Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI&PESA! – SEHEMU YA 24. - Naomi Simulizi

MAPENZI&PESA! – SEHEMU YA 24.

Siku ikaanza kwa wote wawili busy ofisini kwao. Kila mmoja akawa wa kwanza ofisini kwake. Bosi huyo akawepo ofisini kabla hata ya Fina, sekretari wake. Naya anachapa kazi mezani kwake, Joshua anachapa kazi ofisini kwake tena wala sio kwenye simu zao wakiwa instagram au facebook, hapana. Kazi zakuzalisha kwenye hiyo kampuni, mida hiyo alfajiri wakati wenzao bado wamelala majumbani mwao! Huwezi kushindana nao hata kwa majungu! Naya akaendelea kufanya kazi kwa bidii zote, na Joshua akipanga kazi kuhakikisha pengo la Njama halionekaniki. Watu wanaingia kazini mida hiyo ya asubuhi Joshua alishapanga kila kitu, nani awepo wapi na afanye nini.

“Kumu ameitisha kikao saa mbili na dakika ishirini na saba.” Aliingia Jamal akihema kwa nguvu kama aliyekuwa akikimbia. “Tafadhadhali sana jamani, ifikapo saa mbili na dakika 25, nawaombeni jamani, wote muwe mmeshakaa kwenye viti pale chumba cha mkutano. Ikifika na dakika 26, kwa sababu zako binafsi kama utakuwa hujafanikiwa kufika pale, usije tena, sisi tutakuwakilisha. Isijetokea unaingia muda mmoja na Kumu. Tafadhalini naombeni siku ya leo iishe vizuri isiwe kama jana. NIMEOMBA. Sasa msitake tuanze kurudishana nyumbani asubuhi hii kabla siku haijaanza. Swali?” Wote kimya. “Nauliza kama kuna swali ili msiniabishe, Kumu awe amesimama pale, ndio na wewe unaingia kwa kuchelewa kana kwamba sijawataarifu. Nauliza kama mmeelewa.” “Mimi nimeelewa Jamal na kuna kitu naomba ukiangalie kabla ya kikao, pengine utahitaji.” Naya akamwita.

“Ninachohitaji ni ripoti nzima ya angalau siku 10 tu Naya. Kilichofanyika hapa ofisini. Hicho tu, mengine naomba yasubiri. Kumu ataniwajibisha leo.” Jamal akasikika kama ameshapaniki na kumshangaza Naya, akatoka kwa haraka kama anayekimbizwa. “Kwani kazi yake huyu Jamal hapa ni nini, kama anachanganywa na vitu vidogo hivyo!”  Akawaza Naya akiwa amerudisha macho kwenye kompyuta yake. Akamaliza alichokuwa akifanya, akakusanya vitu vyake, akawahi chumba cha mkutano, na hapo akawa wa kwanza. Akatafuta kiti mwisho kabisa, akakaa. Watu wengine wakaanza kuingia. Naya akabaki akiwa ametulia tu macho kwenye kikabrasha alichokuwa ameingia nacho. Watu wakaendelea kuzungumza na kucheka.

Ilipofika na dakika 26 Jema akaingia, wote wakanyamaza. “Naamini kila mtu anaripoti yake kama nilivyowataarifu kwenye barua pepe niliyowatumia. Msije kunikana kwa Kumu kwamba hamjapata! Au kuna ambaye hajapata?” “Mimi laptop yangu aliangusha Njama jana.” Jema akaanza kutingisha kichwa akikataa. “HAPANA Jamal. Jana nilikwambia kabisa ita mtu wa IT akusaidie kufufu hiyo laptop au akutolee taarifa zote zilizokuwepo kwenye hiyo laptop yako. Siku nzima ya jana Jamal! Leo ndio unatoa hizo sababu!?” “Sasa nifanye nini Jema? Tafadhali nisaidie.” “Wewe unamjua Kumu, hawezi visingizio!” Naya akamuomba mtu wa pembeni yake ampe Jamal moja ya kabrasha.

“Nini wewe? Sio muda wake...” “Inatoka kwa Naya.” Jamal akafungua, alishituka kukutana na ripoti ya siku 20. “Naya!” Akashangaa Jamal, akabaki mdomo wazi, ametoa macho. “Za asubuhi!” Kumu akaingia na hiyo salamu, akamkabidhi tablet Jema. “Niunganishie tafadhali.” Jema akaipokea kwa haraka. Joshua alikuwa amependeza haswa. Suti safi na tai aliyokuwa amepewa na Naya siku iliyopita. Naya hakuwa amemuona vile. Asubuhi alikuwa amevaa tu shati, koti la suti alikuwa amening’iniza nyuma ya gari.

Kumu alikuwa msafi haswa. Rangi ya maji ya kunde iliyong’aa vizuri sana mwilini mwake. Nywele imekatwa vizuri na kuwekwa dawa. Akachongwa vizuri. Mustachi ukachongwa na wenyewe vizuri, ukaunganishwa mpaka pembezoni mwa nywele za kichwani na kuongeza uzuri wa uso. Mwili wake wa kawaida haukuwa mnene wala mwembamba. Saa tu aliyovaa ilionyesha ipo pesa. Meno meupe na yamejipanga. Alikuwa anavutia kumtizama. Naya mwenyewe hakuwa akiamini kama ni wake, tena wake peke yake! Hakuna mwanamke pale kwenye chumba kizima amemuona akiwa uchi! Hilo likampa ujasiri.

“Tunaanza na nani?” Kumu akamuuliza Jema. “Ilikuwa Jamal lakini Jamal...” “Ninayo ripoti. Tena ya siku 20. Hii hapa.” Jamal akaingilia kwa haraka tena akasimama na kukimbilia pale mbele, Jema akakunja uso akishangaa, Joshua akabaki akiwatizama Jamal na Jema. Yeye Jema ndiye akaipokea. “Wewe Jamal si umesema...” “Jema! Umetaka ripoti, ripoti hiyo hapo.” Jamal akamkatisha kama asiyetaka Joshua ajue kama yeye hakuwa amefanya kazi.

Wakamuona Joshua anaangalia saa ya mkononi, Jema akaelewa. “Sawa. Naomba basi wewe uanze.” “Naomba aanze mwingine wakati mimi najiweka sawa.” “Acha kupoteza muda Jamal! Upo hapa mbele na ripoti ya siku 20, changamka tuokoe muda.” “Si mtu yeyote yule anaweza kuwakilisha kutoka kwenye idara yetu? Basi Naya njoo tuwakilishe.” Wote wakashangaa. “Jamal!” “Sasa wewe shida yako nini Jema? Si kinachotakiwa ni ripoti ya kitengo changu? Ndio nimemchagua msaidizi wangu azungumze. Yeye ndio macho na miguu yangu huko ninapowatuma kwenye field!” Joshua kimya akisikiliza.

“Karibu Naya.” Jamal akamkaribisha kwa haraka bila kusubiri Jema ajibu tena. Naya akaingiwa na hofu haswa, lakini akakumbuka Joshua alimwambia kila akipewa nafasi, aitumie ipasavyo. Akasimama. “Lakini sio hivyo Jamal!” “Kwani wewe vipi Jema?! Mbona unataka kuanzisha jingine wakati kazi uliyotoa imefanyika?” Wakabishana kwa sauti ya chini pembeni watu wakimwangalia Naya. “Hili juma limekuwa baya sana kwangu. Na wewe unajua. Unashindwa vipi kunielewa?” Jamal akaendelea na Jema pembeni kabisa, wakati Naya anazipanga karatasi kutoka pale alipokuwa ameacha Jamal alipokuwa akiziangalia, alikuwa amezichanganya. Lakini kwa kuwa Naya ndiye aliyefanya hiyo kazi, alijua ni nini kinaanza.

“Tutaanzia kuzungumzia safari ile ya Mbeya. Pesa iliyokuwa imekabidhiwa kwenye idara yetu, matumizi na kazi kwa jumla.” Akaanza Naya huku akiendelea kupanga. Wazi alionekana anatetemeka kwa mikono kucheza mpaka karatasi zilionekana zikitetemeka, ila akajikaza akaendelea kuziweka zile karatasi vizuri, Joshua kimya kabisa, amesimama pembeni akisikiliza na kumwangalia. “Pesa taslimu kwa safari nzima ilikuwa.” Naya akaitaja. “Tulikwenda watu 12. 10 tulitangulia, wawili waliungana nasi siku ya mwisho. Walipata malazi ya siku mbili.” Naya akaeleza vizuri mchanganuo wa bajeti nzima mpaka akamshangaza Jamal kuwa yote hayo aliyapata wapi asijue uzembe wa wenzake kutofanya kazi, yeye aliyekuwa akifanya hizo kazi, amefanikiwa kukusanya taarifa zote hizo. Katika kujifunza kwake kuandaa ripoti bila ya kutumwa, imemsaidia siku hiyo.

Naya akaendelea kiutalamu. “Watu tuliowafikia kwa jumla na kwa survey tumekadiria kuwa wanaweza kufikia.” Naya akataja na kueleza aina ya changamoto walizokumbana nazo walipofika kule na maoni ya watumiaji. “Ukweli bidhaa zetu wamesifia kwa ubora wake. Hilo hakuna aliyepinga. Ila kikubwa tulichokumbana nacho kutoka kwa watu tuliozungumza nao, na hizo karatasi 98 tulizofanikiwa kukusanya za survey ilikuwa bei na ufikiwaji wa bidhaa. Walilalamikia bei, na upatikanaji wake kirahisi. Wengine walisema inawalazimu kufuata mjini, hazifiki kwa wingi vijijini mpaka vipindi vya sikukuu.” Naya akaeleza vizuri, akiwa anaendelea kuzungumza, akasikia hofu imemuisha na ujasiri umeongezeka.

“Kwa hiyo wote tuliokwenda kule na kiongozi wetu, tuliona jinsi walivyofurahia ile punguzo la bei. Na ukweli tulimaliza bidhaa zote. Siku ile ya mwisho tuliwahi kufunga kwa kuwa tuliishiwa. Tuliuza na zaidi.” Joshua alikuwa akijisikia vizuri, wakati Naya akijieleza kwa ufasaha mpaka akamaliza ripoti nzima bila hata kukosea namba na mahesabu kamili.

“Hiyo ni kwa kifupi. Ila kila kitu kipo humu kwenye kabrasha ya ripoti.” “Nikabidhi mimi.” Akawahi Jamal. “Nipe mimi.” Joshua akaingilia. “Hii ni ripoti ya kitengo chenu, umeandaa wewe Jamal, si ndiyo?” Lilikuwa swali la mtego lililombambaisha sana Jamal, Jema akabaki akimsikiliza kwa kumsuta, Naya akabaki kimya akizirudishia zile karatasi kwa kuzipanga tena maana kila alipokuwa akizungumza alizipekua zile kurasa na kuweka chini ya zote akiendelea kusoma ya juu. “Okoa muda Jamal. Ndiyo au hapana?” Joshua akamkatisha. “Nahitaji kopi sababu laptop yangu Njama aliingusha jana, kama nilivyomwambia Jema, nikasem..” “Peleka kwa watu wa IT, waambie wakuokolee taarifa zako. Hizo nabaki nazo mimi. Nani anafuata? Jema?” Wakajua Joshua ndio amefunga huo mjadala, anabaki na kabrasha la Naya.

Joshua akaangalia saa, akaona wote kimya. “Jema!?”  Akaita kwa ukali kidogo. “Kama hakuna anayejitolea, basi nitakuwa nikiwaita. Product Manager.” Jema akaita. Felix kiongozi wao akasimama. Alizungumza kwa ufupi sana juu ya bidhaa zao. “Kama mlivyosikia kutoka kwa Advertising department,” Akimaanisha kitengo cha kina Naya, cha matangazo. “Ubora upo vizuri ila bei.” Joshua akakunja uso. “Hivi taarifa ya ripoti hii ninayotaka watu wote wasikie hapa, Jema aliwatumia lini? Mbona inakuwa kama hakuna maandalizi?!” Joshua akauliza kwa ukali kidogo. Felix alikuwa mtu mzima wa kutosha kwa Joshua. “Ni jana tu!” Wakajitetea. “Lakini mwisho wa mwezi unakaribia jamani! Inamaana kila kitengo kingekuwa kina ripoti yake tayari, na pengine ingekuwa haijakamilika kwa siku chache tu!” Jema akalalamika.

“Naomba niulize hivi. Kati ya Public Relations Manager and Markerting reseach Manager, nani yupo tayari kati yenu ili tuokoe muda?” Joshua akauliza akiwatizama hao viongozi wa hivyo vitengo. Pakazuka ukimya kidogo. “Umeshaunganisha tablet yangu?” Joshua akamuuliza Jema akionekana amebadilika na hana muda wakupoteza zaidi. “Tayari.” Jema akajibu akionekana na wasiwasi tayari. “Labda niseme hivi.” “Kama nikujitetea, sina huo muda, tafadhali Mwita.” Joshua akamkatisha mapema kabisa akionekana ameshakasirika. “Nimeitisha kikao ili wote tuwe ukurasa mmoja kwenye kazi. Sio matatizo binasfi tunayopambana nayo. Kila mmoja akianza lake hapa, ninauhakika hatutatoka leo humu ndani.” Joshua akawa mkali kabisa. “Nimeelewa kiongozi.” Akajibu Mwita, na kunyamaza.

Mara tablet ya Joshua ikaonekana kwenye ukuta mkubwa ambao wanatumia kama screen yao kwenye hicho chumba cha mkutano. Picha yake na Naya wakiwa kwenye boti, ikaonekana pale mbele. Joshua akiwa ameiweka kama screensaver yake. Naya akainama. Wote kimya wakiingalia ile picha, Joshua ameinamia tablet yake akitafuta jambo bila kuangalia screen iliyoonyesha picha yao. Ukweli walipendeza sana yeye na Naya. Wote kimya macho kwenye picha.

Joshua akapekua kidogo na kurusha baadhi ya taarifa kwenye hiyo screen ikafunika hiyo picha yao, na ndipo na yeye akaangalia. “Hii ni taarifa kwa ufupi juu ya survey iliyofanyika mkoni Mbeya, tena sehemu moja tu, sokoni. Niliiomba kibinafsi ili kupata picha ya kile kinachoendelea kwa watumiaji. Naya.” Akaanza Joshua. “Ndiye aliyeandaa hii ripoti. Aliindaa bila kutumwa na yeyote, ila kundi zima walilokwenda safari, walitumwa na kiongozi wao kusambaza hivyo vipeperushi kama mara nyingine zote tunavyofanyaga kuwapatia watumiaji ili kujua maoni yao, lakini sijawahi kuona ripoti nzuri kama hii ambayo Naya mwenyewe katika kujifunza kwake, aliiandaa, na imenifikia mimi.” Wote kimya wakiingalia pale kwenye screen.

“Nirudi kwenye ripoti ya kitengo chao ambayo ametoka kuisoma.” Hata hiyo walijua ni Naya tu ndiye ameitengeneza kwani hata Jamal alipopewa ile ripoti, wote waliona na Jamal mwenyewe alishindwa hata kuitetea na kumtaka Naya ndiye aisome kama mwakilishi wa idara. Joshua aliizungumzia ile ripoti kwa kifupi ila kwa utaalamu sana akifafanua mengi yanayoendelea kwa kila kitengo kupitia ripoti hiyohiyo ya kitengo cha masoko, upande wa matangazo. Advertsment department.

 “Tunaposambaza hivi vipeperushi kwa watumiaji, kuna kuwa na sababu.” Joshua akaweka msisitizo. “Kwa mara ya kwanza nimeona hili wazo kufanyiwa kazi na kutengenezewa aina hii ya ripoti.” Kumu akaendelea. “Kwa sehemu, sio jumla. Kwa sehemu hawa watumiaji wa mkoni Mbeya, ni kama wamewakilisha mawazo ya watumiaji wengine. Sasa basi..” Kumu akaendelea, wengine wakipiga picha ile ripoti ambayo kila ukurasa kwa chini iliandikwa jina la Naya. Na Joshua alifanya makusudi. Akaieleza vizuri mpaka wote wakabaki wameduaa wasiamini kama ni kazi ya Naya, mtu mgeni kabisa pale.

“Mbali na viongozi wa vitengo. Yupo mtu binafsi ana kitu chake pekee anachofikiria kinaweza kusaidia kitengo kizima?” Joshua akatoa hiyo nafasi ambayo hutoa mara kwa mara kwa watu wote. “Usiogope. Wote tunategemeana. Naya alijitengenezea hii ripoti, kwa ajili yake tu akitaka kujifunza yeye mwenyewe. Hakujua kama leo itakuja kusomwa hapa na kuwa msaada katika kila kitengo.” “Ni kweli. Hata mimi nimechukua kwa nafasi yangu.” Mwita akajikuta anakubaliana naye kwa sauti huku akiandika.

“Tunang’aa kama kitengo kizima, lakini kibinafsi pia. Unachochote unachoona kitanufaisha kampuni, kiandikie vizuri. Weka jina lako ili tutambue mchango wako moja kwa moja kabla ya idara yenu.” Joshua akaendelea. “Sasa je, yupo mwingine mwenye nyongeza kabla sijafunga kwa leo, ili kesho muda kama huu turudi hapa na viongozi wote wa idara wakiwa na ripoti zao ndipo nizungumze nilichotaka kuzungumza leo?” Kimya.

Mmoja kwenye idara ya Research akanyoosha mkono. “Karibu Faith.” Joshua akamkaribisha. “Sisi tunatatizo...” “Hapana Faith. Sicho nilichouliza. Inawezekana ni muhimu, lakini hiki kikao sio cha kueleza matatizo yetu. Kazi tu. Nataka kusikia matokeo. Katika ugumu wote. Matatizo yote tunayokumbana nayo, nani ameweza kutoa kitu au suluhu? Ndicho ninachotaka kusikia muda huu.” Faith akarudi kukaa, wote kimya. Joshua akawaangalia kwa zamu. Kimya.

“Hiki kilichotokea leo, kukutana bila matayarisho, naomba kisirudie tena.” Joshua hapo akatulia kidogo kutaka kuweka msisitizo akiangalia viongozi wa idara mmoja baada ya mwingine kisha akaendelea. “Tutarudi hapa tena kesho ila saa mbili kamili.” Joshua akatulia tena kidogo, kisha akaendelea. “Hii ni kwa viongozi wote wa idara. Ukiona huna ripoti ila sababu, tafadhali wewe na watu wako, wa idara yako nzima, msihudhurie kikao cha kesho ila kabla ya siku ya kazi kuisha nitataka kujua kwa maandishi, sababu ya watu wa idara yako na wewe mwenyewe kutotokea kikaoni.” Joshua akazima tablet yake wakajua ndio anatoka. “Tafadhali Kumu.” Joshua akanyanyua kichwa kumtizama.

Alikuwa ni kiongozi wa idara ya Markerting reseach . Joshua akasimama wima akamtizama. “Tafadhali sana Kiongozi. Nisaidie ukurasa wa tatu unaozungumzia maswala ya survey iliyofanyika huko mkoani Mbeya. Natoa tu kopi narudisha.” Alikuwa ni dada, alionekana umri unakaribiana na yeye Joshua. Jona Chege, alijulikana kwa maringo akitaka watu watambue yupo juu, mbabe na mkorofi. Watu wa chini yake hakuna aliyempenda kwa unyanyasaji na ukali. Akamsogezea Jema file zima watu wote wakiwatizama, akatoka na tablet yake, ndipo kila mtu akahema kwa nguvu kama waliopata aghueni. Naya na yeye akasimama ili atoke, Jamal akamuwahi kwa haraka. “Naya mama, nisitiri mjini hapa. Nitumie ile ripoti kama unayo.” Naya akatulia kidogo. “Si unayo kopi yake? Usiniambie kama hukuwa na kopi Naya! Utaniii..” Akamkimbilia Jema, akampokonya lile faili zima alilokuwa nalo na huo ukurasa wa tatu kutoka mkononi kwa Jona, ambaye ni kama wanalingana kwa cheo.

“Wewe Jamal vipi?!” “Nitawapa nikimalizana nalo.” “Mbona hukumwambia hivyo Joshua?” “Jema leo wewe vipi?! Mbona kama upo kinyume yangu?” Jamal akamlalamikia Jema, na Jona akimshangaa Jamal. “Mimi nimepewa na Kumu mwenyewe! Kwa nini unipokonye? Mwambie Naya akupe kopi! Wewe vipi?” Wakaanza kubishana, Naya akamsogelea Jamal. “Hii kazi ninayo kwenye kompyuta Jamal!” Naya akamwambia kwa sauti ya chini tu kwa utulivu, Jona na Jema wakamgeukia Naya.

“Sasa mbona hukuniambia Naya, unaniacha naonekana kama mjinga!?” “Unakumbuka nilikuita asubuhi kabla ya kikao nikakwambia nataka kukuonyesha kitu, ukakataa?” Jamal akapoa kabisa. Akanyamaza. Jona akamcheka. “Aibu zako Jamal.” Jona akachukua ile karatasi mkononi kwa Jamal na kuondoka nayo. “Nitakuletea baada ya muda mfupi tu Jema.” “Sawa.” Jema na Jona wakatoka.

Jamal akamgeukia vizuri Naya. “Kumbe afadhali ningekusikiliza Naya!” “Naweza kwenda kukutumia sasa hivi, ukafanya mabadiliko unayoyataka. Naona nimechanganya mpaka mambo ya idara nyingine! Sikuwa najua. Bado najifunza, na ndio maana nilitaka uangalie kwanza, uchukue kitakachokufaa.” “Basi nisitiri Naya. Nina mambo yananitinga ya kifamilia na hapa! Mke wangu kaanza kuumwa ghafla, akili haijatulia. Nitumie kama ilivyo, sasa hivi nakwenda kuifanyia kazi, ili kesho hata Kumu akitaka turudie, niwe najua chakuzungumza. Kumu hadanganyiki.” “Sawa.” Naya akakubali bila shida.

“Nikuombe tena Naya, siku hizi mbili wakati nikijiweka sawa, nisaidie mambo ya pale idarani. Kusimamia kila kitu.” “Tafadhali Jamal, labda uwaambie wewe mwenyewe kama nitawasimamia. Hivihivi haitakuwa sawa.” “Basi acha tukafanye kikao kifupi.” Jamal akawaambia watu wote wa kitengo chake warudi ofisini kwao wana kikao.

Naya kimya, akatangulia na kuanza kufungua kompyuta yake ili amtumie Jamal kazi. Jamal na wengine wote wakaingia. “Kuanzia leo, Naya atakuwa akiwasimamia na kuwagawia kazi zote.” Wakanyamaza kimya. “Kuna swali, kipingamizi au wasiwasi wowote?” “Mimi nilikuwa naulizia kuhusu hatima ya sisi wengine tusiojulikana hapa kwenye hii kampuni, tunaajiriwa lini?” “Tena wewe ndio usinichanganye kabisa. Huna unachofanya ila kujizungusha na kusambaza maneno ya hapa.” Jamal akambadilikia kabisa.

“Tena nawaambia kabisa, kuanzia sasa, nataka taarifa ya nini mmefanya kila siku. Sio mnakuja kukaa tu hapa. Naya ameanza na wengine kati yenu, na wengine amewakuta hapa, lakini amekuwa akifanya kazi na kujituma zaidi! Anayeona hawezi, mlango huo hapo, ondoka. Acheni kujaa hapa huku hamna mnachokifanya.” Jamal akazidi kuwa mkali. “Mnakazi ya umbea tu na kusambaza habari za watu!” Wakati Jamal akiendelea kugomba, ujumbe ukaingia kwa Naya. Am so proud of you, Naya Kumu.’ Naya akasoma nakujikuta akicheka baada ya kusoma huo ujumbe wa Joshua akimwambia kuwa anajivunia yeye. 

‘Asante. Leo nimejitahidi? Sikuwa nimejiandaa vizuri.’ Akamuuliza. ‘Ulifanya vizuri sana na ndipo nilipojua kama ilikuwa kazi yako hata kabla Jema hajaniambia. Kazana mama. Juhudi zako zinaonekana.’ Naya akajisikia vizuri. ‘Nahitaji kujifunza kuandaa ripoti kitaalamu zaidi. Hii nimeiandaa nakuweka mpaka ripoti za idara nyingine! Haijakaa kitaalamu.’ Akaanza kujikosoa mwenyewe. ‘Ipo vizuri tu, kama ripoti ya kitengo chote cha masoko kwa ufupi. Ukitulia, jaribu sasa kuitengeneza kwa ajili ya idara yenu tu. Halafu tuipitie tena kwa pamoja. Kama kuna marekebisho tutayaweka pamoja. Ila umenifurahisha SANA.’ ‘Nakushukuru Joshua.’ ‘Karibu.’ Naya akaweka simu chini na kurudisha mawazo pale Jamal alipokuwa akigomba. Akatulia akisikiliza.

“Sasa Naya atawasimamia maana naona ndio mwenye kujituma zaidi ya wote na anaelewa mambo kuliko wote. Mwenye shida na hilo, mlango uko wazi. Ondoka ili kutupunguzia majungu humu ndani.” Jamal akaweka msisitizo. “Sasa Naya?” Jamal akamsogelea Naya. “Nimeshakutumia bosi wangu.” “Asante mama. Ukikwama na hichi kizazi humu ndani, wewe uniambie. Wala usijibishane nao. Kwanza nataka kupunguza watu humu ndani.” Kidogo akawatisha.

“Sasa acha nikapambane na watu wa IT, wakishindwa kufufua taarifa zangu na laptop yangu, nikadai laptop mpyaaa. Tena safari hii nitataka yakisasa. Kufa, kufaana.” Jamal akataka kutoka ila akarudi. “Naenda kukuombea access kwa watu wa IT ili uweze kuona kompyuta zao wote hao. Itakurahisishia. Ila kwa sasa, fanya hivyohivyo. Wakikupa tu access, nitakupigia.” “Sawa bosi.” Naya akajibu. Wengine kimya. 

Juhudi Haimtupi Mtu.

Naya akainamia kompyuta yake. “Kwa hiyo ndio tunafanyaje, we Naya?” Mmoja akamuuliza kishari. “Nipeni kama dakika 5 tu. Nitawaambia chakufanya.” Wakaanza kucheka. “Pumu imepata mkohozi!” Wakamkejeli, Naya kimya akaendelea na alichokuwa akifanya. Baada ya kama dakika 7 akawageukia wote walikuwa kwenye simu zao. “Kila mmoja wenu nimemtumia kazi yake kwa leo. Na Jamal pia nimemtumia nilichowatumia ila kwa email. Itoe kwenye email na kuipakuwa kwenye kompyuta yako kisha fanyia kazi. Upo huru kufanya au kutofanya. Ila chini kabisa nimeweka mistari kadhaa inayoonyesha jina lako na kama umemaliza au la.” “Naya!” Wakaanza kulalamika. “Umewekwa tu leo na unaanza unoko!” “Unataka kutuharibia?” “Ili iweje sasa?” “Kama kuna sababu ya msingi itakayofanya kazi isimalizike?” Wote wakamshambulia.

Wala msinilalamikie au kupaniki. Siku ndio imeanza. Dharula zipo na ndio maana nimewaachia mistari chini kabisa, itakayoeleza sababu ya kutomaliza hiyo kazi niliyowapa kwa siku ya leo, kisha kumtumia Jamal hizo sababu, wala si mimi.” Naya akaongea kwa kujiamini. Ashaongoza mabinti wa mjini. Warembo na wajuaji wakati akifanya kazi akiwa shuleni mpaka kwenye kampuni aliyofungua Malon, hao hawakumtisha hata kidogo. Na wenyewe pia wakamuogopa wakijua ni Kumu wa pili hapo ofisini kwao.

“Na pia kama hujaridhika, Jamal ametoa nafasi ya kumpelekea malalamiko. Huna haja yakufanya nilichokutumia. Si lazima, kwa hiyo usipoteze muda kunilalamikia. Ila kama unaswali, hujaelewa kazi, nipo tayari kukuelekeza.” “Kwamba unajua sana?” Akamuuliza kwa kumkejeli. “Oooh yeah. Hakuna nisichojua kwenye hii idara. Kwa hiyo karibu kwa swali lolote lile.” Naya akajibu kwa kujiamini sana. Wote kimya. “Basi kazi njema.” Akageukia kompyuta yake, akaendelea na kazi. Kimya.

Mapenzi.

Ilipofika mida ya saa 5 asubuhi akaingia Joshua. “Nilitaka kumtuma mtu.” Naya akageuka aliposikia sauti ya Joshua. Akacheka na kushika mdomo kwa mshangao uliojaa furaha ya kutoamini. “Joshua!” Naya akasimama. “Hicho ndicho sikutaka nikikose.” Naya akacheka akanyoosha mkono kupokea hayo maua. “Uliniambia leo upo busy, Joshua!” “Umenifurahisha ndio maana, nikaona kila kitu kisubiri kwanza, nikwambie kwa vitendo, am so proud of you. Umempita mbali sana hata Joshua Kumu wa wakati ule.” Naya akacheka akimshangaa vile Joshua alivyofurahia ile ripoti.

“Sasa mbona hata ripoti yenyewe sio nzuri!?” “Nani amesema!?” Naya akacheka. “Kama mimi Joshua nimeikubali, jua ni nzuri. Nimeipitia mara mbili na kusambaza kwa ninao waamini. Vichwa vya uhakika vya masoko kwenye makampuni mengine hapa mjini, na wenyewe wameikubali na kubisha kama inatoka kwa mwanafunzi!” “Joshua wewe! Usingeitangaza bwana! Ungeacha labda ya pili!” “Usinitanie kabisa. Najivunia mwenzio.” Naya akajisikia vizuri sana.

“Asante kunitia moyo.” “Kabisa. Jua umenifurahisha sana. Sikujua kama unafanyia kazi kitu kama hiki! Nimefurahia mno. Ni kama umetengeneza ripoti ya kitengo kizima cha masoko kwa ufupi! Inamaana ungekuwa na taarifa sahihi, ungetoa ripoti nzuri sana! Itabidi unipe siri ya mafanikio na unionyeshe huko ulikotoa shule ya hii namna ya kutengeneza hii ripoti.” Naya akacheka sana.

“Kweli ni ngeni. Nimewatumia vichwa kama vitatu ninavyoviamini kuwa vinajielewa, wenyewe wamekukubali. Tena wameniambia tukikushindwa tu, wao wanakuiba.” Naya akacheka sana. “Unataka kuniuza!?” “Si thubutu! Kwanza nimewapiga marufu hata wasikutafute.” Naya akacheka sana. Kisha akayaangalia maua yake na kuyanusa kisha akayakumbatia akicheka. “Umeyapenda?” “Sana. Na nimefurahi kukuona na wewe.” Joshua akacheka.

“Sijapokea maua muda mrefu mnooo! Mpaka nishasau zawadi za maua!” “Mbona ni zawadi moja tu ndio imeangaliwa!?” Joshua akalalamika, Naya akacheka. “Hii ndio imevuta macho.” Naya akafungua mfuko. “Naomba uwe unatumia hiyo laptop.” Naya akamtizama, akajua ndio anamwambia asitumie tena laptop aliyopewa na Malon. “Asante Joshua.” Naya akaendelea kuifungua ili kuitoa kwenye boksi lake. Wengine wakiwasikiliza tu. “Kila kitu mpaka kuweza kupata internet popote vipo hapo. Ayush, yule kiongozi wa IT amesema ukisoma ni rahisi tu. Ukikwama, amekuwekea hapo namba yake ya simu. Mpigie yeye mwenyewe moja kwa moja kwenye simu yake ya mkononi, amesema atapokea kwa haraka tu na kukuelekeza.”  Naya akajua amehangaika kweli kufikisha hiyo laptop hapo.

“Asante na pole kwa kunihangaikia Joshua. Nimeipenda.” “Karibu. Na endelea. Chapakazi. Endelea na ubunifu kama huo. Itakuja kukulipa sana baadaye. Pandisha kiwango. Jichalenji. Kadiri unapokutana na kitu kigumu, itakufungulia milango ya kujua mengi. Kama sasa hivi tafuta jinsi ya kutengeneza ripoti ya hapa tu. Kitengo hiki tu.” “Sawa. Basi nitafanyia kazi.” “That’s my girl.” Akajisifia Kumu na kuanza kutoka. “Nawahi. Tutakula wote jioni. Chakula chako cha mchana utaletewa.” Joshua akatoka, Naya akiangalia yale maua na laptop akicheka asiamini jinsi Joshua anavyomuhangaikia. 

Akaamua kumtumia ujumbe hapohapo. ‘Wanaume wengi wamefanya mengi tena makubwa ya kusisimua ulimwengu. Lakini wewe. JOSHUA KUMU, umepita woooote.’ Naya akautuma huo ujumbe. Joshua akaupata nakucheka asiamini hiyo furaha aliyoiamsha ndani ya Naya, kwa ajili ya maua tu! Tena wala Naya hakuonyesha kuchanganywa na laptop kama maua. Akacheka na kujipongeza. “100 points. Bem!”  Akazidi kujipongeza akirudi ofisini kwake kuwa kwa alichofanya hapo kwa Naya, amejipatisha alama kwa asilimia 100!

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Jioni Naya alimfuata mpaka ofisini kwake bila hata kumuita. Joshua akamuona alivyoingia na furaha usoni. “Ni maua tu!” Akajiuliza. Huku akimtizama. Alikuwa akizungumza na mtu kwenye simu. “Fina aliniambia naweza tu kuingia. Nimekutana naye mlangoni akitoka.” Akanong’ona akiwa amesimama mlangoni kama anayejishauri atoke nje kumpisha amalizie mazungumzo ya kwenye simu. Joshua akamuashiria aingie akae. Naya akafunga mlango na maua yake mkononi na pochi begani. Akakaa kwenye kiti macho kwenye maua. Joshua akizungumza kwenye simu. Aina ya majibizano, na lugha, akagundua ni ya kikazi tu. Akatulia.

Alipokata tu simu, Naya akaanza kwa furaha hata asijue mwenzie hayupo sawa. “Unajua sijapokea maua tokea kwenye mahafali yangu ya kidato cha nne?” Ikabidi tu Joshua acheke. “Kweli tena! Unajua ni nani alinipa?” “Sijui Naya.” “Baba. Basi tokea hapo, sijawahi kupata maua hata mara moja!” “Sikujua kama ni mpenzi wa maua hivyo!” “Sana Joshua. Lakini sikuwahi kupewa. Napenda sana maua. Yaani haya, nitayatunza utakuja kuyaona hata baada ya miaka mitatu kuanzia sasa.” Joshua akashangaa.

“Naya! Si yataharibika?” “Ooh nooo! Hata kidogo. Najua jinsi yakufanya yasiharibike. Nikikwambia napenda maua, jua napenda haswa. Yale aliyonipa baba, yalipotea tu wakati nikihamia hostel. Nafikiri tuliyaacha kwenye ile gari iliyosaidia kunihamisha. Najua jinsi yakuyakausha na kuyatunza. Yanakaa muda mrefu sana.” “Naya! Umefurahi kupitiliza!” “Sana Joshua. Mno. Nakushukuru. Umeifanya siku yangu kuwa nzuri mno!” “Na ile laptop!? Umepata hata muda wakuiangalia lakini?” Naya akacheka macho kwenye maua yake.

“Ukitaka hii zawadi ikamilike, ungenitafutia na vessal.” Joshua akatingisha kichwa kama anayesikitika. “Sawa mama. Twende tukatafutie sehemu yakuweka hayo maua. Lakini na mimi huwa napend..” “Acha kuiga Kumu! Leo ni siku yangu mimi.” Joshua akanyanyua mikono juu kama aliyekubali kushindwa, akachukua funguo za gari yake, akaanza kutoka akicheka. Naya akamfuata.

“Haya maua ya leo, watakuja kuyaona mpaka watoto wangu.” “Naya!” “Kweli Joshua. Nitayatunza na haya hayatapotea.” Akamsikia anaanza kuimba na kuzidi kumshangaza Joshua. “Haya maua leo yamefanikiwa kutoa wimbo ndani ya Naya!” Joshua akawaza na kutulia kumsikiliza akiimba kwa sauti ya chini huku akiyanusa na kuyapanga vizuri hapo mkononi, asiamini kama amefurahi kwa kiasi hicho. “Sema harufu inaweza ikapotea. Lakini uzuri unabakia palepale.” Akaendelea Naya hata walipokuwa ndani ya gari. “You are the best.” Joshua akacheka sana. “Leo napendwa!” “Sana.” “Sifa zote hizo zangu?” “Nilikuwa hata sijaanza.” Joshua akacheka sana. “Naona leo hata ningeomba kuoa ningekubaliwa.” Joshua akamtania. “Ungeoa bila mahari.” Joshua akazidi kucheka.

Akaona asimwambie chochote ili asimuharibie siku yake. Akampitisha dukani, akamnunulia chupa nzuri sana yenye mdomo mpana, ya glass, nzuri sana, na nzito. Ukweli pesa ilimtoka na hapo Joshua, lakini alifurahia sana vile Naya alivyoyathamini hayo maua. Akamkabidhi hapo alipokuwa amemuacha garini. “Sasa hapa, ndio umezidi kupatia. Hiki chungu cha kioo, kitatunza haya maua kwa muda mrefu sana, japo kimezidi ukubwa.” Joshua akacheka na kuondoa gari. Naya akazidi kuongea hapo garini. Akasimulia mengi tena bila hata kuulizwa, Joshua akicheka tu.

Walipokaribia nyumbani kwao Naya akaanza kuimba tena. Wakaingia ndani getini, wakakuta gari ya Malon. Naya hakuonekana kujali kabisa japo Joshua hakupenda ikamuongezea wasiwasi. Hakusubiri hata afunguliwe mlango. Akashuka akikimbilia ndani. “Njoo Joshua.” Hakumsubiria, akaingia ndani. Alimkuta Malon na Bale mezani, Zayoni sehemu ya makochi kwenye tv.

“Baba Naya?” Akaita Naya bila hata salamu kwa yeyote yule akiwa ameficha maua yake nyuma mtu asiyaone. Joshua akamsikia akimwita baba yake kwa sauti. “Baba yuko wapi?” “Acha kelele Naya bwana! Baba ameingia ndani muda si mrefu.” Baba yake akatoka wakati Bale akimkatisha Naya. “Kwema mama?” “Unakumbuka yale maua ulinipa wakati ule namaliza kidato cha nne?” “Ukayatunza kwa muda mrefu sana?” “Ewaa.” “Nayakumbuka.” “Sasa mwenzio leo nimepewa mengine. Ona na chungu chake chakuwekea, chakioo.” Baba yake akacheka.

Joshua akaingia. “Amenipa Joshua. Pongezi ya kuandaa ripoti bila yakutumwa na mtu.” “Na nzuri sana.” Joshua akaongeza. “Shikamoo mzee wangu.” Akaunganisha Joshua akicheka. “Marahaba. Karibu Joshua.” “Asante.” Akageukia wengine na kuwasalimia. “Baba Naya, kaa nikuimbie wimbo amenifundisha Joshua.” Joshua akacheka huku akitaka na yeye kusikia huo wimbo. Baba yake akaenda sehemu ya kukaa. “Unataka kusumbua tu Naya na lisauti lako baya!” “Usimjibu maana ukimjibu tu utaanza kulia na kushindwa kuimba.” Baba yake akamtahadharisha. “Kwanza wala sijamsikia, halafu mimi nakuimbia wewe baba yangu na Joshua.” “Na mimi nataka kukusikiliza Naya.” Zayoni akaongeza. “Basi punguza sauti ya tv ili mnisikilize vizuri.” Bale akaanza kucheka.

 “Bale!” “Sasa kwani mimi nimefanyaje, baba!?” “Ukimliza tu usiku huu aliokuja na furaha hivi, ujue leo utakuwa mlinzi.” “Hata hivyo tunahitaji mlinzi baba na yeye hana kazi. Mimi naunga mkono hoja. Anakaa tu bure ndio maana anafikiria jinsi ya kunili...” “Wewe ungeanza tu kuimba Naya. Unasauti nzuri sana.” Bale akazidi kumchokoza “Sitaki. Kama ndio hivyo nakaa na siimbi tena.” Naya akakaa.

“Haya Bale.” Baba yake akamtaka atoke. “Jamani baba! Kumsifia pia ni kosa!? Au labda amesahau....” Akataka kumalizia ila akanyamaza. “Nakumbuka sana wimbo wenyewe.” Akasimama. “Joshua kaa hapa, halafu niwekee ule wimbo bila maneno.” Bale akawa anacheka taratibu. “Wala sitakusikiliza. Namwimbia baba.” Wengine wakawa wanacheka taratibu Malon akageuka vizuri akimtizama. Joshua akauweka. Ukaanza. Naya akaanza taratibu nakumshangaza Joshua. Hakuwa anakosea biti anafuatisha tu. “Sasa safari ya pili ndio nakwenda juu. Jiandae baba.” “Wewe ungeimba tu.” “Kwani wewe ndio baba? Wewe ndio baba? Na siimbi tena. Twende zetu Joshua.” “Haya Bale toka.” “Mimi nimefanyaje jamani baba?! Nilikuwa namtia moyo tu!” “Hata hivyo sitaki kuimba tena mbele yako. Labda ulipie hela.” Bale alicheka kwa sauti mpaka wengine wakaanza kucheka. Naya akaenda kujaza chungu chake maji na kuyaweka maua yake.

“Njoo Naya uimbe, nitakulipa.” Bale akamwita akicheka. “Huna pesa yakunilipa wewe.” “Ninayo Naya. Njoo umalizie.” “Sitaki. Nitakuja kumwimbia baba, tukiwa wawili tu. Tena kwa sauti zote mpaka afurahie. Ila ukiwa wewe haupo. Twende zetu Joshua.” “Sasa mbona unamtoa mwenzio bila kula?” Baba yake akamshitua ndio akili zikamrudia Naya. “Halafu Joshua wangu hajala siku nzima! Pole mpenzi wangu, nilikusahau. Sasa mbona hukunikumbusha?” “Uliniambia unaharaka yakuwahi nyumbani Naya. Lakini nilikwambia tukitoka kazini ndio tungekwenda kula.” “Nilisahau swala la kukimbilia nyumbani, kukutana na li Bale. Pole. Acha nikuangalizie chakula.” “Hapana. Nisindikize, tukazungumze kidogo.” Naya akajisikia vibaya. “Samahani Joshua.” “Usijali kabisa. Mimi nitakuwa sawa. Twende.” Akaaga, nakutoka akiwa amemshika mkono Joshua.

“Natamani kukusikia ukiimba Naya.” Naya akacheka sana. “Basi niwekee tena ule wimbo. Si utanisaidia?” “Kabisa.” Wakakaa hapo nje kwenye ngazi. Joshua akawasha tena kutoka kwenye simu yake. Naya akaanza tena. Joshua akamsaidia hapo mwanzoni kwa sauti ya kawaida tu, ila vikaendana haswa. Ndani wakiwasililiza. “Naanza mimi.” Joshua akatingisha kichwa kukubali akicheka kwa furaha. Naya akaanza. “Great is your Mercy towards me, Your love and kindness towards me, Your tender mercy, I see, Day after day. Forever faithful towards me, and You’re always providing for me. Great is your Mercy towards me, Great is your grace.” Joshua akajikuta anapiga makofi kwa furaha, na yeye akampokea kwa sauti nzuri sana, lakini si juu kama alivyomwimbia baharini. Alipomaliza tu, Naya naye akampokea, ila safari hii akamfanya mpaka Joshua akasimama akishangilia. Zayoni akatoka.

“Naya!” Akashangaa. Joshua akaimba tena taratibu, Naya akampokea katikati wakamaliza kwa pamoja. Joshua alifurahi sana. “Naya! Na wewe umeufanya usiku wangu kuwa mzuri! Kumbe ndio unaimba hivyo!” “Alikuwa akiimba sana pale kanisani. Maisha yakamchanganya huyo, sijamsikia tena mpaka leo.” Baba yake naye akatoka, Naya akacheka. “Umenisikia baba?” “Lazima Bale akulipe.” Bale akasikika akicheka sana.

Akatoka Bale. “Hapo kweli nitakulipa. Naya wa aina hii alipotea muda mrefu mno, humu ndani hajasikika zaidi ya miaka! Mimi nilijua umeshasahau kuimba!” Naya akacheka. “Naya na Bale walikuwa wakiimba sana kanisani. Sana.” “Tukisaidiwa na mchumba wa Naya.” Bale akaongeza na kumfanya Naya acheke sana. “Yaani Ino!” Naya akaongeza. “Mara wagombane na Bale. Mazoezi ya kuimba yanasimama.” “Eti mwanaume mzima ana zira!” Wakacheka sana, Joshua akakumbuka kusimuliwa habari za Ino, kuwa ni mjuaji sana.

“Sasa akizira, hapo ujue uimbaji unasimama kwa muda. Bale naye hajui kubembeleza. Anaanza kumcheka. Sasa mimi tena aliyenigombelezea, inabidi tena hasira ziishe, nimbembeleze Ino ili aje atupigie kinanda au gitaa. Inategemea siku hiyo mtaalamu yule ameamua nini!” “Sijaelewa.” Joshua akaingilia.

“Nilikwambia Ino ni mjuaji?” “Nakumbuka.” “Sasa yeye ni mjuaji anayejua haswa. Anajua vitu vingi mno. Sijui Mungu alimpendelea vipi jeuri yule!” Wakazidi kucheka kila wakimkumbuka Ino. “Sasa pia akawa ndio mwalimu wetu wa sauti. Anataka kila mtu aimbe anavyotaka yeye. Ukikosea tu, anagomba mpaka hamu yakuimba inaisha. Sasa kaka huyu.” Akamuonyeshea Bale. “Hataki dada yake nigombeshwe pale. Anamwambia ananitia hofu, mwishoe nitaona kuimba ni kitu kigumu, nikimbie kuimba.” “Ambayo ni kweli.” Joshua akaongeza. “Sasa uongeaje wa Bale kwa Ino ndio huo ulikuwa ukimkera Ino, anazira mpaka Bale akamsemelee tena kwa baba yake, ambaye ndio alikuwa mwenye kanisa, au tena mimi ni mbembeleze.” Wakazidi kucheka.

“Akija siku hiyo anazungumza kingereza!” Wakazidi kucheka. “Ino ana fujo yule mtu!” “Anazungumza kingereza na nani?” Joshua akauliza. “Eti sisi! Wote anaotukuta pale tuliofika mazoezini.” Naya akazidi kucheka. “Sasa Bale alikuwa ana mkera kupita kiasi! Eti akizungumza kingereza, anamsaidia kukalimani kila neno huku akimcheka. Basi Ino alikuwa anakasirika. Akikataa kumfundisha kupiga kinanda, Bale anaenda kumuita baba yake, anamsemelea.” Wakazidi kucheka. “Sasa ulijua?” Joshua akamuuliza Bale. “Nilichoka manyanyaso ya Ino! Nilijiambia nilazima nijue kupiga kinanda na ngoma. Tukasumbuana hivyohivyo mpaka nikajua. Tukawa tukiimba kila siku kanisani na Naya. Kundi lilikuwa la watatu. Na yeye akiwemo huyo Ino. Sasa anataka kutupanga mimi na Naya. Labda tuvae nguo za rangi fulani ili tuimbe naye. Mimi nikawa namkatalia. Namwambia baba yangu hawezi akaingia gharama ya nguo kila jumapili eti sababu ya kuja kuimba na wewe hapa!” “Basi akija siku ya jumapili kama hatujavaa rangi hiyo aliyotaka yeye, haimbi na sisi. Tunabakia mimi na Bale ndio tunaimba. Basi ananuna karibia kupasuka.” Wakazidi kucheka.

“Ino! Na habadiliki. Anamisimamo yake migumu kweli!” Baba yao akaongeza. “Halafu baba yake wala hakuaga hivyo! Alikuwa mstaarabu sana  yule mzee.” Akaongeza Bale. Leo umenifurahisha sana.” “Basi tuimbe ule wimbo wako ulikuwa ukiupenda Bale.” Bale akacheka na kuanza kuimba hapohapo. “You came from heaven to eath!” Naya akampokea. Ulikuwa wimbo wa zamani sana, lakini waliuimba vizuri sana. Bale akaweza kuweka sauti zao sawa, ungependa warudie watoto hao waliokuzwa kanisani. Waliimba vizuri sana.

“Kumbe nyinyi ni waimbaji hivyo!” “Wamechukua kwa mama yao. Huyo alikuwa akifundishwa sauti hapa na mama yake, mpaka akamudu kutumia pumzi yake vizuri kwenye kuimba. Ndio maana ule wimbo wenu mliokuwa mkiimba hapa mpaka ukatutoa wote hapa nje, aliweza kupanda juu sana, na kubakia juu akitetemesha sauti bila kukwama! Basi ni kazi ya mama yake huyo. Alikuwa muimbaji sana.” “Ila Naya amezidi kufanana na mama bwana!” “Basi wakati mwingine akikaa pale kwenye kochi namuona kama mama!” Zayoni naye akaongeza. “Ila hata Bale mnafanana sana na Naya. Kama mapacha!” Akaongeza Joshua. Wakacheka na kutoka kwenye hali ya unyonge iliyotaka kuwaingia baada ya kumkumbuka mama yao. “Shuleni walikuwa wakituita mapacha wa nje! Na hivi huyu alirefuka haraka na kunifikia, ndio kabisa.” Naya akaongeza kukubaliana naye.

Ndio siku ya kwanza angalau Joshua akapata nafasi ya kuwa karibu na Bale na kumsikia akizungumza kwa furaha. Joshua alimuogopa kidogo Bale. Alimuona ni kama hajajifungua kabisa kwake, ila kumtizama tu. “Lazima nikupe pesa ukanywe hata soda.” “Sitaki soda. Ninazo huko kazini, na sinywi.” “Naya naye! Sasa unataka nini?” Bale akauliza akiwa amesimama pembeni ya baba yake. “Unamaanisha kweli? Maana sio nikutajie kitu ninachokitaka, halafu usininunulie!” “Nitakununulia. Niambie.” “Baba unamsikia Bale lakini?” “Atanunua tu. Si ameahidi mwenyewe?” “Sasa sio utaje nyumba!” Wakacheka.

“Hakawiii huyu. Unataka nini?” “Kuna viatu nimeviona kule dukani. Navitaka, vyakuendea kazini.” “Naya! Sio viwe vya hela nyingi mpaka unimalize kabisa!” “Wewe umemwambia utamnunulia. Na ununue Bale.” Baba yake akaweka msisitiza. “Asante baba.” “Naya naye! Kwani kinachokushinda kutaja zawadi za kawaida ni nini?!” Bale akalalamika. “Mimi sio wakawaida. Muulize baba.” Walicheka sana. Ila Naya hakucheka.  “Kweli wewe si wakawaida Naya! Naya niwatofauti sana! Anatushangaza wote pale kazini.” Joshua akaongeza akisifia. “Umesikia wewe Bale? Maana Bale haamini. Mwambie tena bwana!” Wakazidi kucheka.

“Mwenzio Joshua amenipa maua, na laptop mpyaaa. Kunipongeza.” “Naya! Iko wapi?” Bale akashangaa sana. “Ipo kazini nimeifungia. Nimeona isichukue furaha yangu ya maua. Mpaka kesho.” “Naya naye wa ajabu! Yaani maua na laptop unafurahia maua?” “Basi sikupi laptop ile ya zamani uliyokuwa ukiipenda.” “Naya!?” “Wewe si umesema mimi ni waajabu? Nampa Zayoni.” “Asante Naya.” Zayon akafurahi sana. “Hapana Naya. Ile laptop ni ya thamani sana, kama umepata nyingine, mpe Bale mwemye uhitaji kuliko Zayon.” “Afadhali unisaidie baba! Mimi nimehangaika laptop sana, mpaka nikawa nakuazima! Nipe mimi Naya. Nitakununulia viatu unavyotaka. Mwenzio nataka kuja kurudi shule.” Bale akabembeleza.

 “Naya amesema atanipa mimi.” Zayon akalalamika. “Sasa wewe Zayon laptop ya nini kama sio mambo ya picha tu?” “Ndio hayohayo. Mimi nataka. Naya ameshaninunulia kamera. Napata shida yakutengeneza picha zangu. Naya alikuwa akiniazima ile.” “Basi na mimi nitakuwa nakuazima. Na kwa kuwa wewe ni mtunzaji, nitakuachia kwa muda.” Hapo Zayon akakubali kwa furaha. “Basi ndio unifuate kazini tukanunue hivyo viatu.” “Iwe kesho Naya. Mimi kesho kutwa naondoka na Malon.” Naya akapoa.

“Usiondoke Bale! Tutafute kazi hapahapa. Mungu atatusaidia tutapata.” Naya akaongea kwa kulalamika akimsihi kaka yake kwa kumuhitaji. “Nataka biashara Naya. Cheti kikitoka ndio nitatafuta kazi na kurudi tena shule angalau nipate shahada ya pili, lakini biashara ikiwa inaendelea.” Naya akarudi kukaa. Akanyamaza akiwa ameinama. “Nakwenda kwa muda. Nikijiweka sawa na kutengeneza njia zakumfikishia baba mazao huku nyumbani kwa urahisi, narudi.” Naya akanyamaza akiwa ameinama. Wakatulia hapo kwa muda hakuna aliyeongeza kitu, mwishoe wengine wakarudi ndani walipokuwa wamemuacha Malon, akabaki Joshua na Naya hapo nje. 

Naya & Joshua,

Bado Malon Ndani Ya Picha.

Joshua akamchungulia pale alipokuwa amejiinamia. “Naomba usiondoke bila kula, Joshua. Tafadhali sana. Itanisumbua, sitaweza kulala vizuri.” “Nitakuwa sawa Naya. Nataka tuzungumze.” “Tuzungumze ukiwa unakula. Hujala tokea asubuhi! Nilikusahau mpenzi wangu. Nisamehe.” Joshua akacheka. “Ila ujue sitarudia kukusahau tena. Haya maua yamenichanganya Joshua! Sikutegemea. Ni kitu nilikuwa nikitamani, ila sikutaka kuwa nikiomba. Nilikuwa nikisubiria mtu ndio anifikirie, aje anipe kama hivi. Nimefurahi mpaka nikakusahau mpenzi wangu. Ila haitarudia tena.” “Usijali. Hata mimi nimekuona jinsi ulivyofurahia. Ila chakula utapata wapi Naya? Acha nikifika nyumbani nitatafuta kitu nile.” “Bale amepika. Nimesikia harufu ya chakula. Na lazima atakuwa amenibakishia. Twende ukale.” “Subiri kwanza Naya. Pale mezani amekaa Bale na Malon. Sitajisikia vizuri kula pale. Sitaki nionekane nawaingilia.” “Basi nitakuletea kwenye gari, maana hapa kuna mbu. Tafadhali Joshua. Kula kidogo ndio uondoke.” “Sawa. Utanikuta garini.” “Sawa.” Naya akaingia ndani, Joshua akarudi garini.

“Hongera mama. Ni ripoti ya nini hiyo?” Baba yake akampokea. “Asante baba yangu. Lakini acha nimtayarishie chakula Joshua. Nimejisikia vibaya, nimemsahau wakati yeye alimtuma mpishi wake mchana, anipikie na kuniletea chakula kazini! Hapo yeye hajala tokea asubuhi.” “Sasa kwa nini usile naye? Au huyo mpishi alipika kidogo?” Zayoni akauliza. “Hivi unavyomuona amekaa hapa, sio hivyo anapokuwa kazini. Yupo mbiombio kila wakati. Vikao vya ndani na nje ya ofisi siku nzima, hana muda. Alipanga tukitoka kazini ndio twende tukae sehemu tule pamoja, ila nikajisahau, nikamwambia anirudishe kwa baba Naya haraka, nije nimuonyeshe maua. Ukweli nimejisikia vibaya sana.” Naya akamalizia akiwa anaelekea jikoni. Kukawa kimya, lakini kila mtu alikuwa akimsikiliza.

Akamuwekea chakula alichokuwa amepika Bale na kukipasha moto. Huyo Bale akipika hata ugali tu na maharage, hutoona haya kumpa mgeni. Alijaliwa kipaji cha kupika haswa. Usiku huo alitengeneza tambi za chumvi, nyama ya kuku alikata vipande vidogo na kuchanganya na njegere. Kwa kutizama tu ilivutia. Akavipanga kwenye sinia, akatoka jikoni. “Funika bwana Naya!” Bale akamuwahi. “Nilijisahau sababu ya haraka.” “Subiri.” Bale akanyanyuka na kwenda kumtafutia kitu cha kufunika. Akajikuta amesimama pembeni ya Malon, ameinamia simu yake.

Akajifikiria, akaona amsalimie. “Unaendelea vizuri Malo?” Akamuuliza kwa upole. Malon akamwangalia. “Nipo sawa tu. Na wewe?” “Mimi naendelea vizuri.” Bale akarudi na kumsaidia kufunika kile chakula. “Asante.” “Siku nyingine ndio ukumbuke. Sio unatoka na chakula kinapigwa na upepo mpaka unakifikisha huko kimejaa wadudu!” “Naye Bale! Sasa si nimekwambia nimejisahau sababu ya haraka?” “Sasa unaanza kubishana badala ya kupeleka chakula!” Baba yake akamshitua. “Si Bale huyo!” “Mimi nimekushika mguu?” “Naomba usijibu, toka Naya.” “Ananiudhi Bale mimi jamani!” Naya akasikika akilalamika huku anatoka. “Taratibu usimwage sasa.” Baba yake akamtahadharisha. “Maneno mengi mpaka akifika huko sahani tupu, amemwaga chakula chote!” “Wewe unataka arudi.” Baba yake akaongea, wakacheka. “Nimekusikia sana ila sina muda na wewe.” Naya akasikika akijibu huko nje.

Joshua akafungua mlango ili kupokea chakula. “Nitakuwa mama mzuri. Usiwe na wasiwasi. Nikishiba, nitakuwa nikikumbuka familia.” Joshua alicheka sana. “Sasa mbona chakwako sikioni?” “Josee alileta chakula kingi! Nikala nusu mchana. Jioni wakati nakusafishia vyombo, nikamalizia.” “Usingekuwa unasumbuka kuosha!” “Usijali. Huwa nasuuza tu, kuondoa harufu ili visije nuka. Huwa anaweka vyakula vyake kwa usafi sana, mpaka naogopa kuchafua ile bag ya chakula!” Joshua akacheka tu. Naya akazunguka na kupanda garini. “Chakula ni kizuri sana.” “Bale anajua kupika sana. Na anapenda. Sio kitu chakulazimishwa. Anabuni mapishi yake, huwezi kuiga.” Joshua akaendelea kula.

Pesa/Kazi.

“Kuna safari nimekuwa nikiahirisha, sasa inanilazimu kwenda.” Naya akatulia kidogo. “Yule uliyenikuta nikizungumza naye kwenye simu ni Hugo.” Naya akatulia. Joshua akajua hajaelewa. “Hugo Gutsche mwenyewe.” Joshua akaweka msisitizo Naya akabaki ametulia. “Humfahamu Philip Hugo Gutsche? Mwenyekiti au mmoja wa mmiliki wa kiwanda chetu?” “Joshua Kumu!? Pale ndio ulikuwa ukizungumza naye huyo baba mwenyewe!?” Joshua akacheka alipomuona Naya amehamaki vile. “Sasa mbona ulikuwa umetulia vile hata huogopi?” “Nimeshamzoea. Jumbe zake nyingi huwa anapenda kunifikishia yeye mwenyewe, sio mtu mwingine.” Naya akajiweka sawa.

“Joshua wewe si mwenzangu!” Joshua akacheka sana. “Ndio maana pale kazini wanakuogopa sana Joshua!” “Sio kwa ajili hiyo bwana! Mimi ni mchapakazi ndio maana na Mr Gutsche ananiheshimu.” “Nitakumiss Joshua! Unakwenda kwa siku ngapi?” Joshua akameza chakula kilichokuwepo mdomoni. “Nimemwambia nina kikao lazima nikifanye kesho asubuhi. Kwa hiyo tutaondoka na ndege ya mchana.” Naya akakutulia kidogo ila akaona aulize kupata uhakika. “Umesema tuta!? Unakwenda na nani?” “Jema.” Moyo wa Naya ulishituka, kisha akapoa mwili mzima. “Historia inajirudia tena.” Akawaza Naya na kuinama akichezea mikono yake.

 “Huwa haichukui muda mrefu. Mambo yakienda sawa na kufanya vikao vyote kwa haraka, baada ya siku 4 au 5 tunakuwa tunarudi.” “Kwa hiyo muda wote huo mnakuwa na Jema hotelini?” Joshua akashituka hilo swali na kutulia kidogo akitafakari. Haikuwahi kuwa tatizo wala halikuwahi kuwa wazo la kulifikiria kichwani mwake.

“Mara nyingi sana huwa nasafiri na Jema. Ndiye mtu anayepanga kila kitu changu cha ofisini. Zaidi kwenye vikao kama hivi.” “Kwa hiyo jibu ni ndiyo?” Naya akarudi kwenye swali lake tena. “Ndiyo Naya. Wanatutafutia hoteli moja. Lakini Jema ananiheshimu sana. Hajawah..” Akasita kidogo. “Anaujua msimamo wangu.” Akarekebisha usemi wake. Naya akamwangalia. “Hata hivyo anaye mchumba wake, nafikiri watakuja kuona. Ila sijui. Ninachojua hakuna mazingira ya mambo ya nje ya kazi.” Naya kimya. “Kwanza sitampa hata sababu yakufikiria hayo. Anajua wewe upo na mimi.” Naya akacheka taratibu na kusugua mikono yake.

“Tafadhali naomba uniamini Naya. Mimi si mtu wa kigeugeu.” “Nakuombea Joshua.” Naya akajibu taratibu na kutulia. “Nakuahidi nitakuwa mwaminifu kwako Naya. Sio kwa Jema tu, hata kwa wanawake wengine. Nimejiapia hivyo. Kwanza sitaki kumkosa Mungu wangu. Endelea kuniombea tu, nirudi salama.” “Nakuombea Joshua.” Naya akatulia, lakini Joshua akamuona amebadilika kabisa ile furaha yote ikaisha.

 “Swala la usafiri ungependa nikuachie gari au nikutumie dereva?” Naya akakunja uso akiwa ameinama. “Usafiri wa kukupeleka na kukurudisha kazini, na jumapili kanisani.” “Hapana Joshua. Huna sababu ya kufanya hivyo. Hapa mtaani huwa kunakuwa na wezi. Wakijua kuna gari hapa, na hatuna ulinzi, watakuja kuiba vifaa vyake. Baba alitoa ulinzi baada yakurudisha gari ya Malo. Hatuna mlinzi. Halafu swala la kuja kufuatwa asubuhi na kurudishwa jioni na dereva, baba hawezi kukubali.” “Ni mtu ninayemfahamu.” “Hapana Joshua. Mimi namfahamu baba. Hata ukimwakikishia vipi hawezi kukubali.” Naya akaendelea.

“Anasema wanadamu wana mtindo wakubadilika, hasa tamaa yeyote ile ikiwapata. Huwa wanakwenda umbali mkubwa sana, na hubadilika mpaka unashindwa kuamini kama ni mwanadamu au mnyama. Wewe mwenyewe alitaka kukuona kwanza na nikazungumza naye sana juu yako ndipo akakubali. Hawezi kunikubalia kwa mtu baki. Anaona ni heri awe ananipeleka mwenyewe kituoni, anione nimepanda kwenye daladala, na kunisubiria jioni pale kituoni, kuliko anichukue mtu baki.” Naya akageuka.

“Yupo baba mmoja anaishi upande wa juu, kabla kuingia hapa, unaendelea na hiyo barabara hapo mbele mpaka kwake. Anafanya kazi posta. Ana mke na watoto wake. Wadogo kwetu. Mkewe alimwambia baba kuwa mumewe anaweza kuwa akinisogeza mpaka Ubungo, baba akakataa kabisa. Anapita hapo barabarani kila siku asubuhi, lakini baba alikataa asinipe lifti.  Nitakuwa sawa tu. Usijali.” Joshua akapoa kabisa. Akajua mambo yatamuharibikia. Naya anarudia maisha yakupanda daladala baada ya kumtaka arudishe gari! Anaondoka na kumuacha Malon hapo kwao! “Heri hata haya mahusiano yangekuwa yamekomaa! Ndio machanga hivi na ninatakiwa kuondoka?” Akawaza Joshua.

“Umeridhika na chakula?” Naya akavunja ukimya. “Asante. Nimeshiba kabisa.” “Basi acha nikuage. Ili nikirudisha vyombo, nikaoge kabisa, nipumzike.” Joshua akamwangalia. Naya akacheka na kuinama. “Sitakusaliti Naya.” “Nakuombea Joshua.” Akajibu Naya taratibu. “Nenda ukapumzike Joshua. Usiku mwema.” Akashuka garini na kuzunguka upande aliokuwa amekaa Joshua ili kuchukua vyombo. Kuishi na Malon kulimwathiri sana Naya. Imani kuwa mwanamke na mwanaume wanaweza kuwa pamoja sehemu, haswa mwanamke akiwa anamtaka huyo mwanaume! Naya akajua historia inajirudia. Na ujumbe aliokuwa ametumiwa! Akazidi kukosa raha.

“Ila kesho asubuhi unisubirie. Nitakufuata.” “Nashukuru.” “Na nakuomba nikuombe kitu Naya.” Naya akamwangalia. “Hivyo viatu unavyohitaji vya kazini, naomba mimi ndio ninunue.” Naya akacheka kwa wasiwasi kidogo. “Sio kwamba sina pesa Joshua. Zile ulizonipa bado ninazo. Unakumbuka kiasi cha pesa ulichonirushia lakini?” “Tafadhali naomba kununua mimi hivyo viatu.” “Nataka kuvaa na viatu atakavyoninunulia Bale, Joshua. Naona kama nitajisikia vizuri. Acha aninunulie tu. Kwanza akija kesho kunifuata kazini ndio itakuwa vizuri nirudi naye nyumbani. Usijali.” Akampokea vyombo. “Usiku mwema Joshua.” “Mbona unaniaga kama hatutazungumza tena?” “Naomba leo niwahi kulala. Sijisikii vizuri.”  Naya akaongea bila kumtizama.

“Huna haja yakuzungumza. Ila nataka tu kujua upo na mimi kwenye simu. Nisijisikie mpweke. Ni sawa au nitakuwa nikikusumbua?” “Hapana. Sio usumbufu. Basi nikioga, nitakupigia.” “Nitashukuru. Ila usisahau kuwa nakupenda Naya. Na ninakuhitaji wewe.” Naya akacheka huku akiangalia vile vyombo. Maneno mazuri alishayasikia sana. Aliambiwa na Malon mchana na usiku, ila vitendo ndio vilishindwa kulingana na maneno. “Usiku mwema Joshua.” Akaaga na kuondoka na kumuacha Joshua kwenye wakati mgumu. Ni safari ya kikazi! Sio starehe!  Na Jema ameshajua kuwa hiyo safari ipo. Anafanyaje!

Akabaki pale kwa muda, akaamua kurudi kuzungumza na baba yake Naya. Akagonga na kuingia wote wakamgeukia. “Samahani mzee wangu.” “Bila shaka. Karibu.” Joshua akaenda kukaa kochi la karibu yake. “Samahani lakini.” “Karibu.” Joshua akajivuta mbele kidogo. Wote kimya, wakitaka kusikia. “Nina safari ya kikazi ya siku zisizopungua 5. Naondoka na ndege ya kesho mchana. Asubuhi nitakuja kumchukua Naya, ili twende kazini. Jioni hatakuwa na usafiri, na siku hizo 4 mbeleni. Nimemuomba nimuachie hii gari.” “Hapa hakuna mlinzi Joshua. Nilitoa ulinzi. Wezi watakuja kuiba vioo mpaka matairi.” Joshua akacheka kidogo kwa wasiwasi.

“Ameniambia Naya. Lakini yupo kijana huwa namtumia kwa kazi za udereva. Kwa gari hii hii maana kama sio Naya, mimi huwa natumia gari ya ofisini na dereva wa ofisini. Kwa hiyo hii gari inakuwepo tu nyumbani mpaka nikiwa na shuguli binafsi, na ndiyo anayotumia huyo dereva. Naweza kumwambia akawa anakuja kumchukua Naya asubuhi na kumrudisha jioni.” “Nakushukuru sana Joshua kwa huo msaada. Lakini hapana.” Hakutaka hata kuuma maneno. “Huyu atakuwa sawa tu. Huwa nampeleka mwenyewe kituoni, na kumsubiria jioni anapotoka kazini. Hana tatizo. Wewe nenda kafanye kazi kwa utulivu kabisa. Huyu Naya niachie tu mimi. Atakuwa sawa.” Joshua akatulia kwa muda akifikiria.

“Unakwenda wapi?” Zayoni akauliza. “Makao makuu ya hii kampuni yetu. Johannesburg, Randburg, huko Afrika ya kusini.” Akamjibu akiwa amepoa. “Kumbe wewe unaendeshwa na dereva kabisa?” Kila mtu akacheka, kasoro Malon. “Ndiyo Zayoni.” Joshua akajibu. “Baba hataki mtu asiyemjua yeye vizuri, amuendeshe Naya. Kila mtu anajua. Naya hajakwambia?” Zayoni akaendelea na maswali yake taratibu tu. “Aliniambia.” “Basi baba hakubali. Ni heri hata...” “Haya Zayoni, ni muda wakuoga, na wewe ukalale.” Bale akaingilia. Zayoni akasimama bila yakubisha, na kuondoka akiwa ameshaingiwa hofu. Akajua ameongea kitu ambacho hakutakiwa kuzungumza. Joshua akabaki amekaa tu pale.

“Twende nikusindikize Joshua.” Naya akatoka jikoni. “Asante. Usiku mwema.” Akaaga lakini nakushukuru moyoni kuona Naya amemtoa pale. “Asante Joshua. Uwe na safari njema leo, na hiyo kesho ukisafiri. Usiwe na wasiwasi juu ya Naya. Atakuwa sawa tu.” “Nashukuru sana mzee wangu.” Kabla hajatoka, maana alimpisha Naya, baba Naya akamwita.

“Joshua!” “Naam!” Joshua akaitika kwa heshima na kugeuka. “Nakushukuru sana kwa heshima unayompa Naya. Hujichukulii tu mamlaka kwake. Hilo nakupongeza.” Kidogo hapo Joshua akapata ujasiri. “Nakushukuru mzee wangu.” “Kabisa. Unampa heshima kubwa sana! Ila kuna mambo nimejiwekea, sitaki kuja kujuta au niseme kujuta tena. Nahisi gharama ya kuja kulipia huo uzembe au mwanya mdogo ninaokuwa nikiuachia inakuwa kubwa sana, kwa kuepuka kuwajibika kidogo tu. Hapana. Naomba univumilie tu.” “Nimekuelewa kabisa mzee wangu. Na ninashukuru. Asante.” “Usiku mwema.” “Asante na wewe.” Baba Naya akafikisha ujumbe mpaka kwa Malon. Joshua akatoka na yeye baba Naya akarudi chumbani kwake. Kukapoa, kimya.

“Mimi nitakuwa sawa Joshua. Wala usiwe na wasiwasi juu ya swala la usafiri. Hakika nitakuwa sawa. Rudi nyumbani ukapumzike.” Wakamsikia Naya akimtuliza huko nje. “Nilifikiria hata niwe nakuchukulia taksi, lakini nikagundua taksii ndio sio salama kabisa.” Naya akacheka kidogo. “Usiwe na wasiwasi. Nitakuwa sawa kabisa. Nenda kapumzike. Leo umekuwa na siku ndefu.” “Asante. Nitakuona kesho.” Joshua akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Naya akarudi ndani kuoga, na kurudi chumbani kwake akijishauri kama apige simu au aache tu kwa usiku huo. Hofu ilimjaa kila alipokuwa akirudia ujumbe alioupuuza aliokuwa ametumiwa na Njama jana yake. Akaurudia tena na tena. Mwishoe akaona amtumie ujumbe baba yake. ‘Naomba uje tuombe pamoja. Nashindwa kulala.’ Baba yake alikuwa chumbani kwake. Aliposoma ujumbe, akatoka. Bale akashangaa anaelekea chumbani kwa Naya bila hata kuzungumza nao. Malon akaona aage tu. Alishapata ujumbe wake kwa kupitia pongezi alizopewa Joshua, akamuaga Bale na kuondoka.

“Mbona umejawa wasiwasi tena, ile furaha yote uliyokuja nayo leo imepotea!” Baba yake akamuuliza. Naya akazima simu kabisa na kuiweka chini. “Njoo ukae hapa na mimi kidogo. Uniombee, halafu unisubirie nilale.” Akajua hataki kuzungumzia linalo mkera. Akavuta kiti na kumshika mkono binti yake. “Kabla ya kuanza kuomba. Unataka nikuombee nini?” “Kila kitu.” Naya akajibu. Baba yake akamwangalia na kuanza kumuombea kwa jumla tu, zaidi faraja. Akamaliza. “Ukae hapohapo usiondoke.” Baba yake akavuta kiti kwa nyuma na kutulia. Akamuona anawasha tena simu. ‘Nipo na baba. Nashindwa kukupigia simu. Naomba tuzungumze kesho. Usiku mwema Joshua. Na maandalizi mema ya safari.’ Akatuma huo ujumbe na kuiweka simu chini bila kusubiria jibu akiwa amezima sauti kabisa. Akaingia ndani ya chandarua na kulala, baba yake kimya kama kawaida yake. Naya akalala kwa haraka tu, akijua baba yake yupo pembeni yake. 

Asubuhi ya Safari ya Joshua na Jema.

Alilala bila Joshua masikioni mpaka alarm ilipomuamsha. Akachukua simu yake ili kuzima, akakuta ujumbe aliorudisha Joshua usiku uliopita. ‘Nakupenda Naya. Na sitachoka kukwambia jinsi ninavyokupenda na kukuhitaji maishani.’ Naya akatulia kwa muda. Akakumbuka maneno hayohayo aliyokuwa akiambiwa na Malon, kisha kutoka na kwenda kulala na wanawake wengine. Akaweka simu pembeni na kuanza kujitayarisha kwa haraka asijue jinsi anavyomtesa Joshua ambaye bado hakujua ni nini chakufanya.

Alipomaliza, akakuta baba yake alishamwandalia kifungua kinywa. “Siwezi kula baba. Tumbo limejaa gesi.” “Huo ni wasiwasi Naya. Ni nini?” “Sijui baba yangu. Ila ninachojua kwa hakika, kumvumilia Malon kwa muda mrefu sana kwenye mahusiano, kumeniathiri mno baba yangu.” Akafikiria kidogo na kunyamaza. Baba yake akaangalia muda. “Mwenzio atakuwa amefika.” “Jioni unisubirie kituoni.” “Sio hapa. Njoo mpaka Kibaha. Leo kuna mambo nataka niyamalize. Nitakuwa huko mpaka usiku.” “Nitakupigia.” Baba yake akamsindikiza mpaka nje ila hakutoka getini baada yakuona gari ya Joshua hapo.

Naya akaingia garini. “Ulilala salama?” Joshua akamuuliza mara alipoingia. “Ndiyo. Na wewe?” Naya akamuuliza akifunga mkanda. “Sikulala vizuri Naya.” Naya akawa amemuelewa. Akanyamaza. “Niambie ni nini kinakusumbua? Au ni nini nimekosa?” “Hujakosea Joshua. Huna ulipokosea. Ila kama nilivyomwambia baba, kuishi kwa muda mrefu na Malon, nikimvumilia kwa mengi, kumeniathiri Joshua. Kumeniathiri sana, ndio sasa hivi natambua hilo. Ila huna tatizo.” “Labda niulize hivi, unawasiwasi na mimi kusafiri na Jema?” Naya akatulia kwa muda hajui ajibu nini.

“Kama ni Jema, tafadhali usiwe na wasiwasi Naya. Siwezi kukusaliti hata iweje. Kwanza naanzia wapi? Akili zangu na mawazo vipo kwako Naya. Natafuta nini kingine? Tafadhali naomba usiwe na wasiwasi. Mimi sio mtu wa tamaa!” Naya akacheka kwa wasiwasi kidogo kama akijaribu kujituliza huku akikumbuka ujumbe wa Njama unaomfanya azidi kujawa hofu.

Akajishangaa kuona mikono yake inaanza kutetemeka. Akaikalia akijaribu kutulia. “Bale atakuja kunichukua nikitoka kazini. Tutaenda naye kununua viatu.” Akaona abadili mazungumzo. “Nakuhurumia swala la usafiri, sijui chakufanya! Hakika kwa mara ya kwanza nimechukia safari za kikazi.” “Naomba usichukie Joshua.” “Naachaje Naya? Jana usiku umeshindwa hata kuzungumza na mimi kwenye simu?” “Nilikuwa na baba. Tuliomba pamoja, akanisubiria mpaka nikalala, ndipo akaondoka. Nilikutumia ujumbe. Hukupata?” “Nilipata, na nikakujibu. Niliona umesoma ujumbe wangu asubuhi, lakini hukunijibu Naya?” “Nilikuwa najitayarisha halafu nikawa na baba.” Naya akajitetea.

“Tafadhali naomba nafasi ya kukusikia wasiwasi wako. Tafadhali sana. Kama mimi ambavyo huwa nakuomba uniombee hata kwenye simu nikiwa ninauhitaji, na mimi naomba hiyo nafasi unayompa baba Naya. Sihitaji kuchukua nafasi yake, ila angalau unishirikishe tu. Jambo linapokuwia gumu, na mimi naomba kujua, tusimame pamoja huko kugumu.” “Sawa.” Naya akakubali kwa haraka na kutulia, lakini bado Joshua akamuona hayupo sawa.

“Mimi sina tamaa za wanawake Naya.” “Ni kweli. Hata mimi. Halafu mara nyingine na Malon walikuwa wakimfuata wanawake. Wao wenyewe walikuwa wakimtaka alale nao. Halafu Malo alikuwa hajui kukataa. Basi alikuwa akilala nao lakini anasema ananipenda mimi. Kila mtu alikuwa akimwambia mimi ndio mwanamke wake. Na kila mtu alikuwa akijua, lakini bado wanawake walikuwa wakimtaka alale nao.” Joshua akamsikia akiongea kama mtu aliyeshikwa na baridi kali. Akapunguza AC ya gari.

“Wanampenda vile mwili wake ulivyo. Na pesa anazokuwa anawapa. Kwa hiyo wanawake wakawa wanajua yupo na mimi, huku bado wanamtongoza, na yeye akawa hajui kukataa. Kuna siku nilimfumania kwenye nyumba tuliyokuwa tukiishi naye Morogoro, akanipiga kibao. Lakini akaniomba msamaha. Akasea aliingiwa na mshituko. Na huyo dada alikuwa mkubwa kwa Malo, na alikuwa akinifahamu mimi kuwa nipo na Malo, lakini bado alimfuata Malo nyumbani baada ya kujua mimi nimerudi huku nyumbani akamfuata ili Malo amlale.” Naya akajikuta akizungumza tu.

“Pole Naya, lakini...” “Najua wakati mwingine ni kama naonekana kama ninakuwa na wasiwasi tu. Hata rafiki yake wa karibu Malo alikuwa akisema nipunguze wasiwasi. Lakini katika hisia zangu mara zote nilikuwa sikosei. Nakuwa napatia. Ila sisemei kwako wewe! Namzungumzia Malon.” Naya alizungumza mengi. Akasimulia mengi na mengine akawa anarudia japo alishamsimulia huyo Joshua. Aliongea bila kumpa nafasi, mpaka wakafika kazini.

“Mimi nahisi nimewahi sana kuinga tena kwenye mahusiano. Nilitakiwa baada ya Malon, nitulie kwanza. Kama kuna kupona nipone ili niwe tayari kwenye mahusiano mengine. Hivi nilivyo, sitaweza.” Hapo Joshua akashituka. Akaegesha gari na kumgeukia. “Unasemaje Naya!?” “Naombe muda Joshua.” “Nilikwambia nitakusubiri Naya.” “Hapana. Naomba nitulie kabisa. Nitakapokuwa tayari kama utakuwa hujapata mtu mwingine, nitakwambia.” “Ni nini Naya?” “Siwezi Joshua. Nahisi kuchanganyikiwa. Sitarudi kwenye hayo maisha ya wasiwasi tena. Sitaweza.” Naya akaanza kulia. “Naogopa mno. Sina nafasi ya kuumizwa tena. Naomba unielewe tu. Nitashindwa hata kufanya kazi. Nimejawa hofu isiyo na sababu.” “Nashukuru kama umetambua hilo. Umejawa hofu isiyo na sababu Naya!”

 “Siwezi kujisaidia Joshua.” “Nisikilize Naya. Nilikwambia na nitaendelea kukwambia. Sijui uliishije na Malon, lakini hiki tulichonacho mimi na wewe, nakiheshimu sana. Kinaweza kisiwe kimekomaa, lakini mwenzio nimeshaingia agano na nimejifunga kwako. Nilikwambia huwa sijui kuanza jambo na kuishia katikati. Hapo utanisamehe. Ulishanikubalia. Ukaniambia unanipenda, mimi nitasimamia hapo, wala sitarudi nyuma. Mashaka yanaweza kuja, lakini isiwe sababu ya kutengana! Sitakuacha Naya. Kama unachanganyikiwa, jua upo na mimi, na nitasimama na wewe. Changanyikiwa ukiwa na mimi sio mbali na mimi. Unanielewa?” Naya akatingisha kichwa akikubali.

“Basi naomba utulie.” “Sawa.” Akakubali kwa haraka na kuanza kujifuta machozi. “Acha nikaoshe uso, nianze kazi. Kuna kitu nataka kumaliza kabla ya mkutano ulioitisha.” Naya akafungua mkanda. “Nakupenda Naya. Najua umeshazoea kusikia hayo maneno, lakini naomba tulia na kuyatafakari hayo.” “Sawa. Nashukuru kwa usafiri Joshua. Najua unatoka mbali kunifuata mpaka kule. Asante.” “Karibu, lakini ujue wewe ni jukumu langu.” Naya akacheka taratibu lakini Joshua alijua bado kuna kitu kimemfunga. Bado alijawa hofu asielewe ni kwa nini! “Asante.” Akashukuru na kushuka.

 Sumu Ya Chini Kwa Chini.

Baada ya kama ya dakika 15 akiwa anafanya kazi zake, Joshua akaingia na laptop yake mkononi. “Vipi?” Naya akamuuliza. “Nimekuja kufanya kazi hapa karibu na wewe.” Akavuta kiti mbele ya meza ya Naya. Akaweka laptop yake Naya akabaki akimwangalia. “Uliweza kuwasha laptop yako mpya?” “Bado.” Joshua akamwangalia. “Naweza nikawa sijaweza kukufahamu kwa undani Naya, lakini nahisi kuna kitu kinaendelea ambacho hutaki kuniambia.” Naya akatulia.

“Ni nini?!” “Sijui Joshua!” “Hapana. Unajua na ndicho kinachokusumbua. Ila ninaumia kuona bado unashindwa kuniamini Naya!” Hapo Naya akaumia kidogo. “Niambie ni kitu gani bado kinashindwa kukufanya unashindwa kuniamini japo nimejifungua kwako kwa asilimia 100! Ninakupa sababu gani hiyo? Au hujawahi kunipenda?” “Hapana Joshua. Nakupenda na ndio maana naogopa. You are soo good to be true.” Joshua akakunja uso na kutulia.

“Kwamba unanitilia mashaka?” “Hapana. Hivyo ulivyo na kila kitu unachonifanyia, ndivyo nilivyokuwa nikimlilia Mungu anipe. Umekuja ulivyo na zaidi mpaka naogopa Joshua! Afadhali vile alivyokuwa Malon, nilishazoea umalaya wake, lakini naogopa chochote kisijetokea kwako ukiwa na mimi, nitashindwa kuja kumuamini mwanaume yeyote tena. Ndio maana naona ni heri...” “Uwe mbali na mimi ili chochote kikitokea, usionekane ulikuwa na mimi wakati nafanya uzinifu?” Akamalizia Joshua akimtizama.

“Hivi unajua nina miaka mingapi sijalala na mwanamke?” Naya kimya. “Sina tatizo la nguvu za kiume wala sina tatizo la wanawake kwa sasa. Na ninajijua sio mbaya.” Naya akatulia. “Mwanzoni nilikuwa silali na wanawake kwa kuwa walikuwa wakinikimbia. Sasa hivi silali na wanawake si kwa sababu ya shida ya wanawake, au sina hamu ya kulala na mwanamke!” Naya akainama. “Ni kwa kuwa ....” Kabla hajamaliza akashangaa Naya anamkabidhi simu yenye ujumbe. Akajua anataka asome. Akatulia na kuvuta simu ya Naya.

‘Usifikiri Jema anakutetea wewe. Anatetea ajira ya hawara yake. Anajua Joshua akiwa juu na yeye atabaki kuwa juu. Jema anafaidika kwa mafanikio ya Joshua ndio maana hataki chochote kitokee kwa Joshua hapo kazini, anahangaika kuficha ukweli. Lakini huwa wakitoka hapo, wakiwa nje kikazi, wanalalana kama kawaida. Nilishuhudia kwenye safari moja tulienda na jamaa South.’ Joshua akakaa sawa na kuendelea kusoma. 

‘Tulikuwa wote watatu. Tumekodishiwa vyumba kwenye gorofa moja ndani ya hiyo hoteli. Kila mtu chake. Asubuhi, nilimuona Jema anatoka chumbani kwa jamaa anarudi chumbani kwake, tena akiwa hovyo kweli! Nikamuuliza, hakukataa ila kuniambia hayanihusu.’ Naya akamuona Joshua anakunja uso.

‘Baada tu ya kuwafumania, wakajua nimeshawajua, ndipo nilipoanza kuona mabadiliko. Nikaanza kuachwa kwenye safari nyingi za kikazi. Wakawa wanakwenda wao wawili tu. Jamaa anakula Jema nje ya nchi, wanaficha watu hapo kwa kuwa Jema anajulikana anaye mchumba tena anakaribia kuolewa. Na hilo pia halikuwahi kumzuia Jema. Alimwambia Jamaa, akimuhakikishia penzi, anamuacha mchumba wake waliyekuwa wameanzana naye tokea sekondari. Unachezewa Naya. Unanikataa mimi kwa ajili ya Jamaa ambaye anavifichovificho huyo! Na usifikiri kuolewa kwa Jema ndio kutawatengenisha. Joshua na Jema ni watu wa muda mrefu sana hao, wanajua kuzicheza karata zao vizuri tu. Wewe na wa Jema wote mnachezewa tu.’ Ujumbe ukaishia hapo.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ø Historia inajirudia kwa Naya?

Ø  JE, Tabia za Joshua ni kama Malon?

 Kamba yakatika pabaya haswaa!!

Ø Faida kwa nani??

Usikose muendelezo.

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment