Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI&PESA! – SEHEMU YA 29. - Naomi Simulizi

MAPENZI&PESA! – SEHEMU YA 29.

    Jumatatu.

Kama kawaida ya siku nyingine zote za kazi, Naya aliamka akakuta baba yake alishaamkaa na kumwandalia kifungua kinywa na maji ya kuoga. Akamsalimia na yeye akaitika tu, hapakuwa na mengine. Akajitayarisha. Wakati akinywa chai Bale naye akatoka kama anayejiandaa. Akasalimia, baba yake akaitika, akaendelea na mambo yake, Naya kimya hata hakumtizama. Aliingia na kutoka bila kusemeshwa na mtu. Na safari hii hakuazima chochote kutoka kwa baba yake. Kimya tu.

“Joshua amefika baba. Nitakupigia baadaye.” “Sawa mama. Uwe na siku nzuri huko. Ufanikiwe.” “Amina baba yangu.” Naya akachukua pochi yake, wakati anatoka Bale akamuwahi. “Naya, hutanikuta ukirudi.” “Kuwa mwangalifu sana Bale. Usijekuta unachokitafuta mbeleni, unakiacha nyuma na ndicho wenzio wote wamekuwa akikitafuta.” “Wewe ulitegemea nikae hapa nikimsubiria huyo Joshua au bahati inijie hapa ndani mpaka lini?” “Nitakupigia simu baadaye baba. Naomba kama alivyokwambia Joshua na Geb, jana pale kwa kina Magesa msubirie yule fundi akushauri vizuri na akusaidie ili wamalize mapema.” Bale akashangaa sana. Jana wakati hayo yakizungumzwa yeye alikuwa nje akizungumza na Malon.

“Kwa hiyo ndio mnaendesha mambo humu ndani bila mimi kujua!? Yaani mimi ndio nimekuwa mtu wa nje tu, Joshua ndiye anayejua mambo ya humu ndani!? Mipango muhimu ya humu ndani inaendelea bila mimi!?” “Jana pale nyumbani kwa kina Magesa, ulipotea kwa muda mrefu sana Bale. Kwanza hukujua nini kinazungumziwa kwa kuwa katikati ya mazungumzo yote wewe ulikuwa ukichati. Macho kwenye simu muda wote kisha ukatoka kabisa. Na ndio maana nilikufuata nje. Haya yote yalizungumzwa wakati wewe upo palepale na ulipotoka, Bale. Hapakuwa na usiri wowote. Yote yalizungumziwa palepale mbele ya watu wote, Nanaa na mumuwe ndio waliokuwa wakimshauri baba jinsi nzuri ya utunzwaji wa hayo mazao atakayokuwa akiletewa. Palepale mbele ya watu wote na Joshua alisema ananyamaza kabisa akisema wazi huo utaalamu yeye hana, na yeye anajifunza pale. Tena wote wakamcheka. Na James kumtania kidogo kuwa amefikishwa uwanja wa ugenini, lugha ya kichina. Yote hayo yaliendelea pale.”

“Haya, tuliporudi hapa, mbele ya Joshua, kwenye siku yetu muhimu, ukaanza matusi.” “Nimemtukana nani mimi?” Bale akauliza kwa ukali. “Muwahi mwenzio mama. Usichelewe kazini. Na sitagusa chochote tena mpaka huyo fundi aje. Walishanipa namba yake. Wamesema saa nne asubuhi atakuwa ameshafika kule kwenye lile duka letu, Kibaha. Kwa hiyo usiwe na wasiwasi. Nenda kafanye kazi.” “Asante baba.” Naya akatoka.

Joshu&Naya.

Akamkuta Joshua akimsubiria nje ya gari. “Samahani nimechelewa.” “Usijali. Twende.” Baada ya kufunga mkanda na yeye, Joshua akaondoa gari. “Ulilala salama?” “Nilitamani kukupigia lakini nikaona nikuache upumze kwanza.” “Nilijua umenichukia, na mimi nikaona nikuache kwanza.” Naya akawa hajaelewa. “Kwa nini nikuchukie tena Joshua!?” “Mimi najijua Naya. Kuna wakati na mambo mengine nakuwa kama slow. Mchelewaji fulani hivi, kama ninayetakiwa kufanya jambo fulani kwa haraka lakini nachelewa!” “Sivyo nikuonavyo Joshua.  Kwa nini ufikirie hivyo!?” Naya akamuuliza akijaribu kufikiria ni nini kinampelekea Joshua kudhania hivyo.

“Nahisi kama pengine nimechangia kwa asilimia fulani kwa Bale kuondoka nyumbani!” Naya akashangaa kidogo. “Kivipi tena!?” “Basi. Nahisi labda nimejishuku tu. Nilifikiri pengine ungenilaumu kwamba pengine ningemtafutia kazi mapema asingefikiria kuondoka.” Naya akatulia kidogo kama anayefikiria, Joshua akahisi amempa jambo ambalo hata hakuwa nalo kichwani. “Samahani. Nahisi nimekupandikizia mambo ambayo hata hukuwa nayo!” “Umepatia kwa upande mmoja lakini jiulize je, ungekuwa umemtafutia kazi. Halafu pengine isilingane na ahadi alizompa Malon. Maana hatujui ni nini Malon amemuahidi. Kisha akatakiwa aanze kazi leo. Au akawa ameanza kazi kwa mtu ambaye mnaheshimiana naye sana. Kisha akaondoka kwa  mtindo huuhuu. Kwako ingekuaje?” “Daah! Na pengine ndio maana nilikuwa nikisita Naya.” Joshua  akaongea akisikika kupata aghueni ya utetezi.

“Naomba niwe mkweli kwako Naya. Utakuwa mke wangu, nataka unielewe mapema. Ni mambo machache sana ambayo siyafanyi bila kumshirikisha Mungu na kumuomba Roho wa Mungu aniongoze. Nilimuomba Mungu juu ya jinsi ya kushirikiana na Bale, lakini kwa hakika sikupata kibali. Sikujua jinsi ya nini chakufanya naye. Ndipo nikaamua kumpa muda kumwangalia yeye ni mtu wa namna gani kabla sijamuwekea dhamana popote.” “Na mimi nilimwambia hivyohivyo Bale. Tena wala si siku nyingi. Jana tu. Nilimwambia uwezo wa kumtafutia kazi unao. Lakini nimeishi na wewe kwa muda mfupi lakini nimekuona unapenda watu wanaojua ni nini wanataka na kukisimamia. Nikamwambia pengine na wewe unamsubiria yeye. Lakini acha nikwambie ukweli Joshua.” Naya akaendelea.

“Kwanza sikulaumu kabisa. Haikuwa hata kwenye mawazo yangu ila jana nilijisikia tu vibaya ndio maana nikashindwa hata kukupigia simu. Kile ulichokiona jana si kigeni kwetu kwenye ile familia.” “Kipi sasa?” “Aina ile ya mazungumzo kwa baba. Ila mara nyingi tulizoea kuona kutoka kwa mama. Tumekuwa tukiona vile. Malalamiko yasiyoisha kwa baba. Sasa kwa kuwa Bale amekuwa mtoto wa mama tokea anazaliwa. Hujui jinsi nyingine sahihi yakuzungumza na  baba isipokuwa ile aliyomuona mama akizungumza naye.” “Naya! Kwa nini kwa mzee mkimya hivyo!?”

“Nafiri hilo limechangia. Laukimya wakupitiliza ndipo anaonekana kama mzubaifu. Asiyefikiria na mengine mengi. Halafu kwa kuwa yeye alikuwa mfanyabiashara, hakuna inapoonyesha kipato chake kwa mwezi, pesa yake ikiingia ikawa ni ya wote, haikai. Ila ya mama ikawa yakueleweka. Mshahara wa kila mwisho wa mwezi wa uhakika wakupigia mahesabu ya kueleweka kwa vitu vya pale nyumbani. Unapomsikia Bale akisema Malo amesaidia pale nyumbani, hakuongopa. Ni kweli alisaidia kwa mali, kitu ambacho mama hakutaka kabisa. Kilikuwa kikimuuma sana, nakuchukia mpaka ikabidi niache kuwashirikisha kama nalipa madeni kwa pesa ya Malon, ila kazi nilizokuwa nikifanya mimi mwenyewe. Lakini ukweli madeni mengi alitusaidia kulipa na alikuwa hata akitoa na pesa za matumizi kwa kina Bale, bila hata kuombwa. Au kwa haraka kama ulivyomsikia Bale. Hakuwa akijua kusubiri anaamua tu na kuwapa pesa za matumizi. Ndipo Malon akafanyika kama kaka kwao mbali na mahusiano yetu sisi wawili.” Hapo Joshua akapoa.

“Lakini ndipo linapokuja swala la mwisho ninalotaka kukwambia Joshua. Sijui kama unakumbuka majibu uliyompa Malon?” Joshua akamwangalia na kuendelea kuendesha. “Naamini ulimaanisha na hukuongea katika upande wa hasira.” “Japo nilikuwa nimekasirika, lakini unanijua siwezi kuzungumza kitu kumfurahisha tu mtu. Lakini nataka kujua ni upande upi unao zungumzia wewe!”

“Unakumbuka ulimwambia Malon tupo kwenye kujenga msingi wetu? Kwamba itakuja kufikia wakati na sisi tutaweza kusaidia nyumbani.” Joshua akatulia kidogo. “Naomba tusimamie hapohapo. Tafadhali usiyumbishwe na Malon. Mimi namjua, kwa kuishi naye. Na nilikuhakikishia atarudi tu. Tena na sababu ya kueleweka kabisa.” “Aisee sikutegemea kama ingekuwa kwa haraka hivyo!” Naya akacheka kwa kusikitika.

“Ni kwanini anafanya hivyo!?” “Kwanza mimi nahisi ni muoga au hataki kujifunga kwenye mahusino yatakayomfunga nakumfanya kuwajibika moja kwa moja. Nahisi hivyo kama alivyosema baba yake. Ndio maana akiona ameanzisha jambo na mtu, halafu huyo mtu akataka hatua nyingine ya kumfunga, anajitoa. Ndio baba yake alisema watu wote tunataka kitu kimoja tu kwa Malon ambacho hana uwezo wakumpa mtu yeyote yule. Ni bora atoe pesa nyingi, lakini si vinginevyo. Wote tunaishia kuumia, lakini lazima kumuelewa Malon. Hana huo uwezo wa kujifunga kwa mtu mmoja na hajui inakuaje kwa sababu Malon alikimbia malezi ya nyumbani na kujiingiza mtaani. Akachagua fungu baya. Ndio maana baba alifurahia sana aliposema ameokoka. Akamwambia amefanya jambo zuri. Hajachelewa hata kidogo. Akamshauri atafute mazingira, tena akamwambia hata kwa kulazimishia, awe kanisani. Awe mshirika kabisa anayejua mambo ya kanisani kama familia katika mwili wa Kristo. Ili sasa akulie wokovu. Malon akamwambia aina ya biashara aliyonayo inamfunga.”

“Baba akamwambia Mungu yupo popote, hata huko Mbeya lazima atafute kanisa sio lazima mpaka awepo huku Dar ndipo ahudhurie kanisani. Asisubiri miezi kwa miezi ndipo arudi kanisani huku Dar. Akamwambia Mungu anamtaka yeye zaidi kuliko pesa anayotoa kanisani kwao huku Dar. Maana ni kweli Malon anatoa pesa pale kanisani kwao na kusaidia vijana. Zayoni alikuwa akienda huko. Au niseme kwa kifupi ni mtoaji popote na kwa yeyote. Kwao pia yupo hivyohivyo kusaidia ndugu zake sana. Amewainua sana kwenye maisha. Lakini hataki mahusiano na yeyote, na usimwambie chochote. Zaidi kumkosoa kwa chochote. Hapo mtakosana. Kidogo nilimuona anaweza kumsikiliza mama yake ila si mwingine yeyote. Bora akupe pesa, muachane sio mumfuate nyuma.”

Anyways, baba akamshauri ajiingize kanisani, atulie kanisani ajifunze kwa upya. Hajachelewa. Akamwambia ipo garama ya kulipa. Kugawa muda wake mchache, lakini lazima alazimishie na kuwepo kanisani kama vile alivyoweka juhudi za makusudi kwenye biashara yake na kufanikiwa sana, basi aweke juhudi atulie kanisani lasivyo atapoteza kitu cha thamani sana alichopokea. Tena baba akamwambia lile andiko la ‘I Pretro 5:8-9 Mwe na kiasi na kukesha, maana adui yenu ibilisi huzungukazunguka kama simba angurumaye akitafuta mtu ili apate kummeza’. Baba akaongeza kwa kumuwekea msisitizo kwa ule msitari wa 9 kuwa Mungu ameagiza ‘Mpingeni, mkiwa thabiti katika imani’.” “Ambayo ni kweli.” Joshua akaongeza.

“Basi, baba akamwambia hawezi kumshinda shetani nje ya Yesu, lazima ajifunze pia ni jinsi gani yakuishi kwenye imani. Hayo baba anazungumza naye wala hatukuwa kwenye mahusiano naye ya kimapenzi, ila kama kijana wake tu au niseme kama Bale vile. Tena ilikuwa kwenye mazungumzo tu, baba aliporudi kutoka Mbeya na baba kuona vile alivyofanikiwa sana. Katika kuendelea kumpongeza na kumwambia japokuwa anajituma sana, lakini kwa hakika na mkono wa Mungu uko juu yake ndipo akamuuliza kama amefanikiwa kupata kanisa na kule Mbeya. Nimeongea mengi lakini kujibu swali lako, sababu ya kwanza na kubwa ni hataki na hajui kujifunga kwenye mahusiano na mtu. Kwangu yupo kwenye kusitasita kwa kuwa najua amenipenda, ndipo inakuja sababu ya pili sasa.”

“Hakuna jinsi Malon akaniona au kusikia nipo na mwanaume mwingine akatulia, Joshua. Na amekuwa hivyo kila wakati. Anatoka akiamini sitapata mtu. Akisikia tu nina mtu, anarudi kuchungulia. Sasa safari hii ameshindwa kuniingia tena. Mlango wa kwa baba umefungwa, tena kwa kuufunga yeye mwenyewe. Ameshindwa kuutumia kama alivyozoea siku zote. Kutoka na kuingia akijua baba huwa anampokea, halafu mama ndiye aliyekuwa mbali naye. Sasa safari hii baba amemuacha kabisa. Akiamini ameshamwambia yote aliyopaswa kusikia, anamuachia yeye mwenyewe kuchukua hatua.”

“Unakumbuka kuniona nasoma ujumbe siku ile ya kwanza uliponipa maua, tena tulikuwa tunakaribia kufika nyumbani?” Joshua akatulia kidogo kama anayevuta kumbukumbu. “Ukaniuliza nimesoma nini kwenye simu kilichotaka kunibadilisha furaha yangu, nikakwambia ni ujumbe kutoka kwa Zayoni, ila hakuna kipya, nikarudi kwenye kuimba?” “Oooh yeah! Tulikuwa tumekaribia sana nyumbani. Si ndivyo?” “Sawasawa. Basi Zayoni alikuwa amenitumia ujumbe kuniambia Malon yupo pale nyumbani, baba amemkaribisha ndani. Akampa chai aliyokuwa amejitengenezea yeye kwa kuwa alikuwa amefunga. Akampa na Malon. Chakula kilipokuwa tayari akampa na chakula. Ila akaniambia hajazungumza naye chochote amemuacha tu mpaka Bale alipokuja ndio Bale akaendelea kuzungumza naye.”

“Sasa kwa jinsi mambo yalivyokuwa, baba akijaribu kumkarimu na kuzungumza naye Malon kila wakati na akitaka kumsikia kila akifika pale nyumbani, kitendo cha baba kumpa tu chakula bila kuzungumza naye chochote, atakuwa amejua kabisa milango na kwa baba imefungwa. Ndio sasa, sasahivi ameamua kuweka nguvu kwa kumtumia Bale, asijue naye Bale anakaribia kufungiwa mlango na baba.” “Daaah! Ile ni mbaya Naya! Mbaya sana.” “Ni kwa vile alizungumza mbele yako tu. Lakini ndivyo anavyozungumza na baba wakati wote, zaidi anapokuwa na hasira. Na jana nimekwambia nilizungumza naye. Nilimwambia juu ya hilohilo. Lakini najua itachukua muda na maisha kumfunza mpaka aelewe jinsi ya kuzungumza na baba na kuelewa nafasi ya baba. Mungu atamsaidia tu.” Joshua akafikiria kidogo akaona aseme tu.

“Nikuulize kitu Naya?” “Uliza tu.” “Katika amri ZOTE za Mungu. Namaanisha zooote unazozijua hata kusikia tu, unakumbuka ni amri ipi yenye ahadi?” Naya akatulia kufikiria, akakumbuka. “Amri ya 5 katika zile 10 za Mungu. ‘Waheshimu baba yako na mama yako, upate baraka na uishi siku nyingi duniani.’ ” “Sawasawa. Na unafikiri ni kwa nini ile tu ndio yenye ahadi? Wakati katika zote hataYesu mwenyewe alisema wakati yule mwanasheria akimjaribu mbele ya Mafarisayo na Masadukayo alipomuuliza amri kuu ni ipi, unakumbuka jibu la Yesu?” Naya akatulia kufikiria tena, maana swali la kwanza alijibu kwa haraka bila kufikiria.

Joshua akatulia tu kumpa nafasi. “Yesu alisema amri iliyo kuu ni ‘Mpende Bwana Mungu wako, kwa moyo wako wote na kwa roho yako yote na kwa akili zako zote’.” Naya akajibu. “Lakini akamalizia kusema hivi, ‘Hii ndiyo amri iliyo kuu, tena ni ya kwanza. Mstari wa 39 katika kitabu cha Mathayo Yesu aliendelea kusema hivi, ‘Nayo ya pili ni kama hiyo, nayo ni hii: ‘Mpende jirani yako kama nafsi yako.’ Akaongeza kusema kuwa, ‘Amri hizi mbili ndizo msingi wa Sheria yote na Manabii.’ Unakumbuka?” Ikabidi Naya akae sawa akitaka kuelewa ni nini Joshua anataka kusema na aelewe zaidi.

“Aisee nimekumbuka!” “Sasa, katika zote na yote tokea mwanzo Mungu mwenyewe anazungumza na Musa, akimpa hizo sheria mpaka Yesu anamjibu yule Mwanasheria, umesikia ahadi yeyote nyingine Mungu kuahidi kumfanyia mwanadamu, au baraka au zawadi atakayopata endapo atatimiza hiyo sheria mbali na amri ya 5?” Hapo Naya akatulia. “Fikiria tu na nikumbushe kwengine palipoandikwa kwenye bibilia, kwenye amri aliyotoa Mungu kisha akaambatanisha na ahadi/baraka au tuseme zawadi nyingine yeyote, hata hizo sheria mbili Yesu alizosisema ni kuu, kisha akaweka msisitizo juu yake kuwa ndizo msingi wa sheria zote na manabii wote walisimamia hapo. Je, unakumbuka kama kuna ahadi nyingine Mungu kuahidi kutoa kwa atakayetimiza hizo sheria hata ile ya kwanza na ya pili inayomuhusu Mungu mwenyewe, umesikia ahadi yeyote ile mbali na ya 5?” “Aisee hapana Joshua!” Naya akajibu akiwa na mshangao.

“Ulishafikiria kwa nini? Yaani huyu Mungu aliyejitambulisha kwa Musa na kumwambia awaambie watu kuwa yeye ni Mungu mwenye wivuasiabudiwe mungu mwingine yeyote ila yeye tu! Yaani asitoe ahadi hapo kwa watakao tii kumuabudu yeye, eti aje atoe ahadi ya maisha marefu yenye baraka hapa duniani, eti kwa kumuabudu baba na mama yako! Tena wanadamu aliyewaumba yeye mwenyewe!?” Naya akatulia.

“Kwenye kitabu cha Waefeso 6:2-3 hata Mtume Paulo amezungumzia hilo na kusema, ndiyo amri ya kwanza na yenye ahadi! Nenda kasome vizuri wewe mwenyewe jinsi hata Mtume Paulo alipoliona hilo. Yaani huyu Mungu mwenye enzi yooooote, asitoe ahadi kwa yanayomuhusu Yeye, iwe mwanadamu! Inaingia akilini kweli?” “Kweli umenifanya nifikirie, Joshua!” “Basi jua hapo ndipo kwenye siri kubwa na nzito. Mungu akusaidie kuelewa.” Joshua akatulia kumpa nafasi Naya na yeye atafakari.

Kisha akaendelea. “Unajua Naya. Kadiri tunavyokua. Au watoto wanavyokua, ndivyo uelewa unavyopanuka. Na kwa kizazi hiki tumepata na neema ya elimu, ambayo wazazi wamegharamia kwa uzima wao na uelewa wao, kwa kadiri Mungu alivyowawezesha wao. Wengine hata kwa kukopa, halafu sasa tukawa na tekinologia. Maisha na mambo yamerahisishwa mno. Ni rahisi sana kusimama na kukosoa juhudi nzima za wazazi, bila kujua sisi tuna nguvu na uwezo wa kuona yote hayo kwa sababu ya msingi walioweka wao. Ile kuona tu hili ni kosa, haikutakiwa iwe hivyo kwanza ni neema ya ajabu, inamaana umelelewa sahihi kiasi cha kutambua kisicho sawa, si sawa. Sijui kama unanielewa Naya?” Naya kimya akisikiliza.

“Wapo vijana wangapi wameridhika tu mtaani wakilalamikia maisha bila kuchukua hatua? Wapo vijana wangapi wanaishi dhambini tu na hawasumbuliwi nafsi zao? Wewe hudhani kujua hiki si sahihi, na ukapata akili ya kuchukua hatua, hudhani kuwa ni neema na makuzi sahihi? Kule kujua natakiwa kusonga mbele, na nisibweteke. Kukawa na mazingira ya kuita nyumbani, haijalishi pana sura gani, hudhani kuwa ni juhudi fulani iliwekezwa kwa huyo mtu mpaka kufikia hapo?” Naya akatulia.

“Hakuna msingi dhaifu uliowahi kutoa nyumba bora, Naya. Hata bibilia inathibitisha hilo. Hakuna. Sikuwahi kulisema hili kwa mtu, lakini wewe unavyofikiria Naya, mimi sikutambua makosa ya mama yangu? Niliyajua kwa hakika. Hata sasa nikikaa na kutafakari najua kwa hakika mama hakuwa mjinga kiasi cha kutofikiria au hata kuhisi anajiingiza kwenye mahusiano yasiyofaa na baba yangu ambaye alikuwa mtumzima sana kwake. Haya, alikosea kwa baba yangu, akarudia tena kwa aliyemuachia ugonjwa na ndio maana hata nyumbani kwao walikuwa wakimsimanga. Kuwa aliishi maisha yasiyofaa. Lakini Naya, nilirudi kijijini, nikamlea mama yangu mpaka kifo. Sikuwahi kumuuliza wala kumsimanga juu ya hilo kwa kuwa najua na yeye alikuwa akijua alikosea kwingi tu, na pengine kujutia, ila mimi kama mtoto haikuwa nafasi yangu.”

“Mungu anaposema waheshimu wazazi, ni kwa kuwa anajua kuna wakati si rahisi Naya. Ni ngumu kwa kuwa tunafika kipimo cha kupevuka akili, unagundua makosa yao mengi. Ipo hekima ya kukabiliana na makosa yao, endapo Mungu akikupa hiyo neema, ila kama hukujaliwa, ni bora ukae pembeni kwa kuwa na wao ni binadamu. Wanaweza kukubali kosa, au wakakataa. Wengine wanakataa kwa kugomba waziwazi kabisa kwa kukataa kukosolewa. Na wengine hubaki kusononeka tu.” Joshua akaendelea.

“Hawa mapacha wa mama G, hawa. Kwa kumuona Geb na Grace na watoto wao kama unavyowaona. Wanaakili ile ambayo Geb huwa anasema wakati mwingine ni kama laana. Hawasahau kitu.” “Kama Magesa?” “Hivyohivyo. Geb anasema hakumbuki kukosa swali lolote kwenye  mtihani kama alifundishwa na kusoma. Mama yao anasema ni akili ya baba yao wala si yeye. Lakini Naya, wale watoto wanamtii mama yao, hujawahi ona. Geb na mapesa yote yale, na Grace hivyohivyo, mpaka leo, Grace huwa anasema jicho la mama yake linawanyanyua popote pale. Anasema hata kama Geb amekasirika vipi au ametingwa kwa kiasi gani, lakini na yeye akilipata hilo jicho, ananyanyuka bila swali.” “Sijaelewa.”

“Grace anasema yeye na Geb wamekua wakimtizama mama yao. Kuna jinsi akiwaangalia bila hata kusema, hata kama wapo katikati ya watu wanaelewa na kutii. Yule mama harudii neno mara mbili kwa Geb wala Grace.” “Aisee kweli Joshua! Nilimuona pale kanisani pia.” “Sawasawa. Mama yake aliposema asimame na atoke na familia yake, ulimuona alichukua hata dakika?” “Daah! Kweli aisee.” “Basi na Grace huyo dada yake yupo hivyohivyo. Hata Nanaa ulimuona ni kama alilalamika kidogo ndipo akatoka.” “Tena alichukua muda kidogo, lakini si Geb.” Naya akaongeza akijaribu kuvuta kumbukumbu.

“Basi naona umenielewa sawasawa. Ndicho kingine kilichonivutia kwa yule jamaa. Anapesa haswa. Lakini linapofika swala la kuwa mtoto, aisee utashangaa! Sasa jiulize kwa akili kama ya aina ile ya watoto. Na mama kama mama G ambaye na yeye alizaa na mume wa mtu. Wakapita kwingi na hata kwenye historia ya Nanaa na Geb, Grace na yule mume wake wa kwanza pia yule mama kwa kumsikia yeye mwenyewe anasema anayo majuto mpaka leo kama alichangia matatizo fulani hivi, tena anasema makubwa mpaka kujilaumu vifo vya wajuu zake wawili, na kuwatenganisha pia Nanaa na Geb kipindi fulani pamoja na watoto wao, mpaka Nanaa akaja kusamehe.” “Ilikuaje? Maana ukiwaangalia wale huwezi amini kama walishapita huko!”

“Wanahistoria yao ngumu kweli. Utakuja kuwasikia wenyewe siku moja. Lakini katika yote hayo yule mama aliyowatendea wanae, na kukosa kwingi, lakini hata kama Geb anaongea na simu ya muhimu vipi, yule mama akimuita tu, aisee anaitika! Hata kama amekaa chini, atasimama kwa haraka kama Grace tu, mpaka mimi nililiona hilo. Sasa wewe jiulize kwa nini wale watoto bado wanatii? Kwa nini wamebaki kumuheshimu mama yao ambaye ameshawaletea matatizo makubwa hivyo maishani? Kwamba si mama mkamilifu pia. Ni kama wadamu wengine wowote wale. Lakini kwa nini abaki kuheshimiwa vile?” “Mmmh!” Naya akaishia kuguna.

“Basi ndio ujue kuna waliogundua siri. Wakakubali kutii hivyohivyo hata kama ni chungu kumeza, wakakubali ndio wanaopata heri na maisha marefu hapa duniani. Wote tunaishi, lakini kuna wenye heri Naya. Wapo. Na heri zao zinatoka kwenye ahadi ya Mungu mwenyewe. Na wahenga wanasema, sikio halizidi kichwa. Hata ufanye nini, haliwezi kuzidi kichwa. Hata kama unazo shahada tatu, mzee ni mkulima yule aliyekuwa akiuza mahidi au pombe kilabuni ili usome, bado wanasema huwezi kumzidi. Unafikiri kwa nini waseme hivyo?” Kimya, Naya akitafakari. “Basi ujue na wenyewe waligundua siri.” “Mmmh!” Naya akapoa kabisa na  kubaki akitafakari.

Kisha akaongeza. “Tatizo la Bale ni kama anamuona baba hana uwezo mkubwa wakufikiria, ndio maana hatuna mamilioni ya pesa. Mimi nilishamuuliza kwa jinsi alivyozunguka hapa nchini, kwani ameona ni wazazi wangapi wana uwezo mkubwa sana mpaka baba aonekane yeye ndio hafai! Wengine wanashindwa hata kusomesha watoto wao hata na kuwalisha au kuwatunza kwenye nyumba kama ile yetu tu, wanaishia kwa wajomba na mashangazi! Nilipokuwa shuleni wala sikuwa peke yangu niliyekuwa nikihangaika maswala ya ada! Wazazi wengi tu hawana uwezo, wakilia maisha magumu kama sisi tu! Hapahapa nchini wala sio sehemu nyingine! Wazazi wenye pesa ni wachache sana! Lakini asilimia kubwa sana ya watu wanaangukia kwenye kundi letu, na wenyewe wazazi wao wamehangaika mpaka watoto wamekua! Nilishamkumbusha hilo huyu Bale. Nikamwambia wengine wamekuwa mpaka mawaziri kabisa, wazazi wakiwa mafukara tu! Au kwani wote walioko huko maofisini au bungeni walitoka kwa wazazi mamilionea?”

“Si kweli Naya. Utajiri wa mali upo kwenye mikono ya watu wachache sana. Wapo waliochangamka, maneno mengi tu zaidi ya baba Naya na bado hawana pesa. Baba yako au maisha yenu hayana tofauti na wananchi wengi hapa nchini. Geb mwenyewe anasema amesomeshwa na mama yake kwa kukopa na kuuza mali zote alizokuwa ameachiwa urithi na baba yao mpaka akapata shahada tatu! Yule mama alikuwa akikopa, kufanya biashara ili tu wanae waishi. Geb alipofanikiwa ndipo akamuinua tena mama yake pamoja na dada yake. Anasema walishaishi kwenye nyumba ya kupanga, ila chumba kimoja.” “Joshua!” Naya akashangaa sana.

“Hakika tena. Tena eti waliishi kwenye chumba kimoja, ndani ya nyumba ya wapangaji wengi. Yaani wote wale watatu na mume wa kwanza wa Grace humohumo ndani.” “Joshua wewe!” “Acha Naya wewe. Watu wanakufuru bwana! Nyinyi mnaishi kwenye nyumba yenu, mpaka uzio! Nyumbani kwenu na kiwanja kinasubiri nyuma ya nyumba halafu mnaona baba yenu hana akili ya maendeleo! Watu wanahistoria ngumu bwana! Humuwezi nyinyi kujilinganisha hata na walipokuwa kina Magesa tu. Ukisimuliwa habari zao wale, huwezi amini kule walikotoka. Lakini ona walipo sasahivi! Mali walizonazo na bado wanamuheshimu sana mama yao!” Joshua akaongeza na kuuliza.

“Nifanyeje Naya?” Akabadilisha mazungumzo na kurudi kwa yanayo wahusu. “Ukibadilika tu, mimi ndiye utakayeniumiza. Tafadhali endelea kuwa Joshua Kumu Mungu aliyekuleta kwangu, siye Joshua atakayechanganywa na kutengenezwa na Malon. Wote tutakosa kimbilio, Joshua. Tafadhali usiyumbishwe. Si na muonekano wake wa nje na wala aina ya utoaji wake. Fanya kama Joshua Kumu, kama ulivyoanzana na baba na si vinginevyo.” “Ni kwa kuwa nimeona kuwekeza kwa baba yako ni sehemu sahihi. Yupo tayari. Ni kama kumpa maji ya kunywa mtu mwenye kiu sana. Hata Geb ameliona  hilo ndio maana yupo tayari kuwekeza kwake na kumpa fundi wa kampuni yake ili ajue jinsi ya kusaidia, tena kwa haraka.”

 “Basi naomba usiyumbishwe. Tafadhali baki kuwa Joshua Kumu. Fanya maamuzi hata unayoyaona ni magumu.” “Hutanikimbia?” “Siku nitakayokuapia kuwa nitakuwa na wewe mpaka kufa, au siku nilipokwambia nitakuwa na wewe, ujue mpaka wewe mwenyewe utanihurumia.” “Basi nakushukuru kusimama na mimi Naya. Asante kunitia moyo. Jana nilikuwa na hali mbaya! Mpaka nikashindwa kitu cha kukwambia.” Naya akacheka.

“Nini?” “Sikutishi Joshua. Lakini jua Malon atarudi. Atarudi tena. Na kama hatashindwana na Bale, ujue atarudi safari hii Bale akiwa upande wake. Atafanya nini, na akitumia sababu gani, sijui. Ila usiruhusu kutishwa naye. Simama mbele yake kama ulivyosimama siku ile mpaka ukafanikiwa. Hajazoea hivyo. Wewe umemtisha. Na baba kuonekana kukukubali wewe waziwazi vile, ndio maana nahisi amerudi kwa haraka. Hakuchukua muda mrefu. Kwa hiyo naomba tutengeneze msingi wetu ambao tutasimamia bila kuyumbishwa hata na mambo ya familia yangu. Usikubali kuyumbishwa.” Hapo Kumu akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu kama aliyetua mzigo.

“Apatae mke, apata kitu chema. Naye, anajipatia kibali kwa Bwana.” Naya alicheka sana. “Mimi Kumu, nimepata kitu chema na nimepata kibali kutoka kwa Bwana. Nakushukuru kwa kuniamini na kuamua kuongozana na hiki kichwa changu. Umeifanya siku ya leo iende vizuri, na kunirudishia ujasiri.” “Karibu. Sasa turudi kwenye mipango yetu.” Angalau wakaanza kuzungumza mengine na kucheka mpaka walipofika kazini kila mtu akiwa ametulia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alimsindikiza ofisini kwake, akamuacha hapo akifanya kazi kwa makubaliano mida ya chakula cha mchana watoke wakatengeneze pete kufanya ienee kidoleni kwa Naya. Na jioni wakitoka, wakutane na kina Magesa kwa chakula cha jioni wao tu wanne bila watoto. Geb, Nanaa, Naya na Joshua. Hilo likakaa sawa. Naya akahamisha akili kazini kama kawaida yake. Akapangia kila mtu kazi, kisha akaanza kufanya kazi nyingine mpaka mida ya saa mbili kasoro, wenzake walipoanza kuingia hapo, Naya asijue picha zake akichumbiwa zilienea kampuni nzima. Jamali akaanzisha kikao kwa kuanza kumpongeza Naya. Naya akacheka akionyesha hakuwa ametarajia hilo. “Asante bosi wangu.” Akashukuru.

Ndipo akaweka msisitizo wa kazi. “Mama Kumu, si na leo utasaidia kama siku ile? Ule mtindo wako naona utanifaa sana hapa.” “Nishaandaa kila kitu kutokana na kazi nilizokuta hapa.” “Daah! Naona mwaka huu kama kitengo chetu hakitashinda, mimi nitajua kuna mkono wa mtu tu.” Jamal akaongea kwa furaha kama kawaida yake kupenda kufanyiwa kazi. Wakati akimalizia kikao, akaja yule msaidizi wa CEO na Joshua. Wakasubiri ili Jamal amalize. Na yeye hakutaka mengi, hapohapo akafunga kikao.

“Mbona kama Jamal anatukimbia?” Akauliza msaidizi wa CEO aliyekuja na Joshua. “Hataki siri za kitengo chake zisikike.” Joshua akawa kama anamtetea Jamal. “Nimemaliza viongozi.” Akajibu Jamal na cheko akisikika kupaniki kidogo. “Mimi nipo  hapa kibinafsi kumpongeza Naya. Nilikuwa safarini juzi, nikashindwa kuhudhuria tafrija.” Akamsogelea Naya pale mezani, Naya akasimama na cheko akimtizama Joshua. “Hongereni sana.” “Asante. Tunashukuru.” “Tuone pete aliyokupa Kumu. Asitutie aibu hapa mjini.” Joshua alicheka sana, wawili hao walionekana kufahamiana kwa karibu. Alikuwa mtumzima, mkubwa kwa umri kumlinganisha na Joshua. Alionekana kushiba mamlaka kama Joshua tu. Msafi na suti yake pamoja na tai.

“Sijawaangusha bwana!” Kumu akajitetea akicheka sana. “Acha mimi ndio niwe muamuzi wa hili, Kumu. Tusije wote tukaonekana hovyo huko mtaani. Hakuna maandalizi mazuri.” Wote wakaendelea kucheka. Naya akanyanyua mkono, akaupokea kuangalia hiyo pete. Wote wakamuona anacheka. “Vipi?” “Heshima yako Kumu.” Joshua alicheka sana. “Kuoa ruksa?” Joshua akauliza. “Kabisa. Tunakukaribisha chamani. Unaonekana utamudu majukumu, hutatuangusha.” Walikuwa viongozi wao wakubwa sana hapo kwenye kampuni wakifanyiana utani mbele ya Naya. “Hongera sana Naya.” “Nashukuru, asante.” Hilo tu ndilo alilomudu kusema Naya. Hakujua azungumze nini tena mbele ya bosi zake. Wapo kazini.

Wakatoka wakitaniana. “Harusi lini?” Wakamsikia akimuuliza Kumu huko koridoni. “Aisee nasubiri taratibu za kanisani zikamilike, nioe. Sina sababu yakusubiri tena.” “Ndio haraka hivyo!?” “Kabisa. Ndani ya majuma machache sana, nitakuwa na hili nimefunga.” “Hongera sana Kumu. Unastahili aisee! Mimi mpaka nikaingiwa na wasiwasi! Ukimya ulikuwa mzito mno! Hapakuwa hata na fununu kokote hata za mtaani tu!” Wakasikika wakiendelea kucheka, sauti zikiishia koridoni. Naya akarudisha akili kazini.

Wakapita tena viongozi wengine wa hiyo idara yao ya masoko wakimpongeza. Wao walikuwa na vyeo kama vya Jamal ambao Naya alikuwa akiwaona tu na kumpita, siku hiyo walifika kumpongeza. Na walikuwepo siku ya jumamosi nyumbani kwa Kumu akichumbiwa, wakamuomba kupiga naye picha. Nao Naya akawachangamkia tu na kupokea pongezi. Akawashukuru wote kwa kuhudhuria. Kweye hiyo idara yao ni Jamal peke yake ndiye aliyekuwepo siku hiyo yakuchumbiwa kwake, wengine walisikia tu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mida ya chakula cha mchana Joshua akarudi. “Mimi nipo tayari na nimekuombea ruhusa kwa Jamal, maana tunaweza kuchelewa kurudi.” “Nashukuru. Hata mimi nimemaliza. Tunaweza kutoka.” Naya akachukua pochi yake na kutoka akiongozana na Joshua. “Mbona unacheka?” “Nimefurahi Joshua! Bado siamini.” Joshua akacheka wakati anaondoa gari. “Nimefurahi kama na wewe umefurahia. Na mimi ninafuraha sana. Ilitaka kuharibika jana, lakini umenifariji asubuhi, imerudi.” “Namuhurumia Bale! Hakika  namuhurumia sana.” “Umejua amefikia wapi?” “Wakati Zayoni na baba wakiwa wanaelekea Kibaha kumsubiria fundi wa wakina Magesa, amenitumia ujumbe kunitaarifu na kuniambia Bale aliondoka kwenye mida ya saa 12 asubuhi.”

“Nashauri umtafute Bale, kujua amefikia wapi.” “Joshua!” “Hakika Naya. Wewe ndiye dada yao. Wewe ndiye uliyewaletea Malon pale nyumbani. Na wewe ndiye unayejua nguvu ya Malon kwa ukaribu sana.” “Joshua jamani!” “Hutaki Bale apotee, si ndivyo?” “Lakini ameniumiza sana! Anafanya fujo mbele yako, tena siku muhimu sana kwangu! Na bado eti mimi ndio nimtafute!” Naya akalalamika.

 “Unawajibika kwa asilimia 100, Naya wangu. Wewe kama dada yake na uliyemtambulisha Malon kwao. Tafadhali anza kuishi hivyo. Wala usishindane naye, kwa kuwa na yeye anakutegemea umzirie kama alivyozoea siku zote.” “Siku ile yenyewe uliponituma kwake nikatengeneze naye na hata kumsaidia pesa, hakutegemea. Maana nilimtamkia maneno mabaya sana kama kawaida yetu tunavyokuwa tukigombana.” “Basi naomba badilika Naya. Kuwa dada kwelikweli. Na wenyewe waone mabadiliko. Watakuheshimu tu.” Naya akatoa simu yake.

Damu nzito kuliko maji.

Naya akampigia, Bale akapokea. “Umefikia wapi?” Bale akashangaa sana. Akamsikia akicheka. “Sasa unacheka nini, hunijibu?” “Sikutegemea kukusikia hivi karibuni. Nilijua mmenichukia, hamtaki hata kuniona! Nikajiambia nikahangaike kivyangu mpaka nifanikiwe ndipo nirudi.” Naya akamwangalia Joshua kama kumwambia alichofikiria ni kweli. “Hata usipofanikiwa, unajaribu tena na tena.” Bale akashangaa sana. “Kwamba hutanicheka wewe!?” “Kwa nini nicheke juhudi zako Bale? Mimi naamini tutakuja kufanikiwa sana, kwa kuwa nia tunayo na ndoto zetu hazijafa. Sema ni vile hatujajua njia ipi ni sahihi ya kufikia. Mungu atatusaidia tu. Tutembee kwa imani.” “Naya! Wewe umeingiwa na nini!?” “Mimi nataka tusipotezane Bale. Tumekuwa wote kwenye shida na raha. Tumeteteana katika mengi hata yale ambayo wazazi walikuwa kinyume yetu! Naomba tusitengane sasa hivi. Ukikwama kwenye lolote lile. Hata ushauri, tafadhali usijifungie mwenyewe. Bado ukumbuke tunayo hii kazi ya Coca, tunapo pakuishi, na sisi tupo. Usiishi huko mpweke ukitaabika peke yako.” Bale alihisi anaongea na mtu mwingine na si Naya.

Ikamgusa sana. “Daah! Nashukuru Naya. Asante. Na naomba unisamehe. Nahisi niliomba ruhusa ya kujihami ndio maana nikawa mkali bila sababu. Nikawa ni kama najitetea tu. Ila tuyaache hayo. Nashukuru kwa kunipigia.” “Utanijulisha kama utafika salama?” Naya akamuuliza. “Sawa. Nitafanya hivyo.” Bale akakubali bila shida. Naya akakata.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Daah! Kumbe kweli Joshua! Alitegemea tumchukie!” “Mungu amekuweka kuwa dada wa familia, ujue ni dhamana. Mengi itabidi kujikana tu, ili kuweza kuwa dada yao.” “Ni ngumu, hakika ni ngumu! Ila basi tu. Naomba Mungu aingilie kati. Ila sikutamani tuje turudi kwenye maisha ya Malon.” “Kama ulivyosema, Mungu atatutetea lakini pia ni kukusudia kabisa isiwe hivyo kwa kuwa kunakujaribiwa na yeye anaweza kukujaribu kujua msimamo wako kwa sasa. Umeamua kumuacha kweli au ni kama alivyozoea kutoka na akirudi unampokea! Na atataka kukuhakiki zaidi kujua kusudio la safari hii kama ni kweli au ni hasira tu kwamba utakuja kumkumbuka na kugundua unafanya kosa? Hayo yote atakujaribu tu.” Naya akanyamaza.

Walifika kwa sonara wakafanyiwa marekebisho ya haraka kama alivyolipia Joshua. Hakutaka Naya atoke hapo bila hiyo pete kidoleni. Simu ziliwafanya warudi ofisini na kushindwa kukaa mahali na kupata chakula cha mchana pamoja. Joshua alipata simu nyingine tena kutoka kwa Jema akisisitiza kuhitajika yeye mwenyewe ofisini. Ila alimnunulia chakula Naya na kurudi ofisini. Njiani alimsikia Joshua akijibu simu alizokuwa akiunganishwa na Jema, Naya akabaki tu kimya kitini akipanga vidole vyake vya upande wa kushoto akichezea pete yake akiwa bado haamini kama yamekuwa na kwake.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kwa kuwa jioni alijua wanakutana na kina Magesa, na lazima kurudi nyumbani kwao Kiluvya kujiandaa kisha kurudi tena mjini, Naya akajiandaa kutoka kwa wakati. Alipomaliza tu kuweka vitu sawa, akawa anaingia Jema na Joshua. Jema akiongea kwa kusoma kitu kwenye tablet yake, Joshua akimsikiliza. “Twende Naya, tusichelewe.” Naya akanyanyuka na kumfuata. Jema akawa anaendelea kusoma. “Unaionaje?” Akamuuliza Joshua wakati wanataka kutoka kabisa kwenye hilo jengo. “Excellent.” Akajibu Joshua. Jema akageuza njia palepale Naya akamsikia akicheka kwa kushangilia kwa sauti ya chini nyuma yao akiondoka. Naya akamtizama Joshua, wakaendelea kutembea wakielekea alipoegesha gari Joshua.

“Sasa si tutachelewa! Kwa nini wewe usiende kwako, mimi nikachukua usafiri hapa wakunirudisha nyumbani kisha unifuate nikiwa tayari?” Naya akatoa wazo kabla Joshua hajatoa gari getini. Akasimama akifikiria. “Wazo zuri.” Akafikiria tena kidogo, kisha akamuona anatoa gari nje ya geti na kuegesha pembeni. “Wewe nenda na hii gari nyumbani, nitakufuata nikiwa tayari.” Naya akashangaa. “Unakumbuka nina magari mawili na nina dereva hapa kazini?” Naya akacheka na kushuka garini ili aende upande wa dereva. “Nakushukuru Joshua wangu. Hutaki nipate shida! Ila mwenzio hata daladala ningepanda tu.” “Usijali.” Naya akaondoka na gari ya Joshua, na kumuacha Joshua akirudi ndani akitembea. 

Zayoni Naye.

Ilipofika mida ya saa moja kasoro kama 10 hivi Joshua akawa anagonga mlangoni. “Umependeza!” Naya akiwa chumbani akamsikia Zayoni akimsifia Joshua, na Joshua kucheka. “Asante Zayoni. Hujambo?” “Mimi sijambo. Lakini baba ameniambia endapo napokea simu za Malon nisimwambie mambo yanayoendelea hapa nyumbani, ila salamu tu.” Joshua akabaki ameduaa asijue nani anawasikiliza. “Baba anasema hayamuhusu tena. Lakini unajua mimi nimeamua nini?” Naya akabaki akisikiliza, mkono umeshikilia moyo kama utatoka kupitia kwenye kifua, udondoke. “Sijui Zayoni.” Joshua akajibu kwa utulivu. “Japokuwa Malon alikuwa akitupenda sana, lakini mimi naona nisipokee kabisa simu zake. Niepuke kabisa ili wasinitege kwa maswali. Si unafikiri ni sawa?” “Nafikiri baba anayo sababu ya msingi kukwambia hivyo, Zayoni. Wakati mwingine kutii ni bora kuliko chochote kile.” Ikabidi Joshua kutumia akili ya haraka na kujibu kwa hekima.

“Hata mimi nimeona hivyo. Ujue mwanzoni walipanga mipango vizuri na Bale, hata wakamshirikisha na baba. Baba akamshukuru kabisa Malon kwa kukubali kumpa kazi Bale. Ujue Malon alimuacha Bale bila taarifa yeyote ile?” “Nakumbuka kusikia.” “Basi sasa hivi amemchukua tena bila kumtaarifu tena baba! Yaani kimyakimya.” Joshua kimya. “Sijui umeelewa? Yaani kama hivi wewe unavyoomba ruhusa kwa baba kumchukua Naya, yeye hajamuombea ruhusa Bale wala kuwasiliana na mtu mwingine yeyote kusema safari hii amerudi tena, halafu anamchukua Bale, Bale atakuwa kwake kama walivyoanza kwa utaratibu pale mwanzo kabla hajamuacha.” Joshua kimya akisikiliza. Zayoni akaendelea.

“Hivi unajua alimkimbia Bale kabisa, akawa hapokei simu zake? Yaani Bale alikuwa anakesha akimpigia simu kila wakati, akimsihi amchukue. Niliamka siku moja nikamkuta anampigia Malon, usiku. Ila akaniambia nisimwambie Naya na baba kama bado anamtafuta Malon.” Joshua hakujua ajibu nini. Naya naye kimya huko ndani.

“Ile siku ya jumapili, juzi, ujue alimtumia tena ujumbe kama kumjaribisha tu. Maana Malon alimfungia simu zake, akawa hampati tena na jumbe hajibu japo alikuwa akiona zinafika. Sasa siku ile ya jumapili tulipotoka kanisani ndipo akajibu ule ujumbe aliomwandikia kama kumjaribisha tu, kumwambia kama wewe umemchumbia Naya.  Ujue Bale alifurahi sana?” Joshua kimya.

“Nilivyomsimulia baba leo, baada ya Bale kuondoka, ndio amenionya mimi nisifanye hivyo tena. Kutoa mambo ya humu ndani. Ndio naona bora nisipokee tu hata simu zake. Nilishaharibu kipindi  fulani alipiga, sasa mimi kwa nia njema tu nikamwambia Naya alipo. Baba hakufurahia kabisa. Amenionya nisirudie tena. Lakini mimi sikujua kama angemfuata Naya, na Naya hamtaki tena kwa hakika. Kwa kuwa mara zote wanakuaga hivi. Naya anakuwa analia sana, lakini baadaye wanapatana tena. Mimi nikajua na safari ile ninakuwa nawasaidia, kumbe niliharibu!” Naya akaishiwa nguvu na kukaa kitandani taratibu.

“Malon ni mzuri sana wakujirudi. Na mama alikuwa akimchukia anasema anampotezea muda Naya, Malon si mtu wa msimamo. Ila Naya mwenyewe alikuwa akimsamehe. Unajua mama alimfukuzaga Malon?” Bado Joshua na Zayoni walikuwa wamesimama hata hajakaribishwa kiti. Zayoni ananong’ona kwa sauti ya kusikika tu. Akaendelea. “Ila Naya akawa analia sana. Mimi na Bale tukasema atakuwa anamlilia Malon tu. Ndio Malon alipopiga nikampa...” Naya akatoka kwa haraka. “Mimi nipo tayari.” Zayoni akajisogeza pembeni kwa haraka kama aliyeshituka.

Naya akamgeukia. “Baba amesisitiza usitoke Zayoni. Anarudi sasa hivi. Unasikia?” “Nikiogopa?” “Huwezi kuogopa. Funga milango na uwashe tv.” Akarudi kukaa kwa upole. “Au tumsubirie baba mpaka arudi? Tusimuache peke yake.” Joshua akatoa wazo. “Baba yupo njiani, anarudi hapa sasa hivi. Ameniambia hayo kama dakika 10 zimepita. Kwa hiyo atakuwa hapa muda mfupi sana, hatachelewa. Twende tusiwachelewe kina Magesa.” Joshua akamwangalia Zayoni pale alipokuwa amekaa. “Utakuwa sawa Zayoni. Na baada ya dakika 10, Naya atakupigia simu kuhakikisha upo sawa.” “Sawa. Ila usisahau Naya. Mimi nitaogopa tu. Najua.” “Nitakupigia. Na wewe baba akija unijulishe.” “Nishaanza kuogopa.” “Jamani Zayoni!” “Kweli Naya. Mimi naogopa tayari.” “Nashauri tumsubirie  baba mpaka arudi. Hatutachelewa.” Joshua akakaa kabisa.

“Mimi siwezi kuwa peke yangu. Nilikuwa na mama kila wakati.” Zayoni akaanza. “Mama hakuwa akiniacha mimi peke yangu. Hakuwa akifanya hivyo.” “Basi Zayoni. Na mimi sitakuacha. Tumsubirie baba.” Naya akakaa na yeye. “Unataka kuangalia nini?” “Mimi sijui tena, Naya!” “Sasa kwa nini unataka kulia tena wakati tunabaki wote? Sikuachi Zayoni.” “Bale alisema haondoki tena, atabaki  hapahapa atafute kazi. Leo asubuhi ameondoka bila hata kuniaga! Na wewe ulikuwa unaondoka nakuniacha Naya! Mama aliniahidi mtakuwa mnanikumbuka. Ila mnanisahau! Mama hakuwa akinisahau hata siku moja! Ila nyinyi mnanisahau.” “Basi samahani Zayoni. Nitaongeza umakini nafikiri sababu ya haraka nikakusahau mdogo wangu. Ila siku nyingine sitafanya hivyo. Mpaka uzoee kubaki peke yako. Si ni sawa?” Joshua akawa ametulia kimya akisikiliza. “Kwa hiyo nikizoea ndio mtakuwa mkiniacha peke yangu!?” Hapo Naya akatulia kidogo.

“Hujui!?” “Nafikiri tuongeze kuzungumza. Tuwe tunazungumza. Chochote unachoona najisahau, nikumbushe. Au hata kama kitu hujapenda, wewe niambie jinsi sahihi. Au unaonaje?” “Hapo sawa.” “Na ninakuahidi nitakuwa nikikusikiliza na kuongeza umakini.” Hapo akamuona ametulia. Na baba yao akawa anaingia malangoni. “Wewe bado upo tu?” “Nilikuwa nakusubiria baba. Umefanikiwa?” “Maneno matupu! Hamna lolote.” Joshua akasimama ili asalimie. “Naya aliniambia mnawahi kukutana na kina Magesa!” “Bado muda mzuri kabisa. Pole na majukumu.” Wakasalimiana na kutoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Kweli inabidi kuongeza umakini kwa Zayoni!” Naya akawaza kwa sauti na kuongeza, akijitetea mawazoni. “Ila mimi nilijua ameshazoea!” “Ila nimependa hitimisho lenu. Jinsi ulivyomwambia.” “Kweli?” “Kabisa, ila tu hakikisha unazingatia ulichomwambia ili asione umemdanganya.” Naya akatulia. “Umependeza sana.” Akamrudisha pale kimawazo, angalau Naya akacheka na kuondoa hofu ya alichokisikia Zayoni akimwambia.

Naya, Nanaa, Joshua na Geb.

Walifika na kuwakuta Nanaa na Geb wakiwasubiria garini, Nanaa akicheka sana, mumewe taratibu tu. Joshua akagonga kioo. Wakatoka. “Leo Magesa mwanangu, kamuweza baba yake, ndio nilikuwa nikimcheka Geb. Kampigia mahesabu, yaani Geb mwenyewe akaingia mtegoni. Anakuja kumaliza ndio akagundua Magesa amemchezea akili.” “Ila mimi nimempongeza! Sijapata kichwa chakunizidi mahesabu ila yeye! Inabidi kuongeza umakini. Sijazeeka kiasi chakumuachia kiti kirahisi hivyo!” “Mimi sidhani kama uamuzzi ni wako GM. Ukizidiwa, huwa unazidiwa tu.” Geb akatingisha kichwa kwa masikitiko huku akicheka.

“Bibi harusi wangu amependeza sana. Na wewe pia Joshua. Wote mmependeza.” “Asante Nanaa, na nyinyi mmependeza.” “Asante, ila sisi ni kawaida yetu.” Wote wakacheka sana. “Nanaa!” “Mimi namfundisha bibi harusi wangu abakie waviwango. Mwenzie nilifundishwa na wifi yangu Grace. Usafi na kupendeza mpaka usiku ukilala. Kwa hiyo leo sisi hatujapendeza kwa bahati mbaya, nilipania. Na wifi yangu na leo alihakikisha yupo na mimi muda wote, sijikosei.” “Nitaiga mama matron wangu.” “Hayo ndio maneno. Sasa twendeni tukale, maana chakula cha hapa mimi huwa kinanichanganya akili. Nakipenda sana.” Wakaongozana huku vicheko vikiendelea, Nanaa ndio mzungumzaji mkubwa akionekana amezoeana vizuri tu na Joshua. Wakabakia wao wawili wakipokezana maneno na kuwaacha Naya na Geb wasikilizaji nyuma yao.

“Niambie Naya! Unaendeleaje?” Naya akamwangalia Geb aliyejua si mzungumzaji. “Naendelea vizuri kabisa. Mama anaendeleaje?” “Amekusalimu. Hivi Nanaa atakuwa anasalamu zako, kama hajasahau.” Joshua na Nanaa walikuwa wametangulia mbele kidogo wakicheka kwa sauti za juu tu. Ila ni kweli macho ya Geb yalikuwa kwa mkewe kila wakati. Akamuona anacheka kama aliyesikia kitu alichozungumza mkewe akiwa mbele yao na Joshua. Naya akabaki kuwatizama wote watatu.

Walifika sehemu ya kukaa ndani ya hoteli. Ukweli palionekana ni pahadhi yao. Naya na yeye akaagiza kinywaji, vyote vikaletwa kwenye glasi  nzuri haswa. Wote walitaka juisi. Akaamua kuuliza. “Kwani nyinyi mlikutana wapi? Na kwani mnaishi na Grace, dada yake Geb? Maana ni kama nilimsikia mama akisema, Grace na familia yake wanaishi Arusha!” “Ni kama tunaishi na Grace humo ndani. Kuanzia asubuhi tukiamka mpaka tunakwenda kulala tunakuwa naye kwenye simu. Ndiye aliyenisimamia harusi.” Naya akashangaa. “Yaani mlisimamiwa harusi na pacha mwenzie!” “Wewe mwenyewe ungemuona, ungeniibia tu! Muulize Joshua. Ni dada mzuri sana. Na alinipenda tokea zamani hata sijaolewa na Geb.” Akamuelezea kwa kifupi juu yake na Grace, na kumfanya Naya kuzidi kuvutiwa.

“Niwaulize swali jingine? Ni katika kujifunza tu. Ni sawa Joshua?” “Uliza tu na sisi tujifunze.” “Matatizo gani nyinyi mnayo kutana nayo kwenye mahusiano yenu?” Nanaa akamwangalia Geb. “Labda niseme yale tuliyokumbana nayo.” Geb akaanza yeye. “Kwa asilimia kubwa sana, sasa hivi ni kama tupo sawa, ila ni baada ya kukosea sana.” Nanaa akacheka kidogo na kuinama. Wakatulia kidogo kama waliokumbuka mengi ya nyuma. “Mbona mnatutisha?” “Hapana. Msitishike. Lakini makosa mengi ndiyo yamefanya ndoa yetu iwe hivi ilivyo sasa.” Geb akafikiria kidogo na kuendelea.

“Labda kwa kuwa tunawasimamia harusi pengine niongeze uwazi kidogo. Tumepita pagumu sana na Nanaa, mpaka kuwa hivi leo. Ilitugharimu mno mpaka kuumiza watoto wetu.” “Ni kama kila mmoja wetu akakubali hakuna maisha bila mwenzie ndipo ikabidi kurekebisha mapungufu yetu kwa lazima na kwa haraka ili kujiponya nafsi zetu.” Akaongeza Nanaa.

“Kikubwa na cha muhimu nafikiri kabla ya kuingia kwenye ndoa, nilazima kila mmoja wenu bila unafiki kujiridhisha kuwa anataka kufanya hivyo. Kwanza kwa ajili binafsi kisha mwenza. Hapo itawarahisishia sana. Msiingie kwenye ndoa kwa sababu ingine yeyote isipokuwa kutaka kwa kibinafsi, mengine ndipo yafuate.” Geb akaongeza.

“Na sisi kitu kilichotugarimu zaidi ni siri.” Nanaa akaongeza na kumwangalia Geb. “Geb hawezi kabisa mambo ya vificho. Hata kama jambo ni baya kiasi gani, ni bora umwambie tu, kuliko kumficha.” “Nafikiri hata mimi nipo hivyo aisee.” Akaongeza Joshua.

“Sasa hapo, kwenye hilo, ilitugarimu sana. Mno. Ndipo nikajifunza kuzungumza na Geb na kuwa mkweli na muwazi kwake.” “Na nafikiri kuanzia hapo, tulipoanza kuzungumza kwa wazi, ndipo tulipofunguliwa kwenye mengi mno.” Akaongeza Geb. “Labda niwasimulie kwa kifupi tu mkasa fulani. Kama Geb ataruhusu.” “Nini?” Geb akamuuliza mkewe. “Juu ya Malii.” “Kama ukiona sawa, ni sawa. Pengine watasaidika wasipite tulikopita sisi.” Geb akaridhia.

“Okay. Huyu Geb alikuwa na kundi la marafiki zake ambao walisoma na kaka tokea sekondari.” Nanaa akawasimulia mpaka mkasa wa Malii na kumbaka. Naya alishituka sana. “Hatujawahi kupita kwenye kipindi kigumu cha mahusiano kama hicho, na kwa hakika tulijua ndio ungekuwa mwisho wetu. Geb alinirudia nikiwa na mimba ya huyu Jimmy, tukijua ni mtoto wa Malii.” “What!?” Joshua akashangaa sana, asiamini Geb aliwezaje! “Nilikuwa sina jinsi, Joshua. Ilikuwa ni eidha nimkose Nanaa, au nimchukue vile alivyo! Na garama ya kuishi bila Nanaa ikawa kubwa kuliko kumchua vile alivyo na mtoto niliyedhania ni wa Malii.” “Na tulifunga ndoa nikiwa na mimba yakukaribia kujifungua huyu Jimmy, bado tukijua ni mtoto wa Malii, ambaye alipatikanika kwenye ule ubakwaji.” “Daah! Heshima yako Mkuu!” Mpaka  Joshua akasimama na kumpa mkono. Wakacheka.

“Hakika ni mapenzi makubwa sana. Mimi sijawahi kusikia. Kumbe nyinyi watu mnahistoria ngumu hivyo!” “Nilimficha Geb nikijua naokoa kumbe ndio niliharibu haswa.” Wakamuona Naya anatoa simu kwenye pochi akafungua na kumkabidhi Joshua. Pakatulia kabisa pale wasielewe Joshua amepewa nini asome kwenye simu ya Naya.

Akasoma, wakamuona amebadilika ila akacheka kwa masikitiko. “Ila mimi sijamjibu.” Wakamsikia Naya akijitetea, Geb na Nanaa kimya. “Umejua sasa kama Bale amefika salama?” “Nimeshindwa Joshua. Alinipigia nikiwa najiandaa, kabla hajazungumza kitu cha maana simu ikakata. Nimempigia zaidi ya mara tatu, simu yake haipo hewani. Moyo wangu umesita kumpigia Malo sababu ya huo ujumbe alionitumia jioni ya leo, muda mfupi hata kabla ya Bale kunipigia. Niliogopa hata kukwambia tena kwa yale aliyokuwa akikwambia Zayoni. Nilijua nitakuchanganya zaidi.” “Sasa kwa kuficha jumbe za namna hii ndio utanichanganya zaidi, Naya.” “Ndio nimejifunza leo, Joshua. Na nimekusikia kwamba ni bora ujue tu.” Nanaa na mumewe kimya.

Joshua akatulia kidogo kama anayefikiria. “Naomba usikasirike Joshua.” “Sasa umejua kama Bale amefika salama au la!” Joshua akarudia tena swali. “Hapana Joshua. Mimi ninamjua Malo. Usifikiri kumchukua Bale ni kwa ajili yakumsaidia Bale! Ni kama hivi. Kwamba nikimkosa Bale, basi nimpigie yeye.” “Basi acha mimi nikampigie.” “Nakushukuru Joshua. Na samahani. Najua nakuingiza kwenye kero.” “Usijali.” Joshua akambusu na kutoka. Akawaacha wao watatu hapo. “Samahanini jamani. Hiyo stori yenu imeniogopesha sana.” “Usijali.” Akajibu Geb na kutulia.

Nanaa akamwangalia mumewe. Naya akashangaa Geb anacheka na kutingisha kichwa. “Nanaa!” “Sio kwa undani sana!” Nanaa akawa kama anajitetea kwa mumewe aliyekuwa akimwangalia tu, Naya akawa hajawaelewa maana akili zilikuwa nje kwa Joshua. “Natamani nikamuangalie Joshua, lakini naona bora nimuache tu. Malon ni mkorofi sana. Atatutibua wote wawili usiku huu, kusiwepo hata wakumliwaza mwenzie. Acha tu nimuache apambane naye.” “Kwani ni nani?” Akawahi Nanaa kutupia swali alilotaka kuuliza tokea mwanzo, mumewe akimwangalia. Alimjua mkewe kwa kupenda stori, asingeweza kuacha apitwe.

“Tulikuwa kwenye mahusiano naye kuanzia nipo sekondari kidato cha nne, mpaka nikamaliza chuo.” “Kumbe ni mtu mliyekuwa naye kwa muda mrefu hivyo! Kwa nini ulimuacha sasa au ni kwa sababu ya Joshua?” “Ndivyo na yeye pamoja na wadogo zangu au kaka zangu wanavyodhani. Mahusiano yalishaisha muda tu, na wote wanajua. Lakini tulikuwa na mtindo wa kuachana na kurudiana. Au niseme matatizo kwenye mahusiano yetu lilikuwa jambo la kawaida. Leo asubuhi tunakuwa tumeachana, jioni au hata baada ya mwezi tunakuwa tumerudiana. Kwa hiyo safari hii wanalalamika wanasema nashindwa kumrudia au kumsamehe sababu ya Joshua.” “Ambayo ni kweli?” Akauliza Geb.

“Najua hamnifahamu na ninaweza nisiwe na ushahidi wa kutosha hata kwa Joshua, maana na yeye haya ninayowaambia yakugombana na kurudiana, na yeye amethibitishiwa leo na Zayoni, yule mdogo wangu wa mwisho. Lakini kwa Malo nilifika mwisho hata kabla ya Joshua. Siku chache kabla ya kuanzana na Joshua, alikuja nyumbani na pete yake akitaka kunichumbia. Hakika nilimkatalia na kumwambia yeye hatakuwa mwanaume atakayenitoa kwa baba Naya. Sasa leo kati ya mengi aliyoniandikia ndio ananiambia, yeye ndiye atakuwa mwanaume wa kunitoa kwa Joshua, kwa sababu nilishatoka kwa baba Naya na mengine mengi.” “Hee!” “Subiri kwanza Nanaa.” Geb akataka kumtuliza.

“Ni kwa nini ulikataa kuolewa naye.” “Geb, hiyo pete aliyonipa usiku ule niliililia kwa miaka mingi sana mpaka hata kwa wazazi wake.” “Naya!” Nanaa akashangaa. “Kweli tena. Yalikuwa ni mahusiano ya kudhalilishwa kupita kiasi, hamna tofauti na huo umalaya wa huyo Malii mliyetusimulia, sema sisi tulifika umbali wa kuishi pamoja. Kuanzia tunaanzana mpaka karibu na mwisho. Tuliishi kama mke na mume kabisa. Umalaya aliokuwa akiufanya na kusingizia ni bangi, halikuwa jambo geni na la siri. Kila mtu alimjua jinsi alivyokuwa akilala na wanawake, tena mpaka wa karibu yangu mimi. Nanaa, hapakuwa na sehemu tunakwenda mimi na yeye Malon, kusiwepo na wanawake amekwisha lala nao.” “Naya!”

“Kweli Nanaa. Ilikuwa fedheha ya hali ya juu. Maisha ya aibu na manyanyaso mabaya sana. Baba yake mzazi alituambia tukiwa na baba, wakati nikikusanya pesa za kumtoa jela, aka..” “Naya! Jela tena!?” Na yeye akapata moyo wa kuwasimulia baada ya Nanaa na yeye kujifunua kwao mpaka kusema alibakwa na rafiki ya mumewe pamoja na kaka yake. Naya naye akawasimulia kwa kifupi habari zake na Malon. Wote wakabaki wanamshangaa.

“Sasa  kwa nini ulikuwa ukiyafanya yote hayo Naya!?” “Kwanza ndiye aliyekuwa mwanaume wangu wa kwanza. Halafu kwa ukweli Malon ana jinsi fulani hivi, akiwa na mimi, utatamani masaa yasisogee. Kila mtu alijua mimi ni mwanamke wake, na akiwa na mimi popote, atatulia mno na heshima. Watu wanajua nipo kwenye hiyo sehemu kwa utulivu anaokuwa nao, hata fujo hawezi kufanya. Alinipumbaza kwa mengi nikawa nikijiambia pengine atakuja kubadilika. Na kingine nafikiri kikubwa ni kama akawa aliweka deni kubwa sana moyoni, kwa misaada ya kiuchumi aliyonisaidia tokea tunaanzana. Alisaidia sana. Kwa hiyo nikawa kama nipo naye kumthibitishia kuwa sikuwahi kumpendea pesa zake ila yeye. Nilikuwa nikimlilia, nikimsihi atulie tu anichague mimi, nibakie peke yangu, lakini haikuwahi kubadilika. Nilifanya kila kitu mpaka nilipomtoa jela na bado hakunichagua! Pale ndipo nilipojiridhisha kuwa Malon hakuandikiwa kuwa mume wangu, na hatakaa awe wangu, napoteza tu muda. Na umri unazidi kwenda, historia yetu itaendelea kujirudia vilevile. Kuachana na kurudiana kila kukicha kwa kila sababu anazochagua yeye kwa wakati huo.” “Inawezekana alikuwa ni daraja tu. La kukuvusha sehemu moja kwenda nyingine ila wewe ukang’angania darajani, hutaki kuvuka. Ndio maana hukufika popote. Huwezi kujua Naya!” Nanaa akaongeza akisikika na yeye akiwaza.

Kisha akawa kama amekumbuka kitu. “Naomba nikwambie kitu Naya. Kwa ufupi tu bila kukupoteza, ila kutaka ufikirie.” “Niambie tu.” Naya akakubali na kuangalia mlangoni kuona kama Joshua ataingia hapo. “Kuna mambo mimi nimejifunza kibinafsi kwenye haya maisha na kule tulikopitishwa na makosa mengi tuliyofanya, sababu ya kung’ang’ania watu na vitu vilivyotakiwa kupita kwenye maisha.” Nanaa akaendelea.

“Wapo watu Mungu huwatuma kwenye maisha yetu kutimiza kusudi fulani, na wakimaliza hilo kusudi wanatakiwa kuondoka kwa kuwa wameshatimiza kusudi lao. Liwe kubwa sana au dogo sana. Wakati wao ukiisha, wanatakiwa kuondoka. Iwe kusimama na wewe kwenye msiba, au shuguli fulani maalaamu hata ya kimungu. Wakishatimiza kusudi, wanatakiwa kuondoka. Ukiwang’ania wabaki, huwa wanaweza kuleta madhara kwako binafsi au kwenye lile kusudi zima waliloitiwa na kulisimamisha. Kwa kuwa hawakupewa uwezo wa kubeba lile jambo ila kulianzisha au kulisogeza sehemu moja kwenda nyingine. Chukulia mfano wa nabii Elia. Alipokimbilia pangoni, akiogopa kuuwawa na Malikia Yezebeli. Unakumbuka habari zao kwenye kitabu cha 1 wafame 18?” Naya akatulia akisikiliza kwa makini.

“Nenda kasome vizuri. Kote alikopita nabii Elia. Yote MAKUBWA aliyofanya mpaka kufikia kwenye kujificha pangoni, njaa ikimuuma, akimuomba Mungu kufa tu, kwa kuwa alifika mwisho kwenye maisha, anaogopa kuuwawa na malikia tu. Tena mpagani, hata hamjui Mungu wake aliyetenda miujiza mbele za watu wote wakishuhudia! Yeye mwenyewe nabii Elia alifanya mambo makubwa yaliyojulikana sana mpaka Mfalume, mumewe Yezebeli akawa anamtafuta kwa makubwa aliyoyatenda. Kuzuia mvua isinyeshe. Haya, akaja kuita moto kutoka mbinguni, Mungu akafanya yote hayo kujidhihirisha kwake na mbele ya wote kwamba yeye ni Mungu mwenye nguvu. Lakini utisho tu wa maneno matupu ya malikia Yezebeli, akakimbia akaenda kujificha pangoni. Hana chakula, hana malazi anaomba kifo! Unakumbuka Mungu alimtumia kunguru ili amlishe?” Naya na Geb kimya wakisikiliza wakitaka kusikia analinganisha nini na ya Naya.

“Kwani yule kunguru aliendelea kumlisha mpaka mwisho wa maisha yake yote?” Nanaa akauliza na kuendelea. “Wewe unafikiri kama Elia angemng’ang’ania kunguru amlishe, na kukataa kumtii Mungu ili atoke pale, unafikiri aliyotenda yote baada ya pale mpaka kuandikwa kwenye bibilia yangetokea?” “Asingeweza kufanikisha.” “Sasa? Wakati mwingine Mungu huwa anatuambia kwa njia nyingi sana mpaka kwa matukio fulani fulani akitaka tuendelee kwenye maisha lakini tunakuwa wagumu kukubali, kuchukua hatua. Kwa hofu au kwa sababu ya kuona tulipo ni bora kuliko kukubali kukabili adha ya mbeleni. Tunaridhika palepale kwa sababu za kibinadamu na kuishia na vile tunavyodhani vinatustahili kumbe Mungu anakusudia makubwa zaidi juu yetu. Na Hawezi kuweka divai mpya kwenye kiriba cha zamanikilichochakaa. Sasa wewe akili kumkichwa. Endelea, nisikuchanganye na mengi.” Nanaa akaona amuache aendelee tu.

“Inawezekana upo sahihi Nanaa! Inawezekana  kabisa. Ila ukweli alijua nimetulia, nimejifunga kwake na ni mwaminifu sana tu. Nikimsubiria yeye achukue hatua ingine. Hilo alikuwa akilijua na ndilo anang’ang’ania mpaka leo hata kwenye huo ujumbe akiniomba msamaha, anasema hatuko pamoja kwa sababu yake yeye mwenyewe kushindwa kusimama kwenye nafasi yake, ila sasa hivi yupo tayari akiujua moyo wangu, kuwa nipo namsubiria tu yeye achukue hatua ya msingi. Hakuwahi kutegemea mimi kuja kumwambia nimefika mwisho na sitabadilika tena. Hii mara ya mwisho ndiyo amejua ni kweli nimemaanisha kwa kuwa pia ameniona nimetulia na Joshua, kitu ambacho hakutegemea mimi kuja kupata mwanaume kama Joshua. Aliyetulia na akili za kiutu uzima hivi.”

“Maana alishanitoa kwa wanaume wawili ambao wao walikuwa wababaishaji tu na hilo pia amenikumbusha kwenye huo ujumbe niliompa Joshua asome. Mmoja alinikuta naye kijana tuliyekuwa naye kanisani. Kila mtu alijua angenioa, kama hivi Joshua. Mpaka wazazi na mama walimpenda sana. Lakini niliachana naye nikaanza mahusiano na yeye Malon. Lakini huyu kijana wa kwanza mimi sikuwahi kumkubali na ndio ukawa ugomvi wangu na mama, na ndio maana mama hakumpenda Malon akahisi ananipotosha. Ila sio kwamba nilikuwa kwenye mahusiano mazuri na Ino ndipo nikamuacha sababu ya Malo! Hapo Malo hajasema ukweli. Hata bila yeye Ino asingenioa!” Hapo napo Naya akawasimulia kwa ufupi kama akijitetea kwa ujumbe aliotuma Malon na kumpa na Joshua asome.

Huku kwa Joshua.

Joshua akaanza kwa kumpigia Bale. Haikuwa hewani. Akarudia tena na tena, hakumpata. Ndipo akajaribu kumpigia Malon akitumia simu ya Naya. Akapokea kwa haraka. “Naya, mama!” “Ni mimi Joshua.” Joshua akamuwahi. “Umempokonya na simu yake?” Malon akamuuliza kwa kejeli. “Tulitaka kujua kama Bale alifika salama.” “Wewe kama nani?” Malon akamuuliza tena. “Kama mpenzi wa Naya, mume mtarajiwa na shemeji yake Bale.” Malon akacheka kwa kejeli. “Ndivyo unavyojiaminisha hivyo? Hujui walipita watu kama wewe kwa Naya, uliza wapo wapi sasa hivi!” “Tunataka kujua tu kama Bale amefika salama.” “Kama unayejali vile! Si wewe aliyekuomba kazi ukamkatalia? Si niliwaachia Bale ili muweze kuyatengeneza ya familia, ukashindwa? Ule ulikuwa mtihani kwako, lakini ulishindwa vibaya sana kama wanaume wengi tu waliopita kwa Naya na kushindwa kama wewe. Mimi nimeweza kuwa na Naya pamoja na familia yake, tukatengeneza familia yakueleweka. Lakini wewe ni mbinafsi, mtu unayejiangalia wewe tu, na ni hatari kwa familia ya kina Naya, na sitakuruhusu.” Joshua kimya akisikiliza.

“Walipita wenzio kama wewe, wakakubaliwa na kujulikana mpaka kanisani, nikifikiri watamfanya Naya awe na furaha, lakini wamekuwa wapuuzi tu kama wewe, pamoja na elimu zao kama wewe, nikaishia kumchukua Naya wangu. Na yupo mwenzio alimchumbia kabisa Naya, kama hivyo wewe, kanisani kabisa, Naya alimuacha kwa ajili yangu. Sembuse wewe hata ndugu zake tu hawakutaki! Kwanza wameshakuona wewe ni mnyanyasaji tu. Umeingia kwenye maisha ya Naya umekuwa mtu wakuchukua tu bila kujali furaha ya Naya mwenyewe na ndugu zake! Masharti mengi ya kiwivu tu na kumbana tu Naya. Sasa kama unafikiri kukubaliwa na baba yake Naya ndio kila kitu, uliza historia yangu mimi na Naya. Hata mimi huyo mzee alinikubali sana tu. Amehangaika kunitoa jela na mengine mengi.” Malon akaendelea.

“Upo na Naya kwa sababu mimi niliruhusu. Naya ananipenda mimi. Hajawahi na wala hatakaa akampenda mwanaume mwingine, kama anavyonipenda mimi. Hilo ukae na uelewe, ili usijipotezee muda. Ilikuwa ni mimi tu sikuwa tayari, nikitaka nijijenge kwanza ili Naya asije ishi kwenye mazingira mabaya. Ila sasa hivi nipo tayari na Naya wangu, narudi. Tena narudi na kumchukua mwanamke wangu moja kwa moja. Siwezi kumuacha Naya kwa mwanaume mpuuzi, mbinafsi na mchoyo kama wewe!” “Kama umemaliza kuzungumza hicho unachoamini kipo sahihi kichwani mwako tafadhali tujulishe tu kama Bale alifika salama na upo naye.” Joshua akarudi kwenye swali lake.

“Kwani unajali nini au unafiki tu? Unataka kumdanganya nani ambaye ameshindwa kukusoma wewe? Hata Bale mwenyewe anakujua tabia zako. Hana mpango hata wakuwa karibu na wewe. Kwa hiyo acha unafiki, usimtafute. Umejawa sifa tu kujitangaza utajiri unaonufaika nao wewe mwenyewe, lakini huna chochote! Acha kumbana Naya, mrudishie simu yake. Na ukiendelea hivyo nitamnunulia simu ingine. Uache manyanyaso.” Simu ikakatwa.

Japokuwa alijaribu kutulia, lakini kwa hakika Joshua alikuwa ametibuka moyo na akili vibaya sana. Akashindwa hata kurudi ndani, kwa kuwa hakuwa na jibu la kurudisha juu ya Bale ila kashfa tupu. Akabaki amesimama hapo nje akijaribu kutulia. Mengi aliyoyasema Malon, hayakutofautiana na ujumbe mrefu aliokuwa amemuandikia Naya. Akimkumbusha walipotoka, waliyopitia, waliopita kwenye mahusiano yao, na ahadi nyingi tu na nzuri kwa Naya pindi watakapoendeleza mahusiano yao ambayo hayakuwahi kubadilika. Joshua alibaki palepale amesimama, na kushindwa hata kujisogeza. Maneno ya Zayoni nayo yakajirudia kama kumthibitishia kuwa ni kweli Naya na Malon huwakuwahi kuachana moja kwa moja. Wakati wote hurudiana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Kwa hiyo huyo Ino sio kwamba kweli alikuwa amekuchumbia kisha kumuacha sababu yake?” “Hapana Geb! Hapo Malo hajasema kweli. Ni ile kudhania kwa watu au wazazi kutamani itokee hivyo kwa kuwa tulikuwa pamoja. Sikatai kama tulijaribu. Lakini Geb, hata baba na Bale walikuwa wakijua nitaishia pabaya sana endapo nitakubali kuolewa naye. Na nikawa muwazi kwake na mama pia. Nikamkataa mbele ya mchungaji na mama. Ikaisha hiyo. Tukaanzana na kuendelea na Malon.” Naya akawasimulia mpaka mambo ya Joshua, ila kwa kifupi tu. Mpaka hapo Joshua akawa hajarudi.

          “Sikuwahi kuacha kulia na kumbembeleza Malon anioe. Nilijifunga kwake nikiamini anachosema mimi ndio mwanamke pekee amewahi kunipenda na hataruhusu mwanaume mwingine awe na mimi. Nilisubiria hiyo ndoa, bila kuchoka mpaka niliposalimu amri na kusadiki Mungu hakukusudia mimi niwe na Malo.” “Kweli Naya ungekubali kuolewa na mtu wa namna hiyo!?” “Angewahi kabla ya mkasa wa Ritha na kifo cha mama, hakika ningekubali Nanaa. Hata baba aliniuliza swali kama hilo. Nikamwambia nisingejali hata kama kipato chetu kingeishia kumtoa yeye jela tu, nilikuwa tayari kuwa naye. Na yeye anajua hilo na anajiaminisha nalo mpaka sasa. Baba alikuwa akiumia sana. Alikuwa akiniombea kupita kiasi, nafikiri mpaka Mungu akaamua kuingilia kati kunikomboa kwenye hicho kifungo.” Joshua akarudi.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

          Ukweli alionekana kubadilika kabisa usoni. Akakaa kama ambaye hajui azungumze nini tena. “Tafadhali usimsikilize Malon, Joshua. Usikubali akakutibua moyo, kwa kuwa mimi namfahamu Malon. Naomba tulia mpenzi wangu. Tuangalie ya kwetu tu.” “Umefanikiwa kujua kama dogo amefika salama?” Geb akauliza kwa kujali. Joshua akajicheka. Wote wakatulia wakimwangalia akiwa ameinama akiitizama simu ya Naya mkononi mwake.

          “Mimi ngoja niwashauri Joshua. Nimemsikiliza kwa makini sana Naya. Na nashukuru amekubali kuwa muwazi kwetu. Ninachotaka kuwahakikishia ni hiki, mnakopita nyinyi si pageni wala si pahatari kama inavyoweza kuhisika sasa hivi, kipindi hiki mnachopitia. Na sisi tulipita hapo. Mimi na Nanaa, tena kwa garama kubwa sana, nafikiri Joshua nilikusimulia kwa sehemu. Ambacho sikukwambia au kuweka msisitizo ni kwamba, kote tulikopita, tulipita kila mtu akiwa kinyume na mimi kumuoa Nanaa isipokuwa James na mama, pamoja na Grace tu.”

“Watu wakaribu yetu walijaribu kupinga si kwa maneno haya ya kashfa tu, hapana. Walikwenda umbali wa mpaka kutoa uthibitisho kanisani wakipinga nisimuoe Nanaa. Mmoja wao alisema na kutoa uthibitisho akipinga hiyo ndoa kuwa alishamuoa Nanaa, nchini Nairobi. Kwamba Nanaa ni mke wake kihalali.” “Haiwezekani!” “Kweli Joshua. Na mbaya zaidi, yule mama mkubwa niliyekusimulia alinilea, ali...” “Mama yake James?” Joshua akauliza. “Ewaa! Alithibitisha ni kweli kuwa alipokea mahari ya Zinda, rafiki ya Geb na kaka James, na alinioa.” “Haiwezekani Nanaa!” “Wewe msikilize Geb.” Nanaa akataka mumewe aendelee.

          Walishaagiza chakula. Kikaletwa. “Naombeni tumshukuru Mungu kwa chakula kabla hatujaendelea.” Nanaa akaomba. Ndipo yeye mwenyewe Nanaa akaanza kula kama kawaida yake. Chakula hakisubiri kwenye sahani. Naya na Joshua wakataka kumsikia Geb ambaye yeye aliomba tu Samaki wakuchomwa na tango pamoja na nyanya, basi.

          “Haikuwa rahisi kama hivi mnavyotuona sasa hivi. Rafiki wote waliokuwa kama familia. Wakila na kunywa alivyotayarisha mama G, baadaye akaja Nanaa aliyekuwa akiwakarimu nyumbani kwetu. Maana sisi tulianza kuishi pamoja, sio kama nyinyi. Maisha ya ndoa yalianza ndipo tukaja kubariki ndoa. Anyways.” Geb akaendelea. “Kila mtu alitugeuka. Nilikuwa nikichafuliwa mno kwenye kundi letu la hao marafiki. Walituwekea mitego mpaka ushirikina wakitaka kumdhuru Nanaa, akaharibiwa miguu ikawa kama matende lakini yaliyojaa malengelenge.” “Nakumbuka kumsikia Nanaa kusema hivyo kwa baba Naya, siku ile ya mahari ya Naya! Aisee!” Joshua akahamaki. Geb akacheka.

          “Acha kaka. Na usiombe akurudi mtu wa karibu yako, anayekujua vizuri mpaka  madhaifu yako. Anahakikisha anakupiga pale anapojua utaumia haswa.” “Ndivyo anavyotaka kunifanyia Malon.” Akalalamika Naya. “Sasa nyinyi nguzo yenu iwe umoja.” “Sawasawa Nanaa. Hicho anachowaambia Nanaa, ndio kitu pekee kilichotufanya mnatuona hapa na furaha na watoto wetu wanakuwa vizuri. Walituvuruga, kiasi ya kwamba kama si Nanaa, mke wangu kukubali yaishe na kujenga familia hii unayoiona na kumsikia Grace akimtaja kila mara, tusingekuwa hivi. Na wanangu wasingekuwa vile. Ndio maana mama anamchukulia Nanaa si mkwe, ni mziwanda wake aliyechukua nafasi yangu.” “Geb linamuuma hilo! Wewe kubali yaishe.” Nanaa akaongeza wakacheka.

          “Mimi nilishazoa kuwa kiziwanda! Lakini sijawahi pewa mapenzi anayopewa Nanaa na mama.” “Basi kilio hicho cha Geb, hata Grace anacho.” Nanaa akaongeza akiendelea kula. Angalau wakacheka. “Hata Joshua aliniambia hata kabla sijawaona aisee. Alivutiwa sana jinsi mama G anavyokupenda. Alisimulia mpaka nyumbani!” “Na si kwa unafiki Naya. Yule mama ananipenda haswa. Mimi nimeyajua mapenzi ya mama, nikiwa mkubwani hivi, kwa kupitia mama G. Ila niweke msisitizo hapo kwa Geb, kwenu Joshua na Naya, majaribu yenu yatakuwa mepesi sana mpaka watawashangaa kama mtasimama pamoja bila usiri. Sisi tuliwaziba midomo, mpaka leo hawaamini.” Nanaa akaongeza.

          “Nikuulize Nanaa, sasa Malii alitoka jela?” “Geb alihakikisha anaweka fundisho kupitia Malii, Gozi na Zinda. Hakuna anayetusogelea. Kesi zao zilinguruma, na Geb alihakikisha anatumia pesa, haki ifuate mkondo. Yupo dada mzuri sana, anaitwa Sonia, mtoto wa Tambo. Yule aliyekuwa jaji mkuu kipindi cha awamu ya tatu ya uraisi.” “Namkumbuka yule jaji, na yeye alipataga hekaheka ya familia kweli!” “Ewaa! Alikuja kutusimulia Sonia mwenyewe kipindi fulani baada ya kesi kuisha, mama alimualika nyumbani kama kumshukuru. Akaja na familia yake. Tukayazungumza hayo. Na yeye anahistoria ngumu! Nitakuja kukukutanisha naye. Ni dada mzuri tu. Na hata kwenye harusi nitawaomba tumualike. Sio dada mbaya, hana mambo mengi.” {Simulizi juu ya Sonia Tambo ipo kwenye Simulizi ya “Zaidi ya Kutamka”. }

          “Ila kujibu swali lako, Malii yupo jela.” “Na hatakaa akatoka.” Akamalizia Geb. “Kweli!?” “Oooh yeah! Kosa la ubakaji na vitisho alivyofanya mpaka kutupiga na kuwalevya walinzi wangu, kutuvamia na silaha, ni kusudio la kutaka kuua!” Geb akaongeza. “Daah! Na hao wenzie.” Nanaa akacheka.

          “Bwana Geb aliwatenda wale watu, hawatakaa kutusahau!” Nanaa akaongeza. “Siku wanakamatwa Gozi na Zinda, kwanza alikuwepo mwanasheria wa kwanza kabisa ambaye ndiye aliyetutambulisha kwa Sonia baada ya yeye kuugua sana. Siku hiyo tuliwatega Gozi na Zinda mpaka wakakiri wakitaka kumuumiza Geb, mbele ya wazazi wa Malii waliokuwa wamewaleta kwa makusudi mjini, kutokea migombani, kuja kwa Geb kudai mtoto wa Malii, ambaye naye tayari tulishamfungulia kesi ya ubakaji ila hajulikani alipo.” “Nyinyi jamani! Mtu akiwaona hivyo hawezi kudhania kama mlipita huko!” Naya akashangaa.

          “Nakiri hayo yote ndiyo yaliyotusogeza pamoja, na kuongeza mapenzi kwetu, na kushikamana. Sisi majaribu yalituweka pamoja zaidi.” “Naomba nisimulie kidogo Nanaa juu ya usiku huo mpaka kuwaweka jela.” Joshua akataka kusikia. “Kuleni sasa. Usiku huu tumekubaliana na Geb tuwe kwa ajili yenu tu. Uzuri wa Geb huwa si mwepesi wakusema ‘ndiyo’ kwa watu. Ila akikukubalia, ujue atasimama na wewe. Ndio uzuri wa mume wangu. Na hana ‘ndiyo’ za hovyo au niseme nyingi kumfurahisha mtu.” “Nimemuona leo mpaka ameongea yote haya! Nikashangazwa na kumshukuru Mungu wangu! Hakika alijua nitawahitaji. Malon amenisema maneno mabaya sana, yanayoendana na ukweli. Nikaingiwa hofu kwa kuwa amefanikiwa kumvuta Bale upande wake!” “Lakini sio mimi, Joshua! Mimi nipo na wewe na ndio maana Malon anahangaika. Alitegemea ingekuwa rahisi kama alivyozoea kurudi na kunichukua kama mzigo anaokuwa ameacha mahali. Lakini amejua amenikuta kwenye mikono sahihi, ni wewe.” Naya akamgeukia vizuri Joshua.

          “Anachojaribu kukifanya ni kukutingisha mpaka utingishike, kama siku ile mbele ya baba juu ya maswala ya gari! Unakumbuka?” “Nakumbuka Naya.” “Sasa ataendelea kukujaribu sana ili tu ushindwe, kwa sababu kwanza umeshamtisha na Malo hapendi kushindwa.” “Kumbe afadhali sikumjibu.” “Tena kama hukumjibu ndio umemuumiza zaidi. Malon mtoto wa mtaani na mtu wa ugomvi. Ungemjibu ndio ungejishusha kwenye hadhi yake. Tafadhali tusigombane sababu ya Malon au Bale.” “Na hilo mlikumbuke aisee. Si kwa leo tu, hata baadaye kwa sababu majaribu yanaendelea kuwafuata. Mwanamke wako ni mzuri Joshua! Yupo kama mwanamitindo! Anavutia kwa macho. Watawasumbua sana.” Wote wakacheka.

          “Mimi nawaambia kweli. Muulizeni Geb kama changamoto zimeisha.” “Wanamtaka Nanaa wangu mpaka leo. Ila sema sasa hivi wanao msumbua sio watu wa ngazi ya chini, wenye kipato cha juu kama sisi, tunaokutana nao kwenye biashara na maisha.” Naya akajikonyeza kuwa Geb anajitambua anayo pesa! “Sasa mnafanyaje?” Joshua akauliza. “Kwanza mimi mwenyewe nampenda Geb wangu. Sithubutu kujijaribu wala kujaribiwa.” Wakacheka sana. “Kweli Joshua. Shetani mjanja na hila zake nyingi kwa kuwa na yeye anatufahamu kwa kipimo karibu na Mungu. Kumbukeni habari za Ayubu kwenye bibilia. Alimjaribu Ayubu kwa vile alivyomfahamu hata kumwambia Mungu! Hawezi kukujaribu kitoto. Anakujaribu haswa akijua lazima atakupata tu.” “Yeye mwenyewe Nanaa akaanzisha siku ambazo ananiachia simu yake.” Wakacheka sana.

          “Haiwezekani!” “Kweli kabisa. Hata tukiwa ofisini, anakuja kuniletea. Jumbe na simu zake napokea na kujibu zile ninazoona hazimuhitaji yeye. Wanaume ninaoona hawana heshima, ila nataka pesa yao na wao wanataka huduma yangu, nimehakikisha wanaelewa kumsogelea Nanaa ni kosa ambalo siwezi kusamehe haswa kujua ni mke wangu na mama watoto wangu!” “Na hapo Geb hana aibu jamani! Anamuweka sawa huyo mtu mapema tena kwa wazi kabisa.”

“Kingine, tunapendana kiasi ya kwamba watu wanatujua. Hata mimi nilimuomba Nanaa anilinde kabisa. Akihisi hatari, asiache kuniambia na kuomba kwa ajili yangu. Hakuna safari nakwenda bila mke wangu. Nikitoka hivi lazima awe kama hivi pembeni yangu. Nipo naye kila mahali na narudia tena. Sisi tunaomba. Tulishajijua sisi ni waharibifu mno, bila Mungu. Hakuna kipindi tulimuacha Mungu tukabaki salama. Muulizeni mama au huyu Nanaa. Na huwa tunaharibu haswa. Kwa hiyo kwa upande fulani sisi kwetu maombi tumefanya ni dini kabisa. Wala tusidanganye. Linapofika swala la kuomba, hata kama hatujisikii, tumetoka kufanya ibada ya familia, tumechoka na siku ya kazi pengine ilikuwa ngumu, sisi wawili, lazima tukifika chumbani tupige magoti na kuomba. Hata maneno machache tu. Na tunajua kabisa, wakati mwingine hatumaanishi sababu ya uchovu, lakini katika hilo tulikubaliana tufanye tu. Kujihudhurisha mbele za Mungu sisi wawili, kwa pamoja.”

          “Tena hata kama tumeudhiana. Kwa sababu maudhi yapo wala tusiwadanganye. Wakati mwingine hata kama Geb au mimi nimekasirika, lakini tutapiga magoti tu hata tukiwa tumenuniana.” Naya na Joshua wakacheka. “Tuliwaambia katika hilo tulikubaliana iwe kama dini tu.” Geb akaongeza na kuendelea.

          “Joshua ulitaka kujua juu ya Malii, Zinda na Gozi.” “Aisee kweli Geb husahau kama mwanao Magesa!” Walicheka sana walipomkumbuka Magesa. “Na wale wengine wapo vilevile, sema mwanangu Magesa yeye mdomo huwa unamponza! Hawezi kunyamaza Magesa mwanangu, kama mama yake!” Walicheka sana.

          “Anyways. Kwa ushahidi wa kukiri usiku ule mbele ya wazazi  wa Malii, yule mwanasheria pamoja na sisi wote wakisema wanajua kama Malii alinibaka, moja kwa moja wakageuka mashahidi wangu. Na Geb akakusanya ushahidi wa jumbe walizokuwa wakitumiana kabla na siku yenyewe niliyobakwa kwenye sherehe nyumbani kwetu kumtaarifu Malii kama ni muda mzuri wa kuja au la ili aje afanye uchafu wake!” “Haiwezekani Nanaa!” “Kweli Joshua. Geb anapokwambi ogopa kupigwa na watu wa karibu yako wanao kufahamu, hakika ogopa.” Nanaa akaongea kwa unyonge.

          “Kaka aliumia sana kwa walichonitendea marafiki zake. Na yeye alisomea mambo kama Geb.” “Yeah, si mlisema wote walikuwa darasa moja?” “Ewaa! Ila sema Geb alikwenda kumalizia shule yake nje ya nchi, wao wakamaliza hapo chuo kikuu cha Mlimani pamoja, wakawa kama familia. Kwa hiyo kaka bila kumwambia mtu akaanza uchunguzi kujua Malii alijuaje kama ule ndio ulikuwa muda sahihi wa yeye na majambazi wenzake kuja na kuweza kufanya uharamia! Ndipo akagundua siku ile Gozi alikuwa akisaidiana na Malii. Anamwambia kila kitu kinachoendelea pale, na akaanza kufukuza wageni kwa utani akiwaambia watu waondoke ili nipumzike, kumbe ilikuwa ili tubaki peke yetu, Malii aje na majambazi yake.” Nanaa akawasimulia kwa uchungu kama aliyekumbushwa machungu.

          “James aliponiambia tu hivyo. Nilihakikisha Gozi anahukumiwa kama Malii. Akae ndani ili asije kumdhuru mtu mwingine. Hakika nilihakikisha, na Sonia alinisaidia vizuri sana. Na yeye akahukumiwa kwa kosa la kushiriki ubakaji na mauaji. Zinda yeye hatakaa akatoka japo mwanzoni alihukumiwa muda mfupi kwa kosa la kukiuka restraining order lakini nilimsaidia Grace. Zinda akiwa jela kwa kosa la kwanza, tukamshitaki kwa kosa jingine, alihusika na vifo vya watoto wa Grace, hiyo nayo ni habari ingine lakini kwa upande wa kiushirikina. Ilinigarimu sana mpaka nikapata ushahidi wa kuhakikishia mahakama kuwa anahusika na vifo vyao. Tulinyaka mazungumzo kati yake na mama yake walivyokuwa wakipanga njama ya kutoa kafara familia ya Grace ili yeye Zinda akombolewe kiushirikina.” “What?!” Joshua akahamaki.

“Kwamba ilikuaje?” Ndipo Geb akawaeleza kwa ufupi historia ya Grace na Danny, mpaka vifo vya mapacha wao. {Simulizi nzima ipo kwenye naomisimulizi.com katika Simulizi ya “Ni Wangu!”} “Nyie shetani jamani?” “Acha Naya. Wale marafiki walitugeuka vibaya sana. Zinda amefungwa na mama yake.” Nanaa akaongeza. “Nilihakikisha natafuta ushahidi mpaka akaongezewa hukumu ingine ya kifungo cha maisha, mama yake naye alikamatwa na kuhukumiwa kama mwanae, pamoja na mganga wao pia nilihakikisha anakaa ndani ili asije dhuru familia ingine.” Geb akamaliza na kutulia kabisa.

“Aisee walishika adabu. Hakuna mwenye hamu ya Geb. Na hapo mkumbuke mwanzoni kabisa Geb aliwaonya mpaka kwa kupitia mwanasheria. Wasiwahi kurudi nyumbani kwetu. Waliwekewa restraining order.” “Na ndilo lilisaidia kumuweka ndani Zinda wakati nikitafuta ushahidi wa vifo vya watoto wetu.” “Sasa kipi kiliwapelekea kuwawekea hiyo restraining order tokea mwanzo?” “Katikati ya machafuko ya mwanzoni, wake zao walikwenda kumfanyia mama fujo, akiwa kazini kwake.” Geb akawasimulia tena kwa kwa ufupi. “Ndipo waliporudi nyumbani tena...” “Ikawa wamekiuka agizo la kisheria!” Akamalizia Naya.

“Sawasawa. Ndipo Zinda alipowekwa ndani kwa kosa hilo la kukiuka restraining order, nikiwa sina ushahidi wa kutosha wa mauaji waliyoyafanya kiushirikina. Na Sonia aliniambia kosa la ushirikina ni kesi ngumu sana. Mpaka ushahidi wa kueleweka kweli uwepo ndipo kesi zake zinaweza kushinda. Sasa kwa kuwa nilikusudia haki itendeke kwa watoto wa Grace waliokuwa wameuwawa kikatili, Zinda akiwa ndani ndipo nilipopata sasa nafasi kumfanyia uchunguzi wa kutosha wa hayo mauji ya kishirikina waliyofanya kwa hao mapacha wetu. Nilifunga nakuomba nikimlilia Mungu kilichotokea kwa watoto wa Grace, wasije weza kukifanya kwa watoto wa mtu mwingine. Nikamsihi Mungu anipe uwezo na aniinulie watu watakao nisaidia kuwakamata na wahukumiwe kwa haki. Basi Mungu akasadia. Huyohuyo Sonia akapata taarifa kamili. Nafikiri ni kutoka Usalama wa Taifa, yeye mwenyewe hakukiri, ila nahisi tu kwa kuwa anatoka kwenye familia ya watu wanaofanya kazi huko Usalama wa Taifa kwa miaka mingi tu. Aliweza kunyaka mazungumzo yaliyokuwa yakiendelea kati ya Zinda na mama yake. Na jumbe zao zote walizokuwa wakiandikiana wakiwekeana mipango ya kuwaita huko kwao Tabora na kumwaga damu yao njiani.” Geb akawasimulia mengi waliyoyafanya na kuwaacha hoi.

“Daah! Kumbe afadhali tumezungumza. Binafsi mmenijenga sana. Nilifikishwa sehemu nikawa nimehisi nimebanwa!” “Usitishwe na maneno hata kidogo. Na wewe Naya hivyohivyo. Wanaweza kukuletea maneno yanayofanana na kweli tupu juu ya Joshua, tena hukohuko ofisini kwenu.” “Mbona tayari! Natamani ningewafahamu mapema.” “Huu ndio wakati wa bwana. Tushukuru hatujachelewa.” Joshua akaongeza kwa Naya. “Aisee tunawashukuru sana.” 

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

          Wakaanza kula. “Sasa mbona wewe huli? Au kimeshapoa?” Nanaa akamwangalia Geb, na kuanza kucheka. “Naya anakuuliza.” Geb akacheka huku anaangalia yule samaki mzuri kwenye sahani. “Anavutia!” Naya akasifia jinsi alivyowekwa kwa ustadi pale kwenye sahani, akiwa na rangi nzuri ya kuokwa. “Sio machoni kwa Geb. Hapo ameshamtoa kasoro huyo samaki, na hatakwambia hizo kasoro wewe kwa kuwa sio mama au mimi. Alivyoletwa tu hapa, mimi nilipomuona tu na kumwangalia Geb, nikajua hatamla.” “Kwa nini!?” Naya akauliza akishangaa asione tatizo. “Wewe jiachie tu. Huyu kwenye swala la chakula hutamuelewa. Nasubiri mimi nishibe, niombe wanifungashie huyo samaki, nimpelekee mama yangu, akale wakati nampigisha stori.” Akarudi kuendelea kula. Geb akabaki akimwangalia Nanaa alivyokuwa akila kama ametoka jangwani kusikokuwa na chakula. Akamuita muhudumu achukue kile chakula chake akakifunge. Nanaa akamwambia akaongezee na ndizi tatu za kuchoma.

          Naya akawa hajaelewa. Nanaa akaona amsaidie asibaki anashangaa. “Geb ni mvivu wakula. Na anashida ya kula kama yule mwanae Liv, ndio maana unamuona Liv wangu hana mwili kama wa Magesa. Ila angalau kidogo Jimmy kuna vitu vyake ukimpikia anakula. Ila hawa wawili ni shida ya familia. Kwa hiyo kabla sijatoka naye huyu kwenda popote, nahakikisha anakula na kushiba, ndipo tunatoka. Lasivyo analala na njaa, na haimsumbui hata kidogo.” “Sasa hivi tunavyokula, hatamani?” “Hata kidogo.” Akajibu Geb mwenyewe. Wakacheka.

“Na usifikiri anakutania. Adhabu yakumnyima Geb chakula sio adhabu kwake. Ni nafuu kubwa, kwanza atashukuru hata usipompa tena chakula, endapo amepata hata mlo mmoja wa siku. Wewe kula tu muache huyu.” “Lakini umenifanya nifikirie, ni kweli sijawahi kumuona Geb akila.” Joshua akajaribu kuvuta kumbukumbu.

          “Sina shida mbaya kwa kiasi hicho bwana, Joshua! Wewe utakuwa umesahau tu. Ukija nyumbani huwa na kula, labda inaweza kuwa isiwe chakula mnachokulaga nyinyi wote, au muda wenu nyinyi wakati mkila, ila nakula bwana!” Akawasogelea mtu ambaye alimfanya Nanaa kushituka mpaka Geb akageuka, na yeye akabaki ameduaa.

Asiyesikia la Mkuu.

         “Huwa napenda juisi ya hapa.” Danny akaanza. Kimya. Naya akashangaa Nanaa wa maneno mengi na Geb kimya wanamwangalia. “Najua nimebadilika sana, ni kwa sababu ya kuugua. Niliugua sana.” Kimya. “Halafu bwana Nanaa ulikuwa sahihi, yule Sara hakuwa ametulia, yupo kama mwehu! Kanisababishia matatizo na kuniacha na gonjwa! Mimi nilijua tu atakuwa ni yeye kwa sababu mimi na Grace tulikuwa tumetulia sana. Sasa nilipopatwa mkanda wa jeshi, homa kuwa kali sana, nikahisi tu. Eti yule mtoto nampigia simu, ananiambia kama jambo la kawaida vile! Eti niache kupaniki, UKIMWI ni jambo la kawaida sana siku hizi, wala si jambo la ajabu. Watu wanakufa na maradhi kibao na kuwaacha wenye UKIMWI, mimi natakiwa tu kuwahi dawa, yeye amekuwa akitumia dawa muda tu na yupo sawa. Ndio ikabidi kwenda hospitalini wakaniambia ni kweli, nikaanzishiwa matibabu, hivi hapa ninanafuu sana.” Kimya.

          Naya akawatizama Geb na Nanaa, waliokuwa wamemgeukiwa Danny. Kisha Danny akawageukia na wao. “Samahanini sikutaka kuwaingilia, nilikuwa naingia hapa kufuata juisi, nilipowaona nikaona nisiwapite tu, si uungwana.” “Hichi unachokifanya hapa sasa hivi, ndio sio uungwana.” Akajibu Geb. “Mimi sitaki ugomvi Geb. Ni salama tu. Vipi Fili?” “Nakuonya, si kwa kukutisha Danny, usinijaribu.” “Si kwa ugomvi Geb, nataka kujua hali yake na angalau kumuona sijui mwisho wangu ni upi!  Tafadhali Geb.”

          “Huko ni kunijaribu ambako nakuonya Danny!” “Mimi ni baba yake. Na wewe ni baba Geb, kweli unataka kuniadhibu mpaka kifo changu nisimuone mwanangu!? Najua nimekosa, na ninawaomba msamaha. Tafadhali naomba kumuona mtoto wangu.” “Kama Mungu wangu aishivyo, nakuhakikishia hutamuona Fili, mpaka Fili aje akutafute yeye mwenyewe ambayo sijui ni lini.” “Hivi unajua pesa iliyotumika kumrudisha Fili kuwa mtoto wa kawaida, sababu yako wewe Danny?” Nanaa naye akaongeza.

          “Fili alikuwa kama amechanganyikiwa kwa ajili yako na Sara! Mtoto hakuwa akilala! Tunashukuru Mungu mume wa Grace alimchukua yule mtoto kama wake na kuhangaika naye sana akisaidiana na Geb mpaka Fili akaweza kurudi kuwa kama mtoto wa kawaida, japo umembadili Fili na kumfanya kama bubu! Mtoto ameingiwa hofu ya kuzungumza wakati Fili alikuwa mtoto mzungumzaji, mzuri tu! Umembadili kabisa Fili! Halafu eti sasa hivi unarudi tena na kutaka kuanza machafuko tena!” “Na sitakuruhusu.” Geb akaongeza.

“Nimebadilika.” “Kama kweli umebadilika Danny, anza kwa kumfikiria yule mtoto. Wewe ni baba wa namna gani ambaye unajua kuua tu, hujui kutengeneza!?” Geb akamuuliza akimshangaa kabisa. “Kwanza Fili mwenyewe hataki hata kukuona. Akisikia jina lako yule mtoto anatetemeka mpaka anajikojolea! Imebidi wote tujifunze kutotamka jina Danny, akiwepo Fili! Haya, usiku mtoto alikuwa akiamka anakimbia mpaka nje akimtafuta mama yake, analia asirudishwe ndani akidhani wewe na Sara mpo ndani! Hakubali kuingia ndani mpaka Grace mwenyewe atoke na aamini wewe na Sara hampo ndani!” Nanaa akaongezea kwa mumewe na kuendelea.

“Muulize kaka atakwambia jinsi alivyokuwa akimlilia Geb asirudishwe kwako! Anamlilia Geb mpaka anapiga magoti, anasihi asije akarudishwa kwako na Sara, msije mkamkatakata na kumponda kichwa kama wadogo zake! Eti bila aibu unarudi kumdai na Fili naye! Unawazimu wewe!” Nanaa akawa mkali kabisa.

          “Uuwe watoto wa Grace wawili halafu urudi tena utake kummalizia aliyebaki! Hivi unajua Grace amebarikiwa watoto wengine wawili lakini bado analia msiba wa Fillius na ndugu yake mpaka jana? Umeharibu vibaya sana maisha ya Grace na Fili, halafu eti unarudi unasema nini!? Nahisi huo ugonjwa umeanza kukula ubongo wako, si kawaida. Twendeni Geb.” Nanaa akasimama na kuchukua pochi yake.

          Bila kuzungumza neno Naya naye akasimama na Joshua. “Sitarudia kukuonya tena Danny. Usiwahi hata kutaja jina la Fili, kwangu, Grace, mama, Nanaa na watoto wangu. Sikutishi, lakini jua sikutanii. Na kukuthibitishia hili, kwa kuwa umenianza, utapokea mashitaka yangu kutoka kwa mwanasheria wangu.” “Hapana Geb. Tafadhali naomba yaishe. Sikutaka...” “Twende Nanaa.” “Samahanini sana jamani! Tafadhali naomba tusifike mbali. Naahidi sitorudia tena.” “Na nitahakikisha hilo hutakaa ukasahau mpaka kifo chako.” Geb akamuhakikishia. Akabeba samaki na hizo ndizi vilivyokuwa vimefungwa vizuri kwenye boksi, wakaondoka pale. Geb akapitiliza kwenda kulipia. Hakutaka kumsubiria muhudumu ndipo amlipe pale, wakamsubiria wote hiyo sehemu ya kulipia, ndipo wakatoka nje kwa pamoja wala Joshua na Naya hawakuwa wamemaliza chakula chao.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mambo Juu Ya Mambo. Ni nini kitaendelea?

Endelea kufuatilia.

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment