Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Chozi Langu! - Sehemu ya 13. - Naomi Simulizi

Chozi Langu! - Sehemu ya 13.

 Kwa Lara.

L

ara na Jerry waliondoka jijini Mwanza, Lara akiwa hajui kitakacho endelea wakifika jijini Dar. Hakuwa na pakwenda ila tu kwa Jerry. Kama kawaida ya Jerry alikuwa busy na simu yake mpaka wanaingia ndani ya ndege, Lara kimya akiwaza huku mapigo ya moyo yakienda mbio asijue kama ndio mwisho wa hizo starehe au la. Kwenye ndege nako kukawa kimya, Jerry akisoma magazeti mpaka wanafika Dar. Alichojiamulia Lara moyoni, safari hii hataondoka tena mpaka afukuzwe. Na akijirudi, ajinufaishe kwa haraka, kwa kuchukua pesa nyingi ndipo aondoke. Akapoa.

Walifika wanakoishi wawili hao, Jerry akamwambia anakwenda nyumbani kwake Masaki, atarudi baadaye. “Sawa.” Lara akakubali bila swali. “Au unataka nikwambie nakwenda kufanya nini?” “Huna sababu yakufanya hivyo, lakini ukiona ni sawa, nipo kukusikiliza.” Jerry akamtizama na kutingisha kichwa kama anayesikitika, akaondoka hata hakukaa. Alichofanya Lara ni kuingia chumbani kwao kwa haraka na kuanza kukusanya nguo zake za maana tupu, alizojua ni za gharama sana. Viatu na dhahabu zake zote. Akaweka kwenye masanduku, akafunga vizuri, akachukua moja ya gari ya Jerry aliyomwambia ni yake, lakini akajua atakuja kumbadilikia siku moja kama alivyoanza kumuhesabia walipokuwa Mwanza. Akakimbilia kituo cha mabasi makubwa yaendayo mikoani.

Bado ilikuwa mapema tu maana walirudi na ndege ya asubuhi. Mpaka wanafika nyumbani ilikuwa saa 7 mchana. Lara alitaka kuwahi basi la mwisho linalokwenda Dodoma. Alishampigia simu baba yake kuwa atatuma masanduku mawili na boksi ambalo anaomba visifunguliwe mpaka afike mwenyewe nyumbani. Lara aliendesha kwa haraka. Akafanikiwa, akasafirisha vile vitu vyote alivyojua ni vya maana sana kwake ambavyo hataki kupoteza hata kama ikitokea kama alivyoachwa na Jax, basi hatapoteza vitu vyake vya thamani. Alishang’atwa na nyoka, jani likitikisika tu, anajua ni nyoka.

Shilingi Yapinduka Tena.

Akapitia sokoni kununua vyakula na matunda, ndipo akarudi anakoishi na Jerry. Nje alikuta gari ya Jerry. Akajua amerudi. Akatoa mizigo aliyorudi nayo kutoka sokoni na mkoba wake pembeni. Akapitiliza jikoni, hakuwa amemkuta Jerry sebuleni. Wakati yupo jikoni anashusha vitu, akashitukia Jerry yupo nyuma yake. Akampiga kibao cha mgongoni, Lara alishituka akaachia mfuko na kuinama kwa mshangao.

“Umeanza umalaya! Natoka tu kidogo na wewe unatoroka, halafu unarudi na upuuzi huu, kama kisingizio! Mlinzi ameniambia umetoka mara tu na mimi nilipotoka.” Lara alikuwa kwenye mshituko, asitegemee kama mikono ileile iliyokuwa iking’ang’ania kiuno chake na hips zake, ndio imeishia kumpiga! Jerry akamsogelea akiwa amejawa hasira, Lara akapiga magoti na kuficha uso. Hapakuwa na pakukimbilia kwani ni kama alimbana kwenye kona. Lara alishindwa hata kulia kwani alikuwa kwenye mshituko mkali sana.

“Unatumia mali zangu kujinufaisha! Nikikuuliza unaleta jeuri! Hapa ni kwangu, unatakiwa kuwa na heshima.” Hakumpiga tena ila Lara akashitukia ananyanyuliwa na kwenda kutupwa nje. “Kama umeshindwa kuishi kwa unyenyekevu, unaleta kiburi kujidai wewe ni mjuaji, nenda kaonje maisha ya wenzio wanavyoishi huko nje.” Hapo anamfukuza bila hata pochi yake. Akarudi ndani na kufunga mlango.

Lara akarudi kugonga, akamfungulia. “Naomba nijihifadhi mpaka kesho. Tafadhali Jerry. Sasa hivi ni jioni tayari. Sina pakwenda.” “Kumbe unajua kuomba! Nilijua wewe nikiburi, hujui kujishusha.” “Samahani kama nilikuudhi.” “Sasa hivi ndio unajirudi baada yakugundua huna maisha bila mimi! Nimehangaika sana kufika hapa nilipo! Eti wewe unakuja tu, nakutaka kunitawala! Unajua nilifikaje hapa?” Jerry akazidi kugomba. Na hawakuwa na eneo kubwa. Inamaana hata mlinzi alikuwa akisikiliza anavyotukanwa.

Hapo Jerry alikuwa akimtukana huku Lara na yeye akijitukana vile alivyoweza kuacha kazi na kukimbia na Jerry kwa ahadi ya maisha mazuri. Akawa anawaza pakwenda jioni hiyo akifukuzwa bila pochi yake wala simu. Wapi pakwenda! Akaanzie wapi! Lara akabaki ametulia hapo akiwaza huku Jerry akiendelea kugomba. Hata hivyo alishamchukia Jerry kutoka moyoni, alisimama hapo akiomba Mungu amguse amfungulie tu, aingie ndani.

“Mali zote hizi ni zangu. Ulitakiwa kunyenyekea sio kuleta kiburi.” “Samahani Jerry. Samahani sana kwa kuudhi. Mimi ninaondoka, lakini nilitaka kukuomba msamaha kabla sijaondoka. Natambua upendo wako na vile ulivyojitoa kwangu. Nasikitika tunaachana, lakini sitaki tuachane ukiwa kwenye hali hiyo. Umenipa maisha mazuri sana Jerry. Ni kweli hakuna mtu anaweza kunitunza kama wewe. Naomba tuagane tu vizuri. Tafadhali Jerry.” Jerry akapoa.

Ilikuwa kama amepandwa na wazimu wa gafla, akapoa. “Kwa hiyo upo sawa?” Lara akamuuliza taratibu tu akijikomba. Kimya. “Kwani ulinisubiria sana? Nilikwenda kutuma mzigo nyumbani labda ndio maana umeniona nimechelewa. Samahani.” Lara alikuwa akibembelezea malazi ya siku hiyo na vifaa vyake vilivyobaki hapo ndani. Jerry akampisha mlangoni. Lara akaingia. “Naomba nioge kwanza, nimechafuka, halafu nije nipike.” Lara akaongea kwa tahadhari. Jerry hakujibu lakini alikuwa amepoa kabisa.  Akakimbilia jikoni, akachukua pochi yake na kwenda nayo chumbani.

Akaoga harakaharaka akatoka wakati anataka kwenda jikoni, Jerry akamuwahi. “Subiri kwanza Lara. Sasa hivi lazima uishi hapa kwa masharti yangu. Huwezi kunipelekesha. Sasa je, upo tayari kujibu kila swali langu?” “Hapana.” Bila kufikiria Lara akajibu na kumshangaza sana Jerry! “Naahidi kukujibu ukweli kwa yanayotuhusu Jerry, sitaki kuwa muongo kwako. Mengine siwezi kuzungumza na wewe.” “Kwa hiyo unataka kuzungumza na nani!?” Akauliza kwa ukali mpaka uso ukabadilika.

“Tafadhali usinipige tena Jerry. Nimekuwa muwazi kwako, usinipige. Tuzungumze, ikishindikana basi, nipo tayari kuondoka. Uniache kama ulivyonikuta. Kwa amani kabisa.” “Una nini wewe Lara!? Ni nini unaficha kikubwa hicho chakukubali kupoteza kila kitu?” “Siwezi kupoteza kitu ambacho sikuwahi kuwa nacho Jerry!” Lara alijibu bila woga na kumshangaza sana Jerry.

“Hiki ulichonifanyia muda mfupi tu uliopita, ni kwa hivi unavyonifahamu. Ningekwambia undani wangu kidogo tu, ungezidi kunidharau na kunidhalilisha. Wewe ni mbinafsi Jerry. Umeruhusu maisha yako ya nyuma na watu walivyokutenda vibaya, wageuze moyo wako. Unaweka mali mbele kuliko utu.” Lara akajishangaa anaongea bila hofu.

“Unawezaje kusema hivyo na vile nilivyokuthamini!?” “Hii ya leo, hiki unachofanya na maneno yaliyokutoka, yamekufungua moyo wako na kukuanika undani wako. Vile ulivyo kwa halisi. Hujui kupenda Jerry, unajua kutawala. Unapoona unapoteza nguvu yako kwa mtu, ndipo udhaifu wako unapojidhihirisha. Huwezi kuishi na mtu mtulivu kwa kuwa hujui amani inakuaje. Hufahamu kupendwa, halafu pia unaogopa kupendwa na kuthaminiwa. Ukiona kuna dalili ya kupendwa tu, wewe kama Jerry, wala si vitu vinavyokuzunguka, au mali zako, ukigundua ni mapenzi halisi, unatafuta sababu ya kukimbia ili kuepuka yaliyokupata utotoni pale mama yako alipokuacha. Unaogopa yasijirudie.” “Usimwingize mama yangu Lara! Tafadhali sana.” “Sawa Jerry. Mimi ni mbaya. Acha nikuache na maisha yako.” “Utanikumbuka Lara!” Lara akamtizama na kutabasamu.

“Unanidharau!?” “Hapana. Wewe ndio utanikumbuka Jerry. Na utakaponikumbuka, nasikitika hata pesa na mali zako ulizokuwa ukijisifia nazo tokea jana, hazitakupa ninachokupa.” Lara akaongea kwa kijiamini mpaka akamshangaza zaidi Jerry.

“Naomba nikuombe kitu kimoja cha mwisho Jerry.” Jerry akabaki akimtizama. “Nakwenda kukusanya vitu vyangu niondoke, naomba usinipige kama ulivyonifanyia pale jikoni. Nimekubali kuondoka, usinipige tena. Na kama uwepo wangu hapa unakupandisha hasira, unaweza kunisaidia kukusanya vitu vyangu na kuniwekea pale kwa mlinzi nikaja kufuata hata kesho. Usinipige tafadhali. Kosa nililofanya ni kukupenda sana na kuwa mwaminifu kwako, sidhani kama ninahitaji adhabu kwa hilo.” Lara akarudi chumbani kuanza kufungasha kwa haraka akiwa na furaha yakuruhusiwa kuchukua vitu vyake japo lengo halikutimia na aliogopa kuendelea kuishi hapo asije akatoka maiti. Akakazana kukusanya.

“Mke wangu anaumwa sana.” Lara akageuka. Jerry alikuwa amesimama mlangoni. Akashindwa hata asijue ajibu nini. “Alikuwa na kansa, imerudi tena. Jana nilipotoka pale hotelini, watoto walinipigia simu kunijulisha. Na kumbe safari hii amechelewa kuigundua. Amekuja kurudi hospitalini ikiwa imesambaa vibaya sana.” Jerry akaendelea. “Alikuwa ndio kila...” Jerry akasita. “Pole sana Jerry. Pole. Lakini anaweza kupona.” “Hapana. Safari hii ni mbaya. Maisha yangu yanabadilika Lara. Nampoteza mke wangu na wewe kwa pamoja! Ndio maana nachanganyikiwa.” “Pole sana, Jerry. Pole.” Hilo ndilo Lara aliweza kusema, hakutaka kujiingiza hata kidogo kwenye matatizo ya kifamilia ya mtumzima huyo. Akabaki amesimama akimtizama.

“Maisha yangu yananibadilikia! Wakati nalala juzi, sikujua kama nitapitia hii hali. Nimempoteza mama yangu, sasa hivi wewe, kisha mke wangu! Napaniki.” “Pole sana Jerry.” Lara hakutaka hata kumpa wazo la kumuomba abaki. Akaendelea kukusanya vitu vyake vyote, Jerry akimwangalia. “Natamani kama ningeweza kukupa kila kitu Lara.” Lara akasimama tena. “Hata mimi Jerry. Natamani kama ningeweza kukupa kila kitu nikakuridhisha. Au hata kuweza kukutuliza nikawa kimbilio kipindi kama  hiki. Lakini inaonekana mimi sio msaada Jerry. Nakuongezea matatizo.” “Sio kweli Lara.” “Ni kweli. Au basi niseme nakuwa ndio mtu wakunimalizia hasira. Sio sawa kwangu. Nimepita hapo kwenye magumu Jerry! Hapo ulipo wewe, mimi nimepita nikiwa peke yangu, lakini nilipita kimya kimya, sikuwa na wakumuumiza ila nikabeba mpaka ukanikuta Zanzibar.”

Lara akajieleza. “Mimi sijui ugomvi Jerry. Hiki ulichonifanyia leo ni kipya, hakijawahi kunitokea tokea nazaliwa. Na si kwa bahati mbaya. Hata shuleni sikuwahi kuchapwa. Hata walimu walipokuwa wakitaka kuadhibu watu wote, mimi nilitolewa pembeni. Sijisifii, ila ni kwa vile nilivyo. Sijui ugomvi, wala kelele za kumkera mtu. Najua ni wakati gani wakuzungumza na wakati gani wakunyamaza. Ndio asili yangu. Wakorofi huwa wananikimbilia. Wewe umeweza kupata sababu ya kunipiga na kunitupa nje! Hakika mimi sio msaada kwako sasa hivi. Acha nikupe nafasi tulivu ili uweze kufikiria na kusaidia familia yako.” Lara akaendelea kukusanya.

“Kwa hiyo unashindwa kunisamehe japo nimekuomba msamaha!?” Jerry akaanza. “Yote niliyokutendea, unashindwa kunisamehe wakati nimejieleza mpaka nimekupa ya undani! Bado huoni sababu yakuwa na mimi japo kwa kipindi hiki tu!” Lara akanyamaza akajua anatafuta kumpiga tena. Akataka kujutia misaada aliyochukua ya Jerry, lakini akakumbuka furaha aliyoweka kwa wazazi wake. Moyoni akapata faraja, akatulia na kuamua hata iweje hapo hatabakia tena, lazima aondoke.

“Unaondoka lini?” Lara akajaribu kuuliza ili kumtoa kwenye mawazo kwa kile alichokuwa anataka kukifanya. Kujipandisha hasira. “Naweka mambo sawa, ndipo niondoke.” “Unataka nikusaidie nini kwenye kujiandaa?” Hapo akamfanya atulie kabisa. “Sasa hivi nimechanganyikiwa, hata sijui.” “Sanduku la safari ndio hilihili ulilokwenda nalo mara ya mwisho?” Lara akaendelea kuuliza. “Nitatumia hilohilo, unataka kunisaidia kuandaa?” “Kama ni sawa.” Lara akamtoa kwenye ile hali wakaanza kuandaa safari angalau Jerry akawa amepoa lakini Lara akawa hataki hata kumuona tena.

“Kesho unataka nikusaidie nini kurahisisha maandalizi yako.” “Natakiwa kwenda benki kufuatilia na kupanga mambo yangu ya biashara angalau kuweka sawa kabla sijaondoka.” Wakazungumza hapo Lara akamtuliza, wakaweka mipango nini anahitaji Lara amsaidie. Huo usiku ukaisha kwa shida, kwa uzito mno. 

Asubuhi ya Machozi Mengine ya Aibu Kwa Lara.

A

subuhi Jerry alimka kisirani, hata Lara alimuona. Akabaki kujiwinda. Kwani alimuona akisoma jumbe bado wakiwa kitandani. Akamuona akijibu, akaona aondoke. “Acha nikaandae kifungua kinywa.” Lara akajiwahi kutoka kitandani. “Umekuaje Lara!? Unaniachaje hivihivi! Jana sikupata kitu sababu uliwahi kulala. Wakati narudi kuzungumza na simu nikakukuta umeshalala! Sikulalamika wala kukuamsha, nikaamua kukuacha. Asubuhi hii nayo unakimbilia jikoni, unaniacha peke yangu! Unamaanisha nini? Kuwa umeshanichoka?” Lara akabaki ameduaa, maana usiku ni kweli alitoka nje kabisa kwenda kuzungumza na simu. Na yakawa mazungumzo ya muda mrefu, akaamua kwenda kulala. Hata hivyo hakujisikia kwa penzi baada ya kumtenda unyama.

“Unaona ni kama nakubebesha majukumu yasiyokuhusu? Yaani unakuwa ni mtu wa starehe tu, mwenzio nikiwa na shida unashindwa hata kuwa na mimi?!” “Nimekuona upo kwenye simu Jerry. Halafu mimi na wewe mapenzi siku zote hayajawahi kuwa wajibu. Tunakuwa tunaanza tukiwa kwenye hali nzuri. Ukiwa umetulia na mimi nimetulia.” “Kwa hiyo sasa hivi kosa ni langu?” Lara akanyamaza. “Huna tofauti na wengine Lara! Upo na mimi sababu ya pesa tu, lakini si mimi kama mimi. Nimekwambia pale ninapopitia. Unashindwa vipi hata kuniulizia maendeleo ya mgonjwa! Unalalaje hata hujui ripoti ya huko? Jana ulijua kabisa kwamba nazungumza na watoto pamoja na mama yao ambaye ni mgonjwa, umelala kabisa na kuniacha usiku nakesha kwa mawazo! Unafurahia kitanda ambacho nimenunua kwa jasho langu halafu mimi mwenyewe mlipa garama hunitaki!” Lara akabadilika sura akawa mwekundu asijue ni hofu au hasira.

“Wewe ni jeuri. Na ninajua chakufanya na huo ujeuri wako.” Alipotaka kutoka tu kitandani Lara akakwapua simu yake na kukimbilia choo cha hapohapo chumbani nakujifungia kwa hofu akijua anataka kumpiga tena. “Fungua Lara.” Lara akaanza kutetemeka huku akiwaza jinsi ya kujitetea. Wanapoishi ni patulivu, hajui jirani hata mmoja ambaye angempigia kwa haraka kuja kumsaidia maana Jerry alikuwa akigonga kwa hasira na kunguruma kama simba.

Mjini hapo hana tena shoga. Alihama jiji bila taarifa, alirudi bila taarifa. Akili ikaendelea kufikiria kwa haraka jinsi ya kujiokoa wakati Jerry akiendelea kutoa vitisho nje ya mlango, akimtaka afungue. Hakujua wazo lilipotoka, kwa haraka akajikuta akimpigia simu Tino. Japokuwa alikuwa na namba mpya, lakini namba za watu wake wote wazamani hakufuta kwenye simu yake.

Baada ya Raha, karaha.

S

imu ikaita. Tino hakupokea. Akatuma ujumbe. ‘Mimi Lara. Naomba msaada wako.’ Akautuma. Akaona simu inaingia. Tino. Akaanza moja kwa moja kumuelekeza anakoishi na Jerry. “Mbona kuna kelele? Upo sawa wewe!?” “Umeelewa, nilivyokuelekeza?” Lara akauliza swali kwa sauti ya juu akisikika anaanza kulia. “Nimeelewa, mbona unanitisha? Unataka nini sasa?” “Njoo sasa hivi unitoe Tino. Usimwambie mtu, iwe siri yako. Tafadhali. Haraka, Jerry ataniua.” “Fungua mlango Lara. Nitauvunja huu mlango!” Jerry akasikika akiunguruma kama simba.

Lara akakata simu huku akilia na Tino akionekana ameshapaniki kwenye simu. “Kwa nini unataka kunimalizia mimi hasira zako, Jerry? Nimefanya nini?” “Nimekwambia fungua mlango.” Lara akaendelea kulia. “Nitavunja huu mlango na nitakuumiza vibaya Lara! Fungua.” Lara akawa analia kwa uchungu. Akiwaza ni nini kibaya amewatendea hawa wanaume kiasi chakumuadhibu vibaya hivyo kila anapokuwa nao! Lara akaendelea kulia kwa kuadhibiwa na Jerry kwa kupokea starehe alizoahidiwa tokea mwanzo!

Akakumbuka na ndio sababu ya kukubali hayo mahusiano na mwanaume mwenye majukumu  ya familia yake, tena aliyemuonyesha tokea mwanzo kuwa familia yake kwanza, yeye yupo pale kumridhisha tu. Amemnunua kwa kumtumikia kimapenzi. Bila yakujua au kwa kushindwa kufikiria sababu ya hofi, Lara amesahau uthamani wake ni pale Jerry anapokuwa na furaha. Ili awepo kwenye maisha ya Jerry, ni Jerry aendelee kuwa na furaha na sivinginevyo.

Hapakuwa na kudanganyana kati yao ila kutofikiria tokea mwanzo, madhara ya makubaliano yao, kwa pande zote. Sasa wote wamekutana na uhalisia. Pengo la Jerry maishaini haliwezi kuzibwa na mwanadamu yeyote yule, ni mpaka kumpa Mungu nafasi amsaidie tokea chini kabisa, kukarabati pale wanadamu waliharibu moyoni mwake. Na ndipo angepata utoshelevu wa kweli na wala si kuhangaika kwa kutafuta wanawake kwa kuwahadaa kwa mapesa mengi akidhani watakuwa kile anachodhania.

Na kwa Lara hivyohivyo, kutoka kuumizwa na mwanadamu mmoja, haraka sana kabla hajapona, kuelewa na kujua jinsi gani ataishi tena na ile hali ya usaliti, akakimbilia kwa mwanadamu mwingine akidhani atatulia au itakuwa tofauti.

‘Kufanya kilekile, au vilevile wote wawili wakitegemea matokeao ya tofauti.’ Ndio asubuhi hiyo wameishia hapo. Lara analia upande wa pili akimlaumu Jerry kwa usaliti wa ahadi zake mwenyewe, na Jerry naye anakaribia kuvunja mlango akiahidi kumuumiza vibaya sana huyo Lara aliyekuwa akimfaidi kwa muda wote huo. Akimridhisha atakavyo bila kikomo wala kulalamika akidhani Lara ndio angetakiwa awe na uwezo wa kuwa kile alichotaraji au anachokosa nafsini mwake. Anataka kumuadhibu kwa kushindwa kwake.

Tino siye mtu aliyetaka hata ajue kama anamatatizo. Alitamani aje akutane naye akiwa mambo safi, lakini akajikuta hamna tena namna. Hana kimbilio jingine ila Tino ambaye ni mwepesi kutenda. Muda na wakati wowote unapomuhitaji Tino, huwa hana sababu nyingi sana za kukataa ila kutenda. Akaishia kwake akijua wazi akijua Tino, ni kama watu wote watajua tena. Ila hakuwa na jinsi. Hakuwa na ndugu hapo jijini pengine wangemfichia hiyo siri ya kukutwa anadhalilishwa na Jerry. Tino akabakia ndio mtu pekee wa kumpa msaada kwa haraka, kwa wakati ule.

Akaendelea kumsikia Jerry akigonga mlango kwa nguvu. Akamtisha kwa maneno mengi lakini hakufungua akiendelea kuomba Mungu Tino aliyemuacha Mwanza, awepo Dar ili afike hapo kwa haraka, kama amepaelewa. Mara akasikia kama Jerry anatumia kitu kizito kugonga mlango, Lara akazidi kulia kwa sauti akijua Jerry atafanikiwa tu. Aliendelea kama kwa dakika 20 akimsikia anazidi kupandwa na hasira, alisukuma mlango kwa nguvu ukafunguka na kumgonga vibaya sana Lara mkononi. Alilia Lara. Akalia kwa hofu kubwa sana kwani Jerry aliyeingia hapo hakuwahi kumuona kabla.

Alimvuta mpaka nje, Lara akiwa na nguo za kulalia tu akamtupia kitandani kama paka. Mlinzi akawa anagonga kwa nguvu sana. Jerry akatoka kwa hasira. “Salama huko? Imebidi kupiga simu kituoni kuomba msaada. Nimesikia kelele.” “Wewe ulitakiwa kulinda watu wabaya wasiingie ndani. Sio kuwa mbea wa mambo ya ndani. Umeona mtu ameingia ndani mpaka kuomba msaada kituoni?” Jerry alikuwa akilindwa na kampuni kubwa ya ulinzi ambayo makao yake makuu yalikuwa hapo karibu tu, Kinondoni. Si mbali na hapo.

“Ni katika kutaka kusaidia tu.” Yule mlinzi akajitetea. Wakati wanazungumza gari ya kampuni hiyo ya ulinzi na walinzi wengine wanne waliovaa sare za ulinzi wakaingia na risasi. Kwa kuwa geti liliachwa wazi na mlinzi akitarajia wenzie waje kumsaidia. Wakasogea pale mlangoni alipokuwa amesimama mwenzao na Jerry, mwenye nyumba. Lara alikuwa akilia sana, amefungiwa chumbani akilia, aliposikia sauti ya wale walinzi nje akaongeza kilio na kuomba msaada. ‘Naomba mniokoe’. Akaongeza kuwa Jerry anataka kumuua. Wakashituka sana.

“Haya ni mambo ya unyumba, hayawahusu. Nyinyi mnalinda nje sio ndani.” “Naelewa mkuu. Lakini hatuwezi kuondoka tukiwa tunasikia mtu akilia kwamba maisha yake yapo hatarini! Chochote kitakachotokea kwake na sisi kuwepo hapa tukasikia na tusitoe msaada, sisi na wewe wote tutakuwa na hatia.” Hapo wakapandisha hasira za Jerry. Akaanza ubishi na ukali.

Baada ya muda polisi na Tino wakaingia wakiuliza kama pale yupo mtu anaitwa Lara. “Hii ni nyumba yangu. Hayupo mtu anayeitwa Lara humu.” Jerry akawakatalia. Tino akampigia simu Lara wakiwa wamesimama palepale kwani Tino aliwahakikishia kuwa lazima Lara atakuwepo humo ndani, kwani aliwaona wakiwa pamoja jiji Mwanza. Simu iliita na kweli Lara akaisikia ikiita chooni akakimbilia kwenda kuikota. “Jerry ataniua Tino. Kama upo mjini tafadhali niokoe.” “Uko wapi? Mimi nimefika hapa na polisi kwenye ile nyumba uliyonielekeza. Nimemkuta Je...” “Basi nipo chumbani amenifungia. Naomba usiondoke hapa bila mimi Tino. Amenivunja mkono tayari, nipo na maumivu. Nisaidie. Usije ondoka bila mimi. Ata...” Tino akashituka sana. “Lara yupo ndani ya hii nyumba, jamani. Nimeongea naye kwenye simu. Amemfungia chumbani na ameshamvunja mkono.” Tino akawaambia askari polisi aliofika nao hapo.

“Muongo.” Jerry akakanusha. “Kwa hiyo unakubali kuwa yupo ndani?” Askari mmoja akawa amemkamata uongo. “Kwani kuwepo ndani kunamfanya hapa kuwa kwake?” “Ninachotaka ni kuzungumza naye tu. Nikimsikia yupo sawa na anataka kubaki, hayupo hatarini, basi nitaondoka. Au sisi tutaondoka. Lasivyo hatuwezi kuondoka tukipuuza ombi la mtu anayelilia msaada! Itakuwa sisi tunashirikiana na wewe kwa chochote kitakachomtokea baada ya hapa!” “Ndivyo na sisi tulivyomwambia hivyo hivyo.” Kiongozi wa walinzi wa ile nyumba akaunga mkono hoja.

Jerry akiwa amewaka hasira akaanza kuwatukana. Wao hawajosoma na hawana uwezo wakufikiria. Wanaongea kama wajinga tu kwa kuwa hawana pesa. Akawatukana hapo akikataa wasiingie ndani, Tino akimshangaa Jerry. Alionekana ni mtu aliyefanikiwa sana. Akiwa anapeleka pesa nyingi sana pale benki! “Kumbe wewe ni hovyo hivyo!” Tino akajikuta akitamka waziwazi. “Nilikuona ukiwa unakuja pale benki nikawa nakutamania maendeleo yako mpaka kuanza kutafuta siri ya mafanikio...” “Hata ufanye nini, huwezi kunifikia.” Jerry akajibu kwa kiburi. “Na mimi sitaki tena. Sitamani hata kuwa kama wewe. Hovyo tu! Huna hata hekima! Pesa yako hapo inakusaidia nini sasa?” Tino akamuongelesha kwa ukali.

“Na ngoja nipigie simu magazeti ya udaku waje hapa wapate habari ya kesho.” Tino akamtisha. “Unang’ang’ania mtoto mdogo wakumzaa mwenyewe wewe baba mzee hivyo! Acha kinuke magazetini kesho.” Tino akatoa tena simu yake. Kabla hajabonyeza, Jerry akataka kumkimbilia kule alipokuwa, hapo ndipo wakamkamata na kumuweka chini, akawa amelala chini kabisa.

Kwanza alishawaudhi kwa kuwatukana. Wakamshikilia pale chini kwa nguvu, Tino akakimbilia ndani. “Lara!” Akamuita akifuata sauti alipokuwa akilia. “Amenifungia. Kama funguo haipo hapo mlangoni, basi anayo mfukoni.” “Haipo hapa. Usilie sasa. Nilikuja na polisi, wamemshikilia.” Lara akashituka sana. “Tino! Nilikwambia usimwambie mtu!” Lara akalalamika tena akiwa ndani. “Ulifikiria ningefanyaje Lara? Wewe umenipigia simu ukilia, halafu nikasikia kelele nyuma! Sikujua hatari iliyokuwa ikikukabili! Nisingeweza kuja tu mwenyewe.” Lara akanyamaza huko ndani. “Usiwe na wasiwasi. Sijawaambia watu. Niliomba tu ruhusa kwa bosi nikamwambia ninadharula kwa kuwa tulikuwa kwenye kikao, natoa ripoti ya kanda ya ziwa, nikakimbilia polisi hapo Surrender, nikaja nao na gari yangu.” “Nashukuru Tino. Ila naomba usiniache hapa.” “Acha ni..” “Yuko ndani kweli?” Polisi mmoja akaingia.

“Yupo huko chumbani amemfungia. Funguo atakuwa nazo mfukoni.” Wakatoka tena, Jerry akiwa chini ya ulinzi. Tayari walishamfunga pingu. “Tunaomba funguo ya chumba kile ulichomfungia Lara.” Akaanza Tino. “Lara ni mpenzi wangu, na nimekuwa nikiishi naye hapa ndani. Ulizeni hawa walinzi wanaokuja kulinda hii nyumba kila siku. Kilichotokea kati yetu ni mambo ya unyumba tu, tutayamaliza wenyewe.” “Hayo ayakubali na Lara pia. Msikubali kusikiliza upande mmoja. Lara analia ndani, amemvunja mkono, anahitajika huduma za hospitalini. Na hivi mnavyochelewa kufungua, hatujui tunahatarisha vipi maisha yake.” Tino akaongeza. Askari mmoja akaanza kuingiza mikono mifukoni kwa Jerry kikatili bila kusubiri, Jerry akiwa bado na pingu.

“Mnaingilia mambo ya kiunyumba.” Akalalamika Jerry akiwa amekalishwa chini. “Lara ni mkeo?” Askari mwingine akauliza. “Haikuhusu.” Jerry akajibu kwa jeuri. Wakapata funguo wakaenda kumfungulia Lara akiwa ameshabadili zile nguo za kulalia zilizokuwa zimemuacha uchi. Tino akamsogelea. “Amekupiga?” Lara akaendelea kulia. “Kuna nini?” “Naomba usiniache hapa. Jerry ataniua kwa hasira.” “Unamaanisha nini?” “Nilishakusanya vitu vyangu. Nataka kuondoka kabisa Tino.” Tino akatulia kidogo.

Lara akasogea kumuonyesha mizigo yake. Kumbe wakati akilia alikuwa akiendelea kukusanya vitu vyake. “Nisaidie Tino!” Tino akasogelea ile mizigo. Akabeba yote kwa pamoja mikono yote. “Nihivi tu?” “Ni nguo tu na viatu ndio vyangu humu ndani. Na nimemaliza.” “Haya twende.” Wakati wanatoka chumbani na polisi mwingine akaingia akampokea Tino, ndipo wakatoka kabisa nje barazani.

Jerry akataka kusimama wakamzuia. “Huwezi kuniacha kipindi nina matatizo Lara!” “Umeniumiza Jerry. Sijui umepatwa na nini lakini umeniumiza na isingekuwa kuingiliwa, sasa hivi ungekuwa umeniua. Sitakuwepo hapa kuendelea kuteseka, halafu na mimi unisababishie matatizo! Hapana Jerry. Mimi sio mkeo, sina sababu ya kukuvumilia.” “Kwa hiyo ulitaka starehe tu?” “Ndivyo ulivyoniahidi, starehe imeisha, naondoka. Umeniumiza naenda kutibiwa.” “Huwezi kuondoka. Kwanza hivyo vyote ni vitu vyangu.” “Tino naomba nisaidie kufungua aangalie hapahapa mbele ya polisi ajue nimeondoka na vitu vyangu tu sijaiba hata kijiko. Wewe ni mnyanyasaji Jerry.” “Ningekuwa mnyanyasaji ungechezea mamilioni yangu ya pesa?” “Si kwa kuwa na wewe ulikuwa ukichezea mwili wangu! Wewe vipi? Bakia na pesa yako uone kama utapata wakati mzuri kama niliokuwa nikikupa mimi.” Tino akaanza kufungua mizigo ya Lara huku akiwasikiliza wapenzi hao wanavyojibishana.

Vitu vya thamani tupu. “Hizo zipo set nzima, nilikununulia mimi.” Tino akashika. “Hizi?” Tino akamuuliza. “Ndiyo.” Wakashangaa Tino anacheka. “Sasa Mkuu, unataka uanze kujipaka na kujipulizia pafyumu za kike!? Maana hivi vyote vya kike!” “Kama yeye ameshindwa wapo wanawake wenzie wanalilia hiyo nafasi anayoichezea.” Jerry akaongea kwa kiburi. “Kwa hiyo unataka kuja kuwapa wanawake zako makombo ya Lara!? Umeishiwa kiasi chakupokonya mafuta!?” Wale polisi wakacheka. “Ni jasho langu. Kwa hiyo ni haki yangu.” “Aisee wewe ni wa ajabu! Haya, mbali na haya mafuta na hivi vitu vya kike, na hizi chupi za Lara pia unataka?” Tino akamuuliza kwa kejeli.

“Hata ukinikejeli ni vyangu.” “Umeishi na Lara kwa muda gani hapa?” Kimya. “Eti Lara?” Yule polisi akamgeukia Lara. “Miezi 7 sasa.” Lara akajibu kwa aibu. “Sasa huyu si kama mkeo kabisa! Kisheria anatakiwa adai haki zote kama mkeo, mtakapoachana.” Yule polisi akawa mkali. “Tino, funga hiyo mizigo, twende kituoni. Huu ni udhalilishaji wa hali ya juu. Rudisha hata hayo mafuta ndani, tukaandikishe kesi, tuone sheria inataka kumgawia nini Lara baada ya kuachana.” “Mimi sitaki kumuacha.” “Kwa kipigo ulichompiga, umemvunja mkono na kumchubua mpaka usoni! Hataki kuishi na wewe, anaondoka kisheria. Wewe si ni mkorofi na unamatusi? Sasa twende ukatukane jela. Umepiga mwanamke.” Wakamuingiza kwenye gari ile ya kampuni ya ulinzi pamoja na askari polisi mmoja, Tino akachukua mizigo ya Lara na polisi mwingine, wakaelekea kituoni wakitumia gari ya Tino.

“Mimi sitaki kesi Tino.” Njiani Lara akaongea taratibu. Wote wakamgeukia pale alipokuwa amekaa kiti cha nyuma. “Huyu jamaa anaonekana ana pesa sana, usiondoke na maumivu tu. Wakimbana vizuri pale kituonia, utaondoka na pesa hata ya matibabu, ukaenda kuanza maisha kwengine ukiwa umetulia. Usiende kulala njaa.” Yule polisi akamshawishi. “Na anapesa kweli! Mimi namfahamu kwa kuijua pesa yake.” Tino akaongeza. “Hapana. Jerry alikuwa mtu mzuri sana kwangu. Sana. Kuanzia Juzi sijui amepatwa na nini! Hakuwahi kuwa hivyo. Sitaki kumtia matatizoni.” “Na alivyokupiga vyote hivyo!” Polisi akamuuliza. “Hajanipiga. Leo hakunipiga ila kuvunja mlango ndio ukaniumiza.” Gafla Lara ndio akawa mtetezi wa Jerry tena.

“Unamtetea nini mshenzi tu yule! Ametutukana sana. Lazima aadabishwe.” Lara akanyamaza akimfikiria Jerry. Anatakiwa na familia yake. Mkewe mgonjwa. Akamuhurumia. Wakafika kituo cha polisi, wakamshusha Jerry kama mtuhumiwa, wakaenda mapokezi. Wakataka kuandikisha kesi. “Mimi sitaki kuandikisha kesi.” Lara akashangaza wote. Aliongea kwa upole akiwa ameshikilia mkono wake. Usoni akionekana ameumizwa. Jerry akashangaa. “Ninachotaka ni kuondoka na kumuacha kwa amani. Sitaki kesi.” Lara akaweka msisitizo. Mkuu wa kituo hapo akatoka kumbe anafahamiana vizuri sana na Jerry.

“Unafanya nini hapa, wewe!?” Akamuuliza akionekana kufahamiana kwa karibu. “Waulize vijana wako! Wamenivamia nyumbani kwangu na kunitia pingu.” Jerry akataka kuwageuka. “Hapana Jerry. Ukifanya hivyo kwa hakika nitakufungulia mashitaka.” “Ni nini kinaendelea?” Yule mkuu wa kituo akauliza. “Jerry alitaka kunidhuru ndio mimi nikapiga simu kuomba msaada.” Lara akawahi yeye hujibu. “Nani alikwambia nilitaka kukudhuru wewe Lara!?” “Huu mkono na uso mpaka shingoni, ni wewe umeniumiza Jerry. Acha kubisha na kutaka kufanya watu wote wajinga hapa. Ukitaka kufanya ubishi nafungua shitaka.” Lara akamjia juu, mkuu wa kituo akaomba wakazungumze ndani ofisini kwake.

“Pesa ni kila kitu jamani!” Akasikika Tino akilalamika kwa sauti ya chini wakati Lara, Jerry na mkuu wa kituo wakiingia ofisini. “Ilikuaje?”  Akauliza mkuu wa kituo wakati wanakaa. “Ni mambo ya kifamilia.” Akawahi Jerry. “Na kama nilivyowaambia wale askari, ni mambo ambayo tunaweza kuyamaliza sisi wawili.” Yule askari akaonekana kama hajaelewa. “Labda nianzie kwenye swali la mwanzoni kabisa nililotakiwa kuuliza. Huyu binti ni nani?” Lara kimya.

“Mpenzi wangu na tulikuwa tukiishi pamoja. Ikatokea kutokuelewana, mwenzangu akapiga simu kuomba msaada, nashangaa navamiwa!” “Husemi ukweli Jerry. Unamdanganya.” Lara akaeleza tokea wapo Mwanza mpaka siku hiyo. Alivyompiga jana yake, yule polisi mwenyewe akabaki ametoa macho.

“Nilimueleza ni kwa sababu ya matatizo yakifamilia.” “Jeremiah!” Lara akawasikia wanabadilisha lugha. Wanaongea kilugha kwa muda mrefu tu  lakini alionekana kumsemesha kitu kwa kuweka msisitizo na ukali kidogo. Ila kuna sehemu Lara akasikia akimwambia, ‘hasira zinaweza kukusababisha ukaua’. Akaendelea kwa kilugha tena. Akasikia, ‘haitajalisha sababu, ila utaishia jela na pesa yako ije iliwe na watu baki’. Alizungumza naye kwa muda mrefu wakimuacha Lara ametulia anasikiliza bila kuelewa.

“Tafadhali naomba myamalize Jerry. Yamalizeni hapahapa. Mwache aondoke kwa amani kabisa. Kama mnakuja kuanza, mje muanze wakati mwingine. Huyu anao ushahidi wa kukutwa na hawa polisi amefungiwa na umemuumiza. Unataka haya mambo yaende mbali? Unataka aje adai haki za kama mke?” Akauliza kwa ukali kidogo.

“Mimi sitaki kesi. Nataka niondoke kwa amani na aahidi asinitafute kuja kunidhuru tena. Hilo tu.” “Kwa hiyo unaniacha Lara?” “Wewe ndio unaniacha Jerry. Tulikuwa na amani, ukaamua kuvuruga. Tukiwa Mwanza nilikuhakikishia mimi sina mwanaume na wala sina mpango wa kuondoka, lakini umeendeleza fujo na manyanyaso ukinihesabia vitu ulivyonipa! Hata kama sasa hivi tunasema tunarudiana, naishije tena na wewe kwa mabaya yote hayo uliyonifanyia na vile ulivyoninyanyasa!?” “Ni hasira tu Lara.” “Hasira za nini kwangu mtu ambaye nimetulia tu sijakufanya chochote?!” Lara akaanza kulia tena.

“Nasikia maumivu makali. Naombeni niende hospitalini. Naona mmekutana ndugu, mnaongea mambo yenu sasa hivi mnanisahau mimi.” “Jerry!” Yule mkuu wa kituo akamuita kama kumkumbusha kitu. “Kama unamkumbusha ili aniombe msamaha, usijisumbue. Mimi namjua Jerry. Hawezi kuniomba msamaha na wala mimi sihitaji msamaha wake. Nimesamehe na sitaki afunguliwe kesi. Ana mambo ya kifamilia yanamsubiri. Kumfungia kokote ni kuadhibu familia yake. Mwacheni tu ila naomba mwambie asinifuatilie tena, wala asinitafute hata kwa ujumbe. Tukiachana hapa, ndio iwe basi.” “Kweli Lara una roho ngumu!” Wala Lara hakumwangalia tena. Akabakiza macho kwa yule mkuu wa kituo. Baada ya mazungumzo marefu hapo, ikabidi wamalize na kuwaruhusu maana Lara alizidi kulia maumivu, Jerry akimng’ang’ania mpaka ikabidi yule mkuu wa kituo awe mkali sana kwa Jerry.

Tino alisimama wakati Lara anatoka akijifuta machozi. “Acha basi nikupeleke mimi hospitalini. Naomba Lara. Ili tuachane kwa amani.” Jerry akatoka na hilo ombi akiwa hana pingu. “Asante, lakini hapana Jerry. Inatosha. Twende Tino.” “Lara! Ni hospitali tu! Sita..” “Hapana Jerry. Tumezungumza. Naomba fanya kama nilivyokwambia, ondoka. Mwache huyo binti kwa sasa.” “Nataka kusaidia tu.” Jerry akaendelea kung’ang’ania wale polisi pale wakimshangaa.

“Twende Tino.” Lara hakutaka hata kumjibu. Wakamuona anatoa walet yake. Lara akajua ameambiwa awalipe wale polisi waliofika nyumbani kwake na kumchukua. Lara hakusubiri. Akatoka, Tino akamfuata baada yakuwashukuru wale polisi walioongozana naye mpaka nyumbani kwa Jerry na kumsaidia kumtoa Lara. Kwa kuwa alijua Jerry atawalipa, aliwanong’oneza kitu wale polisi, wakacheka na kutoka akiwaambia ulaji mkubwa unakuja. Akimaanisha kutoka kwa Jerry.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment