Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Chozi Langu! - SEHEMU YA 15. - Naomi Simulizi

Chozi Langu! - SEHEMU YA 15.

 Ikabidi Nelly akubali kushindwa tu. Kwa kuwa kweli alikosa jibu. “Ni nini jibu lake?” “Nothing.” Ilibidi mpaka Nelly asimame. “No way! Haiwezekani Billy!” Billy akazidi kucheka. “Wewe fikiria tu. Nothing is greater than God, Nothing is more evil than the devil, poor have Nothing, the rich need Nothing, and if you eat Nothing, you'll die.” “Mimi nalia.” Billy alicheka mpaka akasimama na yeye. “Hakika nalia. Hangaika yote ile, siku nzima mpaka nikashindwa kazi kumbe jibu ni rahisi hivyo!” “Tatizo unapenda kufikiria vitu vigumu sana. Wakati mwingine tunapishana na majibu yetu mlangoni wakati tunakwenda kuyatafuta nje.”

“Hakika nimeshindwa. Na hata ungenipa muda kiasi gani, sikuwa hata karibu na hilo jibu lako. Sawa bwana.” Wakaendelea kuzungumza huku wakifanya mazoezi mpaka walipomaliza. Walikuwa wamebakisha siku chache tu wote wachukue likizo fupi, kuelekea Kilimanjaro. Ukweli hata Nelly alikuwa akiitizamia hiyo safari kwa hamu sana. Kwani hakuwa amechukua likizo kwa muda mrefu! Halafu safari yenyewe anakwenda na Billy ambaye hajui kumpunja! Akawa anahesabu masaa, muda ufike.

 Atafutae Hachoki.

B

aada ya siku 10 wakashangaa Jax amerudi tena. Tena safari hii alifika nyumbani siku ya jumamosi usiku wa saa tatu inaenda saa nne. Waliposikia hodi Lucas mpenda kufungua milango aliposikia mlango unagongwa tu, akakimbilia mlangoni. “Nani?” Akauliza Lucas kabla yakufungua. “Mimi Jackson.” Wote wakashangaa na kuangalina. Lara akanyanyuka kwa haraka na kukimbilia chumbani kwa kunyata. Baba yake kimya. Lucas akauliza kwa sauti ya juu ya konong’ona. “Nimfungulie au nimwambie hatupo?” “Fungua bwana Lu, anakusikia!” Bibi yake akamuamuru kwa sauti ya chini akijua Jax anasikia nje.  Lucas akafungua. “Lara hayupo.” “Jamani Lu! Ni nini baba!?  Mgeni hata hajaingia ndani?! Mpishe bwana.” Lucas akampisha.

Jax akaingia akijua wazi hatakiwi. “Samahanini wazazi wangu, nimekuja usiku usiku. Nilikosa usafiri wa mapema. Ndio nimeingia mida hiihii na kuamua kuja angalau niwaone.” “Karibu. Karibu sana.” Lily na Lea wakasimama na kuondoka pale kumpisha mgeni. Walikuwa wamekaa wakiangalia taarifa ya habari, ilipoisha zikaanza stori hapo wakiongea huku wakila hapohapo sebuleni. “Kuna chakula baba. Sijui umeshakula?” Akaongea mama Chiwanga akisimama. “Nitashukuru mama.” Jax hakujivunga. Mzee Chiwanga kimya baada yakuitika salamu tu, akanyamaza.

“Pole na majukumu baba yangu.” Jax akaanza taratibu. “Tunashukuru Mungu. Pole na safari na wewe.” “Asante.” Kidogo Jax akatulia kuona angalau mazungumzo yake yamepokelewa. Akaletewa chakula. Wali, maharage na mboga za majani. Akapokea kwa shukurani kweli. “Hapakua na nyama yeyote baba, naona mpishi wetu ametupikia hivyohivyo! Na sisi ndio tunarudi, tumechoka, nimeshindwa hata kupika zaidi. Nimeona tule hivyohivyo.” “Usijali mama yangu. Hiki ni bora kabisa. Nashukuru sana.” Mara ya mwisho anaondoka hapo hata maji hakukaribishwa. Jax akala bila hata kumuulizia Lara.

Kimya kikaendelea Jax akiendelea kula. Ni tv tu ndiyo ilisikika hapo, wote kimya. “Lara anaendeleaje na mkono?” Akaanza Jax. “Namsikia ameanza kumlalamikia baba yake hapa. Naona umeanza kuwashwa. Anataka kutoa, lakini baba yake anamsihi avute siku kidogo.” “Bado. Walimwambia angalau majuma 6 ndipo watoe na kupiga tena x-ray wajue kama umeunga.” Jax akajieleza. “Nimemletea na dawa zake za maumivu.” “Usingesumbuka Jackson mwanangu. Hata simsikii akilalamika maumivu. Hanywi dawa, na si unamjua alivyo na dawa?” Jax akacheka kidogo. “Lara muoga kwelikweli wa dawa. Hatazinywa.” “Basi nitaziacha tu.” Wakatulia akiendelea kula mpaka akamaliza, akataka kuondoa chombo alicholia. “Usihangaike, huyohuyo Lu aliyekufungulia mlango atatoa vyombo.

Lucas akasikia. Akawa anasogea huku akicheka. “Muone! Wewe mgeni anakuja, humfungulii mlango bwana!” Bibi yake akamwambia. “Nilitaka kujua kwanza!” Jax akacheka kidogo. “Haya toa vyombo na hiyo stuli.” “Nikuletee na maji?” Lucas akamuuliza Jax. “Nitashukuru.” Jax akakubali kila kitu. “Vipi biashara lakini?” “Tunaendelea vizuri, tunamshukuru Mungu.” “Naona mna eneo zuri kweli! Pako barabarani.” “Pazuri ila ni garama kweli. Hivi huu mkataba ukiisha, Chiwanga anataka tuhame pale. Pesa yote inaishia kwenye pango bwana!” “Oooh! Hiyo ni kweli.” Jax hakutaka kuongeza asije akaharibu.

Akaletewa maji. Akayanywa yote. “Najua usiku umeenda na nyinyi mmechoka na kazi. Niliona nipite kuwasalimia tu kabla hamjalala. Nashukuru kwa chakula wazazi wangu.” “Hivyohivyo chakulamba lamba.” “Inatosha.” Jax akatulia akisugua mikono akionekana amejawa wasiwasi. Kimya. Hakuna hata aliyemuongelesha tena. “Naweza kuzungumza na Lara?” Akamuona mama Chiwanga anamuangalia mumewe ambaye alikuwa kimya muda wote, macho kwenye luninga. Kimya. “Hata hivyo Lara mwenyewe alikuwa chumbani. Sijui atakuwa amelala!” Akaona ajibu mama Chiwanga na kuongeza. “Lea mama mazazi, niangalizie Lara. Mwambie Jax yupo.” Akaongea mama yao taratibu kama kawaida yake.

Baada ya muda Lea akarudisha jibu. “Lara amelala, mama.” Wote wakijua ni uongo, Jax akawa mstaarabu. “Basi nitarudi tena kesho kumwangalia mida ileile mkishatoka kanisani, kabla sijaondoka.” “Sawa baba. Karibu, na uwe na usiku mwema.” Jax akasimama na kuaga kwa heshima, akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kesho yake tena walipotoka kanisani walikaa kama dakika 20 tu, Jax akarudi tena. Safari hii alikuja na taksii yenye vyakula. Alionekana ametoka kununua vyakula. “Usingehangaika baba.” “Sio usumbufu hata kidogo. Vyote nimepata sehemu moja, pamoja na huu usafiri.” Wakasaidiana na dada zake Lara, wakaingiza vyakula vyote walivyoleta, ndani. “Asante.” Wakashukuru hao kina shemeji. “Karibu.” Jax akarudi sebuleni ambako alijua ndipo anatakiwa akae hapo, hakumkuta mzee Chiwanga. Ikawa hivyohivyo. Lara alishakimbia kabisa hapo nyumbani kwao. Jax anagonga mlango wa mbele, yeye akatokea mlango wa nyuma kwa haraka. Jax akala chakula. Akasubiri bila kuchoka akijua pengine Lara atarudi, lakini wapi.

“Inabidi niondoke tu. Lasivyo nitaachwa na ndege.” Jax aliongea macho kwenye saa yake ya mkononi akiwa amebakiwa na mama Chiwanga tu hapo sebuleni. Hata binti zake waliingia chumbani baada ya kula. Mzee Chiwanga ndio hata hakutoka hata kwa chakula. “Basi uwe na safari njema.” Ndilo aliloweza kuzungumza mama Chiwanga. “Naomba nikuachie bahasha ya Lara.” “Naomba niwe mkweli Jax. Hizo bahasha Lara hapokei. Hata zile za mwanzoni ninazo, hakupokea. Nashauri uache tu mwanangu. Unapoteza hizo pesa za nauli za kuja huku bure, wakati hiyo pesa yako ungefanyia kitu cha maana. Lara hayupo tayari kwa mazungumzo.” Mama Chiwanga akamuhurumia.

Jax akafikiria kidogo akiwa ameinama. “Mimi namuelewa kabisa Lara. Najua ni ngumu kwa vile tulivyokuwa tukiishi mpaka kumbadilikia!” Jax akawa kama anawaza. “Najua nimemuumiza sana Lara. Natamani hata na mimi nisiwe narudi mama yangu niwaache mpumzike, lakini nashindwa. Kila siku ikipita, ndivyo ninavyoona jinsi nilivyopoteza kitu cha thamani mashaini. Najuta mama, najuta sana.” Mama Chiwanga kimya. “Natamani anipe nafasi nyingine. Hata asifanye chochote kile. Mimi nitahangaika na kila kitu.” Jax akaendelea taratibu. Kimya, mama Chiwanga akishindwa chakusema tena.

“Basi naomba nikuombe kitu kingine mama yangu.” “Karibu.” “Nitunzie tu hizi barua. Naomba zitunze tu, ila umwambie nimeacha na leo. Ajue tu, halafu uzitunze.” “Sawa Jackson mwanangu.” Safari hii ilikuwa bahasha moja tu. Akapokea. Jax akashukuru na kuondoka.

Ya Nelly.

Mara ya Tatu.

W

aliondoka jijini Dar kuelekea Kilimanjaro wote wakiwa na furaha na wakitizamia kuupanda huo mlima siku inayofuata. Walitaka kubakiza siku nyingi baada ya kupanda ili kupata muda wakutosha kupumzika kabla ya kurudi kazini. Sasa kampuni waliyoitumia ya utalii kupanda huko mlimani walipojua ni mwanamke na mwanaume na wanapanda pamoja, swala la vyumba viwili wakalipuuza na kuwatafutia chumba kimoja.

Billy na Nelly wanatua uwanja wa ndege na kupelekwa hotelini, wakajikuta na chumba kimoja. Billy akapaniki, Nelly akimwangalia. “Hakika nili book vyumba viwili. Nafikiri tumekuja msimu ambao watalii ni wengi, wameishiwa vyumba. Acha niulize kama tunaweza pata kingine.” Nelly kimya. Billy akahangaika mpaka akachoka. Ikabakia chaguzi ya kuhama hoteli. Ambako huko angepata chumba kimoja. Kwamba iwe yeye au Nelly ndio akahamie huko.

“Tafadhali usinifikirie vibaya.” “Wewe mwenyewe uliniambia kuna mambo unaweza kuyabadili, ukiwa na maana kuwa, una control nayo na mengine hata ukiwa na pesa, yapo nje ya uwezo wako. Naomba tulia Billy. Mimi nakuamini.” “Sitaki uone kama nataka ku take advantaje ya hii hali.” “Hapana. Naomba tulia. Usiharibu safari tuliyojiandaa kwa muda mrefu, ikaonekena kama mbaya wakati ni malazi ya usiku mmoja tu! Mimi hata kwenye kochi nitalala, ilimradi kesho tuamke na furaha tukiwa na nguvu ya kwenda mlimani.” Hilo likamtuliza Billy ambaye ni bwana mipango. Na hata ajira yake ni mipango. Kwa hiyo alitaka kila kitu, wakati wote kiwe kwenye utaratibu fulani, akakutana na Nelly, maisha yake mwenyewe hayakuwa kwenye mipango. Amefika hapo kwa kupambana.

Wakapewa kadi ya chumba, wakaelekea chumbani. Kilichomshangaza Billy ni vile Nelly jeuri alivyo. Hakutegemea. “Unataka nikusaidie nini, chakutoa kwenye mizigo yako na kupanga hapa nje kwa muda huu mpaka tunapoondoka kesho?” Billy akajidai akifikiria kumbe anashangaa kule kujaliwa. Hakuishi na mwanamke kwa muda mrefu, kwa hiyo vitu  vingi alikuwa akijifanyia mwenyewe. “Sabuni za kuogea, lotion, mafuta ya nywele, nguo za jioni hii, nguo za kulali, na vitu kama hivyo. Ili usisumbuke kuanza kuvitoa kimoja kimoja.” Nelly akampa wazo akiwa ameshaweka mizigo yake pembeni.

“Nashukuru, Nelly. Ila naona nipo sawa. Nisikusumbue. Najua na wewe utataka kupangilia vya kwako.” “Basi mwenzio jinsi ninavyoweka vitu vyangu, nilimfundisha mpaka Jax. Anasema akisafiri hapati shida kabisa. Naweka mizigo yangu kwa siku, na matumizi. Hapa nikiangalia kila mkoba wangu najua ni wasiku gani na wakati gani. Kuna ambayo sitafungua hapa mpaka mlimani na kuna ambayo sitagusa mpaka siku narudi.” “Haiwezekani Nelly!” “Kabisa. Mimi sipendi mtindo eti unatafuta mswaki kwenye kila mzigo! Au eti nguo ya kulalia unaisaka mpaka unamwaga mizigo yote! Hapana. Huwa naweka vitu vyangu kwa mpangilio na sipati shida. Na nyumbani hivyohivyo. Kila mahali. Siwezi nikawa jikoni eti natafuta kisu mpaka hamu yakupika iishe! Unafungua kila kabadi na droo! Hapana. Na kila mfanyakazi anayefanya kazi kwangu sharti la kwanza ni asichanganye vitu. Ni bora aniachie hapo, nije nipange mwenyewe kuliko nianze kukuta vijiko kwenye visu au mashati kwenye sketi au suruali! Hapana. Kwa hiyo mimi sina shida na wala sihitaji nafasi yote hii. Sehemu kidogo tu inanitosha.” “Umenifanya nijutie chumba changu.” Nelly alicheka sana.

“Kweli. Mimi nikianza kutafuta soksi hapa, mpaka jasho linanitoka. Naweza kukuta ipo moja, ingine niliacha nyumbani, naanza kununua tena.” Nelly akazidi kucheka. “Kama hapa umenikumbusha nguo za kulalia, sidhani kama nilibeba.” “Jamani Billy!” “Maadamu tunalala wote, bora nijisalimishe tu. Na huo ndio ugonjwa wangu. Sasa nikiwa peke yangu sina shida, nalala tu na boxer.” “Nipe mizigo yako nikupangie vizuri na kinachopungua, tukanunue.” “Hapo utanisaidia.” Nelly akatoa vitu vyake vyote na kuweka kitandani. Akaanza kwa kuweka vinavyotakiwa kuwa pamoja na kutafuta wenza. Na kweli vingine vilikuwa kimojakimoja, kama soksi. Akamuwekea huku akiandika vitu anavyohitaji kununua kabla ya kesho yake ndipo wakatoka kwa manunuzi.

Walishanunuliwa vitu vya kuvaa huko mlimani. Kama kawaida ya Billy, alishalipia kila kitu. Alichofanya Nelly ni kuongeza tu. Walizunguka na taksii, wakaishia kurudi na chakula chumbani. “Katangulie kuoga wakati naandaa chakula, ukitoka ule.” “Nataka tule pamoja Nelly. Nipo na wewe hapa, unataka niendeleze maisha ya upweke tena!?” “Basi utanisubiri.” Akaenda bafani na kutoka na taulo.

“Eti natamani ingekuwa tofauti nikwambie twende tukaoge wote, tukitoka tunatoka pamoja na kula pamoja.” Nelly alibaki ameduaa kama asiyejua aseme nini. “Basi acha tu nitangulie. Samahani, sijui naongea nini!” Akarudi bafuni na kumuacha Nelly amesimama na mshangao.

Alitoka kuoga na Nelly akaingia bila ya kusemeshana. Ni kama ikapita hali fulani hivi, ya tofauti. Hata wakati wa kula kukawa na hali ya ukimya. “Samahani Nelly. Sikukusudia kukunyima raha.” “Hata kidogo. Sema sikuwa nimetegemea.” “Ni kitu cha ajabu eeh!?” “Sidhani, ila kwangu ni kigeni kwa sababu sijawahi.” Nelly akafikiria kidogo. “Najua kuna mambo fulani unaweza kufikiria naweza nikawa na uelewa nayo au ukashangaa ni kama sifanyi, ni kama nilivyokwambia Billy. Mimi sipo kama wanawake wengine. Ndio maana nilikushauri utafute mwanamke ambaye anaweza kukufaa. Mimi najijua. Sipo sawa.” “Nahisi nimeshachelewa. Nimekuzoea Nelly.” “Hata mimi nimeanza kukuzoea. Ila natamani upate kitu kizuri. Mimi sina huo uwezo. Na sitaki upoteze muda kwangu.” Billy akanyamaza.

Wakamalizia kula. Wote wakaenda kusafisha kinywa kwa ajili ya kuwahi kulala kwa safari ya kesho. “Ungependa tulalaje?” Ni swali lililomfanya Nelly aanze kufikiria hapo sehemu ya bafuni. Akajisafisha mdomo vizuri na kuweka mswaki pembeni. “Lakini mimi naweza hata kulala kwenye kochi Billy. Haina shida.” “Ni sawa tukilala wote kitandani? Sitaki ulale kwenye kochi na mimi siwezi kulala kwenye kochi wala chini. Unafikiri kutakuwa na shida?” “Hata kidogo. Nitafurahi.” Wakacheka na kurudi chumbani.

Walizima kila kitu na wote wakaingia kitandani. “Eti nimefurahi!” “Nini sasa?” Nelly akamuuliza akicheka. “Tunalala wote.” “Ujue Billy wewe una mambo ya ajabu!” “Mimi napendwa kupenda Nelly. Wala sitakudanganya na ndio maana sitaki kuwa mnafiki wakujidai eti nitakufa peke yangu! Hapana. Kwa nini iwe hivyo!?” “Natamani huo moyo!” “Hakika wawili ni bora kuliko peke yako. Wewe hufurahii huu wakati tunokuwa nao?” “Nikwambie ukweli Billy?” “Nakusikiliza.” “Sikujua kama utanibadili kwa kiasi hichi! Sikumbuki kucheka kwa kiasi hiki maishani. Umenifanya akili zangu kuwa busy, sijifikirii sana kama zamani. Na najiona hata uchungu unapungua.” “Hata mimi mwenyewe nakufurahia Nelly. Sana. Hapa nilikuwa nikifikiria tunafanyaje baada ya kumalizia hizo mara nne! Nimepata sababu ya kutizamia weekend zangu, nikijua nitakuwa na Nelly.” Wakanyamaza.

“Njoo huku karibu ulale nikiwa nimekukumbatia.” Nelly akajisogeza ila akampa mgongo. Akamsikia pumzi zake shingoni. “Unanukia vizuri!” “Asante. Hata wewe huwa unanukia vizuri Billy. Mpaka baada ya mazoezi huwa unanukia vizuri!” “Mimi nina very sensitive sense of smell. Yaani kuna weza kukawa na harufu mahali, wote msiipate, mimi nikawa wakwanza kuipata. Kwa hiyo najitahidi sana kwenye swala la harufu. Na pia sio mzembe, nawekeza kwenye harufu nzuri.” “Ndio maana mpaka nguo zako zinanukia!” “Nguo zangu hazifuliwi na kila sabuni Nelly, na huwa najua. Nikishasikia inaharufu ya tofauti, sivai. Na ndio maana huwa sivai vitu vipya mpaka vifuliwe kwanza. Si umeona nimenunua na kutafuta na sabuni pia?” “Na kuweka msisitizo huyo mtu atakayefua hapa hotelini ni lazima atumie hiyo sabuni pamoja na fabric softerner yake!” Billy akacheka.

“Kumbe pale mapokezi ulikuwa ukinisikiliza?” “Sana tu.” Wakacheka. “Ndivyo nilivyo. Utanizoea tu, usinikimbie sababu ya hilo. Nateswa sana na harufu.” “Sio sifa mbaya. Uchafu ndio kitu kibaya.” “Ila na wewe huwa unanukia vizuri Nelly. Sijakusikia ukitoa harufu mbaya.” Nelly akacheka. “Kwa hiyo ungenisikia ungeniambia?” Billy akacheka sana, ila hakujibu hilo.

Kwa mara ya kwanza Nelly akalala mikononi mwa mwanaume akiwa amekumbatiwa vizuri. Hata hakugeuka ili asimsumbue Billy. Akajituliza akimsikia alivyolala vizuri nyuma ya mgongo wake na kuhema taratibu. Ile hali ilimfurahisha sana Nelly. Asubuhi waliamka, Billy akalala chali na kumtaka amkumbatie kifuati. “Billy!” “Njoo acha kujishauri. Huwezi pata bahati kama hii.” Nelly alicheka sana. “Billy wewe!” “Usifikiri nipo na wewe hapa kucheza, Nelly. Nikikwambia nakufurahia, naomba uelewe. Ukija kumzoea huyo binti yangu mkubwa, atakwambia. Mimi si mtu wa kila aina ya mwanamke. Hakika nakufurahia Nelly. Tukiachana huwa nafikiria ni wakati gani tutakutana tena.”

“Sasa unafurahia huu ukorofi wangu!?” “Wewe si mkorofi. Ila uliumizwa, ukashindwa kuachilia. Ndicho kilichokuwa kikikutesa. Nipo na wewe hapa nikiwa sina hofu ya Billson kama Director of Strategy wa World bank ila Billson kama mimi mwenyewe. Kwa kuwa huyo Director of Strategy wa World Bank ulishamfukuza tokea mwanzo.” Nelly alicheka mpaka akajifunika.

“Nelly! Hakika sijakupatia mwenzio.” Nelly akazidi kucheka ndani ya mashuka. “Hivi sasa ulishasamehe?” “Ndicho kilichonitia hamu ya kukufahamu zaidi. Pengine ungekubali siku ile usingekuwa hapa na mimi leo, japo nakiri ulivutia sana macho yangu. Ulivaa nadhifu mno. Umbile lako likaonekana vizuri sana. Sasa alipoongeza Jax kwenye neno la shukurani, nikajiambia lazima nikufahamu zaidi.” “Mimi huwa najua wanaume ni waharibifu tu, bwana!” “Sio wote.” “Sijui. Ila wengi niliokutana nao mimi ni waharibifu ndio maana hata Jax aliniudhi sana. Japokuwa nilimlea mwenyewe, lakini eti na yeye akaungana na wengine kunithibitishia ukweli niliokuwa nao! Hakika iliniuma sana.”

“Sasa yeye ulimpa adhabu gani?” “Naona aliamua kujisalimisha mwenyewe na kuniambia kwa vitendo kuwa si wanaume wote wapo hivyo. Amekosa na hatarudia kosa. Mpaka namuhurumia! Amerudi kuishi pale makusudi na anatunza muda kama mtoto anayebalee!” Billy akacheka sana. “Yupo nyumbani kwa wakati, na anajali huyo! Sijawahi ona. Najua hapa atakuwa amenitumia ujumbe kutaka kujua kama nililala na kuamka salama. Halafu nahisi, sina uhakika, nahisi anahangaika kumrudia Lara, ila naona hajafanikiwa.” “Lara mchumba aliyemuacha?” “Mpuuzi sana Jax. Lakini nahisi Lara amemkataa. Ameniambia rafiki yake, Tino. Inamuuma sana Jax. Ila nimemuacha katika hili arekebishe mwenyewe. Pengine yeye atajifunza mapema kuthamini vitu vya thamani asiwe kama baba.” Akamuona mpaka amebadilika.

“Mimi naenda kuoga.” “Acha bwana Nelly! Usiumizwe na maisha ya nyuma kiasi chakushindwa kuishi leo.” “Mimi nipo hapa na wewe Billy. Sijashindwa ku..” Ukanyamaza. “Unashindwa kuchukua hatua Nelly. Una kusitasita kwingi sana. Jax si baba yako na mimi si baba yako. Kuna makosa yanatokea, lakini hayamfanyi mtu kuwa hivyo. Mimi nina makosa yangu pengine nilichangia kuvunjika kwenye ndoa yangu. Lakini..” “Makosa gani?” Nelly akauliza kwa haraka.

“Katika malalamishi yake makubwa niliyomsikia wakili wangu akisema ni kutanguliza kazi kuliko familia.” “Kivipi?” “Alisema ninafanya sana kazi kuliko kuwepo kwenye maisha yao. Kwamba hata nikiwepo nyumbani nakuwa kazini.” “Ni kweli?” “Ndiyo. Lakini unakumbuka nilikwambia ni kwa wakati ule nikitaka kujitengenezea jina?” “Sasa na yeye..” “Nilimwambia Nelly. Tena kwa kurudiarudia. Mbaya zaidi garama zetu za maisha zilikuwa juu sana, ilibidi kufanya kazi kwa bidii ili kuwafanya waishi vizuri. Na nilitaka kulipia ile nyumba mapema nikiwa na nguvu, ndipo nikusanye sasa pesa za kustaafia. Tuje tupumzike uzeeni! Kumbe mwenzangu yeye alikuwa akipumzika na Carlos!” “Kwani Carlos hakuwa na majukumu mengi?” Billy akafikiria.

“Sijui nikwambie nini juu yake. Carlos ni wale watu wasiopenda makuu tokea tupo wadogo. Alizaliwa na wazazi wenye uwezo, kama mimi, akaridhika na utajiri wa kwao. Hata hakwenda chuo kikuu ila chuo cha miaka miwili tu. Ni mtu ambaye anapenda maisha ya kawaida. Hana ndoto kubwa sana. Ale vizuri, alale pazuri, basi. Sasa wanawake wazuri, wanao jielewa hawapendi wanaume kama vile yeye asiye na mikakati, ndio akaishia kwa familia yangu, mpuuzi mkubwa yule.” Billy akakaa vizuri, Nelly akajua hasira zinaanza kumpanda.

“Yaani wakati mimi nakuja kuoa huku Africa, nilimwambia kabisa. Akasema yeye hadhani kama ni jambo la busara kutoa mwanamke huku. Itachukua muda mrefu kumfanya aendane na sisi, alingane na maisha yetu ya kule. Halafu leo ndio nimekumbuka.” Akazidi kuwaka. Nelly akajua hiyo siku imeanza vibaya tayari. “Eti akaongeza wasiwasi wa hichi alichonifanyia yeye. Eti iweje akubali nimuoe ili tu aje aishi nchini Uswiz tu na mali, halafu akishazoea anibadilikie iwe sio mapenzi ya kweli! Mchezi yule yeye ndio akafanya kilekile! Akanipora mke wangu!” “Pole Billy. Pole sana. Ila naomba utulie. Umeshapandisha hasira. Unahitaji akili na nguvu tulivu kwa ajili ya safari yetu leo. Acha mimi nitangulie bafuni.” Nelly akaona atoke hapo kitandani kwani Billy alishabadilisha ile hali tulivu pale.

Na yeye Billy akajishitukia maana alimtamka Anele kama bado mkewe. Akajua amempa uthibitisho wa hofu aliyomwambia anayo juu yake na mkewe, wakati wapo kwenye ndege wakielekea Afrika ya kusini. Akabaki pale kitandani akijaribu kukumbuka kwa makini kile alichoulizwa na Nelly wakiwa kwenye ndege ili akitoka hapo bafuni atengeneze. ‘Kwa jinsi ulivyompenda Anele. Amekuzalia watoto unaowapenda hivyo. Akakupitisha alikokupitisha mpaka ukaumia kwa kiasi hicho, unafikiri unaweza kuja kumpenda mtu mwingine kwa kiasi hichohicho?’ Billy alikumbuka neno kwa neno mpaka akakaa kwa hofu. Akakumbuka jinsi alivyokanusha kwa maneno ya busara. Lakini asubuhi hiyo akajikuta akilalamikia juu ya kuporwa mke wake na wala si mzazi mwenzie au aliyekuwa mkewe. “Oooh No!” Billy akahamaki kwa sauti na kujua ameshaharibu.

Nelly alipotoka kuoga akamuwahi. “Naomba uelewe, kinachoniuma si Anele, ni binti yangu. Amenipokonya na mtoto wangu pia!” Akajaribu kusawazisha. “Hata kwa Anele inaeleweka kabisa. Alikuwa mwanamke uliyempenda ndio maana ukamuoa. Amekuzalia binti wazuri wawili, hakuna jinsi ya kuwa sawa juu ya hilo, na hakuna mwanamke anaweza kushindana na hilo.” Hapo ndipo Billy akajua amesharibu kwa hakika. Nelly akaendelea kujiandaa. Akaona na yeye asiongeze neno zaidi, akaoge tu.

 Huku nyuma mtu wa kufua wa hapo hotelini akagonga kuleta nguo mpya za Bill alizotaka zifuliwe kabla hajavaa. Na kweli aliletewa zikiwa na harufu nzuri. Nelly akazipokea na kuziweka kitandani. Billy alitoka akijikausha. “Wameleta nguo zako. Ila nimewaambia kama utakuwa hujaridhika, nitawapigia waje wachukue warudie tena.” “Nafikiri itatosha. Muda wa kuja kuchukuliwa umefika. Nataka tule kabla hatujaondoka.” “Sawa.” Nelly akachukua simu yake. “Acha nizungumze na Jax kabla hatujaondoka. Naona amesahau kama mimi ni dada yake sio mtoto. Ameanza wasiwasi wa makoti, soksi nzito sijui na skafu.” Billy akacheka. “Mwambie tuna kila kitu. Utakuwa sawa.” Nelly akatoka nje kabisa kwenda kuzungumza na Jax, lakini Billy alimuona amebadilika. Siye Nelly aliyeamka asubuhi hiyo mpaka akahisi hiyo simu angeweza kuzungumza hapohapo ila anamkwepa tu. 

MLIMA KILIMANJARO.

K

ulikuwa na utulivu wa namna yake hata walipokuwa huko mlimani wakipanda mlima. Nelly alitulia sana. Sura yake ilitulia mno. Si ile ya ukorofi ila akawa kama mtu aliyetingwa na mawazo. Billy alijaribu kumuongeleza mara kadhaa, na kupewa majibu ya jumla ila matulivu tu bila jazba. Hawakutaka kuharakisha kupanda. Na kwa kuwa pesa ilikuwepo, wao walichukua safari ndefu ya siku 8 kufika kileleni, UHURU PEAK, kwa kutumia njia ya Lemosho, kitu kilichofanya wafikie lengo, kufika kileleni japo ni kweli pesa ilimtoka Billy.

          “Billy.” Nelly akamuita wakati wanapumzika siku ya nne. “Nimezungumza na huyu anayetusindikiza. Nimejua hii safari imekugarimu sana. Na najua umeshalipia. Tafadhali niruhusu kukufidia garama zangu.” Billy akabaki akimtizama. “Mimi nina pesa Billy. Matumizi yangu ni mimi tu, sina majukumu hata yakumnunulia mtu soksi. Acha nikufidie.” “Unaogopa kuingia kwenye kundi la Anele?” Ikawa kama Billy amemgundua. “Namlalamikia Anele kwa kuwa amenitenda vibaya, Nelly. Sio kwa ajili ya pesa nilizotumia kwake. Halafu wewe hujaniomba, nimeamua mwenyewe. Wewe si nusu ya Anele.” “Unajuaje?” “Kwa hiyo huo ndio wasiwasi wako?” “Mimi ninachotaka kukwambia ni kuwa, ninayo pesa na sina majukumu. Hii safari nimeifurahia sana ila ni garama! Hakuna sababu ya wewe kugaramia peke yako wakati na mimi pesa ni nayo na inaendelea kuingia. Ni hilo tu Billy. Na sina nia ya kukuudhi au kukuumiza.”

“Na mimi ninayo pesa. Na nimeamua kuitumia kwa namna hii. Tafadhali naomba usijilinganishe na Anele. Nimekosea kumleta katikati yetu, tena kwa siku kama ile ambayo tuliamka vizuri. Lakini kam anilivyokwambia, mtoto wangu ndiye anayeniuma Nelly. Mke naweza pata mwingine, lakini kwa umri huu napata wapi mtoto mwingine?” Hapo Nelly hakujibu. Wakatulia kidogo. Nelly akaona aage. “Acha nikalale. Usiku mwema Billy.” “Na wewe.” Hiyo siku nayo ikaisha hivyo. Nelly akaenda kulala kwenye hema yake na kumuacha hapo. Billy akaona amuache tu.

Siku ya nane walifika kileleni, wakapiga picha za kutosha tu na kupewa certificate zao, kila mmoja wao akafurahia na safari ya kurudi ikaanza. Ilichukua tena siku mbili tu kurudi hotelini. Walifika mida ya jioni hotelini. Nelly alitangulia kuoga. Akaja Billy. Wote walikuwa wakitamani tu kitanda. Wakaagiza chakula kiwafuate hapohapo chumbani. Wakala na kujitupa kitandani wote kama wafu. Hakuna aliyekuwa na habari na mwenzie mpaka asubuhi Billy alipomsikia Nelly bafuni akioga. Akabaki amejilaza tu kitandani.

Trouble in Paradise.

Tamu Yaingia Shubiri.

Nelly alitoka, akaanza kuvaa. Alipomaliza, akamuona amejitengeneza vizuri na kutoka taratibu kama asiyetaka kumuamsha. Baada ya muda akamuona amerudi tena hapo chumbani. Macho yakagongana na Billy pale kitandani. “Billy?” Billy akamtizama akiwa bado amejilaza hapo kitandani. “Nashukuru kwa wakati mzuri niliopata tukiwa wote.” “Ooohooo! Mbona kama naagwa moja kwa moja?” Nelly akacheka taratibu na kuendelea. “Umenisaidia kunifungua akili na moyo kuwa naweza kuwa na furaha, na maisha sio mabaya hivyo. Ila naomba safari yetu mimi na wewe iishie hapa.” Billy akabaki tu kimya.

“Naomba mimi niondoke leo, nikamalizie likizo yangu nyumbani kwangu na Jax. Nahisi ananihitaji sana sasa hivi. Nahofia asije kuharibikiwa na mimi nikishindwa kumsaidia. Ni hilo tu.” “Labda niulize kwa nini umeamua kuhitimisha kwa haraka?” “Binafsi sioni kama ni haraka. Tumekuwa na wakati mzuri zaidi ya tulivyopanga. Na nafikiri na wewe ulimaanisha uliposema ulifurahia. Halafu Billy, mimi sijioni kama ni mtu sahihi kwako.” “Kwa nini?” “Unakumbuka nilikwambia nilikuwa nashindwa hata kujitizama kwenye kioo baada ya kufanya mapenzi na mjomba?” “Nakumbuka.” “Si kwa sababu alikuwa mjomba wangu. Ni kwa sababu alikuwa mume wa mtu. Kitendo cha kujua anaye mke nyumbani na mimi nalala naye, kilikuwa kikinimaliza mno. Ndivyo ilivyo kwako.” “Lakini mimi si mume wa mtu, Nelly!” Billy akashangaa sana mpaka akakaa.

 “Kwenye makaratasi si mume wa Anele. Lakini bado moyo wako umeunganishwa naye, sioni kama unayo nafasi kwa mtu mwingine, Billy.” Nelly akaendelea. “Anele ni mwanamke inaonekana ulimpenda sana na umeshindwa kumuacha. Bado unamlalamikia Carlos kukupokonya mke wako na si aliyekuwa mke wako.” Billy akakunja uso.

“Inawezekana wewe hujajisikiliza, ila mimi nakusikiliza Billy. Moyo wako hauna nafasi ya mtu mwingine, na hata kama unayo, mimi si mtu sahihi kwako. Sitaweza. Utanimaliza kabisa. Sitaweza kuishi kwenye hiyo hali. Katikati yako wewe na Anele! Hakika sitaweza Billy. Samahani, lakini mimi sio mtoto mdogo au binti mdogo. Siwezi kupoteza muda zaidi. Naomba mimi niondoke, kabla hatujaharibu chochote kilichotokea kati yetu.” Billy akachoka kabisa.

“Nimepata ndege na usafiri wa kunipeleka KIA. Naomba nikuache upumzike na mimi nikapumzike kabla sijarudi kazini.” “Unaondoka Nelly?” “Kabisa Billy. Naondoka. Na ninaomba tukubaliane hivyo. Naijua nguvu ya mapenzi kwa kuiona kwa watu, hata kwa Jax. Linapokuwepo penzi mahali, halivunjwi kwa kuandikishana kisheria. Upendo upo na nguvu ya ajabu sana.” Nelly akajiweka sawa. “Billy, Jax alivunja uchumba uliokuwa umebakisha siku chache ifungwe ndoa! Eti sababu ya mwanamke anayempenda kurudi kwenye maisha yake! Alimuacha binti mzuri sana, tena akiwa mjamzito! Yule binti aliachwa na hali mbaya sana Billy. Sitaki kuja kufika pale. Mimi sina nafasi hiyo.” Nelly aliongea taratibu tu kama aliyekwisha kufikiria na kufikia hayo maamuzi.

“Sasa hivi Jax anajutia kuvunja uchumba na binti mzuri, akijilaumu sana. Lakini mimi najua ni mapenzi tu. Msichana aliyemrudia kama angetulia na hakuwa amerudi sababu ya pesa ya Jax, nina uhakika kwa asilimia 100, Jax asingerudi tena kwa Lara. Anarudi kwa Lara kwa sababu upendo wake wa dhati kwa yule binti wa kwanza, umeshindwa kupokelewa. Inamaana Tula angejishusha kidogo tu na kumdanganya Jax, Jax asingerudi kwa Lara kabisa. Angesamehe pesa, muda, mtoto na mapenzi ya Lara sababu ya mapenzi ya kweli aliyonayo kwa Tula. Nimekataa kuwa Lara, au mama yangu, kwa yeyote yule.” “Na hiyo ndio hofu yako.” Akamalizia Billy.

“Sijui Billy, lakini sidhani kama niliumbwa kuwa mtumwa wa mapenzi. Hapana. Ni rahisi kuwa peke yangu na maisha yakiendelea, kuliko ile hali niliyokuwa nikiiona kwa mama yangu na kwa Lara mara baada ya kuachwa na Jax! Hapana Billy. Sidhani kama hata nastahili kulipa hiyo garama kwa yeyote yule. Sitaki na sipo tayari.” Kama utani tu, Nelly akachukua mizigo yake, alikuwa amerudi na gari ya kubebea mizigo ameacha nje ya mlango. Akapandisha mizigo yake yote. Akarudi pale alipokuwa amerudi kujilaza Billy. Akazunguka kabisa kwenye ule upande aliokuwa amejilaza. Akainama na kumbusu shavuni. “Nakushukuru sana Billy. Asante. Uwe na mapumziko mema.” Nelly akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment