezo, bila aibu Malo anafanya mapenzi na yule mwanamke. Dada mtu mzima kama yule dada yake mkubwa.” “Haiwezekani Naya!” Chezo alishtuka sana. “Mungu wangu nishahidi. Nisingeweza kumsingizia Malo. Nikajiambia ni dharau ya namna gani hiyo kuleta mwanamke ndani!”

“Nilishtuka sana. Nikamuuliza kwa nini anafanya vile? Hivi unajua Malo alinipiga kibao?” “No way!! Haiwezekani Naya.” “Muulize. Alinipiga mbele ya yule dada, tena wakiwa uchi vilevile. Mimi nikaondoka, nikarudi nyumbani. Hakika niliumia Chezo.” “Pole Naya. Sasa naelewa ni kwa nini ameshindwa kuniambia.” Chezo akaumia sana.

“Basi. Zikaanza simu na jumbe zakuomba msamaha. Kwamba alipaniki. Hakukusudia kunipiga. Ikawa msamaha ni wakunipiga, sio kumfumania. Sikumjibu. Nikaamua kunyamaza tu. Chuo kilipofungua sikumtafuta, nikapitiliza kutoka nyumbani mpaka huku Mzumbe. Sijui alijuaje kama chuo kimefunguliwa, siku hiyo nimelala, nikamshtukia amenisimamia pembeni ya kitanda, anataka niondoke naye.”

“Mwanzo nikamkatalia. Lakini kama unavyomjua Malo, akabadilika akataka kuanza kufanya fujo. Nikaona yaishe, nisijiharibie na hapa chuoni. Tukarudi naye nyumbani kwake, nikakuta ameninunulia cheni nzuri sana ya mguu, eti ndio ananiambia ananiomba msamaha wakunipiga, sio kumfumania! Na maneno yake yaleyale anayowaambieni na nyinyi kuwa mimi ndio mpenzi wake huku wote tukimshuhudia akilala na kila mwanamke.”

“Nikamuuliza kwa nini anafanya hivyo kama kweli ananipenda? Ndio akasema mimi ndio mwanamke wake na ndio maana analala na wanawake wengine nje ya kitanda chetu. Ndio nikamwambia basi na mimi nitalala na wanaume wengine nje ya kile kitanda. Acha apagawe. Kapiga ngumi dressing table. Akaangusha kila kitu sakafuni aka..” “Ndio maana ameniambia ameumia tu, ila hajaniambia ameumiaje!” “Mbona sikuona kama alitokwa na damu!?” “Ametegua kidole cha kati. Amefungwa mabendeji. Kama POP.” “Mimi sijui Chezo. Nimechoka. Malo ataniua kwa magonjwa.”

 “Hawezi. Hilo nimemuuliza. Amenihakikishia anatumia kinga, hapo hajisahau.” “Sasa hilo ndio litatakiwa liwe sawa? Ananidhalilisha kupita kiasi! Hakuna tunapokwenda sehemu hata kwenye migahawa asiwe amelala na hao wanawake mtakao kutana nao hapo. Wawe wahudumu au mmiliki wa hilo eneo kama ni mwanamke. Basi jua Malo alisha lala nao. Analala na kila mwanmke! Nimechoka Chezo. Niambie ni kwa nini niendelee naye?”

“Malo anakupenda Naya. Mimi sijui anakuwa aningiwa na tamaa gani, lakini anakupenda sana. Yupo kama mgonjwa.” “Sidhani kama ni kwa ajili yangu Chezo. Itakuwa ni hicho kidole alichokitegua.” Chezo akacheka. “Kweli Chezo. Anachotaka kwangu ni nini ambacho hakipati kwa wengine?” “Mimi nashauri ukazungumze naye. Unamjua Malo. Amenyamaza, hatujui anawaza nini. Akija kuibuka, anaweza kuja kukufanyia fujo huku. Nashauri ukamtulize Naya.” “Mpaka lini Chezo!?” “Akili kichwani. Wewe si ndio umeanza chuo? Mtumikie kafiri upate mtaji wako.” Naya akabaki kimya.

Akakumbuka ada anayolipiwa na mapesa anayompa. Akaona Chezo yupo sahihi. Malo alikuwa kama mvuta bangi. Kichaa kikimpanda, hakawii kuja kumtoa katikati ya darasa. Hata hivyo bado alikuwa akiiihitaji pesa yake. Bado Chezo alikuwa akimtizama anavyofikiria. Naya akamgeukia. “Nisubiri nikaweke haya madaftari, nitarudi sasa hivi twende wote.” “Hayo ndio mambo. Mjini watu wanaishi kwa akili Naya. Panga karata zako vizuri. Ukipata chako ndio unaota mbawa. Sasa unataka kuota mbawa wakati kujajua hata kuelea angani!?” Naya akacheka na kutoka kurudi chumbani kwake. Akachukua vitu baadhi akatoka na kuondoka na Chezo.

Njia nzima Chezo alikuwa akimpa mikakati. Nini chakufanya huku akimuonya asije kumwambia Malo. “Fungua akaunti yako ya pembeni ambayo yeye haifahamu. Rushia humo pesa.” “Wewe unamjua Malo. Anafahamiana na kila mtu! Watu wa benki wakimwambia?” “Basi weka kwenye akaunti ya mama yako. Jiwekee akiba. Kuna leo na kesho, Naya. Huwezi jua.” Naya akanyamaza. 

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

     Chezo alimshusha getini nyumbani kwa Malo, akaondoka. Naya akaingia getini na kuanza kutembea taratibu huku akiwaza. Alikuta magari yote ya Malon yapo ndani. Akajua yupo ndani. Alikuta mlango umefungwa, lakini si kwa funguo. Alipofungua, ukafunguka bila shida. Hakumkuta sebuleni. Akajua yupo chumbani. Alimkuta amejilaza kitandani anabadilisha tv huku na kule. Wazi alionekana hakuna anachoangalia.

Ni kama hakuamini alipomuona Naya. Akapitiliza bafuni bila yakumsemesha. Akaoga na kurudi kitandani. Akamvuta mkono. “Unauma?” “Mpaka niutoneshe. Lakini hivyo walivyonifunga sasa hii inasaidia.” Malo akajibu. “Pole.” Akajiweka sawa. “Umepata mwanaume mwingine?” Malon akamuuliza. “Mimi siwezi kufanya au kuishi kama wewe Malo.” “Kwa nini unapenda kurudia mambo!?” “Hivi unajua hata mwezi haujaisha na hivi unajua hiyo sio mara yako ya kwanza, Malo!? Kilichobadilika ni kumleta mwanamke humu ndani kitu ambacho hukuwa ukifanya tangia tumeanzana! Ulikuwa ukikutana nao huko huko. Ukaniahidi umebadilika, haitarudia tena. Matokeo yake umeleta mwanamke kama dada yako humu ndani!” “Nimeomba msamaha Naya.” Naya akakunja uso.

“Au unataka nifanye nini?” “Malo! Kwa hiyo ndio inatakiwa iishe na maisha yaendelee mpaka nikufumanie tena?” “Kwa nini unafikiria nitarudia tena?” “Kwa nini nisifikirie hivyo? Niambie ukweli Malo. Kipi kitakuwa kimebadilika kwako? Mimi ni Naya yuleyule. Sijabadilika. Kile unachokikosa kwangu na kukufanya unahangaika na wanawake wengine, sikijui mpaka leo! Na tabia yako hiyo haijawahi kubadilika Malo. Na mimi ni mwanadamu.” “Unamaanisha nini?” Malo akauliza. Naya akachoka kabisa kuona ni kama haelewi. Akashindwa hata amjibu nini.

 “Naya?” “Nitachoka Malo! Nitachoka. Na mimi natamani mtu wangu. Ambaye ataniheshimu na kunipenda mimi tu. Sio hivi unavyonidhalilisha.” “Hakuna anayenifahamu mimi, asikufahamu wewe Naya.” “Inasaidia nini Malo!? Kama sio kuzidi kunidhalilisha tu. Wanajua huridhiki kwangu ndio maana unahangaika nje.” “Sio kweli Naya. Nakupenda wewe.” “Sasa kwa nini hutulii Malo? Unataka nini?” Malo akakaa. “Nakuahidi haitakaa itokee tena.” “Kweli Malo?” “Kweli nakuapia.” “Na mimi naomba kwa mara ya kwanza na itakua ya mwisho, nikuapie Malo.” Malo akajiweka sawa.

“Nakusikiliza.” “Siku nitakayokufumania tena Malo, ndio itakuwa mwisho wa kurudi kulala kwenye hiki kitanda. Na ndio itakuwa mwisho wetu. Nakupenda, lakini nitakuwa nimefika mwisho. Nakuapia Malo, huo ndio utakuwa mwisho wetu.” Malo akashtuka sana asitegemee. “Naya!?” “Kwani unampango wa kurudia tena?” Malo kimya. “Wewe si umeahidi hutarudia? Basi hapatakuwa na shida. Naomba tulale. Nimekuwa na week ndefu yenye mitihani kila siku, nilikuwa silali.” Naya akageuka pembeni nakujifunika.

“Nilikuwa na hamu na wewe Naya! Umeniacha majuma mawili!” Naya akamuhurumia, akageuka. “Hukutoka?” “Mungu wangu ni shahidi Naya. Sijatoka kwenda kwa mwanamke yeyote. Kwanza yule dada ni kama..” Akasita. “Basi. Acha nibebe makosa yangu mwenyewe. Ila naomba ujue sikutoka na wala sijafanya chochote. Naomba yaishe tafadhali.” Kwa kuwa alikuwa anaumwa mkono, Naya akamkalia na kumlalia kifuani.

“Na mimi nina hamu na wewe Malo.” “Naomba usije kulala na mwanaume mwingine Naya. Tafadhali sana.” “Hapana Malo, wewe naomba utulie. Kila kitu kina expiring date. Mwisho wa matumizi yake au uhai wake. Hata mwanadamu anayo expiring date, ndio maana ya kifo. Na mapenzi ni hivyo hivyo. Lazima kuyapalilia. Na sitaweza kufanya mimi mwenyewe. Siwezi kukuahidi Malo. Usharudia kunisaliti mara nyingi sana. Tafadhali badilika. Binafsi sina mpango wala nia na mwanaume mwingine. Nimetulia shuleni. Najua na wewe unayo hiyo taarifa. Sina mwanaume yeyote yule. Ni wewe na shule tu. Sasa naumia kuona mwenzangu unahangaika wakati mimi nakuwepo, Malo! Nipo na wewe karibu kila siku na kila mahali! Unanidhalilisha sana. Sina hata ujasiri kwa rafiki zako. Wote wanajua uchafu unaofanya na mimi nikiwepo!” “Lakini wanakuheshimu wewe Naya. Wanakuheshimu kama vile mimi tu au kama mke wangu.”

“Hapana Malo. Wanaheshimu pesa yako. Wala sio sisi kama Malo na Naya. Wanahisi nakuvumilia kwa yote sababu ya pesa. Hakuna mwanadamu anaweza kukuvumilia kimapenzi kama mimi Malo. Ushanifanyia makubwa yakutisha na mimi ndio naishia kujirudi. Watu wanafikiri ni kwa sababu ya pesa kumbe ni kwa sababu nakupenda Malo. Nakupenda sana. Tafadhali naomba badilika.” Malo akavuta pumzi kwa nguvu, akamgeuza Naya. Yeye akawa juu. “Nitabadilika Naya.” “Asante.” Malo akaanza mabusu ya kila mahali. Ilisikika sauti ya Naya akifurahia mapenzi ya Malon usiku huo. Aliujua mchezo, Naya hakuwa akijivunga pale Malo anapomshika.

 Huba.

N

aya hakujua kama ni hofu iliyomuingia Malo au ni kweli ameamua kubadilika! Mapenzi yale ya mwanzoni kabisa wanaanzana kimapenzi, yakarudia. Malon aliyemtongoza kwa kumbembeleza karibu kuchanganyikiwa akarudia enzi zile za mwanzo. Hata Naya alijua anapendwa. Kutoka katika kashfa, kumsaliti hata mbele za watu, Malon akarudi kumtetemekea Naya. 

Mara ya kwanza Malon alipomuona Naya.

Siku hiyo Naya akiwa chuoni Mzumbe, akakumbuka siku anakutana na Malon. Akacheka na kuinama huku akivuta kumbukumbu. Alikuwa amekaa peke yake ilikuwa bado mapema tu, baada ya vipindi vya asubuhi kuisha hapo chuoni. Wenzake wanaosoma darasa moja wakila, wakisubiria vipindi vya mchana. Wengine wakiingia madarasani. Yeye alikuwa amekaa tu, hakutaka kula chakula cha mchana hapo chuoni. Kumbukumbu zikamrudisha miaka michache nyuma akiwa na wenzake kipindi anaishi hosteli akiwa shule ya sekondari na warembo wengi tu, ila yeye kuchaguliwa na Malon na kuacha warembo wengine hawaamini.

 ~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Usikose Sehemu ya 2, iliyobeba historia ya mwanzo wa Naya na Malon uliobeba uzito mkubwa wa Simulizi hii.

CONVERSATION

1 Comments:

  1. Wow!amazing .Natamani kuona wanaishia vp ila mapenzi matam bwana.

    ReplyDelete