Naya akatoa simu kwenye pochi yake akampigia
Malon. Iliita mara mbili tu akapokea. Naya akaweka speaker. “Pole, nimekuamsha?” “Hapana. Nilikuwa nasoma bibilia,
niombe.” Malon akajibu. “Mbona sauti
yako ipo kama haupo sawa?” Akauliza kwa kujali kama anayemfahamu
sana Naya, hata kwa sauti tu. “Tumbo linaniuma.
Halafu unajua sikuwahi kujua ni dawa gani zile ulizokuwa ukinipa na soda ya
Sprite mpaka linatulia!” “Pole Naya. Pole sana.” “Asante.” Joshua
kimya akisikiliza. “Malon?” Naya
akamwita sababu ya ukimya. “Kuja kwangu jana
kulikuumiza?” Malon akauliza kwa kujutia. “Ndiyo Malo.” “Samahani Naya. Sikutaka kukuudhi ila
kukusaidia tu. Sikutaka makosa yangu yakufanye uendelee kupata shida Naya.
Unastahili usafiri mzuri wa kuzunguka hapa mjini. Hii gari niliona ingekufaa
sababu ya ulaji wake wa mafuta na matengenezo yake yapo chini. Isingekugharimu
hata kama mimi mwenyewe nisingekuwepo kukusaidia, bado ungeimudu tu.” Malon
aliongea kwa kujali.
“Unisamehe mama. Nisamehe sana. Sikukusudia kukuudhi.” Naya akajifuta
machozi. “Jana hatukupata muda wa kutosha
kuzungumza. Lakini pia sababu ya kurudisha gari, ni kwa kuwa nimepata mwanaume
mwingine.” Kimya. “Sio sawa
kuingia kwenye mahusiano mengine nikiwa na mali zako. Si sawa?” “Ni Joshua?” Naya akashituka sana mpaka
akamwangalia Joshua. “Naya? Si yule jamaa mlikuwa
mmekaa naye Mbeya kwa muda mrefu tu mkizungumza?” “Ndiyo. Anaitwa Joshua Kumu.” Wakatulia
kidogo. “Anakupenda na kukujali?” “Ndiyo, Malon.” “Anakuthamini
wewe kama Naya mbali na muonekano wako wa nje?” Malon akauliza
tena, Naya akaanza kulia.
“Ni maombi yangu uishie pazuri mama. Wewe ni mtu mzuri sana.
Unastahili mwanaume atakayekupenda kwa dhati na kuenzi huo moyo wako.” “Joshua ananipenda. Na yeye anampenda sana Mungu.” Akamsikia
akivuta pumzi kwa nguvu. “Dawa niliyokuwa nikikupa
ni yakutuliza tu maumivu.” Akamtajia jina lake. “Sema nilizungumza na nesi fulani akasema hajui kuna nini
kinatokea. Lakini hiyo dawa ukimeza na soda ya Sprite, inakata maumivu na
kichefuchefu na yeye alifundishwa tu mtaani ikawa msaada. Unakumbuka ndiyo
niliyokuwa nikikupa?” “Sikuwa najua kwa jina hilo.” “Halafu unakumbuka
mwanzoni nilikuwa nikikuwekea taulo la moto hapa chini ikawa inakusaidia mpaka
tukanunua heatpad?” “Sijui niliipoteza wapi! Nahisi niliiacha kwenye ile nyumba
ya Morogoro.” “Nitakutafutia ingine.” Akamuona Joshua anatingisha
kichwa akikataa kabisa.
“Ila kwa sasa chukua taulo, weka maji liwe na unyevunyevu. Liweke
kwenye microwave, lipate moto au tumbukiza kwenye maji ya moto kisha kamua
kabisa, ndipo uweke chini ya kitovu kabisa. Acha kwa muda utajisikia vizuri.”
“Asante sana. Ila huna haja yakunitafutia hiyo heatingpad. Nitamuomba Joshua
akaitafute pamoja na dawa. Umenisaidia vyakutosha Malon. Naona
ni wakati na mimi niendelee pale tulipoishia. Ukiendelea kunifanyia
mambo, haitakuwa sawa. Unakumbuka wakati ukiniacha kwa yule Joshua mwingine?
Joshi.” Malon
akanyamaza. “Uliniambia hutaki kunichanganya kwa
kuwa unakuwa ni kama unaingilia mahusiano yetu. Ukaondoka na hukurudi tena na
wewe ukaenda kuanzisha mahusiano na Rita. Unakumbuka?” Malon kimya.
“Basi naomba na safari hii iwe hivyohivyo Malon. Endelea kuniombea
na mimi nitakuwa nikikuombea. Ila ujue Mungu amenirudishia furaha ile
niliyokuwa nimepoteza. Kuna utulivu tena moyoni mwangu.” “Kwa hiyo unadhani
Joshua ndiye mwanaume atakayekutoa kwa baba Naya?” Naya akakumbuka maneno
aliyomwambia. “Niombee Malon. Kwa
kheri.” “Naruhusiwa hata kupiga simu kukujulia hali?” Naya
akamwangalia Joshua, akamuona ameinama kimya tu. Akajifuta machozi na kuhema
kwa nguvu kama anayejaribu kujituliza.
“Sitaki tupotezane Naya. Tumetoka mbali mno mimi na wewe. Ni salamu
tu.” “Hapana Malon. Itakuwa namfanyia Joshua kile nilichokuwa
nikikikataa wewe usinifanyie mimi. Joshua ametulia sana, Malon. Sitaki kuanza
kumchanganya tena kwa wewe kuwepo katikati yetu. Nataka nitulie, niangalie kama
naweza kujenga na kupata kile nilichokuwa nikikililia wakati wote. Nisipofanya
hivyo, nahisi nitajichelewesha. Niombee, na amini Mungu atatenda.”
“Kwa hiyo hutaki hata salamu yangu Naya!?” “Haijawahi kutokea
hivyo Malon. Huwa ukiondoka unaondoka moja kwa moja. Kwa nini tuanze sasa?
Sitaki maumivu na kilio nilichokuwa nacho kwako, kimpate na Joshua. Haitakuwa
sawa kwake. Tafadhali naomba uliheshimu hilo kwa kuwa sitabadilisha namba ya
simu kwa ajili yako Malon. Naamini utaendelea kuwa Malon kama wa zamani.
Ukiondoka, umeondoka. Kwa kheri.” “Kabla hujakata
simu, naomba nikuombe kitu Naya?” Malon akaongea kwa kubembeleza.
“Ni nini tena Malon?” “Siku utakayojisikia kunisamehe kutoka
moyoni, tafadhali nijulishe hata kwa ujumbe.” “Nimekusamehe
Malon.” “Hapana Naya. Mimi nakujua, na ninajua kama si mimi,
usingehangaika kwa wanaume wengine. Najua hata huyo Joshua asingekuwepo kwenye
maisha yako. Najua nimekusababishia mengi maishani. Uliniambia kunipenda mimi
ilikuwa ni adhabu kwako. Na ninaelewa na nimekubali. Naomba hiyo siku. Sijali
hata kama ni miaka 20 kuanzia sasa, kama Mungu akinipa uhai. Na mimi sitabadili
namba yangu ya simu kwa ajili hiyo, kwa hiyo tafadhali nijulishe. Kwangu
itakuwa na maana kubwa sana.” Naya akalia sana.
“Ni hilo tu Naya.” “Mungu amekusamehe
Malo.” “Najua kama Mungu amenisamehe, Naya.
Lakini italeta maana kubwa sana kwenye maisha yangu yaliyobaki hapa duniani
kama na wewe ukija kunisamehe hata na la Rita hili lililotokea hivi karibuni,
kushindwa kuwa faraja ulipompoteza mama, na hata madhara niliyoyasababisha sasa
hivi na mengine mengi tu. Wakati utakapopata hiyo neema yakunisamehe mimi
kushindwa kusimama kwenye nafasi yangu, tafadhali nijulishe Naya. Ujue ni deni
ambalo unalo kwangu. Kila la kheri.” “Asante.” Wakakata
simu.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Naya
akajifuta machozi na kumtizama Joshua. “Ni
sawa?” Joshua akavuta pumzi kwa nguvu na kusimama kutoka pale
alipokuwa ameegemea. “Nakwenda kukutafutia hizo dawa, nikuletee.” “Nataka unijibu Joshua kama umeridhika.” “Nimeridhika
na ninakushukuru. Naomba unisamehe Naya. Nakupenda, nataka nafasi ya peke yangu
kwako bila muingiliano na yeyote yule, ili kama nikishindwa, nijue nimeshindwa
mimi mwenyewe sio sababu ya mtu mwingine.” “Kwa
hiyo sasa hivi umeridhika upo peke yako?” “Kabisa. Ila hiyo siku ya
kulipa hilo deni la kumwambia umemsamehe, na mimi nataka kujua.
Kwa hiyo ujue upo na madeni mawili.” Naya akachoka zaidi.
“Nitarudi
sasa hivi. Acha nikakutafutie dawa. Halafu heating pad nitamtuma mtu akaangalie
maduka yakifunguliwa.” Kitu kikampanda Naya, akasimama kukimbilia
chooni na kumpita Joshua kwa haraka mpaka choo cha upande wa kike.
Joshua akamsikia akitapika sana huko ndani chooni.
Ikabidi
tu Joshua aingie kumsaidia. Akamshika mbavuni, akatapika mpaka akamaliza.
“Nashauri urudi nyumbani ukapumzike.” Naya akabaki kimya akijisafisha huku
machozi yakimtoka. Joshua akataka kumshika ili amuweke kitu sawa, Naya
akamkwepa kabisa kama anayekataa asimguse. Akashangaa. “Ni nini!?” “Tafadhali usiniguse.” “Kwa nini!?” “Siwezi hata kupumua. Nahitaji nafasi.” “Unamaanisha
nini Naya!?” “Niache kabisa. Nahitaji
kupumua.” “Naya!” “Tafadhali
Joshua. Niache kabisa. Nenda tu ofisini kwako. Mimi narudi nyumbani.” “Kwa
hiyo hutaki hata nikurudishe?” “Hapana.
Nahitaji muda wa peke yangu.” Naya akatoka hapo Joshua asiamini.
Akarudi
ofisini kwake akamuandikia email Jamal akimtaarifu yupo kazini, lakini anaumwa
na kutapika sana. Hajisikii vizuri. Anaondoka. Wakati akiandika, Joshua
akamfuata hapo. Hata hakumtizama. Akamtumia huo ujumbe Jamal, akachukua pochi
yake na kutoka akimpita Joshua. Bado ilikuwa mapema sana. Hakuna mtu kwenye
hilo jengo la masoko. Naya akatoka akitembea.
“Naya?”
Naya akageuka na uso uliojaa machozi haswa. “Sasa hivi bado kuna giza nje.
Huwezi kwenda peke yako.” “Sasa hivi sijali
chochote kile Joshua. Sijali.” Naya akaondoka, lakini Joshua akawa
akimfuata nyuma akamsikia akilia ila akashangaa hata baba yake hampigii simu.
Joshua akamkimbilia mpaka akamfikia. “Nimpigie simu baba Naya?” “Nahitaji muda wa peke yangu Joshua. Tafadhali niache.” Hapo
kidogo Joshua akaridhika. Kusikia hata baba Naya kwa wakati ule haitajiki,
akatulia wakitembea kuelekea kituoni Mwenge. Kimya.
“Nahitaji kuwa peke yangu Joshua. Tafadhali niache.” “Sitafanya hivyo
Naya. Ni mpaka nijiridhishe upo salama.” Naya akaanza kulia tena. Mara akamuona
anakimbilia tena pembeni kutapika. Akaenda kumshika, akatapika mpaka akakaa
chini kabisa kwenye majani. Hakuna kilichokuwa kikitoka. Akaanza kulia tena.
Joshua
akamnyanyua pale na kurudi naye tena kwenye gari yake walipoiacha ofisini.
Walinzi wakiwaangalia wakiingia na kutoka tu. Kimya. Ni Joshua Kumu. Wote
nidhamu. Akampandisha garini. “Hutarudi nyumbani ukiwa na hali hiyo, Naya.
Nakupeleka hospitalini wakuchome sindano ya kuzuia kutapika, kisha unywe dawa
tulizoelekezwa. Hutuwezi kuwa tukimpelekea baba Naya matatizo tu, kila wakati!
Tunakuwa wote kama Zayoni! Hapana Naya. Lazima kuonyesha utofauti wako na
Zayoni, na kumpa baba nafasi yakufikiria mambo yake mengine.” Kimya. Naya
hakujibu. Joshua akatoa gari hapo mpaka kwenye hospitali ya kawaida tu maeneo
ya Mwenge.
Hospitalini.
Akamfungulia
mlango pale alipokuwa amejikunja kimya. “Twende.” Akamfungua mkanda, Naya
akashuka garini. Akaanza kumtoa michanga na majani kwenye nguo na kumfuta
machozi kabla yakuingia. Hakukataa. Akamtengeneza vizuri. “Pole.” Naya akaanza
kulia tena, Joshua akamshika mkono taratibu akimuongoza kuingia ndani mpaka
mapokezi. Akamueleza aliyemkuta hapo mapokezi na kuongeza. “Anashindwa kuweka
kitu chochote mdomoni tokea jana. Mara ya mwisho ametapika, hakuna kitu
kimetoka.” “Anaonekana kabisa.” Akaongea nesi aliyekuwa amesimama hapohapo
mapokezi akionekana anaandika kitu.
Baada
yakutolewa damu, daktari akashauri achome sindano na awekewe maji. Akapewa
chumba cha kupumzika, akiambiwa baada ya hapo ataruhusiwa. Naya alikuwa
amechoka mpaka mbavu sababu ya kutapika. Alipochomwa tu sindano, akapotelea
usingizini akijua Joshua yupo. Akalala.
Baada
yakupitiwa usingizi mzito, akiwa bado usingizini akasikia ni kama Joshua
akizungumza, akielezea hali yake. Bila kufungua macho akajaribu kusikiliza,
akagundua ni Jamal na Jema wamefika hapo kumuona. Naya akatulia kimya. “Aisee
poleni sana.” “Atakuwa tu sawa. Wamempa dawa yakuzuia kutapika, na hayo maji.
Wamesema watamruhusu baadaye wakijaribisha chakula nakuona hajatapika.” Joshua
akaeleza. Akamsikia Jema akizungumza na Joshua, akampa maelekezo, wakaondoka.
Ndipo
Naya akafungua macho akakuta Joshua akimwangalia. “Vipi?” Naya akatulia.
Akamshika mkono vizuri kwa upendo kwa kupishanisha vidole kama kawaida yake.
Naya akaanza kutokwa na machozi. “Pole.” Akamfuta machozi. “Tumbo bado
linauma?” Akatingisha kichwa kukataa. “Umenichukia?” Joshua akamuuliza kwa
upendo, Naya akatingisha kichwa kukataa. Akamfuta tena machozi. “Ila nilikuwa sipo tayari!” Naya akaongea kwa
kulalamika, Joshua akaelewa. “Najua Naya. Na usifikiri kama ingefika wakati
ukajikuta upo tayari. Ilibidi kufanya tu.” Naya akalia sana. Joshua
akambembeleza. “Mimi nipo Naya. Naomba unipe nafasi. Naamini tutakuwa sawa tu.
Sawa?” Naya akatingisha kichwa kukubali. Hapo Joshua akaridhika.
“Nikwambie
kitu Naya?” Naya akajifuta machozi. “Tusingefika kokote, endapo ungebakiwa na
daraja linalokuunganisha na Malon. Ungekuwa nusunusu kwangu, ukijua au
ukitegemea kuwa...” “Malon yupo tu, nikimtaka
yupo.” Akamalizia Naya mwenyewe na kuendelea. “Ilikuwa ikinisaidia kwa sehemu. Nikawa siumizwi tena na
mtu mwingine kwa kuwa sikuwa nikiwafungulia moyo wangu wote, nikijua Malo wangu
yupo tu sehemu fulani ni mimi tu kumtafuta.” Naya akaendelea
taratibu kama anayekiri sasa. “Ikajengeka kama
kisiwa cha salama, ndani yangu. Hakuna mwanaume atanifanya kitu, nikaumia kwa
kuwa nilikuwa najua bado ninaye Malon.” “Na mimi nilijua Naya. Na
samahani nimejuta kuzungumzia hili ukiwa mgonjwa.” “Hakuna siku ungezungumzia hili ikawa salama. Hata hivyo bado nahitaji
muda.” “Lakini isiwe mbali na mimi. Nakupenda Naya. Na nipo tayari
kukusubiri, ila tukiwa pamoja.” Naya akajisikia vibaya lakini ni kweli Malon
amekaa kwenye maisha yake na kuathiri mfumo mzima wa maisha yake kwa muda mrefu
sana. Hapakuwa na Naya bila Malon. Akamuhurumia Joshua na kutamani kama
angekuja mapema kwenye maisha yake, yeye ndio akawa Malon.
“Nisamehe kukufukuza Joshua. Nilikuwa na hali mbaya! Nilihisi
siwezi kuhema tena. Mbavu zilikuwa zimebanwa, siwezi kutulia.” “Nilielewa.
Unajisikiaje?” “Mwili umetulia kabisa. Ila natamani
kulala.” “Jozee yupo njiani, analeta supu. Unywe ndipo urudi nyumbani
ukalale.” “Pole na samahani kukuweka hapa wakati ulitakiwa kazini.” “Usijali.
Kila kitu kipo sawa.” Naya akatulia. “Jamal na Jema walikuja kukuona. Wamekuletea
na juisi.” “Nashukuru.” Jozee akawa anapiga simu kuulizia walipo. Joshua
akatoka kwenda kumpokea, akarudi na chakula bila Jozee. Akatamani kuuliza ila
akaona hayamuhusu. “Ametengeneza nini?” “Amesema supu ya mbogamboga ila amesema
utaipenda tu.” Naya akakaa ili ale.
Joshua
akamuweka vizuri kwenye bakuli na kijiko maalumu kwa kunywea supu, Naya akaanza
kunywa. Kijiko tu cha kwanza akapenda. “Ina ladha nzuri ya ndimu.” Akasifia,
Joshua akafurahia. “Nimefurahi kama umependa. Vipi kichefuchefu?” “Kimeisha.”
“Nimemtuma zile dawa na soda hiyo ya Sprite. Akirudi tutaondoka. Acha nikalipie
kabisa hapa.” “Nakushukuru Joshua. Asante.” Baada ya yote, Naya akatolewa hapo
akiwa na nafuu kubwa tu.
~~~~~~~~~~~~~~~~
“Kwa
nini mimi nisirudi tu nyumbani, wewe ukawahi kazini? Bado ni mapema.” Joshua
akakunja uso. “Yaani nikuache hapa!?” “Hakuna shida kabisa Joshua. Tena
sasahivi daladala zinakuwa wazi tu. Nisogeze tu mpaka kituoni. Nakuhakikishia
nitakuwa sawa.” “Mimi huwa sijui kufanya mambo nusunusu Naya. Utanisamehe kama
utaniona ni kama nalazimishia mambo fulanifulani. Naomba unielewe na kunizoea.
Nikiamua kufanya jambo, na nikajua mkono wa Mungu upo na mimi kwenye hilo
jambo, huwa nafanya kwa hakika bila kuzembea. Ndivyo nilivyo.” “Sitaki wote
tukwame kwenye jambo moja, Joshua!” “Sihesabu kama nimekwama hapa na wewe,
Naya. Usiwe na wasiwasi. Nahesabu nimepata nafasi ya kuwa na wewe kwa kipindi
hiki wewe ni mgonjwa. Basi.” “Nashukuru Joshua.” “Usijali kabisa.” Safari ya
kurudi Kiluvya nyumbani kwa kina Naya, ikaanza.
Naya
alijituliza kitini, akajikunja na kuegemea kiti akiangalia nje. Mkono mmoja
akapenyeza kifuani kwenye tisheti ya kazini aliyokuwa amevaa. Akatulia kimya.
“Nafurahia muda na wewe Naya.” Naya akamwangalia. “Kama nilivyokuwa nikifurahia
tulipokuwa kwenye boti, ndivyo hata pale hospitalini, hapa na popote pale.
Ilimradi niwe na wewe.” Naya akavuta pumzi kwa nguvu na kutulia bila ya kujibu.
Joshua akaendelea kuendesha, Naya ametulia tu.
Joshua
hakuzungumza tena mpaka walipofika nyumbani kwao. Baba yake akatoka akiwa ameshituka.
Naya alikuwa amekaa kitini akisubiria kufunguliwa mlango, wakati Joshua
ameshuka garini. “Kwema!?” Baba yake Naya akauliza akishuka ngazini akisogelea
gari. “Sasa hivi anajisikia vizuri. Nimemrudisha apumzike.” Joshua akamfungulia
mlango, baba Naya naye akasogea. “Vipi mama?” “Sasa hivi najisikia vizuri.
Joshua alinipeleka hospitali. Wamenichoma sindano ya kuzia kutapika,
wakaniwekea maji. Na nimekunywa supu, ameniletea mpishi wa Joshua. Najisikia
vizuri, ila usingizi, nataka kulala.” Baba Naya hakuamini alichosikia. Naya
amekuwa hospitalini bila yeye! “Amepewa mapumziko ya leo na kesho ili
kujiangalia. Kama atahitaji siku zaidi, daktari ameniambia nimpigie, ataongeza
ED.” Baba Naya alikuwa na mshangao mpaka akashindwa kuzungumza.
“Karibu
ndani Joshua.” Ikabidi Naya amkaribishe. “Karibu Joshua.” Ndipo baba Naya
akaongeza kama aliyerudiwa na ufahamu. Naya akawapita hapo na kuingia ndani
moja kwa moja. Wakamfuata nyuma Joshua akiwa na dawa pamoja na soda. Naya
akapitiliza chumbani kwake, Joshua akamfuata nyuma, baba yake Naya ikabidi
asubiri nje. Naya akapanda kitandani. Joshua akimwangalia. “Njoo nishike mkono
kama vile ulivyonishika hospitalini. Nikilala ndio uondoke.” Joshua akacheka
kidogo, lakini moyoni alifurahia sana. Akaona ni kama amezawadia zawadi ya
thamani haswa. Akamfunika vizuri na kukaa pembeni yake. Naya akampa mkono.
Akaubusu kwanza ndipo akamshika vizuri kwa kupishanisha vidole, akaupakata huo
mkono. “Asante.” Akashukuru na tabasamu lililojaa usingizi. “Karibu.” Akamgusa kidogo
usoni kama kumuweka sawa nyusi, Naya akalala hapohapo. Joshua akaangalia saa,
ndio ilikuwa ikitimu saa 5 na nusu asubuhi hiyo. Akaona arudi kazini. Akamuweka
vizuri na kumfunika. Akatoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~
“Naona
amelala.” “Pole kwa hekaheka?” “Nashukuru Mungu ametulia. Wamempa matibabu,
lakini pia tulifanikiwa kupata dawa alizokuwa akipewa na Malon. Nimeziacha hapo
kwenye meza chumbani kwake. Nashauri akiamka hata kama tumbo halitakuwa
likiuma, anywe tu ili asirudie ile hali.” “Nitafanya hivyo. Nashukuru sana.”
Yule mzee akawa kama na maswali, na Joshua alijua ila hakutaka kuingilia mpaka
aulize mwenyewe. Alipomuona amecheka tu akifikiria, Joshua akamuaga. “Acha
niwahi kazini mzee wangu. Nitarudi tena jioni.” “Nashukuru sana.” Joshua
akatoka.
Ofisini.
Joshua
alirudi kazini akiwa amebeba sura ya kazi tu. Aliingia hapo akijua Jema anayo
maagizo yake yote ya siku hiyo ila Njama hakuwa amezungumza naye kabisa. Jema
alishangaa hata hakumuulizia, akapitiliza moja kwa moja mpaka ofisini kwake
baada ya Fina kumtupia salamu. Wakajua siku ndio imeanza hapo. Fina akaingia
ofisini kwake na kuzungumza naye maswala ya kazi, alipomaliza tu. “Namuhitaji
Jamal, sasa hivi.” Fina akatoka kwenda kumpigia simu Jamal kumuita. Bila
yakupoteza muda Jamal akafika hapo. Jamal alikuwa mkubwa kwa umri
ukimlinganisha na Joshua.
“Naya
hatakuwepo kazini leo na kesho. ED yake hii hapa. Daktari anataka apumzike
kabisa kama nilivyokwambia.” “Poleni sana.” Jamal akapokea hiyo ED. “Nataka
kazi ile niliyomkabidhi Njama na Naya, uifanye na jioni niwe nayo hapa mezani.
Fikiria mchango wa Naya. Kama unaweza kuweka pamoja na...” Njama akaingia.
Jamal akamuona jinsi alivyobadilika. “Kwa nini unaingia ofisini kwangu kama
chooni!?” Akamuuliza kwa kumshangaa na ukali kama ni kitu kigeni wakati
Jema na Njama huwa wanaingia hapo bila hodi kila wakati hata kama Joshua
anakuwa na mgeni, wao huingia tu nakufanya yao na kutoka. Siku hiyo akambadilikiwa.
“Nilitaka kukukabidhi ile...” “Nimekuuliza swali, acha dharau.” “Samahani,
sikujua kama una mtu.” Njama huyu alipoa kama siye aliyeanzisha fujo.
“Kwa
hiyo kusipokuwa na mtu ndio inakupa ruhusa yakuingia humu utakavyo?”
“Samahani.” “Fuata utaratibu tafadhali. Na ninajua wewe ni mzuri sana wa
kufuata utaratibu kwa hiyo hilo halitakusumbua. Unanielewa?” “Sawa.” “Fina
yupo nje kwa ajili hiyo au angalia ratiba yangu kwa Jema, upange naye muda
ambao anafikiri nina nafasi. Acha kufanya fujo zisizo na sababu.” Mpaka Fina
nje akajua mambo yameshambadilikia Njama. Kwamba anatakiwa kuomba miahadi na
Joshua! “Samahani sana.” Njama akataka kutoka. “Na Njama.” Njama akageuka.
“Hiyo kazi mkabidhi Jamal aipitie.” Mpaka Jamal akashituka.
“Sijaelewa!
Yaani unataka kazi yangu mimi aipitie Jamal!?” “Unashida na hilo?” Joshua
akamuuliza akimtizama, machoni. “Sijaelewa?” “Kama unafikiri ninao uwezo wa
kukuelewesha juu ya sintofahamu yeyote kichwani mwako, pitia ratiba
yangu kwa Jema, zungumza naye uone kama nina nafasi ya kuzungumzia hilo ili
niyajibu maswali yako. Vinginevyo hiki ni kitengo CHANGU. Mimi. Narudia
tena, mimi ndiye ninayepanga timu ya humu ndani. Najua nani nimuweke wapi na
acheze vipi ili kufanikisha lengo kuu lililotukutanisha hapa kwenye hii
kampuni, tena bila kupoteza muda. Hujaridhika kufanya kazi kama timu iliyopo
chini yangu ukifanya kazi na wenzio, nenda kapeleke malalamiko yako popote
unakotaka. Tafadhali funga mlango nyuma yako.” Akamgeukia Jamal.
“Ifikapo
jioni, kazi iwe imekamilika. Chukua alichokifanya Njama. Pitia, andika kwa upya
na weka sawa. Kuna swali?” “Nimeelewa kiongozi. Acha nikaanze sasa hivi.” Joshua
akahamisha macho kwenye laptop yake. “Sitampa Jamal kazi yangu. Maana itakuwa
ni kama yeye anaandika kitu kipya kutoka kwenye kazi yangu! Halafu itajulikana
ni yeye amekamilisha! Hapana.” Jamal alikuwa amefika mlangoni akashangaa sana.
“Wewe
vipi Njama!?” “Unataka upate sifa kwa kupitia kazi yangu!?” “Wewe umeandika
mawazo yako hapo au ni kile alichozungumza Naya siku ile na kila mtu
akakipenda?” Jamal akauliza kwa kumshangaa sana. Joshua kimya. “Msitake
kunifanya..” Jema akaingia kwa haraka. “Mimi naomba nikushauri kitu Jamal.”
Jema akamkatisha Njama.
“Kila
mtu alimsikia Naya siku ile. Na akaongezea kwenye mawazo ya kundi lenu. Huna
cha ajabu utakachopata kutoka kwa Njama isipo...” “Na kwa taarifa yako Jema,
nimepanga hii kazi vizuri sana. Mtu kama Jamal hawezi...” “Jiangalie
Njama!” Jamal akamtahadharisha. “Utanifanya nini?” Njama akauliza
kibabe.
“Jamal,
nisikilize mimi tafadhali. Achana na Njama. Nenda kafanye kazi. Kwanza kundi
lao siku ile ndilo lilichemsha, na kutoa mchango wakijinga kabisa. Huna
kipya utapata kwenye alichoandika huyu, isipokuwa aliyoiga kutoka kwenu na
Naya.” “Jema jiangalie wewe!” “Nenda Jamal. Nenda kafanye kazi. Achana naye.
Ameingiwa na roho ya uvurugaji, anataka kutuvuruga tu, wakati sisi wote
tulikuwa tukifanya kazi kwa kuheshimiana humu ndani na umoja.”
“Unafiki
tu. Wakati kumejaa hofu na...” “Twende Jamal. Hakuna wakukusikiliza hapa.” “Una
dakika moja yakuondoka ofisini kwangu Njama. Ukiisha huo muda na bado umesimama
hapo, utakuja kutolewa. Na ukitolewa hapa, ujue hutakaa ukarudi hapa ndani.
Kama unafikiri nakutisha, ujue zimebaki sekunde 40 tu.” Joshua akanyanyua
simu. “Niitie askari.” Akamuamuru Fina.
Fina
akatekeleza alichotumwa na bosi wake, kisha akamfuata Njama pale ofisini kwa
Joshua. “Kwa nini umeamua kupigana na ukuta Njama?! Umepatwa na nini mdogo
wangu?” “Mimi sijakataa kutoka ila nataka ku...” “Umeambiwa nini? Fuata
utaratibu!” “Yameanza lini?” “JANA. Na wewe ndiye umeyaanzisha yote haya Njama!
Sasa kwa nini hutaki kufuata utaratibu ulioanzisha wewe mwenyewe? Toka kabla
hujatolewa!” Njama akatoka akabaki Fina. “Joshua, naomba nipe siku ya leo tu.
Nitazungumza naye, atatulia.” “Iwe hivyo Fina. Nataka tufanye kazi, sina muda
wa malumbano. Ifikapo jioni awe yupo tayari kufanya kazi kama timu, na
sivinginevyo.” “Sawa, Joshua.” Wakaingia askari wakimtafuta Fina.
Akatoka
kwa haraka. “Kila kitu kipo sawa. Samahanini kwa usumbufu.” Joshua akamsikia
Fina akituliza hao askari. Akawasikia wakitaka kujua ni kwa nini waliitwa hapo,
nao wakaweka ulazima. Fina akajua Joshua anasikiliza, hawezi kudanganya.
“Yameisha. Mnaweza kuondoka tu.” “Sisi kama watu wa usalama ni lazima kutunza
rekodi ya cha chochote kinachotokea humu ndani ya kampuni. Hata kama
mnamalizana nyinyi kwa nyinyi, nilazima na sisi tujue. Ili ikija kutokea tena,
tunakuwa na kumbukumbu yetu.” Ikamlazimu sasa Fina kueleza kwa ufupi wakaandika
kila kitu na kuchukua jina kamili la Njama.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Joshua
akaendelea na kazi, tena akaanza kufanya kazi ileile aliyompa Jamal ila kwa
kiwango kikubwa na kizuri. Baada ya muda Fina akampigia simu kumwambia Jema
anataka kumuona. Akajua na yeye amepata ujumbe. “Baada
ya kama dakika 5, tafadhali.” Akajibu Joshua na kukata simu.
Haikuwa kawaida yao hata kidogo. Jema akajua Joshua amekasirika sana. Akatulia
hapo nje akingalia muda. Ilipotimu dakika 5 tu, akagonga na kuingia.
Joshua
akanyanyua kichwa na kumtizama. “Nina mambo mawili.” Jema akajikaribisha kwa
kuvuta kiti na kukaa mbele yake. Joshua kimya akimtizama. “Wanawake wengi
wakiwa kwenye hali kama ya Naya, huwa wanakuaga na hamu na kitu fulani. Inaweza
ikawa sio chakula kile chakushiba. Lakini unajikuta labda una hamu ya kitu
kitamu. Labda chocolate. Wengine inakuwa ni keki na iwe keki maalumu. Labda
vanilla tu, au chokoleti. Haya wengine ubuyu, au ice cream na mengine mengi
tofauti tofauti. Kila mmoja anakuwa na hamu ya kitu chake. Wewe unajua
Naya anapenda nini?” Joshua akatulia kidogo, lakini akamuona mpaka uso
umebadilika, akacheka kidogo.
“Kweli
sikuwa najua hilo!” “Basi iwe ndio kazi ya leo. Umdodose ili ukienda jioni,
uende na hicho kitu. Na ukijua mapema, naweza nikamtuma mtu akakununulie ili
ukienda, uwe nacho.” Hapo akawa amempata Joshua, hata uso ulionyesha
amefurahia. “Sawa. Na ninashukuru kwa wazo.” Hapo Joshua akatulia kabisaa. Jema
akamfanya atulie hata kuweza kumsikiliza kwenye mambo ya kazi.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kila
mtu akiwa anaendelea na kazi siku hiyo baada ya chakula cha mchana, Njama
akapata simu kuwa anaitwa kwenye ofisi ya usalama hapo kazini. Fina akaingiwa
na wasiwasi. Njama akaenda asijue hata kama kulikuwa na hiyo ofisi hapo.
Alihojiwa kwa muda mrefu tu huku maelezo yake yakiandikwa. Akaongea mengi na
kukanusha askari wakimsiliza tu.
Baada
ya kama lisaa tena Fina akapigiwa simu kutoka kitengo cha Parsonel Relations au
HR relations ambacho ni kitengo maalumu kwa mambo ya nidhamu kilichopo ndani ya
ofisi ya mwajiri, HR kwa kifupi cha Human Resources, tena na Mama
Masinga. “Ametoka kidogo, ila nitamtaarifu kuwa
unamtafuta.” “Na mwambie aangalie email yake. Hajajibu kama ameipata.” Mama
Masinga akakata simu hofu ikamwingia Fina zaidi. Alijua mambo yameshafika
mbali.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Akili
ya Joshua ikawa imehamishiwa kwa Naya. Akawa ana kazi ya kuangalia simu yake
kila wakati kuona kama Naya ameamka na kama amemtafuta. Akaamua kuiweka mezani
kabisa ili ujumbe utakapoingia tu, asome bila kuchelewa. “Mama Masinga amepiga
simu anakutafuta.” Fina akasikika. “Jamaa ashaenda kuniharibia nini?” Akasikia
Njama akimuuliza Fina. “Wewe unamjua Joshua. Hana muda wa kijinga kama wewe
Njama. Umeingiwa na nini Njama!?” “Nilikuwa nawajibu wale askari, bwana.
Walidhani nina silaha. Wameniweka muda kweli!”
“Acha
kunizunguka Njama! Ni nini kinakupata wewe!? Kweli unataka kuharibu maisha yako
sababu ya mwanamke!?” “Mimi sitaki kudhulimuwa Fina. Sipendi ujinga.” “Sawa
Njama! Na mimi nakuwa kama Jema kukuonya. Unashindana pabaya sana.” “Kwani
watanifanya nini!? Mimi sio mjinga Fina.” Akapunguza sauti kama asisikike na
wengine na kuendelea. “Nishazungumza na mwanasheria anayejua maswala yahaki za
wafanyakazi.” Joshua akaona simu yake ya mezani kwake, inawaka taa, kutokea kwa
Fina. Akabonyeza bila kuzungumza lakini akasikia sauti ya Njama akizungumza kwa
sauti ya chini kidogo. Akatulia, akijua Fina anataka amsikilize na yeye.
“Nishazungumza na huyo mwanasheria. Nimemweleza kila kitu
kuhusu hapa. Nasubiri wajichanganye tu, niwashitaki na ameniambia makampuni
mengi huwa hayapendi kesi, wanapenda kumaliza kesi kimyakimya. Utashangaa sana
Fina, nitaondoka hapa na mabilioni ya pesa na kukuacha hapa unahangaika
na kutengenezea waume za watu chai na kuwapelekea maji kila wakati.” Fina
akashangaa sana mpaka akaangalia simu kama Joshua ameweza kusikia.
“Mjini hapa Fina! Jamaa anajidai ndio mungu wa hapa. Na
makaburu wanamtetemekea! Sasa itawagarimu. Na watanijua mimi ndio Njama,
mtoto wa jiji.” “Yaani fujo zote hizo kumbe ili ufukuzwe kazi halafu
ukaanzishe kesi uje ulipwe fidia?!” Joshua akatulia
akisikiliza. “Siwezi nikaendelea kuwa mtumwa wa
mwanaume mwenzangu! Wote tunakimbia kama wajinga! Akifungua yeye mdomo kampuni
nzima inatetemeka mpaka wanawake zetu wanamkimbilia yeye! Sifanyi huo ujinga
aisee. Na siondoki kijinga. Hilo ujue. Kila kitu naandika.” Fina
akaingiwa hofu akimshangaa sana, asiwe na uhakika kama Joshua amesikia yale
yote.
“Nashauri nenda kamuone mama Masinga.” “Naye yule ni walewale tu
kama Jema na haya makaburu. Sijui jamaa analoga wapi!? Wakimuona wanakimbia
kama wajinga! Kama anadhani uchawi wake unampata kila mtu hapa duniani mpaka
makaburu aliyoyafanya majinga basi ajue hapa amegonga mwamba. Akaloge tena.”
“Ndio unatakiwa ujue Njama, kama mpaka mtu kama mama Masinga anafanya hivyo
ujue ni kwa kuwa amejua siri.” “Sasa wewe muache ajichanganye.
Nitawanyoosha hapa, hawatakaa wakanisahau. Faida yote ya huu mwaka, itaishia
mfukoni kwangu.” Fina mpaka akaogopa na kunyamaza kabisa, Njama
akaondoka akicheka kwa ushindi.
Naya
kwa Joshua.
‘Najisikia
vibaya jinsi nilivyokufanyia asubuhi, Joshua. Tafadhali naomba unisamehe na
usinielewe vibaya. Sipo kama ulivyoniona asubuhi. Hata mimi sijui nilipatwa na
nini! Nisamehe tafadhali. Na naomba usichoke shukurani zangu za kuwa na mimi
hospitalini. Nakushukuru sana. Na samahani kwa usumbufu.’ Huo
ujumbe ukaingia kwenye simu ya Joshua na kumtoa mawazoni. Akajua Naya ameamka.
Hapohapo akapiga. “Vipi sasa hivi unajisikiaje?!” “Najisikia vizuri. Asante kwa
kujali. Ulisoma ujumbe wangu wote?” Joshua akacheka
taratibu. “Nilikwambia hamna shida Naya.” “Hapana Joshua. Si sawa. Mimi sitaki
uje unifanyie hivyo. Ingeniuma sana.” “Ujue haitakaa ikatokea hata siku moja.
Kwa sababu sitataka muda wa kuwa peke yangu mbali na wewe Naya na sihitaji
kufikiria kama nakuhitaji maishani au la. Najua kwa hakika nakuhitaji. Hata
Mungu anajua nakuhitaji .” Naya kajisikia vibaya zaidi.
“Unazidi
kuniumiza Joshua!” “Hapana Naya. Sio nia yangu, nakwambia tu ukweli.” Naya
akajifuta machozi. “Naomba nisamehe. Hakika nimejisikia ni kama vile Malon
alivyokuwa akinifanyia mimi. Wakati wote nilikuwa nikimuonyesha namtaka yeye,
na yeye hakuwahi kulithamini hilo! Ikawa mimi ndio nina kazi ya kumfuata nyuma
hata alipokosa ilibidi kumfuata na kumtangazia msamaha ili turudi kuwa wote
kwenye mahusiano. Sitaki na mimi nikufanyie hivyo Joshua. Najua nimekukosea.
Nimemuomba na Mungu msamaha, nimejionya, sitarudia tena. Kabla
sijazungumza neno au kukufanyia kitu, nimeomba Mungu anisaidie kunikumbusha.
Sitaki kukuumiza Joshua. Mimi nimekuwa kama hivyo wewe. Ikawa nipo na maumivu
wakati wote. Ikafanyika kama adhabu! Sitaki na wewe nikupitishe hapo.
Hustahili. Ni bora nikishindwa nikwambie mapema, kuliko kukufanya uishi kwenye
mateso.” “Tafadhali naomba usishindwe Naya. Hapo ndio nitaumia zaidi.
Nakuahidi kukuombea.” Naya akaumia zaidi. Akabaki kimya.
“Nakupenda
Naya. Naamini ipo siku na mimi nitakufanya uwe na furaha tu.” Naya
akaumia sana. “Unanifanya niwe na furaha Joshua.” Joshua
akanyamaza. “Kweli. Ni vile maisha yamenipitisha kwa wanaume waajabu ajabu sana.
Wakautia tatizo moyo wangu mpaka nimekuwa kama nimekufa ganzi! Nasubiri tu
chochote tena kitokee. Na imekuwa hata na kwako pia. Nakuwa nasitasita.”
“Nimeliona hilo. Moyo wako upo mguu mmoja ndani na mwingine nje. Ukijua na mimi
ni walewale tu. Kuna mwanzo mzuri ila mabadiliko mabaya mbeleni.” Hapo Joshua akawa
amemziba mdomo.
“Lakini
Naya, kama umenisikiliza vizuri, mwanzoni kabisa mimi sikuvutiwa na chochote
chako cha nje. Mungu aliniunganisha moyo wangu na wako mpaka ikabidi sasa
nianze kukuangalia mtu wa nje, kwa sababu ndani nilijua Mungu ameshakuleta
kwangu. Ndipo nikabaki kukutizama nje kujua safari hii Mungu amenipa zawadi ya
namna gani! Ndio maana naamini, kama hutanikimbia, Mungu atatusaidia tu. Usiogope.
Tupo kwenye mpango na makusudi ya Mungu. Atatuponya na kote tulikopita na
kujeruhiwa. Atatuwezesha kuchukuliana pia.”
“Natamani
ningekutana na wewe muda mrefu Joshua!” “Mungu alijua sikuwa tayari, Naya. Bado
alikuwa akiniandaa kuja kuwa mume wako. Huu ndio wakati wa Mungu. Ndio maana
nina imani kubwa na huu wakati wa Bwana. Tutakuwa sawa tu. Naamini
hatujachelewa.” “Sasa huoni kama Mungu amekupa kitu kisicho kikamilifu?” Naya
akauliza akimuhurumia.
“Kwa kuwa
bado hujaunganishwa na mimi Naya. Wewe ni mfupa kutoka kwangu na nyama
zilizotolewa kwangu. Huwezi kukamilika, au hata mimi sikamiliki mpaka wewe.” Naya
akashangaa hiyo hekima. “Jamani Joshua! Mpaka nimekuwa na hamu ya kukuona tena!” Joshua
akacheka. “Nitakuja kukuona. Unataka nikuletee nini?” “Nakutaka wewe.” Joshua
akacheka tena taratibu. “Mimi nitakuja. Lakini niambie unahamu ya nini?” Naya
akatulia kama anayesita kusema kisha akamsikia kama akicheka akiwa mawazoni.
“Hichohicho
ulichokicheka ndicho nataka uniambie.” “Chakijinga!” Naya
akajibu akicheka. “Ndicho hichohicho nataka kujua.” “Kwanza natamani kula kitu kitamu.
Chenye sukari, lakini sio soda.” Joshua akajua Jema
alikuwa sahihi. “Kuna chocolate fulani hivi tulikuwa tunazinunua. Sio nyeusi sana,
ni kama zinakaribia rangi hizo. Basi tulikuwa tukinunua nyingi, zinakuwa kwenye
friza. Siku ninazopatwa hamu nazo, natoa kwenye friza, nakula zikiwa zimeganda
kama barafu. Ni leo tu nilikuwa nakumbuka hilo. Basi nilikuwa nikifurahia, japo
sikuwa nikila kila wakati. Ni mara mojamoja tu ninapopatwa hamu kama leo,
lakini tulihakikisha siishiwi. Zinakuwepo ili kila ninapojisikia kula, nipate.
Lakini hiyo nizaidi hata ya mwaka sasa! Sijui leo imekuaje nikakumbuka!” Joshua
akacheka taratibu akifikiria.
Lakini
akajua ni Malon ndiye aliyekuwa akimnunulia hizo. “Kuna jina
maalumu za hiyo chocolate unataka?” “Sasa sijui kama nilipendea jina au aina!
Japo Malon aliji...” Akanyamaza. “Ni sawa tu. Niambie.” “Samahani
Joshua.” “Hatuwezi kuepuka hilo. Ehe?” Joshua akataka
aendelee. “Alikuwa akinunua aina hiyohiyo moja. Brand name hiyohiyo.”
“Zinapatikana hapa nchini?” “Nilikwenda na Malo, mara moja tu. Akaninunulia.
Nikazipenda sana, kwa hiyo yeye ndio akabakiwa na kazi yakuzinunua aina
hizohizo na kuziweka kwa wingi kwenye friza, ili niwe nazipata kila wakati
ninaohitaji. Sikufuatilia tena ununuaji wake kujua ni wapi aliendelea
kuzipata.” Naya akamuelekeza mpaka sehemu waliyonunua kwa mara ya
kwanza na kumtajia jina lake.
“Basi
nitakwenda kuziangalia.” “Lakini usisumbuke Joshua. Sio kwamba ni kitu ambacho
sitaweza kuishi bila hicho. Ni hamu inayonijia mara chache sana.” “Usijali.
Umekula vizuri lakini?” “Nilikunywa tena ile supu niliyoletewa na Jozee
hospitalini.” “Na hukutapika?” “Hata kidogo. Najisikia mzima kabisa. Nilikuwa
nimekaa tu hapa kitandani na baba Naya. Ametoka hapa muda si mrefu. Nilimuita
nilipoamka na kukukosa wewe, nikajua ulishakwenda kazini. Ikabidi nimuite baba
Naya, nikae naye.” Joshua akacheka.
“Pole.”
“Ndiye mnyonge wangu. Ameshanizoea. Eti haamini kama kweli nilikuwa
hospitalini, mpaka nikawekewa maji, bila kukutaka umpigie aje!” Joshua
akacheka. “Mpaka ikabidi nimuonyeshe nilipochomwa sindano. Eti anasema ni
muujiza.” Wakacheka hao wawili, Joshua akamsimulia alichoambiwa na
Zayoni. “Wala hakukudanganya. Huwa siponagi bila baba. Leo yeye mwenyewe
ameona ni muujiza! Mama mwenyewe alishajua. Hata nikiumia tu, atampigia baba
simu na kumtaka arudi nyumbani. Lasivyo nalia, na sitanyamaza mpaka baba aje.
Hapo matibabu yeyote ukinipa ndio yatafanya kazi. Na ninahisi ni imani tu.” Wakaendelea
kucheka.
Wakati
Joshua alipokuwa akizungumza na Naya, hapo hapo akamtumia ujumbe mama Masinga
kwenye simu yake ya mkononi. ‘Kuwa makini sana na huyo
kijana. Anayoyatenda kumbe ni makusudi tu. Anakusanya ushahidi ili kuweza
kushitaki kampuni kwa ajili ya mabilioni ya fidia.’ Mama
Masinga alishituka baada ya kusoma ule ujumbe. Lakini akajibu. ‘Hakika
nakushukuru Kumu. Leo ningeharibu.’ Joshua hakujibu tena.
Akaendelea kumsikiliza Naya.
Njama Kwa Mama Masinga.
Njama
alifika kwa mama Masinga, hata yeye alikubaliana na Joshua. Alijawa jeuri.
Majibu mabaya kama aliyekuwa akimtafutia sababu. “Kwanza nataka kujua ni kwa
nini nipo hapa, muda huu wa kazi. Sikusikii unachongea, unanipotezea tu muda.”
Mama Masinga hakumjibu. Akanyanyua simu na kumuita Afisa Mkuu mwajiri na
kumuomba afike hapo ofisini kwake mara moja. Alishazungumza naye kile
alichoambiwa na Joshua kabla ya Njama hajafika hapo. Bila kupoteza muda, akafika
hapo.
“Hakuna
tatizo. Ila naona tunashindwa kuelewana na Njama. Nilitaka mtu wa tatu.” “Labda
kabla sijaendelea, naomba haya mambo yaende kiofisi kama Njama mwenyewe
anavyopendelea.” Akaitwa sekretari, akaambiwa aje na rikodi. Njama akashangaa.
Akaambiwa akae hapo aandike na arikodi yale mazungumzo. “Labda nikuulize Njama.
Unajua ni kwa nini umeitwa na Personel Manager? Sio mama Masinga kama yeye,
hapana. Yeye kama anayehusika na mambo yetu wafanyakazi hapa kwenye hii
kampuni?” Afisa Mkuu wa ajira kwenye kampuni hiyo Tanzania nzima akamuuliza kwa
heshima tu. “Ameongea mambo ambayo hayaeleweki. Hayana mashiko ni kama majungu
tu.” Akajibu Njama bila heshima. Yule mama akacheka tu lakini sekretari alishituka
mpaka akashindwa kuandika.
“Basi
naomba mimi niliweke hili swala wazi.” Akaendelea. “Afisa wa mambo ya usalama
hapa kwenye hii kampuni, amekuja akishitaki kwanza fujo ulizofanya ofisini kwa
Joshua na matusi mengi uliyozungumza getini ukitukana uongozi wa hapa.” “Upo
ushahidi au hayo ni majungu tu?” “Nilikuwa nikizungumza mimi bwana Njama.
Naomba nimalize.” Pakatulia. “Sasa kwa kuwa mama Masinga ndiye anayehusika na
hayo mambo nikamuomba yeye ndio azungumze na wewe kujua kama lipo tatizo. Kama
ataweza kulitatua, basi afanye hivyo au achukue malalamiko yako apeleke mahali
husika.” “Kwanza ninahisi kudhulumiwa na sidhani kama mtaweza kunisaidia.”
Akaanza Njama.
“Siwezi
kufanyiwa mambo ya dharau. Mimi nazijua haki zangu.” “Ni katika upande upi?”
Mama Masinga akauliza. “Jamaa yenu ananiambia eti mimi nikabidhi kazi
niliyofanya mimi mwenyewe, kwa mtu kama Jamal!” “Unamaanisha nini ukisema mtu
kama Jamal?” “Mdogo kwangu kwa majukumu!” “Labda kabla hujaendelea Njama,
labda nikusaidie jambo moja mimi kama Afisa Mwajiri. Hukuwahi kubadilishiwa
cheo, ila majukumu. Narudia tena Njama, ulipo sasa hivi ni nafasi aliyoiunda
Joshua, akakutaka wewe uwepo ili kumrahisishia kazi ya vikao na kila mtu
asubuhi. Akakutaka wewe uwepo pale, mtu mmoja tu, utakayeelewa kwa upesi
anachotaka kifanyike, kisha wewe sasa, uweze kufikia wenzako pale kitengoni.
Sijui kama umenielewa? Maana kama hilo linasumbua, na umekosa imani na sisi,
tafuta mwanasheria wa nje ambaye atakusaidia kukuelewesha.” “Hilo halina
mashaka. Nikishindwa kupata haki zangu hapa, nitazitafuta popote.” “Hilo ni
wazo zuri.”
“Kama
nimekuelewa vizuri Njama, leo umegoma kufanya kile ulichotumwa na mkuu wa
kitengo chako! Si ndiyo?” Mama Masinga akauliza kutaka uhakika. “Si kugoma, ila
kutokukubaliana naye.” “Na ndipo ukaanzisha fujo ofisini kwake?” “Jamaa ni mjinga
kabisa. Ndivyo alivyokuja kujiliza kwenu!?” “Acha matusi Njama. Na hapa
upo si kwa sababu ya Joshua, ila watu wa usalama. Tumekuita kwa heshima kabisa,
kutaka kujua tatizo lipo wapi? Kama unashindwa kufanya kazi na wenzio kwa
sababu ya kuona wapo chini yako sana, nalo hilo nataka kujua.” “Huo ni uzushi.”
“Sio wewe
uliyekuja ukiwa na malalamiko juu ya Naya uliyetumwa kufanya naye kazi, lakini
ulisema umeshindwa kwa sababu alichelewa kwa dakika 9?” “Naya ali..” “Na leo
unafanya fujo zote hizo kwa sababu umeambiwa umshirikishe Jamal kazi
uliyofanya?” Njama akababaika ila akajitetea. “Kwani Joshua huwa anatoa kazi
zake kabla hajakamilisha?” “Maelezo uliyotoa getini ulisema ulikuwepo ofisini
kwa Joshua kumkabidhi kazi aliyokuwa amekupa. Ila tatizo lilitokea pale
alipokwambia umpe Jamal! Je, hayo nayo ni uzushi unataka kurudi tena ofisi za Usalama
kubadilisha?” “Mimi sijui wamekwambia nini, lakini ninachotaka kusema, hamuwezi
kunionea. Nazijua haki zangu.” Hicho kikao kiliendelea bila kufikia
mwafaka.
Joshua kwa Naya.
Alipomaliza
mambo yake pale ofisini kwa siku hiyo, Joshua akampigia simu Fina kumtaka
amletee chocolate ambazo alishaagiza na kutaka baadhi ziwekwe kwenye friza.
Fina akaleta zote bila kuchelewa. Joshua akamshukuru bila hata kuzungumzia
maswala ya Njama. Akashangaa sana. “Nakushukuru Fina. You are the best.”
Alishazoea hiyo sifa. Akacheka. Akatamani kama Joshua angeanzisha hayo
mazungumzo, lakini alionekana na haraka yakuwahi kutoka. Fina akatoka bila
nyongeza. Joshua alimwambia dereva hatahitaji usafiri jioni hiyo, akatoka na
gari yake mbio akiwahi Kiluvya nyumbani kwa kina Naya akiwa na matunda
pamoja na galoni ya maziwa, juisi, kreti ya soda aina ya Sprite. Na vyote hivyo
aliagiza mara baada ya kuzungumza na Naya. Hahutaka kwenda ukweni mikono
mitupu.
Naya
alijikuta moyo ukifurahia geti lilipokuwa likifunguliwa na Zayoni, akajua ni
Joshua tu. Hawakuwa na mgeni wa kuwatembelea usiku huo, tena na gari! Akajua
huyo ni lazima ni Joshua. Akatoka na yeye. Gari ya Joshua ikawa ikiingia, Naya
akajikuta akipunga mkono na giza hilo. Joshua alimuona, akacheka. Akafungua
kioo na kutoa mkono kumpungia na yeye huku akisogeza gari karibu zaidi. Naya
akacheka. Kwa kumuona Naya nje, tena mida ile, Joshua akajua anasubiriwa
kwa hamu. Akashuka garini akiwa amejawa tabasamu, Naya akamfuata.
“Nimefurahi
umekuja Joshua.” “Na mimi nimefurahi kuja.” “Kweli? Sio usumbufu kwako kuja
mpaka mbali kote huku!?” “Kama isingekuwa kuja huku, inamaana ningekuwa
nyumbani peke yangu. Ni bora hivi kuja kukuona wewe.” Naya akacheka kwa furaha.
Akamshika mkono. Zayoni akawasogelea kutoka getini. Akamsalimia
Joshua. “Upo msafi! Halafu unanukia kama zile nguo za Naya nilizomsaidia kufua
leo.” Naya na Joshua wakacheka. “Nilikwambia pafyumu yako inanukia vizuri na
inakaa kwenye nguo muda mrefu.” “Asante Zayoni. Habari za kushinda?” “Nzuri.
Leo nilikuwa nikimsaidia baba kazi kwenye fremu yake mpya. Naya amekwambia kama
tunataka kufungua duka la mazao kule Kibaha?” “Bado.” Joshua akajibu huku
akimwangalia Naya.
“Tunapajenga.
Namsaidia baba kupaka rangi, halafu kupajengea vizuri. Naya amesema akipona
atakuwa akiungana na sisi zaidi siku ya jumamosi. Si unajua siku za jumamosi
huwa anafanya kazi nusu siku?” “Nafahamu Zayoni.” “Basi atakuwa akija
kutusaidia mimi na baba.” “Unafanya vizuri kumsaidia baba, Zayoni. Na mimi
nikipata nafasi nitakuja.” “Wewe utachafuka.” Mpaka Naya akacheka.
“Kweli Naya. Mwambie jinsi kulivyo kuchafu!” “Ni kijijumba kilichokuwa
kimetelekezwa sehemu. Ndio baba amekodisha hapo anapakarabati. Kweli ni
pachafu, bado hata hapajachukua sura yeyote ile. Tutakukaribisha pakitengemaa.”
“Mimi sitaki kuwa mgeni ramsi. Nataka na mimi niwe katika wakaribishaji.” “Basi
tutakwenda wote siku ya jumamosi.” Zayoni akafurahia na kukimbilia ndani
kumwambia baba yake. Akawaacha wakicheka hapo pembeni ya gari.
“Njoo
hapa.” Akamvutia kwenye gari yake na kumuegemeza. “Funga macho na uwe
mwaminifu.” Naya akaanza kucheka. “Naya!” “Nafunga na sitachungulia.” “Sawa.”
Joshua akajaribu kupitisha mkono mbele ya macho, akagundua kweli amefunga.
“Haya. Subiri.” Naya akaendelea kucheka akiwa amefunga macho. Akamsikia
akifungua mlango wa gari, baada ya muda mfupi akamsikia akifunga tena. “Bado
umefunga?” “Kabisa.” Naya akajibu akicheka. “Kumbe wewe mzuri wa suprise?”
“Sana. Ushindwe tu wewe.” Joshua akacheka sana.
“Sawa.
Sasa bila kufungua macho, fungua mdomo.” Naya akawa ameshaelewa. Akacheka sana.
Kisha akafungua mdomo, Joshua akamuwekea chocolate mdomoni
ilikuwa baridi haswa. Naya alisikia kuburudika mpaka kwenye nafsi. “Fungua sasa
macho!” “Acha kwanza nile hata mbili! Kama naota niwe nimefaidi ndotoni.”
Joshua akacheka, akacheka sana. “Acha utundu Naya! Niangalie bwana nijue kama
umependa.” “Sana Joshua. Sikutegemea kuzipata leo. Nilizikumbuka tu, nikajionya
na kujiambia nayo hiyo enzi yake imepita. Asante Joshua.” “Karibu. Kama
umefurahia na mimi nimefurahi. Nimekununulia nyingi na zimeganda.”
“Nimeona. Naomba na wewe uonje Joshua. Ni nzuri sana.” Joshua akacheka na kumuwekea
nyingine mdomoni na yeye akaonja moja, kweli akapenda.
“Ni
nzuri.” “Sasa utakuwa ukielewa ni kwa nini tulikuwa tukizipenda. Nzuri sana.
Halafu nyingine alikuwa aki...” Naya akashituka mpaka usoni. Akamshika mkono.
“Twende ukamsalimie baba Naya.” Akabadili mazungumzo akiwa anamvuta kidogo.
Joshua akajivuta nyuma na kukunja mikono. “Maliza ulichokuwa ukitaka
kuniambia.” “Ni nzuri sana.” Joshua akakunja uso. “Nilitaka
kukwambia hata Malon alikuwa akizipenda.” “Naomba usinidanganye Naya. Naogopa
sana kudanganywa, ni heri usiniambie kuliko kunidanganya.” “Kweli hata
Malo alikuwa akizipenda. Sidanganyi.” “Lakini sicho ulichotaka
kuniambia.” “Hapana.” Naya akajisalimisha. Joshua akatulia akimwangalia.
“Karibu
ndani.” Naya akapoa kabisa mpaka usoni. “Nakupenda Naya.” Naya akaingiwa hofu.
“Naomba usinikatie tamaa Joshua.” “Kweli? Maana sitaki kukupotezea muda au
kujaa kwenye maisha yako halafu ikaja kuwa ni kero tu.” “Mbona kama umeanza
kunikatia tamaa Joshua! Uliniambia Mungu ame, ame...” Naya akashindwa hata
kumalizia. Akanyamaza. “Wewe unaniamini?” “Nakuamini sio tapeli.” “Hapana Naya.
Unaamini kama ni mtu ambaye naweza kuzungumza na wewe na kukusikiliza na bado
ukabaki salama?” “Sijui Joshua! Sijui ni kwa kiasi gani naweza kuwa wazi
kwako.” “Unafikiri lini au kipi kitakufanya uwe wazi kwangu?” “Muda na
kufahamiana zaidi. Kukujua kama unao uwezo wakunifahamu hata kwa undani na bado
ukanipenda na usinihukumu. Kumbuka nilikwambia niliishia na Malo
kama mke kabisa, yaani kuishi naye nyumba moja!”
“Unakumbuka na mimi nilikwambia niliishia na
Benadina nyumba moja?” “Hata jina hukuwa umenitajia Joshua! Halafu hiyo ilikuwa
zamani sana kwako. Mimi ndio nimetoka kwenye mahusiano!” “Ni kweli umetoka?”
Joshua akauliza tena. “Nimetoka Joshua. Au umesahau nilivyozungumza na Malon
mbele yako, leo asubuhi?” “Sasa ni kwanini unashindwa kuniamini kama umeamua
kuwa na mimi?” “Nani amekwambia itakuwa rahisi Joshua?” Naya akauliza swali
mpaka akamshangaza Joshua.
“Nimeishi
na kujengwa na Malon kwa miaka zaidi ya 5, nikawa hivi nilivyo. Alimuondoa yule
Naya wa zamani na kumtengeneza huyu Naya aliyesimama hapa mbele yako. Nimejawa kutoamini
na kutomiliki. Nakuwa na mtu kama sipo naye hujui nini kitatokea kesho
au hata baada ya nusu saa! Na imekuwa hivyo kwenye historia yangu yote na
wanaume kasoro kwa baba tu. Ndiye mfano wa mwanaume ambaye najua anayo maadili
na anaweza kumvumilia mtu. Akasimama na huyo mtu katika kila nyakati, kwa
kumuona vile alivyoishi na mama. Wewe tuna siku chache tu pamoja. Nawezaje
kujenga imani kubwa na kujifunua kwako kwa kiasi hicho cha kukwambia kila
kitu?” Joshua akatulia.
“Nilikwambia
kwa asili mimi sina marafiki. Wala sijawahi kuwa na marafiki kwa hofu ya kuja
kugeukana kama nilivyokuwa nikiona kwa wengine. Nikajijengea tabia yakutunza
mambo yangu mimi mwenyewe. Hata Malon alipokuwa akiniumiza nilikuwa nikiyabeba
mwenyewe. Sina wakumwambia. Hata mama yangu mzazi hakuwa akijua kama naishi na
Malon kama mume. Nisingethubutu mimi mtoto wa kanisani kuja kulilia kusalitiwa
mapenzi kwenye familia kama yetu, wakati stori za baba na mama ni kwamba walisubiriana
mpaka walipoingia kwenye ndoa.”
“Haya,
walionizunguka wenyewe walikuwa wakitembea na Malon na wakimsubiria kwa hamu.
Wakipokezana huyo Malon kama mpira! Nikafungiwa uwanja wa kuzungumza na yeyote,
ila kupambana mwenyewe. Ni tabia iliyojengeka miaka na miaka. Nahitaji muda, na
kukujua uliposimama na mimi. Nijenge imani kwako na kujua kama naweza
kuzungumza kwako lolote na bado nikabaki salama, Joshua!” Kimya.
“Unakumbuka
nilipokuuliza huoni kama Mungu amekupa mtu asiyefaa?” Kimya. “Unakumbuka
jibu lako? Maana mimi najua nilipo Joshua. Moyo wangu umejeruhiwa vibaya
kweli. Niliishi maisha ya fedheha kwa muda mrefu sana nikikubali kudhalilika
sana ili niwe na Malo. Mpaka rafiki zake na wazazi wake wenyewe Malon, walikuwa
wakinishangaa. Na nilikwambia tokea Mbeya. Nilijua ni nini chakufanya,
lakini nilijawa hofu hata kukubaliana na taarifa ya nini chakufanya. Lakini
wewe mwenyewe, tena leo tu, ulinituliza Joshua. Ukaniambia sitakamilika bila
wewe!” Joshua akavuta pumzi kwa nguvu na kutulia kabisa.
“Haitakuwa
rahisi Joshua.” “Lakini ulisema inaweza ikawa rahisi! Wewe mwenyewe ulisema
Naya. Unakumbuka tulivyotoka kwa mara ya kwanza tukaenda kuendesha boti?”
“Nakumbuka Joshua.” “Basi nirahisishie Naya!” “Ukibahatika kunioa mimi
Joshua, utabaki ukimshukuru Mungu kila siku.” Joshua alicheka, akacheka sana.
“Naya!”
“Kweli tena. Ujue utapata mwanamke wakusimama na wewe katika kila hali. Halafu
mimi nitakuwa faraja yako. Sitakukimbia wala kuiba penzi la nje.
Utakuwa na uhakika wa maombi ya watu wawili. Yaani kule mbinguni wewe unakuwa unatajwatajwa
tu. Pakipoa kidogo tu, baba Naya anawakumbusha. Haya, bado na Naya
mwenyewe! Huwezi ukabakiwa hivyo ulivyo.” Joshua alicheka sana tena kwa sauti.
“Wewe hayo masomo uliyosomea yamekuharibu Naya.” “Biashara matangazo
Joshua.” Joshua hakuwa akiamini. Alibaki kucheka.
“Wewe
usikasirike Joshua. Maadamu mimi mwenyewe nimekuahidi nitakuwa na wewe, ujue
mimi ni wako tu. Hayo mengine nisaidie kunirekebisha taratibu.” “Hutakasirika?”
“Nitajitahidi.” Joshua akatingisha kichwa kama anayesikitika akimwangalia na
tabasamu. “Niambie kitu gani kingine.” “Niambie ulichotaka kuniambia ukasita.”
“Niamini mimi, hutaki kujua Joshua. Ila kwa kuanza tu kutaka kukwambia,
ujue moyo wangu unaanza kufunguka kwako. Nipe muda.” “Ni juu ya nini? Maana
kama ni Malon, usiwe na wasiwasi.” Akamuona anamwangalia kisha akaanza
kutingisha kichwa taratibu akikataa kama anayepingana na wazo la kwamwambia.
“Ni nini
hicho?” “Joshua wewe! Nikikwambia kitu hutakiwi kujua, basi amini hivyo
na uache.” “Basi ndio udhaifu wangu huo mwingine na wewe unatakiwa kuuvumilia.”
“Joshua, tafadhali tuzungumze jambo jingine kama habari za kazini.” “Nzuri
kabisa. Lakini bado nataka kujua.”
“Kama
utang’ang’ania hivyo. Nashauri ukamsalimie baba kwa kuwa ameshajua umekuja hapa
ndipo utoke hapa. Tukae hapo kwenye ngazi nikwambie. Maana...” “Unahisi
nitakimbia?” Naya akatulia tu akimwangalia. Joshua akachukua mizigo kutoka
kwenye gari na kumpita Naya akielekea ndani. “Acha nikupokee.” Joshua
akamsubiria, akampa baadhi, mingine akabeba mwenyewe. Wakaingia ndani.
“Naona
unaongeleshwa tu hapo nje na kila mtu humu ndani, huna wakukukaribisha ndani!”
Wakacheka. “Hamna shida mzee wangu. Shikamoo.” Wakapeana mkono na kusalimiana.
“Naona Bale anarekebisha chakula huko jikoni.” “Basi acha nisubirie na Naya
hapo nje. Maana niliambiwa mapishi hayataki mikono mingi.” Wakacheka. “Mimi
ndivyo nilivyoambiwa. Ningesaidia.” Wakataniana kidogo ndipo wakatoka na Naya
ila Bale hata hakusogea hapo kumsalimia Joshua japo walikuwa wakimuona hapo
jikoni. Naya aliumia, lakini akanyamaza tu. Akajua bado anahasira na Joshua
sababu ya gari Naya alilorudisha kwa Malon.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Naomba
kesho nirudi kazini.” Akaanza Naya mara baada ya kukaa tu nje. Walikaa kwenye
ngazi. “Una ED ya siku mbili! Unatakiwa kupumzika, Naya.” “Unaona hivyo vichwa
vyote humo ndani?” Joshua akanyamaza. “Vinategemea kazi moja tu kwa sasa. Hiyo
ya Coca. Leo Bale ametoka chuo katikati ya juma la mitihani, ili kuja
kuniangalia mimi kama dada yake, lakini pia anahofia nisije poteza hii kazi.”
“Haitakaa ikatokea.” “Basi naomba kesho nirudi Joshua. Tafadhali.” “Haina shida
kabisa. Ila nilitaka tu upumzike.” “Sio kwa sasa, tafadhali. Najua ipo siku
tutakuja kupumzika, lakini sasa hivi tupo kwenye kupambana ili kujikwamua
kiuchumi.” “Ndio maana hata mmerudia kufanya kazi na Malon?” Joshua
akaunganisha swali lililopo moyoni akikumbuka mazungumzo yao ya mwisho, Naya
mwenyewe alisema hawatafanya naye biashara.
“Ndiyo na
hapana.” Naya akatulia kidogo na kuanza kusugua mikono taratibu huku
akifikiria. “Malon alikuwa akinifanyia mambo mengi mazuri sana Joshua. Sana.
Yaliyokuwa yakinifanya nakuwa kama mwendawazimu kwa kuwa nilikuwa ninajua
ndivyo anavyowafanyia watu wengine.” “Unamaanisha wanawake wengine?” Naya
akatulia kidogo. “Kama mambo ya chocolate?” Naya akamwangalia na
kucheka kwa kujidharau. “Ila alisema hafiki umbali huo na wanawake wengine.
Anakuwa anawaonea kinyaa. Kwanza umejuaje kama...” “Wewe umeniambia.” Naya
akakunja uso kwa woga kidogo. “Sijasema Joshua! Wewe
ndio...” Akasita na kubaki akimtizama.
“Anyway,
mbali na mapenzi, Malon alikuwa akinifanya situlii. Nilijawa hofu na fedheha ya
usaliti kila wakati, kila mahali. Si kwenye mahoteli au baa, lazima utakutana
na wanawake asilimia kubwa tu, alishalala nao, zaidi pale Morogoro. Chuoni,
shuleni au hosteli nilizokuwa nikiwepo, sikuwahi kujikuta nipo peke yangu.
Sikuwahi kutulia. Kumpenda Malo ikawa kama adhabu kwangu. Chungu na tamu.
Kumuacha siwezi kwa vile anavyonifanya nijisikie kwa muda ninaokuwa naye,
tofauti na wewe.” Hapo Joshua akakaa vizuri kumsikiliza.
“Hatujafika
umbali mrefu na wewe Joshua. Sikufahamu au hunifahamu kwa undani, lakini
nimejawa amani ya ajabu. Ile tu kuwa na mimi inanituliza. Sifa zako nimezisikia
pale kazini kwa vijana na wazee, mpaka nasikia fahari wewe kunichagua mimi!
Nafurahia kuwepo kazini. Nafurahia kulala ukiwa masikioni kwangu kwa kuwa najua
kesho utabaki kuwa Joshua yuleyule niliyekuacha usiku. Unajiheshimu Joshua,
kitu kinachonipa heshima na mimi sio kama nilivyokuwa nikidhalilika! Uthamani
wangu umeongezeka kwa mimi kujulikana nimechaguliwa na wewe!” Joshua akacheka
kidogo.
“Halafu
mbali na yote, wewe ni mtu mzuri Joshua. Mzuri sana. Kwa muda mfupi
niliokuwa na wewe, tukapita hali zote hata kukukera mpaka mwisho, lakini
nimekuona jinsi ulivyo na stamina ya kuhimili mshindo, upo kama baba
yangu.” Joshua akakunja uso kidogo. “Hiyo ni habari nyingine lakini baba yangu
ni mvumilivu mno Joshua. Kifo cha mama kimemuumiza baba si kupoteza mke, ila
kukosa nafasi yakumdhihirishia kuwa anaweza kumpa anachokitaka.”
“Kivipi?” Naya akacheka kidogo.
“Nadhani
kwa namna fulani umeshaelewa sisi ni watu wa namna gani. Kwa aina ya mazingira
yetu tu. Na si kwamba tumeamua kuwa hivi. Kuishi kwenye nyumba kama hii au
kutumia thamani za aina hizo unazoziona hapo ndani kwetu, au hatujui vitu
vizuri! Hapana. Ni uwezo tu. Mama amekufa akiwa analipia mikopo ya pesa
alizokopa kujenga hii nyumba. Kwa biashara ya kusambaza mayai na maziwa pamoja
na kuku tulifanya kipindi fulani, vilisaidia kulipa madeni mengi sana
tuliyokuwa tukidaiwa mpaka kanisani na humo kwenye maduka, pamoja na Malon pia
alisaidia sana tu. Kwa hiyo tumekuwa tukiishi maisha fulani hivi,
yakudunduliza. Kwa kifupi, hali ya uchumi ya humu ndani haijawahi kukaa sawa.
Na ikikaa sawa, ni kazi yakulipa madeni na ada za shule.” Joshua kimya.
“Kwa muda
mrefu baba alikuwa akijaribu kutafuta kitu chakufanya kujikwamua kiuchumi.
Tokea mama yupo hai na kushindwa. Sijawahi kumuona amehamasika na
biashara kama hiyo ya mazao. Ubaya au uzuri sisi familia yetu tuna umoja.
Tukiambizana jambo tukakubaliana, kila mmoja anasimamia hilo. Niliwapokonya
gari na kulirudisha kwa Malon, nikijua itakuwa shida kwetu wote, lakini
walikubali wote. Baba alikusudia kuiacha hiyo biashara ya mazao kwa ajili yangu
na Malon! Nimeona si sawa Joshua. Nitakuwa mtu dhaifu sana na sitaendelea, kama
nitakuwa nikimkwepa Malon kwa namna hiyo. Baba ni mtu mzima. Ananipenda na
kunilinda. Sidhani kama atafanya kitu anachojua kina madhara kwangu.”
“Nilizungumza
naye na Bale. Nikawaambia mimi sitakuwa na tatizo wakianzisha hiyo biashara na
Malon kama watataka. Nikawaambia Mungu amenilipa kwa njia ya ajabu sana. Amenipa
wewe. Kuendelea kumkimbia Malon, ni kutangaza bado ananguvu
kwangu. Sitamkimbia tena. Wala sitaogopa kuja kumuona tena popote na wala
sitaumia kwa lolote. Nimejiambia lazima nikubali kutoka hapo kwa kuwa Mungu amenitoa.
Kwa hiyo ndio Bale amejinyima pesa kutoka kwenye pesa anazolipwa chuo, na mimi
nimewaongezea yeye na baba, wataanzisha hiyo biashara.”
“Bale
anakaribia kumaliza chuo, amemwambia baba watasaidiana. Ikitokea anatakiwa
kusafiri kwenda kusaka mazao hata mashambani, amesema atafanya, sio lazima
kuanza au kuendelea na Malon. Wakimaanisha ikilazimu, wataanza naye kisha
waendelee peke yao. Lakini Joshua, mbali na tabia hizo za wanawake na udhaifu
mwingine wa Malon ni mzuri sana wa biashara na ana roho nzuri sana. Kisha
wakatokea kuelewana sana na Bale. Sitaki kumfunga sababu ya
maisha niliyoishi mimi. Nimemwacha awe huru kabisa. Atakachoamua kufanya na
Malon, iwe juu yake. Kwa hiyo ndio hivyo.” Joshua akavuta pumzi kwa nguvu sana,
akatulia.
“Naomba
nivumilie tu Joshua. Sina jinsi.” Joshua akamshika mkono. “Niahidi hutaniacha
katikati ya safari yetu sababu ya Malon.” “Nawezaje Joshua!?” “Nyinyi mnahistoria
ndefu na nzito Naya!” “Tafadhali tutengeneze ya kwetu ambayo haina
maumivu. Yakuaminiana. Tutaweza Joshua. Nakuahidi ni rahisi kuliko vinginevyo.”
“Sawa. Nakuamini Naya.” “Hiyo itanipa ujasiri sana. Itanisaidia.
Nakuahidi sitakusaliti Joshua. Sio mimi na wala Malon hawezi kunibadili mawazo,
nikakusaliti.” “Sawa.” Wakatulia, Naya akamuegemea begani.
“Unajua
wewe ndio sababu ya kuwa hivi?” “Vipi?” Joshua akamchungulia akimuuliza. “Hivi
nilivyo sasa hivi. Nimepata uhakika kuwa nipo salama kwa kuwa wewe upo
na mimi.” Joshua akampitishia mikono mabegani na kumkumbatia vizuri. Naya
akajivuta karibu. “Malon alikuwepo, lakini sikuwa na amani hivi Joshua, wewe ni
shahidi. Uliona hata siku ile uliposema tulikuwa na kikao na wewe kwa mara ya
kwanza kule kazini. Sasa ujue ile hali ya wasiwasi uliyoniona nayo haikuwa hata
nusu ya vile ninavyokuwa nikiwa na Malon. Sidanganyi kama sikuwa nampenda.
Sana. Lakini ilikuwa ni maumivu ambayo sina jinsi yakueleza. Sasa hivi nalala
nikijiambia sio jukumu langu tena. Hainihusu. Siwajibiki kwake tena. Hayupo
kwenye maisha yangu. Moyo umetulia nikijua Joshua wangu yupo.” Wakatulia
kwa muda.
“Kesho
huna haja yakunifuata huku Joshua. Nitawahi kuamka, baba atanisindikiza mpaka
kituoni. Nitapata usafiri bila shida. Usije huku.” “Ni kama mimi uniambie
nipande daladala kwenda kazini.” “Hapana. Sitaki uhangaike kuja mbali kote
huku!” “Kwani wewe unajua ninapoishi?” Naya akatulia. Akakumbuka hata hajawahi
kumuuliza anaishi wapi. “Ukweli sikumbuki kama ulishaniambia.” “Kwa nini
hukuuliza?” “Mimi naona kuna mambo mengine ni mpaka mtu aamue kusema mwenyewe!”
“Kwa hiyo na mimi unanihesabu kama mtu mwingine tu?” “Hapana Joshua. Mimi
nilipotaka ufike kwetu, nilikwambia na kukuelekeza mpaka hapa. Ila kabla ya
hapo sikuwa tayari ufike kwetu. Unakumbuka tulipokuwa tukitoka Mbeya?” Joshua akatulia.
“Japokuwa
baba alisema niwakaribishe, lakini mimi sikuwa tayari mpaka nilipokuwa tayari
na wewe. Kwa hiyo nikadhani na kwako ni hivyohivyo. Unisamehe kama nilielewa
vinginevyo.” Joshua akanyamaza. “Eti Joshua Kumu, unaishi wapi?” Ilibidi tu
Joshua acheke. “Naya wewe! Sawa bwana.” “Niambie Mr. Kumu. Unaishi
wapi?” Joshua akamwangalia. “Unataka kweli kujua au kwa kuwa nimeanzisha hili?”
“Sasa ukiumwa nani atakuja kukupa maji ya kunywa?” “Hayo ndio umekumbuka sasa
hivi?” “Taratibu Joshua. Nilikwambia akili ilikuwa imevurugwa. Kadiri
siku zinavyoendelea, ndio natulia nakuweza kufikiria na kurudia hali ya
ubinadamu. Mwenzio nilikuwa nalelewa tu.” Joshua akacheka sana.
“Kweli.
Malon alikuwa akinifikiria kwa kila kitu. Nafikiri ilikuwa njia yakunitawala vizuri,
sijui. Haya, hapa nyumbani nilikuwa nalelewa kwa kila kitu. Kazi zangu zilikuwa
na baba nje, mpaka mama alipotaka nianze kufikiria kama mwanamke. Ndipo
nikaanza sasa. Kwa hiyo akili bado haijazoea. Sasa hivi ndio nipo kwenye kuanza
kumfikiria Zayoni, kama vile mama. Kuanzia anapoamka, mpaka siku anapokwenda
kwa mkewe.” Joshua akacheka sana. “Kweli. Ndio wosia wa mama huo. Aliniomba
rasmi. Sasa niambie Joshua, si bado nina safari ndefu?” Joshua akamwangalia na
kuamua kuendelea.
“Naishi
Goba. Nilipata eneo kubwa sana kule. Ndipo nilipojenga na ndipo ninapoishi.”
“Hongera sana. Swali jingine, unataka watoto wangapi?” Joshua akakunja uso
akicheka. “Hilo swali unamaanisha?” “Kabisa.” Joshua akacheka akifikiria.
“Nikuulize na wewe unataka wangapi?” “Joshua Kumu, jibu swali.” Wakacheka.
“Familia kama hii ya kwenu sio mbaya. Ila wawili ndio ningependa.” “Jinsia?”
“Naya!” “Hivi ndivyo unajaliwa Joshua! Jibu.” Joshua akacheka sana. “Nitajuta!”
Naya akacheka. “Nikipata jinsia zote sio mbaya. Ila nitapokea kile Mungu
atakachoona ninaweza kukikuza. Na wewe unataka watoto wa ngapi?” “Nilishakuwa
na watoto wawili mawazoni na wa kwanza alikuwa wakiume, wapili wa kike.” Joshua
akacheka akifikiria.
“Lini?”
“Mwenzio nilifikiria, nikimaliza tu chuo, basi nitaolewa. Nitashika mimba
kwenye fungate, nitazaa mtoto wa kiume ndani ya mwaka mmoja, huyo kaka
akifikisha tu mwaka na nusu, nashika mimba ya dada yake, nimemaliza.” “Kumbe
ulikuwa umejiandaa hivyo?!” “Sana Joshua. Nilijua baada ya chuo tu, kazi ya umama
na kusaka pesa vitaanza. Sikuwahi kufikiria kama ningerudi kuanza tena kwenye
swala la mahusiano.”
“Nikuulize
Naya. Maana najua mume uliyemtegemea alikuwa Malon. Kweli ulikuwa tayari
kuendelea naye hivyohivyo!?” “Hata baba aliniuliza hilo swali. Lakini Joshua,
hakika nilikuwa tayari. Kwenye swala la wanawake ni kama alianza kubadilika na
aliniambia anafanyia kazi. Swala la uwezo wa kipesa, sikujali. Nilijua
nimesoma, nitapata tu kazi. Na tabia yake yakufungwa jela mara kwa mara,
nilikuwa radhi kabisa hata kama ndio yatakuwa maisha yangu yakumtoa jela kila
wakati, nisingejali ilimradi tu niwe naye.” Joshua akashangaa sana.
“Na yeye
alikuwa akilijua hilo?” “Nategemea awe alikuwa akilijua hilo. Niliishi naye kwa
vitendo. Kumthibitishia mchana na usiku namtaka, na mimi ni mwanamke wa tofauti
na wote anao wachezea, nikimuomba aje anioe mimi. Ninapokwambia nimekataa pete
ya Malon, ni kwa kuwa sina nilichobakisha kwa Malon. Nimegundua hakuwahi
kukusudiwa awe wangu, na Mungu aliruhusu nifanye yote ili leo, nisiyumbe
tena. Hakika nilifanya yote Joshua. Na nikikwambia sitakusaliti sababu yake
hata kama tuna historia, ni kwa kuwa kweli sina sababu yakufanya hivyo. Sina
jipya lakumpa Malon, na nimekuja kugundua hata yeye hana sababu ya msingi ya
kuwa namimi, ila tu uhakika wa mtu kama mimi kwenye maisha yake. Kwa hiyo wala
usiwe na wasiwasi na Malo. Nimekuwa naye akiwa anavuta bangi na havuti.
Nimekuwa naye akiwa jela na huru. Nimekuwa naye akiwa mtaani
na kanisani. Namjua haswa, zaidi yakumfahamu.” Joshua akatulia
kidogo.
“Nikuulize
kitu kingine, Naya?” “Chochote kile, niulize.” “Ila usione ni kama
nakuharakisha.” “Sitajali hata kama utaharakisha. Najihisi nimejichelewesha
vyakutosha, ni wakati wa kuchangamka.” Joshua akacheka kidogo. “Mbona kama
unasita?” Joshua akamwangalia na kuamua kuongea tu. “Unakumbuka ile familia ya
kina Magesa?” “Ile uliniambia ndio familia pekee au watu pekee
uliopenda kujisogeza kwao?” “Kumbe ulitilia maanani!?” “Kwa nini unasema
hivyo!?” “Siku ile nakuambia juu yao, hukuonekana kujali sana.” Naya akataka
kujitetea lakini akaona atulie. Akaanza kumuhisi Joshua ni mtu wakujali vitu
vidogovidogo, akajiambia inabidi kuongeza umakini kwake, yeye sio Malon.
“Nisamehe
Joshua kama huwa naonekana nakuwa sikufuatilishi. Nitaongeza umakini, ila nilikusikia
siku ile. Vipi?” “Unafikiri ni sawa nikikutambulisha kwao?” “Ningefurahi na
mimi kuwafahamu. Lini?” “Utakapokuwa tayari. Maana huwa mkewe, tena mna majina
yanayofanana kidogo, yeye anaitwa Nanaa.” Naya akacheka. “Basi huwa
ananisisitiza sana kuoa na kusema nisichelewe, halafu mama yake Geb, anaitwa mama
G, huwa ananiambia nisichague sana. Na ameniomba rasmi, nikipata tu
mwanamke, kabla ya kumtambulisha kokote kule, nimpeleke kwake kwanza.”
“Wanaishi
pamoja!?” “Nakwambia hiyo familia utapenda. Huyo mama G, alizaa mapacha wawili,
Grace na huyo Geb mume wa Nanaa. Grace naye anahistoria ndefu, ila ameolewa
tena wanaishi Arusha. Geb na mkewe Nanaa, wana watoto watatu na wanaishi na
huyo mama G. Geb sio mzungumzaji sana, lakini ile kuwepo tu nyumbani kwao, kuna
hali ya tofauti. James ambaye ndiye alimlea Nanaa, alinitambulisha kwao mara
moja tu tena kwenye sherehe, ilibidi kumuomba James anipeleke tena kwao, ndipo
nikaongeza watu wengine.
Joshua
akamsimulia mengi juu ya Geb, Nana, mama G, James na Grace mpaka Naya akatamani
kweli kuwaona. {Historia yao zaidi ipo kwenye simulizi ya ‘Ni Wangu’ Karibu
ujisomee kwenye website ya NaomiSimulizi.com.}
“Joshua!
Kweli hao watu wanavutia. Nipeleke na mimi nikapate huo upako wa mahusiano.”
Joshua akacheka sana. “Ndicho kikubwa nilichosikia hapo.” “Kwa hiyo kweli upo
tayari nikakutambulishe?” “Kabisa Joshua. Mimi ni wako, na sitabadilika.”
Joshua alifurahi sana. Alicheka huku akimwangalia Naya. “Sikutanii Joshua.
Mungu anipe nini tena ili niridhike na kutulia!? Au hujaelewa nikikwambia hichi
ndicho nilichokuwa nikikilia na kukisubiria kwa Malon!” “Akirudi hapo
katikati?” “Alisharudi na pete mkononi, wewe ukiwa haupo kwenye maisha
yangu, na nilimkataa. Baba huyo hapo ndani ni shahidi. Nimeamua kusonga mbele.
Na acha kutishwa na Malon, Joshua bwana!” “Lazima anitishe. Amejaa
mdomoni mwako kwa makubwa matupu!” Naya akatulia kidogo kama anayefikiria kisha
akamgeukia Joshua.
“Nimeamua
kutulia kwako Joshua. Nitambulishe kokote utakapo, sitakukimbia wala kukubadilikia.
Nakuhakikishia.” “Nakushukuru Naya. Basi nitaweka mipango mizuri.” “Sawa.”
Wakakubaliana na kutulia.
Zayoni
akatoka kuwaitaa sababu ya chakula, wakaingia ndani. “Baba ameniambia Naya
alikuwa hospitalini. Akawekewa mpaka maji na kupewa dawa bila baba kuwepo!”
Bale akaanzisha hayo mazungumzo wakila. Wote wakacheka. “Ni kweli kabisa.”
“Naya!?” “Ndiyo Naya.” “Hajakwambia mpigie simu baba, yeye amezidiwa,
atakufa bila kumuona ba..” “Sio hivyo Bale. Anasema atakufa bila
baba kumuona yeye.” Zayoni akamrekebisha Bale, wote wakacheka. “Nope.”
Joshua akakataa huku akicheka. “Hajakwambia baba Naya atapata sana shida
yeye akifa!?” Bado Bale hakuwa akiamini akaendelea kuuliza. “Kumbe hali ndio
inakuaga mbaya hivyo!?” Joshua akauliza akimcheka Naya. “You have noooo idea!”
Bale akamjibu nakufanya wazidi kucheka.
~~~~~~~~~~~~~~~~
v Njama
ameahidi kutokubali kushindwa, amejipanga.
v Na Joshua naye ameapa kuwakilisha onyo kwake,
kuhakikisha anaelewa amegusa sehemu ambayo hakutakiwa kugusa.
v Malon naye
ndio ameelewa na kukubali kukaa pembeni kama afanyavyo nyakati zote amuachapo Naya?
Vita ya Mapenzi&Pesa inaendelea.
Kwa umbali gani?
Usikose Muendelezo.
0 Comments:
Post a Comment