Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & pesa – sehemu ya 10. - Naomi Simulizi

Mapenzi & pesa – sehemu ya 10.

Kwa Malon.

M

alon alikaa pale akiwaza. Akapanga na kupangua. Naya ni msichana anayempenda. Hajutii kuondoka kwake, kwani ndilo lilikuwa lengo lake. Alitoka jela akiwa amefilisika haswa. Na alijua amefilisiwa tokea alipokuwa jela kwani maafande walikuwa wakimwambia makusudi kuwa watu wamekusudia kumfilisi. Hakujua


ataishije. Hakutaka Naya aangamie naye. Alitoka jela akifikiria maisha yake na deni kubwa alilokuwa nalo kwa Naya. “Hakuna jinsi naweza kumlipa Naya, isipokuwa na yeye kumuweka huru mbali na mimi. Hiyo ndio zawadi pekee ambayo naweza kumpa Naya.” Malon aliwaza akiwa njiani kurudi Dar akitokea jela baada ya wosia mzito pia kutoka kwa Mati. Akakubali kuwa, kuendelea kuwa na Naya kwenye mahusiano ni kutomtendea haki.

Alipomuona usiku ule alipokuwa na Ozi, akabadili mawazo, akaamua aendelee naye, atajitahi mbele ya safari. Lakini akakutana na Naya wa zamani. Amerudisha msimamo wake. Sio wa michezo tena kukubali kukimbilia kitandani.  Anajielewa na baba yake amerudi kwenye picha. Amesimama na binti yake. Malon asiyejua kusimama kwenye mahusiano yakueleweka. Asiyeelewa kujifunga kwenye chochote kwa yeyote, akabadili tena msimamo. Akaona anatakiwa kujitoa tena kwa binti kama Naya.

‘Naya anataka ndoa!’ Malon akakumbuka alichoombwa na Naya siku hiyo nyumbani kwao. “Nikimuoa nitamlisha nini mimi Naya? Sijasoma, sina chochote! Siwezi kuishi nyumbani nikilishwa na Naya.” Hali ya uanaume ikainuka ndani ya Malon. Sasa kuja kusikia yupo Joshi. Tena anayemfanya acheke mpaka atokwe na machozi! “Huyu ndiye atakayemfaa Naya wangu. Angalau atamfariji.” Aliwaza Malon wakiwa njiani kupeleka maziwa huku akiendelea kumsikiliza Naya anavyocheka kwenye simu na Joshi. Malon akaadhimia kumuacha mikononi kwa Joshi.  “Namwachaje kabla sijamuumiza tena?” Ni swali lililoanza kumuumiza. “Kwa kuwa ameshasikia mengi mabaya juu yangu, na ananijua mimi ni mkorofi heri ni mtafutie sababu ya maana, anichukie na aende kwa mwanaume mwingine, aendelee na maisha yake.” Wakiwa kwenye gari yeye na Naya wakielekea Kunduchi, Malon aliendelea kuwaza kitu chakufanya.

Ndipo akaona atumie kigezo cha Joshi na Ozi. Huku akimsukumizia kwa Joshi na kumkumbusha kuwa hana uwezo wa kumfanya awe na furaha kama vile Joshi anavyo mfurahisha. Akaibua ugomvi, na hasira kwa Naya mpaka Naya akakolea. Akaongea mengi kama kawaida yake, Malon akimsikiliza tu, mpaka akaondoka na kumtaka asirudi tena kwao. “Ni heri aondoke akijua sina shukurani, kuliko kuja kuteseka naye kwenye maisha. Kwanza itamsaidia kunichukia kabisa na kuendelea na mwanaume mwingine. Ni kweli simstahili Naya. Sina uwezo wa kuja kuwa mume au baba wa watoto. Naanzia wapi?” Malon aliendelea kuwaza akiwa peke yake kwenye ile nyumba ambayo haina hata chakula.  Kwa kuwa alikula nyumbani kwa kina Naya, alilala hapo hapo kwenye kochi, akiangalia tv akikubaliana na maamuzi aliyoyafanya kumuacha Naya.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~ 

A

subuhi siku ya jumatatu aliamka na kwenda kukimbia baharini baada ya kulala na siku ya jumapili siku nzima. Malon ni mtu wa mazoezi. Hata alipokuwa mahabusu, alichofanya ni mazoezi. Alikimbia muda mrefu mpaka alipochoka, akaamua kurudi nyumbani. Njaa ilishaanza kumuuma. Hana chakula ndani ila pesa kidogo aliyopewa na Naya siku ya ijumaa alipotoka mahabusu. Akayatizama yale mahoteli yaliyokuwa yamejipanga ufukweni. Akajiambia akiingia tu pale kula na kunywa, anaweza kukosa nauli yakutoka nyumbani kwake kama atataka kutoka. Akaamua kujikaza. Arudi tu nyumbani kwake, akaoge, anywe maji. Aendelee kufikiria chakufanya.

Alitembea taratibu pembeni ya hayo mahoteli huku akikumbukia enzi zake anapesa ya kufanya chochote. Ni miezi karibu mitatu tu iliyopita, Malon huyu alikuwa na uwezo wa kuchukua chumba kwenye mahoteli hayo, akaenda kulala na mwanamke yeyote anayemtaka, nakutoka baada ya muda mfupi wakutimiza haja yake, huku akimuachia huyo mwanamke hicho chumba. “Nimelipia mpaka kesho. Unaweza tu kuendelea kukitumia hiki chumba.” Ndio zilikuwa kauli zake kwa wanawake anaokwenda kuwatumia kwenye majumba hayo. Anaondoka akiwa amelipa mapesa mengi, kwa starehe ambayo haikuwa ikichukua hata masaa mengi. Na akitoka hapo, anarudi zake kwa Naya. Anatulia.

Leo anapita hapo nje, hana hata pesa ya kununulia soda! Malon akajicheka nafsini kwake. Akamkumbuka Side na Futi. Wao hakutaka kuwalaumu sana. Alijua alikowapitisha. “Nani asingetaka kuokoa nafsi yake?” Akawatetea nafsi mwake huku akikumbuka jinsi walivyokimbia na mapesa yake, na magari yake. Wamemuacha Malon hana usafiri! Malon akaendelea kutembea taratibu akiwaza mpaka akatokea barabarani akirudi kwake.

Akakuta mtu anabandika tangazo dogo tu. “Tunauza na kununua nyumba.” Malon akamsogelea. Akamsalimia. “Wewe ni dalali?” “Hapana. Mtu wa masoko kwenye kampuni yetu. Tunatafuta nyumba kwenye haya maeneo.” “Mimi ninayo nyumba. Nakodisha. Ina vyumba vitatu. Kila kitu ndani kimekamilika. Jiko lina kila kitu, sebule ina mpaka tv na vyumbani kuna vitanda pia, upande wa uwani geti linaingilia baharini kabisa. Ukinitafutia wateja, kama watalii, au watu ambao wanatafuta sehemu ya kwenda kupumzika kwa muda. Nitakuwa nikikulipa asilimia fulani ya hayo malipo.” Yule baba akashawishika.

“Lakini hiyo sio kazi ya kampuni yetu. Kampuni yetu ni kununua na kuuza nyumba.” “Mimi siuzi. Nakodisha. Na nimekupa dili. Ukipata mteja, mlete kwangu.” “Nionyeshe basi nyumba yenyewe na unipe namba za simu yako.” Wakaongozana na Malon, Malon akiwa anafikiria jinsi ya mawasiliano kwani hakuwa hata na simu. Alipokwenda kujisalimisha polisi, alivuliwa kila kitu na kukabidhi kila kitu kwa afande aliyemkuta mapokezi. Lakini wakati wakutoka aliambiwa hakuacha kitu chochote pale. Mpaka waleti yake hakupewa na ilikuwa na kadi zake zote za benki ambako na kwenyewe alikuta wamemmaliza kabisa. Hakuna afande aliyekubali kupokea au kukabidhiwa vitu na Malon siku alipoingia hapo rumande. Siku anatoka hapo polisi walimkatalia kabisa. Malon hakujali, alijua wanamfanyia kusudi tu.

 Akabaki akiwaza watawasiliana vipi na huyo anayemuomba amkodishie nyumba! Wakaendelea kutembea kuelekea kwake. Alipofika getini mlinzi akamwambia Naya ametoka hapo muda sio mrefu, ameacha bahasha. Malon akapokea hiyo bahasha. Ilikuwa kubwa na ilionekana na kitu kizito ndani.

Wakamuona anakunja uso wa mshangao huku akifungua. Akakuta ile simu ya Naya. Ilikuwa imezimwa na bahasha ndogo ndani. Akafungua. Akakuta pesa na kikaratasi. ‘Hiyo ni simu niliyokuwa nimenunua kutokana na pesa nilizokuwa nimekusanya. Ni ya kawaida tu. Sio smartphone, lakini ilinisaidia kwa mawasiliano. Naamini na wewe itakusaidia kwa kipindi hiki ambacho unajiweka sawa. Samahani jana niliondoka, nikasahau kukuachia pesa. Sina hela nyingi Malon. Lakini naamini hizi zitakusogeza kwa mizunguko ya hapa na pale mpaka utakapojiweka sawa. Nimekupikia maandazi jana nilipotoka kanisani. Ndio kitu pekee nilijua naweza kupika na ukaweza kula.’ Malon akacheka kidogo baada yakukumbuka mapishi ya Naya, akaendelea kusoma.

‘Nimekuletea maziwa na mayai trei mbili pia. Vyote nimemuachia huyo mlinzi. Sio vingi, lakini naamini vitakusogeza. Nakutakia mwanzo mwema Malon. Mungu atakusaidia tu, usikate tamaa. Mwanzo unaweza ukawa mgumu, lakini nakuamini una akili nzuri. Wewe ni zaidi ya vyeti vya shule ambavyo ungekaa darasi na kupewa na walimu. Nizaidi ya magari waliyokuchukulia. Zaidi ya hata ile nyumba waliyokuchukulia kule Morogoro. Kwa sababu vyote wewe ndio ulifanya vikawepo. Havikuwahi kuwepo mpaka wewe ulipofikiria na kufanya viwepo. Naamini ukitulia na kufikiria, na kutumia njia sahihi, utafanikiwa tu. Nimeishi na wewe, nimeona utendaji wako kazi. Najua ni nini nazungumzia. Unao uwezo mkubwa sana Malon. Nitakuwa nikikuombea popote ulipo, na chochote utakachofanya, Mungu akufanikishe. Ni hayo tu ndio nilipanga kukwambia ukitoka jela. Nasikitika hatukuweza kupata muda wa maongezi, ila namshukuru Mungu ameweza kukutoa ukiwa salama. Mungu awe nawe Malon. Halafu nilisahau kukwambia kuwa nililipa ulinzi wa hapo mpaka mwisho wa mwezi huu.Naya.

 Macho ya Malon yalibadilika yakawa mekundu sana. Kwa sekunde kadhaa akashindwa hata kusogea. Akabaki amesimama pale kwenye kibanda kidogo tu cha mlinzi huku yule aliyekuja naye kumuonyesha nyumba, amesimama nyuma yake. “Ameacha na mizigo hii hapa.” Mlinzi akasogeza mifuko kadhaa. Malon akaitizama, akarudi kwenye ile bahasha. “Naona nimepeta na simu.” Akamgeukia yule mtu. “Naomba namba yako na jina lako kamili. Nitakapopata namba tutawasiliana.” Hayo yote Malon anazungumza akikwepesha macho huku akijaribu kutulia.

“Naitwa Tembe na hii ndiyo business kadi yangu.” Akajitambulisha. “Unaweza kuandika tu Malon. Nitakupigia ili upate mawasiliano yangu. Hapa ndipo nyumbani. Ukipata mteja, wewe unijulishe.” Wakaagana pale pale getini. Malon akabeba vile vyakula, akaingia ndani.

Bila kuoga, harakaharaka akapasha moto yale maziwa, mengine akayaweka kwenye friji. Akala kwanza, akashiba ndipo alipotoka kwenda kusafisha chumba kidogo cha nje ambacho walikitumia kama stoo. Alikiandaa ili awe anaishi hapo, ikitokea anapata mteja wakukodisha nyumba kubwa. Kiu ya bangi ikaanza kumsumbua. Akili ikavurugika kabisa, akaona atoke pale, akazungumze na mlinzi anayemlindia pale getini. Ili kama anayo hata kidogo, ampe. Akatoka kwa haraka mpaka pale getini. Akazungumza na mlinzi. Mwanzoni mlinzi akaonekana kuogopa. Akakataa. Alikuwa kijana tu. Karibu wanalingana na Malon. Malon akamuonyeshea pesa. Yule mlinzi akajua na yeye nimvutaji. Akampa. Moyo wa Malon ukafurahia sana.

Akarudi nyuma ya nyumba kule alikokuwa akisafisha. Akatafuta kivuli kabisa, akaiwasha. Alipotaka tu kuiweka mdomoni, akamkumbuka Naya. “Hii ndiyo imenikosesha kila kitu!” Malon akawaza. “Isingekuwa wewe, sasa hivi ningekuwa na Naya na maisha yangu mazuri tu. Umenipokonya kila kitu.”  Malon aliiambia ile bangi kwa kuumia sana. Gafla ile harufu ya bangi ikaanza kumkera sana rohoni. Akasimama na kuizima kabisa. Kisha akaifukia. Akatoka pale na kwenda kusimama mbali kidogo na pale alipoifukia. Mpaka yeye mwenyewe akajishangaa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

S

iku zilikwenda, wiki ya kwanza ikaisha, mwezi nao ukakatika, Malon hana kazi, hawezi kurudi kwao. Akashindwa kuwalipa ile kampuni ya ulinzi. Akabaki yeye peke yake. Hakusikia chochote kutoka kwa Tembe ambaye alishamtumia mawasiliano yake. Akajua bado hajapata mteja wa kukodisha nyumba yake. Njaa, upweke vikaanza kumsumbua Malon aliyezoea watu. Chakufanya ili kumuingizia pesa, hana! Biashara ilitaka mtaji. Anapata wapi mtaji? Nani wakumkopa na hakuwa na namba za simu za watu wengi na aliokuwa na namba zao kichwani wengine ni maadui waliokusudia abakie chini, ndugu wa karibu ndio hao wamemchangia kumtoa jela! Akabaki akifikiria.

Malon aliondoka kwao akiwa kijana mdogo sana. Akawa mtoto wakujitegemea. Hata wazo lakurudi kwao halikuwepo. Akakumbuka alipokuwa kijiweni, alijifunza ufundi wa magari. Alikuwa akitengeneza magari. Akazunguka kutafuta hata kazi yakutengeneza magari, nayo akakosa. Kupunguza garama za maisha, akazima kila kitu kwenye nyumba hiyo kubwa, akahamia kwenye nyumba ndogo. Akawa anatumia hicho chumba kimoja. Anawasha taa za nje tu. Tena usiku. Yeye mwenyewe akawa mlinzi wa nyumba yake. Usiku analinda nyumba yake, mchana anazunguka kutafuta kazi. Malon akaanza kulijua jiji la Dar kama Moro. Alikuwa akitembea kutafuta kazi bila mafanikio.

Hata wale aliokuwa akiwadharau akiona wanafanya kazi za kishenzi, alitafuta kazi zao, akashindwa kupata. Alikuwa kama ameingiwa mkosi. Hakuna aliyemwajiri, na hakuwa na uwezo wa kujiajiri. Hata mazoezi kitu anachokipenda sana akaacha sababu ya njaa. Akawa mtu wakutoka asubuhi, kwenda kuzunguka kutafuta kazi nakurudi jioni kabla giza halijaingia, kulinda nyumba yake. Akarudia maisha ya kukaa kijiweni. Akapata vijana waliomkumbusha mwanzo wa maisha yake akitafuta kutoka kimaisha. Na wenyewe wakafanana na yeye. Akaona watamfaa kipindi hicho hana chakufanya.  Akawa akishazunguka kutafuta kazi akichoka, anakwenda kukaa nao mpaka jioni. Wakianza kuvuta bangi, anaondoka kabisa hapo.

Jingine tena kwa Malon.

S

iku moja akiwa amekaa tu kijiweni na vijana wa jijini Dar, maana Morogoro hakurudi tena. Hapakuwa mbali sana na nyumbani kwake. Akapita kijana mmoja amevaa shati jeupe, suruali nyeusi, amefunga tai. Mchana, jua linawaka. Ameshika bibilia, anashuhudia. Wakaanza kumcheka pale kijiweni. “Sasa wewe huwezi kusema neno la Mungu mpaka ufunge tai na joto lote hili!?” Mmoja akamkejeli. “Basi hata kanisa lako likupe gari!” Wakaendelea kumtania, lakini kwa heshima kidogo kwa kuwa alionekana ni mstaarabu. Hakuna aliyemtukana. Malon akamwambia akae kidogo ili angalau afute jasho. Wakacheka. Malon akampa na maji ya kunywa aliyokuwa ameshika mkononi. Tena na yeye Malon alikuwa amepewa tu. “Ni ya bomba lakini!” Malon akamtahadharisha. Yule kijana akanywa kidogo, mengine akaoshea uso, akakaa pembeni ya Malon aliyempa maji na bado hakuwa amemkejeli.

“Nikuulize kitu?” Malon akaanza. “Karibu.” Yule kijana akamgeukia Malon. “Kuna mtu aliniambia mimi nina mapepo. Hebu niambie. Yaliingiaje na yanatokaje? Na je, nitajuaje kama ni kweli ninayo na nifanyeje ili yasiwahi kunirudia kama yapo?” Wale vijana pale wote wakamgeukia yule kijana huku wakicheka. “Mimi mwenyewe mama yangu wakunizaa ananiambia nina mapepo!” Wakaanza kutaniana vijana hao huku wakicheka, mpaka yule kijana akaanza kuzungumza nao maana ni kama Malon aliweka tena msisitizo wa maswali yake akitaka watulie wamsikilize akijibu. Aliongea nao kwa kimapana na mifano ya waziwazi. Wapi shetani hupenda kukaa, nini kazi zake. Zawadi zake na madhara ya kupokea zawadi zake. Jinsi ambavyo anapenda kutumikisha watu ambao ni wana wa Mungu.

“Shetani hana zawadi ya bure.” Akaendelea Gwamwa, kama alivyojitambulisha kwao. “Kazi yake shetani anapokuja kwenye maisha ya watu, kwenye bibilia kitabu cha Yohana 10:10 inasema ni kuiba, kuu, na kuangamiza. Atakuibia amani yako, mahusiano yako na watu wako wakaribu sana. Atahakikisha anakutenga na kukuacha peke yako sehemu ambayo ataweza kukufikia ili kukuangamiza kabisa. Atahakikisha anaangamizia furaha yako ya kweli na kukupa furaha ya vitu fulani fulani ambavyo furaha zake ni lazima ikugharimu sana kuipata, na pia huwa ni za muda tu.” Tarimu akaendelea.

“Inakuwa inakulazimu ufanye mambo fulani ili kuipata hiyo furaha. Atahakikisha anakupokonya uhuru wako kabisa. Hata kama utakuwa ukitembea nje na kuongea mambo mengi tu kiujasiri, lakini moyoni mwako utajua wazi huna ule uhuru wa nafsi. Yapo mambo atakufunga nayo tu. Atahakikisha unakuwa mtumwa wa hayo mambo aliyokuonyesha kama vile huwezi kuishi bila hayo mambo. Anahakikisha unaishi ukitumikia hilo jambo tu. Hiyo kiu tu. Hiyo tamaa ambayo unakuwa ulishamruhusu aitumie kwako.” Akaendelea Tarimu kwa lugha rahisi sana. Wote kimya kama alioanza kuwagusa.

“Halafu hataishia hapo, kabla hajakuua kabisa kwa kukuangamiza wewe mwenyewe baada yakuua nafsi yako, kama nilivyowaambia mwanzo kuwa anahakikisha anaua hata mahusiano yako na watu unao wapenda sana au wanao kupenda sana. Hufika umbali mkubwa sana wa wakufanya ukachukiwa na kutengwa kabisa na jamii. Si kwamba inatokea hivyo kwa bahati mbaya. Ni katika mikakati yake juu yako. Kwa yale atakayokutumikisha uyatende, yanakuwa chukizo kwa wakupendao au uwapendao kiasi ya kwamba hakuna jinsi wakakuvumilia. Niweke msisitizo hapa.” Tarimu akajiweka sawa.

“Niliwaambia anakutumikisha ufanye maovu yakutengwa?” Akawaona wote kimya. “Lengo lake la kwanza la kuiba, kuua linakuwa sasa limefanikiwa. Bado lile la tatu kuangamiza. Ameshakuibia marafiki, familia. Ameshaua nafsi yako. Umekufa katika haki mbele ya Mungu na jamii. Huna uwezo wakufanya tena mema. Ameua uhuru wako. Ameua kila kitu. Sasa ndipo lile jambo la tatu la kuangamiza ndipo linafuata. Atakutumia wewe vile atakavyo kwa kuwa ameshafanikiwa kukuweka kwenye upande wake. Umatekwa sasa. Hakuna anayekufikia tena kukurejesha, maana umechokwa, umeshindikana, kila mtu amekukatia tamaa. Huna nafsi iliyo hai. Huna ufahamu. Umekufa. Unayoyasikia na kuyatenda ni maovu tu.”

“Basi ndipo anaanza kuangamiza. Sio wewe tu, hata walio karibu na wewe. Atakutumia vile yeye atakavyo. Unakuwa ndio mtumwa wake yeye, akikutuma ufanye mambo ambayo hata baadaye ukishayafanya, ukikaa chini, unajishangaa kama ni wewe kweli umeweza kufanya hivyo au kumfanyia mtu jambo kubwa na baya la kiasi hicho! Lakini napo hata ukijutia, unakuwa huna jinsi yakubadilisha kwa kuwa umeshaharibu sana na huna huo uwezo. Ameshakufunga kupita kiasi hujui ni wapi pakuanza kujifungua ili kurekebisha msururu wa mambo mabaya aliyokusababisha kuyatenda pale alipokuachia kiu ya kufanya hilo jambo unaloshindwa kulala bila kulifanya, na kwa watu wanao kuzunguka maana umeshafanya kwa kurudia rudia mpaka wanajitenga na wewe na hawakuamini tena.” Hapo kila mmoja akabaki akijifikiria nafsi yake. Tarimu akaona wametulia. Mzaha tena hakuna.

“Lakini lipo tumaini kwenye andiko hilohilo la Yohana 10:10 linaloongelea kusudi la shetani kwa wana wa Mungu.” Tarimu akafungua ile bibilia aliyokuwa ameshika. Akasoma. “Yesu akamalizia hivi, lakini mimi nimekuja ili wawe na uzima, tena wawe nao tele.” Akawatizama. “Mimi ni shahidi wa mambo haya ninayowaambia. Nilikuwa teja kabisa wa pale kituo cha Fire. Nilishamwibia kila ninayemfahamu ndani na nje ya familia yangu. Hakuna aliyekuwa tayari kunifungulia mlango. Nilifika hatua, nauza mwili wangu ili tu, kupata pesa yakununua unga.” Wakamkazia macho na kujiweka sawa maana hakuwa kiendana kabisa na anayo zungumza juu yake.

“Niliteseka karibia ya kufa kwa maradhi au niseme magonjwa ya zinaa. Nilikuwa nikikaa sehemu, huwezi kupumua, jinsi nilivyokuwa nikinuka! Maisha haya ya kijiweni yalikuwa ni yangu na sikuwa na jinsi nyingine yakuishi ila hii kama nyinyi hivihivi. Hapakuwa na lugha safi na fasaha inaweza kutoka kinywani mwangu isipokuwa matusi tupu. Kufupisha habari yangu. Yesu ameniokoa. Amenisamehe dhambi, amenitakasa na kuniponya maradhi yote. Tena mimi mwenyewe nilikwenda kwenye mkutano palepale jangwani. Lengo lilikuwa nikutafuta hata mtu nimwibie, nipate pesa ya kula. Lakini nikakutana na mahubiri, yakutangaziwa kuwa huru. Yule muhubiri aliongea kama aliyekuwa akizungumza na mimi. Mimi sikuwa mkristo wala sikuwa namjua Yesu. Kwa vile nilivyokuwa nimechoka, nikakubali kuombewa niwe huru.” Akacheka.

“Nilipata nguvu ya ajabu ambayo sikujua ni nini kinaendelea kwa wakati ule. Walinisimulia kuwa nilitupwa mbali na pale jukwaani nilipokuwa nimesogea ili nisikilize anachozungumza. Nikalipuka mapepo, nusura nikimbie barabarani nikagongwe na gari ili nife. Walinikamata, nikaombewa na kuwekwa huru. Sijawahi kwenda kutibiwa chochote hata ulevi au ugonjwa wa zinaa niliokuwa nao kwa wakati ule. Lakini huyu Yesu siku ile aliniponya. Nikisema kuponywa, ni yote. Kijana mmoja, aliyekuwa akihudumu pale, alinichukua na kunipeleka kwake. Nikaoga kwa mara ya kwanza baada ya miaka mingi sana, nikala chakula kizuri na kulala kitandani. Hiyo ni baada ya miaka mingi sana yakulala nje tu nikitumiwa na ibilisi atakavyo.”  Wakabaki wamekodoa macho.

“Ni kweli kanisa halinipi gari, kwa kuwa nafanya hivi mimi mwenyewe kwenye siku ambazo siendi kazini. Nazunguka tu sehemu kama hizi zinazofanana na sehemu ambazo na mimi nilikuwa nikiishi nakuteswa na ibilizi. Lakini mimi sikuwa kama nyinyi hivi, eti na jioni mnapo pakwenda! Mimi nilikuwa nikikaa na kuishi sehemu kama hizi. Ndio maana nazunguka kujaribu kuzungumza na vijana kama nyinyi. Japokuwa nikiwaangalia nyinyi nawaona mpo bora sana kuliko vile nilivyokuwa mimi kipindi kile, mimi nilifikishwa pabaya zaidi, naomba Mungu asiwafikishe huko.” Akatulia kidogo kisha akaendelea.

“Nafunga tai sio kwa sababu nyingine yeyote, ni kwa sababu naweza tu. Nilishatamani sana kuwa msafi kama hawa watu waliosoma, wanaokwenda kwenye maofisi makubwa. Basi, siku ambazo na mimi huwa siendi kazini, navaa shati nakufunga tai.” Wakacheka. “Kwani unafanya kazi wapi?” Mmoja akauliza. “Nafanya kazi kwenye kampuni moja ya ulinzi. Ni mlinzi. Tunalinda kwenye mabenki, sonara, majumba ya watu wenye pesa. Inategemea unapangiwa wapi.” Malon akawa amevutiwa sana na yule kijana. Wakauliza maswali mengi sana. Yeye Malon akataka zaidi. Akamuomba aongozane naye mpaka nyumbani kwake. Tarimu akakubali wakaondoka hapo. 

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

 “Naitwa Malon, na hapa ni nyumbani kwangu, japo naishi kinyumba cha uwani.” Tarimu akamtizama tena Malon. Alikuwa amechakaa Malon, kama siye yeye Malon na hata hakuwa akifanania kama mmiliki wa hiyo nyumba. Hata Naya angekutana naye, asingemtambua. “Na mimi naitwa Tarimu kama nilivyowaambia pale kijiweni.” Akajitambulisha tena. “Sikubadilisha jina langu. Sasa kwa nini unaishi kwenye chumba kidogo wakati unayo nyumba nzima?” Tarimu akauliza baada ya kuingia kwenye kile chumba. Ndipo Malon akamueleza historia yake kwa ufupi.

“Katika walioibiwa mahusiano, basi mimi ni mmoja wao. Shetani ameniibia msichana mzuri sana. Kwa jinsi nilipokuwa nimefikia, nisingekuwa mtu sahihi kwake. Tamaa ya bangi ilikuwa ikinitesa. Na kila nilipokuwa nikivuta, ilikuwa ni lazima kulala na wanawake. Nimemuumiza sana Naya.” Akampa historia yake Naya, Malon huyu, alikuwa mchovu. Akieleza kuwa yeye alimsomesha Naya, usingeamini.

Tarimu akazungumza naye tena. Akampitisha kwenye mafundisho mengi. “Kwani wewe unaweza kuniombea?” Malon akauliza. Taribu akacheka. “Kabisa. Nataka uweke imani yako kwa Yesu, Malon. Haujafika umbali niliofika mimi. Na bado Mungu aliniokoa! Hata wewe anaweza kukusaidia.” Tarimu akaanza maombi. Ni kweli Malon alikuwa na mapepo. Akashangaa hakutumia hata muda mrefu, mapepo kwa Malon yakatoka. Akawekwa huru. Alimuongoza sala ya toba. Akamwachia ile bibilia yake.

“Huyu atakuwa mwalimu wako wa pekee na mkubwa sana. Huwezi amini nguvu iliyokuwepo kwenye hiki kijitabu tu. Ukiwekeza muda wako hapo. Hata kidogo tu. Soma utakuja kunishuhudia siku moja.” “Nitaelewa kweli?” “Yaani wewe soma. Soma tu. Utashangaa ule uwelewa wako unavyobadilika. Ipo nguvu ya ajabu sana kwenye hicho kijitabu. Kina nguvu ya kufungua ufahamu na kumuweka mtu yeyote wa namna yeyote, huru. Hata kama fahamu zako zimefungwa kwa upana wa namna gani, basi hiki kitakuweka huru. Kesho nitaingia kazini asubuhi. Na kesho kutwa. Ila baada ya siku mbili, nitakuja hapahapa kukutembelea.” Malon akabaki akipekua ile bibilia. Tarimu akamuachia pesa kidogo, akatoka.

Malon hakulala siku hiyo. Alibaki akisoma ile bibilia. Kulikuwa kuna furaha fulani ndani yake. Lakini hofu ya kurudia yale maisha ya zamani yaliyopokonya furaha na utu wake ikaanza tena na kutaka kuanza kumpokonya hata furaha mpya aliyopokea. Shetani akimnong’oneza jinsi atakavyoshindwa. Akamkumbusha vile alivyokuwa akijitahidi na kunuia kuacha lakini akawa akishindwa. Akawa akimkumbusha tena na tena vile ambavyo haitakuwa tofauti hata safari hii. Lakini Malon akaendelea kusoma tu ile bibilia na kukutana na majibu mengi sana humo ndani yaliyoanza kumpunguzia hofu. 

 Siku ya Mahafali Ya Naya.

N

aya na familia yake waliwasili mjini Morogoro mapema tu, wakaelekea Mzumbe chuoni alipohitimu Naya miezi mitano na siku kadhaa zilizopita. Hakuwa amealika watu wa nje ya familia yao isipokuwa Joshi ambaye familia nzima walimtarajia kuwepo hapo mapema tu kwani walishaanzisha mahusiano zaidi ya salamu na Naya. Joshi alishawatembelea kanisani kwao mara kadhaa. Kwa haiba yake ya utulivu na kwa kuwa alikuwa mcha Mungu na elimu aliyokuwa nayo, mama yake Naya alimpenda sana Joshi. Hakuacha kumtaja hapo nyumbani kwao na kumzungumzia mara kwa mara ili tu, Naya amfikirie kwa ndoa. Alishamkaribisha hapo nyumbani kwao mara kadhaa. Joshi alishakwenda na kuwepo nyumbani kwa kina Naya, Kiluvya akipata mapokezi mazito kutoka kwa mama Naya ambayo hata Malon hakuwahi kuyapata. Lakini baba yake alimjua Naya. Jinsi alivyokuwepo na Joshi, sivyo alivyokuwepo na Malon. Ni kweli Naya alibadilika kwa kiasi fulani. Joshi hakufanikiwa kumchekesha tena kama siku ile. Alikuwa akicheka, lakini sio kama zamani. Aliongeza utulivu hata kwa baba yake alikuwa mkimya sana.

Siku hiyo ya mahafali yake alikuwa amejitengeneza vizuri, akapendeza kwenye joho lake. Mahafali yakaanza. Wakatakiwa kujipanga kwenye viti vyao. Naya akakaa pale, akawa ameinama. Kwa kuwa baba yake alikuwa hawezi kuweka macho yake kwengine kama yupo Naya, muda wote alikuwa akimtizama alivyoinama. Walipotakiwa kusimama akasimama, walipotakiwa kukaa alikaa. Wakaitwa majina mmoja mmoja kupokea vyeti, akaenda. Mama yake alikuwa amechangamka kuliko hata Naya mwenyewe. Zayoni ndiye aliyekuwa akipiga picha.

“Mwanao picha zote ameinama.” Akamnong’oneza baba yake. “Ona!”  Akaanza kumuonyesha picha alizompiga dada yake. Na zote alikuwa ameinama. “Kasoro hii moja tu aliyokuwa akienda kupokea  cheti.” Akaendelea kumuonyesha. “Tutamwambia anyanyue kichwa baadaye.” “Sasa mbona hafurahii wakati amefaulu vizuri? Kwani wewe ndio umemlazimisha kuja kwenye mahafali yake?” Baba yake akampa jicho hilo, akajua ndio anyamaze. Akajirudisha kwenye kiti chake akatulia.

Wakati wanakaribia kumaliza, Joshi akaja. “Nimepitwa nini?”  Akaongea kwa sauti ya chini, akiuliza familia hiyo iliyokuwa imekaa pamoja. “Wanamalizia tu. Vipi?” “Shikamoo mama. Nilitingwa kazini, hivi nimelazimishia tu kuja.” “Pole.” Wakaendelea kuzungumza kwa sauti ya chini. Wakatulia wakati wanamalizia. Ikaisha, Naya akawasogelea. “Joshi!”  Akashangaa kumkuta Joshi pale. “Nimechelewa kazini. Tulikuwa na mambo mengi, lakini nikalazimishia tu.” “Asante kwa kuja.” “Hongera mama.” Baba yake akampongeza. Naya akacheka kicheko cha kawaida sana. “Asante baba.” Mama yake naye akampongeza. “Njoo ni kukumbatie mwanangu. Hongera sana mama.” Naya akacheka, akamsogelea mama yake, akamkumbatia wakati mdogo wake anapiga picha.

Wakapiga picha nyingine ya pamoja. Wakati wamesimama, wakamuona Naya amegeukia upande mwingine ameduaa. Wote wakageukia ule upande. Wakamuona Malon amesimama kwa mbali anawatizama. Alipoona wote wamemuona, akapunga mkono. Naya akabaki ameduaa kama wenzake. Malon alikuwa amebadilika sana kama sio yeye! Amekonda na kweli amekuwa mweusi haswa kama alivyomwambia Naya kipindi wanaanzana na Naya hakumsadiki kuwa huwa akiishiwa hubadilika mpaka rangi ya mwili wake!

Akapunga tena mkono, akawasogelea pale huku akimtizama Naya. “Hongera.” Aliongea taratibu, Naya akainama. Ndipo akasalimia kila mtu kwa kumshika mkono. Malon huyu alikuwa na hali mbaya ya muonekano kuliko hata alivyotoka jela. “Umekuja kwenye graduation ya nani?”  Baba yake Naya akauliza. “Nilikuja kumpongeza tu Naya. Sikutaka kusumbua.” Naya akamwangalia akiwa amekunja uso kama haamini. “Kumbe ulikuwa hapa muda mrefu!?”  Akauliza tena baba yake, wengine wakiwa wanashangaa tu. Malon alibadilika, akawa mtulivu sana. “Ndiyo, nilifika mapema.” Malon akajibu, Bale alikuwa kimya akimtizama kwa mshangao haswa.

“Basi naomba niwaage. Ili niwaache muendelee kusherehekea.” “Huna haja yakuondoka Malon. Tumekuja na soda kidogo, na keki. Ungesubiri tule.” “Nashukuru baba. Lakini naingia kazini usiku. Inabidi niwahi tu. Maadamu nimehudhuria shuguli nzima ya muhimu ya mwanzoni, huko kwengine mfurahie kwa niaba yangu.” Naya akamtizama tena kama asiyeamini.

Muda wote huo alipowasogelea tu Malon, mama Naya alikuwa kimya kabisa hakuongeza chochote kwa yeyote akabaki kimya tu wazi akionyesha kuingiliwa lakini pia akawa kama akimkumbusha Naya na baba yake juu ya alichozungumza kuhusu Malon. Ukweli mama Naya hakuwahi kumkubali Malon tokea alipojua tu ni mfanyabishara asiye na elimu. Kilio cha mama huyo ni Naya aolewe na mwanaume aliyesoma. Hata kama hana pesa kama huyo Joshi mwenye elimu tu ila hana pesa kama alizokuwa nazo Malon, lakini yeye alimpenda kwa haraka sana pale alipojua amesoma, na ni muhasibu kwenye kampuni ya wanasheria.

Alishamwambia Naya kuwa hatakaa akalala njaa kama ambavyo angeolewa na mfanyabiashara kama yeye, yaani vile alivyoolewa na baba Naya. Wakati wote alisema biashara huwa na mtindo wa kufa na mtu kufilisika, lakini mwenye shule kichwani, hata akifukuzwa kazi, anaweza pata kwengine. Au mwenye shule anaweza kuajiriwa na kuwa na biashara pia. Lakini si biashara bila elimu. Sasa siku hiyo pointi yake ikathibitishwa pale alipotokea Malon aliyekuwa anayopesa haswa, lakini amechoka vile, akatamani kimuingie Naya vizuri na kuelewa alichokuwa akizungumzia.

“Huu ni mzigo wako Naya. Hongera sana. Am so proud of you.” Akaongea Malon kwa tabasamu, akimkabidhi Naya mfuko mzuri maalumu kwa zawadi. Naya akapokea na kushukuru.  “Asante kwa kuja.” Malon akacheka kidogo. “Muwe na wakati mzuri.” Malon akaaga na kuondoka. Naya akaanza kulia. Alijifuta machozi tena na tena. Akainama akiwa ameshika mfuko aliokuwa amekabidhiwa na Malon. Ukimya ukatanda kwa muda. Ni kama walimuona mzimu wa Malon. Kila mtu alibaki akiwaza lake. Naya akampa baba yake ule mfuko, na yeye akaaga. “Nitarudi baada ya muda mfupi.” Naya akaondoka.

Baada ya muda, Naya alirudi akiwa ameosha uso na ametulia kabisa. Wakakata keki, wakanywa na soda, wakaamua kuondoka pale wakatafute chakula sehemu nyingine. Joshi alikuwa amekuja na gari yake. Bale akapanda gari ya Joshi, wakaondoka mjini Morogoro. Naya alikuwa ametulia kwenye gari. Akavuta ule mfuko aliokuwa amekabidhiwa na  Malon. Akakuta kadi ya kumpongeza. Akasoma maneno yake, chini akakuta Malon ameandika jina lake. Akakuta na barua ndani akaifunua.

‘Naya, inawezekana sijakupongeza vyakutosha. Hongera sana kwa kuwa makini na mzuri kwenye kufikiria. Wewe ni zaidi ya hicho cheti walichokupa leo. Unao uwezo mkubwa sana ndani yako. Nimeishi na wewe, nimekuona. Hujawahi kujaribu jambo ukashindwa. Shule yako na mambo mengi unayofanya hujawahi kushindwa, wewe ni shahidi wa hayo yote.’ Naya akakumbuka ni kama maneno aliyomwandikia na yeye.

‘Nakushukuru kwa kujali kwako. Na msimamo ulioonyesha kwenye maisha. Wewe ni mdogo kwangu, lakini nimejifunza mengi mno kutoka kwako. Umekuwa sababu ya kubadilika kwangu. Najua unaweza ukashangaa vile nilivyo sasa. Lakini Naya, ninayo amani ya ajabu. Yesu amenisamehe na kunitakasa. Huwezi amini niliweza kuacha bangi bila hata matibabu. Nimewekwa huru. Kwa kichache nilichonacho, nalala kwa amani. Maisha yangu yamebadilika Naya.” “Haaa!” Wakamsikia Naya akishangaa kwa sauti ya juu huku akilia. Wote wakamgeukia kasoro baba yake aliyekuwa akiendesha, akamtizama kwa kupitia kioo.

‘Naomba iwe hiyo ndio zawadi yako kwa leo Naya. Furahia pamoja na mimi. Mungu amenibadilisha. Yale yaliyokuwa magumu kuyafanya, Mungu ananiwezesha. Najua ndio yalikuwa maombi yako, Mungu amefanya. Natamani ningekuwa na pesa nikakununulia kitu kizuri sana, lakini kwa sasa mambo hayajakaa sawa. Naomba upokee kidogo nilichokuletea.’ Naya akajifuta tena machozi. Na kuinama. Ili kutafuta hiyo zawadi. Akakuta sheni nzuri ya dhahabu. Ilikuwa nyembamba tu. Wazi ilionyesha ni ya bei ndogo. Naya akaina nakuanza kulia tena. Alilia huku ameshika ile cheni mkononi. Mdogo wake kimya, pembeni yake.

Baada ya muda, akaendelea kusoma. ‘Nilipata kazi ya ulinzi. Ndio hapo nipo kwa sasa huku nikitafuta mteja wakupangisha ile nyumba. Nakusanya pesa ili nije kurudi Dubai. Nafikiria nirudie ile bishara ya sukari, bado naamini italipa tu. Namuomba Mungu anifanikishe katika hilo, ili angalau mambo yawe marahisi zaidi kwa upande wa kifedha. Ni hayo tu. Nimeona nikushirikishe pale nilipo kwa sasa. Nakutakia kila la kheri. Nakuombea mchana na usiku, ufanikiwe. Malon!’

Naya akainama nakuendelea kulia taratibu. Kilichosikika ni mlio wa kuvuta kamasi tu. Alilia Naya, nakushindwa kujisaidia. Walifika jijini Dar. Kwenye hoteli nzuri ambayo walichagua kwa ajili yake ili wapate mlo wa pamoja kama familia na huyo Joshua, kama kumpongeza Naya kwa kuhitimu, lakini walifika pale Naya akilia nakushindwa hata kutoka garini.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment