Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 12. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 12.

Baada ya muda akiendelea kulia, akaona Jack akipiga. Akapokea. “Umeishiwa nini? Mbona umepotea?” Sabrina kimya kwenye simu. “Sabrina!?” Kimya. “Upo mzima?” Akaendelea kuuliza ila ni Jack. Wazi akasikika ni swali la kujali. “Hapana Jack. Nipo matatizoni.” Sabrina akaongea machozi yakimtoka. “Nini tena mama!?” Jack akauliza kwa upendo akionyesha wazi kujali. “Sijui hata niseme nini Jack! Naona mpaka aibu!” “Si kwangu.” Jack akajaribu kumtuliza.

Sabrina akashindwa ajieleze lipi aache lipi. “Kwanza uko wapi?” Jack akaendelea kuhoji taratibu akimsikia Sabrina akilia. “Nimeachwa kwenye Villa hapa Moshi. Hata sijui pakwenda Jack! Nipo peke yangu.” “Njoo Singida. Kesho asubuhi nenda kapande mabasi ya Singida, mimi nitakupokea kituo cha mabasi Singida?” Sabrina alilia, akalia sana, Jack akimsikiliza. “Umenielewa?” “Naogopa Jack, naogopa sana. Sijawahi kuogopa hivi!” Sabrina akaongea akilia kwa kwikwi. “Kwa kuwa upo peke yako. Njoo huku tutajua chakufanya. Hata kesho njoo. Usikae huko peke yako. Njoo, nitakupokea.” “Asante Jack. Nakushukuru.” Akakata simu na kuanza kujifikiria. Anakwendaje kwa Jack na tumbo hilo! Na mabaya yote aliyokwisha kumtenda mpaka hapo ana huo ujauzito!

Akaangalia pale alipo na vinavyomzunguka, akazidi kupatwa ugumu. Abebe kipi na aache kipi! Na wapi! Amemuona Jack na mwanamke, anakwenda kule kama nani! Sabrina akazidi kuwaza, na kuona sio sawa kwa Jack. Starehe apate yeye, shida akale na Jack! Jack amekuwa mwema sana kwake. Hajawahi kumchoka. Akakumbuka chuoni. Jinsi alivyomtukana. Alivyoachwa vibaya na Emma, Jack akamuokoa. Miezi michache iliyopita wakawa kwenye mawasiliano mazuri mpaka kufikia hatua ya kukubaliana kuanza biashara pamoja, huku akimtamkia waziwazi anamkaribisha nyumbani kwake na bado akitaka anaweza akawa yeye ndio mama mwenye nyumba! Tino akaingilia kati. Akamtumia tu ujumbe wakuahirisha makubaliano yao, na kumblock kila mahali. Leo aende akiwa na mimba ya mtu mwingine, tena Jack akiwa amebahatika mwanamke mzuri vile! Akaona hatamtendea haki. Anastahili pumziko na mwanamke wake mpya. Sabrina akawaangalia tena pichani na kujikuta mawazo yanamtoa pale kwenye profile ya Jack.

Chuoni.

K

umbukumbu zikamrudisha alipokuwa chuoni kabla ya kutendwa na Emma. Akakumbuka kipindi hicho Jack alipomtongoza na kumshushua vibaya mbele ya mawaziri waliokuwa wakifanya kazi chini yake Jack aliyekuwa anababaikiwa sana hapo kwenye hicho chuo. Kwanza alikuwa ni Jackson Msindai! Mtoto wa Msindai! Jina linavuma nchini sababu ya mama yake na kaka yake ambao wameshika nyadhifa za juu sana serikalini. Hata yeye uongozi wake hapo chuoni ulikuwa bora. Kijana aliyetoka kwenye familia ya uongozi. Walimu wenyewe walikuwa wakimsifia anajua kuongoza. Halafu hata muonekano wake ulikuwa unavutia. Jackson hakuwa mbaya! Wakati wote ni msafi. Mtanashati. Halafu pia alisifika kwa akili nzuri za darasani. Kila mtu alikuwa akimfahamu Jackson Msindai na kutaka kuwa naye karibu lakini haikuwa hivyo kwa Sabrina. Alimtenda kinyume na kila mtu na kushangaza wengi na kumuacha Jack akionekana kicheko hapo chuoni kwa jinsi alivyomkataa bila heshima. Jack alichora vikatuni mpaka kwenye kuta za vyooni huko chuoni akidhihakiwa sababu ya huyo Sabrina. Akachafuliwa vilivyo kwa sababu ya huyohuyo Sabrina.

          Lakini Jackson huyohuyo akiwa amemuumiza kwa kumtia aibu chuo kizima kwa kiasi hicho yeye kama raisi aliyeheshimiwa sana, akageuka kichekesho kwa watu sababu yake, napo baada ya kuachwa kikatili na Emma, bado alimsaidia bila kinyongo mpaka akamaliza chuo alichokuwa akikaribia kufukuzwa. Sabrina akabaki akimtafakari Jack asielewe moyo wake.

          Sabrina akakumbuka siku aliyomfuata wakiwa chuoni vile ambavyo hakuzungumza maneno mengi ila tu kumtaka amfuate. Kwa fedheha aliyokuwa nayo Sabrina, alishindwa hata kusimama hapo alipokuwa amemfuata mafichoni. Akakumbuka kushindwa kumjibu kabisa wala kusimama. Akabaki ameangalia pembeni.

Hivi ndivyo ilivyokuwa kati ya

Sabrina na Jack Chuoni.

J

ack akamwita tena taratibu tu baada ya kushindwa tena kusimama. “Sabrina!”  Sabrina akamtizama. “Naomba tuongozane.” Sabrina akajifuta machozi, akanyanyuka bila ya kusema neno. Jack akaongoza njia mpaka kwenye jengo ambalo ni la viongozi. Kila mtu akimshangaa Sabrina aliyepoteza sifa pale chuoni, akiongozana na mtu kama Jack! Moja kwa moja mpaka kwenye chumba cha Jack alipokuwa akiishi peke yake kama raisi. “Kaa ule kwanza.” “Mimi sina njaa.” “Najua hujala, acha hasira zinazokuumiza wewe mwenyewe. Kula halafu upumzike.” Sabrina akaangalia kitanda, akarudisha macho kwenye chakula. Akatulia. “Nimekukaribisha chakula, ndipo ulale. Halafu tutazungumza.” “Juu ya nini!?” Akauliza Sabrina kwa ukali kidogo huku amekunja ndita.

          Jack akakaa. “Naomba ule, ulale ndipo tuzungumze. Mimi sina vipindi vya mchana huu. Najisomea hapahapa chumbani. Naomba ukae, acha kusimama.” Sabrina akakaa kitandani badala ya kwenye kochi dogo hapo pembeni ya kitanda. Jack akabaki akimtizama. Kimya amejiinamia. Baada ya kama dakika, akamuona anavua viatu, akajilaza kitandani kwake. Jack akasimama na kumfunika. Hapohapo Sabrina akapitiwa na usingizi. Hizo kumbukumbu nazo zikamrudia Sabrina. Akavuta pumzi kwa nguvu na kuendelea kukumbuka.

          Habari zilienea kwa haraka sana kuwa Sabrina amelala chumbani kwa Jack, raisi wa hicho chuo. Naye Sabrina kama mfu, alilala karibu siku nzima. Alifungua macho jasho linamtoka kwa kufunikwa, Jack anavaa nguo ametoka kuoga. Akajifunika kwa haraka mpaka kichwani. Akamsikia Jack akicheka. “Sasa kwa nini unavaa mbele ya mgeni bwana!” Sabrina akalalamika. “Mimi nilijua bado umelala!” Akamsikia amekaa palepale kitandani.

          “Mama wewe umelala ugenini kama kwako!” Sabrina akacheka ndani ya shuka. “Unakoroma mpaka nimeshindwa kusoma!” “Muongo Jack, mimi huwa sikoroni.” Akabisha Sabrina. “Mbona nilijua utabisha tu, ikabidi nikuchukue video kabisa usije sema nimekusingizia!” Sabrina alicheka sana. “Ujue huna akili wewe Jack! Sasa kwa nini ualike mgeni halafu uje umdhalilishe?” “Mimi huu ni ushahidi wangu mama. Wala si kukudhalilisha.” Akamuwashia simu yake na kumuweka hiyo video. Sabrina alicheka sana, alijiona vile alivyokuwa amelala huku akikoroma. “Bwana Jack!” “Mimi naomba uangalie mpaka mwisho, kuna swala la mpaka ute, udenda kabisa humo ndani ya hiyo video!” Sabrina akafuta ile video kwa haraka akamrudishia simu yake. “Sitaki. Kwanza huyo sio mimi!” “He! Unajikana mwenyewe!” Kidogo wakacheka.

          “Nilikuwa nimechoka Jack! Sana. Halafu sikuwa napata usingizi.” “Haya, usingizi umeisha sasa tuzungumze maswala ya shule wakati unakula.” Sabrina akakaa. Jack akampashia moto chakula, akaanza kula. Hicho chumba cha raisi wa Chuo kwanza ungependa kuwepo humo. Mama Msindai aliwekeza hapo kwa ajili ya kiziwanda wake, utafikiri chumba cha mfanyakazi fulani. Kulikuwa na vitu vichache lakini vizuri vitupu. Kitanda chenyewe cha Jack mama yake alimletea, hakutumia cha hapo chuoni. Mashuka mazuri na blangeti safi pembeni. Kusafi kama Jackson mwenyewe. Sabrina akaanza kutulia mawazo kwa ile mandhari pale ndani.

 “Mambo yako ya shule ni mabaya Sabrina.” “Yepi sio mabaya?” Akauliza Sabrina kwa kuumia. “Naongelea kile unachoweza kubadilisha kwa sasa. Mengine huna uwezo wa kuyabadilisha, lakini hili unao uwezo. Walimu wote wameshakuripoti kwa mkuu wa chuo kama huingii darasani na haupo chuoni. Unajua sheria za chuo. Kwa kifupi umeshajifukuzisha chuo. Leo asubuhi nimetoka kuzungumza na mkuu wa chuo nikimuomba asiwasiliane na wazazi wako kwanza, kuwataarifu kama umejifukuzisha chuo rasmi, nione kama unaweza kurejea.” Sabrina alishituka sana. Wazazi wake! Jack akakaa mbele yake.

          “Wewe sio wa kwanza kuachwa au kukataliwa vibaya Brina!” Vile tu kumuita Brina, kukamtuliza. “Wewe ni shahidi yangu, mimi pia nilishakataliwa vibaya sana, tena mbele ya umati wa watu, cafteria!” Sabrina akashindwa kuendelea kumuangalia, akainamia chakula chake. Akakumbuka aibu aliyomtia Jack. “Unakumbuka kashfa yake! Unakumbuka jinsi nilivyochorwa hapa chuoni? Nilipewa kila aina ya majina baada ya lile tukio. Lakini uliniona nikiacha kuingia darasani? Kwani ilidumu muda mrefu?” Sabrina akabaki ameinamia sahani ya chakula kwa aibu na uchungu. Hata kula akashindwa.

          “Halikuwa kosa langu kukupenda, Brina. Mimi kama mwanaume, nikajaribu bahati yangu. Ukanikataa. Katika yote, nikaishia kujitia moyo kwa kujipongeza kuwa nilijaribu ila sikufanikiwa. Watu waliponiona nimesimama, naendelea na shule yangu vizuri, tena vizuri sana kuliko wao. Mimi ndio wananihitaji niwafundishe na niwaongoze, heshima yangu ikarudi. Sasa tofauti yangu mimi na wewe ni hapo. Wewe umekubali kushindwa ndio maana mpaka leo wewe umebaki kuwa kituko. Darasani haupo. Nasikia ripoti yako ya field mpaka leo hujaiwakilisha wakati wenzako wote washakusanya. Ni kweli au sio kweli?” Sabrina kimya.

          “Darasani huingii, mitihani kufanyi! Labda mimi nikuulize, ni kwa faida ya nani? Maana mmebakisha miezi michache sana, mnaondoka hapa chuoni. Hawa watu wote hawa unawapa nafasi kwenye maisha yako, hutaowana tena. Ushajiuliza itakuaje baada ya haya yote?” Kimya. “Sasa mimi nimeomba uongozi wanipe muda wakuzungumza na wewe nijue kama unataka kuendelea na chuo au unaacha!” “Nilifikiria pengine niombe kuahirisha mwaka huu, ili nije kumaliza mwakani.” Akajibu Sabrina taratibu.

          Jack akabaki amenyamaza. “Hata hivyo nimeshachelewa Jack. Nipo nyuma kwenye kila kitu, siwezi kuwa na wenzangu tena. Naomba uniombee kuahirisha.” “Ukikubali kushindwa leo, ujue hata ukirudi hutamaliza Brina. Ila nakuhakikishia kabisa, ukiamua leo. Na hivi zile safari zako za kila weekend unahamia kulala hotelini au kwenda Dar zimesitishwa, utaweza tu.” Sabrina akamwangalia Jack na kurudisha macho kwenye chakula ambacho hata hakuwa akila tena kwa aibu. “Inamaana alikuwa akinifuatilia kila nilipokuwa nikitoka hapa chuoni!?” Akajiuliza Sabrina akikumbuka utalii aliokuwa akifanya katikati ya hiyo shule yake, hapo chuoni kwa ajili ya kumfurahisha Emma.

“Sikukejeli Brina, ila nakwambia ukweli. Umepunguza sababu kubwa sana iliyokuwa ikikufanya usifanye vizuri darasani. Nimekuwa nikiangalia matokeo yako yote tokea unaingia hapa chuoni. Wakati wote wewe umekua ukipita kwa Pass. Ni kwa kuwa akili yako haikuwa chuoni. Sasa kwa wakati huu ukiweka akili chuoni, ukapambana mchana na usiku, ukiwa hauna kinachokufunga isipokuwa elimu tu, nakwambia hata wale waliopo darasani sasa hivi, utawapita.” Sabrina akakunja uso kama asiyesadiki.

          “Umefikia wapi kwenye ripoti?” “Sijafanya chochote Jack.” “Sasa leo umelala karibu siku nzima. Hujachoka, chakula hicho hapo. Kula. Nenda kaoge, uanze kuandika.” Sabrina akabaki akifikiria kurudi darasani na yale macho ya watu! “Brina?” “Nafikiria sehemu ya kwenda kuandika.” “Wewe ukiwa tayari, njoo hapahapa, tena nitakutafutia mtu wa mwaka wa tatu ambaye amemaliza yake, na nimesikia pale ofisini kwa ma lecturers, walimu, wakimsifia ripoti yake ni nzuri. Nenda kaoge, urudi hapa. Acha kukatakata tamaa na kukimbia.” Sabrina akamaliza kula, akatoka hapo baada ya kushukuru.

Kila alipopita hapo kwenye korido alijua viongozi wote wanaoishi kwenye hilo jengo, wanamshangaa yeye na kule alikotoka, chumbani kwa raisi, Jackson Msindai. Akajikaza akarudi chumbani kwake. Akashangaa msichana anayeishi naye hapo chumbani ambaye alikuwa akishiriki kumkebehi kwa hali ya juu, nakumfanya Sabrina kushindwa hata kukaa hapo chumbani na kukimbia chumba alicholipia hapo chuoni, ni kama ametulia! Hakumsemesha. Akaenda kuoga. Akarudi kujitayarisha, akachukua madaftari yake, na faili alilokuwa amefanyia field, akatoka tena kurudi kwenye jengo la viongozi, gorofa ya juu kabisa ambapo kipo chumba kikubwa cha huyo raisi wa chuo, Jackson Msindai.

          Akagonga mara moja tu, akasikia sauti ya Jack ikimkaribisha. Alibabaika alipoingia nakumkuta Jack amekaa, Phina amemkalia kwenye mguu mmoja, Jack amepitisha mkono kiunoni. Akasita. “Samahani, sijui kama...” “Wewe njoo. Nimekuletea mkali wangu Phina. Ushindwe wewe tu. Atakusaidia na kukuelekeza kila kitu. Nimemuomba leo akusaidie. Sasa mtumie vizuri. Maswali yote juu ya ripoti, atakusaidia. Tena ukimbana vizuri, hata leo mnaweza kumaliza, kesho tukiongozana kwa mkuu wa chuo, hata ukizungumza, una kitu mkononi. Sawa?” “Nawashukuru kwa msaada. Na asante Phina kwa kukubali kunisaidia.” “Wala usijali. Ukituliza akili, utamaliza tu.” Mrembo  Phina akamtuliza.

          Akamgeukia Jack, wakapeana busu kidogo, Sabrina akajibaraguza kama anayeangalia faili lake. Wala hakujua kama ni wapenzi. Hakuwa hata na muda na mambo ya hapo chuoni. “Acha nikasome na washikaji. Wananisubiri. Mkimaliza kabla sijarudi, usiondoke, unipigie.” “Sawa.” Phina akakubali na kusimama. “Haya mrembo, kazi kwako. Kesho mimi na wewe kwa washitaki wako. Hakikisha hatuendi mikono mitupu.” “Nitajitahidi.” Akakubali Sabrina, kwa kuumia. Hakujua hata ni kwa nini apatwe wivu kwa mwanaume aliyemkataa. Akakumbuka jinsi Phina alivyohangaika naye mpaka wakamaliza hiyo ripoti na Jack kufanikisha kumrudisha chuoni baada ya kumuombea kwa mkuu wa chuo.

Sasa Hivi.

Alipoyakumbuka hayo yote, Sabrina akajiambia hata iweje, hatakwenda tena kwa Jack huko Singida. “Yaani mimi nitakuwa mtu wa kukombolewa tu na Jack! Yaani nakuwa narudi kwake nikiwa matatizoni tu! HAPANA.” Sabrina akakataa kwa kutingisha kichwa kabisa akijifuta machozi ya majuto. “Ni heri nihangaike mpaka mwisho wangu mimi mwenyewe, kuliko kumfanya Jack ndio kuwa mkombozi wangu kila siku, tena safari hii na mimba juu! Hapana.” Aibu ikazidi kumsumbua. Akakubaliana na mawazo yake, kutomfuata. Lakini kile kitendo tu cha kuzungumza naye Jack kikamfanya ajisikie vizuri sana, angalau akaupata usingizi wa siku hiyo bila shida. Akapata usingizi mzito wa mimba, akalala wala asijue alipo.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

          Akaja kuamka saa nne asubuhi. Akakuta missed calls 5 za Jack. Akampigia. “Nilikuwa nimelala Jack. Mzima?” “Mzima. Sasa unakuja saa ngapi?” Jack akauliza. “Naona sitakuja Jack.” “Kwa nini tena!?” Jack akauliza akisikika kukata tamaa. “Nimefikiria, nikaona sitakuwa nikikutendea haki Jack. Naomba wewe uwe na amani. Endelea na maisha yako tu. Unastahili kupumzika. Nishakupitisha kwenye mengi magumu, Jack. Inatosha. Acha nipambane mwenyewe, pengine nitafanikiwa. Naamini nitakuwa sawa.” Kimya. “Jack?”  Sabrina akaita na kuiangalia simu yake kama imekatika au la! Sabrina akagundua simu haijakatika.

“Naomba uwe na amani Jack. Naamini nitakuwa sawa.” “Umepata kazi au biashara yakufanya?” Jack akauliza. “Hapana. Nimehangaika karibia miezi miwili sasa. Kila nilipoenda waliniambia ndio wanapunguza wafanyakazi. Ila juzi nimekutana na mtu mwingine. Anayo baa karibu na stendi kubwa ya hapa Moshi. Ameniambia anafungua baa nyingine maeneo ya soko la Kiboriloni, kama nitasubiri anaweza kunipa kazi. Nimechukua namba yake ya simu, na yeye nimempa yangu. Nimemwambia nitasubiri. Na kama atakuwa na kazi yeyote kabla ya hapo, nimeomba anikumbuke. Amekubali. Ndio nipo kwenye kusubiri huku nikiendelea kutafuta.” Sabrina akajieleza kwa upole.

“Unaishije sasa hapo?” Jack akauliza kwa kujali. “Ni Villa yenye vinyumba, kama apartment zilizo na kila kitu ndani.” Akamtajia jina la hizo Villa na kumuelekeza  zilipo. “Nina vifaa vichache tu, hasa vya jikoni ndio vyangu. Kwa hiyo nimepewa hifadhi hapa mwezi huu unaoanza, ukiisha ndio mwisho hapa. Nafikiria kutafuta chumba kama nitapata hapa kazi.” “Ukikosa?” Jack akauliza tena. “Hata sijui Jack! Nitajua mbele ya safari.” Jack akatulia kwa muda. “Lakini nakushukuru sana Jack. Asante kwa moyo wako.” Kimya. “Naamini nitakuwa sawa tu.” Sabrina akajaribu kumpa moyo kana kwamba sio yeye aliyekuwa akilia usiku uliopita.

          Baada ya kutulia kidogo kama akifikiria, Jack akauliza. “Unaruhusiwa wageni hapo?” “Karibu Jack. Muda na wakati wowote ukifika getini watanipigia simu, nikiwaruhusu wakufungulie, watakufungulia geti.” Kisha akajishitukia tena, Jack aliuliza swali tu, yeye akaweka ukaribisho. Akaona aulize ili apate uhakika. “Kwani unataka kuja kuniona, Jack?” Sabrina akauliza kwa unyonge. “Ndiyo. Nafikiria hivyo.” Sabrina akaanza kulia tena. Akalia hapo, Jack kimya. Mwishoe akakata simu yeye mwenyewe.

Old is Gold...

I

likuwa siku ya ijumaa kama kwenye saa moja usiku hivi. Sabrina alikuwa amejilaza kwenye kochi baada yakuzunguka sana mjini siku hiyo akipita kwenye mabaa na maduka akitafuta kazi bila mafanikio. Akasikia simu ya mezani ikiita. Akaamka. Akaikimbilia, akaambiwa ana mgeni. Moja kwa moja akajua ni Jack tu. Akawaomba wamuelekeze alipo. Akatoka kwenda kumsubiria nje. Baada ya dakika chache tu akaona Range Rover Sport inakuja. Akashanganzwa kidogo. Hata kwa kina Tino wenye pesa hawakuwa na aina hiyo gari. Akaanza kubabaika akidhani si Jack pengine amejichanganya. Akajituliza ili angaalie linapoelekea na anayeshuka. Ilivyokuwa ikimkaribia akaanza kumtambua Jack. Ndipo akaangalia hiyo gari tena vizuri. Ilikuwa nzuri sana. Rangi nyekundu inayokwenda damu ya mzee, ila imeiva ya kuwaka hata gizani. Akajua Jack alinunua gari ingine sio kama ile aliyokuwa nayo chuoni. Akamuelekeza kwa kidole ni wapi pakuegesha gari yake, Jack akaelewa, akaegesha kama alivyoelekezwa.

Sabrina akakimbilia mlango wa dereva, akafungua. Kwa hakika Jack alibadilika. Si mwanafunzi tena. Jack muajiriwa. Alipendeza haswa, akaonekana mambo yake ni mazuri na hali ya uwanafunzi imeisha. Sabrina akarudi nyuma kidogo. Jack aliyemtegemea akutane naye si huyu. Jack akamuona amebabaika. “Hujambo mama?” Sabrina akaanza kulia tena akiwa amesimama hapo pembeni ya mlango, Jack akimwangalia akiwa amekaa kwenye kiti cha dereva. “Pole kwa matatizo.” “Nimefurahi kukuona Jack. Umependeza!”  Akacheka. “Hata wewe umependeza.” Sabrina akamwangalia na kuinama. “Mbona sikaribishwi! Nimechoka Brina! Nimeendesha kwa masaa karibu saba!” “Pole Jack. Twende ukapumzike. Una mizigo mingi?” “Kibegi kidogo tu, nitabeba.” Jack akashuka, akafungua mlango wa nyuma, akatoa kibegi kidogo tu, Sabrina akaongoza njia. Jack akifuata nyuma, wakaingia ndani.

“Nipazuri sana. Si itakuwa ni aghali sana?” Akauliza Jack. “Ni ghali kwa hakika. Njoo huku chumbani. Najua ungependa kuoga.” “Nitaoga wakati wa kulala. Acha tupate muda kidogo.” “Basi nikuwekee begi ndani.” Sabrina alimuona jinsi Jack anavyomuangalia kwa makini. Akampokea begi, akaingiza ndani na kuelekea sehemu ya kupikia. “Acha nikutengenezee hata chai Jack. Kunabaridi!” “Nina njaa Sabrina. Nataka chakula kabisa, sio chai peke yake. Kama hamna chakula, twende tukale nje.” “Nina mboga nilizounga tayari. Nipe muda mfupi nikupikie ugali.” Jack akasogea pale jikoni, akakaa kwenye kiti cha meza ya hapo karibu na jikoni. Jiko lenyewe ilikuwa safi na la kisasa na vimeunganishwa kwenye umeme.

“Umebadilika Jack!” “Nimekuaje?” Jack akauliza huku akicheka. “Umezidi kupendeza. Wanakulipa vizuri eeh!” “Siyo mbaya. Siwezi kulalamika. Halafu pia tulianza ile biashara niliyokwambia tufanye, lakini ukaja kubadili mawazo. Ukasema hutaweza tena kuungana nami huko Singida na wala hutafanya tena hiyo biashara. Nilipopata ule ujumbe nikawa kama nimekata tamaa kidogo, lakini baada ya siku chache, nikaona nianze tu.” Sabrina akajutia sana. “Vipi lakini, unaonaje?” Akajikaza na kuuliza. “Mwanzo sio mbaya. Lipo tumaini. Japo kila biashara inakuwa na changamoto zake, ila sio mbaya.” Sabrina akanyamaza huku akiendelea kupika na kupasha moto chakula.

Akamuona anatoa simu, akapiga. “Nilifika salama, japo tairi ya nyuma iliisha upepo. Nikadhani ni pancha. Walipoiangalia, kumbe ilikuwa ni upepo tu.” Akamsikia Jack akiongea. “Asante sana. Vipi na wewe?” Akamsikia akiuliza. Akajua anazungumza na mpenzi wake. Akacheka kidogo huku akisikiliza. “Mpuuzi yule, achana naye. Anakutisha tu.” Akajibu Jack huku akicheka. Akacheka tena na kuendelea kusikiliza. Sabrina akapotelea mawazoni huku akipika na kupasha moto hiki na kile wakati Jack anaendelea kuzungumza. Akamuwekea chai hapo mezani. “Asante.” Akashukuru kwa kunong’ona huku akisikiliza simu. Sabrina akaendelea na mapishi yake.

Hata hakujua Jack alimaliza kuzungumza na simu muda gani, lakini wakati anamuwekea chakula mbele yake, akagundua alikuwa akimtizama muda wote. “Karibu.” Akamuwahi ili asimwangalie zaidi. Tumbo la Sabrina bado lilikuwa halionyeshi sana kutokana na umbile lake. Usingemgundua kwa haraka kama ni mjamzito. Akampisha Jack anawe hapo kwenye sinki ya jikoni, akakaa pembeni yake. Jack akamwangalia kidogo kabla hajaanza kula. “Nimefurahi umekuja kunitembelea Jack.” Jack akacheka kidogo. Akamuona anaombea chakula na kuanza kula.

“Mbona wewe huli sasa?” “Nilikuwa na siku ndefu. Nimerudi hapa nikiwa na njaa, nikala viporo vyote ndipo nikalala.” “Ulikwenda wapi?” Jack akauliza na kuendelea kula. “Nazunguka kutafuta kazi Jack. Leo niliwapitia wote walioniambia wangenipigia, lakini sijafanikiwa. Ndio nasubiria hiyo baa ifunguliwe. Natamani nipate kazi mapema ili nijue natafuta maeneo yapi yakuishi. Ila nimejiwekea mwezi huo unaokuja wakati muda wa hapa ukiisha, kama sijapata kazi, niondoke kabisa hapa Moshi, nihame mji.” Jack akamwangalia.

Kisha akatupia swali jingine baada ya kumeza. “Unataka kuhamia mji gani kama si hapa?” “Sijajua kwa hakika, lakini nahisi naweza kurudi Dodoma ambako tulishaishi. Sitaki nihamie kwenye mji nikawa mgeni sana. Nahisi itanichukua muda mrefu kujijenga.” Jack akaendelea kula.

“Unawasiliana na nyumbani?” “Hapana Jack. Nimeona niwaache kwanza mpaka nitakapojijenga, ndipo niwatafute. Nisiwe mtu wa kuwavunja moyo kila wakati.” Jack akaendelea kula. “Huu ugali na mahare, na nyama ya kukaanga ni vitamu sana Brina. Naomba ule kidogo.” Sabrina akacheka. “Ungeniona jinsi nilivyokula mchana!” “Kula tena kidogo. Fungua mdomo nikuwekee kidogo uone ninavyofaidi.” Sabrina akacheka sana. “Kama ni hivyo acha nioshe mkono nile kidogo.” “Hayo ndiyo maneno.” Sabrina akaosha mkono, akajiwekea kidogo kwenye sahani akaanza kula. “Hujabadilika sana Brina. Mwili bado mdogo! Umegoma kunenepa?” Sabrina akacheka kidogo nakubaki akifikiria.

Akakumbuka alitoka kwao akikimbilia kwa Sabina dada yake ili akapumzike, akaishia mikononi kwa Lela aliyemuachia jukumu la Tino. Ulalaji ukawa wa shida kwa kuuguza. Tino anapata nafuu ndipo huo ujauzito na kutelekezwa. Akanyanyua uso, akagundua Jack anamtizama. Akarudisha macho kwenye chakula. “Bado sijatulia Jack. Pengine nikija kutulia, naweza kuongezeka.” Ikabidi ajieleze tu. Jack akaendelea kula. Wakamaliza kula, akasafisha meza, wakabaki wamekaa hapohapo mezani.

“Ulipata kazi gani hiyo iliyokufanya ukatupilia mbali mipango yote tuliyokuwa tumezungumza?” Jack akauliza taratibu tu. Sabrina akainama akijaribu kuzuia machozi, mwishoe akaanza. “Unakumbuka nilikwambia nimechoka pale nyumbani nataka kwenda kwa dada Sabina?” “Nakumbuka na hata ulipopata hiyo kazi ambayo uliniahidi ungekuja kuniambia ni kazi gani tukikutana kabla hujagairi, tulizungumza.” Sabrina akapoa kidogo. “Ulikuwa ukifanya kazi gani?” Jack akauliza kwa upole tu akimtizama.

Sabrina akamuelezea tokea akutane na Lela, mpaka akaachiwa jukumu zito la Tino. Jack akimsikiliza tu. Jinsi alivyomuuguza kwa shida na hali aliyomkuta nayo mpaka kuondoka kwa Lela na kuachwa wao wawili. Akanyamaza. “Nakusikiliza Brina.” “Walifikia hatua yakuachana Jack. Hapakuwa na dalili yakuja kurudiana tena. Ile hali ya vitisho, Tino akihofia kuja kuuwawa na Lela na mpenzi wake, akaonelea tuhamie huku kwa matibabu wakati mwanasheria wake akiendelea na kufuatilia talaka.” Jack akamuona midomo inaanza kumcheza kwa hofu, akajua lipo jambo hapo linatafutiwa jinsi ya kuelezwa. Akatulia kumsikiliza.

“Tulitulia kwa majuma kadhaa ndipo mkewe akaanza tena fujo akisema yeye bado anampenda mumewe, ila mumewe ndiye amemtelekeza. Hapo akawa analalamika. Hata mimba iliyosemekana anayo akawa hana tena kitu kilichomtia hofu Tino maana alijua hiyo ndiyo ingekuwa silaha yake.” Sabrina akanyamaza baada yakumuona Jack ametulia sana akimsikiliza.

“Ehe?” Jack akamtaka aendelee. Sabrina akanyanyua uso kumtizama. “Ndipo sasa ikabidi Tino arudi Dar ili kufuatilia mambo yake ya ndoa.” Akahitimisha hivyo, Jack akajua lipo la ziada. Akatulia kidogo kisha akaona aulize tena. “Kwa hiyo amekuacha hapa kwa makubaliano gani? Sijaelewa.” “Ndio kazi imeisha.” Jack akakunja uso kidogo. “Mbona nahisi kama kuna kitu nyuma ya hilo jibu la sasa hivi.” Sabrina akabaki ameinama. “Brina?” “Aliniacha hospitalini.” Akajibu macho chini. “Ukiwa unaumwa na nini?” Kimya. “Brina!?” “Akiwa amenipeleka kutolewa mimba.” Jack akabaki kama ameduaa. Ni kama hakuwa ametegemea hilo jibu kabisa.

“Kwa hiyo akaondoka akiwa ameridhia kuwa nimetoa mimba, kumbe nilimdanganya. Nilipoingia chumba cha kutolea mimba, nikamwambia yule daktari..” Sabrina akamuelezea tena Jack kila kitu. “Kwa hiyo hapo ulipo ni mjamzito wa mimba ya miezi mitatu!?” “Ndiyo Jack.” Akajibu kwa aibu na unyonge, Jack akimwangalia. Akamuona mishipa ya pembeni ya macho imesimama. Macho yakabadilika yakawa mekundu haswa. Akabaki akimtizama. Sabrina akainama. Jack akasimama na kuondoka pale bila yakuongeza neno akahamia sebuleni. Lakini akashindwa hata kukaa, akabaki amesimama amegeukia tv. Sabrina akashindwa hata chakuzungumza tena. Kimya.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Hata Jack kimbilio la mwisho wakati wote kwa Sabrina hapo amesalimu amri. Ni nini kitaendelea?

Usikose muendelezo…. 

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment