Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! - SEHEMU YA 9. - Naomi Simulizi

MAKOSA! - SEHEMU YA 9.

Sabrina & Tino.

Walitoka hapo Tino akiwa mtulivu sana. Sabrina akamuacha kabisa mpaka walipofika hotelini. Wakaoga, wakati wapo kitandani akaona amuulize. “Niambie wasiwasi wako upo wapi, Tino.” “Huu mkono Sabrina. Maisha yangu yote yanategemea huu mkono. Itachukua miaka kama hii niliyonayo kunijenga kisoikolojia kuwa naweza kuishi bila huu mkono. Ndio kila kitu changu! Ndio unaonipa pesa na faraja. Kwenye kuchora pekee ndipo kulikokuwa kukinifanya hata kuweza kuishi na Lela nyumba moja na nikaweza. Hata nikiwa nimekasirika vipi, nikianza kuchora, akili zangu zinazama huko. Siko mpweke tena. Hakuna tatizo linasimama nikiwa nachora. Huu mkono ulikuwa kila kitu changu tokea mdogo naishi na baba pamoja na yule mke wake. Huwezi kunisikia nikilalamikia kitu nikiwa na huu mkono. Sijui maisha mengine bila huu mkono!” Tino akaongea kwa masikitiko.

“Mtu akiniambia nianze kufikiria maisha mengine mbali ya huu mkono!” “Hudhani kama unaweza kufanikiwa....” “Mbali na huu mkono!?”  Akamkatiza na kuuliza kwa kuhamaki. “Nataka kusema zaidi ya kuchora. Unaweza kutafuta faraja mbali na uchoraji Tino. Watu wana mafanikio, amani na furaha na hawachori!” “Kwa kuwa Mungu ndivyo alivyo waandikia hivyo. Mungu amenipa kipawa hiki kwa sababu Sabrina. Huu mkono umeniketisha na wakuu wa nchi mbali mbali. Umenitoa nchi nyingi sana hapa ulimwenguni. Kuna kipindi nilikwenda Italy kwa familia yangu upande wa mama, nilikwenda kumuona jamaa mmoja anachora, aliziona kazi zangu, alishangaa sio ile yakujisifia. Akanichukua tukaenda naye Ufaransa akitaka nikakutane na kazi za watu wengine kwenye maonyesho ya picha za wachoraji mashuhuri. Kwa kukiri yeye mwenyewe, alisema hakuna hata kazi moja inayopita ujuzi wangu.” Tino akakaa.

“Sabrina, huu mkono wangu wa kulia umebarikiwa! Si kwa kujisifia, ni kwa kile kipaji Mungu ameweka ndani yangu. Kama isingekuwa mkataba wa hii kazi kunifunga, ningekuwa nikifanya naye yule jamaa. Nilitaka mkataba wangu huu uishe, nijiongeze. Mbali yakuchora ramani za majengo, nilifikiria hata kuhamia Italy, au Ufaransa. Nisome kidogo tu kupata leseni kule, niendelee na kazi. Hapa najiona nimerudi nyuma haswa.” Sabrina akaona hana jinsi akambadili mtazamo kwa haraka ila kuungana naye, matokeo ndiyo yatambadili. “Basi tukatafute ushauri huko KCMC. Tuone watakachotuambia.” Usiku huo wakalala, bila mapenzi.

Moshi.

W

aliondoka jijini Dar asubuhi na mapema kabla hata jua halijachomoza. Wakiwa njiani alimsikia  Tino akiwasiliana na mtu. Baada ya mazungumzo ya muda, wakitaniana kidogo, akamsikia Tino akimwambia, “Huu ndio ule wakati wakulipa deni yako Swai. Nitakuwa mjini kwako kwa muda, lakini sitataka mtu alijua hilo.” “Unamkimbia nani?” Wakataniana tena kidogo, akaendelea. “Nahitaji hifadhi mjini kwako.” Akamalizia hivyo. Wakataniana kidogo, akamsikia anasikiliza. “Yaani hapa nipo njiani.” Akaongeza Tino. Mwishoe akamuona amefurahia, akamshukuru sana na kukata.

“Yesss!” Akashangilia Tino. “Umeona jinsi huu mkono unavyoniketisha na wakuu na kunipa mengi hapa duniani?” Sabrina akamgeukia kidogo na kurudisha macho barabarani kuendelea kuendesha. “Huyu Mzee alikuwa rafiki yake baba. Wakati nipo chuoni baba alimleta kwangu na kumuombea nimtengenezee ramani nzuri sana ya hoteli. Bila shida, nikamchorea ile ramani. Akaipeleka kwa mjenzi wake. Huyo mtu alikuwa na kampuni kubwa tu ya ujenzi. Alirudi kwa baba, akasema yule mjenzi alimshangaa sana kuwa amepata wapi ramani kama ile. Wakamsifia sana. Sasa akataka kunilipa pesa nyingi, nikamwambia anisaidie ada ya mwaka ule tu. Badala ya baba kunilipia, yeye ndio alipe. Akashangaa akasema mbona nikidogo hivyo, nikamwambia nyingine nitakuja kudai wakati mwingine.” Tino akaendelea akisikika kuhamasika haswa.

“Sasa tokea wakati ule, akiwa na kazi zake na matajiri wenzake, walikuwa wakinipa mimi. Ile nyumba yangu ya Kunduchi nimejenga kwa kazi zake alizokuwa akinipa na marafiki zake. Kazi za pembeni tu sio ile kampuni. Ana mahoteli huko Kilimanjaro, Dar na Mwanza. Ila apartment anazo mbili tu, Dar na Moshi. Sasa leo ndio nimemkumbushia deni ya kazi ya kwanza kabisa. Ametupa sehemu ya kuishi kwenye moja ya apartment zake hapo Moshi. Sijawahi kufika, lakini huwa anapenda vitu vizuri. Naamini patatufaa kwa muda tutakao kuwa hapo Moshi.” “Hongera Tino.” Sabrina akatamani kuuliza juu ya ushauri waliopewa na mkewe Max, wakununua nyumba mbali na ile ya Kunduchi, akaona anyamaze kwanza.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Walifika jioni kukiwa kumeshakuwa na baridi. Walisimama mara kadhaa njiani. Lakini Sabrina aliweza kuendesha bila shida. Walielekea moja kwa moja kwenye hizo apartment. Zilizojulikana kwa jina la Luxury Villa. Kwa hakika zilikuwa nzuri. Walifika hapo wakakuta sehemu ya Mapokezi wanayo magizo yao. Wakasindikizwa mpaka kwenye hiyo sehemu yao waliyopewa. Chumba kimoja, sebule na jiko. Ukitoka baraza la mbele uliweza kuona sehemu ya kuogelea, nyuma bustani nzuri. “Hakika hapa ni pazuri!” Akakubali Sabrina. Tino akatoa simu na kumpigia huyo mmiliki, Swai. Akamshukuru kwa mapokezi mazuri, wakataniana tena kidogo wakaagana.

“Nashukuru Sabrina. Asante kuwa na mimi. Nashukuru kutembea na mimi.” Shukurani hizo zikaendelea. Usiku uliopita walilala bila mapenzi, lakini usiku huo Tino alitoa shukurani zake zikisindikizwa na penzi zito kwa Sabrina. Kwa uchovu, Sabrina akalala kama nusu mfu. Aliamka asubuhi ya saa nne, Tino ndio anatoka mazoezini. “Najua hata huko hospitalini wataniongezea mazoezi  ya kitaalamu zaidi. Acha na mimi nikazane.” Katika hilo Sabrina akawa mtu wakutia moyo tu, kwa kuwa alijua hakuna jinsi angemwambia Tino vinginevyo wakaelewana.

Wakatulia hapo juma la kwanza. Wakifurahia kuwa mbali na Lela na purukushani za jiji la Dar. Mapenzi kila wakiangaliana, bila kuchoka. Mazoezi mengine Tino aliyamalizia mwilini kwa Sabrina wakicheka na kufurahia bila ya kujali kesho. Ukweli walikuwa na wakati mzuri zaidi Tino ambaye kwa mara ya kwanza maishani ni kama amepata faraja ya kweli. Sabrina alikuwa akimjali sana. Akimfariji bila kuchoka. Akimuona amepotelea mawazoni, basi Sabrina atamuongelesha kwa hili na lile, mpaka watacheka. Kufuatana ndio ilikuwa kila mahali. Sabrina akiwa jikoni akipika basi ujue Tino atakuwa naye hapo jikoni akimwangalia jinsi anavyompikia hivyo vyakula vya kumpa nguvu huku akimuongelesha mpaka amalize kupika na kulishana.

Palipo Amani, Uharibifu nao Hunyemelea.

W

akati Sabrina na Tino wakiendelea kufurahiana wakithibitishiana walikusudiwa kuwa pamoja tokea mwanzo, kufutana machozi kwa haja, naye shetani alikuwa kazini akipanga yake. Huko kwa Max akakutana na Lela halisia. Alidhani wanamfahamu Lela, kwamba vile Lela alivyo ndivyo amemaliza, lakini akaja kukutana na Lela mwingine, aliyemjia kivingine kabisa, tena akiwa amejipanga vilivyo, tena na mwanasheria aliyekuja na hoja za nguvu mpaka Max mwenyewe, mtaalamu wa kesi, akasalimu amri na kuwakimbia kwa kuwaambia waahirishe kicho kikao chao, yupo na majukumu mengine, wapange wakati mwingine wa kukutana.

          Baada ya Lela na wakili wake kuondoka ofisini kwa Max, Max alibaki akitafakari kwa kina alichokisikia kutoka kwa Lela. Kila alivyopanga hoja zake kumkabili Lela, tatizo lililokuwa limebaki ni Sabrina. Utetezi wake mkubwa Lela ni kumleta Sabrina nyumbani kwake kwa ajili maalumu ya kumlea mgonjwa, mumewe. Akajitetea kwa machozi kuwa hajawahi kumtelekeza mumewe, ila kumpa huduma bora bila ya kujali garama ambazo zilikuwa juu sana. Lela alisema alimuacha na msichana msomi kama Sabrina aliyempa pesa nyingi na usafiri kabisa ili chochote kikitokea, aweze kumkimbiza mumewe hospitalini. “Kama mimi ningekuwa nimemtelekeza mume wangu au simjali, ningemuachia msichana kama Sabrina ambaye nilimlipa mshahara mkubwa vile, pamoja na usafiri?” Akauliza Lela akilia kwa uchungu sana.

“Kama nia yangu ni kumuangamiza huyo Tino, ningemuacha kweli kwenye mikono salama na nyenzo za kumsaidia?” Ushahidi wa ujumbe kutoka kwa Sabrina mwenyewe akisema Lela alimuachia mgonjwa, tena baada ya kulipwa huo mshahara anaosema Lela ni mkubwa sana, wa miezi mitatu, Lela alikuwa nao. Ujumbe alioandika Sabrina kwa Lela akidhani utamfunga Lela ndio ukawa msaada kwa Lela. Ubaya wa ule ujumbe wa Sabrina haukuwa na kiasi cha pesa alicholipwa na Lela kama mshahara wake, kwa hiyo Lela akataja pesa anayotaka yeye. Ambayo ilikuwa kubwa ya kushangaza. Akasisitiza kwa masikitiko kwamba hicho ndicho kiasi chote alichokuwa amemlipa Sabrina, na akawaambia ndio waamini jinsi kumuuguza Tino ilivyokuwa ikimgarimu.

Akaendelea kujitetea akitumia ujumbe huohuo wa Sabrina juu ya kuwatelekeza. Lela alikuja na uthibitisho wa ugonjwa wake mpaka wa kutoka kwa daktari aliyekuwa akimuhudumia maradhi ya pressure yaliyosababishwa na kumuuguza huyohuyo Tino kabla hajalemewa na kutafuta msaada wa Sabrina. Lela alieleza kuwa alikuwa akiugua kwa muda mrefu ila kukosa muda wa matibabu yake sababu ya kumuuguza mumewe ambaye kwa asilimia kubwa ndiye aliyechangia maradhi yake mpaka kulazwa. “Nilipompata Sabrina, tukakubaliana anisaidie kumtunza Tino, ndipo nilipokwenda na mimi hospitalini.” Lela akaeleza mengi kwa machozi akionyesha Tino ndiye amekosa fadhila.

Nani wakutolewa muhanga….

M

ax akaendelea kuwaza akipanga hoja zake kutokana na kile alichokizungumza Lela na Tino ambaye ndio mteja wake kwa wakati ule. Kila alipopanga hoja zake, bado tatizo likabaki ‘Sabrina’. Kwamba akimtoa Sabrina pichani, na yeye akatunga yake ya kumfundisha Tino kujitetea mahakamani, lazima kushinda tu maana itakuwa ni maneno yake Tino dhidi ya Lela. Ikabaki jinsi ya kumtoa Sabrina kwa Tino. Max akajua haitakuwa rahisi Tino kumuachia Sabrina. Kwanza Tino alishasema ni bora apoteze kila kitu kuliko kumuingiza Sabrina matatizoni. “Huyu Sabrina hawezi akaninyima pesa ndefu namna hii!” Max akawaza akipigia mahesabu pesa atakayolipwa na Tino. Akajiambia nilazima amuendee kwa hoja za kueleweka. Ipi? Kazi ya kuanza kumpeleleza Sabrina, kumjua yeye ni nani ili kumfitini kirahisi, ikaanza.

          Max akampeleleza Sabrina kutaka kujua ni msichana wa namna gani, ikashindikana kwa sababu Sabrina si mtoto wa mjini, hana kashfa, hajulikani na yeyote yule. Akajua Lela mwenyewe ndiye atakayempa habari za Sabrina. Kwa kuwa Lela ni muongeaji sana, Max akaandaa maswali yakumchomekea hapo katikati wakati akijieleza ili akiwa anaongea yake, na yake yajibiwe. Na kweli. Bahati kwa Max hasara kwa Sabrina. Max akampigia Lela akiwa amejiandaa na maswali yake, na kweli Lela aliyajibu kwa undani mpaka Max akaridhika kuwa amepata nondo za kumtosha kusuka yake.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Siku inayofuata kwa Max ambayo ndio alipanga azungumze na Tino ndio ikawa siku ya Tino kwenda KCMC kumuona daktari kwa mara ya kwanza. Sabrina na Tino waliamka na furaha, wasijue linalowasubiri mbeleni. Tino alikuwa na tumaini kubwa kwa daktari atakayeenda kumuona kana kwamba ndio alikuwa anakwenda kupokea upanyaji wake wa huo mkono wa kulia aliokuwa akiutegemea sana. Moyo ulijawa furaha, hata akaomba penzi la asubuhi kabla hawajatoka maana hakuwa amekwenda mazoezini. Sabrina akiwa ametoka tu bafuni na taulo lake, akaliachia na kuanguka sakafuni mbele ya Tino. Tino akapiga magoti mbele yake kwa haraka, akamshikilia hips zake kwa nguvu, midomo ikaanza kutembea mwilini kwa Sabrina. Akiwa amesimama vilevile, midomo ya Tino ikatulia sehemu ambayo Sabrina akasalimu amri akafanikisha bao la furaha. Akacheka sana, asiamini. Tino akamuinamisha kitandani na yeye akafaidi penzi ndipo wakatoka.

Huyo huyo Mzee Swai akamtambulisha kwa daktari ambaye alikubali kuwaona bila kusubiri muda mrefu.  Baada ya siku 5 mbeleni, Sabrina akamsindikiza mpaka KCMC. Mzee Swai alimwambia yule daktari kuwa Tino ni kijana wake aliyeachiwa na marehemu baba yake. Kwa hiyo amuhudumie kama ni kijana wa Swai. Na kweli, alimpokea akiwa mcheshi. Akamuhoji maswali kadhaa. Akaangalia pressure yake. Akamwitia mtu wa kufanyia ule mkono mazoezi. Wakamwambia hakuna dawa yakumpa ili mkono upone, ila akiendelea hivyo bila kuwa na pressure ya juu, mazoezi ya ule mkono na viungo kwa jumla, baada ya muda ataona mabadiliko. Hilo halikumfurahisha Tino ambaye aliuliza maswali mengi akitaka kuona kama kuna njia ya haraka ya kuponyesha ule mkono. Wakapewa siku za kwenda mazoezini wakaondoka, Tino akiwa hana furaha hata kidogo.

Sabrina akidhani wamemaliza siku kwa habari mbaya, ili usiku atafute jinsi ya kumtuliza mpenzi wake, kwenye saa 12 jioni Max naye akapiga simu. Tino alipoona tu simu ya Max, akapokea kwa haraka. “Mambo yametibuka Tino. Lela amerudi kivingine.” Tino akakaa kwa haraka pale alipokuwa amejilaza kochini, macho kwenye luninga, amekumbatia mkono wake hata hamuongeleshi Sabrina aliyekuwa amekaa kochi la pembeni yake. “Nini!?” Tino akauliza kwa mshituko sana. “Amekataa kusaini talaka. Anasema yeye bado anakupenda. Aliondoka nyumbani akiwa mgonjwa, akaona asimlemee msichana wa kazi aliyekuwa amemleta pale nyumbani akuhudumie wewe. Akaonelea yeye akauguzwe kwa rafiki ambaye ni kama ndugu. Ameleta uthibitisho wa siku alizokuwa akienda hospitalini. Anaonekana pressure ilikuwa ikimsumbua.” “Haiwezekani Max!” Tino akashangaa sana.

“Huwezi amini Tino, amekuja ofisini kwangu na wakili wake. Lela analia, anasema umekosa fadhila. Amepatwa pressure kwa kukuuguza wewe. Yeye ameondoka akiwa amekuachia msichana mzuri kabisa, ambaye ni Sabrina ili akuuguze wewe, halafu huku nyuma umemfungia nyumba!” “Na maswala ya pesa?” Akauliza Tino. “Anaakili sana Lela. Ameonyesha ujumbe wa Sabrina aliomwandikia. Ubaya ule ujumbe wa Sabrina haukuwa na kiasi cha pesa alizotaja kulipwa na Lela. Kwa hiyo Lela ametaja yeye kiwango kikubwa sana cha pesa ambacho alimwachia Sabrina akidai ilikuwa ni kwa ajili ya mshahara wake Sabrina akimlipa kwa muda mrefu ili asije kukukimbia maana wafanyakazi walikuwa wakikukimbia sababu ya jukumu zito la kukulea wewe na kumuacha yeye akihangaika na wewe peke yake. Anasema sasa, alipompata Sabrina ndipo akaona amtie moyo kwa kumlipa pesa nyingi ili akae na pia akamuachia pia pesa ya matumizi, lakini anasema Sabrina ndio hakuelewa, alidhani pesa yote hiyo ni ya mshahara tu. Ambacho hicho kiasi alichotaja Lela, ni kingi sana Tino. Kwa kipindi hicho mpaka sasa, kinatakiwa kiwatoshe.” Max akamtajia Tino hicho kiasi alichosema Lela alimpa Sabrina. “No way!” Tino akahamaki kwa sauti.

“Muongo kabisa, anamsingizia Sabrina. Mimi ni shahidi wa Sabrina.” Tino akatetea, Max akajua bado yupo upande wa Sabrina, lazima kuongeza nguvu. “Sasa hayo ni maneno yake Sabrina dhidi ya Lela maana hata wewe hukuhesabu pesa alizomkabidhi Sabrina.” Tino akatulia. “Pesa yote si alimkabidhi Sabrina na Sabrina ndio alikuwa akitoa za matumizi ya pale nyumbani?” Max akauliza. “Ndiyo lakini…” “Sasa ndio nakwambia, huwezi kusema wewe ni shahidi wa Sabrina kwa imani tu, Tino! Ni mpaka uwe ulizihesabu hizo pesa na kuthibitisha. Na hilo watakubana nalo mahakamani. Kuwa makini kwa kila unachozungumza.” Hapo Tino akapoa.

“Na kuna jambo nitakwambia baadaye tukiwa wawili. Ila kuhusu pesa za benki hata hajagusia kabisa ila kulalamika garama za kukuuguza wewe zilikuwa juu sana. Ila nilizungumza na yule muhasibu, anasema tarehe 15 juzi, Lela alimpigia simu akimuulizia mshahara wako. Alipozikosa nafikiri ndipo alipokimbilia nyumbani kwenu.” “Sema kwangu.” Tino akamkatisha kwa hasira. “Kisheria ni kwenu wote wawili, Tino.” Max akamuweka sawa na kumuumiza Tino zaidi.

“Sasa alipofika Kunduchi, ndipo mlinzi akamkatalia kuingia mlangoni. Nafikiri sasa ndipo akafungua simu yake, akatafuta mwanasheria, na huyo mwanasheria anaonekana amejipanga Tino. Lela amerudi akiwa na lawama sana na wewe.” “Huo ujauzito niliosikia anao?” Tino akauliza. “Mimi sikuona tumbo. Kama anayo mimba basi bado haijatokeza au ilitoka. Ila hivi ninavyokwambia Lela anataka ndoa yake. Anakulaumu wewe ndio unamkimbia baada ya kukuuguza kwa miezi sita mchana na usiku mpaka yeye ndio ameugua.” “Haiwezekani Max! Haiwezekani!” Tino akasimama. Sabrina aliishiwa nguvu, hata kusogea alikuwa hawezi tena.

“Kwa kifupi nakusubiria wewe. Na kwa sasa inaonyesha wewe ndio unamuacha bila kosa. Na unamjua Lela, atakuwa ameshachafua kila mahali.” “Hilo sijali. Juu ya ile nyumba yangu?” Akauliza Tino. “Hapo lazima ucheze kwa makini sana Tino. Ukionekana wewe ndio unamuacha bila makosa, kuna athari zake.” “Leo ni siku mbaya sana kaka. Naona kila kitu kipo vibaya. Kila ninapoenda habari ni mbaya!” Akalalamika Tino. “Mimi ninachoshauri ni utulivu na umakini. Lela bado hajajua kama upo na Sabrina. Hilo moja.” Hapo Tino akashituka.

“Na kama upo naye, mpoje naye! Upo naye hapo karibu?” Max akauliza kama anayetaka kumteta Sabrina. Tino akakubali kama Sabrina yupo hapo. Max akaendelea akisikika amegairi alichotaka kuzungumza. “Kwa hiyo muwe makini sana kusiibuke sababu ingine tena itakayomfanya akakushinda. Maana hakuna uthibitisho kama Lela alikuwa kwa mwanaume, maana hana ujauzito wala uthibitisho. Anasema alikuwa akiuguzwa. Kama alifukuzwa kazi kwa kuugua, tena anasema wewe ndiye uliyesababisha maradhi kwake, unajukumu lakumtunza kama mke mpaka kuhitimisha.” Tino akatupa simu kwenye kochi kwa hasira na kuingia chumbani. Sabrina alibaki ametoa macho kwa mshituko.

Kisicho Riziki, Hakiliki.

S

abrina akabaki amekaa hapo kwenye kochi kama aliyepigwa sindano ya ganzi baada ya kama dakika 10 akamuona Tino ametoka na nguo za mazoezi. “Naomba uwe makini Sabrina.” Tino akaongea akitaka kupita ila akasimama kama kuweka msisitizo. Sabrina akamgeukia. “Kwenye nini?” “Kama ulivyosikia. Lela hana mimba. Max anasema ikitokea sisi tunaharibu, atashinda.” “Unamaanisha nini sisi tusiharibu?” Sabrina akauliza taratibu tu. “Katika kila kitu, lakini zaidi kwenye mambo ya ujauzito. Hakikisha hushiki mimba.” “Hudhani kwamba hilo angalizo limechelewa?” Sabrina akauliza akiwa ameshakasirika na yeye. Tino akashituka sana. “Inamaana umeshashika mimba tayari!?” Akauliza kwa kuhamaki sana kama ambaye alikuwa akibakwa na Sabrina.

“Sijui!” Sabrina akajibu akiwa anamtizama. “Hapana Sabrina. Sipo kwenye wakati ambao naweza kulea. Angalia afya yangu. Sijui hata mwisho wa maisha yangu utakuwa vipi! Mkono ambao ndio nautegemea maishani ndio huo nimeambiwa hakuna tiba ili upone kwa haraka. Huyo mtoto atakuja kwenye mazingira gani!?” Sabrina akabaki akimtizama. “Yaani la ugonjwa halijaisha, tunaingiza watoto! Tutampa sababu Lela kunishinda.” “Hebu subiri kwanza Tino. Acha kunichanganya tafadhali. Mbona gafla inakuwa ni kama unatoa lawama kwangu!? Halafu unaposema Lela atakushinda, unamaanisha unalinganisha thamani ya nyumba na watoto!?” Sabrina akauliza.

“Tafadhali fikiria Sabrina, hata mara moja tu kama mtumzima na uliyesoma.” Sabrina akatoa macho kwa kumshangaa. “Huyo mtoto tutamuweka wapi? Hapa tulipo sisi wenyewe tumehifadhiwa! Hatima yangu na Lela ni kama ulivyosikia. Unafikiri itakuaje?” “Subiri kwanza Tino. Maana naona unazidi kuwa mkali na mwishoe utapandisha pressure kwa kitu ambacho kilishatokea.” “Inamaana umesha shika mimba?” “Tafadhali Tino, naomba utulie. Kumbuka hata mwezi haujapita tokea tuanze kukutana kimapenzi. Kwa hiyo sijui. Naomba tusiazime matatizo ya kesho leo, ukajikuta unaongea mambo ambayo utakuja kujuta baadaye.” “Siwezi kujuta. Hili naomba ulizingatie Sabrina. Sina mazingira yakuanza na watoto sasa hivi. Nipo kwenye wakati mbaya sana kwenye maisha yangu.” Tino akachukua simu yake pale alipokuwa ameitupa kwa hasira. Akamuona amesoma ujumbe fulani uliokuwa umeingia, kisha akaondoka bila kuaga. Akamuacha Sabrina amepigwa na butwaa asiamini alichokisikia kutoka kwa Tino.

Kwa Tino..

Max alimuomba akiwa peke yake ampigie ili wazungumze. Akaelekea gym akiwa na hasira na maumivu rohoni akampigia akijua wazi huko alipo Sabrina hatasikia. Max akapokea kwa haraka kama ambaye alikuwa akimsubiria yeye. “Sasa mimi sina habari nzuri sana Tino na nina sikitika sina jinsi nyingine ya kufanya ila kukwambia tu. Ili ujue chakufanya. Au nikupigie wakati mwingine, tuzungumze vizuri?” “Tafadhali niambie tu. Hii siku ishakuwa mbaya.” Tino akaongea kwa jazba.

          “Nimepata tetesi kutoka kwa mtu wa karibu sana wa Lela ambaye wapo kundi moja na dada yake Sabrina. Nimesikia huwa wanakuwa baa na sehemu za starehe pamoja, ila sitakutajia jina lake. Lakini mimi kama kaka yako, nimeona nikwambie tu, wewe mwenyewe uamue na ujue jinsi ya kujipanga kuanzia sasa.” “Juu ya nini tena?” Tino akauliza. “Sabrina. Kumbe huyo binti yupo hapo kwa malengo tokea mwanzo kabisa. Nasikia kumbe dada yake yupo karibu sana na Lela. Anajua jinsi ulivyo na pesa na jinsi Lela anavyoichezea pesa yako. Sasa nasikia dada yake alipoona Lela anafaidi na hakutunzi, ndipo akaona mwanya. Akaamua kumuunganishia mdogo wake. Nasikia Sabrina maisha yalikuwa yamemshinda kabisa huko nyumbani kwao. Ndio dada yake akamuita mjini. Akamueleza juu yako, ndio Sabrina akakubali kuja kupambana kufa na kupona akikuonyesha anakujali kwa hali na mali ili ukipona tu, akubane.” Tino akaumia sana maana ni kweli hata Sabrina alimwambia maisha yalikuwa magumu sana kwake, hakufanikiwa kupata ajira baada ya kumaliza chuo, akabaki nyumbani akisaidia kazi za nyumbani.

          “Hawa mabinti wawili hawa, Sabrina na dada yake, nasikia kwao ni huko Chalinze. Wanahali ya ushirikina sana kwao. Huyo aliyeniambia ambaye wapo kundi moja kwenye starehe, nasikia anasema huyo dada yake huko kazini hawawezi kumgusa jinsi alivyojizatiti. Hata viongozi wake wanamuogopa. Akitaka jambo lake huko kazini, nasikia anajisifia kuwa ni lazima liwe hata kwa numba. Ndio maana ana safari nyingi za kikazi za nje ya nchi kuliko wenzake wote huko kazini, kumbe ni kwa kuzisuka kiushirikina. Sasa tetesi zilizopo, nilizosikia eti wana mpango wa mambo mawili. Sabrina kujishikisha mimba na kutumia mbinu za uchawi kukubana mpaka ndoa.” “Basi nimeshachelewa kaka. Nahisi ameshashika mimba.” Tino akaongea kwa kuumia sana akikumbuka juhudi za Sabrina kwake akidhani ni upendo kumbe nia ni kuja kula pesa yake! Tino akabaki akitingisha kichwa kama ambaye haamini.

Max akafanikiwa kupata moyo wa Tino. Akajua yupo upande wake. “Sasa ujue huyo atakuangamiza. Akizaa tu huyo mtoto, ukitoka kwenye tatizo Lela, unakuja yeye ambaye atakuwa amekuzalia na mtoto.” Tino akakaa kabisa. “Na Lela akishajua tu kama umekuwa na mahusiano naye, ndio ujue utakuwa umepoteza kila kitu, wanawake hao watakuacha barabarani.” “Sijui  nina mkosi gani kaka yangu! Kwa Sabrina nilijua nimepata, na nikamuamini sana, kumbe ni tapeli mtupu! Amekuja kwangu na maneno ya kitapeli, akinionyesha ananijali, kumbe macho yake yapo kwenye mali zangu!” Tino akaumia sana.

          “Ila nafikiri kwake huyo hatujachelewa. Tunaweza kumtoa kwenye picha kirahisi sana akiwa hukohuko Moshi kabla hajaja huku kuungana na dada yake. Acha nijipange mimi kwanza, ndipo nikupe na wewe muongozo. Ila kuanzia sasa, jitahidi sana kumkwepa na kuwa naye makini ili.” Max akaendelea kumtia hofu mpaka akaridhika kwamba hata Tino akirudi kwa Sabrina, hakuna kutengeneza tena. Yeye ndio ameshika masikio ya Tino sasa. Alipojiridhisha ndipo, akaaga akiwa amemuacha Tino ameishiwa nguvu kabisa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mpaka Tino anarudi, Sabrina alikuwa amebaki hapohapo alipokuwa amekaa. Tino akaingia kuoga, akatoka, Sabrina amebaki hapo hapo. “Nataka tukatafute ushauri wa madktari. Kama imetungwa, kabla hajawa mtoto, tutafute dawa ili uanze kupata siku zako kama kawaida.” Sabrina alishangaa na kuumia sana. “Unamaanisha kutoa mimba! Yaani kuua mtoto sababu wewe na Lela hamjafikia muafaka!?” “Unang’ang’ania nini wakati wewe mwenyewe umesema haijafika hata mwezi!? Inamaana hajakuwa mtoto bado. Tafadhali kuwa mtu wakufikiria Sabrina. Hata mtoto wa darasa la saba ataelewa hili. Huyo sio mtoto, itakuwa donge tu la damu. Unataka aje kuwa mtoto halafu aje aishi wapi? Mazingira gani!? Fikiria.” Sabrina alimtizama Tino akatingisha kichwa kwa kuumia sana. Huku akimshangaa. “Kwanza, kama mimba imetungwa tayari, hakuna cha donge, huyo ni mtoto. Na naomba nikutoe wasiwasi Tino. Uzuri ni kwamba kama ni mimba imetungwa, itakuwa kwangu sio kwako. Mwambie Max anayekufundisha jinsi ya kuishi, kuwa wewe upo huru kuendelea na maisha yako kama kawaida.” Sabrina akaondoka kuingia chumbani kwao, bafuni.

 ~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Sabrina alikuwa kwenye mshtuko wakupita kiasi. Hakutegemea kama Tino angembadilikia hivyo! Na ni kweli alijiachia. Akajishika tumbo nakuanza kufikiria mara ya mwisho kupata siku zake. Akili ikawa ilishachanganyikiwa. Hakukumbuka. Akaanza kulia kwa hofu. ‘Itakuaje kama nimeshika mimba? Nitakwenda wapi na nitafanya nini?’ Hofu ikazidi kumuingia. Akakumbuka alivyoondoka nyumbani bila kuaga ila kuwafikishia ujumbe kupitia Sabina.

“Nitakwenda wapi?” Sabrina akazidi kuwaza huku akilia. “Jack!” Akamkumbuka Jack. Kijana aliyemvumilia na kumsubiri bila kuchoka. Ukaribisho aliompa kwenda kuanza upya. Makazi na malazi. Akakumbuka ujumbe wa mwisho aliomtumia na kumblock bila kutaka kumsikia anamjibu nini. Akaendelea kujiachia kwa Tino bila kufikiria. Akazidi kuumia. Akakumbuka mazungumzo kati ya Tino na Max. Akajua lazima Tino atarudi kwa mkewe. “Kweli mimi fungu la kukosa!” Sabrina akazidi kujikatia tamaa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~ 

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment