Tino afanya mapinduzi.
“Si
umesema mpaka tukubaliane?” Sabrina akatingisha kichwa kukubali. “Basi bado
tutakuwa wote. Mambo mengi nakutegemea wewe.” Sabrina akajisikia vizuri. “Sasa
naomba msaada wakubeba begi. Nimeliandaa lipo tayari. Weka kwenye gari kabisa,
pamoja na kila kitu chako. Usichukue kitu chochote kile alichokupa Lela au ulichokikuta
huko chumbani. Sitaki aje akulaumu.” “Bado atanilaumu tu Tino. Ataona
nimemgeuka.” “Nikuombe kitu kingine kigumu?” Sabrina akakubali. “Kwa kuwa
umekuwa ukiwasiliana na Jack, mwambie hutakuwa hewani kwa muda. Kisha zima simu
kabisa ili usichanganywe na simu za Sabina, na pengine Lela mwenyewe.
Sitashangaa kama atakwenda kukutafuta hata kwa wazazi.” “Tino!” “Kweli tena.
Linapokuja swala la pesa, huwa Lela hana undugu wala aibu. Sasa nataka
nikafunge mianya yote ya pesa zangu alizokuwa akimtunzia mwanamme wake hapa
mjini. Kisha nitamtafuta sasa tuje tuwekane sawa. Nitampigia kumtaarifu kuwa
mimi nimekutoa pale nyumbani.” “Basi naomba na mimi nimtumie huo ujumbe kuwa
umenitoa hapa nyumbani, nimekwenda kuanza maisha yangu. Hivyo hivyo kwa Sabina,
ndipo nizime simu.” “Sawa.” Wakakubaliana.
Tino
akachukua hati zote za nyumba na magari. Akaweka kwenye gari wakati Sabrina
anakusanya vitu vya muhimu ambavyo alijua angevihitaji kwenye kuanza na Tino.
Akaweka kwenye gari. Wakati wanahangaika kukusanya vitu, kwa mara ingine tena
baada ya muda mrefu sana Tino akawa ameweka simu yake kwenye umeme ili arudi
kuwa hewani. Sabrina alikuwa amejawa furaha, asijue kwa nini. Wakapata kifungua
kinywa pamoja, Tino akajisaidia tena, wakatoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Wakaanzia saluni. Safari hii Tino alishuka kutoka kwenye gari akitumia magongo, lakini la upande mmoja tu. Akachechemea mpaka ndani. Wale vijana wakashangaa. “Naona sista umekazana mpaka ametembea!” Wakacheka. “Vipi, staili ni ileile?” Wakamuuliza Tino wakati wanamfunika ili asichafuke. “Tafadhali.” Akajibu Tino na tabasamu. Sabrina akakaa. Walimtengeneza Tino vizuri! Na kwakuwa aliongezeka mwili na uhai ulisharudi usoni, akapendeza sana. “Umependeza!” Sabrina akanong’ona. Tino akacheka wakiwa wanaangaliana kwa kupitia kioo. “Asante.” Na yeye akashukuru kwa kunong’ona akimwangalia kwa kupitia kioo.
Akasubiria
hapo mpaka akamalizwa na kusafishwa kabisa. Akatoka Tino wakuvutia zaidi. “Sasa
twende kwanza benki, niangalie hali ilivyo huko.” Wakaamua kwenda kwenye tawi
la benki lililopo Mlimani City ambako ni karibu na hapo walipokuwa. Tino
aliingia moja kwa moja ofisini kwa meneja akiwa na Sabrina, akaomba salio za
akaunti zake zote. Akaandikiwa kila moja. Sabrina akashangaa amebadilika rangi,
anatetemeka. “Haiwezekani!” Akasikika Tino. “Unauhakika hujakosea namba hata
moja?” Akamuuliza tena yule meneja. Akaanza akaunti ya kwanza, akamgeuzia laptop.
Sabrina akaona 0.00. Ya pili nayo ilikuwa ya mshahara, ikaonekana kila mshahara
ulipokuwa ukiingia, unatolewa kama ulivyo. Ya tatu ambayo ilikuwa yake na Lela,
ndiyo ilikuwa na pesa ambazo wakamuona Tino anafuta machozi. Ni akaunti ambayo ndipo
ilipoingia pesa aliyolipwa baada ya kushinda kesi. Yalikuwa mamilion ya pesa,
Lela alishatumia kama nusu yake.
Akainama
kwa muda mbele ya yule meneja na Sabrina. “Tino!” Sabrina akaita kwa upole.
Akamwangalia na macho mekundu haswa kisha akamtizama yule meneja wa tawi hilo
la benki. “Nafunga akaunti zote, nataka kufungua mpya. Inawezekana au nihamishe
pesa yangu sehemu nyingine?” Akawa amekasirika, Sabrina akamshika mkono.
Akatulia. Yule meneja kwa haraka akamsaidia kufungua akaunti ingine kwa jina
lake tu. Akahamisha pesa yote hapo. Akafunga akaunti zote akabakisha moja tu
ile aliyokuwepo pamoja na Lela lakini hakumbakishia pesa hata shilingi moja. Akachukua
pesa kiasi. Alipomaliza hapo, wakatoka.
Akamuelekeza
ofisini kwao. Ilikuwa Kinondoni karibu na Ubalozi wa Ufaransa. Sabrina akatoa gari
hapo Mlimani City kuelekea huko. Tino alikuwa amekasirika, akashindwa kuficha
hisia zake. Akamuona anapiga simu ya kwanza. Akamsikia anasalimia kwa heshima,
akajua ni mtu mzima. “Naomba huduma yenu tena.” “Mkeo
alitufukuza Tino. Kwanza alitangaza unakaribia kufa, umepoteza ufahamu kabisa,
yeye hana uwezo wa kutulipa.” “Naelewa Mzee wangu. Lakini alishahama pale. Na
mimi nasafiri kwa muda, naomba ulinzi wa mchana na usiku. Kusiruhusiwe mtu
yeyote kuingia hapo mpaka nitakaporudi.” Sabrina akashangaa sana.
Akamuomba baada ya lisaa, wakutane nyumbani kwake na mlinzi atakayeanza.
Sabrina kimya.
Akampeleka
mpaka ofisini kwake, kimya. “Tunaweza kwenda wote.” “Kama si lazima, naomba
nikusubiri hapa Tino. Naepuka maneno.” Sabrina akaongea kwa kujihami. Tino
akafikiria kidogo, akakubaliana naye, akashuka. Sabrina akabaki akifikiria hapo
kwenye gari. Baada ya kama dakika 13 hivi akamuona anatoka. “Umefanikiwa?” Akauliza
taratibu wakati anamsaidia kumfunga mkanda. “Nimemaliza. Kwanza hawakuamini
nilipoingia pale. Ilikuwa ni kama wameona mzimu. Muhasimu ikabidi aongee tu. Akaniambia
waliambiwa na Lela hata madaktari wamesema sitapona tena, eti nimepewa muda
mfupi wa kuishi.” Sabrina akashangaa sana. “Tino!” “Najua ni kwa nini
amewaambia hivyo pale ofisini. Kwa kuwa ili kila mwezi nilipwe mshahara, masharti
ilikuwa nilazima wahakikishe na mimi natibiwa ili nipone, nirudi kazini
nisiendelee kuwaingiza hasara bila kuwaingizia faida. Maana hakuna anayetaka
kuendelea kumlipa mtu ambaye hafanyi kazi. Mpaka lini! Sasa ndio alikuwa
akiwadanganya ili kuwafariji mwisho unakaribia, akijua wazi nitakufa, alipwe
sasa pesa nyingi ya mwisho.” Sabrina akaumia sana.
“Sasa
na mimi nikajaza fomu zakumtoa kwenye matibabu wanayomlipia hapa kazini, na
kuhamisha mshahara wangu kuwaambia uingie kwenye hii akaunti mpya. Namuhurumia
sana Lela.” Akaongea akisikika na hasira. Sabrina akavuta pumzi kwa nguvu.
“Tunakwenda wapi?” “Tunarudi nyumbani kwanza.” Sabrina akatoa gari hapo
Kinondoni kurudi Kunduchi. Akamuona anapiga simu ingine tena. “Ni wewe mwenyewe bosi wangu au!?” Sabrina akamsikia
mtu wa upande wa pili akihamaki. “Ni mimi mwenyewe
Chalii! Habari?” “Habari ya mji ni umekuwa mlemavu wa mwili na akili. Nilisikia
huna hata uwezo wakuzungumza bosi wangu!” Tino akatingisha kichwa kwa
kuumia sana. “Sio habari za uongo sana. Mungu
amenirejesha. Lakini ninashida na huduma yako. Unakumbuka aina ya vitasa
ulivyoniwekea mlango wa mbele na nyuma?” Sabrina akabaki akisikiliza,
akajua Tino ameamua.
“Ninavyo ila bei imepanda sana. Si unajua uimara wa vile vitasa?”
“Ndio maana navihitaji vilevile. Unaweza kuja baada ya lisaa ili unibadilishie
kabla sijasafiri? Naondoka leo.” Wakazungumza
kidogo, wakakubaliana wakutane nyumbani kwake. Sabrina akaendelea kukanyaga
mafuta kurudi Kunduchi.
Ukweli kwa
Kilichompata Tino.
S |
abrina
akamgeukia kumuona anahali gani ili amuulize swali lililokuwa kichwani mwake. “Nikuulize
kitu Tino?” Tino akamgeukia. “Kwa nini ofisini kwenu wanaendelea kukulipa kama
walishakulipa fidia?” “Nina hasira nao wale, acha waendelee kunitunza tu.
Wamenisababishia matatizo ambayo leo ndio nilikuwa nikiwaambia. Nakwenda
kufanya matibabu ya mwisho. Nikishindwa kupona, wataendelea kunilisha mimi na
vizazi vyangu vyote.” Akamuona hasira inazidi kupanda.
“Huu
mkono ambao hauna nguvu, ndio mkono unao niweka mjini.” Sabrina akawa
hajaelewa. “Kwa kuwa ni wa kulia?” “Kwa kuwa ndio niliokuwa nikiutumia kufanya
kazi. Mimi ni mchoraji. Nikipaji nilichokuwa nacho tokea mdogo. Nilikuwa nikichora
kitu au mtu, utafikiri umepigwa picha. Ile kampuni ipo pale mpaka sasa wanamamilioni
ya pesa ni kwa sababu yangu. Niliwaingizia sana pesa na bado mpaka sasa wanajiingizia
pesa kwa kutumia ramani zangu. Niliingia nao mkataba. Walipoona wanauza sana
ramani zangu mimi, tena kwa mapesa mengi sana kuliko vijana wengine tuliokuwa
nao kitengo kimoja, na mkataba niliokuwa nimeingia nao wao ulikuwa
tumekubaliana kila wakiuza, mbali na mshahara wanipe asilimia fulani ya hayo
mauzo. Sasa wawili wa wale vijana tuliokuwa nao kitengo kimoja na mmoja wa
mmiliki wa ile kampuni wakanigeuka. Wakati huo Lela alikuwa anataka niondoke
pale, nifungue kampuni yangu kwa kuwa alisema kazi zangu zinauzwa sana. Sina
sababu yakumfanyia kazi mtu.” Akaendelea.
“Sasa
mimi nilikuwa najua aina ya mkataba nilioingia na ile kampuni. Ulikuwa
hauvunjiki mpaka kwa miaka hiyo tuliyokuwa tumekubaliana. Lela haelewi anataka
nitafute mwanasheria anisaidie kuvunja mkataba. Mimi sio mtu wa tamaa ya pesa.
Nikamwambia napenda pesa ila naheshimu makubaliano niliyofanya na kampuni.
Nitasubiri mpaka muda uishe. Sasa kama nilivyokwambia, mmoja wa wamiliki wa ile
kampuni akaungana na wale vijana, wakaiba moja ya ramani ya jengo moja tulilokuwa
tumekubaliana kuwauzia watu wa Nairobi. Mimi nikaitengeneza vizuri. Kumbe
wakati mimi nahangaika ikamilike, wao wanatafuta mteja mwingine.” “Tino!” Sabrina akashangaa.
“Sasa
walivyo wajinga, wakauza kwa mtu ambaye na yeye akarudi kumuuzia yuleyule mteja
wa kwanza. Wakapata pesa nyingi sana, wakagawana. Kampuni inampelekea mteja
ramani, mteja anasema haitaji tena, amepata ingine kama ileile ila kwa pesa
nzuri. Kuona, ni kama ile. Ikaanza kesi. Mteja akasema ameuziwa. Alipokamatwa
aliyemuuzia, akasema na yeye ameuziwa na mfanyakazi wa pale, anaitwa Costatino.
Moja kwa moja wakaja kunikamata huku nchini na kunifunga bila kutaka
kunisikiliza. Si ndio nikatafuta mwanasheria?” “Ndiye huyo da Lela
alikutafutia?” Tino akamwangalia kwa kushangaa.
“Lela
anitafutie mwanasheria wakunitoa jela wakati aliniambia nimejitakia mwenyewe!
Hakutaka hata kujihusisha mwanzoni mpaka aliposikia nimeshinda kesi, nalipwa
fidia. Hapo ndipo akajirudi. Lakini nilishaanza kuugua. Sababu ya mshituko
nilipokuwa jela, pressure ikaanza kunisumbua wakati sikuwa na hayo matatizo.
Hata nilipotolewa kwa dhamana na kesi ikawa ikiendelea, nilikuwa nimepokonywa
mpaka ile nyumba.” “Tino!” “Acha Sabrina. Pale ndipo nilipojua rangi zote za
Lela. Alininyanyasa yule binadamu! Mpaka nikaanguka na stroke. Kesi inaisha,
nashinda kesi, sina hata raha na ile pesa. Alichofanya baada ya kurudishiwa
kila kitu ni kunifungia kwenye kile chumba, basi. Na nikwambie tu ukweli
Sabrina, sikupata stroke mbaya sana. Inaitwa partial stroke. Kama
angenihudumia kama ulivyofanya wewe tokea zamani, nisingefikia ile hali
uliyonikuta nayo.” “Pole Tino.”
“Hali
ilizidi kuwa mbaya kwa kukosa lishe nzuri, wala si stroke na ndio maana ulipoanza kunihudumia wewe sikuchukua muda
mrefu sana kusimama. Sasa ndipo mwanasheria wangu akaniambia kwa kuwa wao ndio
wamesababisha kupoteza nguvu za huu mkono, tena Lela alikuwepo siku nazungumza
na yule mwanasheria. Akasema naweza kuendelea kudai ule mkataba wa zamani wa
kazi. Na hata ukiisha, uongezwe ili nibakie kuwa mfanyakazi wao waendelee
kunilipa hata kama sitaweza kuwafanyia kazi kama zamani. Ndipo nikamuomba sasa
anisaidie kisheria.” “Sio Lela?” Tino akacheka akitingisha kichwa.
“Wewe
kwa sehemu umeishi na Lela ulishamjua. Kila jambo anakimbilia kulisema yeye nje
kwa watu ili watu wamuone yeye ndio amefanya, asifiwe. Lakini mwanasheria wangu
ndiye aliyenifuata pale nyumbani akaniambia. Tukaweka hayo madai. Wakanilipa na
mshahara wangu wote tokea nipo jela na kuendelea kunilipa na wakaamuriwa na
mahakama, wahakikishe napona. Yaani wagaramie matibabu yangu yote. Yule mmoja
wa mmiliki aliyehusika, alifukuzwa kwenye ile kampuni bila kulipwa kitu pamoja
na wale vijana wakafukuzwa kazi bila fidia ili wasifungwe.”
“Ila
Sabrina, Lela amekula pesa yangu vibaya sana. Na ninajua ni kwa kuwa alijua
malipo ya mwisho baada ya kifo changu yanakuja hivi karibuni ndio maana
alitapanya hivyo.” Sabrina akabaki akisikiliza huku akiendesha. “Na ninajua
hata huyo mwanaume wake anampenda sababu ya pesa yangu tu. Lela sio mwanamke wa
kuweka ndani kama yule mwanamke uliyenisimulia Emma alimkimbilia badala yako.”
“Kasandra?” “Yeah! Kasandra.” Tino akakubali.
Walifika
nyumbani, Tino akamuomba Sabrina amasaidie kuongeza baadhi ya vitu alivyojua
angevihitaji zaidi, akamuongeza na nguo. “Kwani tunakwenda wapi Tino?” “Moshi.
Nataka niwe mbali na huu mji kwanza mpaka nipone kabisa. Nitatibiwa katika
hospitali ya KCMC mpaka nipone ndipo nijipange kwa upya.” Sabrina akalifurahia
hilo. Hata yeye alikuwa tayari kuwa mbali na watu wa nyumbani kwao.
Mwenye
kampuni ya ulinzi alifika muda mfupi baada ya fundi vitasa. Alishaanza kung’oa
vilivyokuwepo na kuweka vipya. Tino akarudisha mkataba wa zamani waliokuwa nao
na hiyo kampuni ya ulinzi akitaka ilinde hapo masaa 24. Akalipia na kumwambia
yule Mzee awaambie walinzi wake kuwa, wasimfungulie yeyote yule hilo geti.
Wakakubaliana akaondoka wakati Sabrina akiendelea kupakia vitu garini. Akahamia
vya jikoni alivyojua angehitaji kwenye makao mapya. Mashine za kusagia vyakula
na juisi. Na vyombo baadhi. Akawa amemaliza. Akatoka kumsubiria Tino.
Maisha
mapya ya Tino & Sabrina.
Hotelini.
M |
paka
wanamaliza kila kitu hapo nyumbani kwa Tino, ilishafika saa 10 jioni. Tino
akamwambia wakatafute hoteli walale, waanze safari asubuhi na mapema. “Pumzika
leo dereva wangu. Kesho tuanze safari ya Kilimanjaro. Nakutegemea wewe
kulifikisha hilo gari huko.” Sabrina akacheka huku akifikiria. “Usiogope.
Ukichoka, tunalala hotelini, kesho yake tunaendelea na safari.” “Nitakufikisha salama.
Usiwe na wasiwasi.” “Wewe tena! Mbona mimi nitakuwa nalala tu.” Wakacheka na
kuendelea kutafuta hoteli yakulala usiku huo.
Sabrina
akashangaa hoteli aliyochagua Tino. “Sasa hapa si itakuwa mahela mengi sana!”
“Yeah! Nataka upumzike vizuri baada ya kuuguza kwa muda mrefu.” Sabrina
akacheka taratibu kwa kuridhika. Wakapata chumba, wakaingia humo. Ilikuwa siku
iliyojaa hekaheka, wote walikuwa wamechoka. “Nimebeba chupa ya uji Tino. Kunywa
kwanza halafu nitaangalia wanachakula gani kitakachokufaa. Au unahamu ya kula
nini?” “Acha ninywe kwanza uji. Naona kama nishazoea uji! Siku haiendi bila uji.”
Sabrina akamuwekea kwenye bakuli. “Kwani ulibeba na vyombo!?” Sabrina akacheka
tu. “Nimekukubali.” Akamsaidia kumpa, mpaka wakamaliza.
“Nataka
kuzungumza na Sabina.” “Si kumtumia ujumbe tena?” Sabrina akakaa. “Lela ni
muongeaji Tino na ndio kitu amekuwa akikifanya hata kwenye mahusiano yenu. Kila
mtu kwenye kitu chochote kinachomuhusu yeye au wewe anahakikisha yeye ndiye
anakuwa msemaji wa kwanza ili atengeneze stori zake vile anavyopenda. Mimi nina
familia Tino. Ipo siku nitarudi nyumbani. Sitajali watakachokiamini, lakini nakuomba
Tino, katika hili mimi ndio niwe wakwanza kusema.” “Sawa.” Tino akakubali.
Kwa Sabina.
A |
katoa simu
yake akampigia Sabina dada yake, Tino kimya ametulia. “Za
siku wewe mtoto!? Umepotelea baharini?” “Nipo dada yangu. Hata kupiga kunijulia
hali!?” “Nilitingwa bwana. Vipi lakini?” Akamjibu mdogo wake kirahisi tu
na kuongeza swali jingine bila kujua jinsi Sabrina anavyoumia ambavyo hawamjali.
“Ile kazi pale iliisha. Lela aliondoka, akaniachia
mgonjwa. Tokea aondoke mpaka naondoka pale leo, hajarudi wala kupiga simu
kutujulia hali wakati aliniacha pale kwa makubaliano atatafuta daktari niwe nampeleka
Tino.” “Subiri kwanza we Sabrina! Huo ni muda gani?” Ikabidi Sabina
aulize. “Kama mwezi sasa na majuma mawili hivi.”
“Haiwezekani!” “Kweli tena.” “Ujue Lela amechanganyikiwa yule msichana!”
Sabina akashangaa sana.
“Na amenidanganya juzi nilipoenda kumwangalia hospitalini.”
“Anaumwa?” Akauliza Sabrina. “Tena
hakutaka hata nijue kama yupo hospitalini. Mdomo wake umemponza yeye mwenyewe.
Nasikia kashika mimba. Ndiyo inayomsumbua. Hana anachoweza kula. Tena nafikiri
ndio sababu ameshindwa kuja hapo kwa Tino. Sasa mmoja wa shoga zake akanipigia
kimbea kuniambia Lela mjamzito, ila hataki watu wajue kama anamimba, mpaka
mumewe afe, wakishazika ndipo atakapojitokeza.” “Da Sabina wewe! Yaani
anasubiria kifo cha mwenzake!” Sabrina akashangaa sana.
“Kweli tena. Sasa sijui wanapanga kumuua huyo Tino yeye na mwanaume
wake au la! Mimi sijui. Lakini ndio habari niliyosikia kwa shoga yake wakaribu
sana. Sasa mimi nikasema niende nikajionee mwenyewe. Siku hiyo nilipopigiwa
nakupewa hizo habari, nilipotoka kazini tu nikasema niende nikamwangalie
makusudi huko hospitalini alipolazwa kabla hajatoka ili ajue najua. Maana kila
nikizungumza naye namuuliza mbona simuoni baa siku hizi, ananipa maneno mengi. Baada
ya muda, nikawa simpati tena! Ndio sasa ikabidi nimfuate. Eti nimemkuta wodi ya
kina mama wajawazito pale Agakhani, ananiambia anaumwa malaria! Wakati shoga
yake alishaniambia mimba imekuja na maradhi, kutwa yupo hospitalini na huyo
bwana ake.” Sabrina akatulia kidogo.
“Sasa nikamwambia, wewe upo hapa, mgonjwa wako umemuachia mdogo
wangu, halafu mimi huniambii kama unaumwa umelazwa, nitajuaje juu ya mdogo
wangu huko ulipomuachia mgonjwa! Akaanza kujitetea hapo mbele ya mwanaume wake,
kuwa simu ilipata matatizo lakini angeniambia. Hata hivyo amekuacha vizuri sana
nisiwe na wasiwasi. Kutokurudi nyumbani ni kutotaka kukupa wewe mzigo wa watu
wawili kwa kuwa wewe unajituma sana, ungeishia kuwahudumia watu wote wawili
ndio maana ameona yeye augulie hospitalini na akitoka ataenda kukaa kidogo kwa
mwanaume wake mpaka apone kabisa, usilemewe. Ila nisiwe na wasiwasi kabisa,
amekuachia gari na pesa ya kutosha. Akasema tena hapo ilikuwa amtume Rama, huyo
mwanaume wake akurushie pesa nyingine.” “Mmmh!”
Sabrina akachoka kabisa.
“Ninachoweza kukwambia dada yangu, si kweli. Lela ni muongeaji sana
asiyeweza vitendo. Alinipa huo mshahara.” Sabrina
akamtajia dada yake kiasi cha pesa alicholipwa na kuishia kufanya mshahara wote
matumizi ya hapo ndani. “Haiwezekani Sabrina. Pesa ya
kitoto kiasi hicho!?” “Mungu wangu ni shahidi, tena alisema mlikubaliana naye.”
“Mimi nikubaliane malipo yako kwani mimi ndiye ninayefanya kazi! Yeye mjinga
nini?” “Mimi mwenyewe nilishangaa, lakini kwa sababu nilimkuta mgonjwa na hali
mbaya sana, nikikwambia mbaya, niamini ilikuwa mbaya dada. Na hakuwa na matunzo
kabisa. Nikaona nisiweke pesa kwenye uhai wa mtu.” “Sasa hilo ndilo kosa lako. Kwa
nini ulikubali kuendelea naye bila pesa yakueleweka! Lela ni mshenzi
kupitiliza. Ukimchekea yule, atakufanya mjinga. Na usimuone vile, anamahela ya
Tino kibao. Anayachezea yeye na mwanaume wake
bila huruma! Halafu leo anakupunja! Atanitambua. Na huwa ananijua mimi huwa
sitaniani na vima. Hawezi kunichezea akili mimi, nitamtia adabu mshenzi mkubwa
yeye!” Sabina akasikia ameshakasirika.
“Mimi nilifanya kwa sehemu yangu dada yangu kwa kadiri Mungu
alivyonijalia.” “Ndio maana wanakuonaga mjinga na wewe! Mpaka wadogo zako
wanajua kupata pesa palepale nyumbani kwa baba na mama wanaojulikana ni
mabahili, halafu wewe umeshia kukaukwa mdomo! Acha kuwa mjinga wewe Sabrina.
Simamia haki yako!” Sabrina akacheka kidogo bila nyongeza katika
hilo. Akaona aendelee na yake.
“Sasa nilichokupigia simu dada yangu nikutaka kukutaarifu kuwa
nimepata kazi kwengine. Nikitulia na mambo yakienda vizuri nitawatafuta. Sitaki
sasa hivi kuongea mengi, ikaja kushindikana huko mbeleni, wazazi wakaendelea
kuniita fungu la kukosa.
Acha nikapambane na dunia. Nitajijua huko huko.” “Mmh! Kwa hiyo hutaki kuniambia
unapokwenda?” “Acha nisimame dada yangu. Nimekuwa mtu wakusema kila kitu ndio
maana naona nikishindwa, nakuwa kicheko cha familia.” “Sawa, lakini
nakuhakikishia Lela atanitambua. Anajidai anakupa mahela na vitu, tena kwa kutangaza
kila mahali kuwa amebadilisha maisha ya mdogo wangu, kumbe muongo!” Bado
Sabina alisikika na hasira na Lela, wala si mdogo wake kwenda wasipopajua.
“Mimi sijui amesema nini, lakini sijachukua chochote kutoka kwake
dada. Nilimuona ni mtu wa maneno maneno hata zawadi alizokuwa ameninunulia za
chupi, lotion na sabuni yake nikamrudishia.” “Kweli!?” “Kweli dada. Na Mungu ni
shahidi. Alimtuma kijana mmoja huwa anamuuzia nguo, akaja kuchukua kila kitu
chake.” “Atanikoma Lela. Katangaza kila mahali kuwa amekupa vitu kibao!”
“Hasemi kweli.” Akakataa Sabrina.
“Mimi naomba nikuage dada yangu, na utanifikishia salamu kwa baba na
mama.” “Wewe Sabrina! Huwapigii?” “Unajua tutakapoishia na wazazi wako dada
yangu. Wataniharibia mipango yote kwa vitisho, kunikatisha tamaa kwa kuniambia
sina nitakapofanikiwa kwa chochote nitakachofanya na kutaka nirudi nyumbani
nikawafugie ng’ombe na kuku wao bila shukurani, halafu matusi yaendelee wakinitolea mimi
mifano mibaya mpaka kwa wale watoto wao wadogo wa kiume. Hata hivyo sidhani
hata kama watajali nilipo, au hata kuhisi kuna mtu amepungua kwenye maisha yao.
Hakuna anayenitafuta kwenye ile familia. Mpaka mimi ndio niwatafute.”
Kwa mara ya kwanza Sabina kikamuingia moyoni na kujisikia vibaya. Hata yeye
tangia atoke nyumbani kwake ni Sabrina amekuwa akimpigia kumjulia hali na
kumuuliza hili na lile juu ya Lela na Tino, lakini si yeye kumtafuta mdogo wake
kujua anaendeleaje.
“Acha nikahangaike na mimi na maisha yangu, nitawatafuta
kikieleweka.” “Mmmh! Haya mwaya. Kila la kheri. Kuwa tu mwangalifu huko.”
“Nashukuru dada yangu.” Sabrina akakata haraka. Na kumblock
kila mahali ili asije kumpigia tena akampata au hata wazazi wake. Nao
akawablock wote, familia nzima.
Kwa Lela.
“Sasa
nishamalizana na familia yangu yoote kwa kupitia Sabina. Acha nimtumie ujumbe
da Lela. Nasikia ni mgonjwa, hapatikaniki kwa simu. Mimi namtumia ujumbe hivyo
hivyo atapata ujumbe wake atakapofungua simu.” Tino kimya ametulia. Sabrina
akamwangalia. Akamuona amebadilika rangi tena. Mwekundu. Akajua amesikia kila kitu,
ndio amekasirika. Akaona amalize kwanza na Lela, aliyemtangaza vibaya. ‘Da Lela. Naona muda mrefu sana umepita tokea tuwasiliane au
tokea uniachie mgonjwa pale nyumbani. Najua ulinilipa pesa ya miezi mitatu ili
nifanye kazi kwa muda huo, lakini hukuacha pesa yeyote ile ya matumizi ila
ahadi tu yakuja kuwasiliana mbayo hujatimiza. Ilikuwa ikinilazimu kutumia
uleule mshahara ulionilipa, kununua umeme ulipoisha, vyakula na matumizi
mengine ya pale ndani. Kwa hiyo ile pesa yote iliisha na naona na kazi pia iliisha.
Kuanzia leo nimetakiwa kuondoka pale. Mambo mengine nashauri uzungumze na Tino
mwenyewe. Ila ndio nataka kukutaarifu kuwa nimeondoka. Na Tino ni shahidi, sikuchukua
chochote zaidi ya vitu vyangu nilivyokuja navyo. Nakutakia maisha mema.
Asante.’ Akamaliza kuandika. “Naomba nikusomee kabla sijatuma.” Kabla
Tino hajajibu, akaanza kumsomea. Tino alipokubali, akautuma na kumblock na yeye
kila mahali. Hakutaka awasiliane naye tena.
Aluta
kontinua.
A |
lipomaliza
Sabrina na yeye Tino akatoa simu yake. Akamuona na yeye anapiga. Kimya
akisubiria ajue na yeye anampigia nani. “Ni wewe Tino
au Lela anatumia simu yako?!” “Ni mimi kaka.” “Daah! Nimeona simu yako ikiingia
nikataka kutupa simu.” “Kwa nini kaka?” Tino akauliza akijua wazi ni
nini kinachoendelea kwenye jamii juu yake. “Nilikuwa na
Lela kama mwezi mmoja uliopita akiulizia juu ya malipo yako ya mwisho kwenye
ile kampuni!” “Unamaanisha nini!?” Akauliza Tino akitetemeka kwa hasira.
“Madai baada ya kifo chako. Alitaka kujua yeye kama
atakayeachwa mjane kwa kifo walichosababisha wao kama kampuni, atalipwa fidia
kiasi gani! Na kama tunaweza kuwadai zaidi.” Tino akazidi kuumia.
“Sasa alichofanya kibaya zaidi, kabla hatujamalizana mimi na yeye,
maana mimi nilimwambia ile kampuni mpaka sasa wamekuwa wavumilivu na waungwana
sana. Wanaendelea kumlipa mshahara wako japo hawaoni maendeleo yako ya
hospitalini. Tusiwatibue kwa madai mengine. Akaondoka hapa kwa hasira, akaenda
kumfuata muhasibu wa pale kwenye ile kampuni, anamuulizia malipo ya mwisho
baada ya kifo chako! Yule muhasibu akanipigia akilalamika akisema tunadai vipi
pesa ya mwisho wakati hatujapeleka hata kopi ya hati ya kifo chako!” “Yule
muhasibu amenisimulia yote hayo.” Tino
akaongeza. Sabrina akashangaa sana.
“Ndio maana nimeshituka sana kukusikia. Maana Tino niliyemsikia mimi
mara ya mwisho ni wa kufuatilia hati ya kifo siye Tino anayeweza kuzungumza
mkasikilizana!” “Naelewa kaka, najua anatafuta kifo changu ili apate pesa
zaidi. Ameniacha pale ndani bila pesa wala kujali kwa lolote huu ni mwezi sasa
na majuma kadhaa. Na kabla ya hayo alikuwa akiniacha, ananifungia ndani
chumbani, gizani, bila chakula wala mtu wakunisaidia hata maji, makusudi tu na
mengine mengi.” “Ndio maana alikuwa akikataza tusije kukuona nini? Maana hata ndugu
zako walinilalamikia kuwa anawazuia kufika pale!”
Mwanasheria, ambaye alijulikana kwa jina moja tu, Max, mashuhuri hapo jijini
kwa kushinda kesi ngumu, akaongeza. “Asingekubali
mnione kwenye ile hali aliyokuwa akiniacha nayo, kaka. Ilikuwa mbaya, yeye
mwenyewe alikuwa hataki kuniona jinsi nilivyotisha na kunuka.” Tino
akazungumza kwa kuumia sana.
“Atakuwa yuko wapi sasa? Au kwa mwanaume niliyesikia anaishi naye?”
“Ndio nilichokupigia ili unisaidie, kaka. Hapa nazungumza kwa kuwa Mungu
alinitumia malaika wake kunitoa kwenye ile hali. Bila yeye, pengine kweli sasa
hivi mngekuwa mlishanizika, na yeye Lela anasubiria malipo kama mjane wakati
kiukweli Lela alishaanza maisha yake.” “Nakuelewa kabisa Tino, lakini kisheria
bado ni mke wako. Na kama unavyomjua mkeo ana….” “Tafadhali muite Lela tu.”
Akamkatisha Tino kwa hasira.
“Sawa, Lela.” Max akarekebisha. “Lela amejaa kwa kila anayekufahamu wewe akijionyesha
anakujali na kukushugulikia kwa hali ya juu. Ameniambia hata mimi kuwa ameajiri
msichana wa kukuhudumia japo upo kwenye hali mbaya sana, lakini hajakukatia
tamaa, amekutafutia mfanyakazi maalumu kwa ajili yako.” Sabrina
akashangaa sana. “Muongo kabisa. Anamuacha msichana
pale huku akimwambia asinihudumie kwa lolote, na wala asiingie kwenye chumba
changu. Ni kama Mungu tu alimgusa akiwa amemkataza, akaingia. Alinikuta nimeoza
kaka. Sifai kwa madonda, nina kinyesi, mikojo, halafu amenizimia taa, na
kufunga madirisha nikawa naishi gizani! Eti anasema nini?” Tino akaongea
kwa hasira.
“Sasa Tino mdogo wangu, hayo ni maneno yake dhidi yako. Hakuna
uthibitisho. Ila alichokuzidi mwenzio anaongea sana Lela. Iwe uongo au ukweli,
amejaa kila mahali.” “Je kwa hilo lakunitelekeza na kutokuwa nyumbani zaidi ya
mwezi?” Akauliza Tino. “Labda
nikuulize Tino, unataka nini sasa hivi?” Ikabidi Max, mwanasheria wake wa tokea mwanzo kuuliza. “Kwa yote hayo niliyokwambia bado unaniuliza tu? Au unataka
kunisikia nikiongea nini? Au unataka kusikia nini kimetokea kwenye maisha yangu
ndipo ujue naishi na mtu hatarishi kwenye maisha yangu? Hivi unajua ile pesa
yote niliyolipwa ameitumia zaidi ya nusu?” “Haiwezekani Tino! Pesa yote ile!?”
Max
akashangaa sana.
“Acha kaka, hapo bado pesa yangu ya akiba iliyokuwa kwenye akaunti
zangu nyingine. Nimekuta hakuna kitu kaka, halafu anashindwa hata kuninunulia
chakula mimi mwenyewe! Hata kuajiri mtu wakunitumikia ameshindwa kumlipa! Hata
kama kwake nilikuwa nikinyaa, hata kumlipa mtu anihudumie! Pesa zote za dawa na
vitu vyangu vya hospitalini alivyonunua mwanzoni kabisa kwa kushauriwa na
daktari, yule muhasibu anasema alikwenda pale kudai kwa vitisho!” “Aliniambia
yule muhasibu.” “Halafu usifikiri hata vilitumika kaka! Alinunua vifaa vyote vya
kisasa alivyoshauriwa na daktari ili kunisaidia kujisaidia mimi na msaidizi
atakayekuwepo, lakini kaka, havikuwahi kutumika. Tena kwa makusudi tu, wakati
yule daktari alimwambia nikitumia vile vifaa, kwa muda mfupi sana kwa kuwa
sikuwa na stroke mbaya, ningeweza kujitegemea. Akamsisitiza, nahitaji mazoezi
na kula vizuri, nitapona.” Akaendelea kulalamika
Tino kwa sauti yake yakuumia.
“Kwa makusudi kabisa, akaanza kufanya kila kitu kinyume na
alivyoshauriwa na daktari. Makusudi kabisa kunifanya niwe dhaifu. Akajidai
mwanzoni amechukua likizo kuniuguza.” “Nakumbuka. Alitangaza kwa kila mtu. Na
kuomba nihakikishe ndugu zako hawafiki pale ili wakuache upumzike, na
wasikutapeli tena.” “Basi ile ilikuwa njia yake yakunitenga na kila mtu ili atimize
kusudi lake. Alinifungia kaka, karibu siku 4, mchana na usiku nipo peke yangu
gizani.” “Haiwezekani Tino!” “Mbona hiyo ilikuwa mwanzo tu kuhakikisha sina
tena nguvu! Ndipo sasa nikaishiwa nguvu kabisa hata kukaa ikawa shida. Si kwa stroke,
ila njaa. Na ndipo mateso yalipoanza. Kila alipomleta mtu wakunisaidia ili kuonyesha
hayupo mtaani akizurura tu bila kunipa mimi msaada, alihakikisha anampotosha
huyo mtu makusudi. Kumuwekea chuki dhidi yangu. Akionyesha ana moyo wa kukaa,
anaanza kumnyima malipo makusudi. Basi mfanyakazi anaondoka, naachwa peke yangu
hapo. Huyu binti aliyekuja kuniokoa, alinikuta nimejawa na kinyesi na mkojo,
ngozi ina madonda matupu. Natetemeka kwa hofu, baridi iliyokuwa ikinipiga bila
kufunikwa nikiwa mnyevu mpaka nakauka, na maumivu. Alichokuwa akifanya Lela,
kama ambaye alikuwa hataki nikate roho, ni kunipa maji tu kila akija, kama
aliyekuwa akimwagilizia ua alilolifungia mahali. Ananikuta nanuka, ananiacha
hivyo hivyo na matusi juu!” Tino aliongea kwa
uchungu sana.
“Pole sana Tino. Pole.” Max akamuhurumia
sana. “Na kwambia kaka, ni Mungu tu. Alikusudia Mungu
mwenyewe kuniokoa kwenye ile mikono maana wote mliacha hata kuja kuniona!
Nilibaki sina mkombozi.” “Unamjua Lela, Tino mdogo wangu. Alihakikisha kwa
vitisho hakuna anayepita.” “Hata kutaka kunisikia kwa simu! Hata kupita jamani!
Zaidi wewe ambaye ulikuwa ukimsaidia madai! Angalau ungemwamuru kuwa nilazima
unione ndipo uendelee na madai, kaka! Lakini ni kama na wewe ulinitelekeza.
Ukaishia kupokea malipo yako, ukaachana na mimi!” Sabrina akajua Tino
hatambakisha mtu. Alikuwa mwekundu, anatetemeka kwa hasira.
“Samahani sana Tino. Nahisi nikutingwa na maneno mengi ya Lela.”
“Sikutegemea kaka! Kila mtu alinisusa wakati nilikuwa kwenye maisha ya watu
nikisaidia kwa hali na mali! Nikapata shida mimi, hata wale waliojua ukweli juu
ya ndoa yangu waliniacha kwenye mikono ya Lela, mwanamke waliyejua wazi
alinigeuka hata kabla sijapata matatizo. Hata wale waliojua anatumia pesa yake
yote kumtunza mwanaume wake, huku akitapanya yangu, waliniacha kwenye vitisho
vya maneno matupu ya Lela! Mtu baki kabisa, ndiye aliyeniokoa! Asiyenijua wala
hanitambui ndiye aliyehangaika na mimi mpaka leo nazungumza na wewe hapa!”
“Lela alimleta nyumbani kama kumlindia nyumba wakati akihamia kuishi
kwa mwanaume wake, kusudi tu alimuacha ili mtu akipita pale nyumbani, akute mtu
asilaumiwe kuwa ameniacha nyumbani peke yangu, halafu anamuacha hapo nyumbani
huku akimuonya kabisa hata chumbani kwangu asiingie, aniache tu. Halafu akaishia
kutangaza kwa kila mtu ameajiri tena mfanyakazi mwingine na amemlipa mshahara
wa miezi mitatu,..” “Hata mimi aliniambia baada ya kutaka kujua unaendeleaje na
kwa wakati huo upo chini ya uangalizi wa nani anapokuwa kazini.”
Max akajaribu kujitetea.
“Basi kama alivyokuwa akifanya kwa wengine aliokuwa akiwaleta
wanihudumie, ili waondoke na kuniacha peke yangu na yeye kupata nafasi
yakuendeleza kuniangamiza, huku huko nje akitangaza na kunisema vibaya kwa watu
kuwa ninamatatizo ndio maana wafanyakazi wa kunihudumia hawakai, nakwambia akaanza
kumpandia chuki huyu binti dhidi yangu. Alipomuona huyu binti anahangaika
mchana na usiku bila kuchoka, akaendelea kumsisitiza asihangaike na mimi, hata
asiingie chumbani kwangu yeye atanihudumia. Kwa kumsikia mwenyewe akimkataza.
Wakati alikuwa akiondoka hapo nyumbani hata siku nne, na akirudi haji hata
kuniangalia chumbani kwangu. Alipomuona huyu binti hamsikilizi, amekazana
kunisaidia, ndipo akatutelekeza sasa na hiyo pesa aliyokuwa akiwatangazia
amemlipa mshahara wa miezi mitatu. Bila chakula wala pesa ya matumizi. Ndipo
hapo sasa nasema ni yeye Mungu mwenyewe alikusudia kuniokoa maana aliona
binadamu wote ambao wananizunguka wamenisusa na kunichoka. Akaniletea na
kuniacha kwenye mikono iliyokuwa na ubinadamu na upendo.”
Sabrina akajisikia vizuri.
“Ilimbidi yule binti atumie pesa yote ndogo aliyokuwa amelipwa na Lela, kuendesha maisha ya pale huku akijitahidi kuninunulia virutubisho ambavyo najua vilimgarimu. Aliondoka Lela akimdanganya huku akijichanganya na mimi nikimsikia, mara amuage anasafiri kikazi, mara aseme anataka akupumzike kwa kuniuguza muda mrefu. Mara atakuwa hapahapa mjini, mara nje ya mji, lakini yule binti akamuomba atafute appointment ya daktari, tena alimwambia kwa kumsikia, yeye mwenyewe angenipeleka, Lela akasema atafanya hivyo. Sijamsikia akimtafuta huyu binti, ila alimpa masharti kuwa asinitoe kwenda popote kuhudumia kwa lolote hata kukatwa nywele, mpaka amwambie yeye, yeye ndio awaambie watu huko atakapotaka kunipeleka ili watu wajue yeye ndiye aliyetoa wazo, wajue yeye ndio ananihudumia.” “Haiwezekani Tino! Alimwambia kabisa?” Max akashangaa.
“Kabisa kaka. Sasa huyu binti alipoona nimepata nafuu yakuweza kukaa
mwenyewe, na alinikuta ngozi ya kichwa kimejaa ukoko, kama ambayo haijahudumiwa
miaka na Lela hapatikaniki, akanipeleka kwa kinyozi wakati alimkataza.
Akamwambia asinipeleke kwa kinyozi ni aibu.” “Kwa nani sasa?” “Labda yeye, mimi
sijui! Lakini alisema naweza nikajisaidia huko, ikawa aibu. Kwa hiyo
nisipelekwe, yeye huwa analipa watu wakunipunguza nywele palepale nyumbani.
Sasa huyu binti, hapana, acha nimtaje jina, anaitwa Sabrina. Sabrina alipoona
siku zinazidi kwenda, na hakuna simu wala hodi pale kwangu ndipo akanipeleka
yeye mwenyewe saluni anayojua yeye. Tulipotoka sasa ndipo akamtumia ujumbe Lela
kumtaarifu kuwa alinitoa pale lakini alinirudisha salama. Hivi unajua Lela kwa
mara ya kwanza tokea aondoke na ya mwisho alipiga simu akimlaumu huyu binti
huku akishangaa!” “Analaumu nini na alikuwa akishangaa nini?”
Akauliza.
“Alidhani Sabrina alinipeleka kwenye ile saluni wanayotufahamu mimi
na yeye, bila yeye kujulikana ndiye ameamuru nipelekwe. Kwamba sifa atapata
Sabrina, yeye ataonekana amenitelekeza. Si kwa kuwa watu wanamuona mtaani! Na
nilisikia saluni ileile niliyokuwa nikinyoa mimi na wakinifanyia waxing ndipo
alipomuhamishia mwanaume wake.” “Haiwezekani Tino!”
Max akahisi kama ni hadithi tu na si kweli.
“Nakwambia kaka. Aliniambia yule kaka anayeninyoa pale nilipoenda
mara ya mwisho wakati nilipoanza kuumwa, na yule msichana aliyekuwa akinifanyia
waxing akathibitisha makusudi ili kumuharibia Lela, kwa kuwa ni wagomvi,
walishapigana pale. Akimkataza asiwe ananihudumia.” “Lela!”
Max akamtaja kwa masikitiko. Sabrina akishangaa na yeye, asiamini ujasiri wa
Lela.
“Na ndio maana hakutaka mimi nirudi pale, japo nasikia alimtafutia
mwanaume wake kinyozi mwingine. Yule aliyekuwa akinihudumia mimi alimkatalia
akamwambia tayari anao wateja wengi, hapokei wateja wengine.” “Lakini pale
wanabei!” “Sana, lakini alikuwa na shida gani wakati pesa yangu anayo!” “Na
kweli. Sasa ukute na hofu ilimuingia aliposikia umeweza kutoka ndani wakati
huku nje alikuwa anakutangaza upo mahututi, haja zote hapohapo mpaka
wafanyakazi wanakimbia nyumba.” Max akajikuta
anaongeza. Asijue anavyozidi kumuumiza Tino. Kama kweli aliyajua hayo yote, alishindwa
vipi kupita na kumsalimia tu!
“Kumbe na wewe uliyasikia hayo!?” Tino
akauliza kwa kuumia sana. “Ni hivyo alikuwa akikataza
wat…” “Hapana kaka. Naomba achana na hicho kisingizio. Unazidi kuniumiza tu.
Kumbe mlijua nina hali mbaya kwa kiasi hicho! Hata kuja kuniona jamani!?
Angalau kujua kama nina matibabu au la!” Max akanyamaza.
“Anyways ndio nilikuwa nikisema hakutaka nitolewe tena ndani. Zaidi
kwa watu wanao nifahamu na aliowafikishia taarifa zangu. Anawaambiaje walimwengu
tena? Tena naonekana na kuhudumiwa na mtu baki tu. Halafu mdogo kuliko yeye!
Sabrina amewezaje, yeye ameshindwaje? Sasa ili kufunika aibu yake, na watu
wajue kweli nakaribia kufa, nahisi anazo njama zakutaka kuniangamiza kaka.
Japokuwa sijamsikia tena tokea siku ile alipolalamika na kumlaumu Sabrina kwa
simu, lakini uhakika wa kifo changu aliompa yule muhasibu wa kampuni yetu ili
amwambie ni kiasi gani atapata baada ya kifo changu ndio unanitia wasiwasi na
kunifanya niondoke pale kwa muda.”
“Asingepata nguvu ya kutangaza kifo changu wakati Sabrina
alimuhakikishia ninaendelea vizuri, na wala sijajisaidia saluni. Inamaana
amejua naendelea vizuri. Lakini tujiulize tu mimi na wewe, ujasiri wa kuendelea
kutangaza kifo changu anautoa wapi kama si kuna hila nyuma yake!” “Hawezi kuona
unapona kabisa Tino. Kuwa kwako kitandani kunawasaidia kupata pesa kila mwezi. Na
wanajua wazi, kifo chako kitawanufaisha zaidi. Watapata Bingo kubwa ya mwisho
ambayo alijua ni pesa kubwa zaidi.” Akaongeza
Max akisikika anafikiria zaidi.
“Ndio maana nimeona niondoke kabisa pale. Nikajifiche mbali kabisa.
Huku ukinisaidia jinsi ya kuachana naye moja kwa moja. Na hata tukiachana,
asiniache nalala nje. Yaani akaniacha mavumbini kabisa! Yaani mahakama iamuru
tugawane kidogo alichoniacha nacho!” “Lakini kama nimekusikia vizuri Tino, ni
kama sasa hivi umeishiwa kabisa. Huna chakupoteza mkiachana, si ndivyo?”
Ni kama Max akataka uhakika. “Bado nina zile pesa na
nyumba yangu. Najihisi nastahili ile pesa yote jamani! Ameshatumia nyingi mno.
Halafu ile nyumba nilijenga mwenyewe kwa msaada wa marehemu baba yangu. Ndio
urithi na ukumbusho pekee kutoka kwa marehemu baba yangu. Alinisaidia hata kusimamia
ujenzi wakati mimi nikienda shule. Lela aliikuta tu. Kweli anufaike nayo tu!”
Akaongea kwa kuumia na kulalamika.
“Katika hilo huna jinsi Tino. Mtatakiwa mgawane tu. Lela amekuwa na
sauti kubwa kukupita wewe. Yeye ndio anaonekana amehangaika na wewe tokea upo mgonjwa
hujiwezi. Watu watasema sasa hivi umepona ndio unamgeuka! Yote uliyonieleza
mimi, ni mageni kabisa kwangu. Lela anapita mtaani akitangaza halali mchana na
usiku akikuhudumia wewe. Pesa yote inaisha kwa kukuhudumia wewe. Wewe mzito wa
kuzungumza Tino, nani atajua hayo yote uliyoniambia mimi na kukuamini wakati
ulifungiwa ukiwa una hali mbaya, unatoka ukiwa na hali nzuri! Sabrina umemfahamu kupitia yeye mwenyewe Lela,
kwa kumleta nyumbani akuhudumie. Sijui kama unanielewa pointi yangu?”
Tino akaumia sana, akabaki ameinama.
“Kwa kuwa mimi nawafahamu nyinyi wote wawili, tena tokea zamani.
Nakuamini, na ninajua uwezo wa Lela. Lakini nakwambia huu ukweli mgumu kukufungua
ufahamu wako si kama Max, ila mwanasheria. Nataka uelewe utakavyosikika mbele
ya watu na sheria! Kwa hakika najuta sana Tino. Natamani hata hapo katikati
ningelazimishia kuja kukuona ili niweze kumshinda kwa hoja.” “Hatuwezi kuanzia kwa kunitelekeza mimi na msichana
aliyemwajiri? Yaani huku kutokuwepo nyumbani muda wote huo, hatuwezi kuanzia
hapo?” Tino akauliza kwa machozi akiwa anaona
tayari hoja za msingi atakazomshinda nazo Lela.
“Ukiwa tayari tunaweza kujaribu. Hakuna kinachoshindikana. Na kama Sabrina,
aliyekukuta kwenye hiyo hali akikubali kuwa shahidi yako….”
“No way! Siwezi kumuingiza Sabrina kwenye ugomvi wangu
na Lela. Ni heri nipoteze kila kitu lakini si kumuanzishia vita huyu binti na
Lela. Lela na mwanaume wake watamsumbua sana. Itakuwa ni kama namlipa
Sabrina ubaya kwa wema alionitendea! Hapana. Tafuta njia ingine.” Hapo Tino akakataa kwa ukali kabisa na kwa
msisitizo, akiona ni bora kushindwa kuliko Sabrina! Mbaya zaidi, msamiati au
neno kushindwa halijawahi kukubalika kwa Max, tokea aanze hiyo kazi
iliyomjengea heshima mjini. Leo Tino anataka huduma yake na kuweka mazingira ya
kushindwa! Max akaona awachukulie taratibu kwani hata hivyo Tino alishakuwa na
hasira naye. Akaona amrudishe kwake kwa hatua.
“Basi niachie nianze kulifikiria hilo au kulifanyia kazi. Nitatafuta
njia zote zitakazo saidia kesi.” “Na mimi nimemdhibiti kwenye pesa yangu yote.
Hata matibabu. Sasa nataka uwe shahidi na uwe upande wangu. Sijui utamjulisha,
lakini ujue kuwa nimedhibi mianya yote ya pesa. Nimemtoa kwenye matibabu kazini
na nimebadili ulinzi ili asiweze kuingia tena nyumbani kwangu.” “Sasa hapo
lazima kutumia akili, Tino. Cha kwanza, nitamuandikia barua kuwa umemripoti
kuwa aliondoka nyumbani kwa muda wa mwezi mzima na majuma kadhaa akakutelekeza
na binti ambaye alimuajiri, bila matunzo. Sasa umeamua kwenda kutibiwa na kwa
kuwa alishaondoka kwenda kuanza maisha yake na mwanaume wake, moja,
umebadilisha ulinzi wa nyumba kwa ajili ya usalama wa nyumba yako.”
Akili ya Max ikaanza kazi kwa haraka.
“Pili, kwa kuwa hukuwa na pesa na pesa yote amekuwa akiitumia yeye
na yeye pia anayo kazi, umeelekeza pesa yote katika kujitibu wewe mwenyewe.
Tatu, kwa kuwa bado hujapona kabisa na kama nakumbuka, mkataba wako na kazini
kwako ni kama unakaribia kuisha, ila mahakama iliamuru wakulipe mpaka upone.
Sasa nitamjulisha Lela, kwa kuwa alishaondoka nyumbani na kuanza maisha yake,
wewe huwajibiki tena kwenye matibabu yake, na ili kampuni isilemewe na watu
wawili, ielekeze nguvu zote kwako, umemtoa.” Tino
alitamani kulia kwa furaha.
“Nakushukuru sana.” “Bila shaka. Nitahangaika angalau kulipia vile
tulivyokutelekeza.” Tino akajua amepata ujumbe wake wa
vile walivyomtelekeza, hapo hakumjibu akamuacha ahangaike na dhamira yake. “Nitaandaa huo wakala, nitaufanyia utaratibu wote kisheria,
kisha niufikishe mahakamani na yeye nimpe. Tena kesho tu ili asituwahi.” “Hapo
utakuwa umenisaidia sana. Na umwambie chochote anachotaka kuzungumza na mimi,
azungumze kupitia wewe. Namuwekea restrain oder asinitafute kwa simu au
kuniona, kwa kuwa amekuwa akitangaza kifo changu wakati mimi mwenyewe nipo
hai. Kunitafuta ni kutaka kutimiza adhima yake.” “Sasa hapo utakuwa umefanya
jambo la msingi sana. Ufanikishe hilo kwa haraka kwa kwenda mapema polisi
kumshitaki na kuomba hiyo restrain order, kisha uniletee hiyo kopi na
mimi.” Max akachangamkia hilo wazo. Tino akawa ameongeza nguvu kwenye
kazi ya mwanasheria wake.
“Nitafanya hivyo kesho. Nitamripoti sehemu zote alizopita akidai
madai yangu baada ya kifo changu wakati amenitelekeza gizani. Halafu nikuletee
kopi, umfikishie.” “Hapo sawa kabisa.” Max
akaafiki. Sabrina akaingiwa hofu akiwa anamsikiliza Tino na mwanasheria wake
wakiongea na kupanga mipango mizito dhidi ya ndoa hiyo aliyosikia Lela
aliipigania mpaka akaolewa yeye. Akakumbuka stori alizopewa na Sabina juu ya
mwanzo wa Lela na Tino. “Lela anahistoria ya kutokubali kushindwa. Hii vita
ni kali na mimi nipo katikati yao!” Hofu ikamwingia Sabrina.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ni nini
kitaendelea kwa wanandoa hawa walioizoea sheria kuwatatulia kila jambo? Lela
anaijua sheria na Tino naye hivyohivyo. Usikose muendelezo. Mambo ndio
yanaanza.
0 Comments:
Post a Comment