Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 5. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 5.

Ezra akajisogeza tena kwa Jelini. “Nakupenda Jelini.” Akajikuta anaongea hapohapo mbele ya wazazi wake. Jelini akaanza kulia. “Ningekwambia kama nakwenda kukutana na Colins?” Ikawa kama anauliza. “Ndiyo Jelini!” Ezra akamjibu kwa upendo huku amemshika mkono akimbembeleza, wengine wakabaki hawajui watoke au wabaki!

“Nilijua ningeenda, nikamalizana naye kwa amani, halafu nikuletee tu habari njema. Ulikuwa umekasirika Ezra! Vile ambavyo sikuwa nimekwambia juu ya jumbe zake. Nikapaniki. Nikajua utanichoka na matatizo yangu, nikaona bora nirekebishe kwanza ndio nikutafute tena.”

“Naomba wakati mwingine, tutatue matatizo yetu pamoja. Hata kama yanatisha vipi, tufanye pamoja. Umoja wetu ndio iwe nguvu yetu, adui hatatushinda. Ila tukitengana, vita yetu itakua ngumu.” “Nimekosa Ezra. Usikasirike.” “Na mimi nilikosea tokea, mwanzo. Niliruhusu wivu unitawale. Ila wakati mwingine nitafanya vizuri zaidi. Samahani.” Akambusu na mkono kabisa kisha akaanza kumfuta machozi.

“Sasahivi usione tena wivu. Hata Colins nimemwambia nabaki na wewe tu, hata iweje. Kwa hiyo usi..” Junior akaanza kucheka kwa sauti ya chini bila kutarajia. “Mwaya Junior!” Jelini akalalamika. “Samahani Ezra, samahani sana. Hapo Nimeshindwa kujizuia.” Wote wakajikuta wakicheka.

“Sasa unacheka nini wakati mwenzio nipo matatizoni!” “Hivyo ulivyosema juu ya wivu! Hakuna mtu anajiambia naanza wivu au naacha! Halafu wewe umejitafutia matatizo Jelini! Tena wewe mwenyewe.” “Nyie Junior! Ujue mimi nilijua wewe ni mtu wangu!” “Sana tu. Na uwe unalikumbuka hilo wakati wote. Usiwe unasahau.” Junior akaendelea.

“Ulitakiwa kusema tokea mwanzo, juu ya jumbe na kusimamia msimamo wako wa kwanza, ule niliokusifia. Ungebaki salama. Sasa shetani ameona umejipinga wewe mwenyewe, ndio akapata mwanya.” “Si ndio nilipokosea nikapaniki!” “Hata ukipaniki, wewe sema. Usitafute suluhu ukiwa na paniki, tena peke yako. Tutakupoteza, utuache na majonzi daima. Wenzio tunakuhitaji Jelini! Kumbuka ulivyopooza kule Songea?” Jelini akanyamaza.

“Wote tulipoa sababu wewe ulipoa. Ndio ujue wewe ni kiungo muhimu sana kwetu. Ukiathirika kwa chochote, ujue umetuathiri na sisi wote. Ndio maana unaona asubuhi hii tuliyopanga twende kazini, kutunza siku za fungate, tupo hapa. Na bado wamekuumiza!” “Samahanini. Nilikosea na naahidi kuwa mwangalifu zaidi.”

Huyo Jelini anazungumza hapo, hajui hekaheka ya usiku uliopita. Hajui hata kama alishahamishwa hospitali na Kasa. Kwamba wote hapo wanamfahamu milionea Kasa, na amepigania uhai wake, pamoja na mtaalamu Colins. Usiku huo mchungaji na mkewe wakatambulishwa ma ex wa Jelini kila mmoja na hekaheka yake.

Anayetaka Usawa Mwisho Wake Uchawi.

Ndicho kilichompata Raza. Ilikuwa mapema sana wakati Raza, anti lake Jelini akipokea simu ya Kasa. Akashangaa sana. Akapokea kwa haraka. Ni Kasa, anayehonga pesa ya kubadili maisha! “Nataka uende hospitalini sasahivi. Umepelekee Jelini maua na chocolate.” Raza akashituka sana. Hakuwahi hata kuropoka jina la Jelini kwa Kasa, na hata siku moja hawakuwahi kumzungumzia Jelini.

“Unanielewa?” Akauliza kwa sauti ya ukali na amri. “Mbona hamna hata salamu!? Unajuaje kama na mimi pengine nipo hospitalini?” Akamtibua Kasa zaidi, akitaka kujifananisha na Jelini. “Usinipotezee muda Raza. Nina usingizi sijalala usiku kuchwa. Leo sina muda wa kudanganyana. NATAKA uende sasahivi, na unijulishe anavyoendelea yeye. Si vile anavyosema daktari. Hapana. Kwa kuwa wewe ni mtu wako wa karibu, nataka uzungumze naye vizuri, umsikie ili ujue anavyoendelea mpaka anavyojisikia nafsini kwake na unirudishie majibu yakueleweka kwa haraka, ili niweze kufikiria na kufanya kazi.” Raza akashangazwa, asiamini.

“Sasa wewe unafikiri Jelini ataniambia mimi la rohoni?! Kwani mimi kungwi wake?” Akawa kidogo amekasirika, akajikuta anazungumza na Kasa kama yeye na si kama alivyofundishwa na Jelini. Lugha ya kiustarabu.

“Yeye si ndiye aliyekufundisha jinsi ya kuwa na mimi mpaka kitandani?” Raza akashituka karibu atupe simu. Akashindwa kabisa kujibu. “Usifikiri mimi ni mjinga. Uwezo mkubwa wa kufikiria ndio umenifikisha hapa nilipo. Ila nasikitika tu, ulinikuta kipindi cha upweke, nikakufumbia macho mpaka nilipolala na wewe ndio nikagundua nimelala na Jelini kupitia wewe. Nikataka kukuadhibu vibaya sana kwa kunidanganya.” Raza akaanza kuogopa.

“Lakini nikafikiria kwa haraka, nikagundua unafanya kila kitu alichokuelekeza Jelini, bila ya kukosea. Ukawa kile nilichokipoteza kwa Jelini. Ukazungumza lugha yake. Na ukiwa na mimi kwa sababu alikwambia nipo makini, hukosea hata mara moja kama uliyekuwa ukijikumbusha kila unapokutana na mimi. Unavaa ngozi nyingine kabisa, na kuhakikisha hakuna kosa, kila unapokuja kwangu, unahakikisha huji na simu zako.” Raza akazidi kuogopa, maana ni kweli alikuwa hashuki na simu zake garini kila anapokwenda kukutana na Kasa.

“Utulivu unaokuwa nao kwangu si wako, ni wa Jelini. Lugha unayozungumza na mimi pia si yako, ulifundishwa na Jelini. Ukamudu vizuri tu, mpaka sasahivi hapa ulipopaniki, ndio umejisahau nakujitoa makucha, ukazungumza kama wewe. Mpaka hapo umenielewa, au unataka uniudhi zaidi? Nikwambie ni kwa nini nakupa pesa yangu, tena nyingi?” Kimya.

“Ili uache kujiuza kwa wanaume wengi mpaka mawaziri na madereva wao, utulie. Niendelee kumpata Jelini kupitia wewe.” Ulikuwa ni udhalilishwaji wa hali ya juu kwa Raza, lakini aliingiwa na hofu akawa kama amekufa ganzi, ila aliweza kusikia maumivu sawia ya wivu. “Nakufahamu Raza, anti lake Jelini.” Hapo akamalizia na kummaliza vilivyo kwani ndivyo anavyoitana na Jelini.

“Ulitaka nimnunulie maua gani?” “Umnunulie maua kwani wewe ndiye unayempa au mimi!?” “Basi nielekeze vile unavyotaka, nitafanya. Maana mimi haya mambo siyajui.” Haraka sana akakumbuka nafasi yake hapo, kwa huyo mzee. Akajishusha asije haribu. “Ndio maana tokea mwanzo kama ungekuwa umenisikiliza kwa makini, nilikwambia NAKUTUMA kwa Jelini. Ukinunua wewe na kumpelekea itakuwa na maana gani! Si itakuwa ni kama wewe tu ndio umenunua?” “Samahani.” Raza hakutaka kumkorofisha kabisa Kasa.

“Tukutane nikukabidhi vitu vyote ninavyotaka umpelekee. Mimi ndiye nimenunua, wewe ni mpelekaji tu.” Kisha akaongeza kwa msisitizo. “Na Raza, kuwa makini sana unapozungumza na Jelini juu yangu. Chochote kitakachotufanya tuwe mbali zaidi na hivi tulivyo sasa, ukiwa wewe umesababisha, ujue utanikorofisha sana na hutapenda upande nitakao kuweka.” Mzee akapiga mkwara.

“Siwezi kufanya hivyo. Kwanza mwenyewe Jelini ameniambia hataki hata kujua kama ulinikubali au la. Na hataki kujua kinachoendelea kati yetu. Amenionya kabisa tusikuzungumzie tena. Kinachoendelea kati yetu, hataki kabisa kujua. Na amenionya hata nisiwaambie watu kama yeye ndio amet…” “Hayo ni ya wakati mwingine. Sasahivi nataka utoke kitandani, ukamuone.” Kasa alisikika hataki kupotezwa malengo.

“Sasa akiuliza nimejuaje alipo na kama ni mgonjwa?” “Wewe hujapata habari zake kuwa amenyweshwa sumu?” Akashituka sana. “Hapana! Jana nilibakisha simu moja tu ambayo ni ya mambo maalumu. Na niliwahi kufunga hii saluni mpya. Halafu kwenye hii saluni mpya ninayokuwepo muda wote wateja wangu si kama wale wa kule. Ni kina dada wanao jiheshimu. Wakija pale hawana maneno mengi na hata wafanyakazi wangu wa huku hawana maneno maneno. Kwa hiyo sipati yanayoendelea kwa haraka.” Akaongea kwa huruma.

“Sitaki tugombane Kasa. Wewe nitume utakapo, nitafanya. Umenisaidia maisha yangu, angalau sasahivi nalala nikiwa nimetulia nina uhakika wa wanangu kwenda shule bila mahangaiko ya zamani. Sikupenda yale maisha, wala sikuchagua. Ila mume wangu alinitaliki na kuniachia watoto wote na mimi sina wazazi wa kunisaidia. Ikabidi kupambana kwa kila namna ili wanangu wasome na angalau waweze kupata hata mlo. Lakini huyo anayekwambia habari zangu, kama ni mkweli kwako, atakwambia nimetulia. Nimeachana na wanaume karibia wote, nime…” “Kuwa makini sana na unachotaka kuzungumza baada ya hapo. Maana uongo wa namna yeyote ile sitakusamehe Raza, haswa kwa siku ya leo ambayo Jelini yupo hospitalini. Umenielewa?”

“Lakini kumbuka na mimi ni binadamu Kasa! Nipo mpweke kama wewe ulivyosema. Hujawahi nifungulia moyo wako kama Jelini alivyokuwa akiniambia unavyokuwa ukiwa naye. Unaniita nyumba za kulala wageni, hujawahi nikaribisha kwako hata mara moja! Tena unaniita mara chache sana, halafu ni pale unapopenda wewe. Jelini aliniambia huwa hutumii kondumu kabisa, kwanza hupendi, lakini kwangu unakua mkali kabisa kwenye swala la kondomu, tena unanipima UKIMWI kila tukikutana! Unafanya mapenzi na mimi vile unavyochagua wewe, kwa staili zako wewe tu, hutaki kabisa na mimi nifanye kwa uhuru wangu!” Akalalamika ila kwa heshima.

“Hatuzungumzi Kasa! Nakujua kupitia Jelini! Tena kwangu haupo hata nusu ya alichoniambia Jelini! Mpaka nadhania amenidanganya! Hujataka hata kunifahamu mimi moja kwa moja ila kupitia watu wanao kuletea taarifa zangu! Na mimi ni binadamu Kasa. Napendwa kujaliwa.” “Wewe si kama Jelini. Jelini alinipenda mimi kama Kasa. Ni mwanadamu pekee anayenifahamu mimi, na hajawahi niomba pesa hata mara moja ila kunitaka mimi kama mimi.” Raza akashangaa sana, asiamini.

“Lakini wewe ulikuja kwangu kwa nia moja tu. PESA. Na ndizo ninazokupa kila mara unaponiomba. Si kweli?” “Na nakushukuru kwa hilo lakini…” “Tafadhali fanya haraka ukamuone Jelini hospitalini. Hayo mambo mengine unayotaka kuanzisha sasahivi, sina muda nayo. Wewe upo kwangu kama wengine tu. Kutaka kunitumia. Usinidanganye.”

“Kujibu swali lako, ukifika hospitalini, wewe mwambie Jelini umeona mtandaoni ndio umeamua kwenda kumuona. Nakutumia sasahivi video yake ya jana usiku ili ujue utakacho zungumza naye. Kisha mpe pole. Jelini hana makuu, ukimuendea vizuri, hatakuhoji kama hivi. Anachotaka maishani ni kupendwa na kujaliwa tu. Kufika kwako pale, hakutazua maswali ila furaha. Sasa usinicheleweshe. Kila kitu nimeshaandaa. Tukutane upeleke.” “Natoka sasahivi.” Simu ikakatwa. Raza akahema kwa nguvu huku akijaribu kutulia maana alikuwa akitetemeka kwa hofu, hasira na wivu juu.

Wakati Wa Kutafuta Na Wakati Wa Kupoteza.

 Alimkuta Jelini amelala usingizi mzito. Chumba kimetulia kweli. Alibakia hapo na mama mchungaji tu. Wengine wote waliondoka. Emelda alikuwa na ugeni nyumbani. Lazima arudi, asiwaache peke yao na mama yake mgonjwa. Ndio mchungaji akarudi naye nyumbani. Hao mapacha ndio walilala hapo, ikabidi warudi nyumbani kujisafi, na kukimbilia kazini kwani waliambiwa Jelini angelala siku nzima. Hapakuwa na maana ya kushinda naye.

“We Jelini?” Akamuamsha kiafande. Jelini akashituka kutoka usingizini. “Anti, kwema!?” Ikabidi amuulize kwani hapakuwa na tabasamu na jinsi alivyomuamsha pia haikuwa kawaida yao. “Nikuulize wewe uliyelala hospitalini!” Akajibu mpaka mama mchungaji akaweka kila kitu pembeni ya kochi na kubaki akiwatizama na kusikiliza.

Jelini akabaki kimya. “Na maua yako pamoja na chokleti, sijui pipi hivyo hapo. Usijesema hujapokea kutoka kwangu, ukadhania ni mtu mwingine ameleta.” Jelini akageuka kuangalia. “Kwamba huamini au?” “Kwema!? Maana naona umekuja kuniona inakua kama umelazimishwa!?”

“Huna shukurani wewe! Ulitaka nikufanyie nini!? Nimekuja kukuona halafu unanipa maneno ya kejeli? Umenigeuza mimi mtumwa wako! Umeniingiza mahali ulipojua sitapendwa ila ukaniuza ili nikafanywe mimi mtumwa! Sina ninachofanya nikakufikia! Eti leo naambiwa kila kitu nafanyiwa kwa sababu anakupata wewe kupitia mimi!”

“Na wewe ukanifanyia kusudi. Ukanifundisha nikawe kile ulichokuwa wewe, ili yule bwana abakie akikuwaza wewe tu. Umeniuzia mbuzi kwenye gunia, ukiniambia anapenda wanawake aina yetu. Nifanye kama ulivyonielekeza! Matokeo yake ukanifunga kwa uongo! Mwanaume hanioni mimi, anakuona wewe tu! Hanijui mimi na mautundu yangu, kwa sababu ulinidanganya nikufuatishe wewe, ili abakiwe na wewe tu.”

“Na kweli umefanikiwa! Mimi nilikuona mtoto mzuri, kumbe mjanja kuliko magumegume ya mjini! Umenitia kitanzi shingoni, mimi ndiye ninayeteseka, mwenzangu unakula starehe tu. Natumwa kwako kama mtumwa! Tena kwa kuamrishwa! Kwa kipi mno?” Jelini kimya akimsikiliza.

“Nikadhani nimefua dafu kumbe koroma!” Akaongea mengi akilalamikia pia kutokukaribishwa nyumbani kwa Kasa, na mengine mengi. Jelini na mama mchungaji kimya wakisikiliza. Akaongea kwa jazba mpaka akaanza kutulia. Raha ya ugomvi, mgombane. Sasa hakupata uungwaji mkono, akaanza kupoa.

Alipotulia Jelini akamuuliza. “Unakumbuka tokea mwanzo nakuja pale saluni kwako kwa zamani, ukawa unaniunganishia kwa wanaume wenye pesa, jibu nililokuwa nikikupa?” Raza kimya. “Eti anti? Sio kwamba nilikwambia mimi nataka wangu wa peke yangu, kuchangia siwezi?” “Sasa kwa nini mimi ukaenda kunitega?”

“Kwamba umesahau gafla ua la? Si wewe ulikuwa ukinishangaa kwa nini namuacha Kasa, nakupa wewe kwa sababu ulizoita za kitoto? Nikakwambia namuacha, na mihela yake yote, natafuta wangu wa peke yangu. Ukanicheka sana. Nikakupa Kasa na maangalizo yake. Sikukutuma ikaishije naye. Tena nilikwambia namuacha Kasa sababu nimegundua mwanamke aliyeniambia anamuacha ili tubaki naye, hajamuacha. Nimemfumania. Unakumbuka ulinicheka sana tena ukasema wewe unamtaka Kasa kama alivyo, huna shida au hutaki wako wa peke yako kwani yeye roho! Unakumbuka maneno yako mwenyewe?”

“Sasa kwani kugeuzwa mtumwa?” “Kinacho kuliza hapo ni wivu kitu ulichonicheka nacho mimi. Umeona Kasa ameweka thamani kwangu kuliko wewe, ndicho unacholilia. WIVU. Tena ni kitu ambacho unajipinga wewe mwenyewe. Maana si kweli kama nimekuuzia mbuzi kwenye gunia! Nilikutambulisha kwa KASA, ukamkimbilia na ukanishukuru sana, ukiwa umefurahishwa na hayahaya mapungufu yake ukasema ndicho kitu unata, hutaki wa peke yako ili uendelee na wanaume zako wengine. Umesahau?” Kimya.

 “Kwa hakika umenikosea sana anti, na sitaki tena mahusiano na wewe.” Hapo akashituka akajua ameharibu. “Yaani hivi ulivyonifuata hapa leo, na kunitusi mbele ya mama mkwe wangu kwa chaguzi zako mwenyewe za maisha, umeua mahusiano na mimi.” “Acha hasira anti! Nahisi ni usingizi tu.” “Basi beba maua yako na vyote ulivyoniletea, peleka kwako na mwambie Kasa, ameniudhi kupita kiasi.”

“Jelini u..” “Hapana anti. Wewe si mtu mzuri na unataka kuniharibia mwenzio kwa mwanaume ambaye mwenzio nilikuwa nahangaika kumpata, na wewe ulipokuja siku ya kuchumbiwa kwangu, kwa wakwe zangu nilikwambia. Mungu amenipa haja ya moyo wangu, roho yangu kwatu. Leo bila heshima unakuja kusema mambo ya ndani hivi mbele ya mama mkwe wangu! Nia yako nini kama si kuniharibia?”

“Sikuwa nimemuangalia vizuri. Sikujua kama ni mama mkwe wako.” “Hutanidanganya anti. Na wala usitafute mchawi. Upo hapo ulipo na Kasa, kwa kuchagua kwako wewe mwenyewe, na mimi nilikuonya tokea mwanzo, sikukuficha. Nilikwambia pesa utapata, lakini jua hutakuwa peke yako. Ukasema wewe mwenyewe una wako huko nje, hutaki wa peke yako. Na tena nikakwambia ila yeye ana wivu sana, atakuchunga akikuchunguza. Unakumbuka jibu lako.” Kimya. “Ulinijibu kuwa, Utampiga chenga akiwa amesimama. Hatawahi kukukamata. Uongo?”

“Sasa waka…” “Wewe sema umenogewa na Kasa, unamtaka moja kwa moja. Umeshindwa, ndio unamtafuta mchawi. Lakini Kasa ni mfupa wa mbwa, wewe anti hutamuweza hata kama unajiona mtoto wa mjini. Maadamu umeshaanza kupokea pesa zake, tena mbaya zaidi kama ulikuwa ukimuomba, ndio umeharibu kabisa. Ashajua unamtumia kama watoto wake na watu wengine wote, ndio maana hakuthamini.”

“Mimi nimeishi naye yule, sijawahi muomba hata shilingi moja, lakini alikuwa akitoa kama amepagawa. Na nilikuwa naye yeye kama yeye kitu kilichokushinda wewe sababu ya haraka ya pesa, na nilikwambia, Kasa anaakili sana. Kuna ulipokosea kidogo tu, akakukamata na…” “Ameniambia anajua kama wewe ndio umeniunganishia kwake.” Kidogo Jelini akaogopa.

“Ila anasema alitaka kuniadhibu ila akaona anakupata wewe kupitia mimi, ndio maana ameniacha. Ananichunguza kupita kiasi na anahabari zangu za…” “Hayo yote nilikwambia anti. Nilikwambia, huwezi kumchenga Kasa. Ukajiita wewe mtoto wa mjini, hawezi kukukamata. Leo umekamatwa unakuja kunitapikia mwenzio, tena hapa hospitalini!?”

Mama Jema akawa anaingia. “Nisamehe anti langu! Nahisi…” “Hapana anti Raza. Umevuka mpaka na mimi maisha hayo mwenzio nilishayaacha zamani sana. Nilikukabidhi Kasa na nikafunga huo mlango japo Kasa ananitaka mpaka kesho. Yupo tayari kunioa kabisa. Na majuzi tu ameniambia yupo tayari hata kuzaa na mimi kama nataka, ilimradi tu turudiane. Lakini huko mimi nilishatoka. Nilichokuwa nikikitafuta nimekipata.”

“Nimelala hapa sababu ya kupambania penzi la huyu mwanaume wangu wa sasa. Anaweza asiwe kama Kasa, lakini anti, ananipenda na nipo peke yangu kwake. Sitaki chochote kitokee. Aliyetaka kutishia penzi letu nilipoona tu, nikaenda kumpiga marufuku, ndio nimeishia kutaka kuuwawa. Halafu wewe leo unakuja kunitapikia hapa mbele ya mama yake! Heshima yako na shukurani vipo wapi?”

“Ulikuwa ukihangaika na wanaume wanao kuhonga pesa za machungwa, nikakupa Kasa, japo hatuzungumzi juu yake, lakini naona mabadiliko yako. Sasahivi una pesa na vitega uchumi vyakueleweka, tena kwa ajili yangu. Kweli hiyo ndio shukurani yako kwangu?” “Unaninyanyasa Jelini?” “Hapana anti. Si mimi niliyekwambia sitaki hata kujua maendeleo yenu? Sitaki kujua kama alikukubali au la! Na nikakwambia hata kwa mashoga zako usinitaje kama mimi nimekuunganisha kwa Kasa. Amebadili maisha yako, na mimi najua yote uliyonayo sasahivi ni pesa ya Kasa. Bisha.” Kimya.

“Lakini ushawahi nisikia hata kuja kukuomba shilingi au kuja saluni kwako, kuomba nipewe huduma ya bure sababu nimekusaidia kufika hapo ulipo?” Kimya. “Sasa mimi mambo ya uswahili sitaki, na wewe unataka kunipora tonge mdomoni.”

“Sirudii anti yangu. Kwanza nakupangia bonge la kitchen party. Hapo ndio utaona shukurani zangu kwako.” “Sitaki. Na leo ndio uwe mwisho kunifuata. Unataka kunipokonya ndoa, mwenzio naipigania mpaka uhai wangu! Yaani hapa ninapozungumza, naomba beba kila ulichokuja nacho, mrudishie Kasa mwenyewe.” “Jelini anti langu!”

“Hakika kama huondoki navyo, mimi natoka sasahivi na hivi vitu, namrudishia maana kwa jinsi vilivyo najua yeye ndiye aliye nunua na kupanga hivi, wewe mbembaji tu. Bisha.” “Wala hutoki hapo kitandani. Maadamu yeye ndio amevileta, ataondoka navyo. Akikataa, basi mimi nita vibeba, nimrudishie Kasa mwenyewe na ndipo atanijua mimi ni nani.”  Mama Jema akapokea.

“Na nakuonya. Kaa mbali na Jelini. Siku nyingine ukitumwa kwake, mwambie yeyote aliyekutuma kuwa, mama yake Jelini hataki na mwanae. Lasivyo ni kunichokoza, na mimi sipendi uchokozi kwangu wala wanangu. Hapo utaniona mbaya. Wewe si umezaliwa hapa mjini, basi ukinianza, nitakutafutia kijiji chakuishi maana mjini utapaona pachungu. Haya, kusanya vitu vyako vyote, potea. Alipo Jelini, ona kituo cha polisi. Toka.”

Akakusanya vitu vyake yote kisha akamgeukia Jelini. “Najua nimekuudhi anti. Lakini naomba haya mambo yasiende mbali.” “Wewe ndiye uliyeyaleta ya mbali, karibu yangu, tena nikiwa mgonjwa! Umenikosea anti, wala huna mlango wa kurudia kwangu. Ulitaka kuniharibia kwangu wakati kwako nilikutengenezea tena bila hila! Leo unalia wivu wa kuja kugundua Kasa ananipenda mimi dhidi yako! Hakika ondoka, maana mchumba wangu atarudi muda si mrefu, na sitaki kumchanganya kwa mambo ya zamani ambayo sina hata mpango wa kurudia kuyaishi tena. Tafadhali ondoka tu.” “Unakaribia kuniudhi, na hutanipenda. Ondoka kama alivyokwambia Jelini.” Akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~

Jelini akaanza kulia kwa hofu. Mkwe ashasikia kila kitu. Na yeye hasira za kina Love zikamfanya akaongea mengi. Sasa hajui anamtizamaje mama mkwe. “Kwani imekuaje tena!?” Ikabidi amsimulie mama yake. “Nahisi ametumwa kwa kulazimishwa. Ndio ananimalizia mimi hasira zake.” “Sijui nitamfanyaje huyu baba! Kila nikimfikiria, simpatii jibu! Jana katokea, bila kutarajia.” Jelini akashituka sana.

“Kasa alikuja hapa?!” “Wala si hapa tu.” Ikabidi mama yake amsimulie kuanzia mwanzo mpaka mwisho. “Mungu wangu anisaidie jamani! Huyu Ezra atanichoka mama!” “Nisikilize Jelini, na uache kulia.” Mama mchungaji akamsogelea.

“Utaolewa na mwanaume anayekufahamu vizuri sana. Ezra si mkurupukaji, na si myumbaji. Ukilijua hilo, itakusaidia kutulia na kufanya naye maamuzi kama alivyokwambia asubuhi ya leo.” Mama mchungaji akaendelea.

“Wote hao ni maisha yako ya zamani, waliogoma kuondoka japo wewe umesonga mbele. Wala wasikutishe au kukuyumbisha. Wewe endelea mbele na maisha yako hizo ni kelele tu kutaka kukuweka njia panda. Ukiyumba tu, ujue utakosa kitu ulichokuwa ukikihitaji. Wewe tulia. Angalia ya sasa. Unaumwa. Unatakiwa upumzike, ndio jukumu lako la sasahivi. Kasa anafanya nini na kwa nani, hayakuhusu kwa sasa. Rudi kulala.” Akamtuliza mpaka akatulia.

“Sasa na wewe mbona hujatulia nyumbani, umerudi tena?” Mama mchungaji akamuuliza mama Jema. “Siwezi. Hapa siwezi kulala wala kufikiria, labda wamtoe hapa. Kwanza yeye huyu ni muoga kweli wa hospitalini. Kumuacha hapa najiona kama namtelekeza! Acha tu nikae naye. Wewe nenda.” “Mie hapa nimefika.” Wakabaki hapo wao wawili na mgonjwa.

Siku Ya Kufa Nyani, Miti Yote Huteleza.

Akiwa ameamka kwa kuchelewa sana siku ya kazi, na si kawaida yake, akawa akijiandaa kuelekea kazini. Msichana wa hapo kwao akamgongea. “Kuna watu wanakuulizia dada.” “Kina nani!?” “Hawajanitajia majina, ila wanaonekana wana haraka.” “Hivi wewe ni mara ngapi unafundishwa ukipokea wageni uulizie taarifa zao kamili ili unapomuita mtu ajue anakwenda kukutana na nani?” “Wamekataa hata kukaa dada! Wamesema wanaharaka, utoke.” Love akashangaa sana, ila akatoka kwani alishakuwa amevaa anakaribia kuondoka hapo.

“Love Simba?” Wakamuuliza kabla ya salamu. “Niwasaidie nini?” Love akauliza kwa kujiamini. “Twende.” “Hamuwezi kunibeba kama mzoga! Lazima mniambie mnakonipeleka na nyinyi ni kina nani.” Love akaweka mgomo wa kutoka hapo na hao waliomjia nyumbani, tena kwa wazazi!

~~~~~~~~~~~~~~~

Mipango Iliyojaa Chuki Na Usaliti Kwa Colins Inaendelea kwa kina na umakini wa namna yake.

Anapanga Kwa Makini, Ili Kuhakikisha Anamfikia Kila Aliyemuumiza Kwa Namna Moja Au Nyingine. Na Kila Atakayesimama Katikati Yake Na Amtakaye, Amekusudia Kummaliza Vibaya sana.

Anataka Kumfikia Love Na Kemi, Lakini Wazazi wake, yaani Kina Simba Na Chris Tayari Wapo Katikati Yao wakimkingia kifua.

Ni Nini Atafanya Akiwa Hana Tena Chakupoteza.

Mjumbe Raza & Kasa nao Je?

Mapenzi Na Pesa.

INAENDELEA.

 

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment