“Nina
majeraha na madonda moyoni mwangu, kiasi ya kwamba natamani ibakie hivyohivyo.”
“Ndio maana muda wote huo hukuniambia?! Maana nimeona ni ujumbe wa tokea juzi!”
“Kabisa Joshua. Sipo tayari kusikia chochote kuhusiana na hilo. Ndio maana huyo
mtuma ujumbe alipoona nimesoma huo ujumbe, akajaribu kunipigia, lakini sikutaka
kupokea na nimemblock kila mahali. Sitaki kusikia tena.” “Sasa utafanyaje?
Maana chaguzi ya kuachana, haipo mezani.” Naya akanyamaza.
“Sitakuacha
Naya.” Naya akamwangalia na kurudi kufanya kazi yake. “Sijawahi kulala na Jema,
na Mungu wangu nishahidi Naya.” Naya akatulia akijua pengine kuna maelezo,
lakini hapakuwa. Akajua kuna jambo. Akaendelea na kazi. Pakatulia. “Sasa hivi
Jema ananiheshimu sana. Na ameelewa hapatakuja kutokea mahusiano kati
yetu. Nilimuhakikishia, na nikahakikisha analielewa hilo. Amerudisha heshima ya
kazi kwa asilimia zote na akijua mimi ni kiongozi wake. Ananiheshimu na wala
sitakaa nikakusaliti kwa ajili ya Jema.” Naya akabaki kimya akiendelea na kazi.
Kwa kuwa kompyuta ilikuwa ikimwangalia Joshua pale alipokaa nyuma yake, akaona
anarekebisha ile ripoti.
“Naya?”
Akamwita. “Nataka kutoa mambo ya idara nyingine, ibakie kuwa ripoti ya idara
yetu tu, kisha nione itakavyokuwa. Nitamuomba Jamal ripoti yake. Niipitie, na
kulinganisha na hii nitakayoitengeneza.” “Iwe ni baada ya yeye kuwa na yake
tayari.” Naya akamgeukia. “Jamal ana maneno mengi vitendo vyake nivichache na
vimejaa sababu. Ukimpa ripoti yako tu, ujue ndio hiyohiyo atakayonipa mimi.
Hakikisha anayo ripoti yake mkononi.” “Mbona alishachukua ile ya jana?”
“Ulimpa?!” “Ulipomkatalia pale kikaoni, akaniomba nije nimtumie kopi.” Joshua
akatingisha kichwa kama anayekataa. “Nilimkatalia makusudi ili yeye ndio
aandaye hiyo ripoti. Hicho unachokifanya wewe, ujue ndicho atakachofanya na
yeye, kisha kuikabidhisha nakuonekana kama ni yake! Hutapata matokeo ya
tofauti.” Naya akatulia kidogo akifikiria, mwishoe akarudi kuendelea na kazi
yake.
Pakatulia,
Naya akiwa amempa mgongo. Hakujua hata kama anafanya kazi zake au la, yeye
akaendelea na anachokifanya. “Jana alinipa kazi ya kuwa nikiwagawia na
kuwasimamia hapa kazi.” Naya akawa kama amekumbuka. “Ulionaje?” “Niliweza
Joshua. Nikaweka kajiutaratibu.” Akageuka na tabasamu usoni. “Unataka
nikuonyeshe?” Akamuuliza akicheka. “Nionyeshe.” “Basi mwenzio nilijifunza kule
nilikokuwa nikifanya kazi na wale wasichana. Warembo wa mjini. Wabishi na
wajuaji. Sikuwa nataka kelele nao, kwa kuwa yule mama aliniamini na kazi yake,
sikutaka kumuharibia. Nikabuni njia ambayo nikaitumia na kwa hawa wajuaji
wa hapa. Niliowakuta na wageni wenzangu.” Joshua akacheka.
Naya akamtumia kitu kwenye kompyuta yake. “Angalia.” Akafungua kwa
haraka, kwanza alishakuwa ameingiwa na hofu na alichosoma kwenye simu ya Naya.
Na ikawa kama Naya amemuhamishia yeye tatizo. Moyo wake ukapoa, akamuacha
Joshua anahangaika moyoni. “Unaakili Naya!” Wakacheka. “Sasa hapo niambie, nani
anabishana na mimi?” Joshua akacheka. “Hawawezi.” “Basi hapakuwa na kelele, ila
kununa, na mpaka wanatoka jioni, wakawa wote wamemaliza kazi zote nilizowapa.”
Joshua akafurahi sana.
“Mimi naona hiki kitengo wewe utakiweza Naya.” Naya akacheka.
“Mbunifu katika kila kitu!” Ikawa kama anampongeza. “Asante. Hapa nishajua nini
chakufanya leo. Bila kelele, ila kazi tu.” “Niliona ujumbe kutoka kwa Jamal,
akiwapelekea watu wa IT akikuombea access kubwa! Sikujua ni kwa nini! Nilipitia
tu kwa haraka nilikuwa na mambo mengi. Kumbe ndio hivi!” “Jana jioni
waliniongezea. Usinione hivi!” Joshua akacheka akimwangalia.
“Unaonekana unafurahia unachokifanya Naya!” “Sana. Japo mwanzoni
wakati namaliza chuo, sikujua kama nitahangaika ajira. Nilijua tungeendeleza
kampuni yetu ya mavazi, nikajua tungefanikiwa sana kwenye huo upande na
kuanzisha biashara nyingine. Ila nilikuja kukutana na uhalisia wa maisha!
Nikahangaika sana mtaani. Na kwa sasa hiki ninachokifanya ni kama kinategemewa
na familia nzima, ndio maana najituma zaidi. Maisha yameniongezea
nidhamu.”
“Ila na wewe pia unacho kipaji. Halafu Naya, bado unayo nafasi
yakuja kufanya kitu unachokipenda baadaye.” Akavuta pumzi kwa nguvu, nakucheka
taratibu. “Sijui Joshua! Naona itachukua muda! Wakati ule Mungu alininyanyulia
watu wawili wa nguvu, wakawa wakikimbia na mimi kwenye nilichokuwa nakifanya,
nahisi ndio maana ilikuwa rahisi.” “Ni Malon na nani?” “Na Chezo. Rafiki
kipenzi wa Malo.” Naya akawa kama anakumbuka kitu.
Joshua akamuona anacheka, kisha akageukia kompyuta yake. “Ni
nini?” “Hamna kitu. Nilimkumbuka Chezo.” Joshua akajua na hapo ipo stori. “Na
yeye alikuwa kama Malon?” “Hapana. Yeye ulevi wake ilikuwa pombe. Sio mtu wa
wanawake. Hata tabia ya wanawake ya Malon ilikuwa ikimuumiza sana na kunionea
huruma. Ila aliajiriwa, na pombe haikumfanya kuwa mzembe. Ni mtu anayejiheshimu
kwa kweli. Na angalau yeye nilimuona anaweza kumwambia kitu Malo, na Malo
akasikiliza. Wakati ule wa Malo, mkorofi.” “Sasa hivi Malon sio
mkorofi?” Naya akacheka akifikiria.
“Malon alikuwa mkorofi mno. Sio wakujificha. Wala usingeuliza.
Mungu amembadilisha Malo, au anambadilisha. Alikuwa hajui kunyamaza hivyo! Na
hana mipaka. Anyway, nilikumbuka kuna kipindi Chezo alinitongoza. Sasa nikajua
alikuwa amelewa sana siku hiyo, kumbe alimaanisha. Aliniona jinsi nilivyoshituka,
akaja kuniomba msamaha.” “Ulimwambia Malon?” “Nisingethubutu. Walikuwa ni wale
marafiki wa kama ndugu, tokea watoto. Nikajua ni pombe tu. Nikaachana nalo
hilo, ila tukaja kusikia baadaye alikuwa amewaambia wenzie na yeye alinipenda
na kuchukia vile Malon alivyokuwa akinifanyia. Akataka kunitoa kwa Malon. Mbali
na hivyo, alikuwa mtu mzuri sana. Alinisaidia sana.” “Pengine ni kwakuwa
alikuwa akikutaka kimapenzi.” “Pengine.” Wala Naya hakubisha, akarudi kuendelea
na Kazi.
“Huko ninakokwenda si unajua wapo nyuma lisaa tu na hapa?” Naya
akawa amemuelewa ila akanyamaza. “Naya?” “Nimekusikia Joshua.” “Naomba leo
usiku tuzungumze. Jana sikulala vizuri. Nimeshaanza kuzoea kuwa na wewe
masikioni. Inanisaidia kulala vizuri.” “Si umesema huwa mnakuwa na kazi nyingi
sana mkiwa huko? Utajuaje kama utakuwa na muda wakupiga simu kama huku?” Naya
akauliza taratibu. “Kwa kuwa najua huwa nikirudi hotelini nakuwa sina
chakufanya zaidi ya kujiandaa na mikutano ya siku inayofuata. Na mara nyingi
nakuwa na Jema, akinipa ripoti ya siku hiyo, ijayo na anakuwa akijiandaa. Ila
baada ya muda fulani huwa namruhusu kwenda kulala kwa ajili ya siku inayofuata,
maana ni kweli anakuwa na kazi nyingi.” Naya akatulia. Akajua na hapo kuna
ujumbe anatakiwa kuelewa.
“Sawa.” “Sawa nini?” Joshua akamuuliza. “Hata sielewi Joshua!”
“Ukiwa na mimi, sio kukimbia, utaelewa. Usikusudie kutopokea simu yangu.
Nikirudi hotelini tu, nitakupigia ili tuwe wote.” “Umesema unakuwa na Jema
mpaka usiku, Joshua!” Joshua akajua ameelewa. “Ataondoka na kutuacha sisi mpaka
ulale wewe, ndio na mimi nilale.” Naya akacheka na kumgeukia. “Unacheka nini
sasa?” “Kwamba na mimi nitakuwepo wakati ukiwa naye chumbani kwako?” “Naona
safari hii isiwe chumbani. Nimeona tunatafarisiwa vibaya. Tutaanza kutumia
kumbi za hoteli.” Naya akatulia.
“Unajua mimi huwa kwenye haya mahoteli, nakodishiwa full suite.
Chumba chenye kila kitu ndani mpaka sebule. Kwa hiyo huwa tukirudi hotelini,
kikao chetu binafsi huwa nahamishia chumbani kwangu. Tukimaliza kazi, ndipo
nalala. Hata siku hiyo anayokusimulia Njama, ni kweli Jema alipitiwa na
usingizi hapohapo chumbani kwangu. Mimi nilikuja kumgundua amelala, baada ya
kama lisaa mbeleni. Sikutaka hata kumgusa, nikamfunika hapohapo kwenye kochi.
Maana yeye alikaa kwenye kochi, mimi upande wa mezani. Nikamuacha hapo na
kuendelea na kazi zangu na kulala.” Naya akawaza ni kwa nini Njama hakuwepo.
Ikawa kama kama Joshua amesoma mawazo yake.
“Tena siku hiyo Njama aliniudhi sana. Sikutaka kuzungumza naye,
nikaamua kumuacha ila ni kweli nilimpunguzia safari. Nikawa nikimuacha awe
anabakia hapa akisimamia mambo mengine.” “Alifanya nini?” Naya akauliza.
“Tulikuwa na kazi nyingi sana siku hiyo. Ni kweli huwa wananitumia sana
nikifika huko. Sipumziki Naya. Huwa wananitaka nifanye mambo mengi, na moja kwa
moja na wao kina Jema, wanakuwa wapo busy. Sasa siku hiyo anayokwambia, hatukuwa
tumekula karibu siku nzima. Tuliporudishwa tu hotelini, nikawaambia tule kwanza
tupumzike kidogo, kisha tukutane wote chumbani kwangu. Tufunge kazi ya siku
hiyo na kujipanga kwa kesho yake.”
“Tulimuacha Njama sehemu ya kula, kumbe akahamia baa. Njama ni
mnywaji. Jema hanywi. Sisi tukarudi vyumbani. Muda ulipofika wakukutana tena,
nikashangaa ni Jema tu ndiye amefika, Njama hayupo. Tukamsubiria zaidi ya
lisaa, nikamwambia Jema ampigie. Akampigia sana, ikawa anamkatia simu. Jema
akamfuata chumbani kwake, hakumkuta. Ikabidi amfute kule tulipomuacha, akamkuta
amelewa akaanza kulalamika kuwa tunatumikishwa kupita tunavyolipwa. Akalalamika
mengi, Jema akamuacha.”
“Jema akarudi kuniambia hayupo kwenye hali yakufanya kazi. Amelewa
sana. Anaongea mambo mengi ni bora kumuacha tu. Hapo alikuwa na kazi ambazo
tunazihitaji ili kufanikisha siku inayofuata. Jema akamtumia ujumbe kumuomba
alete laptop yake. Alikuja amelewa, hajitambui. Nikamwambia hawezi kufanya
lolote akiwa na hali ile. Akapumzike tu. Ndipo akarudi kulala, sisi tukaendelea
na kazi. Jema akalala chumbani kwangu, kwenye kochi mpaka asubuhi alipoamka.
Sasa mimi sijui walizungumza nini baada ya hapo. Ila nataka kukuhakikishia
Naya, hakuna kinachoendelea kati yangu na Jema. Kwanza najua ananiogopa
sana.” Joshua akaendelea.
“Alinijaribu nilipofika tu hapa. Maana nilimkuta hapa. Nilipoelewa
nia yake kwangu, nikamuonywa kwa wazi kabisa bila mafumbo. Jema alielewa,
akaomba msamaha. Na ukweli, sijui kwa upande mwingine, lakini najua
anajiheshimu. Si msichana muhuni kwa kuwa kila nikisafiri naye, namuona
ametulia haangaiki na wanaume wa huko na hata hapa sijawahi msikia anamwanaume
ila kazi tu. Nafahamiana na mchumba wake. Najua wanakaribia kufunga ndoa. Hayo
mengine ni ya Njama tu.” Naya akavuta pumzi kwa nguvu.
“Nakaribia kumalizia ripoti yangu. Unataka nikimaliza uione?”
Joshua akacheka akimwangalia. Ila alimuona ametulia hata usoni. Akajua
amemuamini. “Nikiwa nakwambia nakupenda, Naya. Huwa inaleta maana yeyote
ile?” Akamuuliza. “Mimi sikumbuki kama uliniambia unanipenda. Lini!?”
Joshua akacheka sana. “Naya?” “Utakuwa umenifananisha, ila mimi sikumbuki kama
uliniambia hivyo.” Joshua akacheka sana akitingisha kichwa. “Nakupenda Naya.”
“Mimi mwenyewe nakupenda.” Joshua akacheka. “Muone! Wewe unataka kuniacha kwa
maneno ya kizushi tu bwana! Ukoje Naya?” “Nilikwambia kuishi na Malon
kumenithiri Joshua. Nivumilie tu kama ulivyoahidi.” “Ukiwa unapatwa na mashaka,
tafadhali niambie.” “Hii week uliniambia upo leba.” Joshua akacheka sana.
“Sikutaka kukuchanganya.” “Sasa ndio ujue ungeniharibia safari
nzima kama ningeondoka na kukuacha kwenye hiyo hali. Nilikuwa nimeshavurugukiwa!
Hapa nimeshindwa kufanya kazi kabisa.” Naya akamwangalia na kuinama.
“Nimefurahi umeniamini Naya.” “Sasa umejuaje kama nimekuamini?” “Najua. Ila
nataka ujue sitalala na Jema si kwa sababu yako tu, pia kwa ajili ya Mungu
wangu.” “Unakaribia kuharibu bwana!” Joshua akacheka sana. “Naya!” “Wewe
ungeacha tu.” “Sasa hudhani hiyo ndio itakuwa sababu nzuri ya kutokukudanganya!
Nikilala naye huko, nikarudi nikiwa nimetulia. Yeye hasemi na mimi sisemi,
utajuaje?” Naya akanyamaza. “Yaani wewe unamuonea wivu mpaka Mungu!?” Naya
akaanza kucheka. “Usinigombanishe na Mungu bwana. Wenyewe tunapata.” Angalau
Naya akaonekana ametulia.
Watu wakaanza kuingia. “Umeshazaa sasa?” Naya akamuuliza kwa sauti
ya chini. “Mkunga wangu ameniambia nimezaa watoto wazima, tena wana afya
njema.” Naya alicheka sana. “Kwamba umezaa mapacha?” “Hata! Ni watatu mama.”
Joshua akaongea kwa kujivuna. Naya akacheka. “Mkunga wako nani?” “Roho Mtakatifu.
Yeye huwa ndio ananisaidia kwenye kuzaa. Akishapitisha yeye juu ya afya
ya kilichozaliwa, hapo huniambii kitu. Ujue lazima masikio ya watu yatawasha
tu.” Naya akamwangalia akicheka kama anayemtamania. “Ni hivyo nasafiri. Lakini
lazima tungeenda tukasherehekee. Ila nikirudi, kwa mara ya kwanza, nitataka
kusherehekea hiki nikiwa na wewe. Mungu wangu amefanya tena.” “Hongera
Kumu.” “Asante Naya Kumu. Safari hii Mungu anafanya mambo matatu kwa
mpigo! Wuuuu!” Naya akacheka akimtizama.
Wakaendelea kumsalimia. “Acha nikajiandae Naya. Nina vikao vitatu
mbeleni kabla sijaondoka leo.” “Sawa. Uzidi kufanikiwa Joshua.” “Na wewe
zaidi.” Akarudisha kiti kwenye meza alipochukua, nakurudi pale mezani kwa Naya
kuchukua laptop yake. “Usiache kunitumia hiyo kazi. Kabla ya kikao.” “Kweli?!”
Naya akashangaa kidogo. “Nina maana yangu. Nitumie tu.” “Sawa bosi wangu.”
Joshua akacheka nakutoka akitembea mwendo wake watu waliokuwa wakimwiga jinsi
anavyotembea. Naya akamsindikiza kwa macho na tabasamu kubwa usoni, wenzie
wakimwangalia.
~~~~~~~~~~~~~~~~
“Yaani nahisi Kumu atanihamisha kitengo LEO!” Jamal
akaingia akilalamika. Naya akageuka kumwangalia. “Hali mbaya Naya! IT
wameshindwa kunipa kompyuta nyingine. Nimekwama. Hapa nina dakika 10 kabla
yakuingia mkutanoni, niweke ile ripoti yako sawa.” Naya akamshangaa sana
moyoni. Jana yake alimwachia kitengo kizima kwa madai yeye anakwenda kuandaa
ripoti. Asubuhi hiyo bado analalamikia bado ripoti! Naya akaanza kumuelewa
Joshua. Akajua ndio maana Jamal ni mkali sana. Anataka watu wafanye kazi
kumrahisishia yeye. Akabaki akimtizama.
“Au sijui nimtumie ujumbe sasa hivi nimwambie IT wameshindwa
kunipa nyenzo!” Akawa anajiuliza mbele ya meza ya Naya. “Ila ujue sisi wote
kwenye hiki kitengo, hatutakuwepo mkutanoni.” Naya akamkumbusha. “Lakini kosa
sio langu!” Akajitetea. “Ndipo aliposema tusipohudhuria, itabidi kutoa maelezo
ni kwa nini kitengo chetu hakikuwepo kikaoni!” “Na leo anakwenda hukohuko kwa
wenye viwanda. Akiulizwa cha kupunguza gharama kwenye kampuni, naona na mimi
nitakuwa mmoja wao. Lakini kosa sio langu!” Naya akabaki kimya akimwangalia.
“Lakini vipi hapa?” “Hapa pako vizuri, nishamtumia kila mtu kitu
chakufanya leo. Nashukuru hao watu wa IT waliniongezea access.” “Jana
nilishinda ofisini kwao. Nikawasisitiza. Afadhali kama wamefanya.” Naya
akajiuliza moyoni huo muda anaopoteza hapo kuzungumza naye, si angefanya kazi.
“Nina wazo bosi wangu.” “Unayo ripoti nyingine!?” “Sio hilo. Kwa kuwa watu wa
IT wanakuzungusha, kwa nini usichukue hii kompyuta yangu, mimi nikatumia
laptop? Ninayo laptop mpya, nataka kuhamishia kazi zote hapo.” “Nikifanya hivyo
ujue sitapata mpya.” Naya akamshangaa na kubaki amemkodolea macho, mwishoe
akaamua kurudi kufanya kazi zake.
“Ile ya jana hukutengeneza tena hata kidogo?” Jamal akauliza kwa
wasiwasi kidogo akijibaraguza na cheko. Naya akamgeukia tena. “Joshua alinipa
kazi ya pembeni. Akitaka nijifunze zaidi. Nikaitengeneza, leo asubuhi
ameniulizia, nimemtumia.” “Mungu wangu! Hapo atanibana.” Akawa kama amekwama,
lakini akapata tena wazo jingine. “Nipe tu nikaibadili kidogo.” Bila kubisha
akiwa ameshaandaliwa na Joshua, akamtumia. “Tayari nimekutumia.” Jamal akatoka
hapo mbio bila hata kushukuru, Naya akabaki akimfikiria.
Kikaoni.
Kabla ya
dakika 6 za muda wa kikao kuanza, kitengo chote walikuwa wameshafika mkutanoni.
Naya akagundua vitengo vyote wapo hapo na viongozi wao. Akajua ripoti
zimeshaandaliwa. Wakabaki wakitaniana mpaka Jema alipoingia. Naya akaangalia
muda, zilibaki dakika 4 tu. Wakatulia kidogo wakimtizama Jema akijaribu
kuunganisha vitu, mara Kumu mwenyewe akaingia. Moyo wa Naya ukajawa furaha,
moja kwa moja Joshua akamwangalia, Naya akainama na tabasamu usoni. Wote
wakaliona hilo, wakaanza kukonyezana.
Akasalimia.
“Faith, tatizo lako lilitatuliwa?” Akauliza Joshua, macho kwenye saa ya
mkononi. Faith akasimama kama mshale. “Hapana bosi wangu. Nimegonga mwamba.”
Joshua akamwangalia na kumtizama kiongozi wake. “Jona, unajua anachozungumzia?”
Joshua akamuuliza kiongozi wao wa idara yao ya Research macho kwenye
tablet yake. Kimya.
Joshua
akatoa macho kwenye tablet akamwangalia Jona. “Hivi nimeuliza swali kwa sauti
au nimeliwaza tu?” “Nimekusikia. Ndio najaribu kufikiria anachoongelea hapa ni
nini nakushindwa kukizungumza kule idarani!” Joshua akasimama wima. Tayari
mikono akaweka mfukoni. Ungependa kumtizama. “Kwa maana nyingine, mlipotoka
hapa jana, hukutaka kujua ni nini alitaka kuuliza hapa!?” Joshua
akauliza taratibu tu. “Nilikuwa na mambo ya ripoti, Kumu! Siku ya jana ilikaa
vibaya sana. Pengine leo ndio tutazungumza kwenye idara yetu.” “Basi tunaomba
kusikia hiyo ripoti.” “Kwa hiyo mimi ndio niwe wa kwanza!?” Jona akauliza kwa
wasiwasi, Joshua akamtizama kidogo na kumgeukia Faith. “Baada ya hapa, nitakuwa
na dakika mbili, tunaweza kuzungumza, Faith.” Joshua akaonekana kujali.
“Nashukuru sana bosi wangu.” Faith akaonekana kulifurahia hilo, akakaa na cheko
usoni kila mtu akimtizama.
“Naomba
changamka Jona. Hatuna muda mrefu hapa.” Jema akaweka msisitizo. Joshua
akaangalia saa. Huyo dada akasimama na kusogea hapo mbele. Ukweli alikuwa
nadhifu na uzuri wa kuvutia. Ni kama aliyekuwa amevaa makusudi kwa hilo tukio.
Kiheshima, vizuri na kila kitu kilionekana ni cha thamani. Akasoma ripoti yao
vizuri sana tena kwa lugha ya kingereza kilichokaa sawa. Kwa hakika alikuwa
amependeza na anaonekana anaelewa anachozungumza. Akajieleza vizuri mpaka
akamaliza. “Safi sana.” Joshua akawa amesifia. “Imekaa vizuri sana.”
Akampongeza, na Jona akapumua kwa sauti mpaka wengine wakacheka. “Najua mlikuwa
mkimtumia Njama hizo ripoti, kwa sasa naomba mnitumie mimi moja kwa moja.”
“Sawa.” Jona akakubali akionekana kufurahia.
“Kuna
swali lolote kwake kabla hajarudi kukaa?” Wote kimya. Jona akarudi kukaa. “Mimi
jana nilikuwa wakwanza, leo nakuwa wamwisho.” Akasikika Jamal. Joshua
akamtizama na kumgeukia Jema. “Naomba tuokoe muda, tafadhali.” Jema akaweka
msisitizo. Viongozi wengine na wao wakafanya kama alivyofanya dada Chege, ambaye
ni Jona, Joshua akaonekana kuzifurahia. Akabakia Jamal akasimama. “Kama
nilivyosema jana. Bado watu wa IT hawajanifanikishia tatizo langu.
Wanalalamikia...” “Acha maneno mengi Jamal bwana! Wewe soma ulichonacho, na
kama huna pia tuambie.” Jema akawa mkali kidogo.
“Nina
ripoti yangu kabisa.” “Soma sasa!” “Jema naye!” Jamal akaanza. Kabla hajafika
katikati ya kuisoma hiyo ripoti, Joshua alishajua ni ripoti ileile ya Naya, ila
amebadilisha kidogo sana. Na akaiongea kwa ujasiri sana, kitaalamu, mpaka
akamaliza. “Kuna mwenye swali?” Yeye mwenyewe akauliza nakufanya watu wacheke,
kasoro Joshua akarudisha macho kwenye tablet yake. “Naona hakuna mwenye swali
Jamal, unataka porojo tu, nenda kakae.” Jema akamfukuza, watu wakacheka kidogo
na kutulia baada ya kukutana na picha yake na Naya kwenye screen. Wakajua
tablet ya Joshua ndio imeunganishwa hapo kwenye screen. Watu wakatulia
kuangalia picha. Naya alikuwa amekaa kwenye boti, nyuma yake yeye Joshua akiwa
amesimama. Akawa amemlalia begani macho yakitazama shingo. Akawa amejilaza
vizuri hapo kwa Joshua, Na Joshua akawa ni kama akimwangalia pale alipojilaza
begani kwake. Ilipendeza sana.
“Kiongozi
hiyo picha ipo vizuri sana! Unaweza kuuza kabisa, ikaongeza kipato cha
familia.” Felix akamtania Joshua, watu wote wakacheka. “Mimi mwenyewe nitanunua
wa kwanza kuunga mkono biashara.” Akadakia Mwita. Wote walionekana watu wazima
kwa Joshua. Joshua akacheka akiwa ameinama, kisha akanyanyua macho kumwangalia
Naya. “Eti, tuanze biashara ya kuuza picha?” Akamuuliza Naya, Naya
akacheka tu na kuinama. Wote wakacheka, Joshua akarudisha macho kwenye tablet
yake, kisha akasimama akiwa amerudisha sura ya kazi.
“Cha
kwanza, naomba niwapongeze wote. Kama ambavyo nasema. Kitengo chetu ni cha muhimu
na ndicho kinachofanya hii kampuni iendelee mpaka leo.” Wakajipigia sana
makofi. “Ni kweli na ndio maana napigania maslahi yenu wote, nikijua hii
kampuni inamuhitaji kila mmoja wetu.” Joshua akawapongeza na kurudia zile
ripoti kwa ufupi. “Ndio maana, kwa heshima yenu. Nimeona kabla sijazungumza na
yeyote yule kwenye hii kampuni, niwashirikishe nyinyi kwanza, kitu kipya
tunachokitoa.” Naya akashangaa wanapiga miluzi na kushangilia sana.
“Sasa
mbona hata hajasema ni nini!?” Akajiuliza Naya
akiwatizama wanavyoshangilia huku wakipiga meza, mwishoe wakaanza kupiga meza
wakiita jina la Kumu kama wapo bungeni. Wakagonga meza kwa pamoja huku
wakisema, “Kumu! Kumu! Kumu!” Naya akashangaa sana, akabaki ameinama akicheka.
Wote walionekana wamefurahia sana.
“Naomba
nimalizie. Na ninasisitiza, sio mimi bila nyinyi.” Wakapiga tena makofi.
Akatupa picha tatu kwenye screen. Ukumbi wote kimya. “Hivi ni vifaa vya kuuzia.
Tunataka hata wauzaji wa karanga, waweze kuuza bidhaa zetu.” Wote kimya. “Hiki
ni kifaa kwa muuzaji anayetembeza bidhaa zake. Tumemuwekea sehemu maalumu
yakuweza kubeba bidhaa alizokuwa akiuza mwanzo, makusudi ili asione
tumemwingilia. Ila tutampunja sehemu ya kuweka bidhaa zake za awali, kwenye
hiki kifaa chetu tutakachompa kama inavyoonekana pichani, ili sehemu kubwa
itakayobaki, abebe bidhaa zetu zaidi. Na hili sinia ni maalumu, litakuwa na
matundu yake na chini kitu cha kushikilia ni kwa ajili ya kuwekea chupa/bidhaa
zetu ziwe salama, zisiwe zikianguka hata akiwa anakimbilia wateja wake.” Watu
walishangilia sana.
Naya
alibaki ametoa macho. Ilitengenezwa muundo mzuri, picha yenyewe ilivutia
kuitizama. “Kila kijana atakayetaka kuuza bidhaa zetu, tutamkabidhi hii, pamoja
na tisheti 3, mkoba maalumu wa kuhifadhia pesa, pamoja na kofia. Ila kwa sharti
la kutouza bidhaa nyingine yeyote inayofanana na yetu isipokuwa zetu tu.” Watu
wakazidi kushagilia.
“Na hii
picha ya pili ni kwa wale wauzaji wenye vibanda vidogo tu barabarani.
Wanaochoma mishikaki na mahindi, au hata mihogo. Ataweka hapa kwenye coolerbox,
anauza bidhaa zetu, naye tutampa bidhaa kama huyu mtembezaji endapo atataka
kuajiri na mtu wakumtembezea, pamoja na mwamvuli mkubwa kwa ajili ya jua. Na
wote hawa, tutawauzia kwa bei ya jumla ili wajitengenezee faida.” Watu
wakashangilia sana. “Hii ni awamu ya kwanza, kufikia watumiaji moja kwa moja.
Lakini kutakuwa na shindano.” Hapo wote wakatulia.
“Katika
hawa wauzaji wa aina mbili, 10 watakao uza bidhaa zetu kwa asilimia kubwa ya
kiwango tutakachoweka, ndani ya mwezi mmoja, watajishindia pesa tasilimu, na
tutawapa mafunzo maalumu ya uuzaji, kisha kuwafungulia sehemu maalumu ya
kuuzia, ili waendeleze biashara yetu. Na hiyo itakuwa kwa mikoa yote, mpaka
vijijini. Jamal jiandae na idara yako. Nataka timu ya watu watakaochapa kazi, sio
sababu.” Watu wakashangilia sana.
“Zipo
sehemu ambazo hazina maduka, au kuna maduka lakini wanauza vitu vingi inakuwa
shida kwa mnunuaji kupata bidhaa yetu kwa haraka. Hiyo nitakuja kutoa suluhu
nitakaporudi kutoka safari. Inahitaji pesa nyingi, lazima nikaanzie juu.” “Inyeshe.”
Wakaanza tena kushangilia, Joshua akicheka. “Kabisa. Nataka hii nchi nzima,
isambae bidhaa yetu kwa wingi mno mpaka iwe kama alivyosema Naya. Mpaka watoto,
wagonjwa, wasioona kabisa na kuitambua bidhaa yetu kwa macho, wote waimbe
bidhaa zetu, na pia wafikiwe na bidhaa zetu.” Watu wakazidi kushangilia.
“Ndani ya
miezi miwili tu, nataka hivi vifaa viwe vimezagaa mtaani.” Watu wakazidi
kushangilia wakijua ndio ishakamilika. Kumu akisema jambo, hakuna anayepinga.
Akajua hata watu wa fedha watapitisha tu. Akisimama Kumu, ni kama amesimama
mmiliki wa hiyo kampuni. Walimuheshimu mno. “Tukaendelee kuchapa kazi, tukijua
hakuna kati yetu mwenye mchango mdogo. Kila mmoja wetu anahitajika.” Kumu
akafunga kikao. “Faith, bado unazo dakika mbili. Unataka bado kuzungumza?”
“Ningeshukuru.” “Basi twende.” Joshua akatoka kwa haraka, Faith naye akamfuata
akimkimbilia. Alipotoka tu watu wakaanza kushangilia tena na kufurahia Bonus kubwa
ya mwisho wa mwaka. Huwa mauzo yakiwa makubwa sana kama hivyo anavyopambana
Kumu, anahakikisha watu wa kitengo chake wanalipwa pesa ya ziada mwishoni mwa
mwaka.
“mungu wa
Coca, kaongea tena. Neema mwishoni mwa mwaka.” Wakazidi kucheka. “Hicho kichwa
kingine aisee! Daah!” “Na lazima itajibu tu. Acha nikaongeze mkopo, najua
nitalipa tu.” Wote wakacheka na kuzidi kushangilia. Kila mtu akazungumza lake.
Naya akajikusanya na kutoka kimya kimya akiacha watu bado wakishangilia, lakini
hata yeye alishangazwa na Kumu. Muundo wa hicho kifaa, jinsi
itakavyomrahisishia muuzaji kukibeba muda mrefu bila kuchoka, usalama wake!
Akajikuta akicheka huku akirudi ofisini kwao. Alichora vizuri sana na akaelezea
kwa ufasaha!
~~~~~~~~~~~~~~~~
“Kumu
anataka kukuona Jamal.” Jema akamwambia Jamal akisoma ujumbe, wakiwa palepale
chumba cha mkutano akiwa anasubiria hao viongozi wamtumie Joshua na yeye hizo
ripoti walizosoma. Hakutaka kusubiri ahadi ya kutumiwa baadaye, aliwajua
wanaweza wasitume hata baada ya juma. “Nilihisi tu.” Jema akamwangalia. “Naomba
nenda Jamal. Leo hana muda kabisa. Ratiba imebana mno. Kila kitu najaribu
kubana ili tusichelewe uwanja wa ndege.” “Nakwenda mama.” Jamal akaondoka hapo
lakini akajua ni nini Joshua anamwitia.
“Anakusubiri
ndani.” Fina akamuwahi hata kabla ya salamu. Jamal akazidi kuingiwa hofu.
Akagonga na kuingia baada yakumsikia Kumu akimkaribisha. “Naitika wito
Kiongozi.” “Tafadhali fanya kazi.” Jamal akatulia kidogo, hata hakukaribishwa
kiti. “Unanielewa Jamal?” “Nimekusikia Kiongozi.” “Nataka kuona mabadiliko
kwenye idara yako Jamal. Punguza visingizio, fanya kazi.” Jamal akashindwa hata
kujitetea. “Sitaki watu wapya kwenye kile kitengo. Walewale waliopo, nataka
uhakikishe wanafanya kazi. Uza vizuri kazi yako kwao. Hakikisha wanaelewa,
wawekee mikakati inayoeleweka, wafanye kazi. Hakuna chochote kitakwenda kwenye
hii kampuni, isipokuwa idara yako imefanya kazi yake. Hata kama tutabuni vitu
vizuri vya namna gani, bila kuvitangaza ili kuwafikia wateja, hakuna
kitakachotoka hapa. Na SITAKI wewe, utukwamishe.” Hapo Kumu akaweka
msisitizo.
“Sijui
kama unanielewa Jamal?” “Nimeelewa.” “Kama kwa sasa kuna jambo linakufunga,
tafadhali nijulishe ili nijue chakufanya. Sina hata dakika moja yakupoteza kama
hii tunayopoteza mimi na wewe sasa hivi, tukiambiana chakufanya wakati wewe ni
mzoefu hapa na unajua umuhimu wa idara yako. Tafadhali naomba kuona mabadiliko
Jamal. Na kikao kama hiki naomba kisije wahi rudia tena.” “Sawasawa. Lakini
nilifikiria safari hii nibadilishe watu pale ida...” Kabla hajamalizia,
akamuona Kumu akitingisha kichwa kukataa.
“Hapana
Jamal. Inawezekana unao watu wazuri sana ila hujajua jinsi yakuwatumia. Sitaki
mabadiliko ya watu ila utendaji. Asante.” Jamal akajua ndio anaambiwa
aondoke maana Kumu alisharudisha macho kwenye alichokuwa akiandika,
hakumwangalia tena. “Sawasawa.” Jamal akajibu hivyo na kutoka. Fina akamuona
anahema kwa nguvu, hata hakumsemesha.
Kuagana Kwa Naya Na Kumu.
Baada ya
muda Naya akiwa anafanya kazi akasiki, “Nimekuja kuagwa.” Naya akacheka na
kugeuka baada yakusikia sauti ya Kumu akiingia. “Nilijua ulishaondoka?” “Bila kuagwa!?”
Joshua akauliza akimsogelea. “Ripoti nzuri sana. Hongera. Kuna mambo kidogo tu
yakubadilisha, tutazungumza usiku kabla hujalala. Ila nimebakisha dakika 5, kwa
ajili yako.” Naya akacheka kwa furaha. “Twende.” “Hii hapa barua yako.
Nimekuandikia, usome njiani au ukifika.” Joshua akaipokea akiwa amehamasika.
“Wao! Asante.” Akabaki akiitzama, Naya akacheka. “Nimefurahi.” “Nimekuona.
Nimefurahi kama umeifurahia.” Akaiweka mfukoni.
“Kumu!
Kuna...” “Hapana Jema. Nimekwambia nipe dakika 5 zisizo na mwingiliano. Naomba
kila kitu kisubiri, tafadhali.” “Ni makao makuu!” “Zungumza nao.” Joshua
akajibu kirahisi tu na kumshangaza Naya. Maana kama ni makao makuu, inamaana ni
huko wanakokwenda.
“Twende
Naya.” “Wanataka kuzungumza na wewe Kumu!” “Unazidi kupoteza muda Jema. Maana
muda wote huo unaozungumza hapo nakushindwa kunielewa, ujue zile dakika 5
zinabakia vilevile, hazisogei. Kama huna majibu ya kuwapa, waambie nitawapigia
nikiwa njiani. Naomba dakika 5, tafadhali.” Akaweka msisitizo
akisikika kwa ukali. “Sawa.” Jema akarudi kwenye simu aliyokuwa ameshika
mkononi, Naya akamsikia akizungumza vizuri kwa lugha ya kingereza huku
akiondoka. “Twende.” Akamnyooshea mkono ili kumshika. Naya akacheka, akamshika
mkono wakatoka.
“Umekula
sasa?” Ilikuwa imeshafika mchana. “Nilikuwa nakimbia leo, sikuwa na dakika hata
moja ya kutulia. Kikao nilichofanya na nyinyi kwenye idara yenu, ilinibidi
nikifanye zaidi ya mara mbili tena ili kuwakilisha wazo letu.” Wakawasikia
wakizungumza huku wakitoka. “Sitaki kuchelewesha. Imebidi kuwauzia wazo kwa
haraka na kwa muda mfupi, ili utengenezwaji uanze na kama kuagizwa viagizwe.
Kwa hiyo ilibidi kukaa na watu wa manunuzi pia. Watu wote wa idara yao
kuhakikisha wanaelewa ile michoro.” “Umefanikiwa kuwauzia wazo zima?” “Kwa
asilimia 100.” Naya akacheka.
“Hongera
Joshua.” “Umeafikiana nalo?” “Sana! Lakini umenishangaza! Sikujua kama ni
mchoraji hivyo!” “Unapokuwa na mimi kwenye simu usiku, nakuwa nachora huku nipo
na wewe. Huwa napenda mawazo yangu yatoke yakiwa yamekamilika. Cha kwanza inanisaidia
usalama wake. Najua hakuna atakayeiba hapo katikati kabla sijakamilisha, na
pili inanipa muda wa kutafakari zaidi. Ningeweza kutafuta mchoraji, lakini huwa
nafanya mwenyewe. Hata hivyo Mungu alinipa kipaji cha uchoraji. Sifanyii nacho
mambo mengi, ila naona kinanisaidia hapa kazini.” “Hongera.” Wakaelekea ofisini
kwake. “Hujambo Naya?” Fina akamsalimia. “Mimi mzima. Pole na majukumu.”
“Asante. Karibu pande hizi.” Naya akacheka Joshua alishaingia ofisini.
“Asante.” Akaingia na yeye ofisini kwa Kumu.
Akamdaka
na kufunga mlango. Yakaanza mabusu ya nguvu. Alimkumbatia kwa nguvu mpaka Naya
akashangaa. Hakuwahi kumkumbatia hivyo. Akajituliza hapo, akifurahia harufu na
ladha nzuri ya midomo ya Kumu. Kama aliyepulizia kinywani kitu maalumu kwa
ajili ya hilo busu! Na hakuwa amembusu muda kidogo. Naya akafurahia kushikwa na
Joshua. Asiamini hatimaye anashikwa na mwanaume mwenye uhakika hashiki wanawake
wengine hivyo. Hamu ya mapenzi ikampata, akatamani mengi hapo, lakini
akajiambia apokee atakachopewa. Akaendelea kwa muda mrefu tu, Naya naye
akarudisha taratibu kisha akamwachia.
“Tumepita
hatua ya kama tunaachana au tunakuwa pamoja. Si ndiyo?” Joshua akamuuliza
taratibu wakiwa bado wamesimama. “Ndiyo.” Naya akajibu akiwa anatamani arudie
busu. “Ujue mimi nitasimamia hilo neno Naya! Maswala ya jambo linapotokea
unafikiria kuachana, naomba ubadilike. Fikiria ni jinsi gani tunaweza
kutengeneza tulichonacho sio kuvunja. Tafadhali sana Naya. Mwenzio nakuhitaji
sana maishani! Wewe unaye baba ambaye unaweza kumkimbilia, ukalala bila
kunitafuta! Tafadhali uwe unanifikiria na mimi ambaye sina hata mtu mwingine
wakumpigia simu usiku ila wewe!” Naya akajisikia vibaya.
“Samahani
Joshua. Nilipaniki.” “Naomba usisahau kuwa nakuhitaji sana. Sina ndugu, nawewe
ulinihidi utakuwa na mimi. Naomba na wewe usinibadilikie. Tafuta jinsi
yakuniweka karibu sio kunitoa kwenye maisha yako. Utaniumiza mno, Naya.
Tafadhali nifikirie kila kunapotokea tatizo.” “Nitabadilika Joshua. Naahidi
nitabadilika.” Akarudi kumbusu tena, na tena.
“Kingine.
Majibu ya kila shutuma zangu, tafadhali pata majibu kutoka kwangu mimi
mwenyewe. Najua umeishi na Malon muda mrefu, lakini tafadhali usinilinganishe
na Malon. Mimi sio yeye, na hivi nilivyokushika wewe, utabakia kuwa wewe
tu. Tulisema ni mpaka lini?” Naya akacheka na kujibu. “Mpaka kifo.” “Basi
naomba ulikumbuke hilo na naomba uwe unanisikia ninapokwambia nakupenda.
Najua umezoea kusikia hivyo huku ukitendwa mpaka ikapoteza maana. Lakini Joshua
Kumu anapokwambia anakupenda, anamaanisha amemaliza kila kitu, na maisha
yake ameyaweka kwako.” “Jamani Joshua! Kweli?” “Kweli Naya! Safari ya leo
ingekuwa ngumu sana kama tungechana kama jana. Tafadhali naomba nafasi
yakusogezwa karibu sio kunifikiria kuniacha. Nakupenda Naya, na nimeamua kuwa
na wewe. Mimi nitakupenda kwa dhati.” “Nashukuru Joshua.” Naya akajilaza
kifuani kidogo.
“Nikuulize
kitu Joshua?” “Karibu.” Naya akamwangalia. “Kwa hiyo nijihesabu nimeshapata mtu
wangu wa kudumu?” “Mimi mwenzio nimemaliza Naya. Nipo na wewe kwa asilimia
zote. Sitafuti wala kuangalia tena. Mungu amenipa wewe, nimekupokea hivyo
ulivyo, najua mengine Mungu atatusaidia tu.” Naya akacheka. “Nimefurahi Joshua.
Nimekuwa nikihangaika kutafuta mtu wangu mpaka nilikuwa nakaribia kukata
tamaa!” “Mungu alikuleta hapa kwa ajili yangu, Naya. Najua unazo ndoto zako. Na
mimi nitahakikisha lazima uje uziishi, ila ujue kuna mambo Mungu aliyashikilia
kwako, ili ujikute unaishia kwenye hii kazi, anikutanishe na wewe.” “Hapana
Joshua, ni ili anikutanishe na wewe. Mimi ndio nilikuwa
nakuhitaji sana Joshua. Mpaka ikafika kipindi nikahisi namuomba Mungu kitu
ambacho labda ni kigumu sana! Hakuna mtu wa aina yako! Hivi unavyoniona nababaika,
univumilie. Najifunza kuishi na muujiza wangu.” Joshua akacheka na kurudia busu
jingine la muda wa kutosha akiwa amemkumbatia Naya vilivyo mpaka simu ya mezani
ilipoanza kuita.
Akaendelea
kidogo kumbusu, kisha akamwachia. “Huyo atakuwa Jema. Mizigo yote amepeleka
kwenye gari. Inabidi tuondoke.” “Samahani kukuchelewesha. Ila nimefurahi,
natamani tungekuwa na muda zaidi Joshua.” “Na mimi natamani hivyo. Lakini nipe
muda tena kidogo. Nitarekebisha hii hali.” Naya akawa hajamuelewa. “Nimefurahi
tumepata huu muda Naya. Nimefurahi umeniaga vizuri. Nimefaidi midomo yako
mitamu!” Naya akacheka na kujificha uso. “Wewe ndio ulikuwa na ladha nzuri
mdomoni. Nilitamani tusimalize!” Joshua akainama tena na kumbusu, wakasikia
hodi mlangoni. Joshua akavuta pumzi kwa nguvu na kumuachia Naya.
“Bakisha
muda wa usiku kwa ajili yangu Naya. Naomba pokea simu zangu kila
ninapokupigia.” “Nitafanya hivyo. Uwe na safari njema. Subiri nikuombee.” Naya
akamshika mikono. Akamuombea kwa ufupi tu, akamaliza. “Hapo ndio umemaliza
kabisaaa. Naamini nitakuwa na wakati mzuri zaidi.” Naya akacheka. “Ni sawa
nikikusindikiza mpaka kwenye gari au haitakuwa sawa?” “Ndio ningependa zaidi.”
“Basi twende ili tusimuharibie ratiba Jema.” Wakatoka na kumkuta Jema mlangoni.
Jema
aliwapisha, Kumu akatoka akiwa amemshika Naya mkono. “Naomba iwe safari ya
kwenye gari Kumu. Sina dakika nyingine iliyobaki.” Wakamsikia Jema akizungumza
nyuma yao. Joshua hakujibu akaendelea kutembea. Jema akawapita. Alikuwa
amependeza haswa. Na kiatu chake cha juu kama kawaida yake. Naya aliweza kupata
harufu nzuri kutoka kwake. “Unataka nikuletee nini?” “Kwani huwa
kuna nini huko? Hata sijawahi kufika huko. Mimi nilikuwa nikinunua vitu vingi
kutoka Dubai. Hata pafyumu zangu zote nilikuwa nikitoa huko.” “Basi
nitakuangalizia kama wana aina nzuri za pafyumu. Nitumie majina.” “Naomba
usihangaike huko Joshua. Fikiria kurudi huku ili tuwe wote.” “Unataka nisimame
tena nikubusu wakati unajua sina muda uliobaki? Acha kunogewa Naya!” Naya
alicheka sana na kumpiga kidogo ngumi.
“Mimi
sitaki busu. Nataka usihangaike huko!” “Kwa hiyo nikisimama hapa na kutaka busu,
utakataa?” “Nitakufikiria.” Joshua alicheka sana mpaka kwa sauti ya juu huku
wakitoka. “Yamekuwa hayo Naya!?” “Kumbe! Wewe unafikiri unapata mabusu kwa
urahisi tu?” Joshua akazidi kucheka akimwangalia asiamini. “Lakini si
nilichokipata pale ndani ofisini wakati ukining’angania.” Naya akacheka sana
kwa aibu. “Mimi huyu?” “Wewe Naya.” “Utakuwa hukuwa umeelewa.” Joshua akazidi
kucheka mpaka wakafika garini. Ilikuwa imeshawashwa dereva yupo ndani na Jema
amekaa mbele tayari na mkanda. Akamgeukia Naya. Akambusu tena kidogo. “Safari
njema?” “Asante. Na wewe kazi njema. Tutaongea.” Naya akasubiri akapanda kwenye
gari, akampungia mkono, dereva akaondoa gari, ndipo Naya akaanza safari
yakurudi ofisini kwake taratibu na cheko usoni.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Alipofika
ofisini na kuangalia simu yake aliyokuwa amefungia kwenye droo, akagundua
Joshua alimtumia pesa. Akabaki ameduaa. Ikawa ni kama amemlipa mshahara wake wa
mwezi mara mbili yake. Naya alibaki akikiangalia kiwango kile cha pesa, akaanza
kusikia mikono inatokwa jasho asiamini. Akaangalia muda, akagundua ni masaa
mawili yaliyopita, halafu hata Joshua hakumwambia walipokuwa naye ofisini
kwake. Akatamani kumpigia simu, akakumbuka kuna simu alisema atapiga akiwa
njiani. Akamtumia ujumbe. ‘Nashukuru sana kwa pesa, Joshua. Ndio nimeziona!
Zitakuwa msaada mkubwa sana. Mungu azidi kukubarki, usipungukiwe daima.’ Hapohapo
akarudisha ujumbe mfupi tu. ‘Amina. Tutaongea.’ Naya
akajua amebanwa, asijue ujumbe huo anajibiwa huku akizungumza na simu ya muhimu
sana. Jumbe za Naya hazikuwa zikisubiri majibu. Wakati wowote, muda
wowote, ujumbe wa Naya ukiingia tu, lazima ajibu. Ila ujibuji wake ndio huwa
anajua yupo busy kwa kiasi gani.
Muda wa
chakula cha mchana ulipofika, akaletewa tena chakula. Mpaka Naya akabaki
akicheka. “Nakushukuru sana. Sasa vyombo utavipataje?” “Wakati nikileta chakula
kesho, nitachukua vya leo. Kuna kitu maalumu unataka kula kesho?” “Jumamosi
huwa tunakula tu nyumbani. Usihangaike.” “Hujawahi kula chapati niliyopika
mimi.” Naya akacheka. “Kesho nitakuletea chapati, nyama ya foili, na mchuzi wa
maharage. Nitakuwekea vizuri, ukale nyumbani.” Naya akacheka kwa shukurani.
“Nakushukuru sana, Josee. Asante.” “Kesho.” Akaondoka. Huwa Joshua anataka
chakula kiwe kinamfikia Naya mwenyewe moja kwa moja si kukiacha getini au
kumkabidhi mtu mwingine.
“Kama ni
kingi, naomba kidogo Naya. Njaa inauma na nimeishiwa kabisa, wangu.” Kijana
mmoja ambaye alimkuta hapo akaomba kinyenyekevu. “Huwa anaweka kingi. Kalete
sahani nikuwekee. Ila sijajua hata amenipikia nini!” Tayari hadhi ya Naya ikawa
imeshabadilika. Naya aliyekuwa akishinda na njaa kazini, sasa hivi anaye mpishi
wa kumletea chakula! Joshua alijua kumuenzi kwa namna ya juu mno. Aliingia hapo
kazini asubuhi hiyo akiwa amenyongea, lakini Joshua akaondoka hapo nakumuacha
na furaha.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Akapata
simu kuwa anamgeni. Akaangalia muda, akagundua muda wakutoka kazini aliomwambia
Bale ndio huo. Bado kulikuwa na baadhi ya watu ofisini na nje kuna mwanga. Naya
alishazoea kutoka wa mwisho hapo ofisini. Ila akaona asimuweke Bale, atoke tu.
Kuna dada hapohapo kwenye kitengo chao cha masoko, alitangaza kuuza wigi za
nywele halisi kutoka Brazil. Naya akazipenda ila hakuwa na pesa. Kwa kuwa
alitumiwa pesa yakutosha na Joshua, akaamua kununua hiyo nywele bila kujali
gharama. “Nataka kubadilika kidogo.” Akakusudia kumrudisha
Naya wa zamani mwilini mwake. Naya mwenye nywele ndefu. Hapo akiwa na nywele
fupi tu alivutia, sasa akiweka ndefu ndio utafikiri Mungu alimpendelea huko tumboni
wakati akifinyangwa! Na kwa kuwa alijijulia, Naya akajua akija kurudi hapo siku
ya jumatatu, watamsahau.
Akaelekea
ofisini kwa huyo dada upande wa Research. Ndani ya hilo jengo, lakini
upande mwingine. Akamkuta amejiinamia mezani kwake. “Samahani, Zera. Bado unazo
nywele?” “Ninazo mpenzi. Unataka ngapi?” Naya akacheka. “Naomba niangalie tena
picha, ili nichague.” “Na nitakushauri pia.” Akahamasika na kutoa simu. “Hii
ukiweka kichwani, ina baby hair nyingi na imejaa. Usiogope bei, nitakupunguzia.
Utakuwa kama toto la kimanga! Na uzuri huo! Watakusahau.” Naya akacheka
akiendelea kuangalia picha nyingine. “Naona kweli hii nzuri. Naomba basi
uniletee kesho tafadhali.” “Malipo lini?” Naya akakunja uso kidogo kama
hajaelewa.
“Nakopesha
mpaka siku ya mshahara. Ila kama huna mwisho wa mwezi huu basi tutaelewana.”
“Mimi naona nikulipe tu utakaponiletea hiyo nywele.” Zera akafurahi sana. “Ndio
raha yakufanya kazi na wenye nazo. Huwa nakuwa na hereni pia. Hereni zangu za
ukweli, na huwa hazichuji wala kuumiza masikio.” “Basi naomba kuziona pia.”
“Mambo yote kesho. Na nilivyoishiwa! Kesho nakuletea mzigo wote. Nitakuita
kwenye gari uchague.” “Asante Zera.” Naya akatoka. “Mwanamke wa Kumu huyo,
unafikiri atakopa?” Naya akasikia wakianza kumsengenya ndani. Wote wakacheka.
“Na kweli. Nilijisahau. Kesho najaa. Sitaki kukopwa.” “Sasa usianze kujishaua
Zera!” Naya akaendelea kutembea kutoka huo upande kwenda nje. Wala hakujali.
Alishazoea.
Bale na
Naya Juu ya Malon.
Naya
alitoka nje getini akitegemea kumkuta Bale akimsubiria, badala yake akakuta
gari ya Malon. Akajua Bale amekuja naye. Naya alikasirika sana. Akaamua aondoke
tu. Akaanza kuondoka na kuwapita wakiwa ndani ya gari, Bale akashuka kwa haraka
akimkimbilia. “We Naya vipi!?” “Umeniumiza sana Bale! Sijui ni kwa sababu ya
shida tulizo nazo, au vipi! Sijui! Lakini umeniumiza na sikutegemea.”
Naya akaanza kulia. “Shida zote ulizoniona nikizipata kupitia huyo Malon, bado leo
unamshikilia na kutaka aniharibie kwa Joshua!” “Malon amebadilika
Naya.” Naya akashangaa sana.
“Kwa
hiyo?! Unategemea nini Bale!? Unafikiri ni nini kitatokea?” Naya
akazidi kulia. “Mimi sio muhuni Bale na sina tamaa, muulize Malo. Alikuwa na
wanawake wengie tu, lakini sikuwahi kumsaliti. Ndivyo nitakavyofanya kwa
Joshua. Hata kama wewe humpendi, lakini Joshua ananipenda na ananiheshimu.
Nabakia na Joshua wangu. Sina shida ya usafiri wa Malon wala msaada wake. Wewe
endelea kutumia vitu vyake, akutajirishe. Ila mimi sitaki tena
uninunulie viatu. Wewe sio ndugu mzuri Bale. Unaweka pesa mbele kuliko mimi.” “Kweli
Naya ndio unaongea hivyo!?” Naya akaondoka bila kugeuka nyuma.
Malon
akabaki akiwaangalia. Naya analia, Bale anamkimbiza nyuma. Bale akaona ampigie
simu baba yao. “Naomba uzungumze na Naya, baba.” “Unataka nizungumze naye nini?” Baba
yake akauliza kwa utulivu tu. “Anashindwa kuwa muelewa.” Baba
yake kimya akimsikiliza. “Baba?” “Nakusikiliza.” “Nimemfuata kazini twende
kununua viatu, hataki.” “Kwamba ghafla viatu alivyokuwa akivitaka sana
jana, sasa hivi havitaki tena!?” “Naona anachanganya mambo ya Malon hapohapo.”
“Kwamba Naya ndio anachanganya mambo ya Malon!?” Bale akababaika
kidogo. “Mimi niliona nije na Malon ili kumsaidia usafiri.” “Umeanza lini
kujihusisha na mambo ya Naya?” Kimya.
“Wewe
umezaliwa na kumkuta Naya, nilishawahi kukuomba unisaidie hata siku moja kwenye
malezi yake?” “Nilitaka kusaidia tu baba.” Bale akajua
ameshaharibu. “Usikubali shida za muda zikakupotezea utu wako Bale. Unanielewa?”
“Naelewa baba. Ila nilitaka kusaidia.” “Kumsaidia Naya au wewe
mwenyewe?” Baba yake akamuuliza. “Naya, baba! Unawezaje
kufikiri hivyo?” “Unauhakika kuwa ni Naya na si wewe mwenye haraka
ya maendeleo?” “Baba! Nataka kujishughulisha na mimi! Nilifikiria utanipongeza kwa
kuonyesha juhudi na utayari wa kuthubutu!” “Kwa nia na sababu sahihi,
ndiyo. Lakini si vinginevyo Bale. Taratibu. Na katika mipango yako yote,
tafadhali usimuhusishe Naya wala usimguse. Hakuhusu kabisa.
Unanielewa Bale?” “Nakuelewa baba.” Bale akawa
mpole. “Basi ongeza utu. Na Bale?” “Nipo baba.” “Usiwahi kurudia
hata kufikiria kuuza binti yangu na usirudi hapa bila Naya, maana ni wewe
mwenyewe ulisema unakwenda kumfuata.” Simu ikakatwa.
Bale
alibakia kama amegandishwa kwenye friji. Hakutegemea! Akabaki akimtizama Naya
aliyekuwa akiendelea kutembea kuelekea kituo kikubwa cha Mwenge. Malon
akasogeza gari. “Twende Bale.” “Acha nimfuate Naya, Malon. Asante sana.
Tutawasiliana.” Bale akaanza kukimbia, akimkimbilia Naya. Malon akahisi
kilichokuwa kikiendelea. Akaongeza mwendo mpaka akamfikia Naya. Akashusha kioo
na kwenda kusimamisha gari karibu kabisa na Naya.
“Tafadhali
usimlaumu Bale. Nia yake ni nzuri.” “Ipi Malon? Ipi?” Naya
akamuuliza kwa hasira. “Kwa miaka yote niliyokuwa na wewe Malon,
ulishawahi kunifumania, au kunikuta na mwanaume mwingine?” “Unafika
mbali Naya.” “Si mbali. Ni ukweli Malon. Hata siku moja sijawahi
kukuingilia kwenye mahusiano yako. Hata yale ya wizi uliyokuwa ukiyaanzisha
tulipokuwa wote, nikajua, sijawahi kukufanyia fujo wala kukuingilia Malon.
Nilibaki nikiwaheshimu wanawake zako wote mpaka Rita aliyeninyanyasa mbele yako
ukanyamaza. Sikuwahi kukuingilia. Nilikuacha ukawa huru huku ukiniumiza.
Uliniacha, nikikubembeleza usiniache, Malon.” Bale
alishawafikia, akabaki amesimama pembeni.
“Ulinisaliti
nikiwa nakusubiria Malo! Nilikupa miaka zaidi ya mitano, nikikubembeleza,
kukusihi na kukuvumilia ili tu niwe wako. Maisha yangu yalijaa maumivu
makali sana ni kiishi kwa fedheha kwa ajili yako Malon! Uliniacha nikilia
mchana na usiku bila kunijali! Hukuwahi kunithamini ila tamaa uliweka
mbele. Ulilala na mpaka watu wa karibu yangu bila kunihurumia, lakini sikuwahi
kukusaliti ila kukusubiria mpaka uliponiacha rasmi. Wewe mwenyewe Malon uliniacha.
Mungu amenihurumia, amenipa Joshua, kweli bila huruma unataka kuniharibia! Kwa
kosa gani nililokutendea Malo ila kuwa mwema kwako?” “Nataka
kusaidia tu Naya?” “Kwa lipi na kwa nini?” Naya akamuuliza akiwa
analia na kwa hasira.
“Unataka
kumthibitishia nani, nini?!” Naya akaendelea kumuuliza. “Unamsaidia
nani hapa? Nani anataka msaada wako?” “Ni mimi mwenyewe
ndiye nilimtafuta Malon, Naya. Sio yeye.” “Sasa kwa nini
mnaniingiza mimi kwenye mambo yenu?” Naya akamgeukia
Bale. “Wewe ni mtu wa namna gani Bale!? Ulikuwa na mimi Morogoro
ukishuhudia nikihangaika kumtoa Malon jela. Ulisikia vile Malon alivyokuwa.
Ukajua uchafu wake kwa undani kabisa, kutoka kwa wanawake zake mpaka baba yake
mzazi pia alinikataza nisiwe naye. Yote hayo ulijua. Nilifikiri ungekuwa
umeelewa kilio ulichokuwa ukikiona kwangu na kujua ni kutokana na yale
uliyoyasikia kutoka kwa watu mpaka baba yake mzazi! Lakini umenishangaza na
kuniumiza sana Bale. Sijui ni shida, na kuona tunatoka kwa mzazi asiye na
pesa!?” “Usiseme hivyo Naya! Unakufuru?”
“Anayekufuru
kati yangu mimi na wewe ni nani Bale? Ingekuwa wewe ulikuwa na mwanamke kama
Malon, ukaja ukapata mwanamke mwingine, kwa sababu yeyote ile, ungelifurahia
kuona namrudisha yule mwanamke wa kwanza aliyekuwa akikutenda mabaya kwenye
maisha yako, tena nimrudishe karibu na mwanamke mwingine aliyetulia?” Naya
akamuuliza. “Kuwa mkweli Bale. Ungefurahia mimi nikufanyie kama unachonifanyia
wewe? Ukijua wazi ndio nimeanzana tu na Joshua. Ametulia yule kaka, mstaarabu.
Ananijali kuliko nafsi yake. Eti kila siku anakuja nyumbani anakukuta upo na
Malon! Malon amejaa pale ndani na unajua wazi anajua mahusiano niliyokuwa nayo
na Malon! Ingekuwa wewe nakufanyia hivyo ungefurahia?” “Basi
Naya.” “Hakika basi Bale.” Naya akajifuta
machozi.
“Sijawahi
kukuomba umpende Joshua wala Malon. Ni uchaguzi wako wewe ni nani umemchagua
kuwa rafiki yako. Lakini ningetegemea ungenifikiria hata kidogo! Mimi nakupenda
Bale. Wewe na Zayoni ndio watu wangu wa kwanza kuwafikiria. Hakika mimi
nisingekufanyia unachonifanyia.” “Samahani
Naya.” “Sina shida Bale. Sina shida na chochote chako. Endelea na
maisha yako ila achana na mimi kabisa. Wewe sio mtu mzuri.” “Sasa
unaenda wapi? Baba amesema lazima turudi wote.” “Nitampigia
simu baba, mimi mwenyewe. Achana na mimi, na sitaki kukuona hata unakuwa karibu
yangu. Endelea na maisha yako.” Naya akaondoka, na kumuacha Bale amesimama
nje ya gari ya Malon. “Naomba mfuate Bale. Giza lisimkute peke yake tafadhali.”
“Amekasirika sana. Mwache tu.” “Hapana. Mfuate kwa nyuma, na usimsemeshe.
Halafu ukifika nyumbani ukitulia, naomba unipigie.” “Sawa.” Bale akaondoka
akikimbia.
~~~~~~~~~~~~~~~~
0 Comments:
Post a Comment