Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Makosa! - SEHEMU YA 6. - Naomi Simulizi

Makosa! - SEHEMU YA 6.

Ndoa Ndoano...Mapinduzi Kila Kona

T

ino alimaliza, Sabrina asijue. Alibaki ameinama akifikiria. Akawa amezama kabisa kwenye mawazo. “Mungu wangu! Nimejiingiza kwenye nini hiki?” Sabrina alibaki akiwaza huku amejiinamia, akizungusha simu yake. Akatolewa mawazoni na mkono wa Tino akimshika. “Siwezi nikaruhusu uingie matatizoni Sabrina. Nakuahidi hakuna atakayekulaumu wala kukulalamikia kwa lolote.” “Naogopa Tino!” “Hata iweje, sitakubali uingie matatizoni. Ni heri nipoteze kila kitu ila sio wewe. Naomba usifikirie kunikimbia. Nakuhitaji. Ukibadili tu mawazo, ukaondoka leo, sitakuzuia, ila ujue utanirudisha kule uliponitoa, na safari hii sitasimama tena.” Tino akaongea kwa upole akibembeleza.

“Siwezi kukuacha Tino. Ila nahisi kama da Lela amejipanga zaidi! Kwa nilivyozungumza na Sabina, hawa watu wawili wanaonekana wamekusudia kupata pesa yako kwa namna yeyote ile. Pengine alipanga kurudi na kukumaliza, sijui. Leo agutuke hana pesa

yakuendelea kuwa na huyo mwanaume wake, maana alivyoniambia Sabina ni kama huyo mwanaume anampendea pesa Lela. Na Lela nasikia anampenda sana huyo mwanaume, kwa anayomfanyia kitandani. Sabina anasema Lela ni kama amechanganyikiwa kwa huyo kijana. Amemnunulia gari na amempangishia nyumba nzuri sana, tena ya pesa nyingi. Wanaishi maisha ya hali ya juu sana. Kila weekend wanahamia hotelini. Sasa niambie hayo maisha watakubali kuyaachia hivi hiv!” “Najua hawawezi kukubali, na ndio maana na mimi najipanga.” Tino akajaribu kujiweka sawa.

“Maisha yamenipa nafasi nyingine kupitia wewe. Nahitaji muda wa kupona kabisa. Na siwezi bila wewe. Ukiondoka tu sasa hivi, ujue ndio nimekwisha. Nivumilie tu nipone kabisa, ndipo niweke kikomo na Lela. Nitakulinda kwa kila niwezavyo. Sitakuacha ukapata shida kifedha na....” “Naomba nikukatishe Tino. Najua umekuwa ukitumiwa kwa uzuri wako na fedha pia.” Tino akatulia. “Najua. Sabina ameniambia. Ameniambia kuwa hata Lela alikutoa kwa mwanamke mwingine kwa kupambana haswa. Najua. Lakini sio mimi Tino. Nina shida na pesa, lakini nataka kuanzia mwanzo naomba unielewe, sipo na wewe kwa ajili ya pesa yako. Maombi yangu ni kukuona unasimama na kuweza kujitegemea.” “Basi jua bado sijaweza kujitegemea Sabrina.” Tino akahakikisha hilo anaweka sawa na wazi kwa Sabrina.

“Bado Sabrina. Hata kama unaniona natembea na kufanya mazoezi, ujue zipo nyakati naingiwa hofu kabisa. Nashindwa hata kulala, wakati mwingine naota nikiwa nimefungiwa kwenye kile chumba gizani. Kitu pekee kinachonifanya nitulie na nirudi kulala, ni pale ninapofungua macho na kuona taa inawaka na wewe upo pale na mimi. Na ndio maana ulipotaka kurudi kulala chumbani kwako hata siku ile Lela alipokuwepo pale, nilikutaza usiondoke kurudi kulala chumbani kwako, uendelee kuwepo na mimi. Najawa hofu bila wewe. Naomba Lela asifanikiwe na kwako pia.” “Hawezi Tino.” “Unauhakika? Maana Lela anajua kutumia kila njia ili kunifanya niwe chini ya himaya yake. Mpaka kwa vitisho. Sasa nataka kujua kama unao uhakika?” Sabrina akatingisha kichwa kukubali.

“Ila tuwe makini Tino.” “Ndio maana nataka tutoke kabisa hapa. Tuende sehemu ambayo hakuna atakayetufahamu ila mimi na wewe tu. Nitaanza upya kabisa matibabu yangu, na daktari mpya. Tutaishi mimi na wewe tu mpaka niwe na uhakika nimepona kabisa ndipo nitarudi huku na kumalizana kabisa na Lela.” Sabrina akataka kujua juu ya hatima yake na yeye, akaona awe mpole. Tino alikuwa amekaa mbele yake, kijana anayevutia, anamlilia anamuhitaji. Yeye Sabrina! Sabrina akalainika kabisa. Akajiambia atajua mbele ya safari.

“Sawa. Ila naomba tusiongozane wote polisi au kwa mwanasheria wako Tino. Kwenye mambo kama hayo naomba nisionekane kimbelembele. Nitazungumza na watu wa hoteli kama wanausafiri au nitakuitia taksii.” “Sawa. Nitakukuta hapa hotelini?” “Si umesema tunaondoka kesho?” “Hapana. Naona nimalizane na haya mambo, tuondoke kesho kutwa.” “Basi naomba wakati unashugulikia hayo mambo mimi nikabadili hizi nywele. Sitachelewa kurudi. Nitafumua usiku wa leo, kesho nikienda ni kusuka tu, nakurudi.” Akamuona Tino ameinama.

“Sitakawia kurudi Tino. Nilivyo hivi sio sawa. Hata nywele zinanuka?” “Kweli utarudi Sabrina?” Sabrina akashangaa wasiwasi wake. “Kwa nini nisirudi Tino!?” “Labda umeingiwa hofu kusikia mpaka mambo ya polisi!” “Sio mimi Tino. Nipo na wewe kwa kuwa mimi nimekubali. Huwa ninashida nakufungwa na ahadi zangu mwenyewe. Ingekuwa sio hivyo, ningeshaondoka pale kwako muda mrefu sana. Kumbuka tuliachwa mimi na wewe tu pale, bila pesa huku Jack akiniita Singida. Si ningekuacha na kukimbilia Singida? Lakini nilibaki na wewe nikiwa sijui mwisho wake. Nimekuahidi nitakuwa na wewe mpaka tukubaliane, ujue nitafanya hivyo.” Tino akabaki kimya.

“Unajua ni kwa nini Emma, alinibembeleza sana anioe?” Kimya. Tino akamwangalia. “Nikwakuwa nilimvumilia Emma, nikikwambia nilipopita naye yule kiumbe, usimuone anakuwa kama mwehu akihesabu siku. Ni kwa kuwa anajua wazi, hakuna mtu anaweza kumvumilia kama mimi. Na sikuchoka mpaka yeye mwenyewe aliponiacha kinyama. Na ndipo muda huo tukiwa tumeachana, sio wakati tupo naye, kipindi aliponiacha ndipo nilipochoka, na kupigia mstari mahusiano ambayo hayakuwepo. Na ndio maana alipotaka turudiane huku akituma marafiki zake wambembelezee nilikataa Tino. Nikajisikia sina chakumpa tena Emma. Simu ya mwisho, Emma alilia Tino. Akiomba msamaha na kukiri yote aliyonitenda mabaya, nikiwa hata sijamlalamikia hata mara moja ila kunyamaza na kumuacha tu. Alikiri na kutubu kwa machozi. Akakumbuka siku alizokuwa na shida, nikasimama na yeye. Misiba niliyohudhuria kwao mpaka kifo cha mama yake kilichomuathiri sana, nikasimama naye mpaka akaweza kurudi kazini. Maana alipatwa kama depression akaacha kwenda kazini kabisa. Akawa hawezi hata kutoka ndani. Kitandani tu, mimi nikimuhudumua.”

“Nilipoona atapoteza kazi, nikaamua kumwandikia barua yakumuombea likizo ya dharula, nikaipeleka mimi mwenyewe ofisini kwao, yeye hana habari kwa kuomboleza. Kuja kurudi kazini, meneja wake mwenyewe akamwambia ile kazi bado ipo kwa sababu nilikwenda nikazungumza nao, nikajaza fomu za likizo na kuandika barua pia ndio maana anayo ile kazi. Hakuamini Emma. Sikwambii haya kwa kujivunia, ila kukuhakikishia kuwa, nikikuahidi kitu, jua nitafanya.” Sabrina akaendelea kwa upole tu.

“Jack nimezungumza naye na kumwambia nitamtafuta baada ya mwezi na siku chache kuanzia sasa. Hiyo itakuwa miezi mitatu tangia tukubaliane.” “Ulikubaliana na Lela, Sabrina. Sio mimi. Huo muda ni wako wewe na Lela.” “Tino! Ulitaka nikae kwa muda gani!?” “Ulisema mwenyewe mpaka tukubaliane.” Sabrina akabaki akimwangalia. “Naomba usifikirie kuondoka sasa hivi, naomba jipange kuwa na mimi katika kila khali.” “Mpaka lini Tino!?” “Mpaka tutakapokubaliana vinginevyo.” Sabrina akabaki kama asiyepata jibu lake kwa hakika, na Tino alijua ila na yeye ni kama alipatwa na kusita. Akashindwa kuwa muwazi zaidi ya hivyo.

“Unaenda wapi sasa?” “Naanza kufumua nywele ili kesho nisikawie saluni. Uje unikute humu ndani, usipandishe pressure nikichelewa.” Tino akacheka tu, Sabrina akahamia bafuni. Baada ya muda Tino akamgongea. “Nakwenda mazoezini. Wana gym nzuri sana huko chini.” “Unataka nikusindikize?” “Hapana. Malizia tu.” “Sasa usinogewe ukachelewa kurudi Tino. Mimi nakujua. Uje tulale mapema, kesho uamke na nguvu.”  Akamsikia akicheka huku anaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya mazoezi alirudi, akaoga akatoka kukaa sehemu yenye makochi hapohapo chumbani akiangalia tv, wakati Sabrina akioga na yeye. Alipomaliza akatoka na kumfuata Tino. “Nywele zimeshakauka?” “Ndio nilikuwa nafunga mabutu huko bafuni.” Akakaa chini kabisa kwenye miguu yake, akaipakata na kuanza kuifanyia masaji. Tino akajiegemeza kwenye kochi vizuri. Sabrina akaendelea kuiminya taratibu huku akipitisha vidole katikati ya vidole vyake vya miguu. Tino akawa ametulia kabisa. Sabrina akaendelea kwa muda, taratibu tu. “Twende ukalale kitandani Tino.” “Daah! Hivyo unavyonifanyia najisikia vizuri!” Sabrina akacheka.

“Hamia kitandani ukalale. Bado huo mwili unahitaji muda wa kutosha kupumzika.” Tino akarudi bafuni kusafisha meno, Sabrina akazima tv na taa kwenye ile sehemu pembeni ya sehemu ya kulalia, akaenda kukaa kitandani sehemu ya miguuni huku taa za hapo pembeni ya kitanda zikileta mwanga wa kiasi hapo kitandani. Tino hakutaka kurudi kulala gizani tena, ilikuwa lazima alale angalau taa ndogo ikitoa mwanga. Akatoka bafuni na yeye akapanda kitandani. “Njoo ulale hapa.”  Tino akionyeshea pembeni yake. “Sio unanitaka huku miguuni ili nikufanyie masaji!?” Akauliza kwa aibu kidogo akicheka. “Hapana. Nakutaka hapa.” Tino akapigapiga ubavuni kwake upande wa kushoto. Sabrina akaangalia huku na tabasamu la soni, usoni.

Tino alikuwa amelala chali. Kijana huyo aliyemtoa mate hata Lela! Ngozi nzuri. Ndio ametoka saluni kufanyiwa usafi wa nywele na ndevu. Akatengenezwa vizuri na ukweli alivutia kumtizama. Halafu yupo na Sabrina! Msichana wa kawaida kabisa! Hana mambo mengi makubwa kwenye mwili wake. Kwanza ni kama alinyimwa mwili. Hana rangi ya mwili ya kuielezea na kumsisimua mtu. Ni msichana wa kawaida kabisa. Mpaka awe na wewe, umfungulie mlango kwenye maisha yako, ndipo atakayokufanyia, utashindwa kusahau. Amemuacha msomi Emma, mwenye ndoa na mtoto, kubaki akihesabu siku tangia aondoke kwenye maisha yake. Sasa Tino anamwita kulala ubavuni.

Akaweka miguu ya Tino pembeni, akajivuta upande alipoitwa. Hakujua alale chali, au ubavu. Ubavu wa kulia au kushoto! Akacheka tena alipofika hapo. Alishalala na Tino, lakini wakati wote alilala miguuni. Leo amekaribishwa ubavuni! Akanyanyua mashuka, akaingia ndani, akajivuta mpaka hapo ubavuni, akajilaza kugeukia ukutani. Akamsikia Tino naye akimgeukia. Akamuweka sawa lile chuka mabegani. “Sasa hiyo khanga kichwani, utalala vizuri kweli?” “Inabidi. Kesho nitaenda kuzisuka ili nilalie kofia laini ya kulalia.” Akahisi akimchezea vinyweleo vya chini ya ile khanga, kwenye shingo karibu na kichwani. Sabrina alisikia raha ya ajabu, akatulia kabisaa.

“Nakushukuru Sabrina. Asante kwa kila kitu. Na ninaamini kila kitu kitakuwa sawa.” “Naamini hivyo Tino.” Sabrina akaitika taratibu. “Geuka nikwambie kitu.” Sabrina akageuka na tabasamu usoni. “Nini?”  Akauliza taratibu akiwa amelala wakiangaliana. Tino akapitisha kidole juu ya nyusi zake. “Ukiwa hivi pembeni yangu, najihisi naweza kila kitu.” Sabrina akacheka taratibu akifikiria. “Mbona kama huamini?” “Najua upo kwenye kipindi kigumu Tino.” “Kwa hiyo unaamini nakutumia tu, nikipona ndio basi?” “Sitegemei kitu cha tofauti kutoka kwako Tino. Nipo hapa kama mfanyakazi tu.” “Wote tunajua hiyo si kweli Sabrina!” Akapinga Tino.

“Ulinitumikia kabla ya kulipwa. Na ulilipwa mshahara aliochagua Lela, na bila kukuomba ulitumia hiyo pesa yote kunihudumia mimi. Tena kwa vitu vilivyokugarimu, ulivyojua vitaniongezea  mimi nguvu. Umenilea kwa upendo japo ulishauriwa unidharau kama wengine waliomsikiliza Lela. Walianza wengi tu hapo mwanzoni. Wakavunjwa moyo na Lela mwenyewe kwa namna moja au nyingine. Kila mfanyakazi aliyemleta kwangu, alihakikisha anamfitini na mimi kwa kuhakikisha ananihudumia mimi kama takataka. Waliobaki kwa siku mbili tatu alianza kuwanyima mshahara ili waondoke.” “Haiwezekani Tino!” Sabrina akashangaa sana.

“Kabisa. Wewe si wa kwanza. Na usifikiri ni bahati mbaya. Anafanya kwa kusudi kabisa, kuvunja mahusiano yangu na kila kiumbe anayetaka kunikaribia ili yeye ndiye abakie akinimiliki na kujinufaisha zaidi na zaidi bila kutosheka. Lakini wewe ulibaki ukiwa huna pesa wala ahadi yeyote ile, Sabrina. Kwa hiyo upo na mimi najua sio kwa sababu ya kazi.” Sabrina akashindwa kumwangalia. “Nitalienzi hilo daima Sabrina. Sitakaa nikasahau.” “Tumshukuru Mungu alinileta kwa wakati na kunipa uwezo wakufanya kitu sahihi mpaka ukawa hivyo.” “Niamini nikikwambia sisahau kumshukuru Mungu, Sabrina. Hapakuwa na jinsi ya mimi kutoka pale isipokuwa Mungu kukutumia wewe. Ukawa jasiri kuliko wanaume wote waliopita pale na kunizunguka. Uliweza kummudu Lela na kelele zake zote wakati aliweza kuwamudu mpaka jamaa, ndugu na marafiki zangu! Nikabaki vile peke yangu mpaka ulipokuja wewe. Nakushukuru Sabrina. Nataka ujue namaanisha.” “Najua Tino. Karibu.” Akataka kumbusu midomoni, kwa haraka sana Sabrina akakwepesha akainama kama ambaye hajaelewa.

Pakazuka ukimya kama Tino na yeye amepigwa na bumbuwazi. Lakini Sabrina akaweka mkono kifuani kwa Tino. Alikuwa amevaa singlendi. Nguo ndogo ya ndani ya juu, baadhi ya nywele za kifuani zikawa zipo kwa nje. Taratibu kwa makini akaanza kupitisha vidole kama kutaka kuzirudisha ndani ya ile nguo nyepesi aliyovaa Tino. Alifanya hivyo kuzunguka juu ya kifua. Alipofanikiwa kuziingiza zote, Tino akashangaa anazitoa tena kwa vidole, taratibu. Tino akacheka nafsini kwake. Akajisahau hapo kifuni kwa Tino akichezea hizo nywele za kifuani na kumthibitishia Tino ni kweli aliziacha hapo kwa ajili yake. Alifanya hivyo kwa muda, Tino akiwa ametulia kimya mwishoe akaona ametulia, mkono umebaki hapo kifunia. Akajua anasinzia. Sabrina akasikia busu juu ya kichwa chake, akapotelea usingizini hapo ubavuni kwa Tino mkono kifuani.

Akiwa katikati ya usingizi akasikia. “Sabrina!” Alikuwa Tino akimuamsha. Akaamka. “Nataka kwenda kujisaidia. Samahani, utarudi kulala.” Sabrina akajisogeza pembeni na kutoa mkono kifuani. “Nikuletee chupa? Nilikuja nayo.” “Sitaki kukusumbua. Acha niende tu chooni.” “Sio usumbufu.” Sabrina akatoka kitandani na kwenda kuleta chupa aliyokuwa akiitumia Tino akiwa mgonjwa hawezi kutoka kitandani. “Mbona kama hujalala!?” Sabrina akamuuliza maana alionekana kama ambaye hajapata hata lepe la usingizi! Lakini Tino akatoa tabasamu tu bila yakujibu. “Acha kuwaza bwana!” Sabrina asijue kinachomsibu mwanaume huyo aliyemchezea nywele za kifua. Bila kuwaza, akajisahau kama Tino sio mgonjwa kama vile alivyokuwa zamani, akamfunua shuka taratibu akiwa ameinama pale kitandani, wakati anataka kumtoa suruali ndipo akaelewa kwa nini halali. Akasita, Tino akimtizama. “Huyu si alipatwa na stoke! Nguvu za kiume anazipata wapi?” Akajiuliza Sabrina akiwa anababaika pale mbele ya Tino.

“Au ulitaka ukajisaidie chooni?” Ikabidi Sabrina aulize. “Nilifikiri hutaki nisumbuke!” Akajibu Tino taratibu tu. Sabrina akajua amefanya kusudi kukubali chupa ya kujisaidia pale kitandani ili amuone. Ikabidi akae pembeni yake. Taratibu akamtoa ile pensi aliyokuwa amevaa ya kulalia. Akatamani afunge macho baada ya kushusha nguo ya ndani Tino naye akimsaidia kunyanyuka ili ashushe zile nguo kirahisi. Tino ametulia kimya akajua anamtizama. Inabidi sasa ashike na kulengesha kwenye chupa. “Inabidi kunyoa na hizi nywele Tino. Unatisha huku.” Sabrina akamshika vizuri, akaweka kwenye chupa, baada ya sekunde chache kweli Tino akakojoa mkojo wa kutosha tu. Sabrina akatingisha kuhakikisha hakuna mkojo tena. Kama kawaida yake, akatamani usiku huo abadili na kumwacha kama wanaume wengine, lakini alishamzoesha kumkausha kabisa kama mtoto wa kike, tena yeye mwenyewe akimpa sababu ya kwa nini anafanya hivyo. “Ili lisikudondokee hata tone la mkojo Tino, ukatonesha vidonda.” Sabrina mwenyewe ndiye aliyeanzisha na kumzoesha kumfuta baada ya kujisaidia haja ndogo. Usiku huo amwambie amepona! Akaona hapana, akashika tena na kukausha taratibu, Tino akimwangalia tu bila hata kutaka kumsaidia.

Alipomaliza chupa akiwa ameeweka chini ikabidi kurudishia nguo ya ndani na ya juu. “Nimeyataka mwenyewe! Sijui nilikuwa usingizini!” Akajisuta Sabrina wakati akirudishia nguo. Akamfunika. “Nakwenda kumwaga mkojo.” “Asante.” Akashukuru Tino lakini Sabrina akajua anamcheka moyoni. Alifika bafuni usingizi umepaa. Akaanza kucheka kila akikumbuka. “Mmmh! Tino si mchezo.” Akasifia Sabrina akiwa bafuni. “Sijui ndio ananifikishia ujumbe kuwa yeye bado mwanaume!” Akaendelea kuwaza akiwa bafuni, mwishoe akaona atoke tu.

          Anarudi kulala ubavuni au chini miguuni! Akaanza kujiuliza Sabrina. Mkono kifuani, au arudi kugeukia ukutani! Akakubaliana na hilo wazo. Akamzunguka na kwenda kulala ukutani. Na yeye bila hila akamgeukia. “Nilijisikia vizuri vile tulivyokuwa tumelala kabla sijakuamsha!” Akaanza Tino huku akimchezea tena shingoni. Sabrina akasikia kucheka. Pia alihisi kitu kimemgusa sehemu za chini. Hakujibu. “Utafanya nijutie kukuamsha.” “Naona kama nakufanya hupati usingizi Tino. Nakubana sana.”  Akaongea huku akijigeuza, kumgeukia yeye. “Sidhani kama nakosa usingizi kwa kubanwa, nahisi ni hizi juisi za virutubisho unazonipa ndizo zimeondoa uchovu.” “Si ni kitu kizuri? Au nipunguze aina hii ya matunda! Nilisoma wakasema ni nzuri kwa kukurejeshea nguvu. Ndio maana nilikuwa nikikusaigia vingine kwenye chakula na kusaga unakunywa kama juisi.” “Sasa upunguze tena nirudi sina nguvu! Huoni ni afadhali kunambadiliko sio unanishika nakuwa kama mtoto mdogo wa kiume!?” Sabrina alicheka sana mpaka akajificha hapo ubavuni.

“Eti Sabrina?” Sabrina hakutoa kichwa. “Mimi nilijua utafurahia kuwa kazi yako imezaa matunda! Halafu mwenzangu unataka unirudishe kama joka la kibisa!” “Bwana Tino! Mimi simaanishi hivyo. Nilikuwa naongelea kukosa kwako usingizi.” “Huko kunasababishwa na kunyimwa busu, wala si vinginevyo.” Sabrina akazidi kucheka usiku huo. “Wewe Tino umepona bwana! Acha mimi nikauze alizeti.” Tino na yeye akaanza kucheka. “Mimi naona unakimbia matokeo yako wewe mwenyewe!” “Tulale bwana Tino!” “Basi rudi hapa kifuani.” Sabrina akajitoa pale alipojificha. “Unamaanisha nilale kabisa hapa juu?” “Vyovyote vile utakavyo wewe.” “Bwana Tino! Utanifanya nishindwe jinsi ya kulala.” “Basi mimi nafunga macho. Njoo Sabrina wangu.” Akiwa anacheka, akajirudisha. Lakini safari hii nusu ya mwili kifuani. Akamsikia akipitisha vidole kidogo tena juu ya kifua chake, na yeye akamkumbatia vizuri, wakalala.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakati Tino akifanya mazoezi asubuhi hiyo, Sabrina akajua uzunguni hapo kwenye hiyo hoteli, hatapata mtori. Alibeba chupa za chai, akapanda gari bila kuoga akaenda kutafuta baa ambayo atapata mtori, na mchemsho.  Akanunua na kurudi kwa haraka. Tino anarudi chumbani kutoka mazoezini, akakuta mtori na milk shake ametengenezewa na Sabrina. Akacheka. “Vinavutia kwa macho na matokeo yake pia siyo mabaya.” “Mimi wala sikusikilizi Tino. Naomba ule ndio ukaoge, uondoke ukiwa umeshiba.” Tino akawa anacheka. “Ninavyoringiwa Tino mimi!” Sabrina akawa anacheka tu huku na yeye akila.

Walikula Sabrina akamwambia yeye ndio atangulie akaoge. “Ile ahadi ya usiku ya kunyolewa sijui bado ipo!?” “Mimi nilikuwa usingizini wala sikuwa najua nini nafanya.” Tino akacheka sana huku akielekea bafuni akichechemea bila fimbo yake. “Bisha tu Sabrina. Ila ujue uongo nao ni dhambi kama dhambi nyingine zote.” Sabrina akazidi kucheka.

Alioga Tino akatoka msafi na amependeza. “Urudi Tino, sio ukafichwe huko.” “Wewe si hunitaki bwana! Sasa wivu wa nini?” “Tino!” “Narudi mama, niende wapi mimi watakaponipokea kama kwenye mikono ya Sabrina wangu?” “Ndio mimi nakushangaa. Urudi hapa.” “Nitakuwa nakupigia ili ujue nilipo, sasa na wewe sio kina Jack wakubadili mawazo, unikimbie.” Sabrina akacheka sana. “Nikauze alizeti?” “Ndio naona unapotaka kukimbilia huko! Rudi hapa, kama ni hizo alizeti, tukauze wote.” “Singida huko?” “Mbona nitakufuata tu, nani hataki starehe yakukojoleshwa?” Sabrina alicheka mpaka akaishiwa nguvu.

“Hakika Tino umepona wewe! Twende tukauze alizeti.” “Kwani mimi nitakataa! Nakufuata popote uendapo.” Sabrina akazidi kucheka. “Lakini hivyo sivyo nilivyoambiwa juu yako Tino! Mimi niliambiwa wewe mpole sana Tino. Huwezi hata kuzungumza!” “Kwa wanao niudhi.” “Kwa hiyo Sabina alikuwa anakuudhi?” “Najua amekwambia sana tu. Yeye hajaolewa, hashituki yupo club na mke wa mtu mpaka asubuhi hata hashituki wala kumshauri mwenzie arudi nyumbani! Na yeye Lela, Sabina akamfanya kama Mungu wake, huna unalomwambia juu ya Sabina. Kidogo tu, utasikia hata Sabina kasema! Nikaona wote wananichezea akili, nikaachana nao wote wawili na kundi lao wote.” Sabrina akafikiria kidogo.

“Hivi Sabina anapenda starehe eeh!” “Kwani wewe humjui dada yako?” “Sio sana Tino. Hata huko kwetu Sabina ni kama Mungu mtu. Anaheshimika sana kwa elimu aliyopata, kazi nzuri aliyonayo na alipofika kwenye maisha. Kujenga nyumba kama ile na kununua gari ya kifahari vile! Huna utakachosema nyumbani juu ya Sabina.” “Najua kwenye hiyo NGO anayofanya kazi ya mambo ya reseach, analipwa pesa nzuri sana. Sasa eti ndio Lela, sekretari wa kampuni ya kawaida, alikuwa anakimbizana naye, wakati mwenzake analipiwa mpaka safari za nje ya nchi! Asimuone Sabina ana kitu, hata kama mwenzie amerudi nacho kutoka kwenye safari zake za nje ya nchi, mbona na yeye Lela atanunua! Utadaiwa hiyo pesa mpaka uitoe tu.” Sabrina akanyamaza.

“Nenda kasuke upendeze Sabrina wangu.” Sabrina akacheka kinyonge, akasimama. Akajiweka sawa kidogo na kupasafisha pale, wakatoka. Akamshusha Tino kituo cha polisi, yeye akarudi Sinza kwenye saluni alizozoea. 

Kwa Sabrina.

S

abrina akafika saluni akiwa amepewa pesa yakutosha. Akaambiwa na Tino asuke atakacho, ilimradi yeye aridhike. Sasa kufika saluni, akakutana na mitindo mipya, nywele mpya zimeingia mjini. Akaanza kubabaika. Msichana aliyempokea akaanza kuuza biashara. “Kwa rangi yako hiyo, urefu wa nywele zako na kasura hako, hii nywele ndio itakufaa.” “Wewe umenena, lakini ili awake vizuri, changanya na goldi kidogo.” Mwenzake akadakia. “Msije mkanifanya kinyago na rangi yangu jamani!” Sabrina akawatahadharisha. “Sasa unataka rangi gani?” “Nyeusi.” “Hee!” Kila mtu akahamaki. “Kwa unauzee gani?” “Unaficha mvi?” Kila mmoja akaongea lake.

Sabrina katokea shamba. Akajiambia labda mambo mapya. “Usimtie shemeji vishawishini mdogo wangu. Upo naye, lakini macho yapo kwa warembo wa nje! Wewe bado mdogo. Mwili wako mzuri hujaharibika na machips ya mjini!” “Bwana mtoto kama mzungu! Hana hata nyama ya mgongo!” Sabrina akaanza kucheka asijue kumbe na mwili wake unaweza kuja kusifiwa siku moja. Akamwagiwa sifa hapo wee, mwishoe akakubaliana na staili waliyomchagulia. “Nywele ndefu bebi! Shemeji apate kwa kushika.” Wakaanza upya maneno ya kumpamba, Sabrina hana mbavu kwa kucheka. Akaambiwa kwa aina hiyo ya nywele, lazima wasusi wawe watatu ili wamalize mapema. Nywele akaambiwa zile 100% human hair. Kutajiwa bei, akapima na muda atakao kaa nazo, akaona ni sawa.

Kazi ikaanza ya kusukwa. Nywele ndogo ndogo mpaka urefu wa nywele zake, kisha zinaachwa. Na mawimbi juu. Sabrina akaomba atengenezwe kucha za miguu, na asuguliwe nyayo. Huku anasukwa, huku anaoshwa miguu iliyokuwa bandani kwa ng’ombe ikikanyaga kinyesi cha ng’ombe takribani miaka mitatu! Sabrina amerudi kwenye viwanja vya mjini, acha asuguliwe nyayo na kutolewa uchafu kwenye kucha. Akasafishwa vizuri na kwa kina, na kupakwa rangi. Kwa asili alikuwa na kucha ndefu. Kwa hiyo hakubadikwa. Hata mkononi alitaka apakwe tu rangi. “Mambo si hayo mdogo wangu!” Wakaanza kumsifia tena. “Ukirudi leo lazima shemeji akusahau.” Sabrina akazidi kucheka huku akisukwa.

Akajisahau Sabrina kwa raha ya kurudi mjini. Akapita muuza nguo. Kila mtu akachangamkia. Wengine wakataka mkopo, wateja wengine wakakimbilia ndani kujaribu. Sabrina akabaki ametulia kimya, wasusi wawili waliingia ndani kujaribu nguo. “Sasa hizi zilizobaki za ‘miss world’ wetu, hizo hapo dada.” Akamsogezea Sabrina, akacheka huku akizipokea. Anaanza maisha mapya, nguo zote aliacha kwao. Kwanza alishazichukia. Ndio zile anazomnyanyasa nazo Emma. Akajiambia hazitaki tena, ndio mwanzo wa muonekano wa Sabrina mpya anayefanya maamuzi magumu. Akachukua baadhi alizopenda, akaingia ndani na yeye kujaribisha. Zote akapenda. Akalipia, na kwenda kuziweka kwenye gari ili asisahau. Akarudi kukaa kuendelea kusukwa.

Kwa Tino.

T

ino yeye siku yake iliharibika mara tu aliposhushwa kituo cha polisi na Sabrina na kumpigia simu kabla hajaingia kituoni na kumkosa. Akampigia kama mara tatu, Sabrina hakupokea. Akajiambia labda atarudisha simu yake, asiingie ndani, akabaki amesimama hapo nje ya kituo cha polisi akijua Sabrina atampigia, lakini wapi. Lisaa likapita Tino yupo nje ya kituo cha polisi anasubiri simu ya Sabrina. Baada ya nusu saa nyingine, Max akampigia kumuuliza amefikia wapi.

“Nipo hapa kituo cha polisi Osterbay.” “Upo na nani?” Akauliza na kuzidi kumchanganya Tino. “Iweje Sabrina awe ndio amenitoroka!” Akawaza Tino. “Nitabaki peke yangu!” Gafla akapata panic attack. Hofu kubwa ya gafla ikamwingia. Kutoka kufungiwa kwa muda mrefu gizani, leo yuko peke yake mwangani! Tena na hofu ya kuuwawa na mkewe pamoja na mpenzi wake! Halafu anajikuta peke yake! Akazidi kuingiwa hofu. “Tino?” Max akaendelea kutaka kujua. “Nipo peke yangu.” Akamuhurumia. “Basi nakuja sasa hivi ili tusaidiane.” “Nashukuru kaka.” Baada ya kama dakika 25 nyingine ndipo Max akawasili. Akamkuta amesimama nje juani, jasho linamtoka, simu sikioni. Akamuona amekuwa mwekundu. Akajua anazungumza na Lela.

Akamuona anarudisha simu mfukoni. “Kwema? Nimefurahi kukuona kwa macho, sasa hivi nasadiki kama ni wewe.” “Kwema kaka.” Wala hakuonekana kama ni kwema. Wakapeana, hugi la kiume, akabaki akimshangaa. “Ushamaliza ndani?” “Bado sijaingia.” Akashangaa kidogo. “Twende tuingie.” Wakaongozana, Tino akitumia gongo upande mmoja. Amepoa kama siye waliyezungumza jana wakipanga mipango. Wakafika mapokezi, macho kwenye simu. Ikabidi askari aulize. “Niwasaidie nini?” Kimya kama aliyegairi. “Tino!” Max akamshitua. “Unajua nini, haina maana tena. Hata wakiniua kesho, hivi nilivyo ninafaida gani? Ni heri waje hata usiku huu wanimalize nipumzike.” Tino akatoka pale. Max na yule askari wa mapokezi wakabaki na mshangao wakimsindikiza kwa macho.

Ikabidi Max amfuate nje. “Ni nini kinaendelea Tino?” “Juu ya nini?” Tino akauliza kwa ukali. “Kwa nini unakuwa mnafiki na kushindwa kuniambia? Tatizo ni pesa au nini? Kama unataka nikulipe na kwa kuniambia ukweli basi nitajie garama zake.” Max akapandisha nyusi zote juu kwa mshituko. “Umeniona nachechemea hapa. Mdomo bado haujarudi kama nilivyokuwa. Mkono wangu nashindwa hata kuandika sentensi nzima. Leo nakuja kudai nyumba! Ili nani aende akaishi hapo? Mimi peke yangu! Hivi unajua mimi ni yatima na sina ndugu? Ndugu na marafiki niliowategemea ni kama nyinyi mlinitelekeza, nimebaki peke yangu. Nataka nyumba na mali ili vinisaidie nini? Si ni heri nife yaishe huyo Lela na mwanaume wake waishi hapo na watoto wao? Kama ulitegemea na leo nikulipe, sina kazi ya kukupa. Katafute wateja wengine. Acha nikafe mbele ya safari. Jiandae na malipo yako makubwa ya mwisho baada ya kifo changu wakati ukimsaidia Lela. Lakini mimi sina kazi.” Tino alimfunga mdomo yule Max, akatembea akichechemea mpaka akavuka barabara Max akimtizama.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

  

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment