Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 11 - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 11

 Maamuzi Magumu…

B

aada ya muda yule daktari akarudi kwenye chumba alichokuwa ameachwa Sabrina. Akamtia moyo katika maamuzi yake ili kumfanya atulie na asibadili mawazo kama alivyoagizwa na Max. Maana umbali wa pesa iliyononeshwa na waleti yake huyo daktari ni huyo mtoto tumboni kwa Sabrina. Sabrina akatulia akimwangalia na kumsikiliza jinsi anavyomshawishi mpaka akakinahiwa rohoni. “Nimebadili mawazo.” Sabrina akamkatisha na kukaa. “Max amekuahidi Tino atakulipa pesa nzuri ili umuue huyu mtoto.” Sabrina alikwenda moja kwa moja akiitambua hila ya Max kwa yule daktari, kama akimwambia najua nani yupo nyuma ya huo mdomo wako. Yule daktari akababaika sana Sabrina akimwangalia tu jinsi anavyoongea hili na lile akiokota hekima za hapa na pale akijitetea mpaka Sabrina akajua anaweza akamtoa kwenye malengo yake na yeye.

Akamuwahi kwa kumuweka na yeye sawa. “Mimi naelewa upo kazini na unatengeneza pesa kwa kuua hawa watoto.” “Ukiiweka hivyo unakosea.” Akakanusha huyo daktari, Sabrinaakimtizama kwa kumsuta. “Sasa fanya hivi, tukae humu ndani kwa muda wakutosha tu. Kisha wewe utoke hapa, ukamwambie Tino kuwa wakati ukinishugulikia nimepoteza damu nyingi sana, inabidi unilaze uniangalie kwa siku mbili. Yeye anaondoka na hana mpango wa kuja kukutana na mimi tena. Basi. Wewe utakuwa umepata pesa yako, mimi naendelea na masha yangu. Hutaniona tena na wala Tino hataniona tena.” Yule daktari akasita.

“Hii nafanya kwa ajili yako tu. Kukusaidia kupata pesa uliyoahidiwa. Mimi naweza kutoka hapo kwenye huo mlango, na nikamwambia nimeamua kutoua mwanangu, na asinifanye  chochote ila wewe ndio utakosa pesa. Sasa unataka pesa ya bure au la!” Sabrina akamuuliza kijasiri. “Lakini utataka nikulaze hapa kwa siku mbili?” “Anarudi Dar kesho asubuhi. Nikishauliza pale tunapoishi nikiambiwa kama ameshaondoka na mimi naondoka hapa. Sina haja ya kuendelea kulala hapa siku mbili.” “Sawa. Ila usije nitaja?” “Na wewe hivyohivyo. Jibu lako ni ulifanikiwa kuua huyu mtoto.” “Tafadhali usitumie lugha hiyo.” Sabrina akamwangalia tena kwa kumsuta, yule daktari akanyamaza. Akatafuta na yeye sehemu, akakaa hapo ndani kwa muda. Nje wakijua kazi inaendelea huko ndani, kumbe wote wamekaa tu hapo ndani.

Baada ya muda huyo daktari akaangalia saa yake ya mkononi. “Sasa itabidi hata kukuwekea maji, ili akitaka kukuona angalau aamini.” “Hata ukitaka kunichoma sindano ya usingizi pia sawa. Ili akija ajue nimechoka sana, siwezi hata kuzungumza.” Hilo akalikubali kwa haraka. Akamuwekea dripu vizuri, akamuwekea na dawa ya usingizi, Sabrina akaanza kusinzia. Akamtoa hapo na kwenda kumuweka kwenye chumba cha kupumzikia wagonjwa. Hapakuwa na watu wengine. “Huwa hatulazi watu hapa.” Sabrina akamshukuru na kupotelea usingizini.

Kwa mbali akamsikia yule daktari akizungumza hapo na Tino. Akimdanganya kwa mengi huku akitumia maneno mazito ya kidaktari mpaka Tino akaamini. “Pole Sabrina. Lakini umefanya uamuzi mzuri na sahihi. Kesho nitakuja kukuaga wakati naondoka.” Sabrina akatingisha kichwa kukubali huku amefunga macho. Sababu ya mawazo na wasiwasi, Sabrina hakuwa amelala usingizi mzuri vile. Alilala bila hata kugeuka. Asubuhi sana akamshwa na haja ndogo. Alikwenda kujisaidia huku akipepesuka kwa madawa ya usingizi akiwa peke yake hata Tino hakujitolea kulala naye kinafiki tu, ili amuuguze japo kwa usiku huo mmoja tu angalau akumbuke fadhila! Akamuacha Sabrina peke yake hospitalini akijua mgonjwa na amepoteza damu nyingi. Alipofika tu chooni, kitu cha kwanza akajiangalia vizuri akiwa na wasiwasi pengine yule daktari alimtoa mimba akiwa amelala, akagundua alikuwa muaminifu bado hakuwa akitokwa damu yeyote. Akatoka hapo chooni.

Palikuwa kimya kuashiria hapakuwa na mtu hapo ndani. Akarudi kulala mpaka kama kwenye saa moja hivi akasikia mlango ukifunguliwa, alikuwa yule daktari. “Dripu niliitoa usiku ili usisumbuke ukitaka kwenda chooni. Lakini itabidi niirudishie. Anaonekana atapita hapa kwenye saa mbili kasoro akiwa njiani kuelekea uwanja wa ndege.” “Nakushukuru sana. Asante.” Akamrudishia tena ile dripu, akapotelea usingizini tena.

Mpaka alipoamshwa na Tino. “Vipi?” “Uchovu tu. Ndio unaondoka?” “Hapa nawahi KIA. Nimekuitishia kifungua kinywa. Daktari amesema anaweza kukuruhusu mchana.” “Nashukuru.” Sabrina akafunga macho. “Acha mimi niwahi. Nitamtuma mtu aje achukue gari.” Sabrina akashituka mpaka akafungua macho. Akakumbuka na gari sio yake. “Lini?” “Nafikiria labda weekend hii.” “Sawa.” Ikabidi awe mpole. Tino akasimama hapo kwa muda, akaondoka asiamini kama anafanikiwa kuondoka Moshi bila huyo Sabrina aliyekuwa akisakwa na Lela kwa udi na uvumba huko Dar, awe shahidi yake, Sabrina asijue maana amewafungia watu wote simu. Hapatikaniki.

Max alihakikisha anamwambia Tino, asijerudi Dar au hata kuja kuonekanika tena na Sabrina kwa kuwa ndio ushahidi pekee uliobaki kwa Lela. Lela akifanikiwa kumpata tu Sabrina tu, yeye ndio atakuwa shahidi wake kuwa Lela hakumtelekeza Tino, alimuacha kwenye mikono ya mfanyakazi aliyemtafuta mwenyewe ambaye ni Sabrina. Max akamwambia Tino, hatari kubwa ni pale Lela atakapo kutana na Sabrina aliye mjamzito. Akamwambia kwa hakika watamuacha barabarani asiwe hata na pakuishi. Tino anaondoka Kilimanjoro bila Sabrina, akipongezwa na Max vilivyo.

Mwisho wa Sabrina na Tino.

A

kashangaa kitu kimemkaba kooni anashindwa hata kuhema. Alilia Sabrina. Alilia kwa kwikwi na uchungu mkali sana moyoni. Akakumbuka jinsi alivyohangaika na Tino! Alipokuwa akimpangusa mavi na kumtibu madonda yaliyokuwa yamesuswa na watu wote waliokuwa wakimfahamu Tino mpaka huyo Max mwenyewe! Madonda mabaya yakutisha yaliyokuwa yamejaa matakoni kwake mpaka kufika mgongoni na katikati ya mapaja yakiwa na kinyesi chake! Akakumbuka jinsi alivyomuuguza kwa shida, akisimangwa na Lela mwenyewe. Akakumbuka kashfa za Emma alipomkuta na huyo Tino, lakini akajikaza akimtibu kwa upendo! Lakini leo Tino anamuacha yeye hospitalini! Sabrina akazidi kulia asiamini kama ule ndio ulikuwa mwisho mbaya vile na Tino.

Alishakuwa na wasiwasi na hitimisho lao. Alijua wao hawaendani kabisa, lakini hakujua kama wangeachana vibaya vile. Akakumbuka maneno ya faraja aliyofarijiwa na Tino kuwa wataweza kuishi tu pamoja. Asiwe na wasiwasi juu ya tofauti ya umri na utajiri. Lakini leo Tino anamuacha yeye hospitalini akiwa mgonjwa! Sabrina akajiambia kweli mwanadamu si Mungu. Hubadilika. “Lakini asingekuwa Tino!”  Akazidi kuumia na kulia mpaka akapitiwa tena na usingizi.

Sabrina Aachwa Tena. Safari hii na ujauzito.

            Mchana alimshwa na yule daktari, akamruhusu. Alitoka hapo kwenye hiyo dispensary asiamini anarudi kwenye ile Villa akiwa peke yake. Tino hayupo! Lakini hapakuwa na jinsi, ilibidi aondoke pale na maisha yakaendelee. Alipofika ndani alikuta Tino alichukua nguo zake zote. Hakubakisha hata chupi moja. Sabrina akaanza kulia tena huku amejishika tumbo. Aliitumia siku hiyo na mbili mbeleni kulia tu na kushindwa kufikiria. Alipoanza kusikia kichwa kinagonga kama kuna mtu anapiga ngoma huko ndani, akajiambia asijilize tena, Tino ndio ameondoka, hatarudi tena. Hana mama wala dada wa kuzungumza naye kinachoendelea kwenye maisha yake kwa wakati huo. Akajua anatakiwa kupambana peke yake. Akajituliza.

Ilipofika ijumaa, Tino akampigia simu. Baada ya salamu ya kawaida akamwambia kuna kijana amemtuma huko Moshi kuchukua gari yake. “Sawa.” Bila shida Sabrina akakubali. “Kwaheri.” Tino akaaga bila nyongeza ya kumjulia hali. Hakuuliza hata maendeleo yake tokea amuache hospitalini daktari alipomwambia anamlaza kwa kupoteza damu nyingi! Sabrina akaanza kulia tena, lakini akakumbuka anajihitaji yeye na akili yake ili kuweza kuendelea na maisha. Akanyamaza kwa haraka akijifuta machozi. “Kulia haitanisaidia kwa lolote.” Akakumbuka gari ya watu inakuja kuchukuliwa. Akatoka hapo na kwenda kwenye gari kuangalia kama aliacha kitu chake chochote humo. Akachukua kila kitu na kuisafisha hiyo gari.

Kesho yake asubuhi na mapema gari ikaja kuchukuliwa. Sabrina akilisindikiza kwa macho. Akajishika tumbo asiamini kama ameachwa rasmi na mtoto. Hapakuwa hata na dalili ya tumbo kuwa na mtoto. Kamwili kake kembamba kaliachwa vilevile. Baridi ikamrudisha ndani. Upweke ukamwingia mpaka kwenye mifupa. Kweli akatamani kama angekuwa nyumbani. Gafla akamisi mpaka yale mazingira ya nyumbani kwao. Japokuwa alikuwa akisimangwa, lakini kulikuwa na watu wakuzungumza naye. Kijana wa kushugulikia ng’ombe aliyekuwa akifanya naye kazi, na dada wa kazi pia walikuwa wakipatana sana. Wakiwa jikoni vicheko vilikuwa haviishi kati yao, wakipeana stori za mtaani na gengeni wanapokwenda wakitumwa. Basi hayo ndio yakawa maeneo yao hao wawili yakujidai. Wakajikuta wakipatana hata usiku wakilala stori huwa zilikuwa zikiendelea na vicheko. Lakini siku hiyo Sabrina akajikuta kwenye hicho chumba kizuri sana, Moshi, ndani ya Villa ya kitalii, akipishana na wazungu tupu kuashiria ndio wageni wa hapo na ndio wanaoweza kupamudu hapo kimalipo. Inamaana alikuwa kwenye mazingira mazuri sana kuliko nyumbani kwao, pesa ipo benki sio kama zamani, lakini yuko peke yake na mtoto anayekuwa tumboni, baba yake ameondoka akiridhia amemuua!

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

M

wezi wa kwanza ukaisha akiwa peke yake hata Tino asimsikie. Na wembamba wake mimba ya miezi miwili kitumbo chake kidogo kikaanza kuwa kigumu kwa chini. Taratibu akili ikaanza kuamini kuwa kuna mtoto humo ndani. Akili inatakiwa izidi kufikiri zaidi kabla mtoto hajaja duniani. Wapi atamuweka! Ni kweli kwa wakati huo alikuwa akiishi bure, kasoro chakula ndio alikuwa akigaramia. Huo ukawa mwezi mmoja tokea kuondoka kwa Tino. Akajiambia amebakisha miezi miwili kuondoka hapo. Akaanza kuzunguka hapo mjini kwenye madaladala. Pesa anayo yakufanyia biashara, swali likawa biashara gani atafanya na huo ujauzito! Akapiga mahesabu. Muda wa hiyo biashara kuanza, makosa atakayofanya hapo katikati mpaka aifahamu hiyo biashara na kupunguza makosa na kuanza kupata faida, akajua kwa wakati huo muda haupo rafiki. Anaweza anza, biashara ikiwa ipo sehemu inayomuhitaji zaidi yeye ili iianze kumlipa sasa, ndipo kikawa kipindi cha yeye  kujifungua. Akaona ni bora atafute kazi yeyote yakujishikiza mpaka ajifungue na mtoto akue kidogo ndipo aanza biashara.

Ikaanza kazi ya kutafuta kazi. Kukawa na ahadi tu. Mwezi wa pili wa kuisha hapo nao ukaisha bila kitu chakumuingizia kipato ila kutumia akiba aliyokuwa nayo. Na upweke nao ukazidi. Akamkumbuka Jack. Akalia sana akimkumbuka Jack akijutia nafasi aliyompa akimkaribisha kwake, ila yeye kuamua kumkatalia yeye Jack, ili abakie na Tino. Akaumia sana na kumkumbuka Mungu aliyemtoa nyumbani kwao. Sabrina akalia sana kwa majuto.

Akakumbuka maombi aliyokuwa amemuomba Mungu. Akifunga kwa uwaminifu bila kula japo alikuwa akifanya kazi ngumu, lakini alikusudia kuutafuta uso wa Mungu ili kumsihi amkumbuke pale alipokua. Alimsihi Mungu alainishe mioyo ya wazazi wake wamruhusu kwenda mjini kuwa huko ndiko akakutane na mlango wake wakutokea kimaisha. Mungu akafanya. Ndio ameishia hapo! Akajutia sana akiamini mlango wa kwa Tino haukuwa sahihi, alijipitisha tu huko bila Mungu. Mlango sahihi Mungu aliokuwa amemuandalia kumtoa kimaisha ilikuwa ni kwenda kwa Jack kufanya naye biashara. Akajuta sana lakini asiwe na jinsi ya kubadilisha hilo.

Zoezi la toba nalo likaanza akitubu kwa Mungu aliyempa nafasi na kuichezea. Ikawa hali ya kujilaumu kwa hili na kujifariji kwa lile akijiambia ni Mungu ndiye aliyemtuma kwa Tino ili amtoe kiumbe chake mautini. Basi akikumbuka hilo na kukubaliana nalo kwa wakati huo, zoezi la kufunga akimdai Mungu, Yeye ndio amlipe linaaza. Atafunga akilia bila kula na ujauzito wake akiwa mwaminifu kwenye maamuzi yake hayo mbele za Mungu akitaka yeye aliyemtuma kwa Tino, akawa muaminifu akimuhudumia Tino mchana na usiku bila kumfanyia ubaya wowote mpaka akapona, basi yeye Mungu aliyemfanikisha kwa kiwango kile kwa Tino, basi amlipe. Basi hapo atadai haki zake mbele za Mungu akisimamia milango yake atakayochagua kutoka kwenye bibilia bila kuchoka. Akifanikiwa siku moja na ya pili kumdai Mungu akiwa amefunga, mawazo nayo ya hukumu yanamrudisha nyuma. “Lakini Mungu hakunituma kukimbilia kwenye kitandani cha ndoa cha Tino!” Basi hapo napo Sabrina ataanza tena zoezi la kutubu tena kwa uzinzi. Atafunga akiomba toba mchana na usiku akijitakasa bila kula wala kunywa, ilimradi tu ikawa hali ngumu na mvurugano kwa Sabrina.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

S

iku moja akiwa amezidiwa na upweke asijue hata kama Mungu anamsikia tena na amemsamehe maana mambo yake yalizidi kwenda sivyo, kazi hapati na wala hapakuwa na dalili, akaamua kuingia Whatsapp ili kumfungulia Jack.{Unblock} Ili tu kumuona sura yake ajitulize nafsi. Lakini alipofungua akakutana na picha ya msichana mrembo sana. Ilikuwa usiku. Akalia Sabrina, akajutia sana kuchezea bahati. Jack ameweka mwanamke kwenye profile yake! Inamaana safari hii, kwa mara ya kwanza amepata wa ukweli, ameamua kuweka hadharani! Sabrina akaumia sana. “Nilifikiria nini mimi!?” Akajiuliza bila jibu huku akijilaumu kwa kukimbilia kitandani na Tino ili kumfurahisha mume wa mtu.

Napo alipochoka kulia, akarudi tena kwenye profile ya Whatsapp ya Jack kumuangalia mrembo aliyefanikiwa kuipamba profile yake. Dada alionekana ni wa viwango haswa. Alionekana ni dada anayejielewa, msafi na amejitengeneza, amevutia. Akaona asiwe mchoyo wa pongezi. Akachukua ile picha, akamtumia tena Jack mwenyewe na ujumbe mfupi. ‘Hongera sana Jack. Naona umepata kitu chema.’ Akautuma huo ujumbe. Baada ya muda akamuona yupo online. Akaona amesoma baada ya kuona tiki mbili za bluu. ‘Leo umenikumbuka mrembo?’ Jack akarudisha huo ujumbe. ‘Sijawahi kukusahau Jack. Ni maisha tu. Mzima lakini?’  Sabrina akafurahia kujibiwa na Jack, na yeye akarudisha majibu kwa haraka. ‘Mimi mzima mama. Hofu kwako!’ ‘Nimefurahi kusikia hivyo Jack. Nakuombea ufanikiwe.’ Akarudisha huo ujumbe.

‘Mbona unaninyima kujua hali yako? Unaendeleaje? Kazi iliisha?’ Baada ya kusoma huo ujumbe wa Jack, Sabrina akajikuta akilia. Akalia sana kwa uchungu asijue amjibu nini Jack. Akaona atoke kabisa Whatsapp. Akabaki ameshikilia simu akilia. Alijawa hofu na mimba hiyo ya miezi mitatu, akaamini alichoambiwa na Tino. Na Tino hakutania. Alimuonyesha kwa vitendo hana muda naye. Tokea achukue gari yake, hakumsikia tena. “Ila kwa hakika sitarudi nyumbani na hii mimba!” Sabrina akalipitisha hilo wazo kwa machozi ya hofu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mimba inamiezi mitatu, amebakisha mwezi wa kuishi bure hapo kwenye Villa. Kazi imekua ngumu kupata. Kwa Jack nako kumeshakuwa na Mrembo mwingine.

Ni nini Kitaendelea kwa Sabrina?

Usikose muendelezo….

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment