Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Chozi Langu! - SEHEMU YA 18. - Naomi Simulizi

Chozi Langu! - SEHEMU YA 18.

 Jumanne.

Usiku wa jumanne wakiwa nyumbani, Lara na Lea wametoka, Jax akarudi tena. “Mimi naona uhamie tu huku, baba.” Wote wakacheka jinsi mama Chiwanga alivyozungumza kwa upole lakini akimaanisha. “Nimekuja kumfuata Lara.” “Huyu Lara si alisema anaondoka ijumaa sababu miahadi yake ni jumamosi si alhamsi tena!” “Hata yeye hajui kama ninakuja. Nilifikiria tu leo asubuhi nikaona ni msuprise.” “Haya, baba. Karibu. Ila ametoka na Lea.”
“Acha nimpigie ili niwafuate huko walipo.” Bila kusubiri akatoa simu, mzee Chiwanga na mkewe wakaangaliana. Lara alipopokea tu, Jax akatoka hapo mbio bila ya kuaga kama anayewahi kuokoa kitu. “Huyu kijana atachanganyikiwa jamani!” Mama Chiwanga akaongea kwa kumuhurumia Jax.

Jumatano.

Lara na Jax kabla ya kuondoka hapo, mama Chiwanga akataka kuzungumza nao. Wakaweka mizigo kwenye gari wakarudi hapo sebuleni. “Mimi nitawaambia kwa uwazi kabisa wala sitawaficha kwa sababu sitaki mkarudie kosa.” Lara na Jax kimya. “Mwanzoni mlikimbilia kuishi maisha ya ndoa kabla ya ndoa yenyewe na mnaona kilichotokea.” “Usiwe na wasiwasi mama. Wala sitarudia kosa.” Mpaka Jax akamgeukia vizuri Lara kwa mshangao.

“Jax hatakwenda kuniweka unyumba tena mpaka tutoke kanisani.” Lara akaongea bila wasiwasi akimtizama mama yake, mpaka Jax akapoa. “Nishaamua kubadilika mama yangu. Natulia kabisa. Na ahadi yangu ipo palepale. Natulia kabisa. Ukinisikia tena, ujue ni mke wa huyo mtu. Wala usiwe nawasiwasi. Nakumbuka shida na maombi yako yote juu yangu. Sitajiingiza tena matatizoni. Nimejifunza kwa machozi. Nakuahidi nakwenda kutulia kabisa. Na sitaanzisha safari ingine na mwengine mpaka nihitimishe na Jax rasmi.” Hapo Jax akaridhika.

“Natoka hapa kwenda kuendelea na maisha, nikiwa na Mungu wangu. Nimetubu, tumeomba pamoja mama yangu, ujue nimekusudia kubadilika. Endelea tu kuniombea mama yangu.” “Hapo sawa. Maana nimehofia msije mkatoka hapa, mkaanza tena maisha mliyoishi zamani.” “Hapana mama yangu. Huko sirudi tena. Naendelea tu na naomba Mungu atusaidie. Ikishindikana na Jax, basi anipe mwingi..” “Naomba acha kusema hivyo, Lara! Nimekuomba mara nyingi tu!” “Basi, Jax. Ila huo ndio msimamo wangu.” “Nimekusikia, Lara na mimi nitaheshimu hilo.” Wakapoa kabisa, zaidi Jax mpaka wote wakamgundua ndio ilikuwa nia yake akijua anamtoa hapo Lara kwenda kuishi naye.

“Na wewe Jax, mpe Yesu maisha, baba. Sio dini. Mruhusu akulinde. Wala usitake mengi. Yeye akiwa mlinzi atakusaidia kwenye huo ujana wako. Atatawala maisha yako na utashangaa uhuru utakao kuwa nao ndani ya Kristo. Atakupigania na kukulinda.” Mama Chiwanga akaendelea. “Amani iliyopo ndani yake, inapita yote. Haifananishwi na kiwango cha pesa kilichopo benki, wala elimu iliyopo kichwani mwa mtu. Upo utulivu, Jax mwanangu, na utoshelevu wa aina yake. Ni baba wa yatima. Anayofaraja ya ajabu na atakusaidia kwenye kila hatua kwenye maisha yako. Tafadhali mruhusu, mfungulie mlango aingie kwenye maisha yako.” Lara kimya akimsikiliza mama yake akizungumza na Jax.

“Mtakuwa na ndoa nzuri yenye utulivu. Hata mambo yakiwawia magumu, mnakuwa na kimbilio.” “Nimekusikia mama yangu.” “Mimi nitakuombea, halafu usiache kwenda kanisani. Nendeni tu, huko ndiko utakutana na Mungu na utajifunza maisha ambayo Mungu anataka wewe uishi na yanayompendeza yeye.” Mama Chiwanga akamuongoza sala ya toba. Jax akakubali kumpa Yesu maisha akiwa hata hafahamu vizuri ni nini anatakiwa kufanya, akawatamkia baraka, wawili hao wakaondoka kurudi Dar.

Safari Mpya ya Jax&Lara.

Njiani kulikuwa na hali ya utulivu kati yao lakini kama wageni kwa kila mmoja wao. Hawajui wazungumze nini kati yao. Kila mmoja akijiwinda kwa neno wakati ni wapenzi waliokuwa hawamalizi mazungumzo na vicheko. Wakajikuta wamekuwa wageni kwa kila mmoja wao. Simu ya Nelly ikaingia. “Mpitie nyumbani kwa chakula.” Angalau hilo likamfurahisha zaidi Jax. Kwa mara ya kwanza Nelly anampokea mwanamke wake nyumbani kwake na kumkarimu! Hilo likamfurahisha sana Jax, na likaleta maana kubwa sana asijue dada yake ameamka na hali mbaya, akiwa hajui chakufanya, akaishia kupika. Hakuwa amemtafuta Billy hata kwa ujumbe wa kumjulia hali na wala Billy naye hakumtafuta. Alikusudia kumuacha kabisa kitu kilichomuuma Nelly. Alijua pengine Billy angemtafuta, lakini ikawa kimya kabisa.

“Dada Nelly ametukaribisha nyumbani kwa chakula cha usiku.” Lara hakuamini. “Kweli Jax?!” “Hata mimi nimemshangaa. Ila amebadilika! Sio Nelly nimekua nikimuona siku zote.” “Amekuaje tena?” Lara akaingiwa na hofu kidogo. “Hapana. Amekua wa tofauti kwa upande mzuri. Nashindwa kumuelezea, lakini sasa hivi angalau anaweza kukaa na kueleza siku yake iliendaje huko kazini. Akataka kunisikia ninavyoendelea. Yaani ameongeza kujali kwa namna ya tofauti! Anazungumza na mimi heart to heart. Sijui umenielewa?” Lara mwenyewe alicheka jinsi Jax alivyokosa maneno sahihi kwa dada yake.

“Wewe unafikiri ni kwa nini yupo hivyo?” “Wakati gani sasa? Maana Nelly huyu si yule wa zamani. Hakika amebadilika.” “Namaanisha yule wa zamani.” “Mimi nahisi, narudia tena nahisi maana sipo karibu naye sana kujua kinachoendelea na kilichoendelea tulipoachwa.” Hapo Jax akatulia. “Nini?” “Unajua sikuwahi kumuuliza maisha yalikuaje, au alifanyaje fanyaje kufanya tuishi! Maana niliachwa na wazazi hata sikuwa na miaka 5, na Nelly alikuwa mdogo tu. Na simkumbuki mwanadamu mwingine kwenye maisha yanu ila yeye!” Jax akawa kama ameingiwa na kitu kichwani na kumfanya afikirie zaidi.

“Kuanzia hospitalini mpaka shuleni, ilikuwa ni Nelly tu. Na nakumbuka alikuwa akinisisitiza nitulie shuleni ili asiwe anaitwa, ili na yeye aweze kufanya vitu vingine. Kwa hiyo tumekua tukiwa sisi tu. Sijui alikuwa akifanyaje, nahisi kwenye hicho kipindi ndipo alipokutana na magumu au ndivyo alivyoumbwa, sijui! Lakini nimeanza kujichukia kushindwa hata kupata naye muda kumuuliza ilikuaje kunifikisha hapa! Japo pia kwa Nelly yule, nahisi nisingepata hilo jibu. Alikuwa amefunga sana moyo.” Jax akaendelea kuzungumza lakini kama anayemfikiria dada yake, Lara akabaki kimya akisikiliza kama asiyetaka kumuingilia.

“Halafu pia siwezi kumlinganisha kitabia na hata mmoja wa wazazi wetu kwa kuwa kweli siwakumbuki kabisa zaidi ya kwenye picha chache sana alizonazo yeye mwenyewe Nelly. Sasa sijui! Ila najua japokuwa ni mkorofi sana, anaweza kufanya chochote kwa ajili yangu. Hilo ninalijua na japokuwa huwa namuudhi sana, hawezi kunitupa.” “Kwa hiyo ni kama mtoto wake?” “Kabisa. Nimerudi kuishi naye wala hajaniuliza mpaka leo. Ananipikia na kuhakikisha msichana wake anaingia chumbani kwangu kusafisha, kufua na anamuwekea mashati yangu kwenye nguo zake anazopeleka dry clener.” “Jax!” Lara akashangaa.

“Kweli tena. Hapa nilipo nimerudi kulelewa kama mtoto. Nguo zangu zinafuliwa wala sipati shida. Anahakikisha nakula na chumba changu kinasafishwa.” “Ndio maana umehamia moja kwa moja!” Jax akacheka sana. “Ila acha tu  nikwambie ukweli. Nilikuwa na hali mbaya, Lara! Sikuwa na jinsi ila kurudi tu kwa Nelly. Na nafikiri na yeye alijua nimeharibu kiasi cha kwamba hata marafiki wamenikimbia, akawa kimbilio langu na kunisaidia pale anapoweza. Na kweli imenisaidia.” “Kwani siku hizi hampo na Tino?” Jax akacheka na kunyamaza.

“Nini?” “Hapana. Hatupo tena pamoja.” Vile alivyomjibu akajua kuna ambalo anamficha. Akaona aendelee kumdodosa. “Mbona aliniambia alikwambia aliniona Mwanza!?” Jax hakujibu akaendelea kuendesha. “Mimi nilijua mpo kwenye mahusiano kama zamani!” “Hapana. Tino alinichukia sana. Siku hizi ukiona ananipigia simu, ujue ni kutaka kuniumiza tu.” Lara akakunja uso akionekana hajaelewa. “Yaani akiwa na taarifa anayojua kama itaniumiza, basi ndipo atanipigia. Anasema hataki hata kuonekana na mimi ili wote tusije onekana ni wahuni. Akasema wasichana wanawakataa wakidhani wote tuna tabia zinazofanana.” Hilo likamuumiza Lara.

“Na nafikiri ni kwa ajili ya Suzy pia. Amekusudia kumuoa Suzy, na Suzy hanitaki kabisa. Alinifukuza pale mlipokuwa mkiishi na aliniambia nikija kurudi pale ataniitia mwizi.” “Jax!” “Kweli. Sasa nafikiri ndio maana Tino ananikwepa. Halafu pia nafikiri aliumia kuona dada Nelly amerudi kusimama na mimi japo alimwambia hataki kuniona tena na hatajali hata kama Tula atanifunga jela. Sasa dada Nelly akafanya kinyume kabisa na kunipokea. Tino ameacha hata kufika pale nyumbani kwa dada Nelly na nilimsikia dada Nelly akisema ni kama kuna siku alimpigia, hakupokea na hajamrudishia simu yake tena.” “Jax wewe!” “Ndio hivyo.” Lara akazidi kushangazwa.

“Sasa yeye Tino alitegemea dada Nelly akuchukie moja kwa moja!?” “Hata hivyo amenivumilia sana.” “Nani?” “Tino. Amenivumilia sana ndio maana na mimi nimeona nimuache tu. Tokea chuo, amekua na mimi katikati ya fujo zangu na Tula. Ashatukanwa sana na Tula kwa ajili yangu. Ndio maana hata alipokuwa akinipigia simu akiniambia mambo ya kuniumiza, nilikuwa nikimuacha tu. Ila aliponipigia kuniumiza juu yako akisema amekutana na wewe umependeza na upo na the god, pale ndipo nilipomlaumu sana kushindwa hata kuchukua namba zako za simu. Ila tuyaache hayo. Kwa Tino ninavuna nilichopanda, na nimemuacha kama kumpa mapumziko tu. Nitakuja kumtafuta nitakapoweka mambo yangu sawa. Sitaki niendelee kumchanganya na mambo yangu.” Hapo Lara akanyamaza akifikiria.

Walipokuwa wanakaribia Dar, akaona awe muungwana. “Najua haisaidii Jax, lakini samahani juu ya Jerry. Sikujua kama ni mtu mliyekuwa mkimfahamu. Alikuja kwenye maisha yangu na ahadi ya mapumziko tu bila kutaka mambo ya undani, nikaona atanifaa kwa kipindi kile nahitaji kupumzisha akili.” “Sasa akili zimeshatulia?” “Upo wewe Jax. Umerudi kwenye maisha yangu, naamini kila kitu kitakuwa sawa.” Hilo likamfurahisha Jax. “Naamini tutakuwa sawa Lara. Tutabakia sisi tu, na pengine Mungu ataturejeshea ule wakati tuliokua nao zamani.” “Nimekusikia siku hizi unamtajataja Mungu!” Jax akacheka. “Siku hizi, siku za jumapili kama tupo nchini, mimi na Nelly tunajitahidi kwenda kanisani kama wakristo.” Lara akacheka. “Kwa kweli mmebadilika!” Angalau wakaendelea kucheka mpaka wanafika nyumbani kwa Nelly.

Lara kwa Nelly.

W

alikuta Nelly amepika, meza imejaa. Amechoka mpaka uso unaonekana. Jax na Lara wakamsalimia. “Vipi?” Ikabidi Jax kumuuliza. Alikuwa amepoa sana. “Nipo tu sawa, ila nimechoka! Nilikuwa napika tokea alfajiri.” “Nilikwmbia nakuja tu na Lara, si ndivyo?” “Nyinyi kuleni kitakachobaki tutaweka kwenye friji.” Akasimama. “Lara karibu sana nyumbani. Acha mimi nikaoge, ndio nije tuzungumze.” Lara na Jax wakamsindikiza kwa macho, Lara akamgeukia Jax. Jax akapandisha mabega juu kama na yeye hajui. Akanyanyuka kumuwekea Lara kinywaji. “Nashauri tumsubiri tule naye.” Lara akatoa ushauri. Jax akaona sio wazo baya.

Baada ya muda akatoka akionekana ameoga. “Mbona hamjala?” “Tumeona tukusubiri.” Wakahamia mezani. “Mimi ni muwazi Lara, na sijajaliwa lugha ya kulainisha maneno.” Akaanza Nelly akijipakulia chakula. Lara akaanza kuingiwa hofu. “Swali.” Akaendelea Nelly. “Huyu Jax amekuumiza sana. Amekutenda vibaya, lakini sasa hivi nakuona upo naye, kwa makubaliano gani?” Akamuuliza na kumtizama. “Nataka kukusikia wewe maana yeye nimeshamsikia. Na ameniahidi ya kwake. Amenionyesha kwa vitendo amejutia alilofanya. Sasa je, upo naye kwa makubaliano gani?” Mwili mzima wa Lara ukaanza kutetemeka kwa hofu. Nelly ni mkali na hapendi ujinga.

“Nampenda Jax.” “Kwa upendo uleule wa tokea mwanzo? Maana acha nikwambie ukweli Lara. Tula sikumpenda kwa vile alivyokuwa akiishi na Jax. Sasa wewe nilianza kuvutiwa na wewe kwa sababu Tino aliniambia wewe ni tofauti kabisa na Tula. Sasa kwa hili alilokutenda Jax, unafikiri utaweza kuishi naye kama zamani?” “Naamini hivyo dada yangu. Naamini hivyo. Ni kweli nimemsamehe Jax ndio maana leo unaniona nipo naye. Na nipo naye kwa kuwa na mimi nilipenda tulivyoishi naye mwanzoni. Na mimi nayatamani yale maisha yetu ya mwanzoni kabla hajarudiana na Tula.” “Nilishaachana na Tula.” Hapo Jax akaingilia.

“Najua Jax. Ila ninachotaka kusema, sina shida yakupata mwanaume wa kunioa, ila mtu ambaye nitaishi naye kama Jax. Ambaye ni Jax mwenyewe. Jax sio mjeuri wala mbishi. Hajui kugomba na ni mtu mzuri. Najua atanipa ndoa nzuri kama ya wazazi wangu.” Nelly akacheka. “Kweli dada. Mimi napenda ndoa kama ya wazazi wangu. Wanakitu cha tofauti mbali na mali. Wanacheka mpaka unawasikia chumbani kwao wakicheka na wapo wawili tu! Huwa sisi tunaambiana na kuwashangaa ni nini wanachocheka miaka yote huwa hawamalizi! Na wanakumbushana stori za miaka na miaka hawamalizi! Watu wanaoweza kukaa sehemu kwa muda mrefu na hawachokani! Sisi huwa tunawashangaa, lakini ni kama tulivyoishi na Jax, japo Jax huwezi kumlinganisha na baba yangu, ila ni kama tulivyoishi, tuliwakaribia.” Hapo Jax akakunja uso.

“Kwamba mimi nimepungua kwa baba yako!?” Jax akauliza. “Namaanisha yeye baba yupo na mama akiwa amemaliza. Na mwenyewe baba anasema hivyo ni tokea mwanzoni.” Ndugu hao wakapoa. “Baba anasema alivyoamua kuwa na mama, hakuna alichokuwa amebakisha. Kwa wazazi wake ambao walitaka amuache mama kwa kuwa alichelewa kumzalia watoto na kuja kumzalia watoto wakike watupu, na akamaliza hata kwenye vishawishi vya nje. Usemi wa baba ni kama alivyokwambia Jax. Hasumbuliwi na vishawishi vya nje kwa sababu yeye aliamua kujifunga kwa mama tu. Ndivyo walivyo tokea sisi ni wadogo mpaka leo. Na mimi natamani hiyo dada yangu.” “Lakini mimi nimejirudi Lara!” “Si ndio maana nipo hapa, Jax!”

“Sasa mbona unasema ni kama sipo kama baba yako?” “Na wewe Jax tumia akili acha kutaka sifa ambazo ulishaharibu. Lara hamjui Jax aliyejirudi. Mpe muda aone kama kweli hutarudia kosa. Wewe vipi?” Nelly akawa mkali kidogo. “Ndio mmerudiana kwa kosa la kumwingiza mwanamke mwingine katikati yenu, umejirudi tu! Halafu eti unataka uanze kupewa sifa! Wewe vipi bwana? Ishi hata miaka 10 mbeleni. Pata vishawishi na sisi tukuone umeweza kuvishinda ndipo usifiwe.” Jax akanyamaza.

“Sitamnyanyasa Jax, dada. Mimi si mnyanyasaji na sipendi ugomvi kabisa. Ni bora nikishindwa niondoke kuliko kuishi maisha ambayo hata mimi hayanipi furaha. Siwezi na sijui ugomvi.” “Kwa hiyo unataka ndoa au unataka kusubiri kwanza umchunguze?” Nelly akaongeza swali jingine na kuendelea. “Maana mimi nimezungumza na Jax. Sitaki upuuzi. Asinitie shuguli ya kumuandalia harusi, halafu aje anifanyie kama alichomfanyia Tino. Tino ametuchukia kabisa, hataki hata kutusikia mimi na huyu shoga yake, sababu ya aibu aliyomtia hapa mjini. Na ndio maana leo upo hapa, ili tuzungumze, tuwekane sawa.” Jax akamshangaa dada yake.

“Nelly!” Jax akajikuta akishangaa kwa sauti. “Kabisa Jax. Sina muda wa kupoteza, na sitaki mambo ya kubabaisha. Nilitaka afike nyumbani rasmi na kutaka kupata naye muda kama huu nizungumze naye. Narudia tena, sitaki vijimambo mimi. Jina langu na wadhifa wangu ndio nilichonacho hapa mjini. Sasa sitaki drama. Sio niandae harusi, halafu mje muanze habari za ajabu. Narudi kwako Lara, unataka ndoa? Na upo tayari kwa lini?” “Labda...” “Usiniingilie Jax. Nilishazungumza na wewe. Ukanijibu maswali yangu yote mpaka nikaridhika. Sasa hivi nataka kumsikia Lara. Usiingilie.” Nelly akamgeukia Lara.

“Mimi nataka ndoa na Jax hata kesho.” “Wewe mtoto!” “Nampenda Jax, dada, wala sina sababu ya kusubiri. Mimi sijui unaishi na Jax wa namna gani, ila mimi niliishi na Jax ambaye nilibaki nikimkumbuka mpaka kumuonea wivu Tula.” Lara akaanza kulia. “Nilikuwa nalia natamani Jax anichague mimi. Na hata nilipohisi ataniacha, pia nilikuwa radhi kumtunza mtoto wake mimi mwenyewe nikijua atakuwa mtoto mzuri kama Jax.” Hapo akamgusa sana Nelly na Jax mwenyewe.

Akajifuta machozi. “Na nimemuona jinsi alivyokuwa akirudi kunitafuta pale nyumbani, naamini Jax hajabadilika. Na ananihitaji mimi, ndio maana nipo hapa na Jax. Kama alivyosema Jax, naamini Mungu ataturejeshea maisha yetu ya zamani.” “Yalikuaje?” “Dada Nelly!?” Jax akashangaa sana. Wote wakacheka.

“Wewe unawasiwasi gani, mimi nazungumza na Lara?” “Sasa Lara si ashakujibu! Unataka kumrudisha nyuma bwana!” “Wewe achana na mimi. Nijibu mwaya Lara.”  Lara akacheka kwa wasiwasi. “Tulikuwa hatuna mengi. Halafu tunaishi uswahilini tu. Joto. Chumba kimoja halafu kumebana! Lakini dada, ungetamani kuwepo kwetu.” “Hata Tino alikuwa akisema. Lakini akawa anasema eti hana jinsi ya kueleza.” “Hata mimi sina jinsi nzuri dada yangu, ila kulikuwa na utulivu. Jax hana makuu.” “Mimi nahisi ni wewe tu. Huyu Jax sijui kama...” Jax akacheka na kutingisha kichwa. “Mimi ni mtu mzuri sana, dada yangu.” “Mmmhh!” Nelly akaguna na kusimama kufuata barafu kwenye friza.

Jax akashangaa anatafuna barafu na si chakula. Akashangaa kidogo ila akaona amuache tu. “Sasa mimi nimeambiwa unataka harusi ya kanisani na uvae tena shela.” “Kabisa dada yangu.” Nelly akacheka na kutingisha kichwa. “Huoni aibu?” “Dada Nelly!” Jax akashituka sana. “Hata kidogo dada. Naolewa na Jax! Nilimkubali tokea mwanzo na ndiye huyohuyo ananioa! Sina sababu yakujificha dada. Wakati mwingine natamani angekuwa si yeye Jax, awe mwanaume mwingine tuliyeishi naye kwa fujo. Lakini Jax alikuwa ananipenda. Ananitangaza mpaka kwa marafiki zake! Hanifichi! Anataka watu wajue mimi ni wake! Napata wapi mwanaume kama huyo dada?” Hapo Nelly akapoa. Akakumbuka alivyomkatalia Billy asifahamiane na Jax. Akatulia kabisa wakamuona amepotea kabisa pale.

Jax akamkonyeza Lara. Akajua anatakiwa kuaga, kwani ni sauti ya barafu tu alizokuwa akitafuna Nelly ndiyo iliyokuwa ikiendelea kusikika hapo. “Nashukuru kwa chakula dada yangu.” Nelly akamwangalia. “Hivi na wewe utaendelea kuniita dada mpaka lini?” Lara akacheka. “Mimi ni dada yake Jax tu.” “Haya dada, nimesikia.” Wote wakacheka. “Ni wifi.” Lara akarekebisha. “Haya. Mimi nitaanza maandalizi ya harusi. Naamini tutafanikiwa.” “Nashukuru dada yangu.” “Na mimi nashukuru  kwa kila kitu dada...wifi yangu.” Wakacheka. “Na asante kunikaribisha nyumbani. Nimefurahi na asante kwa chakula.” “Nimepika kingi nikiwa na mawazo. Unachotaka kuchukua, mwambie Jax akufungashie uende nacho.” Akasimama na kutoka hapo kama kuwapisha wawili hao.

“Wala sijivungi. Ndio dada Nelly anapika vizuri hivi!” “Amekwambia uache kumuita dada.” Wakacheka. “Wewe nifungashie chakutosha, nikale huko niendapo.” Jax akamsaidia na kutoka. “Unarudi au unalala kwako?” “Narudi dada yangu. Nampeleka tu na kurudi.” “Ikitokea unabadili mawazo huko, naomba unijulishe, usiniache nikeshe nikikusubiri.” Jax akacheka akitingisha kichwa. Akatoka na Lara.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Jax na Lara wakatoka hapo. “Nakushukuru kwa kunizungumza vizuri kwa dada yangu.” “Ndivyo ulivyo Jax. Wewe si mgumu kuishi pamoja.” “Nafikiri tuliendana tu Lara. Haikuwahi kuwa hivyo kwa Tulla. Kila wakati alikuwa na kitu cha kunilalamikia. Ndio maana na mimi nilikuwa nikikukumbuka.” Wakatulia mpaka nyumbani kwa Jax. Jax akamtambulisha tena getini kuwa yeye ndiye atakuwa akiishi hapo. Kisha akamsaidia kubeba mizigo, wakaingia ndani. Lara akacheka.

“Naona umebadilisha hapa ndani.” “Nimeweka tu tailizi/marumaru nyeusi na kubadili rangi. Umependa?” “Sana. Aina hii ya marumaru ni nzuri.” “Na garama pia. Ila nimeona itapendezesha nyumba zaidi. Karibu.” Akamuona anamuingizia vifaa vyake chumba kingine. Lara akafuata nyuma. “Kile chumba kingine bado kina vitu vyangu. Zaidi nguo. Huwa nakifunga kabisa mpaka niwe nakuja kubadili nguo. Au ungependa kutumia kile ambacho kina bafu ndani? Maana hivi vingine nivyakuchangia choo. Masta ni kimoja tu.” “Popote Jax. Mimi sitachagua. Ilimradi umenipa hifadhi, nashukuru.” “Nikwambie ukweli Lara?” Lara akaweka vitu chini na kumwangalia.

Alimjua Jax ndio jinsi ya zungumza yake. Anataka mtu amsikilize kwa kumwangalia. “Sikutaka kabisa urudi kuishi kwa kina Suzy. Ndio maana ilinibidi kuharakisha uje uishi hapa. Wale wasichana wamenivunjia sana heshima.” Lara akanyamaza. “Najua nilikosa, lakini sikupenda walivyonibadilikia. Walinibadilikia kwa kunidharau sana. Zaidi Suzy! Sikutaka kuja kurudi tena pale hata kwa kuja kukuona wewe.” Lara ndio akaelewa kuwa hataki kuja kuwaona hata pale. “Nimeelewa Jax.” “Ni kwa muda tu. Acha sisi tukae kwanza sawa. Mambo yetu yaeleweke ndipo hata tukirudi kwao, iwe tumeleta maana kwenye jamii. Najua kwa hakika Tino atakuwa amewashirikisha mambo yako pia na Jerry.” Hapo Lara akakosa nguvu kabisa.

“Ndio maana naona tutulie mpaka tujipange sisi wenyewe kwanza, ndipo tuwatafute.” “Nimeelewa Jax.” “Ila watu wa nyumbani wanakaribishwa muda na wakati wowote ule. Nilimsikia Lea akikwambia usimsahau.” “Lea anataka na yeye kuja kujaribu maisha huku Dar. Sasa nilimwambia pengine mpaka nipate mahali pakuishi, pakueleweka ndio nitamuita.” “Basi uwe huru.” “Kweli Jax!?” “Kabisa. Hapa ni kwetu. Kuwa kuru.” Lara akamsogelea kumpa busu la shukurani, ikawa kosa.

Yakaanza mabusu kwa wawili hao. Lara akanogewa. Alikuwa na hamu na huyo Jax wakisubiria fungate. Jax naye akaona asimkumbushe swala la kusubiri. Yakaendelea mabusu ya haja kwa wawili hao waking’ang’aniana. Yalipotaka kuanza tu mapenzi, Lara akagutuka. “Hapana Jax.” “Lara!” “Kweli Jax. Naomba na safari hii uwe mvumilivu kwa hakika. Sio utoke hapa uende ukatafute kwengine. Ukishindwa safari hii basi.” “Nimesubiria kwa muda mrefu Lara! Nihurumie mpenzi wangu. Nakutamani wewe. Nimekaa muda mrefu sana bila ya...” “Sasa wewe utakuwa ukifanyaje nikiwa najifungua?” “Mimi si mdhaifu wa ngono kiasi hicho Lara, na wewe unanijua. Ilimradi nipate mara moja tu, basi natulia. Na nakuahidi sio kwamba na...” “Bwana ondoka Jax! Unanifanya nianze na mimi kukutamani wakati tulikubaliana mpaka mbele ya mama kuwa tutasubiri.” “Wewe ndio ulikubali, lakini mimi sikusema kitu. Nilikubali maombi. Na ninakuahidi hakutakuwa na mwingine badala yako.” “Toka Jax.” Lara akamsukumia nje kabisa, Jax akicheka. Usiku huo wakafanikiwa. Jax akaondoka.

Alhamisi.

N

elly akajifikiria, akaona aende tu hospitalini. Akadamkia ofisini. Akafanya vikao vyake vyote mida ya asubuhi, kwenye mida ya saa tano, akatoka hapo kuelekea hospitalini. Alikaa huko mpaka mida ya saa saba. Akaona simu ya Billy ikiingia. Alishituka karibu atupe simu. Ikaita mpaka ikakata. Ikaita tena, Nelly hakujua amwambie nini. Ikakata akiitizama. ‘Tafadhali pokea simu yangu.’ Ujumbe ukaingia na simu ikaanza kuita tena. Safari hii akapokea. “Uko wapi?” Nelly akatulia. “Nelly?” Kimya akimsikiliza Billy. “Umetoka ofisini tokea asubuhi na hakuna anayejua ulipo. Si kawaida yako. Uko wapi?” “Hospitalini.” Nelly akajibu. Pakazuka ukimya kidogo.

“Wapi?” “Nakaribia kumuona daktari. Namba yangu imekaribia. Bado watu wanne tu mbele yangu. Nikitoka hapa narudi ofisini.” “Sio jibu la swali langu.” Nelly akatulia akifikiria. “Nelly?” “Nafikiria.” “Ulipo!?” “Kama uje au la.” “Kwa nini?!” “Nitakuja kukwambia. Ila kwa sasa naomba muda Billy. Kuna jambo nataka likikaa sawa ndipo nikutafute.” “Sawa. Lakini nataka kujua ulipo.” “Si nimekwambia naomba muda!?” “Na mimi si nimesema sawa? Kwani tokea lini ninachokitaka mimi ndicho unachokitaka wewe?” “Ni kwa nini unakuwa mtu wa kung’ang’ania maamuzi yako hata kama...” “Unapotezea muda Nelly. Uko wapi?” Nelly akamuelekeza.

Billy anafika hapo na namba ya Nelly ikawa ndio imefika anaingia kumuona daktari. Na yeye akaingia bila kuomba ruhusa. Nelly akawa anamkabidhi dakitari baadhi ya makabrasha aliyokuwa nayo baada ya vipimo vya awali kwa manesi. Kabla yule daktari hajashika yale makabrasha vizuri, Billy akampokonya makabrasha yote na kuwashangaza Nelly na yule daktari. Akaanza kusoma.

“Nelly anaumwa nini?” Billy akawa anauliza huku akisoma. “Pressure ipo juu, ndio maana daktari aliyemuona mwanzoni amemshauri aanza kliniki mapema ili kuhakikisha yeye na mtoto wapo salama.” Yule daktari alimjibu kwa lugha ya kingereza kama anavyoongea Billy. “What!?” Billy alishituka na kumwangalia Nelly kwa mshangao.

“Naomba mkabidhi daktari hilo faili na umuache amalizie, tutoke hapa. Nataka kurudi kazini.” “Kwamba ni mjamzito, halafu huniambii!?” “Kwani wewe ulipanga kuzaa na mimi? Mimba ipo kwangu, wewe unashituka nini?” “Umenikosea sana Nelly.” Nelly akashangaa sana. “Wewe vipi Billy?” “Kwa upande wa Jax sina amri nako. Ila linapofika swala la mtoto wangu, mimi nina jukumu la kujua.” “Sasa ningejuaje kama unataka?!” “Uliniambia, nikakataa?” Daktari akabaki akiwaangalia watu wazima hao.

“Eti Nelly?” “Acha kugomba hapa kama baba aliyekuwa amekaa kwenye ndoa mika 50 hajapata mtoto wakati wewe ni baba mwenye watoto wakubwa kabisa.” “Nelly?” “Ni nini Billy wewe? Hivi unajua na mimi ndio nimejua leo kama ni mjamzito? Hivi unajua hofu niliyoipata baada ya kujua mimi mtumzima ni mjamzito?” Hapo Billy akatulia kidogo. “Niliingiwa hofu nusu kuzimia ofisini kwa daktari baada yakusikia hali ninayojisikia ni ujamzito! Hata sikujua mtumzima kama mimi naweza kushika mimba! Nipo hapa sasa hivi baada yakupewa mapumziko mafupi sababu ya mshituko. Tafadhali acha kuniongezea hofu Billy.” “Samahani.” Hapo Billy akasikika ametulia ila na mshituko.

“Kwanza inakuaje mtumzima kama mimi nashika mimba jamani?” Akamgeukia daktari akilalamika. “Maadamu hujakoma hedhi, unaweza kushika mimba.” “Huyo mtoto atazaliwa salama kweli? Maana nilisikia ukiwa mtumzima ukishika mimba unaweza zaa mtoto tahira. Au hata kufa. Kufa mimi mwenyewe au..” “Naomba utulie Nelly?” Billy akamtuliza. “Hivi unajua umri wangu wewe Billy?” Nelly akamuuliza Billy kwa ukali. “Unajua majukumu niliyonayo mimi? Sina muda na kubeba mimba. Halafu sina moyo wakulea mtoto.” Isivyo kawaida yake, Nelly akaanza kulia hapo. Homoni za mimba zikamsaidia kulia bila shida. Akalia hapo akijieleza hili na lile jinsi asivyotaka yeye mtoto, mwishoe wakatoka bila hata daktari kuzungumza chochote, ila wao wenyewe kubishana hapo na Nelly kulia na kuamua kutoka kabisa hapo.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Naomba niache mimi nirudi kazini. Usinifuate Billy. Nataka nirudi kazini.” “Ulisikia kitu chochote kama pressure ipo juu?” “Kwa hiyo?” “Naomba ukapumzike kama daktari alivyokuandikia mapumziko.” “Haijawahi kutokea nalala siku ya kazi. Na hii mimba haitanifanya hivyo.” “Labda mimi niulize, unapingana na nani sasa hapa? Uhalisia?” “Nyinyi ndio mnataka kuonyesha mwanamke hawezi kuzaa na kufanya majukumu mengine. Mimba si ugonjwa wala haimfanyi mwanamke akashindwa kufanya majukumu yake.” Billy akaanza kucheka.

Nelly akaanza kulia. “Maisha yangu yameshabadilika. Ndio nimetoka tu kumwambia Jax juu yako, leo narudi tena na mimba! Hakika si..” “Kabla hujaweka mipango migumu. Acha mimi nikupongeze kwa hatua ngumu ya kunitambulisha kwa Jax.” “Acha kunikejeli Billy!” Nelly akazidi kulia. “Hakika homoni leo naona zipo juu sana. Nashauri ukapate mapumziko Nelly. Unahali mbaya!” “Tafadhali usiendelee kucheka Billy.” “Nakuhakikishia utakuwa sawa Nelly.” “Unajuaje? Nimemuharibia Jax maisha, unafikiri nitawazaje kuwa mama kwa huyu mtoto?” “Hapo nimeelewa wasiwasi wako. Sasa twende ukatulie halafu nikwambie kitu.”

“Sitaki. Wewe niambie sasa hivi.” “Wewe unamoyo wa umama, Nelly.” “Kweli Billy?” “Kabisa. Huoni jinsi unavyomlinda Jax kwa kila baya?” “Kwa hiyo?” “Huo ndio moyo wa kimama. Umemfikisha Jax pale alipo! Hudhani umefanya jambo zuri?” “Kwa hiyo nisitoe hii mimba?” “Kama ni mtoto wangu tafadhali usimuue. Kama ni mimba ya mwingine, nashauri pata naye muda wakuzungumzia hilo, napo sishauri uue kiumbe kisicho na hatia.” Nelly akanyamaza.

“Twende ukapumzike nyumbani.” “Nikirudi nyumbani ndio pressure itapanda. Acha nirudi ofisini ndio nitaamini sina cha kupoteza.” “Hivi unajua kinachokutokea Nelly?” “Maisha yangu kubadilika?” “Hapana. Yaani sasa hivi hapa tunavyozungumza, ndani ya tumbo lako, kuna maisha ya mtu mwingine yanaendelea.” Nelly akatulia akitafakari. “Yaani ni hivi Nelly, hapo ulipo, ndani yako kuna maisha zaidi yako wewe. Kipo kiumbe kimefichwa na Mungu, anakitengeneza. Kwamba ni hivi, Mungu ameangalia kwa wanawake wote, akakuchagua wewe akiona unafaa kwa kiumbe hicho kukua kwako na wala si mwanamke mwingine. Na Mungu huwa hakosei.” “Unauhakika?” “Kwa asilimia 100. Mungu huwa hakosei Nelly. Kinachoendelea kwako sasa hivi ni mpango wa Mungu kwa asilimia 100. Tulia, mwachie Mungu.” Nelly akatulia.

“Kama kurudi ofisini ndio kutakufanya ujisikie vizuri, basi turudi ofisini.” “Acha nirudi ofisini tu. Ndio nimejua leo, acha nipokee taratibu hizi taarifa Billy. Sijui maisha mengine bila kazi. Kwenda kulala sasa hivi nyumbani na jua kali hivi, presure ndio itapanda zaidi.” “Sawa.” Wakatoka hapo kurudi kazini, Nelly akiendesha mwenyewe Billy amekaa pembeni. “Nimekumiss Nelly, ndio maana nilikupigia.” Nelly akamwangalia. “Mimi nakupenda.” “Najua Billy, lakini na mimi sikujua kama nakupenda mpaka nilipoondoka kwako. Kipindi hiki sijui cha siku 4 mbali na wewe, ndipo nilipojua nakupenda Billy.” Nelly akaendelea.

“Mchumba wa Jax amerudi. Nilipata naye muda yule binti, ndipo nikajisuta.” “Kwa nini?” Billy akauliza. “Aisee upo upendo Billy, na nimejifunza kwa wale watoto! Nilishindwa kulala. Ikabidi kumuamsha Jax jana usiku nikamwambia nakupenda.” Billy akacheka. “Jax alihisi naota. Lakini nikamwambia tumekuwa tukitoka, na nikamwambia alikuwa sahihi. Uko upendo huko nje, ila hatukuwa tumebahatika. Nikamwambia nahisi safari hii nimebahatika. Mimi na wewe tumegombana kwa mimi kutokua tayari kukutambulisha kwake. Jax hakuamini kama upo tayari ujulikane kwa watu.” “Na si kwa watu tu, mama yangu anakufahamu Nelly. Binti yangu mkubwa pia anakufahamu. Nakupenda Nelly, na sitaki kukuficha.” Nelly akamwangalia na kurudisha macho barabarani.

“Unajua nimemwambia mama inawezekana wewe ndiye niliyekuwa nimeandikiwa na Mungu tokea mwanzo?” Nelly akashangaa sana na kumgeukia. “Nakupenda Nelly. Na Mungu anajua nakupenda. Tunakuwa na furaha tukiwa wote. Tunakuwa na wakati mzuri. Unanifanya akili zinatulia, siwi kama mtu unayetegemea niwe kwenye kiwango kikubwa. Umeridhika na mimi kama Billy mwenyewe humtaki Billy mwenye hela au cheo. Nakupenda Nelly.” “Tutafanyaje na huyu mtoto Billy? Hakika mimi sipo tayari na vitoto vichanga. Nahofia kuharibu.” Billy akatulia akifikiria. Akanyamaza kabisa kama na yeye ndio anapata nafasi ya kutafakari juu ya hilo.

“Unataka tuwe wote ofisini?” Billy akavunja ukimya wakati wakikaribia ofisini. “Hapana Billy! Mimi nakwenda kufanya kazi.” “Naruhusiwa kukutembelea nyumbani?” Nelly akanyamaza, hakujibu hilo. Akamuona anatoa simu na kutoa maagizo afuatwe ofisini kwa Nelly. Akajua anazungumza na dereva wake. Akamuacha tu na kuendelea kuendesha mpaka ofisini kwake. Wakaachana hapohapo.

Jioni mida ya saa kumi na nusu akamtumia ujumbe Billy. ‘Nakukaribisha nyumbani. Itakuwa vizuri uje hapa, tuondoke wote.’ ‘Nashukuru.’ Billy akarudisha huo ujumbe akiwa amefurahi sana. Akajua Nelly amepata muda wakufikiria na kuamua.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Saa kumi na mbili kasoro Billy akawa amewasili ofisini kwa Nelly. “Unajisikiaje?” “Kwenda nyumbani. Nifikie friji, nipate barafu, nitafune.” Billy akacheka sana. “Hakika nimekamatika mimi!” “Lakini Nelly, niambie umebakiza nini kwenye maisha?” “Sijui Billy. Ila nafikiri pia sijiamini kama naweza kuwa mama, ila hii kazi. Kuhudumia kiumbe ni ngumu Billy, bora kazi.” “Kwa sababu unauzoefu wa kazi wa muda mrefu ila si kubeba mimba, kuzaa na kulea. Naamini utakuwa tu sawa. Jipe muda.” Wakatulia kama wote wamepatwa na kibumbuazi.

“Twende ukapumzike.” Billy akasimama kabisa. “Lakini Billy, naomba usijisikie kama una jukumu na huyu mtoto. Najua ni kitu ambacho hukupanga. Hata mimi pia sikupanga. Kwanza sikujua kama kwa umri wetu tunaweza pata mtoto. Nimekaa hapa nikiwaza, nikamkumbuka Lara jinsi alivyolilia mtoto wake. Hata jana alimzungumzia kwa upendo. Nimejisuta. Nikajiambia kama mtoto kama yule alikuwa tayari kulea mwanae kwa upendo vile, tena akiwa hana uwezo kama wangu, nashindwaje mimi!” Billy akatulia.

“Unanisikiliza Billy?” Akawa kama amemtoa mawazoni. “Billy?” “Nipo Nelly.” “Najua upo. Na ninaelewa ni jukumu kubwa. Tafadhali usione unawajibika kwa namna yeyote ile.” “Nahitaji na mimi muda, Nelly. Swala la mtoto mwingine halikuwahi  kupita akilini mwangu. Hizi ni habari mpya kabisa, ila siyo mbaya. Ila nahitaji tu muda.” Nelly akanyanyua mizigo yake. “Twende.” Wakatoka hapo, wote kimya mpaka nyumbani kwa Nelly.

Nyumbani Kwa Nelly na Jax.

Akamuona Billy anacheka. “Sasa unacheka nini?” “Hivi unajua kwamba Jax ni baba mkubwa na anakaribia kuoa?” Akamuelewa. “Ila hana mfano wa kuiga au mtu wa kumwangalia ila mimi. Hana nyumbani, isipokuwa hapa. Sijui kama unanielewa Billy?” “Nakuelewa na ndio maana nashangaa jinsi unavyojitilia mashaka kwenye swala la umama. Unaweza Nelly na utakuwa mama mzuri tu.” Wakatulia garini nje ya nyumba, mwishoe Nelly akaona washuke.

“Tuingie nikutafutie chakula kabla hujakwenda kulala. Karibu.” Wakashuka garini, kwa mara ya kwanza Billy akakaribishwa hapo wakati yeye Nelly alikuwa akilala kwake. Akaenda kukaa sebuleni. “Nina wazo la tofauti. Badala ya kupika, naomba tuagize chakula, ili wewe upumzike leo.” Nelly akabaki akifikiria. “Dereva atakileta hapa muda na wakati tutakaomwambia. Niambie unahamu ya  kula nini.” Nelly alikuwa akijisikia kuchoka, akamshukuru Mungu wake. Akavua viatu na kwenda kujinyoosha kwenye kochi. Billy akahamia hapo kwenye kochi, akamnyanyua miguu na kuanza kumchua. Nelly akajiweka sawa na kutulia.

Wakati wapo kwenye ile hali, Jax akaingia. Alikaribia kukimbia, akabaki amedua. Ni Nelly na bosi wa mabosi zake, amepakata miguu ya dada yake akiichua! Kimya kikapita kwa muda, akapitiliza hapo bila salamu mpaka jikoni. “Ulifanikiwa kwenda hospitalini?” Akamuuliza dada yake akiwa jikoni. “Ndiyo.” Nelly akajibu. “Wamekwambia nini?” Jax akauliza kwa sauti ya juu tu. Kimya. “Nelly?” “Ni ujauzito.” Nelly akajibu, wakasikia glasi imeanguka huko jikoni. Kimya. Nelly akajua ameshituka sana. Billy akamuona Nelly anafunga macho kwa masikitiko.

Baada ya muda Jax akatoka jikoni na kurudi pale sebuleni kwa dada yake. “Utakuwa mama mzuri Nelly. Hongera.” Mpaka Nelly akaanza kulia. “Aisee naogopa sana. Iweje nimuharibie kama wewe?” “Kwani wewe ukiangalia unaona maisha yangu yameharibika?” Jax akamuuliza vizuri tu. “Nina kazi nzuri na mchumba mzuri tu, na nimekuahidi natulia. Sasa ni nini unaona kimepungua? Utakuwa sawa kabisa, usiogope, na mimi nipo kukusaidia.” “Kweli?” “Kabisa. Huyo mtoto amebahatika kukupata wewe kama mama. Anauhakika wa kuwa mtu mzuri kwenye jamii na anauhakika wa mtu wa kusimama naye hata kama wengine watamchukia.” Nelly akacheka akijifuta machozi. “Halafu pia amebahatika kupata mjomba mzuri sana. Na Lara atakuwepo. Sema tunaweza kumuharibu kwa kumdekeza.” Angalau wakacheka. Nelly alishashusha miguu vile ilivyokuwa imepakatwa na Billy.

“Mimi nakwenda kulala kwangu. Nimekuja kuchukua vitu baadhi, naondoka.” Jax akawa muungwana, na kuamua kumpisha dada yake. Aliona haitakuwa sawa kwao kama ataendelea kuwepo pale. “Hutakula kwanza?” “Lara amepika. Nitakuwa sawa, asante.” Akataka kuondoka, Nelly akamuita. “Huyu ni Billy, na Billy huyu ni Jax, mdogo wangu.” Wote wakacheka. Jax karudi na kumpa mkono. “Karibu nyumbani.” “Asante.” Jax akarudi jikoni akaenda kumletea dada yake barafu. Nelly akapokea kwa furaha sana. “Yaani nilikuwa nikiziwaza hizi barafu siku nzima!” Akaanza kutafuna. Jax akacheka na kutoka hapo. Akaanza kukusanya mizigo yake tena. Ila Nelly alijua wazi hakuwa na mpango wa kuondoka hapo, akamuacha tu. Akapakia kwenye gari mpaka akamaliza. Akarudi. “Mimi sijui kupika. Niagizeni chakula chochote nikanunue. Nelly, najua anachopenda.” “Tumeshaagiza Jax. Asante.” Jax akaaga na kuondoka hapo akiwapa nafasi.

Kwa Lara.

Lara akashangaa Jax waliyeagana wakikubaliana watapigiana simu wakati wa kulala, anaingia na mizigo yake. “Kwema?” Ikabidi amuelezee Lara. “Mimi naona umefanya jambo la busara Jax. Mpe nafasi na yeye aishi kidogo.” Wakatulia. “Acha kuniangalia hivyo bwana Jax!” Jax akacheka sana. “Mimi mbona sijakuangalia tofauti!” “Hapana Jax.” Lara akanyanyuka kabisa hapo sebuleni na kukimbilia jikoni, Jax akicheka.

“Nenda ukaoge uje kula, au ule ndio ukaoge, ulale.” “Acha nioge kwanza.” Jax akaingia chumbani kwake kwenda kuoga, lakini akatoka na taulo tu. “Jax jamani!” “Mimi nimefanyaje Lara?” “Kavae nguo bwana!” Jax akazidi kucheka. “Mimi nipo sawa kabisa Lara, sina shida na hili taulo.” “Unanitamanisha makusudi, bwana!” Lara akalalamika. “Wewe jikaze mpaka siku ya harusi. Usiwe na wasiwasi.” Lara akaacha kumuangalia. Akaendelea kupanga chakula huku hamuangalii. “Nikusaidie?” “Sitaki Jax, na naomba usinisogelee.” “Kwani wewe unaogopa nini?” “Usije bwana Jax!” Jax akamsogelea na karibu kabisa na kumshika kiunoni.

Lara akamgeukia vizuri. “Nikwambie ukweli Jax?” “Nakusikiliza.” “Ni kweli nakutamani. Sana tu. Tena nilikuwa nikiwa na Jerry, namkumbuka Jax wangu.” Jax akatulia akimsikiliza. “Ila kuna kitu hapa, nakitengeneza kwa shida sana.” Lara akajionyeshea moyoni. “Na si moyoni tu. Nafsini mwangu, akilini au mimi kwa ujumla wangu.” Akamuona Jax anakunja ndita kidogo kama ambaye ameanza kumpoteza. “Natengeneza kitu ambacho nataka kije kuwa msaada hata kwenye ndoa yangu na watoto wangu. Najijengea tabia ya kujiwekea mambo na mimi mwenyewe kuyasimamia mpaka yatimie. Hata katika ugumu vipi, basi nisijipinge. Nataka kuwa na tabia kama mama yangu, Jax. Mama ambaye anasifiwa na msimamo wa mambo. Anayeweza kusimama na mwenzie hata katika magumu.” Lara akajisogeza pembeni.

“Baba akikwambia anajivunia mama, amini Jax. Unamuona vile mama yetu ni mzuri mpaka leo, na nyumba anayoishi au maisha aliyokuwa akiishi na baba kabla sijawafungulia lile duka. Maisha ya chini kabisa. Baba akikwambia wanaume matajiri kwenye ule mji wanamsumbua mkewe, ni kweli. Wanamsumbua mpaka leo wakimpa vishawishi mbalimbali, lakini mpaka sisi tunashangaa Jax! Mama hashawishiki hata kwa zawadi ya gari, Jax! Na ametulia na mumewe hana hata wazo la pili. Sasa ile sio tabia ya kuweza kuiishi kwa kwenda tu kanisani au kuombewa. Ni tabia inatakiwa kujengwa. Kujenga stamina. Kwamba kweli kuna kitu kizuri kabisa. Unahitaji. Na pengine hakina madhara kibinadamu.” Lara akaendelea.

“Kwa mfano kama hivi sisi ni wachumba mpaka wazazi wanajua. Tunatamaniana kabisa, na tunaweza kufanya chochote kile tunachotaka sasa hivi. Lakini si sawa Jax. Si sawa na wala hatuna hadhi ya kuishi maisha ya ndoa iliyotushinda kuifikia tena si kwa ugumu, ila kwa kuchagua kutofikia lengo! Sisi wenyewe tulishindwa kujikaza na kufikia ndoa. Eti leo watu wote wakijua tulishindwa kusimamia mipango yetu sisi wenyewe, halafu eti huku nyuma ya pazia, tunaishi ndoa ambayo tuliikataa! Si sawa mbele ya macho ya wazazi wangu, na Mungu zaidi.” Jax akapoa mpaka mzee akashuka kabisa.

“Samahani Jax. Nataka kuwa mke mzuri kwako au yeyote atakayefanikiwa kusimama na mimi kanisani na kupeana viapo.” “Ni mimi Lara.” “Nashukuru Jax. Basi ujue nataka kujijengea tabia ambayo hata kama kesho wewe unatatizo, hujiwezi kwa uzima au hata mali, basi niwe mtu wa kusimama na wewe. Na sitaki nijifunze wakati huo wa tatizo, ila nijijengee hiyo tabia kuanzia sasa.” Lara akaendelea taratibu tu kama ambaye hajakurupuka, asijue huyo binti alishakalishwa chini na mama yake, akazungumza naye sana tena kwa kituo. Baada ya kugundua hata mkono huo si ajali, alivunjwa na mwanaume. Hakumwambia kama anajua anadanganya. Ila mama Chiwanga akafunga na kumuombea binti yake, mpaka akapata hekima ya kuzungumza naye kwa kituo mpaka vikamuingia Lara moyoni.

“Nimekuwa mtu wa kutoka kitanda kimoja hadi kingine na wanaume ambao wote hawajawahi kunioa. Nimebakiwa na idadi zao tu! Wao wametumia mwili wangu, ndoa wamewapa wanawake wengine, mimi nimebaki na idadi zao pamoja na majina yao tu.” Lara akaendelea. “Naomba nivumilie Jax. Acha nijifunze kuwa na msimamo kwenye mambo yangu mwenyewe kwa kuwa mwenzio sitakudanganya wala sitaona aibu kama wanawake wengine. Mimi nataka ndoa ya kanisani. Na hilo nalijua toka mtoto, halijawahi kubadilika moyoni mwangu. Najua kwa hakika nini nataka. Sasa kwa nini huwa najipinga mwenyewe? Ni kwa kuwa sina huo uwezo. Ndio sasahivi nataka kujifunza kama mama yangu. Katika shida na tamaa zote na uwezo wakuweza kukipata hicho kitu, lakini kama si sahihi, basi niweze kujiambia mwenyewe hapana au subiri.” Jax akajirudisha nyuma kabisa.

“Na si tabia ya kujengwa kwa siku moja kama mama anavyosema. Mama anasema kuna tabia zinajengwa kama vile mwanamazoezi anavyokwenda gym. Ile misuli haitengenezeki kwa siku moja. Anasema kuna siku huwa wanachoka na kukata tamaa. Ila kama lengo ni misuli, unakuta lazima warudi, waendelee na mazoezi mpaka misuli itokee. Na mimi nataka hiyo Jax. Nataka na nimekusudia kuweza.” Jax kimya. “Naomba na wewe ujiulize Jax, kama nikivunja hili kwa kukutamani sasa hivi, nitaendelea kuvunja mangapi kwa wengine.” “Basi nimeelewa, Lara. Tusubiri wote.” Jax akarudi chumbani kuvaa.

Akatoka na kumkuta Lara akimsubiria mezani. Akamuona amepoa hata usoni hamwangalii kwa ujasiri. Lara akamuhurumia. “Nikwambie Jax?” Akamwangalia. “Nyumbani kwa wazazi wangu wanafanya ibada kila siku usiku palepale nyumbani kabla ya kulala. Tunaweza kuanza na sisi.” “Sawa.” Jax akakubali. “Lakini itabidi wewe uniongoze Lara. Mimi ni mkristo jina tu.” Lara akacheka, angalau wakabadili agenda. Wakaanza kuweka mikakati kwenye hiyo nyumba yao.

Kwa Nelly.

Ukweli Billy alikuwa kwenye mshituko kama ambaye hajui chakusema na hawezi kukimbia. Ikawa kama amepigwa tu na butwaa. “Naomba nikwambie kitu Billy.” Billy akatoa macho kwenye luninga, Nelly akijua wazi hakuwa akielewa lililokuwa likiendelea kwani  aliweka kwa lugha ya kiswahili ambocho Billy huweza kuokota maneno machache sana na kutumia akili kuyaunganisha ili kuelewa.

“Hili ni jukumu langu kwa asilimia 100 kwa kuwa ni mimi mwenyewe ndiye niliyeruhusu hili litokee. Kwanza sikuwa nikijua kama watu wa umri wetu tunaweza kushika mimba.” “Usijichanganye na mimi. Wewe bado ni mdogo Nelly.” “Kwa nini wewe unafikiria mtoto atakuwa ni wako Billy!?” “Ni wa nani?” “Siwezi kukwambia.” “Kwa nini?” “Kwa sababu sina uhakika.” Billy akamtizama kwa kumsuta.

“Huyu mtoto si wako Billy.” “Uliniahidi wewe hutanidanganya, Nelly.” Akawa kama amembana. Nelly akababaika lakini akapata jibu. “Mimba zinaweza kushikwa kwa njia nyingi sana. Hata kwa kukaa chooni. Unaweza kukalia mbegu za kiume, ukashika mimba kama ni siku zako za kushika mimba. Kwa hiyo anaweza kuwa mtoto wa yeyote yule.” “Unakumbuka lakini ulivyosema wewe hutakuja kunidanganya?” “Ninachotaka kukusaidia Billy ni kuwa, usijihisi unahusika na huyu mtoto. Usijihisi nimekuingiza kwenye jukumu zito ambalo hukuwa umepanga kuja kufanya tena maishani. Mimi nawajibika kwa hili kwa asilimia 100, nitawajibika. Tafadhali naomba uondoke.” Nelly akambadilikia.

“Unazungumza nini wewe?” “Biashara au mchezo wowote uliokuwa ukiendelea katikati yetu, nausitisha kuanzia sasa. Sitaki tena na ninaomba uondoke.” Billy akabaki akimtizama. “Tafadhali ondoka Billy. Nataka nikaoge, nilale.” “Chakula...” “Sina shida na chakula. Nina viporo kibao kwenye friji. Nikisikia njaa nitakula. Tafadhali ondoka nipate muda wa kutulia. Nijipange kwanza kichwani kwangu, nilale ili kesho niende kazini.” Nelly akasimama na kumfungulia mlango. “Tafadhali usinifukuze Nelly.” “Nakufukuza. Ondoka Billy. Mambo yamebadilika, najhitaji nafsi na akili zangu. Nahitaji muda tafadhali. Naomba nipishe. Nipo kwenye mshituko, kichwa kimevurugika. Nikiendelea hivi, naweza kujikuta leo naenda kulala ofisini. Nikafanye kitu nilicho na uzoefu nacho kuliko hofu niliyonayo sasa hivi.” “Niambie hofu yako.”

“Kubeba mimba. Inamaana nitabadilika kila kitu. Kuanzia kula yangu, vaa na maisha kwa ujumla. Kuzaa. Ni maumivu ambayo sikuwahi kufikiria wala kutamani kuja kuwa nayo. Kingine kuja kushika katoto kachanga! Sijui hata kama nina uwezo huo wa kumtuliza mtoto mkononi, akajihisi anapendwa na yupo salama. Sijui ratiba zangu zitaingiliwa kwa kiasi gani na jukumu zima. Nikisema jukumu zima, namaanisha kuanzia ujauzito mpaka kujifungua na kulea. Nina mengi ambayo natakiwa kuyatafakari na kujipanga.” “Nakuhakikishia hayo yote hayatakupa majibu sasa hivi ila kujipandisha pressure.” “Hata hilo ulilosema nahitaji muda kukaa chini na kulikubali. Kuwa nimeshakuwa mjamzito, nini chakufanya na majibu mengine sitaweza kuyapata sasa hivi. Kwa hiyo nahitaji nafasi mbali na kila mtu ila mimi tu. Tafadhali kwa mara ya kwanza naomba heshimu hilo. Nimeshakuitia usafiri, yupo nje. Tafadhali ondoka.” Billy akasimama na kutoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Tamu Yageuka Shubiri. Nini kitaendelea kwa WOTE?

Usikose muendelezo....

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment