Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI&PESA! – SEHEMU YA 37. - Naomi Simulizi

MAPENZI&PESA! – SEHEMU YA 37.

Akaendelea kupiga kinanda chake kwa muda, akahisi mtu anamchungulia koridoni. Hakugeuka kwa haraka, kwa kuwa alijua ni Naya. Akamuona kwa jicho la pembeni ni kama anakaa kabisa chini, ila kwa kujificha akimchungulia. Joshua akaimba kwa muda mrefu mpaka akamaliza. Akageuka, akamkuta ni yeye ila amekaa kwa mbali sana kama asiyetaka amuone. Na yeye alipomuona Joshua amegeuka, akatambaa taratibu kurudi chumbani kwake, Joshua akimwangalia.

Asubuhi yake Joshua alifanya hivyohivyo. Asubuhi na mapema kama kawaida yake, kabla hata hajaoga ndivyo alivyokuwa akifanya mara kwa mara. Akiamka tu, anapata nusu saa ya kuimba, anamuabudu Mungu wake, kisha anaomba ndipo siku inaanza. Na walinzi wake walijua mwenye nyumba wao ameamka kwa kuimba kwake. Akaanza tena kuimba. Kwa sauti ya chini vilevile ili asimsumbue Naya kama amelala. Kwa kuwa hakuwa akienda kazini na siku hiyo akaimba kwa muda mrefu sana, sauti nzuri ya chini huku akipiga kinanda. Akahisi tena mtu kwa nyuma yake. Akajua ni Naya tena ameamka. Akafanya kama jana yake. Akakaa kabisa chini akimsikiliza. Akaimba Joshua kwa muda mrefu sana. Kuja kugeuka, akamuona amekaa amejiegemeza ukutani kama aliyelala. Akaacha kinanda kikiendelea kupiga mziki wa taratibu. Akamsogelea pale. Akawa kweli amelala. Akambemba kumrudisha chumbani. Akamfunika na kumuacha hapo.

Akarudi kama  mida ya saa nne asubuhi. Akamkuta amekaa tu kitandani akiwaza. “Upo tayari kwa kifungua kinywa?” Akakubali. “Unajua unaweza kutoka nje na kuzunguka kidogo?” Kimya. “Ukijisikia vizuri. Utoke kabisa nje ukazunguke kidogo. Na kuna sehemu nzuri tu za kukaa.” Naya hakujibu. Ila akajua amemuelewa. Akapata kifungua kinywa akarudi kulala. Mchana ikawa hivyohivyo. Kula na kurudi kulala ila akagundua anamwangalia sana kwa kujiiba.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mida ya jioni, Joshua alipokuwa ofisini kwake hapohapo ndani nyumbani kwake, simu yake ikaonyesha mtu ameshika mlango wa mbele. Akaangalia, akagundua ni Naya anataka kutoka. Akamsaidia kutoa loki. Akabaki akimwangalia. Akatoka. Alionekana ni kama aliyeoga vizuri tu, ila nywele vilevile kama ambazo hazijaguswa kwa muda mrefu na tokea hospitalini alikataa kabisa kuguswa kichwa. Alikuwa akilia maumivu wakati wote. Akajua hata hapo ameoga ila hajagusa kichwa. Akawa akimfuatilia. Akamuona kweli amezunguka na kwenda kukaa nyuma kabisa ya nyumba. Akatulia.

Alimpa kama dakika 5 hivi, akamuona kwa kupitia simu yake amekaa vilevile anaangalia sehemu moja tu bila hata kusogea. Akaamua amfuate. Akamkuta bado ameduaa tu. Akaingiwa na hofu, ikawa ni kama vile alivyofanya baada ya kumzika baba yake. “Naweza kukaa?” Naya akamgeukia. Akasogea pembeni kidogo kama anayempisha akae pembeni yake. Joshua akakaa. Kimya kikapita kwa muda.

“Kwa hiyo wewe ndio Joshua, mimi sio Joshua?” Joshua akatoa tabasamu kidogo. “Ndiyo.” Akamuona anavuta pumzi kwa nguvu, akatulia. Akamgeukia tena baada ya muda na kuuliza. “Ulisema tulikuwa tukiishi pamoja?” “Ndiyo, Naya. Wewe ni mke wangu kabisa. Na hapa ni kwetu. Hukumbuki kabisa!?” Akatingisha kichwa kukataa na machozi yakamtoka. “Sikumbuki kabisa. Najitahidi lakini sikumbuki!” “Usiwe na wasiwasi. Huna haraka.” “Itakuaje nisipo kuja kukumbuka tena?” “Labda nikueleze juu ya Naya niliyetambulishwa mimi na Mungu. Nikampa muda wa kumfahamu na nikampenda zaidi. Labda na wewe itakusaidia kukutoa wasiwasi na kujijua. Ni sawa?” Joshua akauliza kiustaarabu.

“Hata mimi nilikuwa natamani kujijua mimi ni nani!” “Acha nianze kwa kukuonyesha picha zetu.” Akamtolea simu yake akaanza kumuonyesha picha. Naya akaonekana kushangaa sana. “Unauhakika huyu ni mimi kabisa!?” “Nakufahamu wewe Naya, kwa mapigo ya moyo wangu. Ulipo popote, hata wakiwa wamekufunika, nitajua upo hiyo sehemu.” Naya akashangaa sana kusikia hivyo mpaka akatoa macho kwenye simu na kumtizama Joshua.

“Mungu alikuleta kwenye maisha yangu akijua nakuhitaji sana. Ukaja na kuenea vizuri mno.” “Hapa unaonekana unanipenda sana, hata kwa jinsi unavyoniangalia! Kila picha ninayoangalia hapa, nakuona jinsi ulivyokuwa ukinitizama!” Joshua akacheka na kurudisha macho kwenye simu yake. “Hizo ni picha zetu tulipokuwa fungate. Tulikuwa na wakati mzuri mno. Sana. Unaona hivyo unavyocheka?” Naya akabaki akijiangalia. “Ndivyo ilivyokuwa. Kulikuwa na hali ambayo, Naya!” Naya akamtizama.

Joshua akawa kama anayevuta kumbukumbu na tabasamu. “Sijawahi pata hiyo hali kwa muda mrefu sana. Pengine tokea mdogo.” “Hali gani?” “Usalama wa moyo. Utulivu kwenye hii dunia, na uhakika wa maisha kama hayo, mpaka kifo changu, kwa sababu wewe Naya uliniahidi. Ukaniapia na ukasema ni mpaka kifo.” Naya akamtizama Joshua kama ambaye hakumbuki kabisa, na kurudisha macho kwenye hizo picha. Akaendelea kuangalia hizo picha. Na Joshua alihakikisha baba Naya hayupo kabisa kwenye hizo picha. Alimuonyesha zile alizoziandaa maalumu kwa kuja kumuonyesha siku moja, wakati akiwa ametulia kama hivyo.

Naya akaangalia mpaka akamaliza, Joshua akimwangalia tu. Akamuona anarudia tena. Akatulia. “Usiwe na haraka na wala sikutegemei ufanye au uwe chochote kile. Nimekwambia kukusaidia tu. Ila nilitaka kukwambia juu ya Naya huyu uliyemsahau.” Naya akamgeukia vizuri. “Kwanza ni mvumilivu. Ana upendo mno kwa watu na anajali. Mchapakazi asiyejua kutegea. Mungu alikujalia kipaji cha ajabu sana cha ubunifu. Katika moja ya vitu vyako vilivyopo ndani, kuna kitabu maalumu. Ulikuwa ukichora wewe mwenyewe, mavazi unayobuni. Ukachagua moja ya chumba humu ndani, tukakubaliana kuwa kitakuwa chako cha mambo yako ya ubunifu. Zipo picha tulishauriana tuzitoe kabisa kwa kuzi print na kuziweka ukutani. Kwa hiyo zipo kwenye hicho chumba chako. Naya huyo uliyemsahau, alimpenda na kumchagua Joshua. Akasimama naye kwenye kila hali na wakati. Huyo ndio Naya wangu, kwa kifupi tu.” Naya alikuwa akimsikiliza kwa makini sana.

“Kwa hiyo usiwahi kujitilia mashaka. Wewe ni zaidi ya hapo akili zako zinapogota. Zaidi ya hivyo unavyojisikia sasa. Huo uvimbe ukiisha kabisa huko kwenye ubongo, daktari amesema unaweza, kurudisha kumbukumbu. Lakini mimi nataka nikwambie hivi, hata kama hutakumbuka kitu, sina wasiwasi na hilo. Naya ninayemjua mimi, ni mkubwa mno. Anaweza kuanzisha chochote na kikawa.” “Unajuaje? Pengine huo uwezo utakuwa umepotea kama kumbukumbu!” “Nisikilize na uniamini Naya. Upo uwezo wa ajabu sana Mungu ameweka ndani ya kila mwanadamu. Kutawala mazingira yake. Utashangaa sana. Unajiona hivyo ulivyo sasahivi?” Naya akajiangalia.

“Unaweza kukatwa mikono yako yote, ukiwa mkubwa hivyohivyo. Itakuchukua muda mfupi sana kuja kuweza kurudi kama kawaida. Ukaweza kula na kunywa kama wanadamu wengine." Naya akakunja uso kama asiyesadiki. "Nayaongea haya kwa kuona. Yupo binti au mwanamke ambaye hana mikono kabisa, lakini anaendesha ndege na kuyafanya yote ya mikono kwa miguu.”  Naya akashangaa sana.

“Mimi na wewe hatuyafanyi hayo kwa kuwa tunayo mikono. Na wapo ambao wana mikono na uwezo wa kuendesha hata baiskeli, lakini hawataki tu. Ninachotaka kukwambia ni kuwa, mwanadamua anao uwezo mkubwa sana ila yeye tu hajajipa muda wa kujichunguza na kutaka kutumia. Hata mimi najua kwa hakika, pengine sijafika hata nusu ya uwezo ambao Mungu ameweka ndani yangu. Na sijapoteza kumbukumbu. Nikiamua kutulia na kutafuta zaidi uwezo mwingine, nikawekeza muda wakutosha, unaweza kushangaa nakuwa Joshua mwingine kabisa na  huyu unaye muona hapa, na nikawa pengine bora zaidi. Ila sioni sababu ya kufanya hivyo kwa sasa kwa sababu hichi nilichonacho, Mungu amekiwekea mkono wake, na nimeamua kumuonyesha ninastahili ili asione sifai akampa mwingine.” Naya akaonekana kuanza kutulia.

“Ndio maana nakwambia usiogope kabisa na wala usihangaike ukijitafuta kule nyuma. Huyu Naya uliye naye sasa hivi, basi mtumie vilivyo. Mimi naamini Mungu analo kusudi lake. Ukiwa tayari, na akiona unahitaji ya nyuma, basi jua atayarudisha tu. Yaani jihesabu hivi, huyu Mungu, amekuumbia Naya mpya, akakukabidhi, ni wewe tu kutafuta kumjua. Hilo moja. Uwezo Mungu aliouweka ndani yake huyu Naya, msome. Wewe mwenyewe jifunze kuzitumia hizo karama ndani yako. Yaani inakuwa kama umenunua tv, au simu au pengine kifaa kizuri ambacho hujui jinsi ya kukitumia, ila aliyekuuzia, amekupa na kijitabu cha jinsi ya kutumia hicho kifaa. Ndio ulivyopewa huyu Naya mpya. Usiwe na haraka. Jisome. Jichunguze. Kile unachokipenda sana. Kifanyie mazoezi bila kuchoka. Jua ndicho ulichowekewa ndani yako. Fanyia juhudi mpaka ukiwezee. Utaona maisha yanaendelea bila shida.” “Wewe ni mwema Joshua! Asante. Nilikuwa nimejawa hofu sijui chakufanya!” Joshua akacheka.

“Asante. Utanifanya nitulie. Na nitaacha kutumia jina lako.” Joshua alicheka sana. “Hutaki tena kuitwa Joshua?” Naya akapandisha mabega akikataa na tabasamu usoni. “Basi turudi kwa Naya.” Akakubali akicheka kama anayetafakari. “Utakuwa sawa Naya. Na sijui kwa nini, ila naamini utafanya makubwa na mazuri zaidi.” “Asante.” Wakiwa kwenye ule wakati mtulivu, Nanaa na familia yake wakawa wanaingia getini.

Joshua akaangalia kwenye simu yake. “Nanaa na familia yake waliomba leo waje kula chakula cha usiku pamoja na sisi. Niliwakubalia. Lakini kama bado hujisikii kuwa karibu na watu wengi ambao bado huwakumbuki, basi unaweza kuendelea kuwa hapa au ukarudi chumbani ukapumzike tu.” “Sawa.” Joshua hakuelewa hiyo sawa inamaana gani! Kwamba amechagua kipi! Ila akaamua kumuacha tu. Akambusu begani, upande ule aliokuwa amekaa karibu yake, akasimama. “Asante.” Naya akashukuru. Joshua akacheka taratibu akitamani aulize ni ya nini! Ila akaona amuache tu. “Acha nikawapokee.” Naya akageuka pembeni, akamwangalia kidogo kisha akaondoka.

                                         ~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Joshua akawapokea kina Magesa. Walikuwa familia nzima. Akawapa maendeleo ya Naya mpaka hapo. “Ameanza kukubali jina lake na kuamini yeye si Joshua. Ametulia, ila bado naomba tumchukulie taratibu. Naona lipo tumaini. Leo kwa mara ya kwanza ametoka mpaka nje. Amezungumza na kuuliza maswali.” “Ulimuonyesha zile picha?” Geb akauliza. “Ameangalia, tena kwa kurudia rudia, hajakumbuka kitu.” “Bado hajamuulizia baba yake?” “Yaani ndicho namshukuru Mungu mpaka sasa, mama. Na nilipomwambia sisi tuliona na wote ni yatima, hakuonekana kujali.” “Mungu naye anasiri zake jamani!” “Acha mama. Lakini katika hilo namshukuru. Afadhali aje akumbuke taratibu na ameridhia pia hata asipokumbuka ataanza upya.” “Bora.” Wakaingia ndani. Mpishi wa Joshua alishapika na alishaandaa meza. Ila wakabaki tu sebuleni.

“Tufanyie mazoezi wimbo.” Magesa akaanza. “Kumekucha! Sasa unafanyia mazoezi mara ngapi!?” “Nilikwambia bibi, anko mwenyewe alisema ukitaka kuwa mzuri kwenye kitu lazima ukirudie tena na tena.” “Basi sasa sio umsumbue mwenzio.” “Kwani eti Liv mimi nakusumbua?” “Ndiyo.” Liv akakubali kwa haraka. Magesa akapoa, akamtizama baba yake akakuta akimwangalia. “Mimi siwezi kuimba mpaka Liv ninayemuimbia anisikilize.” Akamlalamikia baba yake kama anayetaka amlazimishe Liv. “Mimi nakusikiliza. Wewe imba. Halafu kesho kwenye  birthday, ndio atakusikiliza.” “Na mimi nakusikiliza baba mzazi. Imba mwanangu.” Nanaa akaongeza kwa mumewe. Magesa akafurahi sana. “Na kwakuwa simsumbui na bibi, na yeye atanisikiliza.” Wote wakacheka. “Anapenda kunipanga huyu! Hata haniulizi!” Bibi yake akalalamika.

Joshua akahamia upande wa kinanda chake, wote wakasogea. Akaanza kupiga wimbo wa birthday. “Sasa nyinyi msiitikie mpaka niwape ishara.” “Magesa kupenda kuongoza mambo wewe!” “Sitaki msahau bibi!” “Tunakumbuka sana. Kila saa onyo ni hilohilo! We imba bwana.” Naya akaingia taratibu kama mwenye wasiwasi. Wote wakageuka kumuangalia kule alipokuwa  akiingilia.

Akawatizama wote kwa zamu, akarudisha macho kwa Joshua. “Anti Naya! Kesho birthday  yangu mimi na Liv. Sisi tulizaliwa siku moja. Sasa unakumbuka nilivyowaimbia kwenye harusi yenu?” Naya kimya akimwangalia huyo mtoto anayeonekana kumfahamu ila yeye hamkumbuki. “Sasa kesho pia nitamuimbia na Liv. Mimi mwenyewe. Halafu nikimaliza, nawapa ishara, ndipo na nyinyi mnaimba. Ila nikiimba mimi, nyinyi msiniingilie.” Ilibidi kila mtu acheke.

“Kazi ipo!” “Njoo unisikilize. Mimi mwimbaji mzuri sana. Ila Liv yeye hataki kuimba. Anasema kichwa kitamuuma. Mimi kichwa huwa hakiniumi hata nikiimba sana.” Naya akabaki kimya palepale sebuleni mbali na walipo. Akabaki amesimama. Joshua akasimama na kumfuata. “Unataka kukaa hapa, au unajisikia kwenda kupumzika chumbani?” “Nitakaa kidogo ndipo nikalale.” “Njoo  usalimie. Nitakutambulisha kwao.” “Nimemkumbuka yule mama. Si ndiye aliyekuwa akija hospitalini?” “Sawasawa. Sasa Nanaa na Geb ndio watoto wake, hao ni wajukuu.” Joshua akawa akiwaonyeshea maana Naya alionekana kama asiyetaka kwenda kule walikokuwa wamekaa wote.

“Anti Naya, na mimi ni rafiki yako. Unanipenda sana kuliko wote!” Wakacheka kule walikokuwa. “Magesa kwa kupenda kupendwa yeye! Sasa aliyekwambia anti anakupenda wewe zaidi ni nani?” “Mimi najua. Alikuwa akiimba na mimi huku akinifundisha jinsi ya kutawala pumzi zangu wakati wa kuimba, halafu ananipigia simu kila siku na kuniambia nimsimulie mambo ya shule. Au umesahau anti!?” “Bwana wee! Acha kumchosha anti kwa maswali. Wewe anza kuimba.” Bibi yake akataka amuache Naya. Joshua akamgeukia Naya akijua ameshakataa kwenda kujumuika nao kule walipokaa.

“Basi kaa hapa.” Akakaa taratibu. Joshua akaondoka. Akaona bado wakimwangalia. Akainama kwa muda kisha wakamuona ananyanyuka. Akaenda chumbani. Nanaa akamfauta. “Nimekuletea vitu vyakuoshea nywele. Tujaribu kuosha leo ili angalau zikae sawa. Au bado kichwa kinauma sana?” Nanaa aliingia na kumwambia hivyo moja kwa moja. “Hakiumi sana. Ila wewe ni mtu mzuri. Umenisaidia sana tokea hospitalini.” Nanaa akacheka akimuhurumia. “Pole Naya. Ni vile hukumbuki. Lakini sisi ni marafiki sana.” “Sikumbuki kabisa!” “Usijali. Sisi wote tunakupenda Naya. Na tupo kwa ajili yako. Hata leo tumekuja kwa chakula cha usiku hapa ili tuwe na wewe. Twende tukaoshe nywele, halafu ukamsalimie mama.” Akakubali.

Akamsaidia kuosha hizo nywele ambazo hazikuwa hazijaoshwa zaidi hata ya mwezi. Zilikuwa zikinuka maana huyo Naya alishalazwa chooni na Malon. Na kwa kuwa zilikuwa zimesukwa chini, Nanaa alitumia muda mrefu sana kuziosha mpaka kutakata na kuzichana bila kumuumiza sana. “Najisikia vizuri. Acha nioge tena.” Akampisha hapo bafuni. Akaoga, akabadili, Nanaa akimsubiria tu. Akamchana tena vizuri. “Vaa na hereni, Naya. Nataka upendeze, utoe hali ya ugonjwa. Hata mumeo akikuona, afurahie.” “Simkumbuki kabisa!” Naya akalalamika na kuongeza. “Ila anaonekana mtu mzuri sana, na yeye mwenyewe mzuri kweli! Halafu msafi!” Nanaa alicheka mpaka akakaa.

“Usicheke kwa sauti, Nanaa!” “Basi na yeye huwa anakusifia hivyohivyo!” “Kwani eti tulikuwa na mahusiano ya aina gani?” “Mazuri sana. Natamani ukumbuke kidogo. Joshua anakupenda kupita nitakavyokwambia.” “Nimemuona! Ila sijui nifanyeje!” “Taratibu tu. Usiwe na haraka. Fungua moyo. Jipe muda. Kwa kuwa anakupenda kwa hakika, utakuja tu kujisikia upendo.” Naya akacheka kidogo na kunyamaza. Nanaa akamuona. “Ushaanza kumpenda nini!?” “Sijui!” Nanaa akazidi kucheka vile Naya alivyojibu kwa aibu kidogo akicheka kwa kujificha.

“Na mimi nataka kucheka na wewe, mama.” Magesa akaingia bila hodi. “Magesa mwanangu wewe! Umeshaimba sasa?” “Nimemwambia anko siwezi  kuimba mpaka mama yangu awepo, anisikilize.” “Jamani Magesa!” “Kwani wewe umechoka kunisifia tena?” Mpaka Naya akacheka. “Sijachoka mwanangu. Twende baba, ukaimbe.” “Na anti naye atakuwepo?” “Anakuja.” “Ila ujue anti sasa hivi umependeza sana.” Nanaa akazidi kucheka. “Magesa kwa kupenda vitu vizuri wewe mwanangu! Macho yako yanavutwa na vizuri tu!” Akacheka Magesa. “Twende sasa ukamsalimie vizuri mama yetu. Tunae mama mmoja tu hapa mjini.” Wakatoka na Naya wa tofauti na alivyoingia hapo.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Mrembo wa Joshua huyo!” Naya akacheka na kujifunika uso. Maana mama G alimuwahi tu alipowasogelea. Naya akamwangalia Joshua na kumsogelea mama G akicheka kwa aibu. “Mimi nilijua mimi ndio Joshua!” Walianza kucheka hapo mpaka machozi. “Msinicheke.” Naya akalalamika akicheka taratibu. “Mimi naomba hili swala tulizungumze vizuri.” Akaanza Nanaa. “Nanaa akanipigia simu, ananiambia tupo na Naya, lakini sasa hivi haitwi tena Naya, anaitwa Joshua.” Wakazidi kucheka, Naya akajifunika na mto.

“Sasa mimi namjua Nanaa yupo kama mwanae Magesa. Nikasema acha mimi nije, nijionee mwenyewe.” Mama G akaendelea. “Sasa Mungu naye alivyo, nafika pale nakutana na daktari wa akili. Anakuuliza unaitwa nani, nasikia Joshua!” Watu wakazidi kucheka. “Nikasema mwanangu Joshua kweli kapendwa! Mke kaamua achukue mpaka jina lake kabisa!” Naya akazidi kucheka huku amejifunika mto usoni. Ila Joshua alijisikia vizuri sana.

“Kila ukiambiwa wewe ni Naya, mwanangu unalia, unataka uitwe Joshua!” “Mimi sijui bwana! Ndio neno hilo tu lilikuwa limebaki kichwani kwangu.” “Kwa hiyo mpaka sasa hivi hukumbuki?” “Ni vile Joshua amenieleza kwa kituo na kunionyesha picha, ndio nimeamini. Lakini nilikuwa naogopa kukubali halafu nipoteze kitu kimoja tu ambacho nina uhakika nacho!” “Basi Naya mama. Wewe usiwe na haraka. Pengine Mungu ameona hataki ukumbuke ya nyuma. Anataka akupumzishe. Usijisumbue na ya nyuma, wewe songa mbele.” “Ila mimi bado sijaimba, nilikuwa namsubiria mama yangu.” “Haya baba. Imba. Na umekuwa mvumilivu kweli!” “Si hata wewe bibi umeona eeh!” “Nimeona baba. Tena sasa hivi ndio nina hamu kweli ya kukusikiliza.” Magesa akafurahia.

Akaanza kuimba, akimuimbia dada yake. Akaimba tena mara mbili ndipo akawapa ishara wampokee. Wakaimba hapo mpaka mwenyewe akaridhika. “Umeimba vizuri sana Magesa. I am so proud of you, son!” Magesa akafurahi san. “Asante dad.” “Mwanangu muimbaji huyo!” “Mpaka unajivunia mimi, mama?” “Kabisa baba mzazi.” “Asante mami wangu. Na asante bibi kwa kunipigia vigelegele. Na anko kwa kunipigia kinanda na makofi. Wewe anti hukupenda?” Akamgeukia Naya. Akawa kama amemtoa kwenye mawazo. “Nimependa sana. Umeimba vizuri.” Akacheka kwa furaha.

Joshua akamuona amebadilika kidogo. Akasimama nakumuita pembeni. “Niambie unachojisikia.” “Kichwa kinaanza kuuma.” “Pole.” Akaweka mkono wake kwenye hiyo shingo ndefu ya Naya. Akamshika vizuri na kumsogelea karibu. “Upande upi unauma zaidi?” Akamuonyesha. Joshua akamshika na kumsugua kidogo kisha akambusu hapo. “Pole sana.” “Asante.” Akamkumbatia vizuri, taratibu kwa tahadhari. “Umependeza sana Naya!” Akamnong’onoza sikioni. Akamsikia akicheka taratibu. “Nywele zinanukia vizuri!” “Nanaa ameziosha. Ni sawa nikienda kupumzika?” “Hutataka kula na kina Magesa?” Akanyamaza.

“Wamekuja hapa kwa ajili yako. Naweza kuwaambia tule sasa hivi ili ukapumzike. Au umechoka sana?” “Kwani muda wa dawa bado?” Joshua akaangalia saa. “Bado Naya. Pole. Naomba ujikaze tena kidogo.” Akakubali. Wakarudi akiwa amemshika vizuri. “Naya anataka akapumzike, lakini nimemuomba tule pamoja. Tupate muda wa kumshukuru Mungu pamoja.” “Ndio wote sasa tusimame na twendeni mezani moja kwa moja, tule ili akalale.” Akasisitiza mama G. Wakahamia mezani.

Wakala kwa pamoja, Joshua akamletea dawa palepale mezani alipokuwa ametulia kabisa, akila taratibu macho kwenye sahani yake tu kama hayupo pale. “Muda umefika?” Akamuuliza taratibu. “Ndiyo. Kunywa kitatulia.” Akameza na kutulia tu palepale mezani. Na kina Magesa wakaona huo ndio wakati wakuaga ili wamuache akapumzike. Wakaondoka.

Joshua & Naya.

Wakabakia wao wawili. “Twende nikusindikize chumbani.” Wakaongozana. “Ni sawa nikikusubiri mpaka ulale?” Joshua akauliza kwa tahadhari lakini akionyesha kujali. “Wewe ni mtu mzuri Joshua! Upo mwema.” Joshua akacheka taratibu akimuangalia. “Naomba tu ukampumzike. Kwa kuwa umenipa dawa, naamini nitalala tu.” “Nikwambie ukweli Naya?” Akatingisha kichwa kukubali.

“Bora vile ulivyokuwa hospitalini, kuliko hapa!” Naya akawa hajaelewa. “Unalala kitandani nikikuona. Lakini hapa nakuwa kule juu chumbani kwetu, wewe uko huku kwenye vyumba vya ziada! Nakuwa sijui umelalaje! Sijui unaendeleaje! Nakuwa na wasiwasi, siwezi kulala mke wangu. Nakuwa nina kazi ya kukufuata tu huku kukuchungulia kujua kwanza kama bado upo hapa, hujaondoka tena. Na pia kama upo mzima!” “Pole Joshua. Na samahani.” “Huna haja yakuomba msamaha. Ila tafadhali niruhusu hata nilale kwenye hilo kochi. Angalau usiku wa leo na mimi nilale nikiwa najua nipo karibu nawewe.” Ikamgusa sana Naya.

“Sawa.” Akakubali. “Basi acha nikasafishe kinywa kabisa na nakuvaa nguo za kulalia halafu nakuja. Nikirudi umelala, sitakusumbua.” “Nitakusubiri.” Joshua akafurahia hilo. Akatoka hapo kama akimbie. Akakimbilia bafuni, akasafisha kinywa haraka. Akaona aoge kabisa. Akayafanya hayo kwa haraka, akarudi alipomuacha Naya. Akamkuta ameshapanda kitandani amejifunika. Akaenda kukaa pembeni ya kitanda na kumshika kichwani akimpapasa taratibu.

“Kinatulia?” Akamuuliza akimbembeleza. “Natamani dawa zaidi.” “Unajua hatuwezi Naya. Pole.” “Hivi walisema ni kwa nini?” “Ila naomba usiogope.” Joshua akamtahadharisha. “Ni nini?” “Walikuta madawa ya kulevya kwenye damu yako. Niliwaomba wakusafishe. Nikawahakikishia wewe si mtumiaji. Hata pombe hujawahi kutia mdomoni. Kwa hiyo nikawahakikishia hutarudia tena. Ndio wakakubali na hilo sharti kuwa hata madawa ya kupunguza maumivu, hayawezi kuwa makali na lazima iwe kwa masaa maalumu.” “Ni nini kilitokea kwangu!?” “Hakuna anayejua mpenzi wangu. Hakuna. Nilitegemea ungekuja kuniambia ni nini kilitokea. Maana..” Joshua akamsimulia ilivyotokea mpaka mwenyewe machozi yalikuwa yakimtoka.

“Pole Joshua. Pole sana.” Joshua akaingia chooni. Akasafisha uso ndipo akatoka akionekana ametulia, akamkuta Naya akimsubiria. “Lala tu. Mimi nitakuwa hapa.” Naya akajilaza vizuri kitandani, wakati akijifunika Joshua akasogea kumsaidia. Kisha akakaa pembeni yake akimtizama. “Usilale kwenye kochi, Joshua.” “Unataka nirudi chumbani kwangu!?” Akajaribisha kwa swali. “Hapana, tunaweza kulala hapa. Hiki kitanda ni kikubwa sana, tutatoshea kabisa. Njoo.” Joshua akahisi anapewa ulimwengu. Akajipandisha kwa haraka , kama anayeogopa asibadili mawazo.

Ila akawa naye makini asianzishe jambo maana bado hakuwa ameusoma moyo wake kujua alipo. Akajiweka pembeni, ila akiwa anamfunika zaidi yeye. Wakatulia. Baada ya muda akamuhisi yeye mwenyewe anamsogolea. Akatulia tu kuona anachotaka kufanya. Akajisogeza karibu kabisa ndipo akamuwekea mkono kwa juu kama anayemkumbatia. Wakatulia kidogo.

“Joshua!” Akamsikia akimuita taratibu. Akamkumbatia zaidi. “Sijui tulikuwa tukiishije mpaka nikaondoka mara ya kwanza. Au sijui nini kilitokea, ila kwa jinsi ulivyo sasa, naona ni afadhali kuwa na wewe.” Ikamgusa sana Joshua. “Wewe ni mtu mzuri Joshua, ningetamani niwe na wewe tu, nibaki kwako. Nisiondoke.” “Ndivyo ilivyokuwa tokea mwanzo Naya. Tulikuwa na utulivu wa aina yake, na ukaniapia kubaki na mimi mpaka kifo. Hatukuwa na tatizo! Na siku nimepokea ujumbe wako kuwa umeamua kuondoka, tuliachana vizuri tena ukiwa umeniahidi usiku mzuri sana. Tuliagana kwa penzi fupi lakini lilikuwa zuri.” Akamsikia Naya akicheka, na kujificha.

“Kweli Naya. Tulikuwa tukifanya mapenzi hapa, bila kutosheka. Kila mahali kwenye hii nyumba kasoro tu hivi vyumba vya huku. Ulikuwa muda mfupi tulioishi hapa pamoja, lakini ulikuwa wakati mzuri sana uliotutoa wote majonzi na simanzi. Tukaomba Mungu pamoja kuwa hii itakuwa nyumba ya faraja. Eti baada ya muda mfupi napata ujumbe kutoka kwenye simu yako kuwa unaniacha! Nilimkatalia kila mtu. Japokuwa kule polisi walikuwa wakiniona nimepaniki tu sababu ya kuachwa, na kushindwa kunipa msaada, lakini Naya, sikuacha kukutafuta na kukufanyia uchunguzi bila kuchoka. Sema tu kuna mambo fulanifulani ya msingi nayo yalikuwa yakinikwamisha. Halafu sasa, kukawa hakuna hata funununu au dalili ya wapi upo.” Joshua akaendelea.

“Nilikufuata mpaka Mbeya kwenye sehemu nilizohisi pengine unaweza kuwepo. Nikisindikizwa na Geb. Lakini wakaniambia hawajawahi kukuona huko. Nikawa kama nimegonga mwamba. Lakini nikabaki kumuomba Mungu yeye aonaye sirini. Nilikuwa nikifanya mikesha hapa! Ijumaa kuamkia jumamosi nilikuwa nikikesha nikiomba mpaka saa sita usiku na kunilazimu kulala kwa sababu ya kazi asubuhi. Ila jumamosi kuamkia asubuhi ya jumapili, nilikuwa nikikesha nikimuita Mungu ambaye hakuwahi kunipokonya vitu anipavyo. Wakati mwingine familia ya kina Magesa walikuwa wakija kuomba na mimi. Mkesha kabisa, tukiimba na kumsihi Mungu anitendee muujiza.” “Jamani Joshua! Pole.” Naya akajisogeza kwa karibu zaidi tena safari hii akamsogelea mpaka usoni.

Akaweka mkono kifuani akaanza kumpapasa nywele za kifua taratibu. “Umesema sina ndugu? Pengine alijua nilipo.” “Ndipo huko uliashiria unakwenda. Ila pia huyo ndugu yako sikuwa nikijua jinsi ya kumpata. Kwanza ni kama alipotea, tukawa tukimtafuta wote na wewe pia hata kabla hujapotea. Kingine hakuwahi kunipenda kabisa.” “Simkumbuki. Sina kumbukumbu naye kabisa! Kwa nini hakuwa akikupenda?” “Yeye aliona sikustahili. Ni kwa kukupenda tu na kukutakia mema. Alitamani uolewe na mwanaume mwingine sio mimi.” Naya akabaki akifikiria.

“Kwa hiyo hajawahi kupatikanika mpaka sasa?” Joshua akafikiria kidogo akisita, lakini akaamua kumwambia. “Sijui kumbukumbu zako zinakurudisha mpaka wapi!” Naya akabaki kimya akifikiria. “Unakumbuka kufika ofisini kwa kina Magesa, ukatakiwa useme jina lako kamili?” Naya akabaki akifikiria. “Ulikuwa ukiumwa sana sijui kama utakuwa ukikumbuka! Ila kwenye hicho chumba kulikuwa na wanaume watatu na wewe wa nne.” “Mume wa Nanaa alikuwepo?” Naya akauliza kama anayeanza kujiwa na kumbukumbu.

“Ndiyo.” “Kuna mtu mwingine alikuwa mkali, akaanza kunipiga akisema mimi sio Joshua! Akawa akinipiga akinielewesha jina langu ila sio kama vile wewe ulivyonielekeza kwa utaratibu mpaka nikakubali japo bado mimi naamini ndilo jina langu!” Joshua akacheka kidogo akijaribu kumpoteza ili asimkumbuke Bale kwa jinsi ile. Joshua mwenyewe siku ile ni kama alikuwa tu kwenye kile chumba cha mkutano na kina Mungai, Geb, Naya na Bale. Kwani muda wote ule alikuwa akisikiliza kila kitu kinachoendelea pale kwenye kile chumba cha mkutano kwa kupitia simu ya Geb.  Geb alimpigia simu Joshua na kumuweka kwenye mute. Geb alitegesha simu yake vizuri ili Joshua aweze kusikia chumba cha jirani kwa kuweka simu yake mezani.

“Mmoja alikuwa akiongea mara chache. Ila yule tuliyekuwa tumekaa naye karibu alikuwa mkali! Tena nakumbuka alinipiga makofi wakati nilimwambia kichwa kinaniuma. Nakumbuka japo si vizuri. Kichwa kilikuwa kikiuma sana nashindwa hata kuangalia! Alikuwa nani yule! Mkali!” “Anaitwa Bale.” Naya akatulia. “Umemkumbuka?” “Hapana.” Naya akawa hakumbuki ila akaingiwa hofu. “Akija kunichukua tena?” “Hawezi kwa kuwa nimemdhibiti kisheria na nimemwambia kuwa nilikukuta na yeye ukiwa na hali mbaya, kwa hiyo haruhusiwi tena kuwa na wewe mkiwa peke yenu mpaka mimi niwepo.” Mawazo ya Naya yakawa yamechanganyika tayari, hofu imemjaa hajui aulize nini, aache nini.

“Sasa kwa nini alikuwa akinipiga!? Kwa sababu nakumbuka hakuwa ameanzia hapo.” Naya akawa kama anavuta kumbukumbu. “Alinichukua sehemu. Mbali. Tukasafiri kwa muda mrefu tu. Nikawa nikimwambia nina maumivu, lakini akawa hajali. Akaenda kunifungia au kuniacha sehemu ingine. Akawa ananifundisha kitu nikawa sielewi. Akawa ananipiga. Ila nikamwambia ni kwa sababu kichwa kinauma. Akaendelea kunipiga tu. Kwani alikuwa akitaka nini!?” “Kwanza naomba usilie. Tulia ndipo tuzungumze na usiogope Naya. Sasa hivi hakuna atakayekuchukua tena. Niambie kama unakumbuka popote ulipokuwa. Hata mazingira tu. Na hata kama si kwa hakika, hata tu kidogo pengine nitajua ulikuwa wapi au kwa nini ulipotea.” Naya akajaribu kukumbuka lakini akashindwa.

“Sikumbuki Joshua! Sijui nilikuwa wapi mpaka pale hospitalini tena kwa sababu ulikuwa ukiniambia kila wakati kitu gani wanataka kunifanyia kabla wauguzi wenyewe hawajazungumza na mimi kunihudumia. Hapo ndipo nikajua nipo hospitalini.” “Sura je? Mbali na yule unayemkumbuka mliyekuwa naye siku ile, yupo mtu mwingine unamkumbuka kumuona?” Naya akajaribu kufikiria.

“Kuna mtu.” Naya akawa kama anayekumbuka. “Niambie zaidi.” Naya akakaa kabisa. “Ni kama ndiko alikonitoa huyu wa pili.” “Anaitwa Bale.” “Huyu aliyenipiga?” “Ndiyo.” “Basi Bale ndiye aliyenitoa kwa huyo mtu mwingine.” Naya akatulia. “Unaweza kunieleza zaidi jinsi alivyo?” Akaendelea kumdodosa zaidi. “Ni kama na yeye hakutaka huyo Bale anichukue, nafikiri. Wakawa kama wanabishana.” “Wanabishana nini?” Naya akakunja uso akionekana anajaribu kukumbuka kwa juhudi zote. “Huyu Bale ndio alikuja kunichukua, nafikiri. Sasa huyu mwingine akawa anakataa kama asinichukue. Naye alikuwa na hasira na mimi. Ila sikumbuki alikuwa akiniambia nini! Ila uso wake ulijawa hasira! Akawa na yeye akinielekeza au kuniambia kitu kwa ukali lakini sikuwa nikisikia vizuri au kuelewa.  Ndio akaja sasa huyo Bale kunichukua hapo, akawa kama anakataa lakini sikujua ni kwa nini kwa kuwa sikuwa nikisikia au kuelewa. Nilikuwa naumwa Joshua!” “Pole. Pole sana. Lakini naomba jitahidi kunielekeza huyo mwingine Naya. Tafadhali mpenzi wangu. Itanisaidia kujua nakukinga dhidi  ya nani.” Naya akamuelekeza taratibu mpaka akajua kama ni Malon.

Joshua akaumia sana kuona Bale na Malon wapo pamoja. Kwamba kwa kumchukia yeye ndio Bale amekwenda umbali wote huo! Akaona anyamaze tu hata asimwambie kama ni kaka yake mpaka yatokee mazingira mazuri. “Njoo ulale ili kichwa kisianze kuuma na kushindwa kunywa dawa, maana muda bado.” Naya akarudi kujilaza.

Akatulia kidogo akamuita. “Joshua!” “Nipo macho bado. Nilikuwa nikiwaza.” “Umeshajua jinsi ya kunilinda lakini? Ili wasinichukue tena.” “Ndiyo Naya. Hutatoka peke yako tena kwa muda mpaka upone kabisa wakati huo nikitafuta jinsi ya kuwadhibiti waliokuchua.” “Umeshawajua?” “Ndiyo. Mmoja anaitwa Bale na mwingine Malon. Popote utakapowaona uniambie.” “Sawa.” Naya akakubali.

“Na wakikwambia uende nao popote kule, usikubali.” “Nitakwambia pia. Ila usikubali ikatokea nakutana nao tena. Sawa Joshua?”  “Nitajitahidi na hata ikitokea wanakusogelea, nitahakikisha hakuna wakukuumiza tena, sawa?” “Sawa.” Naya akaridhika.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Walilala usiku huo Joshua akimbembeleza kwa kuwa kichwa kilikuwa bado kikimuuma ila sio sana. Akalala akikumbatiwa na kubembelezwa. Asubuhi aliamka mapema tu ndio ilikuwa siku ya birthday ya watoto wawili wa Nanaa. Walizungumza wao wawili Nanaa na Joshua, hawakumwambia Naya. Nanaa akafika hapo asubuhi kumchukua, aliwakuta wakipata kifungua kinywa.

“Nimekuja kukuchukua Naya. Twende wote nyumbani. Tukaandae sherehe ya watoto. Itakusaidia kuchangamka.” Naya akamwangalia Joshua kwa wasiwasi. “Utakuwa sawa, usiogope.” “Tunakwenda wote!?” Naya akamuuliza kwa wasiwasi kama ambaye hataki. “Nakwenda kazini kwa masaa machache kisha nitakuja na mimi.” “Kwa hiyo sasa hivi tunakwenda bila wewe!?” Nanaa akajua kazi itakuwepo, akavuta kiti akakaa karibu yake. Akaanza kumueleza uzuri wakutoka hapo na kuweka akili kwenye shughuli mbalimbali. “Lakini sio na Joshua?” Akawa kama bado hajaridhika. “Joshua atakuja baada ya kutoka kazini.” Naya akatulia kidogo na wasiwasi mwingi usoni. Joshua akamuhurumia.

“Naomba nikazungumze naye. Nitarudi Nanaa. Twende Naya.” Akamshika mkono kumsaidia kusimama. “Umesema hatuendi wote?!”  “Mimi nitakuja, na sitakawia.” “Uliniambia utahakikisha wale watu hawanisogelei Joshua! Wakinifuata wewe haupo, si watanichukua tena?  Naona mimi nibaki tu hapa ndani wakati wewe ukienda kazini. Nisitoke. Tafadhali Joshua. Sitaki kuumwa tena.” “Naomba usilie. Nanaa anawafahamu na anakupenda. Atakulinda. Kwa sasa sitamuamini yeyote yule na wewe isipokuwa Nanaa, Geb na mama G. Ni hao tu kwa sasa. Ukiwa nao hao sitakuwa na hofu kwa kuwa najua utakuwa salama. Na ninakuahidi sitachelewa. Nitakuja hukohuko ili tuwe wote. Nahitajika sana kazini ndio maana inanilazimu niende, na mama naye ameomba upelekwe, ili utoke ukawe na wenzio, ukawasaidie kupanga mambo. Itakusaidia.” Ikabidi Naya akubali.

 Nanaa akaenda kumsaidia kuchukua nguo aliyojua atavaa baadaye kwenye shuguli akambebea vitu baadhi, wakawa wanatoka. “Joshua amesema hatachelewa.” Akawa anaongea kama anayejifariji. “Utakuwa sawa Naya. Usiogope.” “Hata Joshua ameniambia hivyohivyo.” Akageuka, akakuta Joshua akiwasindikiza kwa macho na yeye kama asiyekuwa ameridhia tena. “Si unakwenda kazini, halafu utakuja na wewe?” Akawa kama anayetaka uhakika tena akionyesha wasiwasi mkubwa. “Nitakuja Naya, na sitachelewa. Nenda ukafurahie na Nanaa pamoja na wengine.” Wakatoka. Njiani Nanaa akamuona ametulia sana. Amejawa wasiwasi. Kila alipomuongelesha akawa kama haelewi tena au hasikii. Akaona amuache tu na waende hivyohivyo kwani walikusudia kumtoa ndani.

Kwa Kina Magesa.

Walifika nyumbani wakawakuta mpaka Grace na wanae wote wameshafika hapo na watoto wake. Kukawa na shamra shamra hapo, Naya amepoa akiangalia tu. Akakataa kula kitu chochote hata maji, akabaki kimya tu. Nanaa akamfundisha kufunga zawadi akaelewa. Akaanza kufunga ila hazungumzi na akili kama hazipo hapo. Baada ya muda akamuita Nanaa. “Joshua alisema atakuja. Alimaanisha hapa au nirudi kule nikamsubirie? Asije kurudi kule akanikosa.” “Joshua atakuja hapa Naya. Naomba uwe na amani. Hapa hakuna mtu atakuja kuingia na kukuchukua. Umesikia?” Nanaa akajaribu kumtuliza. Akaonekana kama hajaridhika. “Au nimpigie simu uzungumze naye?” “Hapana, amesema yupo na kazi.” Akajirudi na kutulia kabisa.

Mambo yakaendelea yeye akiwa ametulia. Hata walipomteta hakuwa hata akielewa. Kila aliyeingia mlangoni na kutoka, alidhani ni Joshua. Macho yakawa mlangoni wakati wote. Wakahamia kuweka sawa nje sehemu ya maua ambapo watu watakutania kwa shuguli hiyo nzima ya birthday ya watoto hao wawili wa Magesa. Mama G akampa kazi kumfanya asifikirie zaidi ila kazi aliyokuwa akifanya.

Atafutaye Hachoki.

Naya akajikuta amebaki yeye peke yake hapo nje na watoto wakicheza. Akakaa tu akiangalia watoto lakini akili kwa Joshua akiangalia getini. Mlinzi akamsogelea. “Unaitwa na mume wako hapo nje.”  Naya kwa haraka akasimama kama akimbie. Kutoka hakumuona Joshua. Akasogea mbele zaidi kumtafuta. Akamuona Malon. Naya akashituka sana, maana alimkumbuka kuwa ndiye aliyekuwa naye kabla ya Bale kumchukua. Akakumbuka alikuwa akimzungumzisha kwa hasira. Akaanza kurudi nyuma taratibu akitetemeka. “Nitakuumiza Naya, njoo.” Naya akataka kama ageuke, akimbie. Malon akamgundua na kumuwahi kumtisha. “Ukisogea hata hatua moja nyuma nakuhakikishia nitakuumiza, Naya.” Naya akasimama akitetemeka, akaanza kulia.

Naya huyu amekuwa kama asiye na akili nzuri. “Unanielewa?” Naya akatingisha kichwa kukubali akilia. “Haya njoo.” Naya akajifunika uso akaanza kulia palepale aliposimama bila kuweza hata kusogea. Malon akamsogelea akamshika mkono kwa nguvu akaanza kumvuta akirudi naye garini kwake.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment