Kwa
haraka Geb akatumia akili akitumia hofu ya Bale. “Sera. Niitie askari polisi
hapo nje ili awasaidie hawa.” “Nisikilizeni. Sitaki kesi, nataka haki yangu.”
“Ndio hiyo unataka kupewa. Sera, mwite askari.” “Sasa mnaniitia askari wa nini!?”
“Kwanza upo na mke wa mtu kimakosa. Yupo na wewe akionekana kabisa si kwa matakwa
yake na hayupo kwenye akili zake timamu. Anaonekana ni mgonjwa na anahitaji
msaada wa haraka ambao wewe huonekani kama upo hata na mpango wa kumsaidia ila
kutaka yeye asiye na akili timamu, ndio akusaidie.” Geb akazidi kumtia hofu.
“Anaakili
timamu sana tu! Mbona wakati yeye na baba wakinitenga kwenye familia mbona Naya
alisikika vizuri sana?” Bale akajibu kwa uchungu sana akionekana na hasira.
“Hivi wewe Bale unajua kama baba yako alikufa mgojwa kwa sababu yako?” Bale
akamgeukia Nanaa kwa hasira na wasiwasi kidogo. “Baba yako amekufa akikutafuta
Bale.” “Huo ni unafiki kabisa. Nimeyasikia majibu yake yote alipokuwa akiambiwa
jinsi ya kunipata, na kukataa! Alinitoa kwenye familia yake kabla hajafa!
Amekufa kwa yake mwenyewe.” Bale akajibu kibabe.
“Basi
kwa taarifa yako na sisi tunajua sana kama aliuwawa wala
hajafa kwa yake kama unavyosema. Joshua amefanya uchunguzu, ametafuta watu
wakafanya uchunguzi kwa kina kujua chanzo cha moto uliosababisha kifo chao.
Maana ile nyumba ilitengenezwa upya umeme na mafundi wa hapa kwenye hii kampuni
yetu. Hapakuwa na shida ya umeme ila mtu alianzisha moto kwa kurushia chupa
iliyokuwa na dizeli ndani, kisha ikawashwa moto na kurushiwa kwenye nyumba
waliyokuwa wamelala wao. Chupa imeokotwa na ushahidi upo polisi. Uchunguzi
unaendelea. Baba yenu, mdogo wenu, bibi na mjukuu wake wameuwawa kikatili
sana na mtu ambaye anaonekana alikusudia kulipa kisasi kwao. Aliyefanya
au kutengeneza huo mpango, alionekana kufanya kwa makusudi
kabisa. Waliwasubiria wakiwa wamelala kabisa wakijua hawatawahi hutoka
ndani kwa kuwa walishafunga na milango yote.” Bale akapoa kabisa akaonekana
kuna kitu kimemuingia.
Nanaa
akaendelea. “Mimi sijui umesikia nini na wapi! Sijui unakotolea taarifa zako.
Lakini kabla ya siku kama 4 hivi za harusi ya Naya, baba yako alikufuata mpaka
Mbeya! Akaambiwa ulikwenda Tunduma. Yule mzee akiwa amefunga, na kila mahali
akisikia jinsi ulivyoacha sifa zake mbaya kama hivi hapa unavyomtukana kama
hana akili ya kufikiria. Akiwa hali wala kunywa, alikufuata Bale. Tena alitoa
amri Naya aolewe asimsubiri yeye maana alisema yeye hatarudi bila
wewe.” “Uongo huo. Sio kweli. Baba alikubali maisha yaendelee bila mimi.” Bale
akabisha.
“Wewe
amini vile unavyotaka kuamini. Ila baba yako alikwenda mpaka Tunduma
ilikosemekana umekwenda kufanya biashara, tena haramu. Kabla hajakupata
akatekwa nyara sababu alikuwa akikutafuta kupitia mtu hatari sana aliyesikia
wewe mwenyewe, kwa tamaa zako ulimfuata huko Tunduma ukijua aina ya biashara
unayokwenda kufanya. Lakini baba yako alikufuata Bale akitaka angalau
ajiridhishe upo salama kwa kuwa alipata ujumbe wako kuwa humtaki yeye ni mjinga,
hana akili ya kufikiria.” Nanaa akaendelea kwa jazba.
“Watu
wakamkatisha tamaa hata asikufute huko Tunduma, kwa kuwa huyo mtu ni hatari
lakini alikwenda. Na alipofika huko nako wakamtisha kwa kumpa habari za kweli
juu ya huyo mtu kuwa ni kweli ni hatari na analindwa mpaka na askari waovu,
lakini baba Naya alikataa kurudi nyuma, akasema hataogopa wala kurudi mpaka
akutane na huyo mtu aliyesikia anajua ulipo. Tena huyo mtu anaitwa..” Nanaa
akawa kama amesahau.
“Mbabe.”
Geb akamsaidia mkewe maana Joshua yeye akili zilishahama pale kwa Bale, akawa
ameshamsogelea Naya na kujaribu kumtuliza lakini akawa anamkwepa. “Usinipige
kichwani. Naumwa sana kichwa. Nipige huku kwingine.” Naya
akasikika akilalamika akijikinga kichwa. “Sikupigi Naya. Nataka kukusaidia
kukufuta machozi.” “Usinishike kichwa. Kinauma sana.” Naya akaendelea kulia
taratibu akijaribu kusogea mbali kidogo ya Joshua.
“Umelaaniwa
Bale. Unapiga dada yako mpaka anakuwa tahira sababu ya mali alizoacha baba
yenu, aliyekuwa akikupenda hivyo! Tena wala baba Naya hakusema Naya awafukuze
pale. Muulize Joshua huyo aliyeachiwa maagizo yote na baba Naya. Baba yenu
alitaka nyinyi watoto wa kiume mtambue pale ni kwa Naya pia. Ili vikishindikana
huko, basi mumfungulie mlango dada yenu! Hakutaka wake zenu na watoto wenu waje
kumfukuza Naya! Alitaka na yeye Naya awe na sehemu ya kudumu, kimbilio wakati
akihitaji! Lakini si kwa kuwa alikuwa akikuwazia wewe au Zayoni mabaya kuliko
Naya! Yule mzee alikuwa radhi akose sherehe ya Naya akutafute wewe mpaka
akupate bila kujali matusi yako, au vile ulivyokuwa hutaki
mahusiano naye tena ukisema waziwazi humtaki. Baba yako hakujali akasema
ni mpaka akupate ili kujiridhisha tu upo salama. Ila ndio watu wa Mbabe
wakamteka nyara baba yako kabla hajakupata tena akiwa hotelini Tunduma, amepiga
magoti akikuombea kwa simu na huyu Naya unayempiga.” Nanaa akaendelea ila
wakashangaa utulivu wa Bale. Ni kama alitulia kabisa akisikiliza kama
anayetafuta kuelewa.
“Wakampiga
sana mpaka Geb na Joshua walipokwenda huko kumtafuta maana kama nilivyokwambia,
alitekwa nyara kwa kuvamiwa hotelini, ndani ya chumba alichokuwa amefikia,
akiwa amepiga magoti yupo kwenye simu na Naya, tena alianza kwa kumuhusia tena
Naya, maana sisi wote alishatuaga hapa kuwa mambo ya harusi ya endelee hata
kama yeye hayupo maana alisema hatarudi bila wewe. Akarudia tena
kumwambia Naya kabla hawajaanza kuomba kuwa yeye maisha yake yaendelee bila
yeye kwa kuwa yeye hatarudi bila wewe! Na vile baba yenu alivyowapenda nyinyi
watoto, akatuambia wote, kwamba hata kama atauwawa huko alikokwenda kukutafuta,
maiti yake ifungiwe chumba cha maiti, Naya aendelee na ndoa yake. Hakutaka
hata mmoja wenu aharibikiwe zaidi kwa ajili yake.”
“Baba
yenu alikuwa akilalamika na kujutia sana kuwa amefanya makosa mengi,
hakubahatika kufanikiwa kama wazazi wengine, ndio maana hataki tena kuendelea
kuwachelewesha. Tena hayo alimwambia mama kwa simu, maana ilibidi mama
kumtafuta na kuzungumza naye kwa undani akimwambia wosia anaoacha kwetu,
sio picha nzuri kwa jamii endapo kweli lolote baya likimtokea, halafu sisi
tuonekane bado tunaendeleza sherehe ya Naya! Akamwambia anaomba afute
hiyo kauli, wosia wake ni mzito. Baba yenu alikataa akasimamia hapohapo, Naya
huyu akimlilia lakini akakubali kumuacha Naya hapa, yeye akawepo Tunduma
akikutafuta!” Nanaa akamsimulia kila kitu Bale, na kumuacha Bale anatamani
kulia.
“Baba
yako amerudishwa hapa jijini na kina Joshua, akiwa mgonjwa, anaanguka kifafa
sababu ya kupigwa kichwani huko kwa kina Mbabe, akikutafuta wewe, leo
unamfanyia hayohayo dada yako! Umelaaniwa Bale. Mungu hatakuacha
wewe.” Bale kimya akabaki akifikiria. Maana kweli Mbabe anamjua.
“Tena
nikwambie kabisa, baba yako hakuacha kukutafuta Bale. Aliomba watu wamsaidie
kuzunguka mahospitalini na vyumba vya maiti, baada ya kushindwa kupatikana huko
magerezani.” “Tena kwa pesa zake mwenyewe, aliniomba nisubiri malipo yangu, awe
ananilipa kiasi cha chini ya pesa tuliyokuwa tumekubaliana, ili hiyo pesa ya
kukutafuta wewe ailipe mwenyewe wala si Joshua tena aliyekuwa akilipa
watu waliokuwa wakikutafuta. Ndio chanzo cha kuja kuacha hapa hati yake akitaka
kuniaminisha sio kwamba anakwepa kunilipa pesa ya biashara tuliyokuwa tukifanya
naye. Ila akanisihi nimvumilie akinihakikishia lazima atamaliza pesa yote
akiweza kukupata au kujiridhisha upo salama sehemu, yaani haupo matatizoni. Na
hayo yote yalimgarimu pesa ya kutosha tu.” Geb akaongezea kwa mkewe.
“Sasa
hapa huondoki na Naya. Askari yule pale. Ukimgusa tu Naya, nakuitia
mwizi hapa, wakupige kisha nakupeleka jela. Haya mlango huo hapo, toka na uchu
wako za mali. Kijana mzima unapigania mali za kurithi na si kutafuta mwenyewe
kiwanja chako ujijenge kama wanaume wenzio, unalilia mali za mama yako!
Huna aibu wewe! Na kama sio umeanza kuvuta bangi ni nini wewe uliyeshindwa
kukanusha mbele ya baba yako siku ile, mbele za watu wote, tena akasema
alishazungumza hata na mama yenu! Unakuja hapa unamtukana mume wangu eti anataka
kuwadhulumu! Tena toka kabla hujaniudhi zaidi.” Nanaa akazidi kukasirika,
akiongea kwa sauti.
“Na
ukamwambie huyo mwalimu wako anayekufundisha kuvuta bangi, tumemchukua Naya, na
tunakwenda kumuonyesha ustawi wa jamii na polisi ili muanze kuchunguzwa huko
mlikokuwa mmemficha Naya.” “Mimi sitaki kesi ndio maana nilikuja na Naya,
tuyamalize.” “Kwa kumpiga dada yako?” Nanaa akamuuliza kwa ukali.
“Naombeni
nimpeleke Naya hospitalini jamani! Hayupo sawa. Anatetemeka baridi ya ajabu,
kichwa kinamuua mpaka namuona anaogopa kujishika kichwani yeye mwenyewe! Hata
machozi anaogopa kujifuta! Naya hayupo sawa. Naombeni mimi niende.” “Naweza
kukusaidia.” Bale akajirudi. “HATUTAKI. Toka hapa na bangi zako. Na tusikuone
tena. Twende mwaya Joshua.” Kazi ya Nanaa nayo ikaishia hapohapo. Mama bosi
huyo akaingia ndani, akabeba pochi yake akawa amemaliza siku yake ya kazi bila
kuaga, asubuhi na mapema hiyo, siku ikiwa ndio imeanza, na majukumu yake mengi
kuliko yeyote kwenye ofisi hiyo. Lakini hakujali, akatoka kama ni jioni vile,
amemaliza siku ya kazi! Geb akabaki akimwangalia mkewe jinsi alivyonunua
ugomvi. Ila akafurahi kuwa amemuweza Bale.
“Usinishike
mimi. Naumwa!” Naya akalalamika akilia taratibu. “Nataka kukupeleka
hospitalini, Naya. Si unaumwa?” Joshua akamuuliza taratibu, akatingisha kichwa
taratibu sana, akikubali. “Unataka nikusaidie kukushika mkono?” Akakataa.
“Mkono nao unauma?” Joshua akaendelea kumuhoji kwa kujali. Akakubali akijifuta
machozi na kamasi kwa hofu sana kama anayeogopa kujitonesha ila nazo zimemzidi
zikiingia mpaka mdomoni. “Wewe Bale, kwa nini Naya yupo hivi!? Mlikuwa mkimpa
nini?” “Mimi sijui.” Bale akajibu hivyo na kuondoka kwa haraka.
“Basi
sitakushika. Twende hospitalini. Tupitie mlango huo.” Akaanza kutoka akiwa
amejikojolea. Nguo mbichi! Mbali na mkojo, Naya alikuwa akinuka. Alitoa harufu
kama aliyemchafu, hajisafishi vizuri. “Pole Naya.” Nanaa akajaribu kumsemesha.
Naya kimya akitembea kutoka mlangoni. “Joshua. Nendeni na Nanaa, mimi
nitawafuata baadaye.” “Wewe piga kazi GM. Tutawasiliana.” “Basi kukiwa na kitu
chochote tafadhali mnijulishe.” Nanaa alishatoka bila hata kumuaga mumewe,
macho kwa Naya.
Ikawa
shuguli kuingia kwenye gari, Naya analia maumivu hawezi kunyanyua mguu kupanda
kwenye gari ndefu ya Joshua! Hataki tena kwenda. Kazi ya kumsihi apande garini
apelekwe hospitalini ikaanza. “Naumia mimi!” Alipoona wanamkera, akaanza
kuondoka pale taratibu. Joshua akamkimbilia akikumbuka maneno Naya aliyomwambia
siku ya harusi yao, masaa machache kabla yakufunga ndoa akiwa amemuokoa kutoka
kwenye gari yake Malon alipomzuia.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Naya
alimwambia maneno yaliyokuwa yamebaki moyoni mwake, japokuwa
alitaka kumkasirikia kwa nini alimfungulia Malon mlango wa gari, lakini Joshua
akabaki akimtetea nakusema Mungu aliruhusu lile kosa alilofanya Naya, kwa ajili
yake yeye mwenyewe Joshua, ili tu kumsikia Naya akitoa moyoni mwake jambo
alilotamani kulisikia kwa mwanamke yeyote atakayemuoa wakati huo akiwa
amefanikiwa sana. Joshua alitamani sana mapenzi ya dhati. Alimpokea Naya na
kukubali amuoe kwa imani tu, akiamini kuwa, hatua
za mwenye haki huongozwa na Bwana, akampokea Naya kwa
shukurani bila uhakika kama Naya huyu kama kweli angemkubali akiwa na dhiki!
Lakini
katikati ya fujo ile, Joshua akapokea yale maneno kwa furaha akiamini Mungu
amezungumza naye kwa kumtoa hofu au kujibu swali kubwa alilokuwa nalo ila
kushindwa kuliuliza kwa yeyote hata kwa Naya mwenyewe. Akiwa ameingiwa hofu,
Naya akaongea akiwa wala hajajipanga azungumze hayo, akamsikia Naya akimuapia
wakiwa na Geb kwenye simu kuwa hatamuacha hata kama atafilisika na kupoteza
kila kitu, atamchukua na kwenda kuishi naye kwa baba Naya wakijipanga upya.
Tena akaongeza hata akiwa mgonjwa mahututi wakugeuza kitandani, basi Naya
akaahidi atabaki naye kumuuguza mpaka kifo. Hatamkimbia. Naya anajitetea
kwao kwa hofu akijua ameharibu na Malon ameongea maneno yanayofanana na ukweli,
huko moyoni Joshua alikuwa akimshukuru Mungu wake kwa kumpa wakusimama naye mpaka
kifo. Ndio maana walipofika nyumbani, Joshua akalemewa katikati ya mabusu
mazito akiwa amejihakikishia kwa hakika Naya ni wake, akatamani amalize
hapohapo mpaka Nanaa akatokea.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Joshua
akaongeza mwendo na kwenda kusimama mbele ya Naya aliyekuwa ameshafika mbali
kidogo ya alipoegesha gari yake. “Nakuahidi nitakuwa mwangalifu wakati
wakupanda garini, hutaumia. Twende watakupa dawa ya kutoa hayo maumivu.” Ndipo
akakubali na kurudi garini, wakielekea hospitalini. Njiani Nanaa akampigia simu
Sonia Tambo, mwanasheria anayewasaidia ushauri mwingi wa kisheria ambaye naye
alikuwepo kwenye kitchen party na harusi ya Naya pia. Akamtaarifu kurudi kwa
Naya na hali aliyokuwa nayo kwa wakati huo. Akawashauri lazima
waanzie polisi kuripoti lasivyo kila jambo baya atakalokutwa nalo Naya huko
hospitalini litakuwa kwao.
Naya/Joshua.
Japokuwa
Joshua aliona nikupoteza muda, lakini akakubaliana nao. Wakaanzia kituo cha
polisi kuandikisha kesi na kupata RB, jina alilokuwa akilijua Naya, ni Joshua
tu. Akakazania kwamba hilo ndilo jina lake hata hospitalini akajitambulisha kwa
daktari kama anaitwa Joshua. “Kabla ya kukimbilia kuwa ni tatizo la akili,
naomba apimwe kwanza kichwa. Analalamika kinamuuma. Na hawezi hata kusoma. Kama
kweli alikuwa akipigwa, inawezekana wamegusa sehemu ya ubongo.” “Na pia
tusubiri majibu yake ya damu na mkojo. Inavyoonekana alikuwa akitumia madawa ya
kulevya. Hiyo hali ni ya mateja. Akipewa unga hapo, atatulia kabisa.”
Daktari akaongeza akiwa ameshapata muda wakutosha wakumchunguza Naya. Joshua
akaumia sana. Naya hakuwa akielewa wala kutambua chochote.
Vipimo
vya kina na vya haraka vikaanza kwa mke wa Joshua Kumu, mfanyakazi na kiongozi
wa ngazi ya juu sana wa kampuni ya Coca. Mbali ya kuwa bado alikuwa ni kama
mfanyakazi, japo Joshua alimchukulia likizo bila malipo, lakini Naya alikuwa
kwenye hospitali hiyo ya wenye nazo akilipiwa matibabu hayo ya garama za juu
sana na kampuni, kama mke wa Kumu. Huduma zilikuwa ni za haraka, na za kisasa,
halafu na madaktari walikuwepo wakutosha kumuhudumia Naya kwa kadiri ya uhitaji
wake.
Baada ya
yote, vipimo vikaonyesha damu ipo na madawa ya kulevya, kwamba ni kweli alikuwa
akitumia madawa ya kulevya. Na majibu ya vipimo vya CT scan yalionyesha
Naya ana uvimbe kwenye ubongo. Jambo lililopunguza wasiwasi mkubwa kwa Joshua
ni pale daktari alipoeleza kuwa haukuwa uvimbe kama mwenye kansa ila ni uvimbe
mdogo tu wa kama aliyekuwa amegonga kichwa sehemu inayohusika na kumbukumbu, na
ndio ikamsababishia kupoteza kumbukumbu. Na wakaambiwa kwa matibabu, utakuja
kuisha tu. Hilo likawa faraja. Alipoulizwa ilikuaje, Naya hakuwa akikumbuka
chochote.
Matibabu
yakaanza akiwa ameshatolewa nguo za mikojo, na kupewa mavazi ya hospitalini.
Napo walishangaa ila wakaelewa ni kwa nini alikuwa pia hataki kuguswa hata
mkono. Naya alikuwa amevilia damu kila mahali kama aliyekuwa akipigwa sana.
Joshua akazidi kuumia na kushindwa kuelewa nini alipitia huko alipokuwa.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Maisha ya
Joshua yakahamia hapo hospitalini akimuuguza mkewe. Japokuwa Naya hakuwa
akimtambua kabisa, lakini hakuacha kuwa naye mchana na usiku. Siku ya kwanza
anajua Naya analazwa, alikwenda kufungasha vitu vyake akiwa amemuacha hapo
Nanaa, na ombi asije akaondoka hapo kabla hajarudi. Na kweli alifanya haraka,
akakusanya vitu vyake muhimu na vitu vya Naya, akarudi hospitalini kwa haraka.
Akawa kama amehamia hapo hospitalini hata asitoke. Kama ni simu za kiofisi,
alizungumza nje akiwa anaona mlango wa kuingilia chumba alicholazwa Naya peke
yake bila mgonjwa mwingine, akihofia wasije kuja kumchukua tena. Naya alikuwa
akimka, anamtizama kwa muda mrefu ila hamuongeleshi kisha anarudi kulala.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Baada ya
siku tatu ngumu wakijitahidi kusafisha damu yake, akitapika na kulia maumivu
kila wakati huku madaktari wakimkatalia kumpa madawa makali, usiku huo kidogo
akalala akionekana ametulia. Sio kama alivyotapika siku mbili mfululizo
akionekana kama teja. “Vipi sasa hivi kichwa?” Joshua akamuuliza baada ya kutoa
macho kwenye laptop yake na kukuta Naya akiwa ametulia akimtizama.
Akamuona anavuta pumzi kwa nguvu kisha akatulia. Ila akaacha kumuangalia.
“Pole.”
Akageuka na kumtizama tena Joshua. “Ninaumwa nini?” Naya akauliza taratibu.
“Kichwa. Unakumbuka nini kilitokea?” Akafikiria kisha akamuona anatingisha
kichwa akikataa. “Sasa hivi upo na maumivu yeyote?” “Hapana. Wewe ni nani?”
Naya akamuliza taratibu tu. “Joshua.” Naya akabaki akimtizama. Ila Joshua
akaumia sana.
Akasimama.
“Umenikumbuka?” Joshua akamuuliza. “Nakufahamu?” Naya akamuuliza taratibu
akionyesha kushangaa ila na wasiwasi kidogo. “Ndiyo.” Naya akamtizama kwa muda.
Akamuona anafunga macho. “Usijali. Jipe muda. Utakumbuka tu.” Akamwangalia na
kubaki akimwangalia kama anayejitahidi kufikiria zaidi. Joshua akatamani
amwambie mengi ila akaogopa kumchanganya. Akamsaidia kumfunika vizuri, ila kwa
tahadhari, kisha akasogea pembeni kidogo. Wakatulia.
“Hapa ni
wapi?” Naya akauliza tena. “Ni hospitalini. Ulikuja ukiwa unaumwa.” “Sasa hivi
nimepona?” “Kesho asubuhi unafanyiwa kipimo kingine tena, ndipo daktari
atatujulisha. Ila wanajitahidi kukupa dawa ya kupunguza maumivu, ili usipatwe
na maumivu makali kama mwanzo.” “Kweli kichwa kilikuwa kikiniuma
sana.” Akaongea akifikiria. “Pumzika.” Akamuona analala. Akafungua macho
kabisa.
Kisha
akafungua macho na kukuta bado Joshua amesimama akimtizama. “Ulisema unaitwa
Joshua?” Akawa kama anataka uhakika. Joshua akatoa tabasabu la kufariji
akimwangalia kwa kuwa bado alikuwa amesimama pembeni ya kitanda chake. “Ndiyo
naitwa Joshua.” Akatulia akimwangalia, kisha akamuona anasinzia tena. Usiku huo
akalala, akiwa ndio kwa mara ya kwanza kuzungumza kwa muda mrefu. Kipimo
kingine cha kichwa, MRI kilionyesha uvimbe unanywea. Wakaruhusiwa Naya akiwa
anamwangalia sana Joshua.
Baada ya Kuruhusiwa Hospitalini.
Naya
alielewa kuwa ndio ameruhusiwa kutoka pale hospitalini. Madaktari walipotoka
tu, akamgeuki Joshua. “Asante. Lakini mimi naondoka.” Joshua akashituka sana
moyoni ila akajikaza. “Unakwenda wapi?” Hapo akatulia kama anayefikiria. “Ni
kama nimeruhusiwa!” “Ndiyo. Ila unatakiwa kuendelea kutumia dawa na kuhakikisha
hurudii tena kutumia madawa mabaya.” Hapo Naya akawa hajaelewa, akabaki
akitafakari. “Hujanijibu Naya. Unataka kwenda wapi?” “Samahani lakini. Ni kama
hata nimesahau mimi ni nani! Kwani nilitakiwa kwenda wapi baada ya hapa?”
“Turudi wote nyumabani kwetu.” “Unamaanisha nini!?” Naya akauliza akionekana
kwa hakika haelewi.
“Kwani
wewe ni nani?” “Joshua Kumu, mumeo.” Naya akashangaa sana. Akabaki
akimwangalia. “Hukumbuki?” “Hapana! Hata kidogo. Kwani kama sio kwenda na wewe,
ningetakiwa kwenda wapi?” Naya akauliza akionyesha kutoridhia kabisa kuondoka
na Joshua. Joshua akatulia kidogo akifikiria. “Siwezi kwenda na mtu nisie
mfahamu. Samahani. Unaonekana wewe ni mtu mzuri, ila sikufahamu kabisa. Naogopa
sana.” “Unakumbuka kuniona hapa muda wote?” “Ndiyo ila sijui ni kwa nini
ulikuwa hapa!” “Ili kukuuguza, wewe.” Naya akabaki akimtizama kama asiyemuelewa
kabisa. Akajua anamkatalia, ikabidi aongeze ushawishi asipokonywe tonge
mdomoni.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Bado
Joshua alikuwa akitaniwa juu ya ndoa changa na watu wa karibu, ila mke hayupo
nyumbani! Akabaki kupokea pongezi za ndoa tu. Akamchukulia Naya likizo bila
malipo huko kazini ili asije poteza kazi, akiamini tu, Mungu
hajawahi kumpokonya vitu ampavyo. Akabaki akiomba huku
akimsaka Naya kwa udi na uvumba. Na bado aliendelea kufanyia uchunguzi chanzo
cha moto uliomuua baba Naya na ndugu zake mkewe. Akiwa hajui kama Bale yu hai
au la, kwa sababu ni kama habari zake hazikuwa zikieleweka vizuri, ndipo
akapigiwa simu na Geb kuwa Bale yumzima, ametokea ofisini kwake akidai
kiwanja.
Ile Geb
kumkatalia na kumwambia lazima awepo Naya, na Bale hakuonyesha hilo ni tatizo,
moja kwa moja Geb akamwambia Joshua, kuwa Bale anajua Naya alipo. Joshua akaumia
kuona kwamba walishindwa kumfuatilia Bale kujua Naya alipo ili kama kuhitimisha
ndoa, basi ahitimishe Naya mwenyewe kwa mdomo wake, tena mbele ya Joshua
mwenyewe.
Lakini
Geb akamtuliza. Akamwambia uchu aliouona kwa Bale, atarudi tu, tena atarudi kwa
haraka na hapo ndipo wambane mpaka aseme Naya alipo. Tangia asikie hivyo,
Joshua akatembeza mfungo akimsihi Mungu na kumkumbusha ahadi zake mpaka
alipompata Naya na ndipo akabaki akishukuru Mungu kuwa amemrudishia mke, na
safari hii akaaga kwa ujasiri kazini kuwa mkewe anaumwa, amelazwa, anamuuguza.
Kazi zote atafanya akiwa hospitalini. Leo Naya anamuaga kwamba hamtambui!
Joshua akaona ang’ang’anie muujiza wake.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Nikuulize
kitu Naya?” Naya akabaki kimya. “Unakumbuka daktari kukukumbusha kwamba wewe
unaitwa Naya?” “Aliniambia mimi siitwi Joshua ila Naya. Ila sikumbuki kabisa!”
“Umebakia na jina langu moyoni, Naya. Mimi ni mumeo. Naomba uniamini
ujue sina sababu ya kukudanganya.” Naya akanyamaza. “Unakumbuka kuniona nipo
hapa, nikikusumbua?” Naya akatingisha kichwa taratibu akikataa, huku
akimwangalia. “Ndivyo itakavyokuwa nyumbani. Nitakupa chumba chako. Utulie
hapo, mpaka utakaponikumbuka. Ni sawa?” “Hujanijibu swali!” “Kwamba kama sio
kwangu ungetakiwa kwenda wapi?” “Ndiyo.” “Huna pakwenda Naya, ila ni nyumbani kwetu,
mimi na wewe.” Naya akakunja uso kama anayeshangaa.
“Daktari
alishauri tusikwambie mambo mengi kwa wakati mmoja ili tusikuchanganye. Ila
mimi na wewe tuliona, na wote hatuna wazazi ila marafiki tuliojitengenezea
ukubwani wakawa kama ndugu. Unamkumbuka Nanaa? Hata asubuhi hii
alikuwa hapa akakupeleka bafuni kuosha uso?” “Namkumbuka pamoja na mumewe na
mama yake. Si wote wanakuja hapa kila wakati?” “Ewaa! Basi hao ni baadhi ya
watu wetu wa karibu sana. Wanakuja hapa asubuhi na jioni kukuona wewe. Wanatupenda
sana na wamekuwa kama ndugu.” Joshua akaendelea taratibu.
“Nanaa na
Geb walitusimamia harusi yetu. Tukaenda mapumzikoni. Tukawa na wakati mzuri
sana.” Akamuoana anaanza kukosa raha. Akajipandisha kitandani vizuri. “Kwa
nini sikumbuki hayo yote?” “Naomba usilie. Ila naomba jipe muda.
Ulipotea Naya. Ndio nimekupata tu! Tafahali amini sikudanganyi.” “Nilipotea!?” “Ndiyo.
Ila umerudi ukiwa hujitambui, ndio maana naogopa usije ukaondoka hapa, ukapotea
tena.” “Kwa nini sikumbuki hayo yote!” “Naomba tulia kabisa.
Usilie. Taratibu utakumbuka. Na hata kama hutakumbuka, una maisha marefu sana
yakuishi, utaendelea kuanzia utakapokumbuka.” Akamuona anajifuta machozi na
kujaribu kutulia.
“Nikupe
maji ya kunywa?” Akakataa. Muuguzi akaingia na karatasi za kuruhusiwa na dawa
alizoandikiwa Naya. “Hata akilalamika maumivu vipi, usimpe dawa mbali ya hizi
ili kuhakikisha madawa makali hayarudi mwilini mwake.” Naya akamsikia Joshua
akipewa maelekezo. “Nimeelewa.” “Poleni sana, na nawatakia kila la kheri.”
Muuguzi akatoka. Akamsogelea Naya. “Kwa hiyo tunakwenda wote?” Joshua
akamuuliza taratibu. “Utapata wakati mtulivu, bila muingiliano wowote. Nitakupa
chumba chako tu. Twende Naya.” Akakubali.
Geb na Nanaa
nao wakaingia. “Vipi Naya?” Geb akamsalimia lakini akanyamaza akimtizama huku
ni kama akisinzia. “Unajisikiaje?” Nanaa akaongeza swali. “Vizuri.” Akajibu na
kunyamaza. Pakatulia kwa muda. “Naona sisi tupo tayari kuondoka.” Joshua
akavunja ukimya akimwangalia Geb. “Basi acha mimi nibebe mizigo, ndio tutoke
pamoja.” Geb akanyanyua kila kifurushi hapo chumbani kama mzoefu wa kulazwa
hospitalini. Mkewe akamsaidia kubeba baadhi, wakatoka. “Twende Naya.” Maana
alibaki ametulia hapo kitandani. “Nikusaidie?” Joshua akauliza kwa kujali, ila
kwa tahadhari asije muudhi na kubadili mawazo. “Hapana.” Akatoka kitandani
akabaki amesimama. Joshua akamfungulia mlango kama kumuashiria atoke. Akatoka
taratibu.
“Niambie
unavyojisikia.” Joshua akabembeleza. “Kizunguzungu halafu nachanganyikiwa.
Sielewi tena! Kidogo nilicho nacho kichwani, naambiwa pia sicho! Sielewi.”
“Kama jina?” “Najua mimi naitwa Joshua. Ila kila mtu ananiita Nay..” Akasita.
“Naya.” Joshua akamsaidia kumalizia kisha akaendelea kumfariji. “Lakini
usijali. Jipe muda.” “Itakuaje nisipokuja kukumbuka tena?” “Kama nilivyokwambia.
Jipe muda. Kama usipokumbuka, ishi kutokana na vile utakavyokuwa unaelewa na
kuweza. Hakuna mtu anakutegemea kwa chochote. Tulia tu. Sawa?” “Sawa.” Wakatoka
hapo kurudi nyumbani, wakisindikizwa na kina Magesa.
BALE.
Kisasi.
Bale aliondoka
pale ofisi za Magesa akiwa ameumia sana. Hakujua ukweli wote kwa hakika kama
ulivyo. Ili kupata uhakika wa kile alichokisikia kutoka kwa Nanaa, akaamua
aanzie Tunduma. Kuhakiki kama kweli baba yake alikwenda huko. Kwa kuwa alimjua
Mbabe mtu wa madili na mpenda pesa sana, akakanyaga mafuta mpaka Tunduma huku
akijipanga. Alishayajua yale mazingira mpaka na watu wake. Akajua wapi aanzie.
Aliendesha kwa muda mrefu sana na hakutaka kupokea simu za Malon. Ila alimtumia
ujumbe kuwa atarudi baada ya siku 4. Akamzimia kabisa simu.
Alifika
majira ya jioni, akatafuta sehemu akaegesha gari na kulala kabisa mpaka
aliposikia mji umetulia kabisa, ndipo akatoka sasa kumtafuta Mbabe. Alijua
atamkuta kwenye moja ya baa anazopenda kunywa. Hakuingia ila akamtuma muhudumu
na pesa. Akamwambia amuite, amwambie ni dili ya pesa nyingi. Kama jina lake
lilivyo, akatoka akiwa anajisifia akijua mji huo hakuna atakayemfanya chochote.
Akamkuta Bale garini, akashituka kidogo akikumbuka unyama aliomfanyia Bale.
Akiwa
yeye ndiye mwenye mali hizo za magendo, akimuahidi atamlipa asilimia 50 ya
mauzo yote endapo atafanikiwa kuutoa. Lakini walipo kamatwa, akamsingizia Bale
kila kitu. Akamtupia lawama zote. Akatolewa yeye jela akamwacha Bale bila
kugeuka nyuma. “Mimi sijui walikwambia nini wale askari wa mpakani, lakini hivi
hapa nilikuwa nikijipanga, nikutoe.” “Acha woga wewe. Twende nikakupe dili la
ukweli. Pesa ya ukweli bila jasho.” “Kweli?” “Sasa unafikiri mimi ningefanikiwa
vipi kwa haraka kama sio hivyo? Twende.” “Hamna mambo ya visasi?” “Mimi naelewa
biashara na ulishanipa madhara yake kabla, nikakubali mwenyewe. Twende nikupe
dili za kiutuuzima.” Bale akasikika mwenye mamlaka sio kama mwanzoni
alipokutana naye. Bale akionekana mgeni wa mambo.
Mbabe
akapanda garini. “Kwanza kwa nini kama umefanikiwa, umenitafuta mimi?” Akawa
kama bado anao wasiwasi. “Napanua soko langu la bangi na mirungi. Sasa kwa kuwa
wewe mjanja, na umezoeana na askari mpaka wamipakani, naona soko litakuwa zuri
huku.” Mbabe akaanza kushawishika. “Maana mimi nauza bangi daraja la kwanza.”
Bale akaendelea kumvutia akiwa anaondoa gari hapo kwenye hayo maeneo. “Unatoa
wapi?” “Sasa nikwambie halafu iweje!? Wewe mbona kama unakuwa mgeni wa biashara
tena!?” Mbabe akacheka kwa heshima kidogo akijua anaongea na mtu wa maana.
Bale
akaendesha kama anayemtoa mjini. “Tunaenda wapi sasa!?” “Acha wasiwasi wewe!
Mbona unakuwa kama sio wewe? Umeanza lini woga, Mbabe?” Akacheka na kutulia.
Hakumpeleka mbali sana. Giza lilikuwa jingi tu, akaacha njia kuu na kuingia
njia ya vumbi, aliporidhika hakuna mtu huko akasimamisha gari. “Mbona hakuna
mtu hapa?” “Ndio penyewe, sasa wewe unataka na mashahidi tena!?” Akamuuliza
akicheka kama anayemsanifu.
“Shuka.”
Mbabe akiwa na sitofahamu kubwa mpaka usoni mwake, akafungua mlango na yeye
Bale akafungua mlango wake na kutoka garini. Akazunguka kwenye mlango wa nyuma
akatoa gongo akawa amelishika kwa nyuma, akamfuata Mbabe mpaka pale aliposimama
akishangaa. “Unaona kule?” Mbabe akageuka ili kuangalia anapoonyeshwa, Bale
alimpiga gongo la shingoni sehemu aliyojua atapoteza fahamu kama alivyomuona
Malon akimfanyia Naya na kweli akaanguka na kupoteza fahamu hapohapo bila hata
kutingishika. Alishajiandaa kwa kila kitu.
Wakati
yupo chini hajitambui, akamvua nguo zote. Akamfunga kamba ambayo tayari
alishanunua ilikuwa kwenye gari. Akamfunga vizuri mikono na miguu na
kuikutanisha kwa nyuma. Akachana shati lake na kumuingizia baadhi mdomoni ili
asiweze kupiga kelele. Taa za gari zilikuwa zikimulika pale mbele alipomvuta.
Giza kila mahali. Halafu kulikuwa na hali ya baridi na Mbabe alikuwa mtupu
kabisa kama alivyozaliwa.
Bale
aliporidhika amemfunga vizuri, akachukua tena maji aliyokuwa ameyahifadhi
kwenye dumu, nyuma kabisa ya gari. Akammwagia, Mbabe akaamka. Alipangilia kila
tukio atakalomfanyia Mbabe, akiwa njiani na akahakikisha hakosei hata kitu
kimoja. Akaanza kuhangaika akitaka kupiga kelele. Bale akampiga mateke
kumtuliza. “Nisikilize Mbabe. Nina maswali nataka kukuliza. Ukinijibu,
nakuachia. Ukipiga kelele nitakapotoa hilo shati mdomoni, ujue nitakuumiza kwa kuwa
utakuwa ukinipotezea muda. Kama umenielewa kubali kwa kichwa.” Mbabe akakubali
akitetemeka.
“Kama
mwezi sasa umepita. Nilipokuwa jela, kuna mzee alikuja kunitafuta mimi kama
Bale. Unakumbuka? Jibu ndiyo au hapana kwa kichwa.” Akakubali. “Sasa nakutoa shati
mdomoni, ili unielezee ilikuaje. Nakuonya usinipotezee muda kwa kuwa hapa
tulipo hakuna atakayekusikia. Acha kupoteza muda, uongee. Sawa?” Akakubali.
Bale akamtoa kipande cha shati lake mdomoni. Mbambe akaanza kupiga kelele. Bale
akachukua mkanda wa suruali yake na kuanza kumtandika nao kila mahali bila
huruma, tena kikatili sana. “Nitaacha, utakapoacha kupiga kelele.” Mbabe
akanyamaza.
Bale
akampiga teke la tumbo. “Tuanze tena. Eleza kilichotokea kwa mzee wangu
alipokuja kunitafuta.” “Mimi sikujua kama ni mzee wako. Nikajua ni
watu wa usalama wamekuja kunichunguza. Nikawaambia vijana wangu wamchukue,
wakamtoe ukweli. Sasa walichomfanya huko, hawakuniambia.” “Ila
mimi na wewe tunajua walichomfanya ili kumtoa ukweli, na bado
hamkumsadiki!” “Wewe unayajua maisha Bale na umepita nilikopitishwa mimi.
Huwezi kuamini maneno tu! Mpaka walipokuja wale vijana wawili na maaskari
wakasema hawataki kesi ila kumtaka tu yeye, ndipo akaenda kutolewa.” “Kutolewa
wapi!?” “Alikuwa amefungiwa Bale! Si nilisha kwambia?” Bale
akaumia sana.
“Sasa
nipo hapa kulipiza kisasi. Si kwa uliyonitendea, ila uliyomtendea baba yangu.
Kwa kuwa yeye hayupo, mimi nitakulipiza kisasi ikawe fundisho. Na sitakuweka
kitambaa mdomoni. Nakuadhibu ili ulie sana, nataka masikio yangu yasikie kilio
chako. Ukome.” Bale akaanza kumpiga kama mwizi. Safari hii alimpiga na gongo
kila mahali, bila huruma kama aliyepagawa. Akampiga viwiko vya miguu kama
anayetaka asije tembea tena. Akampiga magoti. Kiunoni ndio zaidi. “Hapa ndio
kutakusaidia usiwahi kuja kulala na mwanamke tena.” Akampiga hapo tena na tena.
Akarudia mikononi. Bangi ilimsaidia kuhakikisha anampiga mpaka anasikia sauti
ya mifupa kuvunjika bila huruma. Akatulia akimwangalia.
“Sasa
nimeridhika. Uso na mdomo nakuachia ili ukawasimulie wale askari na vijana
wako. Kawaambie Bale amenilipiza kisasi kwa niaba yenu wote kwa kile
mlichomtendea baba yangu. Waambie nikirudi tena kwenye huu mji, wajue
nilibadili mawazo, nimeona wewe hutoshi, nitakuwa nimerudi kuwalipiza na wao.
Na atakayenifuata, nitamrudisha maiti.” Bale mwenyewe alikuwa akihema.
Akamuingiza
tena Mbabe kwenye gari. Akamrudisha mpaka njia kuu. Akamuacha sehemu ya wazi
kabisa, akilia kama mtoto mdogo. Yeye akaondoka kurudi kwa Malon akimjua Malon
jinsi alivyo mkorofi. Akaanza kujipanga sasa kumkabili Malon.
Kwa Malon.
Alikwenda
alikojua atamkuta Malon huku moyo wake ukimuuma sana akiwa ameamini
alichoambiwa na Nanaa. Akajiuliza mengi juu ya Malon huku akijilaumu akiumia.
Alikuwa akielekea sio sehemu ambayo Malon alikokuwa amejificha na Naya. Alijua
mida hiyo anakusanya mazao kwenye mashamba yake na kuyaweka kwenye gala kuu la
huko Mbeya. Sehemu aliyofikia yeye mwanzo kabisa. Alifika alfajiri tu na
mapema, kila mtu amelala. Akaamua kulala garini nje ya gala.
Akiwa
amepotelea usingizini akasikia kioo kikigongwa. Akafungua macho alikuwa Malon.
“Naya yuko wapi?” Bale akatoka garini. “Kwanza wewe ulikuwa ukimpa nini?” “Acha
kunihoji wewe! Nijibu.” Bale akachukua kibegi chake garini. “Naya yupo Dar
mgonjwa na hajitambui kabisa. Hata jina lake hajui ni nani?” “Hiyo ni janja
yake tu ili kukukwepa. Naya tapeli sana.” “Wewe achana na maswala yangu.” Bale
akampita kama aliyemaliza. “Unamaanisha nini wewe? Kwa nini hujarudi na Naya!?
Tulipanga nini na unafanya nini?” Bale akasimama kwa hasira.
“Hivi
unasikia chochote ninachokwambia Malon?! Nakwambia Naya ni mgonjwa, hajitambui!
Wewe niliyekuwa nimekuacha naye hapa, hukujua kama nimgonjwa?!” “Ningejuaje
mimi?” “Naya tuliyemchukua majuma machache yaliyopita sie huyu! Amekua kama
teja! Nakuuliza umekuwa ukimpa nini, hunijibu! Sasa unamuulizia wa nini?”
“Kwamba yupo anapewa matibabu?” “Matibabu gani, wakati ndio nakuuliza ili
kuweza kumsaidia, hunijibu! Labda nirudie tena, Naya umekuwa ukimpa nini, mbali
na zile dawa ulizoniambia mimi ni za usingizi, ulimpa nini?” “Ni zilezile. Labda
kwakuwa hakuwa akinywa pombe au hajawahi kuweka kileo chochote kile mwilini
ndio maana imemchukua vile. Haya nimekujibu, na wewe nijibu yuko wapi?” “Subiri
kwanza Malon. Naya analalamika sana maumivu. Ulikuwa ukimpiga?” “Maswali gani
hayo Bale kutaka kunifanya mimi mtoto mdogo? Acha ujinga wewe.” Bale akaondoka
pale akitaka kuelekea kwenye nyumba wanayoishi.
Siri Mwangani.
“Umekua
na vijisenti, ndio unaanza jeuri Bale wewe mimi ndio nakufundisha biashara!
Hukuwa na kitu, umekua mtu, unaaza dharau kama ndugu zako!? Kweli nyinyi wote
hamkujaliwa shukurani! Mnapenda kutumia tu watu!” “Ndio maana umemchoma moto
baba yangu na mdogo wangu!?” Bale akamuuliza swali la moja kwa moja kama ambaye
hakuwa amepanga hivyo au silo lililompeleka pale kumbe lengo lilikuwa na hilo
swali pia, kujiridhisha akimtetea Malon kuwa hata kama ni mnyama kiasi gani,
hawezi kuwa alifanya unyama ule kwa familia yake!
Malon
akababaika kidogo. “Eti Malon? Uliamua kuwalipa ndugu zangu vibaya kiasi hicho
ukaamua uwachome kabisa!?” “Kweli Bale huna shukurani kama ndugu zako!
Walikutelekeza jela, mimi nikaja kukutoa, leo unaniambia hivyo!” “Labda
nikuulize Malon, wewe ulijua kama baba alikwenda Mbeya kunitafuta akaishia
kutekwa nyara, wakampiga vibaya sana mpaka Joshua na Geb kwenda kumuokoa
huko, na bado alikusudia kurudi tena kunitafuta!?” “Wameshakudanganya huko Dar,
wamekujaza uongo, unarudi kwangu kwa kiburi! Sio wewe nilikusikilizisha maneno
waliyonijibu juu yako?” Malon akamuuliza kwa ukali kabisa.
“Ulinisikilizisha
ulichotaka wewe, na mimi nikaamini kutokana na nilichotaka kusikia kwa
wakati ule nilipokuwa na hasira, tena hasira ulizosababisha
wewe.” “Mpuuzi wewe Bale na huna shukurani! Kweli wewe unaniambia hivyo mimi!?”
“Acha kupaniki, nipe simu yako tujue leo nani ni muongo.” “SIKUPI.” “Kwa kuwa
unajua nitakutana na rikodi za ukweli. Wewe ulitengeneza mazungumzo Malon.”
“Mjinga tu wewe, Bale.”
“Nahisi
Naya yupo sahihi. Na nahisi ni bangi imekuharibu kichwa mpaka
huamini mtu anaweza kukupenda wewe kama Malon, mpaka uwe na kitu. Ndio maana
unatumia nguvu nyingi sana kuvuta watu kwako. Lakini usingemuua baba yangu
Malon. Mzee alikupenda sana japo mama alikukataa, ila baba alisimama na wewe
mpaka wewe mwenyewe uliposhindwa kuendeleza uongo wako ndipo akaamua aachane na
wewe, na Naya aamue mwenyewe! Naya anaolewa na Joshua, bado mzee
akabaki kuwa mkarimu kwako, akikufungulia milango mpaka ukashindwa mwenyewe!
Kweli unamchoma mzee wangu kwa wewe mwenyewe kushindwa kuwa mwanaume!?”
“Wewe
bangi zinakuchanganya Bale. Sio wewe tuliweka wote mipango hapa, ili
kuwaadabisha na kuwakumbusha wao ni kina nani? Kuwatoa pale walipofikishwa na
kina Joshua, na kuwarudisha chini kabisa! Leo imetokea ajali kazini,
unarudi kunilaumu mimi!?” “Acha kujidai mjanja Malon. Tulikubaliana
tuchome lile gala mida tunayojua kabisa watu hawapo pale
nyumbani. Nyinyi mkawasha moto nyumbani na wala si galani, tena mkijua
wamelala!” “Wewe kama unasumbuliwa na kuuwa ndugu zako wewe mwenyewe, ni juu
yako Bale. Wakati moto unawashwa tulikuwa wote huku. Iweje leo uje unitupie mimi
lawama! Ushanisikia mimi hata siku moja nataka nikawachomee moto wazazi wangu
mali zao au kuwadhuru kwa namna yeyote ile?” Malon akamuuliza akimsuta na
kumuumiza sana Bale akijiona mjinga.
“Hata
siku moja! Wewe mwenyewe ulikubali. Tukaweka mipango. Kwa kuwa wengine hatujui
kuwa vigeugeu, mambo yamefanyika, sasa hivi unakuja kulaumu! Nani amekwambia
kuua mzazi wako au kumwaga damu ya mtu ni jambo rahisi!? Mimi na uovu wangu
wote huu, sijawahi ua. Wewe umemwaga damu ya watu wanne, tena ndugu zako!” “Kwamba
sasa hivi mimi ndio nimeua!?” Bale akashangaa sana.
“Twende
tukajieleze polisi, tuone wataamua vipi hii kesi. Acha kujifanya umechanganywa
na bangi ulizokutana nazo ukubwani wewe! Na ninamtaka Naya, kama
tulivyokubaliana. Kama wewe umeshindwa kusimamia mipango yako, mimi
sijashindwa. Namtaka Naya, bado sijamalizana naye. Umenisikia Bale? Nenda
kamlete Naya kabla hujaniudhi zaidi na haya mambo yakaenda mbali nikakurudisha
jela, na nikuongezee na kosa la uuaji.” Bale akarudi ndani ya gari.
“Nitamrudisha. Ila
naomba nikukute hapahapa sio kule.” “Unafikiri mimi nipo kama wewe! Utanikuta
hapahapa nikimsubiri. Sijamalizana naye na kama ukishindwa kumleta, jua unarudi
jela, na Naya nitampata tu. Hakuna mwanaume wakumficha Naya kwangu, nisimpate.”
Bale akaondoka akiwa ameumia sana ila Malon akafurahia kuwa amemtisha
mpaka ameenda kumchukua Naya.
Kwa Naya.
Naya alifikishwa nyumbani kwa
Joshua, hata wao waliamiani hajui alipo. Alishangaa mpaka uso ukaonekana
ameshangaa. “Karibu nyumbani Naya.” Joshua akavunja kimya maana Nanaa na mumewe
walibaki wakimtizama. Akaonekana kukosa raha kabisa. Joshua akamsogelea.
“Unakumbuka tulichozungumza hospitalini?” Naya akamwangalia. “Nitakupa chumba
chako wewe mwenyewe, hakuna mtu atakusumbua huko. Kwa hiyo usiogope.” “Na hapa
pako salama Naya. Hakuna mtu atakuingilia au kukusumbua.” Nanaa akaongeza.
Akatulia. “Twende nikakuonyeshe chumba chenyewe.” Akamsihi kwa tahadhari.
Wakaongozana.
Alimkabidhi
tu chumba cha chini. Kilikuwa na kila kitu humohumo ndani. Alichofanya Joshua
nikumuhamishia baadhi ya vitu vyake humo ndani. Hakutaka kutoka tena. “Unataka
tukawaage kina Magesa pamoja?” Akakataa. “Hamna shida, basi nitarudi.” Baada ya
kutoka kuwasindikiza kina Magesa, Joshua aliporudi akakuta mlango umefungwa kabisa.
Akajaribisha tena kufungua, lakini ukawa umefungwa kabisa na funguo
kwa ndani. Akaona asimsumbue amuache kama alivyomuahidi. Joshua
akaondoka akizidi kusononeka moyoni.
Akamuacha
mpaka jioni, akaenda kumgongea. “Naya!” Akamsikia ametoka kitandani na
kusogelea mpaka mlangoni lakini hakufungua. “Chakula kipo tayari. Twende ukale
ili unywe dawa.” Kimya. “Naya!” Akamuita tena, lakini ikawa kimya. “Unataka
nikuletee humu ndani?” Kimya. “Naomba unijibu Naya, tafadhali.” “Sitakula.”
Akamsikia kwa sauti ya chini. “Unataka nini?” “Nilale. Sijisikii vizuri. Nataka
tu kulala.” “Unatakiwa kunywa dawa. Lakini lazima ule kwanza.” Kimya.
“Naomba
uniambie ni nini kinauma.” Akamsikia akianza kulia ndani. “Mimi nipo na wewe
Naya. Naomba niruhusu nikuhudumie.” “Mimi sitaki kula.
Nasikia kutapika na kichwa kimeanza kuuma.” “Hiyo hali wamesema
itachukua muda kidogo, lakini wemesema itaisha. Pole sana. Nitarudi tena na
juisi, tafadhali naomba nikirudi unifungulie ili nikupe na dawa.” Joshua
akasubiri ajibiwe, lakini kimya. Akaondoka kwenda kufuata juisi aliyojua
anaipenda sana na alikuwa akiomba apelekewe hata ofisini. Mpishi wa Joshua
ndiye aliyekuwa kiitengeneza.
Aliporudi
akakuta mlango upo wazi kabisa, akajua anaelewa vizuri tu. Akaingia nakumkuta
bafuni akijaribu kutapika. Joshua akamsaidia na kutoka naye. Hakuwa amepewa
dawa kali sababu ya madawa ya kulevya yaliyoluwa yamekutwa mwilini. “Naomba
jaribu kunywa hiyo juisi, ni nzuri sana na ulikuwa ukiomba uletewe hata kazini.
Jaribu.” Akajifuta machozi na uso vizuri akakaa sawa na kuipokea kutoka kwa
Joshua. Akaanza kuinywa. Alipomuona anakunywa mfululizo, akajua ameipenda.
Akaimaliza. “Nzuri. Asante.” “Karibu.” Akampa na dawa.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ø Malon bado anamtaka Naya. Bale Majutoni
kukubali hasira, wivu na haraka ya maendeleo kusababisha kumwaga damu ya ndugu
zake, zaidi baba mzazi na mdogo wake asiye kuwa na hatia. Alikuwa akikubali
kila kitu anachoambiwa na Malon, je safari hii akiwa amejua ukweli kwa asilimia
kubwa sana, atamfanikishia Malon kumpata tena Naya kuepuka
kurudi jela!?
Ø Je kisasi kimeishia kwa Mbabe tu?
Ø Akiwa mke hamkumbuki kabisa, Joshua machozini mbele ya Mungu
anayeamini kumpa Naya, je, atakuja kupata happily, ever after? Kuishia
kwenye furaha na mkewe?
Ø Usikose muendelezo juu ya simulizi hii ya Mapenzi yaliyochanganywa na Pesa
kujua mwisho wake.
0 Comments:
Post a Comment