Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI&PESA! – SEHEMU YA 27. - Naomi Simulizi

MAPENZI&PESA! – SEHEMU YA 27.

 Alhamisi.

Furaha na utulivu ndani ya Naya vikarejea. Joshua alipoenda kumchukua asubuhi hiyo akashangaa jinsi mapokezi yalivyo mazito. Naya aliingia garini, kabla hajafunga mkanda, akamuwahi midomo nakutoa busu zito la alfajiri hiyo. Kisha akamkumbatia Joshua akiwa amekaa palepale kitini. Akatulia hapo akiwa amemkumbatia. Joshua akacheka taratibu kwa furaha. “Naona hii siku imebarikiwa zaidi ya zote nilizokwisha ishi hapa duniani!” Joshua akaongea taratibu
akiwa bado amekumbatiwa. “Nakupenda Joshua. Nakupenda sana.” “Na mimi nakupenda Naya. Nimefurahi sana.” Naya akambusu shavuni na kumuachia. Safari ya kuelekea kazini ikaanza.

Jioni nayo akamrudisha nyumbani wakizungumzia mambo mengine kabisa. Hakutaka kurudia kabisa mazungumzo ya mambo ya ndoa ila kumfurahia Joshua kama Joshua na yale anayompa. Heshima aliyoirejesha kwake na upendo wa dhati. Naya akajionya kutoanzisha kitu chochote kitakachowopotezea amani. Akajiambia japokuwa anatamani sana ndoa, lakini atasubiri. Akapoa kabisa na kuendelea kumfurahia Joshua.

 Walipofika nyumbani kwao akatoa habari njema kwa baba Naya. “Nimezungumza na GM mwenyewe. Amesema kesho mida ya saa nne unaweza kufika kwenye ofisi zao pale Ubungo, mkazungumza. Nikijana mdogo tu, mtulivu sana, lakini kama nilivyokwambia, amefanikiwa sana. Ukiweza kumuweka sawa huyo, ujue ndio umeshafanikisha kila kitu. Muungwana sana na anaakili za upendeleo. Naomba fungua moyo kwa ushauri pia.” “Nakushukuru sana Joshua. Najua kukutanishwa na watu kama hao ni muujiza.” Wakacheka na kuendeleza mazungumzo. Usiku huo Joshua hakuzungumzia chochote juu ya Bale na hakuna aliyemuuliza wakijua anakumbuka juu ya maswala yake ya ajira. 

Ijumaa.

Asubuhi kama kawaida alikwenda kumchukua Naya. Ila safari hii akamsubiria nje ya gari. “Jana nilijipunja. Sikukupata vizuri.” Naya akacheka na kumkumbatia kwa haraka kwani alishajua anachokiongelea, akampokea vizuri. Ilikuwa bado tu ni giza. Peke yao nje ya nyumba ya kina Naya. Yaakanza mabusu kwa wawili hao tena bila haraka, Naya akiwa amejituliza hapo kama ametunikiwa ulimwengu wote! “Nakupenda Joshua.” Akamsikia akinong’ona huku akipitisha vidole taratibu upande aliokuwa amemshikilia wakati Joshua akimbusu na kumshikilia sehemu za shingoni akimchezea na nywele. Akamvuta mbele kidogo na kumwangalia. “Na mimi nakupenda Naya. Nakupenda sana mpenzi wangu. Umeondoa upweke kwenye maisha yangu.” “Hata mimi Joshua. Umerejesha amani na utulivu ndani yangu. Umenipa heshima ya hali ya juu. Nakushuru kwa kunivumilia tokea tunaanzana. Najua haikuwa rahisi. Lakini niliihitaji mtu kama wewe wakunivumilia mpaka nirudie hali ya kawaida kama binadamu wengine.” Joshua akacheka na kurudi kumkumbatia kidogo na kumfungulia mlango, Naya akaingia garini na Joshua naye akarudi kwenye kiti chake, safari ya kuelekea kazini ikaanza.

Jioni akamrudisha na kumkuta baba Naya amejawa furaha haswa. “Naona mambo yamekwenda vizuri. Geb amekusifia sana.” Baba Naya akacheka. “Na yeye mwenyewe amekusifia sana. Nilibahatika na kumuona mkewe, Nanaa. Ni binti mzuri sana. Wanatamani sana kumuona Naya. Lakini nikawaambia hafanani na mimi hata kidogo. Naya anafanana na mama yake.” Naya akashangaa. “Wanaharaka hao! Nanaa ndio msumbufu zaidi.” “Na yeye ndiye aliyekuwa akitaka hata picha ya Naya.” “Nilijua tu ni yeye.” Joshua akaongeza na kucheka kwa pamoja.

“Na mimi nimewakatalia wote na mama yao, nimewaambia watakuja kumuona Naya mwenyewe, kabla ya picha. Naya akacheka akifikiria. “Ila ni kweli ni watu wazuri sana na bado ni vijana wadogo tu. Halafu ni kweli wamefanikiwa kupita kiasi. Geb mwenyewe alinitembeza kwenye hilo jengo zima, akanionyesha mifano ya vitu wanavyofanya, hakika anayo akili yakuzaliwa.” Akasifia baba Naya.

“Amenishauri nisianze na kitu kimoja, kitanichelewesha na ninaweza kukwama. Ameshauri pia kufikiria mkaa. Amesema ni biashara ya mama yake, ila anajua inamlipa sana. Amesema niweke hata banda dogo tu nje, nichukue majunia machache niuze, pamoja na mafuta. Amesema uzuri wa mkaa, hauhitaji uwekezaji mkubwa, ni banda tu lililofunikwa vizuri na vifaa vya kupimia kwa kuanzia, ila baadaye kuanza kuuza kwa junia. Pamoja na mafuta halisi. Ameshauri upande wa mazao nisianze mchele tu, nifanye pamoja na maharage, na hivyo vyote anasema anaingiza hapa mjini kutoka mashambani, na anapitisha hapahapa kwetu, au tuseme pale Kibaha. Kwa hiyo amesema nikiwa tayari, nimwambie ili awaambie madereva wake waanze kushusha. Lakini Joshua!” “Ndiyo mzee.” Baba Naya akacheka kwa kuguna huku akifikiria.

“Yule kijana anajua anachokifanya! Anaujua mchele kwenye junia kwa mahesabu mpaka shilingi ya mwisho! Akikupigia mahesabu ya gunia moja, kuanzia kwa kipimo kidogo mpaka kikubwa, pesa utakayoingiza, gharama utakayowekeza mpaka muda wako wa kusimama wewe mwenyewe na kumuuzia mteja!” “Baba!” Naya akashangaa. “Hakika huwezi kuchezea hata shilingi moja. Kwanza aliniuliza swali lililonifanya nijisikie vibaya.” “Swali gani baba?” Naya akataka kujua.

Baba naya akajicheka. “Aliniuliza ninapanga kuingiza faida kiasi gani kwa mwezi wa kwanza. Hilo ni swali la kwanza kabisa. Akasema akijua hilo, atajua jinsi yakunishauri ninze na nini. Hakika nilijisikia vibaya kwa kuwa sikuwahi kulifikiria hilo. Amenichangamsha na kunifanya nijue ni wapi nimekuwa nikikosea. Akaniambia yeye baba yake alimfundisha ni lazima kila mwaka unapoanza, awe anajua anataka kufunga na kiasi gani cha pesa. Anasema imemfanya kutobweteka. Haoni shida hata kuuza pipi, ili kupata shilingi ya kuhakikisha hiyo pesa inatimia kwa huo mwaka.” “Baba!” “Joshua anaposema amefanikiwa, amini wamefanikiwa. Mkewe mzuri sana. Watulivu, ni kweli utajisikia vizuri kuwa nao karibu. Wale ni watu wakuwaweka karibu.” “Afadhali kama mzee wangu kama umekubaliana na mimi juu ya hilo. Mimi nilihakikisha naomba urafiki. Huwezi kuharibikiwa ukiwaweka wale karibu.”

“Mimi mwenyewe amenichangamsha sana yule kijana. Sana. Tatizo tu ni mtaji. Ila amenipa mawazo mazuri sana. Mkaa wenyewe tu, hiyo biashara anayosema anafanya mama yake, amenipigia mahesabu, mpaka nikatamani nianze kesho!” “Safi sana.” Naya akanyamaza. Akapoa kabisa. Akajua wamerudi palepale kwenye tatizo la pesa. “Ila nakushukuru Joshua. Nimechangamka akili. Nilianza kuona nimezeeka. Lakini nimegundua jinsi hawa watu walivyofanikiwa, ufikiriaji wao ni tofauti kabisa na wengine. Jinsi yule kijana anavyozungumza, utaelewa ni kwa nini amefanikiwa vile.” “Na uzuri wake, ile juhudu ameweka mpaka kwenye ndoa yake.” “Hilo nimeliona.” “Kweli baba?” “Kabisa. Kama alivyosema Joshua, utafikiri ndio anataka kumchumbia yule binti. Kumbe ni mke wa watoto watatu!” Wakacheka.

“Na mwenyewe huyo Nanaa msafi sana. Amependeza sana. Halafu mcheshi, anaheshima. Kwa kweli ni vijana walionivutia.” “Nimepatwa hamu yakuwafahamu.” Joshua akamcheka Naya. “Bwana siku ile unaniambia juu yao nilikuwa na mawazo ndio maana. Ila sikuwapuuza.” “Basi ndio baba amewajua kabla yako.” “Na mimi nitawafahamu tu.” Joshua akatulia kidogo.

“Naomba kuwaalika nyumbani kwangu ramsi siku ya kesho.” Wote wakamwangalia kasoro baba Naya, yeye alitabasamu tu. “Mimi nataka kuja.” Akadakia Zanoyi. “Kesho saa ngapi?” Naya akauliza. “Kuanzia saa 11 jioni sio mbaya. Na kina Magesa watakuwepo, pamoja na wageni wachache. Nimewaalika kwa chakula cha jioni.” Naya akatulia kidogo kama anayefikiria. “Vipi?” “Acha nitazungumza na baba kwanza, kisha nikujibu Joshua. Ila tunashukuru kwa mwaliko.” “Karibu. Ni chakula cha jioni, na kutakuwa na marafiki zangu, ningependa na nyinyi kama watu wangu wa muhimu, wawafahamu au mfahamiane. Zaidi hao kina Magesa.” “Tena Nanaa, mkewe Geb ameniambia atakuwepo kesho na ndipo atanikutanisha na wajukuu.” “Wana watoto wazuri! Naona niache kuwasifia mpaka mkajionee wenyewe.” Wakacheka.

“Kweli. Naona mtaona nimewazidishia sifa. Lakini hakika pale Mungu amempendelea Geb. Mimi mwenyewe nimemwambia Geb, akaniambia hata yeye anajua, ndio maana hazembei kwa chochote zaidi kwa familia yake. Anasema siri ya alipo sasa hivi ni utulivu wa fikra, anaopata kwenye ndoa yake. Huwa ananiambia kabisa, nyumbani kukitulia, huna utakalofanya, ukashindwa kufanikiwa. Na anasema hamaanishi kufanikiwa kipesa tu, anamaanisha mafanikio ya mpaka nafsi. Kwamba na mtu wa ndani atastawi na kupata utulivu wa ndani. Na ni kweli. Geb ametulia kwenye ndoa yake. Hana papara, hata ukimkuta nyumbani, ametulia. Mama yao mcheshi mno na mkarimu. Naona niishie hapo.” Wakacheka sana. “Joshua na kina Magesa!” “Acha uje ukutane nao, ndio utanielewa. Ila naomba msikose kesho.” “Nitakujibu Joshua.” “Sawa.” Usiku huo nao Joshua akaondoka bila kuzungumzia chochote juu ya Bale wala kugusia maswala ya ndoa. 

Jumamosi.

Asubuhi hiyo nayo Naya alipoingia garini akakutana na Joshua mwimbaji haswa. “Ni mapema sana kuwa na furaha ya kiasi hicho Joshua bwana! Leo umeota ndoto gani?” Joshua akacheka sana. “Usicheze na Mungu wangu.” “Amefanya nini tena?” Naya akauliza huku wakielekea kazini. Hapakuwa hata na mazingira ya busu kwani Joshua alijawa furaha na kuimba kwingi. “Mimi naona mpaka uje ushuhudie mwenyewe. Nikikwambia unaweza ukaona nazidisha sifa.” Naya akacheka. “Hajuagi kunipunja.” “Joshua na Mungu wake!” “Ndio Baba yangu. Ananitengenezeaga njia, pasipo na njia. Halafu anapenda kupigana na watesi wangu. Hataki mwanae nitokwe jasho. Kila anayenisogelea, huwa namsemelea tu, halafu kimya, Baba yangu anawashughulikia kwa namna yake, na utukufu unabakia kwake, mimi nasonga mbele.” Naya akamwangalia na kucheka tu.

Joshua akarudia kuimba. Siku hiyo aliimba njia nzima. Naya akamuona amechangamka kweli. “Nisaidie basi Naya!” “Ni asubuhi sana Joshua jamani! Mimi ni mwimbaji, lakini si wa kabla ya jogoo kuwika.” Joshua alicheka mpaka machozi. “Naya!” “Kweli bwana Joshua. Wewe unachangamkaje asubuhi hivi! Kwanza leo jumamosi, mwenzio nguvu ya week nzima zinaniishia siku za jumamosi.” “Basi wewe kaa uburudike.” Naya akatulia kimya akimsikiliza akiimba mpaka walipofika kazini.

“Mbona sasa hujauliza kama tunakuja kwako jioni au la! Au hututaki tena wageni sisi?” Joshua akacheka. “Najua mtakuja tu.” “Hee! Kwa nini?” “Baba Naya sasa hivi anazungumza lugha moja na Geb. Na nimemwambia Geb atakuwepo, lazima amepata sababu ya kuwepo. Zayoni amesema anataka kuja.” “Na mimi?” “Wewe najua lazima uje kwa kuwa wageni wangu ndio wako. Lazima uwepo kukaribisha wageni. Bale naye najua nyinyi mkiwepo, na yeye atakuwepo. Sina wasiwasi.” “Joshua wewe ujue umeelewa vibaya! Baba amekataa.” Joshua akashituka mpaka Naya akamuona, akaanza kumcheka. “Nilitaka utulie kidogo, sio uwe umechangamka zaidi yangu!” Joshua akanza kucheka. “Furaha hii huwezi kushindana nayo Naya. Hata kwa kunitisha.” Wakashuka garini.

“Lakini ulitishika kidogo.” “Hapana. Baba Naya na mimi tunaelewana!” “Nyie Joshua anavyojiamini!” “Nimepewa kibali na Mungu Naya. Acha wivu.” Joshua akaendelea kuimba. “Leo Fina na Jema watakoma.” Joshua akacheka sana, huku akimsindikiza ofisini kwake. Akamuwashia taa. Alipomuona amekaa, akatoka akiimba. “Wala sio vizuri! Bado ni mapema sana.” Akamsikia Joshua akicheka huku akiondoka. Naya akabaki akicheka.

~~~~~~~~~~~~~~~

Naya akaanza kusikia minong’ono ya kulalamika kwa wengine kutoalikwa nyumbani kwa Kumu siku hiyo jioni. Akabaki ameinama akisikiliza. Walikuwa wakimlalamikia Jamal kuwa Jema hajawapa na wao mualiko. Walisimama karibu sana na sehemu ya kuingilia hapo. “Jema ametubania tu!” “Mimi ameniambia amepewa nafasi za watu watano tu. Sasa kila mtu analalamika, angemchangua nani na kumuacha nani? Mngemuelewa Jema.” “Jamal anaongea hivyo kwa kuwa yeye kapata mwaliko. Sasa kulikuwa na ulazima gani kukaribisha watu wa vitengo vingine wakati sisi watu wake Kumu tupo?” Naya akashangaa sana jinsi wanavyolalamikia kualikwa nyumbani kwa Kumu!

“Wewe umezoeana na Naya. Muombe basi amuombe Kumu nafasi hata 3 tu nyingine! Jema amesema yeye...” Jamal akasikika akicheka huku akikataa. “Mnataka nigombane na Kumu! Yaani Kumu aje ajue nazungumza na mwanamke wake mambo kama hayo zaidi ya kazi! Naheshimiana sana na Kumu. Tafadhali msiniharibie. Anayetaka, amfuate Naya mwenyewe.” Jamal akaondoka. “Twende tumfuate Naya sisi wenyewe, Chege.” “Wee! Mimi mwenyewe sitaki matatizo na Kumu. Kama Jema kaamua kutuacha, basi.” Naya akakunja uso asielewe. Akageuka kuangalia ni kina nani, akakuta ofisi nzima wanamtizima yeye. Naya akakunja uso kama anao washangaa. Alipoona kimya akageuka na kuendelea na kazi zake.

 ~~~~~~~~~~~~~~~

“Mzima Naya?” Naya akageuka akamkuta Jema amemsimamia kwenye meza yake. “Mimi mzima. Kwanza asante kwa pafyumu. Joshua ameniambia wewe ndio ulinunua.” “Umeipenda?” “Nzuri.” Jema akacheka. “Mbona kama sio sana?” “Sio mbaya. Niambie.” “Kwanza niambie juu ya pafyumu.” Naya akacheka. “Ila nimekushukuru kwanza.” “Wewe niambie usijali, ili siku nyingine nisikosee.” Jema akaweka msisitizo. “Ila usimwambie Kumu. Mimi huwa situmii pafyumu zenye citrus. Napenda aina za woody.” Jema akatoa macho nakumfanya Naya aanze kucheka. “We Naya! Ndio nini?” Naya akazidi kucheka.

“Mimi naona hilo zoezi la pafyumu tuje tulifanye wote. Na mimi nijifunze. Maana mimi nachukua kutokana na bei na nikivutiwa na harufu.” “Basi tutakuja kulifanya hilo zoezi siku moja. Mimi ni mpenzi sana wa harufu nzuri. Na ninazijua pafyumu kwa harufu.” “Ndio maana hujaitumia?” Naya akacheka.

“Basi nipe mimi Naya.” “Siwezi kukupa kwa kuwa imetoka kwa Joshua.” Jema akacheka sana. “Naya!” “Kweli. Hata yeye usimwambie. Nimefurahia sana kuona amenifikiria na kuniletea.” “Ila siku nyingine nitaenda kununua mimi mwenyewe, aina ya woody.” Wakamsikia Joshua akijibu. Naya alishituka mpaka akasimama, hawakujua kama alikuwa akisikiliza. “Jumatatu tutakuletea pafyumu yako Jema. Haya, naomba tupishe.” Jema akacheka sana. “Tusiigawe bwana!” “Sasa utaiweka mpaka lini? Mpe tu Jema, tutatafuta nyingine, na wala sijaumia.” “Kweli Joshua?” “Kweli. Kwanza nimefurahi kujua aina ya pafyumu unazopenda. Sikuwa nikijua ndio maana nikamtuma Jema wakati akijinunulia vitu vyake, nikamuomba akununulie pafyumu nzuri. Basi. Hata sikumwambia aina gani.” Naya akacheka kwa aibu akamwangalia Jema.

“Sasa sio tumeagana kule, halafu uje huku umgande tena Naya. Natoka naye, kwa hiyo changamka Jema. Malizana naye utupishe.” “Kwani kuna kitu ulitaka kuniambia?” Naya akamuuliza Jema. “Tena nilitaka kusahau!” Jema akawa kama amekumbuka. “Huwa unapenda keki aina gani?” Naya akakunja uso na kumwangalia Joshua. “Mbona unaniangalia mimi badala ya kujibu?” Joshua akamuuliza akicheka. Naya akababaika kidogo akifikiria kisha akajibu. “Yeyote ile.” “Kweli Naya?” Joshua akaingilia kwa swali. “Kweli, kwenye keki si mchaguzi. Unataka kuniletea keki, Jema?” “Kwa kuniletea ile pafyumu jumatatu, nakuletea keki.” Naya akacheka, Jema akaondoka.

“Upo tayari? Nilikwambia leo tunawahi kutoka.” “Sijamaliza jambo moja, Joshua. Wewe tangulia.” Joshua akaweka mikono mfukoni na kusimama vizuri akimshangaa kabisa. Naya akacheka. “Basi kaa hapo nisubirie nimalize, nisiharibu kwa Jamal.” “Naya!” “Sikawii. Kuna kazi imechelewa kuingia, nimeona niifanye tu mwenyewe. Kaa basi nimalizie mara moja.” “Ni nini?” “Njoo uone.” “Hapana bwana! Kwa nini umechukua kazi mpya wakati nilikwambia tunawahi kutoka!?” “Hivyo unavyolalamika, ndio tunazidi kuchelewa.” “Nikupe dakika ngapi?” “13 tu.” Joshua akaangalia saa. “Naomba isizidi Naya. Na usiongeze kazi nyingine. Wagawie wenzio wafanye. Leo nakutaka mapema.” “Hapo dakika imeshaisha tena.” Joshua akatoka bila kuaga, Naya akamcheka. “Nashukuru kwa laptop kiongozi. Nimepewa mpyaa!” Akamsikia Jamal akipaza sauti “Ianze kufanya kazi.” Joshua akasikika akiwa anapotelea koridoni. “Utaona matunda yake.” Joshua hakusikika akijibu tena.

~~~~~~~~~~~~~~~

Walitoka hapo saa sita kamili mchana. “Leo jikaze uje kula nyumbani. Wataandaa chakula kizuri sana.” “Sasa wewe husikii njaa?” Naya akauliza kwa kujali. “Nipo sawa. Kwanza mwenzio mchana si mlaji sana. Mara nyingi nakuwa na kazi.” “Sasa tutafikaje nyumbani kwako? Mimi sijawahi kufika huko Goba.” “Nitakuja kuwachukua mimi mwenyewe. Saa kumi na nusu nitaomba tuwe tunaondoka nyumbani ili wageni watukute tumeshafika Goba, sisi tukiwasubiria. Tuwakaribishe.” “Wageni wenzetu wanaanza kufika saa ngapi?” Joshua akacheka. “Wakifika wao saa 1 usiku, watakuta wewe umeshakuwa mwenyeji, unawakaribisha tu.” Naya akacheka. “Sawa. Utatukuta wote tayari.” Joshua akaanza kuimba tena. Naya akabaki akicheka.

“Umefanya kazi kweli wewe leo?” “Sana. Nimekuwa na masaa 4 ya mchakamchaka, nikikomboa wakati. Nashukuru kila kitu kilienda kama alivyopanga Jema.” “Jema anaonekana anaijua kazi yake, eeh?” “Na anaipenda sana. Ndicho anachonifurahisha. Si mlalamishi hata kidogo, ila mtu wa kutafuta suluhu. Hata kama atashindwa, ujue amejaribu. Halafu mwepesi wa mambo. Ukimwambia unahitaji kumuona au kuzungumza na mtu fulani, hata awe nani, atahangaika mpaka aniunganishe na huyo mtu, tena bila kuchelewa.” “Anaonekana. Hata tembea yake ni kama anakimbia kwa haraka.” Wakacheka, Joshua akaanza kuimba tena. Naya akabaki kimya akimsikiliza na kucheka mpaka wakafika nyumbani kwa kina Naya, Kiluvya.

Hawakumkuta mtu. “Hawa watakuwa hawajarudi. Baba aliniambia walikwenda kukata nywele.” “Acha na mimi nikasafishe kichwa changu.” “Ila nikwambie ukweli Joshua.” “Niambie tu.” “Wewe ni msafi mpaka unavutia.” “Kufanyaje?” Naya akacheka sana. “Joshua!” Joshua akaanza kucheka. “Asante Naya. Nimefurahi kusikia hivyo haswa kutoka kwako. Inaniongezea ujasiri.” “Kwani ulikuwa hujui?” “Hata wakisema watu 1000, lakini sio wewe, kwangu haileti maana kama wewe ukisema.” “Jamani Joshua wangu! Basi ujue wewe ni mzuri na unavutia.” “Naona na sifa imeongezeka.” Naya akacheka. “Asante mpenzi wangu.” Akamsogelea na kumbusu shavuni.

“Upendeze sana leo. Mwenzio nitapendeza.” “Sitakuangusha Joshua.” “Ni kwa ajili yako mwenyewe. Sitaki uje ujisikie vibaya. Mimi sitajali hata nikikuona hivyohivyo.” “Basi nitajiwakilisha vizuri. Usijali.” Joshua akambusu tena shavuni na kutoka kwa haraka.

Kwa Mara ya kwanza Naya Nyumbani kwa Joshua, akiwa na Familia Yake.

Saa 10:20 jioni hiyo Joshua akawa ameshawasili nyumbani kwa kina Naya. Akakuta wote wapo tayari, ila Naya tu alikuwa chumbani, ndugu zake walikuwa wakisubiria sebuleni. “Umependeza sana Joshua!” Naya akamsikia baba yake akimsifia. “Asante mzee wangu. Hata nyinyi mmependeza. Mnaweza kutangulia tu kwenye gari. Nimeacha wazi.” Wakatoka na kuwaacha ndani. Joshua akimsubiria Naya. “Namalizia Joshua.” “Sawa.” Joshua akawa mtulivu tu akisubiria. Naya hakuchukua muda mrefu akatoka na kumfanya Joshua abakie mdomo wazi.

“Naya!” “Nimejiwakilisha vizuri?” Naya akawa akigeuka akicheka. “Nikwambie siri ya hii nguo?” “Tukiwa tunaondoka.” “Basi acha nifunge mlango.” “Umependeza sana, mpaka natamani ungesema unaniwakilisha na mimi!” Naya alicheka sana. “Unaumbile zuri na imekukaa vizuri kwa heshima na kufanya uvutie vizuri SANA.” “Asante. Niliipenda sana hii nguo lakini nikawa sina pesa. Alikuwa akiuza Madamu Vane, yule mama nilikusimulia habari zake, niliyekuwa nikimfanyia kazi tokea nipo sekondari. Nikamuomba asiiuze, anitunzie ila awe ananikata kidogokigogo mpaka nikamaliza. Na aliniuzia kwa bei kubwa sana. Sikuwahi kupata sehemu ya kuivaa, ndio leo naivaa rasmi kwa mara ya kwanza. Nilikuwa nikiivaa tu chumbani nikiwa nina mawazo. Najizungusha kwenye kioo mpaka niridhike ndipo naivua na kuirudishia kwenye mfuko wake.” Joshua akacheka huku akimsaidia kufunga mlango.

“Hiyo nguo kweli ina uwezo wakukutoa mawazo.” “Na wewe umependeza sana.” “Wewe ukisema, ndio najisikia vizuri.” Naya akacheka akimwangalia na kumtafakari Joshua vile anavyomuonyesha anamjali na kumuhitaji. “Sasa mbona haonyeshi kutaka kunioa?” Naya akawaza wakati wakielekea kwenye gari.

“Hivyo ulivyopendeza, naomba heshima ya kukufungulia mlango wa gari.” Walikuta wote wamesimama nje ya gari hawajaingia ndani ya gari wakiwasubiria. Naya akacheka na kumpisha. “Lakini baba ndio atakaa mbele. Mimi nitakaa nyuma.” Naya akamnong’oneza Joshua, akaelewa. “Sawa.” “Akamfungulia mlango wa nyuma ya dereva. Akapanda, Joshua akamfungia mlango, ndipo wengine nao wakapanda garini, wakimpisha baba yao kiti cha mbele. Safari ya Goba ikaanza. “Mjiandae kwa safari ndefu kidogo. Pana umbali!” “Nilihisi tu, ndio maana huwa nakushukuru kuja mpaka huku asubuhi na jioni, Joshua. Kweli nakushukuru.” “Usijali kabisa mzee wangu. Huwa tunapata muda mzuri sana njiani.” Naya akacheka na kunyamaza. Joshua akaendelea kukanyaga mafuta.

“Vipi Bale?” Bale alikuwa kimya sana. Joshua akavunja ukimya. “Nipo tu.” “Safi sana na Zayoni?” “Mimi naendelea vizuri. Gari yako safi!” Wote wakacheka. “Asante Zayoni. Lakini unaonekana unapenda vitu vizuri!” “Sana. Nikiwa na hela nitakuwa nanunua vitu vizuri halafu nakuwa msafi. Hata nguo zangu huwa zinakuwa safi, muulize Naya. Sirudii nguo mara mbili. Nikivaa mara moja, basi. Hata kama hainuki jasho, nafua.” Zayoni akajisifia nakufanya wacheke. “Halafu mimi sio mvivu wakufua.” “Safi sana. Unaonekana pia kama ni msafi.” “Na wewe umeniona kama na mimi ni msafi!?”  Akamuuliza Joshua, wote wakacheka. “Usafi huwa haujifichi. Unaonekana kabisa kama ni msafi.” “Asante. Basi Naya huwa ananinunulia mashati meupe kama mama. Mama naye alikuwa akininunulia nguo nyeupe kwa sababu anasema mimi huwa sijichafui. Nabakia msafi.” Wakaendelea kucheka.

“Kwa hiyo wewe kila kitu chako nikisafi?” Zayoni akamuuliza tena Joshua. Joshua akacheka. “Ninafanya juhudi za makusudi kila kitu changu kiwe kisafi. Na nimtunzaji pia kama wewe. Huwa namwambia Naya, huwa nakuwa na vitu vichache, na huwa navitunza vizuri. Huwa nahakikisha kila kitu changu kinajua kama ni changu na ninakitunza vizuri, hata kama ni soksi tu.” “Basi na mimi nataka kuwa hivyohivyo.” Zayoni akaongeza. Alionekana mkimya lakini akitaka kuzungumza, huzungumza haswa.

“Basi na Zayoni yupo hivyohivyo. Msafi na mtunzaji sana. Pale nyumbani ndio mfano wetu.” “Asante Naya. Na Bale pia huwa ananisifia, si ndiyo Bale?” “Kabisa. Wewe mtunzaji. Ndio maana huwa naona shida kukaa hata kitandani kwako, naona bora kitandani kwa Naya kuliko kwako.” Wote wakacheka. “Zayoni anatandika mashuka meupe kitandani kwake!” Naya akaongeza. “Na akitandika utafikiri amepiga pasi hicho kitanda kwa jinsi kinavyo nyooka!” Bale akamsifia tena. Baba yao akabaki kimya tu. 

 Nyumbani kwa Joshua.

Kwanza wakavutiwa na huo ukuta. Gari zima likatulia. “Baada ya safari ndefu hatimaye tumefika. Karibuni.” Hakuna aliyeitika. Wakashangaa, geti linajifungua taratibu. Wanakaribishwa na madhari nzuri sana ndani. Kila mtu macho yakamtoka. “Haaaa!” Akasikika Zayoni ambaye huwa hawezi kuficha hisia zake. “Karibuni sana.” Naya alipoa kutoka moyoni. Akavuta gari mpaka sehemu yakuegeshea magari. Kulikuwa na gari nyingine. Haikutofautiana sana na hiyo anayoendesha, ila yenyewe ilikuwa nyeusi. Ilionekana bado mpya.

“Na hiyo pia ni gari yako!?” Akauliza Zayoni. Joshua akacheka. “Ndiyo Zayoni. Lakini ni ya muda mrefu, huwa siitumii.” Akashuka na kuwakaribisha tena. Akamfungulia Naya mlango. Akashuka akiwa amepoa haswa. “Vipi Naya?” “Hukuniambia kama unaishi kwenye hoteli ya kifahari hivi!” Joshua akacheka sana mpaka akainama. “Naya!” “Kweli tena. Sasa hapa hata ukija kuoa, huyo mkeo anaanzia wapi kupaita hapa na yeye ni kwake!?” Hilo lilimshitua sana Joshua maana Naya hakuonekana kutania.

Alionekana kuishiwa nguvu kabisa. “Kweli Joshua. Huyo mwanake anakuwa anaanzaje kupaita hapa nyumbani!?” Naya akasikika waziwazi kuwa amekata tamaa. Ndugu zake wote walimsikia, japo alizungumza kwa sauti yachini. Joshua akawa kama na yeye amekosa chakusema. Akapoa kabisa. Kisha akawa kama amegutuka. Akawegeukia wengine ambao walikuwa wakisiliza lakini macho yakiendelea kupata fahari yake. “Karibuni jamani. Karibuni ndani.” “Asante Joshua! Kwakweli umejijenga vizuri sana. Hongera sana!” “Nashukuru mzee wangu.” Akamgeukia Naya ambaye alikuwa amepoa, ameegemea gari kama aliyekwisha kata tamaa kabisa kama anayejishauri hata kuingia ndani. “Ndio maana anashindwa kuoa! Unaingizaje mwanamke tu kwenye maisha kama haya!” Naya akaendelea kuwaza na kumsahau Kumu anayenunuliwa na makampuni makubwa kwa mamilioni ya pesa. Alifikiri zile nyumba za Malon ndio amemaliza, anakuja kukutana na mjengo wa hatari wa Joshua, aliyekuwa ametulia tu, tena mnyenyekevu!

“Naomba tuingie ndani, Naya.” Akashituliwa na Joshua aliyemshika mkono kabisa. Naya akatoa tabasamu, lakini Joshua aliliona halikuwa halisi. “Twende.” Akamvuta kidogo huku akiwa kama anambembeleza. Joshua alijua Naya amepaniki. Mazingira ya nyumbani kwao yalikuwa ya kawaida sana. Vyumba vidogo haswa. Mtu akiwa chumba chochote humo ndani, unasikia yote yanayoendelea sebuleni. Sebule yenyewe hawawezi kukaa watu wengi kwa wakati mmoja jinsi ilivyojibana halafu ikawekwa na meza ya chakula hapohapo karibu! Vyumba vitatu tu, tena sakafu ya kawaida sana, madirisha ya nondo, wavu, na mbao, wamemaliza. Jiko, walipikia nje na kuingiza chakula ndani.

Haya, akakutana na Malon ambaye kwake aliona ni kiwango cha juu sana, akaona kuna mwanya hata wakuja kujijenga naye zaidi. Kwamba wakapambana na kujijenga zaidi na yeye Naya akihitajika. Lakini kwa Joshua ni kama alikuta amekamilika kabisa! Kwenye upande wa kazi, yupo kiwango cha juu kabisa. Hakuna pa kupanda zaidi, amefika mwisho. Kwa Mungu wake, ametulia. Hana papara, Naya hana chakuongeza hapo kumjenga. Joshua anamfahamu Mungu, na anaitambua nafasi yake kama yeye ni mwanadamu, na Mungu ni wakutogusa utukufu wake. Haya, upande wa maisha, amekutana na huo mjengo wa nguvu, ambao kwa nje tu macho hayakuwa yametosheka. Gari ya maana, na nyingine ya kifahari ipo tu nje na bado kwa wadhifa wake, anatakiwa awe anaendeshwa kila mahali. Akaishiwa nguvu kabisa. Akatangulia akiwa amemshika Naya mkono.

“Naomba usinikatie tamaa.” Hayo maneneo ya Joshua yakaingia mpaka moyoni kwa Naya kama aliyekuwa akisoma moyo wake. “Siwezi Joshua.” Naya akajibu lakini Joshua hakusadiki. Akamtizama wakiwa wanatembea.

Mlango tu wakuingilia ndani ulikuwa wa kushangaza. Waliingia ndani wote kwa pamoja wakajikuta wanasema “Waw!” Wakasimama kwa pamoja, nakuduaa, macho juu wakiangalia huo muundo wa wazi, uliopanda hapo katikati kwa ustadi wa namna yake, ukajivuta kwa namna ya kuvutia mpaka kufikia dari ya kioo juu kabisa gorofani. Hiyo dari huko juu ilikuwa ya muundo wake na kona zenye ncha maridadi, nzuri sana. Likashuka rembo kubwa sana. Kutoka juu mpaka katikati hapo sebuleni lenye mataa mazuri sana. Ngazi ilizungushiwa kioo kizuri  chenye maua mazuri mno ya dhahabu kuzunguka hivyo mpaka kufikia vyumba vya juu. Vyumba vya juu vilizungushiwa uzio wa thamani sana nao ni kioo kama kilichotoka chini kabisa kwenye ngazi ya kwanza mpaka juu ila kulikuwa na vyuma vya urembo pia. Naya akavuta pumzi kwa nguvu na kurudisha macho kwa Joshua. Akakuta Joshua ametulia akimwangalia yeye. “Chooni ni wapi?” “Twende nikupeleke.” Akamshika mkano. “Karibuni mkae tu kwenye makochi, tutarudi sasa hivi.” Joshua akaaga. Yeye na Naya wakaondoka.

Akamvuta Naya kwenye kona. “Naomba niambie wasiwasi wako Naya. Tafadhali.” “Hamna wasiwasi. Ila nilitaka kutumia choo.” “Sio kweli Naya. Ulitumia choo kabla hatujatoka nyumbani.” Naya akavuta pumzi kwa nguvu. “Uliniruhusu nikutambulishe kwa watu. Nimeita watu leo, nikijua tutakuwa upande mmoja. Naomba usinigeuke sababu ya hili jengo, tafadhali Naya.” Naya akacheka taratibu akiangaza macho. “Naya?” “Mimi nipo na wewe.” “Mimi nitasimamia hapohapo. Naomba toa hiyo hali iliyokuingia gafla, changamka, nisaidie kuweka mambo sawa, ili wageni watakapofika tuweze kuwapokea vizuri. Nanaa ameniahidi watawahi kidogo ili kunisaidia yeye na mama yake, ni mara yangu ya kwanza kualiaka watu hapa. Sina uzoefu na chochote ndio maana nilitaka na wewe uwahi. Unafikiri unaweza kunisaidia?” “Unataka nifanye nini?” “Hayo ndio maneno. Cha kwanza twende tukaangalie sehemu waliyotayarisha kwa ajili ya chakula. Kisha unishauri.” Wakawaona wanapita upande wa pili.

Joshua akafungua mlango mkubwa sana ulikuwa juu kidogo pakawa kama holi. Napo hapo akampoteza tena Naya. “Naomba punguza hiyo hali Naya, tuandae mazingira mazuri kwa wageni.” Naya akacheka. “Joshua!” “Usifikiri nimejenga jumba lote hili kama kufuru! Au kwa kuwa sina pakupeleka pesa! Nina maana yangu Naya. Kumbuka historia ya maisha yangu. Nimekuwa mtoto wa mtaani nikiteseka. Mama yangu amefia nyumbani kwao wakimnyanyasa. Kweli unataka mke wangu na watoto waje waishi au wapite kule ambako mimi nimepitishwa nakuona ni hatarishi! Nimefanya hivi kwa ajili ya familia yangu. Nawazia familia yangu na ukoo wangu kwa jumla kwa kuwa najua Mungu atanibariki tu uzao. Sasa natamani hata vijukuu na vitukuu wapate kwao. Wajue hapa ni kwao maana mimi sina ndugu, ndio mimi tu niliyesimama hapa. Yaani mimi ndio nitakuwa muanzilishi wa ukoo wangu. Ndio maana hata eneo huko nyuma pia ni kubwa sana. Nimenunua heka nyingi sana, kwa makusudi kabisa, sio kufuru.” Joshua akajikuta akijitetea.

“Nimekuelewa Joshua. Na hongera. Sema nimepatwa tu na mshituko. Sikuwahi kuingia kwenye mazingira ya namna hii tokea nazaliwa! Wewe unajua mazingira yetu. Na nimewahi kuingia kwenye majumba mazuri, lakini sio kama hivi!” “Najua ni ya kipekee. Na haipo hivi kwa bahati mbaya. Nimekwambia niliijenga nikiwa naangalia mbali sana. Na ninataka hii nyumba ibebe historia kubwa ambayo Mungu akijalia, isimuliwe kwa kizazi hadi kizazi ndio maana unaona hata kuna huu ukumbi. Nitakwambia zaidi baadaye. Sasa hivi nisaidie kuandaa.” “Sawa.”

Wakaingia ndani. “Nasikia harufu ya vyakula!” “Wanakaribia kumaliza kupika. Nanaa amenitumia dereva na hivi vyombo.” Akamuonyesha vilikuwa kwenye maboksi. Naya akavutiwa na hivyo vyombo. “Sijawahi kualika mtu hapa. Yaani hata vyombo sikuwa navyo. Nanaa alitaka tukodishe, lakini sikutaka wageni wangu waje nyumbani kwangu, watumie vyombo visivyo vyangu. Ndio akaniambia ataninunulia, wataniletea.” “Vinaonekana ni vizuri sana na ni vya hali ya juu.” “Vyote hivyo wamenipa zawadi, kasoro glasi na vijiko ndio nilimwambia nitamsaidia.” “Mnaonekana mnaelewana sana na Nanaa.” “Sana. Utampenda tu akija. Amesema hatachelewa. Ila kwa kuwa wewe umekuwa wa kwanza hapa, naomba ndio umkaribishe. Tafadhali Naya. Isiwe yeye ndio anakukaribisha hapa.” “Sasa sijui yeye alikuwa na mpango gani na haya yote!” Naya akasita.

“Chakwanza ujue yeye hapafahamu kabisa hapa. Mimi nilimtuma tu vyombo, akamtuma dereva. Naomba wewe shika usukani.” Naya akaangalia ule ukumbi. Alishakuwa na uzoefu wa kuhudumia kumbi. Meza zilikuwa nzuri, zinavutia. “Chakwanza, kwa aina hizi za meza zako, naona ni kosa kuzifunika. Huo muundo hapo juu naomba uonekane.” “Hayo ndio maneno.” “Naomba nimuombe Bale na Zayoni wanisaidie. Tuoshe hizo sahani tuzipande pamoja na napkins.” “Ngoja nimwite Josee akuletee napkins. Alininunulia za rangi nyekundu pamoja na cream, akasema atatusaidia kukunja.” “Si atakuwa busy na mapishi?” “Ana watu wanne wanao msaidia. Usijali.” Naya na ndugu zake wakaanza kazi hapo ukumbini. Alitoa kabisa kiatu cha juu akafunga nywele alizokuwa ameziachia, akazifunga juu pamoja. Akaendelea na kazi kama mwenyeji haswa. 

Magesa. 

“Twende tukawapokee kina Magesa. Wamekuja.” Joshua akamfuata pale ukumbini. “Unapaonaje?” “Sikutegemea! Nimekwambia lakini Naya. Umepapendezesha sana. Na sitaki mtu aguse tena. Patabakia hivyohivyo.” Naya akacheka. “Nimefurahi kama umependa. Twende.” Walimkuta baba Naya amekaa hapo sebuleni kimya kama hayupo, na glasi ya juisi pembeni. “Baba Naya.” Naya akamwita. “Pole nimekuacha peke yako baba yangu, namalizia.” “Hutaki nikusaidie?” “Namalizia. Acha nikawakaribishe kina Magesa.” Naya akamfuata Joshua nje.

Naya alikutana na viumbe ambavyo vilimfanya atoe macho. “Hawa watoto wamewatoa wapi!?” Nanaa alikuwa akimtoa mtoto mmoja upande huu na mwingine Geb akitoa mtoto mwingine. “Salimia bwana Liv, ni nini?” Alikuwa mama G. Joshua akacheka. “Nisalimie basi Liv.” “Huyo ndio anti Naya?” Akauliza Liv akicheka. Wote wakacheka. “Huyo ndiye Naya. Njoo msalimie basi.” Joshua akamnyooshea mkono. Akamshika Joshua na kumchungulia Naya. “Mimi naitwa Liv, binti Magesa. Shikamoo.” Naya alicheka sana. “Jamani binti Magesa! Marahaba. Nimefurahi kukufahamu, nimesikia habari zako nzuri tupu!” Akacheka tu na kujificha kwa Joshua. “Mimi hujanisalimia Liv.” “Nimekusalimia kwenye simu anko. Unataka tena?” Liv akamuuliza Joshua akicheka. “Mimi sikumbuki.” “Na mimi anko. Na mimi!” Alikuwa Magesa.

“Tulia bwana Magesa! Hujapitwa na chochote.” Mama yake akamtuliza. “Na mimi anko.” Naya akawa hajaelewa. “Shikamoo.” Akamsalimia mama G, akaona wanaangaliana na Nanaa, nakuanza kucheka. Geb akatingisha kichwa akicheka. “Wewe mama ungeitikia salamu ya Naya kwanza.” Geb akamwambia mama yake wakati wakicheka na Nanaa kishabiki. “Naya Kumu!” Akadakia Nanaa akiendelea kucheka. “Kwani niliongopa?” Akauliza Joshua. “Hakika hujaongopa Joshua mwanangu.” Mama G akaitika akicheka na kumsogelea Naya. “Sifa zako mama, zimejaa huko kwetu, mpaka dada yake Jimmy ameomba tukupige picha tumpelekee, tumbo linamuuma, ameshindwa kuja.” Naya akacheka kwa aibu na kumtizama Joshua kama asiyeelewa.

“Joshua ameniambia juu yenu. Naamini huyu ni...” “Sasa hapo subiri Naya. Ukitaka kuwe na amani, mwache baba mzazi mwenyewe atoe utambulisho. Hapo mtapatana.” Naya akacheka lakini akawa hajaelewa. “Haya, Magesa. Anti Naya anasubiri.” Nanaa akamwambia mwanae. Akacheka kwa furaha. “Mimi hapa naitwa Magesa Magesa. Mimi ndio kaka mkubwa, Magesa mwenyewe.” Naya akacheka. “Hajamaliza.” Nanaa akamtahadharisha Naya. “Kumbe bado! Ehe?” “Huyu anaitwa Oliva Magesa. Dada mkubwa. Lakini bibi naye anaitwa Oliva Magesa. Kwa hiyo huyu dada mkubwa yeye anaitwa Liv Magesa, binti Magesa, kwa kuwa tuna Liv wawili.” Magesa alikuwa amechangamka, alionekana bado mdogo lakini anaelewa anachozungumza.

“Umeelewa anti? Usije kuchanganya.” “Nimeelewa Magesa. Na huyu?” “Huyu ni mdogo wetu. Anaitwa Jimmy Magesa. Tunampenda Jimmy. Si ndio mama eeh?” “Ndiyo.” Akamvuta na kumbusu. “Taratibu bwana Magesa, usimuumize!” Nanaa akamtahadharisha. “Nambusu tu.” Akarudia tena. “Hajamaliza utambulisho. Naomba mvumilie tu.” Nanaa akamnong’oneza Naya. “Nakupenda Jimmy. Umesikia?” Jimmy akatingisha kichwa kukubali. “Jimmy yeye hapendi kuongea kama Liv. Ila anasikia na kuelewa kila kitu. Na huwa anacheza na mimi. Huwa anaongea na mimi. Si ndio Jimmy, eeh?” Jimmy akatingisha kichwa kukubali. “Nakupenda Jimmy.” Akarudia tena wote wakiwatizama. Naya aliwapenda hao watoto akabaki akiwaangalia.

“Haya, huyu bibi yetu. Ananipenda sana mimi.” “Na mimi pia ananipenda.” Liv akadakia. “Ila mimi zaidi na Jimmy pia.” Mama G alikuwa akicheka huku akitingisha kichwa. “Mimi nawapenda wote.” “Ila mimi zaidi bibi.” “Wote zaidi. Haya maliza basi huo utambulisho mimi nikakae bwana Magesa! Nimechoka kusimama juani.” Bibi yake akalalamika. “Haya bibi. Halafu huyu hapa ni mami yetu. Anaitwa Nanaa. Hata dad anampenda.” Hapo walicheka wote. “Hajamaliza.” “Huyu ni dad wetu. Ila yeye sio Magesa Magesa kama mimi. Kwa hiyo usimuite Magesa. Wewe muite Geb. Mimi ndio Magesa.” Geb akatingisha kichwa akimwangalia. Wakacheka. “Halafu huyu ni anko wetu, anaitwa Joshua.” Walicheka tena. “Huyo anamjua bwana. Umesahau?” “Ninakumbuka. Ila nataka kuingia ndani.” “Sasa taratibu Magesa. Na usishike kitu mpaka tuje.” “Nisimame tu?” “Simama tu.” “Sawa mami.” Akaongoza njia.

Wakabaki wakicheka. “Mna watoto wazuri!” “Lakini muongeaji ni huyo tu. Hawa wengine ndio kama unavyowaona. Wapo kama mimi. Wamechukua upole wangu.” Nanaa akajisifia nakufanya wote wacheke. “Sasa wewe Geb unachocheka ni nini? Kwani uongo?” “Mimi nashauri ungemuacha tu Naya mwenyewe afananishe.” “Mimi namsaidia Naya. Atuelewe mapema. Kuna kundi la wapole na watundu. Sasa Magesa yule ni kama baba yake. Na hapo anakusubiria ndani akakueleze mambo yake ya utafiti. Sisi wapole.” Akijionyeshea yeye na kina Liv. “Mpaka hapo Naya kashapata jibu.” Mama G akaongeza. “Sasa mbona kama mimi sikuelewi mama!?” “Mbona mimi nipo upande wako Nanaa! Upande wa wapole.” Akajibu mama G nakufanya wazidi kucheka.

“Mwaya tumefurahi kukuona Naya. Tulikuwa tukisubiri hii siku kwa hamu kweli! Huyo Joshua alikuwa mpaka anaombewa kwa kushikwa mikono na mama!” Naya akacheka. “Na kweli subira imevuta heri mwanangu Joshua.” “Nilikwambia mama!” Wakaendelea kucheka wakionekana kumfahamu Joshua vizuri na kama wanajua wanachozungumzia zaidi, Naya akabaki akicheka tu akiwasikiliza. “Naya mama, karibu kwenye familia.” “Asante sana. Na mimi nimefurahi kuwaona. Nyinyi ni watu wa kwanza kuwasikia kutoka kwa Joshua. Alitaka kunileta jumamosi iliyopita, ila alikuwa safarini.” “Alituambia.” Akajibu Nanaa.

“Karibuni ndani.” “Asante.” Naya akasaidia kubeba mabegi ya watoto. “Umeona nilivyo na vifurushi! Kama msafiri kumbe watoto watatu tu!” Naya akacheka. “Dada yao mgonjwa. Alitaka sana kuja.” Akadakia mama G huku wakielekea ndani. Geb na Joshua walitangulia mbele yao kidogo tu. “Nashukuru kwa vyombo. Vizuri sana.” Joshua akamsikia Naya akishukuru, hilo likamfurahisha. “Afadhali kama umevipenda. Ni mama huyo. Mama anapenda sana vyombo. Tulienda naye, akanisaidia kuchagua vyombo vyote tulivyoleta.” “Nimeshaosha na kupanga. Twendeni mkaangalie mnishauri.” “Sawa.” Nanaa akakubali bila shida.

“Joshua!” Nanaa akamwita wakiwa wanatembea. Wakageuka pamoja na mumewe, Geb. “Bwana mjengo huu wa hatari! Au unasemaje Geb?” “Ndio nilikuwa nikimpa sifa zake. Sijawahi ona hii ramani! Anasema amebuni mwenyewe.” “Asante Nanaa.” “Hongera Joshua mwanangu. Ndio maana huwa nakusifia, Nanaa anasema nazidisha. Haya ndio maendeleo. Kitu kama hiki kinadumu kizazi hadi kizazi.” “Ametoka kuniambia hivyohivyo.” Naya akaongezea kwa mama G. “Asanteni sana. Nimefurahi mmekuja jamani. Karibuni ndani.” Wakaingia ndani.

“Shikamoo baba Naya.” “Marahaba Nanaa. Hujambo mama?” “Sijambo. Nimekuletea wajukuu wote. Umemuona huyo kaka mkubwa?” “Nimeshasalimiana na Magesa Magesa. Ameniambia baba yake nimuite tu Geb, ila kama ninataka kumuita kwa jina la Magesa, basi lazima niweke Geb ili kuwatofautisha.” Wote wakacheka. “Amesema dada mkubwa anaitwa Liv, na kaka mdogo ambaye wote mnampenda, anaitwa Jimmy. Ila Jimmy yeye haongei. Mpole kama Liv, lakini Jimmy amezidisha upole. Halafu bibi yao pia anaitwa Oliva, kama Liv. Ila wote ni kina Magesa.” Wakazidi kucheka. “Kama ni hivyo basi amemaliza, hakuna aliyeachwa. Mwanangu huyo anaakili kama zangu.” Nanaa akajisifia tena nakufanya wazidi kucheka. “Ila huo utundu na uzungumzaji kachukua kwa baba yake. Akili mimi.” Wote wakacheka tena. “Karibuni sana. Naona mimi na Magesa tumeshakuwa wenyeji.” Baba Naya akaongeza.

“Anko! Unajua hizi ngazi watu wanapanda hapa pakubwa, katikati. Lakini wanaogopa kupanda huku pembeni ili wasianguke. Lakini ujue...” “Hapana Magesa. Nenda kakae.” Baba yake akamkatiza kwa haraka na kumfanya atulie. “Kwani alikuwa anataka kusema nini?” “Wewe humuwezi Magesa. Acha baba yake amtulize. Macho yake yanavutwa na vitu vizuri tupu, pamoja na vya hatari. Hapo alikuwa anakupanga kwa mahesabu, ili atakapokwambia anataka kupanda pale nje ya ngazi, muwe ukurasa mmoja.” “Haiwezekani!?” Naya akacheka.

“Anaakili huyo! Muone hivyohivyo. Akitaka jambo lake, hata kama ni la hatari, utajikuta unamkubalia bila kujijua. Ni mpaka baba yake akimsikia ndio anamuelewa kwa haraka. Akijua jambo ni la hatari, haruhusiwi kufanya, anaanzia mbali. Anakupa madhara yake, kisha faida zake na jinsi ya kuepuka madhara yake, akimaliza hapo, unajikuta wewe mwenyewe ndio unamsaidia kulitenda hilo jambo.” Wakacheka sana wakati Nanaa akiwasimulia.

“Sasa baba yake huwa anamuwezea. Kama hapo si umemuona ametulia na amerudi kukaa, anafikiria jinsi yakumpanga tena baba yake. Apige lugha gani mpaka amruhusu kupanda pale. Au  yeye mwenyewe Geb ahusike katika huo mpango, amsaidie kupanda pale.” “Kwani hapo hajaridhika?” “Hata kidogo. Kwamba ndio jambo limeisha hapo? Hata!” Bibi yake akadakia.

Nanaa akaendelea. “Lakini hapo ashajua nani mwenye kupinga yeye kupanda pale. Baba yake. Ndio anampigia mahesabu jinsi ya kumrudia tena. Hakubali kushindwa. Sasa wakati yeye anampigia mahesabu baba yake, sisi twende tukafanye kazi.” Naya na Nanaa wakaondoka wakicheka, wakamuacha mama G akisalimiana na baba Naya vizuri. “Na mimi nataka kusaidia mami.” Wakamsikia Liv, wote wakageuka. “Njoo kipenzi changu. Ila Magesa wewe kaa na mtoto. Mcheze naye.” “Mimi nampenda Jimmy. Si ndio Jimmy?” “Wewe kaka mzuri Magesa. Cheza na Jimmy.” Akakubali bila shida. Wakaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Naya akampenda sana Nanaa, ikawa rahisi kumzoea. Mwepesi, mchapa kazi halafu mchangamfu. Akavutiwa na uzuri wake pia. Wakaandaa kwa pamoja mpaka wakamaliza, na mama G alikwenda kuwasaidia huku akitaniana na Nanaa. Walionekana kumchangamkia Naya, mpaka Naya akajikuta amewazoea na kuingia kwenye tani zao. Muda wakukaribia kuwasili wageni ulipofika, Nanaa akamshauri Naya akajitengeneze kidogo ili wageni wamkute ametulia na nadhifu. Naya akacheka na kumfuata Joshua. “Nataka ni freshup kidogo.” Mrembo huyo mtoto wa mjini anajua lazima mwanamke kuwa na vipodozi kwenye pochi. Joshua akapanda naye mpaka chumbani kwake.

“Hakika Joashua umejijenga!” “Nashukuru kama umepapenda.” “Mhh! Huku tu chumbani kwako ni kama ile nyumba yetu nzima! Mpaka sebule!” “Niliamua Naya. Nilikusudia.” “Hongera. Mpaka naona shida kuweka vitu vyangu chini! Naona ni kama nakuchafulia!” “Naomba kuwa na amani kabisa, usiwe na wasiwasi wowote!” Akampa kitaulo kidogo na kumuonyesha upande wa bafu, Naya akaenda kujisafisha, na kujitengeneza hukohuko. Akatoka amependeza kama alivyokuwa amekuja hapo. “Nakushukuru kwa kila kitu Naya wangu. Umefanya ile sehemu ivutie zaidi, umeweza kupokea wageni vizuri. Nakushukuru mpenzi.” “Karibu na asante kuniamini, imenipa ujasiri.” “Karibu. Sasa twende tukapokee wageni wengine. Najua leo utachoka, nivumilie.” “Usijali. Nikazi nilikuwa nikifanya usiku kuchwa. Nimezoea.” Joshua akacheka, akamshika mkono wakatoka.

Naya akashangazwa na aina ya wageni walio kuwa wamealikwa hapo. Lakini akajirudi. Ni Joshua! Lazima awe na wageni wa namna hii. Viongozi wakubwa watupu wa kazini kwao walikuwepo hapo. Akashangaa kumuona na Chege pamoja na rafiki yake, waliokuwa wakimlalamikia Jamal kuwa hawajaalikwa, nao walifika hapo. Akajua walihangika mpaka wakaalikwa. Walijawa furaha na kuwaona wakipiga picha kila wakati. Joshua alikuwa amemshika Naya mkono wakati wakikaribisha watu mpaka akaridhika wageni wake wote wamefika pale. 

Mambo Ya Mungu.

Aliporidhika kuwa wageni wake wote wanavinywaji wakiwa nje ya ukumbi wakifanya cocktail tu, Joshua akaomba watu wote watulie, wasikilize kabla hawajaelekea kwenye chakula. Alikuwa amesimama na Naya, akasogea sehemu ya juu kidogo ili aonekane na wageni wake wote. “Naomba niongee kidogo juu ya  historia ya maisha yangu. Najua wengi hawaifahamu.” Akaanza Joshua. “Naahidi sitawachosha na historia ndefu maana harufu ya chakula  imeenea, kuashiria chakula kipo tayari.” Wakacheka kidogo.

“Nilizaliwa kama watoto wengine wanaoitwa ni wa bahati mbaya. Baba alikuwa mume wa mtu. Mwenye familia yake nzuri tu, na mama yangu kama mwanamke duni tu, muhudumu tu wa nyumba ya kulala wageni huko mkoni, na ndipo alipo kutana na baba yangu na mimba yangu kutungwa. Kufupisha habari, mama alipofariki nikawa mtoto wa kukataliwa na kila mtu. Na kwa baba nako nilipoenda nikaonekana kama mtoto muingiliaji tu kwenye familia yake. Ndipo nikaishia kuwa mtoto wa mtaani kabisa. Nikilala mtaani kabisa kwa kuwa hata ndugu walinikataa.” Palizuka ukimya mkubwa sana wakisikiliza.

“Nilifanikiwa kwenda chuoni, nikapata msichana, naye alipogundua historia yangu na hali ya umasikini niliyokuwa nayo, aliniacha na kwenda kuanzisha mahusiano na mwanaume mwingine. Nikarudi kuwa peke yangu tena. Nilihangaika sana mpaka Mungu aliponihurumia na kunirudisha kulala ndani ya nyumba na si mtaani tena ambako alinitetea kwenye hatari nyingi sana za kufa nikiwa nikikimbiwa na watu hata wale ambao huwa hupokea kila mtu, mimi walinifukuza. Nilipofanikiwa, nilijiapia kitu kimoja.” Joshua akatulia kidogo.

“Nilijiambia, sitarudia kosa alilofanya baba yangu. Kwamwe sitakuja kulala na mwanamke ambaye Mungu hajanipa hata kama tamaa za mwili zimenizidia kwa namna gani, nilijiambia nitasubiri tu mpaka Mungu atakaponipa mwanamke wangu. Nilianza kuwa mpweke, na kadiri siku zilivyozidi kwenda ndivyo upweke uliponizidia na kuzidi kumsihi Mungu anipe huyo mwanamke. Hakika nilisubiri na kuwa mwaminifu sana ili Mungu anipunguzie siku za upweke na mimi niwe na wangu lakini ikawa ni kama Mungu anakawia. Wengi hupenda kulikotengenezwa tayari, kwa hiyo sio kwamba nilikosa mwanamke, lakini kila aliyenijia kipindi hiki nikiwa ninapo pakuishi, rohoni nilishuhudiwa kabisa si wangu. Walikuja wa kila namna wa sura, maumbile, lakini sikuwahi kupata amani ya umiliki.” Joshua akaendelea.

“Siku moja nikiwa nimemuachia Mungu kabisa, kwa kuwa nilishaumwa na nyoka, nikawa mwoga wa wanadamu sana. Namjua mwanadamu anapokuwa kwenye nyumba ya ibada na anapotoka nje ya nyumba ya ibada jinsi anavyoweza kuwa mkatili kuliko simba mwenye njaa kali. Na huwa haijalishi jinsia. Awe wa kike au wakiume, Mungu amempa mwanadamu nguvu na uwezo wa ajabu sana. Akiamua anaweza akawa kitu cha ajabu sana. Maisha yakanifundisha kuwa mwangalifu na makini sana kwa kiumbe mwanadamu. Sina haraka naye.”

“Nikiwa nimetoka ofisini kwangu nipo ofisi ya mwajiri, nikiwa na mambo mengine kabisa.” Joshua akacheka kidogo, Naya akainama. “Mnaweza msielewe, lakini ni kama kitu kikaniambia kunyanyua uso. Moja kwa moja nikamuona msichana amekaa nje ya ile ofisi, ameinama. Mapigo ya moyo yakakabadilika, isivyo kawaida macho yakataka kuangalia kilichobadilisha mapigo ya moyo.” Nanaa akaanza kucheka nakufanya wageni wengine waanze kucheka. “Mimi mwenyewe nikashangaa! Sikuwahi kupata hiyo hali! Ikabidi nikae sawa niangalie. Mbaya zaidi alikuwa ameinama, hata haniangalii. Nikajiambia labda ni wa pembeni yake aliyekuwa akizungumza na mwingine wa nyuma yake, nikajaribu kukaza macho, lakini nikarudi kwa yuleyule aliyekuwa ameinama. Nikajiuliza huyu Mungu anataka nini kwangu!” Watu wakacheka.

“Naomba muelewe aina ya wanawake wanaonizunguka, na ninao kutana nao. Leo moyo unashituka kwa msichana aliyekata nywele kama mtoto wa kiume! Hana hata urembo japo hereni! Nikamuuliza Mungu ni nini hicho kinanifanya nimwangalie au kuna kitu kingine! Nikataka kumfuata na kuzungumza naye japo kumfahamu jina kama njia yakuelewa zaidi ni nini kimenitokea, na hapo sikuwa hata na mpango na mwanamke na nilikuwa busy na kazi pamoja na shule, napambana kumaliza shahada yangu ya tatu. Lakini Roho wa Mungu ndani yangu akanionya kabisa nisimfuate, tena hapo nikazidi kushangazwa. Nikaona nitii nisimfuate, ila nikamuuliza Jamal. Ndio maana na Jamal yupo hapa leo, kama atakumbuka.”

“Nilimuuliza katika lile kundi la wasichana pale nje ni kina nani, maana nilikuwa na Jamal karibu yangu. Akaniambia ndio aliowaita ili kuwafanyia usahili kwa ajili ya idara yake. Kwa kuwa na mimi nilikuwa kwenye hali ya sintofahamu, sikujua niulize nini tena. Nikamaliza kilichokuwa kimenileta pale kwenye ofisi za mwajiri, nikamuacha Jamal na usahili. Lakini niliondoka pale nikiwa na maswali juu ya kile nilichojisikia wakati ule. Kabla sijaondoka nikamsihi Mungu asaidie hata anyanyue kichwa, aangalie upande niliokuwepo, angalau basi niione sura yake. Nikasubiri mpaka nikakosa sababu ya kusubiri, Naya alikuwa amejiinamia muda wote. Nikakata tamaa. Wakati nataka kuondoka tu, akanyanyua uso na kutizama upande uleule. Lakini wao hawakuwa wakituona kule ndani. Sitaongeza neno ili kuongeza nguvu ya hiki ninachotaka kuwaambia, lakini aliniangalia, moyo ulipata kama kitu kimepiga.” Nanaa na mama G wakacheka sana. Na wengine wakacheka. Joshua akacheka na kuendelea. Naya alibaki ameinama akicheka taratibu.

“Kama nilivyowaambia, Mungu alinionya kabisa nisimfuate. Niliondoka pale na maswali, zaidi kwa Mungu. Hivi huyu Mungu anataka nini juu yangu na kile alichokipitisha nilipomuona Naya! Mimi sikuamka siku hiyo hata na wazo la mwanamke! Ananiletea Naya, halafu hataki nimfuate hata kumuuliza jina! Nikaacha. Baada ya siku mbili nikamsikia Jamal akilalamika kuwa katika lile kundi hakupata watu anaowataka isipokuwa watatu ndio angalau wananafuu. Akaja kuita watu wengine kuwafanyia usahili, hakupata mtu. Akabaki akilalamika, mwishoe akaamua aite wale watatu wa mwanzoni. Hapo sikuwa nikijua kama na Naya alipitishwa na Jamal. Tena Jamal aliwaita kama kuwajaribisha tu kazi, ili kuona.”

“Naya na wenzake wakaanza kazi mimi nikiwa na mambo mengi mno. Watu ambao wapo kwenye kitengo changu, lakini sikuwahi kukutana nao. Jema msaidizi wangu, anayeratibu ratiba yangu, alishaweka miahadi ya kukutana nao ili mimi kama kiongozi wa kitengo niwakaribishe rasmi, lakini ikashindikana. Kila muda alioweka Jema kukutana nao, ikawa ikitokea kitu kingine kinachonihitaji zaidi. Naya na wenzie wakaanza kazi. Lakini Jamal akawa amempenda sana Naya. Alipenda sana utendaji kazi wake, akawa haachi kumsifia lakini pia sikuwa nikijua kama anamzungumzia yeye. Naya akaanza kujulikana kwa uadilifu pale kazini. Mtu wakuja kazini mapema sana, na akiwepo kazini hana mambo mengi ila kazi. Jamal akaanza kumuamini kwa majukumu ya pale idarani kwao, mimi nikiwa hata sijakutana nao bado na Naya ni mgeni tu. Sekretari wangu akaniambia kwa kumtania Jamal kuwa safari hii Jamal kapata jembe, anamfanyia kazi vizuri, naona amepunguza kelele.” “Fina!” Jamal akahamaki na kufanya wote wacheke.

“Isivyo ya kawaida, Jamal akaanza kupigania Naya aajiriwe akimtaka yeye hata kabla ya muda wa majaribio haujaisha. Siku moja nikamkuta Jamal akibishana na mwajiri akimtaka Naya aajiriwe, akataka utetezi wangu, mimi nikamwambia amalizane na mwajiri yeye mwenyewe, kwanza nina mambo mengi. Jamal alikasirika, lakini sikuwa hata nikiwajua hao wafanyakazi na sikutaka tuajiri mtu ambaye tungekuja kumfukuza kazi siku chache baadaye. Nilitaka Jamal akae nao hao wafanyakazi wapya kwa miezi 6 mpaka ajiridhishe, ndipo kutangazwe ajira, lakini Jamal akawa aking’ang’ania ajira kwa mmoja. Nikaona ni jambo ambalo nimuachie nalo yeye mwenyewe.”

“Kufupisha habari, Jema aliniambia nina dakika 10 tu siku hiyo naweza kukutana na Jamal pamoja na watu wa idara yake na ndipo itakuwa wakati mwafaka wakukutana na wafanyakazi wageni. Hapo sikujua kama yule aliyeni...” “Badilisha mapigo ya moyo.” Akamalizia Nanaa nakufanya wacheke. “Nanaa!” Geb akatingisha kichwa. “Ewaaa! Sawasawa Nanaa. Sikujua kama na yeye yupo, na ndiye Naya anayepiganiwa na Jamal. Niliingia chumba cha mkutano, kwa mara ya kwanza nikasahau ni nini nilitakiwa kuzungumza nao baada ya kumuona Naya.” Watu wakacheka sana.

“Mimi huwa sisahau kitu ninachotaka kuzungumza mbele za watu na huwa siandiki. Ila siku ile nilishituka na nikashindwa kujielewa. Na Naya naye akawa kama amenipuuza. Aliniangalia tu nilipoingia na kuwasalimia, akarudisha macho yake chini ambapo baadaye nilijitahidi kuchungulia na kujua anaangalia nini, nikagundua anaangalia simu yake. Sasa nikaumia kidogo. Nikasema amenidharau. Sifa za Naya nilizozisikia kwa Jamal akiwaambia watu kuwa hana muda na simu. Mimi naongea siku hiyo ndio macho kwenye simu! Kidogo ikanisumbua. Lakini nikajua kuwa katika lile kundi la warembo wote siku ile, Jamal alimwajiri. Kutokana na sifa zake nilizokuwa nikizisikia, nikajiambia labda Mungu alitaka kuniongezea mfanyakazi bora pale kwenye kitengo chetu, lakini zile hazikuwa hisia za mfanyakazi mwenzangu. Nikaona niwe na subira.”

“Siku zilizidi kwenda Roho wa Mungu akinionya kabisa nisimfuate Naya. Ipo siku nikamsihi tu angalau nipate nafasi yakumfahamu nione ni nini cha tofauti alichonacho Naya na Mungu kuona kitanifaa mimi! Lakini sikupata ruhusa kutoka kwa Mungu mpaka siku moja nikapata wasaa. Mungu alinipa kibali wakati ambao hata mimi sikumuelewa Mungu. Ndio nilikuwa naanza mitihani, Naya na wenzake walitumwa kikazi na Jamal Mbeya, ndio na mimi nikapata kibali hata chakuzungumza naye! Nikamwambia Mungu hiyo sio sawa. Naya anakuwepo palepale ofisini, ananizuia hata nisimsogelee, leo yupo nje ya jiji, ninamtihani jumatatu, eti ijumaa ndipo niende nikamuone! Nikanung’unika kidogo lakini ikanilazimu. Nilishasubiri sana, ikabidi kukusanya shule yangu yote na kumfuata Naya mkoni Mbeya nikiongozana na Jamal akijua naenda naye kikazi tu, kumbe nilikwenda nikiwa na agenda ya pili pia.” “Naya!” Akamalizia Nanaa watu wakaanza kucheka.

“Siku nilitaka kumsikia Naya, napo ilibidi kumuomba Mungu. Asubuhi hiyo walikuwa wakifanya matangazo yao sokoni, Mbeya, Naya alikuwa busy mpaka nikaelewa ni kwa nini Jamal anampenda. Hakukaa hata mara moja, alikuwa na kazi wakati wote nikashindwa hata kumsogelea. Niliporudi tu hotelini, wote walikimbilia kula na kunywa, yeye akakimbilia chumbani nikaambiwa amelala. Nikajua ni sababu ya kuchoka. Nilimsubiria Naya, mpaka karibu giza linaingia. Nimekaa sehemu ya kula nikimuwinda pengine atashuka chini sehemu ya mgahawa ale ndipo angalau niisikie sauti yake, maana siku ya kikao alijitambulisha tu jina lake bila maneno mengi akakaa. Wenzake walikuwa wakinywa mpaka wakaanza kulewa, Naya yupo chumbani.”

“Nikaanza kumuuliza Mungu kama anaelewa kipindi nilichonacho. Kwamba nipo kwenye mitihani na kazi inayonisubiria kwa asilimia zote, halafu akaniambia ndio wakati wa kumfuata Naya, Naya mwenyewe hayupo! Nikamuuliza Mungu ule ulikuwa usumbufu au kulikuwa na jambo!” Watu wakacheka. “Wakati nimekaa peke yangu na vitabu vyangu hapo mgahawani na laptop yangu, nikamuona Naya anakuja pale mgahawani. Nilikaribia kutupa laptop kwa furaha. Halafu alikuwa peke yake.” Watu wakazidi kucheka.

“Kazi ikawa ni jinsi gani ya kuzungumza naye maana mimi ni kiongozi wake mkubwa sana Naya. Nikamuacha akae, ndipo nilipomfuata. Akataka kunikimbia kwa hofu. Alikuwa akitetemeka, nikajua hatutaweza kuzungumza. Nikaanza kumsihi Mungu amfanye atulie, angalau arudi kukaa.” “Kwani alishasimama?!” Nanaa akauliza kwa sauti. “Zamani sana. Aliponiona tu nimemsogelea, akasimama kama akimbie wakati nilimuona ameshaagiza chakula, pale alikuwa amekaa akisubiria lakini gafla akataka kuondoka!” Naya akacheka mpaka akajifunika uso.

“Nikaanza kuzungumza naye kwa maswali ili kumfanya afikirie, atulie. Akaanza kunijibu kwa kifupi huku akitaka kuondoka, nikaendelea kumuuliza mpaka nikamuona ametulia. Hazikuchukua dakika 10 mbeleni wakati tukizungumza naye, kuelewa kwa nini ni Naya kwangu na sio msichana mwingine. Moyoni nikasema Aaahaaaa! Nikamuuliza Roho wa Mungu, sasa kwa nini hukuniambia tu tokea zamani, ukanisumbua vyote hivyo?” Watu wakacheka.

“Nilikaa nikimsikiliza Naya akijibu swali fulani hivi, yaani akawa ni kama ameandika insha nzima, na kunielewesha hata kwa machungu niliyokuwa nikipitia na maswali niliyokuwa nayo juu ya hata kukimbiwa na mwanamke wa zamani. Naya alizungumza kwa kawaida tu, lakini Mungu aliyapa yale maneno nguvu ya ajabu nikabaki nikimtizama nakuelewa kuwa Naya ni wangu. Sasa kabla sijanogewa zaidi maana Naya alishatulia, nikanogewa na mazungumzo mazuri, tukaingiliwa na mtu aliyekuwa akimfahamu Naya na yeye alikuwa amemfuata hapo hotelini kama mimi tu. Ila mwenzangu alikuwa na nafasi kubwa ya ushindi kuliko mimi. Nikataka kukata tamaa, lakini Mungu akanionya kabisa kupaniki ila kutulia. Jamani Mungu yupo na humpa amtakae.”

“Mwenzangu alionekana anayo amri kubwa kwa Naya kuliko mimi, ikabidi mimi niondoke pale nilipokaa, nimpishe yeye akae. Niliondoka pale kama niliyenyang’anywa tonge mdomoni. Ila nikawa nimepata jibu ni kwa nini ni Naya na si msichana mwingine. Nilirudi chumbani kwangu nikimuamini tu Mungu na ahadi zake kwangu, lakini kama binadamu nikiwa sijui chakufanya. Usiku Jamal aliingia chumbani kwangu akaongea tu kwa kifupi, kuwa wote wameamua kubaki pale kumalizia weekend hawatarudi Dar siku inayofuata. Moja kwa moja nikajua na Naya naye ameamua kubaki na yule mgeni wake. Jamal aliondoka na kuniacha nakodolea macho vitabu wala sioni maandishi, kwa maumivu.”

“Nikaanza kumuhoji Mungu pengine hakunituma pale Mbeya, nilijipeleka tu mimi mwenyewe, lakini najijua, sina tatizo lakumsikia Mungu. Alinipitisha kwenye mazingira ambayo, hapakuwa na jinsi isipokuwa kujifunza na kuelewa sauti yake. Hata akinong’ona, kama anazungumza na mimi, huwa namjua Mungu wangu. Niliimaliza ile siku kwa kusononeka, lakini sikuwa na jinsi isipokuwa kutii na kutulia pale chumbani.”

“Asubuhi nikiwa najiandaa, Jamal akagonga na kuniambia dereva ameshampigia simu kuwa amefika, tujiandae safari ya kurudi Dar ianze. Nikamkubalia, ila nikamuona ni kama kuna kitu anasita kusema. Nikamuuliza ni nini Jamal!? Akasema anaomba aondoke na mtu mmoja hapo, tumpe lifti mpaka Dar. Akasema ni binti aliyetulia, hataki hata kumuacha pale wasije kumshawishi ujinga. Nikamuuliza ni nani huyo? Ndipo akasema Naya.” Nanaa akaanza kupiga makofi. “Nanaa wewe mtoto acha ushabiki!” Mama G akaongea nakufanya watu wacheke.

“Mimi mwenyewe sikuamini. Nikamuuliza Jamal, anauhakika kama ni Naya na amekubali? Akasema amekubali. Nikaanza kucheka moyoni. Kwamba nitakuwa na Naya safarini! Nikafurahia sana. Alipotoka tu Jamal, nikapiga magoti nikamwambia Mungu wangu, asante.” “Jamani Joshua!” “Nanaa wewe!” Mama G akamshangaa. “Wewe huoni kama ni Mungu huyo!?” Nanaa akamuuliza mama G. “Kweli ni Mungu Nanaa. Ni Mungu. Naya alipoona kwenye hiyo gari na mimi nitakuwepo akaingiwa hofu tena na kutaka kubadili mawazo, hapo nikajikaza na kumuomba Jamal nizingumze naye mimi mwenyewe. Nikamwambia asiwe na wasiwasi, atakuwa salama na hatadaiwa baadaye. Akaonekana kuelewa akatulia. Tukapanda tu kwenye gari, akampigia simu baba yake. Kilichonivutia na kuelewa ni kwa nini Naya, ni pale baba yake alipomwambia Naya afunge macho hapohapo amuombee. Akamuombea binti yake, mpaka akamaliza, nikamsikia Naya akisema Amina’. Nikajiambia kwa hiyo ni muombaji, na baba yake pia anamuombea! Nikasema na mimi nitaponea hapohapo.” Watu wakacheka.

“Ndipo kuanzia hapo nikaanza kumng’ang’ania Naya, asielewe ni kwa nini, asijue mwenzie nilipewa na Mungu. Nilimwambia Naya, huwa namfahamu yeye, au natambua uwepo wake popote alipo kwa mapigo yangu ya moyo.” Watu wakacheka na kupiga makofi. “Sitanii. Alipo Naya, bila kuiona sura yake, moyo wangu unajua yupo. Nilimwambia awe amenenepa, au amekonda. Ananywele ndefu au fupi. Nitamjua tu. Ni nitamtambua hata wawe wamechoma hiyo ngozi yake nzuri akawa kitu kingine tofauti na huo muonekano wake, akiwepo mahali Naya wangu, nitajua kutoka...” “Moyoni!” Akashabikia Nanaa, Geb akaina ana kutingisha kichwa. Watu wakacheka tena.

“Nipo na Naya, naelewa ni kwa nini yeye. Ninayo hii nyumba, lakini sasa hivi nalala nikimsikia Naya akiwa anakoroma masikioni kwangu akiwa upande wa pili.” “Jamani Joshua! Si ulisema nilikoroma mara moja tu!” “Yaah! Ulikoroma mara moja tu, ulikuwa umechoka.” Watu wakacheka. “Naya hakoromi jamani.” “Ushasema nakoroma!” Naya akalalamika akicheka. “Mara moja tu. Yaani nakuwa humu ndani, naendelea na mambo yangu, nikiwa na Naya masikioni. Ameleta maana nyingine kabisa kwenye maisha yangu. Mungu amenipa faraja ya ajabu. Huwa analala, nakuniacha nikimsikiliza huku nikiendelea na shughuli zangu mpaka nikiwa tayari kulala, ndipo nakata simu na mimi nalala.” “Waw!” Watu wakashangaa.

“Hakika sikutegemea faraja aliyoongeza Naya kwenye maisha yangu. Ni zawadi kutoka kwa Mungu. Nina utulivu wa tofauti nikijua Mungu amenipa Naya.” Joshua akamsogelea na kumshika mikono yote miwili, Naya akimshangaa. Kisha akapiga goti mbele yake. Wengi ndio wakaelewa, lakini Naya yeye alibaki na mshangao mkubwa sana usoni. “Hili litabakia kuwa jengo tu Naya, mpaka wewe upafanye hapa nyumbani.” Joshua akaanza taratibu akimtizama Naya. Naya akamuachia mkono mmoja na kujifuta machozi kwa haraka akiwa ameshaelewa anachotaka kufanya. Joshua akatoa pete mfukoni. “Nakupenda Naya. Na wakati wote nimekuwa nikikwambia nakuhitaji wewe kama Naya. Naomba tuone, na mimi nipate familia. Nipate ndugu wa kwanza na sehemu nitakapopaita nyumbani.” Naya hakuamini. Ni Joshua huyu aliyemuuliza anataka wafunge ndoa lini, akashindwa kumjibu.

“Mimi nilijua hutaki ndoa Joshua!” Naya akamwambia akilia asiamini. “Nilikuwa naandaa hii siku maalumu ndio maana nilishindwa kukujibu siku ile kwenye gari. Nakupenda Naya, nimeandaa hii siku maalumu kwa ajili yako.” Naya hakuwa akiamini. Akamwangalia baba yake akakuta akimwangalia, akarudi tena kumwangalia Joshua. “Naya?” Joshua akamwita taratibu akiwa amepiga magoti. “Subiri kwanza Joshua. Usiondoke.” Watu wakawa hawajaelewa. Kila mtu akashangaa sana. Naya akamuacha Joshua amepiga magoti akaenda mpaka alipokuwa amesimama baba yake na ndugu zake.

Akalia hapo mbele yake ameficha uso watu wote kimya kisha akamsogelea baba yake karibu zaidi, mpaka upande wa bega la kushoto alikokuwa amesimama. “Mimi nampenda Joshua, baba.” Naya akasikika akinong’ona. “Haaa! Ndio kina Liv wote hawa!” Akasikika Nanaa akihamaki kwa sauti ya mshangao na kumuangalia mumewe, Geb. Joshua alibaki amepiga magoti akisubiria akacheka akijua alishapata kibali kwa baba Naya, kwani alishamuomba kumuoa Naya, na siku hiyo alishajua kuwa Naya anachumbiwa. Baba huyo alishaomba pamoja na Joshua, akimkabidhi kwa Mungu na kumuombea baraka zote. Ila hakumwambia hata Naya mwenyewe. Joshua anawakaribisha nyumbani kwake, Naya anasema atazungumza na baba yake, Joshua alishazungumza na baba Naya, wakakubaliana.

“Joshua ananipenda kwa dhati na ananijali.” Akarudia Naya akilia. “Mimi nawaombea baraka za Mungu Naya. Mungu yupo na nyinyi.” Naya alifurahi sana, akamuinamia baba yake na kuendelea kulia asiamini. Alikuwa amependeza sana. “Bibi harusi wangu ataondoa urembo wote!” Nanaa akamsogelea Naya. “Bado Joshua amepiga magoti.” Akamnong’oneza Naya huku akimsugua mgongoni taratibu kwa upendo. Watu wakacheka kidogo na Naya naye akacheka na kumwangalia Joshua. Akarudi pale alipokuwa amepiga magoti, Naya akaushika mkono ule usio na pete, akaunyanyua na kuubusu kiganjani kabisa. “Na mimi nakupenda Joshua.” Mama G akapiga vigelegele na Nanaa akampokea na wengine wakaendelea kupiga makofi wakati Joshua akimvisha pete Naya mpaka akamaliza.

Wakaanza kupewa pongezi Naya akiwa ameshikwa vizuri na Joshua. Furaha aliyokuwa nayo Joshua, haikuweza kufichika. Yeye alionekana amefurahi zaidi hata ya Naya mwenyewe. Mabusu shavuni kwa Naya hayakuisha. Hapo mbele ya watu hakuvuka mipaka kabisa, akiweka heshima kwa baba yake Naya, kwa kuyajua na kuyazingatia mahusiano ya Naya na baba yake. Akaishia mabusu ya shavuni tu. “Nimefuhi sana, natamani leo ndio ingekuwa ndio harusi yetu.” Joshua akamnong’oneza Naya sikioni. Naya akamwangalia akicheka. “Inamaana leo usingeondoka hapa, tukabaki wote tukisheherekea. “Mungu atatupa uzima Joshua. Hiyo siku na sisi tutaiona.” “Amina Naya.” Hilo likamfurahisha sana Joshua, na kumuhakikishia ndoa. 

Mahari Yakushangaza Ya Naya. 

Walibakia na kina Magesa tu hapo pamoja na kaka yake Nanaa, James ambaye ndiye aliyemlea Nanaa. Na yeye alihudhuria kwenye hiyo tafrija na baba yake mzazi Nanaa waliyekutana naye ukubwani naye akaonekana kufahamiana vizuri tu na Joshua, alikuwepo hapo kwenye tafrija pia. Na mwenyewe alibakia nyuma baada ya wageni wote kuondoka. Wote watatu, Gebu, Joshua na baba yake mzazi Nanaa walikuwa wanachama wa hiyo club wanakokwenda kuendesha boti huko. Ndio Naya akajua huwa wakati mwingine wanakutanaga huko na kuendesha boti wakishindana kisha kuvua samaki pamoja. Walitaniana kwa hili na lile ndipo Geb akaomba kuzugumza na baba Naya.

“Naona leo mambo yamekwenda vizuri, tunamshukuru Mungu.” Watu wote wakatulia kusikiliza. Watoto wao walishalala. Joshua na Naya wakawalaza chumba cha chini ambacho kipo hapo karibu nao. Mama yao alijiandaa mpaka na nguo zao za kulalia kama aliyejua watakuwepo hapo kwa muda mrefu. “Joshua anataka kuoa kwa haraka, na kamati hapa naona imekamilika. Tunaomba tu utaratibu wa mahari, tuje kulipa.” Naya akashangaa kwamba kulikuwa na mipango ya harusi tayari! Watu wote wakatulia. Pakazuka ukimya kama kumpa baba Naya nafasi ya kuzungumza.

“Anachozungumzia Gebu ni ile orodha ya vitu vinavyohitajika kuletwa kama sehemu ya mahari ya Naya.” Naya akabaki ametulia pembeni ya Joshua. “Mahari ya Naya haitakuwa mali.” Watu wote kimya wakitaka kujua na kumsikia baba huyo mkimya haswa. Akaendelea. “Kama kamati imekamilika na ni nyinyi tu mliopanga kuja kuilipa hiyo mahari, tunaweza kumalizana hapahapa. Lakini kama kuna aliyepungua, tunaweza kupanga hiyo siku.” “Nafikiri kwa sehemu unaijua historia ya Joshua. Sisi ndio familia, kwamba tumeshakamilika.” Akajibu Geb. “Basi hii ndio mahari ya Naya.” Baba Naya akajiweka sawa kwa kujivuta kabisa mbele ya kiti ili kuhakikisha wote wanamuona vizuri na kumuelewa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Usipitwe na MAHARI ya Naya. Baba Naya anataka nini kwenye mahari ya binti yake? Kina Magesa ndani ya nyumba. Usikose muendelezo.

ILI KUJUA KISA KIZIMA JUU YA KINA MAGESA, FUATILIA SIMULIZI YAKE YA kuvutia na KUSISIMUA YA “Ni wangu!”

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment