Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 4. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 4.

Ubishani ukaendelea mpaka ikabidi Chris aingilie. “Naona hatufiki popote. Lazima kutafuta ukweli mmoja ambao wote mtasimamia. Lasivyo, kwa jinsi ninavyowasikia nyinyi, kwa hakika mmeshajifunga.”

Chris akaendelea. “Kwanza kabisa nataka niwatoe paniki. Ile video haina ushahidi wa kutosha kumfunga hata mmoja wenu. Kwa sababu haijaonyesha kama Kemi uliweka kitu pale. Unaweza hata sema ulikuwa ukifukunza inzi au mdudu, tutaamua pamoja.” Hapo akampata Kemi. Kidogo akatulia na kuanza kusikiliza.

“Mnaweza sema mlivutiwa na ile juisi ndio maana mkamsimamisha.” “Mara zote mbili?!” “Nisikilize Love. Uzuri hakuna ushahidi wa maneno. Ni maneno yenu nyinyi dhidi ya yakwake. Nyinyi mpo wawili. Mkijipanga vizuri, mkaelewana, na kuweka tofauti zenu pembeni, mnaweza kushinda kabisa na ndipo kuweka madai yenu kwa ile hoteli. Badala yake mkaibuka mamilionea, mchana kweupeee.” Hapo ndipo wote wakatulia. Akawa ameshapata mioyo yao.

“Tunakwenda polisi sisi wenyewe hata kabla hamjafuatwa. Mnajisalimisha na tunafungua mashitaka. Tunashitaki ile hoteli kwa kusambaza taarifa zenu hadharani, mkiwa mmepaamini pale kama sehemu salama ya starehe. Wamewachafulia jina, na kuweka maisha yenu hatarini kwa jamii, inayowatizama sasa kama nyinyi ni wauuwaji.” Chris akawapanga vilivyo.

Mpaka wanatoka hapo, ni kitu kimoja. Wanazungumza ukweli ambao kwanza wameshauamini. Wamejipanga vilivyo. Kemi huyu badala ya kukimbia nchi, anadalili za kulipwa fidia! Stori ikabadilika. Tumaini jipya. Ujasiri ukarudi. Hofu ikaondolewa.

Kuliko Unguzwa Mpini, Kukaachwa Jembe Lina Moto Unaokataa Kupoa.

Colins yeye alishindwa kulala. Alirudi nyumbani kwao, akaingia chumbani kwake na kurudia kuitizama ile video tena taratibu akijiweka upande wa Love na Kemi vile ambavyo wanaweza kujitetea. Mwishoe na yeye Colins akafikia kufikiria kama vile Chris.

Ukweli hapakuwa na ushahidi wa kutosha wa kumfunga Kemi hata Love. Kemi alionekana kunyanyua mkono juu ya ile trei iliyokuwa imebeba glasi ya vinywaji ikiwepo na hiyo juisi ya embe aliyokunywa Jelini. Na kwa sababu ya giza hapakuonekana kama ametia kitu kwenye ile juisi. Na mbaya zaidi, ile juisi hata ilipowekwa mezani ambako alikuwa amekaa Jelini na Colins, mwangani, haikuonekana kubadilika rangi. Bado ilibakia kuwa rangi nzuri sana ya embe hapo kwenye glasi. Colins akabaki akikuna kichwa akijua wazi hawatakamatwa kwa hilo. Akaona aongeze uzito.

Kwa kutumia tena Ip adress ya Love, akaingia tena kwenye akaunti ya kampuni anakofanyia Love, na kuchota mapesa, kisha kumrushia Kemi. Ila safari hii alichota yakutosha tu ili makusudi kugutusha muhasibu siku inayofuata. Akafanya yake na kubaki akifikiria endapo hawata kamatwa, au kutiwa nguvuni na vyombo vya sheria, atawaadhibu vipi! Akabaki akifikiria.

Ujanja Kuwahi.

Wakati hayo yote yanaendelea usiku huo wenye mengi, kila mtu akijipanga kivyake, yeye Jelini bado yupo hospitalini akipambania uhai wake. Kina Kemi wakatokea kituo kikubwa cha polisi cha Oysterbay, wakisindikizwa na wakili wao pamoja na wazazi wa Love.

Wakaonyesha ile video, na hapohapo wakashitaki ile hoteli kwa kuvujisha taarifa zao wakiwa wamepaamini pale ni sehemu tulivu ya starehe, kuwa wangelindwa kama wateja, lakini sasahivi wameanikwa hadharani. Wakasema wao hawapo tena salama, jamii inawachukulia ni kama wauuaji.

Wakaeleza kuwa ile hoteli ndio inayotoa vyakula vyenye sumu, hawapo makini na vyakula pamoja na vinywaji wanavyotoa kwa wateja wao. Wakisaidiwa na wakili wao, wakatengeneza mashitaka yao kwa makini, mpaka wakafanikiwa kuandikisha kesi nzito. Ndipo wakaondoka kituo cha polisi, lakini mpaka hapo hakuna mtuhumiwa aliyekwisha kamatwa. Kila mmoja akimshitaki mwenzie.

Mpaka hapo, usiku huo kituo hicho cha polisi wakafungua kesi mbili. Mashitaka tofauti tofauti, lakini kisa kinachomlenga mtu mmoja. Jelini.

~~~~~~~~~~~~~~~

Saa kumi alfajiri ndio Love na wazazi wake wakaweza kurudi nyumbani. Hata Love aliamua kulala tu kwao. Kwanza bado alijawa hofu. Hakujiamini tena kurudi Kigamboni, ambako wakati wowote alijua Colins, kiumbe aliyekuwa akimdharau sana, gafla akageuka tishio kwake kwa namna ya ajabu sana. Akajua akiwa huko, tena peke yake, anaweza kumfikia bila shida kwa sababu ile nyumba ni kama ni ya Colins pia. Ukimya wake tokea apone, na usiku huo pia, akijua anajua alichomfanyia, ndio ukazidi kumuogopesha zaidi.

 Akaingia kwenye chumba ambacho bado kinatambulika kama ni chake hapo nyumbani kwao, na bado kilikuwa na vitu vyake, akalala hapo kupata usingizi mfupi, kuwahi majukumu ya siku inayofuata.

Kila Jambo Na Majira Yake.

Ni kweli kila kitu kina majira yake, kila jambo duniani lina wakati wake. Wakati wa kuzaliwa na wakati wa kufa; wakati wa kupanda na wakati wa kuvuna kilichopandwa; wakati wa kuua na wakati wa kuponya; wakati wa kubomoa na wakati wa kujenga; wakati wa kulia na wakati wa kucheka; wakati wa kuomboleza na wakati wa kucheza; wakati wa kutupa mawe na wakati wa kuyakusanya mawe pamoja; wakati wa kukumbatia na wakati wa kuacha kukumbatia; wakati wa kutafuta na wakati wa kupoteza; wakati wa kuhifadhi na wakati wa kutupa; wakati wa kurarua na wakati wa kushona; wakati wa kukaa kimya na wakati wa kuongea; wakati wa kupenda na wakati wa kuchukia; wakati wa vita na wakati wa amani. {Muhubiri 3:1-8}

Wakati Wa Kuua Na Wakati Wa Kuponya

Hilo andiko likatimia kwa Jelini naye. Baada ya vipimo vya kina ndipo wakajiridhisha hayupo hatarini tena. Mmoja wa daktari aliyekuwa akiongoza hayo matibabu yake, akawafuata kama aliyekuwa ametumwa kwao. Akawasogelea pale walipokuwa wamekaa. “Jelini amepelekwa kwenye chumba ambacho atapumzika. Mpaka sasahivi  alipo hayupo kwenye hatari ya kifo, na hana madhara yakudumu ya hatari yanayo mkabili.” “Unamaanisha nini, maana tuliambiwa ameanza kutapika damu!” Akawahi Ezra.

“Ametapika sana kiasi cha kukwangua koo. Na kwa jinsi alivyokuwa akitapishwa imekwangua hata tumbo pia. Muda, dawa kiasi, na vyakula sahihi hata utumbo utarudi kwenye hali ya kawaida. Ni kuepuka vyakula na vitu vyenye tindikali. Otherwise, msiwe na wasiwasi. Na bado tutamwangalia mpaka kesho. Akiendelea hivi, ataruhusiwa tu kurudi nyumbani.” Akaendela taratibu akijaribu kuwatoa hofu.

“Kama nilivyotangulia kusema, hayupo kwenye hatari ya kifo. Mnaweza kwenda kumuona, ila amelala. Amepewa dawa ya kuzuia kutapika na ya usingizi ili kumpumzisha kabisa. Ila dawa zikiisha mwilini, anaweza kuzungumza kabisa, na sisi tulizungumza naye kabla hatujamlaza.” Gafla wakamsikia mama Jema anaanza kulia. Alilia mpaka akakaa chini kabisa.

Bwana mama alilia huyo kama ambaye amepewa habari za msiba, mpaka daktari akajaribu kurudia akidhani hajaelewa. Lakini asijue ule mshituko wa kuambiwa Jelini amenyweshwa sumu, ukafunga kabisa hisia za machozi mpaka hapo ndipo alipoweza toa hofu yake.

Yaani hata alipokuwa akionyeshwa tukio zima la Jelini kule hotelini na kutegwa na Kemi mpaka kupasuka kichwa, yeye akili yake na hisia viligoma kupokea na kutafasiri zile taarifa. Yeye mawazo yakabaki kwa mwanae aliyekuwa ana karibia kufa. Yaani hata Kasa alipokuwa akizungumza naye, akili ilikuwa imekufa ganzi, hajui afikirie nini au afanye nini. Ile kumuangalia Ezra ilikuwa ni asaidie ushauri. Jema alipowahi, ikawa bora kwake.

Muda wote alikuwa kama amekufa ganzi kabisa! Kimya mpaka hapo alipoambiwa hakuna hatari tena, yaani, Mungu hakuwa tayari naye, ndipo akafunguka na kuanza kulia mpaka Jema alipomwambia waende wakamuone.

~~~~~~~~~~~~~~~

Wote wakaongozana kwenye hicho chumba, lakini alikuwa amelala hata hajui alipo. Ezra akaenda kuinama pale pembeni yake akimwangalia jinsi alivyolala pale, mwishoe na yeye akaanza kulia mpaka Junior akaenda kumtoa pale na kutoka naye nje kabisa. Mengi yalikuwa yakiendelea kichwani mwake. Alipotulia ndipo wakarudi.

 Walikaa pale mpaka wakaamua kuondoka, ila wakakubaliana mama Jema na Ezra ndio wabaki. Sasa Junior naye hawezi ondoka hapo bila Ezra. Wakajikuta wamebakia watatu. Kwa ahadi ya chochote kitakachotokea watoe taarifa kwa ndugu wote hao. Mchungaji akafanya maombi ya shukurani, ndipo wakatawanyika.

~~~~~~~~~~~~~~~

Kimya hapo chumbani kila mtu akitamani angalau afungue macho tu. Ezra alikaa pale akimsihi Mungu amtunzie huyo Jelini, akimkumbusha Mungu yeye ni yatima, na Jelini ndio kila kitu chake. Akaomba yote mpaka akasogeza kiti kabisa pale karibu ya kitanda, akamshika ule mkono ambao haukuwa na dripu. Akajikuta akirudia maombi yaleyale akimkumbusha Mungu kana kwamba anatatizo la kusahau! Mwishoe na yeye akapitiwa na usingizi. Chumba kizima wakalala kwa uchovu na hofu ya massa machache yaliyopita.

~~~~~~~~~~~~~~~

Majira ya saa 12 alfajiri, wakati mchungaji, mkewe na Emelda wameingia hapo na nesi naye alikuwa ameingia kuongeza dripu ingine iliyokuwa ikienda taratibu. Maana alishawekewa nyingine kwa haraka. Hizo zilikuwa zakumpa tu nguvu. Kwa hiyo zilikuwa zikienda taratibu.

Wakati wanaelezea hali yake kwa waliorudi asubuhi hiyo na kifungua kinywa kwa wote, maana mama mchungaji ni kama alirudi kwake kupika tu. Aligeuza na kurudi hospitalini hapo akiwa na Emelda pia na vyakula vingi tu.  

Wakati wakitoa taarifa zake, Jelini akawa anatoka usingizini. Akawatizama kwa muda kama ambaye anajaribu kuelewa. Wote kimya wakawa na wao kama wamepigwa na butwaa kumuona amefungua macho. Kisha  wakamuona kama amegutuka, akaanza taratibu kuficha mkono wenye pete ile ya uchumba, ambao ndio una sindano ya dripu.

“Huo mkono una dripu Jelini! Acha kujiumiza zaidi.” Junior akamuwahi. “Nilikwenda kuwekana sawa na Colins. Sijafanya jambo baya.” Akajitetea huku akificha mkono, kwa sauti iliyojaa usingizi. Ezra akamuwahi. “Naomba utulie. Mimi mwenyewe sithubutu kutoa hiyo pete kidoleni mwako Jelini. Ni maombi yangu isiwahi kutoka. Nipe huo mkono.” Ezra akamvuta huo mkono taratibu.

“Sikufanya jambo baya!” “Najua Jelini. Hakika wewe ni muujiza wangu. Namshukuru Mungu amenihurumia na kunirudishia wewe.” Akaubusu ule mkono kwa muda mrefu akiwa amefunga macho, wakamuona machozi yakitoka. Jelini akamuhurumia.

“Pole Ezra. Najua nimekushitua. Lakini sikuwa na jinsi ingine. Tumbo lilivyoanza tu kuvuruga, na kwa kuwa nilishamuona pale Kemi na Love, nahisi kama Mungu tu, nikajua kuna kitu wameniwekea. Nikakimbia na kukupigia simu.” “Na ndio pona yako. Ungechelewa tu, usingepona.” Junior akajibu yeye wakati Ezra akijifuta machozi na kujaribu kutulia.

 Wakamsimulia na kumuonyesha ile video. Jelini akashangaa sana, ndipo sasa wakamuonyesha ile ya ofisini kwa Kasa, alishituka sana. “Mmepata wapi hizi video!?” “Kwanza mpaka sasahivi zimeenea mtandaoni! Kazi ya Colins.” Akamwangalia mama yake. “Mimi sijafanya jambo baya, mama. Nilikwenda kumalizana naye tu. Mimi natulia na Ezra.” Akawa akijitetea kwa mama yake akitokwa machozi taratibu. Mama Jema akaanza kulia tena. Ila safari hii kwa kwikwi, mpaka Jelini akamuhurumia na kuzidi kulia. Alilia mama Jema mpaka akatoka hapo chumbani. Mama mchungaji akamfuata.

Baada ya muda wakarudi akiwa ametulia. “Pole mama. Pole sana.” Mchungaji akamwambia mama Jema. Kisha akamsogelea na Jelini aliyekuwa akibembelezwa na Ezra. “Pole sana Jelini, binti yangu. Pole sana.” Akamuongelesha kwa upendo, kama baba kwa binti yake kweli.

“Ningekushika mkono ila mmoja ndio huo una sindano na mwingine umeshikiliwa kana kwamba utakimbia!” Wote ndio wakaangalia na kuanza kucheka. “Acha nishike baba yangu. Niliingiwa na hofu! Hakika sijawahi ogopa vile maishani. Sikujua kama…” Akashindwa kuendelea, wakamuona anapambana na machozi.

“Nilijua. Pole sana Ezra. Pole. Lakini leo wote tuna sababu ya kumshukuru Mungu. Jelini amepona mauti. Mungu akipenda leo atalala nyumbani.” “Nilitaka niombe angalau niende naye nyumbani. Nishinde naye mpaka mama yake akiwa anatoka kazini, ndio nimrudishe.” “Naomba nizungumze na nyinyi wawili hapo nje.” Junior na Ezra wakaangaliana kama wanaoulizana. ‘Tumefanya nini tena!’ Mchungaji akawaona. “Sasahivi, Junior na Ezra.” Akatangulia nje, wakamfuata.

~~~~~~~~~~~~~~~

“Kuna nini tena!?” “Wazo la kwenda kushinda na Jelini, nyumbani kwako, nyinyi wawili, kipindi kama hiki, HAPANA.” Wote wakabaki wakimwangalia kwa mshangao. “Unanisikia Junior na Ezra?” “Kwa nini?!” “Nisikilize Ezra. Jana ulikuwa ukilia, ukijilaumu jinsi mlivyoachana mara ya mwisho na Jelini. Ukawa ukilia ukisema wewe ndio umemsababisha mpaka akaenda kwa Colins. Ungezungumza naye vizuri, ungemuongoza vizuri yasingempata hayo yote. Si ndivyo?” “Wala sipingi!”

“Ewaaah! Sasa katika hali hiyo, na yeye anajilaumu kwa yake, mkajikute mpo wawili tu, baada ya kuombana msamaha, furaha ya kupona Jelini! Unafikiri ni nini kinafuata?” “Baba!?” Ezra akashangaa sana. “Kwani unafikiri faida moja wapo za mpishano ndani ya ndoa ni nini?” Kimya. “Kwenye kupatana. Mkifanikiwa mkafikia sehemu nzuri kila mmoja akakubali yaishe msameheane! Mtakuja kuniambia.” Junior akaanza kucheka akiwa ameshaelewa.

“Mimi nipo makini. Siwezi anguka dhambini.” Ezra akapinga. “Maana wewe mwenzetu si mwanadamu kama sisi? Maana wote tumeamriwa kuikimbia zinaa. Halafu wewe ndio unataka kuikimbilia!? Hapana Ezra. Huyu binti anakwenda kuugulia kwao. Wewe utaenda kumtembelea. TENA baada ya kazi. Huwezi kuacha kazi sababu ya kupendana. Hilo hapana.” “Sasa kipindi hiki si ndio ananihitaji!? Nisipokuwepo kipindi kama hiki, si ndio kutojali huko??”

“Nisikilize Ezra. Hapo ulipo upo kwenye kuweka msingi mgumu sana wa hatima yako na Jelini. Ukitetereka tu, ukaruhusu nahisia zikuongoze, ukatoa mwanya wa kosa dogo tu, ambalo sasahivi unaweza kulitolea sababu ya kwa nini ulifanya, na kujipa amani kwenye hilo. Maana sasahivi si jamii inajua Jelini ni kama mkeo! Una baraka za wazazi! Halafu utajiambia si nitamuoa tu! Si ni kama au atakuwa kama mke wangu tu! Utaruhusu hili na lile. Na kweli Mungu atasaidia, mtaoana, kama hapajapatikanika na mimba kabla ya ndoa. Ambayo si tatizo sanaaaa. Maana sisi si tunaamini nguvu ya toba! Basi tunaamini tukitubu, tutasamehewa. Mtatubu, tutabariki ndoa yenye mtoto tayari, mtaanza maisha.”

“Lakini kumbuka, mlishafungua mlango wa kosa tokea mwanzo. Unajua vipi mkija kujaribiwa huko baadaye, na watu wengine, hamtarudia kosa?” “Baba!??”

“Unakataa nini Ezra, mwanangu!? Huoni msingi wa anguko kubwa sana wa ndoa nyingi, ila hawataki tu kuliweka wazi. Kama ulianguka na yeye, mkapona. Kwa sababu yeyote ile mtakayoichagua nyinyi, unajuaje kama hapo ndio itakuwa mwisho wa kujaribiwa kwenu? Tuseme wewe utaishia kuzini na yeye tu, kisha kumuoa. Unajuaje kama yeye atakapokuja kujaribiwa tena, na mwanaume mwingine je? Hata akiwa ameshakuzalia watoto wa tatu! Akakumbuka alikosea na wewe, ikawa SAWA. Sasa kwa nini asikosee huko na mwanaume mwingine tena na kutubu? Kwa sababu yeyote ile atakayochagua tena, kama mlivyofanya naye.” Wivu tayari kwa Ezra.

“Si Mungu alisamehe uzinzi wa kwanza uliofanya naye! Sasa huyohuyo Mungu atashindwa vipi kusamehe ushareti wa baadaye? Tena na yeye akatafutia sababu nzuri sana, ambayo mimi na wewe hapa tuliposimama, sasahivi, hatuna, kwa kuwa tunampenda Jelini, tunajiambia hataweza kufanya, kwa sababu pia bado hamjaingia kwenye ndoa. Hamjajua changamoto zenu za ndoa zitakazowakabili.”

“Nakuhakikishia Ezra, kwa aina ya mwanamke uliye naye, anavyogombaniwa na kusubiriwa huko nje, kupokelewa kwa mikono yote miwili, utakapo mfundisha kukosea sasahivi hata mara moja tu, shetani atarudi baadaye na mfano wako wewe mwenyewe. Utakuja kukumbuka haya ninayokwambia kama usipokimbia sasa.”

“Tena mbaya zaidi, Jelini anakuangalia sana wewe Ezra, kama mfano wa kuiga. Usifikiri ni jambo dogo kukupigia wewe simu wa kwanza akiwa kwenye hatari ya kifo na hamkuwa mmeachana vizuri. Ana imani na wewe.” “Kabisa Junior!” Mzee akaafiki.

“Na usifikiri pia ni jambo dogo kwa Colins tuliyemsikia ni mkorofi hakubaligi kushindwa linapofika swala la Jelini, eti leo anakutambua wewe! Tena kwaheshima kwa kiasi hiki! Sio kitu kidogo Ezra. Mimi mzee amenifanya nifikirie, nimeona ni bahati imekujia mara moja. Upo na nafasi nzuri sana ya kujenga mke utakayefaidi matunda yake kwa mpaka kifo kitakapo watenganisha au kuweka msingi mbovu, nyumba ije iwaangukie baadaye. Tujikaze tuoe mapema, kufupisha haya maisha ya kukaa mbalimbali.” Wakamuona anavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu.

“Upo sawa?” “Basi naomba leo nikamsaidie huko kwao! Angalau tu nikae naye. Kesho narudi kazini. Nakuahidi baba yangu. Na nimeelewa. Nitaongeza umakini lakini angalau leo niwe naye sehemu itakayonilinda na mimi, lasivyo sitaweza fikiria popote nitakapokuwa bila ya leo kuwa naye na kuwekana naye sawa. Kwanza namuona bado ana hofu akihisi nimemkasirikia kwa kuonana na Colins bila ya kunitaarifu.” “Nimemuona anavyohofia utamuacha. Anaficha pete kabisa!” Junior akaongeza.

“Huyu binti ameamua kutulia na wewe Ezra. Hakikisha unaomba hekima jinsi ya kumuongoza.” “Na namuona si mbishi na ni kama amekubali Ezra amuongoze na kutaka watu wajue yupo chini ya Ezra. Hata Colins alimwambia tokea tupo njiani. Unakumbuka?” “Nakumbuka ndio maana najilaumu. Niliruhusu wivu ukanifanya nishindwe kufikiria. Nitaongeza umakini.” Mzee akaridhika, akajua somo limeeleweka.

“Sasa jioni mama yenu ameamua kuzungumza na mama Jema, tufanye ibada ya shukurani pale kwao. Sisi kama familia namaanisha wakiwepo na wale mama zao wengine. Na sisi ndio tutaleta vyakula na vinywaji.” “Nashukuru mzee wangu. Asante.” Wakataniana kidogo ndipo wakarudi ndani.

~~~~~~~~~~~~~~~

Mipango ikakaa sawa. Mama mchungaji akamruhusu mama Jema arudi nyumbani angalau aoge na kumpumzika. “Huyu atatolewa, wala usiwe na wasiwasi, na sisi wenyewe tutamrudisha nyumbani. Naomba ukapumzike.” “Na kumwangalia Jeremy. Nimemwambia hata shule asiende leo. Yupo kwa Jema. Maadamu unanipokea hapa, acha nikamchukue, nimwandae aende shule. Asikose shule. Ila kukiwa na chochote, tafadhali niambieni. Msiache, hata kwa kidogo vipi.” “Wewe usiwe na wasiwasi. Nitabaki hapa mimi mwenyewe.” Mama Jema akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~

Nani Atalipa Kwa Kilichompata Jelini Ikiwa Wahusika Wamekana tuhuma zao? Na Tayari Wana Mwanasheria Mzuri Anaye wahakikishia Si Ushindi Tu, Bali Kuibuka Hata Mamilionea!

INAENDELEA.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment