Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA! - SEHEMU YA 3. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA! - SEHEMU YA 3.

 Kesho yake Chezo aliamua kumfuata Malon nyumbani kwake. Bado Chezo hakuwa ameoa, baba yake ndio alikuwa mfanya biashara kama Malon. Malon alifanya biashara tokea anakataa shule, mwenzie Chezo akiendelea na shule. Wakati 

Chezo anamaliza chuo kikuu cha Mzumbe hapohapo Morogoro, tayari Malon akawa amefanikiwa sana kibiashara, lakini urafiki ukaendelea tu. Mmoja mlevi sana wa pombe, Chezo. Mwingine mlevi wa wanawake, Malon.

Chezo alimkuta Malon ametulia tofauti na alivyomzoea. “Kwema Malo!” “Aaah, nipo tu.” “Leo hujatoka kabisa?” “Nimeona leo nipumzike tu nyumbani. Vipi wewe?” “Ndio tumetoka kanisani, nikaona nije kukuangalia. Jana tuliachana ukiwa haupo sawa.” “Kawaida tu. Nafikiri uchovu.” Chezo akasimama na kwenda jikoni akajua bado hayupo tayari kuzungumzia ya Naya.

Akarudi anatafuna apple alilopata jikoni kwa Malon. “Vipi Naya?” Chezo akaona asiendelee kuzunguka. “Alisema hayupo tayari kwa mahusiano. Au ni kama yupo na mahusiano mengine yanayofahamika kwao.” “Kwa hiyo?” “Amekataa kabisa. Na kwa vile nilivyomsoma, sio mbambaishaji. Ila daah!” Malon akasita. “Vipi?” “Nimejuta kupata naye muda jana.” “Kwa nini tena?” “Nahisi kama nimejichanganya zaidi! Hata sielewi.” “Kwamba?” “Nampenda yule mtoto, Chezo. Hakika nimempenda na ninamtaka haswa. Sijui nafanyaje. Na sikukosea. Anaonekana kweli ametulia.” Chezo akatulia. “Namtaka yule mtoto Chezo. Nahisi kama nitachanganyikiwa!” Chezo hakuwahi kumuona Malon kwenye ile hali.

“Labda kwa kuwa yeye amekukatalia Malon, ndio maana unazidi kumfikiria. Jipe muda tu. Sidhani kama...” “Hapana Chezo. Kwake imekuwa tofauti. Mimi unanijua linapofika swala la wanawake. Nawajua kwa kuwaangalia. Kama ingekuwa ni kumvua chupi tu, nisingehangaika. Kwani ana kitu gani cha ajabu na wanawake wote niliokwisha kulala nao?” “Sasa ni nini kinachokuumiza kicha Malon!?” “Namtaka yeye, Naya. Mimi sijui kwa nini, ila namtaka Naya.” Chezo alikuwa akimtizama Malon, asiamini. Sio Malon aliyemfahamu. Wakatulia.

“Labda umpe muda.” “Mpaka lini Chezo?” “Tulia kwanza Malon. Si umezungumza naye jana tu?” “Lakini amekataa. Amenielekeza mpaka kwa kina Lulu na wenzake. Kwamba nikawatongoze wale hawatanikataa, yeye amekataa.” “Ndio nakwambia mpe muda. Tulia kidogo ili na yeye afikirie. Si umempa namba yako?” “Nakwambia amenikataa, mbona kama hujanielewa!? Hapakuwa na mazingira ya kumpa tena namba yangu.” “Basi mpe hata mwezi, tutarudi kwa kina Tuli tena ili kumfikia Naya. Na hivi jana tuliwanywesha na kuwaachia pesa, watatupokea tu.” Malon akatulia akaona si wazo baya. Atulie. 

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Majuma mawili yakapita, Malon akamuomba Chezo ampigie simu Tuli, aulizie hali tu na kujua kama watakuwa wanafanya kazi weekend hiyo. Chezo akashangaa sana hakutegemea kama bado Malon anamkumbuka Naya. “Haiwezekani Malon! Bado unaye tu yule mtoto!?” “Tafadhali piga simu.” Chezo akajua hali si njema, akapiga simu. Tuli alimwambia weekend hiyo aliitwa Naya tu kazini, kwa kuwa ni tafrija ndogo tu, bosi wao alitaka mtu mmoja, akamchukua Naya. Na Tuli hakuwa akijua ni wapi. Chezo akarudisha ujumbe.

“Muulize kama wanaweza kufanya kazi nje ya Dar. Waje huku Morogoro. Au nipe nizungumze naye.” Chezo akamkabidhi simu, Malon akapiga simu, Tuli akapokea. “Habari Tuli? Mimi Malon.” “Mambo Malo!” “Safi tu. Nilitaka kujua kama huwa mnafanya kazi nje ya Dar?” “Labda uzungumze na bosi.” “Kwani nyinyi hamuwezi mkajipanga mkaja wenyewe mkafanya kazi wenyewe bila kupitia bosi wenu? Maana nina tafrija ambayo nataka nyinyi muhudumie. Na nitawalipa mimi mwenyewe na nitawatumia usafiri.” Chezo akashangaa sana, lakini Tuli akafurahi sana kuona watalipwa pesa yote wao wenyewe bila kukatwa na bosi wake, na watapewa na usafiri! Akamkubalia Malon.

“Basi ngoja niwapange wenzangu.” “Lakini nilazima Naya awepo.” Tuli akanyamaza. “Tuli?” “Mimi nilikwambia juu ya Naya, Malon. Siwezi kuahidi kama atakuwepo. Sitaki uje unione mimi muongo. Kwa nini usimfuate hapa uzungumze naye mwenyewe?” “Wewe mwambie umepata kazi ya pesa nyingi. Nina uhakika atakubali.” “Mmmh! Sijui kaka yangu. Lakini Naya huwa ananionaga mimi namna fulani hivi.” “Namna gani?” “Kama haniamini na sio mtu anayeweza kunisikiliza kama dada Wahija. Ni kama ananiona mimi mcharuko. Sijui kama unanielewa? Huwezi ukamkuta anazungumza na mimi maswala mengine zaidi ya kazi.” “Sasa hiyo si ndio kazi? Zungumza naye, mimi nitakulipa kama akija.” Akajaribu kuongeza nguvu ya hongo ili tu Tuli akubali kumshawishi Naya.

“Nitajaribu kaka yangu, lakini naomba nisikuahidi. Ulitaka tuje lini? Maana weekend hii anakazi.” Tuli aliendelea akionekana kukosa ujasiri. “Ile inayofuata je?” “Sina uhakika. Maana kama ni kazi huwa tunaitwa wakati mwingine hata siku mbili kabla, na Naya huwa hawezi kuacha kwenda kwa yule mama. Lakini kama ni mwanamke naweza kukuletea msichana mzuri tu.” “Acha upuuzi. Nani amekwambia huku nilipo hakuna wasichana wazuri? Nimekwambia namtaka Naya. Kw..” Chezo akampokonya simu alipoona anaanza kugomba.

“Tuli! Tuli!” “Samahani nilikuwa..” “Hapana, hamna shida. Mimi ni Chezo. Nashukuru kwa kupokea simu. Kikubwa ni mje na Naya. Ukifanikisha hilo, itakuwa vizuri sana.” “Sawa. Nitajaribu. Lakini kama nilivyomwambia mwenzio, Naya anaweza asikubali akadhani nataka kuja kumuuza. Mimi namjua Naya, kaka yangu.” “Mimi naomba uniahidi utajaribu.” “Sawa.” “Basi nakurushia pesa ya muda wa maongezi kwa ajili yako tu.”  Tuli akacheka kidogo. “Asante kaka yangu. Basi usisahau na pesa ya soda tafadhali. Jua kali!” Tuli akachangamkia. “Nakututumia na ya soda basi. Ili upate nguvu ya kumpanga Naya.” Wakaagana.

“Vipi Malon!?” “Kuhusu nini?” Malon akauliza kwa jeuri akijua wazi ni nini Chezo anamuulizia. “Unamjia juu demu wa watu wakati yeye ndio anaweza kutusaidia? Au humtaki tena Naya?” “Kwani wewe hujasikia mazungumzo yetu tokea mwanzo?” Malon akauliza kwa jeuri na kuondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

     Siku zilikuwa haziendi kwa Malon. Alitamani masaa, siku zikimbie, Naya afike nyumbani kwake. Chezo alikaribisha watu nyumbani kwa Malon, akawaambia kuna nyama choma, pombe za kumwaga, na warembo wa Dar watakuwepo, wasikose.

Siki ilipofika, mapema tu Malon akamtuma dereva wake Dar kwenda kuwafuata kina Tula. Dereva alipofika, akampigia simu Tula atoke. Girls star wote walikuwa wamejitengeneza vizuri. Tula akaona mpigie simu Chezo kabla hawajapanda gari. “Vipi, dereva hajafika?” Chezo akauliza. “Nipo naye hapa, lakini nimeona kabla hatujaanza safari, nikwambie kabisa. Naya hatakuja.” “Kwa nini tena!?” “Kwanza alianza kugoma kuwa kazi za mikoani hawezi kuchukua. Nikambembeleza na kumtajia ile pesa mliyosema mtatulipa, kidogo akakubali. Jana alinipigia simu kuwa amepata dharula anakwenda kwao, hatarudi mpaka jumatatu asubuhi. Hivi tunavyozungumza hayupo hapa hosteli. Sasa kama safari ilikuwa ya Naya, basi naona itashindikana. Lakini kama mnataka huduma nyingine, sisi tupo.” Chezo akaishiwa nguvu. “Nimealika watu wengi, nitahitaji msaada wenu. Siwezi kuahirisha. Mpo wangapi?” “Wanne, au unataka zaidi?” “Naona nyinyi mtatosha. Anzeni tu safari.”

Chezo akakata simu, lakini akaamua asimwambie Malon. Akajua akijua tu, itakuwa fujo na anaweza hata kuahirisha shuguli nzima hapo nyumbani kwake, wakati yeye ashatangaza kwa marafiki wote kuwa siku hiyo ni mkesha nyumbani kwa Malon! Watu wasile wala kunywa, kwa Malon kutakuwa na kusaza. Akajua itakuwa aibu kwake. Akona anyamazie tu.

Mapema sana akapeleka nyama nyumbani kwa Malon na kumwambia kijana wake aiweke viungo mpaka jioni marafiki zao watakapofika hapo kama yeye hatakuwepo, basi awatolee ili waanze kuchoma. Uzuri hakuwa amemkuta Malon mwenyewe.

Kina Tula walifika hapo ilishakuwa jioni ya saa 11. Malon alikuwa chumbani kwake akihangaika kubadili t-shert kama mtoto wa kike. Alivaa hii na kuvua mpaka akaona anajidhalilisha yeye mwenyewe mbele ya kioo. Akajipulizia pafyumu kidogo, ili angalau anukie kama itatokea anamsogelea Naya. Akafungua vifungo vyote vya hiyo t-shert iliyokuwa imembana vizuri sana, akajitizama. Akaona hapana. Akafunga vyote. Akajikosoa. Akafunga tena vyote na kubakisha kimoja tu cha juu. Akajikubali ndipo akatoka.

Aliwakuta kina Tuli wakionyeshwa jikoni, vinywaji vilipo, sahani na glasi. Chezo alishawaambia wanaweza kuvaa chochote wanachotaka sio lazima sare. Hakika warembo walipendeza. Malon akaangaza macho, akatoka nje na kuingia ndani mara kadhaa, mwishoe akamwita Chezo. “Mbona Naya simuoni!?” “Nilikuja mchana kuleta nyama, sikukukuta.” “Naya amekuja au hajaja? Acha ngonjera Chezo!” “Alipatwa dharula jana. Ameshindwa kuja.” “Sasa kwa nini hujaniambia tokea jana?” “Yaani mimi Tuli ndio ameniambia mida hii dereva alipokwenda kuwafuata. Sikutaka kuahirisha kwa kuwa niliona tuna wageni tayari. Au unataka tuwaage watu waondoke?” “Hapana. Hamna haja yakufanya hivyo. Nyinyi endeleeni tu. Ila naomba niitie Tuli.” Kwa wasiwasi kidogo, Chezo akaenda kumwita Tuli.

 Wakarudi naye. “Nipe simu yako.” Malon akamkazia macho Tuli mpaka akaingiwa hofu. Akaenda alipokuwa wameacha mikoba yake akarudi pale alipokuwepo amesimama Malon na Chezo. “Hii hapa.” Malon akaipokea. Alikwenda moja kwa moja kwenye contacts, akachukua namba ya Naya, na kumrudishia simu yake. Hakutoa hata asante. Wakamuona anachukua funguo za gari nakutoka. Chezo akatingisha kichwa.

“Wewe endelea tu, lakini usimwambie Naya chochote. Namjua Malo, hawezi kukutaja.” “Sasa anakwenda wapi?” “Sijui. Wewe endelea tu na kazi, usiwe na wasiwasi.” “Kwani hapa ndio nyumbani kwako Chezo?” Tula akauliza kwa sauti ya kike. Chezo akafikiria kidogo, akataka kumdanganya, lakini akaona ampotezee. “Kwani vipi?” “Nauliza tu. Pazuri.” Chezo akaondoka.

Baada kama ya lisaa na madakika kadhaa, akampigia simu Malon. “Uko wapi Malon?” “Nakwenda Dar mara moja. Nitarudi, sitakawia.” Chezo akatulia kidogo, akijua wazi wapi anakwenda. “Umempigia simu lakini? Nashauri umpigie ili ujue kama yupo kwenye nafasi ya kukuona.” “Sawa.” Chezo akashangaa amekubali ushauri wake kirahisi sana.

Malon kwa Naya Tena. 

M

alon akampigia simu Naya. Iliita mara moja tu, akapokea. “Haloo!” “Naya!” Kimya. “Mimi Malon.” Kimya. Naomba usinikatie simu, Naya. Tafadhali.” “Siwezi kufanya hivyo. Nilikuwa usingizini nikahisi naota.” “Mzima?” “Mzima.” “Mbona unalala sasa hivi?” “Nilikuwa na kazi nyingi karibu siku nzima leo. Namsaidia mama maswala ya kuku. Alianguka jana, ametengua mguu. Aliangukia bandani. Akamwaga maji, kwa hiyo kukawa kumelowa. Nilikuja jana. Tukawa naye, leo nikaamka na hiyo kazi ya kubadilisha maranda ya kuku bandani. Nimekuwa busy, hata sijala, nikajitupa kitandani ndio na wewe umenipigia.” “Pole.” “Asante.” Naya akakaa.

“Vipi mama?” “Wamemwambia aning’inize tu mguu. Atakuwa sawa. Vipi na wewe?” “Safi tu. Nakuja Dar. Nipo njiani. Naomba kukuona.” Naya akatulia kidogo. “Naya!” “Leo?” “Nipo njiani.” “Nipo nyumbani Malo!” “Nafahamu. Natamani kukuona tu Naya.” Malon aliongea kinyonge.

“Labda ukimaliza shuguli zako ndipo unitafute. Nijaribu kuaga hapa kuwa naenda dukani.” “Nikwambie kitu Naya?” “Nakusikiliza.” “Ninakuja Dar kwa ajili yako.” Naya akashangaa sana. “Kwa ajili yangu mimi!?” “Ndiyo Naya. Nimekuwa nikikufikiria. Natamani tu kukuona.” Naya akatulia. “Tafadhali Naya.” “Sipo vizuri Malo. Nimekuwa na kazi siku nzima, sitizamiki.” “Mimi sijali Naya. Ilimradi tu nikuone.” Ikamgusa sana Naya. “Sisi tunaishi mbele ya Kibaha kutokea Morogoro, panaitwa Kiluvya kabla ya Kibamba.” Akaongea Naya kwa upole. “Basi nikifika hapo nitakupigia. Nakuahidi sitakuweka sana. Nashukuru kwa kukubali nikuone.” Naya akacheka kidogo. “Karibu.” Wakaagana, Naya akabaki akiitazama ile simu huku amekunja uso, haamini.

Alitoka hapo chumbani. Akaenda kumuangalia mama yake sebuleni, akakuta wapo nje na baba yake wanaongea. “Umekula?” “Nilikuwa nimelala.” Naya akajibu huku anakaa. “Pole. Naona umefanya kazi kubwa kweli. Lile banda lilihitaji kusafishwa haswa kama vile ulivyofanya.”  Ikawa kama baba yake anamsifia. “Ulikumbuka kunyunyuza dawa?” Mama yake akauliza. “Niliweka.” Naya akajibu. “Ungekula. Bale amepika chakula cha mchana na usiku.” “Nataka kuondoka nirudi hosteli. Nitarudi tena kesho. Nilisahau kubeba vitabu vyangu. Nina mtihani jumatatu. Lazima nijisomee. Jana usiku sijasoma, na leo siwezi kupitisha.” Naya akadanganya.

“Sawa.” Baba yake akakubali bila shida. “Utakuja kesho saa ngapi?” Mama yake akauliza. “Mkitoka kanisani.” “Wewe siku hizi ibada ndio basi?” Mama yake akamuuliza, Naya akanyamaza. “Naya?” Mama yake akaendelea kumuuliza. “Nitakwenda lakini sio kesho.” Akasimama. “Mmewasiliana na Ino?” “Hapana mama.” Naya akajibu kwa ukali kidogo. Mama yake akamwangalia. “Sijawasiliana naye na wala sina mpango wakumtafuta. Ananiongezea matatizo tu kwenye maisha yangu. Najua nyinyi mnampenda, lakini mimi simpendi. Hawezi kuja kuwa mume wangu. Ni mnyanyasaji sana Ino. Hana utu.” Naya akaingia ndani kwenda kuoga.

Alitoka bafuni na kukuta missed call ya Malo. Akampigia. “Nipo kituoni tayari.” “Nilikuwa naoga. Naomba nisubiri kidogo.” “Hamna shida. Nitasubiri tu.” “Pole.” “Usijali kabisa.” Wakaagana tena, akakata.

Naya hakuahangaika kabisa. Alikuwa bado na uchovu wa kusafisha banda la kuku. Akavaa gauni refu tu mpaka chini kabisa, halafu kata mikono. Jeusi rangi moja tu, lilimfanya avutie zaidi kwa ngozi ya mwili wake ambayo wengi walisema anapaka manjano ili kumfanya aonekane na rangi hiyo ya njano kidogo usoni. Lakini ikawa sasa ni mwili mzima, halafu haikuwa nyeupe sana. Ni kama rangi yake ya mwili ikaelekea kwenye weusi. Akawa na rangi ya maji ya kunde nzuri sana kama mama yake ambaye naye hakujaliwa chunusi. Basi japokuwa alikuwa ni wakufanya kazi nyingi, nzito, lakini alijaliwa ngozi safi, hakuna makovu.

Akavaa na sendozi za chini tu. Akachana nywele zake kawaida. Hakubana. Akaachia tu nywele yake ya kiswahili isiyokuwa hata na dawa. Kipilipili kilichoonekana hakisumbui kuchana. Ila hakuweka hata kibanio kama mara ya kwanza alipokutana na Malon alipoongeza kibanio cha mkia mzuri wa mawimbi na kulambisha hiyo nywele Jelly na kulala vizuri. Kwa hiyo hiyo nywele ya asili ikawa imejaa tu kichwani ila hakusahau hereni. Zikaongeza muonekano wa aina yake kwenye sura hiyo ya mchongoko, nyembamba tu na shingo ndefu kuonyesha hata yeye mwenyewe ni mrefu.

Akatoka na kuwaaga wazazi wake. “Kesho unarudi hapa saa ngapi?” “Hata asubuhi. Nitarudi na vitabu vyangu. Naweza kutokea hapa jumatatu na kwenda shule kama utakuwa unanihitaji.” Naya alimjibu mama yake huku akimwangalia kama kuna nyongeza. “Haya. Kuwa mwangalifu.” “Usiku mwema.” Akaaga na kutoka. 

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kweli alifika kituoni, akakuta gari ya Malon mbele kidogo ya kituo. Akaenda, akachungulia dirishani upande wa abiria, akakuta amejiegemeza kichwa kwenye kiti, anaangalia juu. Akagonga, Malon akamfungulia mlango. Akaingia. “Pole na safari.” “Asante. Pole na wewe na kazi.” Naya akacheka kidogo. “Nimeshapoa. Nililala. Najisikia vizuri.” Wakatulia kidogo, Malon akimtizama. Naya akacheka na kuinama. “Nimefurahi umenikubalia nikuone, Naya.” Naya akamtizama kama mwenye swali. “Uliniambia umekuja huku kwa ajili yangu!?” “Huniamini?” “Hapana. Sijaelewa. Maana Tuli aliniambia mmewaitia kazi. Mnatafrija leo.” Malo akanyamaza kidogo.

“Unatakiwa kurudi nyumbani baada ya muda gani?” “Nimeaga kuwa nitaenda kulala hosteli kisha nirudi kesho.” Malon akafurahi sana. “Kuna kitu unataka hosteli sasa hivi?” “Hapana, kwa nini?” “Nilitaka twende mahali tukae tu. Ni sawa?” “Halafu utanirudisha hosteli?” “Ndiyo.” Malon akajibu. “Sawa. Ulitaka twende wapi?” “Sijajua bado. Tufikirie wakati tunaondoka hapa.” Malon akatoa gari.

“Nimekwambia nimeshukuru kwa kukubali nikuone?” Naya akacheka tu, nakubaki kimya. “Vipi lakini?” “Nipo napambana na shule na kazi.” “Ulienda kufanya kazi kwa Ino?” Naya akakunja uso. “Ulijuaje kama Ino ana kazi?” “Nilikusikia ukizungumza na baba yako kwenye simu.” Naya akajaribu kukumbuka. Akacheka kidogo. “Hapana, sikwenda. Yule mama mwenye ile kampuni tunayomfanyia kazi za waitress naona tumetokea kuelewana. Huwa ananiita mara kwa mara. Wakati mwingine hata ijumaa, jumamosi, na jumapili. Nakuwa busy, lakini inanisaidia kutengeneza pesa. Hata leo alitaka niende kazini, lakini nilimwambia mama anaumwa.” “Kwa hiyo kama isingekuwa hiyo kazi, ungeenda kwa Ino?” “Umeanza Malo!” “Nataka kujua Naya.”

“Kwa nini!?” “Kwa sababu nakupenda, Naya.” Naya hakutegemea jibu la namna ile. Tena la moja kwa moja! Akanyamaza. “Kweli Naya. Nakupenda.” “Kwa nini mimi na wakati umeacha warembo kama kina Tuli huko kwenu Morogoro?” “Sio kwenu. Wapo nyumbani kwangu. Chezo, rafiki yangu amealika watu nyumbani kwangu, makusudi ili tuombe huduma yenu. Ili wewe uje.” Naya akatoa macho.

“Malon!” “Kweli Naya. Nimetuma dereva mchana kuja kuwachukua. Nashangaa wamefika wewe haupo. Nikaambiwa umetoa udhuru. Nikaona sina sababu ya kukaa kwenye shuguli ambayo lengo haikuwa kusherehekea tu, ni wewe! Nikachukua funguo na kuondoka kukufuata huku.” Naya akashangaa sana.

“Pole na samahani Malo. Sikuwa na taarifa. Mimi nilijua ni kazi tu.” Akatulia kidogo. “Lakini Malon, unakumbuka nilikwambiamimi sipo tayari kwa mahusiano?” “Nakumbuka.” Naya akabaki akimtizama. “Unamfahamu yule rafiki yake Tuli?” “Mweupe sana hivi, na anamatako makubwa?” Naya akaanza kucheka. Alicheka na kucheka sana. “Kumbe unawafahamu?” “Nawafahamu sana tu. Si anaitwa Lulu yule uliniambia nimfuate yeye?” “Jina lakujipa hilo. Lakini ndio yeye.” “Amefanyaje?” “Anakupenda sana yule msichana. Kwa nini usimkubalie?” “Kwani unafikiri kama ningekuwa na shida ya kulala na yeyeyote yule ingekuwa shida? Hata Morogoro wapo weupe wenye matako makubwa, kuliko Lulu.” Naya akajifunika uso huku akicheka sana.

 “Malo wewe ni muwazi kupita kiasi bwana!” Malo akacheka. “Nakwambia ukweli. Lakini Malo anamtaka Naya. Ukiniuliza kwa nini, hata mimi sijui.” Naya akabaki kimya akifikiria na tabasamu usoni. “Umeshajua pakwenda?” “Bado. Halafu niangalie hivi nilivyo Malo. Tutaenda wapi? Nina sendozi kama malapa! Gauni kata mikono! Nywele nimeosha tu nyumbani baada ya kazi. Sijakwenda saluni. Ona zilivyochachamaa!” “Mimi sina shida ya hivyo ulivyo. Popote naweza kwenda na wewe, Naya. Labda wewe mwenyewe.” “Kweli Malo?” “Kabisa. Mimi sioni kama unakasoro hapo.” Naya akacheka kidogo na kumkumbuka Ino, kaka wa viwango. Msafi na anapenda awe nadhifu wakati wote wanapotoka. Asingethubutu kutoka naye akiwa hivyo. Akaanza kuvutiwa na Malon. 

“Ila kama wewe mwenyewe haupo sawa hivyo ulivyo, tunaweza kununua chakula, tukakaa kwenye gari tu tukala kama siku ile.” Naya akamtizama Malon tena. “Wewe umependeza sana.” “Kwa kuwa nilijiandaa kuja kuonana na wewe.” Naya akaanza kucheka tena. “Kwa hiyo hapo umevunja kabati?” “Sio mchezo. Nimebadili zaidi ya mara tano, nikijua upo njiani unakuja.” Naya akamtizama, asimwamini.

“Nikuulize swali Malo?” “Uliza tu.” “Unamchumba?” “Hapana. Sijawahi hata kumpa mwanamke mimba. Kwa hiyo sina mchumba, wala msichana, wala mtoto. Wewe ndio mtu wa kwanza kukutaka mahusiano. Na usinielewe vinginevyo kuwa sijawahi kulala na wasichana. Ninalala nao sana tu, lakini sina mahusiano yakufuatana nyuma.” “Kwa nini?” Malo akafikiria kidogo.

“Unajua mimi sijasoma. Niliishia kidato cha nne tu, nikawa mtaani. Si unaona hii rangi yangu ilivyo.” Naya akamtizama kwa makini.  “Halafu uwe huna pesa, uwe mzurulaji tu. Hakuna msichana unayemtongoza akakukubali. Labda umwambie unamuomba ulale naye, kisha umlipe. Napo mpaka umsimamishe akubali, nayo ni shuguli ingine. Tuache hapo. Kwa hiyo nikakaa mtaani, nikijulikana kama mtoto mtukutu. Malo mlala hoi, hajasoma. Hakuna mwanamke alikuwa ananitaka.”

“Chezo nilikuwa naye. Yeye amezaliwa kwenye pesa. Wakati anaenda kidato cha tano na cha nne, akaniombea kazi kwa baba yake. Nikawa mtu wakutumwa tumwa tu. Kazi za nyumbani, ofisini, basi. Nikafanya hivyo kwa muda huku na mimi nikijifunza anachokifanya yule mzee mpaka akafanikiwa vile. Maana ni kweli baba yake Chezo amefanikiwa. Nikaiga, na mimi nikatoka kimaisha.”

“Lakini ukumbuke mimi ni Malo yule yule waliyekuwa wakimkimbia na kunikataa zamani. Sasa wakinitaka sasa hivi si ni kwa ajili ya pesa tu? Hainisumbui kuhonga. Lakini kama ulivyosema ndivyo ninavyofanya. Kwa kuwa najua wananitumia na mimi nakuwa mwangalifu. Siendi kichwa kichwa. Sijui umenielewa?” “Nimekusikia.” Malo akamtizama. Wakanyamaza.

Hakujua anapokwenda, lakini aliendesha mpaka sehemu. Ulikuwa mgahawa mzuri tu. “Sasa unataka tukakae pale pale tule, au tuje kula ndani ya gari?” “Kwanza ujue naogopa. Sitaki mtu anayenifahamu mimi na wazazi wangu, anikute nimekaa sehemu kama ile, watampigia simu baba na mama. Naomba nisubirie hapa hapa kwenye gari kama hutajali.” “Hamna shida kabisa. Ngoja nikatoe oda, nimwambie muhudumu atuletee, halafu twende sehemu tukae.” “Sawa.” Malon akashuka. Naya akashangaa harudi.

Baada kama ya nusu saa akarudi na chakula. “Watu walikuwa wengi. Nilijua nikiondoka, hawatanikumbuka tena.” “Asante.” Naya akapokea. “Lakini mbona huna rangi mbaya Malo!” Malon alicheka sana huku anaondoa gari. “Kwa kuwa nipo ndani ya hili gari. Nimetoka kuoga, nikajipaka mafuta, na sikushinda juani. Ungekutana na Malon wa wakati ule, ungeelewa ninachozungumzia.” Naya akanyamaza.

“Utakuja lini kunitembelea Morogoro?” “Sijui Malon.” “Naya kwa jibu la Sijui! Unalipenda!” Naya akacheka kidogo. “Sitaki kukupa ahadi za uongo.” “Wala sitakupa mwanya wakunidanganya. Siku utakayonitajia, nakuja kukufuata mimi mwenyewe.” Naya akacheka sana. “Kama leo?” “Ulinichanganya Naya. Sijawahi kusumbuliwa na mwanamke kwa muda mrefu sana. Mpaka nimeshasahau jinsi wanavyotongoza!” Naya akazidi kucheka.

“Sijakusumbua bwana. Mimi nimejitahidi kuwa mkweli kwako.” “Kwa nini hunipendi Naya?” “Sijakwambia sikupendi Malo. Ila nimekwambia sipo tayari kwa mahusiano.” “Kwa hiyo unanipenda ila haupo tayari kwa mahusiano?” “Sijui Malon.” “Usinipe jibu la sijui Naya. Tafadhali.” “Kwa kuwa kweli sijui Malon!” “Mtu kama unampenda, unampenda tu. Kama humpendi unajua. Nataka kujua vile unavyojisikia juu yangu.” “Labda unipe muda nifikirie.” “Hapo afadhali. Nilitaka kukusikia ukiniambia kama utanifikiria.” Naya akanyamaza.

 Walikwenda mpaka sehemu wanayouza icecream. Malon akachagua sehemu ya nje, ambapo kulikuwa na meza na viti kama ubao, pembezoni kabisa ambako kulikuwa na giza. Isingekuwa rahisi mtu yeyote kuwatambua endapo wangekaa hapo. Akamwambia Naya wakae hapo. Akashangaa haendi kukaa upande wa pili, bali pembeni yake tena meza ameipa mgongo. Naya akacheka. “Sasa utaweka wapi chakula? Si ugeukie meza.” “Hivi unajua hata kule kwangu ninazo meza? Tena nzuri tu. Sijaja kuangalia meza hapa Dar. Nimekuja kukuangalia wewe Naya.” Naya akacheka na kuinamia chakula chake. Malon na yeye akafungua mfuko wake. Yeye aliagiza samaki na chips. Naya akamletea chips kuku. Wakaanza kula kimya kimya.

“Malon!” Naya akajirudisha nyuma ili kumtizama Malon pembeni yake. “Nimekuwa nikikufikiria pia.” Malon alifurahi sana. Akacheka. “Umenifikiriaje?” “Sijui.” “Acha bwana Naya!” Naya akacheka. “Niambie ukweli.” “Nilikumbuka muda na mazungumzo tuliyokuwa nayo siku ile. Nikajuta kuondoka kwa haraka. Nilitamani tungeendelea kuzungumza tu.” “Basi leo usifanye haraka kuniaga. Tukae wote mpaka uchoke.” “Utarudi saa ngapi Morogoro!?” “Utakaponiruhusu.” Naya akacheka kwa aibu na kujirudisha mbele kwenye chakula chake. Wakaendelea kula mpaka wakamaliza.

“Asante kwa chakula na asante kwa kuja kuniona.” “Kweli?” “Kweli Malon. Huoni mpaka nimeondoka nyumbani? Sikuwa na mpango wakuondoka nyumbani leo. Hata kazi nilikwambia nimekataa. Ila uliponiambia umekuja huku kwa ajili yangu, nimefurahi sana, japo sikuwa nimeamini.” “Sasa hivi umeamini?” “Sijui.” “Naya!” Akacheka kidogo. “Nafikiri nimeamini kidogo, japo nina maswali na hofu Malo.” “Maswali ni kitu chakawaida. Ila hofu ya nini?” “Sijui.” “Naya! Acha kusema hujui katika kila kitu. Niambie wasiwasi wako ulipo. Labda naweza kukusaidia.” Naya akanyamaza.

“Niambie Naya.” Malo akaongea kwa kubembeleza. “Bado sijajua ni kwa nini mimi Malo! Wewe unayo pesa. Wasichana wazuri wengi wanakutaka. Amebakia Lulu ambaye unamjua, ni kwa kuwa wamekubaliana abakie yeye tu kwako.” “Usiniambie?” “Acha utani na kucheka Malo bwana!” “Sikujua. Ehe!” “Wote wale wasichana walikuwa wakisimuliana siku ile ya tafrija kule jikoni. Wakajikuta wote wanamsifia kijana mmoja, ambaye nilikuja kujua baadaye kuwa ni wewe. Wengi walivutiwa na umbile lako, halafu sijui ni nani aliwaambia pesa pia ipo. Kwa kifupi wanakupenda japo pia wanakuogopa.” “Hilo najua. Nimemuona Lulu ananiogopa japo alimuomba Chezo namba yangu.” “Ulimpa?” Naya akauliza na kumfanya Malo acheke sana.

“Sasa mama wivu wa nini wakati wewe hunitaki?” “Bwana Malon!” “Sikumpa.” “Kweli?” “Mbona huniamini Naya? Sikumpa. Hivi unakumbuka nilikwambia Lulu yupo nyumbani kwangu sasa hivi na mimi nipo hapa na wewe?” Naya akanyamaza na kuinama. “Nakupenda wewe Naya. Nakupenda.” “Kwa nini Malo?!” Naya akauliza kwa upendo. “Nakupenda jinsi ulivyo. Umetulia. Nakutaka wewe kwenye maisha yangu. Nahisi ukiwa na mimi, nitatulia.” “Kwani sasa hivi hujatulia?” Malo hakujibu hilo, akanyamaza. Naya naye akanyamaza.

Walikaa pale kwa muda Malo akaanza kumchora mkono ule uliokuwa karibu yake. Kuanzia begani mpaka kwenye kiwiko. “Unasikia baridi? Naona vipele vya baridi vimeanza!” “Kidogo.” “Nikukumbatie?” Naya akaona aibu, akacheka na kuinama. “Nitakuwa sawa tu.” Malon akacheka taratibu. “Hivi, nimekushukuru kwa kukubali nije kukuona?” Naya akacheka na kunyanyua uso kumtizama. “Zaidi ya mara mbili.” Malon akabaki akimtizama. “Na mimi nimefurahi umekuja kuniona.” “Ungenitafuta?” Naya akatingisha kichwa kukataa.

“Kwa nini?” “Sijui.” “Nimekuomba usiwe unanipa jibu la sijui, Naya! Nataka kujua unachofikiria.” “Nilikwambia kuwa walikubaliana wote wakuache, wamwachie Lulu tu. Sasa ningeanzia wapi kukutafuta wakati nilijua wewe ni wa Lulu? Na alikuwa anasema leo kama mtaonana, angekwambia. Na nikajua kwa jinsi alivyo Lulu, angekwambia, usingekataa.” “Kwani Lulu yukoje?” Naya akatulia kidogo.

“Eti Naya? Lulu yeye yukoje?” “Kwanza hilo jina amejipa na kupewa pia. Wengi wanamsifia kuwa ni mzuri sana. Ni mali hadimu. Ndio maana anajiita Lulu.” “Aaha! Kwani hana mwanaume?” “Si naona watu wanakuwa nao wawili au watatu?” “Kwa hiyo na mimi ilikuwa nikapangwe mstari!?” “Labda angeacha wengine kwa ajili yako.” Malo akanyamaza kama anafikiria.

“Kwa hiyo isingekuwa Lulu, ungenitafuta?” “Sijui Malo.” “Naya!” “Basi niseme ingetegemea.” “Na nini?” “Sijui. Labda na wewe mwenyewe. Niliamua kujipa muda. Pengine ningepata jibu mbele ya safari.” “Mimi nilipewa ushauri wa kujipa muda nifikirie ndipo nikutafute. Nikiwa najua yupo Ino, lakini nilishindwa kuendelea kusubiri.” Naya akacheka kidogo na kuinama.

Malo akageuka upande ule aliokuwa amegeukia Naya, akamvuta karibu yake, akampitishia mkono wa kulia juu ya mabega. Akamuona Naya mwenyewe anajisogeza karibu yake zaidi. Akajua amependa. Akajiegemeza pembeni ya kifua chake. “Naomba uje kunitembelea Morogoro.” Malon aliongea taratibu akiwa amemkumbatia. “Nakuahidi wakati mzuri. Hutajutia.” Naya akacheka taratibu. “Eti Naya?” “Labda nikimaliza mitihani hii.” Mkono ule wakushoto akaupitisha kwa mbele, akafikia mkono wa Naya uliokuwa pembeni, akaendelea kuupapasa. Naya alitoshea kwenye ile mikono bila shida. Wakatulia, Naya akifurahia joto la kifuani.

“Lini mnamaliza mitihani yenu?” “Tutaanza mwezi ujao karibu na mwisho, halafu ndio likizo ya mwezi wa sita inaanza, tukirudi tunajiandaa na mitihani ya mwisho ya kumaliza kidato cha nne.” “Daah! Mbali. Lakini nitakusubiri tu.” Naya akacheka taratibu na kunyamaza. “Lakini si unajua Morogoro sio mbali?” “Nafahamu.” “Basi ukibadili mawazo kabla ya kumaliza mitihani, naomba unipigie, nije kukufuata. Sawa?” Naya akamwangalia. “Nitakuja kukuchukua mapema, na kukurudisha siku hiyo hiyo kama utataka.”  “Tutawasiliana basi.” Naya akajibu kisha wakatulia, Malon akiendelea kumpapasa. “Naona leo nitalala vizuri.” “Kwa nini Malon?” “Nimefurahi sana.” Naya akacheka taratibu nakunyamaza.

“Ulikamilisha swala la ada?” “Tulimaliza, japo kwa shida hivyo hivyo. Mama ameuza kuku, tumepata pesa kiasi. Akanipa, nikachanganya na zile nilizoenda kuchukua kanisani, pamoja na nilizolipwa kwenye kazi ya jumamosi iliyopita. Nimemaliza ada na michango ya shule. Nimebakiwa na deni la kanisani. Nalo nimepunguza kidogo. Sikutaka kumpa sababu Ino.” “Kwani Ino anahusikaje!?”  Naya akaguna.

“Ino ndio msimamizi wa pesa na matumizi yote pale kanisani. Kwa hiyo kama hivi baba anavyokopa pale kanisani, usifikiri ni siri. Ino pia anakuwa ameidhinisha kuwa apewe. Ndio maana unamuona anajeuri yakumwambia baba nikafanye kazi anakotaka yeye. Inamaana ni kumwambia baba ana uwezo wakutokukopa kopa hovyo, kama mimi nitafanya kazi. Yaani kwa jinsi ninavyomjua Ino, anaona tunakopa kwa kuwa niwazembe, hatufikiriii vizuri. Au hatuna mipango inayoeleweka kwenye maisha ndio maana tunakopa hovyo. Unafikiri ni kwa nini nahangaika kufanya kazi?” “Eeeh!” “Namsaidia baba. Hajashindwa kunisomesha, lakini najua wazi anahangaika sana.”

“Kwani baba yeye anafanya wapi kazi?” “Mfanyabiashara tu. Si ndio maana mama hapendi mimi niolewe na mfanyabiashara! Anasema nitakuja kuishia kuwa kama yeye!” “Yeye ameishiaje?” “Si kama hivyo sasa hivi wanakopakopa! Lakini haikuwa hivyo tokea mwanzo. Hakuwa na pesa nyingi, lakini hatukuwahi kukopa sana kama hivi sasa. Mambo yamezidi kuwa magumi, uchumi ulipobadilika, na kuweka juhudi za kuhamia kwenye nyumba yetu. Sisi tulizaliwa kwenye nyumba ya kupanga tu. Sasa nafikiri wakaona umri unakwenda, wanapoteza pesa kwenye nyumba za watu, ndio wakaamua tuhamie kwetu.”

 “Mama akakopa kutokana na mshahara wake, na baba naye kwa biashara zake. Wamejenga hiyo nyumba na mabanda ya mifugo. Imewagarimu zaidi ya uwezo wao. Ndio na baba naye ikabidi kukopa na huko kanisani ili kumalizia na kuhamia, wakati tayari walishakuwa wamekamilisha mabanda ya mifugo. Ndio ikawa sasa kazi ya baba, ufugaji baada ya biashara zake kukwama. Ni kweli mikopo ya kanisani ilitusaidia. Wakamalizia na hiyo nyumba tunayoishi sasa hivi, tukahamia nikiwa ndio naingia kidato cha tatu Jangwani. Kiluvya mbali. Usafiri wa kila siku asubuhi, kwenda na kurudi, tukaona ni afadhali nihamie hosteli. Ndio nilipoingia kidato cha nne, nikapata pale hosteli ninapoishi sasa.”

“Sasa bado mama anadaiwa huko kwenye mabenki. Anakatwa mshahara. Baba ndio mfugaji. Ni kama wote tunategemea huo ufugaji. Kuna mwezi mambo yanakuwa mazuri, miezi mingine mifugo inaugua ndio hasara hata kupunguza deni kanisani ni shida. Sasa naona deni linalowatia presha ni hilo la kanisani. Maana tunadaiwa tena kwa kukumbushwa kumbushwa mara kwa mara. Sasa hapo ndipo mama anazidi kuchanganywa na Ino. Anatudai, na kutoa njia zake za kibinafsi za upatikanaji wa pesa. Acha tu. Naomba tusimuongelee tena Ino. Tumuache tu kama hivyo Mungu alivyomjalia.” Malon akanyamaza.

“Kwanza kwa nini umeniuliza?” “Nilitaka kujua tu. Naona unafanya sana kazi na  bado unajukumu la shule.” “Nitafanyaje Malo? Lazima vyote viende kwa pamoja. Ila najitahidi nisilemee upande mmoja. Nahakikisha hata kama napata kazi za pesa nyingi, basi nisinogewe. Nikifikisha lengo, narudisha akili darasani.” “Hongera Naya. Unajitahidi!” “Namshukuru Mungu kwa kweli. Naona ananifungulia milango. Siwezi kulalamika.”

“Kwenye kazi zako huko hujapata wafadhili?” Malon akachokoza. “Hawawezi kukosekanika. Lakini si unajua hakuna kitu cha bure, Malo? Utapewa misaada yenye masharti magumu, mwishowe unajikuta unakuwa na uwezo wakulipa ada, lakini uwezo wa kusoma tena hamna. Najiona ni heri hivi ninavyohangaika peke yangu, nakuwa huru na kuamua chochote. Najipangia mambo yangu nitakavyo. Najipanga na ninajua wapi nimelemea, wapi niongeze nguvu.” Malon akazidi kumpenda Naya. Akamvuta karibu yake zaidi. Wakatulia.

Malon akambusu kichwani upande aliojiegemeza. Lilikuwa busu moja lakini alilolivuta kwa muda, kama anayesikilizia, huku amemminya kwa nguvu. Mpaka Naya mwenyewe alilisikia rohoni. “Asante.” Naya alimgeukia, akashukuru taratibu na tabasamu. Akabaki anamtizama. Naya akacheka na kuinama.

“Naomba unirudishe hosteli, nikapumzike.” “Sawa. Unafikiri tutakuja kupata muda mwingine kama huu?” “Naamini hivyo Malo. Japo sijui kwa hakika itakuwa lini. Siku za shule najitahidi kuweka akili shuleni, ili weekend jioni nifanye kazi. Jumamosi asubuhi nakuwa najisomea na wenzangu.”  “Nikuulize swali? Uwe huru kujibu au kutojibu. Sio lazima, ila nilitaka tu kujua. Kwa kazi kama hizi anazokuita huyu mama, kwa masaa yote yale, anakuwa anawalipa kiasi gani?” “Wasichana wengi pale wanamlalamikia yule mama kuwa ni mnyonyaji. Lakini wengi wanapenda kufanya ile kazi kwa kuwa wanapata bahati yakuonana na watu kama nyinyi. Kwa hiyo kwa kukujibu tu kwa jumla, sio pesa nyingi hata kidogo. Ila mara nyingi tunafaidika kwenye tip. Kwa hiyo inategemea unawahudumia vipi wateja na ni watu gani.” Malo akamvuta pembeni kidogo, akamtizama.

“Kwa hiyo siku ile tulipokuwepo sisi, uliondoka na tip kiasi gani?” Naya alicheka sana. “Usicheke Naya! Wewe mwenyewe umetoka kuniambia hakuna msaada wa bure.” “Tip sio msaada Malon! Ni shukurani baada ya huduma nzuri.” “Haya ulipewa shukurani ya kiasi gani?” Naya akazidi kucheka. “Siku ile haikuwa nyingi kama nilivyofanya majuzi.” “Naya! Wewe mtoto unataka kuninyima tena usingizi.” Naya alizidi kucheka. “Ni kazi.” “Walikupa tip kiasi gani?” “Uliniambia sio lazima nijibu.” “Naona kama ulazima unaanza kuwepo!” “Usijali. Hakuna kinachofuatia baada ya hizo tip.” “Unaweza kuniahidi kuwa hapatakuja kutokea kitu baada ya hizo tip?” Naya akatulia kidogo.

Akamwangalia Malon, bado alikuwa akimtizama. “Naya!” “Hakuna kitu kitakuja kutokea Malon. Mimi ni mwaminifu. Na nitakuwa mwaminifu kwako.” Bila kujijua, Naya akajikuta anatoa kiapo kwa Malon. Akashangaa anapata busu la mdomoni. Akatabasamu. Malon aliposikia asante, akamvuta kiunoni akamshika shingoni, akaanza kunyonya midomo yake. Hakutumia muda mrefu sana. Akamuachia, Naya akainama.

“Naomba unisindikize mahali kwanza, ndio nikurudishe hosteli. Hatutakawia.” “Sawa.” Wakasimama, Malon akamshika mkono, wakaongozana mpaka kwenye gari.

Safari hii akamfungulia mlango. Akapanda, kisha akamfungia mlango. Naya hakuamini. Alibaki akilamba midomo yake. Alifurahia sana lile busu. Hapakuwa na maongezi, akamuona anasimama sehemu yenye ATM. Akashuka, kisha akarudi. “Hizi zitakusaidia kwenye mahitaji yako.” “Asante Malo. Nakushukuru.” “Karibu.” Wakatoka pale, wakarudi mpaka hosteli. Naya hakuwa akiamini. Pesa na busu la Malo!

Akasimamisha gari nje ya hiyo hosteli yao. Ujasiri wakumtizama machoni ukapungua, na maneno mengi ya Naya, yakapungua. “Asante kwa kila kitu. Na uwe na safari njema ukiwa unarudi.” “Asante. Naamini tutaonana tena hivi karibuni.” Naya akatingisha kichwa kukubali. Malo akacheka. Akamuona anashuka. Akajua anaenda kumfungulia mlango. Akatulia pale pale kwenye kiti.

Akamfungulia mlango. Naya akashuka. Wakawa wamesimama palepale mlangoni. Naya akacheka kidogo na kuinama. “Nitakupigia kujua kama ulifika salama. Ni sawa?” “Nitafurahi kukusikia tena.” Kama waliokuwa wakitaka kurudia busu, lakini wakasita. Naya akajisogeza na kumbusu shavuni. “Usiku mwema.” Malon akamvuta karibu yake, akapitisha mikono yote miwili chini ya masikio, karibu sana na shingo, akaanza kumbusu tena. Alimbusu tena na tena. Naya alitamani asimalize. Alimbusu vizuri, mpaka akajisikia upendo wa kweli. Akamuachia kidogo, akampa mabusu mawili ya juu juu. “Tutawasiliana.” Naya akatingisha kichwa na kuondoka palepale, akamuacha Malo akimsindikiza kwa macho.

Aliingia tu ndani, akamtumia ujumbe. Nimefurahia busu langu la kwanza maishani. Asante kwa kuja kuniona. Asante kwa pesa. Asante kwa chakula, asante kwa kila kitu.” Simu ya Malon ikatoa mlio wa ujumbe ikiwa mfukoni. Akataka kupuuza, lakini akajiambia inaweza kuwa ni Naya. Akaitoa mfukoni. Kweli ilikuwa ikitoka kwa Naya. Akasoma ule ujumbe huku akiendesha. Hakuamini. Akasoma tena na tena. “Inamaana huyu mtoto alikuwa hajawahi hata kupata busu!”  Malon akashangaa sana. Akaanza kulamba midomo yake, nakutamani arudi. Akaanza kujiuliza kama alilitende haki lile busu. Akajuta.

Ningejua kama ni mara yake ya kwanza, ningetendea haki lile busu. Sidhani kama lilikuwa...” Malon akazidi kuwaza akijilaumu kwa furaha. Akajikuta anacheka na kujipongeza kuchukua maamuzi ya kuja kumfuata. Gari liliposimama kwenye mataa, akaamua kujibu. ‘Asante kwa kunipa nafasi hiyo ya kwanza. Nitaienzi daima.’ Akamrudishia hayo majibu. Naya alipopata ule ujumbe, alishindwa kulala. Uzuri, hakumkuta mtu chumbani kwao. Alikuwa akicheka peke yake huku akirudia ule ujumbe tena na tena na kujishika midomo yake.

Akiwa amepitiwa na usingizi, akashtuliwa na mlio wa simu. Akaipokea kwa haraka. “Nimekuamsha tena?” “Nilikuwa nasinzia tu, lakini nilikuwa nikisubiria simu yako kujua kama ulifika salama. Umefikia wapi?” “Nimefika nyumbani salama. Nashukuru kwa kukubali tuonane Naya. Asante.” “Asante kushukuru Malon. Na mimi asante kwa kurudi kuja kuniona.” “Karibu.” Wakatulia kidogo.

“Eti nimeshakuwa na hamu na wewe!” Naya akacheka tu bila kujibu. “Umesema utakuja baada ya mwezi!?” “Ndio tutakuwa tumemaliza mitihani, na mimi akili zitakuwa zimetulia. Na hivi umenipa pesa, itanisaidia kutulia nijiandae vizuri. Asante.” “Kidogo hivyo!?” “Sio kidogo. Kwa kuwa nishapunguza deni kanisani, hizi nazifanya zakupunguza deni la hapa hosteli na za kwangu za matumizi.” “Hosteli huwa mnalipa kiasi gani?” Naya akamtajia. “Okay. Basi pumzika. Nitakupigia tena kesho.” “Usiku mwema Malon.” “Na wewe Naya.” Wakakata simu. 

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Chezo akashangaa  kusikia geti limefunguliwa lakini hamuoni Malon. Baada ya muda alipoona kimya akidhani ni Malon, kwa kuwa hakuwa ameingia ndani, akachungulia dirishani. Akaona gari ya Malon imegeeshwa. Akajua amerudi lakini akashangaa ni kwa nini haingii ndani wakati pale ndio kama kulikuwa kunapambazuka na aliacha wanachoma nyama! Na Malon kwa nyama, utafikiri hawezi kuishi bila nyama choma. Linapokuja swala la nyama hakuwa akijua kujivunga.

Ikabidi Chezo atoke. Akamkuta anamwagilia ukoka na maua huku akipiga miluzi. Chezo akaanza kucheka. “Kuna nyama ndani.” Chezo akamsogelea karibu. “Sitaki kuchafua kinywa changu.” Chezo alicheka sana huku akipiga makofi. “Gafla kaka! Nyama imekuwa uchafu!” “Inategemea na kile kilichoingia mara ya mwisho mdomoni.” Malon akajibu na kuendelea kupiga mluzi tabasamu kubwa usoni.

“Usiniambie umebana mpaka umepewa ulimi!” “Sio kidogo kaka. Nimejitahidi mpaka nikashika na kiuno. Nimekamua kaka, mpaka nikaona nitapitiliza, nikamuacha. Mtamu! Hujawahi onja hapa duniani. Akiwa mkononi, unaweza ukadhani umekumbatia mamilioni ya dola za kimarekani, au zaidi.” “Alumasi?” “Daah! Alumasi nimeshika Chezo, haifikii raha ya Naya, mkononi.” Chezo alicheka sana, nakuendelea kupiga makofi.

“Chezo!” Malo akaita. “Niambie kaka.” “Pale nimesalimu amri. Mungu kanikamata pabaya! Hata mimi sijui imekuaje!” “Umekamatika kaka?” “Kama kondoo! Hata akiniambia niiname, mimi nitambeba tu.” Chezo alizidi kucheka. “Juzi ulisemaje tena kuhusu kunyonya?” Chezo akamchokoza. “Sio kwa Naya. Yule nikifanikiwa kumuweka kitandani, hakika nitamnyonya mpaka kidole kidogo cha mguuni.” Chezo alicheka kwa sauti huku anapiga makofi mfululizo.

“Mimi nakumbuka uliapa na kusema kunyonya haramu kwako. Huthubutu.” “Nakwambia si Naya. Siku akija humu ndani, sitaki hata simu. Nawaambia walinzi, mtu asipite pale getini. Nibaki naye tu humu ndani. Peke yetu.” “Lini hiyo?” “Daah! Yule anatakiwa taratibu. Mtoto wa kanisani yule. Sio kama haya makurubembe yangu unavutia popote.” “Naya wa mrija?” Chezo akazidi kumchokoza. “Tena mrija mwembamba kaka! Yule! Nitabeba mpaka kifo.” “Utaweza Malo wewe, mzee wa sketi!” Chezo alimjua Malo kwa kupenda wanawake.

“Napenda kufunua  tu sketi kama burudani kaka. Fahari ya macho. Najipitia tu kama wengine. Lakini Naya!” “Eeeh!” “Naya natunza mwenyewe. Nakula mimi mwenyewe. Namiliki mimi mwenyewe. Mwanaume atakayepita kwa Naya, kifo ndio adhabu yake.” “Sio kumtahiri?” “Namtahiri kwanza bila ganzi, halafu ndio namtoa hapa duniani kwa kifo.” Chezo alizidi kucheka.  

“Sasa naomba sherehe iishe Chezo. Nataka kulala. Ondokeni na wanawake zenu wote.” “Hutaki tukuachie hata mmoja.” “Sitaki shombo leo. Acha nifurahie busu la Naya.” “Lulu anakuulizia.” “Tena huyo mtoe kabisa. Asiniharibie kwa Naya huko hostelini kwao bure. Wanaongea sana huko hosteli. Sitaki hata kumsogelea asije kwenda kutangaza, Naya akaniacha. Mwambie Side awarudishe sasa hivi.” “Naona wawili wamepata watu hapa hapa.” “Basi wewe mpe Tula pesa yao. Mwambie usafiri upo kwa anayetaka kurudi Dar. Lakini hapa kwangu asibaki hata mtu mmoja.” “Sawa.” “Na umwambie Fido, achangamshe mkono. Nataka nije kulala.” “Tutamsaidia kusafisha kidogo, kabla hatujaondoka.” “Sawa.” Chezo akaondoka akamuacha  Malon akiendelea kupiga miluzi huku akimwagilia maua yake, kazi aliyokuwa anawapa walinzi wake, usiku huo akajikuta anafanya mwenyewe.

 ~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~ 

Tula na Lulu, waliokuwa wakiwamendea Chezo na Malon, waliambulia patupu walirudishwa na dereva mpaka hostelini kwao. Kwa kuwa walikuwa wamelewa, walilala tu. Hawa na msichana mwingine, anayeitwa Naiki, ambaye walimchukua, kufidia pengo la Naya alipokataa kwenda huko Morogoro kwa kazi waliyoitiwa na Chezo, wao walipata wanaume pale pale, wakaenda kulala nao. Kesho yake asubuhi wakarudi Dar kwa basi. 

Moja kwa moja chumbani kwa kina Tula. Zikaanza stori. “Nasikia Malon jana alipotuacha pale, alirudi huku Dar, kumfuata Naya!” Wakaanza stori za yaliyojiri mji kasoro bahari, Morogoro. Maana jana yake kila mmoja alikuwa busy na kazi huku wakiwinda wanaume. “Kwani hukumwambia kuwa Naya hamtaki?” “Chezo kanipa stori za Malon. Kaniambia ana roho ngumu kama chuma. Akitaka jambo lake, ndio hilo hilo. Akaniambia hajawahi kupenda kama alivyompenda Naya. Maana tulivyofika tu, Chezo si aliniita kule upande wa jikoni, unaambiwa Malon akatoka kule juu chumbani kwake, akaanza kumtafuta Naya. Alipomkosa si ndio akamuuliza Chezo! Chezo kumpa taarifa za Naya, bwana yule kaka alibadilika, kama sio yeye! Akaniita kwa ukali anataka simu yangu. Bila kuomba, katafuta namba ya Naya, akaondoka kurudi huku kumtafuta Naya.” “Sasa alimpata huyo Naya?” Hawa akauliza.

“Atakuwa alimpata. Maana mimi nilifuatwa na Chezo, akaniambia niachane na Malon kabisa. Sasa hivi yupo kwenye mahusiano na Naya.” Lulu akajibu. “Heee!” Wote wakashangaa. “Haiwezekani. Naya!” “Ndiyo. Tena Chezo mimi kanionya kabisa, akaniambia Malon bangi ile bangi mbaya. Nisitake kuingia kwenye anga zake. Unaambiwa haogopi mtu. Akaniambia niachane na Naya, na wala asisikie namtaja Malon. Akasema ikitokea Naya anamkataa Malon kwa ajili ya maneno yangu, eti atanipasua kichwa.” “Anakutisha bwana.” Hawa akadakia.

“Mmmh! Hata hivyo mimi basi bwana. Mwenyewe ameshaonyesha msimamo wa waziwazi. Hivi unajua alirudi mida ile ya usiku sisi tukiwepo pale pale, lakini hakutaka kabisa kuingia ndani tulipokuwepo sisi na marafiki zake!” “Kwanza nasikia hanywi.” Tula akaongeza. “Kwani pale ni kwa Malon au Chezo?” Hawa akadadisi. “Mimi nilimuuliza Chezo, hakujibu.” “Mimi yule rafiki yao niliyeenda naye kwake ameniambia pale ni kwa Malon.” Naiki akadakia. “Kweli?” Lulu hakusadiki. “Mimi nahisi ni kweli, pale ni kwake Malon. Unafikiri kwa nini rafiki yao anidanganye?” “Basi itakuwa kweli.” Wakakubaliana na Naiki.

“Ila alivyosema kama alivyokwambia Chezo. Maloni bangi kweli kweli. Mkorofi wakupitiliza. Ila Chezo ndio mtu wake. Wamekua pamoja tangia watoto. Alipo Chezo, ndipo alipo Malon. Ndio maana japokuwa Malon hanywi, lakini Chezo anaweza kuita walevi wenzake pale nyumbani kwa Malon, watakunywa kama vile, na Malon hana neno.” Naiki akaongezea alichosikia juu ya vijana hao. Wakatulia kwa muda.

“Basi Naya kaupatia!” “Si kidogo. Nyumba nzuri!” “Unakumbuka Side alivyotuambia wakati anaturudisha?” Lulu akauliza. “Kuwa hata hii gari iliyotufuata na lile lililoturudisha yote ni ya Malon?” Tula akauliza kama aliyekumbuka. “Eeh. Wakati tunaondoka Moro, unakumbuka ulimpa wazo lakubeba abiria hata wawili apate pesa ya mafuta, akakwambia Malon akijua anaweza kumkata mikono. Ukauliza kwa nini Malon na si Chezo, akakujibu kwa kifupi tu, mali za Malon.” “Ndiyo nimekumbuka. Lakini pale nilikuwa nishalewa. Alisema kweli. Kwa hiyo magari yote yake?” “Lile lililokuja kutuchukua sisi huku, na lile aliloturudisha nalo sababu tuko wawili tu, na alilotoka nalo mwenyewe Malon, yote nasikia ni yake. Bado mapya!” “Daah! Ningempata mimi yule!” “Mbona tungekoma!” Tula akamalizia kwa Lulu, wakaanza kucheka.

Malon kwa Bosi wake Naya.

K

itu cha kwanza alichokifanya Malon siku ya jumapili alipoamka, nikutafuta namba ya simu ya bosi wake Naya, Madamu Vane, ambae anamwita kazini  mara kwa mara. Akazungumza naye nakumwambia hataki awe anamwita Naya kazini. “Kwanza unajua kama wale ni watoto wa shule za sekondari?” “Mimi sijui.” “Basi ndio nakujulisha. Acha kuwapa kazi watoto ili uwanyonye. Ajiri watu wazima. Inakuwa ni kama unawauza kwa wanaume!” “Wakija wanadanganya umri ili niwape kazi.” “Sio kweli. Kama ungekuwa hunufaiki na umri wao, si ungekuwa ukiomba kuangalia vyeti vyao vya kuzaliwa kabla hujawapa ajira.” Kimya.

“Sasa ili tusifikishane mbali, usimtafute tena Naya.” “Naya mwenyewe anataka kazi. Anasema anashida na kazi. Tena nisipomwita, ananipigia.” “Sina muda wakubishana na wewe. Ila ukumbuke nimekuonya.” “Sasa akinipigia simu huyo Naya, nimwambie nini?” “Na mimi unataka niwaambie nini polisi, wizara ya elimu, na haki za watoto?” Kimya. Malon akakata simu.

 Malon azidi kumwaga pesa kwa Naya.

Naya alimka na kushangazwa na pesa aliyokuwa ameingia kwenye simu yake zaidi ya mara 4. Akakaa kwa haraka huku macho yakiwa yamemtoka. Akapangusa macho mara kadhaa, akarudia kusoma salio. “Oooh My!” Naya akazidi kushangaa. Hapo hapo akampigia simu. “Malo!” “Vipi?” “Umenitumia pesa kimakosa!?” “Kwa nini?” “Nimeona umetuma tena pesa, zaidi ya mara 4 wakati jana ulinipa nyingine!” “Naomba ukalipie deni la kanisani na hapo hosteli. Kama kuna kitu unadaiwa shuleni, nijulishe. Sawa?” “Nakushukuru sana. Sijui kama unaelewa Malon?” “Naelewa Naya. Na mimi nilifanya kazi kama hivyo unavyokuwa ukifanya wewe. Kwa hiyo naelewa sana tu.”

“Basi najua unaelewa shukurani zangu. Umenisaidia zaidi ya hivi nitakavyo kwambia. Deni la kanisani lilikuwa likininyima raha sana. Nilichukia kuona baba yangu anafundishwa maisha na mtoto kama Ino! Eti sababu ya kutaka mkopo! Hakika Mungu akukumbuke Malon. Asante sana.” “Karibu.” “Naomba nikuage sasa hivi, ili nijiandae kwenda kanisani, kwa ibada, lakini pia nikalipe deni.” “Utanipigia ukitoka?” “Lazima Malon. Nitakutafuta tufurahie wote. Asante sana. Sana, Sanaaaa....” Malon akacheka. “Utachelewa sasa.” Naya akacheka. “Natamani ungeniona nilivyofurahi!” “Nakusikia.” Wakacheka. Na kuagana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Naya alikwenda kutoa pesa yote aliyokuwa ametumiwa siku hiyo. Akaigawa na kuweka kwenye mahasha mbili kubwa, kisha akakimbilia kanisani kabla ya ibada kuanza, hakuwakuta wazazi wake. Na wakati mara zote wazazi wake wanawahi. Akawapigia simu. Baba yake akamwambia mama yake ameamka mguu ukimuuma sana. Aliutonesha asubuhi hiyo, aliamka unanafuu, akadhani umepona. Akaanza kuutumia, umerudi kuvimba. “Basi nakuja sasa hivi kuwasaidia hapo nyumbani. Nilikuwa hapa kanisani.” “Sasa si usubiri ibada iishe!” Naya hakuwa hata na nia ya ibada ila kulipa deni.

Akaingia ofisini kwa mchungaji kwa ujasiri wote. Akamkuta na Ino, pamoja na mama yake. Alitamani kuruka kwa furaha. Kwa ujasiri wote, akamsogelea mchungaji pale kwenye meza. “Siku ile ulinitajia kiasi mnachomdai baba. Nimekuja kumalizia deni.” “Lote!?” “Ndiyo. Naona tumalize tu.” Naya akamkabidhi zile bahasha mbili zikiwa hazijafungwa kabisa. Mchungaji akazitoa zile pesa nakuanza kuhesabu. Wengine wote kimya.

“Nashukuru sana kwa msaada wenu.” Naya akataka kutoka. “Naya!” Ino akaita. Naya akageuka. “Tunaweza kuzungumza?” “Naomba iwe wakati mwingine Ino. Sio sasa.” “Ujue nataka kuoa.” “Kila la kheri. Mungu akufanikishe.” Mama yake na Mchungaji wakashangaa ujasiri wa Naya. “Hatuwezi kuagana juu juu Naya. Lazima tuzungumze.” “Ulazima huo unatoka wapi Ino? Au ni katika kuendeleza tabia zako zakibabe? Wewe umeshasema unataka kuoa, sasa kuna kitu gani chakulazimishia mazungumzo kati yetu?” Kabla hajajibu, Naya akatoka. Walishamkera, hakuwa na hamu nao.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

     Akampigia simu Malon. “Mbona mapema. Hukwenda kanisani tena?” “Nimeenda lakini sikukaa. Nimelipa tu deni, nakuondoka. Naenda nyumbani kuwasadia kazi. Mama ametonesha mguu, wameshindwa hata kuja kanisani! Najua watataka msaada.” “Poleni sana.” “Asante. Najua nitakuwa busy. Na kesho shule. Nitakupigia jioni, na kama weekend ijayo sitaitwa kazini, naweza..” Naya akasita.  

“Nakusikiliza Naya.” “Tutaongea vizuri wakati mwingine.” “Acha kunifanyia hivyo Naya! Malizia basi.” “Sitaki kutoa ahadi ambazo nitashindwa kutimiza baadaye.” “Nakuahidi nitakusaidia kutimiza. Niambie tu.” “Nilifikiria kuja kukuona Morogoro.” “Naomba usibadili mawazo tafadhali. Nitakuja kukuchukua mimi mwenyewe. Angalau ufike tu nyumbani kwa mara ya kwanza. Halafu wakati mwingine mimi ndio nitakuwa nakuja kukuona Dar, mpaka unapokuwa likizo.” “Sawa. Kwa hiyo tupange jumapili?” “Kwa nini sio ijumaa au jumamosi?” Malo akauliza.

“Ijumaa nakuwa natoka shule mchana. Sitaweza kuja na kurudi.” “Sio lazima ukarudi siku hiyo hiyo. Naweza kukurudisha hata kesho yake.” “Malon!” “Nakuahidi nitakuwa na nidhamu.” Naya akabaki kimya. Akaingiwa na hofu. “Sitafanya chochote bila ruhusa yako, Naya. Ikilazimu mimi nitakuachia kitanda.” “Halafu wewe utalala wapi sasa!?” “Nina makochi pia. Hivi sikukwambia?” Naya akacheka kidogo. “Malon!” “Kweli. Nina kitanda na makochi.” “Haya bwana.” “Kwa hiyo nijiandae na ugeni wa ijumaa?” “Ndiyo.” Naya akajibu na cheko la aibu kidogo. Akamsikia Malon akisema, “Yesss!” Naya akacheka.

“Umefurahi nini sasa?” “Kutembelewa na Naya!” “Lakini kama nikiwa na kazi jumamosi, itabidi..” “Uahirishe.” “Malon!” “Kweli Naya. Nina hamu na wewe.” “Hata mimi nimeanza kukumiss.” Malon akafurahi kusikia hivyo. “Basi nakuahidi wakati mzuri. Hutajutia.” Naya akacheka. “Bye.” “Bye.” Wakakata.

 ~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Juma hilo likawa zito kweli kwa Naya na Malon. Masaa hayaendi. Lakini kila mtu alijua mambo ya Naya yamebadilika. Alijawa furaha kila wakati. Ametulia sio mtu wa wasiwasi kila wakati. Hakuulizia maswala ya kazi kabisa. Akatamani yule mama anayempa kazi, asimtafute ili asimkatalie na kuharibu kazi. Akashangaa mpaka alhamisi hakuna simu yeyote yakuitwa kazini.

 Naya alitoka shule siku ya alhamisi. Akapitiliza sokoni Kariakoo. Akakodi uber iliyomsaidia kupeleka vitu nyumbani kwao. Alinunua vyakula vingi sana. Akiwa njiani ndio akili ikaanza kumjia. Atamwambia nini baba yake? Alimwambia amelipa deni yote, halafu week hiyo hiyo anakuja na vyakula vyote vile! Akajuta kufanya vile bila kufikiria, lakini akajikaza.

Alifika kwao akamuomba mdogo wake na baba yake wamsaidie kushusha mizigo. Walipomaliza baba yake akaanza. “Unapata wapi pesa Naya!?” “Kule ninapofanya kazi, wanakopesha. Nikaona kuliko kudaiwa kanisani wanakokujua wewe, ni heri nikope wasipokujua. Nimemuomba bosi wangu awe ananikata asilimia 75 ya mshahara wangu mpaka nimalize deni. Nilitaka kutuliza mawazo shuleni. Sio nasoma huku nawaza maswala ya madeni!” “Mungu atatusaidia. Na hapo tutatoka tu.” “Naamini hivyo baba.” Naya hakuamini kama uongo wake umepokelewa kirahisi hivyo.

Kwa kuwa alikuwa na nguo za shule bado, angalau akaaminika kuna shule inayoendelea. Sio kazi tu. Mdogo wake akaambiwa amtayarishie chakula haraka. Na yeye alikuwa ametoka shule. Wakala na mdogo wake. Akasaidia kufua nguo za mama yake na baba yake, akaondoka akiwa amezianika, jioni hiyo, akarudi hosteli.

Pale hosteli kila mtu alishajua mahusiano mapya ya Naya na Malon. Na pale chumbani walishazoea kumsikia Naya akizungumza na simu taratibu kitandani kwake kwa muda mrefu tu. Aliporudi, alikuwa amechoka. Akapanda kitandani kwake, akampigia Malon.

 ~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

     “Vipi, mbona sauti ya unyonge tena?” “Nimechoka tu. Nimetoka shule, nikaenda kununua vitu vya nyumbani. Nikafika nyumbani ikabidi kusaidia kazi kidogo, nimeoga kabisa, ndio nimerudi. Nataka nilale kidogo, niamke nisome.” “Pole. Umekula lakini?” “Nimekula nyumbani. Nilikuta ugali, tembele na dagaa. Usiombe kuonja.” Malon akaanza kucheka. “Unajua mpishi alikuwa nani?” “Nani?” Malon akauliza. “Mama.” “Si mgonjwa!” “Sasa angefanyaje na sisi wote tulikuwa shule! Lakini Malon, mama anamkono mtamu! Akipika, utaomba kulamba na sufuria.” Malon akazidi kucheka.

“Inabidi ujifunze, ili na mimi nije nifaidi.” Naya akacheka. “Mbona unacheka?” “Pale nyumbani hawapendi chakula changu. Heri wanipe kazi nyingine, mdogo wangu anayenifuata, tena wakiume, ndio apike, lakini sio mimi.” Malon akazidi kucheka. “Kwa hiyo hujui kupika, mke wa Malon.” Naya alicheka sana. “Umefurahi nini?” “Unataka kuja kunioa?” “Kabisa. Nikumiliki kihalali.” “Basi ujue mkeo mapishi sifuri.” “Tutakula vibichi hivyo hivyo.” Naya akazidi kucheka.

“Kesho umeniandalia nini?” “Wewe mgeni uje ukiwa umejiandaa kufurahishwa tu.” “Utanifanya nione masaa hayaendi.” “Mbona hicho ndio kiliochangu tokea uliponiambia utakuja! Masaa yamenigomea kwenda kabisa” Wakaendelea kuzungumza mpaka Naya alipolemewa na usingizi. Wakagana.

 

Ijumaa.

N

aya alitoka darasani mida hiyo ya mchana, akarudi hosteli kuoga. Wakati anavaa, Tula akaja kumwita kuwa Malon yupo sebuleni anamsubiri. “Asante.” Tula akatoka. Akamaliza kuvaa. Hakujitengeneza sana. Akatoka. Malon alisimama alipomuona Naya. Akamdaka, nakuanza mabusu palepale. Naya hakukataa. Akajituliza. Akamkumbatia vizuri na kumvuta karibu na kuendelea kumbusu. Walianza kuitana na kujiiba kuchungulia. Akaacha kumbusu.

“Nilikuwa na hamu ya kukuona Naya!” Akamnong’oneza akiwa bado amemkumbatia. “Nimefurahi kukuona Malon. Asante kwa kuja.” Malon akarudia kunyonya midomo ya mwanadada huyo taratibu tu. “Twende.” Naya akacheka. Akapitisha mkono kiunoni, wakatoka. Ghafla ule ukimya wa mle ndani ukabadilika wakati wanatoka mlangoni. Wakasikia watu wakishangilia na kuitana. Naya hakugeuka nyuma, akafunguliwa mlango, wakaondoka.

 “Njaa inakuuma sana au unaweza kuvumilia mpaka tufike nyumbani?” “Nitavumilia tu.” “Basi anza na soda.” “Naona mgeni nimeandaliwa kweli!” “Nilivyo furahi! Acha tu.” Naya akazidi kujisikia vizuri. Waliposimama kwenye taa za Ubungo, Naya akamtolea risiti tatu. “Nini tena?” “Nakuonyesha furaha yangu. Risiti ya malipo ya ada, hosteli na kanisani alipewa baba, jana baba alinipa. Hivi unavyoniona, sidaiwi.” Malon akacheka. “Hongera sana.” Waliendelea kuongea na kucheka mpaka walipofika Moro, nyumbani kwa Malon. Giza lilishaanza kuingia.

 

Nyumbani kwa Malon!

“Unataka kuoga kwanza au unakula kwanza?” “Kwanza nikupongeze kwa nyumba nzuri. Nilisikia sifa zake, kule hosteli.” “Daah! Wale watoto wanaongea eeh?” Naya akacheka. “Lakini wameongea kweli. Hongera.” “Asante, na karibu. Jisikie upo nyumbani.” “Asante.” “Kwa hiyo nini kinaanza?”  “Naomba kula kwanza.” “Twende.”

Akapelekwa jikoni. “Vyakula vyote hivi peke yetu tu au kuna wengine wanakuja!?” “Mimi na wewe tu. Chakututosha muda wote utakao kuwepo na mimi hapa. Hakuna kutoka.” Naya akamwangalia Malon, akacheka kidogo. “Nataka nikae na wewe tu. Hata kama ni masaa matatu tu, lakini yasiyo na mwingiliano wowote ule hata njaa. Si sawa?” Naya akatingisha kichwa kukubali huku akicheka. “Basi tule. Wewe pita hapo, chagua chochote unachopenda, pakua. Na mimi nitapakua. Lakini nataka uanze wewe.” “Asante.” Walikaa hapo wakila na kuzungumza mambo ya kawaida tu mpaka wakamaliza.

“Nimefurahia chakula. Asante.” “Kama umependa, nimefurahi.” Malo akabaki akimtizama. Naya akainama. Akamsogelea pale. Akasimama nyuma yake akaanza kumbusu mgongoni, akaja begani kuja mpaka sikioni, shingoni. Kisha akamuacha. “Nisubiri nisuuze hivi vyombo tulivyotumia, tukamalizie matunda na juisi sebuleni.” “Acha nikusaidie.” “Mgeni siku ya kwanza. Leo wewe mgeni wangu.” Naya akacheka. Akambusu kichwani, akaenda lilipo sinki. Akaosha hivyo vyombo viwili na vijiko. Akamaliza.

 

Kisicho Ridhiki, hakiliki.

Naya naye akawa amemaliza juisi yake. “Tuhamie sebuleni au chumbani, tukakae huko. Hapa nimeshakinahiwa na harufu ya chakula.” “Sawa.” Naya alikuwa akiangalia simu yake. “Unategemea simu kutoka kwa yeyote?” “Nimeshangaa yule mama hajanitafuta weekend hii wakati amewaita kina Tula! Sijui niliharibu mara ya mwisho! Nimekosa raha.” “Ulitaka kwenda?” “Hapana Malon. Lakini angalau nikatae. Kutoniita mimi wakati tulifika kwenye ngazi ya juu ya mahusiano, mpaka watu walianza kujiuliza ni kwa nini mimi wakati mgeni, gafla kunibadilikia, sio kitu kizuri kwa malengo niliyokuwa nayo kwenye ile kazi.” “Labda hakuwa na nafasi za watu wengi.” “Hapana Malo. Hata akiwa na nafasi ya mtu mmoja siku hizi, nakuwa mimi kwanza. Ndio maana hata siku ile alinipangia meza za mbele kwa wageni wake anaowaheshimu. Nimekosa raha sana na nimeingiwa na wasiwasi!” Malon akamuhurumia.

“Nikwambie kitu lakini usikasirike?” “Nini?” “Naweza kuwa nimechangia kutokuitwa kwako.” Naya akakunja uso kama asiyeelewa. “Nilimwambia asikutafute tena.” Naya alishtuka na kutoa macho. “Kwa nini!?” Ule mshtuko wa Naya, ukamtia wasiwasi Malon mwenyewe. Akababaika.  

“Ilikuaje Malo? Ni nini kilikupelekea ufanye hivyo!?” “Kwanza nikuombe msamaha Naya. Nahisi ni kama kutaka kukulinda.” “Na nini!?” “Yale mazingira.” “Yapi Malon!?” “Yale ya vishawishi.” Naya akafunga macho. “Naya! Naomba usipaniki.” “Hujui ulinichonifanyia Malon. Ile ilikuwa zaidi ya kazi kwangu. Nilikuwa najifunza vitu vingi sana kwa yule mama. Ili siku moja na mimi nifanye kitu kama kile! Hiyo ni moja. Mbili, ni maisha yangu Malon. Mimi ni mdogo kwa umri, lakini nina malengo Malon! Wewe kuwa mwanaume wangu wa kwanza kukukiss haijawa bahati mbaya. Walishanifuata wenzako wengi kama wewe, wenye ahadi na maisha mazuri tu. Nimekuchagua wewe Malon. Sijui kwa nini! Lakini nilikuahidi nitakuwa mwaminifu kwako! Vishawishi havitaanza baada ya kuwa na wewe. Ninavyo vingi tu. Nategemea ile kazi inisaidie kuishi kwa sasa.”  

“Nitakusaidia Naya.” “Hunijui na wala sikujui Malon. Ndio tumeanza mahusinao. Hujui shida zangu. Hatujui tutadumu kwa muda gani. Hujui kesho yako ikoje. Tumeanza hata hatujamaliza juma, tayari unakuwa kama Ino ambaye nimekusimulia shida zake!” Naya alikuwa anasikia kama kuchanganyikiwa.

“Samahani Naya.” “Nahisi nimefanya haraka Malon. Sipo tayari kuwa kwenye mahusiano yeyote ya kimapenzi kwa sasa.” “Naya! Unaniacha kwa kosa moja!?” “Hapana. Sio kwa kosa hili. Kwa vile ulivyo Malon. Unataka kunifanyia kama Ino! Kutawala kila kitu, wakati hamjui nilipo na ninapopitia. Hujui malengo yangu Malon. Hunifahamu na umeweza kuchukua hatua kubwa kama hiyo kwenye maisha yangu! Halafu nimekuahidi nitakuwa mwaminifu kwako! Inawezekana umeshadanganywa sana, lakini Malon, hushangai kwa mimi mtoto niliyezaliwa Dar, kukulia Dar, katikati ya jiji na kunikuta nafanya kazi kama zile, nazungukwa na wanaume wengi kama wewe, leo wewe kuwa mtu wangu wa kwanza kukuruhusu unishike vile na kunibusu?” Malon kimya.

“Kweli bado umeshindwa kuniamini Malon! Ni nini nitakufanyia baadaye uje uniamini?” “Nilikosea Naya.” Malon akataka kumsogelea. Naya akarudi nyuma. “Hapana Malon. Hukukosea. Hivyo ndivyo ulivyo. Naomba niondoke.” “Tafadhali Naya, usiondoke.” Naya hakujibu. Akarudi sebuleni alipoacha mkoba wake, akauchukua. “Naya!” “Nakuhakikishia Malon, hunihitaji mimi kwenye maisha yako. Mimi sio msichana unayemuhitaji. Nina mambo mengi na malengo makubwa sana kwenye maisha yangu. Kwa sasa najihitaji mimi na akili zangu tu. Wala sio misaada unayonipa na kutaka mimi nifanye unachofikiria ni sawa. Utaua ndoto zangu kabisa Malon. Nitabakia kujulikana mimi ni mwanamke wa Malon. Basi.” Naya akatoka.

Malon akamkimbilia. “Naomba usubiri tuzungumze Naya. Tafadhali.” Naya akasimama. “Kwa kuwa mimi ndiye nimeharibu, naomba nipe nafasi ya kutengeneza.” “Kwa kufanya nini?” “Nitampigia simu yule mama, nizungumze naye.” “Sawa, nitashukuru.” Naya akageuka na kuanza kuondoka. “Sasa unaenda wapi Naya?” “Narudi Dar.” “Sasa hivi!?” “Kabisa Malon. Naenda kwa yule mama sasa hivi kwenda kuzungumza naye.” “Tafadhali Naya, usinifanyie hivyo!” “Angalia hapa.” Naya akamsogelea Malon.

Akafungua simu yake sehemu ya Doc. Akaanza kutafuta sehemu aliyokuwa ameandika mambo fulani. “Soma hapa, na hapa.” Malon akapokea ile simu. “Hayo ni malengo yanayofanana na yule mama na hayo ni makosa niliyogundua anafanya kwenye ile biashara. Chini nimeandika vitu gani vya kuboresha, kama nitafanya biashara kama ile. Mawazo machache ninayompa yule mama, na kumuongezea faida, yamenisogeza karibu naye japo mimi ni mdogo kwa kiongozi wake. Najipendekeza kwake zaidi, ili anisogeze karibu na watu anaowaita wamaana! Ili nikija kuanza kitu changu iwe rahisi nakuwa nimeshatengeneza mtandao wa watu watakao nisaidia. Kunitengenisha na yule mama, nikufuta kila kitu nilichoandika hapa.” Naya akachukua simu yake.

“Umenikatili Malon. Hivyo vitu nilivyoandika, sijakurupuka. Nimeandika nikiwa nimetulia. Unaponiona sina mahusiano na wateja tunao wahudumia sio kwa sababu sina shida au sina tamaa za mwili. Ni kwa sababu naona ni afadhali nikose milioni moja sasa hivi, nije kutengeneza milion 10 baadaye. Sijui kama unanielewa Malon. Kwa kulala na wale watu pale, au watu kama nyinyi kwa pesa chache hizi mnazotuhonga sasa hivi, nikufuta mahusiano mazuri ya baadaye.” Naya akamgeukia vizuri.

“Angalia sasa hivi. Kwa kukuruhusu tu unibusu, umenipa pesa, na kuamua kufuta malengo yangu bila hata kuniuliza! Kwa busu na pesa chache tu ulizonipa. Lakini ningefunga hisia zangu, nikasimamia msimamo wangu tokea mwanzo nilipokukatalia, sasa hivi ningekuwa na yule mama. Pengine kuna kitu kingeongezeka katika malengo yangu ya baadaye. Nimevunja maadili yangu. Nimeruhusu hisia zangu zinizidie. Nimekukaribisha kwenye maisha yangu, umeniharibia jambo kubwa sana lililobeba hatima ya maisha yangu.” Naya hakuwa akiongea akiwa amepaniki.

“Naya, nimeahidi kurekebisha.” “Nitashukuru sana. Lakini sitaweza kuendelea na wewe Malon. Tafadhali tafuta mwanamke mwingine. Hunihitaji mimi kabisa. Nina mambo mengi mno yanayoendelea sasa hivi. Nina shida ambazo haziwezi kutatuliwa kwa misaada unayoahidi kunipa.” “Umekasirika Naya, naomba utulie.” “Sijakasirika, lakini naona sipo tayari kwa mahusiano Malon. Hata hivyo nafikiri sikufikiria vizuri na sijui kwa nini! Sijui nimeingiwa na nini hata mimi sijielewi! Ndio nipo mwaka wa mwisho, nimalize O level, halafu naanzisha mapenzi! Sidhani kama ni wakati mwafaka huu. Tafadhali endelea na maisha yako, Malon. Sipo tayari. Samahani sana kwa kukupotezea muda wako. Naomba niondoke.” “Basi naomba nikurudishe.” “Hapana. Huna sababu yakufanya hivyo.” “Basi naomba nikupe dereva wangu, kama mimi umenichukia kwa kiasi hicho.” Naya kimya.  

Ni kweli hakutaka kutumia masaa mengine pamoja na Malon kwenye gari akimrudisha Dar. Malon akatoa simu yake. Akapiga na kumuita Side. Alimtaka afike hapo mara moja bila kuchelewa. “Side atakupeleka kokote unakotaka kwenda. Hatakuacha mpaka umruhusu. Unaweza kumtumia pia kukupeleka kwa huyo mama.” “Asante.” Naya akashukuru. “Naomba ukasubirie ndani basi.” “Hapana Malon. Naomba nikasubirie nje ya geti. Nitakuwa sawa tu.” Naya alitoka bila kugeuka. 

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

S

ide alifika hapo bila kuchelewa. Akamchukua Naya, wakaondoka. Side alijua amembeba Naya. Alijua habari za Naya zaidi ya Naya anavyofikiria. “Tunaelekea Dar?” Akauliza kiustarabu sana. “Ndiyo.” Naya alijibu kwa kifupi tu, macho kwenye simu yake akimtumia ujumbe Madamu Vane akiomba radhi na kumuomba arudi kazini. Bila kuchelewa akamjibu kwa uwazi kabisa, akimkatalia. Side alimuona Naya ameinama akilia kwa uchungu sana. Alishindwa hata kumtuliza. Alilia Naya. Akalia na kulia huku ameinama kwenye hicho kiti cha mbele alichokuwa amekaa.

       Na Malon naye alirudi ndani, akampigia simu Madamu Vane. Mara ya kwanza hakupokea, mara ya pili akapokea kwa kujihami. “Uliniambia nikae mbali na Naya, nimekaa naye mbali. Mabinti wote ambao wapo kazini sasa hivi, wapo na umri wa miaka 18 na kuendelea. Ni Naya tu ndio hakuwa ametimiza mika 18 bado, ila anatimiza mwaka huu. Sina kosa.” “Hapana. Nimepiga kuomba radhi. Nilikushutumu bila kufikiria na bila kuwasiliana na Naya mwenyewe. Ni kweli Naya anahitaji hiyo kazi.” “Ila kwa sasa siwezi tena kumpokea kwa kuwa ni kweli hajatimiza miaka 18. Ikitokea kweli mtu ananishitaki, mimi ndio nitaingia matatizoni.” “Lakini umesema anatimiza mwaka huu!” “Hata yeye nimetoka kumjibu sasa hivi. Siajiri tena msichana chini ya miaka 18. Akitimiza miaka 18, anitafute, nitaangalia kama nitakuwa na nafasi ya kazi, nitamuajiri. Nampenda Naya kwa kuwa ni binti aliyetulia na anachapa kazi. Lakini umenifungua masikio na macho. Nilikuwa nikifanya bila kufikiria, naajiri kutokana na muonekano tu.” Malon akaanza kuishiwa nguvu.

“Tafadhali naomba umpokee tena Naya. Mimi mwenyewe nitakutafutia kazi na nitakulipa.” “Hii ni biashara. Nikiharibu kwa makosa yakijinga kama hayo naweza kufungwa jela. Sasa pesa utakayonilipa itanisaidia nini nikiwa jela? Nina majukumu ya watoto. Nina binti kama Naya. Nikiwa jela nani atawatunza watoto wangu? Ile simu uliyonipigia na onyo ulilonipa ni vile niliogopa kukupigia tena simu na kukushukuru, kwa kuwa ulikuwa na hasira. Umeniepusha na mengi.” Malon akaishiwa nguvu kabisa, akawa kama amefungwa mdomo. “Naomba nikuage. Nipo kazini.” Yule mama akakata simu. Alimuacha Malon kwenye majuto, asiamini kama amemuharibia Naya kwa kiasi hicho.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Naomba unishushe Kiluvya, tafadhali. Sitafika mjini.” Baada ya kutulia, Naya aliweza kuzungumza na Side. “Bila shaka.” Side akajibu huku akiendelea kuendesha. Naya akapitiwa na usingizi akiwa anafikiria nini chakufanya tena. Aliamshwa na Side kuwa wamefika kwenye kituo alichokuwa amemwambia Kiluvya. “Nakushukuru.” “Unataka nikushushe hapa hapa kituoni?” “Inatosha, asante.” “Naweza kukufikisha kabisa.” “Nakushukuru kaka yangu. Asante.” Naya akashuka na kumuacha Side pale pale kituoni.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

     Kitu cha kwanza alichokifanya, ni kwenda kwenye kibanda cha simu. Usiku huo huo. Akanunua namba nyingine na kuisajili. Ile aliitupa palepale baada ya kuiharibu, ndipo akaelekea nyumbani kwao. Walikuwa wameshafunga milango tayari kwa kulala. Akagonga, baba yake akamfungulia.

Naya kipenzi cha baba yake, alimjua kwa kumtizama. “Mbona leo usiku hivi?” Naya kimya. “Umekula?” Baba yake akaendelea kuuliza. Akatingisha kichwa kukubali. Akaona machozi yanatoka. “Nisindikize bandani. Nimesikia ng’ombe wanalia.” Akafungua mlango, wakatoka tena nje na Naya. Wakazunguka nyuma ya nyumba, wakaelekea kwenye banda la ng’ombe. Hapakuwa na mlio wowote wa ng’ombe. Naya alijua baba yake anamtaka atulie.

“Nimepoteza kazi baba.” “Kwa nini?” Naya akaanza kulia tena. “Umri mdogo. Amesema mpaka nitimize miaka 18.” “Lakini mwaka huu ndio unatimiza miaka 18!” “Amesema hatanipokea mpaka nitimize. Na hapo ujue inategemea kama atakuwa na nafasi ya kazi. Nitafanyaje baba?” “Nilikwambia Naya, Mungu anaona kila mapito. Najua ulikuwa na malengo makubwa na hii kazi, lakini inawezekana Mungu ana malengo makubwa zaidi na unavyofikiria. Jipe muda.” “Sasa wakati najipa muda, unafikiri nitaishije sasa?” “Sijui. Ndio unatakiwa kuanza kufikiria Naya. Bado anakudai pesa ulizokopa kwa ajili ya kulipa madeni?” Naya akakumbuka uongo aliomdanganya baba yake.

“Ndio imeisha hivyo. Nitalipaje nikiwa sina kazi!” “Basi naomba utulie. Fikiria. Mimi nakuona unaakili sana Naya. Zaidi ya unavyofikiria. Na mambo yako hayo ya ubunifu wa mavazi, unaweza kufikiria jambo zuri tu.” “Nitapata wapi pesa?” Naya akamuuliza tena baba yake.

“Kuku wapo hapa. Mayai ya kienyeji yapo. Umeshafanya kazi, umekutana na watu wengi ambao itakuwa rahisi kwako kufunguliwa milango kwao kuliko mimi mgeni kwao ambao hata hawanifahamu. Tumia haya mayai kupata pesa. Wapelekee hata maofisini na majumbani kwao.” Naya akaanza kucheka. “Muone.” “Nilikuwa nimekasirika.” “Nilijua tu. Sasa hao watu wote Mungu aliokuwa amekukutanisha nao, haikuwa kwa bahati mbaya. Anza kuwatumia kujinufaisha na utajiri wao.” “Ndio maana nakupenda baba yangu. Ujue tumefanana akili za biashara?” Baba yake akacheka.

“Halafu mbona sisikii ng’ombe anayelia hapa.” “Alikuwa akilia mmoja. Muda tu. Nikaja, nikakuta amejifunga kamba shingoni. Amejizungusha, ikawa imemkaba. Nikamtoa. Sasa hivi nilikutoa wewe uje ulie hapa mpaka umalize, ndipo ukalale.” Naya akacheka. “Ujue nimelia kama lisaa?” “Nakujua. Na ninajua ukichoka kulia, ndio unakuja nyumbani.” Naya alicheka sana. “Kumbe unanijua?” “Najua sana.” Naya akacheka.

“Kesho nitakwenda kununua trei za mayai Kariakoo. Huku nawasiliana na watu nione kama watahitaji mayai. Nitafanya kesho, jumapili narudi hosteli.” “Kanisani?” “Nikwambie ukweli baba?” “Nakusikiliza.” “Mimi pale siwezi kurudi tena.” “Kwa nini? Au sababu ya deni?” “Walikudai vibaya sana baba, wakati wewe ni mshirika wao wa muda mrefu, tena mwaminifu! Unajitoa pale kwa uaminifu tena bila kutaka kulipwa. Wakati ule kabla mambo hayajakuharibikia ulikuwa ukitoa michango mbali mbali, leo naona kama wanakugeuka!” “Ujana mwingi. Baba yake Ino alikuwa mtu mzuri sana asiyeangalia kipato. Ameacha kanisa kwa vijana wale wanao endesha mambo kisheria, sio kiroho. Kama uliahidi kulipa deni tarehe fulani, basi watataka hiyo tarehe pesa yao ilipwe.” Naya akaguna.

“Mimi nimeshindwa baba. Hawana utu. Halafu pia Ino amenifika kooni baba. Siwezi kukaa naye sehemu moja. Ananikera, halafu..” “Hana nidhamu.” Baba yake akamlizia. “Kumbe unajua! Sasa kwa nini humwambii mama?” “Anasema hataki uishie kama yeye.” “Sasa itanisaidia nini kuishi kwenye nyumba nzuri lakini sina raha baba?” “Mimi pia nilimwambia hivyo. Lakini naona mwenzangu amempenda sana Ino. Sasa sijui.” “Mimi simtaki na nimemwambia kabisa simtaki. Kwanza ameniambia anaoa.” “Muongo.” Naya akashtuka.

“Baba! Mbona ameniambia.” “Anamuoa nani yule. Maneno mengi tu. Nilimsikia mama yake akimwambia mama yako. Si alikwambia mkiwa ofisini kwa mchungaji ulipoenda kulipa deni?” “Umejuaje!?” “Nakwambia mama yake alimfuata hapa mama yako. Akalalamika kuwa ulimvunjia heshima Ino. Lakini hana mwanamke yeyote. Alikwambia vile ili kukutisha tu. Lakini nakubaliana na wewe Naya, Ino atakusumbua sana. Anaujuji mwingi.” Naya akafurahi sana kuona baba yake yupo upande wake. Wakati wote alikuwa anakuwa kimya linapokuja swala lake na Ino. “Asante baba.” “Wewe nenda kalale, kesho uanze siku ukiwa umetulia.” Naya akarudi ndani chumbani kwake. Wadogo zake wakiume walikuwa wakilala chumba chao, yeye peke yake, na chumba cha wazazi wake, nyumba ikawa imekamilika. Vyumba vitatu tu.

Usiku huo alichofanya nikuhamisha namba zote anazotaka yeye, kwenye namba hiyo mpya. Uzuri namba zake alikuwa akizitunza kwenye simu sio line. Akaanza kuandika majina ya watu wakuwasiliana nao kesho yake. Akawapanga vizuri. Ndipo akalala.

Mlango Mmoja ukifungwa.....

A

lichofanya chakwanza ni kumtafuta tena yule yule Madamu Vane akamwambia bado anashida na kazi, kwa kuwa anahitaji sana pesa. Akamwambia kwa wakati huo anafanya biashara ya kuuza kuku na mayai. Kienyeji, akampa bei na ya kuku wa kisasa. Akaandika bei zote vizuri. Akamuomba amtafutie wateja, na akamsihi asiwape kina Tula namba yake. Akamtumia ule ujumbe. Akaandika ujumbe kwa watu wengine aliokuwa akiwafahamu na alio wahudumia kwenye shuguli. Akiwaambia anauza kwa jumla na rejareja. Kwamba anaweza hata kuwapelekea majumbani. Naya alituma huo ujumbe kwa watu wengi tofauti fofauti.

Wakati anaendelea kujibu maswali ya watu aliowatumia ujumbe, simu ya Madamu Vane ikaingia. Akamuelezea mazungumzo yake na Malon. Naya akamuomba msamaha. “Nilitaka kujichanganya tu mama yangu. Lakini basi. Nimeelewa. Na yeye ameomba msamaha. Naomba umsamehe. Nia yake ilikuwa nzuri, hakujua kama wewe ni mama unayejiheshimu. Alijua unatuuza.” Naya akampamba wee, mpaka yule mama akatulia. “Sasa hayo mayai unayo mengi kwa kiasi gani?” “Ya kisasa ninayo mengi.” “Kuna mtu anahoteli mjini. Nimezungumza naye, ndiye ameniuliza hivyo. Una uwezo wakumpeleka trei ngapi kwa siku?” “Naomba nipige mahesabu, kisha nikujibu kwa hakika.” “Unaakili Naya! Ndio maana mimi nakupenda na nilikuweka karibu.” Naya akacheka. “Ila mimi nataka trei mbili za mayai ya kuku wa kienyeji, kila week.” “Sawa mama yangu. Asante kuniungisha. Nikuletee na wewe leo?” “Wewe tu.” Naya akacheka. “Basi nakuletea leo, na nitakupigia tena ili kukupa idadi ya trei ninazoweza kupeleka.” “Sawa.” Wakaagana, Naya akatoka anakimbia.

“Babaa!” “Acha kelele Naya. Mama kalala.” Mdogo wake mdogo, Bale alimjibu akiwa jikoni. “Baba yuko wapi?” “Aliamka alfajiri kwenda Kariakoo. Alisema anaenda kununua trei za mayai.” Naya akafurahi sana. “Mama ameamkaje?” “Mguu ulikuwa ukimuuma. Zayoni amempelekea uji na dawa, amesema anarudi kulala.” Naya akaona aende akamsalimie mama yake chumbani kwao. Aliamka na mambo ya biashara.  

Alimkuta amejilaza tu kitandani. “Kelele za nini asubuhi asubuhi?” Naya akacheka. “Shikamoo mama.” “Uso huo wafuraha. Kuna habari gani njema?” “Nimepata wateja wa mayai.” “Wewe utakua na akili ya biashara kama baba yako! Haya umewapatia wapi hao wateja? Maana yanaharibika tu huko ndani!” “Kule nilikokuwa nikifanya kazi. Nimemuomba bosi wangu anitafutie wateja. Sasa amenipatia kwa rafiki yake mwenye hoteli mjini. Ndio anauliza nina uwezo wa kupeleka trei ngapi!” “Yapo mengi tu.” “Bwana mama! Sema idadi tutengeneze pesa.” Mama yake akacheka. “Hivi ujue hujanijulia hali Naya mwanangu!” “Pole mama. Lakini unajua tukipata pesa hata mguu utapona!” Wakacheka. “Unajisikiaje?” Naya akajiweka kitandani kwa mama yake wakaanza kuongea.

Mara akasikia sauti ya baba yake. Akaruka mbio kutoka pale kitandani. “Baba! Baba!” “Naya kwa kelele! Usipokuwepo humu ndani kunakuwa kimya.” Bale mdogo wake anayemfuata, akalalamika akiwa jikoni. “Nimefanyaje? Si nimemwita tu baba?” “Kwa nini usimfuate nje, kuliko kupiga kelele humu ndani? Nilishakwambia acha kelele, mama kalala!” “Wala hajalala kwa taarifa yako. Tulikuwa naye chumbani.” “Umeshamuamsha!” “Nimekuta hajalala kwa taarifa yako.” “Atalalaje ni kisauti chako hicho chakelele.” “Usinipotezee muda. Wewe ndio unakelele.” “Aliyekuwa..” “Mmeanza, Naya na Bale. Ni nini mnabishana tena?” Baba yake akaingia. “Si Bale huyo!” “Bale gani, wakati ni wewe?” Bale akajibu. “Haya naomba mnyamaze, muache kelele.” Baba yao akawanyamazisha. Bale alikuwa kidato cha pili, wakati Naya cha 4, walikuwa hawaishi kubishana.

Naya akamvuta baba yake. “Umefurahi nini?” “Lile wazo lako la jana usiku limejibu baba yangu. Sasa swala ni mayai. Tunayo yakutosha?” Naya akamuelezea baba yake alichofanya, Bale akimsikiliza. “Akitulia huwa akili zake zinafanya kazi huyo!” “Niache Bale.” “We Naya! Hebu rudisha akili hapa. Sasa mjibu mwambie, tunaweza kwa sasa, kupeleka trei...” Baba Naya akafikiria kidogo kisha akamtajia idadi ya mayai wanayoweza kupeleka. “Na mayai ya kienyeji? Maana nayo nimepata wateja. Ngoja nikalete simu nikupe idadi wanayotaka.” Naya akarudi ndani kwa haraka. Na mama yake akatoka akichechemea.  

“Nimewasikia huko chumbani. Naona unamfundisha biashara mwanao.” Baba Naya akacheka. “Lakini naona mwenzangu amechangamka!” “Akikufuatisha, atafanikiwa.” Gafla baba Naya akaanza kupewa sifa na mkewe. Akacheka. Naya akatoka akiongea na Madamu Vane. “Nakushuru sanaa, mama yangu. Kwa tenda hiyo uliyotutafutia. Leo nakuletea lita moja ya maziwa, na mayai ya bureee.” Wakacheka na kuagana.

“Haya tupe habari.” Baba yake Naya akamtaka asimulie. “Huyu mama ndiye aliyekuwa bosi wangu. Ameniunganisha na huyo mwenye hoteli. Nimezungumza naye hapo chumbani, lakini ameongea kwa haraka tu. Anasema kuna watu walikuwa wakimpeleka mayai. Lakini wameanza kusuasua kwa sababu Mzee mwenye hiyo biashara ya kumpelekea mayai, amekuwa akiugua kwa muda mrefu. Amewaachia wafanyakazi tu. Hawampelekei mayai yakutosha na wakati mwingine hawapeleki kabisa. Sasa anataka uhakika kama sisi tutakuwa tukimpelekea. Nikamuhakikishia. Anasema kama tunayo hayo mayai, tumpelekee sasa hivi.” Wakaanza kushangilia.

“Subirini kwanza. Ila amepunguza bei kwa kuwa anasema anachukua mengi. Na hata kama tunayo zaidi tumpelekee tu.” “Hamna shida. Ni bora hivyo kuliko hivyo yanavyo haribika hapa ndani. Twende ukanisaidie kuyapanga vizuri, tupeleke.” “Baba alivyochangamkia!” “Malaika ndio ametibua maji hivyo. Ukichelewa, ujue mwengine atatumbukia apone yeye, wewe uendelee na matatizo. Nayafunga sasa hivi kwenye pikipiki yangu, nampelekea sasa hivi. Nipe tu namba yake.” Naya na baba yake wakachangamkia kazi. Baba yake akatoka na trei 14 za mayai.

Huo ndio ukawa mwanzo wa kufufuka kwa wazazi wake. Biashara hiyo ya mayai, ikazaa na uhitaji wa maziwa kwenye hoteli hiyohiyo. Kwa hiyo baba Naya akawa akipeleka mayai, maziwa na akishinja kuku pia alikuwa akimpelekea huyo mwenye hoteli. Ufugaji ukakolea hapo, pesa ikawa inaingia, Naya akatulia shuleni.

 ~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kwa kuwa kibarua kiliota majani, Naya akawa anatulia tu shuleni, anategemea kutunzwa na wazazi wake. Akisikia mtu anataka mayai, basi anampigia simu baba yake. Kazi yake ikawa kutafuta masoko. Baba yake akaongeza jihudi yakuzunguka kwa wafugaji. Ananunua kwa jumla, tena kwa bei ya chini sana, anaenda kuuza kwenye masoko anayokuwa anatafutiwa na mwanae. Mambo yakawa mazuri. Utulivu ukawepo hata nyumbani kwao.

Baada ya kama mwezi hivi akiwa amejilaza kitandani kwake, kina Wahija na wengine pia wamejilaza tu wanaongea hili na lile. Wakipeana stori za mitaani na wakitoa uchovu wa shule wa juma zima, wakasikia Girls star wanashangilia nje. “Wameshapata bwana hao watoto!” Wahija akasema. Naya akacheka. Wahija akaita kwa sauti, akimtaka Tula aende. Tula akaingia akiwa amechangamka kweli.

“Haya, kelele za nini?” “Sio mimi da Wahija.” “Ni nani wakati nimekusikia wewe na wenzio?” “Ni Lulu.” Tula akajibu huku anacheka. “Bwana si usimulie? Acha kunifanya nikuulize ulize.” Tula akaangalia nje ya mlango kama wenzie wanamuona. Akaingia na kufunga mlango.

“Naya yupo?” Tula akauliza. “Hayupo, yupo kwao.” Wahija akamdanganya. “Basi, sisi tulisikia Naya kaachana na Malon. Sijui ilikuwa vipi, wewe unamjua Naya kwa maringo! Sasa Malon anapesa sana. Lulu alikuwa anamtaka sana Malon. Sasa Chezo, niliyekuwa namtaka mimi akamuonya Lulu kipindi kile asimfuatilie tena Malon, yupo na Naya. Sasa tulipoona Naya hayupo tena na Malon, Lulu akaniomba nimtafute Chezo, amuunganishie kwa Malon. Sasa mimi jumamosi ile nilimtafuta Chezo, jumapili tukawa naye siku nzima. Nikampa yakikubwa mpaka nikamuona ametulia.” “Wewe mtoto ulienda mpaka Moro!?” Wahija akamshangaa.

“Hapana da Wahija! Wale vijana wanapesa. Alichukua chumba kwenye hoteli ya maana hapahapa mjini. Akaja na akanipa pesa ya maana. Basi turudi kwenye ya Lulu sasa. Mimi nilipoona nimefanikiwa kumkoleza Chezo mpaka akakolea ndio nikamwambia Lulu anampenda sana Malon. Na yupo tayari kutulia naye. Chezo akasema ataenda kuzungumza na Malon, lakini linapokuja swala la wanawake, Malon anakuwa na misimamo yake.” Tula akakaa kwenye kitanda cha Wahija.

“Sasa Chezo ameniambia Malon anampenda sana Naya. Unaambiwa karibu kuchanganyikiwa!” Tula akapunguza sauti. “Usije kunitaja da Wahija. Hata Naya usimwambie.” “We bwana unawasiwasi gani?” “Mwenzio Chezo kaniapisha. Kasikia hapa maneno yanasambaa sana. Ameniambia akija kusikia Malon mwenyewe, hakawii kuja kunivunja mbavu.” “Wewe nisimulie. Mimi nampata wapi huyo Malon wakumsimulia na msikitini haji?” Tula akacheka sana.

“Da Wahija kwa maneno!” “Bwana wewe sema.” “Basi, unaambiwa siku ile Malon alipokuja kumchukua Naya, akamfikisha mpaka nyumbani kwake. Unaambiwa Malon alikuwa amejiandaa. Marafiki zake wote walikuwa wanajua siku hiyo mwanamke wa Malon atakuwepo mjini, hakuna kumtafuta Malon. Wanasema ndio ilikuwa mara yake ya kwanza kwa Malon kuwa na mwanamke, japo nasikia ni malaya, ila hakuwahi kuwa na mwanamke. Sasa hawajui ilikuaje, Malon hajawaambia wenzie, lakini si Naya akaondoka hata hajalala!” Wahija akaka kwa mshtuko.

“Acha masihara!” “Kweli tena. Unaambiwa Malon alikaribia kuchanganyikiwa. Naya aliondoka nyumbani kwake usiku, akamuacha yule kaka amepiga magoti anamsihi asiondoke. Lakini unaambiwa Naya akaondoka. Halafu haijaishia hapo. Si Naya kabadili namba?” “Ndiyo.” Wahija akajibu kishabiki. “Basi nasikia ni kwa ajili ya Malon. Kamkataa yule kaka. Naya kwa maringo! Sijui anataka nini! Basi sisi tukaona tumchangamkie Malon. Maana akipona Lulu, na sisi si tumepona?” “Ehe!” Wahija akataka aendelee.

“Mbona nilifanya sarakasi siku ile kwa Chezo! Siku nzima mtoto nipo ulingoni kumuweka sawa Chezo, akamuunganishie Lulu. Basi ikawa kimya mpaka sasa hivi Malon amemtumia pesa Lulu na ujumbe kuwa, akatafute gauni zuri la heshima, kesho anakuja kumchukua, kuna harusi hapa Dar, anataka kwenda naye. Amemwambia asiende kazini, atakuwa naye kesho.” Moyo wa Naya ulipasuka kwa mshtuko.

Alitetemeka pale kitandani asijue ni kwa nini wakati yeye mwenyewe ndiye aliyemuelekeza Malo kwa Lulu. Ilikuwa kama amemwagiwa maji ya baridi sana, mwili ukafa ganzi. Akaumia sana moyoni. “Lulu kauchinja dada yangu! Sio mwenzetu tena! Chezo aliniambia yule kaka anapesa sana. Hiyo pesa ya gauni tu aliyomtumia Lulu, imetutoa mate. Na Lulu amesema hiyo kesho atamng’ang’ania mpaka amlale. Na amesema akilogwa tu amtoe nguo, hatakaa akamsahau.” Tula akaongea hapo kishabiki, akieleza mikakati ya Lulu mpaka akachoka. “Haya kampe hongera zake.” Tuli akatoka akicheka. Chumba kile kikawa kimya. Hakuna aliyeongeza neno.

 ~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ni kweli Lulu alikuwa amejawa na furaha. Alikuwa akiimba kwa sauti bila kuchoka. Kesho yake siku ya jumamosi ni kweli akaenda kutafuta nguo ya maana na kiatu. Jioni wakasikia wakishangilia. Kuwa Malon yupo nje, anamsubiria. Naya alinyamaza kimya bila kuweka neno. Lakini aliumia sana, asijue kwa nini. Girls star walimkuwa wakimshangilia Lulu, mpaka Wahija naye akatoka kwenda kumtizama. Alirudi akicheka.

“Bwana Lulu kapendeza yule mtoto! Na kweli amevaa nguo ya maana.” Wahija akasifia, Naya kimya. “Sasa Naya mdogo wangu, kwa nini ulimkataa Malon?” “Mimi naomba nisikujibu dada Wahija. Tafadhali dada yangu.” “Nipe tu sababu kwa juu juu bila undani.” “Da Wahija!” “Sasa ubaya upo wapi Naya mdogo wangu?” Wahija akazidi kumbembeleza. “Nimejiona mimi sipo tayari kwenye mahusiano. Ni hilo tu.” “Kwamba wewe mdogo!?” “Sio udogo tu. Ndio mwaka wangu wa mwisho wa O level, siwezi kuanzisha jambo ambalo...” Naya akasita.

“Wewe hukumtaka tu huyu bwana. Lakini huna udogo wakushindwa kuwa kwenye mahusiano bwana! Tena kwa mwanaume anayekupenda hivyo! Kamuulize mama yako au bibi yako aliolewa na miaka mingapi kama sio 14 au 13.” Naya akanyamaza nakuendelea kusoma. Hakuna hata kilichokuwa kikiingia muda huo. Amekosa mwanaume na kazi pia! Aliumia sana.

Kitendo chakutorudi Lulu usiku huo mpaka kesho yake mchana, kilimuumiza sana Naya. Kuwa amelala na Malon. Aliumia sana. Lakini hakuwa na pakusemea. Anamlaumu nani? Hakujua kama anampenda Malon kiasi kile. Akajiambia labda ni wivu tu. Akatulia. Lulu alirudi akiwa amejawa kelele. Kila mtu alijua amelala na Malon usiku huo. Aliongea bila kuficha huku akimsifia vile alivyomtenda.

  ~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Usikose Mwendelezo kujua kilichoendelea kati ya Malon na Lulu aliyempania mpaka amefanikiwa......

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment