Geb
akarudi garini ili kusogeza gari karibu zaidi kumulika vibandani, waweze
kutumia mwanga wa gari huku wale polisi wakimuita baba Naya. Joshua akaingia
kwenye moja ya kibanda. Akamkuta amelala chini kabisa. “YUKO HAPA.” Akapiga
kelele kwa sauti, Gamba akawa wakwanza kufika. Akamwangalia na kumshika. “Ni wa
moto kabisa, na anamapigo ya moyo. Yupo hai.” Geb akasogeza gari. Baba
Naya alikuwa akinuka sana mikojo, kama aliyejikojolea.
Gamba
akaanza kumtingisha akimuita. “Nashauri tutokeni hapa, tukatafute hata
dispensary, aweze kupewa huduma ya kwanza.” Joshua akatoa hilo wazo baada ya
kuitwa mara kadhaa asiitike. Wakatoka hapo, hawajui waendako wala walipo. Ila
Geb akasema alielewa upande waliokuwa wakipelekwa mpaka kufika hapo, na upande
upi ni Mbeya kutokana na alivyoendesha tokea wanashuka uwanja
wa ndege mpaka Tunduma. Wakamuacha aendeshe kwa vile anavyojua. Kila
mtu kimya.
Joshua
akakumbuka kumpigia simu Naya kumpa habari njema. Akampigia. “Tupo na
Mzee hapa.” Naya akaanza kulia. “Nipe nizungumze naye.” “Hajazungumza
chochote. Hapa yupo dirishani, tumemfungulia dirisha ili apate hewa. Tunatafuta
hospitali.” “Amefungua hata macho?” Naya akauliza
akijaribu kutulia. “Kulikuwa giza sana. Hiki kijiji chenyewe ni giza, hakuna hata
umeme! Hatuonani.” “Cha kwanza baba hajala. Alikuwa amefunga. Na nina uhakika
huko alipokuwa amefungwa, hawajampa chakula. Inawezekana amechoshwa na njaa
pia, japo hatujui ni mazingira ya namna gani alikuwepo. Naomba muweke simu
sikioni. Tafadhali Joshua.” “Haongei Naya.” “Wewe weka
tu simu sikioni kwake na uongeze sauti.” Joshua akafanya kama
alivyoomba Naya.
“Ongea
Naya.” “Huyo ndio Naya wa baba Naya?” Akauliza Chui. “Ndiye
huyo.” “Baba!” Naya akanza kuita. “Baba Naya?” Naya
akaita tena akijaribu kutulia kutoa sauti ya kilio. “Pole baba
yangu, pole sana. Una maumivu kokote?” “Nimehisi kama
ametingishika!” Gamba aliyekuwa amekaa pembeni yake, akahamaki. “Joshua, washa
taa ya juu ili tumuone.” Geb akatoa wazo.
Wakawasha. “Haya,
Naya, muulize tena.” Joshua akamwambia Naya. “Baba! Baba Naya?
Unanisikia?” Naya akarudia. Akatingisha kichwa kukubali. “Ameitika.” Wote
walikuwa wakimwangalia yeye kasoro Geb aliyekuwa akiendesha. “Muulize
tena kama yupo na maumivu.” Joshua akataka Naya ndio aulize huku
akimwangalia baba Naya, lakini akatingisha kichwa kabla Naya hajamuuliza. Hapo
Joshua akaridhika. “Pole mzee wangu.” “Asante. Asanteni.” Akaongea kwa sauti ya
chini lakini wakasikia. “Maumivu yapo wapi?” Joshua akauliza. “Nyuma ya kichwa.
Nahisi walinipiga hapo kwa nguvu. Ila njaa ndio inanisumbua. Sijala kwa siku
nyingi.” “Pole baba.” Naya akawa amesikia.
“Nina
wazo.” Akasikika Gamba. “Tutafuteni nyumba yeyote ile, tuombeni chai ya rangi.
Mzee haonekaniki kama ni mgonjwa wa kukimbiza hospitalini kwa haraka ila
anahitaji chakula. Tunaweza kukimbilia hospitalini, tukajikuta tunawekwa hapo
kwa muda mrefu halafu na bado tusipate msaada kwa haraka. Ila mzee akipata chai
ya rangi, akaja kupata chakula, ndipo akapelekwa hospitalini kwa uchunguzi,
hata wakituweka hapo kwa muda mrefu, haitakuwa shida.” “Wazo zuri.” Joshua na
Geb wakajikuta wamekubaliana kwa pamoja.
Walishatoka
kwenye kile kijiji walichompata baba Naya, wakaona wasirudi nyuma waendelee
mbele. Bado Naya alikuwa kwenye simu. “Joshua?” “Nakusikia Naya.”
“Nawashukuru sana. Naomba waambie wote nawashukuru halafu muwekee simu tena
baba.” “Jamani! Naya anawashukuruni sana.” “Karibu Naya wa baba Naya.” Chui
akaitika yeye wakwanza nakufanya wengine wacheke kidogo. “Naweka
simu sikioni kwa baba, japo amechoka sana.” “Naongea naye kidogo tu, na Zayoni
anataka kumsalimia halafu tutamuacha apumzike mpaka ale.” “Haya, naweka simu
masikioni kwake.” “Baba? Nimefurahi sana. Nilikuwa nakuombea.” “Asante
mama.” “Na mimi baba, ila mimi nilikuwa naogopa. Nilijua hutarudi tena.
Unaumwa?” “Kidogo tu. Njaa zaidi.” “Joshua atakupa chakula.
Pole baba.” Zayoni akafanya mle garini wacheke. “Asante
Zayoni.” Akaitika baba yao. “Usilie Zayoni. Tutamtafutia
chakula, atakula. Tukiona asubuhi yupo salama, tutarudi naye wakamwangalie hali
yake hukohuko Dar hospitalini.” “Yesss!” Wakamsikia
Naya akichangilia pembeni. “Na mimi nilikuwa nikifikiria hivyohivyo. Endapo
atakula nakujisikia vizuri, tuondokeni. Matibabu yakaendelee kwenye hospitali
tunazozijua.” Geb akaongeza. Wakakubaliana hivyo, ndipo kukaanza kazi ya
kusakwa nyumba yeyote ile waingie na kuomba msaada.
Geb
aliendesha kama baada ya lisaa ndipo wakaona tena kijiji kingine, lakini kila
mtu alimpongeza kwa uwezo wakuweza kuwatoa maporini na kuwafikisha barabara
kubwa ya lami. Na hilo eneo lilionekana ni kama kijiji chenye maendeleo kwani
kulikuwa hata na umeme. Geb akasogea mpaka kwenye nyumba ambayo ilikuwa karibu
kabisa na barabara. “Nashauri sisi ndio tukagonge.” Akashauri Chui. Akimaanisha
wao askari. Wakakubaliana, wao wawili wakashuka.
“Nasikia
baridi sana.” Wakamsikia baba Naya akiongea kwa sauti ya chini. “Nafikiri nina
koti zito kwenye begi langu. Joshua akashuka kwa haraka. Akashangaa na Geb
anashuka. “Ukimpa mzee koti, tuzungumze kidogo.” “Sawa.” Akalipata koti lake
kwa urahisi tu ndani ya begi lake, nyuma ya gari. Akaenda kumvalisha,
wakapandisha kidogo kioo, ndipo wakajitenga ili wazungumze wakati kina Gamba na
wenzie wakigonga kuomba msaada.
“Nimefikiria.
Kwa kuwa ni kama tumepata fununu za Bale, nashauri huyu askari kanzu, Chui,
tumuombe yeye arudi huko mpakani kunakosemekana anaweza akawa amefungwa huko
Bale. Wakusanye taarifa zozote zile juu yake ndipo tujue nini chakufanya
kuanzia hapo.” “Wazo zuri, lakini naomba zungumza na Gamba, kama anaweza
kuongozana naye. Anaonekana anao uelewa mkubwa sana wa haya mambo.” “Sidhani
kama itawezekana, kwakuwa ni kama Gamba ametingwa na majukumu mengi mno. Hapa
yupo kwa kulipa fadhila tu. Ila aliniambia wazi yupo na majukumu mengi sana.
Isingekuwa ni mimi, hiki sio kipindi angesafiri, kuwepo nje ya ofisi.” Geb
akafikiria kwa haraka.
“Naweza
kumuomba amsimamie Chui kwa simu bila yeye kuwepo huko. Awe ni mtu ambaye
anamuongoza kwa karibu na awe anaripoti kweke kwa simu.” “Sio wazo
baya. Ila Geb, nakushukuru sana. Asante sana.” “Tupo pamoja na ndio
mambo ya familia yalivyo. Mimi nimeshazoea kwa sababu nimekuwa nikizungukwa na
familia wakati wote. Inachukua muda sana kuiweka familia pamoja, ila nikwambie
kabisa, ndio maana nzima ya maisha. Baada ya hili, utakuja kuniambia, hawawezi
kukutizama kama Joshua anayeoa kwao. Ila Joshua wanayemtegemea kwa karibu sana.
Hakuna litakaloendelea kwenye familia yao bila baraka zako. Si kwa pesa, ila
kwa umbali uliokwenda kwa ajili yao. Na ndivyo Mungu anavyofanya. Hakupi
kitu kikubwa kabla hajakujaribisha na kuona kama unao uwezo wa
kukimiliki.” “Yaani na mimi nilifikiri hivyohivyo aisee! Ila kwangu huyu Mungu
amezidisha jamani!” Geb akacheka.
“Kweli
Geb! Mimi mpaka huwa namwambia, ni kwa nini anapenda kunijaribu katika kila
hatua au ngazi anayonipandisha? Mbona ni kama nishamuonyesha kuwa nina uwezo!!”
“Njia zake si zetu. Na mimi huwa ananijaribu hivyohivyo, namwambiaga Nanaa
kabisa. Hili ni jaribu langu kwa sababu nimemuomba Mungu kitu.
Nilishamjua. Huwa ananipitishaga sehemu mpaka huwa nabaki kucheka tu, na kwa
kuwa najua ni yeye, huwa namuomba hekima na uwezo.” Wakasikia
mwenyeji mwanaume akizungumza na kina Gamba. Wakasogea na wao. Wakakaribishwa
ndani, na mkewe naye akaamka.
Uzuri
walikuwa na jiko la mafuta ya taa. Mama huyo akaliwasha kwa haraka. Geb na
Joshua wakaenda kumchukua baba Naya. Wakamuweka kitini na kumfunika. “Samahani
kwa usumbufu aisee.” “Msijali kabisa.” “Baada ya chai, kama tungeweza kupata na
maji moto ili kumsafisha kidogo, ingekuwa msaada sana.” “Bila shida.” Akaitika
mkewe huko jikoni. Wakakaa hapo sebuleni. Sebule yenyewe ilikuwa ya kawaida
sana, lakini ikaongezwa umaana na ule ukarimu wao. Geb na Gamba wakaanza
kuzungumza. Wakaweka mipango hapo. Chui akakubali kwa haraka sana. Akajua kwake
ni kuongeza pesa. Lakini wawili hao wakakubaliana wajipe siku mbili mbeleni
ndipo warudi Dar pamoja. Wakamwambia Geb walishazoea kufanya kazi pamoja na
wakati wote wakiwa pamoja hufanya kazi kwa haraka. Hilo likamfurahisha Joshua
zaidi ambaye aliamini zaidi akili ya Gamba. Ndipo wakamgeukia mwenyeji wao
kuulizi magari yaendayo mpakani. Mpaka baba Naya anawekewa chai, mipango ya
kuanza kumsaka Bale ilishakuwa imekamilika.
Joshua
akamsogelea. “Nikusaidie kukunywesha?” Baba Naya akafungua macho. “Asante,
lakini nafikiri nitaweza tu. Acha nijaribu.” Joshua akamsogezea ile chai
karibu. Akaanza kunywa taratibu tu. Alipomaliza Joshua akamuuliza.
“Unajisikiaje?” “Maumivu tu hapo kichwani na huu mkono. Walinipiga ule usiku
walionichukua wakitaka kunitoa taarifa kama kunitisha tu. Hakikuwa kipigo
kibaya sana. Ila nahisi huu mkono, zaidi bega ndio limedhurika na hapo
kichwani.” “Pole sana.” “Ila nashukuru sana. Nahisi mmewahi kuniokoa. Lasivyo
wangenidhuru zaidi kama kupoteza ushahidi.” Wote wakasogea karibu kusikiliza.
“Sina
mengi sana yakueleza maana walinifungia sehemu ambayo ilikuwa giza. Sikujua
nilipo ila sauti tu nje wakishauriana kitu chakufanya na mimi. Walinipiga siku
ya kwanza tu. Wakitaka kunifahamu. Ila baada ya hapo ndipo ikawa kushauriana,
ila nafikiri walikuwa wakipokea maagizo kutoka kwa Mbabe. Nilisikia wakimtaja
na wakiambiana inabidi kumuuliza nini chakufanya na mimi baada yakujiridhisha
mimi sio askari mpelelezi. Inavyoonekana Mbabe hapendi au hataki kuua.
Anakanuni yake inayosema damu ya mtu mkononi mwake ni mkosi na hataki afuatwe
na damu ya mtu ila pesa tu. Kwa hiyo nafikiri waliafikiana wakanitupe porini,
mimi mwenyewe ndio nitafute njia yakutoka au kama kuna baya litanipata, sio juu
yake.” Baba Naya akaongea taratibu tu.
“Ila sasa
wakati nimelala, nikasikia wakiogopeshana nje kuwa mtoto wangu amekuja na watu
wa usalama, na wakuu wa nchi wananitafuta. Mbabe ameshauriwa na polisi lazima
anitoe. Ndipo sasa nikaja kuachwa pale mliponikuta.” “Pole sana.” Wote wakampa
pole. “Katika mazungumzo yao, umesikia wakisema chochote juu
ya Bale?” Joshua akauliza. “Ni kama waliokuwa wamejionya juu ya
hilo. Walikataa hata kumtambua.” Akajibu baba Naya. “Sisi tumepata habari zake
kwa sehemu.” Joshua akamsimulia baba Naya juu ya Bale kutokana na ujumbe
walioachiwa chini ya mlango wa Geb, hotelini.
“Ndio
nimesikia mkiweka mipango hapo?” Geb na Joshua wakaangaliana. Hawakujua kama
alikuwa akiwasikiliza, alikuwa amefunga macho muda wote. “Samahani mzee wangu.
Naona tumeweka mipango bila kukushirikisha.” “Hata kidogo. Nyinyi endeleeni tu.
Ila mjue nawashukuru sana.” Hilo likapunguza wasiwasi. “Karibu.” Geb naye
akaitika. Maji yakawa tayari bafuni. Joshua akatafuta hekima yakumwambia baba
mkwe aende akaoge abadilishe nguo zinazonuka.
“Wakati
anaoga, nitatengeneza uji.” Huyo mama akawa mkarimu zaidi ya walivyoomba.
“Tunashukuru sana.” Geb akaongeza. “Ungependa nikusaidie?” Joshua akauliza.
“Labda kunisindikiza mpaka bafuni. Bado nahisi kizunguzungu.” Joshua na Geb
wakamsaidia kusimama. “Mkono huo wa kushoto upo na maumivu makali sana.” “Basi
kitakushika upinde wa suruali.” Baba mwenye nyumba akamuwekea kiti huko bafuni.
Baba Naya akajisafi akisaidiwa na Chui, Geb alimnong’oneza akimuomba yeye ndio
aingie bafuni amsaidie kwa kuwa wao ni kama wakwe. Joshua alimpa suruali yake.
Akatoka akiwa angalau msafi.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Waliwaombea
hao askari wawili wabakie hapo ili wasubiri kukipambazuka, waweze kuchukua
usafiri wakuelekea mpakani mwa Zambia na Mbeya. Wao wakaendelea na safari
kurudi Mbeya mjini, usiku huohuo, wasogee karibu na uwanja wa ndege.
Baba Naya alishakunywa uji na dawa ya maumivu, akapotelea usingizini akiwa
amevaa suruali ya Joshua. Simu ya Naya ikaingia. “Umenisahau
mpenzi wangu!” “Hapana. Ila nimeona mzee amechoka na alikuwa na maumivu.
Amelala.” “Ameweza kuzungumza?” “Ameongea. Kilichokuwa kikimsumbua zaidi ni
njaa. Ila tunarudi naye ili aje aangaliwe hukohuko. Naomba ulale Naya.” “Basi
nionyeshe hata kwa video tu nimuone.” Naya akasihi
akimbembeleza.
“Ni giza,
na amelala nyuma! Tunakopita ni giza, hata kwa video hutamuona, Naya. Naomba
ulale kesho mapema tu tutakuwa Dar.” “Acha nizungumze
naye, ili atulie.” Wakamsikia baba Naya akiongea. “Basi
nakupa baba, ameamka.” “Asante Joshua, na samahani kwa usumbufu.” “Usijali.
Mimi ndio nilikuwa nikikuhurumia wewe. Nakupa baba.” Akamkabidhi. “Baba
Naya?” “Nipo mama mzazi. Nimekula, najisikia vizuri. Usiwe na wasiwasi.”
“Maumivu ni ya wapi?” “Naona waliniumiza mkono huu wa kushoto na nyuma ya
kichwa. Ila vinginevyo nipo mzima kabisa. Hapa nilikuwa nimelala, mpaka
nilipokusikia ndio nimeamka.” “Pole baba.” “Acha
kulia. Si uliniombea nirudi nyumbani?” Kimya, Naya
akiendelea kulia.
“Ndio
narudi nyumbani.” “Pole baba.” “Mimi nipo sawa. Mambo yote
yakienda sawa, nitakuona hivi karibuni.” “Nitakuwa
nakusubiria uwanja wa ndege. Mimi na Zayoni.” “Kumbe una
mipango mizuri tayari! Basi ulale ili ukiamka uwe na akili iliyotulia.” Akamsikia
akicheka taratibu. “Ujue nakusubiria!” “Najua mama. Najua.
Zayoni yuko wapi?” “Mwanao muoga huyo! Amelala hapo chumbani kwangu. Imenibidi
kutoka, ili nizungumze na wewe. Alikuwa hapo kitandani kwangu. Itabidi nikalale
kwenye kitanda cha Bale.” “Bora ukalale kitandani kwa Bale si kwake, ili
usimchafulie mashuka yake.” Wakacheka maana Zayoni hutandika mashuka
meupe kitandani kwake. Kidogo wakacheka.
“Wewe
ukiamka nipigie.” “Naomba ulale Naya.” “Nimesema ukiamka baba jamani!” “Hapana.
Wewe ukitulia huko ujue na mimi huku nitalala. Naomba acha wasiwasi. Si
umenisikia mimi ni mzima?” “Basi nalala, baba. Ila nikiamka nitapiga tena.”
“Najua hutalala Naya. Utatulia masaa mawili kisha utapiga tena. Naomba ulale
kabisa, upumzike. Nataka ulale, utulie. Au hauhesabu tena siku?” “Nilipoteza
mahesabu walivyokuchukua. Ila sasa hivi naanza tena. Naolewa na Joshua,
mwenzio.” Wakamsikia baba Naya akicheka.
“Na leo
ulijaribisha gauni?” “Nanaa amekuja kulichukua mwaya! Anasema nitalichafua,
niache mtindo wakulivaa kila saa!” Mpaka Geb akacheka,
ndipo wakajua wanasikiliza. “Nimelimisi gauni langu!”
“Yamebaki masaa mangapi ulivae rasmi?” “Kesho ukija nitakupa mpaka dakika. Acha
nilale nitulize akili. Nilikuwa nalia mwenzio. Nalia kila saa.” “Nakujua.” Naya
akasikika akicheka. Wakaongea kidogo na baba yake akasikika kutulia.
Akamrudishia simu Joshua.
“Sasa hivi
hata ukiniambia nilale, nitalala kama mtoto mchanga.” “Nimekusikia.”
“Nimefurahi sana. Nimeongea na baba Naya, mwenzio! Siamini!” Joshua
akacheka. “Kwa hiyo na leo nitegemee kukoroma.” Naya alicheka sana.
Akasikika amefunguka kabisa. “Nakuweka mute, Joshua.” “Ili
nipitwe!” “Bwana Joshua!” “Wewe koroma tu.” “Kwanza nishasahu siku hizi huwa
watu wanakoromaje.” Joshua alicheka sana mpaka akajisahau kama yupo na watu
karibu
“Mwenyewe
Naya huyo!” “Oooh kabisa. Naya huyu huwa hakoromagi.” “Basi usiweke mute.” Naya
akacheka sana. “Umejuaje?” “Najua janja yako. Unaweza ukaweka mute, nikasema
hujakoroma, kumbe huko Zayoni anakesha!” Naya alicheka sana.
Angalau Naya akatulia na kweli akalala, Joshua akimsikiliza. Huku ameweka na
yeye mute ili asiwasikie pale garini.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Geb
aliendesha mpaka wote wakapotelea usingizini, wakamuacha yeye peke yake. Yeye
ndio alizijua hizo pande za dunia alizokuwa akizifuata. Hakuna aliyemuelewa
wala kujua hapo ni mashariki au magharibi. Lakini yeye alionekana kuelewa.
Wakati akiendesha simu yake ikaanza kuita. Ilionyesha Nanaa. Akakunja uso,
hakumtegemea muda huo. Akapokea kwa haraka. “Vipi?” “Mimi
nalia dad!” Alikuwa Magesa. “Kwa nini tena unalia usiku
huu wewe niliyekuachia familia yangu?” “Mbona
hurudi sasa? Kwani ‘muda si mrefu’ ni masaa mangapi? Maana sasa hivi ni masaa.” Akamtajia
mpaka na dakika baba yake alizoondoka nyumbani. Geb akajua ameamka usingizini,
mida hiyo ya alfajiri lazima aamke ale ndipo aendelee kulala, akaangalia saa
akagundua ni mapema zaidi ya muda wake.
“Muda si
mrefu, inategemea Magesa.” “Na nini?” Akauliza. “Na umbali
au kitu au jambo. Wakati mwingine ni ngumu kutabiri muda kamili.” “Mimi
nalia dad. Muda si mrefu, haufiki!” “Pole
Magesa. Mimi nipo njiani. Si unajua kila nikikanyaga mafuta na kila nikiendesha
huwa...” “Unakuwa unakuja au lengo ni kurudi nyumbani kwa mami, bibi,
Magesa, Liv na Jimmy. Hata kama ndio unatoka hapo getini lengo ni kuwahi kurdi
nyumbani kwa ajili yetu.” Akamalizia Mgesa mwenyewe. “Ewaaa!
Basi ujue sasa hivi naendesha haraka, ila kwa makini sana kwa kuwa nakuja
kwenu. Mami amekupa maziwa?” “Amekataa huyo. Ameamka na kukuulizia. Amekuja
huku akilia. Anakutaka wewe, ndio nikaona nikupigie, mzungumze kwanza. Nahisi
amekuota.” Akamsikia Nanaa akimjibu.
“Eti
Magesa? Kunywa maziwa, halafu urudi kulala. Nikipata ndege ya mapema, ukimka
wewe na ukienda shule na kurudi, mimi nitakuwa nimeshafika nyumbani.” “Muda
si mrefu utakuwa umeshafika?” “Naamini Mungu, utakuwa
umeshafika. Halafu nikiwahi mapema, nafikiria mimi ndio nije kuwachukua shule.” “Ukija
kutuchukua wewe ndio nitakuwa nafurahi sana.” “Basi
kunywa maziwa, rudi kulala. Nitamwambia Jerry, leo mimi ndio nitakuwa dereva wa
wakina Magesa.” Akamsikia akicheka. Akamuaga baba yake vizuri, akamkabidhi
simu mama yake.
“Karibu
aamshe ndugu zake, ndio bibi yake akamwambia eti aje alilie huku chumbani kwetu
mpaka apate majibu yake yote. Yaani mama jamani!” Geb na Nanaa wakaanza
kucheka. “Hapo atakua amemuuliza maswali akaona anamtoa usingizi wake wote,
akaona aje anitoe mimi usingizi!” “Muda si mrefu ndio masaa mangapi?” Geb
akarudia swali la Magesa kwa sauti ya chini, Nanaa akazidi kucheka.
“Mimi
sikujua kama wewe uliwaaga na kuwaambia utarudi ‘muda si
mrefu’.” “Huyohuyo Magesa alitaka nimpe masaa maalumu ili aanze kuyahesabu.
Sasa nikajua nikimtajia masaa, yakiisha kabla sijarudi, wote wataanza kungiwa
na wasiwasi na vilio kama hivyo kwa wote. Wakati naongea na Liv jioni hii yeye
alikuwa ameshalala. Mwenzie nikamuongezea muda si mrefu na Jimmy. Yeye
hakuwepo.” Wakazidi kucheka. “Alilala mapema leo. Liv
alisema alimuona akicheza sana kwenye kuogelea. Akamfuata na kumwambia eti
atulie kabla hajaumia, akashindwa kuimba kwenye harusi ya anko, ndio akatulia.
Lakini anasema alimuona anarukaruka sana kwenye pool, halafu eti
anamwagia wenzie maji mkusudi, ndio akaenda kumtuliza.” Naya
na Geb wakazidi kucheka.
“Kama leo
ilikuwa siku ya kuogela, basi ndio maana ameota. Atakuwa aliwafanyia sana fujo
huko, ndio fujo zote zinarudi usingizini.” “Yaani
Magesa mwanangu! Acha nikamwangalie huko anakopewa maziwa.” “Muda huu akatakuwa
alishamaliza muda mrefu sana. Magesa hawezi kukiweka chakula muda mrefu hivyo.”
“Naomba muache mwanangu, Geb.” Wakazidi kucheka maana Magesa na chakulani
kama mama yake tu. Wakaagana na kukata.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Magesa
huyo?” Joshua akaamka na kuuliza. “Ndiye mwenyewe huyo. Niliwaaga nikawaambia
nitarudi baada ya muda si mrefu. Sasa kumbe yeye anahesabu masaa. Naona
yameshakuwa mengi mpaka huko usingizini kwake, naona ameamka.” “Aisee pole Geb,
na samahani. Ila ujue nilikuwa nakuhitaji sana. Umerahisisha sana mambo.”
“Lakini Joshua, kwa hakika ulijipanga sana mpaka nahisi ungefanikiwa tu bila
mimi. Ile akili yakuchukua taarifa za mzee! Mpaka sasa hivi nafikiria,
najiuliza ulifikiria nini?!” “Nahisi ni Mungu tu wala si akili zangu. Halafu
sikutaka turudie kosa kama tulilofanya kwa Bale. Sikutaka tuje
tujikute wote hatujui chochote kama tuliokuwa hatujajipanga! Anyways, naomba
upokee shukurani zangu sana. Nanaa nishazungumza naye na kumshukuru kwa
kukuruhusu uje.” “Usijali Joshua. Kwa hakika ujue tupo pamoja. Na tunamaanisha.
Ni katika kila kitu.” “Hilo nimelithibitisha aisee. Asante.” Wakaendelea
kuzungumza Geb akiendesha mpaka pakaanza kupambazuka ndipo Joshua naye
akampigia simu Jema ili kuwaangalizia ndege yakuwatoa hapo Mbeya kuwarudisha
Dar.
Baada ya
kuendesha mwendo wakutosha, wakatokea uwanja wa ndege. Kila mtu akamshangaa
Geb. “Haiwezekani Geb!” Geb akawa akicheka. “Ngoja nikupe siri yangu. Biashara
ya kukusanya mazao mashambani, nikilazimika kulala maporini hata kwa watu nisio
wajua, kulinisaidia sana kujua kusoma ramani. Sasa hivi imekuwa kama kasumba
tu. Nikisafiri kokote lazima nijue nimesimama wapi, nimetokea pande ipi. Kwa
ufupi lazima nijue mashariki, magharibu, kusini na kaskazini ni wapi. Hilo ni
lazima nijue.” Wakazungumza hapo kidogo wakisubiria muda wakuondoka hapo ufike.
Baba Naya alikuwa ametulia sana. Ila wakajua ni kawaidia yake. Mara kadhaa
Joshua alijaribu kumuuliza anavyojisikia. Naya alishapiga simu mara kadhaa,
akawa ni kama yupo nao hapo wakisubiria waondoke.
Muda
ulipofika, wakamsadia kuingia kwenye ndege na kuacha viwanja vya ndege vya mji
wa Mbeya wakielekea Dar. Naya na Zayoni walishafika uwanja wa ndege
wakimsubiria baba yao. Baada ya muda mama G naye akafika hapo akiwa anatokea
kwenye shuguli zake, na Nanaa naye akafika hapo akitokea kazini. Bado ilikuwa
mapema tu.
Jijini!
Zikiwa
zimebaki siku 2 tu ndoa ya Naya na Joshua kufungwa, ndege hiyo iliyokuwa
imembeba baba Naya, bwana harusi na msimamizi wake pia, Geb, ikatua kwenye
viwanja vya ndege vya jijini Dar bado ikiwa mapema tu. Naya akawa wa kwanza
kusimama kwenda kumpokea baba yake. Ila akashangaa anatoka akiwa anasukumwa
kwenye kigari. Akamkimbilia pale kwenye whealchair. “Unajisikiaje?”
“Kizunguzungu tu, na maumivu.” “Pole baba. Ila nimefurahi kukuona.” Akamuona
anafunga macho. Akamwangalia Joshua. “Tunaelekea hospitalini ili tujue ni kwa
nini. Ameanza kusema anaona giza.” “Naombeni haya mazungumzo yakaendelee
hospitalini. Unanisikia Geb?” “Sawa mama.” Wakatoka hapo sehemu yakupokea
abiria, baba Naya akisukumwa, amefunga macho.
“Pole
baba.” Zayoni akamsogelea kwa karibu wakati Joshua akimsukuma. “Asante Zayoni.
Unaendeleaje?” “Nyumbani kuna kelele, bora umerudi. Tumewaacha kina mamdogo
wote ndio wameingia na bibi. Wakamkatalia Naya kutoka, ila Naya akawaambia
lazima aje. Wanakelele! Na wameshaanza kugombana.” “Kwa hiyo hali yako baba,
pale hutaweza. Fujo zimeshaanza kama anavyokwambia Zayoni. Bora hivi
tunavyokwenda hospitalini kwanza, ukapumzike.” Naya akaongeza.
“Na kweli
anahitaji mapumziko. Hata safari yenyewe haikuwa tulivu. Na kama walimpiga
kichwani, na barabara tulizokuwa tukipita usiku kuchwa! Sio nzuri kabisa
nafikiri ndio maana hata yeye anasikia kizunguzungu zaidi. Hajapumzika kabisa.
Tutaona daktari atakavyotushauri lakini anahitaji mapumziko kwa hakika.” Joshua
akaongeza, kina Magesa kimya wakifuata kwa nyuma. Tayari Nanaa kwapani kwa
mumewe. Kimya wasafiri wote wakionekana wamechoka. Yalikuwa masaa machache
tokea watoke hapo jijini lakini yakuchosha haswa na hekaheka mpaka wanarudi
hapo.
Walipofikia
gari ya Naya wakati wanamsaidia baba Naya kusimama, huyo mzee alianguka
chini gafla, nakuanza kutetemeka kwa ngvu kama mwenye degedege. Naya aliona
hilo, alianza kupiga kelele akilia kwa sauti. Zayoni naye alishituka sana.
Joshua na Geb walipotaka kumshika, mama G akawaambia wasimguse wamuache kwanza
na wampe nafasi apate hewa. Aliendelea kwenye hiyo hali kama degedege kwa muda
mpaka akajikojolea kabisa ndipo akatulia. Naya alilia sana. “Sasa hivi mnaweza
kumsaidia kusimama sasa.” Mama G akawashitua maana wanaume hao wawili na
wenyewe walibaki wamepigwa na butwaa.
Wakamuingiza
kwenye gari ya Naya, safari ya kumkimbiza hospitalini ikaanza. Walihakikisha
wanampeleka kwenye hospitali waliyojua atapewa huduma kwa haraka. Na kweli.
Baba Naya alipokelewa na kuanza kupewa huduma ya kwanza ikiwemo na kubadilishwa
pia. Alipofanyiwa CT scan, kila kitu kilikuwa sawa huko kichwani, ndipo daktari
aliwaambia inawezekana walimgonga sana, amepatwa Concussion. Kutingishika
kidogo kwa ubongo wake. Lakini daktari akawafariji kwa kuwaambia kwa vipimo
alivyofanyiwa, hakuna kitu cha hatari. Anahitaji mapumziko mazuri ya siku moja
au mbili tu, kisha arudi kwenye shuguli zake za kawaida, ili kurudisha ubongo
kufanya kazi kama kawaida bila kumpa matatizo ya kudumu.
Akatolewa
sehemu aliyokuwa amewekwa kwa muda akipewa huduma ya kwanza na kupelekwa
atakapolazwa. Alishaamka ila wakaambizana watulie kabisa ili
wamfanye na yeye atulie na kupumzika. Alipofikishwa wodini, Joshua
akawa muugwana. “Naomba ukapumzike Geb. Umekuwa ukiendesha usiku kuchwa.
Tukiwahitaji, tutawapigia.” “Unauhakika?” “Kabisa Geb. Nanaa, nakushukuru sana.
lakini huyu anahitaji kupumzika.” Nanaa akamwangalia mumewe. “Naona kweli
akalale, turudi jioni au usiku akishaongea na Magesa.” “Nitawaambia kama mrudi
au la. Nafikiri lengo zima ni mzee apumzike.” “Lakini kweli. Maana tena sio
tuje tujazane hapa, zianze stori, hata ashindwe kupumzika! Naona wazo la Joshua
ni zuri. Tumuache kabisa. Ila kukitokea mabadiliko yeyote yale, tafadhali
tupigie Joshua.” “Bila shaka mama.” Joshua akaafiki kwa mama G.
Wakamwangalia
Naya pale alipokuwa amekaa karibu na kitanda cha baba yake. Joshua akawafanyia
ishara watoke. Wote wakatoka kasoro Naya na Zayoni. Mama G akauliza mara
walipotoka nje. “Unafikiri atakubali tena kwenda saluni kwa masaji? Maana ndio
miahadi ilikuwa leo. Maandalizi ya harusi. Leo awekwe kwenye sauna na masaji.”
“Hawezi kukubali, mama. Ameshituka sana kumuona baba yake kwenye ile hali.
Hawezi kukubali kutoka hapa sasa hivi. Naomba tumuache kwa leo. Akikaa hapo
akaridhika baba yake anaendelea vizuri, kesho hata tukimwambia aende saluni
atakubali. Lakini si leo. Nyinyi nendeni mkapumzike tu. Na kwakuwa na chakula
watampa hapahapa, msihangaike.”
“Basi
akitulia, mwambie aje alale Tabata, asirudi huko Kiluvya kwenye kelele.” Mama G
akatoa wazo. “Hawezi kumuacha Zayoni na hao ndugu za mama yao. Naya anasema ni
wakorofi sana.” “Pale kwetu ni pakubwa sana. Kuna vyumba ambavyo hata
havitumiwi! Waje tu, ili atulie. Akili ibakiwe kwenye harusi yake na baba
yake.” Akaongeza Nanaa. “Nitamjaribisha. Akikubali, nitawaleta. Nawashukuru
sana.” Wakaagana ndipo wakaondoka.
Baba Naya
alilala muda mrefu, akaamshwa ale, akala vizuri tu akarudi kulala tena. Akaamka
tena usiku. “Nendeni mkapumzike. Mimi nipo sawa. Nasikia hata kichwa kimetulia
vizuri. Mpaka kesho nitakuwa mzima kabisa.” “Nataka kubaki na wewe kidogo.”
“Nataka kulala mama. Nikirudi kulala sasa hivi, ndio mpaka asubuhi. Naomba
usiwe na wasiwasi. Nenda ili na mwenzio akalale. Hajalala huyo usiku kuchwa.”
“Basi asubuhi nitakuwa hapa.” “Sasa tena isiwe alfajiri.” “Jamani baba!” Naya
akalalamika. Kidogo wakacheka.
“Itakuwa
hamna maana ya mimi kuwepo hapa. Wewe nenda katulize ile fujo ya mama zako
kule. Wewe unawawezea.” Naya akacheka sana. “Mimi siku hizi sipendi ugomvi na
mtu. Nakuwa mke wa mtu, sina muda huo.” “Kwa ninavyowajua wale, watakutafutia
tu muda.” “Walitaka waanze, nikamwambia bibi, mimi sina muda wa ugomvi, nakuja
kukupokea.” “Bibi akalalamika eti tunatumia pesa za mwanae kupanda ndege.”
Zayoni akaongeza. “Yaani hizo pesa za mama Naya bado tu hazijaisha mpaka leo!?”
Baba yao akaongeza akijiweka sawa hapo kitandani. “Wenzio wanasema ndio
umezichukua zote ukajenga lile ghala na kununua vitu vya ndani, halafu yeye
bibi hajapata urithi wa mwanae.” “Nashauri tumuache baba apumzike kwa leo.”
Joshua akaingilia kwa Zayoni, ili wasiendelee kumchosha.
“Joshua!”
Baba Naya akaita wakati wanataka kutoka. Naya akarudi haraka kama yeye ndio
Joshua. “Hujui ni kwa kiasi gani namshukuru Mungu kwa ajili yako Joshua. Mungu
alikuleta kipindi maalumu akijua tutakuhitaji. Najua unalipa garama kubwa sana
kwetu. Pengine muda uliotumia kunitafuta ungekuwa ukifanya kazi yako, lakini
umehangaika mpaka umenirudisha kwa wanangu na bado unamuhangaikia Bale japo
umejua kabisa, hakukubali! Hakika Mungu akukumbuke na wewe.
Asante sana Joshua.” “Karibu sana mzee wangu. Lakini nakumbuka
ulishanikaribisha kwenye familia. Nahesabu na mimi ni mmoja wenu. Kinachomuhusu
Naya, na mimi kinanihusu, na Mungu ameniweka katikati yenu akijua nitaweza
tu. Kwa hiyo naomba muwe na amani kabisa. Chochote mnachoona naweza kufanya,
msisite kabisa kunishirikisha.” Wakazungumza kidogo na kutoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Twende
ukalale mchumba wangu. Bwana harusi.” Joshua akacheka. “Harusi kumbe bado ipo!”
“Lazima. Hapo tushakubaliana. Haturudi nyuma. Ila sherehe ndio inategemea. Sasa
twende ukapumzike na mimi nirudi kwenye zile kelele nyumbani.” “Mama G anawazo
la tofauti.” “Nini tena?” Joshua na Naya pamoja na Zayoni wakaendelea
kuzungumza wakitoka hapo hospitalini. “Anataka ukapumzike kwao mpaka kesho.”
Naya akacheka. “Wazo zuri lakini ile fujo pale, siwezi kuicha siku nzima eti na
usiku bila sisi kuwepo! Haiwezekani.” “Ndio mbaya hivyo!” “Hujawahi ona ndugu wa
aina ile. Baba yeye anawawezea kwa sababu haongei. Ananyamazaga kimya.
Wanaongea mpaka wanamaliza yote, yeye kimya. Malalamishi yao hayaishi. Kama
kulalamikia kwamba mama alipokuwa hai ni kwa nini alikubali kuolewa na baba!
Haya, alipokufa na wao wakataka urithi wengine wakamsema baba eti amemuua kwa
shida zake. Haya leo wamekuja bibi analalamika kuwa mafao ya mwanae ndio baba
anayatumia sasa hivi kujijenga! Wadogo zake wanasema eti baba alimtoa kafara
ndio amefanikiwa sababu ya kifo cha ndugu yao! Ni fujo na niwazungumzaji
haswa.”
“Sasa
hudhani ndio unasababu ya kwenda kupumzika kwa kina Magesa?” “Mimi
nimeshawazoea. Hawanisumbui. Halafu nimemuahidi bibi nitalala naye usiku nimpe
habari zako kwa undani.” Naya akaanza kucheka mwenyewe. “Sijaelewa Naya!”
“Alikuwa akinikatalia kutoka akitaka kujua naolewa na mwanaume wa namna gani!
Tajiri au masikini! Anayo nyumba au ananipeleka kwenye nyumba ya kupanga halafu
nianze kumlisha! Mzuri au naolewa na mwanaume mbaya ambaye atasababisha nizae
watoto wenye sura mbaya!” “Naya!” “Wewe acha tu niende nikawatulize ili baba
akija wawe wametulia.” “Unataka nikusindikize?” Naya akaanza kucheka huku
akimtizama Joshua.
“Acha
bwana! Watanila nikiwa hai?” “Nakwambia wakiwa wanakutizama hivi! Kuna watakao
kuomba hela. Kuna watakao taka kujua mshahara wako kwa mwezi. Ushakuwa na
wanawake wangapi. Kama ulishazaa. Habari za mama yako na baba yako na mengine
mengi. Wakija kukuachia hapo, huna hamu ya ndoa.” Joshua akacheka sana. “Nenda
kalale upumzike. Achana na ndugu wa mama Naya.” Wakakubaliana Joshua aende
akapumzike. Naya akamrudisha nyumbani kwake wao wakaanza safari yakurudi kwao
Kiluvya.
Siku Moja Kabla Ya Harusi.
Ilikuwa
imebaki siku moja tu harusi ya Naya na Joshua ifungwe. Baba Naya bado alikuwa
hospitalini na Bale bado hajulikani alipo. Usiku uliopita Joshua alilala kama
aliyekufa, akaamka alfajiri na mapema kwenda kazini, angalau kuweka mambo sawa
kabla ya harusi ambayo alijua maadamu Naya anaishi, basi hiyo harusi lazima
kufungwa ila hakujua aina ya sherehe.
Katikati
ya kikao simu ya Geb ikaingia. Akaomba udhuru na kutoka. “Samahani
najua unaweza kuwa sio muda mzuri. Lakini nimetoka kuzungumza na kina Gamba ni
kama wamegonga mwamba huko walikokuwa wakimsaka Bale. Wanasema wengi wanakuwa
na majina ya uongo au wanakuwa hawana vitambulisho wala hati za kusafiria ndio
maana wanatumia njia za panya tu. Kwa hiyo kwa jina hilo la Bale hawajafanikiwa
kupata, na pale mpakani ni kama mahabusu tu. Wakikamatwa hapo wanashikiliwa kwa
muda na ndipo wanasambazwa.” “Wapi?” Joshua akauliza.
“Hapo ndipo
ulipo ugumu. Haijulikani kwa hakika. Wengine huhamishiwa magereza ya Tunduma.
Magereza yakiwa yamejaa na wafungwa wengine wakisema wanatokea Mbeya,
wanapelekwa magereza ya huko. Sasa basi, walianzia magereza ya palepale Mbeya
tulipokuwa tumewaacha, wamezunguka tokea jana na leo lakini hawajafanikiwa
kumpata. Ndio nimewaomba tena, leo warudi tena Tunduma wajaribu kumuulizia tena
kwenye kila magereza.”
“Nakushukuru
sana Geb. Aisee ni muhimu sana. Salamu ya yule mzee asubuhi hii si kuhusu afya
yake ila Bale. Naya naye ni hivyohivyo, mpaka anafikiria pengine baada tu ya
kufunga harusi, yeye mwenyewe ajaribu kwenda huko akasaidie kumtafuta.” “Sio
fungate tena!?” Geb akashangaa. “Akili yake haipo huko
kabisa. Anasema atatulia kama akirudisha familia yao pamoja, hapo ndio hata
akili ya mapumziko itakuwepo.” “Daah! Basi acha niwaambie waongeze juhudi.”
“Nashukuru Geb. Basi tutazungumza baadaye.” Joshua akakata simu.
Reheasal Dinner.
Jioni
hiyo anatoka baba Naya hospitalini, anakutana na ratiba za harusi ya binti
yake, zikiendelea kama alivyoomba mwenyewe jambo lisisimame hata kama ni yeye
mwenyewe asizuie harusi ya binti yake kufungwa. Walikuwa na mpango wa kufanya
reheasal dinner, nyumbani kwa Joshua. Ili kufanyia mazoezi kila kitu
kitakachoendelea kesho yake siku ya harusi. Jinsi watakavyoingia hapo ukumbini,
wakati wa kufunga ndoa na wakati wa sherehe yenyewe. Nani anasimama wapi na
kufanya nini kwa hao walengwa. Bibi harusi, bwana harusi, wasimamizi wote
kujipanga vizuri. Na ndugu pande zote mbili kufahamiana kwa karibu
siku hiyo kabla ya siku yenyewe ya harusi.
Kwa kuwa
Naya alikuwa akitokea saluni, Joshua akaenda kumchukua baba Naya hospitalini,
dereva akatumwa kwenda kuchukua ndugu wa Naya ili na wenyewe wahudhudhurie
kwenye reheasal dinner kama na wenyewe walengwa wakubwa wa hiyo shuguli kuja
kukutana na bwana harusi rasmi pamoja na ndugu zake ambao ndio kina
Magesa.
Naya
alikuwa saluni na mama G, Nanaa, Liv, Grace na mtoto wake wa kike wakianza
kutengenezwa. Kwa hiyo baada ya saluni, muda ulipofika wakaongozana nyumbani
kwa Joshua. Baba Naya alishapelekewa hospitalini nguo safi na Naya wakati
akielekea saluni. Akaoga hapohapo hospitalini na kubadili akabaki akimsubiria
Joshua. Na wao ndio wakawahi kufika nyumbani kwa Joshua. Akaingia Man, mume wa
Grace, Geb na watoto wao wakiume na dada yao wa kuwasaidia kazi. Wakiwa
wanazungumza tu hapo sebuleni Joshua, baba Naya, Geb wakawa wanaingia mama G na
kundi lake la kina Nanaa, pamoja na bibi harusi wao. Vicheko na stori wakicheka
kuanzia huko nje vilisikika ndani walipokuwa wamekaa hao wanaume. Hawakupishana
sana na James. Kundi likakamilika ndani, vicheko na utani vikaendelea wakati
wakiwasubiria ndugu wa kina Naya ambao walishafika Kiluvya, ndio wanaletwa
hapo.
Magesa
akaomba wote watulie wamsikilize aimbe. “Naombeni mumsikilize baba mzazi jamani!
Ameweka juhudi kweli kujifunza na kushika maneno.” Nanaa akamuombea mwanae.
“Mama yangu amesema mimi ni mtoto mzuri, nikikubali kufanya jambo naweka
nidhamu mpaka nahakikisha nafanikiwa.” “Kweli Magesa wewe ni mtoto mzuri sana.”
“Asante dad, kwa hiyo watanisikiliza na leo pia?” “Na mimi pia nitakusindikiza,
pamoja na anti Naya. Tutaimba pamoja.” “Ila mimi ni mpaka nisimame.” “Basi pumu
imepata mkohozi. Kwani wewe huwezi kuimba mpaka usimame bwana Magesa!?”
“Hamuwezi kunisikia vizuri na kuniona, bibi.” Wakaanza kucheka. “Haya baba.”
Bibi yake akamalizia huku akicheka akitingisha kichwa.
“Basi mtu
anikaribishe. Eti dad?” Watu walicheka mpaka machozi. “Jamani mkaribisheni
mwanangu aanze kuimba!” Nanaa akajaribu kumtetea mwanae. Watu wakazidi kucheka.
Mara wakasikia geti linafunguliwa na gari kubwa lililobeba ndugu wa Naya
wanaingia wakiimba. Naya akamwangalia baba yake. “Naona wenzetu wamechangamka
kwelikweli! Wanaingia na vigelegele.” “Hayo ndio mambo.” Akaongeza Grace kwa
mama yake. “Basi hao mtawachoka.” Naya akasimama ili kwenda kuwakaribisha.
Joshua
akataka kumfuata, akasimama kabisa. “Naomba kwanza mimi nikawakaribishe halafu
ndio uje na wewe.” Naya akaongea akicheka na kumtizama baba yake pia. Joshua
akawa hajaelewa. “Sio wote ndio twende tukawapokee kwa shangwe kama
walivyoingia!” Mama G na yeye akasimama kama kumsindikiza Naya, akafuata na
Grace. Ikawa kama Naya ameshindwa awaambie nini akabaki amesimama akimwangalia
baba yake, ikabidi baba Naya amsaidie. “Ana maana yake huyo. Acha kwanza yeye
atangulie kukaribisha mama zake, kisha sisi ndio twende.” Akaongeza baba Naya.
Wakaangaliana, Naya akazidi kucheka. “Naombeni mimi nitangulie kwanza jamani.
Kisha mtakuja na baba.” Naya akatoka kwa haraka bila kuongeza zaidi.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Akakuta
mama zake wadogo, bibi yake, wajomba zake wawili na wake zao pamoja na watoto
wanashuka kwenye hiyo hiace, kibasi kidogo. “Naombeni tuzungumze kwanza kabla
hamjaingia ndani.” “Naya naye! Mbona unataka kutunyima raha na maonyo
yasiyoisha.” “Hapana mama mdogo. Nataka tu kuweka msisitizo ili leo paishe
vizuri.” “Sasa kwani..” “Mnaona wale askari pale?” Naya akaendelea, wote
wakageuka. “Mbwa wamefungiwa ndani kwa sababu yenu tu. Jamani ndugu zangu, hii
nyumba ina kamera kila kona. Hapa tuliposimama hapa, mwenye nyumba anatuona kwa
kupitia simu yake pale alipokaa.” “Mpaka vyooni!? Tutajisaidiaje sasa?” Akaanza
mmoja wa mama yake mdogo.
“Humo
ndani, kila kona, jikoni, sebuleni, vyumbani pia anazo kamera ila anazima
kukiwa na mgeni analala kwenye hicho chumba.” Naya akaendelea taratibu tu.
Akashangaa wote kimya. Hakuna hata shangwe tena. Akatoka Zayoni. “Kujibu swali
lako mama yangu mdogo, ndani ya vyoo hakuna kamera ila nje ya kila mlango
kwenye hii nyumba, ndani na nje ya nyumba, kuna kamera. Sasa hivi ndivyo
zinavyofanya kazi.” Wote kimya. Naya akaendelea akiwatizama wote.
“Mlango
wowote ukifunguliwa ndani ya hii nyumba, kuna mlio unaingia kwenye simu ya
Joshua. Ambaye ndiye mwenye nyumba na kumfanya aangalie. Anaweza kuzungumza na
huyo mtu akiwa popote hapa nchini, ila akiwa nje ya nchi, walinzi wake macho
yao yapo mpaka ndani.” Kimya wote wakisikiliza kwa makini. “Mbona shangwe zote
zimeisha huko nje?” Akauliza mama G. “Naya huwa anaweza kuzungumza lugha
wanayoelewa wao tu. Kuna anachowaambia tu, ndio maana unawasikia wametulia. Ila
utawasikia tena.” Akajibu baba Naya taratibu tu.
“Kwa nini
nimewaambia haya yote!” “Msiibe.” Naya akataka kuendelea lakini Zayoni
akamuwahi. “Ewaa! Zile tabia zakuchukua vijiko, vikombe na kuingia vyumbani
mnaiba na kufichwa vitu mpaka kwenye sidiria, hapa si mahali pake ndugu zangu.
Tafadhali mjihadhari.” “Muache tamaa.” Akaongeza Zayoni. “Huyu naye jeuri kama
baba yake! Sasa aliyekwambia kuna mwenye tamaa hapa nani?” “Usimpandishie
mtoto, kwa kuwa wote sisi tunajuana tabia zetu. Nimewawahi ili msije ingia
aibu. Kitu kikiibiwa hapa, itajulikana. Ukitoka nacho nje ya hilo geti, mbwa
watapata harufu, ndipo mtaanza kusachiwa pale getini. Kwa kifupi tu, mali ya
humu ndani haitoki bila ruhusa ya mwenyewe.” “Kwa hiyo kuomba ni sawa si
kuchukua tu?” Akauliza mmoja wao.
Zayoni
akaanza kucheka. “Ndipo linapokuja swala jingine kabla na la mwisho. Siku ya
leo, kesho kwenye harusi yangu, mtu yeyote kati yenu, haruhusiwi
kumuomba Joshua chochote. Hata pesa na yale matatizo ya pesa ya ada za
watoto shule na pango, hamruhusiwi.” “Mashariti mengi mpaka nishachoka!” “Kama
umechoka bibi, dereva huyo hapo, anaweza akakurudisha nyumbani ukapumzike, mimi
nitakuja kukusimulia jinsi mambo yalivyokwenda hapa maana na leo tunalala
kitanda kimoja bibi yangu. Tupige stori kama jana usiku.” “Nitaondoka vipi mama
yako hayupo? Mimi ndio mwakilishi wake.” “Basi jikaze. Maana mambo ndio
yanaanza, mwakilishi wa mama Naya.” Naya akaongea akicheka kidogo ila walimjua
ni mkali kama mama yake.
“Jamani
kuna mwenye swali? Au mtu hajaelewa chochote hapa?” “Na hivi tunavyoshangilia
ni sawa au napo kamera zinatuangalia?” Akauliza kishari akilalamika. “Wewe mama
yangu mdogo shangilia kwa kadiri ya uwezo wako, mimi mwenyewe
nitawasaidia vigelegele.” Wote wakawa wameshapoa kabisa, kama morari iliwaisha.
“Cha
mwisho na cha msingi, nakumbushia tu. Inawezekana jana wakati nawaambia hili
mjomba na mama mdogo mlikuwa mmelewa sana.” “Nini tena!?” “Hapa tuliposimama
sasa hivi, na yeyote mtakayekutana naye kuanzia sasa upande wa Joshua,
wanamuheshimu sana baba.” “Tena sana.” Zayoni akaongeza. “Mmemsikia Zayoni.
Baba mliyezoea kumtukana na kumbeza kila wakati, hapa anaheshimiwa mno.
SITARUHUSU. Narudia tena. Sitaruhusu, hata kwa bahati mbaya, au kuropoka
yale maneno yenu ya kejeli kwa baba. Nikikusikia tu, hapa unaondoka. Ukiona
huwezi kumuheshimu baba Naya, basi ondoka, tutakuja kukuonyesha picha ya
kitakachokuwa kimeendelea wakati haupo.” Kimya, Zayoni akaanza kucheka.
“Hapo
wenzio wanataka kuondoka wote.” Zayoni akaongea akicheka. “Basi nitawaonyesha
video, gari hiyo hapo, dereva yupo, mambo yafamilia yetu tunayoshindwa kumaliza
kifamilia, tukaendeleze kwetu sio hapa kwa watu.” “Si na wewe patakuwa kwako,
lazima ajifunze kuishi na watu huyo Joshua!” “Sawasawa. Lakini bado hapajakuwa
kwangu. Hajanioa. Akishanioa, ndio tuanze zile fujo zetu hata mbele yake,
atajifunza tu na itabidi ajue jinsi yakuishi na nyinyi. Ila kabla hajanioa, hapana.”
Kimya. Na yeye Naya akanyamaza.
“Mambo
yataenda sawa Naya mjukuu wangu, wala usiwe na wasiwasi.” “Asante bibi yangu.
Kesho na mimi niolewe, niwe mke wa Joshua.” “Unavyojidai!” “Ndio maana ulikuwa
unajishaua na huyo Joshua! Kumbe sababu mambo yake safi!” “Kumbe! Sasa
hamjamuona Joshua wangu. Nyinyi acheni fujo, aje mumsalimie tu. Sio muanze
kumuuliza yale maswali yenu. Au mnasemaje ndugu wa mama Naya?” Kidogo wakaanza
kucheka na vigelegele.
“Hapo
sasa tunaweza kutoka.” Baba Naya akasimama, wengine nao wakamfuata nyuma.
“Kapendeza baba Naya! Kama sio yeye!” “Na wala si mafao ya mama Naya. Mwacheni
baba Naya.” Naya akajibu kwa haraka, vigelegele vikaendelea. Kina mama G nao
ikabidi wachangake, wakawapokea hapo na vigelegele.
Katikati Ya Msafara Wa Mamba,
Kenge Nao Wamo!
Kabla
hawajataka kusalimiana baada ya vigelegele na shangwe, wakashangaa Malon
anatoka kwenye hilo basi lililoleta ndugu wa Naya. Naya akamuona wakwanza.
Akashangaa mpaka ikabidi na Joshua ageuke. Wote wakageuka, kimya. “Huyo kijana
aliomba lifti baada ya mjomba wako kumwambia hawezi kuongozana na sisi akiwa
kwenye gari yake, wewe ulisema wote mje na usafiri mmoja ili kuepuka
kuchanganya askari getini. Kwamba ni hiki kibasi tu ndicho kitafunguliwa geti
na kuruhusiwa kuingia humu. Ndio ameacha gari yake nyumbani na kuongozana na
sisi, anasema anashida sana na wewe, mnafahamiana.” “Kabla yakumpandisha kwenye
gari ungenipigia mimi simu bibi au mjomba!” “Shuguli ni watu mama.” Akajibu
bibi yake bila hila moyoni. “Sie huyo, bibi.” Naya akamalizia.
Malon
akacheka akitingisha kichwa. “Nipo hapahapa nakusikia mimi mwenyewe Naya! Na
nimekuja na habari njema.” Wote kimya wakimtizama wakimsikiliza Malon. “Najua
Bale alipofungwa na naweza kusaidia.” “Sasa mbona umesimama hapa?” Akauliza
Zayoni. “Asante sana Zayoni.” “Subiri kwanza Naya. Kwamba sisi tunashangilia
hapa, kumbe Bale amefungwa jela!?” Akaanza bibi mtu. Kimya.
“Nilikwambia
bibi, Bale atarudi. Na inawezekana akarudi kabla ya harusi.” “Kweli Naya wewe!?
Kaka yako amefungwa jela unashangilia! Kweli Denis wewe, mkeo amekufa juzi tu
nyumba inakushinda mpaka watoto wanafungwa jela! Upo hapa unashangilia harusi
ya Naya, mtoto hajulikani alipo!” Bibi akaanza kulia, wakaja kina mama
wadogo. “Dada atakuwa anageuka huko kaburini!” Mdogo
mtu akaongeza na kuzidi kulia. “Kweli wewe huna nafsi
baba Naya. Umetulia ndani kwenye majumba haya yenye mageti makubwa hujali mtoto
alipo?” Wakazidi kulia. Nguvu ileile waliyotumia kushangilia,
ikageuka kilio. Baba Naya kimya.
“Labda
tungewakaribisha wageni kwanza, angalau wapumzike.” Akatoa wazo mama G. Kila
mtu akawa kama amepigwa na butwaa. “Twendeni jamani. Poleni sana. kuna mahali
maalumu kumeandaliwa kwa ajili yenu. Twendeni mkatulie kwanza, halafu tutapata
muda wa mazungumzo.” Mama G na Grace wakawatoa hapo. “Nani amefungwa jela mami?
Mimi naogopa polisi!” Mama G akageuka haraka. “Haya njooni. Twendeni na
wageni.” “Wana polisi?” “Hapana Magesa. Usiogope, hakuna polisi.” Baba yake
akamtuliza na kuongeza. “Samahani Joshua. Ni sawa dada yao akiwachukua awapeleke
ndani kwenye chumba cha tv, wasiende huko mpaka nitakapokwenda kuwachukua?” Geb
akaweka ombi ambalo halikuwa na jibu la hapana. Anataka watoto wake wakafungiwe
mahali mpaka yeye akawachukue. “Bila shaka.” Dada akaondoka
na watoto.
Naya
akamgeukia Malon kama ammeze. “Sijakusudia kuharibu Naya, nimetaka kusaidia.”
“Labda mimi niulize swali kama alilouliza Zayoni. Samahani lakini. Ni kwa nini
sasa upo hapa? Maana ni kama nimesikia umesema unajua alipo na unaweza
kusaidia!” Akaongeza Geb na swali. “Nisingeweza kufanya bila kuwasiliana na
familia yake kwanza.” “Pengine ufafanue zaidi. Tafadhali, Malon. Maana Bale
yupo matatizoni. Anatafutwa sana. Muda si mrefu tumetoka kuzungumza na askari
wanao mtafuta, bado Bale hajulikani alipo.” “Hawawezi kumpata.” Malon akamjibu
Joshua kwa kujiamini.
Wote
kimya. “Labda mimi niulize japo nimesikia habari hii kwa juu juu wakati Geb
akizungumza na hao askari wanaomtafuta Bale. Mimi naitwa Man, shemeji yake Geb.
Sijui wewe ni nani?” “Wewe uliza swali lako.” Malon akamjibu kijeuri. “Samahani
Man. Anaitwa Malon. Tulikuwa kwenye mahusiano naye kabla ya Joshua. Ni kweli
anafahamiana na familia yetu. Hata Bale amepotelea kwake. Akiwa ametoka
nyumbani kwenda kwake kufanya kazi.” “Bale hajapotelea kwangu, hilo moja. Na
pili mimi siye niliyesababisha Bale aondoke kwangu. Ni ujuaje wake.” “Kama
tazizo ni Bale, na mimi imekuaje niliondoka kwako? Maana wote tunajua tatizo si
Joshua.” “Tatizo ni Joshua. Hata kama ukikataa Naya. Matatizo kwetu ni kawaida,
na tulikuwa tukiyamaliza.” Wakaanza Naya na Malon.
“Wewe
hujui mahusiano Malon. Hujui kuishi na watu. Hutaki majukumu. Kila mtu anayo
mapungufu yake, watu wote wanajua, na watu wanaishi pamoja kwa kuwa wanajua
jinsi yakuchukuliana.” “Sasa hapo kosa linakuaje ni langu tena? Yeye ndiye aliyeondoka
na kwenda kujiingiza kwenye matatizo akitaka kufanikiwa kwa haraka!” “Man
samahani. Naomba uliza swali lako.” “Sitakwenda mbali na Zayoni, kwenye swali
lake la kwa nini upo hapa. Ila mimi nitabadilisha kidogo, kwamba, unataka nini
kwa familia ili kusaidia kumpata Bale?” Man akauliza.
“Cha
kwanza nyinyi wote hapa si familia ya Bale. Siwezi kuzungumza chochote na
nyinyi ila familia ya Bale. Na nikisema familia ya Bale, sio tena na Joshua.
Bale hamtaki kabisa Joshua.” “Unakumbuka mara ya mwisho Naya kukupigia simu
usiku kukuomba namba ya simu ya Bale?” Baba Naya akauliza. “Sikumtafuta tena
kwa...” “Sasa hapo Joshua sikiliza zile sababu zake. Moja nzuri sana inakuja.”
“Acha kunikejeli Naya.” “Mimi sikukejeli Malo. Hata huyu Bale
unayemzungumzia hapa ukitaka kumuumiza Joshua wangu kuwa eti hampendi, naye
nilimwambia hakunisadiki. Nilimwambia huwa hukosi sababu ya kukufanya upotee.”
“Sasa ningerudi vipi na taarifa nusunusu?” “Ingekugarimu nini kurudisha ujumbe
kuwa hujapata taarifa kamili, unashugulikia kupata taarifa kamili kisha
utatutafuta?” Joshua akamuuliza. “Hayakuhusu Joshua.” “Umechelewa Malon.
Yananihusu sana.” “Mimi sidhani kama kweli unazo taarifa za kusaidia bwana
Malon.” Akadakia Man. Grace akamvuta. Alisharudi na kusimama nyuma yake.
“Subiri
kwanza Grace. Mimi naongea kwa vile ninavyomfahamu mwanadamu, pengine wewe uwe
tofauti. Huyu kijana amepotelea kwako. Akiwa mikononi mwako!” “Mtu mzima vile
ameamua kuondoka, unafanyaje wakati hata kwao tu aliondoka bila maelewano na
ndugu zake!?” “Kwa sababu yeyote ile iliyosababisha kuondoka kwako. Kwa staili
yeyote ile aliyoondokea kwako, kama kweli wewe ungekuwa mtu wa kutaka kusaidia,
ungetaarifu familia yake mapema sana pale tu ulipogundua asubuhi yake kuwa
hayupo. Kutoa tu taarifa kuwa, Bale ameondoka kwangu. Hivyo tu.” “Asante
sana Man.” Naya akashukuru.
“Hapo
aliposimama Naya, yupo sehemu sahihi, Malon. Inawezekana si pale ungetamani
kupaona au sivyo yeyote yule kati yetu angefurahia, lakini ni uchaguzi na
matakwa ya Naya. Mimi kama baba yake nimeliheshimu hilo kama nilivyoheshimu
alipokuwa na wewe. Anza kuelewa hilo na kulikubali ili wakati mwingine wowote
unapotaka kuzungumza naye, ujue Naya uliyemzoea wewe siye wa sasa hivi. Naya
ataolewa na Joshua, kesho. Iwe isiwe, ataolewa. Mimi niwepo, nisiwepo,
Naya anaolewa na Joshua, KESHO. Chochote unachotaka kuzungumza juu ya
familia hii, huwezi kumtoa tena Joshua. Amejithibitisha ni mmoja wa familia hii
kwa vitendo.” Akaongea baba Naya.
“Ninachotaka
kukuhakikishia Malon, Bale tutampata tu. Labda kama Mungu hayupo. Ila kama
Mungu yupo, basi yeye aliyenipa Bale, atanirudishia. Hata kama nilifanya kosa,
nimemsihi Mungu anisamehe, anirudishie Bale. Sasa Mungu atamtumia nani
kumrudisha Bale, sijui. Kama unazo taarifa, na unataka kuzungumza na
familia. Wote wataondoka ila ujue Joshua hataondoka. Uwamuzi ni wako.
Utasaidia au unaondoka?” “Siwezi kukiuka matakwa ya Bale mwenyewe. Mambo yake
hakutaka Joshua ayajue, basi itabaki hivyo.” Malon akaweka ngumu.
“Jamani,
acheni tu mimi niondoke. Lengo ni kumpata Bale. Acha mimi niondoke tu kuwapa
nafasi.” “Nakwambia ukweli Joshua. Leo ukitolewa kwa hili, kesho utatolewa kwa
jingine. Tena litakalosikika la muhimu sana, kisha watafanikiwa kuja
kuwatenganisha kabisa. Kama Malon hawezi kuzungumza mbele yako, basi.”
“Nikuheshimu matakwa tu ya Bale.” “Basi hilo ndilo litamgarimu Bale huko
alipo, itambidi asubiri. Lakini hutamtoa Joshua kwenye hii familia, labda aamue
mwenyewe Joshua au Naya.” “Mimi hapa niliposhika ni mpaka kifo baba
yangu.” Naya akajibu kwa haraka bila yakufikiria. Ujasiri kwa Joshua
ukaongezeka. Akaushika mkono wa Naya kwa nguvu zaidi.
“Basi
twendeni.” Baba Naya akageuka na kuanza kuondoka. “Twende Joshua.” Naya
akamtingisha mkono waliokuwa wameshikana. Joshua akamwangalia na kurudisha
macho kwa Malon. “Mlinzi atafunga geti ukitoka.” Joshua akamalizia kama
anayemwambia anaweza kwenda sasa.
“Kweli
Naya unakubali kaka yako akae jela sababu ya mtu baki!?” “Joshua si mtu baki.
Na kukutoa tu wasiwasi Malon. Wakati wewe umefungwa. Wala sikuwa nikijua
umefungwa jela ipi! Nikiwa sina hata pesa, mimi mwenyewe na kwa maombi ya baba
Naya, niliweza kukutafuta mpaka nikakupata. Nikakuwekea dhamana ya mamilioni ya
pesa, ukatolewa jela, tena ukawekwa huru bila kosa lolote. Mungu akakufutia
makosa yote na kukupa nafasi ya pili. Sasa Mungu huyohuyo wa nafasi ya pili, atampa
na Bale.”
“Na sisi
pia kama ulivyosema, familia yetu ina matatizo. Mungu atatusamehe na
atatusaidia. Kama alitenda kwako, hatashindwa na kwa Bale. Kokote alipo,
tutampata tu. Wala usijali Malon. Uwe na usiku mwema. Twende Joshua.”
“Ungependa kurudishwa mpaka Kiluvya ulipoacha gari yako?” Joshua akawa
muungwana, akajirudi. “Sawa.” Malon akajibu hivyo tu na kuondoka hapo akawa
anatoka getini. Joshua akampigia simu dereva amfuate na kumrudisha Kiluvya.
Malon akaondoka bila kusema alipo Bale.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Mimi
naomba nimfuate baba kule kwa kina bibi. Wameshaanza kumlaumu na baba hajisikii
vizuri. Asije akaanguka tena.” “Twene wote.” Bado Joshua alikuwa ameshika mkono
wa Naya. “Acha na mimi nije. Au unasemaje?” Mama G akaongeza. “Twende tu mama
yangu. Si unasikia vilio hivyo?” “Sasa utafanyaje Naya!?” Nanaa akauliza. “Baba
alikuwa akiniambia leo asubuhi nilipomfuata hospitalini. Hatutakuwa na majibu
yote kwa wakati mmoja. Kama hili la Malon na msiba huu alioanzisha hapa sasa
hivi, hatukuwa tumejiandaa nao. Akasema tutembee kwa hatua. Tukabiliane na kila
hali tutakayokutana nayo. Lakini hakuna mpango wakurudi nyuma. Amekataa na
amesema lazima kuendelea, iwe tu mimi nimebadili mawazo nimeamua sitaki
tena kuolewa na Joshua, au Joshua mwenyewe hataki tena. Ila kama sisi
tupo tayari, amesema hata kama itatugarimu kuwepo sisi tu wawili,
tusiahirishe.” Naya akaendelea.
“Kama
ulivyomsikia hapa. Anasema tukija kuahirisha tu kwa moja, kesho litatokea
jingine na jingine na ndivyo maisha yalivyo. Si wakati wote yanatoa fulsa sawa
kwa wote. Anasema wengine hawajajaliwa kutokuwa na vipingamizi kila wakati.
Wengine nilazima kulazimishia ili mambo fulanifulani yatokee.” “Hata mimi
namuunga mkono mzee.” “Man mume wangu wewe jamani!” Grace akashituka kabisa.
“Mimi nasema kweli. Kuna mambo mengine Grace, yanayopatikana kwa nguvu.
Si Mungu mwenyewe amesema, ufalme wa Mungu unapatikana kwa nguvu, nao
wenye nguvu watauteka! Mathayo 11:12. Sasa
kama mpaka ufalme wa Mungu ni kwa kutumia nguvu, je huu wetu! Simama hapohapo
Naya, mpaka upate mume.” Wakaanza kucheka.
“Basi
hapo Man amepata shuguli!” “Wanangu wamejiandaa kusimamia harusi, halafu
wanataka kuniletea mahairisho! Usinitanie mimi.” Wote walicheka kwa
sauti. “Yaani Man wewe jamani! Kumbe maandiko yote hayo ni ili wanao
wasimamie harusi!?” “Vyote bwana Grace. Eti Joshua, kwani uongo?” “Kabisa Man.”
Joshua akajibu akicheka. “Mimi naungana mkono na baba Naya. Lakini si kwa
ajili ya Magesa aimbe!” Geb akafanya wazidi kucheka huku wakielekea walipo
ndugu wanao lia.
Kisha Geb
akaendelea. “Ishini kwa kumuenzi mama. Ndoa takatifu ni heshima kwa mzazi
yeyote yule. Msiache kufunga ndoa. Mengine mtajua mbele ya safari.” “Tunashukuru
kwa kutuunga mkono jamani. Uwepo wenu hapa ni muhimu sana. Hakika
tunawahitaji.” “Tupo pamoja Joshua.” Hapo mpaka James akaongeza. Wakaendelea
kutembea. Kadiri walivyosogelea walipokuwepo hao wageni, sauti ya vilio
ikaongeza simanzi na kuwafanya waaache kucheka.
Kabla
hawajaingia ndani, maana wageni hao walipitishiwa mlango wa nyuma, Joshua
akamvuta Naya, kidogo akageuka. “Nimevumilia nimeona tu nikwambie. Umependeza
sana.” “Sasa hapa bado.” Ilibidi Joshua acheke. “Naya!” “Mimi nakwambia ukweli.
Usifikiri eti hapa ndio nimependeza mpaka mwisho! Subiri sasa kesho. Ndio
utasimamisha kabisa harusi.” “Kwa jinsi utakavyokuwa umependeza?” “Hutaamini
kama ni Naya Kumu.” Joshua alicheka mpaka akapiga makofi. Wakawageukia wao.
“Hivi
wewe Joshua unajua kama wakwe zako wanalia!?” Nanaa akamuuliza akimshangaa. “Si
Naya huyu! Anataka kuniponza ukweni.” “Sasa twendeni tukamsikilize baba
Naya, na wakwe zake.” “Mbona sasa hatumsikii akiongea?” “Huwa
anawaacha kwanza wafanye yao mpaka wakimaliza ndipo anaongea. Akiona hawapo
tayari kumsikiliza basi anawaacha tu. Anabaki kimya.” Wakacheka kwa sauti ya
chini. “Acha mimi nianze kuingia, nikambembeleze bibi kwanza.” Mama G
akatungulia ndipo wengine wakafuata.
Walilia
hapo wakimkumbuka mama Naya. Wakalalamika kwa hili na lile wakimlaumu baba
Naya, baba Naya mwenyewe akawa amebaki tu kimya. Upande wa kina Geb wakabaki
wamesimama hawajui wafanye nini! Muda ukazidi kwenda bado hawanyamazi. Naya
akaona asaidie.
“Mimi
nashauri mnyamaze, tumsikilize baba kwanza.” “Nilimuonya
mama yako kuolewa na Denis. Nilijua hata...” “Unakaribia kuharibu
bibi. Maana hapa mama hayupo, aliyebaki ni baba. Nashauri mtulie tuzungumze
hapa, au tubebe tena huu msiba, tukaanzishe tena kule Kiluvya! Hapa kuna ratiba
inayohusu mpaka watoto. Lazima tufanye mazoezi kabla hawajaenda kulala.” “Kwa
hiyo kweli Naya wewe utaolewa wakati kaka yako hayupo?” “Ndiyo
bibi. Tena kesho. Ndio maana nashauri hiki kilio tukihamishie kwetu, tuache
nyumba ya watu na ratiba zao. Sasa kwa kuwa bado hampo tayari kumsikiliza baba,
nashauri tuhamishe kikao chetu cha familia kule kwetu Kiluvya. Dereva
awarudishe. Mimi na baba pamoja na Zayoni tutakuja hukohuko. Tena
hatutachelewa.” “Labda wangekula kwanza.” Joshua akatoa wazi.
“Wapo na
kuomboleza, sijui kama wataweza kula. Eti bibi yangu? Mtajikaza mle kidogo ili
msilale na njaa. Tena wenyewe tunafanana na bibi yangu. Au huoni Joshua?” Naya
akamchokoza. “Ila huo moyo ni wa baba yako. Mimi moyo wangu si mgumu hivyo!
Wangu wa nyama.” Naya akaanza kucheka. “Sasa bibi na wewe unataka tufanane
kila kitu? Acha bwana kulia. Tule, tumshukuru Mungu, mengine tutaendelea nayo.
Au unasemaje?” “Mbona sasa mimi nilifichwa?” Bibi akalalamika.
“Kwa kuhofia mambo kama haya bibi. Hata hapa usingekuja, kwa kilio. Halafu
wanae mpishi mzuri huyo! Chakula chake sitaki kikupite bibi yangu. Na
wamekutayarishia yale mambo yako. Acha kulia bwana.” “Basi
mwambie baba yako anijibu maswali yangu.” Angalau akasikika
ametulia na wanae pia wakatulia.
“Nyinyi
mnamjua baba Naya. Kelele hawezi. Mkitulia hivyo, na yeye atatulia na
atawajibu. Mkianza kelele ndio mnamfunga mdomo kabisa. Haya anza swali lako
bibi yangu.” “Kwanza nataka kujua habari za Bale. Mtoto yule alikuwa mzuri.
Mama yake alimuacha mtoto mwenye maana! Na yupo chuo kikuu! Leo
mama yake tu ameondoka mnamfunga jela! Nilikwambia mimi baba Naya, hawa watoto
wewe hutawaweza bila mkeo, nibaki mimi nikusaidie kuwalea, ukakataa tena kwa
jeuri kabisa! Umeona sasa kilichotokea? Maana..” “Huko unakoelekea
bibi unaharibi na baba hatakujibu tena.” Zayoni akaingilia.
“Na wewe
si jeuri tu kama...” “Naomba tufupishe hiki kinachoendelea.” Akaanza baba Naya.
“Bale yupo jela na hajulikani yupo jela gani na tutampata lini. Wapo polisi
wanamtafuta Bale angalau kujua alipo ndipo taratibu za kumtoa zianze. Naya anaolewa
kesho. Hata yeye nimetoka kumwambia pale hospitalini leo alipokuja kuniona.
Nilimwambia hivi, kesho ataolewa. Ndoa yake haitasimamishwa kwa sababu
yeyote ile, isipokuwa yeye mwenyewe amaeona hamtaki tena mchumba wake au
mchumba wake mwenyewe amebadili mawazo. Nikamwambia jambo ambalo na yeye
hakutaka kusikia. Hata nikifa mimi leo. Wakaweke mwili wangu chumba cha
maiti, harusi ifungwe.” “Haa!” “Sijamaliza.” Baba Naya akaendelea.
“Harusi
ya Naya ipo kwenye mpango wa Mungu, tumeomba na tumemuamini Mungu kuwa ni siku
yenyewe, mengine tunakutana nayo kama hivi nyinyi mlivyokuja mkiwa na shangwe,
kisha kugeuza hapa kilio, ni yatakayojitokeza mbeleni, hayatabadilisha lengo
kubwa la kesho.”
“Kama
nilivyotangulia kusema. Hata kifo changu hakitabadilisha kuolewa kwa Naya kwa kuwa
hata nikifa leo, na kesho nitakuwa nimekufa, mwezi ujao
nitakuwa nimekufa, na mwakani hivyohivyo hakuna kitakachokuwa kimebadilika ila
ndoa ya mwanangu. Kufupisha hili, au kwa kumalizia hili bila mjadala kwa kuwa
mimi na nyinyi hatukuwahi kukubaliana kwenye chochote kile, kubwa na dogo. Sasa
nani anabaki hapa, nani anaondoka sasa hivi kurudi Kiluvya?” Kimya.
“Narudia
tena. Hapatakuwa na mjadala wa Bale tena kwa sababu kati yenu hakuna
atakayesaidia chochote kile ila kutaka kumchanganya tu Naya. Hakuna msiba
tena wa mama Naya hapa. Anayejisikia kuendelea kulia, basi hapa si
mahali pake. Tafadhali tuheshimu ratiba na mipango ya watu. Sasa nani anabaki
nani anakwenda?” “Tutakuwa hatumtendei haki dada kama kipindi kama hichi yeye
hayupo na sisi tusiwepo! Itakuwa sio sawa shemeji.” Akajibu mjomba. “Basi
naomba tutulie, tupate muongozo.” Baba Naya akamaliza na kunyamaza.
“Karibuni
sana jamani, na poleni kwa matatizo. Ila nataka kuwahakikishia tu, hakuna
aliyetulia kati yetu, Bale anatafutwa na pengo lake lipo bayana. Tunaamini
muujiza wowote ule unaweza kutokea, hata Bale kuwepo kwenye harusi kesho. Kwa
hiyo tunaomba muungane nasi kwenye kumuamini Mungu, na tuendelee na
kile tunachoweza kufanya. Mezani hapo kuna vinywaji. Mnaweza tu kuendelea wakati
wakiwahudumia vitafunwa vidogovidogo wakati tukifanya mazoezi na watoto kabla
chakula cha pamoja ndipo tuagane tukapumzike kwa usiku huu. Karibuni sana.”
Joshua akawakaribisha.
Wakafanya
mazoezi hapo, kila mmoja akajua nini chakufanya kesho yake siku ya jumamosi.
Harusi hiyo ilikuwa ikifungwa saa kumi jioni hapohapo nyumbani kwa Joshua na
kushiriki chakula cha jioni pamoja kumshukuru Mungu kwa harusi hiyo. Kwa hakika
kuliandaliwa. Huyo mpambaji aliyekuwa akipamba hilo eneo, alipatendea haki.
Siku hiyo jioni, kilichokosekana ni maua tu ambayo yalikuwa yawekwe siku ya
harusi yenyewe ili yabakie bado fresh na harufu nzuri. Kwa
hakika palionyesha mwenye pesa anaoa! Maneja masoko huyo aliweka pesa yake
yakutosha kwenye hiyo harusi, akisaidiwa na marafiki wenye pesa kama yeye.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Waliagana,
ikawa Naya anatakiwa kwenda kulala kwa kina Nanaa ili asubuhi wawahi saluni
pamoja na wasimamizi wote. “Naomba unisamehe Nanaa. Sitaweza kwenda kulala,
wakati najua baba hajisikii vizuri halafu namuacha peke yake kule! Hakika sitaweza
jamani. Acheni nikalale tu nyumbani, asubuhi na mapema nikishahakikisha
amekula, amekunywa na dawa, ndipo nimuache akiwa anakwenda saluni na mimi ndio
nije.” “Naya wewe!” Nanaa akaishiwa nguvu kabisa. Joshua na Geb wakawasikia,
wakasogea.
“Kweli
Nanaa. Hakuna kipodozi kitawekwa kwenye huu uso kesho, kikakubali bila leo
kuondoka hapa na baba.” Bila kuuliza wakawa wamepata jibu. “Nimekuandalia mpaka
chumba!” Nanaa akalalamika. “Samahani Nanaa. Samahani sana. Lakini naomba mimi
ndio nimrudishe baba Naya nyumbani. Hakika sitaweza kulala na kesho nitaamka
nimechoka zaidi, hutanipenda.” “Mwezio amejiandaa kweli kwa ajili yako!” Mama G
akaongeza, Naya akaishiwa nguvu akabaki kimya, akamgeukia Joshua.
“Sasa
wewe ndoa utaiweza wewe!” Naya akaanza kucheka. “Kesho utamuacha mume, uende
kwa baba Naya tena?” “Nikienda kwa baba Naya, nambeba na Joshua wangu. Usiwe na
wasiwasi mama.” Wakacheka. “Nanaa usiumie bwana! Naomba unielewe. Ile picha ya
baba kuanguka ile jana pale uwanja wa ndege, inanisumbua kweli, sasa nafikiria
hiyo hali impate usiku akiwa na hii fujo yote hii! Watamuua baba yangu jamani.”
“Kwani hapo bado hayajaisha!?” “Mama! Wewe acha tu. Undugu kazi mama yangu,
acha tu. Hawa watu hawajui kumaliza jambo. Wewe si umesikia bado bibi
analalamikia mama aliyekufa, kuolewa na baba?” “Jamani!” “Basi ndio hivyo. Na
wakijua tu sitakuwepo huko, watampandisha pressure. Hiki kilio kitakuwa cha
usiku kuchwa, alilotabiri baba litatimia. Ndoa yangu ifungwe, yeye asiwepo.
Sitaki kumpa shetani nafasi. Naombeni mniruhusu tu. Naahidi sitachelewa
saluni.” “Sawa.” Na wenyewe wakaafiki. Lakini walimaliza vizuri tu mpaka
wakacheza pamoja na vigelegele viliendelea na ndugu wa mama Naya pia
walisherehekea.
Usiku Baada ya Rehearsal Dinner.
Waliondoka
ndugu wa Naya, nahilo gari. Wakabaki wao kumalizia na maombi wakiikabidhi siku
ya kesho mikononi mwa Mungu, wakamuombea na Bale ndipo Naya na baba yake pamoja
na Zayoni wakaondoka. Walipofika nyumbani wakakuta gari ya Malon bado ipo.
“Hivi nifanyaje baba jamani!? Huyu mtu anataka kuniharibia baba! Mimi namjua
Malon.” “Hakika sitamruhusu. Wewe tulia tu.” Wakashuka na kuingia ndani,
wakamkuta Malon akizungumza na bibi. “Baba Naya huhitaji chai?” Naya akamuwahi
kabla hata ya salamu. “Nitashukuru mama. Naona nina kiu nayo kweli.” “Basi
dakika chache tu, nakuletea.” Baba Naya akakaa kochini, Naya akapitiliza
chumbani kwake anakolala na bibi yake, wengi wa ndugu walishaondoka kwenda
kulala makwao kasoro waliotokea kijijini na bibi. Baada ya dakika chache
akapitiliza jikoni kutengeneza chai ya baba yake.
“Malon!”
Baba Naya akaita. “Naam!” “Ulipokuja nyumbani kwangu kwa mara ya kwanza,
unakumbuka jinsi tulivyokupokea?” “Nakumbuka mzee wangu.” “Nikakufanya mmoja wa
familia bila kukubagua, ukawa kama Bale tu. Ndivyo ninavyofanya kwa vijana wote
wanao jisogeza kwenye hii familia bila kujali dini wala kabila. Uwezo wala
muonekano. Ndivyo nilivyo.” Akaendelea.
“Lakini
wewe unataka kuweka tabaka ndani ya familia yangu, na SITAKURUHUSU.” Mpaka
Naya akashangaa nakusimama huko jikoni. “Joshua ni mmoja wa familia hii. Hilo halitakaa
likabadilika tena, na kesho atakuwa mume wa Naya. Sasa basi, kwa kuwa
wewe umeshindwa kumpokea kama wewe ulivyopokelewa hapa ndani bila kubaguliwa
ila kusambaza sumu kati yake na Bale.” “Mimi nimeongea alichosema Bale.”
“Nilishawahi kukwambia alichokuwa akikisema mama Naya juu yako?”
“Hapana.” Malon akajibu. “Nilinyamaza mpaka wewe mwenyewe ulipopambana naye.
Lakini bado nilipokuwa nikikutana na wewe nilikuheshimu, lakini wewe umeshindwa
kuwa muungwana! Unasambaza chuki waziwazi.” Baba Naya akaendelea akimtizama
machoni kabisa, bila kukwepesha macho.
“Hivyo
basi, hutakuwa tena mmoja wa hii familia. Na hukaribishwi tena
hapa.” “Haiwezekani! Yaani unaniadhibu kwa kosa la Bale?” “Labda
nikuulize Malon, undugu huo unao utaka hapa ni kwa nani na kwa nini? Maana ulianzana
na Naya, ikashindikana. Ukaja kwa Bale. Naye pia umeeleza mapungufu yake mengi
tu mpaka amepotea akiwa kwako, kwa sababu ya mapungufu yake kuwa mengi na
kukukera sana, ulishindwa hata kumfuatilia tena. Haya, Joshua naye humtaki.
Sasa ukisema unaendelea kuja hapa na kuendelea na hii familia unayotangaza
ina matatizo, ni kwa manufaa ya nani? Au utanufaika na nini au
nani sasa?” “Siamini!” “Labda niambie ni nini unataka kuendeleza hapa, Malon!
Ni nini? Au unataka nini? Bale mwenyewe ambae yupo matatizoni, ambaye
alikuamini sana, unashindwa kumsaidia, upo hapa. Unataka nini
Malon?”
“Daah!
Siamini!” Bado Malon akasikika kama hajaridhika, haamini. “Labda sasa wewe ndio
uzungumze Malon. Mimi nikusikilize aina ya mahusiano unayofikiria utakuwa nayo
kwenye aina ya watu wa hii familia!” “Basi bwana.” “Usiku mwema.” Baba Naya
akasimama kabisa nakumfungulia mlango. Malon akacheka na kutingisha kichwa.
Kisha akasimama na kutoka. Naya mwenyewe hakuamini kama ni baba yake.
“Sasa
unamfukuza mtu pekee mwenye taarifa za Bale! Utampataje huyo Bale?” “Tutampata
tu, usiwe na wasiwasi. Kila uamuzi hapa duniani una jinsi ya kuwajibisha. Bale
yupo kwenye kuwajibika kwa maamuzi yake. Nimemuombea rehema, Mungu atamrehemu
tu. Ningetamani iwe tofauti na kukupa majibu ya kukufurahisha lakini sina
jinsi. Nafanya kwa kadiri ya uwezo wangu kumpata. Na tutampata kwa njia
sahihi lakini si kwa kumuharibia Naya. Usiku mwema.” Baba Naya akaingia
chumbani kwake na kuwaacha wote kimya.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Bado Malon Hakubali Kushindwa. Yupo Na Taarifa Za Bale Zenye
Mashariti Yaliyokataliwa Na Baba Naya.
Hajui Kukubali Kushindwa.
Na Ameondoka Akisikika Hajaridhika.
Nini Kitaendelea?
Bale Yuko Wapi?
Harusi Ya Naya Na Joshua Bado Ipo?
Inaendelea.
0 Comments:
Post a Comment