Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Chozi Langu! - SEHEMU YA 12. - Naomi Simulizi

Chozi Langu! - SEHEMU YA 12.

 Mara Ya Pili.

W

akiwa kwenye ndege Nelly akamuona anachukua mkono wake na kuusogezea kwake. Akajiweka sawa kutaka kujua anachotaka kufanya. Akauweka vizuri katikatika ya mkono wake mkubwa kisha akaunyanyua na mkono wake na kufanya kama anavyopenda kufanya wakati wote. Akawa ameegemeza kichwa chake kwenye hiyo mikono, ikabidi Nelly amgeukie vizuri ili asiumie ubavu. Ni viti vya ‘first class’. Vikubwa na nafasi yakutosha. Akajiegemeza kwenye kiti, Billy amejiegemeza kwenye mikono yao akimtizama.

          “Ulikuwa ukiwaza nini? Maana hujaongea tokea tumeondoka Dar.” Nelly akacheka kwa kufikiria kidogo kisha akamwangalia. “Nilikuwa nikijiuliza juu yako.” “Sasa umepata jibu gani?” “Sijapata.” “Sasa kwa nini usiniulize mimi mwenyewe?” Nelly akafikiria na kumwangalia. Billy alitulia tu akimtizama. “Kwa jinsi ulivyompenda Anele. Amekuzalia watoto unaowapenda hivyo. Akakupitisha alikokupitisha mpaka ukaumia kwa kiasi hicho, unafikiri unaweza kuja kumpenda mtu mwingine kwa kiasi hichohicho.” Billy hakutegemea hilo swali, akabaki ametulia tu.  “Ndicho nilichokuwa nikiwaza. Anele yupo na hatawahi kuondoka kwenye maisha yako. Mtu mwingine anaingiaje katikati yenu?” “Kama Carlos aliweza kupenya katikati ya familia kama ile tuliyokuwa nayo, hapakuwa na ugomvi Nelly. Na mimi najijua, si mtu mkorofi na huwa si mtu wa kugomba. Kukiwa na utulivu wa namna ile, akaweza kupenya katikati yetu. Ndani ya urafiki ule kama ndugu, akaweza kuuvunja, na kuchukua familia yangu, na anaweza kuishi katikati yetu bila shida! Sijui ni kwa nini, ndani ya moyo wangu naamini kabisa, sijakata tamaa, naamini kwa asilimia 100, na mimi nitapata mtu wangu atakayenipenda na mimi kwa dhati. Kama Carlos anavyoweza kwa Anele, na mimi naamini, huyo aliyeandikiwa na Mungu kuwa wangu, ataweza tu.” Nelly akapoa kabisa.

          “Sijui itakuaje, lakini maadamu atajua ananipenda mimi, na mimi ni wake, nina uhakika atasimama na mimi. Sijakata tamaa Nelly. Hata kidogo, sijakata tamaa.” Nelly akamwangalia. “Mama yangu huwa anakuwa na wasiwasi eti kwamba nitakuja kuishia peke yangu. Hata jana nilizungumza naye na kumwambia, labda Mungu anichukue mapema, lakini sijakatia tamaa mapenzi. Inaweza isiwe kwa haraka kama ambavyo ingetarajiwa, lakini naamini ipo siku, Nelly. Ipo. Na mimi nitapendwa kwa dhati.” “Ni muda gani tokea muachane?” Nelly akauliza.

          “Niseme tokea aniache. Maana mimi nikiingia agano, huwa sijui kuvunja aisee. Ilibidi kutafuta mwanasheria, anisomee talaka yangu na ajue anachokitaka. Nikamwambia kama akiona kipo sawa, anipe tu niweke saini, basi. Na kweli alinisaidia sana. Yeye ndiye aliyekuwa akikutana naye pamoja na mwanasheria wake. Akampa anachokitaka, nikaweka saini. Wakafanya utaratibu wa kunitolea vitu vyangu pale ndani ya nyumba. Nikawaomba wakaviache kwa wazazi wangu. Nikawaachia nyumba yangu, wakaendelea na maisha yao.” “Pole Billy.” “Kujibu swali lako nafikiri ni miaka 10 sasa tokea hayo yote yatokee. Kama imezidi ni kidogo au pengine nakaribia 11.” Nelly akatulia kidogo.

          Akaona aulize tena. “Kwa miaka yote hiyo, hujawahi kuwa na mahusiano tena?” “Nimekua nayo, lakini si ya uhakika. Ya kawaida tu.” “Unamaanisha nini?” Akamuona ni kama anayefikiria kisha ni kama akapata jinsi ya kueleza. “Niliingia kwenye yale mahusiano nikijua ni nini anataka kwangu. Na mimi sikujali kwa kuwa sikuwa nimepona. Nilihitaji tu mtu wakuwa naye, nisijikute peke yangu. Basi, ikaendelea hivyo mpaka nilipoona nipo sawa, nikasitisha.” “Yeye alitaka nini?” “Billson, Director wa World bank.” Billy akajibu bila wasiwasi. Nelly akamwangalia na kugeukia pembeni.

          “Wewe ulishakuwa na mahusiano?” Nelly akageuka. “Kuna mambo nilipitia hapo nyuma, yalinichefua mno. Nimeshindwa kabisa kuwa na mahusiano ya kimapenzi. Kwanza si kitu nafikiria.” “Hudhani kama unaweza kuja kupendwa?” “Sijui Billy. Nahisi ni kama sipo tayari kupita hiyo njia! Wengi ninao waona wapo kwenye mahusiano, hawajanipa sababu ya kutamani walichokuwa nacho. Najiona ni afadhali mimi hivi nilivyo na niliyonayo kuliko kuongeza kitu kingine au mwanadamu mwingine kwenye maisha yangu.” Nelly akafikiria kidogo.

          “Nimekuja kumwangalia mwanadamu, aisee ni kiumbe cha hatari kuliko simba.” “Kwa sababu sisi tuna akili na utashi, Nelly. Sisi tumepewa uwezo mkubwa mno. Ni miungu wadogo. Sasa unafikiri kwa sifa hizo unafikiri sisi si hatari?” “Ndio hicho kinachoniogopesha kwa mwanadamu.” “Umeshawahi kufikiria, ukija kupatia?” “Sijui Billy. Sijaona waliopatia. Na kama kweli wapo basi pengine wapo wachache sana.” “Mimi nimezungukwa na mifano mizuri sana ya waliopatia, Nelly. Sana. Wazazi wangu na ndugu zangu wanandoa nzuri sana. Mno. Mpaka nimekuja kuamini si sura au rangi ya mwili, ila mtu tu. Mdogo wangu huyo anayenifuata, ameolewa na mwanamme anayempenda sana. Wanawatoto wao na wametulia kwenye ndoa yao. Kaka yangu hivyohivyo. Sasa nawezaje kusema hakuna mapenzi ya kweli?” Hapo Nelly akanyamaza.

          Akaubusu mkono wake, Nelly akamwangalia. “Sio wanadamu wote ni wabaya Nelly. Ila wengi wabaya wanatuachia madonda ambayo shetani anayatumia vibaya. Zaidi kutuogopesha. Mimi naamini ninao upendo mkubwa tu na uwezo wa kuushiriki na mwanamke mwingine mbali ya Anele. Sikuumbiwa upendo mdogo kiasi cha kuishia kwake tu. Naamini Mungu wa second chance. Nafasi ya pili. Na kama nilikosea kwa Anele, nakusudia kutengeneza pale Mungu atakaponijalia nafasi ya pili. Nimejibu swali lako?” “Yeah. Na nashukuru umekuwa muwazi sana na ukafafanua kwa undani.” Billy akacheka na kutulia kwa muda.

          “Tunakwenda ice skating.” Nelly alicheka sana. “Billy!” “Nimepatia?” “Sana! Nilishakuwa na hamu nayo! Asante.” Nelly akaendelea kucheka, mpaka Billy akafurahia. “Umejuaje kama...” Nelly akafikiria akakumbuka alimwambia kwamba alichukua mafunzo yake baada ya kumaliza shahada yake ya 3. “Kumbe huwa unanisikiliza na unatilia maanani!” “Sana. Kwa kuwa huwa sina muda wa kupoteza. Kufikiria, na kuhakikisha nakumbuka hata vitu vidogodogo visivyo na maana kwa wengine ndio asili ya mafanikio yangu.” “Nimefurahi sana.” “Nimekuona.” “Ila sijui kama nitakumbuka! Ni muda mrefu sana.” “Mimi ni mjuzi. Binti yangu huyo mkubwa ndio mchezo anaoupenda. Ni ice dancer. Aisee Mungu alimjalia. Isingekuwa juhudi za shule, angafika mbali sana. Alikuwa akishiriki kwenye mashindano yake, anamedali nyingi sana.” “Hongera Billy.” “She is so beutiful. Ni mzuri sana. Wa kila kitu.” Nelly akacheka.

          “Ungependa nikuonyeshe?” “Tafadhali.” Nelly akajibu akicheka. “Halafu anaakili sana. Ile ya darasani!” “Eeh!” “Anayo. Mungu alimjalia. Na lazima kila siku anisikie na kuniona. Ananipenda sana na anampenda sana Mungu. Mwadilifu tokea mtoto mpaka nilikuwa namwambia mama, wakati Mungu anamuweka kwenye mikono yangu kwa mara ya kwanza amezaliwa, alikuwa akinikabidhi tumaini jipya hapa duniani.” Akatoa simu na kutafuta picha zake. “Hii ni ya jana akiwa kazini kwake.” Nelly akamwangalia na kushangazwa. “Billy! Huyu ni binti yako?” “Oooh yeah. That’s my baby girl.” Akamwangalia Billy. “Ni mzuri kama mwanamitindo!” “Nilikwambia.” Billy akaongea kwa kujivuna.

          “Sasa anafanya nini?” “Ni business Analytical. Na nimzuri kwenye fani yake. Mzuri kwenye namba ndio maana hiyo fani ameiwezea.” “Hongera sana Billy!” “Unaponiona napanda taksii jioni au natumia dereva kunirudisha kupumzika baada ya kazi, basi ujue ndio muda natumia na hao watu wawili kwenye simu. Yeye na mama. Nikiwa nimechoka, nawapigia wote kwa wakati mmoja ili waniulize maswali yao yanayofanana, kama nipo sawa, nimekula, kazi ilikuaje, mbona nimechoka!” Nelly akaanza kucheka. “Wote wanakuuliza hivyohivyo?” “Hivyohivyo na kila siku.” Nelly akacheka na kukumbuka.

          Akaona aulize tu. “Sasa kama siku ile tulikuwa wote mpaka panakaribia kupambazuka kule Unguja, si watakuwa walikokukosa kwa simu?” “Walijua nipo na wewe.” Nelly alishituka mpaka akapaliwa na mate. Alikohoa na kukohoa. Billy akamuita muhudumu awape maji ya kunywa. Akampa. “Pole.” Nelly akayanywa yote na kuanza kujifuta machozi sababu ya kukohoa. “Aisee pole. Upo sawa?” Nelly akatingisha kichwa kukubali huku akijifuta uso.

          Wakatulia. Na Billy naye akanyamaza kama kumpa nafasi ya kutulia. Nelly akamrudishia simu yake. “Hutaki tena?” Billy akamuuliza akimcheka. “Subiri kwanza Billy. Wewe unawaambia upo na mimi kama mfanyakazi mwenzio?” Billy akazidi kucheka. “Acha kucheka bwana!” “Kwani wewe unafanya kazi World Bank?” “Billy?” “Kumbe ndio paliwa yote hiyo! Acha wasiwasi wewe.” “Sasa unawaambia upo kikazi?” “Hivyo ndivyo umemuaga Jax nini?!” Billy akamuuliza kwa kumshangaa kidogo.

          “Eti Nelly? Maana mimi sina sababu ya kudanganya. Sina chakujificha. Tena baada ya kuwaaga hivyo na kuwaambia tunaenda ice skating Afrika ya kusini, ona jumbe zao hizi.” Nelly akachukua tena simu yake na kuanza kusoma ujumbe wa mama yake. ‘Treat her right.’ Mama yake huyo. Binti yake akamwandikia, ‘Tafadhali furahia baba. Hakikisha unafungua moyo na kufurahia kila moment na Nelly. Mungu yupo na wewe, hajakuacha na anakuwazia mema. Nakupenda zaidi ya dunia yenyewe. Nipigie ukitulia, uniambie iliendaje. Nakuombea.’ Mpaka Nelly akapata vipele kama vya baridi. Akamtizama Billy.

          “Hizo jumbe ni za asubuhi hii wakati nakuja uwanja wa ndege.” “Naomba kumuona na mama yako.” “Umemuagaje Jax?” “Billy!” “Nataka kujua.” “Mimi na yeye hatuna mahusiano kama hayo yako na mama yako au binti yako. Sihitaji kujieleza chochote kwake. Niliamka asubuhi na mapema kumpikia, kuhakikisha leo anacho chakula pale nyumbani. Maana yupo kwangu. Nikampikia na kumwambia kimtoshe mpaka kesho nitakaporudi. Basi.” “Unajali, Nelly!” “Kwa sasa hana mtu mwingine ila mimi. Ameudhi watu.” “Kwa kuahirisha ndoa?” Nelly akashangaa sana.

          “Inamaana wewe unatujua kwa kiasi kikubwa hivyo!?” “Ukweli nawafahamu. Ehe?” Nelly akamwangalia na kuendelea. “Kwa hiyo yupo. Na nimemuona amekusudia kunionyesha kwa vitendo kwamba amebadilika na anajutia. Amejirudi mpaka namuhurumia tena. Hajawahi kunijali kama anavyonijali sasa hivi. Amebadilika.  Kwa hiyo kujibu swali lako, sisi hatuna utaratibu kama huo wa kuzungumza kila kitu.” Akaridhika na kumuonyesha mama yake.

          “Anaonekana bado ananguvu! Halafu mmefanana, nafikiri na binti yako amepata uzuri kutoka kwake. Na naongea hivyo kwa kuwa simfahamu Anele.” Hapo Billy hakujibu. “Umebahatika Billy! Mimi sikuwa na aina hii ya mahusiano na mama yangu.” “Katika hilo hata mimi najua. Mama ananipenda na kunijali sana. Sisi watoto wake ndio kila kitu chake. Na yupo hivyo kwa wote. Namshukuru Mungu.” “Nionyeshe mtoto wako mdogo.” Ni kama Billy akasita, kisha akachukua simu.

          “Sijui kama nina picha zake za hivi karibuni. Maana nyingi anakuwa na Carlos na Anele. Kila nikizipata huwa sizitunzi kwa muda mrefu. Zinakuwa zikiniumiza tu.” “Kwani Carlos hakuwa na mke wala watoto?” “Hapana. Ila sasa hivi mwanangu ndio kama mtoto wake. Ila anampenda kwa ukweli. Ni wivu tu kuona anammiliki binti yangu. Ila anampenda sana. Na kwa kuwa na yeye anapenda kupendwa, na kule amejikuta ndio mtoto wa pekee, anapenda sana hayo maisha.” “Huyu mkubwa huwa haendi?” “Hataki hata kuwahisi.” “Sasa huwa anakutana vipi na mdogo wake?” “Nyumbani kwa wazazi wangu. Wanawapenda sana bibi na babu yao. Na baba ndiye alinishauri nimuache tu kwa Carlos. Wote wanamfahamu Carlos. Hakuwa mtu mbaya. Kwa hiyo acha nitafute picha yake kama ninayo.” Akatafuta mpaka akapata moja akiwa na wazazi wake.

          “Hii familia yenu inachanganya. Mnafanana!” Billy akacheka. “Nafikiri mama ndiye ametupa damu yake ndio maana tunafanana.” “Hata wazazi wenu wenyewe wanafanana.” “Tulikuwa tukimtania baba kuwa alioa ndugu yake. Nafikiri ni hiyo rangi ya weupe na kuishi muda mrefu pamoja.” Ilikuwa familia nzuri sana. Walionekana wamefanikiwa. Na kweli kulionekana kuna amani. “Hiyo ni chrismass ya mwaka jana. Wote tulikutana nyumbani kwa wazazi.” Mpaka wanatua uwanja wa ndege wa Johannesburg, Africa Kusini, Nelly alikuwa akiwafahamu ndugu wa Billy wote, kasoro Anele na Carlos.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

          “Tutaelekea hotelini kupumzika na kupata chakula cha mchana. Nimepanga skating ni saa 10 ya jioni. Kisha twende tukaangalie sinema baada ya hapo. Ni ratiba nzuri?” “Sana. Nimefurahia skating.” Billy akacheka. Dereva aliyekuwa na jina kamili la Billson waliyemkuta hapo uwanja wa ndege akiwasubiria, akawapeleka hotelini. Kama kawaida ya Billy alichukua vyumba viwili.

          “Ni sawa tukienda kwenye masaji wote wawili au ungependa ufanyiwe chumbani kwako?” “Hamna shida. Twende wote tu.” “Basi baada ya kama dakika 15, nitakugongea chumbani kwako.” “Sawa.” Vyumba vyao havikuwa mbalimbali. Vilipakana kabisa. “Billy?” Billson akageuka kabla hajamfungulia mlango wake. “Nilikuomba kukusaidia kulipia.” “Usijali, nilishalipia kila kitu.” Akafungua mlango akamkaribisha na yeye akaingia. “Naona pazuri, patakufaa kwa usiku huu.” “Nashukuru. Asante.” “Karibu. Acha basi na mimi nikaweke vitu vyangu kisha tutoke.”

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

          Muda wote wa skating Nelly alikuwa akicheka sana, tena kwa sauti ya juu mpaka Billy alijua akifurahi. Na akaja kugundua Billy alikuwa mjuzi sana. Aliweza kucheza nyimbo mbalimbali juu ya hiyo barafu na viatu hivyo vya ncha nyembamba chini kama soli, bila shida. “Nifundishe Billy.” “Ni kutafuta tu balance na ondoa woga. Hivyo hivyo unavyoskate, sasa ongeza hatua za kucheza, na jua mimi nipo kukudaka, hutaanguka.” Wakaendelea. Na dj aliyekuwepo hapo alikuwa akiweka nyimbo mbalimbali huku watu wakiendelea kuskate. Wakapata wakati mzuri sana. Wakatoka hapo kuwahi sinema.

  Billy alimuona vile alivyojawa na furaha. Huyu si Nelly aliyesikia habari zake na wala siye aliyekutana naye kwa mara ya kwanza. Alikuwa akicheka kwa sauti ya juu kabisa tena mpaka machozi. Hilo lilimfurahisha sana Billson. Akaona pesa yake haijapotea bure. Walitoka sinema ambayo iliwatuliza kimawazo na kuwaacha wakitafakari.

          “Maisha hayatabiriki. Na wakati mwingine ni rahisi kuchezea nafasi.” Wakawa wakizungumza baada ya hiyo sinema, wakiwa wameshashushwa hotelini. Walikaa sehemu ya nje tu wakiendelea kuzungumza upande wa mgahawa kwenye hiyohiyo hoteli kubwa ya kitalii. “Hilo nililiona kwa baba yangu. Unajua baada ya manyanyaso yote hayo kwa mama, akamuua kwa gonjwa la Ukimwi!” “Pole sana Nelly.” Ila akagundua ni kama hakushangaa. Akawa kama aliyekuwa akifahamu.

          “Sasa tulipoachwa naye sasa, akawa hajui chakufanya na sisi. Mimi asiyenitaka, na huyo mtoto wa kiume aliyekuwa akimpigia kelele. Akimtaka kwa hali na mali. Hakuna wakumtumikisha tena. Pesa anayo lakini mama hayupo. Haikuchukua muda akaamua kujinyonga. Na wala yeye hakuugua sana. Na ninauhakika kwa pesa aliyokuwa nayo, angetumia dawa na kuendelea kula vizuri, angekuwa sawa tu. Lakini ninauhakika alifika mwisho.” “Ikawaje baada ya hapo?” Billy akauliza.

          “Ilikuwa mbaya sana Billy. Imeharibu maisha yangu yote.” “Hapana Nelly. Usikubali huo uongo wa ibilisi. Hakuna mwenye uwezo wa kukuharibia maisha ila wewe mwenyewe na Mungu. Na mara ya mwisho nasoma bibilia yangu, Yesu mwenyewe alisema kwenye kitabu cha Yohana 10:10. ‘Nalikuja ili wawe na uzima, tena wawe nao tele.’ Sijui kama unanisikiliza?” Nelly akanyamaza. “Tena hapo ni baada ya kueleza anachokifanya shetani. Kwamba yeye ni mwizi. Anakuja ili kuua, kuangamiza na kuharibu. Ila Yesu yeye ni mtengenezaji. Sikatai kwamba kuna mapito tunapitia na yanaathiri maisha yetu! Najua kwa kuwa na mimi nilipitishwa hapo. Lakini nilikataa Carlos na Anele wawe ndio wa mwisho kuandika historia ya maisha yangu. Naitafuta furaha kwa hali na mali nikiamini na mimi siku moja nitakuja kupumzika. Usikubali Nelly. Mapenzi ni mazuri mno. Nilijaribu nikaona na kujua ni bora kuliko uchungu na kubaki mpweke.” Nelly akavuta pumzi kwa nguvu, akatulia.

          “Niambie ilikuwaje?” “Kama unakumbuka nilikwambia ni kama baba alikataa kunisomesha. Kwa hiyo mama akamuomba kaka yake mmoja ambaye anao uwezo wa kipesa awe anamsadia kunitunza na kunisomesha. Na mimi Mungu alinisaidia uwezo wa darasani, hata mama akajua. Ndio akamsihi sana mjomba na mkewe waniendeleze. Mjomba akakubali. Akawa akisaidia ada. Sasa kipindi hicho kuna shule fulani hivi zipo mkoani Tanga, wilani Lushoto. Ni shule za masista. Sasa hivi inachukua wasichana kwa ngazi ya sekondari. Lakini wakati ule walikuwa wakichukua mpaka shule ya msingi. Sasa mimi na mtoto wa mjomba, ni kama tunalingana, ila yeye alinizidi miaka miwili, ila tulikuwa darasa moja kwa kuwa mimi nilivushwa darasa. Tulipokwenda kufanya mitihani ili kuingia kwenye ile shule, kwa kulipiwa na mjomba, mimi nikachaguliwa, mtoto wake akaachwa. Kile kitu kilimuuma sana shangazi, yaani mke wa mjomba.” Nelly akaendelea.

          “Kukawa kama na kubadilishwa mawazo. Hawataki tena kunisomesha. Muhula wa kwanza mama akahangaika sana, akafanikiwa kunipeleka kwenye hiyo shule kwa wakati ili nisikose nafasi kwa sababu ni shule ambayo ilikuwa ikililiwa sana na watu. Niliweka juhudi Billy, usingenikuta sina kitabu mkononi endapo napata nafasi. Nilikuwa nikikazana nikijua baba ananidharau, na mama yangu anahangaika. Basi, nikawa mtu wakupata 100 tu. Ndipo nikapata ufadhili sasa kutokana na hayo matokeo. Masista wakawa wakinilipia kila kitu, kazi yangu kusoma tu. Likizo nyingine nilikuwa nikibaki tu pale shule.” “Kwa nini?!” Billy akauliza kwa kushangaa.

          “Mazingira ya nyumbani yalikuwa mabaya Billy! Mabaya sana. Zaidi baba alipokuwa akiwepo. Badala ya kufurahia mapumziko, ilikuwa ikininyong’onyeza sana. Halafu pia kama nilivyokwambia, hatukuwa na mahusiano mazuri na mama yangu. Wakati mwingine nafikiri kwa kunihurumia pale baba alipokuwepo, alikuwa akinipeleka kwa mjomba kumalizia likozo yangu huko. Sasa hapo kumbuka mahusiano yangu na shangazi yalishaharibika. Binti yake ambaye nilikuwa naye umri mmoja alishanichukia akisema nilichukua nafasi yake. Kwa hiyo likizo hazikuwa nyakati nzuri kwangu. Ilikuwa bora kukaa tu shuleni, labda niwe nimeishiwa sana. Ndipo ilikuwa ikinilazimu kwenda likizo kwa mjomba ili kunisaidia ninaporudi shuleni.”

          “Anyways, ile shule ya msingi ikaisha, nikaingia tena sekondari palepale na nikawa nalipiwa tena ada, ila michango mingine ikawa ni mama. Nikaendelea vilevile mpaka nilipokaribia kumaliza kidato cha nne ndipo mama akafariki akiwa amemuacha Jax na msichana wa kazi tu pamoja na baba. Mambo hayakuwa mazuri, nilipomaliza kidato cha nne, nilifaulu, mjomba akanitafutia uhamisho ili niwe pale Dar. Kwa kuwa nilifaulu vizuri, haikuwa shida. Nikaanza hapo. Sasa katikati ya kidato cha 5, ndipo baba akajinyonga. Ukumbuke nilikuwa sijafikisha miaka 18. Nisingeweza kurithi chochote na wala nisingeweza kuaminiwa kumtunza Jax.”

          “Halafu hapo ukumbuke nilianza darasa la kwanza nikiwa na miaka 5. Nilimaliza darasa la 7 nikiwa na miaka 11. Kidato cha nne nilimaliza hata mika 15 sijafikisha. Baba anajinyonga ndio nilikuwa nakaribia 17. Kukawa kama kuna dalili za kuchukuliwa na mmoja wa kaka zake baba ambaye na yeye akili yake ilikuwa kama baba tu.” “Ikoje?” Billy akauliza.

          “Kuwa mtoto wa kike si wakusomesha. Na hapo akawa alishasema nimesoma vyakutosha, nitafutiwe mume niolewe. Halafu Jax atunzwe na mkewe, wanachukua nyumba yetu. Na yeye alikuwa mmoja wa watu waliochangia kumnyanyasa sana mama yangu. Nikafikiria kwa haraka, ikabidi kumfuata mjomba. Yuleyule aliyekuwa akinisaidia maswala ya shule, nikamuomba anitetee kwamba nipo umri sawa na binti yake.” “Yasinta?” Hapo ndipo alipojua ni wapi anapata habari zake.

          “Ulimfahamia wapi Yasinta!?” Billy akacheka. “Nimalizie kwanza hiyo habari.” Nelly akakunja uso na kuendelea. “Mjomba akakubali ila akaniambia nilazima nianze kuonekana na kuishi kama niliyekua, sio mambo ya kitoto. Nikakubali kwa haraka bila kuelewa anachomaanisha. Siku moja akaja nyumbani akaniambia lazima tuzungumze. Bado tulikuwa na msichana wa kazi ambaye alikuwa akinisaidia sana maswala ya Jax.”  Nelly akacheka kwa kusikitika.

          “Tukahamia kuzungumza kwenye chumba kilichokuwa cha wazazi na mimi nilikuwa naogopa sana kuingia humo kwa kuwa ndipo alipojinyongea baba. Basi, mjomba akaanza kunipa mikakati aliyofikiria tufanye ili kufanikiwa. Maana wakati huo ni kama yeye aliachwa awe anatusimamia mpaka mahakama itakapoamua.” “Kwani baba hakuacha mirathi kwa yeyote?” “Hapana Billy. Yule mtu alikuwa mbinafsi wa kupitiliza. Hawezi kumfikiria mtu ila yeye tu. Akaacha fujo tupu kila mtu anataka kujimilikisha anachokitaka. Ila kwa kuwa mjomba angalau alikuwa karibu na sisi tokea mwanzo, wakasema aendelee kutusaidia mpaka mahakama itakapo amua.”

“Basi, akasema nilazima kutengeneza hati ya kuzaliwa mpya yenye jina jingine sio Nelinda. Na iwe na tarehe ya tofauti lakini inayoendana na kidato nilichopo.” Billy akakunja uso. “Usiniulize Billy, maana hata sijui. Ila akaniambia nikifanya hivyo, nitaonekana nina miaka 18 tayari na wakili atanitetea kuwa nimefikisha umri wa kumlea mdogo wangu, na kupewa mali zote za baba bila shida ila chini ya usimamizi wake. Nikakubali kwa haraka sana. Ila sasa akasema lazima kuwa na akili za kiutuuzima, niachane na utoto. Akarudia tena, ila safari hii mkono kwenye matiti yangu. Mimi nikakwepa. Akaniambia kama nihivyo, inamaana sina akili za kiutuuzima, siwezi nikaaminiwa. Napoteza kila kitu.” Nelly akacheka.

“Nilivua nguo mimi mwenyewe Billy.” “Nelly!” “Wala sikubakwa. Kwa hiari yangu, nikamruhusu. Ila akaniambia kwa wakati ule hapakuwa na mazingira mazuri, lazima kutafuta nafasi. Alimfukuza kazi yule msichana wa kazi aliyekuwa akitusaidia sana, akimwambia atakuja kumtafuta tena baadaye, mambo yakitulia. Kwamba lazima tuonyeshe mimi ni mkubwa naweza kumtunza mdogo wangu. Akamuanzisha Jax shule. Akamuweka shule anayokwenda asubuhi na kurudi jioni. Mchana najikuta nipo nyumbani nikiwa nimetoka shule, basi nikageuka kuwa mke wake mdogo.” “Nelly!” “Ooh yeah. Nilijua njia zote za kujikinga na ujauzito. Nilijua jinsi ya kumtumikia bila shida wala kushurutishwa. Mwenyewe, nikimbembeleza anisaidie.”

“Nikageuka kuwa kama baba yangu. Mbaya zaidi, niliyafanya hayo nikijua fika mjomba anaye mke wake nyumbani ila nikabaki nikimtumikia kama mke wake wakati nilikuwa ni mdogo kuliko binti yake. Tena bila huruma wala aibu. Akatutafutia mwanasheria. Tukafanikiwa kumuua Nelinda bila shida. Nikandikishwa Nelly. Na akanionya nisiwahi kujiita hivyo tena. Sikufanikiwa kumaliza kidato cha sita.” “Kwa nini tena?!” Billy akauliza kwa kuumia.

“Daah! Acha Billy. Aliniambia lazima kufuta historia yote ya nyuma. Niliposhinda ile kesi, nikapata mali zote, nikamwambia sitaweza kuendelea kuishi kwenye ile nyumba aliyojinyonga baba, ukweli nilikuwa nikiogopa sana. Basi, akanisaidia kununua nyumba ninayoishi sasa hivi na Jax. Zilikuwa nyumba za msajili wa majumba, na yeye alikuwa mkurugenzi huko. Ukweli alikuwa na uwezo mkubwa sana kifedha. Basi, ndipo akanisaidia kutafuta nyumba nzuri tukapata kwa bei nzuri. Kwa jina langu. Pesa iliyobakia ndipo nikaanza chuo sasa nikitumia matokeo yangu ya kidato cha 4.”

“Ikabakia jinsi ya kumkwepa. Maana alikuwa akinisumbua Billy, huwezi kumkwepa. Alikuwa akinitumia zaidi ya mkewe. Nikajiambia sitaweza kuwa naye na kumtunza Jax. Na mbaya zaidi kile kitendo kikawa kimeniathiri sana. Sikuwa mwenye furaha kabisa. Yale mahusiano yalinifanya kuwa na uchungu wa kupitiliza. Nilijawa na hasira ya kupitiliza. Kila nilipokuwa nikilala naye, nashindwa hata kupata usingizi. Nikawa mtu niliyejawa hasira sababu ya kutolala na hukumu.”

“Nikajilinganisha na wanawake wote waliokuwa na mahusino na baba yangu wakijua mama yupo. Nilikuwa siwezi hata kujitizama kwenye kioo. Siku moja alikuja pale nyumbani akitaka alale, nikashindwa. Alisema ameaga nyumbani kwake kuwa amesafiri, nisiwe na wasiwasi. Nikaenda kuchukua kisu jikoni. Nikamfuata chumbani. Nikamueleza jinsi anavyoniumiza nafsi yangu na akili. Nikamueleza vile ninavyojitizama baada ya kumalizana na yeye, nikamwambia furaha yangu ni kumuua yeye kwa kuwa sina chakupoteza tena. Nikamwambia siku atakaporudi tena pale, awe ameamua kuniua mimi au awe amekubali kifo. Aliondoka, hakurudi tena. Ila aliniacha nimeathirika vibaya sana. Ndio nikabakiwa na Jax mpaka hivi tunavyozungumza.” “Aisee pole sana Nelly.”

“Ndio maana jina la Nelinda situmii. Lilikufa kwa garama kubwa sana. Hapa ninamiliki miaka karibu miwili ambayo sijawahi ishi hapa duniani. Na jina ambalo mama yangu hakunipa ila mjomba.” “Yasinta ndiye aliyenipa habari zenu kwa ufupi tu. Ilibidi kumtafuta ili kuweza kukufahamu. Maana nilijua nisingeweza kumuuliza Jax. Kwanza si sawa kwa wadhifa nilio nao pale kazini. Katika kupeleleza hata kwenye faili la Jax, liliandikwa alichokuwa amezungumza siku ile ya tafrija. Ukawa upo wewe tu kwenye maisha yake. Nikasema haiwezekani. Ndipo nikaambiwa na mmoja wa wafanyakazi wenzake Jax aliyekuwa kwenye kamati ya harusi ya Jax, kuwa alisikia rafiki wa karibu sana wa Jax akimuuliza kama atawashirikisha ndugu zenu wengine. Jax akasema huo utakuwa ni uwamuzi wako wewe. Katika kupeleleza zaidi ndipo nikamjua huyo mjomba wenu na binti yake ambaye na yeye anafanya kazi benki. Haikunigarimu sana kumtoa ukweli Yasinta.” Nelly akashangaa sana.

“Kwani ulimlipa!?” “Tuache hilo. Ila nikakufahamu kupitia yeye.” “Yule yupo kama mama yake! Wanapenda sana pesa. Alishakuja kuniomba pesa akinikumbusha jinsi nilivyosaidiwa nyumbani kwao.” “Kweli?!” “Wewe usicheze na Yasinta. Kwanza mlevi. Halafu anapenda pesa kama benki. Nilimpa na kumuonya asiwahi kurudi pale kunitafuta mimi na wala asiwahi kumfuata Jax. Nilimwambia nikimsikia amemsogelea Jax, nitampasua kichwa.” Billy alicheka sana. “Kumbe alisema kweli, hakudanganya!” “Mpuuzi sana. Ila mbona unazo habari zangu mpaka za sasahivi!?” “Hizo nyingine ni za watu wa karibu yako na sitakutajia maana mbali na kuwalipa, niliwaahidi sitawataja kwako. Naomba tuliheshimu hilo.” Nelly akamtizama na kunyamaza.

“Sasa umeridhika kunifahamu kwa asilimia ngapi?” Nelly akauliza na kumfanya Billy kufikiria. “Mmmh! Labda 90.” “Sasa hizo 10 zimebakia wapi? Maana nimekwambia mpaka hofu yangu!” “Hapana. Hapo umepachanganya sana. Nimebakia kubuni tu. Mpaka nahisi umekuwa makini kutonijibu hilo.” Nelly akanyamaza akifikiria, kisha akamwangalia.

“Nikwambie ukweli ambao utakusaidia hata usipoteze muda wako?” “Sitaki.” Billy akajibu kwa haraka. “Sasa unakataa nini wakati hata sijasema?” “Kwa kuwa nimeshajua unachotaka kuniambia.” Nelly akakunja uso. “Si unataka kuniambia wewe si kama wanawake wengine. Moyo wako uliumizwa sana. Haupo tayari kwa hili au lile! Maneno yanayofanana na hayo. Sivyo?” Billy akamuuliza. “Na usinidanganye Nelly.” “Ni kama hivyo ila..” “Hapana.” Billy akasimama kabisa. “Sasa unakwenda wapi?” “Kupumzika. Twende ukapumzike. Naona kwa leo inatosha. Tumekuwa na wakati mzuri naomba tukapumzike.” Nelly akasimama. Wakaanza kurudi chumbani.

“Nakushukuru kwa wakati mzuri. Nimefurahia sana.” “Hata mimi nimefurahia. Zaidi kuona wewe umefurahi.” Nelly akamtizama na kuendelea kutembea. “Nikuulize swali Nelly?” “Mmmhhh.” Billy akamtizama. “Ulishawahi kupenda?” “Ukweli hapana Billy. Sikuruhusu fikra zangu zifikirie hayo maisha kabisa. Kwanza nilijiambia sistahili. Nimekua mwizi. Kuna wakati mpaka nilikuwa nikitamani pengine ningebakwa ili kujisamehe, lakini sikuwahi kubakwa Billy!” “Ni kama ulibakwa Nelly, ila hapakuwa na kutumia nguvu. Ulikuwa ukifanyia kinyume na matakwa yako. Wewe hukuwa mwizi. Ulifanya kile uwezavyo kwa wakati ule ili wewe na Jax muwe hapo mlipo. Tafadhali tafuta jinsi ya kujisamehe. Itakusaidia sana.” Nelly akanyamaza. Wakaongozana mpaka juu kabisa vilipo vyumba vyao. Vilikuwa vikitizamana.

“Kesho tunaondoka saa ngapi?” “Mchana. Lakini nilitaka tupate chakula cha pamoja kabla yakuondoka.” “Basi unijulishe angalau nusu saa kabla.” Wakasimama hapo nje ya milango yao wakizungumza tu. Mwishoe wakakaa kabisa chini kama walivyofanya walipokuwa kisiwani. Lakini siku hiyo Billy alipanga angalau apate busu la shavuni. Ila historia ya Nelly aliyotoka kumsimulia muda mfupi uliopita, ikamrudisha nyuma kabisa. Akaona awe muungwana zaidi, asiwe kama mjomba wake. Wakatulia hapo mlangoni, watu wakipita na kuwashangaa.

“Mara ya tatu inabidi kukwambia ninapopanga twende.” Nelly akacheka na kumwangalia. “Kwa kuwa kunahitajika maandalizi.” Nelly akakunja uso. “Unanipeleka sayari ya ngapi?” “Hutafika kwenye sayari ila mlima Kilimanjaro.” Nelly akatoa macho. Billy akacheka. “Usiogope. Mimi hii itakuwa safari yangu ya tatu. Ya kwanza tulipanda na baba, pamoja na kaka yangu. Carlos pia alikuwepo. Zamani sana. Nafikiri tulipomaliza tu chuo mimi na Carlos, tukaja na mzee. Mara ya pili, nilikuja na watu wa kazini. Na mara ya tatu ndio nataka twende wote. Utafurahia.” “Mimi sidhani bwana. Sasa kwa nini kupanda milimani, Billy!?” Billy akazidi kucheka.

“Usiogope, ni kitu kizuri sana. Nakuandalia mtu atakayekuandaa, mpaka siku yenyewe tunakwenda, itakuwia rahisi.” “Labda hivyo. Mwenzio hata mazoezi huwa sifanyi.” “Sasa kwa nini unamwili mzuri hivyo?!” “Mimi naona tulinyimwa tu miili mikubwa. Si unamuona hata Jax? Anakula sana, lakini hutamkuta na mwili mkubwa hata mara moja. Na yeye pia si mtu wa mazoezi. Basi na wazazi wetu walikuwa hivyohivyo. Sikumbuki kumuona mama amenenepa hata alipokuwa mjamzito wa Jax, alikuwa kama mimi tu.” Wakaendelea kuzungumza.

Lakini Nelly akakubaliana bila ubishi na hilo la kupanda mlima Kilimanjaro, kitu kilichomfurahisha Billy kuona angalau wanakubaliana kwenye mambo fulani fulani japo habari alizosikia juu ya Nelly ni mkorofi, mkali kama simba. Na akamuonyesha hivyo tokea wanakutana. Akijua fika wadhifa wake, lakini akadiriki kumkatalia maombi yake bila kufikiria mara mbili.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment