Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 1. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 1.

Ezra alitoka hapo kama mwehu! Akampigia simu Junior na kumueleza kwa kifupi akiwa ameshatoa gari getini kwake. Junior akatumia akili ya haraka akapiga simu hospitali ya karibu ya pale hotelini na kuomba gari ya wagonjwa akieleza uwezekano wa Jelini kunyweshwa sumu iliyochanganywa kwenye juisi ya embe. Akaomba wakimbilie hapo kwenye hiyo hoteli wakiwa wamejianda na Jelini wanayehisi ameshapoteza fahamu. Kwa hizo tu taarifa, akawa amesaidia hatua ya kwanza ya huduma ya kwanza wakifika kwa huyo Jelini.

Kisha simu ingine kwa mama Jema. Akimwambia alipo Jelini na kile Jelini alichomwambia Ezra. Kisha akawapigia wazazi wake huku na yeye akikanyaga mafuta kuelekea alipo Jelini.

Uzuri ni kweli hapakuwa mbali na kwa kina Ezra. Njia za mkato hata dakika 10 hazifiki. Akaegesha gari katikati ya njia na kukimbilia vyoo vya kike. Hakubisha hodi, akaingia na kukuta wanawake wengine humo, asijue amempita Colins hapo mlangoni akiwa anamsubiria Jelini atoke. Akaanza kuchungulia chini ya milango akamuona Jelini amelalia matapishi sakafuni.

Akasukuma mlango kwa nguvu akafanikiwa kufungua akiwa amemsukuma hata na Jelini hapo sakafuni. Alipomtingisha, Jelini alishaanza kutoa povu mdomoni. Kweli hii ni sumu!” Akawaza Ezra akimtoa pale akikimbia naye. Anatoka nje, na Junior naye anashuka garini.

“Nimeita gari ya hospitalini, wapo njiani.” “Siwezi kusubiri.” “Najua umepaniki Ezra. Lakini hawa watu wanakuja na huduma ya kwanza kumtoa hiyo sumu hapahapa kabla hawajamfikisha hospi…” Wakasikia gari ya wagonjwa ikija kisha mataa. Angalau Ezra akaridhika. Bado hakuwa amemuweka chini. Akaanza kukimbia naye kulifuata hiyo gari ya wagonjwa. Wakasimama katikati ya barabara, Jelini akiwa hana fahamu, akapokelewa. Ezra na yeye akaingia ndani ya gari hiyo ya wagonjwa, safari yakurudi hospitalini ikaanza huku akiwa anapewa huduma ya kwanza.

Alichofanya Junior ni kusogeza gari ya Ezra na kuiigesha sehemu nzuri. Akaifunga na kuondoka huku akipokea simu za kueleza kinachoendelea. “Wameshamchukua, tunaelekea hospitalini.” Akawatajia jina la hospitali, na kuendelea kukaza mwendo.

Mpaka anafikishwa hospitalini akawa ametapishwa sumu yakutosha tu, ila  bado hakuwa akijitambua. Kila alivyotapika, akawa akimaliza, anazima kabisa. Hofu ikaanza kuwangia pale alipoanza kutoa damu mdomoni.

mungu Wa Mitandao.

Huku nyuma Colins alipoona ile hali, akaingiwa na hofu ya ajabu lakini hakuthubutu kuwafuata. Akafikiria kwa haraka. Akajua lazima wanao husika ni kina Love ambao Jelini alishawaona tokea mwanzo. Akaamua kuwafuata ili kuhakikisha kama ni wao, lakini hawakuwepo. Kumbukumbu ya alichoambiwa na Jelini juu ya nguvu ya Kemi, ikapita kichwani kwake. Na yeye bila ya kuchelewa, kwa haraka sana akaomba kuonana na meneja.

“Mna kamera hapa?” Likawa swali la kwanza na kwa haraka. “Baadhi ya maeneo.” “Naomba kuona.” “Unajua hatuwezi kukuonyesha bila kibali maalumu.” “Unatania wewe!? Mteja wenu aliyekunywa juisi ya hapa ameondoka hapa mahututi. Nataka kuangalia ili niwasaidie, unakataa!?” Ile kelele ikamsogeza na mmiliki. Bahati nzuri jioni hiyo alikuwepo.

Alishuhudia lile gari la hospitali na fujo ya mpaka Jelini anatolewa pale. “Hivi unajua kinachokukabili?” Akamuuliza kwa ukali haswa. “Mimi nataka kuwasaidia kabla hawajaingia kwenye mtandao wenu nakufuta ushahidi! Ukichelewa tu, wakifuta ushahidi, ujue utafia jela.” Akamkimbiza chumba chenye kompyuta na vivaa vyakutunza kumbukumbu za kamera za ulinzi.

Zimefika (40)

Colins alipofanikiwa kuingia tu kwenye mitambo ya hapo, akagundua kuna mtu mwingine naye upande wa pili, anajaribu kuingia hapo. Akawaonyesha. “Unaona huyu, anahangaika kuingia kwenye mtandao wako, kufuta ushahidi wa kile cha kweli kilichompata mteja wako.” Colins alihakikisha anamuelewesha jukumu lake kama mmiliki wa ile hoteli. Kwa hakika walishituka sana.

“Tafadhali tusaidie.” Colins akaanza kazi. Viwanja vya nyumbani! Wamegusa TENA penzi lake! Akakusudia kulipiza kisasi haswa.

Kwanza kabisa, akaweka security ngumu mpaka akafanikiwa kumzuia au block yule mtu upande mwingine ambaye alijua kwa hakika atakuwa ni Kevin Kasa. Kisha akamtumia ujumbe mfupi kwa barua pepe. ‘Hilo ni kosa ambalo sitakusamehe, Kevin.’ Ikawa kama amemwambia nakujua wewe ni nani na nimekufikia.

Maana alimtumia kwa email yake kabisa lakini ambayo si kwamba ina jina lake Kevin Kasa, kwamba Colins amejua kirahisi. Hapana. Alimtumia kwa email yake anayotumia kwenye mambo yao hayo ya mtandaoni, yenye nicknames zao za huko mitandaoni, majina ambayo hayana hata herufi za majina yao.

~~~~~~~~~~~~~~~

Kevin alivyopata ule ujumbe, alishituka akasimama kwa haraka karibu atupe kompyuta. Akajua wazi ameingia kwenye anga za Guru. Yupo vitani na akajua alivyotumwa na dada yake safari hii pia ni kikubwa zaidi, na mbaya zaidi, kinamuhusu Guru Colins ambaye mpaka hapo ameshamshinda. Akajua kwa hakika dada yake yupo matatani. Alichotaka kifutwe safari hii, kipo kwenye mikono sahihi, hatapona.

Akampigia. “Umefanikiwa?” Likawa swali la kwanza kutoka kwa dada yake. “Umefanya nini tena Kemi!?” “Acha kunihoji. Nakuuliza umeshafanikiwa?” “Safari hii nahisi umecheza pabaya. Kama ni jambo hatari, nakushauri kimbia usiku huuhuu, nenda hata Nairobi, kesho ukimbilie kwa mama moja kwa moja.” “Acha kunitisha wewe! Fanya kazi yako.”

“Hakika safari hii ondoka na usirudi Kemi. Inavyoonekana umeingia vitani na Colins. Yaani pale kwenye ile kampuni tunapofanya kazi, anajulikana kama mungu wa ile kampuni na mpaka leo hawajaziba pengo lake. Hapa tunapozungumza, amefungia ile system nzima, nina uhakika hata umpigie nani simu umuombe msaada, hataweza kuingia.”

“Na mbaya zaidi amejua kama ni mimi ndiye nimejaribu kuingia kule kutaka kufuta. Maana amenitumia ujumbe kwenye email yangu ya siri, ambayo wanajua watu wachache sana. Na amenitambua kabisa kwa jina langu kamili, mpaka nimeogopa! Umefanya nini tena Kemi!? Na kwa nini unapenda kuniingiza kwenye matatizo yako kila wakati?! Kwa nini unataka niangamie na wewe?” Kemi akakata simu.

~~~~~~~~~~~~~~~

Colins akaendelea kufanya yake mpaka akakamilisha kulitenga na kulitengeneza lile tukio zima vizuri na kifasaha. Tena katikati ya hiyo video, akarudiarudia kuzitengeneza vizuri zile sehemu maalumu kuweka msisitizo. Akajitumia yeye na James kama kujihami.

‘Tafadhali naomba unielewe James na umueleweshe Ezra. Nilimuomba Jelini kikao kwa heshima kabisa ili na yeye asikie upande wangu, asiishie kuniona nitapeli. Niliyemuacha njia panda na kuhamia kuishi na Love, kama muhuni tu na kumdharau yeye kwa kumtelekeza. Najua na wewe unajua, anastahili kusikia ukweli kuliko kumuacha na maumivu ya usaliti.’

‘Sasa kilichoendelea hata hapo kwenye video utaona ni mazungumzo sehemu ya wazi kabisa, nikimwambia upande wangu na mimi kile kilitokea siku ile nikiwa napanga kwenda kwao na nikiwa na nia ya kumuoa kabisa na si kumpotezea muda. Nampenda Jelini na nilikuwa tayari kuishi na kumkuza Jeremy kama kijana wangu.’

‘Tafadhali angalia hiyo video kwa makini sana. Ndio ukweli halisi wa kilichompata Jelini usiku wa leo tulipokuwa pamoja. Nimewahi kabla kina Kasa hawajafuta. Maana nimemkuta na kumblock Kevin akiwa ameshaingia kwenye mtandao wa hii hoteli akijaribu kufuta kama tukio la kwanza walilomfanyia Jelini ofisini kwa baba yao na kumjeruhi vibaya sana.’

‘Ila Jelini alificha hakutaka kuwaambia nyinyi. Ila Kevin anahusika kwenye kupoteza ushahidi hata na kwenye tukio la kwanza alilosababisha huyo Kemi ambalo na leo utagundua amehusika na kuweka sumu kwenye kinywaji cha Jelini, akisaidiana na Love. Ila nakuahidi kuipata na hiyo video ya kwanza aliyofuta Kevin ofisini kwa baba yao. Nitakutumia nikishaipata.’

‘Najua kwa sasa ‘samahani’ haitasaidia, ila hii hoteli ni chaguo la Jelini mwenyewe akitaka tukutane hapa, tuzungumze. Sikupachagua mimi. Na mimi sikuwaona Love na Kemi, wameshakimbia hapa. Utaona kwenye video wakiondoka.’

Akamtumia na huo ujumbe kama akijitetea lakini alijua wazi, hakuna anayetaka kumsikia. Na alifanya bila ya kuwaambia hapo.

Ukweli Wa Kilichompata Jelini.

Alipokamilisha hilo ndipo akawaita wenyeji wake, ili na wao waone. Maana walibaki hapo ndani ya hicho chumba, hawajui chakufanya, roho mkononi, wakimsubiria amalize. “Sasa nimekutolea tukio zima. Maaana mama wa yule binti mimi namfahamu. Jiandae na kujipanga ukiwa na huu ushahidi. Na uwe na maelezo yakutosha, lasivyo, atakuchomea hii hoteli nzima mpaka iteketee.” Akaendelea akiwa ameshawatisha zaidi.

“Na wakati ukijipanga, omba yule binti apone. Ndio itakuwa pona yako hata utaweza kumsogelea mama yake. Ila mimi ningekuwa wewe, ningejiwahi mapema sana.” “Mbona kama unatupa lawama kwangu moja kwa moja wakati hoteli yangu haihusiki? Kama alikuja hapa na ugonjwa wake!” Akawahi kujitetea. “Njoo nikuonyeshe kilichotokea mpaka kufikia yule binti kukimbizwa hospitalini.” Akafungua ile video.

Mwanzoni kabisa akaonekana yule muhudumu anapita. Akasimamishwa kwenye meza ya kina Kemi, Love na wanaume wengine watatu. Ikaonekana kama Kemi amemuuliza kitu. Akaonekana baada ya kujibu yule muhudumu akaondoka.

Kisha baada ya hapo Kemi na Love wakajadiliana kitu, nakuondoka pamoja pale hotelini. Colins alifanikiwa mpaka kuwapata kwa kutumia kamera za nje sehemu ya kuegesha magari. Wakaonekana wakiwa nje wanaondoka na gari ya Love. Kisha baada ya muda wakarudi pale hotelini na kukaa palepale walipokuwa wamekaa mwanzo.

Wakala na kunywa mpaka mara ya nyingine tena yule muhudumu anarudi akiwa na ile juisi ya Jelini na chakula cha Colins. Wakaonekana kumuita, akasimama. Love akaonekana kumzonga na maneno, ndipo ikaonekana kama Kemi akapata upenyo wa kutumbukiza kitu ambacho kwanza, kwa kuwa ilikuwa usiku na walipokuwa wamekaa palikuwa na giza kidogo, Colins akajaribu huvuta lile tukio, ikaonekana kama Kemi amenyanyua mkono juu ya glasi ya Jelini.

Hapakuonekana kwa uhalisia kitu kilichoingia ndani ya hiyo juisi ambayo pia juisi hiyo ya embe haikuonyesha kubadilika rangi. Lakini alipomaliza Kemi, ni kama akarudi kumzungumzisha kidogo yule muhudumu, kisha wakamuona yule muhudumu akiondoka.

Akaonekana hakupitia sehemu nyingine tena wala kusimama popote ila moja kwa moja mpaka mezani kwa Jelini na Colins. Akaonekana aliweka kwanza ile juisi ya embe mbele ya Jelini. Akaonekana Jelini kutosubiri. Palepale akapata funda mbili mfululizo wakati huyo muhudumu akimuwekea Colins chakula chake. Kisha akaonekana Jelini kusimama muda mfupi sana baada ya funda la pili, akielekea chooni kisha kuongeza mwendo kwa kukimbilia.

Baadaye Ezra kuingia pale hotelini, mpaka vyoo vya wanawake. Akaonekana ametoka akikimbia na Jelini kisha kumuweka kwenye gari ya hospitali. Kisha baadaye akaonekana Love na Kemi wakitoka kwa kukimbia kuingia kila mmoja kwenye gari lake na kuondoka kabisa kwenye eneo la hoteli hiyo.

~~~~~~~~~~~~~~~

Yule mmiliki jasho lilikuwa likimtoka kama hapakuwa na A/C kwenye chumba hicho. “Mpaka hapo tupo pamoja?” Colins akamuuliza. “Huna jinsi ya kumkwepa mama yake huyu binti, na vyombo vya sheria kama wewe hutakuwa mbele ya hawa wawili nilio kuonyesha.”

“Tena unatakiwa uwe mbele yao hata kwa hatua 5 zaidi. Kwa sababu hawa wanawake wawili, kwanza wametoka kwenye familia zenye pesa sana. Inamaana watatafuta mtu mzuri kuwawakilisha kwenye mashitaka yeyote yale dhidi yao. Nakuhakikishia usipojipanga vizuri na kwa makini ili kuwawahi, watakushinda,  utafia jela.”

“Pili, nimeshakuonyesha jinsi walivyo wajanja. Wanaakili sana kwenye uovu wao. Wakati wewe hujui kilichokuwa kikiendelea, wao walishamtafuta mtaalamu kuingia kwenye mtandao wako, kufuta ushahidi. Sasa akili kumkichwa.”

“Tafadhali nisaidie kwa ushauri kwa sababu wewe unaonekana unawaelewa vizuri na umeshawashinda!” “Cha kwanza na haraka, huu ushahidi ukulinde. Namaanisha usiulazie damu. Yaani sasahivi wewe jionyeshe upo makini, hakuna mtu anacheza na usalama wa wateja wako.” Akajiweka sawa kumsikiliza.

“Afisa usalama wako aivujishe hii video kwa haraka sana. Kisha kimbia nayo polisi kushitaki. Ili hata kama wakiwahi kukuziba polisi, jamii imeshaona walichokifanya. Watashindwa kukuzima huku nyuma kwenye vyombo vya usalama. Jamii nzima itakuwa nyuma yako.”

“Kingine cha msingi ambacho nakusihi usisahau, ukitoka tu polisi, usiku huuhuu, hakikisha unakwenda hospitalini kumuona mama yake huyu binti. Kikubwa, nguvu yako ni hiyo lafudhi yako. Mama yake ni mkabila sana. Ukimuongelesha kikwenu. Halafu ukaonyesha upo upande wake kwa asilimia 100. Na umeshawashitaki, hawa watu. Utaupata moyo wa huyu mama, na anaweza hata kukusikiliza. Lasivyo ni wakumuogopa kuliko hata kituo cha polisi. Wanaomjua watakwambia.” Kimya amekodoa macho.

“Yaani hapo uliposimama mpaka sasa hivi, umeshaanza kuchelewa. Changamka. Umechezewa mchezo mchafu sana, tena na watu makini, halafu ni makatili wanaojua kujipanga kwa makini sana. God speed.” Colins akasimama na kuondoka bila ya kuaga.

~~~~~~~~~~~~~~~

Ni nini Kitaendelea?


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment