“Ahadi
tu.” Hiyo ndio ikawa mahari anayohitaji kwa binti yake. Kisha akaendelea.
“Ahadi kutoka kwa Joshua kuwa atakuwa mwaminifu kwa Naya.
Lakini, ikitokea macho yake yameona mwanamke mwingine, au akagundua hataweza
kuishi tena na Naya, amepata mtu bora zaidi ya Naya, kabla hajaanzana na
mwingine, tafadhali hitimisha na Naya kwanza. Ukiwa huna haraka ya kuanza
kwengine, ukawa na nafasi, ningeshukuru kama utafanya kama hivi ulivyofanya
leo, kuja kumchukua nyumbani, tukakabidhiana kwa amani, basi mrudishe kwa
maelezo ya wazi utakayochagua wewe, tuagane kwa amani tu. Na wala usijifunge.
Iwe ni kesho yake baada ya harusi au baada ya miaka 20, kumbuka kufanya hivyo.
Jua Naya ni binti ya mtu. Anapo pakwenda. Pale Kiluvya ni nyumbani kwa Naya
tena pako kwa maandishi kabisa.” Watoto wake wakiume wakashangaa na kumwangalia
baba yao. “Hilo nilimuomba mama yao tokea yupo hai. Alipoanza tu kuugua.
Tukakubaliana iwe hivyo. Ile nyumba ni ya Naya.” Bale akamtizama
baba yake kwa mshangao zaidi. Ila hakuwa na chakusema.
Baba yao
akaendelea. “Muda na wakati wowote uwe huru kumrudisha au hitimisha naye kwanza
bila ugomvi au kumchanganya akili ndipo uje umuache. Au zile tabia za
kurudiarudia habari za kuomba msamaha kila wakati, ukirudia jambo hilohilo,
kisha ndio unamuacha na kuamua kuanzana au kuendelea na mwanamke mwingine! Hapana
Joshua. Niwe hai au nimekufa, naomba Joshua, mrudishe binti yangu nyumbani kwa
heshima tu au hitimisha naye kwanza. Niahidi hutaanzana na mwanamke mwingine
yeyote, kabla hujamrudisha mwanangu nyumbani au niseme kuhitimisha naye rasmi.
Usimzungushe katikati ya michezo ya ajabuajabu, itakayo eleweka kichwani kwako,
na kuanza kumvuruga kwenye njia zisizofaa. Halafu yeye akabaki amevurugukiwa
hapo katikati wakati wewe ukiendelea na chaguzi za maisha yako kwa furaha. Hitimisha
naye. Muweke sawa. Ndipo uendelee na utakachokuwa umeamua. Ni hilo tu.”
Palizuka ukimya mkubwa huo, kila mtu akabaki akitafakari.
“Hiyo
ndio mahari ya Naya. Ahadi tu. Sitataka mali. Na kama utataka muda
wakufikiria juu ya hilo, utakapokuwa tayari, karibuni nyumbani. Maana siku
utakapokubali hili, ujue ni ahadi, na nadhiri uliyoingia
kwa hiyari yako wewe mwenyewe mbele za Mungu na sisi tutakuwa mashahidi. Ujue
Mungu hatakuacha, atakutizama ili akupatilize sawasawa na ahadi utakayoahidi
juu ya hili. Maana nimemuomba kwa kufunga na kuomba asimame na mimi kwenye
hili, na anisaidie kusimamia hili hata pale ambapo macho ya Naya na wengine
yasipofika, yeye aonaye sirini, asimame na hili. Sitaki mali yeyote ile,
ila ahadi tu.” Akajirudisha nyuma kabisa na yeye akatulia.
Mzee
hajasoma wala hana mali nyingi kama wao, halafu mtulivu. Mkimya, akisikiliza
kuliko kuongea. Lakini anacho kitu cha thamani wanachotaka. Na Naya mwenyewe
akaongeza uthamani wa huyo mzee, hata kama hakubeba sura ya kitajiri kama wao,
lakini usiku huo wote kimya, heshima, macho kwake. Mkimya. Ila siku hiyo
akaongea kifasaha, akafikisha ujumbe wake. Hata kama haukuleta umaana kwa
wengine, lakini yeye ndiye mwenye mali wanayo itaka, Naya. Akarudia
ukimya wake, akimpa nafasi Joshua atafakari na aamue akiwa anaelewa anachotaka.
Hata bibilia imeandika katika {Mithali 17: 27) Asiyesema
sana ana maarifa. Mtu mtulivu ni mwenye busara. 28) Hata
mpumbavu akinyamaza huonekana mwenye hekima. Akifunga mdomo wake huonekana kuwa
mwenye akili.}
Umaana
wake ukaongezeka katikati wa wasomi na matajiri hao. Joshua, Geb, baba Nanaa
ambaye na yeye ni daktari na James. Halafu uje mama G. Mama mpambanaji.
Anayejua kuzisaka pesa na zenyewe zikatii amri kwenye mifuko yake. Naye yupo
hapo usiku huo mbele ya baba Naya, akimsindikiza Joshua kama mwanae akitaka
kuoa binti yake. Wote mbele ya baba Naya wakitaka baraka zake katika hilo. Wakiwa
wamejiandaa ipasavyo kutoa mali, chochote atakachotaka mzee huyo, walijua
watammudu tu. Mzee wa Kiluvya! Walijua watamalizama tu, hawatashindwana. Lakini
mzee hataki mali, ahadi tu. Wakatulia wakijua hata wao wapambe katika
hilo hawana nafasi tena. Kazi kwa Joshua.
Kwa aina
ya maisha aliyonayo huyo baba Naya, na vile anavyomjua na kumuona Joshua
alivyofanikiwa, pamoja na hali nzuri za maisha za hao watu wanao
mzunguka huyo Joshua, ungeweza kufikiri hapo ndipo angeponea. Kwamba
ataje mahari kubwa sana, alipwe na kuanza biashara yake, lakini bado mzee
amesimamia masilahi ya mwanae. Hakutaka aje atendwe tena kama alivyoishi na
Malon akimuona akilia kila wakati sababu ya usaliti. Akaona aweke dhiki zake
pembeni, mtaji wa biashara anayotaka kuanza, usubiri kwanza, mwanae
kwanza. Hata wao walimuheshimu, hawakutegemea.
Geb, mama
G, Nanaa na James wakakumbuka hekaheka ya mahari ya Nanaa iliyosababisha
vurugu, na pesa nyingi sana kumtoka Geb mpaka kumuoa Nanaa. Nanaa akainama
kabisa akiumia jinsi yeye alivyoozwa kwa mapesa mengi tena kwa kudaiwa kwa aibu
kabisa! Akabaki ameinama tu akimtafakari mama yake mkubwa na kuanza kuona
bahati aliyoipata Naya yakupata mzazi anayesimama naye mpaka na utu uzima huo!
Geb akamuona vile alivyojiinamia. “Hata wakitaka mahari nyingine tena, mimi
nitalipa tu, ilimradi ubaki kuwa wangu.” Akasikia Geb akimnonng’oneza sikioni.
Nanaa akajua Geb amemgundua. Akamwangalia na kutoa tu tabasamu, akarudi
kujiinamia. Geb akamvuta karibu. Wote wakawagekia wao, walikuwa wamekaa kochi
moja. “Samahanini.” Geb aliyesababisha hilo akaomba radhi kwa sauti ya chini.
Wakatulia.
Joshua
akaanza. “Sababu kubwa ya kuomba Geb na Nanaa wawe karibu na sisi nikimaanisha
mimi na Naya, japokuwa Naya hawafahamu vizuri ni vile walivyoweka uthamani wa
ndoa. Nimejifunza kutoka kwao kuwa ndoa ni zaidi ya hisia.” Joshua akaanza.
“Sikuwa nikimjua Naya. Sikumfuata Naya kwa tamaa ya urembo wake au uzuri wake
tu, ila ni zawadi Mungu amenipa. Na ninashukuru Mungu kunipa mwanamke ambaye
mpaka sasa kwangu Naya ameendana zaidi na kile nilichofikiri nahitaji kwa
mwanamke, lakini Mungu amenipa na zaidi.” Joshua akaendelea.
“Nakuahidi
mzee wangu, Naya atarudi nyumbani kutembea tu. Hapa ni nyumbani kwa Naya
na watoto Mungu atakao tujalia.” “Wao!” Nanaa akasikika kuhamasika mpaka
akanyanyua na kichwa. “Nakuahidi nitamuheshimu Naya. Si kwa ajili yake
tu, hata yangu mwenyewe. Siwezi kuchezea kitu alichonipa Mungu kwa heshima
kiasi hiki! Hapana, sio mimi. Najua vitu anavyonipaga Mungu mwenyewe, na huwa
ananipa uwezo wa kuvitunza. Nitampenda Naya, kama nafsi yangu. Akirudi
nyumbani, basi ujue ni kwa muda tu, na mimi nitakuwa nikimsubiria nyumbani,
kama sitakuwa naye.” Mama G akapiga kigelegele kidogo kisha akanyamaza.
Wakacheka.
“Sina
tamaa za wanawake. Nimejawa hofu na kiumbe mwanadamu, kwa jinsia yeyote ile, ni
mpaka Mungu aniruhusu niwe naye karibu ndipo nafanya mahusiano naye. Imekuwa
hivyo na sitabadilika kwa Naya. Kwa hiyo nakuahidi mzee wangu, Naya atabaki
peke yake kwangu, mpaka kifo changu na Mungu anisaidie.” “Kutoka kwenye
midomo yako mwenyewe, mpaka kwenye sikio la Mungu.” Baba Naya akaongeza na
kuendelea. “Nakukabidhi Naya.” Akamalizia hivyo tu baba Naya. Joshua
akanyanyuka na kumpa mkono kwa heshima sana akimshukuru. Hapo hata Nanaa
akapiga kigelele akisaidiana na mama G. “Tunashukuru Mzee wetu.” Wote wakampa
mkono baba Naya kama kumshukuru.
“Kwa
baraka hizo mzee wangu, basi mipango ya harusi inaanza rasmi. Ili kukamilisha
hili.” Akaongea Geb. Wakaelewa ndiye anayesimamia hilo jambo. Wakati wakipeana
mikono, Joshua akatoka hapo kwa haraka na kurudi na champaign mkononi pamoja na
glasi nzuri nyembamba katikati ya vidole vyake akiwa amezipishanisha mkiani ili
zisianguke. Naya akasimama kwa haraka kumpokea zile glasi. “Asante.”
Akamshukuru Naya akimkabidhi. “Naombeni tumshukuru Mungu wangu kwa hili
jamani. Hii champaign ni moja ya champaign nilizonunua miaka mingi nikitafutia
sababu ya kunywa. Maadamu mpaka sasa naona mkono na baraka za Mungu juu yangu
katika hili, naomba tunywe rasmi na kufurahi tukimshukuru Mungu wangu kwa kutenda
kwake kwa muujiza.” Naya akaanza kugawa zile glasi kwa kila mmoja pale wakati
Joshua akifungua ile chupa ya champaign. “Jamani huyu Mungu, humpa amtakaye na
wala hakuna wakumuuliza kwa nini!” Joshua akamalizia akionekana kufurahia
kweli! Akawamiminia kila mtu kwenye glasi, wakicheka na kupongezana.
Wakagonganisha glass zao kwa furaha.
Nanaa kwa Baba Naya.
Wakashangaa
Nanaa anaenda kupiga goti mbele ya baba Naya na kumpa mkono pale alipokuwa
amekaa. Naaa akaona goti moja halitoshi, akapiga yote mawili. “Hakika
nimekuheshimu baba Naya. Na nikakupenda zaidi.” “Kwa nini Nanaa, binti yangu?”
“Natamani na mimi ningepata nafasi kama aliyonayo Naya, kuwa na baba aliyenilea
kama wewe, na kunitoa kwa heshima kubwa namna hii! Hakika nimeona wivu.” Wote
kimya. “Kama Mungu hakuwa ameniandikia Geb, mwanaume anayejua anachokitaka, na
kukipigania, pengine mpaka leo ningekuwa kwa kaka James, sijaolewa. Lakini Geb,
kaka James na huyu mama ambaye ni mama Mungu aliyenipa, walipigana mpaka leo na
mimi nina ndoa. Kwa hakika umenigusa baba Naya.” Nanaa akaendelea.
“Kwa
kutokujua kwangu nikifikiri ni kawaida au watu na mambo yanafanana, nilikuwa
nikimtania Joshua nikimwambia aandae hundi nzito kwa mahari kwa vile alivyokuwa
akimsifia Naya kwetu, nikamwambia baba yake hawezi kumtoa kwa pesa ndogo kama
kweli sifa hizo zote anazo na ni mtoto wa baba kama hivi Liv kwa Geb.
Nikamwambia ajiandae haswa. Tena Geb akasema wazi kabisa kuwa, hakuna mwanaume
hapa duniani anaweza kuwa na pesa yakuja kumlipia Liv kwake. Tukacheka,
tusielewe tukijua ni mapenzi tu ya Geb kwa Liv, lakini kwa hiki ulichokifanya
sasa hivi wewe, ndio nimeelewa Geb wangu alikuwa akimaanisha nini.
Lakini mimi nilikuwa nikimwambia Joshua nikijifananisha na
Naya, kule mimi nilikopitishwa kipindi kama hiki nikitaka kuolewa,
na uwezo alio nao Joshua! Kweli wewe huna tamaa, baba Naya! Na Mungu wa
mbinguni hatakupungukia. Ni heshima kubwa sana umempa Naya. Pengine yeye
anaweza asione, lakini mimi imenigusa sana.” “Naona Nanaa.” Naya akajibu
taratibu.
“Basi
Mungu akusaidie usisahau Naya. Mimi niliuzwa, baba Naya! Niliuzwa kama mtumwa!
Tena kwa thamani ya magari zaidi ya mawili au matatu kama ni haya ya kawaida.
Nikafanyiwa mengi mno. Uchawi, ndoa kuwekewa vipingamizi, ili tu Geb alipe pesa
zaidi, na mengine mengi. Halafu sasa, mahari hiyo ya mamilioni inadaiwa, ilipwe
TENA, baada ya mahari ya kwanza, mimi nipo hospitalini wameniloga na kunipa
ugonjwa wa matende ambao haujawahi kuonekana hapa duniani.” “Pole.” “Baba Naya,
wanamdai pesa Geb. Niseme mamilioni ya pesa, nikiwa navuja maji
laliyochanganyikana na usaha, miguu inamalengelenge kama niliyeungua, lakini
ikavimba, mimi mwenyewe nilikuwa siwezi kuitizama. Geb alishakuwa amenizalisha
mtoto mmoja, huyu Liv. Kwa kifupi sikuwa na thamani ya mapesa yote hayo
waliyokuwa wakimdai Geb.” “Kwangu ulikuwa na hiyo thamani na zaidi Nanaa.
Usiseme hivyo hata kidogo! Ile pesa ni thamani ndogo sana waliyokuwa wameiweka
kwako. Hulinganishwi hata kidogo na ile pesa.” Akaongeza Geb. Nanaa akaanza
kulia.
“Mimi
sikupenda Geb. Natamani heshima hii anayopata Naya na mimi ningepata, sio
kupata heshima kutoka kwa watu baki kama wewe, mama hapa na kina Grace!
Walimzungusha kaka kwenye swala la mahari mpaka kaka akakonda kwa mawazo! Nipo
hospitalini nikiwa sijulikani hata tiba gani nipewe, huku kaka anapambana na
maswala ya mahari!” “Basi hapo sasa Nanaa wanao wote wataamka bwana waje waanze
kulia na wewe hapa! Ni nini lakini? Umeanza vizuri, unataka kuniamshia watoto
sasahivi!” Mama G akalalamika Nanaa akaanza kucheka huku akifuta machozi.
“Pole
mama. Pole sana.” Baba Naya naye akamtuliza. “Mimi ninachotaka kusema
nimekupenda na kukuheshimu baba Naya. Nakuombea
baraka baba yangu, Mungu wetu wa mbinguni asikupungukie.” “Amina
mama.” Akapokea baba Naya. Baba mzazi wa Nanaa kimya kama James.
“Wala
Nanaa hajakosea. Kuna mwenzio amejengewa nyumba kabisa kwa ajili ya huyuhuyo
Nanaa. Ana biashara mpaka leo, na zinaendelea vizuri tu hapa mjini kwa ajili ya
huyuhuyu Nanaa. Hata mimi umenishangaza baba Naya. Kama anavyosema Nanaa, Mungu
akubariki. Hapa nilikuwa nimeshajiandaa na kumwandaa Grace, pacha mwenzake
huyu Geb, yeye yupo Arusha na familia yake. Hivi leo tu ameshindwa kuja sababu
mtoto mgonjwa. Ila nilishamwandaa kwa ajili ya mahari yake huyo Naya. Nishampa
orodha ya vitu vile ninavyojua havikosekani kwenye mahari za makabila mengi
hapa Tanzania. Nikamwambia atusaidie kuanza kununu wakati sisi tukijiandaa kwa
vikubwa. Halafu Joshua na huyu mwenzie Geb wao pesa. Nilimwambia Geb na Joshua
wajiandae kipesa haswa, ili tena wasitukwamishe. Ukitaja tu pesa unayotaka kwa
mahari, tukupe bila kukuchelewesha. Muulize Joshua huyo.” “Ni kweli tulijiandaa
kwa pesa nyingi tu.” Akaongeza Joshua.
“Sio kwa
Naya. Nimeshaona madhara ya pesa zikichanganywa na mapenzi hapo! Zinakuwa
chungu kwelikweli. Unashindwa kujua kama zimekuwa msaada au laana! Hata chakula
kilichonunuliwa na hizo pesa kinakuwa si kitamu, unaishia kufunga tu, na hujui
umwambie nini Mungu! Hapana. Si kwa Naya. Naomba hiyo thamani ya pesa muibadili
kwa kumpenda binti yangu. Kwa muda mfupi nimekuwa na nyinyi hapa, nimeshaona
umoja mlio nao. Upo na nguvu mno. Mumpokee Naya kwa heshima tu, na mumvumilie
kwa madogo mtakayokutana nayo kwake. Mkumbuke na yeye ni binadamu. Kama hivi
mama G ulivyompokea Nanaa, basi mpokee na binti yangu. Mumsaidie kama hivi leo
mlivyofanya hapa kutengeneza mazingira mpaka akafanikisha kukarimu wageni kwa
ustadi. Najua itamsaidia na Joshua kuweza kuwa katikati yenu vizuri.” “Kwa
nilivyomuona Naya na kumsikia, huyo mbona ameshakuwa wetu, wala usijali baba
Naya. Ukimsikia analia sababu ya mama G, ujue ni kwa wema.” Nanaa akaanza kucheka.
“Na
ujiandae Naya. Mama hajui kuficha. Atakwambia tu. Tena atakwambia bila
kukuficha. Mimi nalia na kununa, lakini sina jinsi.” Angalau watu wakaanza
kucheka na kutaniana. Mpaka kina Magesa, James ambaye ni kaka yake Nanaa na
ndiye aliyemlea tokea kachanga, aliyekuwa kimya tu muda wote maana mama yeke
ndiye huyo aliyekuwa akizungumziwa hapo. Aliyechukua mapesa mengi na kuzuia
ndoa ya Nanaa. Na baba yake mzazi Nanaa ambaye alikuja utuuzimani baada ya
kukataa mimba ya mama Nanaa alipokuwa binti mdogo, wote wanafunzi,
walipoondoka.
Mpaka
wanaachana hapo, tayari Naya alishawazoea na kupanga nao mipango mingi tu
yakuja kukutana tena siku za karibuni na kubadilishana namba za simu. Naya na
Nanaa wakawa wametengeneza ukaribu kwa urahisi sana kitu kilichomfurahisha sana
Joshua kuona Naya naye amewakubali na kuwafungulia moyo kwa kiasi hicho.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Waliwaacha
familia ya Naya hapo nyumbani kwa Joshua. “Naona leo nimepata mambo mawili kwa
wakati mmoja.” Naya akaanza waliporudi tu ndani baada yakuwasindikiza.
“Umenivalisha pete. Na kunipa familia nzuri ya kina Magesa. Hakika
nimewapenda.” “Nimekuona.” “Nimefurahi sana. Ukiwa na wale watu, huwezi kuwa
mpweke. Wanaleta uwepo fulani hivi, hujisikii kupungukiwa. Kukiwa na tatizo
wanasema letu na hapohapo wanatafuta suluhu! Mpaka wamenishangaza wakati nipo
nao kule ukumbini! Yule mama mwepesi na akili yake ipo haraka kufanya mambo!”
“Unafikiri hata swala la kuoa nimepata shida kuwaomba! Nilipomwambia tu
nimepata mchumba. Akalibeba hilo jambo kama mimi ni mtoto wake wakunizaa. Na
usimuone vile. Anakauli sana kwa wanae. Huyo Geb na Grace!” “Eeh?”
“Wanamsikiliza sana. Akisema jambo, wanatekeleza tena kwa pamoja. Sasa mume wa
Grace naye amekuwa kama Nanaa, akaweza kuingia katikati yao, utapenda kuwa nao.
Nanaa na Man, mume wa Grace ndio watundu kuliko watoto wa mama G.” “Kwamba na
Grace ni mpole kama Geb!?” “Hivyohivyo. Ongea yake kama hivyo Liv. Mtulivu
sana. Ila mumewe, ndio mtacheka mpaka machozi. Mtundu sana. Maneno yake ya
utundu mno. Ila sasa Grace yeye hakubahatika mtoto muongeaji kama Magesa.” Wote
wakacheka walipomkumbuka Magesa.
“Ukweli
ni watu wazuri sana. Wanaonekana kukubeba, kama mtoto aliyezaliwa na mama G!”
Akasifia baba Naya. “Na ndivyo anavyonichukulia huyo mama, mpaka najisikia
vizuri.” “Mimi nimewapenda sana. Na nimewafurahia. Asante Joshua.” Naya
akaongeza. “Karibu. Sasa kabla hamjaondoka, naomba ni mzungushe rasmi Naya
kwenye hii nyumba. Najua mmechoka, ila naomba mnivumilie tu. Ni sawa baba
yangu?” “Bila shida.” Akajibu baba Naya. Joshua akamshika mkono Naya akimuongoza.
Zayoni akaomba na yeye azunguke aangalie. Joshua akawakaribisha wote kama
wangependa. “Najua mmechoka. Ila atakayependa kuongozana nasi, karibu.” Wote
wakawa wamehamasika, hakuna aliyelalamika kuchoka. Wakaongozana pamoja. Joshua
akawazungusha mpaka juu vyumbani nakuwaacha wakishangazwa na maendeleo yake.
“Kuna
sehemu ya mwisho naomba Naya aiangalie.” Naya akakunja uso akicheka.
“Nilifikiri umetuzungusha kila mahali!” “Bado. Sehemu hiyo nimeiacha maalumu
kwa sababu nataka kukuomba kitu.” “Nini tena?!” “Twende.” Akamshika mkono
wengine wakafuata nyuma mpaka nje. Wakatokea mlango wa ukumbini. Wakajikuta
nyuma ya hiyo nyumba. Napo pakawatoa macho zaidi. Palijengwa vizuri
sana.
“Hakika
umejenga hii nyumba kwa hali ya juu Joshua!” “Nashukukuru mzee wangu. Nilitaka
kumuomba rasmi Naya kama atakubaliana na ombi langu kuwa harusi yetu tufunge
hapa. Najua leo nimemshitukiza na mambo mengi mpaka na wasimamizi wa harusi
kabisa, lakini kuanzia sasa, hakutakuwa tena na suprise juu ya
harusi yetu. Nitakushirikisha.” “Suprise zote mpaka sasa
nimezipenda. Nimempenda Nanaa. Hujakosea hata moja.” Joshua akacheka kwa
kuridhika.
“Unafikiri
nakutania Joshua? Na kama Nanaa ndiye atanisimamia harusi, sina malalamiko
kabisa. Nitakuwa na mfano mzuri sana wakuiga. Aisee ni kweli wanapendana wale
watu. Geb na Nanaa! Aisee mwisho. Mimi nilikuwa nikiwaangalia kwa
kujiiba! Mpaka nikawa nawafurahia.” “Nilijua tu ungewapenda.” “Haya turudi
kwenye suprise ulizonifanyia. Pete yangu nzuri, tena sana.
Japo inatakiwa kubanwa kidogo. Inanipwaya.” “Hilo ni jambo la kwanza siku ya
jumatatu.” Akajibu Joshua. “Basi ujue hujakosea suprise hata
moja. Zote ni nzuri na ninakushukuru sana.” Joshua akacheka, wengine kimya
wakiendelea kuangaza macho.
“Na
kuhusu hapa? Maana nataka kuacha historia hata kwa watoto wetu na vijukuu waone
sehemu tuliyoweka historia. Maana haya makumbi huwa wanabomoa na kubadilisha
majina, ila hapa patabakia kwa muda mrefu. Silazimishii. Kama kuna
mahali ulishakuwa na ndoto za kuja kufungia ndoa, sitapinga.” Naya akajisikia
vizuri. Ndugu zake wote wakabaki kimya wakiendelea kuangaza macho, huku
wakisikiliza. “Sizani kama tutapata sehemu nzuri kama hii Joshua! Hapa ni
pazuri sana na sababu uliyotoa ni kweli na ya msingi. Tufanyie tu hapahapa. Ila
mwenzio bado nipo kwenye mshituko kwa yote yaliyotokea leo! Bado siamini!” Naya
akajiangalia kidoleni tena.
“Umeipenda?”
“Sana. Na zaidi ni kwakuwa inatoka kwako Joshua! Sikutegemea! Maana ni kama
hukua tayari!” “Hapana Naya. Wewe siku ile ulikaribia kuniharibia suprise yangu.
Ila nikashukuru ukatulia.” Naya akacheka. “Ila ungeendelea vile siku ile,
nilijiambia nisingekuacha umepoa vile. Ingebidi kukwambia tu. Lakini nilipoona
umekubali ninyamazie tu lile, nikamshukuru Mungu. Maana siku ile niliingia
nchini mapema zaidi ya muda ule uliponiona pale ofisini. Nilimuomba mzee hapa
tukutane mbali na nyumbani tuzungumze. Ndipo nikamuomba kama ataniruhusu
nikuoe. Tukazungumza vizuri. Tukawekana sawa, mpaka tukapata na muda,
akaniombea mimi kama Joshua! Ndipo nikaja kukuchukua kazini.” “HAIWEZEKANI
Joshua!”
“Muulize mzee hapa. Ni nyinyi tu ndio mlikuwa hamjui kinachoendelea ila
nilimuomba asiwaambie wote nyinyi.” Naya akamwangalia baba yake.
“Nini?”
Baba yake akamuuliza. “Mimi nilijua hunifichi kitu!” Naya akaongea akilalamika
kidogo kwa baba yake. “Ni kwa uzuri mama. Huoni jinsi ulivyofurahia?” “Sana.
Nimefurahi sana baba. Nampenda Joshua.” Wakacheka. “Hata mimi nakupenda
Naya. Naamini tutakuwa na ndoa nzuri sana. Umetulia na umejawa shukurani. Huna
makuu. Namshukuru Mungu kwa ajili yako.” “Asante kwa heshima kubwa uliyonipa
leo! Mbele ya watu wote wale! Zaidi kwa baba yangu! Unamuheshimu sana baba
yangu mpaka nafurahi. Hakika sikutegemea kila kitu ulichofanya! Nashukuru.”
Naya akajisogeza karibu akataka kusahau kama baba yake yupo hapo. Joshua
akacheka akimwangalia kama anayemkumbusha. Naya akaelewa akaishia kumkumbatia
kwa pembeni. “Naoana sisi utusaidie usafiri wa kurudi tu, Joshua. Naona usiku
umeendelea sana.” Naya akacheka akajua amekamatwa. Na Joshua akacheka. “Bila
shaka mzee wangu. Nakushukuru sana kwa kuniamini na Naya. Asante sana.”
“Nawaombea.” “Asante baba.” Na Naya naye akashukuru.
Akawagekia
Bale na Zayoni. “Na nyinyi nawashukuru sana kusimama na sisi leo kufanikisha
hili. Mmejituma vyakupitiliza. Asanteni sana.” “Mimi nimefurahi Joshua. Na
nimepiga picha nyingi sana.” Akadakia Zayoni. “Nimekuona. Nashukuru sana
Zayoni. Ujue uwepo wako hapa ni muhimu sana.” “Kweli?” “Kabisa. Unafikiri Naya
angejisikiaje yote haya yanaendelea kwenye maisha yake halafu wewe haupo hapa?”
“Kweli isingekuwa vizuri.” Wakacheka.
“Kama
tulivyozungumza na baba, kesho wote na kina Magesa tutakuwa kanisani kwenu
kujitambulisha kwa mchungaji, kisha nyumbani kwa kina Magesa. Angalau na nyinyi
mpafahamu kwao kama walivyoomba.” “Yaani yote hayo mmepanga na baba!?” Naya
hakuwa akiamini. “Kabisa. Baba amenisaidia sana. Majukumu yote yakuzungumza na
mchungaji, kumwambia kesho nakwenda kukuchumbia kanisani ameyachukua yeye,
amesema atanisaidia huko ili mimi akili itulie hapa.” Naya akatulia kama
anayetafakari. Wakamuona anacheka.
“Nini
sasa?” “Siamini kama kwenye lile kanisa na kwenyewe watashuhudia kitu kizuri
kinatokea kwenye familia yetu!” Wote wakacheka. “Nakushukuru Joshua. Hakika
nashukuru kwa hii heshima. Mungu akubariki mpenzi wangu.” “Sisi sote. Naamini
tutamaliza mambo yote salama.” Wakazungumza kidogo. Wakakubaliana kwa hili na
lile na kutoka wakikubaliana hata Bale atawasaidia kuimba ule wimbo siku ya
harusi yao. Kwamba waimbe wao watatu. Joshua, Naya na Bale.
Busu la Uchumba
Wakaingia
kwenye gari, Joshua akawasha gari kabisa akawa ni kama amesahau kitu. “Naya?”
Akageuka. “Naomba tushuke mara moja, kuna kitu nataka tuzungumze ndani.
Sitakawia mzee wangu.” “Bila shaka.” Akaafiki baba Naya bila shida. Naya
akashuka mara baada ya baba yake kuridhia. Joshua akaenda kumfuata na kumshika
mkono. “Twende.” “Umesahau nini!?” Joshua akamwangalia na kucheka kidogo.
Wakarudi mpaka ndani. Akamuongoza kupandisha ngazi mpaka juu kabisa chumbani
kwake na kufunga mlango kabisa.
“Ni
nini?” Naya akauliza na cheko kidogo. “Nimetafuta nafasi ya kupata busu,
nimekosa. Kila wakati kumekuwa na mwingiliano. Leo ni siku yetu Naya. Mwenzio
kwa mara ya kwanza, rasmi na baraka za wazazi ninajulikana na watu nina
mwanamke wangu! Siwezi kuacha siku kama hii Mungu aliyoniandikia historia ipite
hivihivi bila kupata busu kutoka kwako!” Naya akacheka na
kumsogelea. “Yaani unamsubirisha baba Naya garini kwa busu tu!?”
“Nimeomba anipe muda kidodgo, nipate hii nafasi ya pekee.” Akampokea vizuri kwa
kumshika kiunoni. Safari hii hata Naya aliona utofauti wa jinsi alivyomshika.
Alihakikisha amemkumbatia mpaka mikono yake imeelewa kuwa imegusa mwili wa
Naya. Akampa mabusu mazito mpaka Naya akayasikia. Kisha akawa na kiasi,
akamwachia. “Angalau moyo wangu umeridhika. Nimepata nilichokuwa nikikitamani.”
Akaongea Joshua akijaribu kuweka sawa nywele za Naya.
“Napenda
hivyo unavyonichezea nywele huku ukinibusu! Nasikia raha.” Joshua akacheka na
kumbusu shavuni. “Twende tusimuweke mzee muda mrefu zaidi. Umesema unaamini
Mungu atatujalia ipo siku na sisi tutakuwa na usiku wote sisi wenyewe
bila muingiliano wowote?” “Naamini hivyo Joshua, na asante, tena na tena kwa
heshima uliyonipa. Nimefurahi sana.” “Na mimi nashukuru sana kwa
kunikubalia kukuoa, maana ilikuwa hatua ya imani tu. Ungeweza kusema hapana, au
unaomba muda lakini ulikubali bila kujiandaa! Nashukuru.” Wakapeana mabusu tena
ndipo wakatoka.
Jumapili Baada ya Kuchumbiwa.
Nyumbani.
Naya
aliamka asubuhi akadhani yaliyotokea usiku uliopita ilikuwa ni ndoto tu.
Akakimbilia kidoleni na kujikuta akicheka peke yake. Alikaa pale akitafakari
hili na lile masaa yakizidi kusogea asiamini na yeye siku hiyo
anakwenda kutambulisha mchumba kanisani kwao! Tena Joshua! Mwanaume wa maana
wakuvutia! Anasindikizwa na kina Magesa! Furaha na shauku ya kufika kanisani
siku hiyo ikaongezeka. Akabaki akitafakari pale kitandani. Bale akagonga.
“Naya!” “Ingia tu.” Akaingia mpaka ndani.
“Toka
sasa kwenye neti!” “Wewe zungumza.” Bale akatoa chandarua na kukifunga.
“Hujisikii raha mpaka unikere! Unataka nini?” “Jana nimeona aina ya watu
waliokuja kwenye ile shughuli yenu. Ukweli Joshua anafahamiana na watu wa maana
sana! Ni kiasi cha kunyanyua simu tu na kuzungumza na mtu, mimi nikapata kazi.
Huu ukimya wa mpaka sasa unaniashiria pengine nilisha mboa tokea mwanzo.”
“Bale!” “Kweli Naya. Huyu mtu kumbuka alikuja hapa na ukayaona mahusiano yetu,
kama wewe mwenyewe ulivyosema. Nilimkumbatia Malon nikimpuuza yeye. Pengine
nilishamtoka moyoni. Unadhani ni sawa nikimuomba msamaha?” Naya akakaa.
“Tunashida
Bale, lakini si yanamna hiyo!” Naya akaongea kwa kujiamini sana akiweka
msisitizo. “Hutakuwa mtu wa kupenda watu kwa sababu wana vitu unavyohitaji
Bale! Hata Joshua atakushitukia. Mahusiano hujengwa si kwa kutumia watu.
Usimtake mahusiano Joshua kwa kuwa unadhani anao uwezo wa kukusaidia. Muweke
karibu kwa kuwa unaona ni mtu mzuri anafaa kuwa karibu na wewe. Tafadhali hilo
ukumbuke Bale. Kwa sababu zifuatazo. Mimi nakuamini wewe ni mtu mzuri, unayo
maamuzi sahihi kwenye kuchagua watu sahihi wakuwaweka karibu yako. Sikutegemei
umkimbilie tu Joshua na kuwa naye karibu kwa kuwa mimi nimemchagua. Na pia
sikutegea pia umfungie mlango kwa sababu unataka kuwa upande wa Malon kujinufaisha
naye!” Bale akabaki kimya. Naya kajua ni kweli.
“Nilitegemea
ungekuwa mtu wa haki na kutambua nani ni nani na wote kujua jinsi yakuishi
nao!” Kimya. “Sasa kwa kuwa umeshakosea Bale, ndipo nakuja kwenye sababu ya
pili. “Joshua ni mwangalifu sana na anajua kusoma watu. Utakapolazimishia
mahusiano sasa hivi ujue utaharibu zaidi mahusiano yenu yote yaliyobaki. Atajua
unataka kumtumia, kitu anachojua wengi wanamtaka sasa hivi sababu anacho.
Sababu ya tatu na ya mwisho pia mimi mwenyewe sitakuruhusu mfanyie
hivyo Joshua mtu mwenye moyo mzuri na hana hila ila kutuomba undungu tu tokea
siku ya kwanza anakuja hapa wewe ukamkataa. Sitakubali umtumie vibaya. Hapo
naomba uelewe Bale.” Naya akaendelea.
“Hata
akikutafutia kazi kesho na bado ukaona siye mtu unayetaka awe karibu yako, mimi
nitakuelewa kabisa. Usirudi kwa Joshua sababu ya kutaka kitu kwake ila kutambua
umuhimu wake kwanza kwangu mimi kama ndugu yako na pili iwe kwako. Hata kama
kwako haleti maana, ningetarajia angalau umkubali kwa kuwa ni mtu wangu mimi!
Napo silazimishii Bale. Ila kwa jinsi nilivyoishi na Joshua kwa muda mfupi,
nimemgundua ni mtu wa maneno yake. Haongei tu jambo ili kumfurahisha mtu.
Pengine huu ukimya tunao uona inawezekana anakusubiria wewe.” Bale akashangaa
kidogo.
“Kivipi
tena!?” “Anataka kujua upo serious kwa namna gani. Hiki kitu unakitaka kwa
kumaanisha au ni kitu tu cha kupoteza muda ukishapata kingine uache halafu
unakuwa umemuharibia yeye mahusiano na huko alikokuwa amekutafutia hiyo kazi!
Sijui kama unanielewa?” “Kwamba anahisi Malon anaweza kurudi akani...” “Sio
kuhisi, mimi nimemuhakikishia kuwa Malo lazima arudi.” “Naya!” “Wewe
humjui Malo kwa kuwa nimemfungua kwenu kwa upande niliotaka nyinyi mumfahamu.
Hili alilokufanyia wewe si geni kwakwe hata kidogo.” “Hawezi kurudi!” “Basi
ndipo utakapomjua Malon kwa uhalisia wake. Atarudi na sababu nzuri tu tena ya
kueleweka.”
“Na
mwanzoni kabisa, nilishamsikia Joshua akisema hivi, mwanadamu akiwa na shida
yake na akijua wewe unao uwezo wa kumpa hicho kitu, huwa anaongea chochote ili akipate
kile kitu.” “Naya!” “Sikudanganyi Bale. Na ndio maana yeye anasemaga
alishakataa kujiingiza kwenye usahili. Hafanyagi interview pale
kazini. Wanamjua. Mzito sana kuamini watu ni mpaka awe anataka mtu wake yeye
mwenyewe, lakini sio vinginevyo.” “Daah!” Bale akaishiwa nguvu kabisa.
“Ndio
maana mimi nakushauri utulie na umuonyeshe kwa vitendo, ulichomwambia unataka,
unamaanisha. Kwamba hata ikitokea anakupatia kazi sehemu basi hata ukipata
fulsa nyingine, utabaki kufanya kazi aliyokutafutia. Vile unavyomuona Joshua
hana watu wengi sio kwa sababu nyingine yeyote ile, ila amekusudia kabisa kwa
kuwa yupo makini sana na watu. Sasa naomba na wewe usiingie kwenye kundi la
watu wanaomlazimu kuwakwepa, maana Joshua atakuwa mume wangu. Mungu akijalia ni
mpaka kifo. Sasa sitaki uniweke kwenye wakati wakutafuta suluhu kati yenu
wakati mimi najua ni muda tu Bale. Iwe kwa kupitia yeye au la, utapata tu kazi.
Mimi sikutafutiwa kazi na Joshua, lakini nipo hapa. Naomba utulie ukijua
hujachelewa kama mwenyewe alivyokwambia. Tafakari maneno yake kwa sababu huwa
Joshua si mropokaji.” “Nimemuona.” “Basi tulia Bale, mimi nakushauri tu.” Naya
akaweka msisitizo.
“Na pia
naomba kukushauri kitu kingine, kuwa makini sana na jinsi unavyoshirikiana
na baba.” Bale akapoa. “Chunga maneno yako hata jinsi unavyomjibu hata akikukera,
kuwa makini. Baba anatuombea sana. Kwa kufunga na kuomba na anaamini
Mungu atatutendea mambo makubwa sana.” “Kama wewe?” Naya akacheka. “Na zaidi.
Jinyenyekeze tu kwake na kwa Mungu. Hata kama unaona unao uelewa mkubwa wa
mambo fulani fulani kuliko yeye, tafadhali tafuta hekima yakuzungumza naye sio
kumrushia tu maneno! Huwa inaniuma sana, na kwa kuwa huwa hakujibu, wewe hujui.
Lakini inamadhara makubwa sana, Bale. Kuwa makini jinsi unavyozungumza naye.
Usimchukulie kama vile mama alivyokuwa akimsema vibaya kwetu kwamba hana akili
ya maendeleo ndio maana mambo yake hayaendi.” “Simchukulii hivyo.” Bale
akapinga.
“Ndivyo
unavyoishi naye Bale. Hata jinsi unavyomkosoa jambo si kwa heshima na yeye huwa
ananyamaza tu. Nipo hapa nilipo na yote niliyonayo mimi, kwa sababu ya ushauri
anaonipa baba. Jumla yangu yote unayoniona nayo ni kwa sababu ya baba. Hata
huyo Joshua, nisingekuwa naye isingekuwa baba. Nazungumza na baba kuliko hata
Mungu. Mchana na usiku natumia hekima zake bila kukoma. Nikiwa hata kazini
jambo linapokuwa gumu nampigia baba, ananishauri na kunifanya niendelee. Mimi
niligundua mengi aliyokuwa akilalamikia mama ni kushindwa kwake yeye
mwenyewe kufikia ndoto zake wala haikuwa sababu ya baba. Kwani kuna wanawake
wangapi hapa duniani ni mamilionea! Wengine wameajiriwa na bado wanafanya
biashara. Yeye alishindwa nini kuyafanya yote hayo kama kweli alikuwa anataka
vingi! Kwa nini yeye alazimishie umilionea ni lazima utoke kwa baba tu!” Bale
kimya. “Kwa hiyo kuwa makini sana, usije jifungia baraka zako au
ukajichelewesha.” “Nimeelewa Naya.” Bale akatoka, Naya akafurahia hiyo nafasi
ya kuweza kuzungumza na Bale na akamsikiliza. Hakuwa akipenda jinsi
anavyozungumza na baba yao ilikuwa ni kama amechukua nafasi ya mama yake hapo
ndani, kuzungumza vibaya na baba yao.
Kanisani.
Joshua
aliwahi hapo nyumbani kwao kama kawaida yake bila ya kuchelewa. “Mama
umepania!” Naya akacheka sana kwa aibu. “Na wewe umependeza, mchumba wangu.”
Joshua akacheka sana. “Hapo umeifanya siku yangu kuwa nzuri zaidi.” “Hata mimi
bado siamini! Nimebaki nikijikumbusha tu.” Walikuwa wakizungumza Naya na Joshua
nje ya mlango alipoenda kumfungulia, maana Naya alikimbilia mlangoni. “Acha
nisalimie ndani kwanza.” “Ila asante kwa nguo. Si umeona ilivyonikaa vizuri?”
“Nimeipenda mwilini mwako zaidi kuliko ilipokuwa dukani.” Naya akacheka zaidi.
“Tunafanana rangi.” “Ndio lengo zima, si ndivyo?” “Kabisa. Acha nijimalizie
kidogo ndipo tuondoke.” “Utaharibu sasa Naya! Umependeza, hapo inatosha.”
“Kidogo tu.” Wakacheka na kuingia ndani, baba Naya alikuwa akiwasikiliza ndani.
Kimya kama kawaida yake kochini.
Joshua
akasalimia. “Nimeshazungumza na viongozi wa kanisa, nimewaambia juu ya
kuchumbiwa kwa Naya, na ugeni wenu leo.” “Nashukuru sana mzee wangu. Naomba
uniombee huko kanisani mambo yasivute ili tumalize hili swala mapema. Tufunge
ndoa yetu mapema.” “Naamini itakuwa hivyo, sioni sababu ya kuwachelewesha. Ila
pia nitajitahidi kuweka msisitizo kwenye hilo.” “Nashukuru sana mzee wangu.”
Joshua amehakikishiwa na baba mkwe, furaha ikazidi kuongezeka.
Naya na
familia yake wakatoka kuelekea kanisani bila ya kuchelewa. Joshua akiwa ndio
dereva, na baba Naya akiwa amekaa mbele, Naya kiti cha nyuma ya dereva, Joshua,
akiwa na pamoja na kaka zake.
Walifika
kanisani na kubaki nje wakiwasubiria kina Magesa. Nao hawakuchelewa. “Mimi namkubali
sana bibi harusi wangu. Upo wa viwango mno!” Nanaa akashuka garini na hizo
sifa. “Nanaa kwa ushabiki! Sasa hapo umeacha watoto wote ndani ya gari
umemkimbilia Naya!” “Kapendeza sana bwana! Wewe ungemsaidia Geb kushusha
watoto!” “Hata mimi nataka kuwahi kutoa sifa.” Mama G na Nanaa wakaanza kucheka
wao wenyewe na kufanya wengine wacheke. “Na nyinyi mmependeza sana.” “Mimi na
bibi harusi wangu tutakuwa gumzo!” Nanaa akaendelea kusifia. “Si umetuona baba
Naya?” “Nakuona Nanaa, binti yangu. Umependeza sana.” “Asante baba Naya. Ila
ujue nimepania.” Wote wakacheka.
“Na
watoto pia hutaki tena?” Joshua akacheka akimuuliza. “Nimeona nimuwahi Magesa.
Akija hapa atataka kutawala mazungumzo yote! Umependeza bwana harusi.”
“Nashukuru Nanaa. Na wewe umependeza sana.” “Na mimi nimependeza anko.
Niangalie.” “Sana Magesa. Hujambo?” Magesa alishushwa garini na baba yake na
kukimbilia hapo. “Sijambo. Mimi napenda miti mirefuuuu!” “Hapana Magesa.” Baba
yake akamuwahi akiwa bado garini akimshusha mdogo wake. Alimsikia. “Na mti huu
ni hatari?” Akauliza taratibu akisogelea mti. “Mti si hatari, lakini sitaki
wewe upande hapo. Kwanza utajichafua, pili utaanguka.” Baba yake akamjibu.
“Mtu
akipanda na viatu lazima aanguke. Lakini mimi mtoto mzuri, nitavua viatu.” “Dad
ameshakwambia hapana Magesa. Tulia.” Liv akamuwahi kaka yake akimuonya. “Mimi
nitakuwa mwangalifu na mami atakuwa na mimi akiniangalia nisianguke, au wewe
anko mwambie dad utahakikisha sitaanguka.” “Kwa kupenda kuuza kesi wewe!
Unataka anko ndio apambane na dad wako?” “Kwani wewe bibi unajua kule juu kuna
nini?” Magesa akauliza. Nanaa akazidi kucheka.
“Uje
umuulize baba yako aliyekukatalia kupanda. Usianze kunitesa kwa maswali mimi.”
Bibi yake akamkatalia. Magesa akabaki akiangalia juu ya mti. “Nanaa una watoto
wazuri!” Naya akasifia. Nanaa akaanza kucheka akiangalia wanae. “Asante mwaya.
Nashukuru Mungu. Wote ni wa miujiza hao. Upatikanaji wao ni wa kufa, kupona,
mpaka tukaamua kuweka kikomo.” “Kwani dad wewe unajua kule juu kabisa kuna
nini?” Magesa akamuwahi baba yake mara aliposogea na Jimmy. Wote wakacheka
walipomsikia bado anahabari ya mti tu! “Mimi nilifikiri kasahau!” “Hawezi hata
kidogo. Atang’ang’ania mpaka kesho atakumbuka.” “Nisikilize Magesa. Mbali ya
yale matawi tunayoyaona sisi wote hapa chini, hakuna kitu kingine kule juu.”
“Ume...” “Kabla hujaniuliza swali la pili kama nimejuaje, najua aina hii ya
miti. Haina matunda na hakuna kitu kingine juu ya huu mti.” “Labda nikaangalie,
leo inaweza kuwa kuna kitu.” Magesa akakazana kwa sauti yake ya tahadhari kama
asiyetaka kuharibu, wote wakazidi kucheka.
“Haiwezekani
Nanaa!” Naya akashangaa sana. “Hajamaliza hapo! Na usifikiri ni yeye peke yake.
Wote wapo hivyohivyo ila wengine wao huwa hawaongei ni kwa vitendo tu. Sasa
mimi na bibi yao huwa wanatuonea. Baba yao ndio kiboko yao. Anayajua majibu ya
maswali yao yote kabla na baada ya kuyauliza, na kuwajibu mpaka wanatulia. Haya
njoo mwanangu, maana huo mti hutapanda.” “Wewe mama hutaki kujua kule juu kuna
nini?” “Hapana Magesa, mwanangu.” Wakazidi kucheka vile Nanaa alivyomjibu.
“Mimi nataka tu kuingia mle ndani kanisani, nikaimbe na kucheza. Si nimekwambia
kwa nini tupo hapa leo?” Nanaa akamuuliza Magesa. “Sababu anko anataka
kutambulishwa hapa kama yeye ndio mchumba wa anti, ili wasije kumuiba mchumba
wake.” Magesa alijibu kwa ufasaha nakufanya watu wote wazidi kucheka.
“Wewe
Nanaa!” “Lakini si amepatia, mama jamani!” Geb akabaki akimwangalia mwanae.
“Haya twende tukaimbe ndani kanisani, acha mawazo yakupanda kwenye miti.” Bibi
yake akaongeza. “Wataimba wimbo wangu mzuri, bibi?” “Utamuomba mchungaji. Haya
ongoza njia.” “Ila nikiingia nisishike kitu labda...” “Hata kinanda usiguse,
Magesa.” Baba yake akamuwahi. “Labda kama nikiomba halafu wakaniruhusu?”
Wakaanza kucheka upya. “Sasa wewe Nanaa unaishije nao hawa watoto.” “Rahisi
sana. Ningekuwa naye mimi, ningeenda huko ndani kanisani na kumuombea apige
kidogo, roho imtulie na mimi nitulie.” “Haya tangulia Magesa.” Baba yake
akamkumbusha. “Lakini nisiguse chochote hata kama wakinikaribisha?” “Usiwe na
wasiwasi, hakuna atakaye kukaribisha.” Walicheka sana jinsi baba yake
alivyomjibu kwa haraka tena vizuri tu. Kweli akaondoka taratibu. “Huyo ndio
Magesa mwenyewe!” Nanaa akaongeza.
Geb
akasalimia wote kwa kuwapa mkono. “Nisalimie Jimmy.” Joshua akamwambia Jimmy
aliyekuwa akimwangalia Magesa akielekea kanisani. “Kwani huyu mtoto anaongea
kabisa, yaani kama vile Magesa?” Naya akauliza. “Subiri uone.” Nanaa akamtuliza
Naya. “Jimmy? Niangalie.” Baba yake akamuita. Akamwangalia. “Umemsikia anko?”
Akarudi kumwangalia Joshua. Akamsalimia vizuri tu. “Shikamoo anko Joshua.”
“Nanaa!” Naya akashangaa. “Nilikwambia nini ukiona watu?” Akamwangalia baba
yake, kisha akamgeukia tena Joshua. Akarudia tena kumsalimia ila safari hii
akampa na mkono. Akafanya kwa wote kisha akamwangalia baba yake. “Sasa hivi
ndio unaweza kumfuata Magesa.” Wakamuona akiondoka taratibu, Magesa naye akawa
anarudi akikimbia.
“Utaanguka
bwana Magesa, halafu ujichafue! Ni nini tena?” Mama yake akamuuliza. “Nilitaka
kumsahau mtoto!” Akawa amemfikia Jimmy. “Sijakusahau Jimmy, mtoto mzuri.
Nimekuja kukuchukua. Umesikia?” Wakamsikia akimuongelesha Jimmy kwa upendo
akamshika mkono kabisa akimuongoza kurudi ndani kanisani. “Ulifikiri
nitakuacha?” “Nilijua tu utarudi kuja kunichukua.” Wakamsikia Jimmy akimjibu
kaka yake huku wakielekea ndani kanisani. “Wewe Nanaa, kumbe anaelewa na
kuzungumza kabisa!?” “Sana.” Bibi yake akadakia. “Na anampenda sana yule mwenye
maneno mengi. Hasikii raha asipomuona, ndio maana macho yake wakati wote
yalikuwa kwake, na Magesa anampenda sana mdogo wake. Hataki alie.” Bibi yake
akaongeza.
“Mimi
nilishasalimia, dad.” “Nilikusikia Liv. Wewe mtoto mzuri sana.” Akamuona Nanaa
na mama G, wakikonyezana. Geb akawaona akacheka akitingisha kichwa. Wakajua
huyo ndio kipenzi cha Geb kwa hakika. “Baba Naya na Naya.” Nanaa akasengenya akimteta
Geb na Liv, wakacheka wote na kuelekea kanisani.
Uchumba Wa Naya Na Joshua Kanisani.
Ukatangazwa
uchumba wa Naya na Joshua na siku hiyohiyo likatoka tangazo la kwanza la ndoa
yao kama alivyoomba Joshua. Naya alijawa furaha na fahari ya aina yake.
Wakaitwa pale mbele ili kuombewa, Nanaa na Geb nao wakaenda ili kuungana nao
kwenye maombi. Joshua akataka tena kumvalisha ile pete pale kanisani. Naya
alishamvulia kabla hawajaitwa pale mbele, kwa hiyo Joshua alikuwa nayo mfukoni.
Akaruhusiwa. Akarudia tena kama usiku uliopita, tena na goti kabisa. Safari hii
Naya alikubali na cheko kubwa ila akambusu tena kiganja cha mkono ule uliokuwa
umemshika yeye Naya, alipopiga goti akimuomba amuoe, kama usiku uliopita.
“Nakupenda Joshua.” “Na mimi nakupenda Naya.” Ndipo akamvalisha. Watu wakaimba
na kushangilia wakimtukuza Mungu.
Lakini
gafla ukapita wakati wa ajabu ndani ya moyo wa Naya wakati yeye na Joshua
wamepiga magoti pale mbele kanisani ili waombewe. Akatamani sana hiyo siku mama
yake angekuwepo na yeye ashuhudie kinachoendelea kwa wakati huo kina mama
wengine wakipiga vigelegele wakishangilia. Akakumbuka jinsi mama
yake alivyokuwa akitamani aishie kuwa na mwanaume kama Joshua! Heshima
iliyowekwa pale kanisani na kina Magesa na huyo mchumba mwenyewe Joshua!
Akajikuta machozi yakimtoka na kuhisi kuna kitu hakijakamilika siku hiyo. Ile
simanzi ikataka kuiba ile furaha yote aliyoianzisha Joshua siku iliyopita.
Joshua akamuona wakiwa wamepiga magoti. Akamwangalia vizuri kwa kuinama
akimchungulia usoni, akagundua yale sio machozi ya furaha.
Akajisogeza
karibu zaidi. “Vipi?” “Natamani mama angekuwepo Joshua! Naumia kuona
haya yote yananitokea halafu ameshindwa kushuhudia! It’s not fare.” Akasikia
kuumia zaidi. Joshua akakumbuka kusimuliwa habari za mama Naya jinsi alivyokuwa
akihangaika kumlazimishia wachumba walioonekana wamejijenga kitaaluma. “Pole
sana Naya. Pole. Ila tumuenzi kwa kuhakikisha hili tuliloanza, tunalikamilisha
kwa heshima.” Joshua akajisahau kama wapo madhabahuni, akamuwekea mkono juu ya
mabega akamvuta karibu ubavuni. Akimsugua pembeni ya mabega taratibu. Naya
akajilaza hapo ubavuni vizuri. “Tutakuwa sawa tu. Tuamini Mungu tutakuwa kile
mama alitamani kukiona kwako.” Joshua akamnong’oneza sikioni, wakati watu
wakiendelea kutulia wakirudi kwenye viti vyao ili waombewe baada ya kuvalishana
pete tena. Wakabaki wachungaji, wazee wakanisa na hao wasimamizi wao kina
Magesa. Watu walipotulia ndipo wakaombewa.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ndipo
mchungaji akaanza mahubiri akisoma habari ya Yesu kutembea juu ya
maji, na Petro kutaka na yeye atembee, akamuomba Yesu amuamuru
atembee juu ya maji kama yeye. Kila mtu alikuwa ametulia kabisa, wakisikiliza.
Wakashitukia Magesa anaanza kuongea. “Mama yangu alinisomea kutoka kwenye
bibilia. Kitabu cha Mathayo 14, mstari wa 22 kuanzia pale.” Watu wote
wakamgeukia Magesa.
Wazazi
wake walibaki wamepigwa na butwaa. Watu wakampigia makofi, Magesa akapata moyo
akasimama kabisa juu ya kiti alichokuwa amekalia ili awaone watu wote. “Ila
nilimwambia mama, Petro alizama sio sababu ya kukosa tu imani. Alikuwa hajaamua
kwa moyo wake wote kutembea juu ya maji. Ukitaka kufanya jambo lako, ukiamua,
unakusudia, halafu unafanya kwa moyo wako wote, utashangaa huogopi na huzami.”
“Watajuta kutukaribisha hapa!” Bibi yake akaongea na kufanya watu wacheke.
“Kweli
tena. Mimi sisemi uongo. Si ni kweli mama?” “Kweli huwa husemi uongo, baba
mzazi. Haya shuka basi hapo juu.” “Mmemsikia mama yangu? Kwa hiyo ukitaka
kufanya jambo, kusudia kutoka moyoni na ufanye. Hata kama unataka kupanda
kwenye mti mrefu sana, usiogope.” Ilibidi mpaka baba yake acheke na
kutingisha kichwa. “Nilijua tu hayajaisha! Magesa mwanangu wewe! Jambo la
kupanda mti mpaka sasa hivi unalo tu? Shuka baba.” Nanaa akamsihi mwanae
taratibu, watu walikuwa wakicheka sana na kumpigia makofi.
“Haya,
naomba ushuke hapo kwenye kiti Magesa, na uje ukae hapa.” Baba yake akaamuru. “Nisiombe
tena ule wimbo wangu aliosema bibi nimuombe mchungaji?” Akauliza na kufanya
watu wazidi kucheka. “Umeona mama wewe!?” “Mimi nilitaka atulie bwana. Sikujua
kama kweli mwenzangu atayabeba tena mpaka huku kanisani!” Mama G, akajibu
akicheka. “Magesa, sitaki kurudia mara ya pili.” Baba yake akaweka msisitizo.
Magesa akapoa gafla baada yakuona sura ya baba yake. “Au labda nikae
hapahapa pembeni ya mama yangu, ila nisiongee tena?” Watu wakazidi kucheka.
Baba yake alivyomtizama bila kujibu, akashuka taratibu. “Labda mama ananitaka
mimi?” Akamuuliza baba yake kwa sauti ya wasiwasi. “Wewe hutanyamaza mpaka ukae
karibu na dad, Magesa. Kila mtu anakujua. Hapo utaongea tena wakati
ulishaambiwa na dad tokea zamani, mchungaji akiongea kanisani, usiingilie.” Liv
akamwambia kaka yake taratibu kwa sauti yake ya chini.
“Wewe
mama unanitaka nibaki hapa?” Akamuuliza mama yake kwa upendo akionyesha
ameshaingiwa hofu. “Sasa hapo na nyinyi mnaanzisha ibada yenu, na kumfanya
mchungaji ashindwe kuendelea.” Mama G akawashitua. “Muahidi dad hutaongea tena,
mpaka ibada iishe, halafu ndio nikuombee urudi ukae hapa.” Mama yake akamwambia
watu wote wakiwasikiliza. “Mimi sitaomba hata ule wimbo. Nanyamaza kabisa.”
Akaongea kwa upole akimtizama baba yake na sura ikawa kama Jimmy vile na macho
yao ya upole na ya kurembua kama baba yao.
“Mimi
naona nikae tu hapa na mami. Si sawa dad?” Akiishaita ‘mami’, wanajua
ameogopa. “Mjibu bwana Geb, ataanza kulia sasa hivi, wote ibada ituishie
hapahapa!” Nanaa akamsihi. “Lakini mtoto amemaliza ibada nzima na ameongea
vizuri sana.” Akaingilia mchungaji kama kumtetea. “Mimi naitwa Magesa.” “Umeona
mama? Huyo hawezi kunyamaza mpaka akae karibu na dad.” Liv akadakia “Kwani mimi
si nimejitambulisha tu?” “Hakuna hata aliyekuuliza jina lako Magesa!
Umemuingilia tena mchungaji.” Liv akaongeza kwa sauti yake ya chini. “Magesa?”
Baba yake akaweka msisitizo. Akaanza kulia huku akimsogelea baba yake macho kwa
mama yake.
“Mimi
nishakuwa mtoto mbaya, mami?” “Mimi nilijua tu jamani! Na hili kanisa
nalo mpaka litatujua! Nyamaza Magesa mwanangu. Wewe usilie.” Nanaa akalalamika
kwa sauti ya chini. “Mimi nimeshaharibu natakiwa kuwajibika tu?” Magesa
akauliza na kilio juu, watu wakazidi kucheka.
“Si
niliwaambia mimi? Hapo mshaanzisha ibada yenu ya vilio, kinachofuata ni
kutapikia watu hapa, wote turudi nyumbani.” Mama G naye akalalamika. “Haya Geb
na familia yako simama.” Mama G akaongeza. Geb akasimama akijua ndio anaambiwa
na mama yake watoke. “Twende Magesa.” “Bila mami wangu, mimi!?” Akamuuliza
baba yake akilia sana. “Mimi nashauri niende tu na mami wangu
jamani!” Magesa akazidi kulia. “Haya, Nanaa na wanao tokeni mtupishe
humu, ibada iendelee.” “Mama jamani! Si Geb anatoka naye?” “Nenda bwana Nanaa!
Wewe unajua mwisho wa yote utakuja tu kuitwa, ametapika na bado analia.
Naombeni tokeni. Haya Geb ongoza njia, mkeo na watoto wanakufuata nyuma.
Mkaendeleze ibada yenu huko nje, na sisi tuendelee na ya humu ndani. Haya
tangulia.” Geb, Liv na Jimmy wakatoka. Kanisa lenyewe lilikuwa dogo tu, kama
darasa kubwa tu, hata hapakuwa pakubwa sana.
“Mimi
nimeshaharibu mimi! Nimekuwa mtoto mbaya.” “Wewe sio mtoto
mbaya, Magesa mwanangu.” “Bado mimi ni mtoto mzuri, unamshukuru Mungu
amekupa mimi?” Watu wakazidi kucheka, Magesa anauliza huku akilia, mama
yake anakusanya mizigo yao watoke. “Ndiyo Magesa, mwanangu. Nyamaza
sasa.” “Nikiendelea kulia ndio naharibu zaidi, Mami?” “Nanaa
na mwanao naombeni mtoke. Wenzenu washatangulia nje, bado nyinyi wawili tu.
Kinachokufanya hutoki ni nini bwana!” “Nakusanya mizigo yetu yote maana
tunaweza tusirudi tena humu ndani. Ila sasa sioni tai yake huyu si unamuona
anavyolia na kuvua shati kirahisi tu? Hana tai ndio maana.” Bibi yake
akamtizama pale aliposimama Magesa akilia huku akikunja shati lake mpaka
kifuani akilifungasha kama kifurushi.
“Tai iko
wapi Magesa?” Bibi yake akamuuliza. “Nimeweka kwenye kapu la
sadaka.” Watu walianza kucheka tena. Nanaa aliposikia hivyo akasimama
wima kama mshale kwa mshituko na kuweka kila kitu chini. Magesa akamuona vile
mama yake alivyoshituka. “Nisingetoa na saa yangu sadaka pia, Mami?
Nimezidi kuharibu?” “Jamani Magesa!? Na saa pia umetoa sadaka!?” Watu wakazidi
kucheka. “Kama yule mama mjane Yesu alimsifia ametoa vyote alivyonavyo!
Unamkumbuka mami?” Nanaa akabaki akimwangalia kwa mshangao. Mpaka bibi yake
alikuwa akicheka.
“Umemsahau
tu mami. Hata Yesu alimsifia akasema yeye ndio ametoa nyingi zaidi kuliko wote
kwa kuwa ametoa vyote alivyo navyo. Kwenye kitabu cha Marko 12 mstari wa...” “Nakumbuka
Magesa mwanangu!” “Ila leo nimeharibu zaidi sikutakiwa kuwa kama yule mwanamke
mjane, tena masikini?” Watu wakazidi kucheka ila kushangazwa naye jinsi
anavyokumbuka maandiko.
“Leo
sikutakiwa kulitendea neno kazi?” Magesa akazidi
kumuhoji mama yake aliyekuwa ameduaa akimwangalia. Watu wakizidi kucheka. Yeye
mwenyewe akilia sana huku akiuliza na kukusanya shati lake kifuani, alishalichomoa
kwenye suruali. “Mnachelewesha ibada bwana!” “Sababu
yangu mimi, bibi? Mungu hataki saa kwa sababu anajua muda na wakati. Mimi ndio
natakiwa kujua muda?” “Kumbe unakumbuka
ulivyoambiwa na baba yako mara ya mwisho ulipotoa saa yako sadaka? Sasa leo upo
matatizoni zaidi. Wewe hufanyii kazi mafundisho ya wazazi, unataka kuyafanyia
kazi yale ya kwenye bibilia tu, tena unayoyapenda na kuyachagua wewe. Sasa leo
upo matatizoni.” Akazidi kulia kwa hofu.
“Jamani
mimi nipo matatizoni!” Watu wakazidi kucheka. Baba yake akarudi na kumbemba pale
alipokuwa amesimama akilia huku akimtizama mama yake kama akimtaka amuhurumie.
Geb akamtoa hapo ndani juujuu akilia. “Ningemsubiri tu mami
wangu jamani!” Magesa akasikika huko nje akilia kwa sauti. “Sasa na wewe
uwahi, maana kinachofuata hapo nje ni kutapika, halafu njaa, anataka kula,
safari ya kurudi nyumbani inaanza tena wakati ibada ndio ipo katikati.” Mama G
akaweka msisitizo, Nanaa akarudi kunyanyua vitu vyake na watoto wake alivyokuwa
amekusanya na kuvitupa tena chini baada ya Magesa kusema ametoa sadaka tai na
saa yake.
“Samahanini
sana jamani.” Nanaa akaomba msamaha akitoka. “Lakini hakukosa. Aliongea vizuri
sana.” Mchungaji akasifia kama akituliza hasira za wazazi na yeye alikuwa
akicheka. “Bora tu watoke baba. Huyo mtoto kukihubiriwa kitu anachokijua,
hawezi kunyamaza. Mahubiri yote atakuwa ni yeye tu akichangia, hutaongea ujumbe
wako. Makanisa yote wanatujua. Waache tu watoke. Watarudi mwishoni kabisa,
tuimbe nao kama hawatalemewa huko nje na kuondoka moja kwa moja.” Watu wakazidi
kucheka. “Mama naye kutusemelea mpaka kwa mchungaji mpya jamani!” Nanaa
akaongea akitoka.
Naya
akamfuata. “Wewe rudi tu ndani. Leo siku yako. Hii fujo niachie tu mimi
mwenyewe. Nishazoea.” “Au tumpeleke kwa watoto?” “Huko ndio baba yake atalala
jela leo. Hajuagi kutulia Magesa mwanangu. Akifika huko atapanda kila mahali
huku akitaka aongee yeye kila kitu. Na mwili wake ule anaweza akaangukia mtoto
wa watu, akamvunja hata shingo.” “Nanaa!” “Nakwambia kila kanisa tulilowahi
kwenda tunajulikana kwa majina yetu wote sisi! Ndio maana unawaona wote tunakuwa
nao ibadani kama watu wazima, sababu yake huyo.” “Anatapika!” Wakamsikia
akitapika huku akilia sana.
“Ndio
kazi yake huyo. Mtundu, maneno mengi, lakini muoga kupitiliza. Sasa hapo yupo
na baba yake mimi sipo ndio hofu inamzidi. Acha niende ndipo atatulia,
tutarudi.” “Kwani huwa anamchapa?” “Chakushangaza, mimi na bibi yake ndio huwa
tunamchapa, lakini haniogopi hata. Baba yake hajawahi kumchapa hata mara moja,
ila akimuita tu, kama amekosa, ndio kilio kama hivyo.” Naya akazidi kucheka.
Joshua
naye akatoka. “Tuwasaidie?” “Wala msijali. Ndio nilikuwa nikimwambia Naya,
arudi tu ndani, na sisi tutarudi baadaye kidogo akitulia. Kwanza hana muda
mrefu, atachangamka sasa hivi, tutarudi. Acha nimuwahi.” Wakacheka, Nanaa
akaondoka na mabegi yake. Naya na Joshua wakarudi ndani.
Baaada ya
kama dakika 15 hivi, Geb na familia yake wakarudi tena, Magesa akiongoza njia.
Mama G akaanza kucheka kimyakimya. “Sasa hivi siongei tena, bibi.” Magesa
akanong’ona kwa sauti ya juu akimwambia bibi yake huku akimsogelea. “Hapo mbona
unaongea?” Bibi yake akamuuliza. Akafunga mdomo na mikono yake yote miwili kwa
haraka na kumgeukia baba yake akamkuta akimtizama. Akatingisha kichwa
akiashiria kukataa. Alikuwa amebadilishwa mpaka nguo. Yeye peke yake,
akiashiria alijitapikia.
Walipokaa,
Joshua akamwangalia na kumuonyeshea ishara aende kwake. Akamgeukia baba yake
kama anayemuomba ruhusa, akamkubalia akanyanyuka kwa haraka na kumfuata Joshua
pale alipokuwa amekaa. “Sasa hivi siongei tena anko. Lasivyo tunarudi nyumbani
wote. Inakuwa namuingiza na mama yangu matatizoni pia. Hamsikilizi mchungaji,
tunafukuzwa naye makanisani.” Magesa akanong’ona kwa sauti ya juu tena,
nakufanya watu wacheke tena. Baba yake akatingisha kichwa kwa masikitiko. “Huku
pia tunakusikia wewe Magesa.” Bibi yake akaongeza kwa sauti ya chini, Magesa
akafunika mdomo wake tena kwa haraka na mikono yake yote miwili. Akamgeukia
mama yake wa kwanza kisha baba yake, akakuta wote wakimtizama. Akaanza
kutingisha kichwa tena akiashiria ishara ya kukataa huku akiwatizama wazazi
wake na mdomo kafunga, ndugu zake kimya wakimtizama.
Baada ya
ibada kuisha, Joshua alikuwa amemwandikia mchungaji kikaratasi akiomba mwishoni
kabisa tai ya Magesa na saa aliyotoa sadaka vipigwe mnada na aimbe. Na kweli,
baada ya kufunga ibada mchungaji akatangaza kutakuwa na mnada wa tai na saa ya
Magesa. Watu wakashangilia sana, na kuhamsika na ndipo alipomkaribisha Joshua.
Wakashangaa anakwenda na Magesa pale mbele. Joshua akachukua gitaa la bezi,
akasimama kwenye kipaza sauti, Naya akamkabidhi Magesa kipaza sauti kingine na
yeye akachukua chake. Bale akaenda kwenye kinanda.
“Upo
tayari Magesa?” Joshua akamuuliza. “Si umesema tutaimba wote?” “Ila wewe
unaanza, halafu anafuata anti Naya, mimi halafu anko Bale. Ila tunataka wewe
ndio utuanzishie wimbo wako.” Magesa akafurahia sana. “Mama utacheza?” “Mimi
naona ungeanza tu kuimba mwanangu.” “Au uje hapa?” “Mama yako hajui kuimba
bwana, wee! Acha kupoteza muda.” “Mama wewe! Ujue mimi nimwimbaji sana!” Nanaa
akashangaa kwa sauti akijitetea. “Mmmmh!” Mama G akaguna. Watu wakacheka,
hakuna aliyetoka. Bale akaanza kupiga kinanda, Joshua akapokea. Na mpiga ngoma
hakuwa ametoka kwenye kupiga ngoma. Akawapokea wimbo wa, ‘Hakuna Mungu
kama wewe, Hakuna Mungu kama wewe. Hakuna Mungu kama wewe, hakuna na hatakuwepo.’
Akaanza Magesa vizuri tu akionekana kweli ni wimbo wake na huwa anaupenda sana.
Kisha akapokea Naya, alipokuja Joshua, ndipo kila mtu akashangilia sana.
Aliimba kwa hisia zote, tena kwa sauti tofauti tofauti. Magesa
alikuwa akicheza sana. Akaja kupokea kuimbisha Bale, akarudia Joshua akipiga
gitaa vizuri na kwa ustadi, wakaimba wote mpaka wakamaliza. Watu walishangilia
sana kwani waliimba vizuri kama waliokuwa wamejiandaa kwa huo wimbo siku hiyo.
Ilipokuja
swala la mnada wa tai pamoja na saa, Mchungaji akawaambia anayetaka upako wa
Magesa anakaribishwa kushiriki. Wengi walianza kwa kutaja bei, wakaishia
mwanzoni kabisa kwani wakabaki Joshua na Geb wakishindana mpaka kufika
mamilioni. “Hakika Geb lazima uniachie. Mimi na Naya tunataka huo upako wa
Magesa nyumbani kwetu.” “Lakini ni nini Joshua! Mimi nimehangaika kutafuta aina
hiyo ya tai, muulize bibi yake ndio maana umeona wote, yeye na Geb wananisaidia
kuweka pesa nyingi ili virudi nyumbani! Nimefanya kazi ya kuagiza, Joshua
bwana! Hiyo tai ni ya tofauti, inafanana na mkanda wake pamoja na viatu vyake.
Acha bwana!” Nanaa akalalamika. “Nashauri huko ulikotoa hii, ukaagize nyingine.
Hii inakwenda kwetu.” Joshua na Nanaa wakabishana tena. Joshua akaongeza pesa.
Geb na yeye akaongeza. Watu wakazidi kucheka. Maana yeye Geb alikuwa akitaja tu
pesa, Nanaa na Joshua wao ndio wanabishana.
“Hakika
tutakesha hapa.” Joshua akaweka angalizo. “Tukifika nyumbani nitawapa tai
nyingine hata na saa yake nyingine hivyo niachie Joshua bwana!” Nanaa
akabembeleza. “Sisi tunataka hivi alivyomtolea Mungu sadaka.” “Mama alishasema
mimi ni mtoto mzuri.” Magesa akakumbushia alivyoona mama yake akihangaikia
kurudisha hivyo vitu vyake kama ishara ya kumkumbusha asije kumgeuka wakirudi
nyumbani. Watu wakacheka.
“Wewe ni mtoto
mzuri Magesa.” “Kwa hiyo unataka upako wangu, anko?” “Ndiyo Magesa.” Akajibu
Joshua na kuongeza pesa. Geb akacheka na kutingisha kichwa. “Basi Joshua. Naona
kweli umekusudia.” “Geb jamani!” Nanaa akalalamika. “Ni siku yao leo.” Watu
wakashangilia sana. Joshua akaandika hundi na kumkabidhi aliyekuwa akifanya
mnada huo, akachukua tai na saa ya Magesa. Watu wakashangilia sana na
kushangazwa na hiyo pesa iliyopatikana sababu ya hivyo vitu viwili tu.
Mchungaji akashukuru, wakaondoka.
Nyumbani Kwa Magesa.
Walikaribishwa
vizuri sana nyumbani kwa kina Magesa. Baba yake Nanaa naye alifika hapo pamoja
na James kwa ajili ya chakula cha mchana pamoja. Zikaanza stori na vicheko.
“Leo Magesa amefanya nini tena? Mbona yupo tena kwenye kona yake ya adhabu? Leo
anahesabu mpaka ngapi?” James akauliza akicheka huku akimwangalia Magesa pale
alipokaa akihesabu, Jimmy akimsubiria pembeni yake ili amalize, aruhusiwe,
wakacheze. Kina Naya ndio wakaelewa ndio adhabu yake kila wakati. “Na leo
kamuingilia tena mchungaji kanisani. Ndio ameambiwa asinyanyuke pale, wala
asiguse kitu chochote kile, hata akimaliza kuhesabu atulie kimya. Akiongea tu,
au akisogea pale bila kuruhusiwa, anaanza kuhesabu upya.” Bibi yake akajibu
nakufanya wote wazidi kucheka. Geb akarudisha macho kwa Magesa. “Leo anahesabu
mpaka ngapi?” James akauliza akizidi kucheka. “Dad amemwambia ahesabu mpaka
elfu moja.” Akajibu Jimmy akimwangalia kaka yake. “Hapo anatamani achapwe, yaishe,
aendelee na shuguli zake kuliko kuwekwa hapo chini akihesabu.” James akaongeza.
Wakazidi kucheka wakimwangalia vile alivyopoa usoni huku akiendelea kuhesabu
taratibu.
Ukweli
Nanaa alikuwa mkarimu sana na walionekana kumkumbali pia Naya. Akamuonyesha
picha zake za harusi, Naya akagundua wao walifunga ndoa wakiwa na watoto wawili
tayari na Nanaa alikuwa mjamzito wa Jimmy. Akatulia akitafakari akakumbuka kisa
Nanaa alichomwambia baba yake usiku uliopita nyumbani kwa Joshua, juu ya
vipingamizi walivyopitia kabla ya hiyo ndoa. Akatamani kumfahamu zaidi Nanaa na
historia yake binafsi mpaka kubahatika mwanaume kama Geb! Akajaribu kujiweka
kwenye nafasi ya Nanaa. Akafikiria ndio angekuwa yeye amezalishwa hao watoto
watatu na Malon! Hofu ikamuingia kidogo akitafakari mwisho wao
ungekuwaje! “Wala sisi tusingeweza kuishia kama hivi Nanaa na Geb. Sasa
hivi ningekuwa na wanangu wote, Kiluvya kwa baba Naya, tunamsubiri Malon akili
imrudie, tuanze tena!” Naya akawaza kwa hofu. Akamshukuru Mungu
alitoka peke yake kwa Malon, sio na msururu wa watoto.
Walikuwa
wamewaandalia haswa ni kama waliacha vyakula vingine wakiwa
wameshapika. Wakasaidiana na msichana wakazi kuweka vyakula mezani wakati
wakiendelea kuzungumza na Naya kuangalia album za picha kuijua hiyo familia
zaidi.
Kweli
aligundua Geb ni mkimya sana. Na ukimya wake ukaongezwa zaidi alipokuja James
ambaye alimtambulisha Joshua kwao, kina Magesa. James yeye alisema hata
kanisani hakwenda, ametokea kazini siku hiyo kulikuwa na dharula. Akaongezeka
na baba yake Naya, naye mcheshi kama mwanae Nanaa. Wakaanza mazungumzo
wakicheka na utani mwingi kwa mama G, hapo ndipo Geb alinyamaza kabisa akicheka
hapa na pale ila kusikiliza kwa kila anayechangia.
Naya
alishamuona Bale akituma jumbe kwa muda mrefu tu nakushindwa kuwepo pale
kimawazo. Hakuchangia lolote muda wote macho kwenye simu akisoma na kurudisha
majibu. Akawa kama anachati na mtu kwa muda tu, kitu ambacho si kawaida yake.
Naya akamwangalia baba yake, akagundua na yeye anamtizama Bale. Wakamuacha. Kwa
kuwa alikuwa katikati ya watu, lakini akituma jumbe zake tu kama hayupo pale au
amepuuza kinachoendelea pale. Kisha wakamuona anatoka nje kwa haraka. Hakurudi
mpaka walipohamia mezani. Ikabidi Naya amfuate nje. Alipomuona ni
kama akakata simu kwa haraka na kuirudisha mfukoni. “Vipi?” Naya akamuuliza.
“Ndio nilikuwa nataka kurudi ndani. Akamsogelea na kumpita Naya aliyekuwa
akimfuata pale nje. Naya akashangazwa kidogo, ila akamuacha tu.
Wakapata
wakati mzuri sana kwa kina Magesa, mipango ya wapi kutafuta nguo za harusi na
wasimamizi ikaanza. Nanaa akiwa amechangamkia kweli hiyo harusi, mumewe
akimtizama tu anavyoweka mipango na Naya. Mpaka wanaondoka pale, Naya akawa
ameshapatwa na hamu ya harusi.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Safari ya
kurudi Kiluvya ikaanza. Lakini Naya akagundua Bale yupo kimya na kama mwenye
wasiwasi hata na kutizama simu yake pale mbele yao. Akarudisha mawazo kwa
Joshua. Wakaanza kukumbuka vituko vya Magesa, mpaka baba Naya alikuwa akicheka
sana. “Halafu huwezi kumuelewa Magesa! Ni kama mpole sana, asiye na hatia
kabisa. Lakini...” Baba Naya akaongeza nakufanya wazidi kucheka kila
wakikumbushana hili na lile la Magesa.
Walifika
nyumbani ikiwa imeshafika saa moja usiku. “Ni sawa nikibaki kidogo, au
unafikiri niwaache tu mpumzike?” Akamuuliza Naya walipobakia peke yao nje
wengine wakiwa wameshaingia ndani. “Jamani Joshua! Naomba ukiwa hapa uwe huru
bwana. Pafanye hapa kama nyumbani.” “Unafikiri iwe wakati huu au angalau
tukishaoana?” “Baba anakupenda na kukuheshimu sana Joshua. Tafadhali kuwa huru.
Mimi pia nataka tubaki wote.” “Kama ndio hivyo sawa.” Wakapeana mabusu ya wizi
ya harakaharaka hapo nje ndipo wakaingia ndani.
“Acha
nitayarishe basi hata chai kama wote mnasema mmeshiba.” Naya akaingia jikoni
baada ya kubadili nguo, Joshua amekaa na baba yao hapo sebuleni. “Nikusaidie?”
Joshua akauliza. “Napika chai ya rangi tu, wala sitachukua muda mrefu. Nisubiri
tu nakuja.” Wakatulia pale sebuleni, Bale mezani kimya. Naya alitengeneza chai
ya tangawizi nzuri ikawa inanukia na hiliki, akaanza kuwagawia.
Bale.
“Mimi
naomba niwaage jamani.” Kila mmoja akamgekia Bale pale mezani. “Naona milango
imefunguka, nakwenda Mbeya.” “Kwa Malon!?” Naya akamuuliza kwa mshangao sana.
“Sio kwa Malon, ila kufanya kazi kwenye kampuni yake. Amenieleza sababu
ya kuniacha. Ameniambia alikuwa na nia nzuri tu ili nitengeneze mambo ya hapa
nyumbani kwanza. Hakutaka kunichukua wakati ule, katikati ya kutoelewana na
familia.” “Bale!” “Subiri kwanza Naya. Maana mimi sio mjinga. Nina akili zangu
timamu, sio mtoto mdogo.” Hapo Bale akawa mkali.
“Ameniuliza
kama niliweza kusuluhisha na tukapatana.” “Leo hiyo!?” Naya akamuuliza kwa
mshangao. “Ndiyo. Pale tulipokuwa kwa kina Magesa na ndipo nikatoka kuzungumza
naye. Malon anasema yeye alikosa nafasi ya kuwa na familia kama hivi mimi,
hataki aone mimi naangamia ndio maana aliniacha ili nitengeneze kwanza. Akataka
kujua kama ipo amani. Nilipomwambia hata wewe ulinisamehe na kunipa baraka zako
juu ya kwenda naye tena siku ileile, na ukanisaidia mpaka kufungasha kabisa. Na
nikamwambia kwa wakati ule tulikuwa wote kwa kina Magesa, ulichumbiwa jana yake
na siku hiyo kanisani pia na tukaimba pamoja, ndipo akasema kama ndio imekuwa
hivyo basi ni sawa. Anasema yeye bado yupo tayari kusimama na mimi.” “Bale?”
Naya akamuita taratibu tu.
“Sasa
mbona husubiri nimalize? Au wewe unaona ni sawa hivi ninavyokaa tu nyumbani
wenzangu wote wanakazi na kutengeneza pesa? Angalia wale vijana wenzangu pale
kanisani! Wote wanakazi zakueleweka.” “Sasa wale kina Ino si walitutangulia
shule! Unawezaje kujiling..” Naya akamwambia, kabla hajamalizia baba yake
akadakia. “Kwanza hujalingana na Ino wewe. Maana najua ndiye anayekuumiza
kichwa.” Baba yake akaongeza.
“Mimi
sijaelewa jamani! Mnataka nini kwangu? Mnataka tu nikae hapa nyumbani niendelee
kulia shida au nichukue hatua? Maana kama mlango umefunguka, ni kwanini mimi
nisichukue hatua?” Joshua kimya kama Zayoni. “Angekuwa ni Naya, najua kwa
hakika ungemkubalia na kumuunga mkono. Lakini mimi unanipinga, na sijui ni
kwanini, baba?” Bale akafoka kwa ukali kabisa. “Punguza hasira Bale!” “Hapana
Naya. Kunakuwa kama kuna upendeleo hivi! Wewe ulianza kufanya kazi tokea upo
kidato cha tano, sijui! Lakini mbona uliruhusiwa? Tena ulikuwa ukifanya mpaka
kazi za usiku! Hatukuwa hata tukimjua mwajiri wako! Mimi mtoto wa kiume nataka
kufanya kazi, tena kwa mtu ambaye wote tunamfahamu, ni Malon. Na wewe
baba ulienda ukafanya kazi huko, ukasema yapo mazingira mazuri sana. Ukamsifia
sana Malon. Sasa kwa nini leo mimi ndio naonekana sistahili! Au wewe
baba unanionaje mimi!? Kwamba Naya ndiye mwenye uwezo wakuhimili mambo fulani
fulani lakini si mimi?” Bale akamuhoji baba yake akiwa anawakwa hasira kabisa
bila hata kumjali Joshua. Kimya.
“Wakati
mwingine mpaka natamani mama angekuwa hai, pengine na mimi ningepata mtu
wakunitetea na angeelewa nia yangu ya maendeleo.” “Ni nini Bale!?” “Hapana
Naya. Huku ni kunidharau! Kwamba wewe mtoto wa kike unao uwezo mkubwa kunizidi
mimi! Wewe umefanya kazi na Malon kwa muda gani na wazazi wakijua, na mbona
wasikukatalie? Kama kweli Malon alikuwa mbaya sana wa kiasi hicho, mbona wewe
usikatazwe kufanya naye kazi mimi ndio nikatazwe!?” “Unagomba bure bila sababu!
Nani amekukataza hapa?” Naya akamuuliza taratibu tu.
“Umeanza
kuzungumza mwenyewe na kuongea mengi wewe peke yako, ukitufoka!” “Kwa sababu
naona mnataka kuniambia mambo nisiyoelewa! Kwa nini kunilinganisha na Ino, na
si wewe uliyeanza kazi ukiwa bado shuleni? Mimi nimevumilia. Sijachanganya masomo
na mapenzi, wala kazi au niseme starehe yeyote ile! Leo nimemaliza chuo, pia
natakiwa kuomba ruhusa kwa kutaka maendeleo jamani!” Wote kimya.
“Malon
amekuwa msaada sana humu ndani na anatujali. Akisikia tu tunauhitaji wowote
ule, anaacha kila kitu, anakuja kutusaidia kwa haraka bila mashariti mengi au
kusimanga mtu, akijishusha.” Joshua akajua anamsema na yeye, lakini akanyamaza
tu. “Amenitumia pesa nyingi tu na nauli juu kwamba nikiwa tayari nimfuate,
atanisubiria kituo cha mabasi ili nisipotee. Jamani, tunataka nini tena? Au
mnataka kuniona nabaki tu hapa nyumbani na kuendelea kuwapikia tu?” “Unapokwenda
huko Bale, unaharibu.” “Wala siharibu. Naongea ukweli. Labda uwe unakuuma kwa
sababu ni kweli.” “Labda Bale, pale ulipoanza ungeishia tu kwenye kuomba
ruhusa, basi.” Mpaka Zayoni akaongea ila kwa kujihami.
“Asante
sana Zayoni. Maana umeongea mengi ambayo wala hayakuhitajika hapa, zaidi mbele
ya Joshua!” “Mimi naomba kabla sijaingia kwenda kulala nikwambie hivi Bale,
ukiwa unatoka hapa, iwe ni kwa ajili yako tu. Isiwe..” “Sasa mbona ulikuwa
ukimuunga mkono Naya, mimi unashindwa nini baba?” “Mwache baba
amalizie, Bale! Umepatwa na nini wewe!?” “Nahisi kama naonewa kwa sababu mama
hayupo!” Naya akabaki akimshangaa sana Bale.
“Unapotoka
hapa kwenda kufanya kazi, iwe ni kwa ajili yako tu Bale. Usije toka hapa kwa
kusema unakwenda kuhangaikia familia yangu. Hapana.” “Naya mbona analeta
pesa hapa na tunazitumia pamoja, kwa nini mimi unikatalie.” “Usikimbilie Mbeya
kwenda kukusanya mazao ukitaka kuniletea mimi. Hapana. Kwa kuwa wewe
umefika umri au hatua yakujijenga, basi, nenda kakusanye mazao, tafuta na
masoko, uzo ili uanze kujijenga usiwe kama mimi.” “Sijasema hivyo
baba!” “Leo na sasa hivi ndio hujatamka maneno kama hayo, lakini
ndivyo umekuwa ukiishi na mimi hivyo na kunionyesha kwa waziwazi kabisa. Mungu
akusaidie na kukufanikisha uzishike hizo pesa unazozitaka na ufikie hayo
maendeleo unayoyatamani. Lakini ongeza umakini. Ni hilo tu. Usiku mwema.” Baba
yao akaingia chumbani kwake.
“Na wewe
acha kuniangalia hivyo!” Bale akamgeukia Zayoni. “Ungemuaga tu baba kwa vizuri
Bale. Ona mpaka amekubariki!” Zayoni akaongea kwa upole tu. “Kwa kuwa ameona
nimemkumbusha juu ya Naya. Mimi sijui natakiwa kufanya nini jamani! Nahisi
nimekuwa mtoto mzuri tu humu ndani ambaye ni mama tu ndiye aliyekuwa akiniona
hivyo. Sasa hivi naishia kuomba msamaha mpaka kwa kuomba maendeleo!” “Joshua,
nenda kapumzike na mimi nifunge mlango. Nitakupigia nikiwa kitandani.” “Sawa.”
Joshua akasimama kwa haraka bila yakubisha. Wakatoka hapo. Ni kama wote
wakabaki hawajui tena ni kitu gani chakuongea. Sivyo walivyoingia humo ndani. Bale
alibadili hali ya hewa hata chai aliyopika Naya haikunywewa. “Usiku mwema
Naya.” “Na wewe.” Joshua akaondoka hapo kama aliyepatwa na mshituko na
kushindwa kuzungumza. Usiku huo hakuna hata aliyempigia mwenzie simu. Wakawa
kama wasiojua muendelezo.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Katikati ya Furaha ya familia, Malon amerudi akiwa na SABABU NZURI
SANA NA YA KUELEWEKA.
Usikose kufuatilia muendelezo KWENYE kurudi kwake. Nia ya Safari hii
ni nini?
.
0 Comments:
Post a Comment