Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 14. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 14.

 

Sabrina alipomuona tu ameweka kituo, akamuwahi ili asipandishe hasira na kuongeza tension pale. “Mimi pia nakuunga mkono Pam. Upo sahihi kabisa.” Jack akamwangalia Sabrina. “Kama hivyo ndivyo ulivyokuwa ukifanya tokea mwanzo, na ukafanikiwa, usibadilike.” Sabrina akaendelea taratibu tu. “Naamini Mungu atanisaidia, nitapata kazi sehemu nyingine.” “Usije nielewa vibaya tu!” Pam akajishusha baada yakumsikia Sabrina amemjibu vile. “Hata kidogo Pam. Kwenye maisha kila mtu anajiwekea kanuni zake. Wanao zisimamia na kuhakikisha hazivunjwi ni wachache sana na ndio mliofanikiwa. Furaha yangu nikuendelea kukusikia umefanikiwa au wewe na Jack mnazidi kufanikiwa. Sio wote tuwe hatuna! Itakuwa haina maana. Niwapashie moto chakula?” Haraka sana Sabrina akabadili mazungumzo.

            “Mimi nipo sawa, mpaka baadaye kidogo. Naona kama bado mapema.” Akajibu Jack. “Na Pam?” “Angekuwepo Emma ningemtuma dukani akalete kinywaji. Nina kiu!” “Kwani ni mbali? Mimi nimelala sana. Nataka kutembea kidogo.” Jack akashituka kidogo, akamgeukia Sabrina na kumtizama kwa mshangao kidogo. “Ningefurahi kutoka. Kama mna kitu kingine mnahitaji mniagizie tu huko dukani.” Pam akamwangalia Jack, Jack akabaki kimya. “Unakunywa soda gani?” Akamuuliza Pam. “Nataka bia baridiii.” Sabrina akacheka. “Aina gani na ngapi?” Akamtajia. “Na wewe Jack?” “Sprite tafadhali.” “Sawa. Hakuna kitu kingine mnahitaji huko dukani?” Wakaangaliana. “Naona ni hivyo tu.” “Basi nitarudi baada ya muda mfupi.” “Mbona huchukui pesa sasa?” “Msijali. Hiyo itakuwa ofa yangu.” Sabrina akarudi chumbani, akachukua pesa na kutoka baada ya kuelekezwa wapi pakwenda.

          Alitoka hapo nia pia ilikuwa nikusoma mazingira. Hapakuwa mbali. Akakuta duka kama alivyoelekezwa. Akanunua hivyo vinywaji alivyoagizwa, akarudi navyo kwa haraka. Akawapangia mezani. “Mmesema bado hamna njaa?” Akauliza Sabrina. “Mimi ningekula kidogo.” Pam akataka chakula. “Na wewe Jack?” Sabrina akauliza. “Mimi naona wakati moyo huo wakutuhudumia ukiwa bado upo, basi kipashe moto tu chote, ukiweke mezani.” Sabrina akacheka na kuanza kuondoka pale. “Naona hilo wazo lako lina akili. Ngoja nikipashe, niwawekee chote mezani.” Akarudi jikoni.

          Akakuta chakula kilichomtoa hata hamu ya kula. Wali mweupe, kama mbichi! Mchuzi mwingi wa nyama ya ng’ombe, ulishaganda mafuta, lakini aliweza kuona maganda ya nyanya. Akabaki amekodoa macho. Akatamani arekebishe, akajiambia asije kumuudhi Pam. Akawapashia moto hivyohivyo kwa kutumia microwave, akawawekea mezani na kwenda kuwakaribisha. “Wewe huli?” Jack akauliza. “Nataka kutoka nitembee kidogo, nisome mazingira ya hapa.” “Usije potea tu?” Pam akatoa angalizo, Sabrina akacheka na kutoka hapo ndani. Angalau Jack akaonekana ni kama ametulia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

J

ack alikuwa akiishi mjini. Sabrina akaanza kutembea huku na kule akiangalia hili na lile. Akapita kwenye baa kadhaa, akiulizia kazi. Mmiliki mmoja akamwambia anatafuta muhudumu wa usiku. Sabrina akafurahi sana. “Naweza kuanza lini?” “Hata kesho.” Hilo akalifurahia sana. Akatoka hapo akiwa na furaha zote. Akarudi nyumbani giza likiwa limeshaingia asijue kama alizunguka siku nzima. Jack akaenda kumfungulia mlango. “Naomba usiwe unafanya hivyo Sabrina. Umenitia wasiwasi.” “Kwani nimechelewa sana!?” Sabrina akauliza taratibu tu. “Umeondoka mchana, unarudi sasa hivi na sikupati kwa simu!” Akamshika mkono.

          “Acha wasiwasi Jack! Mkubwa hapotei. Njoo nikupe habari za nilikotoka.” Akamvutia kwenye makochi, wakakaa. “Nini?” “Mwenzio nimetoka hapa nikaanza kuzunguka kwenye mabaa. Nimepata kazi kwenye Pub ya Macha. Ameniambia naweza kuanza kazi hata kesho. Lakini ananafasi ya jioni.” “Hapana.” Sabrina akatoa macho kwa mshituko, akahisi hajamsikia Jack vizuri. “Napafahamu pale Pub, Sabrina. Na ndiko wanawake wanapokwenda kujiuza. Na yule mzee anapenda wasichana kama wewe ili kuvutia wateja.” “Mimi sio msichana Jack, nakaribia...” “Hapana Sabrina. Hapana. Naomba utulie tutafute kazi sehemu nyingine.” “Jack! Mimi ni mtu mzima, siwezi kufika pale nikajiuza!” “Hapana Sabrina. Huu mji ni mdogo sana. Hivi karibuni utajulikana unaishi hapa na mimi ninayefahamiana na watu wengi. Watu watanishangaa kwa nini ukafanye kazi za usiku za kuuza bia, wakati ninaweza kukuunganishia kwengine?” “Muda haupo rafiki kwangu Jack! Nahitaji kufanya kazi.” Sabrina akaongea taratibu. “Una haraka gani Brina?” Jack akauliza kwa ukali kidogo.

          “Kweli unataka nikujibu hilo Jack!?” “Wewe niambie una haraka gani! Ndio umefika tu hapa jana, leo unaona unachelewa!” “Mimi sianzi maisha Jack. Naendeleza. Ninavyozidi kuchelewa, ndivyo nitashindwa kuajiriwa. Hakuna mtu anaajiri mama mjamzito. Watajua sio mtu wa kudumu. Nitakosa kazi na mwishoe nitashindwa hata kujikimu mimi na huyu mtoto.” “Baa! Hapana Sabrina. Naomba katika hilo ulielewe tu. Tutatafuta sehemu nyingine.” Sabrina akajirudisha nyuma kwenye kochi, akanyamaza.

          “Umenielewa lakini?” “Labda unisaidie kuniambia ni wapi na wapi nisihangaike tena kuomba kazi.” “Kwa nini usitulie ukajifikiria wewe na mtoto?” Sabrina akakunja uso. “Mimi sio mgonjwa Jack! Ni mzima kabisa. Kwa nini nisiingize pesa kwa kipindi hiki? Nitakuwa sawa, tafadhali usiwe na wasiwasi juu yangu.” Jack akanyamaza. “Niangalie Jack.” Jack akamwangalia. “Najua unanifahamu. Mimi sijui maisha yakukaa tu. Maisha yangu yote nikufanya kazi.” “Itakuaje uzidishe kazi, chochote kitokee kwa mtoto?” Ilimgusa sana Sabrina, mpaka akabaki ameduaa. “Mimba changa huwa zinatoka Sabrina!” “Kama kuna tatizo. Lakini mimi sina tatizo lolote, na nitakuwa muangalifu Jack. Asante kwa kujali.” Wakanyamaza kwa muda kila mmoja akiwaza lake. Akamuona amesimama. Akaelekea chumbani kwake.

          Baada ya muda akatoka akiwa ametoa nguo zile za kanisani, amevaa nguo za kawaida tu. “Unataka kuangalia nini kwenye tv?” Sabrina akafikiria. “Kwani wewe unalala saa ngapi?” “Najitahidi angalau saa 4 niwe nimeshalala ili saa 12 asubuhi niwe nimeamka vizuri.” “Na Emma?” “Atakuwa ameshakwenda kulala. Shule yake ipo mbali kidogo, kwa hiyo huwa anawahi kulala na kuamka.” “Njoo ukae hapa.” Jack akaenda kukaa pembeni yake.

          “Huwa unapenda kula nini na hupendi nini?” Jack akabaki akimwangalia. Sabrina akacheka. “Kesho nitakuwepo hapa siku nzima, nataka niwapikie, mkija mkute chakula.” “Aaah! Emma namuona anakula kila kitu, nafikiri kama mimi tu. Hakuna mchaguzi hapa ndani. Chochote. Lakini sio ujichoshe kwa makazi ya humu ndani. Naomba tulia Sabrina.” “Jack ni muoga jamani! Hebu niangalie jinsi nilivyo. Sina ugonjwa wowote ule!” “Ndio sitaki uanze kuugua ukiwa na mimi. Wewe mwenyewe umesema siku hizi mbili tatu tumbo limeanza kukua kwa haraka. Inamaana mtoto naye anakua. Umehangaika huyo mtoto asitoke, sasa utulie mpaka mwisho.” Sabrina akacheka.

          “Usicheke. Mimi namaanisha.” “Nakuona Jack. Naona mwenzangu upo makini kuliko hata mimi! Lakini naomba nikutoe wasiwasi. Hakuna kitu nitafanya chakumdhuru mtoto. Nitaongeza umakini, lakini lazima kutafuta kazi Jack. Ninajukumu la mtoto ambalo siwezi kulikwepa. Kunakutakiwa chakula, malazi, hospitali, kabla na baada yakujifungua. Yote hiyo ni pesa. Ukizungumzia kliniki, ni pesa pia. Kula vizuri pia ni pesa. Jioni hii nimetoka kununua matunda hapo sokoni, ni garama kweli! Lazima nifanye kazi ili hata kuendelea kumtunza mtoto.” “Naelewa. Naomba nipe muda. Usinikatie tamaa kwa sababu nimeshindwa hii mara moja tu.” Sabrina akamsogelea na kumshika mkono.

          “Tafadhali usione umeshindwa Jack. Nafikiri Pam yupo sahihi. Ndugu na marafiki wanaweza kukurudisha nyuma. Pengine ingekuwa ngumu kwake kuniwekea mimi msisitizo kwa kuwa anajua unanihusu. Ndio maana na mimi nimejaribu kutafuta kwengine. Wote tujaribu tu mpaka tufanikiwe. Sawa?” “Kama unachukulia hivyo utanifanya nisitafute kwa kupaniki.” “Tafadhali usipaniki. Mimi mwenyewe najua kupata kazi ni shida. Nimezunguka sana pale Moshi bila mafanikio. Kwa mara ya kwanza leo ndio nimepata hapa kwenye huu mji wako.” “Achana na Macha. Tutapata kwingine.” “Sawa.” Sabrina akamuachia mkono. Wakatulia hapo kwenye kochi wakiangalia tv mpaka Sabrina alipoaga anakwenda kuoga alale.

“Mbona huli wewe?” “Nilikula mishikaki na kachumbari kwenye moja ya hizo baa nilipokwenda kutafuta kazi. Hapa nimeshiba. Nitakula tu matunda kabla yakulala. Wewe nenda kapumzike.” Jack akazima tv na kwenda kulala. Sabrina akaanzia jikoni. Akakuta vyombo vichafu. Akasafisha, akala matunda yake hapohapo jikoni., ndipo akaenda kuoga na kulala akiwa amevaa koti la Jack. 

Jumatatu.

S

abrina hakupendelea kitafunio alichokula asubuhi ya jumapili. Alikiona dhaifu sana. Hata kwao tu kwenyewe walikuwa wakifuga kuku wa kienyeji kwa hiyo swala la mayai ya kukaanga au kuchemsha asubuhi halikuwa jambo la kushangaza. Sasa siku iliyopita alipopita sokoni alinunua baadhi ya vitu, akarudi navyo pale. Aliamka asubuhi, akatengeneza chai na kuchemsha tambi za sukari, akakaanga mayai kwa Jack na Emma. Lakini akawa amemchelewa Emma, aliondoka akiwa ndio anamka. Kwenye saa moja kamili Jack akatoka chumbani akiwa ameshavaa. “Ndio unaondoka?” Sabrina akamuwahi. “Nilikwambia leo nakwenda kazini, mama.” “Nimetengeneza kifungua kinywa.” Jack akacheka. “Wenzio asubuhi humu ndani hakupikwi. Kila mtu anawahi kazini.” “Sasa mimi nimepika Jack. Huwezi kuondoka hapa bila kula.” Jack akakaa.

          “Chakula gani hicho chakulazimishiwa Sabrina!?” “Hata kama hutapenda lazima ule. Mimi nimedamka vyote hivyo!” “Kwani mimi nimekataa kula? Sema hapakuwa na mpikaji asubuhi. Emma naye mapishi yake sijayaelewa vizuri. Huwa namuwekea mazingira yakutopika.” Sabrina akacheka sana. “Kwani anapikaje?” “Natamani nikwambie umuombe apike, lakini tutalala njaa. Tena anajuhudi kweli akiwa hapo jikoni. Unaweza sema utalamba sufuria, lakini akikuwekea kwenye sahani, hata kupitisha vijiko vitatu huko mdomoni ni shida. Nyama inakuwa kama iliungwa, halafu ikaoshwa na maji mengi ikarudishwa tena kwenye mchuzi.” Sabrina akazidi kucheka.

          “Halafu hivyo vyombo atakavyotumia huko jikoni, utashindwa kwa kupita. Jiko linakuwa chafu utafikiri amepika chakula chakuuza mgahawani!” Sabrina akazidi kucheka. “Kwa hiyo nani anapika?” “Mwenyewe. Yeye huwa namuomba anifulie na kupiga pasi. Chakula ndio huwa napika au nanunua. Tukipata mfadhili kama hivyo Pam, anakuja kutuchemshia hapa na yeye, anatuachia tunaendelea kula.” Sabrina akazidi kucheka. Akakumbuka mchuzi na wali aliopika Pam. “Kwa maneno hayo, lazima nije kuonja mapishi yako.” “Wala usiwe na wasiwasi. Sio mtaalamu sana, lakini nahisi kuna niliowapita.” Sabrina akazidi kucheka.

          “Haya, kula uende kazini.” Jack akaanza kula. “Kwa mwendo huu, kunawili lazima.” Sabrina akazidi kucheka. “Una nguo za kufua na kupiga pasi nikusaidie?” “Wewe pumzika Sabrina, Emma atafua.” “Nataka kufua nguo zangu nilizokuwa nazo safarini na ile niliyozunguka nayo jana, naweza kukufulia na zako.” “Nitashukuru. Sasa ukiingia tu hapo chumbani kwangu, nyuma ya mlango nimeweka kwenye tenga la nguo chafu, aliliweka hapo mama Msindai. Hilo ndio linakuwa la nguo chafu. Usiangalie chumba wala kitanda.” “Kuchafu sana?” “Huwa nafanya usafi siku za jumamosi, mama Msindai akiniongelesha kwenye simu mpaka nimalize. Sasa jumamosi hii ndio kama ulivyoiona. Ila nitasafisha nikirudi.” Sabrina akamuacha kumuongelesha ili ale huku akimfikiria Jack na mama yake. Huyo mama ukimsikia na huyo mwanae utafikiri mama asiye na majukumu. Amejaa kwenye maisha ya Jack tokea Jack yupo chuoni habari za ujio wa huyo mama aliyekuwa waziri wa afya akija kumtembelea mwanae huyo alikuwa akizisikia mara kwa mara. Sasahivi yupo naye na huko Singida japo yeye anaishi Dar.

          Akawa anakula huku anaangalia simu yake. Akapitia hiyo simu, akamuona amerudisha mfukoni, akarudisha mawazo kwenye chakula. Akala mpaka akamaliza. “Nashukuru kujali Brina. Angalau leo nakwenda kazini nimeshiba na nimekula kitu kizuri.” “Karibu, na uwe na siku njema. Kwa hiyo ni mpaka jioni?” “Saa kumi na nusu nakuwa nimesharudi. Labda nimpitie Pam pale kwenye biashara.” “Sawa.” Wakazungumza kidogo, Jack akaondoka.

          Sabrina akasafisha hapo jikoni, na kuingia chumbani kwa Jack. Hapakuwa pachafu sana ila kwa jinsi alivyopaona mle ndani na vitu vyake, akajua ni kazi ya mama Msindai tena. Kulikuwa na vitu vizurivizuri, vingine vidogovidogo ungeweza kupuuza. Ila jinsi vilivyopangiliwa humo ndani vikaleta maana na kuvutia, ndipo akajua muwekaji na mpangiliaji lazima awe na jicho la kike. “Nani kama si mama Msindai anayeweza kuweka vitu vya namna hii, tena kwa mpangilio huu?” Akajiuliza Sabrina huku akimsaidia kusafisha na kutandika kitanda. Aina yenyewe ya mashuka yenyewe ni kotoni ile ya maana kama aliyomuona nayo Jack chuoni. Akapangilia viatu na nguo vizuri na kwa usafi, akapiga na deki kabisa, akachukua nguo chafu. Vile amezibeba tu, harufu ya zile nguo chafu za Jack ikamvutia. Akaingia nazo chumbani kwake. Nguo hizo chafu za Jack, Sabrina akaanza kuzinusa mpaka anafunga macho kwa furaha yake. Akaona avae moja wapo kabisa, akajiweka kitandani huku akiendelea kunusa zile nguo mpaka akapitiwa na usingizi hapohapo kitandani. Akaja kushituka kutoka usingizini ni saa nne asubuhi. Akakimbilia nje kufua. Alikuta kuna matanki makubwa ya maji, yamejengewa vizuri, na maji safi. Akafua nguo zake na za Jack, akaanika. 

Sabrina aanza kuwa Kero kwa Pam.

W

akati anaingia ndani, Pam naye akawa anaingia getini. “Karibu.” Sabrina akamkaribisha kwa furaha zote, asiwe na habari kuwa bado amevaa shati la Jack. Akashangaa Pam anamwangalia kwa kutomuelewa. “Karibu ndani.” “Naona umeshakuwa mwenyeji!” “Nitafanyaje wakati wenye nyumba wangu wameniacha peke yangu! Inabidi kuchangamka tu. Nilikuwa nafua huku napika ndani. Tuingie ndani.” Sabrina akaweka msisitizo, yeye akaingia. “Nisije unguza.” Moja kwa moja akaelekea jikoni.

          Sabrina akaongeza maji kwenye nyama, akatoka. Akamkuta Pam ni kama amezubaa pale sebuleni. “Vipi! Kwema? Mbona hata haukai?” “Nilikuwa napita tu.” Akajibu Pam kama aliyekuwa na jambo akagairi. “Nashukuru kupita kuja kuniona. Ila kuna tambi za asubuhi. Nikuwekee kidogo upate chai?” Sabrina akauliza, hana habari. “Kidogo tu, usiondoke bila kula.” “Mimi sina njaa.” Pam akajibu tu hivyo na kuondoka. Sabrina akakunja uso kama ambaye na yeye hamuelewi mpenzi wa Jack. Alipokosa jibu, akafunga mlango nakuendelea na shuguli zake.

Pam Kwa Jack.

B

ila kujua, kumbe Pam alimpiga picha wakati wamesimama sebuleni, akamtumia Jack na ujumbe. ‘Mbona sielewi!!’ Jack akaangalia ile picha na ujumbe, hakufanya haraka kujibu. Akabaki akifikiria. Mara simu ya Pam ikaingia, Jack akapokea. “Mbona hujanijibu sasa!?” Pam akauliza kwa hasira. “Juu ya ile picha? Au juu yakubadili mawazo kumpa kazi Sabrina?” Jack akauliza taratibu tu. “Yote. Maana nimekutumia ujumbe kuwa nafikiri kuna kazi Sabrina anaweza kufanya pale kwenye biashara. Hukujibu. Nikaamua kwenda mimi mwenyewe kuzungumza naye, ndio nimemkuta amejaa kwenye nyumba kama mama mwenye nyumba na amevaa gauni zuri tu, na juu akavaa shati lako lile ulilovaa jana kanisani! Ndio nikakuuliza, sielewi.” “Sikujua kama ni swali.” Pam akashangaa jinsi Jack alivyo jibu.

          “Wewe Jack! Inamaana unaona sawa kwa Sabrina kuvaa nguo zako!? Maana nimeshindwa hata kumuuliza. Anaonekana kama yeye hana cha ajabu alichofanya! Ni kama ni jambo la kawaida tu kwake! Labda mimi ndio sielewi!” “Kwa kufikiria kwa haraka mimi nahisi wakati anafua ile asubuhi, alipatwa baridi, akavaa hilo shati, akasahau kutoa. Vipi lakini wewe?” Jack akaona abadili mazungumzo. “Mmmh! Nahisi kama sielewi tena!” “Juu ya nini tena? Bado tupo kwenye shati au juu ya siku yako?” “Mimi naona kama wewe unaona ni sawa tu!” “Ndio maana nauliza juu ya nini? Tunazungumza juu ya mambo zaidi ya mawili kwa wakati mmoja. Ndio maana na mimi sijui unataka kunisikia nikisema nini!” “Basi bwana. Pengine mimi ndio nakuza. Lakini sidhani kama ni kitu cha kawaida.” Jack akanyamaza. Akaona amekatiwa simu.

          Jack akampigia tena. “Naona simu ilikatika bila kumaliza mazungumzo. Mzima lakini?” “Kama ungetaka kujua juu ya hali yangu si ungenipigia?” “Si ndio tunazungumza hapa, Pam! Vipi asubuhi hii ya leo, kwema?” “Nikuulize wewe! Maana nakwambia juu ya wasiwasi wangu kwa Sabrina, ni kama huonekani kushangaa.” “Ndio nauliza juu ya kazi au shati! Ni nini Pam?” “Mimi sijapenda kumuona anavaa nguo zako. Jumapili alitoka na koti lako. Leo shati! Wote nyinyi mnaonekana kwenu ni jambo la kawaida, lakini si kwangu Jack. Si sawa kwa yeyote yule.” “Mimi naona unakuwa na wasiwasi bure. Sasa uliamua nini juu ya kazi?” “Nilishindwa hata kuzungumza naye kwa mshituko.” Pam akaongea kwa kulalamika.

          “Niliondoka bila hata kukaa!” “Yote hiyo ni sababu ya shati tu ndio amekosa kazi au kuna jingine?” “Nimeona hili tuliweke sawa kwanza kabla hatujaendelea.” “Sawa.” Jack akajibu kirahisi tu bila kuonyesha kujali. “Lakini wewe ni mzima? Uliamka salama?” “Niliamka salama, naona siku ndio inataka kuwa mbaya.” “Usiruhusu iwe mbaya. Maadamu umeamka mzima, hilo ndilo la msingi na ni zawadi tosha kutoka kwa Mungu.” Pam akashangaa sana. Akaamua kumuaga tu. Jack akamtakia siku njema, akakata.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

          Huku kwa Sabrina akaendelea na shuguli zake asiwe na habari. Wakati anataka kukaa ili kuanza kupika rasmi, ndipo akagundua amevaa shati la Jack. Bila wazo la pili, akaenda kulifua, akalianika na kuendelea na kupika. Nyumba haikuwa chafu. Aliisafisha tu kidogo, ndipo akapika chakula huku akiumua maandazi ya kifungua kinywa. Aliyatia hiliki, nyumba nzima ilikuwa ikinukia. Maana hata maji ya wali aliyachemshia na hiliki, lakini wali aliukaanga na kitunguu maji tu ndipo akaweka hayo maji ya hiliki.

Maandazi yalipoumuka, akaanza kuyachoma huku akisafisha pale jikoni. Akayafanya yote hayo. Inakuja kufika saa nane mchana mtoto wa pwani akawa amemaliza kufanya vitu vyake huko jikoni, nakuacha nyumba ikinukia tu. Chakula cha usiku na maandazi kwa ajili ya kifungua kinywa vikawa tayari. Akarudi kwenye nguo alizofua. Za kwake hakuwa akipiga pasi. Akazikunja tu na kuziweka kwenye masanduku yake. Nguo chache za Jack akakunja na alizoona zinahitaji kupigwa pasi, basi akazinyoosha vizuri akitumia pasi. Akaenda kuzilaza vizuri kitandani ili mwenyewe aje aweke kabatini kwake. Inafika saa kumi jioni, Sabrina yupo hoi. Akaamua alale kidogo.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

          Saa 10:30 jioni Jack anaingia ndani, anakutana na harufu nzuri ya chakula. Akapitiliza jikoni moja kwa moja. Akakuta chakula na maandazi. Akacheka na kuchukua andazi moja. Akaelekea chumbani kwake, alipoingia akastaajabu. Chumba kisafi, na pamepangwa vizuri mpaka kitanda kimetandikwa mashuka masafi. Akatulia kidogo akizungusha macho. Hata yeye aliposema huwa anafanya usafi hapo ndani siku za jumamosi, si kwa kiwango hicho! Akaona nguo zile chafu zimefuliwa zote na kupigwa pasi, na kuwekwa kitandani nyingine zikiwa zimekunjwa. Akajua kwa aina ile ya usafi, lazima Sabrina atakuwa amelala.

          Akaenda chumbani kwake. Akagonga mara mbili tatu, kimya. “Brina! Brina!” Akaita taratibu. Kimya. Akapatwa na wasiwasi. Akaona aingie. Sabrina alikuwa amelala hapo kitandani, sio amevaa lile koti lake, ila amelikumbatia lipo usoni kama aliyekuwa akilinusa mpaka kupitiwa na huo usingizi. Jack akacheka taratibu. “Hakika Jack upo matatizoni!” Akajiambia huku akimtizama Sabrina asiamini kama Sabrina yupo nyumbani kwake yeye! Akabaki ametulia akimtizama. Moyo wake ukajawa furaha, asiamini hatimaye amefanikiwa kufika kwake. Alishamsubiri huyo Sabrina kwa miaka mingi sana. Akafurahia kutendwa na Tino, ikawa bahati yake yeye.

          Akamuona jinsi alivyokumbatia lile koti lake. Akakumbuka jinsi walivyolala pamoja Moshi. Akacheka. “Anajua kulala vizuri huyu!” Akabaki amesimama akila andazi lake huku akimtizama. Akaamua akae palepale kitandani. Hakikuwa hata kitanda kikubwa. Sabrina akashituka. “Baba mwenye nyumba, umerudi?” “Nimerudi mama. Umeshindaje?”  Sabrina akakaa. “Pole na kazi.” “Asante. Vipi wewe?” “Nimekuwa na siku nzuri tu, nimelala kujipumzisha.” “Sasa kwa mwendo huu, naona nikuajiri tu humuhumu ndani. Naona hii ofisi itakufaa.” Sabrina akaanza kucheka. Akaanza sasa kulivaa lile koti la Jack.

          “Unataka kuniajiri?” Akauliza huku akiliweka sawa hilo koti mwilini mwake. Akamuona analinusa tena hilo koti kidogo, akamuona jinsi alivyotulia usoni kama amefurahia harufu aliyokutana nayo, kisha akaendelea kuliweka sawa mwilini mwake. Akagundua ni jambo analolifanya bila kufikiria, hana hata habari na anachokifanya. “Sasa kama ndio alifanya hivihivi mbele ya Pam, basi ndio maana Pam alichangayikiwa!” Akajiambia Jack, na kucheka. Sabrina akamwangalia. “Wewe unafurahia maandazi ya chai asubuhi bwana, Jack! Kula wali. Mbona unataka kuniharibia bajeti?” “Nimeonja tu mama! Nikienda kuongeza moja, basi ndio la mwisho. Nakua nimekula sasa mawili.” “Sidhani kama yatafika kesho!” “Yatafika wala usitie shaka. Nikiongeza la nne la kwenda kulalia, basi.” “Umefika saa ngapi la nne, wakati tupo la pili!?”  Wakaanza kucheka. Stori zikaanza.

          Sabrina akimuulizia kazi anazofanya kazini kwake. Anaonaje hiyo kazi. Akataka kujua kwa nini alichagua Singida. “Kwanza nilipangiwa. Wenzangu tuliokuwa tumepangiwa nao na Wizara ya fedha, wengi wakaamua kuacha kabisa kazi baada yakushindwa kupata uhamisho. Maana sheria ilikuwa lazima uje angalau uripoti eneo la kazi, ufanye kazi kidogo ndipo uombe uhamisho. Wakaona hawataweza, wakaacha. Unamkumbuka Ibra?” “Yule aliyekuwa waziri wako wa fedha chuoni?” “Kumbe bado unamkumbuka!” “Mlivyokuwa mkifuatana kama kumbikumbi vile! Kila mtu alikuwa akiwajua ni marafiki.” Jack akacheka.

          “Alikuwa hapa kama majuma matatu yaliyopita. Akichoka tu na kelele za jiji, anakuja huku kupumzika.” “Kumbe! Sikujua!” “Tulipangiwa naye kazi. Ila yeye alipangiwa Mpiji. Bwana alikasirika!” Wakaanza kucheka. “Kwa hiyo hakwenda?” “Wewe si unamjua Ibra anavyojipenda? Mtoto wa mama yule. Hakutaka hata kwenda kuripoti.” “Anafanya nini sasa hivi?” “Biashara tu, Ibra utamuweza? Lakini inaonekana sio mbaya. Halii njaa.” “Hivi alikuja kumuoa yule msichana wake wa chuoni?” “Stela?” “Ewaa, Stela.” “Walikorofishana mwishoni kabisa. Hawakurudiana tena. Yupo amechumbia msichana mwingine, lakini naona anamlalamikia kila wakati. Sasa sijui ataoa!” Sabrina akanyamaza.

          “Nashukuru kwa kunisafishia chumba na kunifulia. Maana nimeingia pale, nikahisi nimepotea chumba! Mwenzio huwa sina hata muda wakupanga vile mpaka siku mama Msindai aje kunitembelea, ndio anapapanga vile. Mimi ni bora kusafi, basi.” Sabrina akacheka akiwa amepata jibu lake. Kazi ya mama Msindai. “Asante.” “Karibu.” Mara wakasikia mlango wa sebuleni unafunguliwa. Wakajua ni Emma. “Ametoka shule huyo!” “Si atakuwa anachoka sana?” “Ndio maisha, atafanyaje?” Mara wakasikia mlango wa hapo chumbani unagongwa. Sabrina akamtizama Jack, akamuona amekunja uso. Akageukia mlangoni.

          “Nani, Emma!?”  Akauliza Jack kwa mshangao. Mara mlango ukafunguliwa bila jibu. Alikuwa Pam. Jack akaonekana kushangaa. “Karibu Pam. Tunakumbushia enzi.” Sabrina akaongea na cheko, lakini Pam akaonekana kama anamshangao. “Vipi, kwema?” Jack akauliza akiwa amekaa palepale kitandani ambako Sabrina alikuwa amejivuta mpaka ukutani amekunja miguu na kuvaa lile koti la Jack. Wote wakabaki wakimwangalia yeye baada yakubaki kimya.

          “Pam, upo mzima?” Jack akarudia tena. “Nimeshangaa hujaja kule kwenye biashara?” Akaongea kwa kulalamika, Jack akakunja uso. “Kwani tulikuwa na miahadi kule?” Akauliza Jack kiustaraabu tu. “Kwani siku zote unaponipitia unakuwa na miahadi? Mbona sikuelewi wewe Jack!?” “Pam, mgeni siku ya kwanza. Nimerudi nyumbani moja kwa moja ili kuangalia huyo mgeni tuliyemuacha siku nzima anaendeleje.” “Mgeni huyo naona mpaka na nguo mnavaliana!” Jack akashituka moyoni, akajua Pam anataka kutibua hali ya hewa.

          “Maana sasa hivi joto, lakini amevaa koti lako!” Sabrina akajiangalia. “Mimi nahisi sio maswala ya baridi. Kuna kijiharufu nakipata kwenye hili koti, inanifanya nitake kulivaa kila wakati! Linanifanya kama natulia fulani hivi! Imetulia.” Wote wakashangazwa vile alivyojibu. Sabrina aliongea bila hata hofu. “Ndio maana basi nikakukuta umevaa shati la Jack!” Sabrina akaanza kucheka. “Nimekuja kujishitukia nipo jikoni, nataka kuanza kupika. Nikasema hapa ndio kuja kukutwa nimevaa nguo ya baba mwenye nyumba. Nilifua zote, nikasahau shati nililokuwa nimevaa.” Akatulia kidogo kama anayejaribu kufikiria.

          “Mimi nahisi ni lotion anayopaka Jack ndio inayonifanya nipende kunusa nguo zake, si bure! Imetulia kweli! Lakini usiwe na wasiwasi baba mwenye nyumba wangu. Shati nililifua vizuri, na nikalipiga pasi kabisa, nimekurudishia. Na hili koti harufu ikiisha tu, nalifua, nakurudishia koti lako. Usikonde.” Jack akatamani kucheka kwa sauti, lakini akajua Pam atakasirika.

          “Najua wote mmekuwa na siku ndefu sababu ya kazi, njooni mezani mle.” Sabrina akatoa lile koti na kulipanga vizuri hapo kitandani. “Pam kipenzi, njoo uonje maandazi niliyopika. Mazuri sana. Nakutengenezea na kikombe cha chai kabisa. Au unasemaje?” Mpaka Pam akaishiwa nguvu. Akamtizama Jack, Sabrina akacheka. “Haya nawapisha wapenzi nyinyi, lakini mje kula.” Sabrina akatoka na kuwaacha hapo chumbani.

            “Wewe Jack!” Pam akanong’ona kwa mshangao, Jack akaanza kucheka. “Si umemsikia mwenyewe?” “Naona na hasira zote zimeisha!” Wakaanza kucheka taratibu. “Ndio nini sasa!?” Akauliza Pam. “Au ndio hiyo mimba yake?” “Mimi sijawahi kuishi naye kama hivi, ila tumekuwa karibu kwa miaka mingi. Naomba tumpe muda tuone. Unaweza na wewe kujipatia rafiki mzuri!” Pam akawa kama ameshaanza kulainika. Akatulia. “Nilishaanza kuingiwa na wasiwasi. Nikajiambia anataka kunipindua!” Jack akasimama na kumkumbatia Pam, akataka kupata busu. Kufika mdomoni akapata harufu ya pombe. Akarudi nyuma.

          “Umeshaanza kunywa mapema hii Pam!? Jumatatu hii!?” “Nimepata mbili tu na wewe Jack, acha wasiwasi. Tena nilimtuma mtu akaniletea palepale kazini. Sijakwenda baa.” Jack akamwangalia akaamua kunyamaza. “Wewe vipi Jack!? Ni bia mbili tu nimekunywa, pia unakasirika? Mimi ndio starehe yangu.” Jack akaamua anyamaze na kutoka hapo chumbani. “Kwa hiyo ndio umesusa hata kunibusu hutaki sababu ya bia mbili tu tena nilizonunua kwa pesa yangu mwenyewe!?” Sabrina akawasikia kwa kuwa walitoka nje ya chumba. “Ningekuwa nimehongwa je?” Hakumsikia Jack kujibu, akawasikia wanaelekea chumbani kwa Jack.

          Baada ya muda akasikia wanatoka, Pam anacheka kilevi kidogo. “Wewe hukuwa na nia. Umenitafutia tu sababu ya kunikasirikia, uninyime. Lakini si hizi bia mbili! Eti Jack?” Akawasikia wanakuja upande ule, Jack kimya. Bahati nzuri Emma naye akawa anaingia. “Pananukia vizuri humu ndani! Huyo atakuwa mgeni tu.” “Nilikwambia mgeni anaitwa Sabrina.” Akamsikia Jack akimjibu. Emma akacheka. “Shikamooni.” Wakaitikia. “Habari za shule?” “Shule ni shule tu kaka yangu. Vipi Shem langu la nguvu? Naona ushakolea mapemaa, kabla giza halijaingia.” “Bia mbili tu na wewe Emma! Acha umbea.” “Hata mimi nakubaliana na wewe, Shem. Mbili tu!” Wakaanza kucheka Emma na Pam.

           “Acha mimi nielekee jikoni. Njaa inauma kweli!” “Hujala mchana?” Jack akamuuliza. “Wala asubuhi kaka. Hapa nina njaa, hata kujisomea sitaweza.” Emma akaingia jikoni. “Mungu wa ajabu jamani! Mgeni njoo, wenyeji tupone. Hii nyumba haijawahi kupikwa maandazi! Kitafunwa chetu, mkate. Si umeona jumapili?” Sabrina akaanza kucheka. “Na hakuna vyombo vyakuosha! Wewe usiondoke humu ndani.” Jack akamsikia. “Vya usiku wewe ndio unaosha Emma. Usimfanye Sabrina kijakazi wako.” “Sawa kaka. Harufu ya chai unaipata lakini huko?” Sabrina akazidi kucheka.

          “Na huyo umpe yale mashariti ya ulaji wa maandazi. Hana kikomo huyo.” Jack akaongeza. “Kuna masharti ya ulaji tena!?” “Kwenye maandazi tu. Ni ya kifungua kinywa.” “Jamani huo mtihani! Mimi naomba kutoa ushauri.” “Usimsikilize huyo. Usimuone mwembamba hivyo, anakula bila mchezo. Ukiendelea kumchekea hapo, asubuhi wote tutakuwa hatuna kitafunywa.” “Mbona hunipi nafasi kaka?” “Haya sema.” “Kwa kuwa ni mapishi ya mara ya kwanza humu ndani, basi tuyasherehekee haya leo. Kesho kupikwe mengine, ya kila asubuhi.” Wote wakacheka kasoro Jack. “Si nilikwambia mimi?” “Lakini wazo sio baya kaka! Najua hata wewe unatamani.” “Mimi nimekuwa mstaarabu, nimekula moja tu.” “Acha basi na mimi nipate moja lakuonja, mengine nitapewa kwa huruma za Sabrina.” Wakaendelea kuzungumza na kucheka, mpaka Jack na Pam wakahamia hapo mezani.

          Wakala, Pam akaaga. “Asante Sabrina. Chakula kitamu kweli!” “Karibu.” “Unaondoka Shem?” “Naona leo upepo unavuma visivyo.” Akaongea akimtizama Jack, Jack wala hakumwangalia. “Eti Jack?” Jack akamtizama bila kuongea neno. Emma akaanza kucheka. “Si umeona mwenyewe?” Akamuuliza Emma. Jack kimya akaendelea kunywa chai. “Mimi naona kweli ukapumzike Shem wangu. Ukitoka hapa, gari yako isisimame sehemu. Moja kwa moja nyumbani. Zibakie zilezile bia mbili tu.” Pam akazidi kucheka. “Hata deni langu nisiende kudai baa?” “Kwani leo ulipoenda hawakukulipa?” “Wameniweka hapo, ndio ikabidi niagize hizo mbili tu.” Jack akamtizama. Maana alimdanganya kuwa hakwenda kunywea baa. Alimtuma mtu. “Ndio nataka nipitie hapo tena, nione kama watanilipa.” Emma akazidi kucheka. “Sasa mimi naona kwa leo, acha tu. Pita tena kesho.” “Eti eeh?” Akauliza tena Pam huku akisimama. Akateuka kwa sauti mpaka Jack akamtizama. “Sabrina huyo! Ametulisha kupita kiasi.” Pam akavuta kiti nyuma.

          Alikuwa dada mrefu. Mwenye mwili uliojaa. Si mwembamba hata. Mnene aliyejazia vizuri. Umbile zuri. Mweupeee! Mpaka ngozi ya kichwa ilikuwa nyeupe haswa. Ukweli kwa kumwangalia, alivutia haswa. “Nashauri uwe mwangalifu huko barabarani.” “Sijalewa Jack na wewe, acha wasiwasi! Au unirudishe nyumbani?” “Unakumbuka leo ni jumatatu, Pam?” “Jack naye kwa maadili! Hivi Sabrina anajua kama unataka kuwa mbunge wetu?” Akauliza Pam na kuendelea. “Mimi nishamwambia ni biashara haramu ya kufilisiana. Siasa ni mchezo mchafu, wenzie mpaka wanajiua! Wanawekeza mipesa yote kwenye kampeni, wakati mshindi alishajulikana tokea mwanzo. Unapoteza pesa, halafu kushinda pia hushindi!” Sabrina akajua hapo hawataelewana na Jack.

          Akakumbuka jinsi alivyomuuliza akiwa Moshi juu ya yeye na siasa. Akakumbuka jinsi alivyofurahia jibu lake. Akajua mpenzi wake ndiye anayemkatisha tamaa. “Si umefika kwenye huu mji Sabrina? Sasa utapata habari zake. Yupo kijana mmoja, wala si mtu mzima. Kijana wa makamu tu, kwa miaka yote yeye ndio mbunge hapa. Hili jimbo la chama pinzani. Hakuna jinsi chama tawala wakawatoa. Wamejaribu miaka na miaka, chama tawala wameshindwa. Sasa eti huyu Jack ndio anakuja na sera za chama tawala hapa! Nani atamsikiliza kama sio kujidhalilisha tu? Yeye baa haendi. Mwenzie akija hapa, anaanzia baa. Anatunywesha usiku kucha. Sasa huyo hutampa kura kweli?” Sabrina kimya.

          “Jamani mimi nina mtihani kesho. Mkishamaliza kula, nitakuja kuosha vyombo. Acha nikajisomee.” Emma akaaga kwa haraka pale tu alipopata upenyo. “Wewe soma tu Emma. Mimi nimetoka kulala. Nitaosha hivi vyombo nakusafisha hapa.” “Udumu Sabrina. Kesho nitakuletea zawadi.” “Na ulete kweli sio umdanganye.” “Kaka bwana! Ungenyamaza pengine Sabrina angekataa.” Wakacheka. “Kumbe ulikuwa ukinidanganya?” “Sio kudanganya, kujaribisha tu!” Wakacheka kidogo, Pam alipoona hakuna uungwaji mkono wa hoja yake, akaondoka bila hata kuaga tena. 

Nyumba Huanzwa Kwa Msingi Imara.

S

abrina akasafisha pale, akamuona Jack amebaki palepale mezani na kikombe chake cha chai. Akajua maneno ya Pam yamemuingia. Akamkumbuka Lela na Tino. Alipomaliza usafi akaenda kukaa pembeni yake Jack. Akamvuta kumgeuzia kwake, akamshika mikono yote miwili. “Niangalie nikukumbushe kitu.” Jack akakunja uso. “Tulianza chuo mwaka mmoja. Ila mimi nikakuacha chuoni. Unakumbuka shida kubwa waliyokuwa nayo wanafunzi waliokuwa wakitegemea mikopo?” “Nakumbuka.” Jack akajibu.

          “Yule waziri wa fedha tuliyemkuta chuoni alikuwa akiwasumbua kwa makusudi tu kuwapa pesa zao. Wasichana wengine walikuwa wakilalamika, hawapi pesa zao mpaka alale nao. Unakumbuka?” Jack akabaki ametulia. “Unakumbuka nani alifanya yale mapinduzi?” Jack akacheka kidogo. “Uliandika historia ya ajabu sana pale chuoni, Jack. Ukiwa mgeni kabisa ukabadili mambo. Ukaingia kwenye uongozi uliokuwa ukisifika kwa ubabe pale. Kuanzia raisi aliyekuwepo wakati ule madarakani, mpaka mawaziri wake, wewe mwaka wa kwanza, ukaleta mapinduzi ya ajabu sana, kila mtu akawa akikusifia na kuimba sifa zak...” “Kasoro wewe, Brina!” Jack akamkatisha. Sabrina akacheka.

          “Acha kunitoa kwenye pointi ya maana. Na achana na Sabrina, mimi mwenyewe simuelewi. Kwanza nimemchukia.” Jack akacheka. “Turudi kwenye kampeni za pale chuoni. Yule raisi alishakuwa na mtu wake au mtu wao, ambaye walitaka yeye ndio aje kuwa raisi. Unakumbuka?” “Nakumbuka na ule ugumu wa kampeni pale.” “Sawa sawa. Sababu ya rusha. Lakini unakumbuka jinsi ulivyofanya kampeni zako kilaini bila kuhonga, na ukashinda kwa kishindo mpaka mkuu wa chuo akaja kukupongeza mbele ya chuo, akasema hajawahi kuona raisi aliyeshinda kwa kura nyingi kwa kiasi hicho pale chuoni, wewe umeweka historia? Unakumbuka lakini?” “Nilijua hukuwa hata ukisikiliza Sabrina! Muda wote ulikuwa umeinamia simu yako!” Sabrina akashangaa sana.

          “Jack! Kwenye ukumbi ule! Ulinionaje mimi siku ile, wakati nilikuwa nimekaa karibu na mwisho kabisa, tena kule juu kabisa!?” “Ilikuwa lazima kabla sijakaribishwa kuzungumza na wanafunzi, nikutafute nijue kama upo kwenye huo mkutano, Sabrina. Sijui ni kwa nini, lakini nilikuwa nikitamani hata kukuona ukisikiliza! Lakini hata makofi ulikuwa hupigi! Kama niliyekuwa nikiongea pumba tu, wakati wengine walikuwa wakinishangilia na kunisifia kweli!” Sabrina akashangaa sana.

          “Sio kwa kukudharau Jack! Nilikuona unauungwaji mkono mkubwa sana, sikujua hata kama unajua kama nipo! Nahisi hata kukujibu vibaya siku ile pale kantini, ni kwa kuwa nilipaniki. Sikukutegemea. Na nikwambie ukweli, siku ile ilikuwa mbaya sana. Natamani ingekuwa wakati mwingine. Emma alikuwa amenikorofisha usiku uliopita. Sikulala. Na kesho yake nikashindwa kuingia vipindi vya asubuhi maana nilipitiwa na usingizi mida ya saa 12 asubuhi, kwa kulia na mawazo. Niliamka nikiwa nahasira, ndipo tukakutana pale kantini nikiwa natafuta chakula, na hasira, huku bado nina usingizi. Nahisi hasira kwa Emma, nikakumalizia wewe Jack. Najua sikuwahi kukuomba msamaha kwa aibu, lakini naomba unisamehe. Nilikuwa nikikufuatilia sana tu.” Jack akacheka kwa kuridhika.

          “Haya nimesamehe.” “Kwani bado ulikuwa umeumia!?” “Sana Sabrina! Kwanza sikutegemea. Kumbuka wakati ule ndio nilikuwa gumzo pale chuoni! Wasichana walikuwa wana..” “Kupigania.” Akamalizia Sabrina na kucheka. “Sio kupigana bwana.” “We Jack! Unakumbuka wale wasichana wa Certificate walipigana wakisema mmoja alimwambia mwenzie anakuja kukutongoza, akasikia yeye ndio akaja akakuwahi?” Jack akaanza kucheka. “Usicheke. Si ni kweli?” “Walikuwa watoto wale.” “Na wale wasichana wa masoko? Wauza sura?” Jack akazidi kucheka. “Umekumbuka eeh?” “Sasa ndio hayo yakawa yananishangaza Brina! Sikuwa na msichana pale chuoni. Eti nikaonyesha nia kwako, na wewe ukanitolea nje kwa dharau vile! Hakika sikuamini!” Sabrina akafikiria kwa kutulia kama anayejaribu kuvuta kumbukumbu, akakumbuka aibu aliomsababishia Jack na kuumia zaidi.

          “Daah! Nisamehe Jack. Najua ingekuwa mtu mwingine na niliyokufanyia, asingeweza hata kunihifadhi hivi! Nisamehe tu, na endelea kunivumilia. Lakini nakuhakikishia nimejifunza Jack. Na ninaona ndio maana Mungu amenipa na huyu mtoto ili nitulie.” “Mtoto ni baraka Sabrina, sio adhabu ili utulie. Na wewe sio kwamba hukutulia. Ni hukubahatika kupata mtu ambaye amekuthamini. Nahisi ni kwa kuwa hawajui uthamani wako.” Sabrina akamwangalia, akainama. Akataka kupotelea kwenye mawazo yake akawa kama amekumbuka kitu cha msingi zaidi ya kujihuzunisha mawazoni.

          “Nilichotaka kukukumbusha Jack, ni hiki alichokuwa akikizungumza mpenzi wako leo, Pam. Hakina tofauti na kile ulichopitia chuoni. Mazingira ni yaleyale, tabia za viongozi wa hapa au wananchi wa hapa ni vilevile kama chuoni.” “Lakini wakati mwingine najikatisha tamaa Sabrina! Najiambia kule ilikuwa chuo, sio huku uraiani!” “Hata kidogo Jack. Unajuaje kama Mungu alikuwa akikuandaa kwa ajili ya nyadhifa za juu zaidi?” Akajiweka sawa. “Ulikuwa mwaminifu kwa kidogo Jack. Kwa nini usimdai Mungu kwa hilo ili akuaminishe kwa kikubwa?” Jack akamtizama kwa macho yaliyoanza kupata tumaini.

            “Wakati nipo hapo jikoni nasafisha, nikakumbuka jinsi ulivyoanza chuoni, kidogo tu. Kwa ujasiri kuhakikisha watu wa mikopo wanapata pesa yao kwa haraka na kihalali bila hongo. Ulihangaika wewe mwenyewe, unakwaenda mpaka bodi ya mikopo Dar. Ukajua tarahe na muda ambao pesa zinatolewa. Ukamuomba mkuu wa chuo dhamana yakuongozana na waziri wa fedha na kumsaidia majukumu hayo ili kuhakikisha wanachuo wanapata pesa yao kwa wakati.” “Unajua niliomba kikao na mkuu wa chuo pamoja na Dean of students?” “Nilisikia. Nikasikia mpaka akaitwa waziri wa fedha kwenye kikao. Akataka kupinga, akaitwa na raisi pamoja na makamu wake, ukajenga hoja mpaka ukapitisha hoja zako zote, mkuu wa chuo akaamuru kuwa kuanzia siku hiyo utaratibu wako uliopendekeza utafuatwa. Unakumbuka furaha na shukurani za wanachuo waliokuwa wakifuatilia mikopo?” Jack akacheka.

          “Sasa nani anaweza kufanya hayo kama siye mtu aliyeumbwa kutawala? Wewe umeletwa hapa duniani kutawala Jack. Nikipaji chako. Na kwa kuwa Mungu amekupa huo uwezo, akaweka ndani yako, hutapata amani mpaka utimize hilo.” Sabrina akainua ujasiri ndani ya Jack. “Tafadhali usije kujisahau wewe ni nani, Jack. Uwezo wako mkubwa wakufanya mambo na shule uliyopitishwa na Mungu pale chuoni. Usisahau sababu ya kukatishwa tamaa na maneno ya watu wasiokujua na kuelewa uwezo wako. Fanya mambo kisha waje waone, sio ukubaliane na vitisho vyao.” Akamuona Jack anavuta pumzi kwa nguvu kama aliyesafisha kifua.

          “Nashukuru Sabrina. Kumbe ndio maana moyo wangu ulikuwa ukitamani sana uje huku!” Sabrina akacheka. “Nina wazo Jack.”  “Niambie, nakusikiliza.” “Kwa sasa hapa kwenye hili jimbo si yupo mbunge wa chama pinzani?” “Tena amekaa hapa muda! Na wala si kijana kama anavyosema Pam, ni mtu mzima tu, sema anapenda kujiweka kama kijana.” “Sawa. Hilo wala si tatizo. Naomba wewe anza kama ulivyofanya chuoni.” “Nifanye nini sasa? Maana mimi mwenyekiti tu wa vijana wa chama chetu hapa Singida. Nitafanya nini Brina?” “Njoo hapa sebuleni kwenye makochi. Mgongo umeanza kuuma kwenye hicho kiti.” “Pole.” Wakahamia sebuleni.

          “Ehe!” Jack akataka aendelee. “Lazima kubadili hiyo ya mwenyekiti wa vijana tu. Wote tunajua wewe ni zaidi ya hiyo ‘tu’. Unaweza ukafanya mambo mengi sana kwenye huu mji, kupanua hiyo ‘tu’. Kwa kuwa kwanza uwezo unao, wewe kama Jackson Msindai. Mzawa wa hapahapa Singida huko vijiji sijui vya wapi sijui!” Jack akacheka. “Isanzu.” “Sasa! Hapa kwenu Jack. Upo viwanja vya nyumbani. Unayo sababu yakutaka vitu vizuri vitokee nyumbani. Kwa hiyo sababu ipo, nia unayo. Sasa nini chakukushinda?” Akamuona amefunguka uso.

          “Nipe wazo nianzie wapi?”  Jack akaomba ushauri lakini akiwa amehamasika. “Cha kwanza, si mnalo jengo la chama hapa?” “Kubwa tu, sema halipo vizuri.” “Hilo hilo Jack. Omba utawala kuwa ukilitumia. Wewe kama kiongozi wa vijana hapa, lazima ulete mabadiliko. Omba wafadhili waje wafundishe ujuzi tofautitofauti. Wewe ni Msindai, jina lako kubwa sana hapa nchini. Umetoka kwenye familia inayojielewa na ni wa tawala. Wapo watu wengi tu wangependa kuja kutoa mafunzo mafupi mafupi kwa vijana wa hapa. Iwe kwa kupenda sifa au msaada kweli. Makanisa na taasisi za watu binafsi. Sijui vitengo vya madawa ya kulevya. Waombe waje wawe wanatoa mafunzo kwa vijana. Badala yakunywesha watu pombe, tufanye kampeni ya kukusanya pesa. Tufungue mradi mkubwa pale, vijana wa chama waache kulalamika njaa, tuwaajiri palepale. Wanajiingizia pesa, na mfuko wa chama unaingiza pesa.” “Yes!” Jack akashangilia sana.

          “Sabrina nimekukubali.” Sabrina akaanza kucheka. “Kuna watu wanakodisha mashamba. Kodisha wewe kwa jina la chama. Waambie vijana walime huko. Haya, tumia kujulikana kwako vizuri. Itisha au tufanye harambee, watanzania hawahawa, wanazo pesa Jack. Tufungue miradi ya visima. Huku kunasifika kwa shida ya maji. Kingine, tuandae tamasha kwenye hoteli nzuri tu. Anza kazi yakuandikia barua viongozi wa nchi. Muombe hata raisi aje kuhudhuria hilo tamasha la vijana. Wafanye maonyesho, kisha tuombe hiyo hela. Uone kama hutaleta mabadiliko hapa Singida, kisha nchini.” Jack akapiga magoti mbele ya Sabrina, akamlalia magotini.

          Sabrina akampapasa kichwani taratibu. Jack akatulia kwa muda akisikilizia mikono ya Sabrina kichwani mwake, kisha akamwangalia. “Nakushukuru sana Sabrina. Asante kwa mawazo mazuri na mazito. Tunaanza kuyafanyia kazi haraka hata kabla ya uchaguzi kukaribia. Wewe utakuwa msaidizi wangu.” “Sina hata kadi ya chama mwenzio!” Wakacheka. “Nakupa usiku huuhuu.” Jack akasimama kwa haraka kuelekea chumbani. Akatoka na kadi moja ya chama. Sabrina akacheka. “Kweli wewe mwenyekiti! Unatunza kadi za chama mpaka nyumbani!” “Jaza, weka saini kabisa.” Sabrina akawa anajaza, Jack akarudi tena chumbani kwake, akatoka na laptop.

          “Umechoka sana au tunaweza kuandika kidogo?” Sabrina akamshangaa Jack. “Mpaka umenifurahisha Jack. Unafanyia kazi usiku huu!” “Na kesho nikitoka kazini, nakuja kukuchukua nikupeleke ukapaone pale kwenye kituo cha chama. Hakuna hata anayepajali wanasema jengo limekaa kushoto, tena mbali na mjini! Vijana huwa wanakaa tu nje. Huwa nakwenda kukaa nao na kuzungumza tu. Hamna chamaana.” “Tena kumbe unayo mahusiano nao?” “Kuna siku za weekend huwa tunacheza soka.” Sabrina akafurahia sana. “Nilisema mimi, umezaliwa kutawala Jack! Unao uwezo mkubwa sana.” “Nashukuru kunitia moyo na kuniamini Sabrina. Nilikuwa nakuwa nao tu, lakini sijui jinsi ya kuwasaidia.” Akawasha kompyuta.

          “Nafikiri tuanze kufikiria biashara ya kuweza kuwafanya wajihusishe.” “Pesa?” Akauliza Jack. “Naomba tusianze na tatizo la pesa, tuanze na wazo kwanza. Biashara gani ya haraka kwa kipindi hiki? Na isiwe ya mafuta. Hutaki kumuumiza Pam. Ulimkuta kwenye biashara yake, muache hapo.” “Sawa. Hapo naona hiyo itakuwa hekima. Labda kwanza kabisa tukifanye imara kile tulichonacho. Kwa mfano timu yetu ya mpira tuliyo nayo tuisajili kabisa, tuipe jina halafu nitafutie mfadhili. Vijana wanacheza hao Sabrina, ni hivyo wapo vichochoroni.” “Sawa sawa. Anza basi kuandika hilo. Hiyo itakuwa njia nzuri sana ya kuwaweka pamoja na kuvuta wengine.” Wakaandika juu ya timu. Jack akawa na majina ya baadhi ya matajiri wa hapo mkoani Singida, wafanyabiashara wakubwa ambao alijua wangependa kujulikana wanagusa jamii huku wakijitangaza.

          “Na wanawake lazima kuanzisha kitu Jack.” “Kama nini? Mimi nimekuwa karibu na vijana wa kiume zaidi.” “Mara nyingi sisi kupika kunatukutanisha kwa haraka. Sasa tukikutana hata mara mbili au tatu, itatusaidia kutuweka pamoja.” “Basi nikutambulishe kwa dada mmoja naye ni kiongozi mwenzetu.” Jack akatoa wazo. “Yaani hilo litakuwa la msingi zaidi. Ndipo nitaweza kujua kwa haraka.” “Basi nitamwambia kesho mchana aje hapa mzungumze.” “Wazo zuri.” Wawili hao wakaandika usiku huo na kujiwekea mikakati yao mpaka wakaridhika. Wakazima taa za hapo sebuleni na jikoni, wakaongozana upande wa vyumbani.

“Nimekwambia nakushukuru sanaaaaa?” Sabrina akacheka na kusimama karibu kabisa na mlango wa chumbani kwake. “Karibu. Na nina uhakika utafanikiwa Jack, kwa kuwa wewe hujajichagua, ni Mungu ndiye amekuchagua. Wakati wote amekuwa akisimama na wewe kuhakikisha kusudi lake linatimia kupitia wewe.” Jack akamwangalia Sabrina kama anayemshangaa. “Kumbe ndio maana moyo wangu ulikuwa ukikutamani sana Sabrina! Umebeba majibu yangu mengi!” “Na mimi nimefurahi tupo wote Jack.”  

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Sabrina Ametua jijini Singida na ameanzisha jambo ndani ya Moyo wa Jack, anataka kugusa jamii. Mungu alimpa Karama ya kufufua hata vyenye muelekeo wa kufa. Safari hii ni Jack, baada ya Tino, Emma na nyumbani kwao ambao wote walishindwa kutambua juhudi zake na kumdharau vibaya sana.

Sasa safari hii yupo kwa Jack Msindai wa Pam. Itakuaje? Huku nako vitakwendaje?

Usikose Muendelezo Kumuona Sabrina na Kwa Jack naye. Vile anavyoanziaga padogo sana, lakini hugeuza mambo na kuwa kama Mkuyu.

Safari hii Kosa Kwa Tino, Faida Kwa Jack.

Na

Kosa kwa Pam, Uwanja wa Sabrina Kufanya yake ambayo Mungu huweka mkono wake.

Itakaje?



CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment