Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Chozi Langu! - SEHEMU YA 20. - Naomi Simulizi

Chozi Langu! - SEHEMU YA 20.

        “Nilikwambia sina shida ya kukosea na wewe.” “Billy!” “Sasa bora lipi Nelly? Tujaribu, tushindwe au tusijaribu kabisa?” “Mimi sijui Billy.” Jax na Lara wakabaki wameshangaa. “Mimi naona ni bora tukubali yote kwa asilimia zote. Maswali mengine yote, yaje yajijibu baadaye. Kama hili la mtoto, hatuna majibu yote, lakini kila siku inajijibu yenyewe. Kama leo umejua hakuna kunywa wine, mpaka azaliwe. Umeacha. Leo itapita, tutakabiliana na kesho tena. Hatuwezi kupanga kila kitu leo wakati hatujui kesho itakuaje. Ninachotaka kukwambia ni kuwa, usifungue milango kwa hofu ya leo, tukashindwa kufurahia leo.” Nelly akatulia.

          “Magoti yanauma!” Nelly akaanza kumcheka. “Nelly!” “Anza tena.” Nelly akamwambia huku akicheka sana. “Kweli Nelly?!” “Juu ya nini?” Nelly akajifanya kama hakumbuki tena. “Unanicheka!?” “Wewe anza upya. Hata sikumbuki kinachokufanya upige magoti hapa ni nini!” Jax akacheka taratibu na kuinama vile dada yake alivyokuwa akimfanyia dhihaka Billy. “Kweli Nelly?” Nelly akazidi kucheka mpaka akainama.

          “Sawa Nelly.” “Usichoke Billy.” “Wewe kwako sitachoka.” “Ona ulivyo mtu mzuri. Haya anza, nakusikiliza.” Billy akaanza kucheka na yeye. Wote wakaanza kucheka. “Si ukubali tu nikuvalishe?” “Nikubali nini?” Nelly akamuuliza. “Sawa Nelly. Acha mimi nianze.” Akajiweka sawa. Mpaka akatengeneza na shati. “Mpigeni picha ili akili yake ikirudi, kiburi kikianza tena, tuje tumuonyeshe huu wakati.” Nelly akafanya Jax na Lara wacheke tena. Jax na yeye akatoa simu yake.

          “Nelly, will you marry me?” “Yes, Billy.” Akataka kunyanyuka ambusu. “Nivalishe kwanza Billy, acha kuruka hatua! Wewe vipi bwana!?” “Acha kwanza nifurahie.” “Hapana Billy bwana! Ujue nitabadili mawazo mimi?” Billy alicheka sana. “Nelly anajua kuniringia!” “Wewe nivalishe pete kwanza.” Akamvalisha ndipo wakaanza mabusu hapo. Nusura Jax aondoke. “Umefurahi?” “Sana. Acha nimwambie binti yangu na mama. Wapo macho wanasubiria kujua kama umekubali.” Wote wakashituka. “Billy?” “Sasa wewe unafikiri ni siri?” Nelly akaanza kujitengeneza.

          Billy na yeye akaanza kumcheka. “Acha bwana Billy!” Billy akachukua simu yake, akapiga videocall, chakushangaza akakuta mpaka baba yake anasubiria. “Amesemaje?” Wote wakauliza kwa pamoja, Billy akaanza kucheka. Akamvuta mkono Nelly akaweka kwenye simu. Wakamsikia binti yake akishangilia. “She said, ‘Yes’.” “Hongera sana Billy.” Baba yake akampongeza. “Asante baba. Lakini usingekesha ukisubiria! Ningekupigia kesho kukutaaribu.” “Nilipomuona Britney amekuja hapa kwa bibi yake na kumuomba wakae naye asubiri ajue kitakachoendelea huko, nikaona niungane nao kusubiri.” “Pole. Lakini nilimwambia Britney asiwe na wasiwasi kila kitu kitakwenda sawa!” Kidogo kama Billy akawa akilalamika kukuta mpaka baba yake alikuwa akisubiria hilo. “Usijali. Tumekuwa na wakati mzuri.” “Basi acha Nelly na mdogo wake wawasalimie.” Billy akamkabidhi Nelly simu.

          Kwa mara ya kwanza Nelly akazungumza na wazazi wa Billy pamoja na binti yake mkubwa. “Ni mzuri zaidi kuliko kwenye picha.” Nelly akamsifia na kumfanya acheke. “Usiwe kama dad!” “Ni kweli. Na nimefurahai kuzungumza na wewe, Britney.” “Nikuulize kitu?” Britney akataka kuweka msisitizo kwenye swali lake akimtaka Nelly kuzingatia. “Niulize chochote tu, karibu.” Nelly akajibu. “Unampenda kwa dhati baba yangu?” Nelly alishituka, akamtizama Billy. Billy akabaki akimwangalia.

          “Nataka kujua.” Akamsikia Britney akiongeza upande wa pili. Mpaka wazazi wa Billy walikuwa kimya. Jax akabaki akimtizama dada yake. Nelly akatulia kama anayetafakari akijua wanamsubiria. Akacheka kidogo, akamtizama Billy na kurudisha macho kwenye simu. Akakuta huyo mtoto ametulia, akisubiria.

          “Labda nikwambie vile ilivyo, pengine utaelewa kwa urahisi.” Akaanza Nelly. “Billy ni sehemu ya maisha ambayo ilikosekana kwa muda wote, na sikuwa nikijua kama kuna kitu nakikosa au nakihitaji mpaka alipokuja yeye.” Nelly akatulia kidogo kisha akaendelea. “Ameongeza maana nyingine ya maisha ambayo sikuwahi kujua kama naiweza kuishi au hata kama nastahili kuipata. Na..” Wakamuona amesita kidogo ila akaendelea. “Naweza nisiwe na lugha nzuri yakueleza, lakini ni mtu ambaye naomba Mungu nisije kuishi hapa duniani bila yeye.” Akamuona yule binti akijifuta machozi.

          “Waw! Jamani dada Nelly!” Akasikika Lara. “Yeah! Nampenda Billy.” Akamwangalia Lara kuweka msisitizo mpaka akatingisha na kichwa. Akarudisha macho kwenye simu. “Kwa hiyo kujibu swali lako Britney, ni ndiyo. Nampenda baba yako. Sana.” “Mimi nilijua tu, lakini ukawa unanibishia.” Billy akaongeza na kufanya wote wacheka. “Thanks sweetheart.” Akamsikia mama yake akisema upande wa pili. Kisha akasogea kwenye simu. “Namaanisha kutoka ndani ya moyo wangu, Nelly. Asante.” Akaongeza huyo mama na kuendelea. “Billy amekuwa akiniambia, na nikatamani kukusikia, lakini sikuwa jasiri kukuuliza kama Britney. Kwanza niliona ni mgeni kwetu, sikutaka kuweka wasiwasi. Lakini nimefurahi kukusikia. He is my baby.” “Sasa hapo mama unaharibu. Nilimwambia Nelly mimi ni kaka mkubwa, mwenye mdogo wangu!” “Dad hakui hapa nyumbani.” Akaongeza mwanae. “Haya kwaherini. Naona mnaniharibia sasa.” Wakazidi kucheka.

          “Love you dad.” “Love you too sweetheart. Ukalale sasa.” “Haya enjoy.” “Billson?” Akasikia baba yake akiita. “Yes, dad.” Akaitika kwa heshima zote. “Hujatutambulisha mdogo wake.” “Ni kweli. Huyu hapa. Ndiye tunayefanya naye kazi.” Akamkabidhi simu Jax. “Wasalimie.” Jax alikuwa ameingiwa na hofu, akapokea akitetemeka. Akawasalimia wote kisha akamtambulisha na Lara. “Mungu akipenda nitamuoa hivi karibuni. Mnakaribishwa.” Akaongeza Jax. “Kweli?” Britney akadakia kwa kuhamasika. “Eti Nelly?” Billy naye akauliza kutaka uhakika wa huo ukaribisho. “Kabisa. Tutapanga vizuri na Billy kisha atawajulisha. Lakini tungependa kuwaona. Karibuni sana.” Wakamsikia Britney anashangilia. Wakacheka.

          “Lakini nafikiri mtaanza safari ya huku kwanza. Kama Billy atakuwa hajabadilika, alisema anataka kuoa kwa haraka.” Nelly akakunja uso. “Sijazungumza na Nelly, baba! Yale yalikuwa mawazo yangu tu.” Billy akajihami. “Oooh! Basi nimeharakisha.” Wakacheka lakini Nelly akabaki akimwangalia Billy. “Usiogope. Tutazungumza.” Wakaagana.

          Nelly akabaki akimwangalia. “Unakumbuka nilikuwa nikikudai kutoka mara ya nne?” “Billy!” “Tulikubaliana Nelly. Najua tumetoka zaidi ya mara nne, lakini naomba kumbuka zangu za makubaliano yetu zilikuwa nne. Tumeshatoka mara tatu. Unguja, Afrika ya Kusini na Kilimanjaro. Ya nne ndio niliwaambia tutakwenda nyumbani, na kama utakuwa umekubali basi ndio tutafunga ndoa. Hii safari ya safari hii sio suprise. Nilipanga kukwambia na tuandae safari.” “Lini sasa?” “Mapema. Hatuna sababu ya kusubiri. Tunakwenda kufanya yote kwa pamoja, kisha tukitoka fungate ndio tuna...” “Hivi wewe Billy ujue unamipango mingi ambayo mimi siijui!” Billy akaanza kucheka kama kawaida yake.

          “Sasa hapo unachocheka ni nini?!” “Kwamba na hili liliendelea kupangwa bila wewe kujua. Hivi nilikwambia ni sawa kuwa sio kila kitu uwe unapanga wewe wakati mwingine ni sawa..” “Acha Billy. Hii natakiwa kujua bwana. Sasa wewe ulifikiri nasafiri vipi bila kupanga likizo yangu!?” “Ningekwambia Nelly. Baba ndiye ameharakisha. Acha wasiwasi. Na utulie usianze kukasirika. Ni jambo zuri.” Nelly akamtizama na kunyamaza.

          “Hongera.” Lara akapenyeza pongezi zake kwa hofu. Nelly akacheka na kuitizama ile pete. “Umeipenda?” Billy akauliza. “Ni nzuri, asante Billy.” “Karibu na nimefurahi kwa kuwa umeipenda.” “Na Lara, asante kwa pongezi. Ila nawashukuru sana.” Lara akawa hajaelewa. “Nyinyi mmenifanya kuamini kama kuna kupendana. Na Jax naye alinifanya...” “Badili lugha, Nelly!” Billy akamlalamikia. “Sio lazima kila kitu kusikia.” “Acha Nelly.” “Hujapitwa bwana. Nilikuwa nikimwambia Lara na Jax kuwa wao wamekua sababu ya kukukubali. Wameweka mfano mzuri wa mapenzi, katika shida zote walizopitia, bado wamethibitishia kila mtu kwamba, kitu walichonacho ni cha thamani kutunza kiasi chakuweka hisia zao pembeni na kurudiana kwa ajili ya hicho kitu.”

          “Ndipo Jax aliponionya juu yako, niache kuwa mkorofi, sio kila mtu ni mbaya, ndipo na mimi nikajiambia nijipe nafasi, pengine naweza kukipata hicho Jax alichokiona au kukipata kwa Lara. Kwa hiyo nawashukuru kwa kuweka mfano mzuri. Japo nyinyi ni wadogo kwangu lakini mmenifundisha kitu.”  Simu ya Billy ikaanza kuita. Wakamuona ameiangalia na kucheka. “Mama bado hajalala huko!” Akaongea Billy huku akicheka na kupokea.

          “Hongera sana. Mama amenimbia.” “Nilimwambia alale.” Akamjibu kaka yake. “Alikuwa na wasiwasi mpaka nikaenda kukaa naye leo jioni kidogo kumtoa mawazo kwako. Hongera sana.” “Nashukuru Mungu. Naamini safari hii na mimi nitapumzika.” Wakamsikia Billy akicheka sana baada ya kusikiliza. Mara akaangalia tena simu. “Beila naye anapiga. Mama atakuwa anakazi ya kutangaza tu! Acha nimuunge.” Billy akamwambia Brandon, kaka yake. Akaishia na kumuongeza mume wa Beila pia. Vikajaa vicheko kwa ndugu hao wakimpongeza Billy. Nelly akashangazwa sana kugundua kumbe upande wa pili huko wote walikuwa wakisubiria kuvalishwa kwake pete! Akabaki ametulia, akapotelea mawazoni.

          Akasikia Billy akisema yupo hapa mwenyewe. Akamkabidhi simu. Nelly akajikaza na kuipokea. Wakamsalimia na kumpa pongezi. Nelly akamtambulisha na Jax, Jax naye akamtambulisha Lara, ndipo wakarudisha simu kwa Billy. Wakazungumza ndugu hao na kuwaaga.

          “Nyinyi kwenu mnaonekana ni watu wa familia!” Nelly akaongeza. “Ni mama huyo. Mama ndiye anapenda kufanya jambo la mmoja ni kama la kila mmoja kwenye familia. Mume wa Beila alikuwa akishangaa, mpaka sasa hivi namuona yeye ndio amekuwa kama mama!” “Nimemsikia. Anaongea kuliko hata kaka yako!” Nelly akaongeza. “Sasa akitoka hapo, ujue yeye anaenda tena kumpigia simu mama na kumwambia kila kitu.” “Tena?” “Nakwambia yeye ndio yupo karibu na mama kuliko hata Beila mwenyewe. Lazima kila siku wazungumze na mama. Na huwa hawana agenda mpaka tumeshawazoea. Wanaweza kupigiana simu juu ya jambo hilo, wote mkachoka, lakini wao ndio likawapa sababu yakuwa kwenye simu hata zaidi ya dakika kumi wakilizungumzia hilo jambo tu.” Wakazungumza mengi wakifahamiana zaidi  na kula na kunywa ndipo wakaagana. 

Safari ya Ukweni.

N

elly na mdogo wake pamoja na Lara waliondoka nchini na mwenyeji wao Billy kuelekea nchini Uswiz, wakiwa wanasubiriwa na familia nzima. Lara alifurahia sana hiyo safari. Hakuwa akiamini kama na yeye yupo safarini. Tena anapokwenda kulihisika ni pa wenye heri! Alijawa furaha akasahau hata mambo ya harusi yake ila harusi ya wifie. Maana ilikuwa ndio wanakwenda kufunga ndoa kabisa, yaani wakirudi wanakuwa walishafunga ndoa.

 Yakawa mapokezi mazuri mno. Watoto wa Billy, Britney na Briana, wote walikuwepo. Ila ni kweli hata Nelly alihisi huyo mdogo, Briana ni kama amelazimishwa kuwepo hapo. Alimuonyesha dharau za waziwazi Nelly. Na hata alipompa mkono, hakutaka kushika mkono wa Nelly. Billy aliona, ikamuuma sana, ila binti yake mkubwa akaingilia kati kwa haraka kwa kuushika yeye mkono wa Nelly. Muda mwingi alikuwa kwenye simu. Hata alipoongeleshwa, alijibu macho kwenye simu yake.

Walikuta vyumba viwili vimeandaliwa kwa ajili yao, hapohapo nyumbani kwa kina Billy. Yaani kwa wazazi wake. Walionekana watu wazima lakini waliostaafu wakiwa na pesa. Weusi hao waliishi kwenye mtaa wa kitajiri sana. Nyumba kubwa nzuri na ya thamani. Akajua ndiko alikotolea maringo yake huko. Alitokea kwenye familia yenye uwezo.

Mama yake aliandaa chakula cha watu wote jioni hiyo, kama kuwakaribisha wa kina Nelly kwenye familia. Walikuwa ndugu tu. Nelly akapata nafasi yakuwaona wote na watoto wao. Bado Briana, mtoto wa Billy akawa akifanya vituko vya kukera kila mtu, na wenyewe wakawa kama wanamuogopa. Akijibu vibaya, wananyamaza tu, hakuna anayeweza kumuongelesha. Ila Nelly akamuona Billy amebadilika.

Wakati wanaandaa chakula na kuweka mezani, akamsogelea Nelly huko jikoni kwani Nelly alivutiwa jikoni na Beila mdogo wake Billy anayemfuata, mtoto wa kike wa pekee hapo kwenye hiyo familia. Dada mtu mzima tu, mkubwa hata kwa Nelly. Beila alipotoka tu hapo na mama yake kufuatilia kitu upande mwingine wa nyumba ndipo huyo binti mdogo wa Billy, Briana akamsogelea. “Kwa nini unataka kuolewa na baba yetu?” Kabla Nelly hajajibu, akaendelea. “Maana wengine wanampendea pesa. Wengine wanataka tu kuitwa jina lake. Sasa wewe unataka nini kwake?” Alikuwa binti mzuri sana kwa kumtizama. Nadhifu lakini alijawa kiburi na dharau mpaka akikutizama unaweza ukajishuku. Sasa akakutana na Nelly, dakika kadhaa mbele. Kwanza hakupenda jinsi alivyomuuliza. Alibaki akimtizama, akifikiria jibu la kumpa huyo mtoto ili asiharibu hapo ukweni, maana alishamkera Nelly mpaka mwisho.

“Nelly!” Billy akaingia hapo bila kutarajia. “Huna haja ya kujibu hilo. Twende.” Billy akanyoosha mkono. Nelly akasimama akataka kutoka, lakini walipofika mlangoni akamwachia Billy mkono na kurudi karibu na yule binti, kwa karibu kabisa, wengine wote waliokuwepo pale jikoni wakawa wamepigwa na butwaa.

“Mbali na pesa. Jina na mengine mengi yaliyokuwepo kwa baba yako. Ukitulia. Ukampa nafasi, ukimtenga na mengine mengi hata mapungufu yake, utagundua katikati ya yote hayo na hata uliyoyataja, ndani yake yupo mwanadamu anayestahili kupendwa yeye kama Billy. Wakati mwingine jaribisha na wewe, utagundua yeye ni zaidi ya pesa, cheo na jina lake.” Jeuri Nelly akampaka kama sekunde 10 hivi kuhakikisha hana swali la nyongeza, akimwangalia machoni kisha akaondoka hapo kumfuata Billy pale alipokuwa akimsubiria kwenye mlango wa kutokea pale jikoni. Ukweli Billy alifurahi sana. Waliacha pale jikoni wote wamesimama kwa mshangao wakimtizama yule mtoto wa Billy.

“Mnashangaa nini sasa?” Akawauliza kwa hasira, bibi yake akaingia. “Kila kitu kipo sawa hapa?” “Wewe unafikiria nini?” Akamjibu hivyo bibi yake na kutoka. Ikaanza minong’ono huko jikoni. Chakula kikaandaliwa na kuwekwa mezani. Watu wote wakaitwa hapo mezani. Huyo binti akaja hapo mezani wa mwisho na simu yake mkononi. “Diva ameingia.” Junior, kijana wa Beila, dada yake Billy akarushia neno. “Nani unamuita Diva?” Wakaanza kubishana wao wawili mbele ya wazazi wao. Junior na Briana.

“Kwanza mimi wangeniambia wewe utakuwepo, nisingekuja.” Akaongea Briana. Billy akaweka uma na kisu chini kwa nguvu. “Huna lazima ya kuwepo hapa Briana.” Kila mtu akashituka mpaka Briana mwenyewe aliyezoea kubembelezwa na baba yake. “Umenisikia na kunielewa?” Billy akauliza kwa ukali mpaka wote wakatulia. “Huna sababu na hulazimishwi kuwepo hapa. Hii ni familia moja, tumekutana kujenga si kubomoa. Kama wewe unajisikia shida kuwepo katikati ya hata mmoja wetu hapa, dereva atakurudisha kwa mama yako.” Mpaka Britney akashangaa.

“Yote haya ni sababu ya kumuuliza swali dogo tu huyo Nelly?” “Hivi karibuni ‘huyo Nelly’ anakuwa mke wangu na yeye atakuwa mama wa mtoto wangu.” Wote wakashituka. “Sitaruhusu yeyote kati yenu amvunjie heshima. Ukiona umeshindwa kumuheshimu, ondoka.” Pakazuka ukimya, Briana akasimama kwa hasira na kuvuta pochi yake. “Na Briana.” Baba yake akamuita kabla hajaondoka. Akageuka machozi yakimtoka. “Huna sababu yakuja hata kwenye harusi yangu. Na ninakuahidi sitakusumbua tena.” Hiyo ilikuwa habari kubwa sana kusikika kwa kila mtu.

Briana mwenyewe alionekana kuingiwa hofu. Akasimama pale kwa muda. Akamtizama babu yake kama anayetaka amtetee lakini ikawa kinyume. “Dereva atakuwa tayari utakapokuwa tayari kurudishwa kwa mama yako.” Watu wote kimya, Lara akabaki kuangalia waafrika hao uzunguni. Wote walionekana wamestaarabika sana. Watoto wengi waliokuwepo hapo kasoro ya hao binti za Billy, walichanganya damu ya kizungu. Na vile wazazi wao walivyokuwa weupe, walibeba rangi nyeupe zaidi. Lara na Jax kimya wakisikiliza na kuangalia ya uzunguni.

Briana akasimama kwa muda, chakushangaza wakamuona amerudi kukaa. Pakazuka ukimya kwa muda, kila mtu akarudi kula. “Billy?” Baba yao akaita, Billy akaitika. “Umesema Nelly ni mjamzito?” “Ndiyo. Amemaliza mwezi wa nne.” Kila mtu akashangaa. Hapo ndipo Briana akanyanyuka na kuondoka kabisa. Hakuna aliyetegemea Billy kupata mtoto tena. Nelly akabaki ameinama.

“Hongereni.” Akadakia mama yao. “Nelly, hongera sana.” Akaongeza akimwangalia Nelly. “Asante.” Ndipo sasa wengine wakaongeza pongezi na utani. “Mbona wewe Britney hushangai?” “Dad alishaniambia.” Nelly akashangaa na kumtizama Billy. Billy akaanza kucheka. Akatamani amwambie kitu, lakini kila mtu alikuwa akiwaangalia. “Wewe sema tu.” Billy akamkejeli akicheka sana. “Mimi sina usemi Billy.” Akamjibu kama anayemwambia tutaonana baadaye.

Wakamaliza kula wakizungumza na kucheka, hakuna hata aliyekumbuka swala a Briana. Lakini Nelly alikuwa amechoka sababu ya safari, akataka awahi kwenda kupumzika. Wakatoka hapo wote wanne. Lara na Jax na wenyewe wakawa wameshatosheka kwa siku hiyo. Wakaamua kwenda chumbani kwao wakatete ya uzunguni.

Maandalizi ya Harusi.

Mama, dada na shemeji yake Billy, huyo mwanamke wa kizungu aliyeolewa na kaka yake Billy wakataka kumsindikiza Nelly kutafuta gauni la harusi. Ikamgusa sana Nelly. Wote walikuwa ni watu na majukumu yao tena mazito. Lakini wakaahirisha na kuamua kumsindikiza yeye! Hilo likamfurahisha na kumgusa sana Nelly. Lara naye akaomba kuongozana nao. Wakiwa kwenye hilo duka la nguo za harusi, Nelly akitafuta gauni lake, Lara naye akaona gauni alilopenda sana. Nelly akamuona kila wakati analishika. Anazunguka, lakini anarudi palepale kwenye lile gauni. Analiangalia. Anajiweka nyuma yake. Akiangalia bei, anaondoka. Nelly akamuona amefanya hivyo kwa muda mrefu tu, akirudiarudia.

“Kama umelipenda, si unajua unaweza kwenda kujaribu kwa kulivaa kabisa sio hivyo unavyosimama nyuma yake?” “Naona kama tamaa! Nimevutiwa na haya manyoya ya tausi walivyoyapanga vizuri kwenye gauni zima! Sijawahi ona kitu kizuri hivi, kilichotengenezwa kwa ustadi wa hali ya juu! Nimelitamani japo bado ninalo lile la mwanzoni.” “Wewe nenda kajaribu, ulinganishe. Nakuona umeshindwa kutoka hapo.” “Kweli nimependa. Ila bei!” “Huyo Jax anamajukumu gani ya kushindwa kununua gauni la harusi? Kama atashindwa kununua gauni lako, basi aache kazi!” Wakaendelea kuzungumza wawili hao kwa lugha ya kiswahili, na wenyeji wao wakiwa sehemu ya kusubiria.

Lara akachukua lile gauni na kwenda kujaribu. Akatoka kwenda chumba cha pili alichokuwepi Nelly. “Asipolinunua hilo gauni Jax, mimi nitakununulia. Umependeza sana, Lara. Sana.” “Ila ni garama!” “Wewe mtoto mbona unapenda kujiliza shida? Si nimekwambia nitakununulia mimi?” Lara akacheka kwa wasiwasi. “Asante wifi yangu.” “Naona umefurahi mpaka umeweza kuniita wifi!” Lara akacheka kwa furaha. Hakuamini kama hilo gauni ndio limekua lake. Nelly akarudi ndani kujimalizia kuvaa.

“Eti mimi naona umependeza na lile gauni la pili!” “Hata mimi naona hivyo, ila hawa wakwe wanataka kuanza kunichanganya. Sasa acha nitoke hapa hii ndio itakuwa mara ya mwisho kabla sijawabadilikia.” Lara akaanza kucheka, alimjua Nelly. “Kwanza hata hili sivai. Nimechoka mimi.” “Jikaze umalizie ukawaonyeshe mara ya mwisho. Unaweza kupendeza zaidi.” “Na wewe usiwe mtu wakuyumbishwa!” Akamjibu na kuendelea kuvaa maana alitaka kuvua.

Mpaka wanarudi nyumbani, Lara naye akawa amenunua kila kitu kipya cha harusi, Nelly ndiye aliyekuwa akimnunulia bila hata kujali pesa. Na Nelly naye akapata nguo nzuri sana, na ya hali ya juu.

Harusi ya Billy na Nelly.

S

iku ya harusi akiwa kwenye chumba alichokuwa akikitumia kwa kulala yeye na Billy watu wakimpamba tayari kwa harusi, hata Lara alikuwepo pamoja na hao watu wanao watengeneza  hapo kwenye hicho chumba. Billy alitaka kaka yake ndiye amsimamie, akamwambia na yeye Nelly yupo huru kumuomba yeyote yule amtakaye amsimamie. Nelly asiye na marafiki na hakuwa na mpango na yeyote, akamuomba mkewe huyo kaka yake Billy na yeye amsimamie. Dada wa kizungu akakubali bila shida. Tena alifurahi na kusema yeye anaichukulia kama ni jambo la heshima kwake.

          Billy akataka harusi yao ifungwe nyumbani kwao tu. Kwa nje kwenye ua. Kwani msimu huo wa ‘Spring’ nchi hiyo maua yalishakuwa yamechanua vizuri sana hapo nje kwao. Nelly hakuwa na shida wala ndoto za harusi sijui ufungwe kanisani, avae shela kama Lara! Akakubali bila shida. Nalo hilo likamuongezea sifa kwa Billy kwamba ni mwanamke asiye na makuu, kumbe hakuwa hata na mipango mingine aseme abishe. Msimamizi wake yeye akasema wao waanze kutengenezwa hapo, angefika mwishoni kabisa kwa kuwa yeye hakutaka kutengenezwa sana zaidi ya uso tu.

          Siku hiyo nyumba hiyo ilijaa hekaheka tokea siku iliyopita, wajukuu wote walishafika hapo tokea asubuhi wakapata kifungua kinywa wote na wazazi wao, pamoja na bibi na babu yao wenye nyuma, kasoro tu Briana hakuonekana. Hawakushangaa. Watu wa chakula, mapambo, keki, picha kila mmoja akileta lake tayari kwa harusi jioni hiyo, wakaongeza hekaheka ndani ya hiyo nyumba. Beila alikuwepo hapo chumbani kwa wifi yake akipambwa, kuangalia mambo yanavyokwenda na mama yao. Wachangamfu yeye na mama yake. Wakaongea hapo wakicheka, wao wakatoka kuangalia mambo ya chakula na keki. Billy, kaka yake na baba yao walikuwa nje wakiangalia mambo yanavyoenda upande wa tafrija watakapofungia ndoa, wakatafuta sehemu wakakaa kabisa wakiongea na kucheka.

          “Hii familia kwa kucheka jamani! Hawachoki!” Lara akamsikia wifie akishangaa kwa sauti ya chini kidogo akiwa anatengenezwa nywele. Walimuanza kichwa. Lara akacheka, Nelly akamwangalia kupitia kioo. “Unamsikia Billy lakini huko chini? Yaani sauti yake inasikika mpaka huku juu, kama kaka yake!” “Halafu wanafanana wote. Baba, mama na watoto wao pia!” “Mpaka hao waliochanganya na damu ya kizungu, wote wanafanana! Nilimwambia hilo Billy.” Wakaendelea kuteta kiswahili, wapambaji wao wakiendelea wasielewe ni nini wanaongelea. Lara alishamuona wakati mwingine Nelly akicheka akiwa anamsikia Billy akicheka kwa sauti. Alikuwa akimwangalia Nelly asiamini kama ni yeye.

          Katikati ya yote hayo mlango ukafunguliwa kwa nguvu mpaka wakashituka. Briana na mama yake wakaingia. Nelly alimtambua kwa kumfananisha na wanae. Na kwa jinsi walivyoingia kwa shari, Nelly akajiweka sawa. “Naombeni nyinyi mtoke, ninataka kuzungumza na huyo.” Nelly akapandisha nyusi zote juu, na kujiweka sawa akimtizama kupitia kioo wakiwa wamsimama nyuma yake. Maana alionyeshea kidole wengine wote watoke, abakie Nelly tu. Wakatoka. Nelly kimya akiwatizama.

Wanasema Mswahili Atakunyima Chakula Lakini Si Neno.

          “Nimetafuta habari zako huko Tanzania, nimejua wewe ni tapeli. Umemdanganya Billy kama ni mjamzito ili akuoe.” Anele akaanza. “Umembambikizia mimba isiyo yake ili akuoe.” “Hilo unalizungumza kwa kuwa alikunyima wewe mtoto wa tatu ndio unafikiri hawezi kwa mwanamke anayempenda?” Nelly akamuuliza taratibu tu na kugeuka akizungusha kiti alichokuwa amekalia. Hilo likamuuma sana Anele lakini akajikaza. “Nakujua wewe ni tapeli. Na sitakuruhusu umtapeli Billy. Kwanza hata ufanye nini ni baba wa watoto wangu daima. Siwezi kukubali umdanganye. Uchukue urithi wa watoto wangu.” Nelly akamshangaa sana pale moyo wake ulipo. Kwenye mali za Billy tu!

          “Umeingia kwenye hii familia kuitapeli. Unataka kunitoa mimi ili ubakie wewe kwenye picha, unufaike! Sasa habari zako ninazo, na nitawaambia wote.” “Tutakutangaza, wote wakujue. Ulimkuta mama, na huwezi kumtoa.” Akadakia Briana. Mmoja wa anayewatengeneza hao wasimamizi wa harusi na biharusi alipotolewa hapo chumbani na Anele akaenda kwa haraka kumtafuta Beila anayefahamiana naye na ndiye anayewalipa kwa hiyo kazi.

          Lara naye wala hakusubiri nje ya mlango, moja kwa moja akarudi chumbani kwao alipokuwepo Jax, aliyekuwa akifanya kazi kupitia kompyuta, kana kwamba ni siku ya kazi. Baadhi ya wafanyakazi wenzake Billy walishafika nchini hapo siku iliyopita, wakiwa hotelini na wake zao wakisubiria muda ufike, waje hapo nyumbani kwao kwa harusi. Jax hakuwa na mtu mwingine wa kualika. Ingekua kipindi yupo kwenye mahusiano na Tino angemualika, lakini hawakuwa kwenye maelewano. Hata hakumshirikisha kama Nelly anaolewa. Na ofisini kwa Nelly viongozi wenzake wawili ndio walifika hapo nchini kuhudhuria harusi. Na walishawasiliana na Nelly kumtaarifu walishafika hotelini na wake zao wanasubiria tu muda wasogee hapo nyumbani.

          Yule mpambaji alikimbia mpaka upande aliokuwepo Beila na mama yake wakiangalia jinsi wanavyopanga upande wa chakula na keki. Walipomuona akija vile. Wote wakaingiwa na wasiwasi. Mpaka kina Billy upande mwingine walipokuwa wamekaa na baba yao, pamoja na Brandon wakashangaa. “Kuna nini!?” Beila akamuuliza. Alikuwa ni mwanamke mweusi wa hukohuko, anayejua kutengeneza nywele za wanawake weusi na alishawafanyia hiyo kazi mara nyingi tu, anaifahamu hiyo familia vizuri tu. “Anele ametutoa sisi chumbani yupo na yule binti yake mdogo, amesema anataka kuzungumza na Nelly. Sidhani kama ni kitu kiz..” “Subiri kwanza. Umesema Anele?” Billy akasikia na kusogea.

           “Yupo kwenye kile chumba yeye na Briana. Wana...” Billy akatoka hapo kwa haraka bila kusubiria amalizie na Beila naye akafuata kwa haraka. Kaka yake na baba yake wakaangaliana na kufuata. Mama mtu naye akaunga msafara.

          “Nashauri usogee kwenye kile chumba cha dada yako.” Jax akatoa macho kwenye kompyuta na kumwangalia Lara akiwa amekunja uso. “Nahisi Briana na mama yake wamemfuata kishari. Maana wametuambia sisi tutoke wanajambo wanataka kuzungumza naye. Sasa wewe unamjua Nelly, atawabadilikia hapa uzunguni, mpaka washangae.” Jax akaruka na kutoka hapo, mbio. Alimjua dada yake. Akaona akaokoe jahazi kabla hawajazijua rangi zote za dada yake.

          Baada ya muda mfupi wakajikuta humo ndani ya hicho chumba mpaka watoto wao nao wakaingia hapo wakiwa wameitana wote. Chumba kikawa kimejaa. “Ni nini kinaendelea?” Billy akauliza akimwangalia Anele. Kimya. Anele hakutegemea uvamizi wa namna ile. Akawa yupo kwenye mshituko kidogo. Kimya. “Nataka kujua unachotaka kuzungumza na Nelly kiasi cha kujiiba kuingia humu ndani?” “Mami hajajiiba kuingia humu ndani. Tumeingilia...” “Wakati mwingine ninapozungumza na mama yako, ukaingilia, utajuta Briana. Wewe huna adabu na heshima.” “Hajui ni wakati gani wa kunyamaza wala kuongea!” Akadakia dada yake aliyekua na yeye kwenye moja ya chumba anachotumia kila akiwa hapo kwa bibi yake, hata usiku huo alifikia na kulala hapohapo, alikuwepo mida hiyo akijitengeneza mwenyewe kwani na yeye alikuwa msimamizi wa harusi hiyo ya baba yake. Mmoja wa bradesmaids. Lakini aliposikia kelele ndugu zake wakiitana kwenye hicho chumba, na yeye akaacha kila kitu na kwenda.

          “Kila wakati anataka yeye tu ndio awe anasikilizw!.” “Sio kweli na wewe Britney. Unafiki tu. Unamwacha mama yetu..” “Sina muda wa kujibishana na wewe Briana. Dad akizungumza, nyamaza kwanza.” “Narudia tena swali langu Anele. Ni nini hicho ulichokitaka kukizungumza?” Wote kimya, macho kwa Anele kama aliyefumaniwa kwenye kitanda cha wakwe.

          “Waambie mami, kile ulichochunguza juu ya huyu mwanamke.” Briana akamwambia kwa sauti ya chini kama kumtia moyo. “Usiogope. Sema mami.” “Usimuite Nelly, huyu mwanamke. Anaitwa Nelly. Ukishindwa kumtamka, acha kuzungumza chochote kinachotakiwa kumtambua yeye kama Nelly.” Isivyo kawaida ya kumuona Billy akizungumza hivyo kwa watoto wake, zaidi huyo Briana, safari hii akasikika akiongea kwa ukali. Wote kimya wamejaa kwenye hicho chumba.

          “Mami?” Briana akaita akisikika kumtia moyo mama yake aongee tu. “Nilitaka tuzungumze tukiwa tumetulia.” “Sisi wote tumetulia hapa. Wewe uongea.” Billy akasisitiza. “Labda ningezungumza na Billy kwanza.” “Katika hili sitakuruhusu. Kwa sababu ulinifuata hapa. Ukatoa watu wote humu ndani, ukionyesha huwezi kusuburi mpaka uzungumze na mimi, tena sasa hivi. Ukawa ukinimbia ni uchunguzi ambao umefanya juu yangu, utakuja kuwaambia wote. Sasa nafikiri hawa ndio watu ambao ungetaka kuwaambia juu yangu kabla hatujafunga ndoa na Billy. Wote muhimu kwa Billy, na Billy mwenyewe wapo hapa. Tafadhali zungumza Anele. Mimi huwa sichelewi popote, sitaanza leo kwenye siku yangu muhimu.” Nelly akaongea kwa jazba kidogo.

          “Ni uchunguzi gani ulifanya juu ya Nelly? Na ulifanya wewe kama nani!?” Akauliza kaka mkubwa. “Asante Brandon! Maana na mimi ni swali lililokuwa likiendelea ndani ya kichwa changu! Wewe kama nani?!” Beila naye akadakia na kuuliza. “Ni mama yetu! Mnawezaje kuuliza hivyo!?” “Mama yenu nyinyi, ndiyo. Lakini anahusika vipi na maisha ya Billy!? Billy anaruhusiwa kufanya maamuzi za maisha yake vile atakavyo!” “Mami anataka mtu asichezee mali za dad, kwa kuwa ni urithi wetu!” Briana akatetea na kuzidi kumuanika mama yake, asijue inasikika vibaya sana.

          Billy akaumia sana. “Yaani wewe mpaka leo bado unalinda mali zangu tu!?” Billy akamuuliza kwa kushangaa sana. “Subiri kwanza Billy. Wewe wakati unaolewa na Billy, nani alikuchunguza?” “Si kwakuwa mimi ni mkewe na nina watoto wawili kwa Billy! Ninawajibika na maisha ya Billy kwa sababu ni baba wa watoto wangu! Acheni kuzungumza kama ambao hamuelewi mambo!” Anele akaongea kwa ukali.

          “Wewe ulivyoachana na Billy si uliomba mahakama mgawane mali sawasawa na Billy, mpaka nyumba iliyokuwa ya kwake Billson, uliichukua wewe ukidai kwa kwa unabaki na Briana?” “Nyumba ilikuwa yetu. Si Billy peke yake.” Akarekebisha Anele. “Vyovyote vile unavyotaka kujiaminisha. Billy alikubali kukupa kila kitu ulichotaka kwa kwa sababu ya Briana aliyetaka kubaki na nyinyi akidhani ni mapenzi, asijue ni maneno yako ya sumu unayomuingiza juu ya baba yake, ili abaki na wewe, uendelee kutumia hata kidogo ulichombakiza nacho Billy!” Brandon akaongea kwa kuumia mpaka akashangaza wote. Hawakuwahi kuzungumzia hilo.

          “Unadanganya mbele ya watoto wangu, Brandon. Na sitakuruhusu.” “Kila mwenye akili ya kufikiria, anajua unamtumia Briana, kuendelea kutumia pesa ya Billy. Wewe na Carlos mnaishi maisha yasiyo na kutafuta pesa kwa bidii kwa kuwa mnajua Billy yupo na anaendelea kuwatunza nyinyi wote watatu.” “Unamsingizia mami!” “Sweetheart, nani huwa anakutuma kuomba pesa kwa baba yako?” Baba yake mkubwa akamuuliza kwa utulivu tu. “Ni mami kwa kuwa yeye ndiye anayehusika na bajeti nzima, kuanzia ada ya shule mpaka..” “Wewe unajua ada yako ya shule ni kiasi gani?” Shangazi yake akapenyeza swali kwa haraka. “Acheni kumuhoji mwanangu ili kumchanganya!” Anele akaongea kwa hasira.

           “Hilo ni swali rahisi sana, ambalo yeye kama msomaji anatakiwa kujua.” Dada yake akachangia. “Sio swali gumu. Jibu Briana.” Britney akaweka msisitizo. “Hayakuhusu.” “Hasomi huyo. Ameacha chuo.” Mtoto wa kiume wa Beila nyuma akasikika. Wote wakamgeukia. “Muongo. Anadanganya.” Briana akadakia kwa haraka. “Rafiki yake waliyekua wakichukua naye madarasa ya ijumaa, asubuhi ameniambia Briana mwenyewe amemwambia ameacha chuo, sababu ilikuwa asubuhi sana. Yeye sio mtu wa kudamka. ‘She is not a morning person’. Abishe nimpigie simu sasahivi rafiki yake, athibitishe. Mwenzie anaendelea.” “Au aingie kwenye Student Portal yake amuonyeshe dad matokeo yake ya muhula huu.” Britney akatoa wazo rahisi na uhakika.

          “Toa simu yako unionyeshe.” Billy akamgeukia Briana. “Lakini nimemwambia mama nitarudi muhula ujao.” Briana akajitetea akisikika amekamatika. “Na ada anayonidai mama yako pamoja na garama za chuo!?” Billy akauliza akimtizama Anele. “Unamsingizia mami sababu ya kutaka kuoa! Mami hadai ada tena, kwa sababu anajua siendi chuo, alinikubalia nirudi nitakapokuwa sawa.” Billy akabaki akimwangalia Anele. “Si umemsikia mwenyewe anarudi chuo mwakani? Sasa si bado pesa itahitajika?” Anele akamuuliza Billy kwa kumshangaa.

          “Mnachezea pesa ya Billy nyinyi watatu nyinyi!” Brandon akaongea kwa kusikitika sana. “Wala Carlos haishi na sisi siku hizi. Carlos alishaondoka. Mnamsingizia mami mkidhani anataka kutumia pesa na Carlos.” Briana akaendelea kumtetea mama yake asijue ndio anatoa siri za kwao. “Sikukwambia mimi mama kuwa Carlos hayawezi mahusiano na ndio maana hata mimi sikumtaka anioe?” Beila akadakia kwa haraka. “Nilisema mimi. Mwacheni tu huyo Anele aende kwa Carlos. Mimi namjua Carlos kwa kukua naye, wala si kusimuliwa.” Beila akaongeza.

          “Carlos alipotaka kunioa mimi, akaja mpaka hapa kwa mama akimuomba anibembeleze anioe wakati ule nipo intern, kabla hata sijamaliza shule yangu ya udaktari, nilimwambia mama. Carlos ni muoga wa majukumu hawezi kuwa mume wa mwanamke yeyote yule zaidi mimi.” “Ni mtu mzuri na alikuwa akinipenda sana.” Akaongeza Briana akinitetea. Beila akamtizama na kuendelea. “Wakati ule alionekana anawaweza na kuwapenda watoto wa Billy, kwa kuwa Billy mwenyewe alikuwepo kwenye picha akifanya yote, yeye kuwepo kuwakilisha kwenye matukio ambayo mwenzie ndiye halali kwa kuyagaramia. Bithday zao hawa, yeye ndio alikuwa mstari wa mbele kuwakilisha, kwa kuwa Billy mwenyewe alikuwepo kugaramia kwenye mahoteli ya garama mama yao aliyokuwa akiyachagua.” “Sio mimi ni watoto wenyewe ndio waliokuwa wakitaka birthday zao zifanyiwe huko. Acheni kunisingizia.” “Wewe ni mama wa namna gani unayesema ‘ndiyo’ kwa kila kitu mtoto anachotaka? Unafaida gani ya kuwa mama kama unashindwa kuongoza wanao kwenye njia sahihi? Acha kuzungumza kijinga hapa.” Akauliza mama Brandon kwa hasira.

          Kimya, Beila akaendelea. “Haya, hospitalini yeye Carlos akawa mstari wa mbele kuonyesha anajali watoto wa Billy kuliko baba yao, wakati Billy ndiye aliyekuwa halali akifanya kazi mchana na usiku ili kufanya watoto wake wawe wanauwezo wa kuonwa na madaktari wazuri hapa nchini. Haya tena, nyumbani kwa mwenzie ndio ikawa kituo, kutwa yupo pale akijionyesha yeye bora kuliko Billy mwenyewe aliyekuwa akihangaika kuhakikisha familia yake ina nyumba nzuri. Umeme usikatwe pale ndani,  maji yapo kila wakati na chakula kizuri kisikosekane kwa familia yake. Wakawa na kazi ya kupika na  kupakua tu mle ndani wakilishwa na Billy kama makinda ya ndege.” “Carlos anapenda watoto wangu na alikuwa akitujali sana kuliko Billy alivyo..”

          “Huo ndio uongo uliokuwa ukimuaminisha Briana ambaye alikuwa mtoto asiyejua maana ya maisha. Mlitegemea maishi mazuri na ya hali ya juu kivipi, na Billy naye aishi kama vile Carlos ambaye hakuwa hata na kazi ya maana?” “Carlos alikuwa na kazi na alikuwepo nyumbani pia.” “Unaongea nini wewe Anele? Yuko wapi sasa hivi huyo Carlos? Yuko wapi?” “Halafu wakiitwa wanaume wenye kazi unafikiri Carlos naye atakwenda?” “Anakwenda sana. Kazi si kazi?” “Anele, tunamfahamu sisi Carlos kama mtoto aliyekulia humu ndani. Tunamfahamu zaidi yako. Beila anapokwambia Carlos hapendi majukumu, anamaanisha ni mvivu. Mvivu watokea shuleni akisoma na Billy. Wewe ulipomtoa Billy kwenye picha, hukujua ndio unavunja mahusino yako ya wizi na Carlos. Ungemtaka Carlos, ni kuendelea kumuacha Billy kwenye picha ili aendelee kuwatunza nyinyi wote. Ona kinachokutokea. Mtoto ambaye mmeaminisha mahakama mnampenda na kumjali mpaka akawachagua nyinyi, amewashinda! Mkaendelea kumtumia mjinufaishe naye, yeye mwenyewe hanufaiki na wewe hujali Anele!”

          “Mimi sijinufaishi na Briana.” “Mbona sasa unaendelea kudai ada ambazo hasomi?” “Briana mwenyewe aliacha shule. Ningefanyaje baba yake hayupo?” “Mbona ukitaka pesa yangu unahakikisha napokea simu zako hata kama nipo kwenye kikao unanitoa? Kweli Briana anaacha chuo, unashindwa kuniambia, unadai tu pesa?” “Au hata kwa nini asiniambie mimi ambaye nipo hapa, sina ninalofanya, nikapata muda na Briana nikazungumza naye?” Babu yake akadakia.

          “Mimi simtumii Briana.” Anele akajitetea. “Sasa ukishalala, usingizi ukikuisha, huwa unafanya nini wewe Briana?” Dada yake akamuuliza. “Shopping.” Akadakia Junior, mtoto wa Beila, mgomvi wa Briana. Wote wakageuka. “Anajulikana kwa kutapanya huyo. Angalieni Istagram yake. Ana watu wanamfuatilia kwa mavazi tu.” “Linafiki wewe, Junior. Una...” “Niwafungulie niwaonyeshe picha zako za majuzi ulipoenda kujirusha beach. Ukawa unaonyesha watu huko Insta hoteli ya kifahari uliyofikia na picha za nguo ulizonunua?” Junior akamuuliza Briana. “Kwa nini hukusema?” Mama yake akamlaumu mwanae. “Tumeambiana wote sisi mpaka watoto wa mjomba, tumuache mpaka aharibikiwe kabisa. Briana mjeuri mama. Anatudharau sisi wote. Hata bibi tuliambiana tusimwambie ili asimuonye mpaka apatwe na janga. Na hana muda mrefu huyu mama, janga litampata maana anavutia macho ya wengi mpaka wahalifu wataanza kumfuatilia. Watu huko Istagram wanajua mpaka chumba anacholala huyo Briana.” Ilimuuma sana Billy. Britney akalia sana, mwishoe akatoka hapo.

          “Hamkufanya vizuri.” Brandon akawageukia wote. “Dad, wewe huyajui matusi ya Briana.” “Anatukejeli pia. Anatuita sisi wote wapuuzi. Hatuna akili kama yeye na dada yake Britney. Eti wao wamejaliwa akili za darasani, sio kama Junior anavyofeli darasani, inabidi afanye summer class kila mwaka ili kulingana na wajinga wenzie huko shuleni kwao. Ndio tukaambiana tumuache, tuone mwisho wake.” Mtoto mwingine wa Beila wa kiume akadakia akimtetea kaka yake. Watoto wengine wote wakaanza kusema madhambi ya Briana.

          “Naomba turudi nyuma kidogo.” Bibi yao akawakatisha maana walikuwa wakimchangia kumsema Briana, mpaka akaanza kulia. “Anele ulikuja kuzungumza na Nelly. Ukisema umemfanyia uchunguzi unataka kuja kutushirikisha. Tafadhali maliza, ili tufikie hitimisho.” Watu wote kimya wakamgeukia Anele. “Tafadhali zungumza, nataka nimfuate Britney nimtulize. Umeharibu maisha ya watoto wangu kwa sababu ya tamaa ya pesa ambayo sikuwahi kukunyima, Anele!” “Mimi siku...” “Tafadhali zungumza kilichokuleta, acha kutupotezea muda.” Billy akamkazania.

          “Ni uchunguzi aliofanya juu yake. Amegundua Nelly amekudanganya wewe kuwa ni mjamzito wako ili umuoe. Kwamba...” Briana akawa kama  na yeye amevurugikiwa hakumbuki tena. Akamgeukia mama yake. “Ulisema ni mjamzito wa mtu mwingine aliyemlipa ampe mimba au alikuwa kwenye mahusiano mengine, dad hajui, au ulisema hana mimba anadanganya tu?” Briana akiwa anamsaidia mama yake kujieleza, akawa na yeye hana taarifa za kutosha. “Bado sijakamilisha uchunguzi vizuri.” Anele akajibu. Briana akakunja uso kama na yeye amempoteza.

          Billy akatingisha kichwa kwa masikitiko. “Kweli Anele, unashindwa kumfanya mtoto wangu atulie shuleni, unamwingiza kwenye maisha yako ambayo umeyachanganya wewe mwenyewe hujui ni nini unataka!?” Billy akaongea kwa kuumia sana. “Unatumia uharibufu wako hata kwa mtoto uliyezaa mwenyewe!?” “Mimi sijamuharibia Briana maisha. Kama ni shule atasoma tu.” “Angesoma kwa ada ipi wakati umekuwa ukitumia pesa yake?” “Pesa yote naitunza ili akija kurudi shule asipate shida. Kuna leo na kesho jamani. Ya kesho hatuyajui. Iweje atake kurudi shule tushindwe uwezo?” Anele akaendelea kujitetea.

           “Bila sisi kuona, muonyeshe Briana mwenyewe hiyo pesa unayomtunzia.” Akadakia Beila. “Toa simu muonyeshe akaunti ambayo unaweka hiyo pesa.” “Hana hela. Mimi najua. Hata hoteli alizofungua huko nyumbani, ni kama amefilisika tu. Watu wanyumbani wamemwambia baba yenu.” “Sio kweli.” Akambishia mama mkwe. “Basi fanya hicho alichokwambia Beila, sasa hivi. Muonyeshe Briana ada uliyokuwa ukichukua kwa baba yake.” Kimya wote wakampa muda.

          “Kama hilo limeshindikana, tuambie huo uchunguzi uliofanya juu ya Nelly. Hata kama haujakamilika, wewe utuambie tu. Binafsi nataka kujua.” Akasisitiza mama mkwe. Kidogo Nelly akaanza kuingiwa hofu. “Mpaka nipate uhakika wa jambo la mwisho ili niwape habari kamili.” “Wewe vipi Anele? Mbona ulimfuata sasa Nelly?” Beila akamshangaa sana. “Kumtaarifu.” “Haya, mtaarifu sasa.” Billy naye akaongeza. “Alikuwa na mahusiano mengine mbali na Billy. Kwa hiyo hata mimba kama anayo, si ya Billy kwa hakika.” Akaanza Anele.

          “Na nimeambiwa na mtu wa karibu yake kabisa. Anasema alishakuonya wewe Billy juu yake huyu, lakini hukumsikiliza. Anasema alikuwa akinitafuta mimi tokea asikie Billy anataka kumuoa huku. Akajua wanakimbia kule Tanzania ili isijulikane.” Anele akaongea. Alipoona kimya akaongeza ujasiri.

          “Aliniomba nisimtaje jina, lakini kwa kuwa hamniamini, namtaja. Alinitafuta yeye mwenyewe kwa njia ya Facebook. Akani inbox. Anasema alianzia kwa Briana Instagram. Alipojua jina langu kamili ndipo akanitafuta mpaka akanipata Facebook kwa kuwa sikuwa na akaunti Ista. Niliifunga. Kufupisha habari ni ndugu yake kabisa. Walilelewa nyumba moja. Anaitwa Yasinta.” Nelly alishituka nusura aanguke.

          “Ingekuwa ni jumbe ningewaonyesha. Ila aliomba nimpigie kabisa ili aniambie ubaya wake huyu. Na kingine ambacho amekiri wazi japo amesema hana ushahidi wakutosha, ndio nilikuwa nikisubiria hilo ili nipate habari kamili, ni kama alisema huyu Nelly alishakuwa na mahusiano na baba yao, ambaye ni mjomba wake kabisa, kaka ya mama yake Nelly pamoja mdogo wake wakiume, anaitwa Jackson, lakini Nelly alimpa jina la Jax.” Anele akaendelea.

          “Anasema Nelly alimtumia baba yao, yaani mjomba wake, kimapenzi mpaka akawapa nyumba na maisha mazuri. Alipofanikiwa kimaisha, akamuacha baba yao vibaya sana. Anasema huyo mzee mpaka alipata stroke kwa mshituko wa kuachwa na Nelly. Na mpaka leo yupo amepalalazi upande mmpoja. Sababu ni huyu Nelly.” Anele akawakilisha hoja. Chumba kizima kilikuwa kimetulia kimya kikimsikiliza. Jax akarudisha macho kwa dada yake.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Hakuna Yanayokaa Gizani Daima. Huwa Ya Gizani Yanamtindo Yakuja Kujiweka Bayana Mwangani. Ni Muda Tu, Ila Yote Huishia Mwangani.

Hakuna Siri Ya Milele. Kuwa makini na nini unafanya sirini.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment