Ule
ushauri wa Joshua kumwambia baba Naya kuweka Location, On,
kulimsaidia kwa urahisi sana James kufuatilia akaweza kujua ile simu ilipo.
Walifika kwenye huo mji wa Tunduma ikiwa mapema tu. Sehemu ilipoonekana bado
ipo simu ya baba Naya, walipofuatilia ikawa kwenye ileile hoteli, lakini chini
ya kitanda. Wakajua ilianguka wakati wa purukushani za kumchukua.
Muhudumu
aliyekuwa zamu siku hiyo na yeye alijeruhiwa vibaya sana, akawa yupo amelazwa
hospitalini. Wale askari wakasema nilazima kwenda kuzungumza naye. Wakaongozana
mpaka hospitalini alipolazwa, akasema alivamiwa na watu waliokuwa wameficha
sura zao kwa kujifunika kwa kuvaa soksi. Wakampiga mpaka akapoteza fahamu.
Hajui kilichoendelea. Yule mtu wa usalama akamuamini. Akawaambia kina Geb
waende moja kwa moja kwa huyo Mbabe bila kupoteza muda.
Wakakubaliana
kwenda kuzungumza naye ana kwa ana. Wakatoka hapo mpaka kwenye maduka yake.
Wakamkosa, wakataka apigiwe simu na kuambiwa ni lazima afike kituo cha polisi,
anasubiriwa. Wakaelekea kituo cha polisi. Geb na Joshua wakaambiwa wasubirie
ndani ya gari, wale askari ndio wakashuka kwenda kuzungumza na askari wenzao
ambao ndio wenye mji.
Baada ya
mazungumzo marefu, wakiwahakikishia wao hawataki kesi ila watu wao tu ndipo
Mbabe akapigiwa simu sasa na mkuu wa kituo. Akafika hapo bila kuchelewa. Lakini
yeye alikataa kabisa kuwa hausiki na utekwaji nyara wa baba Naya, na wala
hajawahi kumsikia Bale. Ndio mara yake ya kwanza kumsikia hapo. Wale askari
waliokuja na kina Joshua, wakasisitiza kusema kuwa hawataki kesi wanachotaka ni
watu hao wawili. Hata kwa kutaja tu sehemu walipo, wao wataendelea kuanzia
hapo. Mbabe akakataa kabisa.
“Labda
niwaambie wote.” Akiwaangalia mpaka wale askari pale. “Watu wanaotafutwa,
wanatafutwa na watu wakubwa sana hapa nchini. Mimi si askari, ni mtu wa Usalama,
nimepewa amri kutoka juu, kuja kuulizia habari zao maana mara ya mwisho huyu
mzee, ametuma kwa familia yake hizi picha na namba.” Akawaonyesha. “Huu ni
uthibitisho kuwa, mji wenu umemshikilia si mtu mjinga, mtu mkubwa sana na
mwenye akili ya kutosha. Asingetoa kwa familia yake habari kama hizi
zinazoonekana si muhimu, lakini kumbe zina uzito mkubwa sana na zinazooonyesha
ametekwa hapa.” Akaanza kuwatisha. “Usalama umeweza kuifuatilia simu yake,
mpaka kuweza kuipata chini ya uvungu wa chumba cha hoteli.” Wale askari wenyeji
wakaangaliana.
“Hiyo
taarifa imeshafikishwa makao makuu uthibitisho kuwa ni kweli alikuwa kwenye
hiyo hoteli na picha nyingi tu zimepigwa kuanzia pale tulipoikuta simu yake,
mpaka jinsi ilivyokuwa. Wazi inaonyesha iliruka katika purukushani za
kuchukuliwa kwa nguvu kama binti yake alivyoeleza alichosikia, wakati alipokuwa
na baba yake kwenye simu akitekwa. Yule binti amehojiwa na maelezo yake
yamehifadhiwa kwenye kabrasha kule Usalama na mimi nikapewa kusoma kabla sijaja
huku.” Gamba akaendelea kwa vitisho.
“Mbaya
zaidi, muhudumu wa pale naye alijeruhiwa. Yupo hospitalini. Japokuwa hakuwa na
maelezo ya nini kilitokea, na kitabu cha wageni alichoandikisha huyu mzee
hakipo pale, lakini zipo picha za kitabu alichosaini huyu mzee aliyetekwa. Hizi
hapa.” Akaowaonyesha. “Usiku wa jana alipiga picha na kutumia familia yake, na
huyu muhudumu aliyejeruhiwa, amekiri ni kweli huyu mzee alikuwepo pale usiku.
Yeye ndiye aliyempokea na kumkabidhi funguo za chumba. Ni nini nataka kusema!”
Gamba akawatizama wote kwa zamu. Akaona ni kama wameingiwa hofu.
“Iwe
bwana Mbabe unahusika au la, jua jina lako lipo makao makuu ya usalama wa taifa
kwa kuwa huyu mzee alikuja kukutafuta wewe, Mbabe. Ujue uchunguzi wa kina juu
yako, kile unachokifanya, familia yako na wanao kuzunguka vitaanza kufanyiwa
uchunguzi kwa kina. Hakuna jiwe ambalo halitapinduliwa kwenye huu mji
mpaka huyu mzee apatikanike, ndipo lije sasa swala la kijana wake. Huyo kijana
wake ametoroka tu nyumbani, lakini ni mtoto wa wenye nazo. Walioshika hii nchi.
Mpaka sasa mimi nimeandika na kutuma ripoti pale nilipofikia. Natoa siku mbili
mbele. Kama sitapata ushirikiano wowote ule, nitaondoka kwa amani kabisa. Ila
natoa angalizo.” Wote kimya.
“Hatujui
nani atatumwa baada ya sisi kuondoka na kupeleka ripoti kwamba tumeshindwa hata
kupata ushirikiano wa polisi wa hapa.” “Mbona mimi ndio nimekuitia
Mbabe!?” Mkuu wa kituo akajihami. “Kumuita si kutatua tatizo. Hakuna
atakayetaka kujua hatua za kumtafuta huyu mzee ila matokeo ndio wanayotarajia.
Na kwa bahati mbaya sana, habari zenu zipo na nasikitika kuwaambia si
nzuri. Watu wanayajua mahusiano yenu na Mbabe.” Wakaangaliana.
“Huyu ni
raia kama raia wengine na kwa kuwa ni mfanyabiashara mkubwa hapa, anasaidia
jamii kwa kila hali, ndio maana pengine watu wanaona anapewa upendeleo! Lakini
si vinginevyo.” Mkuu wa kituo akatetea. “Nasikitika kukuarifu sicho
kilichofikishwa mbele ya chombo cha usalama. Habari za hapa zipo mbali sana.”
“Lakini hawawezi kusikiliza majungu! Watu ni wanafiki na wambea sana. Wanaweza
kuzungumza chochote kwa wivu tu.” “Na hilo nina uhakika kwa asilimia kubwa sana
kuwa litazingatiwa kwenye uchunguzu utakao fuata baada ya hapa.
Itajulikana kama ni uongo au la. Kwa uzito wa hili jambo lilivyo.
Nawahakikishia ukweli utajulikana bila shida tena kwa haraka
sana. Msiwe na wasiwasi, wanataka kuhakikisha huu mji ndio utakuwa mfano kwenye
hii nchi, kukomesha unyanyasaji kwa raia, magendo, ubadhilifu wa mali za uma na
kuweka sawa chombo cha usalama. Si mnajua sasa hivi wanaotaka madaraka lazima
kujionyesha wanawajibika! Sasa jiwekeni sawa, ili fagio linapopita kusafisha,
wenye uchu wa madaraka kujipatia sifa, nyinyi msiwe wahanga.” Gamba akaendelea
kwa kujiamini zaidi maana walionekana ni kweli wametishika. {Na
kilikuwa kipindi cha utawala wa awamu ya 5 nchini. Kuwajibika kwa kila
kiongozi.}
“Kama
nilivyotangulia kusema, hatuwezi kuondoka kesho, tutaonekana hatujasaka
vyakutosha. Maana masikio na macho ya wakubwa yapo huku kwenye huu mji
wenu sasa hivi, wakisubiria matokea. Wanafuatilia ripoti kila baada ya muda,
wanataka ripoti kujua tulipofikia. Sasa sisi tunafunga siku ya kazi. Mahojiano
ya muhudumu na ukiri kuwa huyu mzee alikuwa pale kwenye ile nyumba ya kulala
wageni, tumeshatuma. Wote wamejiridhisha kuwa mzee ametekwa nyara akiwa kwenye
chumba alicholipia, tena alikuwa akiomba na binti yake. Sasa sisi tutakuwa
hotelini na siku ya kesho pia bado tutakuwa hapa. Kama mtapata fununu yeyote,
maana tunaamini nyinyi ni wenyeji hapa. Mkifanikiwa, msichelewe kutufikishia
taarifa zozote zitakazosaidia kupatikana kwa huyo mzee kwa haraka.” Gamba
akaongeza kitisho.
“Mkishindwa,
basi. Sisi tutaondoka na taarifa tulizokusanya tayari, tuwaachie mwenye
nguvu waje kwenye mji wenu. Sasa wao ndio waje wapambane na majambazi wa huu
mji wenu, na hapo ndipo itakuwa kutangazia umma kuwa mmeshindwa kazi. Jioni
njema.” Akasimama. “Na wote sisi tuliokuwepo ndani ya hiki chumba, tuombe Mungu
huyu mzee apatikanike akiwa salama. Lasivyo!” Gamba akawatizama mmoja baada ya
mwingine, kisha akatoka akiwa amewatajia mpaka namba ya kesi waliyoifungua kina
Joshua huko Dar, na kuwaambia wafuatilie wenyewe kujiridhisha juu ya hiyo kesi
kuwa inafuatiliwa vilivyo. Yule askari kanzu aliyeongozana naye, Chui, naye
akafuata nyuma. Wakatoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Wakaingia
garini walipokuwa wamewaacha Geb na Joshua. “Aisee umetumia akili sana! Maana
bila hivyo, hakika tungegonga mwamba. Yule jamaa hafikiki!” Chui akaanza
kumsifia Gamba mara baada ya Geb kuondoa gari hapo kituoni. “Halafu ana jeuri,
haogopi kabisa! Anajibu kibabe mbele ya mkuu wa kituo!” Chui akaongeza. “Hata
mimi nililiona hilo ndio maana ikanibidi niikuze hii kesi. Nafikiri anajua wale
askari wote pale wapo upande wake, wanamlinda.” Gamba naye akaafiki. “Ila
wametishika.” Chui akaongeza na kucheka. “Niliwaona.” Gamba akaafiki na Chui
akaendelea. “Mwanzoni walianza kwa kutufukuza kibabe. Gamba alipowabadilikia,
nikaona wamenywea.” Wakaanza kucheka ndipo ikabidi wawasimulie Joshua na Geb
kilichoendelea wakiwa ndani, kituoni.
“Unashauri
nini baada ya hapa?” Joshua akauliza. “Kama nilivyowaambia pale kituoni. Sisi
turudini hotelini. Tutulie kabisa. Kwa hofu waliyoipata, hakika tutampata huyu
mzee wenu. Awe hai au walishamdhuru. Wawe ni wao walimteka au la, tutampata
tu. Tena tutampata kwa wao wenyewe kuhangaika ili usije fanyika upelelezi hapa,
wakagunduliwa maovu yao. Naombeni tutulie kabisa. Najua ni ngumu lakini mjue na
wao wanatuangalia. Tukianza kuchukua hatua za kupaniki tu, tutawaonyesha
hatujui tunachofanya na ndipo wanaweza kumdhuru kabisa mzee ili kufuta
ushahidi.” “Nafikiri sio wazo baya. Au unasemaje Joshua?” Geb akauliza. “Ni
sawa.” Joshua akaafiki akiwa anafikiria.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Walichukua
vyumba katika moja ya hoteli ya hapohapo mjini kabisa, sehemu ya wazi tu.
Wakatulia usiku huo wa kwanza. Asubuhi wakaenda kupata kifungua kinywa pamoja.
Wakakaa hapo mgahawani kwa muda tu wakizungumza hili na lile. Wakaondoka, kila
mtu akarudi chumbani kwake. Mchana tena wakakutana hapohapo. Hapakuwa na fununu
yeyote ile ya baba Naya. Joshua akaanza kupatwa wasiwasi. Zimebaki siku 3 tu,
harusi yao ifungwe. Baba mzaa chema hajulikani alipo wala kaka wa bwana
harusi pia hajulikani alipo.
“Mnafikiri
vile vitisho vitafanya kazi jamani?” Joshua akauliza akisikika ameingiwa na
wasiwasi. “Na wenyewe wanajiuliza swali kama lako. Hata hapa tulipo,
wanatuangalia tu na kutufuatilia kila hatua tunayochukua. Nakuhakikishia, kosa
dogo tu tutakalofanya, watathibitisha kuwa sisi ni hovyo tu. Nakuhakikishia pia
sasa hivi tumewapa tumbo joto. Naomba muwe wavumilivu.” Gamba
mtaalamu wa mikasa kama hiyo akawahakikishia. Joshua anayetakiwa kutoa ripoti
kwa Naya kila wakati ikabidi kutulia tu.
Jioni
wakati wakila tena hapohapo ujumbe ukaingia kwa Geb kutoka kwa askari aliyekuwa
akiwaongoza nyuma ya pazia tokea walipokuwa Dar na kuwapa habari za Mbabe kwa
kina ila kuhofia kuwa kimbembele. ‘Inaonekana mmetingisha mji.
Matumbo joto! Tatizo ni jinsi yakujirudi. Wameingiwa hofu.’ Geb
akasoma na kuuliza. ‘Kuna fununu zozote?’ ‘Nimesikia hapa kituoni wanashindwa jinsi ya
kufikisha ujumbe kwenu.’ Geb akafikiria kwa haraka, akamjibu. ‘Wape wazo
la kuandika alipo na kutupia chini ya mlango wa chumba cha mmoja wetu.’ ‘Acha
nirushie hilo wazo, bado nipo kituoni. Kila mtu anajipanga na kujitetea
wakijiandaa na huo ukaguzi mkuu endapo watu wa usalama wakija kwenye huu mji.
Kila mmoja anasema lake.’ ‘Sisi shida yetu ni watu wetu tu. Wape hilo wazo.
Sisi tutajichelewesha hapa.’ ‘Sawa. Pengine itasaidia.’ Akarudisha
hayo majibu.
Geb
akarudisha simu mfukoni. Akatulia kwa muda. Akaangalia kulia na kushoto.
Kulikuwa na wateja wengine hapo mgahawani. Kwa kuwa alikuwa mgeni pale, hakujua
yupi mteja na yupi yupo pale kuwachunguza. Akatulia kabisa hata Joshua
hakumuonyesha ujumbe kwa haraka. Uzuri ni mkimya. Hakuwa akichangia sana
mazungumzo yaliyokuwa yakiendelea pale. Hata alipotulia hakuna aliyemuhisi kuwa
analo jambo.
Kila
walipotaka kuondoka Geb aliwaomba wabaki kidogo. Baada ya muda Geb akatoa simu
mfukoni ilipoashiria mtetemeko kuwa kuna ujumbe umeingia. ‘Chumba
chako namba ngapi?’ Akasoma huo ujumbe. Kabla hajajibu, ujumbe mwingine
ukaingia. ‘Nina ujumbe wako. Nimewaambia mimi najitoa muhanga kuleta kwenu.
Wamekubali.’ ‘Nashukuru sana. Tumbukiza chini ya mlango, chumba namba,’ Akamtajia.
Kimya. Baada ya muda kama dakika 10 hivi akapata ujumbe mwingine ‘Tayari.’
‘Tutawasiliana. Nashukuru sana.’ ‘Karibu lakini hutanipata tena. Natoa kabisa
hii namba hewani kwa muda.’ Geb hakujibu lakini akapata tumaini.
Akasubiri kama dakika 20 mbeleni ndipo akawaambia wenzie waondoke pale.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Wakaondoka.
Walipoingia tu garini akamkabidhi Joshua simu yake. “Nimepata habari njema ndio
maana nilikuwa nikiwazuia tusiondoke. Sikuwaambia pale kwa kuwa nilijulishwa
kuwa tunafuatiliwa.” Shauku ya kusoma kwa Joshua ikaongezeka.
“Nilijua tu.” “Hakika huu ni ulimwengu wako Gamba! Nimeambiwa kila kitu
ulichobashiri.” Geb akampongeza.
“Haiwezekani!”
Joshua akahamaki baada ya kumaliza kusoma. “Twendeni tukahakikishe kama
nikweli.” Geb akaongeza. Ukimywa mkuu ukatanda humo garini. Roho mkononi
hawajui karatasi walioachiwa imebeba ujumbe gani. Mawazo ya Joshua yakahamia
kwa mchumba aliyemuacha akiwa na matumaini atamrejeshea baba yake. Swali likawa
atakuwa kwenye hali gani! Yu mzima au la! Geb akaendelea kuendesha na yeye
akiwaza.
“Naomba
kila mtu aende chumbani mpaka nitakapo wapigia.” Geb akatoa mungozo wakati
akigesha gari. “Ni kweli. Nivizuri tuendelee kama kawaida ili wasije kumuhisi
huyo jamaa wa Geb, wakajua anawasiliana naye. Kwamba alishamwambia kuwa kuna
ujumbe.” “Ni kweli.” Mpaka hapo Geb hakuwa amewatajia jina la huyo askari wa
hapo. Maana hata kwenda kuwapokea, Geb alifikiria akaona sio sawa, ni kuhatarisha
maisha yake. Kwa hiyo walipotua uwanja wa ndege, Geb akawa amewasiliana tena na
mwenyeji mwingine wanaofahamiana kwenye mambo ya biashara na kuwapatia hilo
gari. Kwa hiyo waliingia kwenye huo mji wakiwa wageni na hata hilo gari
hawakuwa wakilijua.
Geb aliingia
chumbani kwake na kweli akakuta karatasi ndani, kama iliyopitishwa chini ya
mlango. Akaingia ndani, akafunga mlango, ndipo akaiokota. Hapohapo akampigia
Joshua. “Vipi?” “Aisiee ipo. Sijafungua bado, naona uje kwanza ili ufungue
mwenyewe.” “Nashukuru sana GM.” Joshua akatoka chumbani kwake kwa haraka
kwani hakuwa hata amekaa.
Alipoingia
tu, Geb akamkabidhi. Joshua akaipokea na kufungua kwa haraka. Akamuona anasoma
mpaka mikono inatetemeka. Geb akabaki kimya akimtizama tu. “Mungu
wangu saidia.” Akasikika Joshua, macho kwenye huo waraka. Akaenda kukaa kabisa
kitandani kwa Geb, akaendelea kusoma. Ilikuwa ndefu na imechapishwa. “Naya
anaweza kurukwa na akili. Mungu saidia!” Joshua akaongea na
kumkabidhi Geb na yeye asome. “Lazima tuondoke sasa hivi Geb. Tafadhali sana.
Tuanze na baba Naya kwa haraka. Huwezi jua tutaokoa nini! Maadamu tumeshajua
Bale alipo, basi tutajua nini chakufanya naye, baada ya kumpata baba yake.”
Joshua akaongeza wakati Geb naye akisoma.
Geb
akasoma mpaka akamaliza. “Naona ni wazo zuri.” Akaafikiana na wazo la Joshua
baada yakumaliza kusoma. Hata yeye alionekana ameingiwa hofu. Akawapigia simu
wale askari waje na wao. Kama waliokuwa wakisubiri mahali, wakaingia wote kwa
pamoja. Akamkabidhi Gamba. “Naomba uisome kwa sauti.” Geb akamkabidhi Gamba ile
karatasi. Gamba akaanza kuisoma. Ilijawa kujihami kwingi ila huyo mwandishi
alisema ni fununu wamepata kuwa kijana wa huyo mzee alikamatwa akiwa anavusha
mali ya magendo huko mpakani. Mara ya mwisho yeye na vijana wengine wa kitanzania
walikuwa jela ya mpakani mwa Zambia na Mbeya, lakini utaratibu wa kuhamishiwa
jela ya Mbeya ulikuwa ukiendelea. Hakuna anayejua zaidi. Mwandishi alisema
kuhusu mzee wake, kwa kuwa tokea afike hapo kwenye huo mji alianza kwa maswali
na kutisha wenyeji, ndio maana hakuna aliyeweza kumpa hata fununu ila
kuchukuliwa na kutolewa kwenye mji wao. Amesogezwa mji wa karibu na Mbeya
ambako ni kama msaada wakumsogeza kwa kijana wake. Wakaelekezwa sehemu
ziliposikika fununu kuwa alikwenda kuachwa.
“Sasa
sisi huu mji hatuufahamu. Nashauri turudini palepale kituoni. Tuwaambie
kiuungwana kwamba tumepata Msamaria mwema, ametupa sehemu ambayo huyu mzee
anaweza kuwepo. Tuwaonyeshe hii karatasi na tuombe askari anayejua huu mji na
vijiji vyake, zaidi anayejua hii sehemu iliyotajwa hapa, aongozane nasi.” Wote
wakatulia. “Tukifanya haraka kuondoka hapa tukakimbilia sehemu tusiyoijua,
kwanza tutapoteza muda, na kama tuna nafsi ndogo ya kuokoa, tutapoteza kwa
sababu itatubidi turudi tena hapahapa endapo tukikwama huko. Au mnaonaje?” Geb
akamtizama Joshua. “Naona wazo ni zuri. Nawashukuru sana.” Joshua akaafiki na
kushukuru akionekana akili ilishaanza kuwaza kwingine zaidi.
Baada ya
muda mfupi, kila mmoja akawa yupo garini na mizigo yake. Ndio wanaondoka hapo
hotelini moja kwa moja. Geb akakanyaga mafuta kurudi kituoni. Safari hii wote
walishuka wakijua hawana cha kujificha tena. Wanajulikana wapo wanne.
Walipofika kituoni Gamba akawa muungwa. Akashukuru wakazi wa huo mji kwamba
wametoa ushirikiano mzuri, wamewapa huo waraka. Akamkabidhi Mkuu wa kituo
ambaye chakushangaza bado mida hiyo alikuwepo tu kituoni na askari wengine
wengi tu kama waliokuwa wameitana. Na walipoingia hapo kituoni wakasababisha
ukimya wa hali ya juu. Ila kwa kadiri Gamba alivyokuwa akizungumza nao,
wakaanza kutulia.
Chakushangaza
na ambacho hawakutegemea, askari watatu wa pale kituoni wakakubali kuongozana
nao ili kusaidia, tena kwa usafiri wao wenyewe, wasitumie gari waliokuja nao
kina Geb. “Ili msipate shida ya kuridi tena huku.” Kama waliokuwa wakiwafukuza kwenye
mji wao. “Hata hapo mtakuwa mmetusaidia sana. Na sisi hatutawasahau. Huo wema
wenu utakumbukwa hata kwa Wakubwa. Ila kabla hatujaondoka, nitachukua majina
kamili na namba za utambulisho wa hao maaskari, na kuziripoti juu.” Gafla
pakazuka ukimya tena.
Ila kwa
Geb na Joshua wakapenda hilo wazo la Gamba isijekuwa ni njama ya kuwatoa hapo
na kuja kuwageuka mbeleni. “Ni kwa usalama wao pia. Sisi tunajulikana kama tupo
hapa. Huu waraka umeshatumwa kwa viongozi. Hiki mnachotaka kutusaidia, ni
kujitoa kwa hali ya juu. Sasa lazima ijulikane ni nani yupo safari moja na sisi
kwa chochote kitakachotokea.” “Basi tunaomba mtupishe, tujipange.” “Sawa Mkuu.
Sisi tutakuwa garini tukiwasubiria.” Gamba akakubali bila shida na kuwaambia
wenzie watoke.
Naya.
Simu kutoka
kwa Naya ikaanza kuita. Joshua akafikiria ndipo akapokea. “Vipi?”
“Naomba nivumilie Joshua. Nahisi nimejawa tu wasiwasi. Nikizungumza na wewe
angalau napata utulivu.” “Naelewa kabisa. Tuendelee kuomba Mungu, kila kitu
huku kinaendelea vizuri. Nipe masaa machache tena, pengine naweza kukueleza
kinachoendelea kwa hakika.” “Mpaka sasa hamjasikia chochote?” “Wamejawa
tu hofu. Na watu wenye hofu wanaweza kuzungumza chochote kile kujitetea. Sasa
kusikia ni jambo moja, ila kutendea kazi tulichosikia na kufanikiwa, nafikiri
hiyo ndio habari. Naomba ongeza subira tena kidogo. Sisi tupo macho mpaka sasa,
tukimtafuta baba na Bale. Tuamini tu.” Joshua akawa makini
na kila taarifa anayompa Naya.
“Nawashukuru
sana Joshua. Asante. Na namsihi Mungu pia anirudishie wewe salama. Naona
Geb bado anaendelea na mipango ya harusi kama kawaida. Nanaa ameniambia Geb
amesema chochote kisibadilike.” “Naona ameamua kuniweka mimi pembeni. Katika
hilo hanihusishi kabisa. Tuache tuone mambo yanavyokwenda. Tusiwakatishe tamaa.
Amini siku ya harusi, sisi tutafunga ndoa.” “Na baba atakuwepo, pengine na Bale
kama hatakuwa ametuziria.”
“Iwe kama
unavyonena. Naomba nikuache mpenzi. Kuna sehemu tunakwenda.” “Nakuombea.”
“Sawa. Lakini naomba ulale, usisubiri.” “Siwezi Joshua. Mpaka na wewe ukiwa
kitandani ndio nitajua hiyo siku tumeimaliza pamoja. Usiwe na wasiwasi.
Sijachoka. Nipo tu hapa nyumbani. Na kesho ndio mambo ya saluni yanaanza. Mama
G atakuja kunichukua, mida ya saa tano asubuhi. Kwa hiyo nipo sawa, hata nikichelewa
kulala, nitachelewa kuamka. Usiache kunipigia. Ujue nakusubiria.” “Sawa.” Joshua
akakata simu na kuingia garini wenzake walipokuwa wamekaa wakiwasubiria hao
askari wenyeji.
Ikiwa Zimebaki Siku 3.
Zikiwa
zimebaki siku tatu ndoa ya Naya na Joshua ifungwe, bado bwana harusi alikuwa
Tunduma akimtafuta mkwewe, bibi harusi simu mkononi akisubiri taarifa za baba
yake na akimfuatilia mchumba akiomba Mungu amrudishie salama. Wasimamizi wa
harusi, kina Magesa, waliendelea na maandalizi ya harusi kama kawaida. Kwa kuwa
walishakubaliana ndoa lazima ifungwe tu, ila aina ya sherehe ndio itategemea.
Na kwa kuwa kina Magesa walishapata maelekezo kutoka kwa baba Naya kwamba
harusi isisimame, basi wao wakaendelea kama kawaida.
Baada ya
lisaa magari mawili yalikuwa yakiacha mji wa Tunduma kuelekea ambako waliambiwa
baba Naya anaweza kuwepo. Geb alikuwa makini kulifuata hilo gari la polisi kwa
nyuma. Geb na Joshua wao kimya, ila Gamba na Chui ndio waliendelea kuongea hili
na lile mpaka mwisho na wenyewe wakaishiwa maneno. Wakaanza kusinzia, bado
safari ilikuwa ikiendelea, tena kwa mwendo kasi bila kusimama wala kupunguza
mwendao. Naye Geb hakutaka kuwapoteza, alihakikisha anaendesha kwa mwendo wao.
“Nahisi
tunarudi Mbeya.” Geb akamwambia Joshua ambae alikuwa kimya tu pembeni yake.
Joshua akamgeukia. “Nimehisi kutokana na upande tunaoelekea.” “Sikuwa
nimezingatia kabisa! Mawazo yapo mbali.” “Naamini kila kitu kitakwenda sawa.
Acha tufuate tuone na wao watatufikisha wapi.” Geb akajaribu kama kumtuliza.
Kimya kingine kikaendelea.
Kwa Naya.
Mkakati wa Kukomboa
familia kabla ya harusi, unaendelea. Akamuona anatoa
simu. Akajua anampigia Naya. “Joshua!”
“Hujalala tu!?” Joshua akashangaa jinsi
alivyopokea simu kwa haraka. “Siwezi. Nimekwambia
mpaka wewe ukiwa kitandani unalala na mimi ndio nitahitimisha siku.” “Sasa
unafanya nini?” “Nilikuwa naweka sawa mahesabu ya dukani kwa baba. Napitia bei
zake. Mauzo kwa kila kipimo. Kwa kifupi kuelewa kwa undani hii biashara. Zayoni
ataanza shule baada ya muda mfupi. Sitaki kujikuta...” Akamsikia amesita anaanza kulia.
“Naomba
usilie Naya.” “Naogopa Joshua. Naogopa sana. Iweje msimpate baba yangu? Au
mumpate akiwa amekufa!” “Pole mpenzi wangu. Tuendelee kumuamini Mungu.” “Mungu
hapotezi Joshua! Lakini sisi ndio tutapoteza. Pengo la baba haliwezi
kuzibika kwetu kama la mama. Maisha yanaendelea, lakini pengo lake mpaka leo
halijawahi kuzibika. Naogopa sana.” “Pole Naya. Ila
sikutaka kukupa matumaini ambayo sina uhakika nayo. Lakini kuna fununu anaweza
kuwa kwenye mji fulani hivi. Mpakani mwa Tunduma na Mbeya. Ndiko huko
tunaelekea sasa hivi.” “Joshua!” Naya akahamaki. Ndipo
Joshua akamuelezea kila kitu.
“Nimepiga
picha hii barua. Sikutaka kukutumia kwa haraka. Na nimepiga picha hiyo gari
inayotupeleka huko. Sasa hivi tupo njiani, wao wanatuongoza. Majina ya askari
wawili miongoni mwa hao wanne waliopo kwenye gari pia nimeandika. Sikutaka
kukutumia kwa haraka. Ila acha nikutumie kama tulivyofanya kwa mzee, ikawa
rahisi kutusogeza.” “Nina wazo.” Naya akaanza
akisikika kusita kidogo.
“Ni nini?” Joshua
akauliza. “Unakumbuka nilikueleza habari juu ya kaka Mati? Yule mwanasheria
aliyenisaidia kumtafuta Malon!” Joshua akatulia. Naya
akaendelea. “Nilikuwa sijui ni wapi au jela ipi Malo alifungwa. Ila tu
mji. Kaka Mati akaenda kupeleleza mpaka akajua alifungwa wapi. Ilinigarimu,
lakini alisaidia sana mpaka akamtoa na jela. Nashauri kama huna mtu
unayemfikiria kwa haraka, basi tumtumie yeye. Anaonekana anao uzoefu na analeta
matokea yakueleweka.” Joshua akatulia kama anayefikiria.
“Naomba
usiwe na wasiwasi. Ni mtumzima na anajiheshimu.” “Ni sawa. Sio wazo baya.” Joshua
akaweka kituo akisikika kama kuna kitu angeweza kuongeza zaidi, lakini akasita
kukisema. Wakatulia kwa muda. “Joshua?” “Nipo.” “Nashukuru
sana mpenzi wangu na poleni. Mungu azidi kukubariki. Mfikishie Geb shukurani
zangu za dhati. Najua ameacha familia yake huku na majukumu yake sasa hivi yuko
huko maporini! Hakika Mungu amlipe zaidi na zaidi mpaka ajue amebarikiwa.”
“Amina. Atasikia.” Geb akajua ametumiwa salamu tena.
“Na taarifa
pia za hilo gari mnalotumia sasa hivi hujanipa Joshua.” “Kweli. Acha basi
nikutumie hizi nilizonazo kwanza, kisha nimuulizie Geb. Sijachukua namba za
hili gari.” “Nawaombea.” “Amina. Ila hicho unachofanya ni sahihi kabisa.
Hamisha hayo mawazo ya hofu, weka kwenye kitu cha msingi. Ili uwe ushuhuda wako
siku moja. Huu usiku shetani alitaka autumie kwa hila, ila iwe kwa manufaa
kwako. Usipoteze kabisa.” “Sawa. Usiache kuwasiliana kila wakati.” Joshua
akacheka na kuafiki.
Aluta Kontinua.
Baada
ya mwendo mrefu wakutosha, giza nene maana walikuwa wakipita msituni wala si
kwenye barabara kubwa yenye lami, ndipo wakafika kwenye kijiji. Waliweza
kutambua mashamba na nyumba chache tu, kwa sababu ilikuwa usiku na hakuna taa.
Simu ya Gamba ikaanza kuita. Akapokea kwa haraka. “Mliahidi
hakuna kesi wala mjadala. Tumewasaidia na kuwafikisha mpaka hapa.
Inavyosadikika mzee wenu ameachwa kwenye kituo kidogo cha magari ya abiria,
yatokayo hapa kijijini. Mkifuata hii barabara kwa mwendo mfupi kidogo tu,
mtaona kituo chenyewe. Kwa hali yeyote mtakayomkuta nayo huyo mzee, sisi
hatuhusiki kabisa. Tumewasaidia kusaka habari zake mpaka kuwafikisha hapa.
Kitakachoendelea baada ya hapa, sisi hatuhusiki. Tunaomba amani kwenye mji
wetu.” Simu ikakatwa.
Wakati
Gamba anawaambia juu ya hiyo simu, wakashangaa hiyo gari inakata kona. Geb kwa
haraka akataka kuifuata lakini Gamba akamkataza. “Hao wanarudi Tunduma.
Ameniambia sisi twende moja kwa moja mpaka tukute kituo kidogo tu cha mabasi.”
Akamalizia kuwaambia ujumbe aliopewa kwa simu muda mfupi uliopita. “Maisha
yameharibika sana. Watu tunaotegemea walinde raia ndio wanahusika kwenye
kuwaangamiza!” Akalalamika Joshua. “Maana hawa waliotuleta mpaka hapa, inamaana
mmoja wao au wawili wao wanahusika kumteka baba Naya. Kwa asilimia zote bila
kupinga.” Akaongeza Geb.
“Lakini
tuliwaahidi jamani! Naomba tusiwageuke. Haya mambo yapo halafu kuna leo na
kesho, tunaweza kukutana nao mahali, tukahitaji msaada wao. Ni bora wao ndio
wabakie tunao wadai, ili kuweka mazingira yakuja kuwatumia tena wakati
mwingine, kuliko kutengeneza uadui.” Geb na Joshua wakanyamaza, wazi walitamani
haki itendeke. Waadhibiwe waliofanya huo uovu. Lakini wakajirudi kwa hofu.
Kwanza
wakakumbuka wapo na askari kama hao wa Tunduma hapo garini. Wale askari hata
kama iweje, wale ni wenzao tu. Pili hawakuwa wakijua kama kweli watamkuta huyo
baba Naya! Wasije haribu, wakati hata baba Naya mwenyewe hawajampata. Kingine
wanamlaumu nani? Bale si mtoto mdogo. Kwa hiyari yake, tokea anatoka kwa Malon
huko Mbeya, alitahadharishwa madhara ya biashara atakayokwenda kufanya, lakini
akakubali kwenda kufanya. Hata kama ni kwa kurubuniwa kwa ahadi za uongo, lakini
alikubali kwenda. Wakawa wapole, Geb akiendelea kukanyaga mafuta. Safari hii
kila mtu macho nje kuangalia kama wataona hicho kituo.
Baada ya
kama dakika kumi hivi, wakipita kwenye barabara mbaya haswa, mashimo na vumbi
jingi tu, ndipo wakaona eneo linalofanana kama kituo cha mabasi. Giza nene,
hakuna hata taa. Geb akasogeza gari kabisa mpaka karibu kabisa na
hicho kituo. Kulikuwa na vibasi vidogo na pickup za mizigo, chache,
zimeegeshwa. Wote wakatoka garini. Kila mmoja akawasha simu na kuanza kuzunguka
huko na kule pengine watamuona baba Naya.
Mapigo ya
moyo yakienda kasi kwa hofu. “Anatumia jina gani?” Gamba akauliza ili kuweza
kumuita kwa sauti. “Sidhani hata kama yeye mwenyewe anakumbuka jina lake ila baba
Naya. Kila mahali, kila mtu anamuita baba Naya, na yeye mwenyewe
anajitambua hivyo.” Joshua akaongeza wakiendelea kumsaka wakitumia mwanga wa
simu zao.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kazi ya kumsaka baba Naya inaendelea huku wakiwa hawana hakika alipo
Bale, ila fununu tu. Je, yaliyoandikwa kwenye waraka waliokuta chini ya mlango,
chumbani kwa Geb, ni ya kweli au wametolewa tu mjini Tunduma?
Itaendelea........
0 Comments:
Post a Comment