Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 2. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 2.

Ulikuwa usiku mgumu kwa mama Jema, hajawahi pitia maishani. Aliona uhai wa Jelini upo mlangoni kutoka, hakuna tumaini. Swala la kwamba ametapishwa sumu yote alishahakikishiwa ila aliambiwa ile sumu ilikuwa kali sana imeacha madhara ambayo hawajui imeharibu humo ndani kwa kiasi gani. Baada ya kuanza kutapika damu, ikazidi kuwatia wasiwasi.

Wakiwa kwenye ile hali. Mama mchungaji karibu yake pamoja na mama zake wengine Jelini walishafika hapo hospitalini na Jema akiwepo, James akawasogelea. “Najua tupo kwenye kusubiri, hatujui kinachoendelea ndani, lakini mama Jema, tafadhali jikaze uangalie hii video, ujue kilichokuwa kikiendelea mpaka kumfikisha Jelini hapo alipo. Usibakiwe na yote. Angalau utoe sintofahamu moja.” James akavuta masikio na akili za kila mmoja pale. Mchungaji na vijana wake walikuwa wameinama kila mmoja akimsihi Mungu kivyake.

~~~~~~~~~~~~~~~

Hali ya Ezra ndio alijawa hofu! Vifo vya ndugu zake zaidi alivyoshuhudia akiwa ameitwa kuzika wazazi vilimjia. Hapo alikuwa na hali mbaya. Hata kukaa chini alikuwa hawezi. “Mungu wangu nisaidie!” Ndio neno lililosikika akilisema kila wakati akitembea hapo bila kupumzika, mikono kichwani. Macho mekundu kama aliyevuta bangi ya kupitiliza.

~~~~~~~~~~~~~~~

Aliposikia hivyo, akasogea hapo kwa haraka. “Ezra wewe nimeshakutumia wa kwanza maana Colins ameomba nikuonyeshe wewe wa kwanza.” Wote wakashangaa. “Na ujumbe mwingine kutoka kwake, nitakwambia baadaye maana najua sasahivi haupo kwenye wakati wakuelewa” “Aisee hata sijui simu yangu ilipo!” “Uliacha kwenye gari yako, nimekuchukulia.” Junior akatoa mfukoni na kuitafuta hiyo video kisha kwa heshima akamkabidhi Ezra mwenyewe.

“Naomba tukae hapa tungalie na baba.” Maana mchungaji alibaki ameinama kwenye kiti alichokuwa amekaa kama ambaye bado anaomba. Ezra akatoa wazo la kuthamini uwepo wake, vijana wakasogea alipokuwa amekaa mchungaji. Kwa hiyo kukawa kama na makundi matatu yaliyotengenezwa. Kwa mama Jema na dada zake pamoja na mama mchungaji. James na mkewe. Mchungaji, Noah, Ezra na Junior. Wakaanza kuangalia.

~~~~~~~~~~~~~~~

Colins alikuwa akifikiria kwa haraka huku anahasira kali sana. Akaamua kumtumia ile video na Kevin Kasa. Na ujumbe. ‘Natarajia kupokea simu yako punde utakapomaliza kuangalia.’ Akamtumia na kubaki akimsubiria huku akiangalia saa. Alijua wazi anamuogopa na kule kumkamata akiwa anataka kufuta hiyo video, akajua hawezi kuwa amepata usingizi.

Akasubiri kwa muda wa ile video, kimya. Kevin hapigi. Akaamua kumpigia yeye. Ikawa ikiita bila kupokelewa. Akaamua kumtumia ujumbe mwigine. ‘Nina hali mbaya sana. Kupotezewa muda ni jambo la mwisho kabisa nataka kukumbana nalo usiku huu. Tafadhali pokea simu yangu Kevin.’ Baada ya sekunde chake akaona anampigia.

Colins akapokea. Kimya upande wa pili. “Naomba nitumie ile video ya kwanza uliyofuta ya dada yako alipomtega Jelini, na kumpasua kichwa.” “Nini kinakufanya ufikirie ninayo!?” “Kevin! Rudia ujumbe wangu niliotoka kukutumia. Nimekwambia, kupotezewa muda ni kitu cha mwisho kabisa usiku huu, na sitaruhusu. Sijui kama unanielewa? Kwa sababu mimi na wewe wote tunajua wazi, wewe ukishindwa kunipa hiyo video, ndani ya masaa 24, mimi mwenyewe nitakuwa nimeipata. Lakini haitakuwa nzuri kwako.” Kevin kimya.

“Nitahakikisha nina kuadhibu kama nitakavyo muadhibu dada yako.” “Kwa nini unifanyie hivyo wakati ni Kemi mwenyewe!?” “Nitakuadhibu kwa kusaidia kwenye uhalifu wake. Zaidi kwa kumuangamiza mwanamke pekee ninayempenda hapa duniani na ambaye alinipenda mpaka dada yako akafanikiwa kututenganisha. Na leo amegongelea msumari wa mwisho. Sitamsamehe.”

“Nyinyi si mnahela na najua hata akishitakiwa, baba yenu atamtetea, lakini.” Akaweka kituo cha mkwara. “Kwa hakika atatamani angeshitakiwa kisheria kuliko kukwepa hukumu yake. Na wewe, nitahakikisha kila mwenye kampuni, vyombo vya usalama, vyote vinajua wewe ni mtu hatari sana mitandaoni. Nitakuweka kwenye orodha ya kimataifa. Nitaku blacklist, hakuna security system utapita hapa duniani, zaidi kwenye viwanja vya ndege, ukaruhusiwa. Watakushikilia kama gaidi au mtu hatari, mpaka baba yako aje akuokoe! Utakua umelipa. Na najua, unajua sishindwi, ila pengine unaweza dhania nakutisha tu ili nipate hiyo video.” Kimya. Akajua ametishika.

“Sasa, nakupa lisaa, uwe umeipata hiyo video na imeingia kwangu. Lasivyo, hutakaa ukanisahau kama ambavyo sitakaa kumsahau Kemi Kasa. Nitakulipa mpaka ujue nimekulipa kwa dada yako kunipokonya penzi la Jelini, akiwa amenifanya tahira na leo kukusudia kumuua kwa mara ya pili. Hakika utalipa kwa uchungu, labda ujiokoe kwa hili.”

“Vinginevyo jua kuanzia sasa, cha kwanza huna kazi. Maana nina ushahidi wote wa usiku wa leo ulivyoingia kwenye ule mtandao wa ile hoteli. Mpaka Ip address ya ulikokuwepo ukifanya huo uhalifu, ninayo. Sasa jua mabosi wako wote, ifikapo kesho asubuhi hata kabla ya siku ya kazi kuanza, watakuwa na hizo taarifa kwenye simu zao za mkononi wakiwepo wafanyakazi wote wa ile kampuni.” Kevin alimjua Colins na uwezo wake.

“Cha kwanza naomba nisamehe Colins. Mimi sikujua mchezo wowote Kemi aliokuchezea. Ningejua kama ni wewe, kwa hakika unajua nisingefanya nilichofanya. Ukiweka hasira pembeni, utagundua mimi simjinga wakutaka kukuzidi mahesabu. Na hata ile video ya kwanza, Mungu wangu ni shahidi. Alinipigia kama hivi kwa haraka, akiniomba msaada kwa haraka.” “Unanipotezea muda Kevin. Acha kunifanya mimi mjinga. Na nikikata hii simu…” “Colins! Colins!” Akaita kwa kupaniki.

“Basi na mimi nikuombe kitu.” “Haupo kwenye hiyo nafasi Kevin.” “Kumbuka mahusiano yetu Colins! Mimi sijawahi kukukorofisha hata mara moja, hata jamaa pale ofisini walikuwa wakinitania kuwa nakuogopa, wewe ndio unaniweza. Uongo mkuu?” Colins kimya.

“Sijawahi hata mara moja kukanyaga ulipokanyaga nikakuumiza hata kwa bahati mbaya. Na wewe ni shahidi Colins. Nishagombana na kila mtu pale ofisini lakini haijawahi tokea mimi na wewe tukapishana hata mara moja. Ndio naomba uelewe katika hili, sihusiki Colins. Kwanza nisingethubutu.” Kevin huyu alijishusha na mnyenyekevu aliyejawa hofu utafikiri sio Kasa! Ungejua amekamatika.

“Unataka nini?” Colins akauliza kwa jeuri. “Nakutumia hiyo video sasahivi. Lakini tafadhali naomba usinitaje popote, hata iweje.” “Mimi si mtoto mdogo. Na nakutuma kwa baba yenu. Hakikisha unamfikishia huu ujumbe. Mwambie Kasa, safari hii hakuna umbali atamficha Kemi, malipo yake yasimfikie.” Kisha akakata simu.

Hazikupita hata dakika 5, tayari lile tukio zima la Kemi kumtega mguu Jelini na kuumia vibaya sana, likawa limeingia kwenye simu ya Colins na ujumbe. ‘Tafadhali kumbuka ahadi yako Colins.’ Colins akaanza kuangalia, mpaka akatupa simu hapo garini kwa mshituko. Akabaki akihema kwa hofu, akitafakari ni kiumbe gani anaweza kumfanyia mwanadamu jambo baya kama hilo! Hasira dhidi ya Kemi ikazidi kuwaka ndani yake. Akamalizia kuangalia na kumtumia na James pia.

Mfa Maji.

Huku kwa Kevin akajua maji yameshatibuka, akaona ajisalimishe kwa kujitetea. Akampigia simu baba yake. Simu ile ya dharula ambayo mzee hazimi sauti hata usiku. Ni wachache sana walikuwa nayo, na wenyewe walijua si ya kuipiga hovyo. Ni iwe dharula kwelikweli.

Mzee Kasa akapokea bila ya kuchelewa. “Kuna nini!?” “Safari hii Kemi ameharibu baba! Na ameharibu pabaya sana. Mbaya zaidi alichokifanya safari hii, amekifanya kwa mtu yuleyule ila akiwa na mtu hatari sana. Ametibua siri zote. Hapa tunapo...” “Acha kunizungusha kwa maneno mengi ya mafumbo, muda huu unaojua ninatakiwa kuwa usingizini.” “Amemdhuru tena Jelini ila…” Kusikia Jelini mzee akaruka kitandani.

Kevin akahisi simu imedondoka kwa ule mlio aliosikia. Akaona amtumie ile video aliyotumiwa na Colins na kisha akamtumia na ya kwanza ambayo baba yake anaijua, ila akamdanganya. ‘Mbaya zaidi na hii pia Colins amefukunyua mpaka ameipata. Amenituma nikwambie, safari hii huna umbali utamficha Kemi, malipo yake yasimfikie.’ Akautuma huo ujumbe na kujituliza.

~~~~~~~~~~~~~~~

Hapo Colins alikuwa akifikiria kwa haraka akijiweka kwenye viatu vya Kemi, Kasa, ndugu wa Jelini, kila mmoja wapo na kutaka kuwa hatua nyingi mbele ya kila mtu. Kwa ndugu wa Jelini alihakikisha anawatoa macho na akili zao kwake kabisa wabakiwe wakimfikiria Kemi na Love tu.

Halafu kwa Kemi, alifikiria kwa muda huo atakuwa anapanga kutoroka nchi. Akamuwahi kusambaza zile video zote kwenye vyombo vya usalama. Halafu kwenye balozi zile kubwa, zaidi Uingereza alipokuwepo mama yake, akatuma kwa siri angalizo la Kemi Kasa na kuunganisha na zile video akimsema ni mtu hatari, aangaliwe anafikiria kukimbia nchini kwake baada ya kufanya jaribio la mauaji. Akasambaza picha zake zote kwenye mitandao ya kiusalama kwa wazi kabisa. Yaani kile alichomwambia Kevin angemfanyia, basi akafanyia dada yake.

Akawa amemuwahi yeye hata na baba yake kama angefikiria kumtorosha nchini. Kwamba tayari Kemi akawa amemfunga kifungo cha nje cha nchini hata kabla kesi yake haijatajwa.

Alikuwa na hasira na Love naye, yeye aliomba Mungu asije akafa kabla hajamfikia. Alishampigia mahesabu. Alihakikisha anamuweka kwenye nafasi zote. Alishaanza kuhisi kwa lile tukio moja walilosaidiana na Kemi pale, wanaweza kabisa kujitetea, zaidi Love akashinda. Lakini hata hapo alijiapia kumtenda vibaya sana. “Kicheko alichocheka leo, hakika ndio cha mwisho katika maisha yake hapa duniani.” Akajiapia Colins kadiri alivyomfikiria Love.

Kwamba hata akishinda kesi, kwa kosa la jaribio lakutaka kuua, alinuia kumuadhabu vilivyo huko uraiani. Akabaki akiweka mikakati yake taratibu na kwa akili sana bila ya kuacha hata punje ya kuhisiwa kama ni yeye.

Kujihami Kwa Kila Mmoja.

Mmiliki wa Hoteli.

Wakiwa wametaharuki na ile video ya pili, akawafuata yule mmiliki wa hoteli. Kama alivyoambiwa na Colins, salamu ya kwanza akapiga kwa kilugha. Hapo akapata attension ya mama Jema na dada zake. Akaendeleza kikwao akiwapa pole kwa kuwashika watu wote mikono kwa heshima sana. Wakabaki wakijiuliza ni nani!

Upande wa kina Ezra wakadhania pengine ni mjomba! Kwanza alizungumza lugha ya kwao na kusalimia kwa ukaribu haswa kama aliyeguswa na tukio! Lakini kina mama Jema wao wakabaki hawajui ni nani! Wakabaki wamekodoa macho.

“Nimekuja kumwangalia Jelini kama mteja wangu aliyedhuriwa kwenye hoteli yangu.” Hapo wakakaa sawa. Akaendelea kwa haraka kabla hawajamuingilia. “Tumekamata tukio zima, hapa nimetoka polisi kufungua kesi, zaidi kutaka wasichana wawili tulio waona kwenye video wakamatwe. Kuhakikisha kwanza hawatamdhuru tena mtu mwingine na waadhibiwe kwa hiki walichomfanyia Jelini. Sitatulia mpaka hiki walichofanyia Jelini, nikiwekee kikomo na wahalifu watiwe nguvuni.”

“Yule muhudumu aliyekuwa akimuhudumia Jelini ameshahojiwa kwa undani sana, na taarifa zake zimetunzwa kwa sir...” “Yeye amesemaje?” James akauliza. “Naomba kwa heshima ya Jelini na kwa haki yake, nisitoe ushahidi wake hapa hadharani. Siku hizi teknolojia imekwenda mbali sana. Sitaki mtu asikie haya na kurikodi halafu kusambaza na kuwafanya adui kujipanga dhidi ya uhalifu wao.”

“Hata yeye atafichwa kabisa hata jina lake litahifadhiwa mpaka uchunguzi mzima utakapo kamilika. Hakuna atakayezungumza naye wala kumfikia kwa wema au hata ubaya kutaka kumuhonga au hata kumdhuru ili kuficha ushahidi. Atakaa mafichoni mpaka Jelini apate haki yake kwa kukamilisha uchunguzi mzima. ”

“Hii nawaambia tu nyinyi kwa heshima ya hawa dada zangu tu.” Akimaanisha mama Jema na dada zake. Undugu tayari! “Lakini hata polisi nimeomba wafiche kabisa taarifa za yule muhudumu mtu hatajua alipo ila mimi tu, mpaka kesi itakapokamilika. Ila kila atakapohitajika katikati ya uchunguzi, watawasiliana na mimi, na mimi nitahakikisha anafika kituo cha usalama kutoa ushirikiano, na kurudi mafichoni.” Akaongea mengi akichanganya na kilugha akiweka undugu mpaka akafanikiwa kupata mioyo yao. Kwa hakika alikuwa upande wao, na alionekana kutetea Jelini vilivyo.

“Hapa tunapozungumza nimeshatafuta mwanasheria wakumtetea Jelini. Ni pesa nyingi, lakini pia niwe tu muwazi, nataka kuhakikisha Jelini anapata haki yake na kuweka kikomo kwa yeyote anayefikiria kufanya jambo kama hili pale kwenye eneo langu la biashara. Sitatulia mpaka hili likamilike. Hata kama wao watakuwa na pesa kiasi gani, na mimi nitapambana kama hivi binti yangu Jelini anavyopambania uhai wake, kufa na kupona.” Mama Jema akampa kabisa mkono akimshukuru. Ndipo sasa akataka kujua taarifa za mgonjwa huku akiahidi kulipia garama zote.

Penzi Lililogoma Kutoka Moyoni.

Isivyo ya kawaida, hakuna aliyetegemea, wakashangaa Kasa na askari wawili nao wamefika hapo. Waliomfahamu wakabaki wamepigwa na butwaa na yeye akawahi kabla hawajatoka kwenye ile hali. Akamsogelea mama Jema.

“Najua mimi ni mtu wa mwisho kabisa ungetamani kuniona usiku huu. Lakini mama Jema, nipo hapa kwa ajili ya Jelini. Nimeshajua ameanza kutapika damu, na hapa hapana vifaa vizuri vya kumchunguza. Wataandika vipimo, ambavyo itabidi isubiriwe kesho, tena akafanyiwe kwenye hospitali kubwa, sio hapa, kitu ambacho kitachukua muda mrefu ambao Jelini hana kwa sasa.”

“Ningeweza kujificha na kukimbia kama kina Kemi, lakini siwezi kufikiria wala kupata usingizi nikijua Jelini yu matatizoni, tena kwenye tatizo la hatari kwa kiasi hiki. Sipo hapa kwa ajili ya Kemi, nipo hapa mimi kama Alexender Kasa, nikitaka kumsaidia Jelini. Sasa basi.” Akaendelea wote wakimtizama.

Kwanza ni KASA. Vile tu alivyosimama pale, alivyopendeza usiku huo, msafi, mavazi si ya kiofisi, track suit nyeupe haswa yenye zipu na nembo nyeusi ya under armour. Akavaa sneakers nzuri nayo ni nyeupe na nyeusi, Nike safi. Harufu nzuri na safi ikaenea hapo kutangaza aghueni ya maisha. Yaani mpaka hapo tu, uwepo wake ulishaenea. Anazungumza kwa kujiamini. Halafu ametokea katikati yao, kwenye wakati mbaya kama huo! Ni anayejielewa na kujiamini tu, ndiye anayeweza kufanya alichofanya.

“Taarifa za kinachoendelea huko alipo Jelini sasahivi, wanakomsaidia, zimeshapokelewa na madaktari wanao msubiria kwenye hospitali yenye vifaa vizuri na wanao weza kumsaidia. Najua wamemtapisha sumu, lakini hata wao wanataka kujua juu ya damu inayomtoka. Hapa ninapozungumza na wewe, gari ya hospitali ipo hapo nje, na kama nilivyo kwambia, nina madaktari wapo tayari wanamsubiria yeye tu. Akifika tu huko, apewe huduma nzuri, na ya hali ya juu, kwa haraka.”

“Sidharau kile anachofanyiwa hapa, ila mkumbuke mlimleta hapa kwa dharula, inamaana usiku huu anakutana na daktari wa zamu ambaye wagonjwa wengi wanamtegemea yeye daktari mmoja. Lakini kule anasubiriwa na zaidi ya madaktari wawili, kumshugulikia tu yeye. Nakuomba mama Jema, niruhusu kumtoa hapa Jelini, akatibiwe ndipo adhabu zangu zote zinifuate baada ya hapa.”

“Na nakuhakikishia, akifikishwa tu kule, nikahakikisha wale madaktari wamemshika, nitaondoka kabisa wala hutapata shida ya kuiona sura yangu. Nia nikutaka Jelini si atoke tu kwenye hii hali, bali kutibu madhara ya ndani zaidi. Sio wamruhusu kesho au usiku huu sababu wamefanikiwa kumtoa sumu, kisha kuachwa na madhara makubwa zaidi ndani yake! Hapana. Nataka wamuangalie na wajue jinsi ya kumsaidia. Wakisema amepona, iwe kweli amepona.”

“Na msihofie juu ya garama. Kila kitu kimeshalipiwa. Ninachokuomba ni ruhusa ya Jelini akatibie vizuri na kwa haraka. Ni hilo tu. Tafadhali tuokoe muda ambao umeshapotezwa.” Mama Jema akabaki akimtizama Kasa. Wengine wote kimya wamepigwa na butwaa. Wamemkodolea macho Kasa kama wanaojiuliza gati hizo anapata wapi!

~~~~~~~~~~~~~~~

USIKU WA HEKAHEKA.

WAKATI JELINI AKIPAMBANIA UHAI WAKE, MENGI YALIKUWA YAKIENDELEA.

 KILA MMOJA KWA WAKATI WAKE NA SABABU ZAKE.

INAENDELEA.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment