Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI&pESA! – SEHEMU YA 21. - Naomi Simulizi

MAPENZI&pESA! – SEHEMU YA 21.

Naya Mbele  Ya mshitaki wake, nauongozi wa kampuni.

Walifika na kuambiwa wakae nje, mpaka watakapoitwa. Akaanza kuitwa Naya. “Kila la kheri Naya. Naomba usinichome tu.” “Siwezi Jamal, bosi wangu.” Naya akabeba vitu vyake vyote akaingia navyo ndani. Hofu ikaanza kumuingia baada ya uhalisia. Sura za viongozi wa ngazi za juu kwenye hiyo kampuni ndio alizozikuta hapo kwenye hicho kikao kinachomuhusu yeye kilichoitishwa ndani ya siku moja na Njama, ambapo isivyo kawaida ni ngumu sana kufikia aina hiyo ya viongozi kwa urahisi. Inamaana kuna ratiba zilizovunjwa ili wawepo hapo! Ndipo akaelewa sasa kile Jamal alichokuwa akimwambia Joshua, kuwa jambo limekua kubwa zaidi ya walivyodhania. Na viongozi wote wa kitengo chake cha masoko, yaani waliopo chini ya Joshua walikuwepo kasoro Joshua mwenyewe ambaye aliwakilishwa na Jema. Kila alipozungusha macho kuangalia waliokaa mle ndani ya hicho kikao kinachomuhusu yeye, ndivyo kadiri alivyoelewa kuwa kweli Njama amefanya mambo kuwa makubwa.

“Karibu Naya.” Kiongozi wa nidhamu ndiye aliyemkaribisha. Alikuwa mwanamke ambaye aliogopewa sana hapo kwenye hiyo kampuni. Mkali na mbabe hata kwa kumtizama tu alibeba utisho wa kinidhamu. Alijulikana kwa jina la Mama Masinga. “Unaweza kukaa tu.” Akaongeza. Naya akakaa. “Unajua ni kwa nini upo hapa?” Akaanza Mama Masinga. “Kwa harakaharaka naweza kudhania ni kutokana na barua niliyoambiwa niiandike.” Naya akajibu. “Inaonekana haikuwa na maelezo yakutosheleza.” Naya akatulia akisikiliza. Wote wakamtizama. Naya akajiweka sawa. “Nasikiliza.” “Umesikia kitu nilichokwambia?” Yule mama akauliza kwa ukali kidogo. Jema akabaki akimtizama Naya. “Kwamba maelezo hayakutosheleza?” “Ndiyo. Una lipi la kuongeza kabla hatujafanya maamuzi.” Ikawa kama wanamtisha.

Naya akaweka kijalida chake pale mbele ya meza na kukifungua wote wakimtizama. “Labda kabla sijazungumzia dakika 9 ambazo nimechukua leo nikatoka bila kumuaga Jamal ambaye ndiye kiongozi wangu, mbali na masaa 708 ambayo nimekuwa nikiyatumia hapa kwenye hii kampuni kuzalisha, huku nikiwa nimelipwa masaa 644 tu mpaka sasa bila kulalamika popote, ila kufanya kazi bila kuchoka nikifikiria jinsi ya kuboresha kile mlichoniitia hapa kwenye hii kampuni, naomba nichukue muda mfupi tu kuzungumzia Hili. Naona ni wakati mwafaka kwa kuwa karibu viongozi wa vitengo vyote mpo hapa.” Naya akaanza kwa lugha ya kingereza kile cha kawaida kabisa, kwa kuwa walimpokea kwa lugha ya kingereza, akajua ndio anatakiwa kuzungumza lugha hiyo. Mpaka hapo akawashangaza wote na kuwafanya watulie.

Muda aliotumia kama matron kwenye shule ya watoto wanaozungumza kingereza kitupu mpaka wafanyakazi walitakiwa kuzungumzia lugha hiyo tu, siku hiyo ilimfaa. “Mimi ni mbunifu wa mavazi.” Akaendelea Naya taratibu tu. “Wakati nipo chuoni mwaka wa tatu, katikati ya ubusy wa chuo, pia niliweza kubuni mavazi 29, tofautitofauti kwa size mbalimbali. Nilikusanya watu pale Plaza, nikauza zile nguo  kwa asilimi 85 kwa siku moja tu pamoja na vitu vingine kama sendozi ambazo nilinunua na kuzibuni kuendana na nguo nilizotengeneza. Ninachotaka kusema si kuwaambia juu ya uwezo wangu wakufanya kazi nyingi kwa wakati mmoja, au kuwaambia kipaji nilichonacho, hapana. Nataka kuzungumzia juu ya soko.” Naya akaendelea wote kimya.

“Zile nguo zilirudisha faiza zaidi ya mara mbili ya gharama za uzalishaji. Hapo namaanisha ufundi, vitambaa, umeme mpaka wale warembo waliovaa yale mavazi, nililipa na kuweza kuzalisha hiyo faida. Kivipi! Ndicho ninachotaka kuzungumzia japo najua mngependa kusikia juu ya dakika 9 nilizopoteza leo,” “Mbali na masaa 708 uliyokwisha tumia na kulipwa 644 tu?” Akamalizia Jema. “Asante.” Naya akamshukuru Jema na kuendelea.

“Katika yote niliyofanya wakati nikibuni mavazi, niliwaambia viongozi wangu na ndio kitu nilitakiwa kufanya na Njama leo, lakini kwa dakika 9 tu nilizopoteza, nasikitika nimekosa hiyo nafasi. Lakini kama nilivyosema wakati ule kwenye swala za bidhaa za hapa, ningepata nafasi nyingine ningeweka msisitizo kuwa, kama tunataka tuuze zaidi, na kuweka mabadiliko, tumfikie huyu mtu wa mwisho kabisa, mtumiaji. Siongei kwa nadharia tu, ndivyo nilivyofanya mimi, na ikalipa sana. Na sisemi sicho kinachofanyika hata sasa, ndicho kinachofanyika lakini yapo mambo ambayo ningepata nafasi ya kusema leo ningeyasema, kama siyo nafasi niliyopoteza kwenye dakika 9 za leo,...” “Mbali na masaa 708 uliyokwisha tumia, na kulipwa 644 tu?” Afisa mwajiri mkuu akaongeza, wote wakacheka.

“Kuweka sawa hilo, huwa naingia hapa kazini saa 11:15 asubuhi na nikichelewa sana ni 11:30.” Naya akaongeza. “Muda huyo ninapofika kazini, siji kwa sababu ya mtandao wa bure. Nimekuwa nikifanya uchunguzi. Ningekuwa na nafasi ya kuzungumzia hili, pengine leo ningezungumza na Njama, lakini nimepoteza hiyo nafas...” “Kwa kupoteza dakika 9.” “Asante kwa kukumbuka hilo.” “Mbona ni kama mnafanyia mzaha kitu cha msingi na mnakubali awapoteze malengo?” Njama akalalamika.

“Niliambiwa nizungumze Njama. Tafadhali naomba nimalizie.” Akajibu Naya. “Tulipokuwa Mbeya kikazi, kuna mambo niliyaona juu ya bidhaa zetu. Kama Jamal angeruhusiwa kuingia angekumbuka hili. Tulifanya Survey. Sijui kama zilifanyiwa kazi kiofisi, lakini katika kuwahi kwangu kila siku asubuhi, mimi binafsi, kwa kuamua kwangu, nilifanikiwa kuweka pamoja na kutengenezea kama maelezo, nikalinganisha na mazungumzo niliyozungumza na wenyeji wa pale.” “Naomba na mimi Naya hiyo ripoti uliyotengeneza kutokana na Survey mliyofanya Mbeya, nimpelekee Kumu, mkuu wa kitengo.” Jema akasimama kabisa. “Hapa ninayo nakala moja tu, naomba nije kukutumia baadaye nikishazungumza na Jamal, au kama ni sawa, naomba Jamal akaribishwe wakati nikizungumza. Akiidhinisha, nitaituma mara nitakapofika kwenye meza. Tafadhali Jema, ili isiwe namruka yeye aliyekuwa amenituma hiyo kazi.” Watu wote wakakubaliana. Jamal akaitwa.

Aliingia akiwa amekunja uso. “Kwema?” “Nilikuwa nikizungumzia ile survey uliyotaka tufanye ulipotutuma Mbeya.” Naya akamjibu kwa kiswahili kama alivyoingia na kuzungumza kiswahili. Jamal akaonyesha hakumbuki kabisa. “Niliifanyia kazi kama ulivyonituma, ndio naizungumzia.” Jamal akakaa kwa wasiwasi. “Katika watu 98 ambao nilifanikiwa kupitia karatasi zilizotumika kwa survey, kwa kuwa zilikuwa karatasi 100, tukahakikisha tunapata hao watu 100, lakini kwa bahati mbaya mpaka sasa tunazo 98 tu. Wote. Nikisema wote, namaanisha watu 98 wote walisifia ubora wa bidhaa zinazotengenezwa na kiwanda chetu. Ila wote walilalamikia vitu viwili.” “Nini?” Ghafla wote wakawa na shauku ya kutaka kujua. Jamal kimya.

“Ipo kwenye hii ripoti. Nafikiri Jamal atawakilisha baada ya kupitia na kuridhika, maana nilitaka kukamilisha kila kitu, ili ninapomkabidhi, asipatwe na maswali.” “Lakini unaweza kuzungumza kwa kifupi tu.” Msaidizi wa CEO akaonekana na shauku kubwa zaidi. Naya akamtizama Jamal. Jamal akaonekana kuridhia. “Okay. Naona bosi wangu ameniamini naweza kusema.” Naya akazungumza akiwa ametulia mpaka Jema akafurahi maana aliweza kuvuta wote na kuweza kumsikiliza kwa shauku kubwa, tena si kama mkosaji ila mtu mwenye manufaa makubwa.

 “Tatizo ilikuwa ni bei na upatikanaji wa ile bidhaa kwa urahisi.” Wote wakatulia. “Najua kwa upande wa bei mliyopanga, nikutokana na uzalishaji wa hapa ili kupatikanika kwa faida. Usambazaji je?” Naya akauliza. “Na je, endapo mkipata njia rahisi ya kushusha gharama ya uzalishaji kama nilivyowaambia mimi nilifanya, nikaweza kuzalisha zaidi ya mara mbili? Ipo njia. Na mbali na hapo katika hayo masaa..” “708 .” Akadakia Afisa Mwajiri nakufanya wote wacheke kasoro Jamal ambaye hakuwa anaelewa na Njama mleta kesi. “Ndiyo. Katika hayo masaa 708 niliyokuwa nikiwahi hapa kazini, nimejaribu kufanya utafiti nikilinganisha na uzoefu wangu wa masoko wa nini kifanyike ili kufikia mtumiaji kwa urahisi, nafuu na kwa haraka. Hiyo inaongezwa na ufahamu nilioupata kutoka kwenye nchi za wenzetu pia.”  Naya akawa kama amemaliza.

“Mbona kama umemaliza tena!?” Wote wakawa wamehamasika wanataka kujua zaidi. “Hapana. Naomba nimalizie kwa kurudi kwenye zile dakika 9 zilizogharimu kampuni kutopata mchango wangu leo kupitia kiongozi Njama. Niombe radhi kwanza kwa Jamal ambaye ndiye naripoti kwake. Nilikosea kutoka bila kumuaga, kwa kuwa nilipata dharula. Ubaya wa dharula ni mmoja tu, kuwa ni dharula. Samahani sana Jamal kwa kukufikisha hapa. Jamal ananiheshimu mno na ananiamini. Leo najisikia kumdhalilisha. Na samahanini sana kuwapotezea muda watu kama nyinyi ambao mna majukumu mazito na kuwepo hapa kuzungumzia hizo dakika 9 nilizopoteza leo na si hayo msaa..” “708?” “Hapana, msaa 644 ambayo mmekwisha nilipa.” Naya akamrekebisha huyo mama ambaye watu walimuogopa sana. Akatulia akiwatizama kwamba ameshamaliza walichomwitia.

“Tunaweza kupata kwa ufupi tu suluhu uliyopata kutokana na survey uliyofanya mkoani Mbeya, uzoefu wa biashara ulionao na uliyoona wakifanya wenzetu huko nchi za ugenini?” “Ningependa kufanya hivyo, lakini najihisi nitakuwa navuka mipaka na ninakuwa mtu wa mambo nusunusu kwa kuwa hata wazo la kwanza ambalo nililichangia siku ya ijumaa, nimepoteza nafasi ya kukamilisha kwa dakika 9 nilizopoteza. Kingine nafikiri nawajibika kwenye idara yangu kwanza kabla ya watu wengine.” “Unamaanisha mpaka ukazungumze na Joshua? Akupe kitu gani chakufanya au kusema ndipo uje uzungumze?” Njama akauliza. Watu wote wakamgeukia Njama.

“Nyinyi hamumsikii Joshua akiongea hapa kupitia mdomo wake huyu!?” Njama akajitetea, wote kimya. “Hapo anayezungumza ni Joshua, wala si yeye na ndio maana mnaona hataki kuongea zaidi mpaka akaulize tena. Joshua anampa mawazo ili tu mumuajiri.” Naya akafunga mafaili yake, akamtizama Mama Masinga aliyemkaribisha tokea mwanzo. Wote kimya maana ni kama Njama alitupa shutuma na Naya hakutaka kujibu.

“Si mnaona anashindwa hata kukataa! Kwa kuwa anajua ni kweli. Joshua anamwambia nini chakuja kuzungumza, ndio maana mnamuona ni jeuri.” Njama akaendelea. “Anataka kuendesha kitengo vile atakavyo kwa kuwa anatembea na Joshua. Kampuni haiwezi kuendeshwa hivyo kimapenzi.” Njama akaongea tena kwa kingereza vizuri tu, wakati Naya alimalizia kwa kiswahili baada ya kuingia tu Jamal. “Una chochote cha kujibu Naya?” “Juu ya nini?” Naya akamuuliza Mama Masinga kwa nidhamu, akiwa ametulia tu. “Samahani sijasikia swali ninalotakiwa kujibu.” “Anachozungumzia Njama.” Mama Masinga akawa kama anamkaribisha tena. Ila safari hii kwa utulivu.

“Ofisini kwetu nafikiri kuna kamera kama sikosei, au Jamal kiongozi wangu yupo hapa atawaambia. Nisingeacha kuzalisha nyumbani kwetu, na kuja kupoteza hapa masaa 708 yenye ushahidi na nilichozalisha, kama akili zangu zingekuwa kwenye maneno matupu. Muulizeni Jamal. Mimi si mtu wa kupoteza muda au kunikuta katikati ya maneno mengi. Kwa heshima yenu, naomba msitake leo nianze kuzungumzia majungu. Hizo ni shutuma zake. Mnayo haki yakumsikiliza na kuamua. Lakini mimi huwa masikio yangu hayaelekei kwenye maneno maneno. Lasivyo nisingefika hapa nilipo sasa hivi. Mkitaka nizungumzie kile mlichoniamini nacho mpaka kunipa hii kazi, ningependa na nipo tayari. Lakini si maneno ya uzushi, yakufikirika tu. Tutajikuta tunapoteza muda mwingi sana hapa, na wote tunakwama kwenye ulalamishi bila kutimiza kusudi lililotuweka hapa. Kwa heshima kabisa, viongozi wangu, naomba niishie hapa.” Chumba kizima kimya.

Lakini baada ya muda wakamsikia Jamal akicheka taratibu. “Unakumbuka nilikufuata Mkubwa, nikakuomba katika kundi la kwanza na la pili tuliowapa kazi, tumpe ajira mmoja wao, mkanikatalia mkisaidiwa na Njama kuwa mpaka mjiridhishe?” Jamal akamuuliza HR, Afisa Mwajiri kiongozi, tena akamuuliza kwa kujiamini kabisa. Kimya. “Basi kama huwa mnanisikia nikisema jembe langu, ndiyo huyu Naya. Ndio maana japokuwa walikuwa peke yao, niliwatuma mkoani Mbeya, nikijua safari hii kazi itafanyika. Nikamwambia hata Njama, kama atabisha, aseme leo, kuwa, nimetuma jembe langu kule, sina shida. Nitakwenda kufunga tu. Awe mkweli kama wakati ule huyu mtoto alikuwa ameshaanzana na Kumu.” “BADO.” Akadakia Jema kwa haraka.

“Basi ndio mjue hichi ni kichwa bila Joshua.” Akaongeza Jamal kwa kujivuna haswa. “Na ndio maana Joshua hakutaka kuwepo hapa kwenye hiki kikao yeye kama mkuu wa kitengo ili kufanya msishindwe kuzungumza. Lakini siku ile ya kikao, Joshua hata hakuwa akijua kama Naya alikuwepo bado hapa ofisini. Bisha Njama.” Jema akaongeza. “Mnafiki tu wewe Jema, unataka Joshua akusogeze karibu zaidi.” “Umekasirika tu Njama na kusahau! Kumbuka mpaka Joshua akauliza kwa kulalamika kwa Jamal ni kwa nini anamjazia Naya kazi mida ya jioni wakati yeye ndio anafika hapa kazini wakwanza! Tena akamuita ili aje amsubirie! Sasa alimpa saa ngapi jibu la kuja kwenye kikao ambacho hata Naya hakuwa muhudhuriaji?” Wakaanza kubishana wao wenyewe wenye kitengo cha masoko mpaka viongozi wengine wa idara hiyo ya masoko wakitetea kwamba ni kweli siku ile Naya alipotoa mchango hakuwa amepangwa na Joshua. Alishitukizwa na kuwashangaza na wao kama siku hiyo hapo kikaoni. Ndipo Jamal na Jema, wakapata nguvu na kumshambulia Njama. Naya kimya ametulia tuli.

Katikati ya huo mzozo, Naya akaruhusiwa kuondoka. Akasimama na kumsogelea Jamal. “Zimebakia dakika chache tutoke, sijisikii vizuri, naomba nikapumzike. Kisha utanijulisha mwafaka.” Akamnong’oneza Jamal. “Pole sana. Wewe nenda kapumzike, nitakujulisha.” “Asante.” Akageukia wengine. “Asanteni sana na samahanini kwa usumbufu wote niliosababisha.” “Hakuna tatizo Naya. Wewe endelea na kazi. Tunachotaka ni uchapakazi na inaonekana Jamal anakutegemea sana. Tutajipanga vizuri ili kuweka mazingira mazuri ya wewe kufanya kazi.” Akajibu Afisa Mwajiri wao mkuu. “Asante sana.” Ukweli kichwa kilikuwa kikimuuma sana Naya, halafu katikati ya kikao tumbo nalo likaanza kumuuma. Na akakumbuka hana usafiri ni kwenda kuwahi daladala. Hata hakugeuka nyuma, akatoka kuwahi daladala kabla fujo za watoka kazini hazijaanza.

Kwa Naya.

Kichwa kilikuwa kikimuuma kwa kulia siku hiyo na sababu ya hofu, Naya akaanzwa na siku zake akiwa njiani. Akampigia simu baba yake. “Naumwa sana, mimi sijui kama nitafika nyumbani.” Baba yake akajua tayari hilo juma limeshaharibika. “Unataka nikufuate wapi?” “Nipo kwenye daladala, nimesimama. Tumbo linauma, kichwa kinagonga karibu kupasuka. Mimi naumwa baba, sijui kama nitakuona tena!” Naya akaendelea kulia taratibu kwa sauti ya chini watu wengine kwenye daladala wasimsikie. “Utanikuta kituoni nikikusubiri. Nakuombea ufike salama. Tulia kabisa. Maana unajua ukilia na kichwa kitazidi kuuma.” “Nasikia na kutapika. Nimezidiwa.” “Pole mama. Pole sana mama mzazi.” “Heri nikukute tu kituoni lasivyo sitaweza kufika nyumbani.” “Nimeshaanza kutafuta viatu ili nisogee kituoni.” Hapo Naya akaridhika. Ndipo akakata simu na kurudisha mfukoni.

Kikaoni.

Huku nyuma kikaoni kukaendelea kutupiana maneno. Jamal anatetea kazi yake huku Naya naye anatetewa na yeye Jamal, Jema pamoja na viongozi wengine walioweza kubishana zaidi waliokuwepo kikao cha kwanza Naya alipotoa wazo. Halafu sasa Naya mwenyewe akawa ameacha jina tofauti na walivyotegemea. Naya waliyemuhoji anajiamini na anajua kazi yake. Kubishana kukaendelea, ikageuka ugomvi sasa. Ugomvi nao ukaendelea, ikawa tena lawama.

Mwishoe ikabidi msaidizi wa CEO aulize wanaweza vipi kupitisha hata mwezi bila kumuajiri mtu kama Naya! Ambaye anaonekana atasaidia kampuni! “Hana lolote huyo, ni Joshua tu ndiye anayezungumza.” Njama akapinga. “Sasa kuna shida gani ya kutumia Joshua Kumu wawili, tena kwa wakati mmoja, kwa kazi tofautitofauti, halafu kwa bei nafuu!?” Akauliza yule msaidizi wa CEO na kufunga wote mdomo.

Maana Jamal na Jema walikuwa wakitetea ni akili ya Naya mwenyewe, Njama anapinga ndipo akauliza tatizo lipo wapi na kunyamazisha wote. “Maana hebu tufikirie kwa pamoja tukiwa tu tumetulia. Je, Joshua ameshindwa kufanya kazi yake?” Akauliza. Wote kimya. Hakuna anayeweza kumgusa Joshua Kumu kwa utisho alioweka hapo kwenye hiyo kampuni. “Kwa ukimya huo inamaana jibu ni hapana. Au sivyo Njama?” Wote wakamgeukia yeye. “Sema sasa Njama. Unatatizo na Joshua?” Jema akamuuliza kwa kumsuta. “Mimi sijasema ninatatizo na...” “Kwa maana nyingine jibu ni hapana.” “Kwa nini unanikata?” “Ushatupotezea muda mwingi sana Njama. Siku ya leo umeiharibu vibaya sana kwa kutokuwa mwanaume wakuweza kupokea jibu la ‘hapana’.” Hapo pakalipuka ugomvi mwingine.

“Mimi sijawahi kumtaka Naya, ila Naya mwenyewe ndiye aliyenitongoza nikamkataa.” Hapo napo Jamal na Jema wakambadilikia kwa kelele kubwa mno. Watu wazima hao na majukumu yao wakageuka kama wasio na kazi, wasutanaji. “Naya aliona mimi sina mpango naye ndio akajisogeza kwa Joshua. Lengo lake...” Wakaanza kumcheka, ghafla yeye Njama ndio akageuka kichekesho pale.

“Binafsi naomba kukutahadharisha kabla sijaondoka, Njama.” Mama Masinga akafanya wote watulie. “Huko unako kwenda, kama hujachelewa, nashauri rudi kwa haraka.” “Sikukwambia mimi Njama? Nilikuonya wewe.” Jema akaingilia. “Unafanya mchezo wa hatari sana ambao unaanza kukugharimu. Sijui kama unanielewa Njama?” “Mbona kama umeshaamua kuwa upande wa ....” “Upi Njama?” Mama Masinga akauliza kwa ukali kabisa.

“Wote mnanijua mimi sina ninayemuogopa hapa, ila kusema kweli. Na ndicho ninachokwambia. Unashika maeneo na watu hatari sana, itakugharimu wewe mwenyewe. Unanielewa Njama?” Akauliza kwa ukali zaidi. “Sikutishi, ila nakutaarifu tu. Wote tumeajiriwa hapa. Lakini wapo ambao wameshika hii kampuni. Ajira zao zipo kwa wino usiofutika kwa urahisi, wengine tumeandikwa kwa penseli tu. Kufutika kwetu ni rahisi sana. Hawa waajiriwa wa aina ya kwanza hawa, bila wao mambo hayaendi hapa. Na kampuni inalipa gharama kubwa sana kuhakikisha kila siku ya asubuhi, wanajulikana kama ni wafanyakazi wa hii kampuni. Halafu hawa wezangu na mimi hawa ambao ajira zetu zipo kwa maandishi ya penseli, hata tusipokuwepo hapa, hakuna anayejali au kuona utofauti. Sijui kama unanielewa?” Yule mama akauliza kwa ukali zaidi. Jamal na Jema wakaanza kucheka taratibu.

“Gharama ya kuwepo kwao kwenye hii kampuni haiangalii mtu yeyote, ila wao tu. Na wapo watu wanawekwa maalumu, kwa ajili yao tu. Wanaweza kuwa hata watano ila lengo ni mtu mmoja tu. Unanisikiliza Njama?” Kimya. “Ukitoka wewe hapa, ukaenda kutafuta kazi sehemu nyingine, bado watapiga simu kuulizia ulikuwa mtu wa namna gani hapa kazini. Unataka kuharibu maisha yako kwa dakika 9 tu ambazo ninauhakika hata wewe huwa unafanya kama alichokifanya huyu binti! Leo unafanya haya yote kwa mtu unayejua kabisa ni muhimu sana kwa Jamal!” Akamshangaa kwa hasira kabisa.

“Acha Njama. Kama hujaharibu bado kiti unachotakiwa kukalia kesho ukirudi kazini, nashauri tengeneza. Unanielewa Njama?” Aliuliza lakini kila mtu alijua anachomaanisha. “Nafasi yako ilitengenezwa Njama! Usisahau hilo.” Afisa Mwajiri mkuu akaingilia. “Binafsi niliipinga kabisa hiyo nafasi yako, sikuona sababu, lakini Joshua aliing’ang’ania mpaka ikakubaliwa  kwa sababu yeye ndiye aliyeitaka na kutaka wewe uwepo ili wewe usimamie utendaji, Jema mawasiliano upande huo wa masoko.” Huyo Afisa Mwajiri ikabidi aweke wazi kabisa, wote kimya. Mama Masinga akasikitika kwa sauti. “Hivi unaelewa unapoambiwa unacheza mchezo hatari, Njama?” Akamuuliza. Njama kimya. “Hawa vijana hawakumbuku wanakotoka! Ila ukumbuke nimekuonya Njama.” Mama Masinga akakusanya vitu vyake.

“Binafsi sioni kesi yakuendelea kupoteza muda hapa. Kama unatatizo jingine, utafuate njia kama ulizofuata leo. Tutakuja tena kukusikiliza. Ni haki yako.” Akamgeukia Afisa Mwajiri. “Kama na nyinyi hamjachelewa, nafikiri mnahitaji mtu kama Naya kwenye ofisi hiyo ambayo Jamal amekuwa akilia wakati wote hapati watu wa kueleweka. Yule binti anajielewa. Wakimkamata kampuni nyingine, mjue sisi tumekula hasara.” Yule Mama Masinga akaondoka. Ikaanza mipango juu ya Naya. 

Kwa Joshua.

Tayari ilikuwa saa 12 jioni wakati Jema anarudi ofisini na kumkabidhi Joshua rekodi nzima ya kile kikao. “Naya yupo na hali gani?” Hilo likawa swali la kwanza hata kabla hajafungua hiyo rikodi kusikiliza. “Alitoka pale, nilimsikia akimuomba Jamal  ruhusa aondoke, hajisikii vizuri.” “Kwa hiyo muda wote huo hakuwepo kwenye kikao?!” “Aliondoka, lakini Joshua!” Joshua alishasimama. “Nini?” “Yule mtoto ni kichwa kilichokamilika! Halafu kumbe anajua kuzungumza lugha ya kingereza vizuri bwana!” Joshua akamtizama na kuanza kumpigia simu Naya. Ikaita bila hata kupokelewa. “Habari imegeuka, sasa hivi wanataka kumuajiri.” Joshua akamtizama na kurudisha macho kwenye simu. “Naomba tuzungumze kesho Jema. Natoka.” “Kila kitu nimerikodi. Utasikiliza kwa wakati wako.” Joshua akatoka kama anayewahi.

Muda wote alikuwa akimsubiria Naya atoke kikaoni amrudishe nyumbani akijua baba yake amejua kuwa yeye ndiye amemwambia arudishe gari kwa Malon. Alishaagiza gari yake iletwe kutoka nyumbani, akijua Naya akitoka kwenye kikao, atarudisha yeye mwenyewe nyumbani kwao asijue Naya alishatoka. Joshua akajaribu kumpigia tena lakini pia haikupokelewa. Akaingia garini na kutoka kuelekea nyumbani kwa kina Naya ili kumwangalia huku akihukumiwa moyoni na kushindwa hata kusikiliza rikodi aliyopewa na Jema.

Kiluvya.

Alifika kwa kina Naya giza lilishaingia kabisa. Zayoni ndiye aliyemfungulia geti. Akafunga na kumfuata. “Karibu.” Joshua naye ndio alikuwa akishuka garini. “Tumeanza kufunga geti muda wote kwa kuwa Naya hana tena gari.” Akaanza Zayoni. “Ulikaa sana getini?” “Hapana Zayoni. Nimepiga honi mara mbili tu.” “Basi sikukusikia mara ya kwanza. Baba ndio alinituma nitoke niangalie ili tusimuamshe Naya.” “Naya ameshalala?” “Amerudi akilia anasema anaumwa. Alikuwa akitapika kwa muda mrefu tokea atoke kazini, lakini ametulia. Naya akiwepo baba hazidiwi. Baba asingekuwepo huwa anazidiwa sana. Atapona. Baba alikuwa naye chumbani kwake, anasema na kichwa pia kinamuuma sana. Ila amelala sasa hivi.” “Poleni sana.”

“Ila kwa kuwa baba yupo, atakuwa sawa tu. Hata nilipompigia simu Bale kumwambia Naya amerudi nyubani analia, akaniuliza kama baba yupo. Nilipomwambia baba alikwenda kumpokea kituoni, akasema nisiwe na wasiwasi, kwa kuwa baba yupo, atapona tu.” Zayoni mkimya lakini mzungumzaji haswa akiamua.

“Ujue Naya akiwa anaumwa, ukitaka apone haraka, sio dawa. Hata mama alikuwa anajua. Akiumwa yeye, baba awepo. Hapo hata ukimpa dawa zinafanya kazi. Ila kama baba hayupo, hata ukimpa dawa zinakuwa hazimsaidii. Anazidiwa kabisa mpaka mnampeleka hospitalini. Baba akija tu, akikaa naye kidogo, anapona. Kwa hiyo atapona.” “Naamini hivyo.” Joshua akajibu maana hata ndani hakuwa amekaribishwa, Zayoni alikuwa akizungumza tu hapo. “Naya..” Kabla hajaongea jingine baba yake akatoka. “Kwa nini humkaribishi mgeni ndani?” “Nilikuwa namwambia Naya anaumwa.” “Hayo unamwambia akiwa ameshaingia ndani, Zayoni!” “Hamna shida kabisa mzee wangu. Shikamoo.” Joshua akasogea mpaka pale mlangoni.

“Marahaba. Karibu ndani.” Wote wakaingia ndani. “Sikujua kama Naya alishaondoka! Nilikuwa nikimsubiri nimrudishe nyumbani!” Joshua akawa kama anajitetea. “Ameniambia imebidi arudi alianza kuumwa katikati ya kikao walichokuwa wamemwita huko kazini kwenu. Lakini atakuwa sawa tu.” “Au tumpeleke hospitalini?” “Hapana. Atakuwa sawa tu. Amelala muda si mrefu, baada ya kumeza tena dawa. Za mara ya kwanza alitapika, naona hizi za pili zimekaa tumboni.” “Au ni malaria?” “Hapana. Ana miezi yake huwa anakuwa hivyo. Atakuwa sawa tu. Anahitaji kupumzika tu. Nafikiri pia amelia sana leo. Kesho atakuja tu kazini.” Joshua akabaki ametulia lakini akawa ameelewa kinachomsumbua Naya mbali na kichwa.

“Ni sawa nikienda kumuona?” “Acha Zayoni akuonyeshe chumbani kwake.” Zayoni akaongoza njia, Joshua akafuata mpaka alipoonyeshwa mlangoni, Joshua akaingia, Zayoni akaondoka. Akaenda mpaka pale kitandani. Akakuta amewekewa taulo kichwani. Akajua ni baba yake tu. Akabaki akimwangalia. Mwishoe akaamua kukaa pembeni ya kitanda. Akamtoa kitambaa na kumshika kichwa. Kikawa baridi tu. Akamkausha usoni vizuri akamvuta tena shuka kumfunika. Akamvuta mkono wake uliokuwepo karibu. Akaubusu kama mara mbili, Naya akageuka. Uzuri akageuka upande aliokuwa amekaa. Akaupakata ule mkono na kupishanisha vidole akabaki ametulia.

Joshua alijawa hukumu kujua Naya alifika kwao na daladala, tena akiwa anaumwa, na baba yake ndiye aliyekwenda kumpokea! Akajisikia vibaya, akatamani hata angezungumza na Naya mwenyewe, lakini akaambiwa Naya alikuwa akitapika, kichwa kilikuwa kikimuuma, ndio amelala. Hawezi kumuamsha. Akabaki amekaa pale amemshikilia mkono, Naya amelala hana habari. “Njama ameniharibia siku yangu nzima ya leo!” Akalaumu mawazoni na kuchukia kabisa. Akaona huo ndio muda muafaka wakusikilizakiliza kilichokuwa kikiendelea kikaoni.

Akaunganisha ile rikodi na bluetooth yake sikioni, akaanza kusikiliza kwa kupitia bluetooth ili asimwamshe. Akaendelea kusikiliza huku akimwangalia Naya na kucheka taratibu bila kujijua kwa furaha ya ushindi. Akajisifu kila alipokuwa akimsikiliza Naya. Akarudia kipengele cha Naya tena wakati akizungumza huku akizidi kujawa furaha. “That’s my girl!”  Akashabikia nafsi mwake. Alipomsikia Njama ametupa shutuma na kusikiliza jibu la Naya, akazidi kufurahia. “That’s what am talking about!” Akamsifia huku akimwangalia. “Kweli Mungu umenipa wa kufanana na mimi. Mfupa kutoka kwenye mfupa wangu na nyama kutoka kwenye nyama zangu.” Akapata nafasi ya kumshukuru Mungu wake huku akimwangalia Naya kwa kumpenda zaidi.

Akasikiliza ile rikodi mpaka mwisho kabisa na majibu ya wote waliokuwepo kwenye kikao. Akajua Njama ameshindwa, na bado hajapoteza heshima hata kwa viongozi wenzake wa ngazi za juu. Bado wanamtambua kama yeye ni kiungo muhimu sana kwenye hiyo kampuni. “Well!”  Akaanza tena Joshua kuzungumza na Mungu wake. “Umenguruma tena Baba yangu. Nashukuru hata kwa hili jema jingine unalokusudia litendeke kwenye hili pia. Asante Mungu wangu kwa kuwa hata sasa bado unatembea na mimi. Na bado unaendelea kudhihirisha uwezo wako mbele za wanadamu. Nipo tayari kupokea na uniongoze kule utakap...”  Wakati anaendelea kuomba akasikia Naya amevuta mkono wake, ikabidi kufungua macho. Akamuona kama anayeugulia maumivu usingizini.

Machozi yakaanza kumtoka akiwa usingizini bila kufungua macho. Akageuka upande wa pili akiwa ameshika tumbo. “Baba!”  Akaanza kwa sauti ya chini. Kisha akaita tena kwa sauti akiwa amegeukia ukutani. “Babaa!” “Naya!” Joshua akamwita taratibu. Akatulia kama aliyehisi amesikia akiitwa lakini kabla hajaelewa, baba yake akaingia kama aliyekuwa akisubiria mlangoni. Joshua akasimama kwa haraka kama mshale utafikiri mtoto aliyevunja kikombe, anamkimbia mama yake asimkute kwenye tukio, anajihami. “Vipi mama?” “Tumbo linaniuma mpaka nimetoka usingizini! Nifanyaje baba? Au nimpigie tu nimuulize?” Akalalamika Naya akiwa amelala akifinya tumbo nakushindwa kugeuka. “Pole Naya.” Joshua alimfanya Naya kushituka mpaka akakaa.

“Joshua!?” “Pole sana.” Naya akawa kama haamini. Akamwangalia baba yake, baba yake akamsogelea. “Pole sana.” “Asante.” Akavuta mkono wa baba yake akauegemea kwa upendo akatulia. “Kwani mara ya mwisho ulimpa dawa gani?” Joshua akauliza. “Za maumivu tu za kawaida. Ila kipindi mama yake alipokuwepo, baada ya Malon ambaye huwa anajua hizo dawa ambazo hata mwenyewe Naya anasema hazijui, ilikuwa likimuanza, anampeleka kwa rafiki yake kwenye dispensari fulani pale Mbezi, wanamchoma sindano fulani hivi. Inamsaidia kutulia. Lakini yule nesi naye aliacha kazi pale, mama anayejua hiyo dawa aliyokuwa akichomwa hayupo na hataki tumuulize Malon ni dawa gani alizokuwa akimpa, anasema zilikuwa zikimsaidia sana.” Joshua akamwangalia Naya alivyokuwa amejiegemeza kwenye mkono wa baba yake amefunga macho akilia maumivu bila yakutoa sauti ila machozi kumtoka.

“Napo sio kwamba ndio kila mwezi anakuwa hivi! Hapana. Sio kitu cha kila siku ndio maana naona hata mimi unaona nimeshindwa kushika hayo matibabu. Naweza kusema ni tokea kifo cha mama yake. Wakati ule wa msiba aliiugua hivihivi, lakini tokea apone, hajaugua tena ndio linarudia tena leo! Sasa inakuwa kama linakuja akipatwa na mshituko mkali, ndio hayo maumivu na mengine yote yanakuja kwa pamoja.” “Pole sana Naya.” “Asante, lakini nitakuwa sawa tu.” “Unataka twende hospitalini?” Joshua akamuuliza kwa upendo. Naya akabaki kama akifikiria kisha akamwangalia baba yake. “Wewe unataka nini?” Baba yake akamuuliza. “Sitaki kwenda wasije kunipa madawa ambayo siyo nikawa napoteza tu muda.” “Basi tumpigie Malon, tumuulize alikuwa akikupa nini, na sisi tukanunue kwa haraka.” Naya akamwangalia vizuri Joshua kama hajamuelewa.

“Ni sawa?” “Malon ameniudhi sana leo. Ningefukuzwa kazi kwa sababu yake na ungekuwa sio wewe ni mtu mwingine mwenye akili za kijinga, pengine usingetaka hata kuja kuniona tena! Sitaki kumuona kwa sasa. Acha tu nivumilie. Maana mimi namjua Malon, akijua kuwa naumwa, atajaa hapa na dawa zake na yeye mwenyewe na hatakubali kuondoka humu ndani.”  Akalalamika Naya. 

“Kama hivi anakuwa ametulia kabisa huko. Anasubiri nimtafute. Nikimtafuta tu, ndipo anakuwa mwingi mpaka amenigharimu sana leo kama vile hakuwa akijua kama nafanya kazi pale, leo ndio amejua na kunifuata! Heri nimuache tu nitumie dawa alizonipa baba.” “Basi naomba tujaribu kwenda hospitali Naya. Mimi nitakuwepo na nitaulizia matibabu wanayotaka kukupa au watakayokupa na nitahakikisha nayajua ili wakati mwingine tujue ni nini chakukupa.”

Naya akaanza kulia. “Mimi naona ni kama nakusumbua tu Joshua! Acha baba anipe dawa zake, nitakuwa sawa.” Joshua akarudi kukaa. Akamvuta mkono ambao haukuwa umeshikilia mkono wa baba yake na kuubusu pale mbele ya baba yake. “Nipo hapa kwa ajili yako Naya. Siwezi kuondoka mpaka nijue upo sawa. Sina ninapokwenda, sina ninakowahi, wewe unajua. Nisipokuwa masikioni na wewe kupitia simu, unajua nakuwa peke yangu nyumbani. Hapa nipo sehemu sahihi na muda sahihi. Hunisumbui hata kidogo. Sawa?” Naya akatingisha kichwa kukubali. “Lakini kama limeanza kutulia!” Akaonekana kusita tena.

Wakatulia kidogo, ni kama Joshua akawa anasita kuzungumza chochote mbele ya baba Naya. Baba Naya akagundua na kukumbuka huyo sio Malon asiyeweza kusubiri anapotaka kuzungumza jambo lake. Liwe la hasira au heri. Atalizungumza tu. Hajui kujizuia anaongea chochote, popote mbele ya yeyeote. Joshua yupo makini na maneno yake. Akatoka kuwapa nafasi.

“Njoo.” Joshua akamwita kwa upendo, Naya akamsogelea. “Jilaze hapa. Likirudia tena, tunakwenda hospitalini. Sawa?” Naya akajilaza hapo alipoambiwa na Joshua. Akamuwekea mto chini ya tumbo, kichwa akajilaza miguu kwa Joshua kama aliyekipakata, akaanza kumsugua mgongoni. “Nimefurahi kukuona Joshua.” Joshua akacheka taratibu. “Kwa nini hukuniambia?” “Nilijua unamajukumu mengine. Halafu kulizuka ugomvi mle ndani ikachukua muda mrefu, nilitoka muda wa kazi unakaribia kuisha kabisa, nikajua na wewe utakuwa ulishaondoka au upo na majukumu mengine. Tumbo nalo likaanza kuuma katikati ya kikao, nikajiwa na hali ya kutapika. Nikaona heri niwahi kurudi kwa baba.” “Pole sana Naya. Lakini mimi nilikuwepo ofisini kwangu. Nilikuwa nikikusubiri nikurudishe nyumbani. Nisingeweza kuondoka na kukuacha katikati ya ile kesi.” Ikamgusa sana Naya.

Akageuka na kumwangalia. Joshua akamfuta machozi. “Nakupenda sana Naya. Sana. Shida yako ni yangu.” “Sikujua kwa umbali huo Joshua. Asante pia kwa kuniamini. Niliingiwa hofu habari zilipoenea kuwa Malon alikuja, na nikaenda kuzungumza naye nje!” Joshua akacheka taratibu na kumfuta tena machozi. “Huwa sikubali kuchindwa kirahisi hivyo.” Naya akacheka taratibu. “Hujamjua Malon wewe!” “Na kwa kuwa na wewe hujanijua vizuri mimi.” Akaongea kwa kujiamini. “Kile chenye jina langu. Nikajua ni changu kwa hakika na Mungu amekusudia kunipa mimi, huwa siachii hata kidogo. Nitapambana mchana na usiku, magotini nikimsihi Mungu na mimi mwenyewe mpaka kinakuwa changu. Hakuna umbali ninaocha kwenda kwenye changu.” Naya akajisikia vizuri. Akarudi kujilaza vizuri, Joshua akarudi kumpapasa mgongoni taratibu. Naya akatulia.

“Tumbo likiwa linauma hivi, huwa unakula nini?” “Siwezi. Nikiweka kitu mdomoni nakuwa natapika sana. Bora nisile chochote.” “Nahisi ni kama hujajua ni nini unapenda.” “Malon alishajaribisha vyakula na vinywaji tofautitofauti nikawa naishia kutapika tu. Lakini ni hali ambayo huwa haidumu kwa muda mrefu. Siku mbili zikizidi ni tatu tu, natulia kabisa. Ila hizo dawa alizokuwa akinipa yeye, ni kweli zilikuwa zikinisaidia. Alikuwa akinipa na soda ya Sprite. Nakunywa kwa pamoja. Sijui aliambiwa na nani! Lakini ilikuwa ikinituliza sana.” Joshua akatulia akifikiria.

“Au baba yeye ndio ampigie?” “Wewe humjui Malon. Mwache tu.” “Kwa nini?” “Hanaga aibu yule. Wewe unaweza ukaondoka hapa, ukamwacha. Na akamwambia hata baba akalale yeye atabaki hapa. Wanamjua humu ndani. Anaweza kulala hapahapa ndani, pale kwenye kiti alichokuwa amekaa baba kama tupo wodini, hospitalini. Akizidiwa ndipo anaenda kulala na Bale. Masaa machache, anarudi hapa ndani. Akitaka jambo lake, hajui hapana na hana mipaka. Utashangaa wewe, yeye haelewi ni nini kinakushangaza.” “Alishafanya hivyo?”

“Mara mbili alifanya hivyo tena mama akiwa hai na alijua mama hampendi, lakini alibaki hapa siku mbili tukiuguza hili tumbo tena yeye mwenyewe ndiye alinisababisha kuumwa. Akawa anakwenda kuoga na kubadili nguo hapo chumbani kwa kina Bale anarudi kukaa hapa. Nilipoona tumejaa humu ndani, nyumba yenyewe bafu ni moja, nikaamua niondoke naye tu. Mara ya pili, alilala usiku mmoja hapo chumbani kwa kina Bale, kesho yake tukaondoka. Na hakusubiri hata kukaribishwa, yeye mwenyewe akaomba akalale na kina Bale. Hapo usiku ulikuwa umeshaenda, na akasema alitokea Morogoro. Ikabidi aachwe tu. Kwa hiyo Malon kichwa chake, anakijua yeye peke yake. Mwache tu. Likinizidia tena, tutaenda hospitalini.” “Sasa hivi unajisikiaje?” “Limetulia kiasi. Sio sana.” Joshua akaendelea kumpapasa hapo mgongoni.

Naya akaanza kusinzia tena, akawa kama amekumbuka kitu. “Joshua!” Akamwita taratibu. “Vipi?” “Maumivu yamepungua. Nataka kurudi kulala. Nenda na wewe ukapumzike, tutaonana kesho kazini.” “Wewe usijali.” “Hapana Joshua. Najali. Tafadhali kapate masaa machache yakupumzika, ili kesho mmoja wetu awe na nguvu. Mimi nitakuwa sawa tu.” Akamvuta mkono na kuubusu. “Asante kwa kuja kuniona.” “Karibu. Lakini naomba usinifukuze sasa hivi. Ukilala kabisa, ndio nitaondoka.” “Kwa hiyo utaendelea kunibembeleza?” Joshua akacheka taratibu. Akainama na kumbusu shavuni. “Sikujua kama unapenda!” “Najisikia vizuri zaidi kwa sababu ni wewe unanishika.” Joshua alifurahia sana kusikia hivyo. Akamvuta karibu zaidi, akamfunika shuka tena, nakuendelea kumpapasa mgongoni, Naya akalala kabisa. 

Joshua na Baba Naya.

Ilipofika saa tano na nusu usiku, Joshua akamlaza kwenye mto vizuri akamfunika na kutoka hapo chumbani. Akamkuta baba yake amekaa sebuleni. “Naona amelala muda mrefu, nahisi tumbo litakuwa limetulia pia. Maana amesema kichwa kimepoa kabisa. Nitarudi tena saa 11 asubuhi.” “Mapema hivyo!” “Nataka kupata naye muda kabla ya kwenda kazini. Nimeshaanza kuzoea kuanza siku nikiwa namuona pale ofisini kwao. Naona siku itakuwa nzito sana. Heri tu nianzie hapa ndio nijue siku nzima itakuaje.” “Sawa. Lakini mimi namjua Naya. Kesho nilazima aende kazini, pengine akute ujumbe kutoka kwa kiongozi wake kumwambia amefukuzwa kazi.”

“Hakuna mtu atamfukuza kazi Naya bila idhini yangu. Mimi ndiye napanga timu ya idara yangu. Najua ni nani anatakiwa awepo na acheze wapi ili kuweza kufunga kwa urahisi. Na hiki kilichotokea leo mzee wangu, ilikuwa ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu tu. Mungu alitumia mpumbavu mmoja ili kumpa Naya kile anachostahili.” Joshua akakaa kabisa. Baba Naya asielewe.

“Mimi huwa Mungu wangu akitaka kufanya jambo lake, huwa namjua. Hata Naya nilimtuliza mchana na kumwambia, huyo ndio Mungu anapotaka kufanya jambo. Kwanza kabla hajakupa kitu kikubwa, anajaribu tabia yako kuona kama utaweza kumiliki ile baraka anayotaka kukukabidhi!” Baba Naya akaanza kuvutiwa. “Ndio maana nilimwambia Naya, nilazima abaki amesimama.” Akamuona Joshua anacheka.

“Nini? Ameharibu?” Akauliza kwa wasiwasi kidogo. “Hapana baba yangu. Natamani hata nijichukulie sifa. Lakini hata mimi Naya amenishangaza. Amethibitishia uongozi wa pale kuwa anao uwezo mkubwa sana wakufanya kazi ‘under pressure’. Sijui kama unanielewa?” Akamuona Joshua anahamasika.

“Katika moja ya maswali ya kwenye usahili kabla hujapata kazi, ni mwajiri kutaka kujua kama wewe unauwezo wa kufanya kazi na wenzio, na je, unaweza kufanya kazi kukiwa na mazingira si tulivu pamoja na mengine mengi. Sasa leo, Naya ameyajibu hayo maswali bila kuulizwa, kana kwamba anafanyiwa usahili aje achukue nafasi yangu!” Baba Naya akacheka sana.

“Ni vile hana uzoefu tu kwenye hicho kitengo cha masoko, na ndio anaanza kuijua ile kampuni. Lakini nina uhakika kwa uwezo alio nao, alitakiwa kuwa hata mtu wangu wa karibu pale ofisini. Nikimaanisha msaidizi wangu mimi. Lakini kwa kifupi tu, hili la leo ilibidi litokee ili Naya ajulikane, apewe haki yake pale kama mwajiriwa. Anajituma sana pale bila kulipwa anachostahili, nafikiri juhudi zake zimefika mbele za Mungu ndipo ameamua kushuka mwenyewe ili afanye kitu.” Baba Naya akafurahi sana. “Nashukuru kusimama naye. Alikuwa na wasiwasi sana akihofia kufukuzwa kazi na kukufedhehesha.” “Hata kidogo. Ndio ameniongezea sifa.” Wakacheka. Akamuona kama anayefikiria aseme jambo. Baba Naya akatulia kumpa nafasi.

“Najua unaweza kusema ni kama naharakisha mambo, lakini mzee wangu, Naya ni mfupa kutoka kwenye mfupa wangu na ameumbwa kutoka katika nyama yangu.” Baba Naya hakutegemea. “Kama kuna ulikosikia kuna msaidizi hapa duniani aliyeumbwa kwa mwanaume, basi Naya ni msaidizi wangu. Nilikuwa nikisikiliza rikodi ya mazungumzo yao kwenye kikao alinirikodia mmoja wa wasaidizi wangu, hata wao wamekiri ni mimi nazungumza kupitia kinywa cha Naya, wakati si kweli. Naya anazungumza lugha yangu mimi ambayo amenipa Mungu, mpaka nashangaa! Jinsi anavyozungumza na kufanya, kwa hakika Naya ni wangu mzee wangu. Mungu ananithibitishia kila leo kuwa subira yangu, imefika mwisho, ameshaniletea wakufanana na mimi. Ni Naya.” Joshua akaendelea.

“Na kwa kuwa ni Mungu amenipa, nakuahidi nitampenda Naya, kama nafsi yangu na nitamuheshimu kwa kuwa najua Mungu ananingalia katika kila kitu anachonipa kwa upendo. Kabla sijamtenda Naya dhambi, ujue nitakuwa nimekosana sana na Mungu, na hilo siruhusu litokee, kwa kuwa sina kimbilio jingine ila Mungu wangu. Kwa hiyo kama ulikuwa ukimuombea Naya kama anavyoniambia mwenyewe huwa unamuombea sana, naomba sasa hivi utuombee mimi na Naya, mzee wangu. Najua zipo historia nyingi katikati yetu, lakini namuomba Mungu atusaidie kuweza kujenga msingi wetu, mimi na Naya, kwake Mungu.” “Na hapo ndipo mtabakia salama. Hata pepo zikipiga, bado mtabakia salama.” “Asante sana mzee wangu.” Joshua akafurahi sana maana ni kama huyo mzee alishamkubali.

“Nashukuru sana. Naomba mimi nitoke, ili niweze kurudi. Na naomba mwambie Naya hata kama ataamua kwenda kazini, anisubiri nitakuja kumchukua, sitachelewa.” “Sawa.” Wakasimama. Joshua akafungua mlango kisha akageuka. Akamkuta baba Naya akimwangalia. “Nikuulize jambo?” “Karibu.” “Unadhani mimi naweza kumfaa Naya?” Akauliza swali la moja kwa moja. “Mimi sijui, ila Mungu. Na kwa kuwa Mungu anajua, na nilikwambia namuombea Naya tokea akiwa na mwaka mmoja, aje aolewe na mume wake. Si mume wa mwingine. Mume ambaye Mungu amemuandaa kwa ajili yake Naya. Sijawahi kuacha kuliombea hilo. Hata ulipokuwa hapo chumbani kwake pia nilimkumbusha Mungu juu ya mume wa Naya. Kwa hiyo naamini Naya ataolewa na mume wake Mungu aliyemwandalia.” Akajibu kwa ufasaha kabisa na kumuacha Joshua ametulia. Kimya. Kisha akamuona anacheka kidogo.

Akaaga. “Usiku mwema mzee wangu na samahani kukuweka macho mpaka mida hii.” “Usijali kabisa. Hata hivyo bado. Nitakwenda kukaa naye tena kidogo ndipo nikalale.” “Sawa. Na ikitokea unataka kwenda hospitalini, nipigie ili nirudi twende.” “Huku ni mbali sana na huko mnakoishi nyinyi. Nina namba za simu za watu wenye biashara za usafiri. Usiwe na wasiwasi.” “Ila tafadhali naomba unijulishe kabla hujampigia mtu yeyote simu au niseme kabla hamjaenda hospitalini.” “Sawa.” Akakubali lakini si kama aliyeridhia, Joshua akajua. “Tafadhali mzee wangu.” Akasihi. “Nitafanya hivyo Joshua. Ila tuamini atakuwa sawa tu.” “Amina.” Wakaagana tena na kutoka. 

Jumanne.

Saa 11 asubuhi Joshua akawa ameshawasili nyumbani kwa kina Naya, akamkuta Naya akimsubiria. Naya alisimama wakati akiingia. Baba yake ndiye aliyekwenda kufungua geti na kumkaribisha. “Usingehangaika Joshua! Baba huwa ananisindikiza mpaka kituoni, nachukua daladala. Huku kwetu mbali!” “Kwanza umeamkaje? Maumivu?” “Naendelea vizuri. Nataka kwenda kazini.” “Kwa nini leo usipumzike?” “Sitaki kuwapa sababu. Halafu hata hivyo najisikia vizuri. Twende tu tuwahi foleni.” Wakamuaga baba Naya na kuondoka. “Nilifurahi ulivyokuja jana.” “Kweli?” “Kweli Joshua. Nililala vizuri.” Baba Naya akawasikia wakizungumza wakati wanatoka.

Akamfungulia mlango, akapanda ndipo akafunga na kuelekea upande wa dereva. Wakaondoka. “Bado hujaweza kuweka kitu tumboni?” “Sio leo. Nikijaribu tu, nitarudia kutapika siku nzima. Acha leo ipite, labda kesho.” “Kweli hutakula kitu chochote!?” “Sitaweza Joshua. Nitashindwa kazi.” Joshua akatulia lakini kama ambaye hajaridhika. “Nitakuwa sawa tu Joshua. Ni mshituko. Ndivyo ninavyokuwa nikipatwa mshituko. Inanisababishia hii hali na kupata siku zangu tarehe ambazo sizo.” “Lakini nimesikiliza mazungumzo yenu kwenye kikako! Naya wewe unaakili sana.” “Kweli Joshua?!” “Hakika umenishangaza. Umekwenda umbali ambao hata sikukutegemea! Ulisikika ukiwa umetulia sana.” “Pale nilitulia kwa sababu nilijua upo upande wangu. Lakini kabla ya pale niliingiwa hofu sana. Sikujua utanielewa vipi juu ya ujio wa Malon pale kazini na watu wakawa wameshatengeneza picha mbaya! Nikajua utakasirika. Nikaingiwa hofu ya ajabu.” Joshua akatulia kidogo kama anayetafakari kitu.

“Ni kweli nilishtuka Naya. Sikutegemea kuja kumsikia tena Malon akikufuata kazini na wewe kutoka naye nje kabisa kama uliyetaka naye faragha! Ikanishitua sana.” “Pole Joshua.” “Lakini pia sikuwa nikijua kama umerudisha gari! Imenifanya nijisikie vibaya.” “Kwa nini tena!?” “Aaah!”  Hakutaka kuzungumza sana, akanyamaza. “Ndio maana umekuja kunichukua leo?” “Hilo, na pia sitaki upate shida Naya. Wewe ni wangu. Nijukumu langu. Napaswa kukufikiria. Itakuwa haina maana mimi nazunguka na gari, halafu wewe unahangaika usafiri!” Naya akanyamaza. Wakaendelea kwenda wote kimya.

“Nikuulize swali Joshua?” Naya akavunja ukimya. “Karibu.” “Itakuaje hatima yangu pale? Unafikiri wataniwajibisha?” “Hujanisikia nilivyokwambia ulizungumza vizuri sana!” “Sasa ndio itakuaje?” “Kwanza watakutaka kukuajiri. Nina uhakika leo Jamal atakuletea karatasi za ajira, na mshahara mpya. Ni vile tu huna uzoefu kwenye hii kazi. Lakini ungewadai mshahara mkubwa na bado wangekupa. Ila najua kutakuwa na mabadiliko mazuri tu. Jamal anakupenda na kukuheshimu sana.” Naya akatulia kidogo akitafakari.

“Ni nini?” “Na wewe utafanyaje juu ya Njama?” Akamuona anacheka taratibu. “Najua kila mtu anajiuliza na kusubiri kuona itakuaje.” “Utafanyaje?” Joshua akatulia. Naya akamuona akivuta pumzi kwa nguvu. Akatulia kidogo kisha akaanza. “Nimemuomba Mungu na kumsihi anipe uwezo, kwanza kumuonyesha ameshika eneo nyeti sana la maisha yangu. Akielewa hilo, kisha kuhakikisha anaelewa haruhusiwi kurudia tena.” “Kazi yako?” Naya akauliza akiwa hajaelewa ni wapi hapo Njama ameshika, anatakiwa onyo kali hivyo kutoka kwa bosi wake!

“Kazi yangu hakuna mtu anayeweza kuitishia, kwa sababu hata mimi najua sina mpinzani na wananihitaji sana pale.” Naya akakunja uso. “Sasa nini?” “Amekugusa wewe. Tena si kama mfanyakazi wa pale, kama mpenzi wangu mimi. Hilo ni kosa ambalo kwa hakika litamgharimu sana.” Naya akafurahia moyoni kusikia hivyo. “Isingekuwa ni Mungu, sasa hivi tusingekuwa hapa Naya. Alikusudia kuharibu mahusiano yangu. Amesababisha umepatwa na mshituko. Ameharibu mpango wangu wa jana. Na...” “Mpango gani tena wa jana!?” “Nilikuwa nikikusubiri utoke kwenye kikao, ili tutoke kwa chakula cha usiku ndipo nikurudishe nyumbani! Nilitaka tupate muda na wewe. Lakini Njama ameniharibia!” Akaongea kwa kulalamika.

“Jamani Joshua! Sikujua! Ungeniambia.” “Haukuwa kwenye hali yakusikia hilo kwa wakati ule.” “Ni kweli. Kichwa kilijawa mambo mengi nikijipanga nini chakuzungumza. Na nini kingine?” “Unafikiri baba amejisikiaje kuona unarudi nyumbani ukiwa unaumwa, tena peke yako?” Naya akatulia. “Lazima aliumia ila hakusema tu. Ameniharibia sifa kwa baba.” “Lakini usijali Joshua.” “Oooh! Lazima nijali Naya. Nyumbani kwenu hawanifahamu mimi. Wote wapo kwenye kuniangalia kwa karibu sana wakinilinganisha na Malon au wanaume wengine. Kitendo chakujua tunafanya wote kazi na umeondoka pale mimi sina habari! Unafikiria nini?” Naya akafikiria kidogo.

“Lakini baba anakuona wewe umekuwa, kuliko wengine wote, Joshua.” “Sasa kama nimekua na ninashindwa kutimiza wajibu wangu, nitakuwa na tofauti gani na kubwa jinga?” Naya akanyamaza. “Njama ameniumiza sana. Na sijui nia yake ni nini! Hicho ndicho kinanitia wasiwasi.” “Labda wivu tu.” “Umbali aliokwenda mpaka kumpata msaidizi wa CEO, ndani ya siku moja mpaka kuweza kupata nao kikao, akinishutumu bila woga! Hapana Naya. Nimemuomba Mungu aingilie kati lakini nitahakikisha anaelewa mambo yamebadilika. Na nitamuonyesha yeye ni hatari kwangu. Hakika ataelewa na nitahakikisha anajutia alichofanya, na hatakaa akarudia kwa mwingine tena.” “Asante kuwa upande wangu Joshua. Nashukuru.” “Nawajibika kwako Naya. Nisipokupenda wewe kama nafsi yangu, inamaana huna sababu ya wewe kuwepo kwenye maisha yangu!” Ilimgusa sana Naya na kujichukia kupoteza muda na Malon. 

 Ofisini.

Joshua ni miongoni mwa viongozi wa chache sana kwenye hiyo kampuni ambao wana nafasi maalmu ya kuegesha magari yao. Alifunguliwa geti na kwenda kuegesha sehemu yenye jina lenye cheo chake. Akamfungulia mlango akamshika mkono, Naya akamuegemea wakitembea. “Joshua?” Joshua akamungalia wakitembea. “Asante kwa kuja kunichukua nyumbani. Nashukuru.” “Lakini natamani kama ungekula kitu!” Naya akanyamaza. “Naomba niagize uletewe hata supu tu.” “Itanitibua, na kuharibu siku nzima.” “Usiogope, mimi nitakuwa na wewe. Leo sitatoka, nitakuwa hapahapa. Ukianza tu kutapika, mimi mwenyewe nitakuwepo.” “Hapo sawa. Lakini huoni kama itakuvuruga kazini!” “Ndio Joshua mpya huyo.” “Utajuta kuwa na mimi!” “Mungu anajua nipo tayari kwa ajili yako Naya.”  Naya akamwangalia na kurudi kumuegemea akimshika mkono vizuri tena kwa kupishanisha vidole. Wakatembea mpaka ofisini kwake Naya.

Joshua akamvutia kiti na kuegemea meza. Naya akakaa na kujiegemeza kichwa pembeni ya kiuno cheke kidogo akatulia akiwa ameegemea upande mwingine. Joshua akamuwekea mkono mgongoni. Akatulia si kukimbilia kufungua kompyuta na kutafuta kazi kama kawaida yake. “Leo ungetakiwa kupumzika Naya.” “Najua Joshua. Lakini jana niliharibu. Hapa navuna nilichopanda mimi mwenyewe.” “Unajisikiaje lakini?” “Tukae wote kidogo kabla hujaondoka. Ni sawa?” “Sawa.” Naya akaweka mkono pale alipoegemea kwa Joshua kama ametengeneza mto kwa mkono, akajilaza vizuri. Joshua akarudisha mkono mgongoni akawa kama anamsugua mgongoni wakatulia. 

“Naya?” Joshua akamuita. “Najua ni mapema kukuuliza hili, lakini nataka kujua kama Malon anajua kama mimi nipo?” Naya akashituka nafsini kwake, lakini akabaki ametulia tu. “Au unafikiri ni mapema sana?” Joshua akauliza tena. “Alituona kule Mbeya.” Naya akajibu. “Mimi kama mfanyakazi mwenzio.” Naya akatulia akifikiria na kukaa vizuri. “Ulitaka nimwambie nini juu yako?” “Wewe uliweza hata kunitaja kwake?” “Hapakuwa na hayo mazingira ya hata kukutaja kwake hiyo jana alipokuja, Joshua. Halafu sijui nakutambulishaje kwake!” Joshua akabaki akimwangalia. “Kama ulivyosema, ni mapema hata kusema lolote. Ua nilitakiwa nikutambulishaje?” “Kama isingekuwa mapema, ungenitambulisha kwake?” “Kabisa Joshua.” “Siku ya kwanza tu kuwa na wewe, nilijua yupo Malon.” Ikawa kama analalamika. Naya akamuelewa.

“Joshua, naomba amini sikufichi kwa Malon na sina sababu ya kukuficha kwake. Lakini hatupo kwenye wakati mzuri wa kuzungumza na Malon, kama hivi ninavyozungumza na wewe. Wewe unanifanya natulia, ndio maana nikaweza kuzungumza. Lakini si kwake. Kwanza naona ni kama kumfaidisha bila sababu.” “Mimi nataka anitambue kama nipo na wewe sasa hivi.” “Sawa Joshua. Yakitokea hayo mazingira, nitamwambia.” Joshua akaonekana kutoridhika.

“Ameniumiza sana Malon, na hatupo kwenye wakati mzuri wa mawasiliano. Siwezi kumpigia tu simu na kumwambia wewe upo!” “Basi mimi nimpigie nimuombe dawa, na pia uniruhusu nijitambulishe ili ajue hawezi kurudi tena kwako hata iweje na haruhusiwi hata kukugusa tena kwa kuwa mimi mwenyewe sasa hivi nipo. Kwamba hata kama anakuja kukuona leo au kesho kwa swala la ugonjwa, awe na heshima akijua sasa hivi mimi nipo na aache kukufuata tena akitaka kukuhudumia wewe. Haruhusiwi.” Naya akachoka kabisa.

“Malon hawezi kurudi tena. Ni mpaka mimi nimtafute.” “Chakwanza watu wanabadilika. Huwezi jua baada ya kumrudishia gari atafanya nini tena. Chapili, hatujengi uadui au hutakiwi kumuogopa hata kumuulizia dawa kwa kuhofia anaweza kurudi tena! Akijua mimi nipo, hawezi kurudi kama alivyokuwa akirudi kwako zamani akijua huna mtu.” “Hakuna kipindi Malon amerudi kwangu kusiwepo na mtu mwingine!” “Asante sana. Sasa hiyo ndio pointi yangu. Mimi sitaki huo mchezo wake.” Mpaka Naya akafunga macho.

“Nataka akija kukutana na wewe, kwa mazingira yeyote yale, ajue mimi mwenyewe nipo. Nasitaki michezo isiyo na maana kwako. Iwe mwiko kukuhonga. Awe na nidhamu ofisini na nyumbani pia. Hawezi akawa mtu wa kutokea bila miahadi.” Naya akamwangalia Joshua na kushindwa chakuongea.

“Labda kama uwe huna uhakika na sisi.” “Nakupenda Joshua.” “Hiyo haitoshi kwa sababu wewe unajua wakati mwingine mapenzi tu huwa hayatoshi. Inatakiwa commitment ya hali ya juu. Hata ukiamka asubuhi ukagundua hujisikii kunipenda, au nimekuudhi kwa namna yeyote ile, lakini uwe unajua Joshua ni wangu mpaka kifo. Jua litoke, mvue inyeshe, tumejifunga kwenye mahusiano yetu. Sasa pengine uwe hutaki hiyo.” “Nata Joshua. Nilikwambia nitatulia na wewe na sitakusaliti.” “Basi naomba namba ya Malon.” “Unafikiri ni lazima iwe leo?” “Ulitaka iwe lini? Maana mimi sina ninachosubiria kwako. Nishakuthibitisha wewe ni wangu. Nakutaka wewe Naya. Nimemaliza. Sasa pengine ndio uniambie wewe, kama bado kuna unachosubiria kwangu!” “Nakupenda Joshua.” “Hilo nimekusikia Naya. Lakini ninachokipata hapa ni kuwa haupo tayari kunitambulisha kwa Malon, si ndiyo?” “Kwa kuwa sioni sababu?!” Joshua akakunja uso.

“Naya, wewe ni smart mno. Naamini umenisikia na kuelewa hoja yangu ila hutaki kunitambulisha kwa Malon, kitu kinachoanza kunitia wasiwasi.” “Usiwe na wasiwasi na Malon, Joshua! Malon si mpinzani wako na wala hatakuwa.” “Sivyo unavyofanya hapa. Hayo ni maneno yanayosikika vizuri sana. Lakini vitendo vinapingana. Jana ulikuwa na sababu tosha yakunitaja kwake kama na mimi nimechangia kurudisha hilo gari. Kwamba upo kwenye mahusiano mengine, huwezi kushikilia mahusiano yaliyopita. Hivyo ndivyo mimi ningefanya. Pengine labda uwe huna mpango wa kudumisha tulicho nacho, unataka iwe kitu cha muda tu kama kina Josh na Ino ila Malon akiwa ndiye mmiliki mkuu. Na unatazamia pengine siku moja atakuwa unachokitaka awe, na kukufanya uwe na furaha. Kwamba unaamini ni yeye tu ndiye anayeweza kukufanya uwe na furaha.” Naya akajua Malon ameshamtisha Joshua. Ameweka picha kubwa sana ya Malon kiasi cha kumtisha.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Naya atafanyaje? Mapenzi!!?? Na Pesa je! PESA ambayo ndiyo Ajira yake inayotegemewa nyumbani kwao?? Bado ni Malon tu.

Usikose Muendelezo.

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment