Walifika hospitalini moja kwa moja Tino alimpeleka kitengo cha mifupa. Bado Lara alikuwa amebeba mkono wake akinung’unika maumivu. Wakakaa hapo wakisubiria kumuona daktari. Walikuta foleni kubwa. Tino na Lara wakapata sehemu ya kukaa, wakakaa. Watu waliokuwa wametangulia wakaendelea kuonwa na daktari, wakiitwa namba zao, Lara akiwa amejiinamia hata hakuwa na wazo na simu, ila Tino akiwa kwenye simu yake muda wote wala hawakuendelea kuzungumza.
Alikuwa ameshika chupa ya maji na mfuko mdogo. Akamkabidhi Tino bila
hata salamu akamsogelea Lara karibu. “Pole.” “Asante.” Akamshika shingoni kule
kwenye alama nyekundu na shavuni. Lara macho chini. “Wamekuangalia na
huku?” Lara akatingisha kichwa kukataa,
na kujifuta machozi. “Ndio tunasubiria hapa kumuona daktari. Bado hata
hatujamuona!” Tino akamjibu. “Ni mkono upi? Huu ulioshika?” Jax akaendelea
kuuliza taratibu akionyesha kuumia na yeye. Lara akatingisha kichwa kukubali.
“Jax ameleta dawa za maumivu ili kupunguza maumivu wakati tunasubiri.” Tino
akampa dawa na maji. “Asante.” Lara
akashukuru na kumeza vile vidonge viwili alivyopewa na Tino.
“Tukae.” Jax akaongeza wakati na yeye akikaa, kuashiria na yeye ndio
amefika. Lara akajikuta amebakiwa na nafasi ya katikati ya Jax na Tino. Akakaa na
kumgeukia Tino kama kumuuliza ni kwa nini alimuita! Tino akajidai anapiga simu
akaondoka pale, akamuacha hapo na Jax. Lara alitamani kumfuata nyuma, lakini
ikabidi awe mpole, atulie tu. Aibu, asijue Jax aliambiwa nini juu ya tukio lake.
Akatulia.
“Upo namba ngapi?” “Tino ndio anacho kikaratasi nafikiri 55.” “Hapo
nikumuona tu daktari?!” “Ndiyo.” Jax akafikiria kidogo. “Ninawazo la tofauti
Lara. Hapa tutakaa sana, twende kwenye hospitali yakulipia.” “Hapana Jax. Mimi
nitasubiri tu hapa.” “Kwa nini?!” Lara akabaki kimya. “Utaendelea kuwa na
maumivu ukisubiri hapa mpaka muda gani? Foleni ni kubwa sana, bado hata
hawajafika 20!” Kisha akamgeukia vizuri kama aliyeshangazwa na kitu ambacho
hakutarajia. “Tumeanza lini kupishana mawazo!?” Jax akamuuliza kwa upendo tu.
“Naepuka gharama.” “Kipi cha muhimu na haraka? Kuweka pesa benki au kupata
matibabu yako?” Lara akainama mbele yake wakiwa wamekaa pale.
“Twende.” Akasimama na kumnyooshea mkono kama kumsaidia kusimama.
“Acha tu, nitaweza kusimama. Asante.” Akasimama peke yake. Akampigia simu Tino,
wakakutana nje. “Vipi tena?” “Naona hapa tutakesha. Acha twende kwenye
hospitali ambayo watafanya mambo kwa haraka, hii siku iishe na yeye Lara
akapumzike. Lasivyo tutalala hapa.” “Wazo zuri. Sasa mimi nitawafuata huko.
Maana natakiwa kazini mara moja.” “Hamna shida, nitakujulisha tutakapokuwa.”
Lara akashituka sana. Inamaana anaachwa na Jax! “Naomba tuzungumze Tino, kabla
hujaa... Naomba tuzungumze.” Akamsukuma kwa nguvu Tino kwa mkono wake wa
kushoto ambao hauna maumivu. Tino akajua anachosukumiwa ni nini. Akaanza
kucheka taratibu.
“Kabla hujapaniki, sijamwambia kila kitu ila nilimwambia nipo na Lara
hospitalini.” Lara akabaki akimsikiliza. “Nilimwambia umeumia mkono.” “Tino!
Mbona humalizii unarudiarudia tu?” “Kwa kuwa Jax mwenyewe ananiangalia, na wewe
umenisimamia hapa kwa ukali, nashindwa kuzungumza.” “Nilikuomba usimwambie mtu!”
“Sijamwambia mtu yeyote ila Jax, uliyemuacha akikutafuta na kujilaumu kama
mwehu. Nilimwambia nilikuona Mwanza, akanilaumu sana kushindwa kujua ni wapi
unaishi au kukuomba hata namba! Nilimwambia upo na mtu wako, na ni Mr Kembo.”
Lara akatoa macho.
“Kwani Jax anamfahamu Jerry?!” “Kabla hajahama pale CRDB yeye ndio
alikuwa akihusika na akaunti zake. Kwa zile pesa alizokuwa akiingiza pale, mimi
na Jax tukaanza kumwita ‘the god’. Kwa hiyo ndiyo, Jax anamfahamu vizuri sana.” Lara akachoka.
“Naomba usiniache naye, tafadhali Tino. Twende wote.” “Natakiwa kazini mama!
Acha nikachungulie tu, nitawafuata.” “Sasa kwa nini ulimuita hapa?” Lara
akalalamika akimshikilia shati kama asimuache. “Nilikwambia jinsi alivyonilaumu
jinsi nilivyokuacha kule Mwanza. Nilimwambia ulikuwa na ‘the god’, pia hakuona
kama nisababu yakueleweka kutokukufuatilia. Naomba utulie Lara, utibiwe tujue
ni nini kinakusumbua.” “Muda unazidi kwenda.” Wote wakamgeukia Jax.
“Acha mimi niende.” Tino akakimbia kwa haraka. Akawaacha hapo. Lara
alishindwa hata kumuangalia. “Twende.” Jax akaweka msisitizo. Lara akamfuata
nyuma. Jax alikuwa bado na gari yake ileile. Akamfungulia mlango, Lara
akapanda. Ile hali ya utulivu moyoni aliyoipata mle ndani ya gari ya Jax mara
baada yakupanda kitini, hata kabla Jax hajapanda na kukaa kwenye kiti chake,
Lara akajikuta anatokwa machozi. Alilia sana mpaka Jax anapanda garini,
akamkuta akilia.
Akamshitua Jax. “Maumivu makali?” Akatingisha kichwa na mabega
kukataa. “Nisikilize Lara. Uso wako ni mwekundi na macho mekundu na yamevimba
sana, kuashiria baso upo kwenye tension. Mimi nipo hapa na wewe, naomba
jaribu kutulia. Sawa?” Lara akatingisha kichwa kukubali. Jax akaondoa gari
kuelekea hospitalini.
Walikaa na Jax hapo hospitalini akifanyiwa vipimo mpaka mwisho
akaonekana anahitaji PoP, wakaelekea upande huo kusubiri ili afungwe.
“Nimefurahi kukuona Lara.” Hilo neno likamuuma sana Lara, akainama nakuanza
kulia tena. Alilia sana Lara, hata hakujua anacholia. Akajichukia kupita kiasi
na kujidharau. Hao watu alitamani kuja kukutana nao wakati mambo yake yapo
safi. Amependeza anayo mafanikio. Hapo alipo hajui hata baada ya hapo anakwenda
kulala wapi!
Ingekuwa mapema kidogo,
angepanda basi kukimbilia nyumbani kwao, Dodoma. Yeye yupo hapo hospitalini na
Jax, lakini mizigo yake ipo kwenye gari ya Tino. Ametolewa kwenye ugomvi
nyumbani kwa mume wa mtu! Mtu mzima kabisa! Akiwa ameumizwa vibaya sana.
Alikuwa kwenye aibu hajui hata anamtizama vipi huyo Jax aliyemkimbia tena akiwa
amemuonya huko anakokimbilia hatakuwa salama.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Tino alirudi hapo akiwa ameshafungwa PoP mkononi. Jax alilipia
akachukua dawa za maumivu, wakaanza kutembea kuelekea sehemu waliyoegesha
magari. Mapigo ya Lara yakienda mbio, hajui anafanyaje kwa wanaume hao wawili.
Mmoja anayo mizigo yake kwenye gari, Jax amekuwa naye mpaka akatibiwa. Anawaaga
anakwenda wapi! Lara akawa anatembea taratibu huku akiwaza chakusema na jinsi
yakuachana na hao watu wawili. Wakatembea mpaka wakafika kwenye eneo yalipo
magari. Wakasimama hapo kama waliopoteza dira na wao.
“Naomba nikushukuru Jax. Asante kwa matibabu. Naomba Tino mwenye mizigo
yangu unipeleke nikapumzike.” Lara
akaongea taratibu akiwa hata hajui atapelekwa wapi. Ila tu alitaka kuachana na
Jax kwanza. “Unakwenda wapi?” Jax akauliza taratibu tu. “Kupumzika. Najihisi
kuchoka na kichwa kinaniuma pamoja na macho. Nahitaji kulala.” Lara akajieleza
akikwepa swali la ni wapi anakwenda. “Lara!” Jax akamuita tena kumkumbusha
swali lake. Lara akanyamaza. “Kwa chochote utakachoamua, naomba isiwe kujificha
tena. Au safari hii sio kunitoroka tena. Mimi ni mtu mzima, nakuahidi kupokea
na kuheshimu maamuzi yako lakini si kwakutengana.” Jax akawa muwazi kabisa.
“Umenielewa Lara?” Lara akajifuta machozi na kutingisha kichwa. “Samahani niliondoka bila kukuaga Jax. Lakini
nilihitaji...” Akasita Lara. Akajifuta tena machozi. “Nilikuwa siwezi kupumua! Nilihisi nimebanwa pua! Siwezi
hata kupumua! Nilihitaji kuondoka.” “Ungeniambia, ningeelewa Lara. Na
ningeheshimu kuliko kuondoka tu! Kwanza ulikuwa mgonjwa. Huna damu, halafu
hukuwa umenijibu chochote! Tulikubaliana nikirudi tuzungumze. Sikujua ni nini
kimekupata! Sikujua kama ulikuf..” Wakamuona Jax anageukia pembeni. Anajifuta
machozi. “Samahani Jax. Samahani sana.” Lara
naye akajikuta akilia na yeye. Tino amebaki hajui azungumze nini.
“Naomba kujua unaelekea wapi Lara.” Jax akauliza baada yakutulia.
“Nataka kujua kwa hakika. Sitakusumbua, nakuahidi nitafuata matakwa yako ila
nataka kujua wapi upo.” Lara akajifuta machozi na kusafisha koo. “Kesho
nitarudi nyumbani.” “Kwamba unarudi kuishi Dodoma kwa wazazi!?” Tino akauliza
kwa mshangao. “Nahitaji muda wakupona. Nitulie na nijipage upya, ndipo nijue
baada ya hapo nini kinafuata.” “Mimi bado hujajibu swali langu Lara. Sasa hivi
unakwenda wapi?” Jax akauliza tena. “Nilitaka Tino anisindikize mpaka hotelini,
nilale kwa usiku wa leo, kesho ndio nirudi nyumbani.” “Kweli Lara?!” Tino
akauliza kwa mshangao sana na kuumia.
“Nitafanyaje Tino? Wewe unajua hapa mjini sina hata ndugu na...”
“Sisi hapa tuliosimama mbele yako ni kina nani?” Tino akauliza. “Wewe unajua
nina nyumba, na Jax ananyumba. Upo mgonjwa, kweli unataka kulala hotelini
halafu urudi kwa wazazi ndio wakuuguze baada ya kula starehe mjini, unarudi kwa
wazazi kuwapa wao shida!” “Usinilaumu Tino.
Ningejuaje nafasi zenu?” Lara akajifuta machozi. “Nilikuacha ukiwa unatengeneza mahusiano na Suzy! Nimeondoka kwenye
maisha yakina Suzy miezi mingi imepita. Siwezi tu kurudi nijifanye mambo yapo
vilevile Tino! Sijui nafasi yako sasa hivi kwenye maisha.” “Na Jax je?
Hata kama ndoa ilishindikana, lakini sisi tulikuwa marafiki Lara!” Tino
akasisitiza.
“Ndio maana uliponiita asubuhi hata sikufikiria, nikakimbia kuja. Kwa
nini na wewe unashindwa kuonyesha moyo huohuo, kwetu? Inaonekana bado
hujasamehe Lara!” “Wewe nimekupa sababu Tino. Kwa nini nimeshindwa kukufikiria
kuja kwako. Pia sio heshima kwa Suzy! Hata kama hamuishi pamoja, leo aje
agundue nilihama pale kwetu tulipokuwa tukiishi pamoja, eti naishi na wewe! Sio
sawa. Na kwa Jax.” “Ehe! Kwa Jax kuna nini?” Tino akauliza.
“Jax alinipeleka kwake Tino. Haki nilishindwa kukaa. Naomba niwe
mkweli. Nilijiona naingia nyumbani kwa Tula na Jax sio kwa Jax tu.” “Lara!” Jax
akashangaa sana. “Kweli Jax. Uliniacha mimi. Au ulikimbia pale tulipokuwa
tukiishi wote, mimi na wewe. Ukipaona hapana hadhi kwa mpenzi wako. Ukahama
naye sehemu ambayo hata sikuwa nikiijua! Ukaona mpenzi wako hastahili kuishi
sehemu kama ile tuliyokuwa tukiishi mimi na wewe, ukaenda kumnunulia nyumba au
kumuhamishia kwenye nyumba ya thamani ambayo ulikuwa nayo wakati tupo pamoja,
tukilala tunapepewa na feni, huku joto na kelele za mtaani zikiendelea usiku kucha!
Ukaona yeye hastahili shida niliyokuwa nikiipata mimi! Ukaenda
kuishi naye sehemu nzuri!”
“Eti yameshindikana kati yenu, ndio eti unanipeleka
mimi palapale kwenye ile nyumba uliyomthaminisha mpenzi wako, mkaishi naye kwa
mapenzi yote! Leo eti mimi ambaye ulikuwa radhi kuishi na mimi kwenye joto
vile, nyumba hiyohiyo ikiwepo ila hukutaka kunipeleka tokea mwanzo, ndio leo niombe
hifadhi! Kweli jamani!? Hata kama mnanidharau sio kwa kiwango hicho.” “Haikuwa hivyo Lara!” Jax akajitetea
akiwa ameishiwa nguvu kabisa. Hakujua kama kile ndicho anachofikiria au
kinachomuumiza Lara, tena kwa upana huo!
“Lakini ndivyo inavyoonekana Jax. Hapo hata mimi namtetea Lara.” Tino
akaongeza akionekana na yeye kumuelewa Lara. “Kwa
vyovyote ilivyokuwa Jax, kama ungeona kuna uthamani wa mimi niliyekuwa na wewe,
ukikusudia kunioa, nastahili vitu vizuri, ungenipeleka pale mapema kabla ya
Tula! Hukukusudia mimi niwe pale. Ile nyumba ni ya Tula na yako, Jax.
Mimi siwezi, na nimeshindwa kabisa kuwa pale. Nilihisi kubanwa punzi. Nikajiona
najidhalilisha au naungana mkono na wewe kunidhalilisha. Siwezi kufanya watu
waniheshimu, lakini siwezi kujipinga mimi mwenyewe.” Wote kimya.
Wakabaki kama wakiwaza. Lara aliongea kilichokuwa kikiendelea moyoni mwake.
Akatulia kwa muda akijaribu kutulia.
“Nyumbani ni nyumbani tu. Mama alinilea nikiwa
nimeachwa na kila mtu, nimeharibikiwa mimba. Nilikuwa mgonjwa wazaidi ya huu
mkono. Tino ni shahidi damu zilizokuwa zikinitoka, wakisaidiana na mama kufuta
njiani. Unakumbuka maneno ya mama aliyokuwa akikwambia na kukushukuru kumsaidia
kunirudisha nyumbani?” Kimya.
“Kwa kifupi tu, hata jana nilizungumza na baba,
akaniambia bado hajashindwa kunilea na haitakaa ikatokea ninakuwa kwake. Nitabaki
kuwa kiziwanda wake daima. Hapo ndipo ninapotaka kwenda sasa hivi nikapumzike.
Tafadhali Tino, nisaidie kunifikisha hotelini nilale, kesho nirudi kwetu.
Nakushukuru Jax kwa kuwa na mimi leo. Asante. Safari hii nimeaga. Narudi kwetu.
Sijui itakuaje baada ya kupona. Lakini safari hii naaga. Sitoroki. Tino
nakushukuru, na samahani kwa ukimya wa muda wote niliokuwa nimeondoka.” Kimya. Lara akaongoza njia kuelekea kwenye
gari la Tino, akawaacha marafiki hao wawili, wamesimama hapo.
Akaona gari ya Tino inawaka taa na kutoa mlio, akajua amefungua,
akapanda kiti cha mbele cha abiria, akafunga na mkanda, akawaacha bado wapo nje
wamesimama, pembeni kidogo kwa gari la Tino. Wakazungumza kidogo, Lara akaona
Tino anafungua mlango. “Nitakupeleka hotelini, utakuwa hapo mpaka jumamosi
asubuhi tutakuja kukusindikiza mpaka nyumbani.” “Hapana Tino. Jax alishaniacha
na mlishakwenda kuzungumza na wazazi. Wewe na dada Nelly mlishayamaliza
mahusiano yangu na Jax kwa heshima. Madeni ya ile harusi nilishayalipa yote.
Nimelipa ndugu, jamaa na marafiki wote waliokuwa wamechanga na kudai wazazi
wangu. Jax sio mpenzi wangu, ananirudisha vipi nyumbani? Inakuwa nikutibua
wazazi wangu tu!” “Na mimi?” Tino akauliza.
“Mimi sihitaji msaada wakurudishwa nyumbani. Msaada ninaokuomba wa
mwisho ni uniache hotelini, basi. Tafadhali usianze mambo mengine Tino. Mimi si
mke wala mpenzi wa Jax tena.” “Na mahusiano tuliyojenga?” “Nayathamini ndio
maana nilipopatwa na shida umekuwa mtu wa kwanza kukufikiria na kukukimbilia.
Naomba mimi ndio nikuombe msaada. Naomba mimi ndio niseme ni nini nataka,
msinipangie. Na ndio maana mara ya kwanza niliondoka bila kuaga kwa sababu
nilijua kila mtu atataka nifanye vile anavyofikiria yeye.” “Samahani Lara. Ni
kweli. Nitaheshimu hilo. Basi twende ukapumzike, halafu kesho asubuhi nitakuja
kukusindikiza kituo cha mabasi. Ni sawa?” “Nitakujulisha usiku kama nitahitaji
huo msaada, kutokana na nitakapokuwa nimelala na umbali mpaka kituo cha mabasi.
Naweza pata taksii, ambayo itanifikisha kituo cha mabasi bila shida.” Tino
akanyamaza na kuondoa gari.
Wakaondoka hapo kila mtu
kimya, Lara akajiegemeza vizuri. Tino akakanyaga mafuta akitafuta hoteli karibu
na Ubungo. “Naomba nije kukupeleka kituo cha mabasi Lara.” Baada ya muda Tino
akavunja ukimya. “Uliahidi kuheshimu maamuzi yangu, Tino.” Lara akamjibu
taratibu tu. “Sawa. Basi nitasubiri unitafute.” “Nashukuru.” Wakanyamaza.
Walipokuwa kwenye mataa, akamuona anatuma ujumbe mpaka taa za kijani ziliruhusu
lakini Tino alikuwa akituma ujumbe. Lara akahisi anawasiliana na Jax.
Akajituliza kimya.
Tino alimfikisha hotelini, akamchukulia chumba na kuanza kuhangaika
yeye mwenyewe kuingiza mizigo ya Lara ndani, mpaka chumbani. “Hiyo mizigo ni
mingi na ipo kwa mafungu mafungu madogo madogo Lara. Unataka nikakutafutie
sanduku tujaribu kuiweka pamoja?” Lara akanyamaza. “Utasafirije na mizigo mingi
hivi? Acha nikakununulie masanduku.” “Nitapanga vizuri, yote itaingia kwenye
haya masanduku. Hayajajaa. Nilifungasha kwa haraka tu. Lakini nikitulia na
kupanga vizuri, vitaenea tu. Nakushukuru kwa kila kitu. Asante, ila naomba
uondoke, nipumzike.” Tino akabaki amekaa hapo kitandani.
“Sasa unataka nini Tino? Nenda mimi nilale, nimechoka sana.” “Basi
nikalete chakula.” Lara akamwangalia na kukaa pembeni yake. “Nimechoka na
kichwa kimechanganyika Tino. Nina uchungu wakupitiliza. Nahitaji utulivu tu.
Tafadhali niache nilale.” “Unaahidi kuja kunitafuta tena? Maana najua kesho
hutanitafuta Lara.” “Nipe muda Tino.” Tino akatulia kidogo. Lara akamwangalia.
“Umependeza Lara! Umependeza sana. Tofauti na mara ya mwisho tulivyoachana
baada ya tukio la Jax. Naomba usirudi kule.” Lara akawa amemuelewa.
“Nisikilize Tino. Jerry sikumpenda kama Jax. Jax nilimpenda haswa.
Lakini Jerry nilimkubali ili kustarehe tu. Na ndivyo alivyonitongoza na
kukubaliana starehe. Ugomvi ulionikuta nao na Jerry, ni pale alipotaka awe Jax.
Nilimkatalia kabisa. Kwa kuwa nilijua Jerry ameoa na anafamilia yake. Ni mtu
mzima hawezi kuja kuwa mume wangu ndio maana Jerry alikasirika. Mkewe anaumwa
anakaribia kufa huko nchini kwao. Jerry anataka mimi nije kuwa mkewe!
Nikamwambia hapana.” “Lakini yule jamaa anapesa Lara!” Tino akamjaribu.
“Hivi kwa hivi nilivyo Tino, unafikiria nilikosa mwanaume wakunitoa
pale tulipokuwa tukiishi na Jax, na kunipa kile Jax amempa Tula?” Lara akauliza
kwa pole tu. Tino Kimya maana Lara alijaliwa mvuto haswa. Jibu akawa nalo.
“Niliumia kwa kuwa nilijifunga kwa Jax, nakujinyima yale ambayo watu kama Jerry
walikuwa tayari kunipa. Niliumia kuona Jax ameniacha sababu ya mwanamke
mwingine wakati mimi nilikuwa nawaacha wanaume wengine wathamani kuliko Jax,
kwa ajili yake Jax! Nilimkubali Jerry kwa hasira tu, Tino. Nikaona nijipe kile
nilichokuwa nikijipunja. Na kweli nilikipata. Haswa. Usinione nipo hapa, pesa
ya Jerry nimeitumia haswa na bado ninayo. Na najua ningetaka ningeendelea
kuitumia tu, lakini bado nina tumaini Tino.” “Tumaini gani?” Lara akainama.
“Lara?” “Sijakata tamaa Tino. Naamini ipo siku na mimi naweza kupata
mwanaume atakayenipenda kwa dhati kama vile Jax kwa Tula. Atakayekubali kulipa
kila garama kwangu, akakubali tukafunga ndoa na mimi, tukaanzisha familia. Bado
nina imani Tino. Kile baba yangu alichompa mama, naamini na mimi ninaweza
kupata. Sitaki watu kama kina Jerry wanipokonye hilo tumaini. Najua ipo siku
itatimia tu.” “Nimefurahi kusikia hivyo. Nilijua umeamua kutupilia mbali maisha
yako sababu ya kilichotokea kwako na Jax.” “Hapana Tino. Nilikuwa napumzika tu.”
Tino akamwangalia vizuri.
“Sasa umemaliza kupumzika? Maana serikali ipo kwenu Dodoma. Wazito
wote wapo huko. Na wewe unavutia hivyo! Nitasikitika kuja kusikia umeharibu
maisha yako kwa magonjwa.” “Sitarudia tena.” “Kweli Lara?” “Mungu anisaidie.
Nimejaribu, imeishia pabaya. Basi. Mungu amenitoa hapo salama, naahidi, na wewe
nakuahidi, hutapata tena simu kama hizi za leo.” “Na kutokukuona kwenye mabaa
Lara. Tafadhali. Wewe ni mzuri sana na mtulivu, sio msichana wakutembea na
wanaume za watu! Kwanza ni dhambi.” Lara akacheka sana vile Tino alivyosema.
“Unadhani mimi simjui Mungu sababu ya kunywa pombe?” Lara akacheka zaidi.
“Sikosi kanisani kila siku jumapili.” “Najua Tino.” Lara akajibu huku ameinama
akifikiria. “Mbona hapo hutoi ahadi, Lara? Au unataka kwenda kuanza na Jerry
mwengine?” “Hapana Tino. Nimemaliza. Sasa hivi nitatulia. Utakayekuja kunikuta
naye baa, ujue nimemchunguza, nikaona atanipa ninachokitamani. Sio michezo
tena.” Wakatulia kidogo.
“Nikwambie ukweli Tino?” “Niambie tu.” Tino akaonyesha utayari
wakumsikiliza. “Kesho sina mpango wakuja kukupigia simu ili unipeleke kituo cha
mabasi.” “Mbona najua. Hilo nilishajua.” Lara akacheka taratibu. “Yaani tokea
unaniambia kule, kabla hatujafika hapa, nilijua hutanitafuta.” Lara akacheka na
kunyamaza. “Na mimi nikuulize Lara?”
Lara akamwangalia. “Ulinisamehe kabisa kutoka moyoni?” “Najua unanipenda Tino,
na unanijali, hutaki uniumize. Najua uliniumiza bila kukusudia. Nilikusamehe.
Lakini hivi unajua sasa hivi na mimi ningekuwa nina mtoto?” Tino akanyamaza kwa
kuumia.
“Tuyaache hayo Tino. Naomba unipishe, nioge, nilale.” “Wakati wowote, muda wowote, popote, ukiwa na shida, nipigie kama ulivyofanya leo. Umenifurahisha.” Lara akasimama akicheka kinyonge. Tino akaondoka na kumuacha.
Nyumbani ni
Nyumbani tu.
L |
ara alitua
jijini Dodoma akapokelewa na baba yake. Akashangaa alivyo. “Niliangukiwa na
mlango baba. Nipo sawa kabisa. Ila mkataba wangu wa kazi uliisha, tokea majuzi,
nikaona nije nipumzike huku nyumbani kabla sijarudi tena kazini.” “Pole mama.
Pole sana. Sasa watakupokea tena kazini?” “Nipo kwenye kufikiria. Nirudi tena
kazini au nifanye biashara mimi mwenyewe. Ndio maana nimeona nipumzike huku
nyumbani bila kumaliza pesa kwenye nyumba za kupanga.” Lara akampanga baba yake
mpaka akapangika “Umefikiria vizuri. Na hivyo ulivyo mgonjwa, itakusaidia
kupata muda mtulivu wakupona huku ukifikiria.” Baba yake akamsaidia kuingiza
mizigo kwenye gari. Wakaondoka hapo.
“Umechoka sana au unataka nikupitishe kwa mama yako kwanza?” Lara
akacheka. “Nimetoka kuzungumza naye tulipofika tu hapa na basi. Ameniambia
nimpitie pale, nikae naye mpaka jioni tutoke naye akanipikie chakula kizuri.”
Lara anarudi kwao akiwa ameongeza heshima haswa. Alibadilisha maisha ya
nyumbani kwao. Amerudi akiwa amevunjwa mkono, akiugulia maumivu ya nafsi na
mwili, lakini wazazi wake wanacheka. Amebadili historia ya kwao. Kutoka
kudharauliwa na kashfa aliyowaingiza baada ya Jax kuvunja ndoa, akawainua
wazazi wake kibiashara, angalau wanaheshimika.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Maisha yakaanza. Juma la kwanza ikawa ni kujiuguza na kupumzika tu, Lara hakutoka nje kabisa mpaka zile alama za wekundu zikapotea kabisa, ikabakia mkono tu ambao bado ulikuwa na PoP. Akaanza kutoka asubuhi na baba yake na dada yake au mama yake kama haendi kazini, anaungana nao kwenye biashara yao hiyo ya duka alilowafungulia. Anasaidia huko hata kusogeza vitu vidogo vidogo au tu kukaa nao akiwaona vile wanavyofanya kazi, kisha usiku wanarudi nyumbani. Wakaendelea hivyo kichwa cha Lara kikiendelea kuzunguka. Nini chakufanya baada ya hiyo Pop kutoka! Simu yake aliweka pembeni kabisa akitaka kutulia kwani Jerry alimpigia mara baada yakufika Dodoma. Alipoacha kupokea akamtumia ujumbe akitaka kujua kama alipatiwa matibabu na anaendeleaje! Lara hakutaka hata kumjibu. Akazima simu kabisa na kutulia.
Kulikoungua Mpini....
S |
iku moja ya
jumamosi Lara akiwa na wazazi wake dukani, mida ya saa tano asubuhi hivi akaona
gari inayofanana na Jax inasimama mbele ya duka lao. Moyo ukampasuka kwa
mshtuko. Aliposhuka mdogo wake wa kiume, ndipo akajua ni Jax, Lara akajificha
kwa kushuka kutoka kwenye kiti alichokuwa amekaa, kwa haraka mpaka wazazi wake
wakashangaa. Akatambaa na kutoka pale dukani kwa haraka akitumia mlango wa
nyuma. Mpaka Jax anashuka garini, Lara alishapotea. “Karibu baba.” Mama yake
akamkaribisha wakati baba yake, mzee Chiwanga akimuhudumia mteja. Jax
akasalimia wote na kutaka kuwashika mkono lakini mzee Chiwanga akaonekana ana
kazi, hawezi kumshika mkono Jax.
“Naona biashara nzuri wazee wangu.” Jax akasifia. “Tunashukuru Mungu,
mwanangu. Lara huyo ndiye ametusukuma. Ametupa wazo, mtaji na kuhakikisha
biashara inaanza na kusimama.” Mama Chiwanga akaongea kwa majivuno kidogo,
mumewe kimya. “Pongezeni sana.” Jax akasifia akijua ni pesa ya Jerry tu hiyo.
“Kumbe upo hapa Dodoma!?” “Hapana mama. Nimeingia asubuhi hii, nimekuja kumuona
Lara.” Wakaangaliana na mumewe. Mumewe akaendelea na shuguli zake.
“Lara alikuwa hapa, naona ametoka.” Ikabidi mama mtu ajibu. “Hamna
shida, naweza kumsubiri tu.” Jax akasimama hapo pembeni ya duka. Lisaa
likapita, na nusu. Mama yake akaamua kwenda kumtizama nyuma.
Akamkuta amelala stoo. Sehemu wanapotunza bidhaa zote wanazouza.
“Lara!” Lara akakaa. “Ameondoka?” “Sasa kwa nini unamkimbia? Si umsalimie tu!”
Lara akapandisha mabega, kukataa. “Sasa mimi nitaenda kumjibu nini? Unajua
siwezi kusema uongo. Na amekaa pale nje ya duka anatia huruma! Jua kali,
anatokwa jasho!” “Si aondoke! Wewe mwambie Lara hatarudi hapa leo. Utakuwa
hujadanganya maana ni kweli sitarudi. Naondoka zangu sasa hivi.” “Lara! Si
umsikilize? Ametoka Dar kwa ajili yako.” “Akuu! Kwani hii ni mara yake ya
kwanza kuja kwetu kwa ajili yangu? Si alishakuja mara kadhaa mpaka akaleta na
watu? Sasa hivi anakuja kufanya kipi kipya? Naomba mniache kabisa.” Lara akawa
mkali kabisa. Mama Chiwanga akatoka hapo akiwaza. Ni mama aliyempenda sana
Mungu. Mpole na mnyenyekevu. Hana makuu wala hajui ugomvi.
Akarudi pale dukani. “Mimi naona ungeenda tu ukapumzike baba. Jua
kali kweli hapo na naona Lara hatarudi leo hapa.” “Kwani anayo simu? Nisaidie
hata namba zake mama yangu. Niliyonayo haipo hewani.” Jax akauliza na kujieleza
kinyenyekevu. “Lara hana simu.” Jax akatulia kidogo kama anayefikiria. “Basi
nitarudi tena jioni kabla hamjafunga ili nione kama nitaweza kumuona.” Jax
akaondoka, mzee Chiwanga kimya. Lara naye akaondoka kabisa pale dukani.
Alichukua kabisa mkoba wake akarudi nyumbani.
Jioni kweli Jax akarudi tena pale dukani akiwa na nguo nyingine.
Akaonekana alioga na kubadili kabisa. Akafika hapo na kusalimia tena. Alikuta
wateja wengi mida hiyo ya jioni. Akakaa hapo akisubiria mpaka walipopungua.
“Pole baba, jioni kunakuwa na wateja wengi!” “Ni jambo zuri.” Jax akatulia
kidogo kama anayesita kuuliza. Na wao wakamuacha tu.
Mwishoe akauliza. “Sijui Lara amerudi?” “Hapana. Hajarudi.” Akajibiwa
tu hivyo, kimya. “Basi naomba nimsubirie.” “Hatarudi tena hapa maana hata sisi
tunakaribia kufunga.” Akajibu mama mtu. “Na kesho huwa mnafungua saa ngapi?”
“Kesho ni jumapili baba. Tunapumzika. Biashara zote tunafunga.” Akajibiwa hivyo
bila hata kukaribishwa nyumbani.
Jax akapoa. Akajua alishafedhehesha hao wazee, hata wao hawataki
kumuona tena nyumbani kwao. “Naomba nije kujaribu kumuona nyumbani.” Akamuona
yule mama anamwangalia mumewe. “Usiku tunakuwa na ibada.” Akajibu mzee Chiwanga
akiendelea na kazi bila hata kumtizama Jax. “Oooh! Sawa. Basi naomba nije kesho
kabla sijarudi Dar.” Kimya. Jax akamtizama mama Chiwanga anayefanana na binti
zake kama aliyejizaa. “Kesho kanisani baba.” Akajibu kinyenyekevu. “Naweza kuja
kabla au baada.” “Sawa.” Hivyo tu akajibiwa bila hata kuambiwa muda. Jax alijua
hatakiwi lakini akakusudia.
“Sijui muda gani ni mzuri?” Jax akamuuliza mama Chiwanga. Yule mama
akamgeukia tena mumewe. Akawa ni kama anabanwa hana jinsi. Alimjua mumewe na
binti zake. Alichukia sana kwa Jax kumkatili binti yake. Hakuwahi kusahau hali
aliyorudishwa nayo Lara alipokwenda kuchukuliwa na mama yake akiwa anavuja damu
kama aliyekatwa sehemu na akiwa na Tino sio yeye Jax, tena na yeye akiwa na
gari! Mzee Chiwanga alimuona ni kijana asiye na hekima na hajui anachotaka.
“Huwa tunakwenda kanisani asubuhi na kurudi mchana.” Yule mama
akajibu akionyesha wasiwasi, mzee Chiwanga kimya. “Basi mida ya kwenye saa saba
mchana nitakuja tena kujaribu kama naweza kuzungumza naye.” Kimya. “Basi muwe
na jioni njema.” “Asante.” Akajibu yule mama akimtizama mumewe ambaye aliongeza
shuguli hapo ndani nakushindwa hata kukaa wala kupumua mpaka Jax akaondoka.
Hata alipoaga hakumtizama.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kesho yake asubuhi walikwenda kanisani wakarudi familia nzima mpaka
mjukuu. Wakati Lara yupo jikoni na dada zake wakipika pamoja na kuzungumza
wakicheka na mama yao, Jax akarudi. Lara aliposikia anafunguliwa mlango na Lucas,
akakimbilia chumbani. “Sipo humu ndani. Mwambieni sipo na hamjui nitarudi saa
ngapi.” Lara akanong’ona na kupotea kabisa pale. Jax alimkuta mzee Chiwanga
pale sebuleni, akamsalimia, akaitika, kimya. Mama Chiwanga akajua huyo kijana
yupo matatizoni maana alipoondoka jana yake, mzee Chiwanga alimsema vibaya
sana.
“Nimekuja kumuona Lara.” “Unataka nini kijana!?” Akaanza mzee
Chiwanga kwa ukali. Jax akashituka. “Ni nini unataka kwa Lara tena? Tafadhali
zungumza acha kuzunguka nakutufanya sisi wote kama wendawazimu!” Mkewe
akakimbilia hapo sebuleni kwa haraka. “Chiwanga! Nakuomba hapa chumbani.”
Akasimama kwa hasira. “Labda kabla hamjaondoka, naomba niombe radhi wazazi
wangu. Nilikosa sana na najutia kosa. Nipo hapa kwa kuwa nampenda Lara.” “Hilo
umegundua lini?” Akauliza mzee Chiwanga kwa hasira.
“Sio wewe ulikuja hapa ukaomba kumuoa Lara?” “Nilikuja mzee wangu.”
Jax akajibu kinyenyekevu. “Tulikunyima Lara au tulikubariki na kukukarimu?
Hatukukufanya kama kijana wetu hapa?” “Mlifanya yote yaliyo sahihi mimi ndio
niliharibu mzee wangu, ndio maana nimerudi baba yangu.” Jax akapiga magoti
kabisa. “Kabla hujaomba msamaha, nataka uniambie ni kwa nini ulikuja mwanzoni, halafu
kwa nini ukamkataa mwanangu, na kwa nini leo tena upo hapa? Huu ni usumbufu na
udhalilishwaji usiomstahili yeyote yule! Ulikuja hapa, ukatudharau ndio maana
ukaenda kumtenda mabaya binti yangu!” “Hapana mzee wangu. Nampenda sana Lara,
nilikosa tu.” Mzee Chiwanga akarudi.
“Pengine mimi na umri huu uelewa wangu ni wakijinga sana kama
unavyonifikiria.” “Hapana mzee wangu. Wewe unahekima na ndio maana nimerudi
baba yangu. Ingekuwa ni mzee mwingine hakika nisingerudi, nilikosa tu.”
“Ulikosaje Jackson? Ulikosea nini pengine mimi nimeshindwa kuelewa. Hebu wewe
unieleweshe. Maana umenitia aibu hapa kwenye jamiii! Umefanya mke wangu
adhalilishwe kupita kiasi. Hii nyumba ilikuwa ikijaa wanawake wakija kudai vitu
vyao kwa mke wangu! Matusi yalitufuata kila mahali tukawa kama watu tunaotembea
bila nguo! Tumemaliza madeni uliyotusababishia, hata hatujapumzika, na wewe
unarudi tena! Unataka nini wewe kijana? Umetumwa na shetani wewe!? Umetumwa
kutuharib..” “Chiwanga!” Mkewe akamuita kwa upole.
Akamgeukia. “Humu ndani hakuna shetani bwana! Tulia.” “Basi muulize
wewe anachotaka ni nini tena baada ya yote aliyofanya! Anataka nini hapa? Maana
kama ni msamaha tulishamwambia dada yako, na mwenzio Tino, sisi tumesamehe.
Unarudi kutafuta nini?” “Namtaka Lara, mzee wangu. Nilikosa ndio maana nimerudi
kuomba msamaha kwenu na kwa Lara. Nakiri nilikosa.” Jax bado alikuwa magotini.
Nyumba nzima kimya akisikika mzee akigomba.
“Naomba nieleze ukweli mama yangu. Tafadhali.” Jax akiwa amekunja
mikono akamsihi mama Chiwanga aliyeonekana angalau anahuruma. “Kaa baba,
tuzungumze.” Akamwambia Jax, na yeye akaenda kukaa. “Nashukuru sana. Nianze kwa
...” “Tafadhali mwambie asiombe radhi.” Akaingilia mzee Chiwanga. “Wewe usiombe
radhi. Tueleze kilichotokea Jax. Ulikuja na kuonekana kijana muungwa sana
mwanzoni. Mpaka baba alikusifia sana. Ulionekana na hekima, unajua
unachokitaka! Lakini ikaja kuwa tofauti kabisa mwanangu! Ilikuaje?” Mama
Chiwanga akauliza kwa upendo kama mama.
“Kaa tu. Rudi kukaa tuzungumze.”
Jax akarudi kukaa. “Nilikuwa na msichana tokea nikiwa chuoni. Sisi
hatukujaliwa familia mama yangu. Hatukukua kama hivi Lara alivyojaliwa na kukua
akilelewa na wazazi na familia inayomzunguka. Na naomba nikuhakikishie
siwadharau ila nilipokuja kupaona hapa, ikaniongezea ujasiri wa kuwa na Lara
nikijua na mimi nitapata familia.” Jax akaendelea.
“Yule msichana ndio akawa kila kitu changu kwa muda mrefu sana.
Kuanzia sina chochote, dada Nelly akinitunza mpaka alipokuja kuondoka nchini.
Tukapotezana kwa miaka yote hiyo, akaja kunitafuta wakati ule wa harusi yetu.
Sijui niliingiwa na nini wazazi wangu, nikawa ni kama nimechanganyikiwa kabisa.
Na Lara ni shahidi, mimi si muhuni. Muulizeni Lara. Sina maadili hata ya utani
na watoto wa kike, hajawahi hata kunishuku. Sijawahi kupishana na Lara hata
mara moja jinsi nilivyokuwa nikiishi naye kwa amani.”
“Naomba niwe mkweli wazazi wangu nilifanya kosa ila nikiwa najifariji
kuwa kwa uzuri wa Lara, hatapoteza muda atapata mwanaume mzuri, ataolewa na
kuwa na furaha. Hata nilipokuja kumwambia kuwa naahirisha ndoa, sikujua hata
kama ataona shida. Nilijua ni kama atashukuru Mungu.” “Jackson mwanangu!
Uliwezaje kufikiria hivyo?” “Kipindi cha mwisho Lara alibadilika, mama.
Alibadilika ikawa kama nalazimisha mambo mengi mno mpaka nikamlalamikia Tino,
kumbe mwenzangu ni mjamzito! Mimi sijui, nikajua ni kama swala la ndoa anaona
ni mzigo na hayupo tayari kwa ndoa. Kwa hakika sikujua kama Lara ni mjamzito na
pia kama angejali mimi kumuacha. Kwa kuwa hata nilipokuwa naye mimi, Lara
alikuwa akitongozwa sana tu. Sikuwa na wasiwasi.” “Sasa, sasahivi nani
amekwambia anashida na wewe?” Mzee Chiwanga akauliza.
“Ulipomkataa alikufuata na kukulazimisha ndoa tena?” “Hapana mzee
wangu. Mimi ndio nilimuomba msamaha na kumuomba turudiane.” “Wewe kijana ni
mvurugaji na hujui ni nini unataka. Unataka kuoa wanawake wangapi? Unataka
kumchukua binti yangu, ukamchanganye tu akili! Hapana. Ondoka.” “Sina mwanamke
mwingine tena ila Lara. Mungu wangu ni shahidi baba.” Mpaka akamuita baba.
“Sina nimebakiwa na Lara tu. Yule msichana nimeachana naye mpaka
nimempeleka polisi kuwa asije kunifuata tena.” Kidogo wakashituka. “Ninayo
mashitaka yake hata kwenye gari. Sina msichana mwingine ila Lara. Na safari hii
akinikubali, sitachangisha mtu, namuoa kwa pesa yangu mwenyewe. Niliporudiana
tu na yule msichana wa kwanza ndipo nilipogundua kosa kubwa nililofanya. Najua
mtasema namrudia Lara kwa sababu kule imeshindikana. Ndiyo ni kweli. Namrudia
Lara kwa kuwa tulikuwa na maisha mazuri sana na Lara. Amani, utulivu na
kuheshimiana. Lara alinipenda na kuniheshimu sana. Hata nikisema nikaanze
kwengine, najua sitampata mwanamke kama Lara, ndio maana ninarudi wazazi wangu.
Naombeni mnisamehe. Samahani kwa fedheha kubwa niliyowaingiza. Lakini naomba
mnitizame na mimi kama Lucas tafadhali. Kama mtoto wenu tu.” Jax akapiga tena
magoti. Nyumba nzima kimya, mpaka dada zake Lara walikuwa wakisikiliza huko
jikoni.
“Mimi ni yatima, sina wazazi. Ningekuwa na baba, ningesema aje
azungumze na wewe pengine yeye ungemuelewa zaidi au angeongea lugha
inayoeleweka. Lakini sina mtetezi hapa duniani ndio maana kwa aibu yote hii
bado nimerudi mimi mwenyewe kwenu. Ningekimbia au nisingerudi kabisa, lakini ni
kwa vile ninavyompenda Lara. Naombeni msinitupe wazazi wangu. Nipokeeni. Hakika
nimejifunza kutokana na makosa. Hamtakaa mkasikia lalamiko lolote kutoka kwa
Lara. Hata siku moja. Nimejifunza, nimekoma, na sitarudia tena. Nimebakiwa na
Lara tu, na Mungu wangu ni shahidi.” Mpaka Mzee Chiwanga mwenyewe akapoa.
“Mimi nimeelewa Jax. Ila nina swali. Sasa huko ulikomuacha msichana
mwingine tena, hayatatokea kama haya tena, ukaamua kurudi kwake na kuomba tena
msamaha kama huu?” “Nimemaliza mama. Nimemaliza mama yangu. Naomba niamini mimi
sio muhuni. Na ninajua naweza nikaonekana ni kama mtu ambaye sijui ni kitu gani
ninataka lakini...” “Na huo ndio wasiwasi wangu kijana. Huo ndio wasiwasi wangu
mkubwa sana. Sidhani kama unajua ni kitu gani unataka.” Mzee Chiwanga akarudi
kukaa kabisa.
“Muangalie mke wangu.” Jax akamwangalia. “Huyu nipo naye tuna miaka
35 sasa. Unanisikia?” “Nimesikia mzee.” “Tulikaa miaka 5, hashiki mimba, mpaka
wazee wakaniambia nioe mwanamke mwingine. Achilia mbali, nimekaa mjini hapa,
wanawake wanatongoza wanaume. Wanawake wadogo kabisa, wanatongoza. Zipo sababu
nyingi tu za usaliti na wakati mwingine zinasikika zikiwa na maana kabisa
zikitetea usaliti wa mtu kutokuwa mwaminifu. Lakini mimi nakwambia na Mungu
ananisikia, sio kwamba kwa sababu mwenyewe amekaa hapa, sijawahi.” Mzee
Chiwanga akasogea mbele ya kochi kama kuweka msisitizo kwa Jax.
“Sijui mwanamke mwingine mbali ya mke wangu, tokea siku namuona,
nakumtongoza, mpaka nimekaa naye hapa. Wanawake wote mbali na mke wangu huyu,
ni dada zangu, na mama zangu. Hiyo ndiyo heshima niliyoweka kwa mwanamke
niliyemchagua tokea mwanzo. Kwani huyu anatofauti gani na wanae? Mke wangu
mzuri bwana! Walihangaika kweli hapa Dodoma wakitaka kuoa mke wangu, lakini
sikuwa na wasiwasi, nilijua hawawezi kumtoa kwangu.” Mama Chiwanga akacheka
kidogo.
“Wanamtongoza huyu mpaka leo. Muulize. Lakini najua kwa hakika,
hakuna mwanamme atamtoa kwangu huyu. Wanamuahidi magari na nyumba nzuri, lakini
ametulia kwangu tokea tunatembea na miguu hata baiskeli hatuna. Ametulia, hana
papara mke wangu. Tuna nyumba yenye amani, waulize binti zangu. Mpaka
wanatuonea wivu! Ni kwakuwa nilijua nini nataka, Mungu akanijalia, nikapokea
kwa heshima, nakutulia. Najua watakuwepo huko nje wanawake wengine wenye vigezo
vingine, lakini hainihusu mimi. Sijisumbui, kwa kuwa ninaye mwenye vigezo
vyangu hapa. Hata mwanamke atembee uchi, hainihusu kwakuwa ninaye wangu mimi.”
Mama Chiwanga akajisikia vizuri.
“Lile duka pale ndio utajiri wa kwanza tunakuwa nao hapa ndani. Ndio
kitu kikubwa na cha thamani ameshika mke wangu, lakini ukarimu wake siku ya
kwanza unakuja hapa na leo ni tofauti?” “Upo vile vile mzee wangu.” “Basi
ndivyo walivyo binti zangu wote. Nina ujasiri wakusema hivyo kwakuwa nalea
wanangu mimi mwenyewe nikisaidiana na mke wangu. Nawajua binti zangu. Huwa
namwambia na kumshukuru mke wangu kila siku, kuniletea mabinti wazuri kama
yeye. Tabia zao na mioyo yao pia wapo kama mama yao. Hao binti zangu mimi
najisifia kokote kule. Sina daktari humu ndani, wala mwanasheria, lakini
napenda sana binti zangu. Tunakaa uswahilini hapa watu wakiishi kwa kusutana, lakini
hutasikia wakifuatwa kwa ugomvi hata mara moja. Tokea wanakua mpaka leo wapo
hivyohivyo. Mama yao huyu ndiye wakwanza kuja kufuatwa na maneno sababu yako
Jackson! Hii nyumba ilikuwa haina kelele. Hata mimi kelele huwa zinaniisha kwa
utulivu wao hawa. Wanangu na mke wangu hawana maneno kabisa. Hawajui kumkera
mtu. Ndio maana uliniudhi sana ulipomtenda vibaya Lara! Hakustahili hata
kidogo.” Mzee Chiwanga akaongea kwa uchungu sana.
“Huyo Lea alileta kijana hapa. Msomi tu. Nilipomuona na kumwangalia
kwa kukaa naye hapahapa, nilimwambia wazi kabisa. Huwezi kumuoa binti yangu,
utamsumbua sana. Muulize mama yake. Wote walishituka, lakini nilimwambia wazi
kabisa. Pesa yake itamzika mwanangu, nikamwambia ni heri nibaki naye hapa,
kuliko ahadi alizokuwa akitupa hapa. Na kweli, alipoondoka tu, Lea mwenyewe
akanifuata nakunishukuru. Akasema nilimsoma sahihi yule kijana. Hata yeye
alikuwa akisita moyoni. Nikijana aliyekuwa amefanikiwa sana, ila amejawa kiburi
na majivuno. Sasa kuja kurudishiwa Lara anatokwa damu kama mbuzi aliyechinjwa
machinjioni, tena anarudishwa na Tino! Wewe haupo! Nililia mimi, muulize mama
yake. Nikajilaumu niliwezaje kuruhusu binti yangu kuangukia kwa kijana katili
kama wewe, halafu nikashindwa kukusoma wakati ulikaa hapohapo na mimi
nikikutizama!”
“Nililia nikimuuguza Lara kwa uchungu sana. Nikijutia kukukaribisha
hapa na kujuta kwa nini nilishindwa kumlinda binti yangu! Leo unarudi tena,
ukimtaka binti yangu, si unataka nije niletewe yupo kwenye jeneza! Nimeweka
agano na Mungu, binti zangu ndio watanizika. Nimemwambia atanipa binti niwalee
na kuwafikisha anakotaka niwafikishe, lakini nimekataa kazi yakuzika binti
zangu. Sitazika mtoto wangu hata mmoja. Lakini wewe...” “Hapana Chiwanga.
Naomba usimalizie tafadhali. Basi baba.” Akanyamaza na kuondoka kabisa pale.
Mkewe akamsindikiza kwa macho ya majonzi.
Alipopotelea chumbani akarudisha macho kwa Jax. “Labda uache baba.
Acha mwanangu. Hapa naona imeshindikana. Umemuumiza sana Chiwanga. Hata Lara
akikupokea, mtakuwa na mahusiano gani na baba yake?” “Hata hivyo bila baba,
Lara hawezi kukupokea shem. Lara ni mziwanda wa baba.” Lea akasogea hapo
sebuleni na kuongeza baada ya baba yake kuondoka.
“Mimi naungana na mama, hapa hapatakufaa tena. Heri ukajaribu kuoa tu
kwengine. Hata Lara mwenyewe nimezungumza naye, bado anauchungu kama haya mambo
yametokea jana. Bado analilia mtoto ambaye hata hakuwa akijua jinsia! Lara
hayupo tayari Jax. Kama mmeandikiwa, haitakuwa sasa.” “Daah!” Jax akainama kwa
majonzi.
“Naombeni mnisamehe sana. Nisameheni jamani, nimekosa.” Kimya. Wote
hawakujibu mpaka Lea mwenyewe aliyeingilia mazungumzo akashindwa kupokea huo
msamaha. Akamgeukia mama yao. “Nifanyaje mama?” Jax akaomba ushauri akiwa
amepiga magoti. “Mimi naona uache tu Jackson. Muda uje ujibu. Ila usiache kuwa
karibu na Mungu. Huko nje shetani atakutesa mwanangu. Shetani anapenda vijana
kama nyinyi mlio na maendelea hivyo, anapenda kweli. Anafanya akili zenu zinakuwa
kwenye mambo yanayowayumbisha, akitumia nafasi zenu za maisha. Pesa zenu, ujana
huo na maendeleo inakuwa ni kivutio chake, inakuwa ngumu kutulia na Mungu.
Lakini baba, Mungu yupo. Wakati mwingine anaonekana anachelewa, lakini yupo.”
Mama Chiwanga akaongea kwa unyenyekevu.
“Pata muda na Mungu, halafu vuta subira. Unaonekana wewe ni kijana
mzuri sana. Unamaendeleo mazuri. Gari hiyo nzuri na watu wanaokuzunguka
wanamaendeleo mazuri tu. Ninauhakika utapata mke mzuri tu huko. Au hata huyo
uliyemrudia tena baada ya kumuacha Lara, rudi baba. Rudi hukohuko. Pambana na
huyo mwenzio mliyeanzana naye tokea zamani kama ulivyosema. Muombee ili na yeye
aje kuwa mke mzuri. Huwezi pata mtu mkamilifu Jackson. Hata mimi ninamapungufu
yangu, japo Chiwanga amenipamba hapa. Lakini kuna anayoyavumilia. Utahangaika
hivi ukienda na kurudi kwenye njia mbili mpaka lini?” Mama yule akaongea kwa
upole tu.
“Kile kilichokutoa kwa Lara, na kukurudisha kwa mchumba wako wa
zamani, kishikilie baba. Shikilia. Kama kunamapungufu huko kwa mwenzio, muombee
huku na wewe ukijifunza kuishi naye. Hutapata mwanamke mkamilifu baba.”
“Nimeshampata, ni Lara.” Jax akamkatisha kwa ujasiri, wote wakamwangalia.
“Najua mnaweza msinielewe kwa kile nilichofanya, ila kile nimekipata kwa Lara,
sijakipata kwa mtu mwingine yeyote yule na ninajua sitakipata kwa mtu mwingine
ila Lara, na ndio maana nimerudi. Nimefanya kosa kubwa sana. Najua, ila
nimerudi mama yangu. Nimerudi kwa Lara. Hapo ndipo nitarekebisha sio
kwingineko.” Jax akasimama.
Akakaa pembezoni mwa kochi kama anayetaka kuondoka. “Nashukuru hata
kufunguliwa mlango mama yangu. Najua sikustahili. Hii ni barua ya Lara na hii
ni bahasha yake. Naomba mumpe tafadhali.” Jax akasimama na kumkabidhi mama
yake. “Sawa. Nitamkabidhi.” “Nashukuru mama. Acha mimi niwahi safari ya kurudi
Dar.” “Uwe na safari njema. Mungu akusaidie ufike salama. Nisalimie dada yako.
Ni muungwana sana.” Jax akatamani kujua walichozungumza na dada yake mkorofi
yule mpaka kuitwa muungwana! “Nitamsalimia mama.” Jax akatoka kimya kimya.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Mmmmhhh!” Akasikika mama Chiwanga akivuta pumzi kwa nguvu. Na Lily
akatoka jikoni na chakula. Akaanza kupanga kimya kimya. “Lara yuko wapi?”
“Chumbani.” Lily akajibu akiendelea kupanga chakula. Kweli binti hao ni
watulivu haswa. Akamfuata Lara chumbani. Akamkuta ametulia kitandani. “Ameacha
hizi bahasha mbili.” “Akuu! Mimi sizitaki.” “Lara! Umeingiwa na nini?” “Wewe
usipokee mama. Mimi sitaki. Jax aliniacha mimi.”
Lara akaanza kulia. “Sasa hivi anataka nini?
Anataka kunichanganya tu. Usimpokee vitu vyake, mama. Mimi sitaki tena.
Nilitulia kwake, akamchagua mwanamke mwingine! Vimeshindikana huko ndio
anarudi! Hapana mama. Mimi sitaki.” “Basi tulia usitoneshe huo mkono.”
Mama yake akamtuliza akijua bado anahasira. Akatulia na kuondoka na zile bahasha
mbili akijua moja ina pesa.
Kwa Nelly.
W |
akati
Jax yake yakimuendea kombo, yeye Nelly na Billy yao yakawa kwenye mstari.
Wakawa wote wanasababu ya kukutana kila siku jioni baada ya kazi kufanya
mazoezi kama maandalizi ya kupanda mlima Kilimanjaro. Walipewa aina ya mazoezi
yakufanya na kocha wao akiwasimamia. Wakitoka hapo wanakwenda kupata chakula
cha pamoja. Ukweli ilimbadilisha Nelly. Ikamuongezea kitu kingine chakufanya
mbali na kazi. Akapata mtu mwingine wa kumfikiria mbali na Jax. Huyo Billy.
‘What is greater than God, more evil than the devil, the
poor have it, the rich need it, and if you eat it, you'll die?’ Huo ujumbe ukaingia kwenye simu ya
Nelly mida ya mchana kutoka kwa Billy. Kisha mwingine ukafuata. ‘Na usiigilizie,
Nelly.’ Nelly akacheka baada ya huo ujumbe wa pili kuingia baada ya hicho
kitendawili. Nelly alifikiria mpaka akashindwa kufanya kazi, bila kupata jibu.
Akaandika kabisa kwa kiswahili. ‘Ni nini kikubwa
kumzidi Mungu, kiovu kumzidi shetani mwenyewe, masikini hawana, matajiri hawahitaji,
na kama usipokula hicho kitu, utakufa!’ Akili ya Nelly iliendelea
kuzunguka mpaka jioni anakutana na Billy.
“Umeharibu siku yangu yote leo!” Nelly akalalamika na kumfanya Billy kucheka
sana. “Hamna jibu?” “Mimi mpaka nakuhisi vibaya bwana, Billy! Kitendawili gani hicho?”
Billy akazidi kucheka. “Rahisi sana. Wewe kubali kushindwa nikusaidie.” “Nipe hint
hata moja.” “Huko ndiko kuigilizia. Kubali kushindwa.” “Ona unavyofurahia
kushindwa kwangu leo! Mpaka nguvu ya kukimbia leo imeongezeka!” Billy akazidi
kucheka akikimbia kwenye mashine.
0 Comments:
Post a Comment