Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA! – SEHEMU YA 8. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA! – SEHEMU YA 8.

 huko kwa Malon!

Malon alirudi Morogoro, moja kwa moja kituo cha polisi. Hata polisi wenyewe hawakuamini walipomuona Malon anaingia kituoni. Kila mtu aliyemkuta pale kituoni alinyamaza wakimtizama Malon aliyekuwa akifahamika kama chumvi kwenye mji huo mdogo wa Morogoro. Polisi walibaki na butwaa, kwani habari za kutafutwa Malon, zilizagaa kila mahali. Inamaana hakusikia kama anatafutwa au!? Ndio swali lililopita kwenye kichwa cha kila mmoja wao pale kituoni.

“Nimepata taarifa kuwa natafutwa, na dereva aliyekuwa akiendesha gari yangu amekamatwa.” Malon alianza hivyo. “Una makosa mengi sana, Malon.” Mmoja wa askari akadakia. “Basi, kwa kuwa ni mimi ndiye ninayetafutwa, nimekuja kujibu shutuma zangu,

naomba mumuachie Side. Hausiki na chochote kile. Gari ni yangu, na mimi ndiye huwa ninamtuma sehemu mbali mbali kwa kutumia gari yangu.” “Kwa hiyo unakubali kosa?” Mmoja wao akauliza. “Kosa gani?” Malon akauliza na yeye.

“Shutuma zako.” “Zipi?” Malon akauliza tena, kwa utulivu tu. “Maana ninachozungumza hapa ni kile alichokamatiwa Side. Nadhani hamkuwa na tatizo na Side, ila mimi. Mmemkamata Side, kwa kuwa alikuwa kwenye gari yangu. Sasa ndio nasisitiza kuwa, Side ni mjumbe tu. Mimi ndiye mtumaji. Nipo hapa kuchukua nafasi yangu na shutuma zozote. Naomba mumtoe Side.” Malon akashangaa hakuna hata kipingamizi, wala hakutakiwa alipe pesa yeyote ile kumdhamini Side. Kama waliookota alumasi, wakamfunga pingu yeye, wakamtoa Side. Malon akawekwa jela.

Kwa kushindwa kusomewa shitaka hata moja, Malon akajua hawajamkamata Side na mzigo wa bangi. Na kwa kuwa walikataliwa kuzungumza, Side akaondoka huku akimwambia Malon atarudi tena hapo kituoni kesho yake, Malon akaingizwa lupango, akiwa ametulia tu. Ila anafikiria kilio cha Naya. Hakujua ni wangapi wapo nyuma ya huo mpango. Hajua watafanya nini na yeye, kwa kuwa alijua nia yao ni kumkomoa, sasa watakwenda umbali gani kumkomoa! Watamuweka hapo mpaka lini na kwa shutuma gani? Malon akaona atulie kwanza. Maombi yake ni kuwa Naya, aelewe, asirudi Morogoro. 

Kwa Naya!

Agonga Mwamba hata kwa wazazi wake Malon.

A

lisubri simu ya Malon usiku kucha. Na kwa bahati mbaya, Side naye akawa hapatikaniki kwa simu. Alfajiri, akaamkia chumbani kwa baba yake. “Naenda Morogoro.” “Naomba utulie Naya.” “Siwezi baba. Labda unipeleke. Kama hutaweza, mimi nakwenda mwenyewe. Siwezi kumuacha Malon peke yake.” “Sasa umeshajua alipo?” “Siwapati kwa simu! Na sina namba za wazazi wake. Naona niende tu kwao.” Ikabidi baba yake ajiandae, waondoke na Naya.

Walifika Morogoro mida ya saa 4 asubuhi. Moja kwa moja mpaka kwa wazazi wake Malon. Waliwakuta wametulia kama hakuna kinachoendelea. Kwanza wakawashangaa wao. “Swala la Malon kuwa jela, ni kama mtu kwenda kanisani au msikitini.” Aliongea baba yake nakumshangaza Naya. “Nani atamtoa sasa!?” Naya akauliza kwa kushangaa. “Wavuta bangi wenzake wa huko huko mtaani.” “Safari hii ni tofauti Mzee Saduki. Marafiki zake Malon wamemgeuka.” Naya akajaribu kutetea.

“Mama wewe ni mgeni kwa Malon. Sisi tunamjua huyo, tokea analetwa hapa duniani. Na mama yake alishamkalisha kwenye kochi hilo alilokaa baba yako. Akamuonya mtindo wa kutembea hovyo na wanawake za wenzake. Tena akamwambia wazi kabisa, hakuna vita mbaya, kama ya mapenzi. Huwa vita vyake haviishi kwa mshale wala bunduki. Kama kawaida ya Malon, hakuna aliyemsikiliza. Akatoka pale mlangoni, bila kujibu wala kuruhusiwa. Kila leo yupo jela! Kwa makosa yanayopishana majina tu. Mama yake ambaye angalau huwa anamsikiliza, ashazungumza na Malon, zaidi ya umri wako wewe Naya mwanangu. Akimsihi abadili maisha yake. Pale alipo hana shule, hana chochote. Kwa mara ya kwanza tokea azaliwe, wewe ndio kitu cha maana tulichokiona anacho huyo Malon, mbali na magari pamoja na hizo nyumba mbili alizo nazo.” Yule baba akaendelea.         

“Tuliposikia amepata msichana, akatulia hapa kati, tukamwita hapa, tukampongeza. Mama yake akamsihi kama ampigie magoti vile! Akamuomba atulie sasa. Aoe. Akasema Naya anasoma, akimaliza chuo ndipo mtaoana. Hee! Hatujakaa sawa, tunasikia na wewe umemuacha, sababu ya umalaya. Mama yake akamwita hapa siku moja kabla ya ile sherehe yetu. Maana mama yake ndiye mtu ambaye angalau akimwambia kaa chini, anakaa. Mimi hanisikii kabisa yule mtoto, kama hana masikio! Akaja dada yake, shemeji yake, mimi na mama yake. Tukamkalisha kikao hapahapa. Hakuna ambalo tulimbakisha Malon. Tulizungumza naye kwa undani, kwa wazi, mpaka mama yake akalia. Mama yake akamuomba abadili maisha anayoishi. Tukazungumza naye hapa, akaondoka. Akaendelea na maisha yake yaleyale. Mtoto kama huyo, unamfanyaje? Unamtoa jela ili aje aishi huku mtaani aendelee kuchafua watu?” Baba yake akauliza. Naya kimya.

“Baba Naya!” Mzee Saduki akamgeukia baba yake Naya. “Mimi nina mabinti watatu kama Naya. Nazungumza na wewe kama mzazi mwenzangu. Malon sio mwanaume wa kuoa, wala kutulia. Umesomesha binti yako, shukuru Mungu, muweke mbali na Malon. Malon ni mtoto wangu nimemzaa. Damu yangu kabisa, lakini ninachokwambia, sio kijana wakuoa. Vilio kama hivyo vya mwanao hapa Morogoro, vimetapakaa mji mzima. Malon analiza watoto wa watu, ni hivyo Mungu ametusaidia kuwa ni yeye peke yake ndio kondoo aliyepotea. Ndugu zake wanamaadili. Hakuna mtoto wa kike asiyemjua na kulizwa na Malon hapa Morogoro. Huu ni ushauri wangu tu. Uuchukue au uukatae, itakuwa juu yako, na hakika mtanikumbuka.” Baba yake Naya kimya akisikiliza, Naya akilia.

“Mchukue huyo binti yako, sasa hivi, panda basi, rudi Dar. Achaneni na Malon. Mimi ni baba yake, najua ni nini ninachozungumza. ACHANENI NA MALON. Hakuna jela inayoweza kumfunga, hakuna nyumba inayoweza kumuweka, na hapajawahi kutokea mwanamke aliyewahi kumtuliza Malon. Sasa kabla binti yako hajaharibikiwa, kimbia. Nikisema kimbia, namaanisha kimbia, na mfunge milango, msuruhusu majanga ya Malon nyumbani kwenu. Maana Malon, hana janga moja. Ni hayo tu.” Akamgeukia Naya.  “Naya, nakuhusia binti yangu, achana na Malon. Nimesikia sifa zako, nitaumia sana, kuja kusikia na wewe umeingia kwenye mkumbo wa wanaolizwa na Malon. Kimbia mama. Ndio itakuwa salama yako.” Yule mzee akamaliza. Naya na baba yake wakaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Na kweli, baba yake Naya alihakikisha wanapanda basi kurudi Dar. Naya alikuwa akilia sana. Baada ya muda, akapitiwa na usingizi. Alimuamsha basi liliposimama Kiluvya. Naya alimka na kuanza kulia tena. “Nampenda Malon, baba.” Naya aliongea huku wakitembea kurudi nyumbani. “Na Malon alikubali kubadili maisha.” “Unajuaje Naya?” “Mimi nimezungumza na Malon, najua. Huwa hawezi kunidanganya Malon. Ni heri nimkasirikie kwa kuniambia ukweli, hata tugombane, kuliko kunidanganya. Malon hajui kunidanganya. Sipingi chochote alichosema baba yake, lakini Malon alifika kwenye kubadilika. Siwezi kumkatia tamaa.”

“Basi msubiri, atoke jela uone.” “Hawawezi kumtoa jela. Marafiki zake watamwacha aozee jela. Wanamlipiza kisasi. Na kama ulivyoona wazazi wake, wameshamchoka.” “Basi tumpe muda tuone. Tukiona kimya, tutajua chakufanya.” Wakawa wameshafika nyumbani. Naya akaingia chumbani kwake.  Alimsikia baba yake akimuelezea mama yake kila kitu. Akasikia mama yake akiguna. Akajua na pale kwao hatapata msaada kwa Malon.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akamtafuta tena Side, simu yake ikaita bila kupokelewa. Akapiga tena na tena, kimya. Akaona amtafute Chezo. Chezo akapokea. “Hivi unajua alipo Malon?” “Unakumbuka ule ushauri wangu wa kucheza kadi zako kwa akili, ukishazipanga, ukaona zimekaa sawa, chukua chako mapema, kisha ondoka?” Naya kimya. “Basi sasa hivi ndio muda wakuchukua chako Naya. Malon amefungwa, hatakaa atoke. Jamaa wanahasira naye, na polisi hivyo hivyo. Alikuwa akitafutwa muda mrefu sana, lakini polisi wakawa hawajapata ushirikiano wa raia. Sasa, sasa hivi, rafiki zetu wa karibu kabisa, ndio wanashirikiana na polisi. Polisi wameambiwa habari zote za Malon. Kwa undani na nje. Tena na wafanyakazi wa Malon ndio wamemuharibia zaidi kwa kumlipa Malon, sababu ya ukorofi wake. Kila kitu cha Malon, kitachukuliwa. Sasa ndio nashauri, chukua chako mapemaaaa. Kusanya kila kitu, tunza, kabla kiberiti hakijawashwa.” “Wewe unajua walipomfunga?” Naya akendelea kuuliza.

Ninachokwambia ni hivi, Malon sio wakutoka leo wala kesho.” “Hilo nimelielewa Chezo. Nataka kujua alipofungwa, basi.” “Nakuonya Naya. Kaa mbali na Malon. Huo ni moto umeshawashwa, usikubali ukakuteketeza na wewe.” “Malon yuko wapi?” Naya akaendelea kuuliza. “Amefichwa, ili asije kutoroka, au kutoroshwa.” “Inamaana wewe hufahamu alipo?” “Sifahamu.” Akajibu Chezo, lakini Naya akajua anamdanganya.

“Unajua alipo Side?” “Ni wewe peke yako umegoma kuelewa Naya. Nakwambia sasa hivi kila mtu anachukua chake mapema, anaondoka. Hakuna anayetaka kufa na Malon. Futi alishaondoka na ile gari ingine na pesa za Malon. Tokea jana hayupo mjini, na amekataa kuwaambia watu ni wapi anakwenda. Side naye ameniaga kuwa anahamisha familia yake hapa Moro. Mkewe mjamzito, na ana mtoto mdogo. Malon hana chakupoteza, lakini anasema yeye anavyo vyakupoteza. Akienda jela, nani atalea wanae na mkewe! Hivi tunavyozungumza, na yeye anakwenda kuweka mambo yake sawa polisi, anaondoka. Amesema hataki kuondoka halafu polisi wakamfuata nyuma. Anakwenda kutoa ushahidi wake, aagane vizuri na polisi, aondoke, akaanze maisha sehemu nyingine, mbali kabisa na Moro.” Chezo akaendelea.

“Na ujue kabisa, Side sio wakumchoka Malon. Ashamtoa Malon jela zaidi ya nitakavyokwambia, lakini na yeye amefika mwisho. Anaona ataishia pabaya. Sasa na wewe nakuonya. Mwenzio Side anajishindia lile gari la Malon. Kasema ndio analoondoka nalo. Sasa na wewe wahi chako. Changamka, usizubae.” Chezo akakata simu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Tumbo la Naya likaanza kuuma kwa mshtuko baada yakusikia kuwa mpaka Side anamkimbia Malon! Hakuamini. Akaumia sana, na kumuhurumia Malon. Kwamba amebaki peke yake. Swali likawa, amefichwa wapi? Ndio ukawa mtihani.

Mtoto huyo aliyeamua kuyavulia maji nguo akatoka tena. “Mimi kesho narudi Morogoro kumtafuta Malon.” Naya akawafuata wazazi wake. “Huwezi kufanya hivyo Naya. Huyo kijana ataku…” “Naomba mama usiungane na watu wengine kuwa kinyume na Malon wakati wewe mwenyewe ulisema alinisaidia sana. Mimi kesho naenda. Naomba baba unisindikize. Lasivyo mimi nakwenda mwenyewe. Wakinikamata na kuniua, basi. Lakini mjue niliwaaga.” “Sasa Naya mwanangu, na kazi za hapa?” “Basi wewe baki. Lakini mjue mimi kesho asubuhi, nitarudi Morogoro kwa Malon.” Naya akaingia chumbani kwake nakuanza kulia.

Bale akatoka chumbani. “Huyo, ni heri umpeleke tu baba. Akili imeshachanganyikiwa. Mimi nitaamka asubuhi, nisadie kukamua maziwa, nitayapeleka hayo maziwa huko hotelini na mayai wakati nakwenda shuleni. Nitazungumza nao, niwaombe tuwe tunawapelekea mara moja kwa siku, ila idadi ile ile. Niwe nawapelekea kila siku asubuhi kabla ya kwenda shule au wakitaka iwe jioni baada ya kutoka shule. Mchana mama akirudi, na kama wewe baba utakuwa hujarudi, mama asimamie ukamuliwaji. Ili maziwa yasishuke. Tutayaweka kwenye friji, tutachanganya na ya asubuhi, kisha niwe napeleka hiyo asubuhi. Siku ambazo mimi siendi shule, nitakuwa nikimsindikiza mimi mwenyewe huko Morogoro mpaka akili yake itulie. Lasivyo atagongwa na gari, tuanze matatizo mengine bure.” Wakakubaliana na Bale. Kwa mara ya kwanza, Bale akawa upande wa Naya.

 Naya na baba yake waanza kumsaka Malon.

W

alifika Morogoro mapema ya siku inayofuata, jumatano. Moja kwa moja mpaka kituo kikubwa cha polisi Morogoro. Naya na baba yake wakajitambulisha kwa majina tu. “Tunataka kumuwekea dhamana Malon Saduki. Alikuja hapa kituoni siku ya jumatatu. Dereva wake alikamatwa na gari yake, ndio akaja yeye mwenyewe. Mkamuweka ndani.” “Hiki ni kituo cha polisi dada, sio jela. Kama alikuwepo hapa tokea jumatatu, basi ujue hawezi akawa bado yupo hapa. Atakuwa rumande akisubiria kesi yake itajwe.” “Wapi?” “Wewe unauliza kama nani?” Kimya.

“Ni mume wako?” Polisi akamuuliza Naya lakini Naya alijua wazi wanamjua ila ni kumkejeli tu. “Hapana.” Naya akajibu. “Mwanasheria wake?” “Hapana.” “Ni ndugu?”  Akaendelea kumuhoji kwa makusudi ili kumkatisha tamaa. Baba yake kimya, ametulia kwenye benchi anamsubiria binti yake. “Sasa kama wewe sio ndugu, wala mke, au mwanasheria, hatuwezi kukwambia kwa sababu za kiusalama.” Naya akajua ni kweli kisheria hawawezi, ila pia wamekusudia kumbania Malon. Akaondoka na baba yake.

“Sasa hivi tunakwenda wapi tena mama?” Baba yake akamuuliza Naya kwa upole tu. “Turudi nyumbani wakati natafuta mwanasheria.” “Sawa.” Wakiwa njiani kurudi nyumani akajaribu kumpigia simu tena Side, simu ikawa imefungwa. “Side amefanya vibaya sana. Anamtoroka Malon, wakati Malon ndio alikwenda kujisalimisha ili akamatwe yeye, halafu Side atoke!”  Baba yake alimsikia akilalamika wakati anaendelea kurudia kupiga simu ya Side bila mafanikio. Akamuona ametulia. Akajua anafikiria.

Joshi.

Akatoa tena simu mfukoni. “Nina shida sana, naomba nisaidie.” “Ni Naya?” “Ndiyo, Joshi. Mimi Naya.” “Kwema?” Baba yake akaendelea kusikiliza tu. “Si uliniambia unafanya kazi kwenye ofisi za wanasheria?” “Ndiyo. Lakini kama muhasibu.” “Naomba unisaidie kunikutanisha na mwanasheria unayemwamini, anisaidie. Nina shida sana.” Kimya. “Joshi?” Naya akaita. “Nafikiria Naya. Hawa wa hapa, wanashugulikia kesi nyingi za kibiashara, yaani wanashugulikia kesi za biashara, makampuni makubwa na kadhalika. Halafu wanagarama sana. Bei zao zipo juu.” “Ninachotaka ni mwanasheria mzuri. Pesa sio tatizo.” Baba yake akamgeukia kama anayemshangaa.

“Tafadhali Joshi. Nisaidie ndugu yangu. Wewe nikutanishe na mmoja unayemfahamu ni mzuri na mwepesi. Mambo mengine niachie mimi mwenyewe.” “Sawa. Nitakupa jibu jioni. Maana mida hii wengi wanakuwa wanatoka. Na ninayemfikiria hapa, hayupo.” “Nasubiria basi simu yako.” Wakaagana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Nimesikia mazungumzo yako mama. Umesema pesa sio tatizo. Unapata wapi pesa?” “Mimi na Malon, tulifungua akaunti yetu ya biashara. Ndiyo akaunti inayoendesha kile kiwanda. Ameniweka na mimi kama muweka saini. Kuwa na mimi naweza kutoa pesa. Hata zile pesa zote za maonyesho ya mavazi, japokuwa tuligombana na Malon, nikamuachia yeye pesa yote, lakini aliniambia aliiweka huko. Nitakwenda kuangalia.” “Sasa kama wamemkamata, si wanaweza wakawa wameshikilia akaunti zake zote?” “Inawezekana. Lakini hii tulifungua kwa majina yetu, au tuseme ya ile kampuni yetu. Mpaka wajue na waishikilie, itachukua muda.” Baba yake akamtizama.

“Naomba tupitilize mpaka benki, nikatoe pesa yote nihamishie kwenye akaunti yangu kabla hawajaifikia hiyo akaunti.” “Mimi nina swali mama. Na uwe makini unaponijibu.” Naya akamwangalia baba yake huku basi likipita Kiluvya kituoni ambapo walitakiwa kushuka. “Ni kweli umekusudia kutumia pesa ya biashara kumtoa Malon ambaye huna uhakika wa nini atafanya tena kesho? Huoni kwamba huo ndio utakuwa mchezo. Unamtoa jela, mnafanya biashara, anakamatwa, unaenda tena kumtoa jela na pesa yote ya biashara!? Mtajijenga saa ngapi?” Naya akanyamaza. “Baba yake mwenyewe anasema Malon ni mtu wa kukamatwa kamatwa. Kweli mama yangu mzazi, umeamua maisha yako yaishie kwa Malon!?” Naya akafikiria kidogo.

“Nampenda Malon, baba. Hata nikiwa na mamilioni ya pesa bila Malon, sitafurahia. Hujui ni kiasi gani Malon anavyonipenda na kuniheshimu. Kila mtu analijua hilo. Malon ni mkorofi sana na anamatatizo yake mengi tu. Mimi namjua. Lakini kwangu ni tofauti baba yangu. Sitakuja kupata mwanaume anayenipenda na kunithamini kama Malon. Nimejaribu kanisani. Wewe ni shahidi. Lakini angalia Malon alivyokuwa akiwapenda na kuwathamini pale nyumbani kuliko hata Ino! Malon alikuwa akinifikiria mimi na familia yangu kwanza. Wewe unafikiri kwa nini japokuwa Bale ni mkorofi kwangu, lakini anampenda sana Malon?” Kimya.

“Kwa kuwa Malon ameonyesha kunipenda na kujali hata ndugu zangu! Zawadi alizokuwa akinisaidia kuwanunulia kina Bale wakati tupo safarini ni za mapesa mengi mno.” “Hilo nililihisi.” “Sasa unafikiri ni kwa nini alikuwa anatumia pesa yote hiyo? Au kila nilipokuwa nikimpa wazo, hakuna jinsi Malon akapinga. Ilimradi nimeongea mimi, Malon atafanya bila shida, ananisikiliza na kunithamini kuliko nitakavyokwambia. Nyumba ya Kunduchi sijui ameandika majina gani, lakini mimi amenipa funguo mpaka leo ninazo. Aliniambia niishi pale muda na wakati wowote ninaotaka, hata kama yeye hatakuwepo, au nikiwa nimemkasirikia niende tu pale na walinzi wote wananijua. Nimeishi naye pale kidato cha  5 na 6, akinitumikia kama nini sijui.” Naya aliropoka, Baba yake akashtuka sana.

“Lakini si nilifaulu?” Naya akajitetea. “Mimi nilijua unaishi hosteli kama ulivyokuwa ukiniambia Naya!” Naya akainama. “Nampenda Malon, baba. Sitapata mwanaume anayenipenda nakunijali kama yeye. Nisaidie nimtoe jela, mengine nitahangaika naye mwenyewe.” Naya akatulia kidogo. “Hakuna kitu nataka kwa Malon asinipe baba. Hakuna wazo nitampa, asinipongeze. Wamemfunga nikiwa nimempa wazo la biashara, akalifurahia na kunipongeza. Tulikuwa tunaweka mikakati yakufanya pamoja hiyo biashara. Niambie baba yangu, napata wapi mwanaume wa namna hiyo? Hata kama napata pesa yakuwa namtoa yeye tu jela, sitajali. Ilimradi awe anarudi kwangu.” Baba yake akamtizama, Naya akainama.

“Usiwe na wasiwasi, atanioa.” “Naya, mama yangu wewe!” “Nitaolewa na Malon, baba. Hivyo hivyo alivyo, atanioa. Na kama ukitaka kuniona ninafuraha wakati wote, basi uniombee Malon anioe. Ndio nitakuwa na furaha. Nampenda Malon.” Baba yake akamtizama tena na kunyamaza.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Naya na baba yake walifika benki. Naya akahamisha ile pesa yote kwenye akaunti yake, baba yake akimwangalia tu. Alifanya mambo akiwa ametulia kama aliyekuwa na mipango ya muda mrefu. Alipomaliza, akamuona anatoa simu wakiwa palepale benki. Akampigia tena Joshi. “Nipo hapa posta mpya na baba yangu. Tunaweza kuja hapo ofisini kwenu tukasubiria.” “Sijazungumza na yeyote yule bado, Naya! Labda ungesubiri.” “Naomba tuje tusubirie hapo. Tafadhali Joshi.” “Sawa. Karibuni.” Ilishakuwa mchana, Naya hazungumzii chakula, bado akili ipo na mipango ya kumtoa jela Malon.

“Hudhani kama tunahitaji kutulia kidogo, Naya! Mpe muda huyo mtu. Akiwa tayari atakutafuta.” “Kwamba nikatulie, wakati sijui walipomuweka Malon! Sijui wanamfanya nini sasa hivi! Sijui anahali gani! Malon anachukiwa baba. Pale Morogoro kwa sasa hana rafiki hata mmoja. Malon alikuwa akitafutwa na polisi. Hakuna atakapoangukia, akawa salama. Lazima nimtoe Malon popote alipo, kwa garama yeyote, tena kwa haraka. Mimi sitaki kutulia, baba.” Naya akaanza kulia.

“Mimi naweza kufikiria ukiwa na mimi. Naomba usiniache peke yangu.” “Haya twende. Lakini tupitie hata soda, mama. Njaa inauma.” Naya akajifuta machozi, nakuanza kucheka. “Twende nikupeleke ukale, halafu twende tukatafute msaada wa mwanasheria.” Wakatoka pale maeneo ya benki. 

Msaada wa Mwanasheria.

N

aya na baba yake walifika kwenye ofisi za mwanasheria baada ya kula. Wakapata bahati yakumpata mwanasheria aliyekubali kuwasikiliza. “Ninachotaka unisaidie, ni ujue yuko wapi. Na aweze kuwekewa udhamini, atoke.” “Kwa hiyo kama nimekuelewa vizuri ni kuwa, hajakamatwa na bangi?” “Hapana. Hata gari yake haikukutwa na bangi.”  “Sasa kwa nini walimkamata?” “Ndio nakwambia wanamtafutia sababu yakumlipiza kisasi. Ukimpata, yeye wenyewe atakueleza ili ujue ni jinsi gani yakumsaidia.” Yule mwanasheria akafikiria.

“Unayo pesa yakunitoa Dar kwenda Morogoro?” “Ndiyo.” Yule kaka akamtizama Naya. “Umesikia swali langu lakini?” “Umeuliza kama ninayo pesa.” “Ndiyo. Maana mimi sitakufanyia kazi ya kubabaisha. Tutampata. Lakini inahitajika pesa ya kulipa watu ili kutoa siri kujua alipo, kama polisi wakishindwa kutusaidia. Halafu najua kwa kuwa hawataki kumtoa, wataweka pesa nyingi yakumdhamini. Sasa sitaki wote tuonekane wababaishaji. Tunaanza jambo, halafu tunafika katikati tunakwamwishwa na pesa.” “Kwani unafikiria kiasi gani?” “Nyingi. Tunaanza na pesa zangu mimi za usafiri, na mfukoni wakati nashugulikia kujua ukweli wa nini kinachoendelea. Pesa ya kuweka sawa watu wakuniambia ukweli. Ndani ya polisi, nakuweza kumtoa.” “Hamna shida. Nitajie ni kiasi gani.” Baba yake alibaki akimshangaa Naya.

 

Harakati za kumtoa Malon Rumande wakati raia wamekusudia kumtoa mtaani. 

B

aada ya kukabidhiwa pesa aliyomtajia Naya, akaanza kazi. Ni kweli ilikuwa ikimgharimu Naya kila siku zilivyozidi kwenda. Na Mati, huyo mwanasheria alikuwa akimpa taarifa ya kila alipofikia. Ni kweli alikuwa anakutana na ugumu mkubwa. Baada ya kuhangaika sana, akaweza kujua alipo Malon. Alikuwa amefungwa, na kunyimwa haki ya kuonwa na yeyote wakati bado hakuwa amehukumiwa. Yule mwanasheria akaanza kupambana na hilo. Akidai haki ya Malon yakuonana na mwanasheria wake. Baada ya kupeleka barua hii, kuhangaika vile, ndipo akaruhusiwa.

“Jamaa yako anaonekana anamaadui kila mahali! Mpaka hakimu hamtaki mtaani!” Mati alimwambia Naya, jioni hiyo akiwa anaelekea kumuona Malon. Mwezi ulikuwa umeshapita. “Naomba msalimie sana. Mwambie nampenda.” Mati akachekaa. “Atasikia.” “Nipigie ukiwa naye au ukitoka.” Wakaagana.

Mati alifanikiwa kukutanishwa na Malon. Akamwambia ametumwa na Naya, ili kumsaidia. Anataka amueleze ukweli bila kuficha kitu. Ndipo Malon ikabidi kueleza ukweli wote bila kuficha. “Kama nimekusikiliza na kukuelewa vizuri. Ni kwamba, kwa upande wa hiyo biashara ya bangi, hujawahi kukamatwa hata mara moja?” “Hata mara moja ila tu kuhisiwa. Hapajawahi kuwa na ushahidi.” “Kuhisiwa na wafanyakazi wako wamekiri kituo cha polisi, Malon. Wapo mashahidi wawili. Waliosema wamekufanyia hiyo biashara.” Malon akashtuka sana.

“Haiwezekani!” “Kwa kifupi tu, nataka ujue unao maadui wengi.” “Hilo nalifahamu wa huhitaji kuniambia. Lakini sio wafanyakazi wangu. Wafanya…” “Side na Futi?” Malon akatoa macho. “Si ndio hao waliokuwa wakikufanyia kazi?” Kimya kwa mshtuko. “Wewe usijali. Na mimi ni mzuri kwenye kazi yangu. Nishafanya uchunguzi wakutosha, wanachotaka ni kukukomoa, na kukutoa mtaani, ndio maana upo hapa. Wanataka pesa nyingi tu kwa ajili ya kuwekewa dhamana. Kwa kuwa wewe umekamatwa kama uliyekuwa ukifanya biashara haramu. Na dhamana yake ipo juu sio sawa na aliyekamatwa akiuza kidogo. Ili kutoka hapa, wanahitaji pesa nyingi.” Akamtajia mamilion ya pesa zinazohitajika ili tu kutolewa kwa dhamana. Malon akabaki kimya.

“Unajua sehemu ya kupata hiyo pesa?” “Kwa sasa sina, kwa kuwa pesa nyingi zilikuwa chini ya Side na Futi, kwa ajili ya kufanyia au kuzizungusha kwenye biashara. Nilizokuwa nazo, nimewekeza na Naya. Kwa hiyo, hiyo pesa yote, kwa sasa sina.” “Basi, nitakwenda kuzungumza na Naya, nimwambie. Na sijui atakuwa kwenye nafasi gani! Maana kujua, kukupata na kukaa hapa kama hivi, imemgarimu sana Naya. Lakini nitamfikishia ujumbe.  Mkishajipanga, mtanitafuta tena.” Malon akafikiria. “Mwambie auze nyumba yangu ya hapa Morogoro. Anajua ni wapi naweka hati. Na hata kama hatapata mteja, basi akakopee benki.” “Sawa.” Wakaagana. 

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mati alitoka pale akampigia tena Naya. Alimweleza kila kitu. “Lakini mbona pesa yenyewe ya dhamana ni kubwa hivyo!?” “Nilikwambia ni kama wanamkomoa, halafu ukumbuke wanamshikilia kama mfanyabiashara haramu. Lazima dhamana yake iwe juu.” “Nakushukuru.” “Sasa hiyo pesa utakuwa nayo tuendelee?” “Naomba unipe muda, nitakutafuta tena Mati. Nimeshatumia pesa nyingi sana. Hiyo pesa itabidi kuuza vitu. Nitajitahidi kukusanya, naamini nitafanikiwa tu.” “Naomba kukupa ushauri Naya.” Naya akatulia.

“Unaniruhusu?” “Nakusikiliza Mati.” Naya akaitika. “Kuna watu hapa duniani, wanakuwa salama huko magerezani, kuliko mtaani. Kwa watu wengine, jela sio kitu kibaya, ni msaada. Wanatoka wakiwa wamejifikiria na huwa wanabadilika kuwa watu wema katika jamii.” Kimya. “Kwa jinsi nilivyopata habari za Malon, kutoka kwa polisi, mpaka kwa huyo hakimu, nafikiri Malon yupo sehemu sahihi. Usijimalize kwa ajili yake Naya. Wewe bado ni mtoto mdogo sana. Some people are not worth saving, Naya. Wewe bado ni binti mdogo sana, ndio umemaliza tu chuo! You have bright future a head of you. Naomba utulie kidogo tu, utafakari kabla hujaendelea sana.” Naya hakujibu.

 “Naelewa kuna kupenda au mapenzi huwa hayachagui, jiulize, at what cost Naya!? Kwa gharama ipi? Mimi ni kama kaka yako mkubwa sana. Nimeoa, ninafamilia. Nayajua maisha. Nakushauri ujijenge kwanza wewe mwenyewe kabla hujaangamia kama wengi wa mabinti wa hapa Morogoro. Ni hilo tu.” “Nashukuru kwa ushauri Mati. Nitakutafuta nitakapokamilisha hiyo pesa yote.” Naya alijibu tu hivyo, nakukata simu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alilia Naya nakushindwa kujisaidia. Alikumbuka mapenzi ya Malon kwake. Jinsi alivyompenda na kumuheshimu. Tatizo ni umalaya. Naya alilia kila akimkumbuka Malon. Jinsi alivyomsadia kulipa ada, kumtunza kuanzia kidato cha 4. Mapenzi waliyokuwa wakifanya na Malon anapokuwa naye. Jinsi anavyombusu. Japokuwa alijua anakuwa na wanawake wengine nje, lakini alithamini sana muda anaokuwa naye. Malon alikuwa akitulia sana kila Naya anapokuwa karibu. Kila kitu huwa kinasubiri, kila mtu huwa anajua, na kuelewa kuwa Naya yupo, na Malon hataki usumbufu kwa muda huo awapo na Naya. Aliweka heshima kwa Naya, kila awapo karibu na marafiki wa Malon, walimtambua kuwa ni mtu muhimu sana kwa Malon.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

     Wazazi wake walimsikia akilia chumbani kwake. Japokuwa walishamzoea kumsikia akilia humo ndani, lakini walijitahidi kutokuzoea kilio chake. Mama yake akamtizama baba yake, akaelewa. Akasimama na kumfuata chumbani. “Mwanasheria amekwambia nini?” “Twende nikawaeleze na mama.” Hilo likamfurahisha hata baba yake. Wakatoka.  Akaenda kunywa maji, kisha akarudi kukaa palepale sebuleni. Ilikuwa jioni, kina Bale nao ndio walikuwa wanatoka shule. Naya akawaeleza yote aliyoambiwa na Mati.

“Malon amesema niuze nyumba ya Morogoro.” “Utauzaje bila hati?!” Mama yake akauliza. “Najua anapoficha au kuweka hizo hati. Nitamuomba Bale anisindikize. Baba wewe pumzika.” “Mnakwenda Morogoro!?” Mama yake akauliza. “Hapana. Huwa anafungia kwenye Safe ya Kunduchi. Nataka leo nikachukue, kesho ndio niende Morogoro. Nikajaribu kuiweka sokoni au hata kuiombea mkopo benki.” “Nitakusindikiza Naya.” Bale akakubali kwa haraka.

Naya akaanza kulia tena. “Utanisindikiza wapi sasa?” “Kesho sitakwenda kujisomea na wenzangu. Nitakupeleka Morogoro, na tutakwenda wote Kunduchi sasa hivi. Nisubiri nile, nibadili nguo, twende.” “Asante Bale.” Naya akasimama huku analia, akarudi chumbani kwake. “Huwezi ukamwachia Bale. Usipokwenda naye huyo, hatanyamaza mpaka anarudi hapa. Na hatafikiria chochote. Ni heri umwambie akusubiri, uchukue maziwa, mpeleke, ndio muende huko Kunduchi.” Mama yake alitoa huo ushauri. Baba yake akaafikiana nao.

Walitoka jioni hiyo, wakamsindikiza baba yao kushusha maziwa na mayai kwenye hoteli mbili tofauti, ndipo wakaelekea Kunduchi. Pale kwenye nyumba ya Kunduchi hakuna aliyekuwa akiishi hapo, lakini Malon alikuwa ameweka kampuni ya ulinzi. Morogoro alikuwa ameweka mtu tu wa kawaida ndiye aliyekuwa akilinda nyumba yake. Walipokezana kulinda. Mchana mlinzi mmoja na usiku walikuwa walinzi wawili.

Naya aliwakaribisha pale sebuleni. Ilikuwa nyumba nzuri sana. Ndogo tu, lakini ilijengwa maeneo karibu kabisa na mahoteli, karibu na ufukweni. Mmiliki wake alionekana alikuwa na ramani nzuri. Kwani ilipangiliwa vizuri sana. Ndani na nje. Ilikuwa na vyumba vitatu tu. Hapakuwa na uwanja mkubwa sana mbele, na nyuma hivyo hivyo. Lakini ilikuwa karibu kabisa na baharini.

Naya aliingia chumbani kwao. Akatoka na bahasha kubwa. “Umepata?” “Nimepata. Lakini lazima kulipia ulinzi. Nisubirini niandike kundi ya malipo. Nizime taa zote na Ac, niache taa za nje tu, ili umeme usiishe.” Baba yake alibaki akimtizama. “Unataka nikusaidie nini?” Bale akauliza. “Naomba niangalizie hapo jikoni kama kuna uchafu wowote kwenye ndoo ya takataka hapo pembeni ya friji na kwenye sinki. Kwa kuwa nazima kila kitu, panaweza kunuka kama tukiacha uchafu.” “Unazima na friji?” Bale akauliza. “Hapana. Kuna nyama humo na vyakula vingine. Nikizima vitaharibika. Labda..” Naya akafikiria. “Naomba niangalizie vitu vilivyopo kwenye Friza. Hiyo nilazima niizime. Huwa inakula sana umeme.” “Sasa kama ina vitu?” Bale akauliza, Naya akafikiria tena kidogo. “Hamishia kwenye friji ndogo, unavyofikiria kama utatumia nyumbani, chukua. Weka kwenye gari, turudi navyo nyumbani.” Naya akaanza kupekua ile bahasha.

Baba yake akamuona anatoa hati moja, ingine akarudisha ndani. “Hiyo nyingine ni ya wapi?” “Hati ya nyumba hii, kule kiwandani, na documents za magari yake.” Naya akanyamaza kidogo, akamsikia anaguna. “Magari yenyewe wameondoka nayo yote. Yaani kila mtu amejimilikisha mali za Malon! Tena baada ya kumkamatisha mwenyewe polisi! Mungu atawalipa lakini.” Akamuona anaandika hundi. “Sasa hizo pesa za kulipa hao walinzi, utapata wapi?” “Kwenye ile akaunti yangu na Malon, nilibakisha pesa kidogo. Sasa kwa kuwa naona watu wanajichukulia tu, heri niimalize kabisa. Nalipia hapa, na kule kiwandani.” Wakamsubiria, akaweka mambo yake sawa. Wakaondoka.

 Hakuna msiba usiokuwa na mwenzie.

Mji Kasoro Bahari, Malon Alizwa vibaya sana. 

S

aa 12 alfajiri, Bale, Naya na baba yao walikuwa wapo kituoni wakisubiria mabasi ya kwenda Morogoro. Naya akamsogelea baba yake aliyekuwa mbali kimawazo, akamshika mkono. “Asante baba.” “Kwa kuwa ni wewe Naya, mama yangu mzazi. Lakini hakika sioni sababu mama. Naona ni kama nashiriki kwenye kukuangamiza tu.” “Nampenda Malon, baba. Hakuna jinsi nikasikia yupo matatizoni, nikaweza kulala.” Baba yake akamtizama. “Nimefurahi unakuja na sisi. Asante.” Baba yake akavuta pumzi kwa nguvu bila kujibu, akajisogeza kwenye huohuo mkono wa baba yake aliokuwa ameushika, akamuegemea. Bale alikuwa kimya, ameingiza mikono yake mfukoni. Alifanana na Naya, utafikiri mapacha. Urefu na sura kama mama yao.

Basi lilifika, wakaingia humo ndani, safari ya Morogoro ikaanza wote wakiwa wamejawa tumaini kuwa  hayo mamilioni ya pesa yanayohitajika kwa ajili ya Malon, yatapatikana kwenye hiyo nyumba ya Morogoro. Walitua jiji kasoro bahari, wakapanda tena daladala mpaka kwenye nyumba ya Malon.

Naya akashtuka sana akiwa bado nje. “Nini?” Baba yake akauliza. “Mbona kama wameng’oa geti! Halafu hakuna hata mlinzi!” “Kwani panalindwa hata mchana!?” Bale akauliza. “Mchana huwa anakuwa na mlinzi mmoja, usiku ndio wawili. Ila hapa wanalinda watu tu wakawaida, sio kampuni ya ulinzi kama kule Dar.” Naya akaongeza mwendo kufikia lilipokuwa geti, kuingia ndani! Macho yalimtoka Naya, wakamuona machozi yakimtoka huku ameweka mikono mdomoni. Bale na baba yake walikuwa hawaifahamu hiyo nyumba. Ni yeye peke yake Naya.  Wakaongeza mwendo na kumfikia.

“Mbona unalia tena!?” Baba yake akauliza. “Wewe huoni kuwa imebaki gofu tu!?” “Kwani hii ilikuwa nyumba kabisa?” “Ndipo tulipokuwa tukiishi tukiwa hapa Morogoro. Ilikuwa nyumba yenye kila kitu, kama vile ya Kunduchi ila hii kubwa zaidi!” Naya aliendelea kulia. “Mungu wangu!”  Wakamuona anaingia ndani. Hapakuwa na mlango wala dirisha. Kweli lilikuwa gofu. Waling’oa kila kitu. Wakachukua kila kitu mpaka vyungu vya maua! Bale na baba yake hawakuamini. “Hii kweli ilikuwa nyumba iliyokamilika!?”  Bale akauliza huku na yeye anazunguka mle ndani.

“Wameiba nguo zetu zote!” Naya alitoka chumbani kwao huku akielekea jikoni. “Huku nako wameiba mpaka vijiko! Mafriji wamechukua, makabati ya ukutani wameng’oa!” “Yaani hapa kwa ufupi ni kwamba wamebakisha kuta na paa.” Baba yake akaongeza. “Nashauri huku usiingie Naya. Wameandika ukutani matusi matupu na kunanuka sana mikojo.” Bale alikuwa kwenye chumba kingine. Naya akaendelea kulia.

Chumba kimoja kilionekana kuna mtu huwa analala hapo. Walikuta matandiko chini, na visufuria. “Uwii, Mungu wangu!” Naya alisikika akilia taratibu huku akizunguka. Baba yake na Bale wakatoka kumfuata hapo nje alipokuwa amekaa akilia.

Ghafla wakamuona amenyamaza. Akatoa simu, akapiga. “Chezo, ni mimi Naya.” “Unataka nini kwangu wakati uliniambia mimi sio mtu wa kuaminika? Mbambaishaji. Na hutakaa ukanitafuta tena wala kuniamini.” “Sikusema hayo yote Chezo, lakini pia nilikuwa nikikutania tu.” “Unajisahau sana Naya. Ulisahau mimi ndiye niliyekuwa nikihangaika kukufanikishia shuguli yako yote!? Niliacha mambo yangu yote huku Moro, nikaja Dar ili niwe na wewe, ufanikiwe. Japo sikutoa pesa, lakini nilitoa muda wangu na mawazo, wakati Malon akilala na wafanyakazi wako! Nikahangaika mchana na usiku, ukaja kunitukana mbele za watu!” “Chezo! Tulikuwa mimi na wewe, pamoja na Malon tu! Halafu nilikuwa nikikutania! Tafadhali naomba usikasirike. Nakuhitaji sana sasa hivi.” “Ili unitumie tena, halafu aje afaidi Malon?” Naya akaishiwa nguvu.

“Mimi nimeamua kukaa mbali na nyinyi bwana. Nilikuwa nakufuata mpaka Mzumbe, pale Malon alipokuwa akikukosea. Malon alikuwa analala na wanawake wengine, anakupiga, mimi nilikuwa na wewe Naya. Ukaona mimi sina kitu, ukaamua kubaki na Malon aliyekuwa akilala na kila mtu aliyekuwa akikuzunguka. Ni aibu mara ngapi amekutia Malon, mimi nikasimama na wewe? Mara ngapi nimekuwa na wewe Naya? Ukaja kunigeuka! Nimeondoka kwenye shuguli yako, usijue nimekwenda wapi, hata usinitafute! Nakuja kukutana na wewe, nakusalimia, na wewe unanipa lawama?” Chezo akaendelea kutoa ya moyoni.

“Umekuwa na tabia kama za Malon! Mnapenda kutumia tu watu. Hamna utu. Sasa kila mtu amewajua tabia zenu. Wamewakimbia. Kama na wewe unaakili, ondoka kwenye huu mji. Masela wakikukamata, watamlipa Malon kisasi, kupitia mwili wako. Tafadhali usinipigie tena simu wala usinitafute Naya. Nina maisha yangu. Sitaki uniingize matatizoni. Sasa hivi hata usalama wanaangalia. Yeyote anayejihusisha na Malon, wanamkamata. Sasa sitaki uniingize matatizoni. Tulifahamiana kupitia Malon. Malon ameondoka, tafadhali kaa mbali na mimi. Usijaribu hata kukosea kunipigia.” Chezo akakata simu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Naya alibaki amepigwa na butwaa, kama dakika mbili hivi. Akaitazama simu yake kama asiye amini. Baba yake na Bale walikuwa wamesimama hapo kimya. Wakamuona anasimama. “Naombeni msinisindikize nyumbani kwa kina Malon.” Akaongoza njia, wakafuata. Bado ilikuwa mapema tu, asubuhi. Jua kali.

Kwa kina Malon Tena.

Wakapanda tena daladala mpaka nyumbani kwa kina Malon. Walikuta wamekaa tu, siku hiyo ya jumamosi. Baba yake Naya, alitamani kama asingerudi tena kwa yule mzee aliyemuonya kwa wazi kabisa. Lakini hakuwa na jinsi. Ni binti yake wapekee. Alijiambia ni heri apotee au aharibikiwe akiwa anamuona, kuliko kumuacha peke yake.

Walikaribishwa vizuri tu. Tena mama yake Malon akataka wanywe na chai. Naya akakataa. “Nina shida yakuzungumza na nyinyi, niombe msaada.” Baba yake Malon akatulia kabisa, akimsikiliza. Naya akaeleza alipofikia yeye na mwanasheria na pesa zinazohitajika. Na ushauri wa Malon kuwa auze ile nyumba. “Naomba mnisaidie chochote mlicho nacho, nitahangaika kuuza hiyo nyumba kwa kiasi chochote kile, tumuwekee dhamana.” Naya akawaangalia kwa zamu.

“Hata nikiuza suruali zangu zote, siwezi kupata hata robo ya hiyo pesa. Gari alilotununulia Malon, hilo hapo nje, ndio usafiri pekee tulio nao. Mama yake ana matatizo ya miguu. Umri umekwenda, hawezi kukimbizana na daladala tena. Haya, tukisema tuuze hii nyumba aliyo tujengea, wote tutaishia kulala barabarani. Malon sio mtu ambaye utasema atatoka, aanze maisha ya tofauti na aliyozoea kuishi. Mimi ninamjua Malon, ni mwanangu. Atarudia yaleyale, kama sio kesho, basi kesho kutwa atakamatwa tena na polisi. Atafungwa. Hapo tutakuwa hatuna tena gari yakuuza au hata nyumba yakuishi, na  yeye yupo tena jela.” Yule mzee aliongea kwa utulivu tu.

“Naya mwanangu, narudia tena. Huyu Malon unayemuhangaikia, huko aliko, wala sio kugeni kwake. Ni maisha aliyochagua. Mbaya zaidi, amekataa kubadilika. Kukamatwa na kufungwa kwa Malon ndio maisha yake na ndipo pesa yake inapoishia huko. Kuwekewa dhamana na wenzake, kuhonga mapolisi. Kilichobadilika tu ni wazazi wa hapa Morogoro wamechoshwa naye, wameungana, nakuomba msaada kwa vyombo vya usalama vya mpaka Dar-es-Salaam ili tu kumkamata huyo Malon. Ana vilio vya wazazi wengi sana huyo Malon. Anaharibu watoto wakiume na wa kike. Bangi na mapenzi. Wazazi wamechoka. Ndio maana wameamua kumchukulia hatua kubwa zaidi. Sasa hivi kesi ya Malon wamechukua usalama wa taifa, ndio maana unaona hata wenzake wanakimbia. Huko alikofichwa, sio kwa bahati mbaya. Na hata hicho kiwango walichoweka, sio bahati mbaya. Wamekusudia asitoke kabisa. Na hata akitoka, awe amefilisika kabisa.” Naya akatulia kidogo. “Umenielewa mama?” “Nimeelewa.” “Afadhali. Endelea na maisha yako mama. Wewe bado mdogo.” Mzee Saduki akasisitiza na kudhani wapo upande mmoja na Naya.

“Kwa hiyo hamna pesa yeyote ambayo mnaweza kunisaidia? Hata kama nikidogo tu. Sio lazima mkafikia nusu au robo. Chochote mlicho nacho. Naomba mnisadie au hata kama hamna sasa hivi, naomba mtakapo pata, mnipe. Napokea chochote.” Yule baba hakuamini. Akabaki akimtizama Naya.

Naya akamgeukia mama yake Malon. “Tafadhali mama yangu. Naomba uongee na ndugu zake. Chochote kile, mimi napokea. Hata shilingi moja, itanisaidia. Asanteni, naomba sisi tuondoke.” Naya, baba yake na Bale waliondoka hapo kimya kimya, hakuna hata aliyeongeza neno.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~ 

“Tunakwenda wapi tena?” Ikabidi baba yake aulize tena. “Nakwenda kuzungumza na watu wa benki, nione kama watanunua kile kiwanja, sijui nyumba ya Malon au gofu, hata sijui niiteje! Kwa jinsi ileile ilivyo, nione watanipa kiasi gani.” Hakuna aliyejibu, wakafuata nyuma. Walifika wanakaribia kufunga benki. Naya akaingia ofisi za mikopo. Kwa bahati yake mbaya, akakutana na dada ambaye naye alishalizwa yeye na mdogo wake na huyohuyo Malon. “Nakufahamu sana Naya. Tushakusikia na kukuona na huyo Malon. Wala wewe usifikiri ni tofauti na wengine. Malon ni tapeli wa mapenzi na pesa. Hapa benki hakopesheki.” “Sitaki kukopa. Nataka kuona kama benki inaweza kununua.” “Nini?” Yule dada akauliza kwa kejeli. “Lile gofu lake? Wala sio siri, kila mtu amepita pale kuchukua anachotaka. Habari ya kuwa Malon, tatizo la mji ameondolewa mtaani, kila mtu analijua. Na kwa taarifa yako ni furaha na kujibiwa kwa maombi ya kila mmoja wetu hapa Morogoro. Hakuna atakayenunua ile nyumba ya laana. Ile imejengwa kwa vilio vya wengi. Pesa ya laana ya bangi. Anageuza watoto wa watu vichaa ili ajinufaishe yeye.” “Nahisi sio wote wanaoona ni laana.” Akajibu Naya.

“Uliza hapa ndani au nenda hata kwa meneja wa tawi uone kama atakusaidia kununua hiyo nyumba ya laana ya Malon.” “Kwa hiyo kilichokuwa laana pale ni kuta tu. Vingine vyote sio laana? Maana mmechukua mpaka chupi zetu. Sijakuta hata vijiko!” “Naya! Naya!” Bale akamwita. “Simama hapo, twende.” Naya akafyonza. “Wanamsema Malon sasa hivi wakati alikuwa akiwalala na kuwapa pesa, mbona wakati anawahonga wasikatae waseme ni za laana?” Bale akaenda kumshika mkono, akamnyanyua pale kitini kwa nguvu. “Unatukana, na baba anakusikia Naya. Twende.” Naya akaendelea kulia, nakutoka hapo bila yakujibiwa na mtu yeyote pale ofisini. Baba yake akafuata nyuma kimya kimya.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakiwa njiani kurudi Dar, wakamuona anatoa tena simu yake. “Sasa hivi unampigia nani?” “Kuna mama ambaye alizipenda sana zile mashine tulizonunua na Malon. Yeye anatengeneza magauni ya harusi.” “Kwa hiyo!?” “Nataka kumuuzia.” Baba yake alishtuka sana. Akampokonya simu. Naya akashangaa sana. “Baba!” “Tafadhali, tulia kwanza Naya. Vuta pumzi kwa nguvu. Mara tatu tu. Tafadhali Naya. Ukiuza zile mashine ndio utakuwa umeua ndoto zako zote, mama yangu. Tafadhali tulia ufikirie. Mwisho wa yote unataka kukamilisha nini?” Naya akanyamaza. “Naya mama?” “Umeniambia nifikirie baba na umenipokonya simu yangu!” “Tafadhali sana. Jipe muda wakufikiria kabla hujachukua hatua nyingine. Tukifika nyumbani, ukipumzika. Nitakurudishia simu yako.” Naya akavuta pumzi kwa nguvu, akajirudisha nyuma ya kiti vizuri. Akalala.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Hakuomba simu yake wala hakuwa akilia. Usiku huo akasaidia kazi pale nyumbani, wakakaa pale sebuleni kila mtu akapumua. Hapakuwa na kilio usiku huo. Naya akaonekana amekuwa mtulivu, tofauti na walivyotarajia. Akala vizuri, akawa ametulia tu. “Kesho tunakwenda wote kanisani?”  Baba yake akamuuliza taratibu. “Ndiyo.” Naya akakubali. Kila mtu hakuamini.

Na kweli, asubuhi akawa yeye wa kwanza kuamka. Akasaidia kuandaa kifungua kinywa, wote wakala, ndio wakaondoka na hiyo gari ya familia, kuelekea kanisani. Njiani alikuwa ametulia tu, mpaka wakafika kanisani. Walipofika, baba yake akampa simu yake. Naya akacheka taratibu wakati anaipokea. “Sio uanze kupiga simu zako sasa hivi. Tulia ibadani.” Baba yake akatoa onyo. Wakiwa wamesimama palepale, wakaona Ino anaingia getini, na gari yake nzuri sana.

Ukweli mama yake Naya alikuwa akiumia kila alipokuwa akimuona mkewe Ino, mtoto ambaye walishajaliwa. Maisha matulivu yaliyokuwa yakionekana dhahiri kwa familia hiyo ya Ino, alimuhurumia mwanae, nakubaki akijiuliza ni wapi walikosea kwa mtoto huyo ambaye walifikiri walifanya kila kitu mzazi alihitajika kufanya kwa binti yake, lakini akaishia kwa Malon!

Ino, na mkewe wakiwa na katoto kao ka kike, wakawasogelea. Walikuwa wasafi, kwa kuwatizama tu, walionekana wanamafanikio. Msichana aliyemuoa, hakuwa ametokea kwenye kanisa hilo. Walishakuwa na ndoa ya miaka miwili. Ino alioa wakati Naya yupo mwaka wa kwanza chuoni Mzumbe. Naya alionekana wazi amechoka usoni. Wakasalimia. “Mzima Naya? Unaonekana umechoka!” Kama kwaida yake Ino, bila kuficha hisia zake akaanza mara walipowafikia. “Nahangaika kazi Ino. Naomba nisaidie kazi yeyote ile.” “Sasa si vyeti bado havijatoka? Utaajiriwa vipi?” “Ndio maana nimekwambia kazi yeyote ile!” Maongezi hayo wanazungumza wakiwa wamesimama hapo nje ya kanisa, watu wote wakiwasikiliza.

“Ungekuwa unajua kuendesha gari, tungekupa kazi ya kumpeleka mtoto wetu daycare na kumrudisha. Dereva wake ameacha kazi. Na kama unavyojua, mke wangu anafanya kazi world benki. Anatoka alfajiri sana. Kwa kuwa ofisi zao zipo…” “Najua kuendesha gari na ninayo leseni pia.” Naya akamkatisha wakati akiendelea kujigamba hapo, wote wakamgeukia. “Mtanilipa kiasi gani, na saa ngapi mnataka niwe nimefika nyumbani kwenu kumchukua mtoto na kumpeleka huko shule?” “Actually ni some sort of daycare, not shule!” Ino akamsahihisha kwa majigambo. “Popote mnapotaka nimpeleke mtoto wenu, mimi nitampeleka.” Kwa aina ya uongeaji wa Ino, mama yake alijua Naya angekataa.

Ino akamgeukia mkewe. “Eti darling!” Akamuuliza mkewe. Yeye ndiye aliyekuwa amebeba mtoto wao huyo wa kike wa mwaka na miezi michache. Kilikuwa kitoto kizuri, afya nzuri. Wamemvalisha vizuri na kumbana nywele vizuri sana. “Labda tuzungumze halafu tutampigia simu.” Mkewe akajibu. “Kwa nini? Vitu vingine nivyakutolea maamuzi hapo hapo. Wewe unajua unaondoka nyumbani saa ngapi na kurudi saa ngapi! Swala ni unataka awepo hapo ukiwepo wewe au haina haja. Yaani kama unataka kumuona kabla hajamchukua Princess au la. As simple as that! Hatuwezi kufikiria jambo dogo kama hilo, wakati tuna mambo mengi sana yakufikiri.” Naya akajichekea nafsini kwake na kujiambia, “Huyo ndio Ino, bwana!” Akamgeukia mkewe kujua atakachojibu.

“Ni kweli. Labda awepo nyumbani saa moja na nusu. Atakuwa Princess yupo tayari. Na saa kumi jioni utatakiwa uwe umeshafika tena shule, kumchukua na kumrudisha nyumbani.” “Sawa, mama Princess. Natakiwa kuanza lini?” “Kesho.” Akadakia Ino. “Na gari linatakiwa kuwepo wapi wakati Princess yupo hapo kwenye daycare?” “Alipo Princess ndipo linapotakiwa kuwepo gari yake.” Akajibu Ino kwa kiburi kidogo. “Sawa sawa bosi. Kesho saa moja na nusu, nitakuwepo getini kwenu. Au hamna geti?” Naya akauliza kwa uchokozi kidogo. “Lazima kuwe na geti! Ni nyumba gani haina geti?”  Akauliza Ino kwa dharau akishangaa kabisa. “Ya kwetu haina geti.” Bale akamjibu kwa haraka, Zayoni akaanza kucheka. Na Naya naye akacheka. Ino akaondoka, mkewe akafuata nyuma.

          “Bale nyinyi!” Mama yao akataka wanyamaze. “Mpuuzi sana Ino! Anajidai kama anaishi nchi gani sijui! Yeye anapitia wapi kufika hapa kanisani?  Inamaana anakutana na nyumba zenye mageti tupu?”  Wakazidi kucheka wote. “Ni kweli utaenda kuwa dereva wao?” Baba yake akauliza. “Nitaenda. Na kwa jinsi anavyopenda sifa, najua atanilipa vizuri tu ili kunionyesha anazo pesa na nimechezea bahati.” “Alivyo bahili yule, wala usiweke tumaini kubwa.” “Nitatafuta na kitu kingine chakufanya nikishamshusha mtoto wao.” “Umejifunza lini kuendesha?” Mama yake akamuuliza. “Malon mwenyewe alinifundisha. Nilikuwa nikitumia moja ya gari yake wakati nipo kidato cha 5 na sita.” “Acha masihara Naya! Yaani ulikuwa ukienda shuleni kwa gari!?”  Akashangaa sana Bale.

“Alikuwa akinipeleka, au kama ikitokea anataka kulala zaidi siku hiyo, hataki kuamka asubihi sana mida yangu ya kuwahi shule, nilikuwa nikiondoka na gari yake.” “Subiri kwanza Naya. Kumbe ulikuwa ukiishi naye!?” Akauliza mama yake kwa mshangao sana. Naya akagundua ameropoka akainama, bila kujibu. Bale akakohoa huku akimtizama baba yao. Mama yao akashtuka sana. “Usiniambie baba Naya kama wewe ulikuwa ukijua.” “Mimi mwenyewe nimejua jana! Ametuambia jana. Na mimi nilijua alikuwa akiishi hosteli.” “Sasa kwa nini na wewe hukuniambia?” “Ingesaidia nini?” Baba yake akauliza.

“Naombeni twendeni ibadani. Hayo mambo tuyaache kama yalivyo.” “Na huko Morogoro pia ulikuwa ukiishi naye kama mumeo?” Mama yake akauliza kwa ukali. Naya akajisogeza nyuma ya baba yake. “Naombeni twendeni ibadani. Mambo mengine utazungumza na Naya, tukiwa nyumbani. Tena kama utaona kuna umuhimu.” “Ujue baba Naya huyu mtoto unamuharibu wewe!” “Punguza sauti mama. Naya amesoma. Amekuletea vyeti vyote ulivyotaka.” Bale akaingilia. “Sio vyote. Bado cha Chuo.” “Basi kinakuja mama yangu. Sasa hivi tutulie, tukamuabudu Mungu.” “Na mimi natamani kujifunza kuendesha gari.” Akadakia Zayoni. “Hata mimi.” Bale akaongeza. “Nitawafundisha.” Akaitikia Naya akiwa nyuma ya baba yake. Mama yao akaondoka pale kwa hasira. Wakamfuata nyuma.

 

Baada YAKUSHINDWA KUWA MKE, NAYA AWA MFANYAKAZI WA INO.

A

subuhi ya siku ya jumatatu kila mtu alimka na shuguli zake. Mama yake akaenda kazini, kina Bale shuleni, baba yake akampa lifti Naya mpaka nyumbani kwa Ino, yeye akiwa anapeleka maziwa na mayai mjini. Aliwahi kidogo, kwa kuwa alimfahamu Ino, hakutaka shida. Naya akaamua kukaa nje ya nyumba yao, asubirie muda.

Wakati anasubiria, akamtafuta Ozi kwa ujumbe. ‘Ukiamka nipigie.’ Hapo hapo Ozi akapiga. “Niambie mrembo.” “Bado nataka tuuze zile nguo.” Ozi akaanza kucheka. “Unacheka nini sasa?” Naya akamuuliza. “Unavyoringa Naya! Mara useme unamtaka Malon. Malon akifungwa jela, unarudi kwangu!” “Malon ni mpenzi wangu. Wewe nakutaka tufanye wote biashara. Kama unaona huwezi, basi.” “Bado Malon ni mpenzi wako tu!?” “Kwani umesikia amekufa?” “Habari nilizonazo za Malon, hazina tumaini ya kuonekana kwake kwenye uso wa dunia hivi karibuni. Nimesikia amechimbiwa.” “Utafanya kazi na mimi au la?” “Tena dada anatafuta watu wa kazi. Nikutaje tuone kama anaweza kukuajiri? Wewe huwa anakupenda sana. Atakuajiri.” “Basi zungumza naye.” “Lini unaweza kuanza?” “Hata leo.” “Basi nitakujulisha. Ngoja nizungumze naye kwanza. Halafu nitakupigia. Ameanzisha vimiradi vingi. Lazima atakuhitaji tu.” “Nitashukuru Ozi.” Wakaagana. 

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alimkuta Ino akimsubiria na masharti mengi. Juu ya gari  na mwanae. “Tafadhali sana kuwa makini na gari ya Princess na Princess mwenyewe. Hairuhusiwi kula chochote ndani gari yake. Wala kudondosha kitu. Ibakie safi ndani na nje. Kuwa mwangalifu sana humo barabarani na hakikisha umemfunga mkanda Princess wakati wote. Acha gari hapohapo daycare kila unapomshusha. Hakikisha…” Aliendelea Ino, Naya akimtizama tu. “Hivi unanisikiliza lakini?” “Unanipotezea muda Ino. Hayo mambo unarudia rudia, wakati mmesema mtoto anatakiwa kuwepo shuleni saa mbili kamili.” “Nataka umakini, na..” “Ino, hivi ujue unazungumza na mimi Naya? Najua ni nini unataka. Wewe nipe hizo funguo za gari, tuondoke.” Ino akamkabidhi funguo. “Tafadhali kuwa makini Naya.” “Sawa bosi Ino.” Naya akajibu. 

 ~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akamshusha mtoto wao shuleni kwao. Uzuri ilikuwa ni upnde huo huo wa Mbezi walikokuwa wakiishi Ino, ila karibu na Kibamba. Akatafuta sehemu nzuri, akaegesha gari ya watu kama alivyoambiwa, akamtafuta mtu aliyejua atanunu zile mashine. Akampigia simu mwanamke ambaye anashona nguo za harusi. Yule mama akakubali kuchukua zile mashine zote kwa haraka sana. Baada ya kubembelezana bei, akakubali kwenda kuzifuata hizo mashine palepale kiwandani. Swala la usafiri nalo akawa ameua ndege wawili kwa jiwe moja.

Kesho yake yule mama ndio alimwambia atakwenda kuzifuata hizo mashine. Bado pesa ilihitajika. Naya akafikiria kuuza kile kiwanda pia. Aliwaza siku nzima nini chakufanya ili kupata pesa yakumtoa Malon rumande. Mwishowe akakubali kuuza kile kiwanda na kiwanja chake.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya mwezi mmoja akiwa anahangaika kuuza vitu ili kufikisha ile pesa, akapata simu kutoka kwa mama yake Malon. “Umefikia wapi?” “Bado nahangaika mama yangu. Lakini nimefika pazuri. Naamini nitafanikiwa mama yangu. Mnaendeleaje huko?” “Na mimi nilikuwa  nahangaika kuuza mikufu yangu. Sijapata pesa nyingi, lakini naona zitakusogeza.” “Nakushukuru sana mama yangu. Mungu akubariki.” Ikawa Naya ndiye anajiona anawajibila kwa Malon kuliko hata mama yake wakumzaa. “Nikushukuru wewe Naya. Najua kila mtu amemkatia tamaa Malon, lakini nakushukuru kuchukua nafasi yangu.”

“Malon ni mwanangu. Hata nifanyeje, au aweje, nilibeba mwenyewe. Ningetamani Mungu angenipa kiumbe kingine, lakini amekuja Malon. Sijachagua, mama! Na mimi nilipewa hivyo hivyo. Naomba usije ukamuelewa vibaya baba yake. Amehangaika sana na Malon, tokea huyo mtoto anaanza kutamka neno la kwanza. Hatujawahi kupumzika na Malon, mpaka leo.” “Naelewa mama yangu. Naomba nikushukuru kwa kuniunga mkono.” “Pole mama. Mungu akutie nguvu. Nitakurushia hizo pesa.” “Asante mama yangu.” Wakaagana.

Baada ya juma moja, na baba yake Malon naye akamtumia Naya pesa. Akaja na kaka yake Malon. Yeye ndio aliongea, mpaka Naya akamwambia basi. “Nitahangaika kwa njia nyingine. Asante.” “Usione kama nakusimangia! Malon ni tatizo. Hapa imebidi kuhangaika kukopa ndio nimepata hicho kijipesa.” “Asante.” Naya akakata simu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Nini kitaendelea? Baada ya kila mtu kuwa kinyuma na Malon, Naya atafanikiwa kumtoa Malon? Usipitwe..

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment