Kwa Malon.
A |
kiwa ndio
amefika tu jijini, yupo kwenye chumba chake hicho akibadili nguo kutoka
alizokuwa amevaa na kuvaa sare za kazi, akasikia simu yake ikiita. Alikuwa
Tembe. “Mpaka nimekusahau Tembe ndugu yangu! Upo mheshimiwa?” “Nipo. Vipi
ile nyumba yetu, ilipata mtu?” “Bado kaka. Vipi, umepata mteja nini?” Malon
akauliza huku akiendelea kujiandaa kwa haraka asichelewe kazini. “Naona zitakuwa
habari njema sana. Yupo dada, amerudi nchini na mtoto mmoja, anatafuta nyumba
yenye mazingira kama yako kabla hajaanza kujijenga upya hapa nchini. Anaonekana
alikuwa masomoni huko nje ya nchi,
ndio amerudi na huyo mtoto. Si bado vifaa
vipo?” “Njoo uitazame kesho kwenye mida ya saa 4 asubuhi.” “Basi nitakuja na
bosi wangu. Ndio anahusika na hao wageni. Na nimemwambia umeahidi utamkatia
pesa kidogo.” “Tutazungumza tukionana.” Wakawekana sawa katika hilo, Malon
akaaga ili kuwahi kazini.
Alikwenda kazini akiwa amejawa tumaini. Ni kweli alifanya kazi
hapo kwa takribani miezi miwili. Pesa aliyokuwa akilipwa, alikuwa akikusanya
huku akijinyima sana. Hakuwa akilipwa mshahara mkubwa. Ilipokwenda kwenye
mahafali ya Naya, akachukua asilimia 85 ya pesa yake aliyolipwa mshahara, akamnunulia
yeye hiyo cheni ya dhahabu. Kwa hiyo ni kama alijimaliza kabisa kwenye akiba
zake. Alifika kazini akiwa na wenzake wanne. Wao walikuwa wazoefu. Usiku huo
walikuwa wakilinda sehemu wanayouza magari. Waligawana wawili wawili, wakapeana
zamu yakuzunguka.
Malon alikuwa amepoa sana. Sura ya Naya akiwa ameinama wakati wote
pale kwenye mahafali yake haikumtoka. Aliwahi mapema tu pale chuoni Mzumbe.
Japokuwa watu walikuwa wengi, lakini alitafuta sehemu ambayo aliweza kuona kila
kitu kinachoendelea. Tokea Naya na familia yake wanaingia pale, aliwaona. Macho
yake yakaweza kufikia alipokuwa amekaa Naya. Naya aliyemuacha mara ya mwisho
siye huyu aliyemuona kwenye yale mahafali. Alikuwa amepoa haswa. Hata Joshi
alipoingia, pia alimuona. Alikuwa akiangalia kila kitu, huku akijiuliza kama
akasalimie au amkabidhi vile vitu mtu, akampe Naya bila yeye kujitokeza! Akiwa
anajiuliza, ndipo Naya akamuona. Na hata alipoaga kuwa anaondoka, pia alikwenda
kujificha mbali kuangalia kinachoendelea baada ya pale. Alimuona Naya akilia.
Usiku huo walimfurahia Malon hapo kazini. Maana alikuwa akizunguka bila
kuchoka.
Wenzake walipeana zamu za kulala, lakini sio Malon. “Naya!” Malon aliwaza na kuvuta pumzi
kwa nguvu. “Mungu nisaidie. Fanya muujiza.
Nifungulie milango. Nibariki tena.” Malon aliomba huku akizunguka. “Nitendee lililokubwa sana. Mpaka watakaosikia,
wakajue upo Mungu mtenda miujiza. Usimsahau Naya wangu. Mfariji, mtunze.” Malon
aliomba karibia usiku kucha. Malon huyu mlinzi, hata akisema anamfahamu Naya,
watu wasingemwamini. Naya alionekana wajuu sana. Alikuwa amechoka kwa kujinyima
chakula, akifunga na kumuomba Mungu amfungulie milango tena, ila afanye
biashara halali tu si haramu kama alivyofanya ile ya bangi na kumfanikisha kwa
haraka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Asubuhi baada yakutoka kazini akarudi nyumbani kwake. Alijitupa
akiwa na usingizi, mpaka simu ya Tembe ilipoita tena. Akashtuka. “Tupo getini.” Malon
alikurupuka na nguo zake za kazi vilevile. Akatoka. Alikutana na Tembe na
mwanaume mwingine, yeye alikuwa mdogo kidogo kwa Tembe. “Ulisema unanikutanisha
na mwenye nyumba, sio mlinzi Tembe. Sina muda wakuzunguka.” Malon alimsikia
yule kijana akilalamika kwa kiburi cha pesa. “Aliniambia yeye ndiye mwenye
nyumba.” Malon alimsikia Tembe akijibu kama asiye na uhakika. Akawafungulia
geti na kuwakaribisha ndani.
Kwa muonekano wake na maneno aliyoanza kuzungumza, Malon akajua
hata akimpa mkono, asingekubali salamu ya kupena mikono, akaona awe mpole tu.
“Karibuni.” Malon akasimama akiwatizama. “Tunataka kuzungumza na mwenye
nyumba.” Akaongea yule kijana. “Ndiye mimi, karibuni. Niwasaidie nini?” “Unazo
karatasi zote na upo tayari kuandikisha kisheria? Maana sitaki utapeli. Watu
watakao kuja kuishi hapa sio wababaishaji. Sitaki ubabaishaji.” “Hata mimi
ningependa iwe hivyo. Ninaye mwanasheria ambaye atatusaidia kuingia kwenye
mkataba mzuri tu. Usiwe na wasiwasi. Lakini kabla hatujafika huko, karibuni
muangalie ndani. Ili muone kama ndio kitu ambacho mnatarajia.” Malon
akatangulia kufungua geti la kwanza lakuingilia ndani. Uzuri alikuwa akiishi
hapohapo, kila wakati alikuwa akisafisha. Kwa hiyo nyumba ilikuwa safi sana,
japo kulikuwa na joto.
Ni ijumaa tu alikuwa humo ndani akisafisha na kuomba Mungu
amkumbuke na amtafutie mteja. Kwa hiyo hata alipofungua milango, alifungua kwa
kujiamini. “Kuna AC humu ndani kweli!” Akauliza
yule kijana ambaye ndiye bosi wake Tembe. “Ipo, na inafanya kazi. Nimezima kwa
sababu hakuna anayetumia hii nyumba.” Malon mtoto wa mjini, na mfanyabiashara.
Lugha ya biashara aliijua, na alikuwa mjanja. Dharau za yule bwana ilikuwa ni
asili yake kabla hajafikishwa hapo na maisha pamoja na rehema za Mungu. Akamzungusha
mle ndani akizungumza naye, mpaka wanamaliza, yule kijana yeye mwenyewe
akajishusha nakuanza kucheka na Malon akitaka mpaka wagonge. Malon akajua
amependa nyumba. Lakini alitaka wao walipwe asilimia 15, sio 10 kama
walivyozungumza na Tembe.
“Nakulipa pesa ya mwaka Malon! Pesa taslimu!” “Ndivyo
nilivyotarajia ndugu yangu. Nikisogea sana, ni asilimia 12, tena hapo ni kwa
kuwa siwapi chumba cha nje na mimi mwenyewe ndio nitalipia huduma za kisheria.
Sitaki mikataba ya hovyo.” Kwa kuwa Malon alishajua amepapenda pale na vitu
vyake ni vya kisasa, hakubabaika. Akajua hata akiondoka, atarudi tu.
Lakini akashangaa anataka wamalizane kisheria ili ampe pesa. Malon
akampigia simu Mati, akampa hiyo kazi. Mati akamwambia asubuhi hiyo ana mambo
mengi sana. Atakuwepo hapo ofisini jioni, ataandaa kila kitu, kesho yake ndio
afike hapo ofisini yeye kwanza na nyaraka za hiyo nyumba. Tembe na bosi wake
wakasikia. Wakaafikiana kutafutana baada ya hapo. Wakaondoka na kumuacha Malon
akiomba Mungu. Aliufunga ule mkataba katika ulimwengu wa roho huku akiomba
chochote kisitokee. Hata dhuluma au kubadilika kwa mawazo. Maana ni kweli
waliipenda ile nyumba na wakabaki wakimuuliza Malon ni wapi alinunua vile vifaa
vya mle ndani.
Pesa.
M |
paka inafika
siku ya jumatano jioni, Malon alishakuwa na pesa yake benki na amekabidhi funguo
za nyumba. Hakuna jinsi Malon angeeleza furaha yake na shukurani yake kwa
Mungu, mtu akamuelewa. Alipopata tu ile pesa kwa kuwa alishafanyia uchunguzi
biashara yake ya sukari nchini Dubai, na wateja wake walikuwepo, akataka kwenda
na Cocoa. Aliulizia soko huko. Akaambiwa kama atapeleka Cocoa grade A, basi
itapokelewa. Hilo likamtia moyo, na akawa ameshatafuta mtu wakutokea Mbeya.
Akamwakikishia Cocoa nzuri. Malon akaaga kazini na kuondoka akiwa hana uhakika
wa hiyo nafasi ya kazi pindi atakaporudi.
Kitu cha kwanza akaenda benki kukopa pesa. Akaweka dhamana hiyo
nyumba, akaongezea na pesa ya kodi, akaenda Mbeya, Kyela mpaka mashambani kwa
wakulima. Alikaa huko karibia majuma mawili akikusanya Cocoa nzuri huku
akiwasiliana na watu wa Dubai. Kwa kuwa haikuwa mara yake ya kwanza kusafirisha
bidhaa hasa mazao nchini huko, ikamuwia rahisi. Alijua ni bandari ipi atumie.
Nani wakumsadia kutoa pindi mzigo wake utakapofika huko. Akaweka mambo sawa
akiwa bado yupo huko huko Kyela kwa wakulima. Akapenda na mchele. Akakusanya
kidogo tu kama kujaribu bahati yake akifika Dubai.
Akakatia ushuru na kulipia kila kitu. Safari hii hakufanya magendo
kabisa. Alitaka kila kitu chake kiwe cha halali. Baada ya majuma mawili akawa
anarudi Dar na mzigo wa Cocoa na mchele. Akaelekea bandarini yeye mwenyewe na
makaratasi yote. Akapakia mzigo wote na kupigia simu watu wa kule. Alikuwa
amebakiwa na pesa kidogo. Akaanza kuzunguka maduka ya mchele, akionyesha mchele
wa Kyela. Akawaambia anao na anaweza kuwauzia kwa bei ya jumla. Akakusanya oda
kwenye maduka kadhaa, akarudi tena Mbeya. Wakati huo anasubiri mzigo wake ufike
Dubai, aufuate.
Akakusanya mchele, karudi nao yeye mwenyewe Dar na kusambaza siku
hiyo hiyo, kwa kuwa hakuwa na sehemu ya kuhifadhi na dereva wa Lori
alishamwambia nilazima washushe mzigo siku hiyo hiyo. Mpaka anamaliza kushusha
mzigo, Malon akawa ameingiza pesa nzuri sana. Hakuamini. Alirudi kwenye chumba
chake, akabaki akicheka. Wageni wake walishahamia. Kwa hiyo tayari walishaweka
ulinzi pale wa masaa 24, ila kwa garama zao wenyewe, sio Malon. Ikawa kama
mchezo hivi. Akaona akajaribu kutafuta tena soko la mchele. Tena alijiambia
anajaribu tu. Hana chakupoteza sababu anasubiria kwenda Dubai kwenye kazi
kubwa.
Siku hiyo nayo alitoka amefunga. Hakula kitu wala kunywa.
Alielekea benki kupunguza deni ili riba isiwe kubwa sana, akaanza kuzunguka.
Akashangaa anakutana na wauzaji wanaolalamika kuwa watu waliokuwa wakiwaletea
mchele wameacha sababu ya ugumu wa maisha. Malon hakuelewa maana yake. Maana
alipokuwa akiutoa huo mchele, huko Kyela, ilikuwa mashambani, na ulikuwa
mwingi. Na wao walimuuzia kwa bei ya chini, wakisema maisha ni magumu wapate
pesa kidogo tu. Hakupoteza hata muda. Kesho yake, akarudi tena Kyela. Akaingia
mashambani na vijijini kwenye maghala ya watu. Malon mfanyabiashara, aliyejawa
na maombi. Akapata kibali kwa wanakijiji wengi. Alikonunua mwanzoni,
wakamtambulisha na kwa wengine. Akakusanya mzigo, baada ya juma moja, akarudi
tena mjini na mzigo. Akauza wote, akapata pesa yake. Malon akabaki akijiuliza,
ni nini kinamtokea.
Ilikuwa kufumba na kufumbua, Mungu anamtendea jambo la ajabu na
kubwa. Tayari akaunti zake zikaanza kuwa na uhai. Angalau kukawa kuna jambo linaendelea
kwenye maisha yake. Akarudi chumbani kwake, pembeni ya kitanda, akapiga magoti,
akamshukuru Mungu kwa machozi.
I |
likuwa siku
ya alhamisi. Malon aliamka asubuhi, akaamua kwenda nyumbani kwa kina Naya.
Alinunua baadhi ya vitu vyakupeleka. Kwa asili, Malon alikuwa mtoaji. Na linapofika
swala la Naya, hajui kubania. Hakuwa na uhakika kama atamkuta mtu hapo nyumbani
kwao Kiluvya. Akagonga mlango wa hapo mbele, hakuna aliyeitika japo alisikia
redio ikimba ndani. Akaacha hapo mizigo, akazunguka nyuma ya nyumba. Akamkuta
Naya, baba yake na kijana wa ng’ombe wakiosha ng’ombe. Baba yake Naya ndiye
aliyemuona wa kwanza, akamwambia Naya ageuke. Naya akabaki ameduaa.
Malon aliwasogelea na kuwasalimia. “Mikono michafu hii baba. Ina
dawa ya kuua kupe.” Akaongea baba Naya. “Acha niwasadie.” “Usisumbuke kabisa.
Utaingia uchafu, utashindwa kabisa kurudi kwako. Hata hivyo tumebakisha kidogo
tu. Karibu ndani utusubirie, tutakuja baada ya muda mfupi tu.” Naya kimya.
Alikuwa amevaa buti za mvua, amebeba mgongoni galoni kubwa la dawa ya kuoshea ng’ombe,
na mkononi ameshikilia bomba ambalo alikuwa akinyunyuzia ile dawa kwa ng’ombe. Malon
akamtizama, akakwepesha macho na kuendelea na kazi yake. Malon alikuwa
akimtizama akifanya ile kazi bila shida na alionekana ni mzoefu nayo.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Naya alimwambia kila kazi anayofanya baba yake, na yeye anaijua
kuifanya tokea mtoto. Kwani mara zote alikuwa akienda kucheza pembeni ya baba
yake na ndipo alipozijua hizo kazi. Ikatokea hivyo hivyo na kwa Bale. Alipenda
kucheza pembeni ya mama yake. Ikawa tofauti. Naya alijua mpaka kubadili tairi
la gari. Mzuri sana kwa kazi za mkono, za nje. Sio ndani. Afadhali kaka yake
Bale, alijua zote zote, lakini kwa kuwa walikuwa wakigombana na Naya kila
wakati, usingewakuta wawili hao sehemu moja. Kwa hiyo wakakua Naya yupo nje na
baba yake wakati wote, Bale na Zayoni ndani na mama yake.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Malon hakuondoka pale. Akabaki amesimama tu akiwaangalia
wanavyofanya ile kazi mpaka wakamaliza. Walitoka hapo kujisuuza na kusuuza
vyombo vya ng’ombe. “Leo hukwenda kazini? Au unaingia usiku tena kama siku
ile?” Baba yake Naya akauliza wakati yeye na Naya wakiosha miguu. “Ilikuwa kazi
ya ulinzi. Niliacha.” Alijibu Malon kwa kifupi tu, Naya akamtizama nakuendelea
na kujisafisha. “Ulipata kazi sehemu nyingine?” “Mungu alinifungulia milango ya
biashara.” Ile kauli aliyozungumza Malon, ikamfanya baba Naya asimame na
kumtizama Malon.
“Umebadilika sana Malon! Sio muonekano wa nje. Hapana. Upo
tofauti.” Malon akacheka. “Nilikutana na Yesu, baba. Nilifungwa na nguvu za
giza. Niliombewa na kuwekwa huru. Nafikiri mabadiliko haya ni lile pumziko la
ndani. Unakumbuka mara ya mwisho kuzungumza na mimi ukaniambia nahitaji
mapumziko?” Malon akauliza na kuendelea. “Wakati ule nilikuwa sielewi kabisa.
Ila sasa hivi naelewa. Japokuwa huu mwili umechakaa sio kama nilivyokuwa
zamani, ila nimepata pumziko la ajabu sana. Ipo amani hata katika kukosa, au
kupungukiwa vitu hivi vya nje. Ile hali ya wasiwasi sana imepungua. Sina hofu
yakukamatwa na polisi. Sina hofu ya kuingiliwa niibiwe. Nalala usingizi mzuri.”
Baba Naya akacheka.
“Juzi nilikwenda Morogoro kwenye ile kesi yangu, hata mimi sikuwa
najiamini ile hali ya utulivu Mungu aliyokuwa amenijalia. Sikuwa najua litakalo
nikabili. Nani atakuja kutoa ushahidi gani. Lakini niliamka mapema tu, nikaenda
mpaka mahakamani. Nazungumzia ile amani na utulivu wakujua sio mimi tena
ninayeishi, yupo anayepambana vita yangu. Huwezi amini baba,” “Eeeh!” “Nilikaa
pale. Kesi yangu ikatajwa, hakuna shahidi hata mmoja aliyejitokeza, hakuna
wakunishitaki. Tumebaki mimi, Mati na hakimu tukiangaliana. Mwishowe hakimu
akaniruhusu niondoke, kesi imefutwa. Nilimshukuru sana Mungu kwa kunifutia ile
kesi.” “Hongera sana Malon. Hongera sana.” “Nashindwa hata kusema asante baba
yangu. Hakika ni Mungu tu.” Wakati Malon akiongea na baba yake, Naya aliyekuwa
amesimama nyuma ya baba yake akisikiliza, akaondoka kurudi ndani. Malon na baba
yake Naya wakazungumza kidogo, wakarudi na wenyewe ndani.
Walikuta Naya alishaingiza ile mizigo ndani, lakini ameacha sebuleni.
Baba yake Naya akaona. “Kumbe ulikuja na mizigo?” “Nauza mchele. Huo ni mchele
wa Kyela kabisa. Mzuri sana. Nimewaletea na mafuta ya mawese yale ya wenyewe
kabisa.” Wakacheka. “Asante sana.” Malon alikuwa amenunua na vitu vingine, sio
ule mchele na mafuta tu. Alileta na unga wa ugali, maharage, sukari, mafuta ya
kupikia kwenye dumu kubwa kabisa la lita 20 na chumvi. Akakaa wakati wenyeji
wake wameenda kuoga.
Baada ya muda, Naya akatoka. Akaenda kukaa pembeni yake. Malon
akamsukuma kidogo kwa bega lake. Naya akamwangalia macho yakiwa yamejaa
machozi. “Umekula?” Naya
akamuuliza. “Nitakula jioni.” Naya akaelewa amefunga. Akanyamaza. “Umechoka?”
Malon akamuuliza. Naya akatingisha kichwa kukataa. “Una kazi gani baadaye?”
“Sina. Niliacha kwa Ino. Na zile za matangazo waliingiza mambo ya mapenzi, baba
akaniambia niache. Ndio nipo kwenye kutafuta kazi.” Malon akambusu kichwani.
Naya akainama. “Naomba unisindikize Morogoro.” Naya akanyanyua kichwa na
kumtizama. “Hatutakaa sana. Naenda mahakamani kufuatilia pesa ile uliweka
dhamana. Kwa kuwa sikushitakiwa mahakamani, na kesi imefutwa, natakiwa
kurudishiwa. Nilienda mara ya kwanza, wakaniambia nirudi leo. Halafu tutaenda
kumuona mama, tunarudi.” Baba yake Naya akatoka akawakuta wamekaa.
“Sasa mama, si ungemwandalia mwenzio chai!” “Amefunga.” Naya akajibu moja kwa moja na kujifuta machozi. “Umekubali?” Naya
akatingisha kichwa na kumwangalia baba yake. “Nini?” “Nimemuomba anisindikize
Morogoro, hatutachelewa kurudi.” “Kwema?” Baba Naya akauliza huku akikaa. “Nafuatilia
malipo ya ile pesa Naya aliniwekea dhamana, na kwenda kuwasalimia wazee kidogo.
Juzi nilikwenda, nilikuwa na haraka, sikukaa sana nyumbani. Nilimuacha mama
anawasiwasi na afya yangu. Nataka niende nikakae naye hata kidogo tu,
kumtuliza.” “Utakuwa umefanya jambo la msingi.” Akaongeza baba Naya. “Niende
baba?” Naya akauliza. “Nyinyi nendeni, lakini naomba muwe waangalifu huko.”
“Sitampeleka sehemu nyingine mbali na mahakamani na nyumbani. Kisha tutarudi.”
“Sawa.” Naya akarudi chumbani kwenda kubadilisha nguo.
Alitoka chumbani kwake, akiwa amebadilika akaonekana amejitengeneza kidogo na hata baba yake aliyaona mabadiliko ya mpaka usoni. Aliweka tabasamu la ukweli, likaonekana lina tumaini. Wakaaga hapo, wakatoka wakitembea tu. Safari hii hapakuwa na gari la kifahari ila kutembea tu kuelekea kituoni ili kutafuta basi la kuwapeleka Moro, wala sio Side tena.
Malon & Naya tena.
M |
alon akamtupia
jicho wakiwa wanatembea kuelekea kituoni. Akamuona ametulia sana, akamshika
mkono na kumvutia karibu. “Unaendeleaje? Sio kwa ujumla.” Akamuuliza
akimaanisha kutaka majibu kwa kina. Naya akatoa tabasamu akifikiria kidogo. Akamuona
anajifuta machozi mara kadhaa. Malon akatulia akiwa amemshikilia mkono na
kuuminya taratibu, akimsubiria atulie. “Naendelea vizuri kiafya. Ila kazi
zinasumbua! Baba alinikataza nisiendelee na zile kazi za usiku. Unakumbuka mara
ya mwisho ulinikuta na Ozi?” Malon akaitika. “Ilikuwa tukafanye tangazo la
kinywaji, lakini pombe.” Malon akacheka. Alimjua baba yake Naya. “Lakini
ilikuwa inilipe vizuri bwana!” “Kama vile nilivyokuwa nikiwauzia watu bangi?”
Malon akauliza. Akamkumbusha baba yake naye alimuuliza hivyo hivyo. Akatulia.
“Ehe!” Malon akataka aendelee. “Kabla ya kufanya lile tangazo,
ikabidi nimwambie baba. Kwanza nilijuta. Akaonyesha kushangaa sana. Ni kama
ambaye hakutegemea hata ile tu mimi kufikiria kufanya hivyo!” Malon akacheka
tena. “Basi, nikaacha lile tangazo wakati nilichaguliwa na Ozi akiwemo. Yule
meneja wa ile kampuni ambayo alikuwa akitutafutia kazi, akaumia sana. Kwa kuwa
alikuwa alipwe pesa nzuri tu, kama endapo mimi na Ozi, tungefanya lile tangazo.
Ikabidi afanye msichana mwingine ambaye sio wakutoka kwenye kampuni yake. Basi,
ndio baada ya hapo akaanza usumbufu sasa. Mara aseme kuna matangazo mengine
yanafanyika nje ya Dar!” “Ulishawahi kwenda naye?” Malon akauliza.
“Nilikwenda Malon. Alinichukua mpaka Dodoma. Akaniambia ndio kuna
matangazo. Tumefika kule, naona anafanya mambo yake. Tukafika hotelini
akachukua chumba kimoja. Sikumbishia. Nikatoka nje, nikampigia simu baba.
Nikamuelezea kila kitu. Baba akaniambia nirudi ndani, nichukue mizigo yangu, nirudi
nyumbani muda uleule. Nikafanya hivyo. Nikarudi nyumbani. Baada ya siku tatu
akanipigia tena simu, ananitaka kazini. Ndio baba akaniambia nisirudi tena, na
kazi za usiku hataki tena. Basi. Ndio nipo naye hapa nyumbani. Nimejaribu
kutuma maombi ya kazi kwenye makampuni tofauti tofauti, ndio nasubiri.”
Walikuwa wameshafika kituoni.
Malon akamwangalia. “Na Joshi?” Malon akauliza. “Yupo.” “Nilimuona
nilipokwenda kuzungumza na Mati. Nilipata mpangaji kwenye ile nyumba. Ndipo
nilikopatia pesa za mtaji.” Basi likafika pale, Naya na Malon wakaingia ndani.
Hawakupata nafasi za kukaa, wakasimama kwa ahadi ya kupata viti wakifika mbeleni.
Hawakujali. Wakasimama, Malon akaanza kumsimulia Naya. Kuanzia siku anakutana
na Tarimu, alivyomuombea na kumpa bibilia. Tarimu ndiye aliyemtafutia kazi
kwenye kampuni ile ya ulinzi ambako na yeye ndiko anakofanya kazi. Akamuelezea
jinsi alivyokutana na Tembe na mpaka akamtafutia mteja.
Walipofika Kibaha kabisa kwenye kituo cha mabasi, ni kweli
wakapata nafasi, wakakaa. Malon akaendelea kumsimulia mpaka siku hiyo
alipokwenda pale. “Nakushukuru sana Naya. Asante kwa mema yote uliyonifanyia.
Lengo la kukuomba uje na mimi huku, ilikuwa nikushukuru. Ulinitendea mambo ya
ajabu mpaka leo unamshangaza mama yangu. Siku natoka jela, mama alizungumza
sana na mimi mpaka nikajiona sikustahili Naya. Nilitaka tuachane kwa makusudi
ili upate mwanaume atakayekupenda na kukutunza vizuri zaidi yangu.” Naya
akainama.
“Siku ile nilifanya makusudi ili uondoke umenichukia ili uendelee
na maisha yako. Iwe Joshi au Ozi, sikujali tena. Kwa kuwa nakuamini,
nikajiambia utakayemchagua, ni kwa kuwa unajua atakufaa. Ulipoondoka ukiwa
umekasirika, nikashukuru Mungu kuwa lengo langu lilifanikiwa. Sasa kuja kukukuta
tena kesho yake umeniletea maandazi, sijui mayai na maziwa kwa mlinzi! Na simu
unaniambia unaniombea na hivyo vitu vitanisogeza. Hakika uliweka hukumu kubwa
sana moyoni mwangu. Nikajuta kukuacha, lakini sikuwa na jinsi. Hofu ya maisha
ilikuwa imeniingia. Sijui nini chakufanya. Shule sina, na pesa sikuwa nayo.”
“Nikapatwa na kiu ya bangi. Nikatafuta, mlinzi akanipa. Nikaenda
kukaa sehemu ili nivute. Nikakukumbuka. Nikaichukia ile bangi na kuifukia.
Nikajiambia ndiyo iliyonisababisha kukuumiza tokea mwanzo, ndio imenifikisha
pale mavumbini nilipokuwa nimekaa jua kali, njaa na kiu. Kuanzia siku ile nikaichukia
bangi kabisa. Hata nikisikia harufu inaniumiza. Unakumbuka wakati ule
nilikwambia nilitafuta msaada wa daktari?” Naya akacheka. “Basi safari hii
nimeiacha bangi mimi mwenyewe bila tiba.” “Hongera Malon.” Malon akabaki
akimtizama.
“Mati ameniambia mpo kwenye mahusiano na Joshi.” “Ndiyo.” Naya
akajibu na kuinama. “Unampenda?” Malon akamuuliza. Naya akanyamaza.
“Anakujali?” Malon akamuuliza zaidi. Akamuona anageukia dirishani na kunyamaza.
“Ni maombi yangu uwe na furaha Naya. Unastahili.” Naya akainama. “Unanielewa?”
Naya akatingisha kichwa kukubali. “Nakuombea sana.” “Asante Malon.” Wakatulia.
“Unakwenda lini Dubai?” “Kesho kutwa. Mzigo umefika. Nataka niwepo
wakati unapokelewa na kusambazwa. Nataka niangalie kama naweza kupata soko
zaidi.” “La nini sasa?” Naya akauliza. “Vyote. Sukari na Cocoa. Unajua sikujua
kama tunayo Cocoa nzuri hivyo hapa nchini! Halafu nyingi. Nimeulizia masoko,
yapo mengi tu. Ila kufika huko nchi nyingine ndio kazi. Watu wengi huko nje za
nchi wanatumia sana cocoa. Au niseme inayo matumizi mengi sana. Acha niende
kwanza Dubai, nitajua chakufanya nikifika huko.” “Hongera Malon. Nilijua
utafanikiwa tu.” Malon akacheka.
“Nikuletee nini?” Naya akainama nakuvuta pumzi kwa nguvu. “Naya?”
Malon akamwita na kumshika mkono. Akamwangalia. “Nimefurahi umekuja kunioana.”
Malon akacheka taratibu huku akimwangalia. “Kazama kula Malon. Mwili umeisha!”
“Sidhani kama ni chakula tu. Bado sijatulia. Nina kazi nyingi. Nimekaa huko
Kyela, mpaka wamenizoea wanafikiri ni Mnyakyusa mwenzao.” Wakacheka. “Nazunguka
mashambani kukusanya mazao, mchana na usiku bila kupumzika masaa mengi. Lakini
inalipa, huwezi amini Naya. Hizi safari chache tu nilizokwenda, nimezalisha
pesa nzuri!” “Hongera Malon.” Naya
aliendelea kumpongeza.
“Naruhusiwa kukupa zawadi?” Malon akauliza kwa upole. “Au nitazua
matatizo kwa Joshi?” Naya akainama bila kujibu. “Nimekununulia hereni nzuri
sana za dhahabu. Nilijua utazipenda. Naruhusiwa kukupa?” “Nitashukuru.”
Naya
akajibu nakujifuta machozi. Akazitoa mfukoni, akamkabidhi mkononi. Naya
alishazoea kuvalishwa kila anapoletewa zawadi hizo na Malon. Lakini safari hii
alimkabidhi mkononi. “Naomba usilie Naya. Tafadhali. Natamani kukuona
unafuraha. Hayo machozi nilishayona sana. Tena wakati ule, mara nyingine
niliyoona nikiwa na bangi kichwani. Sasa hivi naomba usilie tena. Sawa?” Naya
akatingisha kichwa kukubali. “Vaa basi.” Naya akacheka huku anafuta machozi na
hereni zake mkononi. “Asante Malo.” “Karibu.” Naya akatoa alizokuwa amevaa,
akavaa hiyo dhahabu.
Wakatulia kidogo. “Nikuulize kitu Naya?” Naya akamwangalia.
“Ukipata pesa sasa hivi, unataka kufanya biashara gani?” Naya akabaki
akifikiria. “Bado ndoto za ubunifu wa mavazi bado zipo?” Naya akanyamaza
kidogo. “Ni nini Naya? Naya niliyekuwa naye ni Naya wa mipango bwana!
Usiniangushe.” Naya akatabasamu. “Nahisi kukaa na kumsikiliza sana Joshi
kunaanza kuniathiri Malon.” “Kwa nini?!” “Unakumbuka nilikwambia Joshi alianza
biashara ya sabauni?” “Nakumbuka, na ukamsifia sana.” Naya akacheka.
“Sikumsifia bwana!” “Sijasahau kata sauti yako ya msisitizo.” Naya akaanza
kucheka.
“Imekuaje?” Malon akataka aendelee. “Alikopa pesa. Akawekeza kwenye hiyo biashara. Anasema imemuingiza hasara tu. Hamna wateja! Amebaki na bidhaa, hana pakuuza. Amechukia biashara kabisa. Ananisisitiza kuweka mawazo kwenye ajira ndio kitu cha uhakika. Hivi yeye ndiye anayenisaidia kutafuta kazi kwa nguvu zote. Hata maswala la mavazi ameshauri niache kabisa. Anasema nikupoteza pesa na muda. Sasa hivi Tanzania maisha magumu. Watu wanafikiria nini chakula, sasa nikiwekeza pesa kwenye mavazi, nani atanunua hizo nguo?” Malon akashangaa na kukasirika sana moyoni, lakini akaamua kunyamaza tu, mpaka Naya akamshangaa.
Malon wa zamani angeshatukana na kuongea kwa ukali sana. Lakini
Malon huyu akanyamaza kabisa. Hakuongeza neno. “Malon!” “Nakusikiliza Naya.”
“Ndio hivyo.” “Kila mtu anamtizamo wake Naya. Siwezi kuingilia maamuzi yako na
mwenzio. Nyinyi wawili ndio mnahusika kujenga msingi wenu. Ila unanijua mimi.
Huwa nathamini sana mawazo yako, kwa kuwa huwazi kijinga. Sijawahi kuona
ukifikiria jambo, na kulitendea kazi, likakwama. Huwa linafanikiwa sana tena
kwa asilimia za juu sana. Hapa hapa Tanzania, na mimi na wewe ni mashahidi kwa
vile Mungu alivyojidhihirisha kwako. Kwa uchumi huu huu wa Tanzania, nimeona
Mungu akikufanikisha.” Naya akajiegemeza pembeni yake. Akatulia na Malon naye
akajiweka sawa ili amuegemee vizuri.
“Mnaoana lini?” Akamuuliza. “Anataka kurudi shule. Amesema mpaka
amalize CPA ndio atafikiria swala lakuoana.” “Anarudi lini shule?” “Hata sijui
Malon!” “Na wewe unataka kurudi shule?” “Sio kwa haraka. Ingekuwa amri yangu,
ningeanza kazi au kufanya kitu kwa muda fulani, huku najenga familia kwanza.
Sina haraka ya shule, japo najua nikitaka kurudi sitashindwa. Ila natamani
kufanyia kazi hii shahada ya kwanza, kwanza. Na hata nikiishia hapa,
sitajisikia vibaya.” “Niambie ni nini unataka kufanya kama ungepata pesa na
kama Joshi angekubali.” “Hata simwambii tena.” “Tufanye kwamba atakubali
kirahisi tu, endapo utamshirikisha. Nini ungependa kufanya?” Naya akanyamaza
akiwa bado amemuegemea Malon.
“Naya?” Malon akauliza tena. Akainama na kumchungulia kule
alipokuwa amegeukia. Ni kama alikuwa amempa mgongo kidogo. “Biashara.” “Hilo ni
jibu la jumla sana Naya. Mimi nakufahamu. Huwa unaandika ndoto zako mpaka na
pesa unayohitaji.” “Niliacha uliponiacha Malon. Nilitupa kila kitu.” Malon
akambusu kichwani. “Kwanza naomba ujue sikuwa nimekuacha. Nilitaka uwe na
furaha.” “Ndio kuniacha kwenyewe huko.” “Kwa nia nzuri lakini.” Naya
akanyamaza.
“Sasa nakupa kazi, Naya. Ni juu yako kumshirikisha Joshi au la.
Ila ningeshauri umshirikishe baadaye ukiwa umekamilisha ili usikutane na
vikwazo mwanzoni.” “Kazi gani?” Naya akamgeukia. “Nataka utulie, ufikirie ni
kitu gani unataka kufanya. Usijali swala la pesa na jinsi itakavyorudi. Hayo
tutajua mbele ya safari. Nikirudi kutoka safari, uniambie.” “Kwani utanitafuta
tena!?” Malon akacheka. “Ndiyo. Au siruhusiwi?” “Unaruhusiwa Malon.” “Haya.
Naomba Naya ninayemfahamu arudi kazini. Huko unakojificha, sio wewe. Na wala
hutakaa ukawa na furaha. Umenielewa?” Naya akacheka na kutingisha kichwa
kukubali.
“Nikwambie kitu ambacho nilitamani?” “Hayo ndio nilitaka
kuyasikia.” Naya akacheka tena. “Ningekuwa na pesa, ningefungua fremu au niseme
duka au bucha ya nyama. Kubwa lenye yale mafriza makubwa yakulala. Halafu hivi
baba anavyouza hao kuku wake, mimi ndio niwe nanunua kwa bei ya jumla kama
hivyo anavyowauzia huko mahotelini kwa bei ya hasara. Halafu wale kuku mimi
nikiwanunua, nauza kwa muundo tofauti tofauti. Naweza kuuza firigisi tu, au
maini tu, miguu, mapaja na kadhalika. Kisha kuku wengine naweza kuwauza nikiwa
nimewaweka viungo mbali mbali, nauza wabichi. Sehemu ya pembeni na hapo, naweka
viti vichache tu. Namuomba Bale anipe recipe yake fulani hivi ya kuku
wakuchoma. Natafuta yale maoveni marefu kama tuliyoyaona kipindi kile
tulipoenda Dubai kwa mara ya kwanza, kwenye ile sehemu ukapenda nyama choma
yake, tukawa tukirudi pale kula nyama kila tukienda Dubai?” “Napakumbuka sana
tu. Si pale The City Grill?” “Ewaa! Kama vile sasa. Na mimi niige. Niwe nikiuza
na kuku wakuchoma pia. Wale wazima. Naweka na friji ya juisi anayoitengeneza
mama na soda. Nakuwa nauza. Kwa hiyo anayekuwa anakuja kununua kuku wakuchoma,
anakutana na ile juisi ya mama na kuku wabichi pia yakupeleka hata nyumbani.
Kuku walio na viungo tayari na wasio na viungo. Kisha nitengeneze nyama ya
kusaga yakuuza pia.” “Sasa huyo ndiye Naya ninayemfahamu mimi. Anayefikiria
kuzalisha jangwani. Mawazo makubwa zaidi ya mfuko wake.” Naya akacheka sana.
“Kweli tena Naya! Sasa hivi wewe ndiye unayeongea. Na kwa
kukusikiliza tu, hilo wazo lako ni faida kubwa sana. Hata kama maisha magumu
hapa nchini, watu wanakula na kunywa. Biashara ya chakula huwa haifi kirahisi,
labda iwe haijawekwa sehemu nzuri au hapajawekezwa vyakutosha. Ukitafuta eneo
zuri, ukafanya kama ulivyonieleza, baada ya mwaka mmoja au miwili, utakuwa
mbali sana. Hata Joshi mwenyewe atakupongeza.” “Kweli Malon au unanitia tu moyo?”
“Sikwambii hivyo ili kukuridhisha tu, Naya! Hiyo biashara ni nzuri sana.” Ujasiri
ukaanza kurejea kwa Naya.
“Sasa mtaji Malon?” “Subiri tuone huko mahakamani kama huyo
muhasibu atakuwa ametuandalia hiyo hundi yetu. Kama atatulipa, tutaiweka kwenye
ile akaunti yetu. Mimi nitaomba kidogo ili niongeze kwenye biashara ya sukari.
Unakumbuka nilikwambia kwenye biashara ile ya sukari mtaji ukiwa mkubwa na
faida inakuwa kubwa na ya haraka?” “Nakumbuka.” “Basi. Tukishatoa hizo,
zitakazobaki wewe wekeza, tena ukiwa huna presha. Taratibu, ukiipa muda. Na
maombi Naya. Ipo nguvu kubwa sana kwenye maombi. Weka mipango yako kwenye
maombi, ongeza juhudi, lazima Mungu atabariki kazi ya mikono yako.” “Siamini
kama naongea na wewe Malon! Umebadilika.” Malon akacheka.
“Lakini Malon, nahisi ndio maana nilikuwa nakukumbuka sana.”
“Kumbe ulikuwa ukinikumbuka!?” Malon aliuliza huku akicheka. “Sana Malo. Hakuna
siku inapita nisikufikirie. Najiambia angekuwepo Malon hapa, angefanya hivi au
angesema hivi. Au angenitia moyo katika hili. Hivi unajijuaga vile unavyokuwa
ukiwa na mimi?” Malon akacheka akifikiria. “Nakuaje?” “Kila kitu kinasubiri, anakuwa
Naya tu. Wakati mwingine hata simu unazima unapokuwa na mimi. Mawazo na akili
zako zinakuwa kwangu tu. Nilimiss sana hiyo Malon. Nikawa mpweke wakati
nilikuwa nimezungukwa na watu!” “Pole sana mama. Ila ujue sikutaka uangamie na
mimi. Hata baba alinitisha sana. Aliniambia sikustahili hata kidogo. Tena
akanishauri nikuache mapema kabla hujaharibikiwa zaidi. Hata Mati alichangia.”
“Mati!?” “Mati ametokea kukupenda sana Naya. Amekuheshimu mno. Njia nzima
kutokea Morogoro alikuwa akizungumza na mimi bila kuchoka.” “Anakwambiaje sasa!?”
Malon akafikiria kidogo.
“Tuache hayo. Tupate muda wakuomba kidogo, ili Mungu atutangulie huko tuendako. Ombea huko mahakamani. Mungu atupe kibali. Kwa sababu mimi kama Malon, hakuna anayeniangalia kwa jicho la heshima. Nilishaharibu sana kwenye huo mji. Lakini Mungu akiwa na sisi, atatustahilisha. Tuombee ugeni wetu pale nyumbani. Japo hatutakaa sana, lakini basi tukafanyike baraka.” Naya hakuamini kama mzungumzaji ni Malon. Wakatulia, kila mtu akiangalia dirishani wakiomba.
Jiji
Kasoro Bahari Tena.
W |
alifika
Morogoro, kwa kuwa alikuwa na Naya, akachukua taksii. “Sitaki nikurudishe
nyumbani umechomwa na jua.” Naya akacheka. Alimjua Malon jinsi anavyomjali.
Walifika mahakamani, wakaambiwa wamsubiri muhasimu. Wakatafuta sehemu wakakaa.
Naya akampigia simu baba yake kumtaarifu walifika salama. Wapo hapo wakisubiria.
Walikaa zaidi ya masaa matatu, ndipo muhasibu akaja na maneno mengi. Lakini mwishowe
wakapewa hundi yao. Malon na Naya wakaangaliana, wasiamini.
“Umeona ukiwa na mipango na pesa huwa inakuja?” Malon aliongea
wakati wanatoka hapo mahakamani. Naya akacheka. “Kuanzia kesho lazima uanze
kuzunguka kutafuta sehemu ya hiyo biashara. Mungu ameshakujibu kuwa pesa sio
tatizo.” “Asante Malon.” “Sasa twende kwa mama Saduki. Anione kidogo,
nimtulize, nikurudishe nyumbani, mchumba wa Joshi. Sitaki apige simu, akute
nakuzungusha Morogoro.” “Joshi yupo busy sana.” Naya aliongea kwa upole. Malon
akamtizama na kuamua kubadili mazungumzo. “Sasa kesho unaanzia wapi?” “Na hivi
utanisaidia pesa, nitazunguka kesho siku nzima.” “Ingekuwa sawa,
ningekusindikiza tukazunguka wote.” “Sasa kwa nini isiwe sawa!?” Naya akawa
hajaelewa.
“Maana hapo ningepata na ushauri kutoka kwako. Wewe huwa unajua
mambo mengi zaidi Malon. Nikichagua kitu, huwa unakifikiria kwa mapana kuliko
mimi. Huwa unaona mpaka kesho yake kabisa. Naweza kuchagua sehemu kwa ukubwa,
nikajisahau kwenye eneo.” “Kama haitaleta shida, basi nitakutafuta kuanzia
kwenye saa tano hivi. Asubuhi kuna kitu lazima nikamilishe ili kunihakikishia
safari yangu ya kesho kutwa.” “Nitashukuru Malon. Asante.” Wakatulia.
“Lakini Malon.” Naya akamwita wakati wapo kwenye taksii tena kuelekea nyumbani kwa kina Malon. “Vipi?” “Hatuwezi kwenda nyumbani mikono mitupu.” “Wanashida na pesa zaidi. Nilizungumza na mama. Akaniambia wanachakula, lakini hawana pesa ya kununua vitu vidogo vidogo. Akataka pesa. Nitawaachia pesa.” “Basi naomba tupitie hata mafuta yakupikia tu. Tusiende mikono mitupu kabisa.” “Nitawaachia pesa Naya! Wametaka pesa.” “Sawa. Lakini mafuta yakupikia huwa hayaharibiki. Hata wakiwa nayo mengi kiasi gani, yatawasaidia tu siku moja. Mimi nitalipia kama zawadi yangu kwa mama Saduki. Shukurani ya kusimama na mimi kipindi nina shida, alikuwa upande wangu japo kila mtu alinipinga, yeye alinitia moyo ndipo wengine wakafuata.” “Dada alinimbia. Nakushukuru Naya.” “Sio mimi sasa! Leo tunamzungumzia mama Saduki.” Wakacheka na kukubaliana wanunue vitu kidogo. Walimuomba dereva taksii apitie kwenye duka la jumla. Wakanunua vitu zaidi ya mafuta ya kupikia, ndipo wakaelekea nyumbani kwa kina Malon.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Mama yake Malon alifurahi sana kumuona Naya. “Yaani hata sasa hivi
nikifa, sina wasiwasi. Najua nimemuacha Malon kwenye mikono salama kama ya kwangu
au zaidi na ya kwangu.” Naya akacheka na kuinama. “Angejua mwanae alishachelewa!” Malon akamnong’oneza Naya
sikioni. Naya akaelewa, lakini mama yake hakujua ni nini Malon amemnong’oneza
Naya. Ile kuwaona pale pamoja, akajua wapo pamoja. Baba yake Malon alikuwa
ametoka.
Walikuta ugali hapo. Naya yeye ndio alikula wakati Malon akizungumza
na mama yake. Akamsikia akimuaga mama yake kuwa atasafiri kibiashara. Mama yake
akamuuliza maswali akionyesha wasiwasi. “Nimebadilika mama. Nakuahidi hutasikia
nimeingia matatizoni tena. Ni kweli nimepeleka mchele na Cocoa. Mambo ya bangi
nimeacha.” “Mungu akusaidie Malon, usirudi tena huko, baba.” “Amina mama. Uzidi
kuniombea. Na nikifika huko nitakupigia simu mama yangu.” “Tafadhali upige.
Hata usipofanikiwa naomba upige tu Malon.
Usiniache nikiwa na wasiwasi kama hapa majuzi.” “Nimekuahidi sitarudia tena.
Nitapiga mama.” “Nakuamini baba.” Naya akamaliza kula na kurudi pale alipokuwa
amekaa Malon na mama yake. Wakatulia kidogo na kuaga. “Basi muwe na safari
njema mkiwa mnarudi Dar. Naya mama, usitutupe. Uwe unatukumbuka hata kwa simu.”
“Nitafanya hivyo mama.” Wakaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Wakiwa njiani wakirudi Dar, hapakuwa na mazungumzo mengi sana.
Kila mtu aliwaza lake. Bado Naya alikuwa kwenye mshtuko wa kupata pesa ya mtaji
bila kutarajia. Malon akamuona anamvuta mkono, akaushika na kumuegemea.
Akamuhurumia, akambusu kichwani, kisha akamchungulia. “Niambie unawaza nini?”
“Kulala masikini na kuamka tajiri.” Malon akacheka. “Ushajiona tajiri?” “Kumbe!
Kuna watu unakua nao kwenye maisha, inakuwa ni zaidi ya pesa na mali.” “Hilo
mimi nalijua na nishahidi.” Wakatulia.
“Malo!” Naya aliita taratibu akiwa amemuegemea. Malon
akamchungulia. “Utarudi lini?” “Sijajua Naya. Sijui kama safari yangu itaishia
hapo hapo Dubai au la! Sijui itachukua muda gani na itaanzisha nini! Niombee
tu.” “Nitakuombea.” “Lakini nataka uendelee Naya. Usiwe mtu wakurudi nyuma
bwana! Kama sasa hivi tumeshazungumza, nakupanga, naomba Naya wangu wa zamani
arudi. Yule Naya aliyekusanya mamilioni ya pesa mpaka akafanikiwa, ndie huyo
huyo namtaka arudi, usimamie hilo wazo lako mpaka ufanikiwe. Umenisikia?” Naya
akatingisha kichwa kukubali. “Pambana sana. Mimi najua utafanikiwa.”
“Nimefurahi umerudi Malon na umenitafuta. Nashukuru kutafuta muda wa
kunisikiliza tena, na kunitia moyo.” Malon akavuta ile mikono yao Naya
aliyokuwa ameikumbatia, mpaka kifuani kwake, akabusu mkono wa Naya.
Naya
akafunga macho kama anayeruhusu faraja ipite moyoni mwake. “Nikuombe kitu
Malo?” “Nakusikiliza.” “Naomba turudishe mawasiliano. Tuwe tunawasiliana. Hata
kama haitakuwa kila siku, lakini niruhusu nikiwa na swali, nikupigie
unishauri.” “Bila shaka Naya. Muda na wakati wowote wewe piga. Hata saa sita za
usiku, nikiona simu yako nitapokea kwa haraka sana.” “Na wewe utanipigia?”
“Ukiniruhusu, na ukanipa muda ambao sitawasumbua wewe na mwenzio, nakuahidi
kupiga, japo kukujulia hali.” “Basi naomba na mimi unijulishe utakapofika
Dubai. Hata usipofanikiwa, nipigie.” “Muda gani ni mzuri wakupiga?” “Wakati
wowote.” “Hapana Naya. Lazima tuwe na nidhamu. Sitapenda nikuingize matatizoni
au kumfanya Joshi ajisikie vibaya.” Naya akainama nakuanza kulia. “Basi tufanye
hivi, uwe unanitumia ujumbe muda unaokuwa unanafasi ambao unaona tunaweza
kuzungumza. Sawa?” Naya akatingisha kichwa akiwa ameinama. Malon akaweka mkono
mgongoni kumtuliza.
Walishushwa Kilivya, kituo cha kwenda nyumbani kwa kina Naya. Ilishakuwa
saa 12 jioni. “Unafikiri tumechelewa sana?” “Hapana. Usiwe na wasiwasi.
Nilishamtumia ujumbe baba kumwambia tupo kwenu. Na wakati tupo njiani nilimtumia
ujumbe. Hana neno.” “Nimefurahi umenisindikiza. Kitu cha kwanza nitakachofanya
kesho asubuhi kabla ya kukutana ni kwenda kuiweka hii pesa benki. Nikishamaliza
shuguli zangu, nitakupigia ili tuzunguke wote.” Malon na Naya walikuwa
wakizungumza huku wakitembea kurudi nyumbani kwa kina Naya.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kila mtu alimuona vile Naya alivyorudi tofauti. Baba yake
akacheka. “Naona unawaka masikioni!” “Zawadi amenipa Malon.” Naya alimjibu baba
yake huku akimsogelea na cheko kubwa usoni. “Umependeza mama mzazi.” Baba yake
akamsifia. “Asante Malon kwa zawadi. Nimerudi nimekuta vyakula. Mungu akubariki
baba. Naona una moyo wa utoaji kweli!” Akashangaa wengine wanacheka. Hakuwa
ameelewa. “Kidogo tu mama. Naomba mimi niwaache. Muwe na usiku mwema.” “Na chakula?”
Akauliza baba Naya, Malon akamtizama Naya. “Kama kipo ningeshukuru. Ili nile
kabisa, nikifika iwe mambo mengine.” Malon akakaa.
“Kwani sasa hivi unaishi wapi Malon?” “Pale pale Kunduchi nyumbani
kwangu. Lakini chumba cha uwani. Mbele nilikodisha. Ila nafikiri nikirudi
kutoka safari, nitafute chumba kikubwa kidogo.” “Unakwenda wapi?” “Kuna
biashara nilikuwa nikifanya zamani kidogo. Ya sukari. Natoa Brazili napeleka
Dubai. Sasa kujibu swali lako, naelekea Dubai. Kuna mizigo nimetanguliza huko.
Nimepata taarifa umefika. Nataka niwepo wakati inatolewa bandarini na kupelekwa
kwa wateja, ili chochote kisitokee. Baada ya hapo ndipo nitajua pakwenda tena.”
“Kwa hiyo utakaa Dubai kwa muda mrefu?” “Nafikiri hivyo. Nitajua nikifika
huko.” Malon akajibu mama Naya kwa heshima zote.
“Bado chakula kidogo.” Naya alirudi na hiyo taarifa. “Basi,
nitakula wakati mwingine.” Malon akataka kusimama. “Kwa kuwa ulikuwa umefunga,
nimekubandikia chai. Uanze kunywa chai kwanza wakati unasubiri chakula.” “Hapo
umefanya vizuri, Naya.” Baba yake akampongeza. “Hongera Malon. Nilisikia ulimpa
Yesu maisha yako.” Akaongeza mama Naya aliyekuwa akimuhoji maswali. Malon
akacheka kidogo. “Ni neema ya ajabu kwakweli. Hata mimi sikutegemea. Nilipokea
nikiwa sijui thamani yake.” Malon akaendelea kuzungumza taratibu akiwashuhudia
kile Mungu alifanya siku ile kupitia Tarimu. Akawasimulia mapepo aliyokuwa nayo
na vile alivyowekwa huru.
Bale akaleta chai. “Muone! Anapenda stori huyu! Hapo amekaa
ametulia tuli, amesahau hata kama amebandika chai jikoni!” “Kwani wewe ungeleta
kimya kimya tu, ungepungua wapi?” “Bale na Naya, naomba msianze hapa. Sisi
tunasikiliza mambo ya maana.” “Si Bale huyo!” “Bale gani, wakati ni wewe? Unaogopa
jiko kama nini sijui!” “Siogopi jiko ila sitaki kuwa na wewe huko jikoni.”
“Basi natoka nikupishe.” “Sitaki. Nina mgeni.” “Muongo. Hutaki tu kukaa jikoni.
Kwani Malon anakuja hapa kila siku? Mbona jana hukuingia jikoni?” Malon akaanza
kucheka. Akamkumbuka Naya na kaka yake.
“Haya, Bale, ondoka.” “Ungetufukuza wote baba!” “Ili mkazidi
kubishana huko huko jikoni?” Baba yake akauliza. “Ondoka. Baba amekwambia uondoke.”
Naya akaweka msisitizo. Bale akaondoka huku anamkazia macho Naya. “Sijui ukoje
Bale?” “Wewe ndio sijui ukoje!” “Sasa na wewe Naya unamtafuta mwenyewe. Yeye
alikuwa anaondoka, kwa nini unamuanza tena?” Mama yake akaingilia. Malon
akazidi kucheka huku akinywa chai yake. Malon alimaliza ile chai, akamuomba
Naya akamuongezee. Akarudi na chakula kabisa. Wakala huku wakizungumza, mwishoe
Malon akaaga na kuondoka akiwa ameshiba.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Naya
akaanza kucheka. “Muone alivyofurahi!” Mama yake akamrushia neno. “Unampenda
Malon wewe!” “Kwa kuwa ananijali sana mama. Hapo alipo anajua kama nipo na Joshi.
Aliambiwa hukohuko ofisini kwao, lakini bado alikuja kuniona. Ona dhahabu alizo
ni nunulia! Yaani Malon, kila akipata pesa, lazima anifikirie mimi kwanza.
Huwezi kumlinganisha na ..” “Joshi!” Kila
mtu akadakia wakaanza kucheka. Mara zote Joshi akienda hapo, anakwenda mikono
mitupu. Hakuna zawadi hata moja Naya alishaonyesha hapo kwao kwamba imetoka kwa
Joshi. Hata siku ya mahafali yake, Malon ambaye alikuwa mlinzi, alipeleka cheni
ya dhahabu. Joshi alikwenda mikono mitupu akilalamikia kutingwa na kazi.
“Baba!” Naya akamgeukia baba yake. “Unakumbuka ile biashara ya
kuuza kuku niliyokuwa nimekwambia?” “Nakumbuka. Si ndio ile uliniambia
ulimwambia Joshi, hata kabla hujamaliza kumueleza, alikwambia uachane nayo?”
“Kumbe unakumbuka!?” “Siwezi kusahau.” “Basi Malon aliniuliza. Nikamwambia.
Ungekuwepo, ungesema sijaongeza baba. Malon amefurahia na kunipongeza sana.”
“Sasa mtaji? Maana wazo lipo sawa, sasa pesa unapata wapi hata kama wazo zuri?
Labda ndio maana mwenzio Joshi aliona uache tu.” Mama Naya akatetea kidogo.
“Sasa subiri kwanza mama. Hapo Malon ananiuliza tukiwa njiani
tunakwenda Morogoro. Na mimi nikamwambia tatizo ni pesa. Malon akaniambia
tatizo sio pesa, tatizo ni wazo sahihi, ndipo pesa zinapokuja. Na kupata faida
kwenye wazo sahihi ni sehemu sahihi, juhudi na maombi.” Kila mtu akastaajabu
kasoro mama Naya, akatulia tu
akisikiliza.
Naya alikuwa akiongea kwa kujivuna. “Amenipongeza na kuniita nina
akili sana. Hapa tunavyozungumza, amelipwa pesa yake yote. Anakwenda kuiweka
kwenye akaunti yetu. Ameniambia nianze kesho kutafuta sehemu. Nishajua sehemu
yakupata mafriji makubwa. Na atanisaidia kuzunguka kesho kutafuta yale maoveni
marefu na sehemu nzuri. Pesa itakuwa benki. Ameniambia nianze.” Wakashangaa
sana. “Husemi ukweli Naya!” “Kweli baba. Malon amenitia moyo na kunitaka nianze
bila kuchelewa. Ameniambia nitafanikiwa nijipe muda.” “Sasa utamwambia nini Joshi?”
Hapo mama Naya akauliza akionyesha wazi kuna mwingiliano ambao asingetaka
utokee.
“Joshi yeye anaonekana ni
muoga wa kuthubutu.” Naya alisema hivyo.
“Na mbahili.” Akaongeza Bale nakufanya wacheke kidogo. “Bwana mwanaume muoga
wakutoa pesa yule! Sijawahi ona. Anaona shida hata kulipia maji aliyokunywa
yeye mwenyewe! Alinizungusha siku ile alipokuja kanisani nikawaambia tunaenda
kununua maji nje!” “Kwani siku ile hakulipa?” Mama yake akauliza kwa mshangao.
“Alihangaika mama, mpaka nikaona ni heri mimi nilipie maji yote. Kwanza alitaka
alipie yake tu. Sasa mwenye duka akamwambia hana chechi. Eti akataka atoke
hapo, akatafute chechi kwengine wakati alishayanywa maji! Ikabidi mimi nilipie
tu.” Wakashangaa sana.
“Inawezekana kwa sasa anamajukumu mazito! Si alisema anajiandaa
kurudi shule?” Mama Naya akatetea. Wote kimya maana walimjua jinsi anavyompenda
Joshi. “Basi. Nimeona nianze tu. Ikishakomaa ndipo nimwambie.” Naya akaendelea
bila kutaka kuongeza hapo kwa mama yake. “Kwanza hana muda wakufuatilia mambo
mengine zaidi ya kazi yake anayolalamikia mchana na usiku.” Akaongeza Naya.
“Mimi nikupongeze mama
yangu mzazi, kwa mawazo mazuri ambayo huwa hujawahi kuacha kuyafikiria hata
katikati ya ugumu. Ingekuwa rahisi kujipuuza pale unapokatishwa tamaa. Hongera
sana.” Yeye baba Naya kama kawaida yake akasimama na binti yake. “Asante baba.
Nimefurahi sana. Si unajua nilivyokuwa natamani kujiajiri?” “Ndio maombi yako
siku zote. Naona Mungu amekujibu.” Ujio wa Malon ukawa wa furaha kubwa sana kwa
Naya lakini si kwa mama Naya. Naya wa kucheka na maneno mengi akarudi. Yeye
akawa ndio mzungumzaji mkubwa usiku huo mpaka wakaenda kulala mama yake
akimsikiliza tu.
Naya kwa Malon.
‘Ulifika salama?’ Naya akatuma ujumbe. ‘Bado nipo
mtaani mama. Sijarudi bado. Unalala sasa hivi?’ Malon akamuuliza kwenye
ujumbe aliorudisha. ‘Bado kidogo. Nikilala sasa hivi, inamaana itabidi nivue hereni
zangu, wakati bado hamu haijaisha.’ Malon alicheka sana alipokuwa akisoma
ule ujumbe. ‘Nitakucheki nikifika nyumbani. Kama utakuwa umelala, basi nitakuona
kesho.’ ‘Naomba nisubiri simu yako Malo!’ ‘Basi nitakupigia. Nitajitahidi
kuwahi ili nisikuweke sana.’ ‘Usijali.’ ‘Sawa.’ Malon akarudisha hayo majibu.
Baada kama ya lisaa, Malon akapiga simu. “Umeshavua
hereni?” “Zimegoma sikioni. Nimeona nilale nazo tu mpaka hiyo siku zitakapokubali
kutoka.” Malon akacheka sana. “Asante Malo.” “Nini tena mama?”
“Hereni, kuja kupata muda wakunisikiliza. Kwangu inamaana kubwa sana.
Nilihitaji hiyo. Na asante kwa kuniamini. Nashindwa kulala kwa mshtuko. Siamini.”
“Karibu sana. Ila nataka ulale ili kesho uamke na nguvu. Una kazi kubwa
mbeleni. Inakuhitaji zaidi wewe. Sawa?” “Sawa.” “Basi acha tuombe kabla
hujalala.” Malon akamuombea kwa kifupi tu. Wakaagana.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kesho yake Naya aliamka mapema akiwa amejawa na furaha sio Naya
waliyemzoea akijiweka na shuguli nyingi mpaka jikoni! “Basi leo huko jikoni
kutavunjwa kila kitu! Si umwite huko nje?” Mama yake alinong’ona walipokuwa
mezani wakinywa chai alfajiri hiyo ili kila mmoja awahi kwenye majukumu yake. “Ili
mumwambie mwanangu anakimbia jiko? Mwacheni avunje tu.” Wazazi wake wakacheka,
wakasikia tena kijiko kimedondoka. Wakaangaliana na kucheka tena taratibu.
“Vipi mama? Kwema huko?” “Sio mimi, baba. Ni Bale.” “Ujue Naya unapata dhambi
wewe!?” “Sasa aliyenitingisha hapa mwanzoni nikaangusha sahani ni nani kama sio
wewe? Unahangaika huku jikoni hutulii!” “Na hicho kijiko cha sasa hivi?” “Si
bahati mbaya na wewe! Nini usichoelewa?” “Umesikia majibu yake mwanao, baba? Hana
chakutingishwa wala nini! Mikono yake ndio yote ipo yakushoto.” Kila mtu
akacheka.
Akaoga na kuvaa. Akataka kutoka, akarudi. “Nisindikize baba.”
“Sasa na wewe utakosa mengi. Mtu amekwambia anasafiri kesho. Leo anataka
akusindikize. Na mimi unataka niwepo! Utaolewa kweli wewe!?” “Mkweo Joshi,
mwenyewe sijamsikia tokea jana asubuhi.” “Ndiye anayekuoa? Au unamdanganya tu mama
yako?” Naya akacheka sana. “Mama anavyompenda Joshi! Anatamani niolewe naye
hata kesho! Acha nimuwahi Malo.” “Akiondoka ndio nitakuwa na wewe huko.
Tuhangaike mpaka tufanikishe hilo swala la duka la nyama na vingine vyote.”
“Ndio maana nakupenda baba yangu.” Naya akatoka huku akicheka kwa furaha. Akajua
hivyo alivyojibiwa hapo ndio amesharudisha kuaminiwa na baba yake.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kwa kuwa kuanzia maeneo ya Kibaha mpaka Kibamba kualinza kujengeka
sana, Naya akaona asianzie mbali sana. Akaangalia maeneo hayo. Akapanda na basi
mpaka Kibaha kabisa, akazunguka maeneo ya wazi, akitafuta sehemu zenye
makusanyiko ya watu wengi huku akibania pesa ya kodi ili kuweza kununua vifaa
vingine. Alizunguka Naya bila kuchoka huku amehamasika akijua pesa ipo benki.
Akatoka hapo na kupanda basi mpaka mjini kabisa, akiacha hilo eneo la upande wa
Kibaha.
Ilipofika
saa 6 mchana Malon akampigia. “Uko wapi?” “Nimekaa mahali naandika. Maana
nimezunguka sehemu nyingi ninazopenda, kodi zake zipo juu! Sasa nikaona lazima
kufikiria kitu kingine zaidi chakufanya kama nikipata hizo fremu ili
ziniongezee pesa ya kulipa kodi.” “Kwa hiyo?” “Hapa nimetoka kuongea na dalali
mmoja wa hapa Ilala. Ana maneno mengiiiii! Nimemuomba aniache kwanza, anipigie
akifanikiwa.” Malon akacheka.
“Ila amenipa namba ya simu ya
dalali mwingine. Amesema kuna fremu kubwa, na nzuri, maeneo kabla ya Ubungo
kutokea posta. Anasema ni mpya bado, na hakuna kituo cha daladala. Na bei
nzuri, kwa kuwa huyo baba ndio anatafuta wateja. Sasa nimemwambia nitakwenda.
Amesema mwenye hizo fremu atakuwepo hapo saa nane mchana. Ndio nimekaa hapa,
nawaza. Nafikiria ni lazima hiyo sehemu iuze kitu ambacho kitavuma sana. Ambacho
wenye pesa na walionazo za kati, itawalazimu hata kushuka kituo kimoja kabla au
baada ya hapo ili tu kufikia hilo duka langu.” Malon akafurahi sana.
“Safi sana. Sasa na mimi nimemaliza huku. Naweza kukufuata hapo
ulipo au tuzungumze tu kwa simu.” “Uliniahidi leo tutakuwa wote Malo!”
“Sijabadilika. Nataka kujua tu kama naruhusiwa kuja sasa hivi? Maana hii mida
ya chakula cha mchana. Mnaweza mkawa mpo sehemu mnataka kula. Sasa sitaki
kuingilia.” “Nipo tu hapa nimekaa peke yangu. Njoo, haina shida.” Baada ya
kumuelekeza alipo, wakaagana. Naya akaanza kumfikiria Joshi. Hakuwa amemsikia
kwa simu zaidi ya neno la Mungu alilokuwa amemtumia asubuhi hiyo. Akabaki
ameshikilia peni yake, akifikiria. Alipotea kabisa pale, akabaki akiwaza.
Akaamua kumpigia. Ikaita kwa muda mrefu, haikupokelewa. Akaamua kuacha, akabaki
ameinama anachora lile karatasi.
Akamsikia mtu anamshika bega. “Malon!” Akasimama. “Unawaza nini?”
“Napanga tu mambo. Njoo ukae hapa uone.” Malon akakaa. “Kwanza niambie kama
umefanikiwa mambo yako.” “Nimefanikiwa. Nina tiketi, kila kitu. Naondoka kesho.
Na hii ni risiti ya benki.” Malon akamtolea na kumkabidhi. “Kumbe pesa inaingia
hapo hapo! Mimi sikuwa najua.” Naya akakiangalia kile kikaratasi cha salio,
akakiweka chini. “Utanipigia ukifika huko?” “Nimekuahidi kukupigia Naya.
Nitafanya hivyo.” “Jitahidi pia usikawie kurudi.” “Ukiona nimekaa huko muda
mrefu, ujue mambo yanakwenda vizuri.” Naya akainama, akendelea kuchora. “Lakini
tutawasiliana. Utakuwa ukijua kinachoendelea. Usihofu.” Naya akatingisha kichwa
kukubali.
“Umeshakula?” “Bado. Nilitaka nimalize kwanza.” “Tule wakati
tunapitia ulicho andika.” Wakaita muhudumu, wakatoa oda zao. Naya akaanza
kumueleza Malon. “Ningekuwa mjuzi wa kupika kitu fulani, ningepika hapo eneo la
biashara, kikawa kama kivutio. Sitaki kuweka tumaini langu kwa mtu mwingine,
halafu asipokuja kazini nakuwa nimekwama.” “Lakini mimi sioni sababu yakuongeza
kitu kingine Naya. Wazo lako la mwanzoni ni zuri sana. Naomba tulifanyie kazi
hilo. Jifunze hiyo ya nyama choma. Ukiweza kutoa kuku wazuri, watu watapitia
kama chakula cha majumbani kwao. Yaani mboga ya siku hiyo. Kuwa ipo tu tayari
au ukapata wateja ambao watataka tu kukutana hapo na kula hiyo nyama na juisi
ile ulisema mama anatengeneza vizuri.” Malon akaendelea.
“Cha msingi, uwekwaji. Tafuta maboksi mazuri, yenye
kuonyesha yule kuku aliyeiva vizuri ndani, atauzika tu. Kingine, hata
utakavyowahifadhi hao wabichi, itavutia wateja. Na bei. Isiwe kubwa sana
yakuogopesha wateja. Kwa kuwa na wewe unanunua kwa bei nafuu, fremu hulipii
pesa nyingi, basi, usiuze kwa bei ya tamaa sana. Weka bei itakayowafanya wateja
warudi. Tafuta na mashine yakusagia. Uza na nyama ya kusaga ya kuku kama
ulivyosema. Nashauri fanya na ya kusaga ya ng’ombe. Hifadhi kwa size tofauti
tofauti. Unaweza weka na samaki pia. Anzia hapo, tuone.” Akamuona anacheka.
“Na usisahau Naya, biashara matangazo. Tengeneza vipeperushi.
Mwanzoni jitahidi kusimama vituo vya daladala, gawa. Nenda maofisini na sample,
waonyeshe watu. Ukipata wateja wa maofisini, hata kama ni wa chache tu, haohao
ndio unawakamata, wanakua watu wako wakukutangazia.” Wakaanza kupanga hili na
lile, mara simu ya Naya ikaita. Akamuona amebadilika sura. Sio ya furaha. Ikaita
akiitizama, kisha akapokea.
“Joshi!” “Mzima?” “Mzima, nilitaka kukujulia hali. Nimeona kimya
tokea jana!” “Sasa kwa nini usipige?” Joshi akauliza. “Nilijua labda
upo busy, maana tokea jana utume ujumbe asubuhi wa neno la Mungu, sikukusikia
tena mpaka asubuhi hii ulipotuma tena ujumbe kama jana wa neno la Mungu. Ndio
maana nikaona nikupigie nikusalimie.” “Kumbe ulipiga?” Naya
hakutaka kujibu hilo. Alijua anamdanganya tu, ameona missed call ndio maana
amepiga.
“Uko wapi?” Akamuuliza. “Mtaani tu.” Naya akajibu bila maelezo
mengi. “Unafanya nini badala ya kutafuta kazi!? Lazima
ujitume Naya. Hakuna atakayekufuata nyumbani na kukupa kazi! Au huko mtaani
unakozunguka sidhani kama utakutana na watu sahihi wa kukusaidia. Wewe unakuwa
unajifungia huko Kiluvya sijui Kibamba nyumbani kwenu tu, kazi haziwezi
kukufuata huko. Toka, na ujichanganye na watu wa maana. Zungumza na watu. Sio
unasubiri kupigiwa tu. Hata kama unaomba, Mungu hawezi kutuma malaika. Musa
aliulizwa una nini mkononi? Sasa wewe ulichonacho ni cheti kizuri, pesa huna,
tumia hicho cheti acha kupoteza muda ukifikiria mambo yasiyo…” Malon akaona aondoke pale. Aliumia sana. Akatoka hapo na
kuacha Naya anaelimishwa na mpenzi wake.
Malon alikwenda kusimama mbele kidogo. Ilikuwa sehemu ya wazi.
Naya akabaki akimwangalia huku akimsikiliza Joshi. Akamuona anatoa simu yake
nakuanza kupiga na yeye. Mawazo ya Naya yakatoka pale kwenye ile simu aliyokuwa
akizungumza Joshi, akili zikabaki kwa Malon. Akabaki akimtizama huku Joshi bado
yupo sikioni akiendelea kuongea. Akapunguza sauti ya simu yake, kisha
akairudisha sikioni. Joshi akaendelea. Akatoa mifano ya bibilia na kuelezea kwa
kina. Naya akaona aweke mute na kuweka ile simu pale juu meza. Malon alipomuona
ameweka simu chini, akajua amemaliza. Akarudi.
Alipokaa tu, akamsikia bado Joshi anaongea. Akakunja uso kama
anashangaa. Akamwangalia Naya. “Kaa tu tuendelee. Bado ana mifano kama mitatu
yakunieleza ndipo amalize. Sasa sio leo. Huwa akifikia hapo, anachukua muda
mrefu sana kunieleza. Tuendelee tu.” Malon akabaki ameduaa. “Malon!? Tuendelee
bwana. Hasikii.” “Akikuuliza swali?” “Hata maswali yake huwa nayajua. Usiwe na
wasiwasi. Akitoka hapo atamuelezea Ibrahamu. Alivyochukua hatua yakutoka kwenye
mji wao na kwenda asikokujua, akifuata maelekezo ya Mungu. Ndio maana
akafanikiwa. Utakuja mfano wa Naomi na mkwewe Ruthi. Ruthi alikubali ushauri wa
Naomi. Akachukua hatua, akafanikiwa na ndio maana yupo kwenye bibilia mpaka
leo. Atakuja Yona. Alikuwa mbishi, hakufuata maelekezo, akamezwa na samaki.
Ilimbidi Mungu amfungie jela ambako ni kwenye tumbo la samaki, akamfundisha na
kutii akiwa hukohuko tumboni. Nisiwe kama Yona. Sasa hapo huwa anaeleza kwa
kirefu sana, sio kama hivi ninavyokwambia mimi kwa kifupi. Hatakaa akamaliza
sasa hivi.” Malon akashangaa sana.
“Sasa hatumii pesa nyingi sana!?” “Cha kwanza ujue ndio muhasibu
mkuu pale kwenye ile kampuni inayotoza mamilioni ya pesa kutoa huduma zao.
Analipwa pesa ya simu na usafiri. Cha pili, anahesabu hiyo ni kama huduma
anamtumikia Mungu.” Malon akatulia kidogo kisha akaona aulize tu. “Ni nini
anataka ufanye?” “Anasema nazembea kutafuta kazi. Napenda kukaa tu nyumbani.
Sitaki kuchukua hatua. Nina visingizio vingi.” Malon akashangaa sana. Naya
anayemfahamu yeye sio huyo anayemfahamu Joshi. Akanyamaza, hakuuliza tena
swali.
“Kwa mfano Ruthi.” Wakamsikia Joshi anaendelea. Malon akashangaa
sana. “Haiwezekani Naya!” “Mimi nilikwambia. Naomba tuendelee tu Malon. Sitaki
uondoke uniache katikati.” “Siwezi. Samahani kwanza Naya. Sasa huwa
unafanyaje?” “Ndio namsikiliza mpaka amalize. Na hata ukiwa naye umekaa tu hivi,
hakosi cha kukosoa. Unakumbuka kipindi kile nacheka sana nasema ana maneno
mengi?” “Nakumbuka mpaka ulikuwa ukitokwa na machozi!” “Basi wakati ule alikuwa
akiongelea mambo ya kanisani. Akikosoa taratibu fulani na nyimbo fulani za
kanisani.” “Anasemaje?” “Havina maana, lakini watu huwa wanafanya bila
kufikiria. Sasa mimi nikawa nacheka. Nikifikiri utani. Kumbe ni tabia yake! Ni
mkosoaji sana Joshi. Hadhani kama kuna watu wanauwezo wakufikiria kama yeye.”
“Mbona ni kama anafanana na Ino!?” “Basi ndio ujue bahati
niliyonayo kwa wanaume. Ndio maana nimeona nitulie tu. Nimchukulie hivyo hivyo.
Mama ananiambia hakuna mkamilifu. Na ni kweli. Nitabadili mpaka lini? Ino
ameoa, na ana mtoto mzuri kweli wa kike. Namapungufu yake niliyoshindwa mimi,
anaye mwanamke mzuri tu, msomi, ana kazi nzuri, anaishi naye. Wana maisha
mazuri tu. Huo mfano mama ananipa kila siku. Huna jinsi ukamlalamikia mama juu
ya Joshi akaelewa. Anampenda, na anataka nijifunze kuishi naye. Ndio tupo na Joshi
wangu. Hamna tofauti yeyote ile na Ino. Lakini tupo tunaendelea.” Malon akanyamaza.
“Tuendelee. Sasa mashine za kusagia nyama sio gharama sana?”
“Nitakuangalizia Dubai na kama nitapata nafuu China, nitaagiza. Usijali. Ila
nataka usipaniki Naya. Tafadhali sana. Biashara nitofauti na ajira. Unaweza
usiingize pesa kwa muda mrefu tu, lakini ukivumilia, na kukazana na kumuomba
Mungu, utafanikiwa tu. Sawa?” “Sawa.” “Tulia. Mawazo yako ya mwanzo ni mazuri
sana. Naomba tuanze kuyafanyia hayo kwanza kazi kabla hatujaanza kuongeza.
Sitaki uwe na vitu vingi kwa wakati mmoja. Utaishia kupaniki, kuchoka, na
kujichanganya. Usijue lengo kubwa lilikuwa ni nini.” “Basi nitatulia kwenye
nyama, mbichi na kuchoma. Juisi, maji na soda.” “Hapo sawa.” Wakazungumza mambo
hayo ya biashara mpaka wakamaliza.
“Bado tuna kama nusu saa. Tusogee?” “Sawa, lakini nikuulize swali
Naya?” “Juu ya nini?” Naya akamtizama. “Najua umefanya kazi kwa Ino. Umeona
maendeleo yake. Mtoto, nyumba na kila kitu Mungu alichomjalia. Unajutia
kumkataa.” “Hata kidogo Malon. Nilipata nafasi yakujua kama naweza kupendwa kwa
dhati na kuthaminiwa mimi kama Naya. Mungu kupitia wewe ananionyesha mawazo
ninayowaza, mipango ninayoifikiria, nimejua vyote vinatoka kwake Mungu na ni ya
msingi hata kama wanao nizunguka wakiona ni ujinga. Nilipata kipindi cha
kujifunza kuwa chochote nitakachowekea juhudi, nitafanikiwa. Namshukuru Mungu
kwa hiyo miaka michache aliyonipa na wewe, kuliko ya mpaka kifo kinitenganishe
na Ino. Nipo na Joshi sasa hivi nikijiambia inawezekana mimi ndio tatizo.”
“Hapana Naya. Hata kidogo.” “Usikatae Malon. Kama sio kweli, niambie kwa nini
mpaka sasa hivi kwa umri huu bado nahangaika kwenye swala la mahusiano?
Sijabahatika kupata mwanaume wa kunihitaji kiasi chakutaka kuniweka nikawa wake
maisha!”
“Ni Ino tu ndio alionyesha nia yakutaka kunioa. Napo alitangaza
kwa kiburi tu. Nimekuwa ni kama njia tu. Wanaanza kwa kasi, nikishawakubali
sijui wanakutana na kasoro gani, dharau inaanza. Ule uthamani wa mwanzo unaisha
kabisa. Nabakia kuwa mtu wakuvumilia tu.” Malon akaumia sana, akashindwa hata
chakuongeza.
“Twende Malon. Au kunamahali unataka uwahi?” “Hapana. Kwa sasa
nimemaliza kila kitu, nasubiri tu safari yangu ya kesho. Tunaweza kwenda.
Ulishiba lakini?” “Nimekula mpaka nimesaza. Asubuhi niliamka, nikapika chapati
za maji.” Malon akacheka. “Walikula?” “Tena Bale ndio alikula mpaka nikampokonya.
Mtu gani hashibi!?” Malon akacheka sana.
“Hivi wewe na Bale huwa mnakaa na kuzungumza jambo na kumaliza?” Naya akacheka
huku akifikiria.
Akakumbuka. “Ulipofungwa, alinihurumia kama sio yeye! Huwezi amini
Malo.” “Nini?” “Li Bale lilikuwa jema hilo! Kama sio lenyewe. Nikawa namcheka
rohoni. Wakawa wanagawana kazi yeye na Kiziwanda. Walikuwa mpaka wananifulia!
Nikiwa natoka siku za weekend alikuwa ananisindikiza bila hata kumuomba. Usiku
tukawa tunazunguka naye. Hakunichokoza hata mara moja na hajawahi kunitania
kuhusu hicho kipindi, mpaka leo.” “Kumbe anakupenda?” “Sana. Sema hatambui kama
mimi dada yake wakati nimemzidi mbali tu. Anafikiri kwa sababu tunashindana
urefu, ndio basi.” Malon akazidi kucheka.
“Ila kina Bale wanakupenda sana Malon! Sijawahi kuwasikia
wakikukosoa hata mara moja!” “Kwani wanamkosoa Joshi?” “Sana. Wakianza kumsema,
ni kama Ino. Tena afadhali Joshi wanamuheshimu kidogo kuliko Ino. Ino ndio
wanamkejeli mbele yake. Huwezi kumkuta Ino anaongea na Bale hata sekunde tano
zikaisha kwa amani. Bale mchokozi wakupitiliza. Anamchokoza waziwazi ili
amsikie akijisifu, halafu anamkebehi.” Waliongea wakicheka mpaka kwenye hiyo
fremu.
Walipanda daladala mpaka Shekilango. Wakashuka na kutembea kidogo
kama wanaelekea Ubungo kituo cha mabasi. Upande unaoangaliana na kicho kituo
ila nyuma kidogo. “Sio mbali sana na kituoni.” Malon aliongea baada ya kufika.
Walipenda fremu na bei. Mwenye nyumba akawaambia anapokea kodi hata ya miezi
mitatu mitatu japo ni mkataba wa mwaka. Hilo Malon akaafikiana nalo.
Wakaandikishana na Naya pamoja na Malon. Malon akaomba mwezi mmoja wa
kupatengeneza pale. Mwenye nyumba akakubali. Wakamlipa, nakuondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Nimefurahi Malo. Asante.” “Karibu. Sasa unataka kufanya nini?”
“Kuna mama mmoja huwa analeta mafriji, majiko na vitu mbalimbali vya umeme
ambavyo vilishatumika Ulaya. Nataka nikaangalie kama anayo mafriji
ninayoyataka. Ndio nirudi nyumbani.” “Unanunua vilivyotumika tena!
Vikikuharibikia?” “Uzuri anakuwa anatoa na warranty. Vitu vyake vizuri. Hata
lile friji jingine pale nyumbani, tulinunua kwake. Na halijawahi kusumbua.
Nataka nianzie na vitu vyake kwanza. Biashara ikichanganya, ndio ijinunulie
vitu.” “Unataka nikusindikize?” “Ningefurahi Malo. Ila naona nimeshakuchosha
sana.” Malon akacheka.
“Hujanichosha hata kidogo. Ulivyonifurahisha, natamani kuona
maendeleo yake.” Kisha Malon akacheka kidogo kama aliyekumbuka kitu. “Nini?”
“Umenikumbusha kuchoka. Nilichoka kipindi nimetoka jela. Nilikuwa nikitembea
Naya, kama mwendawazimu. Jua kali, sina hata pesa ya kununua maji.” “Sasa kwa
nini hukunitafuta Malo?” “Ulinipiga marufuku hata kufika kwenu.” Naya
akajisikia vibaya. “Nakutania bwana. Wewe si unanijua mimi? Katika hilo huwa
hunitishi, kwanza sijawahi kukusikiliza. Ningekuja tu.” Naya akaanza kucheka.
“Kweli. Ila niliona nikuache na wewe upumzike. Ulishanihangaikia vyakutosha.
Halafu bado nilikuwa na tabia zile zile. Sikutaka nije kukuumiza tena. Nikasema
kukaa mbali na wewe ndio itakuwa shukurani yangu kwako. Nikuache ufurahie na Joshi.”
Naya akanyamaza.
“Nikwambie kitu Naya?” Naya akamwangalia. “Katika vitu ambavyo
sijawahi kutilia mashaka ni wewe. Nimeishi na wewe Naya. Huna kasoro. Unao
upendo wa dhati. Kwa upande wako, hakika sijaona kosa lolote. Ila sisi wanaume
tunaokuja kwako ndio tuna matatizo. Sio wewe hata kidogo.” “Kama lingekuwepo
ungeniambia?” “Mimi na wewe kwani huwa tunafichana?” Naya akacheka sana
akakumbuka jinsi wanavyo ambizana wote wanapokuwa na hasira.
“Ningekwambia kabisa. Kwa hiyo naomba usiishi kama wewe ndio
mwenye tatizo. Naomba utuhesabu hivi, sisi ndio tumechezea bahati. Na ndivyo
ninavyojihesabu mimi. Nilipata nafasi yangu ya thamani, nikaichezea. Ni mimi
nimepoteza, wala sio wewe. Na hata Joshi ni hivyo hivyo, na Ino pia. Nitabia
zetu tu ngumu ndio zinatufanya hivyo. Lakini wewe Naya, ni msichana wa kuwekwa
ndani, ukawa mke mzuri sana. Katika kila eneo. Mimi nimeishi na wewe kama mke
wangu, najua. Nilikuwa nakimbilia nyumbani nije tuwe wote. Na wewe ni shahidi.
Tuliishi vizuri sana. Ila mimi tu.”
“Haya, nina uhakika kwa aina ya familia bora uliyotoka, unamifano mizuri
sana ya wazazi, utakuwa mama mzuri sana tu. Naomba usikate tamaa, ukaharibu
hiyo sifa. Vitu vizuri vinakuja. Naomba uvumilie. Wakati wako ukifika, uutumie
vizuri. Na ninakuomba usifikiri umechelewa. Hapana. Mungu anao mpango mzuri
sana juu yako. Fanya kile unachoweza kwa sasa. Jua na mimi nipo. Nakuombea.
Sawa?” “Nimefurahi kusikia hivyo Malon.” “Na ndivyo ilivyo, na ni kweli.”
Malon na Naya walizunguka kila sehemu waliyojua kuna friza nzuri kwa biashara bila mafanikio. Mpaka giza likawakuta mtaani. “Naomba ukapumzike Naya. Inatosha kwa leo. Utaendelea kesho.” “Nashukuru kuwa na mimi leo.” “Karibu.” Wakabaki wakiangaliana. Naya akacheka. “Utanisindikiza kituoni?” “Wakikuiba huko njiani wakati baba yako anajua nipo na wewe!” “Kwa hiyo?” “Nakurudisha mpaka nyumbani, ndio na mimi nitakuwa na amani.” “Asante kujali Malo.” Wakaondoka na kurudi nyumbani kwa kina Naya, Kiluvya.
“Uliniahidi kunipigia Malon. Naomba usinisahau?” “Haijawahi
kutokea Naya. Wala huhitaji kunikumbusha. Na hivi umenipa kibali cha kupiga
wakati wowote, wala usijali mama. Utanisikia tu.” Hilo akalifurahia Naya. Wakaendelea
kutembea kutoka kituoni waliposhushwa kuelekea nyumbani kwa kina Naya. “Naomba
nikuombe jambo la mwisho, kabla sijakuacha.” Naya akasimama na kumwangalia. “Tafadhali
Naya, usikubali maisha yako yakaendana na matakwa ya mtu mwingine. Au ukakubali
kuwa mjinga, bila sababu! Usijisahau kuwa wewe ni smart, Mungu amekujalia uwezo
mkubwa sana wakufikiri. Anayeshindwa kukuelewa, inamaana Mungu hakumkusudia, au
mpe muda wa kuja kukuelewa baadaye, lakini sio kubadilika kwa ajili ya mtu.
Unanielewa?” Naya akatingisha kichwa huku analia.
“Hivi ni kwa nini inakuwa ngumu wakati wote kupata kitu
unachotamani Malon?” Naya aliuliza huku akilia taratibu. “Wakati mwingine unajitahidi.
Unafunga na kuomba, lakini hupati! Hivi umeshajiuliza ni kwa nini?” “Ngoja mimi
nikwambie kitu Naya. Nimejifunza hivi majuzi tu kwenye kuhangaika kwangu.
Nilifunga siku nyingi sana nikimuomba Mungu anitafutie mteja pale. Sikupata
majibu kwa wakati wangu. Siku natoka Morogoro kwenye mahafali yako, nikiwa sina
hata habari, ndipo nikapokea simu. Kwa hiyo wakati mwingine sio vile
tunavyoomba sana ndipo tunapata hapohapo. Mungu anajua ni nini tunahitaji, na
kwa wakati gani. Naomba uwe mvumilivu katika yale unayotamani. Kwa kuwa
umeshamwambia Mungu, tafadhali amini kwa wakati muafaka, atakujibu tu. Sawa?”
Naya akatingisha kichwa kukubali.
“Kabla sijakuacha, naomba tuombe pamoja. Nikuache ukiwa na furaha.
Njoo.” Naya akasogea. Walikuwa barabarani tu. Giza lilikuwa kubwa, na nyumbani
kwa kina Naya palikuwa na umbali kidogo kutokea kituoni, na miti pembeni ya
barabara. Akajivuta pembeni kabisa, Naya akamfuata. Malon akamsogeza karibu
yake, akamkumbatia na kuanza kuomba.
“Hata sasa, najua unatusikia na unatuona
Mungu wangu na Baba yangu. Nakushukuru kwa ajili ya Naya. Natubu kwa niaba yake
na yangu. Tumetenda mengi na kukukasirisha mfamle. Turehemu na ututizame kwa
upya. Nashukuru kwa mawazo mazuri unayompa Naya. Nakusihi ukamfanikishe. Tenda
kwa ajabu mpaka watakaoona na kusikia ulichotenda kwa Naya, masikio yao
yakawashe na kustaajabu ukuu wako kwake. Tembea naye katika kipindi hiki.
Anakuhitaji kwa karibu na waziwazi. Mfungulie hata ile milango iliyokuwa migumu
kufunguka kwa wengine. Mpe kibali kwa watu. Nilindie Naya wangu mpaka
nitakaporudi tena. Katika jina la Yesu, nimeomba na kushukuru. Ameni.” Yalikuwa
maombi yaliyomfariji sana Naya. “Amen.” Naya
akaitika huku akicheka.
“Naomba uniage hivyo hivyo ukiwa unacheka. Sitaki niondoke
nikuache ukilia. Itanisaidia kutulia huko ninapokwenda.” Naya akambusu pale
alipokuwa amefikia. “Asante Malon.” “Karibu. Sasa hivi twende nyumbani.”
Wakarudi mpaka kwao. Alimkuta baba yake amekaa sebuleni. “Mbona sasa umepooza
halafu upo peke yako?” “Mama yako yuko jikoni. Bale kaondoka hapa na mdogo wake
kupeleka maziwa, hawajarudi mpaka sasa hivi. Amepiga simu kuwa kuna mahali
anataka kupitia, atachelewa kidogo. Ndio maana nipo hapa.” “Ungemwambia
unamruhusu alale huko huko, asirudi hapa hata mpaka kesho au week ijayo
kabisa.” Malon akacheka. “Nani atapika?” Naya akatulia kidogo. “Umeona eeh!”
“Basi heri leo asirudi. Angalau tupumzike.” Akatoa simu yake akampigia Bale. “Baba
amekuruhusu ulale huko huko, leo usirudi hapa.” “Nipo hapa nakaribia nyumbani.
Ndio uandike maumivu.” Naya akakata. “Linapenda nyumbani hili! Sijui likoje! Halikui
tu?” Mpaka mama yake huko jikoni
akacheka. Na kweli hawakukawia kufika.
Malon alikula ndio akaaga. “Sasa mbona umepooza tena?” Malon
akamuuliza kwa sauti ya chini pale walipokuwa wamekaa. “Nakuombea usafiri
salama na urudi salama.” “Amina.” Malon akaitikia. “Nisindikize kidogo. Mpaka
hapo nje tu.” Naya akacheka. Malon akaaga, wakamtakia safari njema, Naya
akamtoa. “Wakati natengeneza hizo hereni, nilitengeneza na cheni ya mkononi.
Nilikuwa nimepungukiwa pesa ndio maana sikuweza kuchukua zote kwa pamoja. Leo
asubuhi nimeenda kwa sonara kummalizia pesa yake, ndio nikachukua. Hii hapa.”
Akamtolea na kumkabidhi mkononi.
Naya hakuamini. “Malon! Usingehangaika! Herini zinatosha!”
“Ingekuwa haijakamilika. Ni muundo mmoja. Tukipata pesa, tutatengeneza na cheni
yake nzito. Sasa hivi naomba uwe na hivyo tu.” Naya alibaki akiangalia ile
bracelet. “Nenda kapumzike, na mimi niwahi kulala.” “Nakushukuru sana Malon.
Asante kunijali.” “Najifunza kwako Naya. Najua sijafika hata nusu yako, lakini
nivumilie tu. Taratibu.” Naya akambusu shavuni. “Nitakupigia asubuhi kabla
hujaondoka.” “Nitashukuru.” Wakaagana, Naya akaingia ndani, Malon akaondoka.
Akaenda kukaa pembeni ya baba yake. “Umenunuliwa na cheni nyingine
tena!?” “Hiyo ni ya mkononi.” Akamkabidhi baba yake. “Sasa mbona umekosa raha?”
Bale akamuuliza. “Mimi hata sijui bwana!” Bale akaenda kuichukua ile cheni
kutoka kwa baba yake, mama yake akatoka jikoni. “Tuone.” Bale akamkabidhi.
“Anasema alitengeneza pamoja na hereni, lakini akaishia kulipia hereni hakuwa
na pesa. Ndio amepata pesa ameenda kuchukua na hiyo.” “Mmmh! Malon anakujali
sana, Naya!” “Sana Bale. Najua humtaki kusikia kama niliishi naye. Lakini
kipindi hicho, alikuwa hataki nipande daladala. Ilikuwa kama amebanwa na kazi
Morogoro, ni heri amtume dereva au anitumie pesa ya taksii au Uber.
Alinifundisha kuendesha gari ili nisipate shida ya usafiri. Ananijali kuliko
nitakavyoeleza. Kabla sijalia shida, Malon ananitimizia. Halafu anaamini sana
mawazo yangu.” “Nilikuona ulivyokuwa umebadilika. Nikakuuliza mwenzangu hiyo
kazi inayokulipa kiasi cha kuvaa kama mwanamitindo wa nchini Marekani, niambie
na mimi niende. Ukasema ooh mama, hutaweza ni ya kuvaa viatu virefu!” Naya
akacheka sana.
“Malon huyo! Acheni tu. Nilifika pale chuoni Mzumbe wakati naanza
mwaka wa kwanza, watu walikuwa wakiniita mwana mitindo. Walikuwa wanasubiri
nitoke chumbani kwangu ili waone nimevaa nini siku hiyo. Yote hiyo ilikuwa pesa
ya Malon. Akiniona nimependeza ndio ilikuwa furaha yake. Wakati mwingine
tulipokuwa tunakuwa naye Dubai, atanizungusha kwenye maduka ya wanawake ili ninunue
nguo na viatu. Tunarudi Tanzania nakuwa na masanduku utafikiri yabiashara!
Mpaka rafiki zake walikuwa wakiniuliza nimemfanya nini Malon. Na wakati
mwingine walipokuwa wakitaka kitu kigumu kwa Malon, basi wananitafuta mimi,
ndio niwaombee.” Mama yake na baba yake walibaki kimya wakisikiliza.
“Ungemuona jinsi anavyohangaika leo! Mpaka nikamuhurumia. Amehakikisha
nimepata fremu, na akalipia.” “Naya!” Bale akashangaa sana. “Kweli Bale.
Tumetoka hapo, tukaenda kutafuta mafriza, sema hatukufanikiwa, ndio akaona
usiku umeingia, akasema niendelee kesho, baba atakuwa na wasiwasi. Ananiombea.
Yaani amenishika, akaniombea. Anamsihi Mungu anifanikishe na amlindie Naya wake.” Naya
akajifuta machozi. Kisha akaendelea.
“Unakumbuka ile akaunti ulinisindikiza benki nikaenda kuhamisha
pesa zote kwenye akaunti yangu, baba?” “Nakumbuka.” Baba yake akajibu. “Basi huko
ndiko amekwenda kuweka ile hundi ya pesa aliyolipwa na mahakama. Ameniambia
niitumie kuanzisha hiyo biashara huku akiniambia nisiwe na wasiwasi. Hata kama
haitajibu kwa haraka, niipe muda.” “Mmmh! Mungu naye! Kwa nini hampi mtu mmoja
kila kitu?” Mama yake akaongea kwa kunung’unika. Wote wakamgeukia. “Kwa nini?”
Bale akauliza. “Namfikiria huyo Malon na mapenzi yake kwa Naya. Natamani hata
angekuwa na shule kidogo kichwani!” Wote wakashangaa.
“Naombeni msinishangae jamani! Biashara huwa zinakufa. Lakini kama
umesoma, umesoma tu. Ukikwama hapa, unakimbilia kwengine. Sasa huyu Malon
akikwama biashara ndio familia yote imekwama, kwa kuwa hana mbadala!” Naya
aliumia sana. Akainama. Baba yake katika hilo hakuwa akiongea, maana na yeye ni
muhanga wa hayo maneno. Alishakwama kwenye biashara, wakawa wanaishi kwa
mshahara wa mkewe. Na huyo mama alishamwambia hataki Naya aaishie kama yeye.
Baba yake alinyamaza kimya.
“Najua Malon hajasoma mama na anamapungufu yake, lakini sidhani
kama nitakuja kupata mwanaume atakayenipenda na kunijali kama Malo. Ananipenda
kuliko nafsi yake.” “Naelewa kuna mapenzi, lakini hakuna mapenzi na njaa jamani!
Tusidanganyane. Ndoa sio cheni za dhahabu. Itafika kipindi inatakiwa maisha
yaendelee. Hapo labda wapo watoto. Wanatakiwa wale na waende shule. Pesa hamna.
Mnafanyaje? Njaa huwa haichagui kwenye mapenzi. Ikipiga hodi sehemu haichagui.
Mkubwa na mdogo itammaliza mpaka kuliwe. Sasa huyo Malon na umri huo bado
anaanza maisha tu! Mpaka leo anahangaika hana biashara ya maana anayofanya.
Yaani ndio anakwenda kutafuta huko. Akifanikiwa safari hii na kukosa hayo
masoko safari nyingine si ndio biashara imekufa tena?” Kimya.
“Sasa wewe na uzuri wako wote huo utakuwa mtu wakuanza kila siku?
Hapajulikani hata kipato cha mwaka kikoje! Hamjui kesho yenu inakuaje, hamuwezi
hata kuweka malengo! Biashara ikifa ndio anarudi tena kuwa mzigo wako wewe!” Kila
mtu kimya. Walimjua mama yao na shule. Hakuna utakalomwambia bila elimu ya
darasani mkaelewana. Na hivi tayari alishakuwepo Joshi, na anajulikana yupo na
Naya kwenye mahusiano, mama yake alimuona Malon ni kama mvurugaji. Naya
alinyanyuka na kwenda chumbani kwake, wengine nao wakatawanyika kimya kimya
wakamuacha mama yao pale sebuleni.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Huku nimekutana na wazo jingine zuri ya jinsi yakutambua grade ya
Kahawa na Cocoa. Ipo mashine nzuri tu. Lakini inahitaji pesa kubwa kidogo. Na
sitaki kuua biashara, au niseme sitaki kuanzia chini tena. Kuna kitu nakifanya
hapa na Brazili, nataka kuzungusha hii pesa kidogo, faida ndio niagize vitu
China. Usiwe na wasiwasi tena wala usihangaike. Mimi nitashugulikia kila kitu.
Ila itabidi usubiri kama mwezi au zaidi.” “Na pale kwenye ile fremu?” Naya
akauliza. “Patasubiri Naya. Ni afadhali uanze vizuri, kuliko kuanza kama
mbambaishaji wateja wakakukimbia tokea mwanzo.” “Kweli.” Wakaafikiana.
“Unapata muda wa kula?” Naya akauliza. “Nahangaika
mama. Nikipata kifungua kinywa asubuhi, situlii mpaka usiku. Labda hapo baadaye
patatulia na nitakuwa na ratiba yakueleweka.” “Pole Malo. Nakuombea ufanikiwe.”
“Amina mama. Hilo ndilo la msingi. Tutafanikiwa tu. Mungu yupo upande wetu.
Naomba na wewe uamini na ujaribu kutulia. Tafuta kitu chakufanya ukiwa umetulia
sio kwa kupaniki. Na hata ukikosa, jua upo mapumzikoni, kitu kizuri kinakuja.” Naya akaridhika.
“Unapaonaje huko?” “Nimeanza kupapenda. Mpaka nashawishika kuhamia
huku.” “Malo!” Naya akashangaa. “Kwa baraka zako mama. Sitakimbia.” Naya
akacheka kidogo. “Urudi.” “Hata kama nikuhamia, sio kwa sasa. Bado nyumbani kuna
malighafi nyingi zinazoweza kuuzika kwingi. Kuna ugumu kidogo tu napambana nao.
Nipo kwenye kumsihi Mungu, naamini atatufungulia milango.” “Ni pesa?” “Na hilo
pia. Tunahitaji mtaji mkubwa.” “Sasa kwa nini usichukue na hizi? Biashara ya
nyama inaweza kusubiri.” Malo akatulia kidogo.
“Ongeza mtaji Malo. Mimi nitasubiri. Ukifanikiwa, ndipo na mimi
nitafanya. Sio lazima tukawekeza wote kwa pamoja.” “Lakini pia sio vibaya
tukatupia shilingi kila mahali. Huwezi jua wapi patajibu. Anyway, kwa kuwa
nimefika tu, acha nione Mungu ataniongoza vipi. Si ulisema unaniombea?”
“Nakuombea Malo.” “Basi usiache. Niombee Mungu anipe muongozo mzuri, awe na
mimi huku na anifungulie ule mlango nitakao fanikiwa.” “Na urudi nyumbani
salama.” Malon akacheka. “Na hilo pia.” Wakazungumza, na kukata simu.
Joshi!
J |
uma hilo
likaisha, Naya akiwa ametulia sasa, akijua Malon ataleta vifaa. Joshi kimya
kama kawaida yake. Kumtafuta Naya sio kipaumbele. Na yeye Naya akaacha
kumpigia. Jumamosi hiyo akaona ujumbe wake na neno la Mungu. Hakusoma wala
hakujisumbua. Akaangalia tu na kuweka simu pembeni. Ilipofika usiku wake,
akapiga. Ikaita mara ya kwanza mpaka ikakata. Wote wanamwangalia. Ikaita tena,
hakupokea. “Nani huyo ambaye simu zake hazipokelewi?” Mama yake akauliza
akihisi ni Joshi tu. Naya akazima simu kabisa na kuondoka pale.
Kesho yake wakati wapo kanisani wakamuona Joshi naye anaingia na
gari yake. Walikuwa wamesimama tu nje, ndio na wao wamefika. Naya alipomuona,
akajisogeza karibu na baba yake, akatulia. Kila mtu akamuona. Baba yake
akamgeukia kule alikojificha nyuma yake kisha akamgeukia Joshi aliyekuwa
akiwasogelea. “Nakuona mzee umeingia na kifaa!” Bale akamchokoza. “Kitu
kisafiii, kama kimetoka kiwandani!” Bale akaendelea, Joshi akacheka. Akasalimia
kila mtu. “Vipi Naya?” “Safi tu.” Naya akajibu akiwa amesimama palepale pembeni
ya baba yake kama anayemchungulia kidogo. “Nimejaribu kweli kukupigia simu jana
na leo asubuhi.” “Simu nimeiacha nyumbani.” Naya akajibu kwa ufupi tu. Wakatulia
ila jibu likapatikana kuwa aliyekuwa hapokelewi simu zake ni Joshi.
“Kwema baba?” Akaanza mama
Naya. “Kwema tu. Nimekuja kuwatembelea, lakini zaidi kumuona Naya.” Naya
akakunja uso huku ameinama. Akajivuta taratibu zaidi kwa baba yake. “Karibu
sana. Tumefurahi kukuona.” “Asante mama. Alhamisi kuna sherehe kazini, nilitaka
Naya aungane na mimi.” Naya kimya. “Afadhali umtoe kidogo. Amekuwa tu ndani na
baba yake.” Wote wakamwangalia mama yao ambaye ndio alikuwa akijibu. Na wala
hakuishia hapo. Yeye ndio akaendeleza mazungumzo na Joshi mpaka kuingia ndani
ibadani. Wakatoka bado mama Naya akawa anamsemesha Joshi kwa uchangamfu sana,
kisha wakaagana.
Baada ya mama kuweka ubabe na kulazimisha lazima Naya aende huko
anakotaka Joshi, ikabidi Naya kumpigia simu na kumwambia Joshi kuwa itabidi
amfuate hapo nyumbani. Kwa kurudi kwa Malon, japo hakumwambia anataka kumuoa,
ila kila kitu kusema ‘changu, chetu, Mungu atatufanikisha’, kuliibua
kutokubabaishwa ndani ya Naya. Hakumtetemekea tena Joshi na alikwenda kwa
sababu mama yake alishikia bango hiyo safari kana kwamba ndio siku ya harusi.
Hakuna lililozungumzwa kwa amani humo ndani isipokuwa Naya kwenda kwenye hiyo
shuguli na Joshi. Akilala na kuamka ni Naya atoke na Joshi.
“Wewe ndiye unayeharibu akili za Naya, baba Naya.” Kibao kilimgeukia
na baba yake. “Unamtia moyo kwenye vitu visivyo na maana. Kutwa yupo mgongoni
kwako. Huyo Malon akimuoa na kumzalisha, akashindwa kuwatunza, utambeba huyo
Naya na watoto wake? Mwanaume mpaka sasa hana linaloeleweka maishani!
Anahangaika na maisha mpaka leo! Akifanikiwa ndipo anaonekana. Anafanya maonyesho
yake hapo weeee! Akifilisika anapotea. Mungu ametuma rehema, huyu Naya apumzike,
bado unatetea upuuzi wa kijana ambaye hana hata maadili! Hajui hata kutulia ni
nini!” “Malo ameokoka mama.” Bale akaingilia.
“Ameokoka ndio, wala sikatai. Lakini hana wala hajui maadili. Mpaka aje aanze kujifunza maisha na kuelewa kutulia ni nini, au kijana anatakiwa aweje kwenye jamii, huyo sio wa leo. Kwanza kama atatulia sehemu moja. Maana kukua inatakiwa utulie na ukuzwe. Mara yupo Mbeya vijijini, mara Dubai kwa Waarabu. Hajulikani leo yupo wapi na amelala wapi na nani! Hakuna atakayejua kama bado anamsimamo wa wakovu au alisharudia njia zake chafu! Imani ni ya kujengwa jamani. Sasa unafikiri utamfananisha na vijana kama kina Joshi? Alishakataa kuwa chini ya malezi ya wazazi, hajui kijana anatakiwa awe vipi, anabaki akihangaika tu. Hilo alitakiwa baba yenu alione, na kuzungumza na Naya, lakini…” “Mama! Mama!” Naya akamwita. “Nishampigia simu Joshi, tutatoka hiyo siku ya alhamisi.” “Hiyo ndio akili. Utakuwa mtu wa kuhangaika mpaka lini wewe! Unataka maisha yako yawe kama yangu yalivyoharibika! Hata uki…” “Naomba yaishe mama. Naya ameshakubali kutoka. Naomba yaishe.” Bale akaingilia. Baba yao akatoka bila hata jibu, Naya naye akafuata nyuma. Akamfuata baba yake.
Joshi & Naya.
Naya alikwenda Salon siku hiyo ya alhamisi. Akatengenezwa vizuri. Akavaa
vizuri na kupendeza. Akavaa cheni, hereni na bracelet au cheni ya mkononi. Akajiangalia
nakuweka vipodozi kadhaa usoni, akajipenda. Akasikia gari nje, akajua ni Joshi
ameshafika. Mama yake akawa yeye wa kwanza kumfungulia mlango. Akasikia
akisalimia, akatoka. Kila mtu alimshangaa jinsi alivyopendeza. “Umependeza
mama.” Baba yake akamsifia. “Asante.” Naya akacheka. Hakuna aliyemsikia Joshi
akisifia, ila kumtaka Naya waondoke ili wawahi foleni.
Wakiwa njiani ikabidi Naya aulize kwani aliona vile Joshi
alivyojawa wasiwasi usoni kama amechelewa au kuna jambo. Honi za kila mara
hazikuisha humo barabarani. “Kwani inafanyikia wapi?” “Ni ofisini kwetu tu ndio
maana nashangaa jinsi ulivyovaa na kujitengeneza kama tunakwenda kwenye kumbi
kubwa sanaa!” Naya akaumia sana. “Sasa kwa nini hukuniambia nibadilishe pale
uliponifuata nyumbani?” “Hivi unajua kama kuna swala la muda hapa duniani? Watu
wanakwenda kwa mipango na muda. Huwa hatupeleki mambo kiholela holela.” Naya
akanyamaza akiwa amekosa raha. Ikabidi atulie huku akitamani avue hiki au atoe
kile.
Wakafika ofisini kwao. Akajifungulia mlango na kutoka haraka
akimfuata Joshi nyuma. Akafunga gari yake kwa rimoti bila hata kugeuka nyuma.
Naya akaendelea kumfuata kama anayemkimbilia akiwa na wasiwasi. Anajishuku kwa
kujishika hiki na kile huku akiongeza mwendo asije kuachwa. Ni kweli Naya
alikuwa binti mzuri, jasiri, anajiamini. Lakini si mbele ya Joshi. Kuna jinsi Joshi
alikuwa akimfanya ajione si kitu tofauti na Malon. Joshi aliweza kumshusha kwa
sekunde, na kujiona sifuri. Ila Malon alikuwa akiweza kumwinua na kujiona ni
kila kitu.
Wakaingia kwenye huo ukumbi mdogo tu, Joshi akiwa ametangulia
mbele, Naya nyuma. Akatafuta meza wakakaa. Kimya kimya Joshi akiwa kama
amekasirika hivi au ameboreka. Naya akatulia. Akawasogelea Mati. “Mbona mpo
kama mpo msibani? Simama kwanza Naya mdogo wangu. Naona unavutia kwa mbali.”
Naya akatabasamu na kusimama. “Shikamoo.” “Marahaba, Naya. Umependeza sana. Tena
Sana. Twende nikakutambulishe kwa mke wangu. Nilishampa habari ya viumbe
wachache kama wewe, mliobaki hapa duniani.” Naya akacheka, Mati akanyoosha
mkono amshike.
“Vipi Joshi! Upo kwenye maombi nini? Mbona sura hiyo mkuu!?” Mati
akamtania. Joshi alikuwa kijana wakuheshimika sana pale ofisini. Alijulikana ni
kijana mwenye maadili na mcha Mungu. Mnyenyekevu na mwadilifu. Mati akapokea
mkono wa Naya, akashtuka kidogo. “Nini?” Naya akauliza kwa kushangaa. “Hii
bracelet niliiona kwenye wallet ya mtu!”
Mati akaongea kama anayefikiria. Naya akajishika shingoni kwa wasiwasi.
Mati akahamia shingoni kwa Naya akiwa ameduaa.
“Uliona kwenye wallet ya nani?” Akauliza Naya taratibu. “Mmmh!”
Mati akaguna na kuhamia masikioni. “Hii si ni set nzima?” Akauliza Mati, kisha
akacheka kidogo. “Nimeshajua vilipotoka.” Akajijibu Mati mwenyewe, na kumvuta
mkono Naya. “Naamini kasisi hutajali?” Akimaanisha
Joshi. Walikuwa wakimwita Kasisi hapo ofisini kwao. “Bila shaka.” Joshi akajibu
kwa heshima, Naya na Mati wakaondoka.
Alipofika kwa mkewe, akamvutia kiti Naya. “Huyu ndiye Naya.” Mkewe
aliyekuwa akinywa kinywaji fulani kwenye glasi akageuka. “Ulivyomchanganya mume
wangu! Haishi kukutaja. Hujambo Naya?” Naya akacheka. “Sijambo, shikamoo.”
“Marahaba mama. Hongera kwa kumaliza chuo na kuwa mtoto mzuri. Mati anakusifia
sana, au umebadilika?” Naya akacheka na kutingisha kichwa huku akikataa. “Sasa
nasikia umemuacha Malon, upo na Joshi. Unampenda lakini au?” Mke wa Mati
aliendelea kumuuliza taratibu tu huku akinywa. Alionekana ni dada anayejitambua.
Mtu mzima kidogo, mrembo tu japo alikuwa na mwili kumpita mumewe. Kwa harufu
ile, Naya akajua anakunywa kinywaji kikali.
Mati akabaki akimtizama. “Lakini umebadilika Naya! Umekua mtulivu
kuliko ninavyokufahamu. Naya ninayemjua mimi ni machachari. Vipi bwana?” Naya
akamtizama Mati na kucheka. “Au Joshi anakupitisha kwenye maombi mengi?” Mati
aliendelea kumtania, mpaka mkewe akacheka. “Ila Umependeza na unaonekana ni binti
mzuri. Nimefurahi kukufahamu Naya. Ukaribie nyumbani.” “Asante.” Naya akamjibu
mkewe huku akimtizama Mati na kucheka. “Twende tukacheze mziki halafu tutete
kidogo kabla hujarudi kwa Joshi.” Akamshika mkono. “Narudi mama. Ngoja
nikacheze na Naya.” Mati akamuaga mkewe, na kuondoka.
Akamshika vizuri Naya kwa heshima tu, wakaanza kucheza mziki wa
taratibu. “Malon yupo wapi?” Mati akauliza swali la moja kwa moja. Naya
akacheka kidogo na kuinama. “Najua hivyo vitu vinatoka kwa Malon.” Mati
akaendelea. “Amesafiri kwenda Dubai.” “Kwema?” Mati akaendelea kudadisi.
“Kwema. Ni mambo yake ya kibiashara tu.” “Kumbe alifanikiwa?” “Kwenye nini!?”
“Hakuniaga kama anaondoka, lakini mimi ndio namsaidia kwenye mambo yake ya
biashara. Sio kiofisi, lakini huwa akikwama au akitaka ushauri wa kisheria
kwenye mambo ya biashara, huwa ananipigia. Hata mkataba wa ile nyumba yake ni
mimi nilimsaidia. Ila sikujua kama bado mpo pamoja! Nilipomkuta na hii bracelet
peke yake, alikuwa akitoka kwa sonara. Akasema alitoa cheni, lakini haikuwa
imekamilika. Hakuwa na pesa. Ndio amemalizia bracelet. Siku nyingine akiwa
anashugulikia kibali chake cha kusafirisha mzigo kuutoa hapa nchini, aliniomba
tukutane nje ya sonara moja kule posta. Nikamuuliza pale anafanya nini,
akanikumbusha ile bracelet, akasema ilikuwa pia haijakamilika kwa kuwa haikuwa
na hereni zake. Ndio alikwenda kupunguza pesa hapo kwa sonara. Nikajua amepata
mwanamke mwingine. Sikukufikiria kama ni wewe, kwa kuwa wewe najua upo na Joshi!”
Naya akashindwa hata ajibu nini.
Mati akamuona kama anafikiria na kukunja uso. “Naya?” “Abee!” Naya
akamwangalia. Lakini safari hii hata macho yalikuwa yameshajaa machozi. “Upo na
Joshi au Malon?” “Hizi ni zawadi tu kaka Mati. Nipo na Joshi. Hata Malon
anajua.” Naya akajibu kwa unyonge. Mati akabaki akimtizama machoni huku
wakicheza. “Ni zawadi tu kaka yangu.” Naya akasisitiza. “Siku ya mahafali
alikuja mpaka kule Mzumbe, akaniletea hii cheni. Lakini sikuwa najua kama
havijakamilika. Kwa kuwa alinikabidhi na kuondoka. Baada ya siku chache, kama
majuma mawili hivi, ndipo akaniletea na hii ya mkononi. Siku kumi kabla
hajaondoka kwenda Dubai akaleta na hereni zake. Akaniambia sasa ndio
imekamilika.” “Joshi anajua?” Mati akadadisi. “Joshi yupo busy sana na kazi
zake. Hana muda wa mambo kama haya.” Hilo jibu likatosha kabisa kumfanya Mati
aelewe kila kitu. Walicheza mpaka mziki ulipoisha, akamrudisha Naya kwa Joshi.
“Kasisi! Nimekurudishia mrembo wako. Naona jamaa wanameza mate,
wasije kumpora mikononi mwangu bure. Sitaki kesi.” Mati aliongea huku akimvutia
kiti Naya. Akakaa. “Asante.” “Karibu.” Mati akajibu na kuondoka pale. Kimya.
Baada ya muda Mati akarudi tena na kinywaji cha Naya, maana alikuwa amekaa tu
hana hata kinywaji. “Asante.” Akashukuru Naya, na tabasamu usoni. Alipoanza tu
kunywa, Joshi akamgeukia. “Nataka kuwahi kulala. Naomba umalizie kicho kinywaji
sijui pombe, nikurudishe nyumbani, ili nikalale.” Naya akashangaa sana. Hata
hawakula wakati harufu ya chakula ilikuwa imeshaenea mle ndani. “Hii ni juisi Joshi!
Na hakuna ulazima wa kuimaliza. Tunaweza tu kuondoka.” Naya akajibu kwa upole. Joshi
akavuta kiti, akasimama na kutoka pale ukumbini. Ikabidi Naya afuate nyuma tena.
Akamkuta amesimama pembeni ya gari lake kama anayemsubiria. Naya
akamsogelea. “Unaumwa?” Naya akauliza tu kwa upendo. “Hivyo vitu umevipata
wapi?” “Vitu gani.” “Si hivi!” Akamvuta
mkono kwa nguvu. “Unaniumiza mkono Joshi! Kuna nini!?” Naya akashangaa.
“Nakuuliza umepata wapi haya maurembo?” “Amenipa Malon.” Naya akajibu huku
anavuta mkono wake ambao Joshi alikuwa ameushikilia kwa nguvu. “Kwa hiyo
unahongwa na Malon?” “Unaniumiza Joshi! Tafadhali naomba niachie mkono wangu?”
“Nakuuliza unahongwa?” Naya akauvuta mkono wake kwa nguvu nakuanza kulia. “Hii ni
zawadi alinipa kwa sababu ya kuhitimu chuo. Hata wazazi wanajua.” Joshi
akazunguka upande wa dereva akapanda kwa hasira. Kitu kilimkaba Naya,
akashindwa hata kusogea.
Joshi akawasha gari na kumpigia honi wakati yupo palepale
akimtizama. Alipoona Naya hazunguki upande wa abiria, amebaki akijiangalia
mkono wake aliokuwa amemuumiza, akashusha kioo. “Panda wewe. Unashangaa nini?
Kaa hata nyuma kama unashindwa kutembea sababu ya maviatu hayo marefu uliyovaa
bila sababu.” Naya hakumjibu. Moyo wake ulikuwa umeumia sana. Akaamua aondoke.
“Unakwenda wapi sasa? Ingia mlango huu.” Naya hakujibu. Akainama, akavua viatu
vya juu alivyokuwa amevaa, akaondoka pale bila hata ya kugeuka nyuma, akielekea
posta mpya kufuata daladala. Joshi naye hakutaka kubembeleza, Naya akamuona
anatoa gari yake na kuondoka bila hata kujua ananauli au anarudije nyumbani
kwao Kiluvya.
Naya alifika posta, akasubiria hapo daladala. Kwa kuwa ilikuwa
siku ya kazi kwa mida ile bado akapata daladala. Akaunganisha daladala mbili
mpaka kufika kwao ilikuwa saa 3 usiku. “Joshi yuko wapi!?” Baba yake akauliza
wakati anamfungulia mlango. Naya alikuwa akilia kabla hajafika hapo. Baba yake
akajua. “Kwa nini umerudi peke yako?” Kimya. Akarusha viatu na kuelekea jikoni.
“Wewe unatoka kwenye sherehe, unakuja kula nyumbani!” Bale akamuuliza kama
kumsanifu. “Joshi aliniambia anataka kuwahi kuondoka ili awahi kulala.
Hatukula.” Ukimya ukazuka. Naya alijibu huku akifunua masufuria ya huko jikoni.
Wote bado walikuwa sebuleni, Bale mchokozi alikuwa kwenye meza ya chakula,
akifanya mambo yake ya shule kwenye komputa.
“Sasa kama ana usingizi wa kipuuzi hivyo kwa nini alikuja
kukufuata? Kwanza kwa nini hakukurudisha?” Bale akahoji kwa hasira kidogo. Raha
ya Bale ni yeye ndio amlize Naya, lakini sio vinginevyo. Na tokea wadogo wakiwa
wanacheza. Usimguse dada yake huko nje. Ila wakiwa ndani, yeye ndio mchokozi,
na hatulii mpaka amuone analia ndio furaha yake. Naya akanyamaza. Akachukua
chakula, na kwenda kukaa pale pale mezani. Kimya. “We Naya?” Bale akamuuliza
tena. “Nilimuacha nje sehemu ya kuegesha
magari.” “Kwa nini?” Naya akasimulia mwanzo mpaka mwisho. “Anahaki yakuchukia.”
Mama yake akadakia na kushangaza kila mtu. Mpaka Bale akabaki ametoa macho.
“Unasema kweli mama!?” Bale akauliza kwa mshangao mkubwa sana. “Ndiyo. Sasa kwa nini apokee hongo kwa mwanaume mwingine?” “Hongo au zawadi hii ya kumaliza chuo? Yeye alikuja kwenye mahafali ya Naya hata kadi ya pongezi hakumletea Naya!” “Si alisema ametoka kazini?” Mama yake akazidi kutetea. “Kwani hizi zawadi zakutoka kwa Malon alizileta lini? Au swala la kuwa Naya anahitimu Mzumbe yeye alikuwa hajui? Zawadi inaandaliwa mama. Na kwa sababu yeyote ile, asingemuacha Naya usiku huu anarudi nyumbani peke yake! Sasa hivi Malon hana usafiri, lakini anamrudisha Naya nyumbani kwa daladala! Anahakikisha Naya yupo ndani ndio anaondoka. Ni nini unatetea mama!?” Bale akauliza kwa hasira. “Kwani wewe hujamsikia jinsi Naya mwenyewe alivyosimulia? Anasema aliondoka pale. Sasa mlitaka yeye Joshi afanye nini?” Mama yao akazidi kutetea. Bale akasimama pale kwa hasira na kuingia chumbani kwao. Hakutaka kuongea tena.
Siku ya Ijumaa, Mati kwa Joshi.
M |
ati
akachungulia ofisini kwa Joshi, alipomuona yupo akamsalimia na kuingia. “Vipi Kasisi?”
Joshi akanyanyua kichwa. “Karibu Mkuu.”
“Upo busy sana?” “Karibu tu.” Mati akaingia ndani kabisa na kufunga mlango.
“Jana mbona mliwahi kuondoka, kwema?” “Nilikuwa sijisikii vizuri nikaona
nikapumzike.” Mati akabaki akimwangalia kama bado hajapata ukweli, Joshi
akababaika na kuongeza. “Hata hivyo niliona muda umekwenda sana. Halafu nikaona
mambo yanavutwaa.” “Saa mbili!” Mati akashangaa kidogo. “Sijui lakini, ila
nahisi uliharakisha Joshi. Yule binti alikuwa amejiandaa kwa shuguli.
Kumwingiza kwenye shuguli na kumtoa bila hata chakula, sidhani kama ilikuwa
uungwana!” Joshi akanyamaza.
“Mimi ni mkubwa kwako, Joshi. Na ninaheshimu kumfahamu Naya
kupitia wewe. Ila unanijua jinsi ninavyoweza kumsoma mtu kwa haraka. Mtu
akishazungumza na mimi maneno machache tu, najua mengi hata ambayo bado
hajazungumza. Nakumbuka kukupongeza mwanzoni kabisa mlipoanza na Naya.
Simfahamu kwa undani, lakini kwa kile ninachokijua kwa yule binti, na mapito
aliyopita na Malon, ni binti wa kumuenzi sana.” Mati akavuta kiti akakaa mbele
ya Joshi.
“Nazungumza na wewe kama nilivyozungumza na Malon. Mwanaume
atakayefanikiwa kumuweka ndani Naya, atanufaika kwa mengi.” “Labda muonekano
tu.” Akaropoka Joshi. Mati akatulia kidogo. “Namaanisha maisha yanataka zaidi
ya muonekano.” Akasisitiza Joshi. “Mimi sijui huwa unazungumza nini na Naya,
lakini nafikiri upo na Naya wa tofauti na ninayemfahamu mimi na Malon. Nilikaa
zaidi ya lisaa, nikimsikiliza Malon akimzungumzia Naya. Lakini siye Naya
niliyekuona naye jana.” Mati akacheka kidogo.
“Naya aliyemzungumzia Malon, Naya niliyemfahamu mimi, ni binti
anayeweza kukusanya mamilioni ya pesa, kwa muda mfupi sana. Tena kwa nchi hii
hii ambayo mimi na wewe tunasikia watu wakisema na kulalamika uchumi ni mgumu.
Naya huyu unayesema ni muonekano tu, siye huyu aliyekuletea mamilioni ya pesa
kumtoa Malon jela?” Mati akamuuliza na kuendelea. “Mbali na hizo pesa, Naya
alinipa pesa zingine zakuharakisha Malon atolewe jela. Akihangaika kwa jasho
lake. Malon anakiri kwangu hajawahi kukutana na binti mwenye akili na uelewa
mkubwa wa mambo kama Naya. Anasema anaweza kugeuza kitambaa cha pesa ndogo
sana, kikawa kitu cha thamani kubwa sana watu wenye pesa na akili zao,
wakanunua kwa kugombania. Anauwezo wa kugeuza kandambili au sendozi ya mmasai,
ikawa kitu cha thamani akauza kwa pesa nyingi. Malon anasema akiongea Naya,
huwa anaandika au anatekeleza kwa haraka. Na anasema hajawahi kutofanikiwa
kwenye mawazo ya Naya.” Joshi kimya.
“Kuna kasumba. Na wengi tunaanguka hapo.” “Kasumba gani?” Joshi
akauliza. “Ni wachache sana. Tena narudia ni wanaume wachache haswa, ni kama
Malon ndio namuona baada ya miaka mingi sana kuona mwanaume anakuwa na kitu cha
thamani mkononi, na kutambua kama ameshika kitu cha thamani na kukienzi. Na
wakati mwingine, ni ngumu kuishi na wanawake hawa wenye uelewa mkubwa sana. Ni
ngumu. Kwa hiyo badala ya kuwaenzi, upo udhaifu wa kuwadidimiza.” Mati
akasimama na kutoka akiwa ameshamchukia sana Joshi.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Joshi akabaki pale akifikiria. Akaamua kumpigia simu Naya.
Akagundua ni kama haiendi kabisa. Akajua amemblock. Akampigia na simu ya pale
ofisini kwao. Ikawa hivyo hivyo. Akajua kwa hakika amemfungia kabisa kila aina
ya namba aliyojua Joshi anaweza kumtafuta nayo. Jioni alipotoka kazini akaamua
kwenda nyumbani kwao.
Sababu ya foleni, akafika nyumbani kwa kina Naya usiku wa saa
mbili. Akakaribshwa vizuri sana na mama Naya. Bale, Zayoni walikuwa mezani,
Naya na baba yake wanaangalia mpira, Naya akishangilia kama kocha wa hiyo timu.
Ila kwa sauti zaidi ili kumkera Bale ambaye walikuwa upande mmoja. Nyumba nzima
waliipenda hiyo timu. Ila ushangiliaji wa Naya ndio uliokuwa ukimkera Bale.
“Acha kelele Naya! Ni nini bwana?” Alipoingia Joshi, kila mtu kimya. Mbali na
kuitikia salamu, baba yake Naya hakutaka hata kuongeza neno.
Mazungumzo yakawa ya mama Naya na Joshi. Pongezi za hapa na pale
zikasikika. “Kesho kuna tafrija nyumbani kwa dada. Mdogo wangu yule aliyemaliza
na Naya chuoni analipiwa mahari. Wazazi na ndugu mbalimbali watakuwepo pia.
Nilitaka na Naya awepo ili kumtambulisha kwa ndugu. Bahati kama hizo za ndugu
kukusanyika pamoja huwa hazitokei mara nyingi.” “Ni kweli baba. Mambo kama hayo
huwa ndiyo yanakutanisha watu.” Akajibu mama Naya. Wengine wote kimya. “Basi
nitakuja kumchukua kwenye saa nne asubuhi, ili apate muda na familia.
Wafahamiane kabla ya shuguli ya jioni.” “Wazo zuri kabisa.” Akajibu mama Naya.
“Mnafanyia wapi?” Akadakia Bale. “Nyumbani kwa dada.” “Hilo
nimelisikia. Nataka kujua eneo kabisa ili tujue pakumfuata usiku, utakaposhindwa
kumrudisha hapa nyumbani.” Ukimya mzito ukatanda. Joshi akajikaza kiume na
kujibu. “Jana ni Naya mwenyewe aliondoka.” “Na wewe ukamuacha mtoto wa kike
anarudi nyumbani peke yake! Wangemkamata huko usiku na kumtenda vibaya?” Bale
akaendelea kumuhoji. Kimya. “Halafu ulivyo wa tofauti, hata usipige simu kujua
kama alifika nyumbani salama au la. Unarudi tena leo kumtaka tena!” “Ilitokea
kutoelewana tu.” Joshi akajitetea. “Ndio na mimi nakuuliza ni wapi mnakofanyia
hiyo shuguli ili ikitokea kutoelewana tena, tuje tumfuate wenyewe?” “Siwezi kurudia
kosa. Hata mimi nimejifunza. Naomba radhi kwa Naya, na kwenu. Ikitokea
kutoelewana tena, na Naya akaondoka kama jana, nitamfuata. Hata ikibidi kupanda
naye daladala mpaka nimfikishe hapa, nitafanya hivyo ndipo nirudi nikafuate
gari yangu.” Hapo akawa amewafunga mdomo. Baba Naya kimya.
Wakati anatoka, akamuomba Naya amsindikize. Naya akatoka naye.
Alijishusha mpaka Naya akashangaa. Akaomba msamaha, akajinyenyekeza mpaka Naya
hakuamini kama ni Joshi. Akaongea maneno ya upendo na yakiuungwana, mpaka Naya
akaona asamehe tu yaishe. “Kwa hiyo nitakuona kesho?” Akauliza Joshi na
tabasamu baada ya kusamehewa. “Ulisema saa nne?” “Ndiyo.” “Utanikuta nipo
tayari.” Wakaagana, Joshi akaondoka.
Naya ukweni, Malon naye arudi nchini.
Apambana na mama Naya, nakumfukuza vibaya sana.
I |
lipotimu kama
saa 4 na robo asubuhi, Joshi akawa anaegesha gari nyumbani kwa kina Naya.
Akaingia ndani, akamkuta mama yake Naya. Wakazungumza kidogo, Naya akatoka.
Baada ya kusalimiana, wakatoka. Baba yake Naya alitoka na kina Bale. Bale
alikuwa akishushwa Ubungo, akielekea chuoni Mlimani. Nyumbani alibaki mama Naya
tu.
Wakati anafua nje, Malon naye akaingia akitembea tu. Akamsogelea
mama Naya. Alijua wazi yule mama hampendi, na alitamani awe anamkuta Naya au
angalau baba yake. Akamsogelea kwa tahadhari kidogo. Akamsalimia. “Karibu.”
“Asante mama.” “Umerudi lini?” “Nimeingia na ndege ya leo asubuhi, nilikwenda
nyumbani kubadilisha tu, nikaja hapa.” “Na hapa napo nipo mimi tu. Naya amekuja
kuchukuliwa na mchumba wake, anakwenda kutambulishwa kwa wakwe zake.” Moyo wa
Malon ukaumia sana.
“Na sidhani kama watarudi mapema. Maana jana walikuwa wakizungumza
hapa kuwa asubuhi hii utakuwa muda wa familia tu. Kuwa pamoja na kufahamiana
zaidi. Jioni kuna shuguli. Mdogo wake Joshi analipiwa mahari leo. Ndio wakwe
nao wanataka kumuona Naya.” Malon kimya akisikiliza. “Naona Joshi amekazana
kweli!” Akaongeza mama Naya na kucheka kidogo. “Anaonekana ni kijana
aliyetulia. Mwenye maadili, msomi, anampenda Mungu na Naya. Juzi pia alikuja
kumchukua hapa na kwenda naye kwenye pati yao yakiofisi. Naya amejawa furaha na
ana amani.” Malon kimya. Wakatulia kidogo.
“Basi nitarudi wakati mwingine.” “Hapana Malon. Huko
nikumchanganya Naya. Labda niulize tu, nia yako ni nini kwa Naya kama si
kumchanganya tu? Eti Malon?” Yule mama akambadilikia. “Umekuwa mtu wakutoka na
kurudi bila taarifa wala kuaga. Umeharibu maisha ya Naya. Sasa hivi unarudi na
miradi ambayo haina kichwa wala miguu. Unataka nini kitokee kwa Naya? Kwa nini
unataka kumvuruga? Cheni na hereni havijawahi kujenga maisha ya unyumba.
Unakuwa mtu wakurudi na kumvuruga, halafu unapotea. Wewe mwenyewe hujajiweka
sawa. Si kimaisha tu, hata na Mungu wako! Hujulikani utalishwa na kukua kiroho
Mbeya au Dar! Tanzania au Dubai! Hujatulia sehemu moja! Halafu eti leo unataka
kumchanganya na Naya kwenye kuchanganyikiwa kwako!” Malon kimya kama amepigwa
na kibumbuwazi.
“Hebu kuwa mtu mwenye utu wewe kijana. Au kwa kuwa hujawahi
kulelewa unakuwa kama upepo tu!? Hapana, sitakuruhusu uendelee kuharibu maisha
ya Naya. Kama unazo pesa, tafadhali nenda ukajijenge wewe kwanza. Tulia
kanisani angalau ukue kiroho. Kwa umri huo umechelewa kujengwa na wazazi,
lakini sidhani kama na Mungu naye atakushindwa. Tulia sehemu moja. Kubali
kulelewa kwenye kanisa moja. Chini ya mchungaji mmoja, pengine utasaidika.”
“Nimeelewa mama.” Malon akageuza hapo hapo nje, nakuondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ilipofika jioni, watu wakaanza kurudi hapo nyumbani. Kwenye mida
ya saa mbili Naya naye akarudishwa akiwa amepooza sana. Joshi akaingia naye
ndani. Akasalimia. Mama Naya akamkaribisha chakula, akasema ndio wametoka kula
tu. Hakukaa sana, akasema anawahi kanisani kuandaa ibada ya kesho yake,
kanisani kwao. Akaondoka baada yakusifiwa sana na mama Naya. Baba yake
akamtizama Naya, akajua mambo hayakwenda vizuri. Hakuna aliyeuliza. Kimya.
Wiki hiyo ikaisha kimya. Naya hakumsikia Malon. Kwanza hakujua
hata kama amerudi nchini. Akaanza kukosa raha. Kila wakati macho kwenye simu.
Hapakuwa na ujumbe wala simu. Jumapili waliondoka hapo kwenda kanisani akiwa
amepooza, akashindwa hata kunywa chai. Waliwahi kidogo kufika kanisani. Wakawa
wamesimama tu nje ya gari yao wakisalimiana na watu. Mara wakaona tena gari ya Joshi
inaingia. Naya alipoiona tu akakunja uso. Akashuka kwenye gari yake akiwa
amehamasika kweli, akawasogelea pale akiwa ameshika karatasi.
“Nimemletea Naya habari njema. Nahisi Mungu wetu amejibu kwa
moto.” Akamkabidhi Naya zile karatasi. Naya akaisoma kwa muda kidogo, ilikuwa
imechapishwa. Akasoma na kuigeuza huku Joshi akicheka kwa ushindi. Kama ilivyo,
Naya akamkabidhi baba yake karatasi zote kisha akasimama nyuma ya baba yake
kabisa, akainama. Baba yake akamgeukia akamtizama vile alivyoinama. “Ni nini?”
Mama Naya akauliza. “Au labda Naya hujaelewa. Hiyo ni scholarship. Wanakulipia
kila kitu. Bahati kama hizo haziji mara mbili hasa kwa aina ya masomo hayo
mliyosoma nyinyi.” Akasisitiza Joshi.
“Kwani ni nini!?” Mama Naya akavuta zile karatasi kutoka mikononi
kwa mumewe akaanza kusoma. “Masoma hayo aliyosomea Naya hayana ajira baba
yangu.” Joshi akamgeukia baba yake Naya. “Wanaitwa wauza sura. Hakuna kazi hapa
nchini ndio maana mpaka sasa unaona Naya anahangaika hapati kazi.” Yale maneno
yalimkasirisha sana baba yake Naya. “Bahati kama hizi haziji mara mbili. Kwanza
aniambie mwenyewe Naya ni wapi ameshawahi kuona scholarship za watu wa masoko!
Atahangaika hapa nchini mpaka…” “Nani amekwambia Naya anahangaika?” Akadakia
Bale huku anacheka.
“Si anahangaika kutafuta kazi hapati?” “Wapi umemuona Naya
anahangaika kutafuta kazi!?” Bale akauliza tena. “Wewe ndiye unayehangaika.
Huna habari yeyote unayozungumza na Naya isipokuwa kuajiriwa kwake. Wakati wote
unamtia pressure kumuonyesha amechelewa, hajafanya juhudi zakutosha, anatakiwa
afanye hivi au vile. Unamtia wasiwasi na kuonyesha hajafanya au hana uwezo wakufikiri.”
“Hapana Bale. Anataka kumsaidia Naya.” Mama yake akaingilia. “Anamsaidia
kufanya nini? Eti mama? Kipi kinakufanya ufikirie Naya anahitaji msaada wa Joshi?”
Bale akawa amekasirika kabisa nakushindwa kujizuia.
“Kabla Joshi hajaja kwenye maisha ya Naya, Naya alikuwa mtu wa
mipango ya kueleweka. Wote tumeshuhudia akili ya Naya. Ni zaidi ya kukaa
darasani na kufaulu. Naya kabla hajamaliza chuo, alijaza watu pale ubungo
Plaza, akafanya mambo makubwa ya kihistoria hapa nchini. Wapo wanamitindo wa
ngapi hapa nchini jamani? Tena kwa umri mdogo wa Naya? Wewe mwenyewe mama ulikuwa
huamini kama ni Naya amesimama pale mbele siku ile akipigwa picha na waandishi
wa habari. Ghafla amekuja Joshi, amemgeuza Naya kama mjinga asiyeweza kufikiri!
Kwa kuwa yeye anayo kazi ya uhasibu?” Bale akapata jukwaa.
“Unamgombesha nani sasa hapa?” Mama yake akauliza kibabe. “Mimi
sigombi mama, lakini nataka tufikirie na tusipelekeshwe. Kwanza wewe mwenyewe Joshi
hata humfahamu Naya, halafu unajichukulia tu mamlaka juu yake.” “Ulitaka
amfahamu vipi?” Mama yake akauliza kwa ukali. “Usikasirike mama. Lakini nina
uhakika kama Joshi angekuwa anamfahamu Naya hata kidogo tu, asingekuwa
anazungumza hata kidogo mbele yake. Watu wanaomjua Naya, akiongea huwa
wanasikiliza.” “Ni huyo Malon?” Akauliza mama yake kwa kejeli.
“Huyu Naya anasehemu zake tatu anazosimama akiwa na mwanaume
yeyote anayemtaka, akiwa na baba. Nyinyi hamjamsoma Naya na kumfahamu.” Wote
wakamgeukia yeye Bale, mpaka Naya mwenyewe. “Kwanza anayo sehemu moja tu
anayotupa mambo yake. Pale kwenye ile mikono ya baba. Iwe furaha au huzuni.
Akiwa na mwanaume anayemtaka yeye, na anayejua anampenda kwa dhati na
kumuheshimu yeye na mawazo yake, atasimama mbele kidogo ya baba. Anakuwa kama
ametangulia hivi. Akisimama pembeni yake, ujue unayo nafasi. Hata mama
akiongea, anaweza kumsikiliza, akakusikiliza tena. Lakini kwa wanaume kama wewe
Joshi, akishafika hitimisho kama hivi leo, kwa mara ya kwanza katika watu wa
sampuli yako, anasimama nyuma. Kama pale alivyo kwa baba. Nyuma kabisa. Huna
utakalomwambia tena pale Naya, akakusikiliza tena. Hata kwa vitisho vya mama,
au hata umwambie unampa gari, hatakusikiliza tena.” Naya akainama na kujivuta
nyuma ya baba yake zaidi.
“Kumtoa pale anaposimamaga, inahitaji mwanaume haswa, sio
wavitisho wala gari. Ndio anaweza kukutizama tena na akakusikiliza. Na
usifikirie wewe ndio mwanaume wa kwanza kumfuata Naya ukiwa na gari.
Usijidanganye, na wala hutakuwa wa mwisho. Washakuja wasomi, wenye nyumba na
magari mazuri tu, hakuna aliyembambaisha Naya. Naya anayo mapenzi ya baba,
anajua kupendwa ni nini. Hizo scholarship zako hazimtishi. Na nikupunguzie tu
matatizo, hivi unavyotuona sisi, hatuna shida wala hatuhitaji mkombozi. Usije
kwa Naya kama unayetaka kumsaidia. Naya hahitaji msaada wala mtu wa kumkomboa.
Kama unataka mke, njoo ukiwa umejipanga kuwa mume, acha kumnyanyasa Naya.” Bale
akaondoka kabisa pale kanisani.
Naya akabaki vile vile ameinama pale nyuma ya baba yake. “We
Naya?” Mama yake akamwita kwa ukali kidogo. “Mimi sitaki kwenda kusoma popote
pale. Hata Joshi mwenyewe simtaki.” Mpaka baba yake akamgeukia. “Utakuja kujuta
Naya wewe! Huyo anayekupa kichwa hivyo sio..” “Acha kumtisha mtoto mama Naya!”
Baba yake akapokonya zile karatasi, akamkabidhi Joshi mkononi. “Usiku uliomuacha
mtoto wangu peke yake, akarudi anatembea peke yake na giza, ulifanya kosa kubwa
sana. Ni heri ungenipigia mimi mwenyewe simu, nikamfuata mtoto wangu, kuliko
kuja kumfuata nyumbani, na kwenda kumtelekeza katikati ya jiji.” Baba yake
aliongea tu hivyo na kuondoka pale. Naya akamfuata kwa haraka. Walipofika tu
ndani kanisani Naya na baba yake, wamekaa, Zayoni akaingia. “Mama amesema
tuondokeni. Anataka tumrudishe nyumbani.” Bila kujibu kitu, wakanyanyuka.
Naya akajua moto utawaka. Na kweli, walipoingia tu ndani ya gari,
akaanza kuongea mama Naya. Aliongea mengi bila kunyamaza wala kutulia. Aliongea
kama anataka kutoa laana. Akalaumu. Akampa angalizo Naya, akamtisha mpaka
wakafika nyumbani. “Naomba usinitafutie mwanaume mwingine tena na wala usining’ang’anize
kuolewa.” Kila mtu akashtuka. “Umeniambia nini Naya?” “Mimi sipo tayari kuolewa
mama. Naomba niachwe kwa sasa.” “Basi hata huyo Malon nisimuone hapa nyumbani
kwangu.” “Sawa.” Naya akajibu nakushuka garini.
“Unakufuru mama Naya, mke wangu! Kwa yote haya Mungu aliyotupa,
jitihada zangu zote. Mchana na usiku nahangaika, bado unamtisha Naya kwa
kumwambia ataishia kama wewe! Kana kwamba maisha yako ni mabaya sana! Kweli!?”
Baba Naya naye akashuka, na Zayoni naye akashuka. Walimkuta Bale nyumbani. Siku
hiyo hapakuwa na ibada, kila mtu akaingia chumbani kwake.
Ilipofika mchana, Naya akasikia anaitwa kwa ukali. “Unalala ukitegemea nani akupikie? Ingia jikoni uandae chakula.” Naya akaingia jikoni. Hakuwa anajua hata anatakiwa kupika nini. “Na itabidi ubadili maisha yako. Kwa kuwa umekataa kuolewa, unaonekana unataka kuendelea kuishi humu ndani na baba yako, itabidi sasa uanze kujifunza kupika. Kuanzia leo, kazi za jikoni ni zako. Na ninaomba uivishe. Hakuna wakukusaidia. Maana muda mfupi tu Bale ataondoka na kuhamia chuoni kabisa, atakuacha hapa. Na mimi nitakuwa kazini. Sasa wewe ambaye huolewi, huna kazi na hutaki kuendelea kusoma tena, huwezi kukaa bure tu. Kule mabandani yupo mtu wakumsaidia baba yako, kunakohitajika mtu ni humu ndani. Anza kujipanga. Kufua, kupika na mambo yote ya humu ndani ni wewe.” Kila mtu akajua ndio adhabu yake. Na wakajua mama yao anafanya makusudi kuwaadhibu wote. Lakini hakuna aliyejibu. Na kweli Naya akaanza majukumu ya ndani muda huohuo, mama Naya hakumtania.
kukosa Bara na Pwani...
A |
kiwa amechoka
sana, usiku huo wa jumapili, akiwa amelala kitandani kwake, akaamua kumpigia
simu Malon. Kama kujaribisha tu, kujiliwaza. Kwani alijua Malon yupo bado
Dubai. Akashangaa simu yake inaita. Akakaa kwa haraka. “Malo!?” Naya akaita
kwa mshtuko. “Pole nimekuamsha.” “Hamna neno. Vipi?” “Upo Tanzania!?” Naya akauliza
kwa mshangao. “Ndiyo.” Naya akahisi hajaelewa. “Upo Tanzania hii hii!?” “Nipo Naya!” Naya
akatulia kidogo kama mwenye maswali. “Umerudi lini?” “Kwani vipi mama, mbona
maswali?” Naya akaishiwa nguvu kabisa asiamini kama ni Malon.
“Nilijua ukirudi utanitafuta!” Naya aliongea kwa unyonge akisikika kuishiwa
nguvu kabisa. “Nakumbuka mara ya mwisho wakati tupo
kwenye mahusiano, kilio chako ilikuwa nitulie na wewe Naya. Hukupenda jinsi
nilivyokuwa na wewe, huku nikiwa na wanawake wengine. Sasa na wewe usiwe kama
mimi. Au usiige tabia mbaya. Sitaki mimi niwe sababu ya kukuharibu. Unaye
mchumba wako, ambaye mpaka unafahamika kwa wazazi wake, nashauri utulie naye.
Na mimi kuwepo kwenye maisha yako, sio salama na si sawa hata kwa Joshi.
Inakuwa kama nakusababisha kumsaliti mwanaume uliyemkubali kwenye maisha yako.
Hata wazo lakufanya mambo bila kumwambia, nimefikiria, nimeona sikukushauri
vizuri. Hamtajenga mahusiano mazuri.” Naya
alikuwa ametulia tu akisikiliza.
“Si sawa kuwa kwenye mahusiano ya kueleweka ambayo unaingia mpaka
kwenye ndoa, huku nikikushauri mambo kinyume na mwenzio. Nafikiri unahitaji
kumsikiliza na kujenga mahusiano yenu bila kuingiliwa. Nakiri nilifanya kosa
kukupa ushauri mbaya, nimetubu kwa Mungu na ninatubu kwako. Naomba nikupe
nafasi ya kujijenga. Nimeshakubali mimi sio wako, na umeshakuwa na mahusiano na
mtu mwingine, naona nichukue hatua yakukaa pembeni. Kwa faida yako Naya.
Nakutakia kila la kheri. Maisha yenye furaha na amani. Mungu akufanikishe.” Kimya. Naya
akavuta pumzi kwa nguvu.
“Naya?” Malon akaita. “Nimekusikia Malon. Asante. Nakuombea Mungu
akufanikishe zaidi.” Naya akakata simu. Naya alibaki haamini. Kulikuwa kuachwa ambako hata
hakutegemea! Mara ya mwisho waliachana kwenye mapenzi na makubaliano mazuri tena
mazito yenye tumaini mpaka kuombewa! Naya hakutegemea hata kidogo! Aliwaza
usiku huo, akamkumbuka Malon huyu aliyekuwa amerudi kama mcha Mungu na
kurudisha tumaini la ajabu sana kwake. Alikuwa kama aliyeona mzimu akabaki akitetemeka,
ametoa macho na kushindwa hata kusogea pale alipokuwa amekaa kwa hamasa ili
kumsikiliza Malon. Lakini akaamini kama alivyosema baba yake Malon, Malon sio
wamahusiano. Naya akaumia sana moyoni.
Itaendelea.....
0 Comments:
Post a Comment