Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI&PESA! – SEHEMU YA 26. - Naomi Simulizi

MAPENZI&PESA! – SEHEMU YA 26.

Simu ya Naya ikaanza kuita, moja kwa moja akajua ni Bale. Hata hakuangaika kuitoa kwenye pochi, akaendelea kutembea akilia. Ikaita tena na tena ndipo wazo likamjia kuwa anaweza kuwa Joshua. Akatoa haraka na kupokea baada ya kuona mpigaji ni Joshua. “Vipi Naya wangu? Bado upo kazini?” “Hapana. Leo nimetoka kwa wakati.” Joshua akatulia kidogo. “Mlifika salama?” “Nina kikao kimoja jioni hii, ndipo niende hotelini. Kwa hiyo bado nipo safarini, ila tulishafika nchini. Upo sawa?” “Ndiyo. Nimefurahi kukusikia Joshua. Nimeshaanza kuwa nahamu na wewe!” “Lakini mbona kama husikiki kama upo sawa?” “Nipo sawa tu. Mwenzio nina pesa leo, naenda kujinunulia viatu.” Joshua akacheka kidogo.

“Nimefurahi kama unakwenda kujinunulia vi...” “Hapana. Nanunuliwa na mpenzi wangu Joshua.” Joshua akacheka akisikika amelifurahia hilo. “Ukirudi lazima utanisahau. Naya wa zamani anarudi, lakini huyu atakuwa wa tofauti.” “Siwezi. Wewe nakujua kwa mapigo yangu ya moyo.” Naya akajisikia vizuri sana. “Jamani Joshua!” “Hakika. Hata ukonde sana au unenepe sana. Ukate nywele au uwe nazo nyingi, ukiwepo sehemu, moyo wangu utatambua uwepo wako Naya.” Naya akacheka taratibu akifikiria. “Nakupenda Naya.” Naya akaanza kulia akijifikiria alikopita na kumbe upo upendo mkubwa hivyo! Akaumia kugundua alivumilia maumivu bila sababu.

“Niambie tena.” Joshua akacheka kidogo na kurudia. “Nakupenda sana Naya.” “Na mimi nakupenda Joshua. Rudi tuwe wote.” “Nitarudi mpenzi. Niombee huku mambo yaende vizuri.” “Nakuombea Joshua. Na utafanikiwa sanaaa.” Joshua akacheka. From your mouth to God’s ears.” Naya akacheka taratibu. “Naomba nikuage kwa sasa, nitakupigia nikiwa naelekea hotelini. Na nikikupigia naomba uniambie ni nini kimekuudhi.” “Usiwe na wasiwasi, mimi nipo sawa.” “Sawa, lakini pia nitataka kujua. Kuwa mwangalifu huko madukani.” “Na wewe kuwa mwangalifu ukijua nakusubiria.” “Hilo litaniongezea sababu ya kuendelea kupambana. Nashukuru Naya wangu.” Naya akacheka taratibu akifikiria mazungumzo hayo wanafanya na Joshua akiwa njiani, inamaana Jema anawasikia. Akajisikia vizuri kwamba Joshua hana shida kuzungumza naye mapenzi akiwa na Jema! Hofu ikapungu kabisa. Wakaagana, Naya akasikia kutulia kabisa, mpaka hasira zikaisha.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Bale aliendelea kumfuata Naya kwa nyuma kila anapokwenda. Naya alijua kuwa anamfuata lakini hakutaka hata kumwangalia. Kila alipoingia na yeye alimfuata kwa nyuma. Naya akajinunulia vitu vyake alivyokuwa akitamani bila kuhofia fedha. Akamnunulia na Zayoni, pamoja na baba yao, ndipo akahitimisha manunuzi yake kwa siku hiyo. Akampigia simu baba yake kutaka kujua alipo. Akamwambia atakua akimsubiria kituoni, nyumbani kwao. Akalifurahia hilo. Akapanda daladala, na Bale naye akapanda daladala hiyohiyo kurudi kwao bila ya kumuongelesha Naya mpaka kituoni nyumbani kwao Kiluvya.

Walimkuta baba yao kituoni. Akampokea Naya mizigo mpaka nyumbani bila kumsemesha Bale, ila kuzungumza wao wawili. “Mfuko huo wako na huu wa Zayoni.” “Mbona manunuzi makubwa na mwisho wa mwezi bado, mama! Tutafika kweli?” “Joshua amenipa pesa kabla hajaondoka. Nikaenda kujinunulia vitu nilivyokuwa nikitamani ila kuhofia pesa.” Baba yake akafungua ule mfuko. “Asante Naya. Na mimi umeninunulia nguo za matajiri?” “Sio zote. Shati moja tu la kanisani ndio la pesa nyingi. Vingine nimenunua kwenye maduka ya kawaida. Lasivyo tungeishiwa.” “Lakini pia nakushukuru Naya. Asante.” “Na mimi?” Bale alikuwa kama amepuuzwa na wote. Kimya.

“Zawadi ya Bale iko wapi?” Akauliza Zayon. “Ndio nani?” Naya akauliza huku akimsaidia baba yake kutoa zawadi zake. “Zawadi za Bale?” “Kama huna taarifa, huyo sio ndugu yangu tena. Na sitaki uje unitajie jina lake tena, lasivyo na wewe utakuwa sio ndugu yangu. Nitakuwa sikuletei zawadi.” Zayoni akajua safari hii sio utani. “Kwani amefanya nini?” “Anataka kuniuza kwa Malon, ili Malon ampende awe anampa pesa.” “Naya! Unanitukana.” “Huo ndio ukweli Bale. Na wewe ni mtu mbaya sana. Hakika sitaki kukusikia.” “Nilitaka kukusaidia Naya.” “Muongo mkubwa wewe. Unanisaidia mimi au wewe mwenyewe?” “Na mimi nilimuuliza hivyohivyo. Na ninakuonya Bale. Haraka hizo za maisha na kushindwa kuweka utu mbele, zitakuponza!” Baba yake akaingilia.

“Baba! Nataka kusaidia. Unafikiri mimi ndio napenda kwenda maporini?” “Nakuuliza swali kama analokuuliza Naya. Unayetaka kumsaidia hapa ni nani mwenye shida? Nani ameomba msaada wako?” “Sio lazima niombwe baba! Nimeona uhitaji ndio na mimi nimeona naweza kufanya kitu ili kubadilisha maisha ya hapa.” “Kwa hiyo unataka maisha kama ya Malon?” Baba yake akamuuliza. “Kwamba umemuona amefanikiwa sana, ndio unataka kuambatana naye, uwe kama yeye?” “Kwa upande wa biashara ni kweli Malon amefanikiwa baba. Hata wewe ulimsifia. Siku chache nimekuwa naye, amenionyesha alipo, yule mtu amefanikiwa baba! Na hana roho mbaya. Ameniahidi kunisaidia mpaka nisimame.” “Sawa Bale. Ila nakuonywa. Kuwa mwangalifu. Usije kusimama alipo Malon.” “Kwani kuna tatizo gani kusimama alipo!?” Bale akawa hajaelewa.

“Mwache baba. Ila naomba umuonye asiwe ananiingiza mimi kwenye harakati zake zakujigeuza kuwa kama Malon. Na mkumbushe tu, baada ya yote hayo anaweza kujikuta na pesa, lakini peke yake.” Bale akacheka kidogo. “Nikifanikiwa mimi, ujue na nyinyi mmefanikiwa.” “Mimi sina shida Bale. Tafadhali katika hangaika zako usinihesabu mimi. Na katika heshima niliyojipatia kwa Malon, nikumuonyesha wakati wote mimi namuheshimu na kumpenda yeye kama Malon na wala si mali zake kama wewe ambaye upo radhi unione nateseka, ilimradi niwe naye ili unufaike.” “Sijasema hivyo Naya!” “Lakini ndivyo unavyofanya. Unaonyesha mpaka kwa vitendo kuwa moyo wako wote unamtaka tu Malon, na kufungia moyo watu wengine wote.”

“Unamaanisha Joshua?” “Ndiyo Joshua. Sijawahi hata kukuomba umpende, lakini unaonyesha kabisa umemfungia moyo wako, na umekataa hata kujaribu kumfahamu japokuwa anaonekana ananipenda mimi.” Naya akawa mkali kabisa. “Macho yako na moyo wako vyote vipo kwenye pesa ya Malon na kukutoa utu. Na upo huru kuniona nateseka ili ufikie pesa ya Malon!” “Sio kweli Naya. Mimi nakujali, sitaki uumizwe tena. Naona ni heri Malon ambaye tunamfahamu, na kama ameahidi kubadilika, inamaana nirahisi kuwa na Malon kuliko Joshua. Kumbuka zimwi likujualo, halikuli likakwisha.” Baba yake akashangaa sana.

“Subiri kwanza baba. Wewe unamfahamu Malon kwa kumuona amekaa na wewe hapa na mnakutana naye kwa sekunde chache! Mimi namfahamu Malon kwa kuishi naye. Ana mwanzo, mwisho hana. Na...” “Subiri kwanza Naya. Yaani wewe Bale ndio umegeuka kuwa mwamuzi wa mwisho wa maisha ya mwenzio!” “Mimi namsaidia baba. Asijekuwa anafungwa macho na vitu fulanifulani na kumsahau Malon ambaye amekuwa naye tokea zamani. Naya mwenyewe alisema Malon amemsaidia mambo mengi sana. Anawezaje kumtelekeza Malon aliyejishusha na kuahidi mabadiliko kwa ajili ya mwanaume aliyekuja juzi tu?” Bale akamuuliza dada yake akimshangaa kabisa.

“Sisi tutakuwa watu wa namna gani ambao tunajua kujinufaisha tu na watu, tukifanikiwa, tunawaacha na kuanza na wengine?” “Haa! Ndivyo unavyofikiria kinachotokea kati yangu na Malon? Ndivyo alivyokudanganya?” “Mahusiano yanakuwa na changamoto Naya. Sio kukimbia.” Bale akawa na msimamo na yeye. “Kama wakati wote ulikuwa ukimsamehe Malon. Kinachokushinda kumsamehe sasa hivi ni nini kama si Joshua tu?” Naya akamshangaa sana.

“Kweli kabisa Naya. Na nakushauri ujiulize. Ukishindwa na kwa Joshua, unakimbilia wapi?” “Kwa hiyo wewe ulitaka niendelee kumvumilia Malon mpaka lini!?” Naya akamuuliza akiwa na mshangao mkubwa sana. “Ameokoka. Ungempa tena nafasi! Watu wanabadilika Naya.” “Nimekuwa na Malon huyuhuyu unayemtetea wewe akiwa ameokoka na akiwa hajaokoka! Sijaona mabadiliko yeyote yale! Maswala ya Rita si yametokea akiwa ameokoka?” “Naelewa Naya. Lakini ukumbuke Malon hajalelewa kama sisi. Hana maadili kama yetu. Kwa yeye kutaka kuwa karibu na sisi, ilitakiwa tumsaidie na kumuelekeza njia iliyo sahihi sio kumtupa mbali kipindi ambacho wote sisi kama wakristo tunajua kuna kukua kwenye wokovu!” Bale akawabadilikia.

“Nyinyi mlitegemea nini kwa mtu kama Malon ambaye alikuwa mtaani muda wote akisumbuliwa na mapepo! Hajawahi kufundishwa na yeyote yule. Nani amfundishe kama sisi tukimsukumilia mbali?” Naya alishangaa sana. “Kumbe ndio maana umemng’ang’ania hivyo!?” “Sisi si ni wakristo? Kwa nini tunashindwa kuishi ukristo? Tunashindwa kusamehe!? Bibilia imeandika tunatakiwa kusamehe 70 mara 7.” “Baba, naomba mimi nikaoge, nasubiria simu ya Joshua.” “Sawa Bale. Lakini nakuonya uwe mwangalifu. Angalia usije ukaanguka vibaya sana.” Baba yake akamtahadharisha. “Mimi sifanyi kitu kinyume na bibilia inavyoagiza. Malon alikuwa akitujali sana humu ndani. Kwa haja zetu binafsi! Leo tunamtupa! Sidhani kama ni sawa. Najua mnaweza mkanichukia, lakini huo ndio ukristo.” Naya akaondoka bila ya kumjibu.  

“Kwani baba amemfukuza Malon tena?” Wakamsikia Zayon akimuuliza Bale. “Aaah! Hajamfukuza ila naona si sawa.” “Labda hujaelewa Bale. Baba hajamfukuza Malon. Hata juzi yeye ndiye aliyemkaribisha ndani na kumwambia asikae nje peke yake, aingie ndani. Maana mimi ndiye niliyemfungulia geti. Alipojua wewe na Naya hampo akasema atakaa tu nje, ndio baba akatoka kuzungumza naye, akamkaribisha mpaka ndani. Akaja kukaa hapa akampa mpaka chai na chakula kidogo, kilichokuwa kimebaki. Akakaa hapa mpaka wewe ulipokuja ndio baadaye akaja Naya na Joshua. Baba hajamkataa Malon, ila Naya hataki kumrudia kama mpenzi wake. Unakumbuka alipokuwa anaumwa hakwenda kazini, Naya mwenyewe alikwambia wewe uendelee tu na Malon, ila yeye ndio hataki kujihusisha naye?” “Sasa si kwa sababu ya Joshua!” “Wewe Bale humtaki Joshua?” Wakamsikia Zayon akimuuliza taratibu tu, ila hakujibiwa. Bale akatoka hapo ndani kabisa. Akabakia Zayoni asiyependa ugomvi peke yake hapo sebuleni. Kimya.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Pakawa kimya jioni hiyo. Hakuna aliyezungumza na mwenzie. Hapakuwa na Joshua wala Malon usiku huo ila ndugu hao tu, ila Bale akijisikia mshindi kuwa amewashinda familia yake kwa hoja za kiMungu. Amewapa ukweli mtupu uliowafunga midomo. Baba yao hakuzungumza naye kabisa, akabaki Bale akijindaa kwa safari ya kesho yake. Aliingia na kutoka chumbani kwake na miluzi. Akiazima hiki na kile kutoka kwa baba yake vile alivyotumia akiwa Mbeya na Malon. Baba yake alimpa bila tatizo, mwishoe akamtolea mpaka begi. “Hapo umenisaidia zaidi.” Akaongeza Bale akiwa amejawa furaha, kama kazawadiwa benki nzima na huyo Malon. Naya alibaki chumbani kwake akiendele kujifunza laptop yake mpya aliyonunuliwa. 

Joshua Tena.

Joshua akampigia. “Pole mpenzi wangu.” Joshua akacheka kidogo. “Asante. Ila namshukuru Mungu mambo yamekwenda vizuri. Na nakushukuru na wewe kwa maombi.” “Nimefurahi kama umefanikiwa. Ndio unarudi hotelini?” “Ndio narudi. Njaa inauma! Na kesho nina vikao nahitaji kujiandaa. Hapa natamani kuiona sura yako tu.” “Pole ila ukifika hotelini kula kwanza.” “Na kuiona sura yako?” Naya akacheka. “Ukirudi utaniona. Ujue nakusubiri.” Wakaendelea kuzungumza wapenzi hao wawili taratibu wakibembelezana.

“Ni nini kilikuudhi?” “Husahau tu! Nilivyojitahidi kuchangamka hivyo!” “Niambie?” “Hamna kitu, usijali. Utakwenda kula nini?” “Huwezi kunitoa kwenye hilo swali Naya. Nimekuwa nikilifikiria. Nani amekuudhi? Ni kazini?” “Hapana Joshua. Nipo sawa.” “Sasa hivi upo sawa. Lakini nataka kujua wakati ule ni nini kilikuudhi?” “Naomba nisikwambie Joshua!” “Ni nini hicho ambacho ni kikubwa hivyo kiasi  cha kunificha?!” “Naomba wewe uangalie mambo ya huko, mimi huku.” “Hapana Naya. Huko nikunifanya nijisikie dhaifu sana na unanipokonya wajibu wangu. Nawajibika kwako kwanza ndipo mengine. Nikishindwa kuwajibika kwako, Mungu hawezi kuniamini na mengine. Tafadhali niambie ili wakati wangu huku usiwe mgumu. Au ni mambo yanayohusiana na Malon?” Naya akatulia.

“Alikufuata tena kazini?” Joshua akaendelea kuuliza. “Naya?” “Naomba tuzungumze ukirudi Joshua, japo hakuna lakuzungumza. Kila kitu sasa hivi kipo sawa.” Joshua akanyamaza. “Joshua?” Naya akaita. “Joshua?” Akaita tena taratibu, Naya akaangalia simu yake akakuta bado haijakatwa. “Nipo. Ila kama huoni umuhimu wa kunishirikisha, basi.” “Naona sio kitu cha msingi.” “Kwa nini mimi nisiwe msemaji juu ya hilo? Kitu kinachokuudhi wewe kwa nini kwangu kisiwe cha msingi?” “Nilikasirika kwa sababu si kwa Malon kuja, ila Bale kuja naye. Ndicho kilichoniudhi Joshua. Bale anaamini namkimbia Malon wakati sasa hivi ndipo anaponihitaji kama mimi nilivyomuhitaji wakati nina shida.” “Lakini yeye ndiye aliyekukataa!” “Asante Joshua.” Hapo Naya akaona ameeleweka.

“Nashukuru kwa kulikumbuka hilo, maana inaonekana ni kama namkimbia sasa hivi kwa ajili yako, wakati wewe ulinikuta ameniacha! Lakini Bale anaona ni kama namtelekeza sasa hivi wakati ndio ameamua kumpa Yesu maisha! Kwamba ndio kipindi kizuri tunatakiwa kuwa naye karibu na kumuelekeza njia iliyo sahihi! Analalamika na kuona ni kama tunamtupa wakati anatuhitaji.” “Malon ndio amesema anawahitaji?” “Joshua, mimi namfahamu Malon kwa kuishi naye wala si kusimuliwa. Ana mwanzo mzuri sana ambao sasa hivi ndiko aliko na Bale. Malon si mtu wa mahusiano jamani! Anajua kujaa kwenye maisha ya mtu mpaka anakulevya kabisa kisha anakuacha. Na ukiwa naye, anakuonyesha vile ulivyo muhimu kwake mpaka akikufanyia jambo unashindwa kumuacha unabaki kumsubiria Malon unayedhani atakuja kuwepo, kumbe hajawahi kuwepo.” Naya akaendelea.

“Mimi nilikuwa hapo alipo Bale sasa hivi. Nilitaka kumkasirikia sana leo na nilishamtamkia maneno mabaya sana, lakini kadiri nilivyozungumza naye, na hoja alizokuwa akizitoa, hakika amenikumbusha Naya wa wakati ule, nikaona si sawa kumkasirikia Bale kwa kuwa mimi nilikuwa kwenye hicho kifungo kwa miaka mingi sana. Sikuwa nikiambilika ila kutoa nafasi zaidi na zaidi mpaka nilipoishiwa kabisa. Lakini katika yote, nilikuwa na pakurudia. Baba. Baba alikuwa kimbilio langu. Nikilemewa huko, nilikuwa nikirudi kulia kwake na ananiombea. Nikajiambia kumkasirikia Bale, nitakuja kumuumiza zaidi pindi atakapogeukwa na Malon, maana naye hana muda mrefu.” “Na Zayoni naye anasemaje?” Joshua akauliza.

“Zayoni hapendi kumuumiza mtu na hapendi ugomvi kama mimi na Bale. Akishaona mtu amekasirika, anakata kauli kabisa. Anashindwa kuzungumza. Yeye yupo kama baba.” “Kwa hiyo baba anajua?” “Anajua! Kama kawaida yetu tulianza kugombana ndio baba akatusikia. Amekasirika sana na kumuonya asijewahi kurudia kuniuza kwa wanaume. Bale anatulaumu mimi na baba kuwa hatuishi ukristo. Hatutaki kumsaidia Malon akue kwenye ukristo.” Joshua akavuta pumzi kwa nguvu.

“Lakini ukimsikiliza Bale ni kama anaongea ukweli.” Joshua akaongeza taratibu kama anayefikiria. “Ukweli mzuri sana na unasikika kiutakatifu kabisa, lakini si kwa Malon, Joshua. Mimi nisingekuwa mtu wakumtupa Malon kipindi cha shida yake. Malon hayupo hapa sababu anashida. Hata kidogo. Amerudi kama kawaida yake anavyoanza jambo. Kurudi, akikuta kuna hitaji basi anaanzisha jambo kwa nguvu kama hivi kwa Bale. Alirudi kwa kuwa nilimpigia swala la ugonjwa, nikamuomba jina la dawa, akarudi ndio akakutana na Bale. Amejaa hapa nyumbani kama siku nyingine zozote anavyokuaga anarudi. Na pia Zayoni amemkumbusha Bale kuwa Malon hajafukuzwa hapa ndani. Baba alimkaribisha mpaka ndani kabisa, sisi tukiwa hatupo na alimpa chakula na chai.  Hajafukuzwa humu ndani. Lakini ndio hakuna maswala ya mahusiano kati yetu.” Naya akaendelea.

“Malon hana shida yakusaidiwa kiroho. Alirudi kwa ajili yangu akiwa na uhakika hata safari hii nimepata mwanaume wa ajabu kama siku zote ili aanzishe jambo kama kawaida yake. Sasa amekuta safari hii nimetulia na wewe, halafu unajielewa. Mtu wa mipango na mimi sina mpango wa kumrudia tena wala kuanzisha michezo yake, ndipo Bale anaona tumembadilikia Malon kwa kuwa anaona safari hii hatuchezi naye michezo yake anayopendaga kucheza wakati wote.” “Unamaanisha kurudiana na baba kukuunga mkono?” Joshua akauliza.

“Si hivyo tu. Maana nikwambie ukweli tu Joshua. Baba hajanikataza nisirudiane na Malon ila kunitaka kumuelewa na kuamua kwa hakika. Hata ningesema nimeamua kumrudia leo Malon, wala baba asingenikatalia kwa sababu hataki kuwa kwenye nafasi ya kunichagulia kama vile mama. Maana alishaniambia ndoa ni lazima niwe nimeamua kwa hakika kwa sababu sio yakuingia na kutoka.” “Ambayo ni kweli.” Joshua akaunga mkono.

 “Ndicho sasa ninachokwambia nilichoka kucheza michezo ya Malon. Anaogopa kujifunga kwenye mahusiano yeyote yale, zaidi yakiwa yakaribu sana. Hajui na hataki, hata baba yake anamjua. Akishaanzisha jambo. Akaona linampelekea kwenye kujifunga kwenye hayo mahusiano, sijui anaingiwa hofu au anajiona hayupo tayari, anajitoa kwa sababu yeyote ile anayochagua yeye kwa wakati huo. Waliokuwa wanaweza kumvumilia, tena sio kumvumilia ila kumtumia wakimfuata nyuma kila wakati bila kuchoka hata Malon akiwa analala na wanawake zao ni wale waliojifanya ni rafiki kwake ili kujinufaisha naye, kwa kuwa ni kweli Malo ni mtoaji haswa. Si mchoyo kabisa.” Joshua kimya akisikiliza sifa za Malon tena.

“Ukifanikiwa kukaa naye meza moja, kama anayo pesa, ujue na wewe hutalala njaa. Hata Chezo hilo alikuwa akilisema. Kwa mapungufu yake yote, Malon ni mtoaji sana. Kwa hiyo hata waliokuwa karibu naye wakawa wanalazimishia mahusiano, na yeye alijua wazi wanamtumia, lakini aliendelea nao ili tu kuwathibitishia kuwa, japokuwa wao hawakukimbia shule kama yeye, lakini amewapita. Akaishi maisha ya kuwatawala japo hana shule kama wao, hiyo ikamuongezea kiburi. Haamini kama anacho kitu cha kutoa kwa mtu ila pesa. Ndio maana akiishiwa tu, anakimbia watu. Sasa hebu niambie Joshua, maisha yenyewe ndio haya, mambo yanakubadilika, maisha hayajawahi kuleta uhakika kwa yeyote ila imani tu. Unaweza kuwa nazo leo kesho huna. Sasa hapo ndio amekuachia pete mkononi, biashara zikayumba, anakimbia tena. Unabaki na pete kidoleni, umsubirie afanikiwe, umtafute. Umbembeleze. Kama ukimkuta alifanikiwa na na ameanzisha mahusiano mengine, ndio usubiri atafute sababu ya kuachana na huyo mtu, umfuate tena, ndipo akurudie tena. Ndio hiyo michezo mimi nimekataa kucheza, Joshua. Malon si mtu wa kujifunga kwenye mahusiano. Ingekuwa kutaka kwake, sasa hivi tungekuwa na yule mtoto wa pili niliyekwambia. Kwamba angeshakuwa amenioa muda mrefu tu na tulishaanzisha familia. Lakini haikuwahi kutokea, si mtu wa mahusiano. Hataki kujifunga kabisa, kila siku sisi tunaanza!” Joshua akatulia akisikiliza.

“Ndio maana nakwambia hata kwa Bale, nimejutia sana kumsemea maneno mabaya.” “Ulimwambia nini?” Naya akatulia kidogo. “Naya?” “Nilihisi hajali hisia zangu. Hafikirii vile nilivyokuwa kipindi nipo na Malon, na utulivu nilio nao sasahivi nikiwa na wewe! Nikamlaumu kwa mengi na kumkasirikia ni kwa nini hajakupa wewe nafasi, anamng’ang’ania tu Malon!” “Mimi naungana na wewe Naya. Mwache kabisa, na wala usimuonyeshe hasira. Ni bora yakamshinde mwenyewe, kuliko wewe umkatalie, halafu aje akulaumu baadaye. Nimemsikia jinsi alivyo na matumaini makubwa na Malon. Nashauri muunge mkono kabisa.” “Kivipi?” Naya akauliza. “Tafuta kutengeneza naye kabla hajaondoka ili apate pakurudia.” Naya akatulia kidogo kama ambaye hataki kwenda umbali huo.

“Unanisikia Naya?” “Nakusikiliza Joshua.” “Tena ikiwezekana mpe hata pesa za kujikimu, asiondoke akiwa hana pesa na mkiwa hamjapata. Unaweza ukakuta wewe ndiye ulishindwana na Malon, lakini si yeye. Pengine yeye atafanikiwa, hutaki muharibu mahusiano. Sijui kama unanielewa?” “Nakuelewa Joshua.” Naya akaitika taratibu. “Lengo ni kutengeneza na wala si kuharibu. Tunataka Bale afanikiwe sana. Basi muunge mkono. Mengine yaache yatajiweka sawa yenyewe. Sawa?” “Nashukuru kwa ushauri. Nakupenda Joshua. Nakupenda wewe kama Joshua sio sababu nataka kukutumia.” “Mimi sioni hivyo Naya. Mimi najua ukweli. Na ninakupenda sana. Najua yote hayo yanatoka katika sehemu ya upendo tu. Bale anakupenda, anataka uishie pazuri.” “Nashukuru. Basi acha nikazungumze na baba kisha na Bale, halafu nitakupigia. Kumbe ni afadhali nimekwambia umeweza kunishauri vizuri!” Naya akawa anacheka. “Usiwe unanificha mambo! Tuzungumze tu.” “Sasa hivi nitakuwa sikufichi tena. Nikupigie saa ngapi?” “Sasa hivi nipo huru mpaka nikiwa nalala. Muda na wakati wowote unipigie. Ukiona sijapokea ujue naoga, nitarudisha simu yako nikitoka kuoga.” “Sawa.” Naya akakata na kurudi kwa baba yake.

Kwa Baba Naya.

Alimkuta amekaa sebuleni ametulia. “Naomba tukazungumze hapo nje, baba.” Baba yake akatoka naye. Wakaenda kukaa sehemu ambayo kulikuwa na mabanda ya ng’ombe. “Unakumbuka nilipokuwa na Malon, wewe ulikuwa upande wangu? Vipindi vya vilio vyangu, ukinibembeleza, kuniombea na kunisubiria nilale?” Baba yake akamwangalia tu. “Kipindi kile ungeniambia niachane na Malon, pengine nisingeelewa?” “Uliniambia hutajali hata kama utakuwa ukifanya kazi na pesa yote unayolipwa uwe unaitumia tu kumtoa yeye jela!” Naya akacheka na kuinama. Akafikiria kidogo na kuendelea.

“Pale baba ilikuwa mwishoni mwishoni, lakini tokea tunaanzana na Malon, haikuwahi kuwa rahisi. Ukiniuliza ni kwa nini niliendelea kuwa naye kwa miaka yote hiyo, nafikiri na mimi ni miongoni mwa wale waliokuwa wakisubiria kubahatika kwa Malon. Nikidhani pengine mimi ndiye nitaweza kufanikiwa kuwa wa Malon. Ninachotaka kusema ni hivi, nilianza kugombana na Bale tokea hatujafika hapa. Nikataka kumkasirikia sana. Lakini baba, alipo Bale kwa Malon, mimi nimekuwa naye kwa zaidi ya miaka 5. Hivyohivyo nikimtetea kwa watu wengi tu, kama hivyo Bale, na wewe nishahidi jinsi nilivyokuwa nikimtetea mpaka kumtafutia mwanasheria kwa pesa nyingi tu. Ana jinsi fulani yakumpumbaza mtu, unashindwa kujitoa kwake mpaka Mungu aingilie kati. Naomba tumuelewe Bale, na naomba mimi niwe kama wewe ulivyokuwa kwangu. Nimsubirie pale atakapohitaji msaada, niwepo kumsaidia. Na mimi namjua Malon, hana muda mrefu, atamgeuka tu Bale. Sitaki Bale apotee kwa muda mrefu kama mimi.” Baba yake akawa amemuelewa.

“Sawa.” “Nakushukuru kwa uelewa.” “Umenishangaza!” Naya akacheka. “Nikwambie ukweli?” “Niambie.” “Njiani niligombana sana na Bale pamoja na Malon. Joshua alipiga, akanikuta nalia huku nikienda madukani. Leo amenipa pesa nyingi sana. Sasa nikakataa kumwambia ni kwa nini nalia, muda huu aliponipigia, akataka kujua. Akaweka msisitizo mpaka nikamuona ameumia akidhani namficha kwa ubaya. Nilipomsimulia na kumwambia najilaumu kwa kumchukia Bale, na yeye akaniunga mkono. Amesema tumuunge mkono tu. Tusimtenge, wala kumkasirikia kwa kuwa nia yake si mbaya. Ameniomba hata nimpe pesa ya kujikimu na kumuwekea mazingira ya kuwa chochote kikiwa kibaya huko, awe huru kurudi kwetu, hatutamuhukumu. Kwa kuwa hatuna nia ya kubomoa chochote ila kujenga. Tena amesema inaweza ikawa ilikuwa ngumu kwangu kwa Malon, lakini ikawa rahisi kwa Bale. Na Bale akafanikiwa sana. Kwa hiyo tusimvunje moyo.” Baba Naya akashangaa sana ila akanyamaza kama kawaida yake. “Acha nikazungumze naye kabla hajaondoka kesho.” “Sawa.” Naya akarudi ndani na kumuacha baba yake hapo nje. 

Naya Kwa Bale.

Akamkuta Bale chumbani kwao. “Bale!” Bale akamwangalia. “Naomba tusigombane kwa ajili ya Malon. Najua wote tunampenda Malon na hatutaki kumuumiza. Upo sahihi. Malon alitusaidia sana. Inawezekana kwenye swala la mapenzi ilikuwa ngumu, au hakuwa tayari, lakini akawa mzuri kwenye mahusiano mengine.” Bale akawa kama haamini. “Unisamehe kwa maneno ya ukali niliyokuwa nimekwambia. Sitaki tugombane. Mimi bado ni dada yako.” Bale akacheka. “Mimi ni dada yako tu.” “Sawa Naya. Nikifanikiwa utafurahi. Nachukia hii hali hapa ndani! Kama kuna jinsi yakufanya, kwa nini nisifanye?” “Nimezungumza na baba, nafikiri na yeye amekubaliana na hilo. Nia yako nzuri. Nakuombea ufanikiwe.” Bale akafurahi sana asijue dada yake anampa ruhusa ya kwenda kujaribu akishindwa apate pakurudia.

“Asante Naya. Na tukiwa pamoja hivi, nitafanikiwa tu. Ila ujue nia si kutaka kukuuza.” Naya akacheka na kukaa. “Acha nikusaidie kufungasha.” Wakaanza stori, ndipo Zayon akaingia na yeye nakuanza kufurahia vitu vipya alivyonunuliwa na Naya. Watatu hao wakacheka na kutaniana. Naya akampa pesa Bale. “Ukiwa na uhitaji usiache kuniambia.” “Nakushukuru sana Naya.” Wakapata wakati mzuri sana usiku huo, na wakaomba kwa pamoja na baba yao. Kila mtu akarudi chumbani kwake kupumzika. 

Jumamosi Ya Safari Ya Bale Na Malon.

Kama kawaida yake Naya aliondoka asubuhi na mapema kuwahi ofisini akisindikizwa na baba yake kituoni. Alimwambia siku hiyo japokuwa anawahi kutoka, lakini atakwenda kutengenezwa nywele. Alishanunua vazi la jumapili kanisani, Naya akawa na hamu ya kuweka nywele mpya. Akajiwekea mikakatati ya siku hiyo. Akiwa kituoni na baba yake, Joshua akampigia simu. “Joshua! Mbona mapema sana?” “Nakusindikiza kazini.” Naya akacheka kwa furaha. “Usingehangaika! Nipo na baba kituoni amenisindikiza.” “Basi mimi nitakusindikiza mpaka kazini.” “Jamani Joshua wangu! Usingehangaika bwana! Ungelala tu.” Baba Naya akawa anawasikiliza tu, kimya akisubiria binti yake apate gari, aondoke ndipo na yeye arudi nyumbani. “Nililala salama, na wewe?” Akamsikia Naya akimuuliza. Gari ikaja, Naya akamuaga baba yake na kumshukuru, daladala ilipoondoka, ndipo baba Naya naye akaondoka.

          Siku hiyo ikawa imejaa furaha kwa Naya. Amepatana na Bale, na Joshua yupo upande wake. Pesa anayo, hana shida. Akaletewa nywele nzuri sana pamoja na hereni na urembo mwingineo. Naya akalipa pesa yote bila kubabaika. Na kweli mpishi wa Joshua naye akamletea chapati kama alivyomuahidi pamoja na mboga. Akampigia simu baba yake kuwa Zayoni aende kufuata chakula ofisini kwao kwa kuwa yeye atapitia saluni kabla ya kurudi nyumbani.

“Lakini na Bale bado yupo.” Naya akashangaa sana. “Si alisema walipanga waondoke saa 12 asubuhi? Malon amebadilisha muda?” Naya akauliza na wasiwasi kidogo. “Nilivyoambiwa na Zayoni ni kwamba hakuwa akimpata tena kwa simu.” Naya akaumia sana. “Sasa yuko wapi?” “Zayoni ameniambia amekwenda kumwangalia nyumbani kwake.” Wakatulia kidogo. “Nitamtuma Zayoni. Naona nimuache tu Bale.” “Asante baba.” Naya akakata simu.

~~~~~~~~~~~~~~~~

          Ilipofika mida ya saa 11 na nusu jioni Naya ndio akawa anaingia nyumbani kwao. “Mbona hukunipigia nikufuate?” “Nilijua ungenipotea tu.” Naya akaongea kwa kujisifu, baba yake akacheka akimwangalia. “Umependeza mama! Umependeza sana.” “Si ungenipotea?” “Uzuri huo, naujua.” Naya akacheka sana. “Enzi zinarudi baba yangu. Bale yuko wapi?” “Hajarudi mpaka sasa.” “Mizigo yake?” “Ipo hapo nyuma ya kochi. Alikuwa amekaa hapa kwenye kochi asubuhi nzima. Mimi nilitoka mida ya saa nne, nilimuacha amekaa hapo na Zayoni.” Naya akaumia sana. “Mmependa chakula?” “Nimemsikia Zayoni akila bila kumaliza.” Naya akacheka. “Na wewe?” “Mimi nitakula usiku.” Akajua baba yake alikuwa amefunga.

“Basi acha nikutengenezee chai. Nimekuletea na sendozi zakuvaa kwenye shughuli zako.” “Utaishiwa Naya, mama yangu!” “Wala si gharama. Acha nikapike chai.” Naya akaelekea jikoni na kuandaa chai ya nyumba nzima ili kula na hizo chapati. Akandaa meza kabisa.

          Kwenye mida ya saa moja kasoro Bale akawa anaingia, macho mekundu haswa. “Pole na mihangaiko Bale.” Naya akamuwahi. “Asante. Njaa inauma kweli!” “Kuna chapati na mchuzi.” “Wewe ndio umepika?” “Nimeletewa kazini na mpishi wake Joshua. Ila chai napika.” “Ningeshangaa jinsi ulivyopendeza na mapishi ya chapati ungeyafanya saa ngapi!” “Baba alikuwa anaomba ili aje tule. Unaweza kuanza kula kama umezidiwa.” “Acha nisubirie.” Akakaa sehemu ya kulia chakula, Naya akamuona jinsi alivyonyongea. Akajua tayari ameshatendwa. Hakutaka kumuuliza. Akaona amuache tu. Walikula kwa pamoja, Bale hakuzungumzia chochote ila wakamuona anarudisha begi lake ndani kimyakimya. Naya akarudi chumbani kuzungumza na Joshua, kila mtu akaenda kulala. 

Jumapili.

Kwa kuwa walikuwa na kitafunwa tayari, Bale hakupata shida kuandaa kifungua kinywa asubuhi hiyo. Wakamuona Naya anatoka kwa haraka, wakashangaa kuona anafungua geti, gari ya Joshua inaingia ndani. Wakajua Joshua amerudi nchini, kumbe dereva aliagizwa alate hilo gari na kurudi kulichukua atakapoambiwa na Naya. Naya alijawa furaha kutumia gari ya fahari siku hiyo! Akarudi ndani na kuwaeleza ndugu zake. “Itakuja kuchukuliwa usiku. Joshua anataka tuwe na usafiri wa kanisani na wakutupeleka sehemu tukapate chakula cha mchana pamoja.” “Joshua anakupenda, Naya!” Zayoni akaongea kwa kumaanisha. “Sana mpaka huwa namuhurumia.” Naya akaanza kushangilia. “Leo tunaingia kanisani na usafiri wa maana, na nataka tupendeze.” Naya akawa amepata moyo wa kwenda kanisani, si kwa ajili ya Mungu, bali kujionyesha.

          Na kweli alitoka amependeza haswa. Baba yake hivyohivyo. Alivaa mpaka saa aliyonunuliwa na Naya. Nguo nzuri za maana tupu, Naya mwenyewe alifurahi. Waliingia kanisani, ukweli watu waliwashangaa. Kama sio wao! Zayoni na mwenyewe alikwenda kunyolewa nywele siku iliyopita, akawa amependeza. Ila Bale alikuwa amenyongea sana. Walikwenda sehemu ya kula baada ya ibada, wakakaa wanne hao na kuagiza kila mmoja anachotaka. Hapakuwa na mazungumzo mengi sababu ya Bale kuwa kimya sana, walikula na kuamua kurudi nyumbani ndipo njiani Naya akampigia simu Joshua kumshukuru kwa siku nzuri na kumwambia dereva anaweza kwenda kufuata gari.

          Wakiwa wamekaa tu hapo sebuleni, Bale akaingia chumbani kwake akatoka na vitu vyote alivyoazima vya baba yake. “Naona sitavihitaji tena. Malon alishaondoka kwenda Mbeya, na simpati kwa simu.” “Weka tu hapo kitandani kwangu.” Baba yake akajibu hivyo tu kwa ufupi, ila kwa kuumia. Naya naye aliumia sana. “Inamaana ameondoka bila kumuaga!” Akaumia sana Naya, na kurudi chumbani kwake. Akajisikia machozi kumtoka, asijue baba yao ndio analia zaidi ndani ya nafsi yake akiwahurumia wanae jinsi wanavyohangaika.

~~~~~~~~~~~~~~~~

          Zikapita siku mbili Bale akiwa ametulia tu hapo ndani kama aliyekosa dira. Akawa ameishiwa morali kabisa. Naya akatoka kazini siku hiyo ya jumanne akamfuata jikoni. “Bale, ungependa nizungumze na Joshua kama anaweza kukusaidia kupata kazi hata pale kazini kwetu?” “Kwa cheti gani Naya!? Nimeishiwa nguvu kwa kuwa niliweka tumaini kubwa sana kwa Malon! Ingekuwa ni rahisi kufanya kazi kwake na kutengeneza pesa kwa haraka bila maswala yakuingiza elimu. Hata kama ningesema nitumie matokeo ya nyuma, wewe unajua mimi sio kipanga, Naya. Sina matokeo ya nyuma yakutisha. Napatiwa kazi wapi, na nani na kwa sifa gani?” “Acha Joshua arudi tuone. Anasikilizwa sana pale kazini. Wamiliki wa ile kampuni wote wanamuheshimu sana. Na hata kama sio pale, basi anaweza kutusaidia kwengine. Unakumbuka kule tulipokwenda kuendesha boti?” Naya akamuuliza taratibu tu.

          “Nakumbuka.” “Ni club ya watu wenye pesa zao na wasomi watupu wenye vyeo vinavyolingana na yeye. Hawezi kukosa mtu wa kukuunganisha naye.” “Naogopa hata kuweka matumani Naya! Malon amenigeuka vibaya sana. Sasa hivi naona simu zinaingia ila hataki kupokea!” “Mungu atatusaidia Bale. Tupambane bila kukata tamaa. Ipo siku na sisi naamini tutafanikiwa tu.” Bale akanyamaza, Naya akajua bado anauchungu na Malon.

Mapenzi!

Siku ya jumatano karibu na siku ya kazi kuisha, akiwa amejiinamia mezani kwake kama kawaida, akahisi ukimya wa ghafla kwamba hakuna hata stori zilizokuwa zikiendelea wakati wenzake walikuwa wakizungumza na kucheka bila yeye kuchangia chochote. Naya akashangaa ule ukimya, akageuka. Alishituka sana kumkuta Joshua amesimama kwenye sehemu yakuingilia hapo ameegemea. “Joshua!” Naya akashangaa sana, hakutegemea.

Balada amfuate, akajikuta anainama na kulia. Watu wote wakashangaa. Joshua akamsogelea na kwenda kuinama pale alipokuwa ameinamia meza akilia. “Mimi nilitegemea unikimbilie, unikumbatie!” Naya akaendelea kulia taratibu. “Nimekuletea maua.” Naya akajifuta machozi na kumgeukia. “Mwenzio nilikuwa nahamu na wewe mpaka nikaanza kujisikia kuumwa! Kwa nini hukuniambia kama unarudi leo!?” Naya akalalmika kwa sauti ya chini.

          Joshua akambusu shavuni. “Hujanipigia simu.” Joshua akaanza kucheka. “Sijakusindikiza mpaka kazini wewe?” “Sasa baada ya hapo ukawa kimya!” Joshua akamcheka. “Nina hamu na wewe Joshua! Nilitaka kukuringishia nilivyopendeza, ona sasa umeharibu suprise yangu!” Joshua akazidi kucheka. “Lakini yangu imefanikiwa.” “Wala hujafanikiwa!” Joshua akazidi kucheka. “Mwenzio nimekumiss Joshua!” “Na mimi sana. Twende basi.” Naya akaanza kucheka kama anayejua ni wapi anapoitiwa. “Muone!” “Nimefurahi kukuona Joshua! Sikutegemea! Nilijua hutarudi leo!” Bado walikuwa wameinama. “Kweli umeniletea maua?” “Haya hapa mkononi.” Naya akakaa akijifuta machozi.

Yalikuwa mengi na ni aina ya roses tupu. Inanukia vizuri kama rose halisi. Naya akabaki akiyanusa, Joshua akimwangalia. “Nilikuwa na hamu na wewe Joshua!” Naya akarudia tena. “Na mimi Naya. Unafikiri kwa nini nipo hapa leo?” Naya akapandisha mabega akiashiria hajui. “Kwa ajili yako! Vikao vingine nimehamishia kwa simu. Nilitaka tuje tuwe wote.” Naya akambusu hapohapo tena mdomoni. Joshua akacheka. “Asante kwa maua.” “Twende.” Wakatoka. “Nilikuwa na hamu na wewe Joshua! Nilikuwa natamani kukwambia ufanye haraka urudi tuwe wote, lakini sikutaka kukufanya ushindwe kutulia na kazi. Nimefurahi umerudi.” Wakawasikia wakizungumza huku wakiondoka.

Wakaelekea ofisini kwa Joshua. “Sitaki simu Fina!” “Sawa bosi. Kwanza hakuna anayejua kama umerudi.” “Na ibakie hivyohivyo nitakuwa kazini kesho. Leo sipo kikazi.” Naya akacheka huku wakiingia ofisini kwake. Alichokifanya Joshua ni kufunga mlango na kumvuta Naya karibu yake, yakaanza mabusu ya kina. Naya akajitoa kidogo. “Nilikuwa na hamu na wewe Joshua! Umeshanizoesha kuwa na mimi asubuhi na jioni.” “Usizoee. Gari yako inakuja.” “Tutafanyaje? Naona kama nimeshazoea kuwa na wewe! Au nivibaya?” Joshua akacheka taratibu akimwangalia na kumpapasa shingoni. “Sio vibaya.” “Nakupenda Joshua. Wewe ni wakuaminika.” “Na mimi nakupenda sana Naya. Nafurahi, nakuona umebadilika. Sasa hivi hata ukisema unanipenda, naisikia moyoni mwangu.” “Kweli?” “Umebadilika Naya. Nakushukuru kunifungulia Moyo.” Naya akajilaza kifuani. “Nimefurahi umerudi Joshua wangu.” Joshua akamkumbatia vizuri wakatulia.

“Bado natamani kukukiss Naya.” Naya akacheka taratibu kwa deko. “Nilimiss hiyo midomo!” “Na mimi.” Akanyanyua uso akakuta Joshua akimwangalia. Akajisogeza midomo yake karibu, Joshua akampokea, yakaendelea mabusu ya muda mrefu bila kuchoka, Naya akitoa mihemo mizuri kwa Joshua ambaye hakuwa ameshika mwanamke kwa miaka mingi sana, Naya mzoefu wa penzi. “Natamani unikumbatie hivi tu.” Joshua akacheka taratibu.” “Nimekuletea zawadi nzuri.” “Zaidi ya hivi!” Joshua akacheka. “Umependeza sana Naya! Umezidi kuwa mrembo!” “Nimependa ulivyokuwa ukizichezea nywele huku ukinikiss.” Joshua akacheka taratibu akimwangalia pale alipojilaza kifuani kwake.

 “Kweli huna kazi zakufanya kwa leo?” “Nimekufuata wewe hapa. Isingekuwa wewe nisingekuwa hapa. Kwanza nisingerudi leo.” “Nimefurahi umekuja hapa kwa ajili yangu. Nilikuwa ninahamu na wewe Joshua! Nimefurahi sana. Na asante kwa zawadi japo sijajua ni nini. Na mimi nilikununulia zawadi.” Joshua akatoa tabasamu. “Ni nini?” “Mashati yanayofanana na magauni niliyojinunulia. Jumapili nilipendeza! Acha nikuonyeshe picha.” Akatoa simu na kuanza kumuonyesha. “Kweli ulipendeza! Aina hii ya Naya sikuwahi kukutana nayo! Ndio unapendeza hivi!” Naya akafurahi. “Umependa?” “Sana.” “Sasa hujaniona nikiwa kwenye gari yako! Mpaka Ino akashindwa kunisalimia.” Joshua akacheka sana. “Nilipendeza sana. Mimi mwenyewe nilijiona.”

“Upo na kazi nyingi sana?” “Nishamaliza kazi za Jamal. Pale ulinikuta nilikuwa nikifanya vitu vyangu binafsi. Unataka kunipa kazi bosi wangu?” “Sasa hivi ni mpenzi wako, kazi ninayotaka kukupa ni kutulia hapa mikononi mwangu, nikukumbatie tu. Hamu haijaisha.” Naya akarudisha simu mfukoni haraka, akajisogeza karibu yake. “Mimi mwenyewe nataka kazi ya kukumbatiwa ila na kubusiwa.” Joshua akacheka sana. “Naya!” “Midomo yako mitamu Joshua! Unajua kunishika vizuri na kunibusu. Unanichezea nywele vizuri mpaka nimefurahia kuwa na nywele ndefu! Sikujua kama nilikuwa nikijipunja hivi!” Joshua akamshika tena vizuri na kuanza kumbusu tena na tena mpaka yeye mwenyewe hali ikawa mbaya.

Akamuachia na kwenda kuhema pembeni akiwa ameinamia meza yake. Naya akaenda kumlalia mgongoni. “Nakupenda Joshua.” Joshua akamgeukia pale alipokuwa amemlalia na yeye akimchungulia. Akavuta pumzi kwa nguvu. “Inabidi tuondoke hapa ndani. Twende nikakuonyeshe zawadi zako.” Naya akambusu pale alipokuwa amemuegamia. “Nisindikize nikachukue pochi yangu.” Naya akajiweka vizuri nywele zilizokuwa zikichezewa na Joshua. Akazifunga kama zilivyokuwa kabla Joshua hajazivuruga.

“Nimefurahia sana maua. Yale mengine bado nilikuwa nayo.” “Hujayakausha?” “Bado. Nimebadilisha tena maji. Ila itabidi ninunue vessal nyingine ya kuwa naweka yakiwa bado fresh, ile uliyoninunulia ni ya kutunzia yakikauka.” Joshua akacheka kidogo, wakatoka hapo. “Kesho Fina.” “Mimi sijaletewa zawadi?” Akauliza akicheka. “Anayo Jema.” Akajibu Joshua akiondoka, Naya akamsikia Fina akishangilia. Wakaelekea ofisini kwa Naya, akamsubiria akifunga laptop yake.

“Kiongozi nimeambiwa umerudi?”  Akaingia Jamal akikimbia. “Bado.” Joshua akajibu kwa haraka nakumfanya Jamal acheke. “Maana hamkawii! Mimi nipo hapa kwa ajili ya Naya tu. Kazini kesho.” “Jambo dogo tu. Najua ukiweka neno wewe, IT watachangamka.” “Bado unasumbuana nao tu!?” “Huoni nimekimbia niliposikia upo mjengoni? Nisaidie kaka. Wale hawatafanya mpaka uwaambie.” “Unaniharibia mipango yangu Jamal!” “Kwani utaongea sana? Wala huna haja yakutoka hapo ulipo simama, nakusogezea simu hapohapo.” “Halafu Fina nilimwambia mimi leo sipo! Kwa nini ametangaza kama nipo?” “Anaijua shida yangu, Kiongozi. Nikunihurumia tu. Sema neno moja tu, wanipe haki yangu.” Joshua akamwangalia Naya.

“Nivumilie Naya wangu.” “Usijali.” Naya akavuta kiti na kukaa. Jamal akamvutia simu ya mezani. “Mwambie Fina ampigie Ayush, kisha aniunganishe naye.” “Hapo umemaliza. Maana ukiongea na Ayush mwenyewe, itakuwa umeua mzizi wa fitina.” “Muda Jamal!” Joshua akasisitiza. Jamal akampigia Fina. “Naomba muunganishe Kiongozi hapa na Ayush.” “Dakika moja.” Fina akajibu. “Ni wewe mwenyewe au!? Maana nimeambiwa upo safarini.” “Ni mimi. Unanikwamisha Ayush.” Jamal akalifurahia hilo. Akabaki akisikiliza. “Ni nini tena!?” “Issue ya Jamal ipo kwenu zaidi ya week sasa, mnategemea afanyeje kazi na wewe unajua namtegemea sana?” “Hilo sikujua Kumu. Acha nifuatilie.” “Naomba likamilike tafadhali.” “Bila shaka.” Ayush akajibu na sauti yake ya kihindi. Joshua akakata simu.

 “Si umeona Mkuu. Maneno machache tu, mimi kesho napewa haki yangu.” Joshua akamtizama na kumgeukia Naya. “Twende.” Jamal akacheka. “Nakushukuru lakini.” “Umeniharibia mipango yangu.” “Mbona Naya mwenyewe hana shida Kiongozi! Naya anajua tatizo langu.” Joshua hakumjibu, akamshika Naya mkono nakutoka. 

Naya Na Joshua Tena.

“Unataka twende wapi?” Joshua akacheka. “Unataka unitoe?” “Popote unapotaka. Mimi nitalipa. Nimefurahi umerudi kwa ajili yangu Joshua. Nilikuwa na hamu na wewe!” Hilo Naya alilirudia bila kuchoka. “Na mimi Naya. Sasa hivi naanza kuchukia kuishi mbali na wewe.” Naya akacheka kidogo na kuinama. Joshua akatoa gari. “Unafikiria nini sasa?” “Sijui.” “Acha bwana Naya.” Naya akacheka kidogo akiwa anafikiria. “Nini?” “Nafikiria maisha yakuja kuishi na wewe.” “Unafikirije?” Joshua akamuuliza. “Naogopa hata kufikiria.” Joshua akakunja uso. “Kwa nini tena?” Naya akacheka kidogo. “Naona kama wakati mwingine sikustahili Joshua! Halafu naogopa usije ukanizoea ukaanza kunipuuza.” Kidogo Joshua akaridhika alidhani Naya hamtaki.

“Cha kwanza ujue mimi ni wako Naya. Hilo nina uhakika nalo, sina wasiwasi nalo. Pili, sijitahidi kukufanyia chochote na mimi sio mwigizaji. Hakuna kitu nakufanyia cha maigizo ili tu kukuvuta kwangu. Hapana. Nafanya kwa kuwa nakupenda. Namuomba Mungu anisaidie nisipelee ila kunipa hekima ya kuishi na wewe kwa kila hatua ya maisha yetu. Ukiwa mchumba, mke na mama. Ila kwenye kuwa mke, hapo nitaomba tusubirie kwanza watoto. Nataka nibaki peke yangu kwanza kwa muda kabla watoto hawajaja na kukuchukua mwili na akili.” Naya alicheka mpaka akajifunika uso.

“Joshua!” “Nakuwa mkweli na nimewahi mapema. Acha nikufaidi mimi kwanza, ndipo lije swala la watoto.” “Kwa muda gani?” “Kama unayo haraka ya watoto, basi nipe mimi miaka hata miwili tu. Iwe mimi tu. Akili na mwili wako vyote vije kuwa vyangu tu. Baada ya hapo, hata ukitaka kuzaa mchana na usiku, sina neno.” Naya alicheka sana asiamini mipango ya Joshua. Alimwangalia na kurudia kucheka. “Mimi nimekuwa mkweli. Nimeeleza haja yangu.” “Acha Joshua.” “Kweli Naya.” “Sasa unataka tuanze tu kwenye ndoa, na uzazi wa mpango?” “Hata kabla ya harusi. Naomba tutafute mtaalamu wa kutushauri. Tufanye yote. Ili tukiingia kwenye ndoa, tusiwe na wasiwasi.” “Lini?” Naya akauliza taratibu, Joshua akacheka na kunyamaza. Naya akashangaa ila hakutaka kulazimisha, akaona anyamaze kwa kuwa alijua amemsikia.

Wakatulia kimya Naya akiwa amejiinamia. Ghafla akajisikia kukosa raha. Akahisi Joshua hataki kuja kumuoa kwa haraka. Akajua yatatokea yaleyale yakuja kuachwa kama kwa Malon, mahusiano yasiyo na mwisho. Akabaki ameinama, ameshikilia maua yake. “Unataka tupitie vessal sasa hivi?” “Abee!” Ikawa kama amemtoa kwenye mawazo. “Kifaa chakuwekea hayo maua?” Naya akabaki kama hajaelewa. “Mbona mawazo yamehama tena?” “Samahani, sikuwa nimekusikia tokea mwanzo. Kifaa cha nini tena!?” Naya akawa kama amechanganyikiwa kabisa.

“Ni sawa tukienda sasa hivi kununua kifaa chakuwekea maua yakiwa mabichi?” “Hapana.” Joshua akawa hajamuelewa. “Hapana tusinunue!?” “Ndiyo.” “Naya! Sikuelewi mpenzi wangu. Tukanunue sasa hivi au tusinunue?” “Sio lazima kununua sasa hivi. Naweza hata kununua wakati mwingine.” “Leo utayaweka kwenye nini?” “Jagi. Tunalo jagi.” “Kama hutajali, basi naomba tupitie sasa hivi.” “Sawa.” Naya akajibu na kutulia kabisa.

Joshua akaendesha mpaka sehemu ya kupata kifaa, wakanunua. “Nimependa. Asante. Ila nilitaka kulipia. Sikutaka kukuongezea tena gharama.” “Usijali. Upo sawa?” “Nipo sawa kabisa.” Naya akajibu na tabasamu la wasiwasi usoni, Joshua akamuona. “Ila naomba ule kabla hatujaachana, Joshua. Kama hutakubali chakula cha kununua, basi niahidi utakwenda kusubiria chakula cha nyumbani. Angalau ulale nikijua umeshiba.” Ilimgusa sana Joshua. “Sawa. Naomba nikasubirie chanyumbani ili nipate muda na kina Zayoni pia.” Naya akacheka kuonekana ameridhia. “Si ni sawa?” “Ningependa hilo, japo nahisi wanakuogopa kidogo.” “Nimeliona hilo.” Wakaanza safari yakurudi kwa kina Naya.

“Kwani tofauti yangu na Malon kwao ni nini?” Naya akacheka akifikiria kidogo. “Kwanza ujue Malon ni mtoto wa mtaani, aliyefanikiwa. Anamjua binadamu kwa kuishi naye.” “Mbona ni kama mimi tu.” “Wewe ulikwenda shule, na ukakusudia kubadili maisha kwa uzuri. Upo kujenga jamii. Malon hakurudi shule, yupo kuthibitishia jamii shule si kila kitu, na alijitahidi kuifikia jamii kwa kuiharibu. Hiyo ndio tofauti yenu. Alihakikisha anatenga muda wakutosha mtaani, kumfikia mwanamke na mwanaume kuonyesha shule si kila kitu ndio maana wanawake zenu bado wanaweza kulala na yeye muda na wakati wowote anaotaka yeye. Akawaonyesha haohao wanaume kuwa, shule zao si kila kitu kwa kuwa bado haziwasaidii kukidhi mahitaji yao ya muhimu. Aligawa pesa kwa kadiri ya uwezo wake, japo pia amejaliwa utoaji. Anao muda wakutosha kumfikia mtu yeyote yule amtakaye. Mama yangu alimuonyesha hamtaki sababu hakusoma. Na yeye akamuonyesha yeye ni bora kuliko wanaume wote wosomi waliokuwa wakinitaka. Ndipo akajaa pale nyumbani. Yeye mwenyewe na pesa yake.” “Hapo nimekuelewa.” Joshua akacheka.

“Huwezi kushindana na Malo kwa kuwa yeye alitaka ushindani na kudhihirishia watu hajaharibikiwa. Alichokiacha kwa ndungu zangu sasa hivi, ni majonzi kama waliompoteza ndugu wa maana, wakati ni Malon! Mimi namjua. Atakuja kurudi tu.” “Haiwezekani Naya!” Naya akacheka. “Mimi namjua Malon. Na ninashukuru kunitia moyo kuwa karibu na Bale. Amemuumiza sana Bale. Nilikwambia amemuacha kama amepigwa na butwaa?” “Bado tu!?” “Utamuhurumia Bale. Na ninahisi ameingiwa hofu kwa baba, maana alitusema vibaya sana mimi na baba. Na ubaya wa baba si mzungumzaji kujua la moyoni. Heri ingekuwa mama. Angemsema, yakaisha. Ila baba amenyamaza kimya wala hajamuuliza ni kwa nini hajaondoka. Hajamuuliza chochote kile mpaka natamani kumuomba baba angalau azungumze naye, ili atulie. Hali wala hazungumzi. Unaweza ukamkuta amekaa pale mezani, ameangalia sehemu moja bila hata kusogea.” “Lakini subiri kwanza Naya.” Joshua akawa kama hajaelewa.

“Huyu Malon unasema anaweza kurudi tena!?” “Tena na sababu inayosikika vizuri mno. Itakayoeleweka na ukamuunga mkono. Sijui aliumbwa vipi Malon! Lakini ndivyo alivyo. Na akirudi ndio anakuwa vile kama unavyomuona. Mwingi mno. Anajaa kila mahali na kwa kila mtu mpaka mjisikie vizuri. Anarudi na mipango mizito kama vile ulivyomuona kwa Bale. Ikifika sasa karibu. Akaona itamfanya ajifunge kwako. Ikawa ni jambo la muda mrefu. Sio la muda mfupi. Ukamuwekea mipango ya kudumu kama vile Bale mpaka sijui kufanya biashara naye ikawa kubwa, sijui huwa anaingiwa hofu, sijui ni roho chafu inakuwa inamuingi! Anakimbia. Kwa sababu nzuri tu.” Joshua akachoka kabisa.

“Wewe kweli mvumilivu Naya. Mimi mtu mwenye sababu siwezi. Nachoka haraka sana.” “Wanakujua pale kazini.” “Basi nafikiri ni kote. Hata huko nilikotoka. Ninapoacha jambo lifanyike, ukakubali utalifanya kwa muda tuliokubaliana, huwa nataka matokeo. Hata yawe mabovu, yawepo tu. Si maneno matupu! Hapana. Hata wale makaburu wameshanijua. Na huwa nahakikisha wanaelewa tulichokubaliana. Sitaki kupotezewa muda.” “Joshua! Mpaka huko kwa wazungu?” “Kwani uzembe ni rangi ya mwili?” Akamuuliza.

Hauchagui unazungumza lugha gani au una rangi gani ya mwili. Yuko jamaa alisemaga huu usemi, nikauelewa sana. Alisema hivi, unaweza ukawa mweupe, yaani mzungu, lakini ndani yako ukawa mweusi kabisa akimaanisha kujawa giza lakupita kiasi. Uzembe ni roho inayofanya kazi ndani ya mwanadamu bila kuchagua. Zipo sababu 100 zakutowajibika, lakini huwepo moja au mbili za kuwajibika. Ndipo ujue ni wapi mizani hulemea.” Joshua akaongea.

“Sipendi kufanya kazi na mwanadamu awaye yeyote yule, mwenye kupenda kutoa sababu ya kwa nini ameshindwa bila hata kujaribu! Hapana. Na huwa sijali rangi yako ya mwili, nitakwambia kabisa. Unanipotezea muda wangu. Kwa hiyo hata kule wakiniita, huwa wanajiandaa. Sitaki nifike kule, waanze kunikwamisha kwa sababu zozote zile! Hapana. Ni bora tokea tunapanga mimi na wewe, uniambie kabisa. Muda tuliokubaliana, hautakutosha. Unataka tuongeze, hapo sawa. Ila ukishasema ndiyo, napenda ubakie hapohapo. Na ikishindikana wakati wa kazi, nijulishe kabla ya ule muda, maana huwa najua kuna mambo huwa yanatokea. Lakini sio sababu kama zile za Jamal! Hata yeye anajua namuhesabia tu. Nikimbadilikia, hataamini.” “Joshua!” Naya akashangaa sana.

“Naya! Nimeaminiwa na kampuni kama ile, unafikiri tungekuwa hapa leo kama ningeruhusu mambo kama hayo!?” “Lakini kweli.” “Siwezi. Juzi Njama alimtuma mwanasheria wake aje amuombee msamaha pale kwenye kampuni.” “Joshua!” “Kabisa. Amegonga mwamba. Wameona hana kesi ila yeye ndio alishitakiwa kwa kufanya fujo na kutukana. Wapi watamuajiri tena?” Naya kimya. “Hakuna.” Joshua akajibu mwenyewe. “Tabia mbaya zinaenea kwa haraka Naya, kuliko njema. Sasa hivi Njama anafahamika kwenye hayo makampuni kwa matusi aliyotukana ofisi ya Mwajiri na mpango wake wakutaka kufilisi kampuni ili ajinufaishe. Waliponiuliza kama naweza kumsamehe na kumrudisha, kwa haraka sana niliwaambia nafasi yake nimeifuta, siajiri mtu kwenye kitengo changu, nataka kupunguza. Hayo niliyajibu kupitia Jema, nilipokuwa safarini. Jema anasema ameambiwa na Fina, wote pale wamejawa hofu ndio maana umemuona Jamal ameniwahi na kuuza kesi.” “Joshua! Kumbe!” Joshua akacheka akitingisha kichwa.

“Jamal mjanja sana. Alijua kama ni kupunguza watu pale, ningeanza na yeye. Jema ameniambia amekuwa akitumiwa ripoti ambazo hata hajaomba.” Naya akaanza kucheka. “Sasa ripoti za nini?” “Basi tu, kuonyesha kila mmoja yupo kazini.” “Kwa hiyo ni kweli umefuta nafasi ya Njama?” “Kabisa. Hata ofisi yake sasa hivi haina kitu chochote kile. Nilimwagiza Fina, isafishwe kabisa, iachwe tupu wakati nikifikiria nini chakufanya.” “Sasa nani anafanya majukumu yake?” “Nafanya mwenyewe.” “Hulemewi?” “Ndiyo na hapana. Sijapata mtu kama Njama. Nikikimbilia kuweka mtu, nitalemewa zaidi. Nitakuja kuijaza, lakini sio sasa hivi. Nataka kupata mtu sahihi kama Njama. Njama alikuwa mtu wa kazi. Mwepesi na muelewa. Mapungufu yake yalikuwa yakawaida tu kama mtu mwingine yeyote yule, lakini alikuwa akinirahisishia sana kazi. Ile fujo ya juzi ya watu kutomaliza ripoti kwa wakati, isingetokea kama Njama angekuwepo. Njama alikuwa akiwaweza, na mkali kwao bila kujali umri ila kazi tu.” Naya akataka kuuliza sasa ni kwa nini hamsamehi Njama na kumrudisha kazini, lakini akaona anyamaze tu.

Wakawa wamefika nyumbani, Naya alishampigia simu baba yake akimuomba Zayoni awafungulie geti. Wakakuta lipo wazi. Joshua akavuta gari mpaka ndani. “Nisubiri wakati nakuandalia chakula.” “Na wewe?” “Mwenzio siku hizi nakula chakula cha nyumbani kwake Joshua Kumu. Naletewa mpaka kazini!” Joshua alicheka sana. “Naya!” “Nakula chakula anachopika shefu mwenzio! Usiniletee mchezo.” “Kweli wewe sio mwenzangu. Sasa usiku?” “Usiku nakula vitu vyepesi. Asubuhi kifungua kinywa cha baba Naya, basi.” “Hutaki kunenepa?” “Ulijuaje?” Wakashuka garini wakicheka.

 “Karibu ndani.” Naya akamkaribisha akiwa amebadilika. Ile hali ya ukimya na kuchanganyikiwa aliyoipata kwenye gari baada ya Joshua kutojibu swala la ndoa, ikamuisha kabisa. Akatulia. “Njoo kwanza Naya.” Naya akarudi upande wa Joshua. “Kuna zawadi hii ya Zayoni. Yakumpongeza kwa kufaulu vizuri. Mwambie inatoka kwetu wote.” “Jamani Joshua! Ni nini?” “Angalia. Ulisema anapenda kupiga picha. Nimemnunulia kamera.” Naya akafungua na kushika mdomo kwa mshangao. “Itafaa?” “Sana. Kikamera tulichomnunulia na Malon, kiliharibika mapema sana. Nahisi haikuwa na ubora mzuri. Asante Joshua.” Naya akambusu shavuni. “Karibu. Na wewe zawadi zako zipo kwenye hiyo mifuko mingine.” “Nakushukuru sana Joshua. Asante.” Wakasaidiana kutoa mizigo garini, ndipo wakaingia ndani.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Walimkuta Bale amekaa mezani kama kawaida yake, ila peke yake. Zayoni sebuleni na baba yake, lakini kimya wote macho kwenye luninga. Naya akapitiliza chumbani kwake, akamuacha Joshua nyuma. “Umerudi Joshua?” “Ndiyo Zayoni. Nimerudi. Naya ameniambia matokeo yametoka, umefaulu vizuri sana.” “Ndiyo. Ila sitaki kwenda shule za bweni. Nataka kusoma hapahapa kama Bale. Baba amesema ataenda kunifanyia mpango, wasinipeleke mbali.” “Hongera sana.” “Joshua amekununulia zawadi ya kufaulu.” Naya akaongea akiwa chumbani. “Ni kutoka kwangu na Naya, sio mimi peke yangu.” Wakamsikia Naya akicheka.

Akamsalimia baba Naya. “Marahaba Joshua. Naona umepokelewa na maneno mengi ya Zayoni.” Wakacheka. Zayoni akamfuata dada yake. “Niingie Naya?” “Subiri kwanza. Usiingie. Kama ni zawadi nakuletea hukohuko.” Zayoni akasimama mlangoni akisubiria. “Vipi Bale? Upo mzima?” “Nipo.” Bale akasimama kwenda kumpa mkono. “Karibu.” “Asante.” Joshua akatafuta sehemu akakaa. “Vipi lakini? Mapumziko yanakwendaje?” Joshua akamuuliza Bale pale alipokuwa amesimama. “Hivyohivyo nipo tu. Nilikuwa na mpango wa kwenda kufanya biashara na Malon, sijui nini kimetokea, naona hata simu zangu hapokei tena.” Bale akajikuta anaongea hapo mbele ya baba yake akimwambia Joshua.

“Nimekuwa kama nimepoteza dira! Sijui niseme nimechanganyikiwa au vipi? Nimekwama.” Akajieleza Bale akisikika kupoa haswa. “Hutakiwi kukata tamaa. Huo ni mlango mmoja tu uliojifunga kati ya mingi inayokusubiria.” “Nahisi hata nimepoteza lengo.” “Haitakiwi iwe hivyo Bale! Lengo lazima libakie ila njia ndio imefunga. Na sio mwisho. Tafuta njia nyingine kufikia hilo lengo. Hakuna kitu rahisi Bale. Usikate tamaa ila fikiria zaidi.” “Daah! Ndio nafikiria lakini nahisi nipo kwenye mshituko bado.” “Inaeleweka kabisa, ila usikae hapo kwa muda mrefu kwa kuwa unajichelewesha kufikia milango mingine.” Joshua akapata ujasiri wa kuzungumza naye.

“Nilikusikia ukiwa unazungumza na Naya, ulikuwa na malengo mazuri sana. lazima uhakikishe unapambana kufanikisha. Nina uhakika biashara ya mazao ni wengi tu wanafanya. Swala ni wanafanyaje?” “Ile ya Malon ilionekana rahisi kweli! Na ingefanikiwa kwa haraka.” “Sasa haipo tena.” Akadakia baba yake. “Utakaa ukiwaza hapo juu ya Malon mpaka lini?” Baba yake akamuuliza kwa ukali kidogo.

“Nahisi niliweka tumaini kubwa sana kwake. Naomba unisamehe baba.” Pakazuka ukimya wa ghafla. “Niliongea maneno yasiyo mazuri kwa kuwa nilimwamini sana Malon. Lakini nimejifikiria, nimeona nilikukosea baba yangu, naomba unisamehe.” Bale akaanza kutokwa na machozi. Akamgeukia tena baba yake akiomba msamaha. Naya akatoka akiwa amebadili nguo, amevaa tu kigauni cha nyumbani. Lakini akapendeza na nywele akavuta juu kabisa, akazibana zikawa zikining’inia na mawimbi mazuri. Akavaa na hereni nyingine sio kama alizovaa akiwa kazini, akaenda kupiga magoti pembeni ya baba yake. Akamvuta mkono na kuuegamia. Lakini baba yake alijua anamuombea msamaha Bale.

“Ni nini?” Baba yake akamuuliza. “Mimi nakupenda baba Naya.” Baba yake akabaki akimwangalia Naya pale alipojiegemeza. “Nimekosa baba, naomba unisamehe. Lakini nia ilikuwa nzuri baba yangu.” “Umeniudhi sana Bale. Nimechukia kutaka kumrudisha Naya kule ulikokuwa ukimuona akiteseka! Yote hayo sababu ya maendeleo! Hapana Bale. Isiwahi kurudia tena. Usiwahi kuuza binti yangu sababu ya pesa. Iwe nikiwa hai au nimekufa, shida isikopotezee utu. Nilikwambia kabla, lakini hukunisikiliza, ukaja kunigombeza hapa mbele ya binti yangu, nikiwa nimeshakwisha kukuonya!” “Nisamehe baba.” Bale akapiga na yeye magoti. Joshua kimya akabaki amenyamaza kama Zayoni.

“Nimekukosea baba yangu. Na zaidi nilikosa adabu kwako. Nisamehe. Lakini nimejifunza. Naogopa naona kama nimejilaani! Kuanzia sasahivi nitakuwa nikikushirikisha kama Naya, ili uwe unanishauri, nisipotee tena. Nimekosa baba.” Naya akamuegemea baba yake zaidi. Akamwangalia. Akamuona na yeye Naya anaanza kulia. “Nimekusamehe. Na wewe acha kulia, nenda kaandae chakula, mwenzio ale kabla hajaondoka.” Naya akaanza kucheka taratibu akisimama. “Asante baba. Hakika nimejifunza.” Bale na yeye akasimama. “Labda Naya angenipa kabisa zawadi yangu, baba.” Zayoni akaongea kwa kujihami kama asiyetaka kuharibu. “Zayoni naye!” “Si mara moja tu Naya?” Naya akaenda kumchukulia. Pakatulia kwa muda.

“Labda niulize kama naruhusiwa.” “Karibu Joshua.” Baba Naya akamwitika kwa kiungwana. “Wazo la biashara ya mazao, linatoka kwa nani?” Pakazuka ukimya kidogo, na Joshua naye akatulia kuwapa nafasi. “Labda niseme ni kwangu.” Akajibu baba Naya. “Kuna kipindi nilikwenda kufanya kazi kwa Malon, nikaona ni biashara nzuri. Niliporudi hapa, nikawaeleza vile alivyofanikiwa Malon kwenye hilo eneo. Nafikiri ndipo hapo Bale napo akapata hilo wazo. Ila jinsi ya kufanya na sisi ndio imekuwa changamoto. Lilianza swala la eneo. Eneo hilo ni kama linakamilika, sasa pakupata bidhaa ndio ikawa changamoto.” “Kwa hiyo kama nimeelewa sawasawa mzee wangu, bado ni kitu ambacho unafikiri ungependa kifanyike?” Joshua akauliza tena. Naya akisikiliza akiwa jikoni. Alikuta Bale alishapika, akaanza kuandaa meza huku akipasha moto.

“Sio biashara mbaya. Ikifanywa kwa njia sahihi. Ukweli inalipa. Na uzuri biashara ya mazao si ya msimu. Watu wanahitaji kula kila siku.” Joshua akacheka. “Ndivyo anavyozungumza jamaa mmoja. Nilimwambia Naya nitakwenda kumtambulisha kwake na familia yake. Nikija wa kama huu umri wangu tu. Lakini baba, yule kijana amefanikiwa. Mimi nikikwambia mtu amefanikiwa, simaanishi mafanikio yakuweza kubadili mboga nyumbani.” Baba Naya akacheka na kugeuka vizuri ili kusikiliza.

Kisha akauliza. “Na ni biashara ya mazao tu?” “Mazao na sasa anakusanya na mafuta. Aliajiriwa na BOT, lakini akaacha kazi. Anafanya hiyo biashara akisaidiana na mkewe. Baba Naya?” Joshua akaita kwa kuhamasika. Mpaka wote wakacheka. “Ndiyo!” Baba Naya akaitika. “Wamefanikiwa! Wamefanikiwa mno. Mimi namtania kwa jina la GM, lakini anajulikana kama Geb Magesa, wengi wanamuita Magesa tu. Na mkewe anaitwa Nanaa. Mtulivu sana huyo jamaa. Sana. Ile mkimya wakupitiliza, ila anaakili na yenyewe niyakupitiliza. Akiongea lugha ya biashara, utaelewa ni kwa nini amefanikiwa.”

“Anafamilia nzuri mno. Nilimfahamu kupitia shemeji yake, lakini nilihakikisha ananisogeza karibu yake kwa vile alivyo mtu wa familia. Anaishi na mkewe kama ndio anataka kuomba kuoa! Jicho lake lipo kwa mkewe muda wote, wakati wote. Popote walipo jicho lake litamfuata mkewe. Na Nanaa mkewe, anajua kama mumewe anampenda. Ni binti mdogo tu, lakini ametulia kwa mumewe. Anaonekana ana upendo, na huwa ananitania na kuniambia, hana mazoea kwa mpenzi wake. Na nafikiri ndio siri ya mafanikio ya ndoa yao. Ni mama wa watoto watatu, lakini mtulivu haswa. Anampenda mumewe na familia yake kupita maneno nitakayo kwambia ukaelewa. Ameweza kujichanganya katikati ya ndugu wa Geb, utavutiwa tu. Wanaishi na mama yake Geb. Ukiwa nao, unaweza sema mama G ni mama yake Nanaa! Wanaelewana sana. Hakika utapenda familia yao.” Joshua akasifia.

“Sasa huyo ndiye anayezungumza kama wewe baba. Biashara ya chakula si ya msimu.” “Ni kweli. Wao wanafanyaje?” “Anayo malori yake, na maofisi pamoja na maghala huko mikoni na hapa mjini pia. Wanamkusanyia mazao, na kuleta huku mjini. Anasema alianza hapa Dar, lakini sasa hivi hapa pamekuwa ni eneo la kuyakusanya, anafungasha kwa muundo wake yeye, na kusambaza. Mimi mwenyewe mchele wangu, aina yote ya mafuta yakupikia nanunu kwao.” “Au ndio hawa mifuko yao imeandikwa Magesa LtD?” “Haohao.” “Bale anapenda kweli mchele wao, japo gharama!” “Basi hata ubora wake upo juu.” Wakabaki wakizungumza baba Naya na Joshua, wakipokezana maneno.

Kwa kumsikia tu baba Naya hapo, ungejua amemfungulia moyo Joshua. “Sasa acha nitazungumza naye kesho. Maana kama nilivyokwambia, yeye ni mtu wa familia sana. Mida kama hii ngumu kumpata, anakwambia anacheza magari na watoto wake.” Baba naya akacheka. “Kesho nitazungumza naye, nione jinsi anavyoweza kukusaidia mzee wangu.” “Nitashukuru sana Joshua.” “Karibu.” Bale akabakia kimya pembeni ya kiti cha Joshua.

Joshua akamgeukia. “Sasa Bale?” “Mimi nimekwama. Vyeti bado havijatoka, naona na biashara imegoma!” “Kuna mambo mawili. Unaweza kuamua kufanya na baba hiyo biashara ya mazao, japo ningemshauri baba aongeze na mafuta.” “Mtaji Joshua!” “Upo na mtu mkubwa sana humu ndani mzee wangu! Mfanyakazi wa Coca! Huwezi kukosa pesa.” Naya akacheka sana. “Usiniangushe bwana Naya!” “Sawa bosi wangu. Tumeni maombi.” Bale akaanza kucheka. “Basi hapo pumu imepata mkohozi.” “Wewe kama unashida, tuma maombi nikufikirie.” “Sawa Naya.” Bale akakubali.

“Joshua, umesema mambo mawili, lapili ni nini?” “Lapili kufanya kazi. Wakati mwingine unaweza kupata kazi kwa kufahamiana tu, si lazima vyeti. Vyeti ni utaratibu tu.” “Sasa nani ananifahamu mimi, Joshua?” “Kwanza jua unataka kufanya nini. Hilo ndilo la msingi. Mimi nilijua sitafanya biashara, ila kuajiriwa. Nikahakikisha nakua kwenye soko la ajira. Kutafuta uzoefu, ndio maana nilikuwa nikisoma  nikiwa kazini. Uzoefu ndio umenifikisha hapa kuliko hata elimu. Sijui kama unanielewa.” “Nahisi.” “Ubora ndio utakufikisha mbali. Ni rahisi mimi kukuamini nikakupa kitengo nikijua nikisafiri kitengo kitabaki salama kwa mtu anayejua kitu gani chakufanya, kuliko mwenye vyeti halafu hajui chakufanya. Sijui kama unanielewa?” “Hapo nimekuelewa.” Bale akakubali.

“Pale kwenye kitengo chetu, kuna mzee nimempa idara ya mambo ya Products. Anaongoza wasomi, hata Naya anamfahamu, lakini yeye hana hata shahada, ila elimu ya chuo ya miaka miwili tu na uzoefu kazini. Sijui kama unanielewa?” “Naelewa.” “Vijana wote wanaokuwa chini yake, sijampata kama yule mzee. Kwanza anayo nidhamu kuliko wengi tu pale. Ukimpa kazi, ataifanya bila kulalamika. Mzee wa muda mrefu, halafu mwadilifu mno. Sasa wewe jiulize ni nini unataka? Kama ni upande kama huu wangu, jiingize kwenye kazi, huku ukisoma. Ni shida. Lakini unapata mambo mawili kwa wakati mmoja. Uzoefu wa kazi na shule. Au jikite kwenye biashara kama huyu jamaa yangu. Halafu anza mapema, ili kama haya yaliyokupata hapa, iwe sehemu yako. Hushituki, ila kutafuta suluhu kwa haraka na kuendelea. Unapata uzoefu.” “Hapo nimeelewa.” “Lakini.” Joshua akageuka vizuri.

“Chochote utakachochagua, hata Naya nimemwambia. Lazima uhakikishe unakimudu, tena kwa kiwango cha juu ndipo utafanikiwa. Kama ni kazini, hakikisha unachagua jambo moja, na kusimama nalo vizuri. Sijui mnazungumza nini na Naya, lakini baada ya mwaka mmoja tu, Naya atakuwa mbali sana. Mimi huwa nachukua kazi zake na kuwaringishia jamaa wengine wa kampuni nyingine ambao wanavyeo kama mimi, lakini tayari wanamtaka Naya. Ana moyo wa kufundishika, na nimchapa kazi. Na Mungu akampendelea akili ya ubunifu. Sikwambii kwa kujivuna tu, lakini Naya wangu ni bora sana kuliko hata baadhi ya viongozi wake.” Bale akacheka na kuinama, vile Joshua alivyoongea. Tena kwa kujivuna na kupunguza sauti.

“Maua yale ya kwanza ilibidi tu kumpa kwa kazi nzuri aliyofanya. Japokuwa ni mgeni, sasa hivi anaongoza kitengo chao kilichokuwa kikilalamikiwa na kiongozi wao, na ameongezewa access, na Naya amekimudu bila kelele. Sijui kama amekwambia baba!” “Ameniambia.” “Basi huyo ndio Naya wangu. Sasa mtu kama huyo, ukimpa mwaka mmoja tu kazini, na akaendelea hivyo, kwa nini usimpe idara nzima?” “Ni kweli.” Bale akaafiki. “Juhudi, kujituma, na ujue unataka nini. Boresha kitu kimoja au viwili, kisha vijue haswa.” Bale akavuta kiti karibu.

“Lakini naona kwa sasa kuna uhitaji wa pesa zaidi.” “Hapana Bale. Wenye pesa tunalilia mlichonacho nyinyi hapa. Familia kwanza. Sijui kama unanielewa?” Bale akainama. “Familia kama hii, haipatikaniki kwa pesa. Weka mipango sahihi, utafanikiwa tu. Unaweza ukadhania unachelewa, lakini Bale, upo katika familia sahihi, na wakati sahihi. Tambua unacho kitu cha thamani sana. Kishikilie kwa kila namna, Mungu ataweka mkono wake.” “Nashukuru kumkumbusha hilo. Bale anahisi amechelewa sana.” Baba yake akaongeza.

“Hata kidogo Bale. Wewe bado kijana mdogo. Unayo maadili mazuri sana. Mungu amekutengenezea njia sahihi ambayo wengi hatukubahatika. Mimi ningetamani nipite ulipopita wewe Bale. Kukuzwa kwenye familia kama hivi wewe, nisome nikijua ninapo nyumbani. Sikubahatika Bale. Ndio namtaka Naya, kwa umri huu, aje anitengenezee nyumbani! Hudhani kama wewe unayo bahati!?” Ilimgusa Naya, mpaka akasimama huko alipo, akajishika kifuani. Bale akainama. “Upo katika njia sahihi sana, usikubali mtu mwingine akakupotosha. Kwanza umesoma. Mimi shahada ya kwanza nimepata kwa shida mno. Kwanza sikupata shahada kama yako. Nimeungaunga kweli! Tulia ndani ya familia. Fikiria ni nini unataka. Swala la biashara tayari ni la mzee. Ukitaka kujiunga naye, sawa. Ukitaka ajira pia fikiria unataka kitengo gani, kisha tuanzie hapo. Lakini ukiwa umetulia na unajiamini.” “Nashukuru Joshua. Asante sana.” “Na mimi asante kwa kamera.” Zayoni akaingilia kwa haraka akicheka.

“Muone naye huyu!” “Nilikuwa nikisubiria na mimi nimshukuru ili nianze kutumia kamera yangu. Amenijia na kila kitu! Asante sana.” “Umshukuru na Naya. Naya anakusifia sana Zayoni. Anasema wewe mtoto mzuri, unapenda shule na mtunzaji pia.” Zayoni akacheka. “Hata baba ananiambia hivyohivyo. Mimi nimefanana na baba, sio kama Bale na Naya. Wao wamefanana na mama yetu.” Wote wakacheka. “Nimefurahi sana.” “Karibu Zayoni.” Zayoni akamfuata Naya jikoni. 

“Nikwambie ukweli Joshua?” Joshua akamgeukia Bale. “Karibu.” “Mimi sina moyo wa biashara kama hivyo Zayoni na Naya. Nafikiri wao wamepata kwa baba. Mimi nilitaka kufanya ili tu kumfurahisha baba, na kusaidia mambo ya hapa ndani. Naomba nisaidie kama naweza kupata kazi. Mimi ni mzuri sana kwenye mambo ya uongozi. Tokea nipo shule ya msingi mpaka chuo, nimekuwa nikiwa kiongozi tu. Nimesomea mambo ya utawala. Na pale chuoni pia nilikuwa kiongozi kwenye sehemu nyingi tu na kuhusika kwenye vikao vingi hata na wakubwa wa nchi waliokuwa wakija pale kuzungumza na wanachuo. Matatizo yalipokuwa yakitokea pale chuoni na mimi nilikuwa miongoni mwa kamati za viongozi waliokuwa wakitafuta suluhu mpaka kwenye uongozi wa chuo. Kwa hiyo nikipata kwenye ofisi za HR, nahisi nitakua vizuri bila shida.” “Safi sana. Yaani mpaka hapo tu, jinsi ulivyojieleza, kama ni usahili, umepata kazi.” “Kweli?” Bale akauliza akicheka. “Kabisa. Umeongea kwa lugha nyepesi tena ufasaha na kuonyesha pia uwezo wakufanya kazi ukiwa kwenye mazingira magumu.” “Joshua unajua kumjenga mtu!” “Lakini si kweli mzee wangu!? Umemsikia mwenyewe.” Joshua akauliza wakicheka.

“Mi kweli Bale amekuwa kiongozi maisha yake yote.” Baba yake akasifia. “Basi ndicho kitu alichopewa na Mungu ili kukifanyia kazi. Kama nilivyomwambia Naya, na wewe hivyohivyo. Jipe muda kazini, na usichezee nafasi yeyote utakayopewa.” “Hakikisha ukiitwa sehemu kwa chochote, unaacha historia ya kuja kuitwa tena.” Akaingilia Naya. “Fanyia mazoezi kila kitu unachotaka kukisema mbele za watu. Namaanisha ofisini.” Joshua akacheka sana. “Umemsikia Naya wangu. Ameiva kabisa.” “Kweli ameiva.” Wakacheka. “Na Naya hakudanganyi. Juma lililopita ametoka kusoma ripoti ya kitengo chao, tena kwa kushitukizwa mbele ya idara nzima!” “Aliweza?” Bale akauliza.

“Usicheze na Naya.” Wote wakacheka. “Nakwambia mimi mwenyewe alinishangaza, nikabaki nikijivuna tu. Kila kitu kilisimama, nikaenda kununua maua.” Wakazidi kucheka. “Ilikuwa ripoti nzuri sana, tena aliiandaa yeye mwenyewe, kiongozi wake hakuwa tayari.” “Ila nilitayarisha ripoti kubwa sana!” Naya akalalamika. “Ule ulikuwa mwanzo tu. Tena sio kwamba ilikuwa mbaya. Hapana. Ila ilikuwa ikifaa kwa kitengo chote, si kwa idara moja. Huoni hata idara nyingine walikuomba wakatoe kopi? Ulifanya vizuri sana. Sasa ndio utaalamu huo, hamishia kwa Bale, wakati tukimtafutia sehemu yakuanza kazi.” “Asante Joshua.” Naya akashukuru, Joshua akacheka.

“Kweli na mimi nakushukuru, Joshua. Nilikuwa nimechanganyikiwa kupita kiasi. Nilikuwa naangalia lakini sioni kitu. Ikawa giza tupu.” “Ndio changamoto za maisha Bale. Unabadili tu gia, bila kusimama.” Wakacheka.

“Karibuni mezani. Kikao kihamie hapa. Chakula tayari.” Naya akawakaribisha. “Naona umefanya haraka?” “Bale alishapika. Nimepasha tu moto.” “Ooh! Nashukuru.” “Ila unampishi mzuri!” Akasifia baba Naya. “Aisee kweli! Ile chapati aliileta Naya jumamosi! Kama kabechi jinsi ilivyo chambuka!” “Ni mpishi mzuri sana. Kila siku Naya anakazi yakusifia chakula chake!” “Nimemwambia baba jinsi ninavyokula vizuri siku hizi huko kazini.” Yakaendelea mazungumzo hapo, mpaka Joshua alipoaga na kuondoka. Akaiacha hiyo familia na kicheko sio majonzi aliyowaachia Malon.

~~~~~~~~~~~~~~~~

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment