Kwa Sabrina & Jack.
|
Huku kwa Jack nako ikawa hivyohivyo.
Akafikiria sababu alizoambiwa na Sabrina zakumtoa pale. Akajiuliza analinda
nini na anapoteza nini! Akahesabu hili na lile. Mipango waliyopanga na Sabrina.
“Brina ananielewa mimi kuliko mtu mwingine yeyote.” Gafla hata mama yake
mzazi akaona hamuelewi kama Sabrina. “Sabrina yupo Singida kwa ajili yangu
mimi!” Jack akaona atakuwa mjinga kama asipochukua hatua. Akatoka kitandani
na kuvaa kwa haraka, akatoka hapo kumfuata Sabrina hotelini.
Alifika na kukuta hao watu bado wakipigana.
Na walifahamiana. Jack akazungumza nao. “Mtaumizana bure muishie jela. Hata
hiyo pesa mnayodaina haitawasaidia. Ona mnavyotokwa damu!” Sabrina akasikia
sauti ya Jack akatoka kwa haraka. Jack
akamuona. “Rudi ndani Sabrina. Nakuja.” Sabrina akarudi ndani kwa haraka.
Aliona kweli sio salama. Wawili hao waliokuwa wakipigana ni kweli walikuwa
wakivuja damu. Polisi wakafika hapo. “Nafikiri tupo sawa jamani. Au mnasemaje?”
Jack akawauliza wale waliokuwa wakipigana. Kwa hofu yakuwekwa ndani, wakaamua
wakubaliane kuyamaliza kwa amani. Polisi wakaondoka, na hao vijana wakaondoka.
Pakatulia.
Sabrina akasikia hodi mlangoni kwake.
Akajua ni Jack. Akafungua kwa haraka. “Nimekuja kukuchukua, turudi nyumbani.”
“Sikujua kama hapa kuna baa, au wanakunywa usiku mpaka sasa hivi!” Jack bila
kujibu akaanza kurudisha vitu kwenye gari, Sabrina amesimama akimwangalia
asiamini anachokifanya. Akabeba mizigo yote, akakusanya na vichache vilivyokuwa
juu ya meza, akaingiza kwenye moja ya begi la Sabrina, akapeleka kwenye gari.
“Ulishalipia usiku wa leo?” “Bado.” “Twende.” Wakatoka hapo chumbani, akalipia
mapokezi. Muhudumu akamshukuru Jack kwa kutuliza ule ugomvi pale. Jack
akazungumza naye kidogo, wakarudi kwenye gari.
“Nilijua utakuwa umeshalala!” Sabrina
akaanza walipopanda tu garini. Jack akamwangalia na kuondoa gari pale. “Mwenzio
sikupata hata usingizi kwa hofu yakubaki pale peke yangu. Nilijua ingekuwa tu
rahisi, lakini inatisha Jack!” “Kwa nini hukunipigia sasa kama ulivyoahidi?”
“Nilijua utakuwa umelala! Ndio maana sikuamini niliposikia sauti yako pale!
Nikatoka kwa haraka kuhakikisha kama kweli ni wewe. Eti nimefurahi umekuja
kunichukua!” Jack akatabasamu tu, akaendelea kuendesha.
Hapakuwa mbali na nyumbani, baada ya
kama dakika 10 hivi, usiku ule na hapakuwa na magari babarani, wakafika
nyumbani kwa Jack. Ile hekaheka ya kuingiza mizigo ndani, Emma akatoka. Akaanza
kusaidiana na Jack. “Bora umerudi, maana nimemalizia kile chakula usiku huu,
nikajiambia maisha yakulala na njaa yanaanza upya.” Sabrina akaanza kucheka.
“Wewe unanipendea chakula tu?” Sabrina akamuuliza. “Nilikwambia usimfanye
Sabrina kijakazi wako.” “Lakini wote tunanufaika kaka. Au unafurahia kutoka
kazini na kuja kuanza kutokosa samaki?” Wakaanza kucheka. “Kumbe Jack anatokosa
samaki?” “Sina muda wa kukaanga mimi. Nikishabandika jikoni, nakatia nyanya na
kitunguu, mchuzi tayari tunakula na wali. Muulize kama sio vitamu. Mwenyewe
anajilambaga.” Emma akacheka kama anayeogopa kusema kitu. “Mbona husemi?”
“Unamuuliza kwa kumtisha bwana!” “Ila huwa tunakula.” Emma akaongeza huku
akicheka. Ukaendelea utani kidogo, wakamaliza kuingiza vitu ndani, Emma akarudi
chumbani kwake, Jack akamfuata Sabrina chumbani kwake.
“Nimefurahi umekuja kunichukua, Jack.” Akarudia tena Sabrina. Jack akacheka na kwenda kukaa kitandani. Sabrina naye akakaa. “Itakuaje Jack?” “Maisha na mipango yetu viendelee kama kawaida. Naomba tusiyumbe tena.” “Sawa.” “Nitazungumza na Pam, afike hapa mimi nikiwepo. Kama sipo, nyinyi si marafiki, asije ili utulie.” Hapo Sabrina akanyamaza. Wakakaa hapo kidogo, Sabrina akamsugua kidogo mgongoni kama kumfanya atoke mawazoni amtizame. Na kweli akamwangalia. “Nenda kalale, kesho kazini?” “Ni kweli.” Jack akanyanyuka na kuondoka.
Jumatano.
Aliamka asubuhi, akamuandalia kifungua
kinywa kizuri, akamuwekea kwenye contena lenye mfuniko baada yakuangalia saa,
nakuona ni saa 1:30 na bado hajatoka chumbani akaenda kumgongea. “Ingia.” Jack
akamkaribisha. Akamkuta anavaa. “Nimepitiwa na usingizi. Alam iliita,
nikazima.” “Nikusaidie nini ili uwahi kazini?” Sabrina akaanza kutandika
kitanda wakati Jack akimalizia kuvaa shati. “Nimeshamaliza. Asante. Ulilala
kweli? Maana nasikia harufu ya mayai!” “Nitarudi kulala. Niliamka kukuandalia
kifungua kinywa.” “Asante kujali Briana. Nakushukuru. Halafu nipe namba yako
hiyo mpya ya simu.” “Siikumbuki Jack. Nitakupigia.” “Hapana Brina. Unasema
lakini hupigi. Sitaondoka hapa mpaka unipigie. Naomba nenda ukalete simu.”
Sabrina akacheka na kutoka.
Akampigia Jack akiwa chumbani kwake.
Jack akapokea. “Mimi naitwa Sabrina.” Jack
akacheka. “Haya, asante.” Akakata. Sabrina
akarudi chumbani kwa Jack akiwa anamalizia kujiandaa, kisha wakatoka pamoja.
“Ndio unapendeza hivyo kila ukienda kazini!” “Mimi muhasibu wa huu mji, Sabrina.
Nahudumia watu wengi wa hadhi tofauti tofauti,
lazima niwakilishe wizara ya fedha vizuri. Kuwahakikishia pesa ya serikali ipo
salama.” Sabrina akaanza kucheka. “Ndio mpaka nakunukia vizuri!” “Harufu hiyo
unaipata wewe tu, mama.” Hapo Sabrina alikuwa amevaa tisheti ya Jack. Alitoka
nayo usiku uliopita hotelini akiwa ndiyo aliyokuwa ameivaa wakati analala. Hata
Emma alimuona ila akanyamaza.
“Sasa hiyo tisheti ya tokea jana mama,
itanuka. Badili. Zipo hapo ndani nyingi tu.” “Hii bado inaharufu nzuri tu.
Ikiisha wala hutapata shida kunikumbusha, nitaitoa mimi mwenyewe.” Jack
akambusu shavuni. “Acha niondoke sasahivi kabla sijachelewa kazini.” Akatoka, Sabrina
akajishika shavu huku akimfuata nyuma. “Usisahau chakula Jack.” “Siwezi,
ninanjaa! Jana sikula.” “Pole.” “Uache kunichanganya Brina! Naomba tulia hapa.”
Jack akachukua chakula, nakutoka. Sabrina akabaki akifikiria alichosema.
Lakini alifurahia sana kufuatwa na
Jack. Kwamba Jack bado anamuhitaji! Alishampa njia zote za kufanikiwa. “Kama
ingekuwa mtu mwingine si angeendelea tu na mchakato akaniacha pembeni kama kina
Tino!” Sabrina akaendelea kumtafakari Jack huku akisafisha pale na kupaweka
sawa. Akagundua Jack aliacha pesa pale alipochukua chakula. Akacheka. “Haya
ndiyo aliyokuwa akiyasema Pam!” Asijue Pam aliongea akiwa ameiona pesa na
kuichukua yeye.
Akarudi kulala mpaka kwenye saa tano.
Akakuta Jack alimpigia na kumuachia ujumbe. ‘Pesa ya
matumizi ya hapo ndani umeiona? Niliicha jikoni, na wewe usiiache hapo.’ ‘Asante
na samahani nilikuwa nimelala sikuona ulivyonipigia.’ Akarudisha majibu,
Jack akapiga. “Afadhali kama ulirudi kulala. Unampango
wa kutoka?” “Nitakwenda tu sokoni na kurudi. Vipi?” “Nataka nikukutanishe na
yule dada. Anaitwa Imani. Ni dada mtumzima, anajiheshimu na hana mambo ya
kitoto. Utampenda tu.” “Si ulisema utamwambia aje hapa nyumbani?” Akauliza
Sabrina. “Kama utaona sawa.” “Kwenye saa nane nitakuwa
nimesharudi. Nataka nijiandae sasahivi, nitoke.” “Nakutumia namba yake, na yeye
nampa yako. Lakini nitamwambia saa nane awepo hapo.” “Sawa Jack. Uwe na wakati
mzuri.” “Na wewe pia. Ila usizunguke sana!” Sabrina akacheka na kuaga.
Sabrina Na
Kwa Jack.
M |
ida ya saa
nane wakati anapika, akasikia hodi. Akajua ni Imani. Akamkaribisha jikoni, wakaanza
kuzungumza. “Mbona kunanukia hivyo? Unapika pilau?” Sabrina akacheka. “Mboga za
majani hizo, nakaangia na kitunguu swaumu tu.” “Mambo ya pwani?” Wakacheka.
Mazungumzo yakaanza. Na kweli alionekana ni dada anayeelewa mambo na huo mji.
Akamweleza Sabrina mambo mengi sana, na watu na sifa zao hapo mjini. Akaeleza
mengi akimtahadharisha awe makini na nani na yupi. Sabrina akawa makini
akimsikiliza huku akipika. Akamuonya mengi na kumwambia mazuri ya huo mji na
ubaya wake pia.
Sabrina akauliza maswali mengi, mpaka
inafika saa kumi kamili Jack anarudi nyumbani, Sabrina alishajua nini chakuanza
kufanya kwenye huo mji. Jack akawafuata jikoni. “Hapa umeniletea jembe, Jack
mdogo wangu. Naona nishindwe mimi mwenyewe!” Imani akamsifia Sabrina.
Wakacheka. “Umeona eeh!” “Aah kabisa. Kwanza sio mapepe. Mdogo lakini
anaonekana akili yake yakiutuuzima. Huyu hata ukiniacha naye siku nzima,
hutanisikia nikilalamika.” “Nashukuru dada Imani kama umeona mtaendana. Hata
yeye anataka mabadiliko na maendeleo.” Wakaendelea watatu hao wakizungumza,
Sabrina akipika. Alionekana ana vingi vyakupika, lakini kwa haraka haraka, wakamuona
akiepua na kuweka tu vyakula juu ya meza.
“Dada Imani kula kidogo ndio uondoke.”
“Hapana. Soda uliyonipa inatosha. Acha na mimi nikapike kwangu.” “Basi beba
hata chapati tatu na wewe ukanywee chai asubuhi.” “Wala kesho hazifiki hizo
mdogo wangu.” Wakacheka. Sabrina akamfungashia zile chapati, mara hodi mlangoni.
Jack akatoka kwenda kuangalia mgeni, wakati Sabrina na Imani wakimalizia
mazungumzo.
“Unataka nini Pam? Mbona kama
nimekueleza vizuri sana mchana?” Wakamsikia Jack akiongea. “Sijaja kukuudhi
Jack. Nimekuja kumuomba Sabrina msamaha. Na ulisema nije hapa wewe ukiwepo.
Nimesubiri muda wa kutoka kwako kazini, ndio nikaja hapa, nikijua wewe upo. Au
nimekosea?” Kimya. “Niambie Jack. Kama nimekosea, nitaondoka. Sitaki kukuudhi
wewe wala Sabrina. Sabrina mtu mzuri sana. Sitaki tukosane.” Sabrina akakunja
uso. “Uzuri wangu ameujulia wapi na lini!?” Akajiuliza Sabrina
akishangaa. “Sasa Sabrina mdogo wangu, acha na mimi nikaivishe kwangu. Maadamu
umesema unapenda mlenda, kesho nitakupikia, ukija kwangu nakupa uje ulie
ugali.” Sabrina akacheka. “Sawa dada yangu. Nisalimie watoto na shemeji.”
“Zimefika.” Imani akaondoka na chapati zake. Akamsikia akisalimia tu na kumuaga
Jack, akaondoka bila mazungumzo mengi kwa Pam.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Sabrina
akaendelea kupika. Alikuwa akisukuma na kuchoma chapati. “Pole na upishi
Sabrina?” “Asante.” Akaitikia Sabrina bila hata kumtizama Pam. Akaendelea na
mapishi. “Najua niliongea maneno ambayo nilivuka mpaka. Nikasema hata mambo
yetu ya ndani ya kimapenzi, lakini...” “Hebu subiri kwanza Pam! Uliongea nini
tena?” Jack akauliza kwa ukali. Sabrina kimya hata hakuwatizama. Akaendelea tu
kupika. “Nahisi ni hasira sijui au pombe! Lakini nimejiambia napunguza pombe.
Natulia kama ulivyonishauri.” “Pam! Acha kunizungusha na maneno mengi.
Ulimwambia nini Sabrina juu yetu?” Pam kimya.
Emma akaingia. “Bwana Sabrina akiwepo
humu ndani, kunakuwa na neema ya ajabu! Naumwa Sabrina!” Sabrina akaanza
kucheka. “Njaa?” “Kama upo huko tumboni. Nikaribishe tu huko jikoni.” “Hubadili
nguo za shule?” Sabrina akamuuliza. “Sina nguvu. Kaka shikamoo.” “Wewe kila siku
unanjaa, kwa nini huli mchana?” “Pesa ya chakula nimenunulia simu kaka yangu.
Nasubiri mwisho wa mwezi, niombe tena pesa nyumbani.” “Simu yako ya zamani
umehonga?” Jack akamuuliza, Emma akaanza kucheka. Wakajua kweli. “Sasa huo si
ujinga wewe Emma?” “Wala hukukosea kaka. Lakini nishafanya, acha tu nije kula
nyumbani. Asubuhi niliondoka na maandazi hapa, nikala njiani.” Wakamsikia Emma akicheka.
“Shem leo hujashitua nini? Mbona kimya?
Ile furaha yetu haipo!” “Siku hizi sinywi tena.” Emma alicheka mpaka Pam
mwenyewe akaanza kucheka. “Sasa huamini?” Pam akamuuliza. “Acha muda ujibu hilo
Shem. Mzima lakini? Naona umepoaa!” Akauliza Emma huku akiingia jikoni. “Mimi
mzima tu. Nimekuja kutengeneza.” “Safi sana. Kutengeneza muhimu.” Emma akaosha
mikono. “Mimi nipo tayari Sabrina. Natetemeka njaa.” “Chapati hizi za asubuhi.”
“Hakuna zakuonja?” “Hapana Emma. Wewe kula chakula kipo mezani. Chapati za
asubuhi.” “Zinanukia hizo!” “Umeambiwa chapati za asubuhi Emma, kale chakula.” Jack
akaweka msisitizo. Emma akacheka na kutoka hapo jikoni.
“Acha mimi nipige picha kwanza ndio
nipakue. Viazi vya kukaangwa, mboga za majani zinanukia kama pilau, na maini!”
Sabrina akaanza kucheka jikoni. “Sabrina udumu mama. Nguvu hiyo ya upishi izidi
kukujaa. Ukipika chapati, upike za asubuhi na za kuonja usiku.” Wote wakacheka.
“Haya, njoo uchukue moja.” “Mungu amenijibu kwa haraka! Sikutegemea.”
“Ukimuendekeza huyo, atamaliza chakula chote leoleo.” “Nitakukatia na wewe
kaka, wala mimi si mchoyo.” Kweli Emma akachukua chapati, akamkatia Jack.
Wakala huku wakicheka. “Umeona mambo hayo kaka? Unalala usiku ukiomba asubuhi pakuche
salama, ili ule chapati.” Sabrina akazidi kucheka. Emma akachukua chakula
chake, akaelekea chumbani kwake. Pakazuka ukimya.
“Kwa hiyo Sabrina umenisamehe?” Kwa
kuwa Sabrina alishapewa habari za Pam na Imani, akajua ni hovyo tu. Akawa
ameshamdharau kabisa. Hakumtofautisha na Kasandra, aliyemchukulia Emma, Emma
akashindwa hata kumuoa. Akajua na yeye hana mwendo mrefu na Jack. Akawa sio tatizo
tena. “Eti Sabrina?” “Mimi nilishakwambia tokea jana. Achana na mimi. Hunijui,
sikujui. Tumekutana hapa kwa Jack. Acha kunifuatilia na kuniingilia, na mimi
sitakuingilia kwenye mipango yako. Mimba niliyonayo na umri wangu, naishije
hapa duniani na nitamuweka wapi mtoto wangu akizaliwa, havikuhusu. Usihangaike
na mimi. Na tafadhali usiniingilie kabisa. Umenielewa Pam?” “Nilitaka
kukusaidia tu.” Akajaribu kujitetea, Jack kimya.
“Nilishawahi kukuomba msaada? Nani
amekwambia nina shida mimi? Nishaishi na watu wa aina yako wengi tu. Nakuomba
achana na mimi. Sijakuomba msaada, na sihitaji msaada wako. Nikihitaji, mimi
mwenyewe nitakutafuta nikuombe. Usinipe msaada huku ukinitukana na
kunidhalilisha. Nikija kuwafanyia kazi wewe na Jack sio kwa sababu nataka
mnisaidie. Ni kwa kuwa na nyinyi mtanufaika na huduma yangu. Kama huoni kama
utanufaika na mimi katika biashara yenu, inamaana hunihitaji. Sasa kwa nini utake
kuniweka sehemu ambayo unajua hutanihitaji? Si ndio utaendelea kuninyanyasa?”
“Sitakunyanyasa. Nitafanya kazi na wewe na tutaheshimiana.” “Basi mimi sitaki
kuajiriwa na wewe.” Sabrina akaongea kwa kujiamini.
Jack akajua alikasirika sana. “Sijui
kama umenielewa Pam?” “Nimekuelewa na naomba msamaha.” “Sawa.” Sabrina
akaendelea na shuguli zake, akawaacha wapenzi hao wamesimama hapo mlangoni jikoni.
“Kwa hiyo si yameisha Sabrina?” “Yameisha. Kama unanjaa, kaa hapo mezani ule
chakula.” Pam akacheka. “Mimi nilijua tu, mimi na wewe hatuwezi kukosana
Sabrina. Nishakuelewa, sasa hivi nitakuwa makini na maneno
yangu. Mwenzio mropokaji, halafu sipendi kumuudhi mtu ila huwa wakati mwingine
napandwa na hasira, naongeaga ujinga mpaka baadaye najishangaa mwenyewe! Mimi najihisi
sipo sawa mimi!” Mpaka Sabrina ikabidi tu acheke. “Kweli tena. Wananiambiaga watu.
Lakini sasa hivi naacha kuropoka. Tena nikiwa na wewe best yangu, nitakuwa
naangalia kila neno. Ukiona nimepitiliza, nishitue tu. Nataka tubaki kuwa
marafiki.” Sabrina akaendelea kupika huku akimtafakari Pam jinsi alivyojirudi. Akahisi
kuna anayetaka kuibiwa tu, si bure. Pam huyu si yule waliyekuwa naye jana yake
akimtukana matusi mabaya vile! Akatulia tu kimya.
Alipomuona Sabrina ametulia anaendelea
na yake hapo jikoni, akachukua sahani, kweli akakaa mezani. “Vinanukia vizuri
hivyo! Ngoja na mimi nionje japo kidogo.” Jack kimya. “Basi chakula kama hiki
kikipata Safari baridiii.” Akajishitukia. “Au hata soda.” Akajirudi, Sabrina alipomsikia
akacheka huko jikoni. “Ukitaka nitaenda kukuletea bia yako ya Safari.”
“Nimeacha mwenzio. Sasa hivi sinywi pombe hata kidogo.” Akaongea akimwangalia
Jack aliyekuwa ameinamia simu yake tu, kimya.
“Mimi ningekuwa wewe Sabrina, ningekuja
kufanya kazi na mimi.” “Mbona umenikazania, wakati ulisema vizuri tu kuwa
huajiri watu wa karibu?” “Nakiona kama kichwa chako kitanisaidia maarifa?”
“Umeniona wapi wakati uliniona mara moja tu, ukaja na matusi?” “Sabrina naye
kwa kukumbushia mambo ya zamani!” “Ni jana tu wala si zamani!” “Basi, nimeomba
msamaha. Ila chakula kitamu!” “Sasa usimmalizie Jack, na mimi ujue tupo wawili.
Nakula sana.” “Sasa mbona hata huna tumbo wala mwili? Mtoto huyo unambembea
wapi?” Sabrina hakumjibu, akanyamaza tu.
“Kaa tule Jack mpenzi wangu. Tushasameheana, yamekwisha. Si ndiyo?” Jack akatoa macho kwenye simu yake, akamtizama na kurudisha macho yake kwenye simu akaendelea na alichokuwa akifanya kwenye simu. “Mwenzio Sabrina amenisamehe. Na tushakuwa marafiki. Nimeacha pombe na kuropoka, si ufungue moyo unisamehe tu?” Jack kimya. Akaondoka kabisa pale. “Naona na mimi niondoke kabla sijaharibu zaidi.” Akarudisha sahani jikoni, na yeye akaondoka.
Alhamisi.
S |
iku hiyo
Sabrina akatoka mapema kumfuata Imani. Walikuwa na miahadi. Akampeleka mpaka
kwenye jengo la chama. Akamzungusha kwenye miradi ambayo ilishakufa.
Akamtembeza hapo mjini, ndipo akarudi nyumbani akiwa na picha kamili. Jioni
aliporudi Jack, wakaanza kuzungumzia aliyoyaona na kuanza kushauriana nini
chakufanya. Wakati wamekaa wawili hao wakiweka mipango yao na kuandika, simu ya
Jack ikaita. Jack akaiangalia, alikuwa Ibra, akapokea. “Unamkumbuka
yule mwanamziki Mganda unayemsifia maneno ya nyimbo zake?” Akamtajia
jina. “Kafariki!?” “Hapana bwana! Weekend hii yupo
jijini. Anatumbuiza. Njooni na Pam, hoteli juu yangu.” Jack akatulia. “Upo kaka?” “Nafikiria.” “Unafikiria nini kwenye tukio la
mara moja kwa miaka, kaka!” “Ulitaka iwe lini?” “Ukitoka kazini kesho, mnaweza
kuja na ndege ya jioni. Mimi na May tutawapokea. Tukale, kisha tutawapeleka
hotelini. Kesho yake tena tutakuwa wote. Njoo uoshe macho mjini. Hujaona
flyover kwa muda mrefu.” Jack akacheka. Ibra akampanga mpaka Jack
akakubali.
Akakata simu akabaki kama
anayefikiria. Sabrina akaona amuache. “Ngoja nikaandae chakula cha usiku. Emma
atarudi sasa hivi na njaa zake.” “Usimuendekeze, atakuwa anakulilia kila siku.”
Sabrina akacheka na kuelekea jikoni. “Napika tu wali, nina kiporo cha mboga.”
Jack akamfuata. “Ibra ametualika jijini. Unataka tuongozane?” Sabrina akacheka.
“Wewe umealikwa uende na mpenzi wako, unataka kubeba na wapangaji pia! Nenda
ukafurahie na wenzio. Mimi utanikuta hapahapa. Kwanza jumamosi nina miahadi na
dada Imani.” Jack akabaki kimya.
Mara Pam naye akaja, akiwa
amechangamka kweli. “Ibra ameniambia.” Jack akamwangalia tu. “Si kuhusu safari
ya Dar! Au amenidanganya hujakubali?” Akajirudi kwa haraka baada yakuona
utulivu wa Jack usoni. “Nimezungumza naye.” Akashangilia Pam. “Ameniambia na kina Ney
watakuwepo. Lazima nipendeze, au unasemaje mpenzi wangu? Nikuwakilishe vizuri.
Na safari hii tukienda sinywi pombe kabisa, ili nisikutie aibu kama vile
Arusha.” Jack kimya. “Inabidi nikasukwe. Tunaondoka saa ngapi?” “Lazima niende
kazini, kwa hiyo itakuwa jioni. Nikikosa ndege ya jioni, basi jumamosi
asubuhi.” “Kesho tukalale Dar mpenzi wangu. Ibra amesema atatutafutia hoteli 5
star. Tukaoshe macho. Maswala ya tiketi niachie mimi, nimpigie simu Doto sasa
hivi, atuangalizie ndege ya kesho. Nikipata mchana wa saa 8 je?” “Isiwe chini
ya hapo Pam, tafadhali.” “Nimekuelewa. Sasa ngoja nikajiandae kwa safari.” Pam
akatoka hapo na furaha zote.
Ijumaa.
K |
wenye mida
ya saa saba mchana Jack akarudi kutoka kazini. Akamkuta Sabrina amejilaza
chumbani kwake. “Upo sawa?” Jack akauliza. “Mzima kabisa. Nimejilaza tu. Vipi,
mbona mapema leo?” “Ile safari ni leo. Pam amepata ndege ya saa 9 na nusu.” “Sawa.”
Jack akabaki akimwangalia. “Vipi?” Sabrina akamuuliza na kukaa. “Najisikia
uzito!” Jack akalalamika. “Uzito wa nini tena?” “Kwenda kwenye hiyo safari!” “Nenda
kafurahi na wenzako Jack. Unafanya kazi sana, halafu bado wewe ni kijana,
unastahili mapumziko.” “Mbona wewe ni kijana na huendi?” Jack akauliza.
“Jamani Jack! Kwanza mimi sikualikwa.”
“Mimi nimekualika.” “Hapana Jack, sipo kwenye nafasi kama yako au yenu kwa
sasa. Sina furaha moyoni yakusema nakwenda kusherehekea au kupumzika. Huku kuwa
busy hapa na kuwaona nyinyi, kunanisaidia kuondoa hofu moyoni. Nipo kwenye
wakati mgumu Jack, Mungu ndiye anayejua.” “Naweza kuelewa Brina.” “Sidhani
Jack. Mimi mwenyewe sikuwahi hata kuhisi ninachojihisi sasa hivi. Natamani haya
yote yageuke kuwa ndoto.” Sabrina akafikiria kidogo. “Umeshawahi kupatwa na ile
hali ya moyo kupasuka? Yaani unakaa hivi, unasikia PAA! Kama kumeanguka chuma
sakafuni!” Jack akamuhurumia sana.
“Ndio hali ninayoipata. Nashukuru
kumpata na dada Imani, namuona ni mtu mzima, anamipango inayonifanya nifikirie,
nisikae nikijiwazia mimi na matatizo yangu. Mimi sio mtu sahihi sasa hivi kuwa
karibu kama unataka kweli kupumzika na kustarehe. Badala yakuwafanya muwe na
furaha, nitawafanya wote muwe na mawazo. Heri wewe uende ukafurahie na wenzako.
Ukirudi hapa uwe na nguvu zakututosha wote, kuliko ubaki hapa. Unastahili
kupumzika Jack. Nenda na ninaomba ukafurahie haswa. Safisha mawazo.” Jack
akainama. “Twende nikakusaidie kujiandaa.” “Hamna kitu kikubwa chakubeba.”
“Basi nenda angalau utoe hizo nguo za kazini, uvae kama unayekwenda kwenye
kupumzika.” Jack akasimama na kutoka hapo.
Pam alikuja kumchukua akiwa amependeza
vilivyo. Sabrina mwenyewe akamsifia. Na vile anavyopenda kucheka, Pam akazidi kuvutia.
Akamchokoza kidogo Sabrina kama anayejikomba, Sabrina akimwangalia tu. Jack
alipotoka na kibegi chake, wakaondoka. Sabrina akarudi kulala mpaka jioni, akaamka
kupika ili Emma akirudi akute chakula. Kwenye saa mbili usiku Jack akampigia. “Vipi?” “Huku tuko salama kabisa. Mlifika salama?” Sabrina
akauliza. “Tulifika salama, tupo hapa hotelini
tunajiandaa tutoke kwa chakula cha usiku, nilipiga kukujulia hali.” “Asante.
Basi muwe na wakati mzuri.” Wakaagana na kukata. Sabrina alipoangalia
muda na kuona ni saa mbili na walishazungumza, akazima kabisa simu. Akaiweka pembeni.
Jumamosi.
I |
mani
alifika hapo kwenye mida ya saa nne asubuhi, akamkuta Emma na Sabrina
wakisaidiana usafi. Akamchukua Sabrina kama walivyokubaliana, wakaenda
kuzunguka kufuatilia miradi mingine. Sabrina alimpenda Imani kwa kuwa alikuwa ni
mzaliwa wa pale, anapafahamu sana mjini. Halafu akatokea kumkubali sana na yeye
Sabrina. Ikawa rahisi kupanga naye mambo. Akawa akiulizia kwa nini hiki
kilikufa, tatizo lilikuwa nini, kama kinaweza kufufuliwa, nini wafanye wasirudi
nyuma tena, na nini kinahitajika. Hapo Sabrina akawa anaandika tu. Imani naye
akawa amemfurahia umakini wake, wakajikuta wanaendana.
Akarudi nyumbani akiwa hoi kwa kuwa
Imani hakuwa na gari, walitembea mpaka miguu yake ikasalimu amri. Alikuwa
amechoka, jua lote la siku lilimuishia mwilini. Hakuwa hata na nguvu ya kupika.
Akaamua kununua chakula. Akarudi na chips yai kwake na kwa Emma. Wakala pamoja
huku wakizungumza. Emma akamkaribisha kesho yake waende naye kanisani kwao, akakubali
bila shida akaona itamsaidia kumtoa hapo nyumbani ambako angebaki peke yake na
kujiongezea hofu tu akijikumbusha matatizo yake.
Jumapili.
A |
subuhi kwenye
saa nne, wakaondoka na Emma kwenda kanisani kwao. Nako mbali lakini wakatumia
usafiri wa daladala. Ibada zakipendwa, zikavuta mpaka saa nane na nusu
mchana. Emma akamwambia Sabrina anahamu na mbuzi choma, na anajua sehemu nzuri
inayotengeneza na ndizi za kukaanga. Akampanga Sabrina kwa maneno mengi mpaka
Sabrina akakubali. Wakaongozana wakitembea, jua kali mpaka wakafika. Wakatafuta
sehemu nzuri wakakaa wao wawili. Ukaanza utani na utundu wa Emma. Sabrina anacheka
kama anayetekenywa. Story za shule anakosoma na msichana aliyemuhonga simu
zikaendelea na muda nao ukienda, hawana habari. Sabrina anacheka hana mbavu.
“Nionyeshe picha yake.” “Ni mweupe huyo, dada!” Sabrina akazidi kucheka. “Wewe
unapenda wasichana weupe?” “Mweusi sioi.” Sabrina akazidi kucheka. Akaonyeshwa
msichana mwenyewe ni wa hapohapo Singida lakini Mnyiramba. Sabrina akamsifia.
“Sasa utamleta lini nyumbani?” “Siku kaka akisafiri kama hivi, ukiniruhusu,
nitamleta.” Sabrina akazidi kucheka. “Unamuogopa Jack?” “Nimekabidhiwa kwake, basi
baba anakazi yakuulizia maendeleo yangu kwake mchana na usiku!” Wakaendelea
kucheka hapo wakila mpaka giza likawakuta mtaani.
Wakaanza kutembea taratibu hawana
haraka wanarudi nyumbani. Wameshiba, hawana wanae muwahi. Vicheko, Sabrina
akawa amefurahi kweli siku hiyo. Simu ya Emma ikaita. “Kaka huyo!” Sabrina ndio
akili inamrudia, hana simu. “Pokea umsikilize.” Emma akapokea. “Uko wapi wewe?” Aliposikia sauti ya ukali, akaona
amrushie lawama Sabrina. “Tulikwenda kanisani na
Sabrina, akasema anahamu ya nyama choma, lakini akataka iwe ya mbuzi. Ndio
ikabidi kumpeleka. Hapa ndio tunarudi.” Sabrina akakunja uso, akimtizama
Emma. “Mko wapi?” Jack akauliza. “Tunatembea kutafuta daladala, leo si unajua ni jumapili
daladala za shida?” “Kama unalijua hilo kwa nini hukumwambia mwenzio mkabeba
mkaja kula nyumbani?” “Sabrina alitaka kula palepale, alisema hana hata nguvu
yakutembea.” “Nisubirini hapohapo nakuja.” Akakata.
“Wewe Emma! Nani aliyesema anahamu ya nyama
choma ya mbuzi kama sio wewe?” “Hiyo sauti yake ilivyo ya ukali, nikaona
nikupambanishe naye tu.” Sabrina akaanza kucheka. “Wewe si umetoka kanisani
wewe?” “Huo sio uongo bwana. Nimeongeza kidogo tu kwenye ukweli. Sasa amesema
anakuja kutuchukua. Hapo karudi nyumbani, katukosa, ndio maana ameamua kuja
kutufuata. Kwanza kwa nini hajakupigia wewe?” “Simu yenyewe sijui hata ilipo!”
Wakaanza kucheka. Wakatafuta sehemu wakakaa. Zikaendelea stori, wanacheka.
Akagundua Emma anakwenda kanisani kupiga kinanda. Mtoto aliyekulia kwenye
ulokole. Na nimpigaji mzuri tu, na huko kanisani pia alikabidhiwa kwa
mchungaji. Kwa hiyo na huko nako baba yake anapiga simu kuulizia. Sabrina
akazidi kucheka.
“Asikwambie mtu! Nina mzee mkoloni,
yule anayekwambia lala chini akuchape viboko.” “Emma!” “Wewe siku muulize kaka.
Alishakuja kunitandika palepale.” Sabrina alicheka mpaka machozi. “Mbele ya
Jack!?” “Kama natania, muulize kaka. Na kanisani sio ombi, wala hiari, ni lazima.
Anapiga simu kila jumapili kuulizia kama nimekwenda, na kama niliwahi.” “Acha
masihara Emma!” “We acha. Utakuja kumuona. Mwezi haupiti, atakuja kuja
kunitembelea. Ongea yake yenyewe utafikiri nipo jeshini!” Sabrina alizidi
kucheka mpaka machozi. Emma alikuwa mtundu wa maneno, alimfanya Sabrina acheke sana.
Wakiwa katikati ya stori, wakaona gari
ya Jack. Wakasimama. “Wewe kaa naye mbele, ngoja mimi nitulie nyuma kimya.
Maana hiyo sauti yake, mimi namjua kaka, si kwema.” Wakawa wanaongea huku wakisogelea
gari ya Jack. Sabrina anaendelea kucheka, Emma kimya. Sabrina akafungua mlango
wa mbele akapanda, Emma nyuma. “Pole na safari.” Sabrina akaanza. “Asante.” Jack
akaitikia kwa kifupi tu, akanyamaza. Wakatulia kidogo.
“Mlirudi
saa ngapi?” “Ungetaka kujua hilo ungewasiliana Brina!” Akaanza Jack. “Umezima
simu tokea juzi nakutafuta kwa simu sikupati bwana! Inakuwa kama umenifanyia
makusudi!” “Tulizungumza juzi Jack, labda umesahau. Kumbuka ilikuwa usiku
ukaniambia ndio mnatoka kwenda kupata chakula cha usiku. Umesahau?” Jack
akamwangalia na kunyamaza. “Pole. Ulinitafuta sana?” Kimya. “Usikasirike bwana
Jack! Mwenzio nilikuwa nakusubiri kwa hamu, nina habari njema kibao za kukupa.
Jana tumezunguka na dada Imani. Halafu hukuniambia kama vijana walikuwa na eneo
pale sokoni!” “Walishindwa biashara, wakaamua kuwa wanakodisha hilo eneo. Kwa hiyo
pesa ya kodi ndio inachukuliwa, napo inalipwa kwa kuvutana kweli!” “Nimemwambia
dada Imani tuangalie mkataba, tuone unaisha lini. Pale tunaweza kupatumia sisi
wenyewe, na tukapata pesa zaidi ya kukodisha. Ni sehemu ya mbele kabisa ya soko!
Tunaweza kuuwa ndege wawili kwa jiwe moja. Vijana wakapata ajira, na bado
tukaingiza pesa.” “Sasa yote hayo kwa nini hukunitafuta na kuniambia?” Jack
akauliza kwa kulalamika.
“Nilitaka upumzike, ufurahie huko ili
ukirudi uwe fresh. Kichwa chepesi, hata nikikwambia jambo, linaeleweka
kwa haraka.” “Wala haijasaidia.” “Tena!?” Sabrina akashangaa. “Hakuja huyo
mwanamziki wakiganda, unayempenda?” Kimya. Sabrina akawa hajaelewa. Akanyamaza
mpaka wakafika nyumbani. Emma haraka sana akakimbilia chumbani kwake huku
akimkonyeza Sabrina. Sabrina akamshika Jack mkono akamvutia chumbani kwake. Wakakaa.
“Niambie nini kimekuudhi Jack?”
“Unanipuuza sana Brina! Hunichukulii maanani. Nakuwa kama mtu baki tu, tena
hata usiyenifahamu! Nikiwepo sawa, nisipokuwepo pia ni sawa!” Sabrina akabaki
ameduaa. “Unawezaje kukaa siku nzima hata usinifikirie hata kidogo!? Siku nzima,
Brina!? Na leo pia! Hata usiwe na wasiwasi kama siku nilipokwenda kula kama
nilirudi salama, au la!? Hukutaka hata kuniambia usiku mwema! Mimi
nisingekufanyia hivyo Brina. Sina nilichofanya huko ila kukupigia tu wewe simu.
Njia nzima nimekuwa nikikupigia wewe simu! Nimefika hapa kama kwenye saa 6 mchana,
sikukuti nyumbani wakati unajua wazi mimi narudi leo! Hujali nitafikaje
nyumbani! Kama nitafika nikiwa na njaa au la! Unanipuuza Brina. Unanipuuza
sana.” Sabrina akamkumbuka Tino, naye alichanganyikiwa hivyohivyo kwa kumkosa
masaa machache tu. Akakumbuka alivyokuja kumbadilikia. Akatulia kidogo,
akakumbuka huyo ni Jack, alikuwepo tokea Emma na Tino.
Akarudisha hapo mawazo kwa haraka. “Nikikwambia
ijumaa nililala kwa shida sababu ya hofu kwa kuwa wewe hukuwepo hapa ndani,
utaamini?” Kimya. “Jana niliweza kulala sababu ya uchovu Jack. Nilitembea juani
karibu siku nzima, nimerudi hapa na chips zangu na Emma, nilishindwa hata
kupika! Nimelala kwa kupitiwa na usingizi nikiwa hapo kwenye kona, hata
sikujifunika. Nimeamka usiku nikiwa nimeshika hiyo tisheti yako Jack. Uchovu na
kukulilia ndiko kulinifanya niweze kurudi kulala tena. Ningekupigia,
ningekuchanganya tu Jack. Nipo kwenye kipindi
kigumu haswa, zaidi ninapokuwa peke yangu.” Sabrina akaendelea kujieleza
machozi yakimtoka.
“Kwa hiyo ninapopata kitu
chakunichukua mawazo, najitahidi nisijikumbuke kwa muda. Ile ijumaa
tulipoongea, kwa kuwa ilikuwa usiku sikujua kama utanitafuta tena. Nikajifariji
kuwa angalau upo na wenzio mpo kwenye wakati mzuri. Nikaweka simu pembeni
nikalala. Sikupuuzi Jack. Niamini kuwa wewe ndio mtu pekee umebaki kwenye
maisha yangu, wewe ni shahidi wa hilo. Naanzia wapi kukupuuza Jack?”Jack
akamvuta kama amlalie. Sabrina akajilaza hapo mapajani. Na yeye akajivutia mto,
akauweka nyuma yake, akaegemeza mgongo. Wakatulia, Sabrina akijaribu kujifuta
machozi.
“Hata mimi nimejilaumu sana kuondoka. Nilifanya
haraka kukuacha. Hapakuwa na ulazima wa kwenda, hasa kipindi hichi ambacho ndio
umekuja tu, na mimi nikakuacha!” “Hapana Jack.
Unayo haki yakufurahia. Huna sababu ya kujinyima raha kwa matatizo yasiyo
kuhusu.” “Wewe unanihusu Brina. Kwa hiyo matatizo yako ni yangu. Hata nikijitahidi
vipi kukwepa, najikuta unapoumia na mimi naumia tu. Siwezi kujisaidia, siwezi
kukimbia. Upo kwenye moyo wangu, hujawahi kutoka tokea nakufahamu.” Sabrina
alilia sana. Alilia, akalia akiwa amemuinamia Jack. Akajitoa na kuhamia kwenye
mto wake, akajifunika na tisheti ya Jack, akaendelea kulia. Jack akamfuata tena
akamrudisha lakini safari hii kifuani.
Sabrina akajiweka vizuri akilia kwa
majuto mengi akifuata wanaume wengine na kukwepa upendo mkubwa hivyo! Akajutia
asijue chakufanya akiwa amebeba mimba ya Tino! “Naomba nisikilize Brina,
tutakuwa sawa?” “Hapana Jack. Niambie kama mimi
ndio nitakuwa sawa. Hakuna ‘tuta’ tena. Huu ni mzigo wangu peke yangu
Jack.” “Nimerudi mapema kwa ajili yako Brina. Haupo peke yako na
samahani nilikuacha. Sitarudia tena, kuanzia sasa tutakuwa wote.” “Sijui Jack! Ila ninachojua sitaki kukuingiza kwenye
matatizo yangu.” “Nilishakwambia matatizo yako ni yangu. Sina jinsi
nikakwepa. Nakupenda Brina, sina jinsi nikajisaidia. Siwezi kuficha na
wala siwezi kudanganya. Nashindwa kuendelea kuvumilia. Nahisi nitachanganyikiwa
kama sitakwambia ukweli.” Sabrina akahisi hajaelewa vizuri, akakaa kabisa.
Akajifuta machozi, akakaa akamwangalia.
“Siwezi kuvumilia tena Brina. Siwezi kuficha tena. Juzi usiku imebidi kuwaambia
wote niliokuwa nao. Niambie kile unachotaka niwe, mimi nitakuwa, nikuoe na mimi
nipumzishe nafsi yangu.” Sabrina hakuamini. Jack akatoa pete mfukoni. “Jana
kaka alinisaidia kwenda kununua hii pete kwa ajili yako. Nimekisia tu size
kutokana na wembamba wako, ukinikubali leo, hii pete ni yako Brina. Na ya ndoa
inakuja kwa haraka. Huyo mtoto hatakuwa wako peke yako, atakuwa wetu.”
~~~~~~~~~~~~~~~~~~
- Jackson
Msindai anataka kumaliza kabisa.
- Safari
hii Sabrina amepata!?
- Wakiwa
na mipango mingi mizuri mbeleni katikati yao, Yepi yanawasubiri kuyakabili!
- Kila
hatua kwenye maisha ina changamoto yake. Je, Safari hii Jack
atahimili mshindo ili kubaki na Sabrina, au Yatamshinda kama Tino
aliyeanza kwa viapo vizito na ahadi nyingi halafu kuja kushindwa vibaya
sana kungali mapema kabisaaa?
- Nini
kitaendelea kwa wooote?
- Mambo
ya Simulizi hili ndio kwanzaaaa yanaanza,
Usikose
muendelezo kuona mengi ya maisha wanakopitishwa viumbe wengine.
0 Comments:
Post a Comment