Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI&PESA! – SEHEMU YA 35. - Naomi Simulizi

MAPENZI&PESA! – SEHEMU YA 35.

 “Kweye majira ya saa tano na nusu, mmoja wapo wa walinzi wa Kiluvya alinipigia simu kuwa kuna moto ulianza pale nyumbani. Anasema ulianza nyumba ya mbele, ikawa kama kufunga na kufungua pakalipuka vibaya sana.” Naya alikuwa akisubiria kwa hamu Geb afike mwisho ajue moja. “Na kama mnavyojua umeme wa kule galani tulichukulia kwenye nguzo inayopita karibu na nyumbani. Kwa haraka sana ule moto ukahamia kwenye gala pia. Na lenyewe likalipuka.” Geb akaendelea.

“Tunavyofikiria labda kulikuwa na gasi ilikuwa wazi pale ndani nyumbani! Maana mlinzi anasema ilikuwa kama kibatari kimewashwa na kuzimwa. Ndivyo nyumba inavyosemekana ilivyo teketea.” “Wakati huo baba, Zayoni na bibi na yule mjukuu wake wakiume aliyekuja naye kutoka kijijini, Luka, walikuwa wapi?” Naya akauliza tena swali la pili wakati hata la kwanza hakujibiwa. “Unajua leo ndio mzee alikuwa akipokea mazao. Dereva anasema alimshushia mazao leo mida ya jioni. Mlinzi anasema mzee alikuwa galani kwa muda mrefu sana. Yaani kama aliyekuwa akisubiriwa hivi! Alipoingia tu ndani, na kufunga milango yote, anasema hata dakika 20 hazikupita ndio huo moto ukatokea.” Naya akameza mate akatulia kidogo. Kimya wote kama ambao hawajui wamwambie nini Naya.

“Naomba nisaidie Geb.” Akaanza Naya baada ya kutulia kwa muda akionekana kama ambaye hapati majibu yake kwa waziwazi. “Nisaidie kuongea hicho unachosita kukisema, maana unanitia wasiwasi zaidi. Baba Naya yuko wapi? Zayoni, Luka na bibi yangu je?” “Baba Naya yupo hospitalini, Naya. Wote wapo hospitalini. Hali sio nzuri, ndio maana mama ameona tuje tuwafuate, angalau mkamuone mzee.” Naya akabaki ametulia kama ambaye bado hajaelewa vizuri na akajua Geb hayupo tayari uzungumza zaidi ya hapo au hajui azungumze nini!

“Twende Naya.” Akamgusa begani mkewe baada ya yeye pia kutoka kwenye butwaa maana wote ni kama wakabaki wamepigwa na bumbuwazi, hawajui waseme nini kwa Naya, wakati wote wanajua fika kilichotokea. Wajumbe na wafikishiwa habari, wote wakabaki kimya.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Fungate waliyokuwa wameambizana wanaihamishia nyumbani, ikaishia hapohapo. Wakaondoka na kina Geb, kwenye gari yao. Joshua na mkewe wakawa wamekaa nyuma. Kama kawaida Geb akawa dereva, mkewe amekaa pembeni. Kimya haswa. Naya akawa amegeukia dirishani ametulia. Joshua akamwangalia baada ya kufikiria huko mawazoni akimuhurumia sana mpenzi wake. “Niambie chochote unachofikiria sasa hivi, Naya mke wangu.” Naya akamgeukia Joshua. “Naogopa sana. Nimeingiwa na hofu ya ajabu Joshua! Hapa tumbo linauma nahisi kutapika na kama kuanza siku zangu. Mikono inakufa ganzi.” Naya akajibu kwa sauti ya chini iliyosikika ikitetemeka. “Pole sana. Pole.” Joshua akatamani aongee mengi ya kumfariji, lakini hata yeye alikuwa kwenye mshituko. “Nishike mkono.” Naya akajisogeza karibu na kumshika mkono vizuri, akajikunja kitini, akajiegemeza akimtizama Joshua anavyosugua viganja vyake kama kuvitoa ganzi. Akapotelea mawazoni, kimya hakuna aliyezungumza tena, na wote wakashukuru Mungu Naya hakuuliza swali jingine. Geb akaendelea kukanyaga mafuta kuwatoa Goba, kwenda Kibaha hospitali.

Hospitalini.

Walimkuta mama G peke yake akiwasubiria. “Pole Naya, mama. Pole sana.” “Naomba niambie ukweli mama. Hali yangu ni mbaya, niambie tu ukweli nijue.” “Inavyoonekana ni kama moto ulianza wakiwa wameshakwenda kulala na wamefunga milango yote, mpaka mageti. Kwa hiyo wote walikutwa mlangoni kama waliokuwa wakijaribu kufungua mlango wakalemewa na moshi, pengine na kuzirai kabla ya kuungua. Na wamesema kuna mwili mwingine umepatikanika pale nyumbani unaonekana ni wa mtoto mdogo wa kiume.” “Ni mjukuu wa bibi alimchukua baada ya bibi yake aliyekuwa akimlea kufariki. Ni wa palepale kijijini anaitwa Luka.” Naya akaongea taratibu akiwaza mpaka akawashangaza.

“Na baba Naya?!” Akauliza tena taratibu. “Hali yake sio nzuri Naya. Mzee aliungua sana.” Mama G akaendelea kwa tahadhali. “Nasikia kutapika, tumbo linanikata.” “Twende chooni.” Joshua akataka kwenda naye yeye. “Acha mimi niende naye Joshua, ili kuingia naye chooni kabisa.” Wakati Naya na Nanaa wanataka kuondoka, Naya akaanza kutapika baada ya hatua chache sana wakiwahi chooni. Alitapika mpaka Joshua akamshika mbavu. “Tumbo linauma sana. Kama nataka kujisaidia.” Nanaa akakimbia naye chooni. “Nenda na wewe Joshua, uhakikishe anarudi kumuona baba yake kabla hajachelewa.” “Ndio hali mbaya hivyo!?” “Sana. Ila tuliomba awekwe kwenye chumba kizuri, apewe dawa ya kutuliza tu maumivu. Lakini hata wewe ujiandae. Ameungua yule mzee, huwezi kumtambua.”

“Madaktari wameshindwa kumsaidia kwa chochote kwa jinsi alivyoiva mwili mzima! Kuna nesi amepita hapo, ametuambia eti tumruhusu, ili akapumzike. Ndio katika kufikiria, tukasema labda anasubiri kumuaga Naya, ndio apumzike.” “Mungu wangu uko wapi leo!?” Joshua akaweka mikono kichwani. “Aisee pole sana Joshua. Poleni sana.” “Mungu wangu!” Joshua akarudia kumuita tena Mungu. Wakamuona Naya na Nanaa wanarudi ametulia tu.

“Twendeni. Uzuri kwenye chumba alipo baba Naya, kuna choo. Jikaze mama.” Mama G akamsaidia Nanaa, akamshika yeye Naya, wakaelekea alipokuwa amewekwa baba Naya. Walitembea kimyakimya mpaka walipokaribia mlangoni ikabidi mama G amuandae. “Naya!” Wote wakasimama. “Baba ameungua sana, ni ngumu kumtambua.” “Amepewa dawa ya maumivu?” Naya akauliza. “Ndiyo. Lakini kwa alipo na alivyo sasa hivi, nahisi anakuhitaji tu wewe.” Mama G akaweka tena msisitizo akitamani Naya aelewe bila kuongea kwa undani. “Nyinyi hamtaingia?” Naya akauliza akidhani wanamuaga. “Mimi nipo na wewe Naya.” Joshua akajibu kwa haraka. “Nashukuru jamani. Asanteni.” Naya akashukuru na kuingia.

Mwili wa baba Naya ulikuwa umefunikwa, lakini hata mashuka yalionyesha damu. Ikawa kama nyama mbichi iliyofunikwa na shuka jeupe. Naya hakuwa ameelewa alivyoambiwa kama baba yake ameungua. Alikutana na kiumbe wa ajabu amelala kwenye hicho chumba cha peke yake, kitanda kimoja tu, kuashiria huyo ndio baba yake. Anatisha, hajawahi ona! Hana ngozi ile ya juu, mwekundu usoni alipoachwa wazi mpaka kichwa ambacho nacho hakikuwa hata na nywele wala ngozi. Ila alikuwa akihema kwa nguvu kwa kituo. Kila pumzi aliyovuta, aliivuta kwa nguvu zake zote. Hapohapo Naya akaanguka na kuzimia. “Mimi nilijua tu.” Mama G akaongea mikono kichwani.

Ikabidi Joshua na Geb wamtoe nje. Akapewa huduma ya kwanza, akazinduka na kukaa kwa haraka. Na hedhi nayo ikaanza. Naya akapatwa na kutapika mfululizo, akaanza na kuharisha. Akakataa kulazwa. “Naombeni nirudisheni tena kwa baba.” “Unauhakika Naya!? Umetapika mfululizo bila kupumzika!” “Kabisa. Ni mshituko tu, lakini baba yangu sasa hivi ananihitaji, jamani! Lazima nirudi na mimi niwepo kwa ajili yake. Amekuwa na mimi kila wakati, kila mahali, katika kila hali. Siwezi kumuacha sasa hivi peke yake zaidi akiwa kwenye ile hali. Lazima na mimi niwepo kwa ajili yake sasa hivi. Nitoeni haya madripu ya maji. Sihitaji. Ni mshituko tu, ila nitakuwa sawa. Naomba nisindikize Joshua. Nataka kuwa na baba yangu.” Joshua akaomba atolewe tu hapo alipokuwa akipewa huduma ya kwanza. Naya akajikaza tofauti na walivyotarajia. Wakamsindikiza tena kurudi alipokuwa amewekwa baba Naya.

Safari hii walimkuta baba Naya hata ule upumuaji wa kwa nguvu umepungua. Anahema kwa mbali sana. Naya akamsogelea pale alipokuwa amelala. Ukweli alikuwa akitisha. “Pole baba. Pole sana.” Naya akabaki ameshika tumbo akimtizama machoni napo akawa hatizamiki ila walibaki wakitizamana na baba yake. Naya akashindwa, machozi yakaanza kumtoka kama baba yake. Baba Naya alikuwa akichuruzika machozi. “Baba yangu mimi jamani!” Naya akasikika akiongea taratibu. “Pole baba. Pole sana baba yangu.” Naya akarudia machozi yakimtoka, akitizamana na baba yake. “Niite tena baba!” Naya akaongea taratibu akimwangalia na kumsihi taratibu, akitamani kumsikia. Chumba kizima kimya, machozi wote yakiwatoka.

Akamuona kama anasogeza midomo. “Nimefurahi baba. Nimefurahi nimekuona. Pole sana baba yangu. Na asante kwa kila kitu baba. Asante umesimama na mimi kwenye kila hali mpaka umenifikisha kwa Joshua! Asante baba yangu.” Akamuona anaendelea kutoa machozi. Hapakuwa na jinsi ya kumshika kwani kila aliposhikwa hata na nguo, nyama ilitoka.

“Baba Naya?” Mama G akamuita. “Pole. Pole sana. Funga macho na wewe upumzike. Sisi tupo hapa na Naya, na atakuwa sawa kabisa. Usiwe na wasiwasi. Hatakuwa peke yake. Tuko naye.” “Pole sana mzee wangu. Pole sana.” Joshua akaongezea kwa mama G. Naya alikuwa akitetemeka kama amepigwa na baridi kali. “Mimi nitakuwa sawa baba. Nipo na Joshua na kina Magesa, sasa hivi. Nitafanya kama ulivyoniambia. Nakumbuka kila kitu na nakuahidi sitasahau. Nakupenda baba yangu. Nakupenda sana.” Wakamsikia baba Naya akihema kwa nguvu, kisha kimya. Wote wakajua ameshakata roho. Naya akabaki ameduaa kama ambaye haamini. Hata machozi yakakoma. Ukazuka ukimya wa ajabu hapo ndani.

 Mwishoe Geb akatoka kwenda kumuita nesi. Akaja kumuangalia. Akamfunika mpaka kichwani ndipo taarifa zikaenda kichwani kwa Naya kuwa ule ndio mwisho wa safari ya baba Naya hapa duniani. Joshua akamshika mkewe, wakatoka hapo. 

Duniani Wote Tunapita. Unatokaje Hapa Duniani! Ni Fumbo Kwa Kila Mwenye Mwili!

Baba Naya alikuwa ameiva sana, kiasi ya kwamba ilikuwa lazima azikwe haraka. Naya alitoa namba za simu za baba zake wakubwa ili kujulishwa kuwa itakuwa hata ngumu kusafirishwa. Ila bibi yeye na Zayon pamoja na Luka ni kama walikaushwa kabisa. Kwa hiyo Joshua na kina Magesa wakafanya taratibu za mazishi kwa haraka, baba Naya na Zayoni wakazikwa siku hiyohiyo jioni karibu na alipokuwa amezikwa mama Naya, safari yao hapa duniani ikawa imeishia hapo. Ndani ya masaa 24, walikuwa wazima na mipango kamilifu. Umauti ukawakuta kiasi chakushindwa hata kuweka msiba kwa masaa mengi mbeleni, wakarudi mavumbini siku hiyohiyo. Kwanza waliagwa katika kanisa la hapohapo hospitalini hata hawakuonyeshwa, na kupelekwa makaburini moja kwa moja.

Kesho yake, safari ya kumsindikiza bibi na kijana aliyekuja naye kuwarudisha kijijini na wenyewe kwa mazishi ikaanza. Ikawa hakuna kupumzika. Watoto wa bibi wakasaidiana na kina Joshua. Wakafanya kwa ufanisi, wakakodi magari kwa kuwa ni kama watoto wengi wa huyo mama na wajukuu walikuwa wamesambaa hapo jijini Dar. Ndani ya huo mwezi wakawa wamekusanyika kwa harusi na msiba.

Kwa kuwa Joshua alishajua dawa za Naya akiwa kwenye siku zake zaidi anapokuwa kwenye hiyo hali ya mshituko, akabeba hizo dawa na soda zakutosha, ndipo safari ya kuelekea kijijini kwa mazishi kwa mara ya pili, ikaanza. Kina Magesa wote mpaka Grace na Man walikuja kwenda kuzika kijijini. Nako huko hawakukaa sana. Walizika, siku inayofuata, baada ya mazishi, kina Magesa, Naya na mumewe wakarudi jijini Dar. Naya alikuwa ametulia sana. Akiangalia sehemu, ni mpaka umshitue.

Ila ikawasaidia na kuwarahisishia sana kuendesha mambo kwa umakini, haraka bila paniki ya kilio cha Naya kitu ambacho kila mmoja wao alitegemea iwe hivyo. Lakini ikawa kinyume kabisa. Kwani Naya alikuwepo kama hayupo. Kimya tu. Joshua akabaki kuweka mipango akizungumza na ndugu wa baba Naya, nao wakampa baraka zote aendeshe mambo vile atakavyoweza. Ndipo sasa kina Magesa na marafiki wa karibu wakaibebe hiyo shuguli nzima kwa wepesi, pesa ikitembea bila kuchelewesha mambo.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Walirudi wote mpaka nyumbani kwa Joshua na Naya, Naya akapitiliza juu chumbani kwao kama anayewahi chooni, hata hakukaa sebuleni. Nanaa akataka kumfuata ili kumsaidia huko chumbani, Joshua akawahi. “Nashukuru Nanaa. Acha nimfuate, pengine atataka kuoga kabisa.” “Mimi nashauri tuwaache wapumzike jamani.” “Nafikiri ni wazo zuri. Tumbo linamsumbua sana, acha nimsaidie alale.” Joshua akakubaliana na wazo la mama G. “Tafadhali mtupigie muda na wakati wowote mkituhitaji.” “Kwa niaba yangu  na mkewe wangu, hakika nyinyi watu nawashukuru. Mungu wa mbinguni awakumbuke kwa hili pia, na naomba anapowabariki kwenye hili awatendee mpaka mjue ni katika hili amewalipa kwa kumsindikiza mtumishi wake kwenye safari yake ya mwisho. Mmemtendea haki baba Naya. Mbarikiwe mpaka mjue Mungu mwenyewe amewabariki.” “Amina Joshua.” Wote wakaitika na kama wakapigwa tena na butwaa. Mwishoe Geb akawashitua, wakasimama na kuondoka bila yakuongeza neno.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakabaki Joshua na mkewe. Akamsaidia kuoga, akapanda kitandani. Joshua akiwa ameshaoga, na yeye akapanda kitandani akaanza kumsugua tumbo na kiuno mpaka akalala bila hata kuzungumza. Mapumziko ya Joshua yakahamia kwenye kuuguza tumbo la Naya. Baada ya siku tatu mbeleni, tumbo likatulia, hedhi ikakoma ila bado Naya alikuwa mtulivu sana hapo kitandani, hana maongezi kabisa. Siku ya 3 mbeleni tena, Joshua akafuatwa na Jema mpaka nyumbani kuwa wanahitaji msaada wake ofisini. Anasubiriwa. Ilikuwa mida ya mchana. Ikamlazimu kwenda tu na ahadi yakutochelewa, chakula cha usiku watakuwa pamoja.

Naya akasubiri mpaka ilipofika mida ya saa 10 jioni, Joshua akampigia simu kumwambia mambo yamevuta kazini, atachelewa kidogo. Naya hakuona shida. Aliyajua majukumu ya mumewe. Na yeye akaona atumie muda huo kwenda saluni angalau akaoshe nywele alizotengenezwa sababu ya harusi karibia mwezi ulitaka kufika na zilishaanza kutoa harufu. Pia alijua anakaribia kurudi kazini, maisha yanatakiwa yaendelea. Ila mwili ndio ni kama ukawa umegoma. Akabaki amejilaza hapo kitandani akiwaza na kushindwa kutoka kabisa.

Ni kama kila kitu kilipoteza ladha na maana ya maisha kwa siku kadhaa, akawa amepigwa ganzi ya namna yake. Akawa kama ameshushwa kwenye ulimwengu anaoutambua, ila majibu ya maisha yake yote hapo duniani yakawa yametoweka. Hajui tena chakufanya. Ila alijua wazi maisha nilazima yaendelee, nilazima atoke tu hapo kitandani. Akamsikia baba yake akimwambia masikioni. ‘Tuliza akili usije kuharibu kazi ya watu.’ Naya akakaa kwa haraka aliposikia usemi aliozoea kuambiwa na baba yake.

Hapohapo akampigia simu Joshua kumtaarifu anatoka kwenda saluni. Hilo likamfurahisha sana Joshua, akajua angalau atachangamka kidogo. Na angalau siku hiyo wakazungumza hata Joshua akahisi utofauti. Naya aliweza kuzungumza zaidi na jibu alilozoea kumjibu tokea msiba wa baba yake, jibu la ‘sawa’, ‘ndiyo’ na ‘hapana’. Akamuahidi atamkuta nyumbani, asingechelewa. Wakaweka mipango ya usiku huo, kidogo akasikika akicheka. Joshua akaridhika, akampongeza moyoni mwake akijua anajikaza. Ni baba Naya! Alijua ameumia. Lakini akajua kutoka hapo kitandani kutamsaidia. Wakazungumza kidogo ndipo wakaagana, Joshua akaendelea kuwajibika. 

Hakuna Msiba Usiokuwa Na Mwenzie.

Akiwa ameshamaliza shuguli zake za saluni, ndio anatoka saluni kurudi kwenye gari yake, akashangaa kumkuta Bale amesimama nje ya mlango wa gari yake. Giza lilishaanza kuingia. Naya alishituka sana. “Bale!” Hakutegemea. “Naona maisha yanaendelea bila mimi, hakuna anayenijali! Nafasi yangu amechukua mwanaume wako. Maswali yanayotakiwa yajibiwe na mimi, yeye ndiye anaye ya jibu!” Naya akabaki kimya akimshangaa Bale. “Hati ya nyumba ya Kiluvya iko wapi?” “Baba alimpa Magesa kwa kuwa walifanya naye biashara. Akamwambia hiyo hati ndio itakuwa kama dhamana, mpaka amalize deni lote ndipo amrudishie!” Naya alijibu akiwa na mshangao mkubwa sana usoni. Bale aliyekuwa akitafutwa, amerudi na lawama, hasira waziwazi usoni, halafu akiwa na swali ambalo Naya hakutegenea kabisa zaidi kwa wakati huo wametoka kuzika!

Kwa aina hiyo ya swali kwa haraka sana Naya akajua inamaana anajua kama baba yao amefariki pamoja na Zayoni. Hakuonekana kujali kabisa. Na pia hakuonekana na hali mbaya. Msafi tu. Hafananii kama aliyekuwa jela au kwenye matatizo! Akiwa kwenye mshangao huo, akashangaa mtu nyuma yake anampiga kwa nguvu sana nyuma eneo karibu na kichwa na shingoni, hapohapo akapoteza fahamu. 

Kwa Joshua.

Joshua akiwa ndio anajiandaa kutoka kazini arudishwe nyumbani, ujumbe kutoka kwa Naya ukaingia. Ujumbe wa Naya huwa hausubiri. Akarudi kukaa na kusoma. ‘Joshua. Naomba kukuaga rasmi. Nimeamua kuendelea na maisha yangu. Nimepoteza mengi sana sababu ya kuwa na wewe. Naokoa kilichobaki kwenye maisha yangu na nafsi yangu pia. Nilifanya makosa kuendelea kukung’ang’ania na kushindwa kuhesabu garama. Nipo kwenye wakati mgumu, nahitaji  kuendelea mbali na wewe. Funguo za gari, zipo kwenye tairi ya mbele kushoto. Ndani utakuta pete zako pia. Nimeamua kukuachia kila kitu nilichokipata kwako mpaka hii simu vyote utakuta kwenye gari yako na gari nimeacha nje ya ile saluni waliyonisuka. Kila la kheri, maisha mema.’ Joshua akahisi hajaelewa.

Tokea wamzike baba yake, Naya hakurudia hali ya kawaida, lakini hapakuwa na dalili ya kuachana! Akakumbuka kwa kituo mazungumzo yao ya mwisho! “Hapana.” Joshua akahisi anamtania. Akajaribu kumpigia tena na tena, simu ikawa ikiita tu. Akatoka kwa haraka kwenda alipoelekezwa ameliacha gari. Dereva alimpeleka mpaka kwenye hiyo saluni. Akaangalia funguo kwenye hilo tairi aliloelekezwa, kweli akaikuta hapo. Joshua akamwambia dereva aondoke tu.

Akafungua mlango, ni kweli alikuta kila kitu cha Naya mpaka pochi! Akaangalia ndani ya pochi, akakuta hata walet yake ipo na ina vitambulisho vyake vyote mpaka na kadi za bima, benki pia zipo! Joshua akahisi kuna kitu hakipo sawa. “Naya anaanzaje hayo maisha bila hata kitambulisho chake!” Joshua akawaza akitumia tu akili zake kwa harakaharaka. Akajua kwa hakika alichoandikiwa kupitia simu ya Naya, si Naya. Na huyo aliyefanya hayo yote kama si mjinga sana, basi hakujipanga vizuri.

Hapohapo akampigia simu Nanaa. “Umezungumza na Naya leo?” “Ndiyo. Jioni hii tu. Alipokuwa saluni, mimi bado nilikuwa kazini. Tena alinipigia yeye mwenyewe kunisalimia. Tukaachana akitaka azungumze na Magesa kipenzi chake. Nikaona wazo zuri ili amchangamshe kidogo. Kwanza kwa nini unaniuliza? Kwema?” “Sijui Nanaa! Mpo nyumbani?” “Wote tupo nyumbani.” “Basi nakuja.” Kabla ya kuondoka, Joshua akaingia pale saluni kwanza. Akawaulizia kama Naya alikuwepo hapo. “Alikuwepo hapa. Alikuja akitaka tu kuosha nywele, lakini akaosha na miguu na kutengeneza kucha pia.” Akajibu dada aliyemuhudumia. “Kuna mtu yeyote aliyemfuata hapa?” Joshua akaendelea kuhoji taratibu. Akafikiria kidogo kama kuvuta kumbukumbu. “Hapana. Ila nilimuona akichati na kuzungumza na simu tu. Mpaka mwisho alipotoka.” Joshua akafikiria akiwa amesimama hapo saluni na wenyewe wanataka kufunga.

Mwishoe akaona aondoke tu. Akatoa gari hapo kuelekea Tabata nyumbani kwa kina Magesa. Njia nzima alikuwa akifikiria. “Haiwezekani!”  Joshua akapinga kabisa kwa sauti. Akaendelea kuwaza mpaka alipofika kwa kina Magesa, akawaonyesha ujumbe. “Mmmh!” Nanaa akabaki akiwaza akivuta kumbukumbu ya mazungumzo yake na Naya. “Alisikikaje kwenye simu?” “Hakuwa amechangamka, lakini alikuwa akicheka maana nilikuwa nikimsimulia vituko vya Magesa. Sasa si unamjua anavyompenda Magesa? Akawa anacheka huku akiuliza maswali. Mwishoe akataka kumsikia Magesa mwenyewe. Nikampigia simu mama, nikamwambia amwambie Magesa ampigie simu anti Naya, anahamu naye.” “Na walizungumza kwa muda tu  na Magesa, akimpa stori za shule.” Mama G akaongeza. Wote kimya.

“Najua mnaweza msinielewe kutokana na huu ujumbe wake, lakini jamani kuna linaloendelea na Naya hakuwa mtu wa kuniacha.” Kimya. “Najua mnaweza msinisadiki pia, mkahisi ni kupaniki sababu nimeachwa, lakini hebu fikirieni tu. Mtu anayekwenda kuanza maisha yake, ndio aache mpaka vitambulisho na kadi za benki! Anakwenda kuanza vipi maisha na hana pakwenda? Nyumba iliungua moto, tulikuwa na mpango wa kupajenga tena! Jamani huyu Naya anayeonekana amenitumia huu ujumbe, anakwenda kuanza wapi na vipi!?” Joshua akauliza taratibu tu wote wakiwaza.

“Nyumbani kwenu je?” “Nimepiga simu pale getini, wameniambia aliyepita hapo baada ya Naya kutoka, ni mpishi tu. Naye alishaondoka. Kwamba hakuna mtu mle ndani!” “Twende Kiluvya.” Geb akasimama. Wakatoka. Walifika nyumbani kwa kina Naya, hakuwepo. Walizunguka mpaka nyuma kwenye kuta zilizobakia za gala. Hapakuwa na mtu yeyote. Wakaita, hapakuwa na dalili ya Naya.

Geb na Joshua wakakumbuka maneno na vitisho vya Malon kwa Naya. Wakakumbuka Malon kuapa kumsaka Naya mpaka kumpata tena akasema labda ahame dunia. Hapohapo wakaenda kutoa taarifa polisi lakini wakawakatisha tamaa baada ya kusoma na ujumbe kutoka kwa Naya mwenyewe. Naya hakuonekana yupo hatarini kwani hata gari haikuvunjwa. Hapakukutwa hata tone la damu kuashiria pengine alivamiwa! Wakaona ni visa tu vya mapenzi. Joshua amekimbiwa.

“Mkubwa hapotei.” Likawa jibu la kwanza kutoka kwa maafande hao walio wakuta hapo mapokezi mida hiyo ya usiku, baada ya kumsikiliza Joshua. Wazi waliashiria fika kuwa Joshua ameachwa, na aanze kukubali matokeo na hapo hapakuwa na kesi. Kwanza hata hivyo vitisho walivyosema Malon alimtishia Naya, hawakuwa wameviripoti polisi. Ikakosa nguvu kabisa ikawa wanamsikiliza Joshua kama anayetunga tu habari sababu ya kupaniki kwa kuachwa. “Moyo wa mtu msitu! Huwezi jua lililokuwa likiendelea moyoni kwa mkeo.” “Na kweli! Pengine aliamua kurudia makoloni yake! Inatokea.” Afande mwingine akamalizia hivyo kwa kebehi akimuunga mkono mwenzie.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Walipanga wakimaliza fungate ndipo wakae kama familia walizungumzie hilo la vitisho vya Malon, wakijua fika, Bale alirudi kwa Malon na kama mwanzoni, amegoma kuwasiliana nao. Wakatulia wakiwa wameshajiridhisha hayupo jela na wala mwili wake haupo chumba chochote cha maiti kwani na huko nako walitembelea mpaka Dar pia Bale alitafutwa huko magerezani, mahospitalini mpaka vyumba vya maiti, ndipo wakaamini yupo na Malon tena.

Kwa Naya.

Naya aliamka akiwa na macho mazito sana. Akagundua yupo garini, tena mwendo kasi, nje giza. Akataka kukaa maana alilazwa kiti cha nyuma kabisa. Akashindwa. Palikuwa kimya, hakujua hata nani ni dereva. Akarudi kulala. Alikuja kushituka nje kunapambazuka. Bado wapo safarini. Akatulia akijaribu kutafakari, napo akapotelea usingizini mpaka akasikia kama anayeshushwa garini. Akafungua macho, akakutana na Malon, pembeni yake Bale. Naya alishituka sana. Kila alipotaka kujishika, mikono ikawa kama haina nguvu yakutosha. Akajihisi kama aliyelevya.

Malon akambeba mpaka ndani. Akamuweka kitandani. “Una njaa?” Malon akamuuliza. Naya akabaki akimwangalia pale alipokuwa amelala. “Acha jeuri Naya. Si unaulizwa wewe?” Akageuza shingo kumuangalia Bale aliyekuwa amesimama mlangoni. Akasikia maumivu ya shingo kidogo pale alipopigwa kabla hajapoteza fahamu. “Niko wapi?” “Hana njaa huyu. Mrudishe tena kulala.” Bale akaongea na kutoka. Malon akamchoma sindano iliyomfanya Naya ajisikie vizuri sana. Alijisikia utulivu wa hali ya juu. Hata majonzi na simanzi moyoni vikaondoka gafla. Ule uchungu wote moyoni nao ukaondoka kabisa. Hakuwa na maumivu popote pale. Si mwilini, si rohoni. Akafurahia ile hali. “Nahitaji kutumia choo.” Akasimama Malon akimwangalia. Hata usoni alionekana ametulia.

Malon akamuelekeza. Ilikuwa nje ya hicho chumba. Akajaribu kutembea, akawa anapepesuka. Mwili mwepesi mno! Akajicheka kilevi. “Nasikia kizunguzungu!” Akalalamika akiwa na tabasamu. Malon akamsaidia kwenda chooni. “Hapa ni wapi?” Akauliza tena, lakini safari hii sio kwa wasiwasi kama mwanzo. “Una wasiwasi gani, wewe tulia. Upo na mimi.” Naya akafikishwa chooni akakaa. Wakati akijisaidia, akili ikawa kama imemrudia.

“Joshua!” Akaita kwa sauti. “Usiniudhi Naya!” Malon akageuka na huo mkwara. “Mume wangu yuko wapi?” Malon alimpiga kibao mpaka akaanguka pembeni ya choo. “Nilikuonya. Sitarudia Naya. Acha kulitaja hilo jina.” Naya alikuwa ameshikilia shavu pale sakafuni akawa kama anayejaribu kuelewa. Malon akatoka na kumfungia mlango kwa nje. Kwa kuwa alikuwa hana nguvu, akabaki amekaa hapo ndani chooni, tena sakafu ikiwa na maji tu, akapotelea usingizini akiwa amekaa chini kabisa.

Kwa mbali akasikia akivutwa kama anayetolewa pale. Tena kwa kuburuzwa kikatili. Akaenda kuwekwa pembeni ya kitanda, akalala. Alikuja kuamka ikiwa imeshafika jioni. Yupo peke yake sakafuni, anatetemeka baridi yakupita kiasi. Akajitahidi kutoka hapo chumbani. Akajikokota mpaka nje kabisa alipoona mwanga wa mwezi na nyota angani, akajikuta yupo katikati ya mashamba na mapori. Naya akashangaa sana. Hapakuwa na nyumba isipokuwa hiyo tu. Giza nene isipokuwa huo mwanga wa angani. Akajaribu kufikiria akivuta kumbukumbu alipo au ni ndoto tu! Lakini kumbukumbu yakumuona Bale na kofi alilopigwa na Malon ikamjia. Akajishika shavu.

Mara akaona gari ikija. Akabaki amesimama. Kumbe alikuwa Malon. Akafika hapo na kuegesha gari yake akasubiri ashuke. “Huku ni wapi wewe Malon, na kwa nini nipo hapa!?” “Unakumbuka nilikuonya usiolewe na Joshua, kwakuwa bado nakudai?” “Unanidai nini!?” Naya akauliza kwa kumshangaa. “Muda na mapenzi. Sasa upo hapa kulipa. Hutaondoka hapa, mpaka nikuruhusu mimi mweyewe. Huruhusiwi kwenda popote, hapo uliposimama na nyuma ya hii nyumba ndio mwisho wako. Na ninakuonya, usinijaribu Naya. Hakika nitakuumiza.” Naya akashangaa sana.

“Umechanganyikiwa wewe Malon?!” “Wakati ukitumia pesa yangu na muda hukuona kama nimechanganyikiwa. Ulinifuata kila mahali bila kukuita. Ulikula vyangu kwa nguvu zote bila aibu. Nilikulisha na kukuvalisha kwa jasho langu, eti sasa hivi ndio unataka kunikimbia! Huwezi Naya. Mimi nina akili ya kuzaliwa, ndio maana hakuna aliyeweza kunifundisha darasani. Hapa umefika. Hutatoka wala hakuna atakayekutoa hapa. Unalipa fadhila. Anza kuzoea mazingira.” Naya akaangalia kulia na kushoto, akashindwa kujua alipo.

“Na hiyo hali unayojisikia, dawa yake ninayo. Nitakuwa nikikuchoma sindano yake, pale nitakapojisikia na utakaponifurahisha. Sasa kwa kuwa wewe ni jeuri, nakuacha mpaka uje mwenyewe kuomba.” Malon akampita pale alipokuwa amesimama. Akasikia harufu ya chakula. Akajua amerudi na chakula. “Ukichoka kusimama hapo nje, rudi ndani, chakula tayari.” Hapakuwa na kubembelezwa tena. Kamasi zilikuwa zikimtoka Naya, hana pakujifuta. Akashangaa na machozi yakimtoka huku akitetemeka. Maumivu yake yote ya shingoni na moyoni yakarudi vilevile.

Akarudi ndani maana baridi ilikuwa kali. “Hiyo baridi unayojisikia ni ya kutoka ndani kwako. Hakuna baridi hapa.” Malon akamwambia kwa kumkejeli. Naya akaenda kukaa kochini. Ilikuwa nyumba ya kawaida tu, lakini ilikuwa imekamilika. Naya akabaki akitetemeka baridi amejikunja kwenye kochi. Jinsi anavyojisikia, haikuwa kawaida. Akakimbilia chooni kutapika. Akatapika kwa muda, kisha akaamua kuoga kabisa na kurudi kulala.

Akamuona Malon amejiwekea chakula chake, anakula pale sebuleni. Akasimama na kufunga mlango ili asiione sura yake. Akaendelea kutetemeka pale kitandani  hata usingizi ukawa mgumu kuja. Baada ya muda akamuona Malon anaingia hapo chumbani na yeye anakwenda kuoga. Ila yeye alioga maji ya moto. Alimuona akiyachemsha hayo maji kwa kutumia jiko la gesi, alimuona kwa mwanga wa kurunzi kubwa aliyowasha mara baada ya kurudi. Alipomaliza kuoga, Naya akashangaa anaingia hapohapo chumbani alipolala yeye akiwa na taulo tu. Bila hata kuongea, Naya akashitukia anavuta shuka aliyokuwa amejifunika, kwa nguvu, akalitupia sakafuni na kuanza kumtoa nguo kikatili kama aliyekusudia kumuumiza. Akiwa amemuacha mtupu kabisa, anatetemeka baridi hapo kitandani, amkandamiza kwa nguvu, akaanza kumbaka. Alifanya kila kitu mwilini kwa Naya, kwa nguvu zake zote akimtizama bila kujali vile alivyokuwa akilia, mpaka akamaliza.

Baada ya muda akaamka na kwenda kutengeneza hiyo dawa. Akamuamuru Naya akaoge tena. Naya akatoka hapo kitandani akilia. Malon akawa anamcheka. “Wakati ukitaka pesa yangu, hata nilipokuwa nimekuudhi mpaka mwisho, ulipokea dhahabu zangu, na penzi ulikuwa ukitoa bila shida, eti sasa hivi ndio unajidai kulia! Acha wizi wewe!” Naya akajifungia chooni. Akaoga na kutoka akiwa na hali mbaya sana. Maumivu ya kubakwa na mengineyo. Malon akarudi na kumchoma sindano. Taratibu Naya akaanza kusikia furaha. Utulivu wa namna yake hata mawazo yakaanza kutulia. Hapo napo Malon akapata mchezo mwingine. Tena safari hii bila ukinzani. Naya alitulia tu wakati akibakwa. Aliyafanya yote atakayo mpaka akamaliza, Naya hana habari.

Bahari Imechafuka.

Asubuhi aliamka akiwa mchovu. Akabaki amejilaza tu hapo kitandani. Wazo likamjia lakutoroka. Akatoka kwa haraka, hakukuta gari ya Malon ila kijana ambaye ni mgeni kabisa kwake. Naya akamuwahi. “Naomba nisaidie simu nimpigie mume wangu. Malon ameniteka nyara. Amenifungia hapa.” Huyo kijana akabaki kimya akimwangalia vile kamasi zilivyokuwa zikimtoka Naya na akitetemeka baridi. “Nisaidie kaka yangu. Mume wangu atakupa pesa yeyote utakayotaka, atakupa.” Huyo kijana akatoa simu. Naya akafurahi sana akijua anampa yeye kumbe anampigia Malon.

“Ameamka. Ila anaomba simu ampigie mtu anayemsema kuwa ni mume wake, na amesema mumewe ni tajiri, atanipa pesa ninayo..” Hapohapo Naya akakimbilia ndani na kujifungia. Hazikupita dakika 10, Malon akawa anaegesha gari nje. Alikimbilia ndani kama mwehu. “Fungua mlango Naya, nitakuua.” Baada ya vitisho vikali Malon akigonga mlango kwa nguvu, Naya akafungua mlango wa chooni akilia kwa hofu. Alimvuta kumtoa pale chooni na kuanza kumpiga. Kile kipigo alichoona na kusimuliwa huwa anawapiga wafanyakazi wake, siku hiyo Naya alikipata. Alimpiga Naya kama mwizi. Alimpiga bila kuchoka mpaka aliporidhika akamuacha. “Nilikuonya, na narudia tena. USINIJARIBU. Maana wakati nahangaika na wewe, na Joshua naye alikuwepo hapa duniani. Lakini sikumsikia. Narudia kukuonya Naya. Usinijaribu.” Malon akatoka.

Naya alishindwa hata kujigeuza pale sakafuni. Alikaa hapo baridi ya sakafu ikimpiga siku nzima bila hata chakula mpaka usiku kabisa ndipo Malon akarudi. Hakumuona tena Bale. Akashindwa kuelewa alipo kaka yake kwani ni kama walionekana wapo pamoja. Malon alimpita hapo chini sakafuni. Akajitayarishia maji, akaenda kuoga na kurudi kukaa sebuleni. Alianza kula bila kumuongelesha Naya. Naya akabaki hapohapo sakafuni. Mpaka Malon akamaliza kula, akaenda kulala na kumuacha hapohapo sakafuni akitetemeka, Naya asijue kama ni baridi au hali inayompata mpaka apewe sindano. Kabaki hapo sakafuni akishindwa hata kusogea ila kugugumia asiamini kinachomtokea.

Bale.

Mahusiano ya Malon na Bale yalibadilika. Ni kama Malon akampandisha cheo Bale akawa msimamizi badala yake na safari hii wafanyakazi wote wakajua kama Bale ni msimamizi mkuu wa Malon. Hata safari hiyo aliyo mfanikishia kumletea Naya nyumbani, alimpa safari ya kwenda Dubai kupokea mzigo waliokwisha safirisha huko na akawa amemtambulisha kwa wenyeji huko nchini Dubai kuwa wamsaidie kama yeye.

Bale aliyekutana na Naya wa safari hii alikuwa mambo safi. Pesa ipo kwani alishafundishwa biashara iliyomsaidia Malon kutoka kwa haraka, mwanzoni kabisa wa maisha yake mpaka kuja kumfunga jela na Naya kumtoa. Kuuza bangi ila sasa yeye Bale  akajiongeza na mirungi pia. Malon akamfundisha jinsi ya kuuza kwa akili bila kukamatwa kirahisi. Na kwa kuwa alionekana ni jasiri na anao moyo wa kuthubutu, Malon akamtia moyo kuwa atafanikiwa kwa haraka sana.

Bale akaweka juhudi. Akayajua masoko yake kwa haraka. Na kweli ilikuwa ni biashara inayolipa papo kwa hapo. Nipe bangi au mirungi, nikulipe. Ndani ya juma moja, akaunti za Bale zikaanza kusoma namba zinazoeleweka. Hilo likamfurahisha sana Bale kuona pesa imeweza kuingia kwa haraka kwa kiasi hicho! Ikamsogeza karibu zaidi na Malon. Hapakuwa na kitu Malon anamwambia, Bale anakataa. Akaweka heshima zaidi kwake.  Na ni Malon huyohuyo kwa mara ya kwanza anamtoa nchini, tena kibiashara!  Hilo likamfurahisha zaidi Bale. Ujasiri wa pesa ukachipuka ndani yake. Bale aliyekuwa na maono ya kuwa na pesa nyingi, akaona tumaini jipya. Akaelekea nchini Dubai kwa biashara halali ya Malon huku ile yale haramu, ikiendelea nchini. 

Kwa Naya na Malon.

Wakati kaka yake akifurahia mafanikio yake bila kujali lolote, huku kwa dada yake  fungate ya kibabe ikaendelezwa na Malon. Baada ya kile kipigo kibaya na cha kikatili alichokipata bila huruma kutoka kwa Malon, Naya alibaki pale sakafuni usiku huo mpaka kesho yake nakushindwa kutoka hapo kabisa. Alijisikia mdhaifu wakupitiliza. Maumivu yakupita kiasi mwili mzima, akabaki akigugumia peke yake. Asubuhi Malon aliamka na kumpita hapo kama hamuoni. Akajitengenezea chai, akanywa peke yake, akamuacha Naya amelala palepale sakafuni, hakumsemesha na Naya naye hakuwa amelala, ila tu akimsindikiza kwa macho kila anapokwenda.

Alitoka na kumuacha hapo sakafuni, Naya hakuomba dawa.  Mchana napo akarudi na chakula. Naya akafungua macho, akamuona anakula macho kwenye simu. Akala alipokaribia mwisho akamuangalia Naya, akakuta ametulia tu amejikunyata hapo sakafuni. “Kama unasubiri kubembelezwa, jua kipigo kingine kitakufuata nikikukuta hapo jioni nikirudi.” “Sikuogopi Malon, na hunitishi.” Naya akajibu akitetemeka sana. “Unasemaje Naya?” “SIKUOGOPI.” “Nitakuumiza Naya!” “Huna uwezo wakuniumiza Malon. Huna. Na kama unahesabu kunisulubisha huu mwili wangu ndio kuniumiza, basi nakuhurumia wewe.”

“Naya utalia wewe!” “Mpuuzi tu wewe. Utamtisha nani? Huna akili ndio maana umekimbia shule. Huna uwezo wakufundishika. Kichwa chako kimejaa maji matupu ndio maana umeshindwa hata kukaa kanisani kujifunza neno la Mungu tu. Huna uwanaume wa kweli kama Joshua wangu, ndio maana umerudi kutisha watu. Kwa kuwa unajua bila...” Malon akasimama pale na kuanza kumpiga mateke. Safari hii Naya akawa anamcheka huku akificha maeneo ya tumbo kwa kujikunja kabisa, magoti mpaka kifuani. Mwishoe Malon akaondoka.

Kwa Bale.

Baada ya safari yake ya Dubai, huku dada yake akitumikia kifungo cha Malon mchana na usiku tena bila chakula cha kutosha, Naya akimvizia akiondoka ndipo ale makombo kama yalibaki, Bale akamfuata Geb siku hiyo ofisini kwake. Akasubiria hapo nje ya ofisi maana sekretari alimwambia yupo na mgeni. Baada ya muda wake aliopanga yeye Bale wa kusubiria kupita, akahesabu anapuuzwa, na kudharauliwa. “Acheni dharau jamani! Hata sisi tuna majukumu yetu na ofisi vilevile. Nimekaa hapa muda wote, huyo Geb hatoki kwa lipi mno!” Bale akaanza kupayuka. Akaongeza sauti kwa nguvu ili hata wa maofisini wasikie.

Askari akaingia. “Kwema?” “Muulize huyo.” Bale akajibu. “Anataka kumuona Magesa. Nimemwambia yupo na mgeni, asubiri. Hata dakika kumi hazijapita, anaanza kelele!” “Kwani unayo miahadi.” “Sina. Nimekuja kumdai Magesa mali yetu. Aache dhuluma. Anatuonea kwa sababu anaona mzee wetu hayupo..” Geb na  Nanaa wote wakatoka maofisini kwao kwa wakati mmoja.

Geb akabaki akimtizama akiwa amekunja uso. “Nataka hati yetu ya nyumba yetu ya Kiluvya.” Geb akamtizama kwa sekunde kadhaa, kisha akamuuliza. “Wewe unaidai kama nani?” “Mrithi wa mzee.” “Wewe sio mrithi wa kile kiwanja cha Kiluvya. Ila Naya. Baba yako aliacha kwa maandishi hapa kwangu, tena mbele ya mwanasheria akiwepo.” “Kile kiwanja kilikuwa mali ya mama wala si baba. Mama aliko..” “Tafadhali subiri nimalize. Usiniingilie ninapo zungumza.” “Utanifanya nini?” “Nitakutoa hapa vibaya sana na hutaruhusiwa kurudi tena hapa. Na siku nyingine unapokuja hapa, hakikisha unaongeza nidhamu kwa kila unayemkuta hapa. Unanielewa Bale? Maana kama haupo tayari kunisikiliza mimi, sitaki upoteze muda wangu. Unanielewa?” Geb akawa mkali kabisa.

“Wewe si umesema na wewe unayo majukumu na ofisi, basi inamaana unaelewa juu ya uthamani wa muda. Usirudi hapa bila Naya ambaye ndiye mwenye kiwanja kwa sasa. Yeye ndiye atakayeidhinisha kupewa wewe hiyo hati na si vinginevyo. Hujaridhika na hilo, nenda kashitaki popote maana mirathi ya baba yenu ipo hapa. Na urudi na pesa yangu tasilimu kwa kuwa ndio yalikuwa makubaliano yangu na baba yako, tena kwa maandishi. Kama hujaelewa, nikusaidie kwa kifupi. Mambo mawili. Hati ni ya Naya. Sitatoa hati kwa mwingine yeyote isipokuwa Naya mwenyewe awepo hapa na asaini mbele yangu na mwanasheria kuwa amekukabidhi wewe hiyo hati. Na pesa yangu yote.” Akamtajia kiasi cha pesa anachomdai baba yao. Bale akapoa.

“Kama huna swali, askari huyo hapo atakusindikiza nje. Na kama unaswali uliza.” Taratibu tu ila akiwa ameweka sura ya kazi. Akamkazia macho Bale. Nanaa kimya akimtizama Bale. “Nitarudi.” Bale akajibu na kutoka.

Huku Kwa Naya Mwenye Mali.

Siku moja jioni Malon akarudi akamkuta Naya amelala kitandani anatetemeka kupita kiasi. Hali mbaya kwelikweli kama teja aliyezidiwa haswa kwa mwili kukosa madawa. “Wewe si unajidai jeuri? Sasa sikupi dawa.” “Ni afadhali nife, kuliko kukuomba wewe mshenzi tu. Nahisi unanipa madawa ya kulevya, unataka niwe teja lako! Hakika bora kufa kuliko na mimi niwe kama wewe. Tena hata nikizidiwa, nikakuomba, usinipe. Jichome mwenyewe madawa yako yakulevya. Tumia bangi na madawa, vyote. Ila sio mimi. Hutanigeuza teja.” Malon akamcheka akimsogelea. “Kwa taarifa yako tu, umeshakuwa teja ni vile hujajiona ulivyo sasa hivi. Mbovu kuliko teja la mtaani! Unatokwa mikamasi na jasho kama teja tu. Sasa kaa na hiyo hali ukijua nimekuweza. Na unakumbuka wakati ukikimbia siku ile nilikuhakikishia nitakukamata tu, ukadhani mwanaume wako ataweza kukuficha kwangu?” Akamuuliza kwa kumkejeli huku akivua nguo zake Naya akimwangalia.

 “Yuko wapi sasa hivi?” Naya kimya. “Nimebaki mimi kukutumia nitakavyo.” Akamvuta pale kitandani akamvua nguo kwa nguvu, akaanza kumbaka huku amemshika kikatili. Naya akaanza kumcheka. Malon hakujali mpaka akamaliza. Naya akakaa pembeni ya kitanda akajifunika shuka bado akitetemeka, akaanza kumcheka tena.

“Huwa nafikiria Malon.” Malon akamwangalia. “Usinipige kwanza. Nisikilize tu.” Naya akawa anacheka kilevi. “Nafikiria kama Mungu angekupa wewe, nusu ya Joshua, sijui ingekuaje!” Malon akamrushia teka. Naya akazidi kucheka. “Mwanamke mmoja tu, mpaka ukanivutie bangi ndio uweze kunilala! Tena hata hujui unachofanya! Unafanya fujo za kupitiliza hapa mpaka upate bao, upo hoi!” Malon akakaa kwa hasira.

“Kama hapo unajiandaa kunipiga kwa kuwa huna uwezo wa hoja, mshenzi na mjinga wewe. Huna akili Malon ndio maana hata wewe mwenyewe unajijua huwezi kufanya kitu bila bangi. Huwezi kumlala mwanamke bila bangi. Huwezi kuishi na watu una...” Naya alishitukia kibao cha nguvu usoni akatema damu akicheka. “Mjinga tu wewe Malon. Huna lolote na huwezi kumiliki chochote.” “Mbona nilikubikiri wewe?” Naya akacheka sana.

“Nilikuwa nikikuchezea nitakavyo!” “Ni wewe au bangi? Huna uwezo huo wewe na wote tunajua. Si ulijaribu kuacha bangi ukashindwa kuwa kama wanaume wengine wanaoishi na uwezo waliojaliwa na Mungu! Au akili yako ndogo imesahau wewe ni nani!?” Naya akamuuliza akimkejeli. “Kaa na wanaume wenzio kama kina Joshua wanaojua kumuweka mwanamke kitandani, wakufundishe. Anakuweka kitandani lisaa, mchezo hauchoshi! Mwanaume hatokwi jasho! Hafanyi mazoezi kama wewe wala havuti bangi na mchezo mrefu anauweza. Wewe ukitolewa bangi hapo, hamna kitu. Unatukana mchana na usiku na kuhesabia watu vitu sababu huna akili. Na hata ukirudi shule wewe, akili yako haina akili utafeli tu wewe, mpumbavu wa mwisho. Fala wa mafala tu wewe Malon. Hata kanisani umeshindikana mtoto wa shetani.” Malon alimrushia teke la nguvu lililomtoa Naya kitandani, akagonga kichwa kwenye ubao wa kitanda, kisha akatua sakafuni, kimya. Malon akaondoka.

Bale Kwa Naya.

Huku kwa Bale alipotoka tu ofisini kwa kina Magesa akaanza kuzungukia biashara yake haramu hapo jijini. Akakusanya pesa na yeye akasaidia vijana wake hao wawili wanao msaidia kuuza, akitaka apate pesa ya Magesa kwa haraka. Akafanya juma zima mfululizo bila kupumzika, akafanikiwa kupata kiasi kikubwa tu cha pesa. Akawaongezea mzigo vijana wake wanao mfanyia biashara, yeye akaondoka jijini kurudi alikomtelekeza dada yake.

Aliadhimia kujenga nyumba nzuri sana nyumbani kwao Kiluvya, yeye kama Bale akitaka kutoa kumbukumbu ya baba yake kabisa pale, ubaki mji wake yeye. Kwa kuwa alikuwa na moja ya gari la Malon, hakusimama hovyo njiani. Aliendesha mpaka usiku mwingi sana. Akafikia hotelini kama kawaida yake. Hataki tena shida, Bale maisha yamembadilikia. Akamtumia ujumbe Malon. ‘Nakuja kukuona kesho. Nataka kuzungumza na Naya.’ Malon alipopata tu ujumbe, akatoka hapo baa usiku huo haraka kurudi alipomuacha Naya.

Alichofanya Malon baada yakumkuta anapumua pale sakafuni, ni kumvalisha tu nguo na kumrudisha kitandani, akamfunika na kumuacha hapo. Akajilaza na yeye pembeni. Asubuhi akaamka na kutengeza kifungua kinywa mpaka cha Naya. Akaona Naya haamki. Akaenda kumtoa pale kitandani kwa nguvu na kumuweka sebuleni. Naya akaamka, akamtizama kwa kumshangaa. “Kunywa chai.” Naya akamwangalia tu. “Wewe Naya?” Malon akamuita kwa ukali kidogo. Kimya. “Nimekwambia kunywa chai, Naya, acha kiburi!” Akawa kama anamtisha lakini akawa kama hamuelewi anachoongea. Akaiangalia ile chai, akajirudisha nyuma ya kochi, akapandisha miguu akajikunyata.

Bale naye akawa anaingia. “Vipi huyu?” “Amegoma kula.” Bale akamwangalia pale alipojikunyata. Akafikiria kidogo akaona asimpoteze malengo. “Naya, nataka hati ya Kiluvya. Magesa anasema hawawezi kunipa mpaka wewe ukaidhinishe, na niwalipe.” Malon akashituka sana kusikia Bale anazungumzia habari za kina Magesa ambao ni kama Joshua! “Ati nini!?” Akauliza Malon kwa kuhamaki. “Nataka hati ya kiwanja cha Kiluvya kwa jina langu mimi na si Naya. Kumbe mzee alikopa pesa ya biashara kwa Magesa, akaweka kiwanja cha mama yangu rehani mpaka alipie. Sasa mimi nataka nikilipie. Ila siwezi kulipia kiwanja ambacho bado hakijawa changu! Twende tukaandikishane mbele ya huyo Magesa. Kuwa nitamlipa mimi kwa awamu, na baada ya kumaliza pesa yote, kiwanja kinakuwa changu sio cha Naya ambacho ni kama cha Joshua tu. Maana Joshua anaweza kuja kukidai na kisheria yeye kama mume wake huyu kihalali, akashinda na kuchukua jasho la mama yangu hivihivi! Hakika sikubali.” Naya kimya. Malon akabaki akifikiria.

“We Naya?” Bale akaita kwa ukali. Naya kimya amejiinamia. “Hakika tunakwenda Naya. Kile kiwanja  ni jasho la mama. Najua wazi mama angetaka mimi ndio niendeleze ule mji sio uishie kwako ambapo itakuwa ni kama mama alimnunulia Joshua! Hakika SIKUBALI. Baba na akili zake mbovu asizoweza kufikiria mbali, anakukabidhi wewe kiholelaholela tu! Twende.” Akamvuta Naya kumtoa pale kitini. Akaanza kulia maumivu kuwa anamuumiza. “Simama sasa!” Bale akamuamrisha Naya.

“Subiri kwanza Bale. Yaani unataka kuondoka naye sasa hivi!?” “Hili zege halilali. Nakwenda kushugulikia haki yangu, nakurudishia mwanamke wako.” “Haiwezekani Bale!” “Hakika INAWEZEKANA Malon. Na ninaondoka naye sasa hivi. Katika hili hakuna mjadala. Kesho asubuhi kama leo nitakuwa nimefika Dar, nataka nikawekane sawa na Geb. Kesho hiyohiyo namrudisha. Kwanza wala usiwe na wasiwasi. Jinsi nilivyokuta hali kule, hakuna yeyote anayemtafuta huyu. Wote wanaendelea na maisha yao kama kawaida. Hakuna anayemtaka tena. Kwanza yeye mwenyewe nikimwangalia ujanja wote umemuishia!” Bale akaongea kwa kumkejeli dada yake. “Muone alivyo! Kwisha habari yake! Huyu utakaa naye mpaka uchoke wewe, umfukuze. Wewe usiwe na wasiwasi.” Bale akatoka na dada yake kwa hasira sana bila kutaka kutoa nafasi ya mjadala kwa Malon. Akamuingiza kwenye gari, kiti cha nyuma, safari yakurudi Dar tena ikaanza.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Naya alilia maumivu huko njiani mpaka akalala, bila hata kuongeleshwa na Bale. Ila Bale alipokuwa akitaka kupiga simu zake alikuwa akimwambia apunguze sauti, kisha kuendelea kuzungumza na simu zake bila kumjali, mpaka akalala. Kilichomshangaza Bale ni pale alipomuamsha na kumwambia Naya ashuke akajisaidie, Naya akawa hajui hata kama anaitwa Naya na hamtambui yeye ni nani kabisa. Bale akaanza kwa ukali akidhania anamchezea akili, lakini akagundua pia yupo kama teja!

Akampigia simu Malon. “Ulikuwa ukimpa nini huyu, mbona amekuwa kama teja!?” “Janja yake tu huyo, ili asikupe haki yako. Wewe humjui Naya nini! Anatumia kila njia kujinufaisha. Akishapata anachokitaka ndio anaanza michezo yake hiyo. Sasa wewe usipomkazania, ujue inakula kwako.” Malon akamkatia simu.

Bale akamuacha hapo garini. Akaenda kula na kujisaidia akarudi garini, safari ikaanza tena. Naya hakuwa amekula muda mrefu. Mwili unamuuma kwa njaa, maumivu ya kupigwa na kubakwa mfululizo. Akalia tena mpaka akalala. Alikuja kuamshwa na Bale usiku kuwa wamefika, ashuke garini. Naya akabaki anashangaa haelewi. Bale akamvuta mpaka ndani. Ilikuwa nyumbani kwa Malon, Kunduchi. Bale alikuwa akipatumia kila awapo hapo jijini Dar, kama kwake tu mpaka walinzi wote walishamjua. Akamuingiza ndani na kumuacha, yeye akatoka kuzungukia dili zake hapo mjini, usiku huo.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kwa kuwa yeye mtoto wa jiji, Bale alizaliwa jijini Dar, mtoto wa uswahilini tu. Akakua akicheza na wajanja wa mtaani. Akasoma jijini pia. Basi hapakuwa na kona ya jiji hilo asipofahamu. Akafanya biashara yake vizuri tu akifuata ule ushauri wa Malon. Hata kama biashara itakuwa kubwa kwa namna gani, alimuonya asiongeze wafanyakazi zaidi ya hao wawili tu, watakao mfahamu yeye. Wabakie hao wawili tu wanao mfahamu yeye kama mwenye mali. Akamwambia kwanza itamsaidia kuwaongoza vizuri na kwa urahisi, na pia kuepuka kukamatwa. Ila akamwambia kama wao watatafuta watu wakufanya kazi chini yao, kusaidia kusogeza mzigo kwa haraka, basi wasimjue yeye na yeye asiwafahamu. Iwe juu ya hao watu wake wawili. Hilo likakaa sawa. Bale akawa bosi wa mabosi, vijana wa mtaani.

Na japokuwa alikuwa ndio ameanza tu hana muda mrefu, ila ikawa ni biashara inayomuingizia pesa hapo jijini na kuonyesha tumaini kubwa sana kwa Bale. Kwani alifanya akiwa anatumia uzoefu mkubwa wa Malon. Kwa hiyo hapakuwa na makosa. Harufu ya pesa ikawa inanukia mifukoni mwake.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alirudi usiku mwingi sana, dada yake bado akilia maumivu. “Vyovyote unavyotaka kujiaminisha, mimi sijali. Uwe teja, mgonjwa, hiyo ni juu yako. Ila nakutaka kesho uwe umetulia, ukazungumze kule kwa kina Magesa, nipewe haki yangu.” Bale akalala bila kujali.

Mungu Hutumia Yeyote Na Chochote Kufanikisha Jambo Lake.

Asubuhi na mapema, Bale akamtoa Naya hapo nyumbani. Tena kwa kumlazimisha achane nywele na kuosha uso. Akamsukumia huko bafuni, akaona anampotezea muda kwani Naya aliendelea kulia tu. Akatoka naye vilevile Naya akiwa na nywele zake zilezile alizokuwa amesukwa sababu ya harusi. Alisukwa nywele ndogondogo. Ila alisukwa chini tu, juu zikawa zimeachiwa. Kwa hiyo akawa na nywele ndefu ila hazikuwa zimekaa vizuri, zimefungana sababu hazikuwa na matunzo hata ya kuchanwa tu tokea atolewe saluni siku kaka yake amemfuata akiwa na Malon.

Njia nzima Bale alikuwa akimwambia Naya kwa kurudiarudia kitu anachotakiwa kwenda kuzungumza kwa kina Magesa. “Ukiharibu Naya wewe, utalia mara mbili ya hivyo.” Bale akamtisha huku akiendesha mpaka kwa kina Magesa. Akamtaka ajifute uso na nguo yake na akamwambia aache kulia. Baada ya kutulia kwa vitisho vingi ndipo wakashuka garini akimkumbusha chakuzungumza na kumuonya asikosee. Safari hii Bale alifika kwa kina Magesa bila ugomvi. Akaomba kuonana na Magesa mwenyewe.

Baada ya muda akaambiwa aingie. Akaingia na Naya. Geb alishituka sana alipomuona Naya. “Hujambo Naya?” Geb akamsalimia, lakini Naya kimya. Akabaki amekalia mikono yake akifuta kamasi na jasho kwa mabega yake huku akitetemeka. Geb akashangaa sana.

“Sitaki kukupotezea muda. Nataka kulipa pesa yote unayomdai mzee. Ila kwa awamu tatu au nne. Ila sitalipa mpaka tuandikishane kwamba nikilimaliza hilo deni, mimi ndio utakayenikabidhi hiyo hati ya kiwanja changu.” “Ni cha Naya, na wakati mzee akizungumza hivyo mbele yetu na wewe ulikuwepo Bale. Kwa nini unataka kufanya fujo sasa hivi!?” “Mimi sifanyi fujo. Kiwanja ni cha mama yangu. Mimi nimebeba jina la ukoo. Pale lazima nipaendeleze mimi mtoto wa kiume, hata mama mwenyewe ndivyo angetaka hivyo. Tatizo la mzee hakuwa na uwezo mzuri wa kufikiria. Anakwenda kumpa mtoto wa kike urithi wa famiia ili akiolewa huko kikapotelee kwa mwanaume wake?!” “Naya alishaolewa na wala mumewe hajataka kiwanja chake!” Geb akaongea akimshangaa sana Bale.

“Nisikilize bwana Magesa. Mambo ya familia yetu wewe hayakuhusu. Uliniambia unamtaka Naya aje akiri tena kwa maandishi kuwa kiwanja ananikabidhi mimi, nimemleta Naya huyu hapa. Sijataka kesi ila kufuata ulichonishauri. Naomba tumalizane. Nikulipe pesa awamu ya kwanza, nitamalizia zingine.” “Sawa. Subirini chumba cha mkutano. Huyo dada hapo atawapeleka. Nataka kuandaa karatasi na kumuita mwanasheria. Tusifanye mambo kiholela.” “Itachukua muda gani?” “Si mrefu.” Geb akanyanyua simu nakumtaka sekretari wake aingie hapo.

“Naomba waonyeshe chumba cha mkutano na uwahudumie chochote wanachotaka.” “Sawa.” Muda wote huo Naya alikuwa kimya tu akitetemeka. “Twende sasa. Unatetemeka nini, wakati nimekupa sweta?” Geb akabaki akimwangalia vile Bale anavyozungumza na dada yake. “Wewe Naya?” Bale akamvuta kwa nguvu, Naya akaanza kulia. “Unaniumiza!” Naya akalalamika akilia kama mtu asiye na akili vizuri. “Twende sasa.” Bale akamsogezea kiti ili apite. Geb akashangaa sana ila akanyamaza mpaka walipotoka.

Kwa Joshua.

Hapohapo akampigia simu Joshua. “Kwema GM?” “Hapana. Hapa tunapozungumza, Bale na Naya wapo ofisini kwangu.” Joshua akashituka sana. “Naya!?” “Ndiyo. Lakini si Naya unayemfahamu wewe.” “Unamaamisha nini?” “Hayupo sawa. Na kwa jinsi nilivyomwangalia na kumsoma kwa harakaharaka, sidhani kama anajitambua kama ni Naya. Nikimaanisha hata kujua jina lake kama ni Naya, nadhani hajui, kitu ambacho ninauhakika Bale hajajua kama dada yake hajitambui.” “Sijaelewa GM!” Geb akamsimulia kwa vile alivyomuona Naya, na kwakuwa walishazungumza tokea juzi yake juu ya ujio wa Bale pale ofisini kwake akiomba hati, Joshua akaumia sana.

“Upo Joshua?” “Nipo kaka. Nipo.” “Mimi naamini ulichosema ndicho kinachoendelea. Japokuwa polisi walikukatalia juu ya kuandishisha kesi yake wakisema Naya hajatoroshwa kwa kuwa aliaga kabisa, lakini mimi naamini. Hivi nilivyomuona, siye Naya aliyekuandikia ujumbe. Ule ujumbe uliandikwa.” “Nisaidie GM, ndugu yangu. Nisadie kaka. Nimekwama kila mahali! Nimemtafuta mke wangu nakaribia kuchanganyikiwa!” “Hapa kuna mchezo nataka kumchezea Bale, hatajua. Subiri nimpigie simu mwanasheria.” “Na mimi nakuja, japo nimuone kwa mbali tu.” “Sawa.” Geb akamkubalia na kukata simu. Hapohapo Joshua akakimbilia Ubungo zilipo ofisi za Magesa akitokea ofisini kwake bila hata kuaga.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya nusu saa Geb, mwanasheria na kabrasha wakaingia hapo chumba cha mkutano. Naya alikuwa ameegemea meza. “Naitwa Mangui, ni mwanasheria. Nipo hapa kumuwakilisha Magesa, na bwana Denis ambaye ni marehemu. Ninayo hati ya eneo lake lilopo Kiluvya, mirathi, na mkataba aliongia na bwana Magesa.” “Kwanza nashangaa ni kipi kilichompelekea kumwachia Naya! Mimi amenishangaza sana! Lakini naomba tuokoe muda. Naya aliyeachiwa huyu hapa, na yupo tayari kunikabidhi mimi. Wewe Naya?” Bale akamuita, lakini Naya hakuitika. Akamtingisha. Naya akanyanyua kichwa kamasi mpaka mdomoni.

“Jifute wewe, acha ujinga!” Naya akabaki akimuangalia. “Nimekwambia futa kamasi.” Akamsukuma kidogo, Naya akawa kama ameelewa kama ni yeye. Macho yalikuwa mekundu sana. Bado anatetemeka. Akajifuta kwa mikono. “Ona lilivyo chafu! Sasa utashikaje kalamu?” Akamsukuma kwa nguvu Naya akaanza kulia. “Unaniumiza!” “Ongea sasa.” Bale akamuamrisha, lakini akawa kama hajaelewa. Akabaki akijifuta machozi.

“We Naya?” “Subiri kwanza bwana Bale. Naomba twende taratibu.” “Nina majukumu yangu!” Akajibu kwa kiburi. “Basi rudi siku utakayokuwa na nafasi. Lakini mambo lazima yaendeshwe kitaalamu ili hata kama ukitoka hapa hujaridhika, huko utakapokwenda kushitaki uwe na habari kamili unazoelewa. Unanielewa?” Mungai akamuuliza. “Basi changamka. Mimi nataka haki yangu leo. Sitaki dhuluma.” “Basi tumeshakusikia. Naomba kuzungumza na Naya, mwenye mali.” “Mali ni ya mama yangu.” Akakanusha Bale. “Ila kwa sasa ipo kwa jina la Naya.” Mungai akamsahihisha Bale na kumgeukia Naya. Geb kimya akiwaangalia na kusikiliza.

“Naya?” Akamuita lakini Naya akabaki kimya akijisafisha uso huku akilia taratibu. Akajaribu kuita tena, ila safari hii kwa majina yake yote mpaka la baba yake, lakini Naya hakuitika. “Una nini wewe Naya? Tulikubaliana nini!?” Bale akamkaripia dada yake. Naya akamwangalia kwa hofu kubwa kama anayejihami asimpige. “Nazungumza na wewe, na naomba umjibu huyu mwanasheria sijui, nani! Mgeukie.” Naya akamgeukia akilia.

          “Unaelewa tunachozungumza?” Mungai akamuuliza Naya, lakini akabaki akimwangalia akitetemeka. “Mjibu!” Bale akamuamrisha. Naya akatingisha kichwa kukubali. “Nitajie majina yako yote matatu.” “Kunywa hayo maji mbele yako kwanza.” Geb akamwambia taratibu. Naya akayaangalia, kisha akanyoosha mkono akitetemeka sana. Akanywa yote kama aliyekuwa na kiu kali. Akamaliza. “Sasa tulia uzungumze.” Bale akamuamuru tena.

          “Nisawa kama ukiacha mimi nikazungumza naye?” “Naona anajifanya mjinga wakati jeuri kama yeye hakuna! Okoa muda Naya.” “Haya. Naomba majina yako yote matatu yanayoonekana kwenye vitambulisho vyako.” Mungai akaongea akimwangalia yeye. Naya akaonekana kufikiria kisha akasema. “Joshua.” Alitamka akivuta kamasi huku akijifuta. “Hilo ndilo jina lako!?” Naya akatingisha kichwa akikubali huku akijifuta. “HAA!” Bale akahamaki. “Kwamba leo wewe unaitwa Joshua!?” Bale akamkaripia kwa nguvu Naya akamwangalia akiwa amekunja uso, kama anayemshangaa yeye.

          “Ujue Naya wewe unanichezea akili na sikubali! Sema jina lako.” Naya akaanza kulia. “Naomba nikazungumze naye, kisha tutarudi.” Mungai akataka kumkatalia, Geb akasema wao ndio wawapishe pale. Wakaacha kila kitu mezani, wakatoka. Walipotoka tu wakaanza kusikia makofi, Naya akaanza kulia kwa uchungu sana. “Unaniumiza mimi. Unaniumiza.” “Wewe tokea lini unaitwa Joshua, kama si makusudi tu! Yaani uitwe jina la mwanaume!? Bora ungetaja la kike! Hayo ni makusudi na sikubali.” Akasikika ni kama anampiga tena, Geb akarudi kwa haraka. Kisha akaingia na yule mwanasheria.

          “Acha kumuumiza dada yako sababu ya mali, Bale!” “Kama wewe unaona kitu kidogo mbona hunipi, unanizungusha tangia juzi?” “Hata kama bwana Magesa atataka kukupa, haitawezekana kwa sababu haya mambo baba yako hakutaka yaendeshwe kiholela. Alinilipa kwa hili ninalofanya. Sasa kwa kifupi tu, endapo Naya atashindwa kunitajia majina yake yote matatu niliyo nayo mimi na yanayoonekana kwenye kitaambulisho. Na kueza kujibu maswali yangu yote nikaridhika, siwezi kuidhinisha mkataba mwingine, kwakuwa tutakuwa tunaingia mkataba na mtu ambaye hayupo kwenye fahamu zake sahihi. Yaani hana akili timamu, na kisheria sio sawa. Hairuhusiwi. Anaweza kurudi kesho, akavunja mkataba kabisa akidai leo hakuwa kwenye akili yake timamu, na kisheria akashinda.” “Hawezi kurudi huyu.” Bale akaongea akimdharau dada yake.

          “Hayo unaongea wewe, sasa hivi kwa kuwa unaharaka, unataka mambo yaishe. Mimi sifanyi kazi kiholela. Nendeni mkakae na kuzungumza tena, ndipo mnitafute. Kwa heri bwana Magesa.” Naya alikuwa akiendelea kulia pale alipokuwa amekaa huku anajificha uso.

“Naya una roho ngumu wewe! Kweli unanikatalia haki yangu! Hakika utanipa tu. Twende.” Akamuamuru, Geb akiwatizama. “Nimekwambia simama.” Akamnyanyua kwa nguvu sana. Naya akazidi kulia. Akamsukuma kumtoa mlangoni. Naya mbele, kaka yake nyuma akimsukuma kumtoa hapo. Alipomtoa tu kwenye hicho chumba akimsukuma kikatili, Naya akajikojolea akilia. “Haa! Unajikojolea kama jinga wewe!?”

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment