Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Makosa!-SEHEMU YA 3. - Naomi Simulizi

Makosa!-SEHEMU YA 3.

Mlio wa simu yake  mwenyewe ndio iliomtoa usingizini. Aliiacha kwenye kochi hapohapo chumbani kwa Tino. Akashituka sana. Akamkuta Tino akimwangalia. “Pole Tino. Nimekusahau!”  Akakimbilia simu. “Da Lela!” “Kwema? Naona kimya! Nimekutumia jumbe zangu hata hujasoma!”
 Akauliza Lela kwa wasiwasi. “Samahani dada yangu. Nahisi sijisikii vizuri. Hapa nilikuwa usingizini ndio naamka. Hata jumbe zako sijaona dada.” “Mimi nahisi nina balaa jamani! Kila ninalopanga haliendi!” Akalalamika Lela. “Hapana dada yangu. Kila kitu kipo vilevile. Sema tu nitashindwa kuja mjini kushugulikia leseni kwa sasa.” “Kwa hiyo ndio unaondoka? Maana mimi namjua Tino. Anachosha sana. Na ndio maana mimi nilikwambia usihangaike naye. Mimi nilitaka uwe unakaa tu. Lakini...” “Da Lela! Da Lela!”  Ikabidi kumkatisha.

“Naomba utulie tafadhali. Nahisi ni hali tu ya mwili. Labda nakaribia siku zangu. Lakini si sababu ya Tino.” Sabrina akatoka kabisa nje ya chumba na kufunga mlango ili asimuumize Tino. Akasogea pembeni kidogo, akapunguza sauti. “Naomba mipango yako isisimame sababu ya hiyo leseni. Mimi nitakuwa sawa kabisa kubaki na Tino. Kukiwa na dharula nitaita taxi au nitampeleka mimi mwenyewe hospitalini kwa kutumia hili hili gari nikiamini hakuna trafiki atakaye nisimamisha njiani.” “Kweli Sabrina mdogo wangu!?”  Akamsikia ametulia.

“Kabisa dada yangu. Kuwa na amani kabisa na mipango yako. Nipe ratiba nzima ya kliniki yake au sijui kumuona daktari! Mimi nitampeleka, nitawaambia ni mfanyakazi wenu, umenituma wewe. Usiwe na wasiwasi kabisa.” Hapo akawa amemfurahisha na kumtuliza Lela. “Kama hivyo, hapo sawa. Maana nilishajua amenikwamisha tena huyo! Maana tokea aanze kuugua huyo, mambo yangu yamekwama kabisa!” “Usijali. Ulishazungumza na Sabina?” “Huyo naye ananiringia! Ameniambia nimpigie baadaye akitoka kwenye kikao tuzungumze vizuri. Hataki nikufanye mtumwa.” Sabrina akacheka kidogo kama kumtuliza.

“Usicheke Sabrina! Mimi namjua Sabina. Mkorofi kweli dada yako! Naomba nisaidie kumwambia sikufanyi mtumwa.” “Hata hivyo hunifanyi mtumwa bwana. Kila kitu nafanya hapa ni kwa kupenda kwangu. Kwani mara ngapi umeniambia nisijishugulishe na mambo ya Tino, lakini si nimefanya mwenyewe!” “Si hata leo asubuhi nimekwambia mdogo wangu, eeh?” “Ndiyo.” Sabrina akakubali akicheka. “Basi naomba na hilo umwambie Sabina dada yako, na uhakikishe anaelewa. Mimi namjua Sabina. Anaweza kuja kukutoa hapo hata sasa hivi!” “Usijali. Wewe uwe na amani. Endelea na mipango yako.” “Hata leo si naweza kusafiri au unasemaje?”  Akamtega kwa swali.

Sabrina alishagundua uwepo wake pale unamkera tu Tino. Akajiambia akiwaacha pale hata kwa siku nyingine tatu, Tino atatulia kabisa. Na alijua wazi hasafiri ila anakwenda kwa mwanaume wake. Sabrina hakujali. Alichotaka ni uzima wa Tino. “Au unaona shida?”  Akauliza tena Lela kwa kubembeleza. “Nisikilize da Lela. Mimi nipo sawa kabisa. Na uzuri huwa unapokea simu zangu. Kukitokea lolote, akija yeyote, kabla sijazungumza naye na kumfungulia mlango, wewe utakuwa wa kwanza kujua. Sitampeleka Tino popote ambako najua kutazua maswali bila wewe kujua dada yangu.” “Wewe unanifaa sana Sabrina. Na ndio maana nilitaka nikutoe leo, ukale chochote utakacho! Sema mwenyewe umekuwa mzito!” Lela akawa amefikishwa.

“Sasa wewe hicho chakula ulichotaka nikakilie hotelini, niletee hapahapa. Wala usijali.” “Hilo tu, wala usitie shaka. Nakuletea kuku mzima wakushoma na chips. Soda zipo hapo ndani. Kunywa tani yako. Unataka nini kingine?” Sabrina akacheka sana. “Ninavyopendwa mimi!” “Sana! Wewe mkombozi wangu mbona! Hata mahitaji yako binafsi niambie mimi nitaenda kukununulia nikuletee hapo hapo.” “Hamna shida dada yangu. Nakushukuru.” “Basi nitaleta na zawadi nzuri, ili ujue nakushukuru.” Sabrina akacheka tena.

“Usisahau kuzungumza na Sabina tafadhali. Mwambie sikunyanyasi na nitakulipa tu vizuri. Angalau na mimi nikapumzike mdogo wangu. Nimekaa kwenye hali ya kuuguza muda mrefu sana. Mwili na akili vinachoka! Acha na mimi nikatulizwe kidogo.”  Akajisahau na kuanza kufunguka. Sabrina akaona amuwahi. Maana Lela ni muongeaji wa ulalamishi. Akianza, hamalizi na yeye alishajua muda wa kunywa maziwa Tino umeshapita,  na Tino yupo ndani anamsubiri. “Usijali dada yangu. Mimi nipo.” Sabrina akakubali kwa haraka, wakaagana. Hakujua ni mangapi ameyasikia Tino, maana alijisahau akaendelea kuzungumza kama kawaida.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alielekea jikoni, akamtengenezea maziwa kwenye kikombe kikubwa. Akaweka na kiini cha yai bichi pamoja na asali. Akakoroga vizuri, akaweka na Milo, akampelekea chumbani. Akampokea kwa macho. “Ujisaidie kwanza ndipo unywe maziwa.” Akaweka maziwa na kwenda kuchukua vifaa vyakujisaidia pamoja na kumsafishia. Akampanga vizuri. “Naomba ujaribu na haja kubwa kabisa. Tokea jana hujajisaidia! Naomba usibane tafadhali, itakusaidia kufungua tumbo.” Sabrina akaongea kwa kujali. “Nakupisha ili upate nafasi. Nipo tu hapo chooni, sitakwenda mbali. Pengine ukiwa na mimi unashindwa kujisaidia.” Akakubali. “Na ujue wazi hutajichafua. Nimetegesha vizuri, mkojo utaenda kwenye chupa, na kinyesi kwenye gazeti, hutachafuka wala kuchafua shuka. Nimekuwekea na taulo chini. Hutachafuka kabisa. Kwahiyo jiruhusu kujisaidia.” Akakubali akionyesha uso wa shukurani. Sabrina akampisha.

Alipopata harufu ya kinyesi, akajua amefanikiwa. Akasubiri tena kidogo akaingia chumbani akicheka. “Afadhali. Sasa hapo utapata njaa.” Akaongea Sabrina kuonekana ameridhika na alichofanya Tino, wakati wengine walimsimanga. Akaenda kuanza kutoa chupa ya mkojo. “Wakati nasafisha chupa, jitahidi kuendelea kujisaidia. Nitarudi baada ya muda mfupi tu.” Akarudi tena bafuni. Akasafisha shupa na kuiweka delto ili isitoe harufu, ndipo akarudi kutoa kinyesi. “Umemaliza au unahitaji muda zaidi?” Akagundua amemuuliza maswali mawili kwa wakati mmoja akacheka mwenyewe Sabrina. “Haya, ngoja nianze tena. Umemaliza?” Tino akakubali. Akatoa kinyesi na kumsafisha vizuri tu. Akampaka tena dawa huku akimsugua.

“Madonda yamekauka Tino. Bado una maumivu makali?” Akakataa. “Afadhali. Nitaendelea kukupa dawa ya maumivu asubuhi na usiku wakati unalala ili usiwe na maumivu kabisa.” Akaendelea kumsugua sehemu ya nyuma vizuri, na mbele napo akampaka cream hiyo yenye dawa, akarudisha diaper. “Unywe sasa maziwa, yasipoe zaidi.” Akamkalisha na kumpa kwa kikombe tayaribu. Akamaliza yote. Hilo likamfurahisha Sabrina. “Nakwenda kupika Tino. Uangalie tv ukiwa umekaa angalau hata kwa lisaa limoja au mawili. Usilale sana. Ni sawa?” Akakubali. “Nitarudi kuwa nikikuangalia kama utahitaji kitu. Sitakuacha kwa muda mrefu, na nikimaliza tu kupika, nitarudi tukae wote.” Akakubali.

Siku hiyo wakashinda wawili hao kwa amani. Sabrina akihakikisha Tino anakula na kushiba. Hamuachi mchafu wala mnyevu nyevu. Kitaulo alichokuwa akimuwekea shingoni ili akitoa ute asilowe nacho alikuwa akikibadili mara kwa mara na kuhakikisha hanuki mate wala haloweshi t-shirt aliyokuwa amemvalisha. “Nitamuuliza da Lela ni wapi huwa ulikuwa unakwenda kukata nywele ili nije kukupeleka. Sitaki kukunyoa mimi nikakuharibu, ukajichukia.” Akamuona ametabasamu. Wakati wote alipokuwa amekaa, kama ni hapo kitandani basi alitaka aminye miguu. Alimuona anatulia. Hata aliposinzia, hakutaka kumlaza. Alimpunguzia muda wa kulala kwa kuwa madonda yalipona, akajua hataumia kukaa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mapema tu kama majira ya saa 10:30 jioni, Lela akarudi. Sabrina akamsikia akizungumza na simu sebuleni. Akasubiri amalize ndio atoke. Lela alijaliwa sauti. Kila alichozungumza huko sebuleni, walisikia hapo chumbani. Sabrina akatulia kama hasikii. Aliweka mipango yake kwenye simu huku akicheka sana. Wote walijua amejawa furaha.

“Sabrina mdogo wangu!”  Wakamsikia akiita. Sabrina akatoka kwa haraka. “Mungu wangu mkubwa, nimembembeleza Sabina, naona amekubali. Amesema atazungumza na wazazi, awaambie kabisa umepata kazi ya miezi mitatu. Ila Sabina nyie!” Akacheka Lela huku anatingisha kichwa. “Amesemaje?” Sabrina akauliza huku akicheka kidogo. “Amesema nikulipe pesa yote ya miezi mitatu ndio tuendelee na kazi ili kichaa changu kikipanda, nikikunyanyasa tu, anakuja kukuchukua.” Sabrina akacheka kidogo.    

“Nitamwambia huninyanyasi.” “Bora asikie kutoka kwako mwenyewe. Lakini hilo nimemwambia halina shida. Tena nina nguo nataka kugawa. Nataka kubadilisha mavazi jamani! Miaka nenda miaka rudi nguo hizo hizo! Sasa nataka wewe ndio uwe wa kwanza kuchagua. Chukua zote unazotaka, zitakazobaki ndio nawapa wengine.” Sabrina hakuamini.

“Chakula chako kipo jikoni. Kama huna njaa, njoo uchague kwanza nguo wakati mimi najiandaa na safari.” “Mbona njaa imeisha! Twende tu.” Wakacheka hapo koridoni. “Ngoja nimwangalie Tino mara moja, halafu nakufuata dada yangu hukohuko chumbani kwako.” Sabrina akarudi chumbani kwa Tino, Lela akaelekea chumbani kwake.

“Dada anataka kunipa nguo. Naenda kuchagua, halafu nitarudi baada ya kumalizana naye. Anaonekana anataka kusafiri leo. Sasa nataka wakati nachagua nguo, niulize na maswali yooote ili tukibaki tusipate shida. Sitakaa huko sana. Unataka maji ya kunywa kabla sijaondoka?” Akamuona amenyamaza kama anafikiria kitu. “Tino?” Sabrina akamsogelea karibu. “Unafikiria nini? Au hutaki tubaki peke yetu?” Akakataa kwa haraka sana. “Sasa ni nini? Au hutaki nikachukue nguo?” Akamuona amekunja uso kidogo, akageuza kiganja kama anayesema hajui.

Sabrina akakaa pale kitandani. “Nikwambie ukweli Tino?” Tino akakubali. “Ninashida sana ya nguo. Manunuzi makubwa ya nguo na ya mwisho alinifanyia Emma kipindi nipo naye. Na hiyo ni miaka mitatu iliyopita. Nguo ninazovaa hapa wewe unaziona. Nyingi napata kwa Sabina. Huwa anazileta nyumbani, nachagua. Tokea namaliza chuo, sijawahi kuajiriwa. Hapa naona kama mwenzio Mungu amenijibu. Acha nikaangalie pengine nitapata vivazi vizuri hata siku tukitoka na wewe kwenda hospitalini au saluni, popote pale nisikutie aibu. Sitakawia.” Tino akakubali. Akamnywesha maji. “Unataka nikuache umekaa?” Akakubali. Sabrina akamuweka sawa, akatoka akiwa amejawa furaha.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

S

abrina akagonga mlangoni kwa Lela. “Da Lela niingie?” “Ingia. Nguo zote nimezirusha kitandani. Kazi kwako. Kuna watu wanapenda sana nguo zangu wao huwa nawauzia. Nikiwa nabadilisha kama hivi, basi nawauzia. Watu wangu wakaribu huwa ndio nawapa bure.” “Mbona nakushukuru dada yangu! Tena ni mpyaa! Mbona nimelala masikini nimeamka tajiri!” Akafurahia Sabrina huku akiendelea kuchagua. “Sijui tamaa! Mbona kama zote nimezipenda!” Lela akacheka. “Wewe tu na nguvu yako. Ulivyonifaa hivyo! Hapa nishatangazia wambea wote kuwa nimeajiri mtu msomi na wa maana wakumlea huyo Tino. Wakome kunifuata nyuma.” Sabrina akajua wanamsema hao wanaomuona kwenye starehe.

Sabrina akaendelea kuchagua. “Na hili gauni dada yangu?!” “Kabisa. Hilo nishaonekana nalo zaidi ya mara tatu! Silitaki tena.” “Acha mimi nichukue. Nitakwenda kubana kwa kufundi.” “Sasa kwa kuwa unaonekana wewe umependa zote, fanya hivi. Chukua zote hamishia chumbani kwako. Zitakazo kukera au usizozipenda, zifunge kwenye mfuko, tupia stoo. Nikirudi safari nitajua chakufanya.” “Kweli!?” Hakuamini Sabrina. “Kabisa. Na mfuko ule pale nimekununulia zawadi yako. Naomba tufanye kama ulivyosema. Akiugua huyo, kabla hujampeleka hospitalini, niambie ili mimi ndio niwe nimetoa habari kwa watu. Akija mgeni kama ulivyosema, kabla hujamfungulia mlango, nipigie simu. Niambie alivyo, nitakwambia kama umfungulie au la. Usikubali maswali juu yangu na Tino. Waambie wanipigie mimi mwenyewe. Sitaki umbea.” “Wala usijali dada. Naamini hakuna litakalo haribika. Kwani unarudi lini?” “Usijali. Tutakuwa tukiwasiliana. Ukinihitaji tu, kama mshale nitarudi. Ila ujue pakiwa na amani hapa, na mimi nitakuwa na amani huko. Angalau na mimi nitulie mdogo wangu. Nimekuwa mimi mtu wa shida tu!” “Basi usijali. Tutakuwa tukiwasiliana.” Akakubali Sabrina bila shida.

Akahamisha vitu vyote alivyopewa chumbani kwake. Akafungua sasa hiyo zawadi kwenye mfuko. Akakuta amemnunulia chupi nzuri sana. “7!” Sabrina akahamaki na kubaki ametoa macho. Akaangalia moja hadi nyingine. Akakuta lotion nzuri, shower gel inayofanana na hiyo lotion na body spray yake. “Yaani set nzima!” Akanusa. Akakuta inaharufu nzuri, akaipenda. Sabrina akaanza kucheka mwenyewe. Nguo zenyewe alizokuwa amepewa na Lela akisema amezichoka, ni kama zilikuwa mpya tu. Akaziweka kwenye moja ya kabati la ukutani hapohapo chumbani, akatoka kwa haraka kurudi kwa Tino.

“Mwenzio nimepata nguo nzuri kweli! Ameninunulia na set ya lotion, sabuni ya kuogea na body spray pamoja na nguo za ndani. Nzuri kweli! Nimefurahi.” Tino akamshika mkono, lakini bila tabasamu usoni. Akarudisha macho kwenye luninga. Sabrina akafikiria ni nini anachofikiria Tino. “Nakwenda kukuletea uji. Ni sawa?” Akakataa. Akamwangalia usoni. Akamuona kama mtu aliyetingwa na mawazo. “Naomba usinikatalie Tino! Unahitaji kula kwa ajili yako mwenyewe. Au hukupenda ule uji asubuhi!?”  Akakataa. “Sasa kama ulipenda, kwa nini ukatae kunywa wakati kila siku nakupa uji asubuhi na saa kumi?” Akabaki akimwangalia. “Hutaki kupona?” Akanyamaza. “Tino?” Kimya. “Umekasirika?” Akamtizama na kuangalia pembeni.

“Naomba hasira zikufanye upambane upone, Tino. Isiwe vinginevyo, tafadhali. Kasirikia hiyo hali. Ichukie na ujiambie utakula chakula kwa kujilazimisha kama dawa, utaanza mazoezi kuanzia kesho. Kwa nguvu zote, mpaka urudie afya yako. Mimi nakwenda kuleta uji. Kama utanikatalia, basi.” Sabrina akatoka. Akaenda kuandaa uji. Akaweka kwenye bakuli, akarudi nao chumbani.

Wakati anamlisha, mlango ukafunguliwa. “Basi hivyo unavyomfanyia huyo, hatakaa akapona. Anapenda kutumikiwa kweli huyo! Hapo kukuona huna unalofanya ila yeye tu, ndio raha yake!” Akaongea Lela akiwa amesimama mlangoni. Sabrina kimya akiendelea kumlisha. Akamfuta mdomoni. Akahisi pengine ndio maana Tino alikataa kula Lela akiwepo, akijua atamsema. “Na kama utaendelea kumlisha vitu vya maji maji, ujue utachezea kinyesi wewe, mpaka ukome.” “Naomba usiongee hivyo da Lela. Tafadhali sana. Zaidi kwangu. Nimechagua mimi mwenyewe. Si Tino wala wewe mlioniomba. Tafadhali usiwe na wasiwasi juu ya lolote.” “Sitaki uchoke mapema!” Akajirudi Lela.

“Hapana dada yangu. Naomba usiwe na wasiwasi. Tumekubaliana kwa miezi mitatu, ujue nitasimamia makubaliano yetu. Sitawakimbia hata iweje. Naomba uwe na amani.” “Basi kama ni hivyo sawa. Sitaki nije nionekane nimekuachia wewe shuruba yote.” “Hapana. Na huna haja yakumwambia hata Sabina jinsi ninavyoishi hapa. Mwache ajue tu kuwa mimi nipo hapa na Tino. Ni nini nafanya, haimuhusu.” Lela hakuamini.

“Kwa hiyo hata akikupigia wewe simu akikuuliza kama ndiwe unayemfuta mavi Tino hutamwambia?” “Da Lela! Nawezaje kutangaza hivyo? Kwanza haimuhusu, na Sabina hana muda huo na mimi. Ni mpaka mimi nimpigie. Na mimi si mlalamishi. Naomba wewe usiwe na wasiwasi. Huna hata haja yakujitetea kwa Sabina kwa chochote. Kwanza hata akijua, nimekuruhusu umwambie ukweli. Kuwa nimependa mwenyewe. Hujanilazimisha.” “Hapo umenituliza. Kuwa ya hapa hayamuhusu mtu.” Akajirudi Lela kwa unyenyekevu kama sio yeye.

“Kabisa. Niliyoyakuta hapa, nitayaacha hapahapa. Hutanisikia nikisema chochote kwa yeyote. Labda wewe mwenyewe.” “Hapo sawa. Angalau tuwe ukurasa mmoja. Nibakie mimi tu ndio msemaji wa hii familia. Maana watu ni wambea kweli! Wivu tu.” “Usijali dada. Mimi sitakuwa msambaza maneno hata kwa Sabina. Wewe niachie maagizo ya nini unataka kifanywe.” “Ukiona nyumba ni chafu, inatakiwa kusafishwa, niambie mimi. Kuna mama huwa anakuja kunisafishia na binti zake. Usihangaike kabisa. Kufua naona unafua mwenyewe. Ukiona umechoka, niambie. Yupo kijana huwa namwita, anakuja kufua na kupiga pasi.” “Labda za kwako tu dada, ili nisikuharibie kama zina maelezo maalumu. Ila sitashindwa kufua kwa mashine na kuzinyoosha mwenyewe.” Lela akacheka.

“Mbona Mungu amenikumbuka mwaka huu! Nakushukuru. Haya, hospitalini huyo labda nipige tena tufufue kliniki zake. Tena utakuwa umenisaidia. Ili maendeleo yake yatumwe huko ofisini kwake, waendelee kutulipa. Maana mimi niliwaambia sitaweza kuwa nakimbizana na mambo ya hospitalini, kumuuguza yeye na kazini kwangu. Tena niliwaambia nikifukuzwa na mimi nawashitaki na wao. Ndio wakapoa.” “Wewe utaniambia ni siku gani na muda wa kumpeleka huko hospitalini.” “Wewe unapenda siku gani?” “Sijali dada yangu. Wewe tu.” Lela akazidi kufurahishwa na  huo utayari wa Sabrina.

“Naona wewe hutaniumiza kichwa! Basi nitampigia simu daktari wake, nitakujulisha ni lini umpeleke. Tena kama utampeleka mwenyewe, nitawaambia wakulipe ya usafiri. Maana walitakiwa kumtuma mtu aje amchukue huyo. Mimi niliwaambia siwezi. Yupo kama mlemavu. Libaba lote hilo unaliingizaje kwenye gari! Ndio wakawa wanalipia gari la hospitali, linakuja kumchukua na kumrudisha.” “Hamna tatizo. Wewe panga kila kitu, kisha unijulishe.” Akamuona anaandika kitu kwenye simu yake.

“Kabla sijasahau dada yangu.” Lela akatoa macho kwenye simu na kumuangalia. “Hivi huwa ulikuwa ukimpeleka saluni gani? Naona kabla sijamrudisha hospitalini, akapunguze nywele.” “Walikuwa wakimkata haohao vijana waliokuwa wanakuja kumsafisha mavi. Wanamkata, nawalipa.” “Sasa kwa kuwa mimi siwezi, naomba nimpeleke saluni.” “Akijinyea huko saluni utafanyaje naye huyo? Si aibu tupu? Wewe mkate tu vyovyote au mkate kipara kabisa wote tupumzike.” “Wewe niachie hilo mimi. Wala usijali. Nielekeze saluni aliyokuwa akienda, na wanayowezea kupunguza aina hizi za nywele zake na wanaojua mitindo yake. Ili nikienda naye hospitalini, wakusifie dada yangu. Kuwa unamtunza vizuri.” Hapo akagusa moyo wa Lela.

“Naona wewe ndio kiumbe pekee unayenitakia mema. Nashukuru mdogo wangu. Maana wakiniona tu mtaani, utasikia Tino umemuacha wapi? Wanataka nimbebe mgongoni! Umbea tu na unafiki kuingilia mambo ya watu. Sasa safari hii nimewafunga mdomo. Kabla hawajaanza umbea wao, nawaambia nimemtafutia Tino mtu mzuri wa kumtunza, ili akija kufa wasije nisingizia kuwa simtunzi, ajifie mwenyewe.” Akamuelekeza ilipo saluni huku Sabrina akitamani kumfunga mdomo. Akamuhurumia Tino, akajua ndio maneno anayoyasikia kutoka kwa mkewe kila akifungua mdomo wake. Lela hakuwa na jema hata moja linalomtoka mdomoni juu ya mumewe!

“Na pia ili usikae sana pale saluni tukaingia wote aibu akianza haja zake huyo, siku ukitaka kumpeleka, niambie ili niwapigie simu kabisa ili wasikuweke. Wote pale washikaji zangu. Walishanizoea kipindi hicho cha uhai wake huyo. Nilikuwa nikienda naye pale, nakaa mpaka wammalize nikiwepo mwenyewe. Sikutaka wale wasichana wa pale wanaojidai kuosha wanaume za watu, waanze mambo ya ajabu. Wanizunguke, waanze kuchezea pesa yetu. Maana wanawake wa mjini nawajua mimi. Utaishia wewe kuitwa mke, wenzio wanashika waleti ya mumeo! Sitaki ujinga.” “Basi nitakwambia. Ila itakuwa siku moja kabla ya kwenda hospitalini, na naomba isichukue muda mrefu. Kichwa kinamuwasha Tino.” “Muongo huyo! Wala usimsikilize. Walikuwa wakimuosha kichwa kila wakati na..” “Na naomba unisaidie picha yake ya zamani. Angalau nijue mitindo yake ya zamani. Wakimkosea, nijue.” Akamkatisha kwa haraka.

“Sijui hata sura yake ipo wapi hapa ulimwenguni! Maana nahisi ana miaka mingi hajapiga picha. Kabla hajaanza matatizo yake yakujitafutia mwenyewe mpaka akafungwa na baada, sidhani hata kama alipiga tena picha. Na usimuone hivyo huyo, mbishi kuliko shetani. Hashauriki huyo, ndio maana amejifikisha hapo. Ni kwa kujitakia mwenyewe!” “Inamaana hamna hata albamu zenu za zamani! Picha za harusi au zozote tu?” “Tino wa wakati ule hatakaa akarudi hapo. Hata umpeleke saluni za mbinguni! Kwisha habari yake. Wewe mpeleke wakampunguze tu nywele, hamna watakachokifanya kwenye hicho kichwa na sura wakamtoa Tino yule.” “Sawa. Nitafanya hivyo. Mambo mengine nitakupigia. Nisikucheleweshe.” Sabrina akaona aondoke tu pale.

“Bahasha yako hii hapa.” Akaweka juu ya meza. “Asante.” “Mimi ndio nikushukuru. Na naomba usisahau kumwambia Sabina kuwa nimekulipa pesa, na nikakupa nguo nzuri sana, kisha nimekupa zawadi nzuri sana nilizokununulia kwa pesa yangu mbali ya malipo ili ajue nakujali.” Sabrina akashangaa na kuumia moyoni. Kumbe tena anatangazwa! Akapoa kidogo kama aliyeshikwa na ganzi ya gafla. “Lakini usijali. Nitampigia wakati nipo njiani, nitamwambia kila kitu. Akikupigia kukuuliza, naomba mthibitishie.” “Sawa.” Akajibu kwa kuishiwa nguvu.” “Funguo za gari zipo zimening’inia pale kama unaingia hapa ndani. Pesa za matumizi ya hapa ndani ni kama hutahitaji kabisa. Maana nimenunua kila kitu ninachojua kitahitajika hapa, kwa hiyo hutahitaji pesa kwa mambo ya hapa ndani. Gari limejaa mafuta. Na umeme huwa nanunua wa mwezi mzima. Hamtakuwa gizani. Maana ukikatika, jenereta linajiwasha lenyewe. Ila pesa zako zote nimeweka hapo juu. Tutawasiliana endapo utakwama popote. Kwanza nitakuwa nikikupigia.” “Sawa dada. Nashukuru.” Lela akatoka. 

Maisha ya Tino na Sabrina peke yao.

T

ino akawa amemuona. Akamshika mkono. Sabrina akacheka kidogo huku ameinama. “Uji utakuwa umepoa. Acha nikaupashe, uje umalize.” Sabrina akatoka bila kumtizama. Alishaumia moyoni. Akajua kumbe Lela anafanya ili ajulikane kwa watu sio kwa moyo wa shukurani kama alivyomwambia! Inamaana kila mtu atajua amechukua nguo zake! Akakereka sana rohoni asijue ni nini cha kumkera hivyo! Asijue alishaanza kukerwa na Lela tokea aanze kumsikia akimsema vibaya Tino aliyekuwa mgonjwa. Alikusudia asiingilie mambo yao, kwa kuwa hakuwa akijua uhalisia wa ndoa yao japo Sabina alishamwambia kwa sehemu, lakini akakuta moyo umelemea kwa Tino mgonjwa. Lela akaanza kumkera. Akachukia kuwepo tena pale, akaona historia ya kama nyumbani kwao inajirudia. Hakuna anayethamini anachokifanya kwa juhudi ila kumtumia vibaya. Akatamani iwe vinginevyo hata kuwepo sehemu ingine isiwe hapo au nyumbani kwao, ila kwa ajili ya Tino, akaamua ajitulize hukohuko jikoni, arudi akiwa ametulia. Akanywa maji ya baridi, akatulia.

Aliposikia mlinzi anafungua geti kisha na kufungwa, akajua ndio Lela ameondoka. Akapumua kwa nguvu. Akarudi chumbani kwa Tino. Akapokelewa na macho ya Tino. “Malizia uji, baadaye nitakupa chakula. Au unaanza kusinzia?” Tino akakataa. “Utapona Tino. Na naomba usiache kujisaidia kwa hofu. Ukiweza kujua kama unataka kujisaidia, niambie. Haja ikitoka bila kujua pia naomba usijisikie vibaya. Nitakusafisha. Sawa?” Tino akabaki mpole. “Na kabla hatujaenda saluni nitahakikisha unajisaidia kwanza, halafu nitahakikisha unavaa diaper ili usijichafue mbele ya watu. Na nitakuwepo pale. Nikisikia tu harufu kama haja itatoka, nitakurudisha kwenye gari, nitakusafisha. Nakuhakikishia hutaingia aibu. Usiogope. Sawa?” Kimya akiwa amepoa.

“Lazima kukubali kutoka hapa. Huwezi kujifungia daima Tino. Sio sawa kwa afya yako na akili yako. Mimi sijui ulikuwa nani zamani. Ulikuwa na hadhi gani! Lakini Tino, yapo mambo hatuchagui kwenye maisha, yanakuja tu. Sasa jinsi ya kukabiliana nayo ndio kipimo cha ubinadamu. Kama wewe ni jasiri au la. Muangukaji na hukai chini au unayekubali kushindwa. Hata kama umesikia kwa muda mrefu sana kama hutapona, naomba amini kwa upya. Usijifiche, na wala huna chakuona aibu. Hujui utakuwa msaada kwa wangapi watakaokuona ulianguka, unapambana na utarudi kusimama. Na mimi nipo na wewe, sitaacha uaibike nje. Nitakusitiri, hutatembea na uchafu. Sawa?” Akakubali na kutaka amshike mkono.

Sabrina akafurahi, akamshika mkono na kuubusu ule mkono wa Tino. “Utakuwa sawa tu Tino. Jipe muda.” Akakubali. Akamalizia kumnyesha uji wote. Akamfuta vizuri, akarudi kukaa pembeni yake. Safari hii bila hofu. Akakaa karibu kabisa na alipokuwa amekaa Tino hapohapo kitandani. Wakatulia wakiangalia tv. Baada ya muda akamhisi anataka kushika. Akamwangaia, akumuonyesha kwa macho anamwita. Sabrina akafikiria kwa haraka. “Unataka ujisaidie?”Akakataa. “Maji ya kunywa?” Akakataa. “Akafikiria tena. “Nikulaze?” Akakubali. “Ila nakupongeza. Umekaa muda mrefu!” Akamuona anatabasamu.

“Kesho tunaenda kukaa sebuleni. Sawa?” Akazungumza naye huku akimuweka sawa. Akakubali. Akampanga hapo kitandani vizuri. “Upo sawa?” Akakubali. “Unataka kitu chochote?” Akakubali. “Maji ya kunywa?” Akakubali kwa haraka, Sabrina akacheka na kutoka. Akakutana na chakula alicholetewa na Lela. Akatamani kuzira kula, lakini akajiambia ni pesa ya Tino, acha na yeye aile.

Usiku huo baada ya wote kula, akaenda kuoga chumbani kwake. Akakutana na zile nguo za Lela. Akafikiria. Akajiambia hapana. Akazikusanya zote. Akajiambia hata kama ni masikini, hajatembea uchi. Akazifunga sehemu moja. Akaenda kuziweka stoo kama alivyoambiwa, akarudi kuoga. Akajifunga kanga yake, na kuvaa tisheti yake aliyochagua yakulalia usiku. Akatoka na mto wake bila shida wala wasiwasi akijua atakwenda kulala chumbani kwa Tino. Akachukua na shuka, akarudi kwa Tino. Akaingia na kuweka ile mito na mashuka kwenye kochi, kisha akamsogelea Tino. Alishamuosha na kumpaka dawa tayari kwa kulala. Kama kawaida yake aliacha kumvalisha soksi miguuni kama kitu cha mwisho chakumbembelezea.

Akapanda kitandani Tino akimwangalia. “Upo sawa?” Akamuuliza kwa upole wakati anapanga miguu yake mapajani kwake. Tino akakubali. “Nikuulize kitu Tino?” Akakubali. “Hujisikii hamu ya kunywa juisi baridii? Maana nimekuwa nikikupa maji tu. Nimeona kwenye friji kuna juisi nzuri mpaka za nyanya na zimeandikwa ni za asili. Ungependa kunywa? Usiogope mkojo, nitakupa chupa ya kujisaidia kabla kujalala na nitakusafisha tena mdomo. Hutalala na meno machafu.” Akakubali.

          Sabrina akatoa ile miguu mapajani kwake na kutoka. Akarudi jikoni kwenye friji. Akaanza kusoma zile juisi. Zilionekana za gharama na zote ziliandikwa zinaongeza Vitamin C na nguvu. Akachukua juisi ya stafeli. Alishaambiwa huwa inavirutubisho vyakuponyesha magonjwa mengi tu. Akamuwekea kwenye glasi pamoja na mrija, akarudi nayo chumbani. “Lini utaanza kuzungumza na mimi Tino?” Akauliza taratibu wakati akimnyeshwa hiyo juisi. Tino akamtizama tu. “Umependa juisi?”  Akakubali kwa kutingisha kichwa taratibu. “Naomba uanze kujaribu kuzungumza Tino. Nitajua ni hatua ya kwanza, uliyokubali kuchukua kufikia uponyaji.” Akakubali. Sabrina akafurahi sana. “Asante Tino.” Akampa hiyo juisi mpaka akamaliza.

Baada yakumsafisha kinywa, na kujisaidia, akarudi kukaa miguuni. Akaanza kumchua taratibu, Tino akimwangalia kwa utulivu. Macho yakagongana. “Unafikiria nini?” Sabrina akamuuliza huku akiendelea kumchua taratibu. Akatingisha kichwa taratibu kukataa. Sabrina akacheka na kuendelea kuminya miguu yake, akivuta vidole. “Umeanza kuhisi hata kidogo upande wa kulia?” Akakubali. “Kweli!?” Sabrina akashangaa. Akakubali. “Tuendelee kuomba Tino. Mungu atakuponya tu.” Akakubali.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Walikaa hapo kwenye hilo jumba wao wawili tu. Amani na kubembelezana kama Sabrina hakuwa amemsikia Lela. Siku ya kwanza na ya pili hakumtoa chumbani. Ila akaendelea vilevile kumfanya akae kwa muda mrefu zaidi. Siku ya tatu baada ya kuamka usingizi wa pili wa asubuhi. Kama kwenye saa nne hivi, Sabrina akamsogelea pale alipokuwa amelala. “Leo nataka utoke hapo kitandani Tino. Tujaribu tu, naamini tutaweza kufika sebuleni. Nitakuweka kwenye kigari chako.” Akafikiria kidogo, akakubali. “Itakuchangamsha akili.” Akamsogezea kile kigari. Kazi ikawa kumsaidia kutoka hapo kitandani kuhamia kwenye hicho kigari. Upande wa kulia haukuwa na nguvu sana.

Sabrina akajaribu mara ya kwanza, ya pili na ya tatu akashindwa kumuhamishia kwenye kigari. Akamrudisha kitandani, akabaki akifikiria. Tino akamkatalia. “Lazima ipo njia wanatumia kwa watu kama wewe Tino. Wewe sio wa kwanza. Naomba nipe muda wakufikiria.” Tino akabaki akimtizama. Akachukua simu yake akaanza kutafuta google na kuangalia video Youtube jinsi yakumuhamisha mtu kama yeye. Akagundua kuna vifaa maalumu. Ila wengi wanatumia misuli ya mapaja sio kiuno ili wasiumie na pia kuwa na nguvu nyingi.

Akaweka kiti upande utakao kuwa rahisi kumuweka. “Nikumbatie kwa kuweka mikono juu ya shingo yangu. Nitakuwa upande wa kulia ambao hauna nguvu nyingi, na wewe nisaidie kwa kadiri utakavyoweza. Tukifanikiwa kusimama, tutageuka pamoja, pole pole mpaka kwenye kigari chako. Umenielewa?” Tino akakubali. “Usiogope, sitakuangusha. Taratibu tu mpaka tutaweza.” Akakubali. Akamvuta mpaka mwisho kabisa ya kitanda. Madonda yote yalikuwa yamekauka. Ila ndevu zilikuwa ndefu sana kuzunguka uso mzima hata sura yake ilikuwa ngumu kumtambua ni mwenye uso wa namna gani! Kwa ufupi alikuwa akitisha.

Akamuweka mikono shingoni, akahesabu mpaka tatu, akamvuta juu akiwa amemshika kiuno. Wakasimama. “Upo sawa?” Akanyanyua uso akimtizama. Akamuhisi anatetemeka sana. “Pole Tino. Naomba usiogope. Sitakuangusha. Tugeuke taratibu, utaweza tu. Umefanya vizuri sana.” Wakafanikiwa kugeuka, akiweka nguvu nyingi kwenye ule upande dhaifu. Wakafikia kigari. Akamkalisha taratibu, hata Sabrina mwenyewe hakuamini kama wameweza. Akaanza kucheka. “Nipe tano Tino. Umefanya kazi nzuri sana.” Wakagonga mikono. Akamtoa hapo chumbani. 

Sabrina afanikiwa kumtoa Tino Kitandani.

“Nakuzungusha nyumba nzima, uone, ndipo ukae sebuleni. Sijui mara ya mwisho ni lini ulipotoka!” Tino kimya akiangaza macho. Akamtembeza nyumba nzima, akamrudisha sebuleni. “Umefurahi?” Akamuona anataka kumshika. Akajua amefurahi. Akafanya vilevile kumuhamishia kwenye kochi. Ikawa rahisi tu. Akampangia mito. Kwa mara ya kwanza baada ya muda mrefu, hatimaye Tino akafanikiwa kurudi kukaa sebuleni tena wima. “Ukichoka nitakulaza hapohapo. Tunarudi chumbani usikuuu! Utaweza?” Akamuuliza huku akicheka. Akashangaa Tino amekubali. Akajua amefurahia.  

Walishinda hapo sebuleni siku nzima. Mara nyingi Sabrina alikaa chini ya miguu akimfanyia masaji ya misuli ya miguu. Akajisaidia hapohapo sebuleni. Akamsafisha. Alimlisha hapohapo, ilipofika usiku akamrudisha chumbani. Safari hii akaenda naye mpaka bafuni. Akamsafisha kinywa akiwa amekaa kwenye kigari chake ameegemea sinki. Akamuosha juu na kumvalisha nguo ya juu ya kulalia akiwa palepale bafuni amekaa. Ndipo wakahamia kitandani. Akamalizia kumsafisha chini na kumvalisha akiwa amemlaza kitandani, alipomaliza akamfunika. Hakuchukua muda mrefu, akalala kabisa. Sabrina akajua alichoka kukaa, ni kitu hakufanya muda mrefu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kesho yake akafanya hivyo hivyo kumtoa kitandani. Ila kwa kuwa alikuwa ameshajifunza jinsi ya kumtoa kitandani, safari hii hakupata shida. Wakahamia sebuleni. Mpaka siku hiyo na muda huo Lela hakuwa amemtafuta hata kwa kuwajulia hali! Na yeye akaona amwache tu, asije akalalamika anamsumbua. Jumapili nayo akamtoa mpaka nje. Akamuona wazi amefunguka mpaka usoni. Akamuacha kwenye kigari chake, yeye akakaa pembeni, chini kwenye ukoka. Tino akawa akiangaza macho.

“Ukichoka niambie nikurudishe ndani.” Akakubali, akaendelea kuangalia. “Unataka nikuzungushe mpaka nyuma ya nyumba?” Akakubali kwa haraka akitingisha kichwa. Sabrina akamtembeza kuzunguka nyumba nzima akimsukuma kwenye kigari chake. {Wheelchair}. Hiyo nyumba ilikuwa imezungushiwa ukuta mkubwa sana, huwezi kuona nje. Na walikuwa wao tu wawili na mlinzi kwenye kibanda cha getini.

Pasafi na ukuta wenyewe mzuri. Umejengwa na kuweka marembo mazuri. Maua mengi na vyungu vya maua vyakuvutia vikitangaza utajiri wa wanandoa hao. Ukweli Lela alijua kutunza nyumba yake. Msafi ndani na nje. Sabrina mwenyewe akazidi kuvutiwa. “Mnanyumba nzuri sana Tino. Na da Lela anajua kupatunza!” Tino kimya. Akamuacha nje kama lisaa, akaamua kumrudisha ndani baada ya kumnywesha maziwa na kukaa tena kidogo. “Umefurahia?” Akamshika mkono, ishara yake yakushukuru. “Karibu.” Sabrina akajibu akicheka.

Akamrudisha tena kwenye kochi. Akamuwekea mito ili asiumie. Akakaa pembeni yake. “Naomba niongeleshe kitu chochote Tino.” Akamuona anatabasamu. Akafikiria kidogo, “Asi-an-te.” Sabrina akashangaa sana. “Tino wewe! Kumbe unazungumza! Sasa kwa nini hutumii maneno?” Akacheka tu. “Tino?” Akamwangalia na kucheka tena kidogo. Wazi siku hiyo alionekana amejawa furaha. Hata aina hiyo ya uchekaji, Sabrina hakuwa amemuona. Alicheka angalau meno yalionekana. “Unatabia mbaya Tino!” Wakazidi kucheka. Akamfuta mate yaliyokuwa yakidondoka, gafla akapoa. Akajua pengine ndio sababu.

Akamvuta mkono. “Naomba usijali juu ya haya mate yanayodondoka Tino. Naamini baada ya muda utakuwa sawa.” Akamtizama na kunyamaza. “Niambie sawa.” “Saa-waa.” Sabrina akacheka. Hiyo siku nayo wakamalizia hapo sebuleni. Hapakuwa hata na hodi siku hiyo ambayo karibu watu wote hawaendi kazini. Mchana wakati amekaa kwenye kiti, Sabrina alimkwangua tena mba taratibu huko kichwani mpaka akalala hapohapo. Akamfunika vizuri na kumuacha amelala huku amekaa.

Alilala mpaka usingizi ukamuisha mwenyewe bila ya kuamshwa. Sabrina alipomuona amefungua macho akamsogelea. “Nimefikiria Tino.” “Nii-nii?” Sabrina akashangaa ameongea bila kuombwa. Akaendelea. “Kwa kuwa da Lela hajapiga simu. Naona twende tu saluni kesho. Nywele na ndevu vimeanza kutisha. Nyusi ndio zimefunika macho kabisa, huonekaniki! Si umejiona pale bafuni?” Akakubali. “Na kama hutaki kurudi kwa wale waliokuwa wakikufahamu ukiwa mzima, tunaweza kwenda kwengine. Ukachagua staili yako unayotaka wakunyoe, ukipata nguvu, tutarudi kule walipokuzoea.” Akakubali kwa haraka.

Sabrina na Tino saluni.

K

wa kuwa alishajua njia zakumtoa kitandani kwa urahisi, hakupata shida kumuweka garini. Alilisogeza hilo gari aliyoachiwa aitumie mpaka karibu kabisa na mlango. Alihakikisha amemlisha vizuri, na kushiba. Amejisaidia. Akamvalisha nguo safi, soksi na viatu, raba, na vyote vilikuwa vya Nike. Nzuri sana. Sabrina mwenyewe akapenda. Alionekana ni mtu aliyejijali sana. Sabrina akajifungulia  geti mida hiyo ya saa tano asubuhi siku ya jumatatu, akatoa gari nje, akiwa amemfunga  mkanda hapo kitini, ametulia tuli akijiangalizia anayoyafanya Sabrina. Akaegesha gari nje, akarudi kufunga tena geti, ndipo akarudi garini.

“Nimesahau kumpigia simu da Lela kumtaarifu kama tunatoka!” Tino kimya. Akaondoka hapo taratibu akiwa amevaa nguo zake zilezile za kawaida tu alizokuja nazo na sendozi. Akampeleka kwenye saluni aliyokuwa akiifahamu, aliyokuwa akiipenda sana Emma, mpenzi wake wa kwanza, maeneo ya Sinza. Alijua hapo watamnyoa Tino vizuri. “Tino, ni sawa wakati wakikushugulikia na mimi niende madukani, pale pale karibu na saluni? Angalau nijinunulie nguo mbili hivi nipate za kutokea na viatu? Sitakuacha muda mrefu.” Tino akakubali.

Akaendesha mpaka hapo saluni. Sasa kwa kuwa pale saluni palikuwa na ngazi, Sabrina akamuacha ndani ya gari, yeye akaingia ndani. Akazungumza na vijana aliowakuta pale, wote walikuwa wageni kwake lakini mmoja wao akakubali kutoka naye kwenda kumsaidia kumleta Tino ndani. Sabrina akashukuru sana. Tino akamuona Sabrina anatoka na kijana. Akafungua mlango. “Tino! Huyo anaitwa Dula, amekubali kukunyoa na kutusaidia kuingia ndani.” “Asa-nte.” Tino akamshukuru Dula. “Hamna shida Mkuu.” “Lakini naomba tuwe makini.” Sabrina akatoa angalizo. Mara akatoka kijana mwingine. “Acha tukusaidie sista.” Sabrina akashukuru sana. Hata hawakutaka kutumia kigari. Wakambeba kwa kumnyanyua chini ya makwapa, kila mmoja upande wake, wakamwingiza ndani mpaka kwenye kiti cha saluni.

“Naomba niwaachie namba yangu. Akinihitaji tu, mnipigie. Nitakuwa hapa karibu, madukani. Sitakawia.” Wakampa karatasi, akaandika. “Sitakawia Tino. Nitarudi. Lakini kwanza naomba mitindo yenu achague anachotaka. Wakamgeuza kwenye kiti, wakamuonyesha picha za ukutani. “Lakini kwa hizo nywele na hizo ndevu, huu mtindo utakufaa broo!” Kinyozi akamchagulia. Tino akamgeukia Sabrina kabla ya kukubali, Sabrina alipocheka baada ya kuangalia vizuri na yeye, ndipo na yeye Tino akaukubali. Ulikuwa mtindo mzuri. Alipoona pako sawa hapo saluni, akaondoka kwenda madukani.

Akaanza kuzunguka madukani akiwa amejawa furaha zote. Sabrina huyu alikuwa amelipwa mshahara wa miezi mitatu. Hamu yake ni kubadili nguo. Angalau hata tatu tu. Baada kama ya dakika 20 hivi akawa anarudi pale saluni.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

W

akati anakaribia mlango wa saluni, akakutana na Emma amebeba mtoto wa kiume. “Sabrina!” “Ni mimi Emma. Habari za siku?” Sabrina akauliza huku akimtizama yeye na mtoto aliyebeba, akajua wazi ni wake. “Naona hujabadilika kabisa Sabrina! Vipi!?” “Safi tu. Hongera naona ulijaliwa na kijana mkubwa tu.” Sabrina akaongea kwa utani. “Wewe si uliniringia ukijua nakutania, sijui! Ikabidi nioe. Na Mungu akanijalia mtoto. Nikajua sasa hivi utakuwa umeolewa, kumbe upo vilevile na nguo zilezile nilizokununuliaga mimi! Ona hasira na moyo wakutosamehe ulipokuacha? Umebaki palepale na kukosa bahati nzuri ya ndoa.” Sabrina akamshangaa sana Emma.

“Una nini wewe Emma!? Nani amekwambia najuta kutoolewa na wewe!?” “Kama hujuti basi unalo tatizo, na nikilema hicho Sabrina. Hivi unakumbuka huu ni mwaka wa ngapi tokea nikuache?” Sabrina akabaki na mshangao ametoa macho, akijua wazi ndani wanasikia. Maana walikuwa nje ya mlango. “Kama umesahau jua huu ni mwaka wa tatu na miezi mitano na siku 12, tokea ukubali hasira zikutawale, ukakataa ndoa. Pengine kama Mungu angekujalia kizazi na ningekuoa mimi sasa hivi huyu mtoto angekuwa wako. Na hizo nguo ungekuwa umebadili. Umebakia na vitu vilevile nilivyokununulia ila ukachoka zaidi, na nywele ukarudia ile mitindo yako ya zamanii! Mwanamke gani bado kwenye karine hii unasuka mitindo hiyo?” Sabrina akabaki ameduaa kama amefumaniwa.

“Shauri yako! Miaka nenda, miaka rudi utabakia umepauka hivyohivyo! Ulichezea bahati sana wewe!” Emma na mwanae wakaingia ndani. Baada ya sekunde kadhaa kama akili ikamrudia Sabrina, na yeye akaingia ndani. Akakuta Emma akisalimiana na wale vinyozi, Tino anasafishwa. Akamsogelea pale kwenye sinki. Wazi alikuwa amebadilika usoni. “Vipi, yupo sawa?” Akamuuliza anayemuosha. “Tumemaliza. Ninauhakika utamsahau.” Sabrina akacheka kwa kujilazimisha, Tino akafungua macho. “Nimerudi Tino. Nakaa pale kwenye makochi.” Akakubali.

Mwili mzima wa Sabrina ulikuwa ukitetemeka kwa hasira. “Niambie mtoto mzuri, ajira wapi?” Emma akamuuliza kwa kejeli huku akicheka. Sabrina akamwangalia na kuamua asimjibu. “Nilijua tu hukupata ajira! Si nilikwambia wewe masomo unayosomea na dunia inapokwenda! Ninauhakika unanikumbuka sana wewe Sabrina.” “Sidhani kama nimekufikia wewe, Emma. Wewe unahesabu siku tokea nikukatae!” “Ni kwa kuwa tu nina kumbukumbu nzuri.” Akapinga, Sabrina akamtizama kwa kumsuta.

“Wengine tulijaliwa kumbukumbu nzuri na za haraka.” “Niambie ni muda gani tokea umuoe mama wa huyu mtoto? Nitajie kama ulivyonitajia mimi muda kamili tokea nikatae usinioe.” Akababaika kidogo. “Lakini hayakuhusu.” Akajikaza na kujibu kibabe. “Unajua nini Emma, ningekuwa sikufahamu wewe, ungefanikiwa kuniharibia siku yangu. Lakini kwa kuwa nakufahamu vizuri, ninauhakika huko ulikokimbilia anakukimbiza mchakamchaka ndio maana bado unanikumbuka mpaka mavazi yangu. Na pia ndio maana upo hapa siku na muda wa kazi kumleta mtoto mdogo hivyo anyolewe nywele, na si mama yake.” “Majukumu ni kugawana!” Akajitetea Emma.

“Si wewe Emma. Na nilikwambia utanikumbuka tu. Ila nikwambie kweli Emma, hata kama unaniona nipo dhaifu namna gani. Sijafanikiwa kama hivyo wewe, ila Mungu amenipa amani na utajiri zaidi yako Emma. Sizunguki kutafuta nani nilimsaidia nani namdai. Sina umasikini huo.” “Kwa kuwa huna ambaye umemsaidia.” “Usingebaki ukinikumbuka Emma. Au usingerudi kunibembeleza unioe na kunitumia marafiki zako wakuombee msamaha.” “Walijipendekeza wenyewe kwa kuwa walitaka nikuoe wewe.” “Sawa Emma. Ila nakuhurumia na ninaomba Mungu afanikishe nafsi yako na roho kama hivyo unavyojionyesha umefanikiwa.” “Sijionyeshi, ni kweli nimefanikiwa.” Sabrina akanyamaza, hakujibu tena.

Emma akaendelea kuzungumza kwa jazba akimsema vibaya Sabrina, watu wote pale ndani wakawa kimya. Akabaki akiongea peke yake. Mmoja akaongeza sauti ya redio. Emma akakasirika sana. “Hiyo ni dharau kubwa sana. Unajua nafahamiana na Dula mwenye hii saluni? Nimeanza kunyoa hapa zaidi ya miaka 7. Tokea nyinyi wote hamjaanza kufanya kazi hapa. Muulizeni Sabrina.” Sabrina akanyanyua uso na kumtizama kwa mshangao. “Sista naona sisi tupo tayari.” Akabaki na mshangao alipomtizama Tino. Tino huyu hakuwahi hata kumdhania kama ndivyo alivyo. Alibadilika na walimtengeneza ndevu zake vizuri sana. Ukatengenezwa mustachi mzuri uliotoa manywele yaliyokuwa yamefunika midomo yake, basi hiyo midomo ikawa kama ya mtoto wa kike maana ilionekana ya rangi ya pinki kama aliyepaka rangi ya midomo! Ikamfanya avutie zaidi. Mpaka macho mazuri ya rangi ya ugoro safi iliyozungushiwa nyeupe nzuri yakaonekana baada ya kupunguzwa mpaka nyusi zilizokuwa na zenyewe nyingi sana. Sabrina hakuamini.

 “Umependeza Tino! Kama sio wewe!”  Akamuona ametabasamu. “Asanteni sana. Nashukuru kwa kila kitu.” Emma akawa amepoa kidogo akiangalia kinachoendelea. Akatoa pesa, akawalipa na ya shukurani. “Msaada tafadhali ili tuondoke.” Sabrina akaongea huku akitoa tabasamu la heshima. “Bila shaka sista.” “Asanteni.” Akamsogelea Tino. “Upo tayari?” Akakubali. “Umependeza sana Tino!” Bado Sabrina hakuwa akiamini kama ni Tino. Alitokea wa tofauti kabisa. Akakumbuka maneno ya dada yake kuwa moja ya kitu alichovutiwa nacho lela kwa Tino ni uzuri. Hapo akaamini.

Vijana wawili akiwepo aliyemnyoa Tino ambaye na yeye ni Dula kama mmiliki wa hapo, wakaenda kumnyanyua Tino pale kitini kumpeleka garini.” Emma akacheka kidogo. “Nimeelewa sasa.” Sabrina akamtizama. “Kumbe mwenzangu upo kazini hapo!” Sabrina wala hakujibu. Akatoka kuwafuta. Akafungua gari, na kukimbilia mlango. Wakamwingiza ndani. “Jamani kaka zangu nawashukuruni sana. Na Mungu awabariki.” “Bila shaka dada. Wewe ukitaka apunguzwe tena, mlete tu. Usiache mpaka zikawa kubwa tena.” “Sitajisahau tena. Nitamrudisha baada ya muda mfupi tu.” Sabrina akaaga, wakaondoka.

“Asa-ntee!” Tino akavunja ukimya baada ya kumuona Sabrina anaendesha, mawazo yapo mbali kabisa na pale. Akageuka, akampa tabasamu wazi alijua hayupo pale. “Umekuwa msafi Tino! Umependeza sana! Tukiendelea kusafisha kichwa kikiwa hivyo mba wote utaisha kwa haraka, miwasho itaondoka.” Alipomaliza tu hivyo, akaendelea kuendesha bila ya nyongeza. Hakuzungumza tena mpaka wanafika nyumbani akafanya kama alivyotoka. Kujifungulia geti na kuingiza gari, kisha kurudi tena kufunga geti. Hiyo nyumba ilikuwa na ulinzi masaa 24, kutoka kwenye kampuni ya ulinzi ambayo Tino alikuwa akilipia na silaha. Kwahiyo hiyo nyumba ilikuwa na askari wenye silaha wakati wote. Lakini Lela aliwafukuza na kuwaambia hawana wanachokifanya, wanakula tu pesa yao. Akatafuta mlinzi wake wa kawaida, wale wa kulinda na mshale wakisaidiwa na filimbi. Anakuja kulinda hapo usiku asubuhi anaondoka.

Akamtoa Tino pale kitini peke yake akihangaika naye bila msaada. Akamuweka kwenye kigari chake. “Kuna joto sana Tino, labda nikutoe jioni. Sasa hivi ukapumzike ndani.” Tino akakubali. Akamsukuma mpaka ndani. “Unataka ujaribu kujisaidia?” Akakubali kwa haraka. Sabrina akakimbilia chooni, akaleta vifaa vyote. “Unataka namba mbili pia?” Akakataa. “Hutaki tujaribu?” “Si sa-asa.” Sabrina akacheka kidogo. Akamuwekea chupa, akajisaidia haja ndogo. “Diaper kavu kabisa! Tuongeze kunywa maji Tino.” Akakubali. Akamuhudumia vizuri kwa haraka, akampanga kwenye kochi. Akampa maji.

“Acha nimjulishe da Lela. Nilimuahidi kuwa nikimwambia kila kitu. Sijui huu ni wakati mzuri wa kumpigia! Au nitume ujumbe?” Sabrina akawa anajiuliza taratibu wakati akimlisha matunda Tino. Tino kimya. “Naona nitume ujumbe.” Akakubaliana na wazo lake. ‘Da Lela, nimefanikiwa kumpeleka Tino saluni. Tulikwenda salama na ndio tumerudi salama.’ Akatuma huo ujumbe. Hapo hapo Lela akapiga. “Sasa mbona hukuniambia ili niwajulishe wale vinyozi mimi mwenyewe!?” Lela akalaumu kidogo kama aliyenyimwa sifa. “Sikwenda kule dada, kwa kuwa sikutaka kukusumbua. Niliona kimya. Nikampeleka kwengine. Samahani kama nilikosea.” “Hamna neno. Nilijua ulimpeleka kule kwa siku zote! Sikutaka uende bila mimi kujulikana ndiye niliyekutuma. Watu wanamaneno mdogo wangu. Wanaweza kusema nimemtelekeza Tino, wakati mimi ndio nakulipa wewe.” Hilo likamuua zaidi Sabrina, akapoa.

“Si unajua binadamu lakini?” Akauliza Lela, Sabrina kimya. “Wanaweza kunisahau mimi ninayekuweka hapo na kukupa gari, wakasema nimemtelekeza Tino. Lakini nikianza mimi mwenyewe, nawaambia kabisa, namtuma mfanyakazi wangu, kumleta Tino. Sijui kama umeelewa?” “Nimeelewa dada. Siku nyingine sitafanya kitu mpaka wewe mwenyewe utangulie kupiga simu huko ninakotakiwa kumpeleka, ili wajue wewe ndio umenituma.” “Nashukuru mdogo wangu. Vipi nguo lakini? Maana nimejisifia kweli kwa Sabina.” “Samahani pia nilishindwa kukwambia. Naona mambo yalikuwa mengi. Sikupata inayonienea. Zote nimerudisha kule stoo!” Mpaka Tino akashangaa. Maana aliiona furaha usoni kwa Sabrina siku alipopewa hizo nguo. Gafla zote hazitaki tena!

“We Sabrina! Katika nguo zote zile yaani hujapata hata moja! Unakumbuka ile yenye madoa mekundu na nyeupe ulivyokuwa umeipenda!” Lela akauliza kama kwa kushangaa. “Wewe ni mpana zaidi chini dada yangu. Mimi kwangu hazikai vizuri. Zinaonekana wazi si zangu! Naona uendelee tu na ule mpango wako wa kuuza na kugawia rafiki zako. Nimezikunja na kuzining’iniza vizuri tu pale stoo.” “Mmh! Sasa hapo ndipo Sabina atakaponiona muongo! Na zile chupi nilizokupa zawadi?” “Nimekuja kuzifungua, ni zile chupi zakuingia katikati huku nyuma kwenye makalio. Mimi huwa sivai chupi za aina hiyo.” “Sasa si ndio za kisichana! Na kamwili kako hako kembamba si ndio zinakaa vizuri? Acha ushamba bwana Sabrina mdogo wangu.” “Naona kweli ni ushamba dada, huwa siziwezi. Zinanishinda kabisa. Nakosa raha ninakuwa na kazi ya kuzivuta kila wakati.” “Mmmh!” Lela akaishiwa nguvu.

“Ila da Lela, bado zipo na lebo zake, sijatoa, unaweza kuziuza kabisa. Ukarudisha pesa yako.” “Au nikabadilishe nikuchukulie nyingine? Au nije nikuchukue ukachague upendazo?” Akasahau kuwa aliaga amesafiri. “Tafadhali usihangaike na mimi dada yangu. Namaanisha kabisa. Wewe kabadilishe, ujichukulie kitu unachopenda. Kwanza mimi ninazo chupi zakutosha, sihitaji nyingine.” “Mwanamke huwa hatimizi nguo za ndani mdogo wangu!” “Hapana. Mimi sihitaji. Naomba ukiweka appointment ya Tino hospitalini unijulishe.” Sabrina akabadili kabisa mazungumzo.

“Kesho itakuwa sawa?” “Naomba iwe kesho kutwa. Leo nimemuhangaisha huko saluni, angalau apumzike kidogo, nimpeleke kesho kutwa kama kutakuwa na nafasi, ila ikilazimu kesho, basi.” “Usimuedekeze huyo. Tino si mgonjwa wa hivyo. Anapenda kufanya wenzake watumwa tu.” Sabrina akasimama kuondoka pale karibu na Tino alipokuwa akimlisha matunda. Akamfuta mdomo. “Basi utanipigia ukipata hiyo nafasi ya  daktari.” Ikabidi Sabrina aage. Alisha kerwa na Lela pamoja na Emma, alitamani angekuwa peke yake alie uchungu uishe.

“Sasa Sabina nitamwambia nini tena?” “Naomba unisikilize vizuri da Lela. Nilishakwambia, labda hukunilewa. Na ninajua tabia zinatofautiana. Mimi sio mtu wakufanya kitu, au kumsaidia mtu, nikamtangaza. Sina tabia hiyo.” “Sio kwamba mimi ndio...” “Samahani naomba nimalizie.” Tino akajua Lela amepata kiboko yake, na akaanza kumuelewa Sabrina. Alikuwa akisikiliza tu wakati Sabrina yupo jikoni.

“Ninapoamua kufanya jambo langu, nakua nimeamua kutoka moyoni, na sifanyi kwa ajili ya mtu.” Sabrina akaendelea akiwa na hasira. “Nitafanya kwa moyo wote nikijua Mungu ananitizama. Sijali ninayemfanyia atanishukuru au la. Na nikijua nimempendeza Mungu wangu, wengine sijali. Sijui kama umenielewa sasa hivi?” Kimya. “Nipo hapa si kwa sababu ya yako kwakuwa unanilipa au Sabina. Ni kwa kuwa mimi nimependa. Halafu mimi si mtoto mdogo ambaye nataka ruhusa ya kila kitu. Ndio maana uliniona nilinyamaza uliponiambia nimpigie simu Sabina eti nimwambie umenipa nguo! Sifanyi hivyo mimi. Kama wewe umetangaza ili upate sifa, utajua wewe mwenyewe jinsi ya kurekebisha. Ila jua vitu vyako vipo stoo.” “Naomba usikasirike Sabrina.” Lela akabembeleza.

“Sijakasirika ila nakwambia ukweli dada yangu. Mimi nilikwambia tokea mwanzo. Sitatoa mambo ya humu ndani kwako nikamwambia hata Sabina. Hivyo ndivyo nilivyo. Nitafanya nitakachoweza si kwa kuwa unanilipa pesa uliyopanga wewe bila kuniuliza mimi, ni kwa kuwa nimechagua kuwepo hapa.” “Kwani pesa niliyokupa ni ndogo?” Akauliza kwa kutulia. “Hilo ni swali ulilotakiwa kuniuliza kabla ya kuamua kunilipa. Nilikuja hapa, nikafanya ninayofanya sio kwa sababu uliniahidi pesa. Naomba hilo usije lisahau. Mpaka sasa nipo hapa si kwa sababu ya pesa, ni kwa kuwa nimechagua. Usisahau hilo tafadhali.” “Basi mdogo wangu. Naomba usikasirike. Kuanzia sasa hivi kabla sijafanya kitu, nitakuuliza.” “Nashukuru. Naomba nikutakie siku njema.” Sabrina akakata simu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment