Alipika
uji wa mchele na nyama ya kuku. Akachemsha kila kitu humo humo ndani. Kitunguu,
kitunguu swaumu, karoti, hoho. Akachemsha mpaka vikaiva akiwa hapohapo jikoni. Vilipoiva,
wakati anasubiri vipoe asage ndipo ampe Tino ili iwe rahisi kumeza, akaenda
kumuangalia. Tino akampokea kwa macho alipotoka tu jikoni. Akakumbuka Tino huyo
sio wa asubuhi aliyejawa mandevu. Sabrina akacheka. “Nusu nikuulize kama
umemuona Tino!” Tino akacheka. “Umependeza sana Tino. Sikujua kama huo ndio
muonekano wako. Sasa ukazane kula, urudishe nguvu.” “Ni-tajitahidi.” Sabrina
akacheka.
“Njaa
imekuzidia?” “Kido-go.” “Pole. Nasubiri kipoe, nikusagie kidogo ndio nikupe.”
Akamuona anamwita. Akasogea. Akamwambia anaomba amtafutie begi jeusi dogo
chumbani. Aliunganisha hayo maneno mpaka Sabrina akaelewa. “Nitalijuaje Tino?” Akamwambia
akifungua ndani atakuta vifaa vya mazoezi, zaidi mipira, mmoja utakuwa mdogo
kabisa. Akamuelekeza chini ya sinki bafuni kwake. Sabrina akatoka hapo na
furaha, akijua Tino ameamua kupona kweli.
Hiyo
nyumba ilipangiliwa vilivyo. Usingepata shida kupata kitu. Na kweli,
alipofungua chini ya kabati chini ya sinki, akakuta hilo begi dogo jeusi.
Akampelekea na kufungua mbele yake. “Unataka nikutolee nini?” Akamuomba mpira
mdogo kabisa kama kitenesi. Sabrina akaanza kupekua ndani ya begi, akakuta mipira
miwili ipo chini kabisa. Kijani na njano. Akatoa yote. Mgumu kidogo akapokea
mkono wa kushoto. Laini akamuomba amuwekee mkono wa kulia. Sabrina akafanya
hivyo. Akamuona anakazana kukunja ngumi, Sabrina akimwangalia. Alipofanikiwa
mikono yote miwili, akamuona anaanza kuminya taratibu.
“Ndio
mazoezi hayo?” Akatingisha kichwa kukubali. “Umenifurahisha sana Tino.
Hongera.” Akacheka huku akikazana kuminya ile mipira. Alikuwa akitetemeka kama
anayefanya kazi ngumu. “Ukimaliza kula, ukapumzika, nitakusaidia ya miguu.” “Sa-wa.”
Akarudi jikoni, akamuacha hapo sebuleni akiendelea kufanya mazoezi ya mikono.
Akasaga chakula, akakifanya kizoto kidogo, akatoka nacho. Akamkuta amekuwa
mwekundu.
“Pumzika
kidogo. Kula kwanza ndipo tuendelee.” Akamuona ametupa mipira yote kwa hasira.
Sabrina akaweka chakula chini, akaenda kuikota, Tino amegeukia pembeni. Akajua
amekasirika. Akaenda kukaa mbele yake kule alipogeukia. “Naomba niangalie mimi
Tino.” Macho pia yalishakuwa mekundu. Akamvuta mikono yote miwili. Akawa
ameishika. Akamgeukia. “Naomba jipe muda. Leo ndio umeanza. Hata ufahamu wako
umeshasahau ni nini unatakiwa kufanya. Mimi nipo na wewe. Nitakusaidia, mpaka
utaweza. Siwezi nikaondoka, nikakuacha huwezi kujisaidia kwa chochote. Sawa?”
Kimya.
Akaokota
mpira wa njano akamuwekea mkono wa kulia ambapo hauna nguvu. akamshikisha, na
kumfungisha ngumi. Akaanza kumsaidia kuminya ule mpira. Taratibu tu. “Unaumia?”
Akakataa. “Akaendelea huku akihesabu kwa sauti mpaka 9, kisha akamwacha,
akaminya mwenyewe lakini haikuwa kwa nguvu kama vile Sabrina alipomuwekea mkono
juu. “Si umeona? Tutafanya wote kwa muda mpaka mishipa, mifupa na misuli ielewe
na kukumbuka kinachotakiwa kufanya. Na kwa kuwa umeamua, nakuhakikishia ndani
ya mwezi mmoja, utaona tofauti kubwa sana.” Akamuona ameanza kutulia.
Akamuokotea
na wa kijani, akamuwekea mkono wa kushoto. “Usiwe na haraka na matokeo. Taratibu
tu huku ukila. Kwanza kule tu kukaa kwenye viganja bila kuanguka hiyo mipira,
huoni kama ni jambo zuri?” Akamtizama. “Usikasirike bwana! Lazima kuwa na
subira. Halafu nikwambie kitu?” “Ni-ni?” “Nilikununulia mafuta yakupunguza
miwasho ya kichwa, na kuondoa mba. Ila yanaharufu mbaya.” “As-ante.” “Karibu.
Halafu ukishiba, nataka nirudi kwenye duka la madawa. Kuna kitu nimeona online.
Unakiweka chini ya miguu yako wakati umekaa. Ukisimama, wakati nataka kukuweka
kwenye kiti, nakuzungusha tu kwa urahisi, kwakuwa kunakuwa kama kinakisahani
kwa ndani kinachozunguka. Nitakwenda duka la madawa la pale Mwenge na Masaki
nione kama wanavyo. Sitachelewa kurudi.” “Na m-imi.” Sabrina akacheka.
“Unataka
twende wote?” Akakubali. “Hujachoka?” Akakataa. “Sawa. Nilitaka tupitie
tulipotoka saluni, sema nilikuwa nimekasirika. Emma alinikera! Sijui yukoje
Emma jamani! Kama amechanganyikiwa!” “Pole.” “Yatapita tu Tino. Ukipona tu
wewe, na nikawa ninauhakika umeweza kujitegemea mwenyewe, nataka nikaanze kutafuta
kujijenga mwenyewe niache kuwa tegemezi. Nimeamua sitarudi tena nyumbani.” Tino
akamtizama kwa huruma.
“Najua
kufuga kuku na ng’ombe. Kwa nini nisianze kufuga kuku wangu mwenyewe nikauza?
Naamini sitashindwa. Eti Tino?” Tino akamkubalia. “Sihangaiki tena kutafuta
kazi, napoteza muda. Mambo niliyosomea ni kweli ajira zake ni za shida. Na kama
hufahamiani na watu, ndio kabisa. Nimepoteza muda mwingi nikitaka kuhakikishia
watu kuwa nimesoma kitu kitakachonilipa, lakini...” Akanyamaza akapotelea
mawazoni huku akimlisha.
“Unakipenda
hiki chakula?” “Zuri.” “Sikupika kingi, sikujua kama utapenda. Niambie unahamu
yakula nini?” Akawa anafikiria. “Niambie
chochote kile, hata kama hakipo hapa, nitakwenda kununua nipike.” Akafikiria,
akawa kama hajapata jibu. “Kwa kuwa sasa hivi unakula, ni vigumu kuchagua
chakula.” Wakacheka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Jioni
Sabrina na Tino wakiwa sebuleni mlinzi akawagongea kuwa kuna mgeni ametumwa kwa
Sabrina, achukue nguo zote alizopewa na Lela. Sabrina akatoka. “Habari kaka
yangu?” “Nzuri tu. Naitwa Jose, nimetumwa na Lela. Huwa namuuzia nguo zake.
Kila akitaka kubadilisha nguo, mimi ndiye huwa namuuzia za zamani.” “Sawa. Naenda
kukuletea, lakini nikuombe kitu, mwambia anipigie na mimi ili niwe na uhakika.
Kuwe na makabidhiano mazuri.” “Kweli kabisa.” Sabrina akarudi ndani, akasikia
simu yake ikiita.
Akarudi
kupokea akijua ni Lela tu. “Sabrina mdogo wangu! Bado umenikasirikia?” “Hapana
sijakasirika bwana. Ila kuna kijana amekuja, anaitwa Jose, amesema umemtuma
zile nguo.” “Ndiye ambaye ananiuzia kwa kina dada wanaojua nguo nzuri. Huwa
ananiletea pesa nzuri kweli!” “Sawa. Na hizi ambazo bado zipo kwenye hangers,
nimpe kama zilivyo au nizitoe nimkabidhi tu?” “Huyo mzoefu. Anavifaa vyote
vyakutunzia nguo. Wewe mpe tu. Atakaa hapo nje kidogo akizipanga kwa uthamani,
ataondoka zake. Usiwe na wasiwasi.” “Sawa.” “Nashukuru mdogo wangu.” “Usijali.
Na zile chupi?” Sabrina akauliza. “Kweli hutaki hata moja?” “Hapana. Asante.”
“Basi mpe tu vyote. Ataniletea huku, kesho nitakwenda kubadili.” “Sawa.”
Sabrina akakata simu.
Akamtolea
nguo zote alizokuwa amepewa. “Na huu ni mfuko wa kumpa yeye mwenyewe. Usiuze
vilivyopo kwenye huu mfuko. Amesema umfikishie.” “Hamna shida.” Akapokea.
Akapanga vitu palepale nje. Akaingiza pikipiki yake ndani. Akapanga vizuri.
“Vitu vyote hivyo unauza?” “Vingi nimeshapata wateja. Mida hii ya jioni
nakwenda kuwapelekea majumbani kwao au bar. Ila vipo vitu vya urembo kama
unataka.” “Hapana kaka yangu. Asante.” “Bado hujalipwa mshahara nini? Nakopesha
pia?” Sabrina akacheka. Akajua na yeye ameambiwa kuwa yeye ni mfanyakazi wake. “Hapana
kaka yangu. Nashukuru. Wakati mwingine.” Jose akachukua vitu vyake akaondoka.
Akarudi
ndani Tino akimtizama. Akaenda kukaa kochi jingine kabisa. Macho kwenye tv.
Akapoa kabisa. Akamsikia Tino anasafisha koo. Akamgeukia. “Nikuletee maji?”
Akamwita na kumuonyesha akae pale pembeni yake. “Hutaki maji tena?” Akakataa
akimuonyeshea aende akakae naye. Ikabidi anyanyuke na kuhamia kukaa hapo
alipokuwa amekaa Tino. Akaona anamshika. Sabrina akacheka kidogo, akamvuta
mkono vizuri, akamshika. Wakatulia wakiwa wameshikana mikono.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
S |
abrina na
Tino ukaribu wao ukaongezeka. Sabrina akawa analala chumbani kwa Tino. Tino
akakazana mazoezi. Hata akiangalia tv, atamuomba Sabrina amsaidie hiki au kile,
ilimradi tu afanye mazoezi. Juma hilo likaisha bila kumsikia Lela kabisa.
Walishatoka kwenda kununua vifaa vyakumsaidia Sabrina kumuhamisha kutoka sehemu
moja kwenda ingine kwa urahisi.
Juma
jingine la pili nalo likaisha bila kumsikia Lela. Tino akaweza kushika kijiko
vizuri kwa mkono wa kushoto na kujaribu kujilisha. Sabrina akiwa pembeni
akimwangalia bila kumwingilia. Hata alipochukua muda mrefu kula, alimtia moyo. “Utazoea
tu.” Wakaendelea wawili hao kutiana moyo peke yao bila hata hodi ya bahati
mbaya ya mpotea njia. Sabrina akawa akikazana na vyakula vinavyotia nguvu
mwili. Anahakikisha anakula kila mlo tena mzuri. Tino akaendelea kuongeza nguvu
hata mwili kuongezeka. Akaacha kuogea kitandani. Sabrina akawa akimpeleka
bafuni. Anamkalisha kwenye sinki kubwa yakuogea. Anamsaidia kumsugua sehemu
ambazo Tino mwenyewe hafikii ila anazoweza kufikia anajisugua na kujisafisha
vizuri tu.
Akaacha
kujisaidia kwenye chupa na magazetini. Sabrina akawa anampeleka chooni. Akishamfikisha,
anamuacha amekaa kwenye choo, anatoka kumpa faraga akimaliza anarudi kumsafisha
vizuri. Akaachana na kuvaa diaper. Tino akawa mtu wakuvaa nguo za ndani za
kiume. Anajifuta midomo mwenyewe. Taratibu nguvu za mdomo zikamrudia. Akaanza
kuweza kutafuna vizuri na kuzuia mate.
Juma
la tatu kuisha tokea Lela awaache hapo rasimi, Tino akawa anaweza kujivuta na
kupanda kigari chake. Akiona Sabrina amechelewa popote, basi alishitukia amemfuata.
Hakutaka kukaa mahali bila Sabrina. “Naona wewe umepona! Mbona sijachelewa
bwana!” Basi watakaa naye kama ni jikoni au chumbani kwa Sabrina kama amekwenda
kuoga. Anatoka bafuni, anashitukia Tino yupo chumbani ameingia anamsubiria.
Watakaa hapo chumbani wakiongea hili na lile. Hakuna aliyemtaja Lela. Lakini
Sabrina akashangaa kama ndio kusahau au la! Hakupiga simu kuuliza la kheri wala
la shari! Hata ile miahadi ya kumtafutia Tino nafasi ya kumuona daktari ili
Sabrina ampeleke, ikawa kimya! Hata ujumbe wa mwendelezo wake ikawa hakuna!
Haya, pesa yao ya matumizi pia hakuwa akituma! Sabrina akashangaa kuwa
anafikiri wao wataishije pale ndani bila pesa ya matumizi! Akaonelea ampe muda
zaidi.
Maisha
yakaendelea Sabrina akitumia mshahara aliolipwa na Lela kwa matumizi ya hapo
nyumbani, kwake na Tino. “Natamani kwenda kusuka Tino. Nywele zimeshakuwa
mbaya. Natisha!” Tino akamwangalia kichwani. “Twende wote.” Sabrina akacheka
sana. “Da Lela ataniua warembo wa pale Mwenge wakikuiba. Halafu huwa inachukua
muda mrefu sana. Utachoka.” “Kwa hiyo unataka kuniacha hapa peke yangu muda
wote huo!?” Hapo Sabrina akapoa, akakumbuka hali ya Tino bado kuna mambo
alikuwa akimtegemea yeye. “Samahani Tino, nimekusahau. Nitafumua, nizioshe tu.
Ukiweza kutumia choo peke yako, ndipo nitakwenda kusuka.” Tino akamwangalia na
kunyamaza.
“Unataka
nikurudishe kwa kinyozi?” “Utapata wapi pesa?” Tino akamuuliza. “Ninazo.” Tino
akamwangalia. “Utaanza kutisha tena. Nitamwambia Da Lela awapigie simu wale watu
wa ile saluni uliyokuwa ukienda zamani.” “Mwache kwanza.” Sabrina akatulia
kidogo kama akitafakari. “Kuna chumba kipo kwa nyuma ya hii nyumba. Kina
mashine zangu za mazoezi. Naomba uangalie funguo sehemu tunayoning’iniza funguo.
Ipo moja tu kwenye kidani cha nembo ya ramani ya Tanzania.” Sabrina akajua
hataki kumsikia mkewe. Hakuongeza neno. Akaenda kuangalia funguo, na kweli
akaikuta pale.
“Ni
hii Tino?” “Asante.” Akamuona anageuza kigari chake anarudi ndani. Sabrina
akamfuata nyuma. “Unataka twende ukafanye mazoezi sasa hivi?” “Kama hujachoka
tafadhali.” Akamsaidia kumvalisha nguo na viatu vya mazoezi, akatoka naye hapo.
Akamzungusha nyuma ya hiyo nyumba, wakafika kwenye hicho chumba. Sabrina
akafungua, wakaingia. “Waooo!” Sabrina akashangaa. “Pazuri!” Palizungushiwa
vioo chumba kizima. Kulikuwa na mashine mbili za kukimbia na iliyobeba vyuma
mbalimbali vya mazoezi. Vyuma vyenyewe vilikuwa vimepangiliwa vizuri.
“Tino
wewe ndio ulikuwa ukitumia huku?” “Kila siku ilikuwa lazima nije hapa. Kuna
utulivu wa namna yake. Na kulikuwa na tv kubwa sana hapa, nchi 72, pamoja na
redio yenye spika 4 kubwa. Nafikiri vimechukuliwa.” Sabrina akaendelea
kushangaa. Kulikuwa na makochi mazuri sana. “Nataka kujaribu kusimama hapo
kwenye mashine nione kama naweza kutembea kwa muda gani.” Wasiwasi ukamwingia
Sabrina. Tino akajua. “Nitaanza kwa spidi ndogo sana. Naomba usimame pembeni
yangu ili nisianguke.” “Hapo sawa. Niliingiwa na hofu! Sitaki uanguke tena na
kuumia.” Akajitahidi mpaka akasimama. Akaweza kuegemea upande wa kushoto,
akamwambia Sabrina awashe mashine. Kwa wasiwasi Sabrina akawasha akiwa
amesimama pembeni yake upande ule usio na nguvu sana. Akaanza kutembea hapo.
Kila Sabrina alipomshauri apumzike, alikataa. Alitembea mpaka jasho likawa
linamtoka kama mvua. Yeye mwenyewe anatetemeka, lakini bado alitembea.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Siku
tatu mfululizo Sabrina alikuwa akimleta hapo asubuhi na jioni. Anatembea,
halafu anaanza kunyanyua vyuma vile vilivyounganishwa kwenye mashine sio vile
vyakujitegemea. Taratibu kwa uzito mdogo mdogo, Sabrina akimsimamia ili
asijiumize. Alifanya hivyo akaweka mazoea, mpaka Sabrina ndiye aliyekuwa
akichoka. Analala kwenye kochi wakati mwenzie akifanya mazoezi. Atalala hapo
mpaka aamshwe kwenye saa nne usiku warudi ndani wakalale. Au mchana anakwenda
kupika, anamuacha hapo akifanya mazoezi.
“Mimi
naona kama unazidisha Tino!” “Nahitaji Sabrina. Naomba nitie moyo.” “Samahani.
Sina nia ya kukuvunja moyo, ila sitaki ujiumize. Vipi lakini?” “Si unaona sasa
hivi naanza kupata hata nguvu upande huu wa kulia! Natembea kwa kushika sehemu,
kitu ambacho kingechukua muda mrefu bila mazoezi.” “Naomba tukapumzike Tino.
Itoshe kwa leo. Umeshinda humu ndani siku nzima!” Tino akanyamaza. “Tino?”
“Sawa. Lakini kesho nataka unisindikize mjini.” “Sawa. Naomba basi nikupokee
hivi vyuma, twende tukale.” Akamkabidhi, wakatoka akitembea. Amemshikilia ule
upande wa kulia, taratibu wanarudi ndani.
“Unanuka
Tino!” Tino akacheka. “Nitaanza kuoga kwanza.” “Hapana. Glasi ya shake
niliyokutengenezea kwanza.” Tino akamwangalia nakunyamza kama anayewaza. Wakaingia
mpaka sebuleni. “Hapana Tino. Usikae bwana! Unatokwa jasho na unanuka. Kesho
utapachukia hapo. Twende bafuni, nakuletea hukohuko.” Tino aliendelea kucheka
tu, wakielekea bafuni chumbani kwa Tino. Akamuacha amekaa kwenye kiti cha
plastiki bafuni kabisa, akarudi jikoni. Alirudi Tino anaoga mwenyewe.
“Namalizia. Nitatoka muda si mrefu.” Sabrina akashangaa.
Tino
alitoka mwenyewe akitembea kwa kushika ukuta, akakaa mbele ya kioo kwenye kiti
maalumu cha hapo bafuni. Sabrina akakaa kwenye sinki kubwa ya pembeni, sinki ya
kuogea, akabaki akiwaza, Tino anajipaka lotion mwilini. Tino alimuona ameinama
kwa kupitia kioo cha ukutani. Sabrina akajua kazi yake inaanza kuisha. Umuhimu
wake kwa Tino unaanza kupungua. Nini chakufanya baada ya hapo? Wapi pakwenda
baada ya kibarua chake hapo kuisha. “Lakini si nyumbani!” Akawaza
Sabrina huku amejiinamia.
Tino
alimaliza juisi yote. Akageuka. “Upo?” Tino akamuuliza. Sabrina akanyanyua
kichwa na kumtizama, akakuta akimwangalia na amemaliza hata shake aliyokuwa
amemtengenezea, yeye hakuwa na habari. “Wakati unavaa, nakwenda kuandaa
chakula. Najua hutanihitaji hapa.” Akasimama na kutoka bila kusubiri nyongeza
kutoka kwa Tino. Tino akabaki kama hajaelewa. Yeye akaelekea jikoni kuandaa
chakula. Alishapika. Akakiweka mezani, akarudi jikoni akabaki akiwaza huko.
Tino kwa kutumia fimbo akaweza kufika jikoni. “Njaa inauma!” “Chakula kipo
mezani tayari. Twende tukale.” Siku hiyo usiku wakala kimyakimya mpaka
wakamaliza, Tino kimya na yeye akimwangalia. Akasafisha pale walipokula na
jikoni.
“Nakwenda
kuoga Tino. Nashauri na wewe ukajilaze upumzike. Lasivyo utashindwa kuamka
kesho.” “Naona ni wazo zuri. Naomba na dawa za maumivu.” Sabrina akampa na
glasi ya maji. Tino huyu alihitaji kulishwa tu vizuri na kutiwa moyo. Uhai wake
haukuwa mbali kama Lela alivyodhania. Ujio wa Sabrina ulirejesha tumaini kubwa
sana kwa Tino, na kuinua shauku ya kurudi kusimama tena. Akamsindikiza mpaka
chumbani kwake. Akamsaidia kuweka kitanda tayari wakati anasafisha meno,
alipokiweka sawa, akatoka hapo chumbani kwa Tino, akijua baada yakutoka hapo
atalala.
Sabrina alizima taa zote, akaenda kuoga, akaenda kujitupa kitandani kwake. Ilishakuwa ngumu kumshika Tino huyu. Anaanzia wapi kulala miguuni kwake tena! Hata kumchezea miguu ikawa kwa woga na aibu sio kama zamani. Tino huyu ni mzuri haswa, sio yule mchovu, mzoga kama alivyokuwa akimwita Lela. Hamfuti tena kinyesi. Alishaweza kujifuta mwenyewe. Muda mwingi aliacha kumuona akiwa mtupu, hata kumuona mtupu akaanza kuona aibu tena.
Tino kwa
Sabrina.
A |
lijilaza
pale kitandani macho kwenye simu. Akasikia mlango unagongwa. Akakaa. Tino
akaingia. “Hauji kulala?” Sabrina akababaika. Tino alikuwa msafi. Amevaa
suruali nyeusi ya kulalia na singlendi nyeupe. Ananukia kutokea mlangoni.
Akachechemea na fimbo yake mpaka kitandani akakaa. “Nilijua utakuwa umeshalala,
sikutaka niingie nikuamshe.” Tino akamtizama. Sabrina akainama. “Lakini
nilipanga baada ya masaa mawili nije kukuangalia ndipo nilale.” Tino akabaki
kimya kwa muda.
“Vipi?
Unajisikiaje?” “Umebadilika Sabrina. Sio kama ulivyokuwa mwanzoni. Nammiss
Sabrina wa mwanzoni kabisa.” Sabrina akacheka kwa woga, akainama. “Nini
kimebadilika? Tunakuwa mbali mbali!” “Hamna kitu. Labda kwa kuwa sasa hivi vitu
vingi unajifanyia mwenyewe ndio maana labda unaona tupo mbali mbali. Zamani
ulikuwa ukinihitaji kwa kila kitu.” Sabrina aliongea taratibu akizungusha simu
yake mkononi.
“Nakuhitaji
Sabrina. Bado nakuhitaji.” “Bado nipo Tino. Sitaondoka mpaka muda alioniambia
da Lela uishe.” “Lela siye anayekuhitaji. Mimi ndiye ninayekuhitaji. Yeye
anaweza hata kuja kesho na kukwambia uondoke, utafanyaje?” Sabrina akanyamaza
akifikiria. “Sabrina?” “Nitakuuliza wewe nifanyaje Tino. Ni kama sasa hivi
tunamtegemea yeye kwa kila kitu.” “Kwa hiyo akikwambia uondoke, utaniacha?”
Sabrina akanyamaza.
“Bado
nakuhitaji Sabrina.” Ikamgusa Sabrina akamwangalia. “Nipo hapa ni kwa sababu
yako. Umenitoa kwenye hali mbaya kwa chakula, maneno ya faraja na kuniombea.
Bado nakuhitaji. Kuna wakati kama binadamu naingiwa hofu, nashindwa kujua
itakuaje, lakini nikikumbuka wewe upo, inanitia nguvu.” Akaendelea Tino,
taratibu tu. “Naelewa kwa nini Emma, amebaki akihesabu siku tokea utoke kwenye
maisha yake. Maana ndiyo yanayonipata na mimi.” “Lakini mimi nipo hapa na wewe
Tino!” Akamsogelea na kumshika mkono. “Nipo Tino.” “Lakini sio kama zamani Sabrina.
Unaanza kuniaga siku hadi siku mpaka unanifanya nichukie kupona!” “Hapana Tino.
Sitaondoka mpaka tukubaliane mimi na wewe.” “Sasa kwa nini umebadilika?”
“Nahisi ni mawazo tu.” “Unawaza nini?” Sabrina akafikiria akimchezea mikono
yake, simu alishaweka pembeni.
Akamgeuza
viganja, akawa anapitisha mikono yake juu chini, juu chini akifikiria. “Nini
unawaza Sabrina?” “Sijawahi kujitegemea Tino.”
Akajifuta machozi. “Kwa muda wote nimekuwa hapa na
wewe, huwezi amini sijapokea simu hata mara moja kutoka kwa wazazi wangu
wakinitafuta hata kujua ninaendeleaje!” “Wewe umejaribu kuwapigia?” “Nilitamani kupata hata robo wanachompa Sabina, Tino. Siku
mbili haziishi bila baba na mama kujua Sabina anaendeleaje. Mimi ndiye
niliyekuwa nikitumwa kwenda kununua vocha/ bando ili apigiwe Sabina. Wakati
mwingine nilikuwa nafuata mbali kwenda kununua, na ilikuwa lazima wapate ili tu
kuzungumza na Sabina.” Tino akamfuta machozi.
“Nilikuwa
nikifanya kazi bila kulalamika pale nyumbani, lakini bado waliniona ni mtoto
niliyewaangusha. Mama alishaniambia mimi nimeandikiwa shida tu. Fungu la kukosa
na sijuagi kufanya maamuzi sahihi, ndio maana nilisoma vitu vya ajabu. Sasa
nilipokuja kuachwa na Emma, ndio ikawa shida zaidi. Maana ili angalau wanione
wa maana, nilipompata Emma, nikamtambulisha kwa Sabina nikijua angalau
atamwambia mama kwa namna yake sitaingia matatizoni, kuwa kwa nini nina
mwanaume, halafu ingeniongezea heshima. Na kweli mama alipojua japo mahusiano yangu
na Emma hayakuwa rasmi lakini angalau nikaheshimika. Sasa aliponiacha, mama
akasema alijua tu nisingeweza kuwa na mtu kama Emma. Sina akili wa uwezo wa
kutunza vitu vizuri.” “Pole sana Sabrina.” Tino akamuhurumia.
“Lakini
Tino, nimeamua kubadi maisha.” “Utafanyaje? Ndio unapanga kunikimbia?” Sabrina
akacheka taratibu huku bado wameshikana mikono. “Nimekuahidi sitaondoka mpaka
tukubaliane.” “Unataka kwenda wapi?” “Jana na leo nimekuwa nikizungumza na Jack.”
Tino akatoa macho. “Jack yule aliyekuwa raisi wa chuo ulichosoma Dodoma?”
“Kumbe ulikuwa ukinisikiliza tokea mwanzo!” “Vizuri sana. Huoni nilianza kuhangaika
ili nipone! Nilikuwa nakula si kwa sababu nilikuwa ninahamu ya chakula,
nilikuwa nakula kama dawa, sababu yako.” Sabrina akacheka.
“Unataka
kurudiana na Jack?” “Hapana. Kusema kurudiana si sahihi kwa kuwa kama
unakumbuka nilikwambia nilimkataa, tena vibaya sana. Nilimaliza chuo yeye akiwa
na msichana wake. Hakuja kunitongoza tena japo alinisaidia sana. Swala la
mapenzi lilishapotea katikati yetu. Ila Jack ni wale watu wanaopenda kusaidia
sana. Hajui kumkatia mtu tamaa, kama nilivyokusimulia vile jinsi alivyosimama
na mimi mpaka nikamaliza shule.” “Nakumbuka.” “Basi kwa sasa yupo Singida. Ni
muhasibu wa wilaya ya Singida mjini. Nilikuwa nikimcheka kuwa amekimbia jiji,
lakini anasema huko alipo kunamsaidia kimaisha. Amenipa dili za biashara. Anasema
naweza kufanya naye biashara. Atatoa mtaji. Tukusanye mafuta ya alizeti ambayo
yapo kwa wingi huko na bei nzuri. Tuyaweke kwenye chupa za ujazo tofauti
tofauti pamoja na ulezi, kisha tusambaze hapa nchini. Anauhakika tutafanikiwa
tu.” Tino akanyamaza.
“Lakini
hata leo nimemwambia nina jukumu nimepewa kwa muda wa miezi mitatu, ndipo
naweza kuanza, ila kama mambo yakibadilika kabla au baada ya huo muda, kwa kuwa
tunaendelea kuwasiliana, nitamjulisha. Kwa hiyo sitaondoka mpaka tuone upo sawa
peke yako. Unaponiona nakuwa kimya, nakuwa na mengi yanaendelea Tino. Lakini
wewe huusiki. Na huwa nakupa nafasi yakufanya mambo yako peke yako kwa uhuru.
Najua ukikwama utaniambia. Si ndio?” Tino akabaki akifikiria.
“Naomba
usiwaze mbali Tino. Siwezi kukuacha nikijua bado unanihitaji.” “Nakuhitaji
Sabrina. Bado nakuhitaji. Najua nakuwa kama nakuchelewesha, lakini ukiondoka
sasa hivi utanirudisha nyuma kabisa.” Sabrina akajisikia vizuri kuhitajiwa na
mtu kama Tino! Japo hakuwa na hela hapo alipo, alikuwa akitumia pesa aliyolipwa
na Lela hata kumtunza huyo Tino, lakini alimfurahia Tino. “Nipo na wewe Tino.”
“Basi iwe hivyo na vitendo. Naomba usibadilike. Tuzungumze kama zamani. Bado
nahitaji masaji ya miguu.” Sabrina akacheka na kujificha uso.
“Kumbe
ulikuwa ukipenda!” Sabrina akauliza kwa aibu. “Nahisi kama ndio imenisaidia kwa
asilimia kubwa kufanya damu isafiri miguuni nakuanza kupata nguvu. Unakumbuka
vile ulivyokuwa ukinifanyia kuanzia juu mpaka chini kwenye nyayo?” Sabrina
akatingisha kichwa kukubali. “Nahisi imenisaidia sana. Bado sijarudi kuwa na
nguvu kabisa. Usiishie njiani. Nguvu ileile uliyoanza nayo ndio uendelee hivyo
hivyo.” “Nilijua hunihitaji tena kama zamani.” “Umesahau tu Sabrina. Wewe ndio
umeniambia niungane na wewe. Nafanya hivi ili kukutia moyo na wewe. Nafanya
haya yote kwa ajili yako, ukiacha na mimi utanivunja moyo.” “Nimefurahi kusikia
hivyo Tino, na asante kuniambia. Nitajitahidi.” Wakatulia hapo.
“Twende
ukalale. Umekuwa na siku ndefu.” Sabrina akaongea kwa kubembeleza. “Unajua
nilipokuwa peke yangu nikawa nikilala kwa shida. Ukaja ukanizoesha kunibembeleza
mpaka nalala.” Sabrina akacheka sana kwa aibu. “Nilikuwa nakufanyia masaji
bwana!” “Na kunichezea nywele pia.” Sabrina akajificha uso. “Kumbe ulikuwa
ukinichora tu! Unajidai huwezi hata kuzungumza!” Tino akacheka sana. “Nilitaka
kukusoma na wewe kujua moyo wako.” “Basi umechukua muda mrefu sana kunisoma.
Mpaka nikakuomba uongee!” Tino akacheka.
“Twende.”
Sabrina akaruka pale kitandani kwa furaha, akamsaidia kusimama. Wakatoka huku
amezungusha mkono kiunoni upande wa kulia. “Kwa hiyo Jack amerudi kwenye
picha?” Tino akarusha swali na tabasamu usoni akimtizama wakiwa wanatembea.
“Hata sijui Tino. Ila ninachojua Jack ni mwema sana. Tumekuwa tukiwasiliana
tokea zamani. Sema mimi ndio nimekuwa mzito wa mawasiliano. Lakini yeye ni mwepesi.
Muda na wakati wowote ukimtumia ujumbe tu, anajibu au kupiga.” Tino
akamwangalia tena, akanyamaza.
Akapanda
kitandani akajilaza Sabrina akapakata miguu yake, akaanza kumfanyia masaji
taratibu lakini safari hii hakulala. Akabaki akimwangalia. “Unataka kesho
twende wapi?” Sabrina akauliza, Tino akacheka kwa kuguna kidogo. “Nataka
kufanya kitu ambacho nilitamani kukifanya muda mrefu sana lakini nilikuwa sina
uwezo.” “Sababu ya kuugua muda mrefu?” Akadodosa Sabrina taratibu. “Nafikiri
sababu ya ujinga kama anavyosema Lela.” Sabrina akatamani kuuliza zaidi, lakini
kwa ujibuji ule, akaona anyamaze. Tino alijibu kwa uchungu. Sabrina akaendelea
kumpapasa miguu. “Unataka nikupitishe kwa kinyozi kabla?” “Huna hela wewe.
Nimekuona manunuzi uliyokuwa ukifanya hapa.” “Sitakosa pesa ya kulipia kinyozi
Tino. Ndevu zinaanza kuwa ndefu na nywele zimeshakuwa. Kama unakwenda kukutana
na watu wa maana, angalau uende ukiwa upo msafi.” “Ni kweli.” Akakubali.
“Unataka
nimtaarifu Da Lela?” “Achana na ‘Da Lela’.” Sabrina akacheka jinsi
alivyomugilizia kumwita ‘da Lela’ na si dada Lela. “Atakasirika akijua kama
nimekutoa hapa bila yeye kujua.” “Na kweli ujiandae. Maana najua kesho atakuwa
hapa.” “Amekwambia?” “Kwa nitakachofanya kesho, lazima mwanamme wake
huko atamfukuza, atarudi hapa kunitukana.” Sabrina akashtuka kidogo. Hakujua kama
Tino anajua kama Lela ana mwanaume. Akaona anyamaze asije akaanzisha jambo jingine.
Akajivuta
pembeni, kulekule chini ya miguu, akajilaza. “Hapo haumii?” “Hapana. Nipo tu
sawa. Kuna kitu unataka kabla sijapotelea usingizini?” “Hapana. Wewe lala tu.”
Akampapasa vinyweleo vya miguu taratibu. “Nywele zimeota Tino. Utataka
nikuonyoe?” Akamsikia anacheka. “Mimi mtoto wa kiume Sabrina. Acha kunitengeneza
ngozi kama mtoto wa kike.” Sabrina alicheka sana. “Kumbe ulikuwa hutaki!? Mbona
hukuniambia?” “Kwa wakati ule nilikuwa sina uchaguzi. Ilikuwa lazima kutoa
vinyweleo vyote ili kutibu ngozi. Sasa nikaona umetoa kote!” Sabrina akazidi
kucheka mpaka akakaa.
“Tino
wewe mbaya mbana. Ulitulia kimya!” “Nikawa nikikusikiliza tu unavyonisifia.
Mara ninangozi ya kitoto. Mara nina nywele nzuri! Sasa nikajiuliza, mnyoaji
huyu mbona hatoi za kifuani! Ukazizunguka wee, ukapunguza tu na kuzichonga
vizuri ila zenyewe ukaziacha! Nikajiambia umezipenda.” Sabrina alicheka mpaka akajifunika uso na mto. “Tino!” “Wewe kuwa
mkweli tu.” Tino akamsuta. “Si kwa kuwa kifuani hukuwa na mapele au madonda!”
“Kwani mgongoni nilikuwa na mapele?” Sabrina akazidi kucheka. “Sasa ukilala
nakunyoa kifuani.” “Huwezi. Ulivyozitengeneza vizuri hivyo! Najua huthubutu.
Kwanza nakuonaga jinsi unavyotuliaga ukifika kusafisha hapo. Mpaka najiambia
sijui kama tutamaliza tena.” “Bwana Tino unanisingizia mimi.” “Sawa! Pengine ni
vile hujijui.” “Najijua sana. Na kesho nazinyoa zote.” “Labda mgongoni kwa kuwa
huko ndiko nilikuwa nikienda wananifanyia waxing.” Sabrina akakaa vizuri.
“Kwa
hiyo huwa ulikuwa ukitoa za mgongoni tu?” “Itabidi nikutafutie picha zangu za
zamani ili unifahamu vizuri.” Sabrina akacheka taratibu kama anayemfikiria.
“Kwa hiyo hapo bado hujafikia zamani?” Tino akacheka tu na kunyamaza. Sabrina
akarudi kujilaza hapo miguuni. Akajifunika vizuri, akaamua alale. Aliamka mara
kadhaa kumtizama, akamkuta yupo sawa. Wakalala hapo mpaka asubuhi.
Sabrina
aliamka akashangaa Tino amelala pembeni yake. “Tino!” “Ilibidi nigeuke,
nilihofia kukupiga mateke nikiwa usingizini.” Sabrina akacheka taratibu Tino
akimwangalia. “Ulilala vizuri sasa?” “Sana!” Akajibu Tino, Sabrina akacheka na
kumruka hapo kitandani akashuka. Yeye akaelekea jikoni, Tino mazoezini.
Akaandaa kifungua kinywa bado Tino hakuwa amerudi. Akaamua kwenda kujiandaa na
hiyo safari ambayo alitamani kumuaga Lela lakini Tino alimkatalia. Akaanza
kuwaza juu ya muonekano wake. Sabrina hakuwa na rangi nyeupe wala mweusi. Maji
ya kunde tu. Na sababu ya kazi nyingi, na mawazo, hakujua kama kwa asili ndio
alinyimwa mwili kabisa au pengine angepata nafasi nzuri mwili ungeongezeka.
Maisha yake yote alikuwa mwembamba. Na wakati wote alikuwa na kazi ngumu au
majukumu yakumfanya afikiri zaidi ya kawaida. Hata mikono yake ilikuwa ni
migumu ya shuruba kama mikono ya mwanaume mwenye shuguli nyingi za mikono.
Rasta za mabutu makubwa alizokuwa amesukwa mtaani kwao, zilishafumuka,
hazikuonekana safi hata kidogo. Akajitizama mara kadhaa kwenye kioo. Hakujua
chakufanya na hizo nywele.
Akaoga
na kuvaa moja ya gauni alilokuwa amenunua siku alipompeleka Tino kwa kinyozi.
Ilikuwa gauni refu mpaka chini. Na mara nyingi alipenda kufunika miguu,
hakupenda miguu yake. Alisema haina umbo. Imenyooka juu mpaka chini. Wakati
mtoto walikuwa wakimtania miguu kama fito. Kama hakuvaa suruali, basi gauni
refu kabisa. Nguo chache sana ndizo zilikuwa fupi, tena fupi haswa ili
kuonyesha angalau unene kidogo wa mapaja. Tena alipokuwa na Emma, lakini si
maeneo ya nyumbani kwao.
Akajipenda
vile lile gauni lilivyomkaa. Akacheka. Akaweka hereni. Mtihani bado ukawa
nywele kichwani mwake. Akahangaika hapo kwenye kioo, mwishoe akaamua vuta zote
juu na kuzisuka butu moja kisha akazungushia kitambaa chembamba cheupe,
kuzunguka kichwa. Gafla akajipenda. Akaonekana msafi sana kichwani. Kule
zilipofumuka, kukazibwa na kitambaa. Juu kibanio kisafi. Na zile hereni, angalau
akajipenda.
Katika
hekaheka zote hizo kumbe na Tino alishakwenda kuoga. Wakati yupo jikoni
akimalizia kuweka mambo sawa, Tino naye akatoka akamfuata jikoni. “Umependeza
Tino!” “Hata wewe umependeza. Lakini nimebadili mawazo.” “Hatuendi tena?”
“Hapana. Ila nafikiri umeshahangaika vyakutosha. Hiki ninachoenda kukifanya
leo, kitaibua kichaa cha Lela. Na ninauhakika hutataka kumuona akiwa kama tembo
aliyejeruhiwa. Utajuta kunifahamu.” Sabrina akabaki kama haelewi.
Lakini
akaona aulize tu. “Kwa hiyo unataka nichukue mizigo yangu niondoke moja kwa
moja?” “Ndiyo. Lakini si uliniambia ulipanga kama ukitoka hapa, utaondoka
kwenda kujitegemea bila kuwataarifu nyumbani kwanza?” “Ndivyo nilivyokuwa
nimepanga.” Sabrina akajibu akiwa ameishiwa nguvu. “Basi naomba ibakie
hivyohivyo kwa sasa.” Sabrina akawa hajaelewa.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Tino anaanza kurudia enzi na kwa mara ya kwanza baada ya muda mrefu, anataka kutoka. Anakwenda wapi? Kipi anapanga kumfanyia mkewe? Usikose muendelezo kujua kitakachojiri kati ya Tino&Lela na Sabrina & Tino.
0 Comments:
Post a Comment