Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 10 - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 10

Tamu Inapogeuka Shubiri..

Mambo hayakurudi kuwa kama zamani. Hapakuwa na mazungumzo tena. Kila mmojaanawaza lake. Lakini Sabrina akaendelea kupika na kumuandalia juisi na smoothie kama zamani. Kumfulia bila kuchoka lakini hapakuwa na mapenzi tena. Wakiwa pamoja simu ikiita, Tino hakuwa akiweka tena kwenye spika. Anatoka kabisa nje. Sabrina akagundua kuna usiri mkubwa sana unaoendelea. Na ni kama yeye hatakiwi tena kujua. “Ni nini kinaendelea?!” Likawa swali la Sabrina kila anapomuona Tino akizungumza na simu kwa kificho. Asijue nini kinapangwa juu yake. Akajiambia lazima kutafuta mbinu ya kujua kinachoendelea.

Mara nyingi awapo nyumbani, Tino akaanza tabia ya kushinda gym. Roho ikamuuma sana Sabrina, kuona alichokuwa akifanyiwa Lela ndicho na yeye Tino anamfanyia. Ametafuta sehemu ya kumkwepa kama alivyomwambia alikuwa akifanya nyumbani kwake, kuishi kwenye kinyumba cha pembeni, akikwepa karaha za Lela. “Sasa mimi nimefanya nini mpaka awe ananikwepa!” Akajiuliza Sabrina bila jibu asijue sumu aliyokwisha mwaga Max juu yake.

Chakushangaza, ni kama Tino akaacha kuzungumzia maswala ya ujauzito kabisa! Akiwa anampeleka mazoezini huko hospitalini, basi atajifanya yupo busy na simu yake ilimradi tu kumuonyesha Sabrina yupo busy, hawezi kuzungumza kabisa, kitu kilichozidi kumtia wasiwasi Sabrina.

Basi akimshusha mazoezini, akiwa anafanyiwa mazoezi ya viungo na wataalamu ili kurudisha nguvu kwenye huo mkono wake wa kulia, yeye Sabrina alibaki nje tu akisubiria asijue hatima ya hayo maisha ni nini ila kutaka kujua kama alishika mimba au la. Akabaki akitamani aanze siku zake/hedhi ili apate kitu chakumwambia Tino pengine amfurahishe asijue chuki aliyo nayo Tino dhidi yake. Tino alimuhesabu kama mtu mbaya sana aliyekaribu yake tokea mwanzo kwa hila tu ili ajinufaishe kwake. Alibaki akijiwinda naye kwa hila zozote Sabrina anazompangia na uchawi wowote alioambiwa anao, akitafuta jinsi ya kumtoa kwenye maisha yake. Ukimya huo uliokuwa ukimshangaza Sabrina asijue ni Max alimwambia Tino watulie kabisa, wampe siku chache, ili Tino ajiridhishe kwa hakika hajamuacha na mtoto ili asije kumtafuta tena baadaye na kudai makubwa zaidi ya Lela kwa kisingizio cha huyo mtoto.

Siku ngumu na za wasiwasi kwa kila mmoja wao, zikazidi kusonga wakiwa wanaendelea na kuhudhuria kliniki ya Tino na Sabrina kutojua kinachoendelea popote hata hapo hospitalini kwani hata hapo Tino alipokuwa akiingia ndani kwa mazoezi au kuzungumza na daktari, basi alianza kumtaka amsubirie nje asiingie naye ndani. Ikawa kukaa nje akisubiri si chaguzi tena ila lazima. Huo usiri na sintofahamu ukaendelea kwa Sabrina ndipo sasa akaanzisha tabia ya kila akisikia tu simu ya Tino ikiita, yeye ndio anatoka na kuacha simu yake ikirikodi mazungumzo yote kwa siri ili kujua kinachoendelea. Akiachwa nje wakati Tino akifanyiwa mazoezi hapo hospitaini, KCMC basi ndipo alikuwa akipata muda wa kusikiliza simu yake kujua walichozungumza Tino na Max kama simu yake ilifanikiwa kuiba mazungumzo yao, ilimradi tu ajue kinachoendelea. Akafanya hivyo bila mafanikio makubwa sana. Kwani aligundua Tino ni mpokea maagizo tu. Hakuwa akimsikia akijibu sana ila mara nyingi yeye anakua msikilizaji wa kile anachoagizwa kufanya na Max au akipewa kinachoendelea huko Dar, Sabrina anaokota neno moja moja na kuunganisha yeye mwenyewe kwa kutumia akili. Ila akajua Max ndiye amemgeuka kwa hakika. Kwa umbali gani na kwa nini, bado akawa hajajua! 

Kisicho Ridhiki, Hakiliki.

S

iku 10 tokea kugeukana kuanze na swala la Sabrina kuwa ameshika mimba kuonekana si tatizo kwa Tino tu hata kwa Max pia, Tino akiwa anafanyiwa mazoezi, Sabrina amekaa nje akimsubiri ikabidi Sabrina atulize mawazo na aanze kuhesabu mzunguko wake wa hedhi. Tangia siku ya mwisho kuona siku zake mpaka siku hiyo. Akahesabu kwa makini kwa kurudiarudia akagundua mwezi umeshapita. Hofu ikazidi. “Au sababu ya wasiwasi nimepitisha siku!?” Akajaribu kujifariji, lakini akakumbuka yeye sio mtu wakupitisha siku hata mara moja. Akabaki akiwaza asijue siku hiyo ndio zimeshatimu siku za Max wakiwa wamehesabu na Tino tokea waanze kukutana kimapenzi na Sabrina, wakapanga kumuuliza kwa hakika kujua kama ameshika mimba au la.

 Tino akatoka akamkuta amejiinamia. “Nimeshamaliza.” Sabrina akasimama. “Vipi lakini, unaonaje?” Sabrina akajaribu kutupia swali la kujali kwa upole. “Nafikiria kwenda nje ya nchi kwa matibabu kama huyu therapist/mtu anayenifanyia mazoezi alivyonishauri.”  Wakaongozana mpaka kwenye gari lakini Sabrina akajua ndio anaachwa, safari haimuhusu tena. Akatulia tu.

Walipoingia tu kwenye gari, Tino akauliza swali la moja kwa moja. “Bado hujapata tu siku zako?” Moyo wa Sabrina ukashituka kwa hofu. Akameza mate kwa wasiwasi, Tino akamuona na kupata jibu lake. “Nisikilize Sabrina, mimi nahitaji tumalize hili swala la huu ujauzito, nikatibiwe. Tafadhali using’ang’anie kubakiwa na ujauzito ambao hata wewe mwenyewe huna pakuishi!” Sabrina akaumia sana, akamtizama Tino, asiamini. Lakini akajikaza kuendesha.

Hapo ndipo akapata jibu lake kwa hakika kuwa anaachwa. “Tino hajakosea. Nikibaki na hii mimba, mtoto nitamuweka wapi?” Akajiuliza Sabrina huku akijilaumu sana. Sabrina akaanza kujiuliza na yeye. Atafanyaje! Hana hata pesa yakueleweka! Ataishije huyo Tino atakapoondoka? Akabaki kimya. Akaendesha mpaka hapo wanapoishi. Akaegesha gari sehemu yao. “Unapatwa ugumu gani kuamua jambo rahisi hivi ukilinganisha na mazingira yako? Kwa nini unang’ang’ania hiyo mimba!? Una malengo gani nayo ya baadaye ambayo labda hukuniambia?” Sabrina akamwangalia akashindwa ajibu nini. Akachomoa funguo za gari. “Nikusaidie kubeba kitu?”  Akauliza Sabrina. “Tafadhali naomba tumalize hili swala nijue moja.” Tino akaendelea kuweka msisitizo.

Sabrina akashuka garini na kuingia ndani, Tino akamfuata. “Sijui kama unanielewa Sabrina!?” “Tafadhali nipe muda wakufikiria Tino. Wewe kwako umeshafikia maamuzi ya mwisho kuwa hutaki mtoto. Mimi bado. Nahitaji muda.” “UNAHITAJI MUDA WA NINI!?” Akauliza Tino kwa ukali sana. “Nimeshakwambia mimi sihitaji mtoto. Nataka nikatibiwe. Mbona kama unataka kunifunga!?” Sabrina akamtizama asiamini kama anazungumza na Tino.

“Natakiwa Dar kesho kutwa. Sina muda wa kupoteza mimi! Nataka tufikie mwisho wa hili. Kama ni muda, nishakupa siku 10 sasa tokea mwanzo tunazungumzia hili.” Sabrina akajua kumbe siku hiyo ndio alipanga amuulize! Alikuwa akimuhesabia tu! Kwamba ameshapanga siku ya kumuacha! Sabrina akamtizama nakushindwa kuamini. Tino sasa hivi anapanga mipango yakumuhusu yeye bila kumjumuisha!

“Na kuna sehemu kabisa naweza kukupeleka hapahapa Moshi, wanaweza kukusafisha vizuri tu ukaendelea na maisha yako kama kawaida. Tukabaki hatudaiani.” Sabrina akashangaa sana. “Kumbe muda huu wa siku hizi 10 nakuona kimya kumbe ndio mipango hiyo inayoendelea kati yako na Max!?” “Tafadhali rudi kwenye pointi Sabrina. Acha kuongea sana, utanichosha. Tafadhali tumalize hili. Na kama utatoka hapo mgonjwa, ninaweza kuzungumza na huyu baba akatuongezea muda hapa zaidi, ukakaa hapa mpaka upone.” “Kama muda gani?” Sabrina akauliza kwa uchungu akijua hakuna chakuokoa tena, mipango imeshawekwa, Tino hataki kurudi nyuma. “Wowote ule utakaotaka wewe. Ila kuwa tu muungwana, ukijua hawezi kukuweka hapa kwa muda mrefu, hili ni eneo la biashara.” Sabrina akabaki akimtizama Tino.

“Tafadhali naomba twende kesho, tukakamilishe hili na sitakuacha mikono mitupu. Nitakulipa pesa yakutosha mpaka kuanza maisha yako.” Sabrina akavuta pumzi kwa nguvu. “Naondoka kesho kutwa Sabrina. Ninayo siku ya kesho tu. Naomba usipoteze muda. Fanya maamuzi sahihi, nimpigie simu huyo atakayekushugulikia, kesho twende.” “Sawa.” Tino hakuamini kama amefanikisha hilo. Akajua pesa ndio imemvutia Sabrina na kukubali. Kwa mara nyingine tena baada ya muda mrefu Sabrina akamuona Tino amerudi kuwa mwenye furaha na kuzidi kumuumiza moyo.

“Sasa mpigie simu huyu mwenye hizi Villa, Mzee Swai. Muombe miezi mitatu mbele. Ili nipate pakuishi wakati nikijipanga. Halafu unipe pesa usiku huu huu nianze kujipanga nijue nafanya nini kwenye huu mji.” “Hutaki kurudi Dar?” Tino akauliza akimpima tu, akitaka kujua kama anarudi Dar na jinsi ya kujipanga kumkabili huko Dar endapo anapanga kurudi. “Naomba mpigie simu mzee Swai tafadhali.” Sabrina akaingia chumbani bila ya kumjibu swali lake. Akiwa chumbani, akamsikia Tino akizungumza na Swai. Wakataniana tena kidogo, akamsikia akiomba hifadhi kwa ajili yake. Akajua amekubaliwa baada ya kumsikia Tino akishukuru.

Akamfuata chumbani kwa furaha. “Amekubali.” Sabrina akageuka maana mlango ulifunguliwa kwa nguvu. “Amesema usiwe na wasiwasi. Kukitokea tatizo lolote, umpigie yeye mwenyewe simu moja kwa moja.” Akabaki akimtizama Tino alivyo na furaha yakumuacha pale, bado Sabrina asiamini kama ni Tino yuleyule! Bila kupoteza muda, Sabrina akachukua hiyo namba ya simu. Akaitunza kwenye simu yake. “Na ujue nitakuachia pesa nzuri tu.” Akasisitiza Tino kama kumtaka asibadili mawazo. Akamtajia hiyo pesa atakayompa, hata Sabrina mwenyewe hakuamini. Akafurahia sana moyoni, lakini hakumwambia. “Nakupa hundi yako sasa hivi.” “Na kabla hatujaenda kuua huyu mtoto, lazima tupitie benki niweke hii pesa kwanza, nikihakikisha imeingia kwenye akaunti yangu ndipo twende tukaue.” “Acha kusema hivyo bwana! Huyo hata sio mtoto.” Tino akakanusha huku akicheka kama kitu kizuri. Sabrina akamtizama na kuondoka pale.

Asubuhi Ngumu Maishani Kwa Sabrina.

A

kiwa chumbani akijiandaa watoke, alimsikia Tino akizungumza na mtu amkatie tiketi ya ndege ya kuondoka hapo Moshi siku inayofuata ili kumrudisha Dar. Sabrina akabaki akimfikiria Tino. Alikuwa na maumivu makali sana moyoni mwake, hata uso ulionyesha lakini hapakuwa na namna. Alijua Max na Tino wote macho yako kwake, akamilishe kumtoa huyo mtoto, asijue ni kwa nini Max ameng’ang’ania kuua mtoto wa mwenzie wakati yeye anao watoto wawili! Ila akanyamaza tu na kumshangaa sana Tino anawezaje kukubali ushauri wa kinyama kiasi hicho! “Labda tatizo ni kuzaa na mtu kama mimi!” Akajidharau Sabrina kwa machungu zaidi.

Lakini kama alivyokusudia asiachwe mikono mitupu, akahakikisha wanaanzia benki. Tino akiwa anamsubiria kwenye gari, yeye akaingia benki. Akahakikisha yale mamilioni ya pesa yanaingia kwenye akaunti yake, ndipo wakaelekea huko kwenye kutoa mimba. Njiani kila mmoja akiwaza lake.

Walifika kwenye hiyo kliniki. Tino akaomba kuzungumza na daktari aliyemtaja kwa jina kabisa. “Anatutarajia.” Akaongeza Tino kwa muhudumu aliyemkuta hapo mapokezi, Sabrina akamwangalia kwa masikitiko. Kwa haraka huyo daktari alipoitwa akatoka. Wakasalimiana. “Kila kitu kipo tayari.” Daktari akaongea akifikicha mikono kama anayesema yupo tayari kwa kazi. “Nashukuru sana.” Tino akashukuru na kumtizama Sabrina aliyebaki akishangazwa na hayo maandalizi. Kwamba kila kitu kilikuwa tayari ila yeye tu na hilo tumbo lake! “Unataka tuingie wote?” Tino akauliza. “Hapana. Wewe nisubiri tu hapa.” Sabrina akakataa wakaondoka na yule daktari.  

Wakaingia kwenye hicho chumba. Akakuta hicho kitanda na vyuma vingi tu kwenye kimeza pembeni ya hicho kitanda, vikimsubiria yeye. Hofu ikamwingia Sabrina kila akifikiria hivyo vyuma vitaingizwa kwake ili kumuua huyo kiumbe asiye hatia! Mwili mzima ukaaza kutetemeka kwa hofu. Wakampisha ili atoe nguo na kuvaa gauni la hapo. Akatoa nguo akavaa kigauni cha hapo alichokuwa amekabidhiwa avae kwa ajili ya shuguli nzima. Sabrina akabaki amejilaza hapo juu ya kitanda alichoambiwa ajilaze baada ya kubadili nguo, akifikiria na vyuma vyote vikimwangalia yeye. Hofu imemjaa, miguu ameifungamanisha asiamini starehe aliyoipata yeye na Tino wakati wa kutungwa hiyo mimba, leo vyuma vinamsubiri kumuingia yeye ili atolewe huyo mtoto!

 Tino yupo nje ya chumba cha kutolea hiyo mimba akisubiria kwa shauku kubwa shuguli nzima ikamilike, aachane na Sabrina moja kwa moja asije akamfuata tena baadaye na arudishe ripoti nzuri kwa Max aliyeamini yupo upande wake anamtakia mema. Max naye yupo kwenye simu wakati wote muda huo, sikioni kwa Tino akihakisha Tino anasimamia zoezi la kuua mtoto wake mwenyewe, linakamilika bila Sabrina kubadili mawazo na Max huyuhuyo pia yupo sikioni kwa huyo daktari aliyemtafutia Tino kuhakikisha anakamilisha zoezi zima la kuangamiza huyo kiumbe bila kukosea ili Tino arudi Dar wakakamilishe kesi yake na Lela na yeye apate pesa yake. Daktari na yeye yupo tayari kukamilisha shuguli nzima ya kuua hicho kiumbe kisicho na hatia, tumboni kwa Sabrina ili apokee malipo yake mazuri ya uhakika.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

                Usikose muendelezo wa Tamu inapogeuka Shubiri. 

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment