Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 10. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 10.

Akahisi kama hajaangalia vizuri. Ilionyesha eneo alipo ndipo na Kamila yupo. Akafunga kabisa ile laptop kisha akafungua tena. Akagundua kuwa yupo karibu naye. Yaani eneo hilohilo.

Kwa kupaniki, asifikirie kwamba pale ni eneo la hospitali, yeye akakurupuka akikimbilia chini ya hilo gorofa. Ile GPS haikutoa eneo kamili alipo. Ila tu kuonyesha yupo hapo.

Akatoka kwenye lift kwa haraka akiangaza macho kila mahali. “Uzuri wa Kamila si wa kujificha. Popote alipo anaonekana tu.” Akawaza Colins huku macho ameyatoa. Hata mpaka hapo bado hakuwa na wazo kwamba yupo eneo la hospitali. Akaanza kuzunguka mpaka akajikuta ametokea mapokezi. Alipoona wagonjwa pale ndipo akili ikamjia pengine amefika pale kwa kuwa ni mgonjwa. Wasiwasi ukazidi kumuingia.

Akamsogelea mmoja ya muhudumu na kumuomba ampishe kwenye kompyuta yake ili aangalie kama kuna mgonjwa mwenye jina hilo. Akavuta keyboad kwa haraka na kuandika jina la Kamila tu. Wakati mtandao unajaribu kutafuta kwenye kumbukumbu zote zilizoingizwa humo, kuona kama kuna jina la Kamila, mlinzi anayesimama pale mapokezi akarudi.

“Umemfanya nini?” “Nimempeleka getini, nimewaambia wale askari wamuitie polisi. Mwaka jana alifanya hivyohivyo! Alikuja hapa akidai mwanaume wake, kana kwamba hapa ni nyumba za kulala wageni! Akasumbua hapa kwa muda mrefu mpaka tukamfukuza. Sasa naona leo ameamkia hapahapa hata kabla hapaja pambazuka.” “Msichana mzuri, yupo kama amechanganyikiwa jamani! Hapo atakua aliiba bwana wa mtu, na wenyewe wakamkomoa kwa kumfanya chizi! Ndio wakomage kuiba mabwana za watu!” Colins akashituka sana.

“Yuko wapi?!” “Ni kichaa tu bosi wangu. Atakuja kurudi tu tena, utamuona. Tumemtoa sababu anasumbua wagonjwa.” Colins akatoka hapo kwa haraka kuwahi getini. Akakuta wakimsukumia nje na yeye amekazana anataka kuingia ndani. Amechoka usoni, hata nywele hazija chanwa.

“Subirini kwanza, msimsukume. Mwacheni kabisa.” Wale askari pale getini wakamuachia baada ya kumuona na kumsikia Colins. Alikuwa akilia sana mpaka sauti ilikuwa ikikaukia. “Tulia kabisa, uniambie unataka tukusaidie nini?” “Mimi nataka kujua walipomuhamishia Mike.” Akaanza akilia na sauti iliyokuwa ikikwaruza kwa kulia.

“Nimekuja naye hapa, jana tu! Nilimleta kwa dharula akiwa anaumwa tumbo. Ila nikawa nimesahau pesa nyumbani. Maana nilitoka naye nikikimbia. Nikamuaga yule muuguzi kuwa narudi nyumbani kuchukua pesa, maana matibabu mengine waliniambia yatahitajika kulipia ndio afanyiwe. Mike alianza kutapika damu. Mimi nikatoka kwa haraka. Kufika njiani tairi ikapata pacha. Mpaka kuja kufanikiwa kufika nyumbani, na kurudi hapa sikumkuta Mike pale nilipomuacha.” Akaendelea.

“Nimemuuliza yule nesi, mpenzi wangu yupo wapi, maana nilimuacha hapa muda mfupi uliopita, ananiambia yeye alikuwepo hapo usiku kuchwa, hamna mgonjwa mwenye jina hilo! Nikaendelea kumuhoji ndio akaniitia askari akitaka nitoke kule walipolazwa wagonjwa, eti napiga kelele, wakati mimi namuulizia mpenzi wangu!”

“Alikuwa akifanya fujo, bosi. Hapo anaongea taratibu. Alikuwa anapiga kelele kabisa, anasema hatoki mpaka atoke na mumewe sijui ni mwanaume gani! Wakati hata pale mapokezi wamemsaidia kuangalia, hamna mgonjwa mwenye jina hilo aliyepokelewa hapa muda aliosema yeye! Akaambiwa kiustarabu pengine amechanganya hospitali, atoke, hataki. Na yupo hapa tokea saa 10 asubuhi!” Colins akawa kama ameelewa ila akawa amemchanganya tena.

“Jina ni nani tena?” Akamuuliza kutaka uhakika. “Kamila.” Akamtajia akilia. “Tafadhali tulia na samahani kwa chochote ambacho umefanyiwa hapa, ambacho hujapenda. Samahani sana.” Kidogo akaanza kutulia. “Nashauri turudi ndani kwenye ofisi yangu, tuanze kumtafuta Mike. Si unakumbuka muda mliofika hapa?” “Ndiyo.” “Jina lake kamili na tarehe yake ya kuzaliwa vyote unakumbuka?” “Ni mpenzi wangu!” Akamjibu kama anayeuliza unaulizaje pingu polisi! Ila Colins akawa mstaarabu, akamchukulia taratibu. “Sawasawa. Tuongozane.” Wakampisha, Colins akaongoza njia, akifuata taratibu akilia.

“Hawaniamini! Wananiona nimechanganyikiwa.” “Pole sana.” Colins akaendelea kutembea akimfuata. Mpaka juu ofisini kwake. Akamkarimu maji lakini akakataa. “Siwezi kula nikiwa sijui Mike alipo! Nahisi kuna kitu hakipo sawa.” “Sasahivi, tutapata uhakika.” Akamjibu hivyo ila akijua kwa hakika Mike alishafariki muda mrefu sana.

Ila akaanza kuhisi pengine alifia pale kwenye hospitali yao. Akamuangalia pale alipokuwa amekaa. Amejawa wasiwasi kama ambaye kweli amepotelewa na mtu muda mfupi uliopita, anamsaka. Akafungua kompyuta ya hapo hospitalini. Akaanza kumuuliza taratibu.

“Unakumbuka kumuandikisha pale mapokezi muda uliokuja naye?” “Ndiyo! Wasinge mpokea wodini bila kupitia mapokezi.” “Ni kweli. Jina lake kamili na tarehe ya kuzaliwa?” Akawa akimuuliza macho kwenye kompyuta akiwa na uhakika kabisa na anachotafuta. Ila akataka kuelewa vizuri. Kwamba bado Kamila haamini kama Mike alifariki au imekuaje! Maana alikumbuka kwenye moja ya jumbe zake ni kama alitambua kutokuwepo kwake! Akaendelea kusaka.

“Ulipotoka kwenda kufuata walet au pochi nyumbani, unasema ulikuwa na usafiri. Ukaharibika njiani. Ulirudije tena hapa?” Akamuona ni kama anajaribu kufikiria. Kisha akakumbuka. “Ilikuwa ni tairi tu. Mike alinifundisha kubadili tairi ili isijetokea usiku naharibikiwa peke yangu njiani, nikakwama. Kwa hiyo najua kubadili tairi. Nilibadilisha kwa haraka nikaendelea na safari.” “Kwa hiyo ndilo lililokuleta au kukurudisha hapa sasahivi? Kwamba lipo hapo nje?” Akaendelea kumuhoji.

Hapo akamuona kama anajaribu kufikiria, kisha anashindwa. Akamwangalia na kurudisha macho kwenye kompyuta. Jina la Michael Zwambo likatokea hapo. Ni kweli alikufa kwenye hiyo hospitali. Kuangalia tarehe ni kama ya siku hiyo. Muda aliokufa ulikuwa saa 7:30 usiku wa siku yenye tarehe kama hiyo. Akajua hiyo ni anniversary yake, ndio imemtibua. Akamuhurumia na kumwangalia.

“Nahisi kama nachanganya!” “Kwa nini?” “Mmmh!” Ikawa kama hana tena uhakika. “Niambie tu unachofikiria.” Colins akamchukulia taratibu. “Sina uhakika sana. Maana ile gari niliyobadilisha tairi, ndiyo Luca alinipokonya jana!” Colins akakumbuka moja ya jumbe zake kwa Mike ni kuwa huyo Luca anayafanya maisha yake kuwa magumu. Ila hakujua ni nani na anahusikaje. Akataka kufahamu zaidi.

“Kwa nini Luca akupokonye?” Akamuona ametulia na kuinama. “Eti Kamila?” “Kulitokea kutoelewana, ndio akasema na gari anachukua. Ni mali inayotokana na kampuni, haikuwa ya Mike. Ndio nachanganyikiwa maana ndiyo hiyohiyo nilikuwa nayo usiku nilipomleta hapa Mike!” Akawa amekwama na sauti ikaisha kabisa.

Colins akaenda kumletea maji ya kunywa. Akamkabidhi mkononi bila ya safari hii kumuuliza. Akayanywa yote. Kisha akabaki kama ambaye amepoteza dira, na yeye Colins akawa amebakiwa na ukweli halisi juu ya Mike, lakini hajui kama amwambie au la! Akarudisha macho kwenye kompyuta ili asome chanzo cha kifo chake. Akaona ni kama madaktari walihisi alikuwa na sumu mwilini.z Lakini ndugu wa familia walipoambiwa mwili wake ufanyiwe vipimo zaidi ili kujua kilichomuua, ilionyesha ndugu walikataa, na kuondoka na mwili wa Mike. Kwahiyo haikujulikana chanzo cha kifo chake kwa hakika. Lakini Mike alikufa akiwa bado hajapokea matibabu yeyote.

Colins akaumia sana. Akamuangalia Kamila. Akakuta amelala na chupa ya maji mkononi. Akashangaa! Maana alilala hapohapo mbele ya meza yake! Kama aliyekuwa amechoka haswa. Ila akagundua ni tarehe tu ndio amechanganya ila alikuwa sahihi.

 “Itakuwa alipoondoka kufuata pesa, huku nyuma Mike alifariki dunia. Hakumkuta tena, ndio maana akili bado inamrudisha hapa!” Akawaza Colins akimtizama asijue anafanya nini na huyo Kamila hapo ofisini kwake.

Nini dawa ya mapenzi!

Gafla kitu kikapita kichwani na kumtia hofu. “Isijekuwa amepoteza fahamu mimi nadhania amelala!” Akapiga simu akitaka aitiwe muuguzi na afike hapo na vifaa vya kupimia pressure.

Baada ya muda mfupi akafika hapo. “Mguse taratibu, mwangalie mapigo ya moyo, oxygen mwilini na BP yake.” Akamgusa taratibu, akaamka. “Nataka kukupima. Nitakuvuta mkono.” Akakubali. Baada ya vipimo kidogo tu akaambiwa pressure ipo juu sana.

“Bora umemuwahi. Angeweza pata shindikizo la damu.” Akamwambia Colins akishangazwa na hiyo pressure ya Kamila. Wakaita mtu mwingine na kitanda cha wagonjwa, akatolewa hapo kwa haraka na kupelekwa wodini kuanza matibabu. “Tafadhali mnijulishe itakavyokwenda.” Colins akabaki ofisini hakutaka kufuata nyuma.

~~~~~~~~~~~~~~~

Kwenye mida ya saa 11 jioni ndio akapigiwa simu kuwa wameweza kushusha hiyo pressure, na wamempumzisha. Ndio akili ikatulia. Akasubiria mpaka wafanyakazi wote wa pale juu alipo waondoke, ndipo akaenda kwenye chumba alichoambiwa amelazwa.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akamkuta amelala kama mtoto. Na ni kama walimsafisha kidogo na tayari alishavalishwa mavazi ya wagonjwa. Colins akapotelea mawazoni akimtizama huku anawaza jinsi maisha yalivyo. Ni kama Kamila alikuwa na kila kitu maishani, gafla amebakiwa mpweke! Tena yeye si kwa kupenda kwake au kukosea kama yeye! Bali maisha yakamuweka kundi moja na yeye. Wapweke waliozungukwa na watu. Wakisaka kitu ambacho hakuna uwezekano wa kuja kupata tena katika ulimwengu huu. Mapenzi ya walio wahi kuwapenda. Jelini na Mike.

Akajikuta anaelewa pale anakopitia Kamila na kumuhurumia sana. Yeye mapenzi yalimfanya kichaa na mgonjwa. Na Kamila naye kila siku ya kumbukumbu ya kifo cha mpenzi wake, huharibika akili, akipoteza kumbukumbu pamoja na hiyo pressure. Akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha. “Mbona huku kupenda kunakuwa ni adhabu tena!” Akawaza Colins. “Nini dawa ya mapenzi!” Akaendelea kuwaza bila jibu asijue muda unazidi kwenda.

Kilichomshangaza, muda wote huo, hakuna hata mtu mmoja aliyemtafuta huyo Kamila japo simu yake ilikuwa hewani. Akaangalia muda. Ilishakuwa saa nne usiku. “Yaani mpaka muda huu hakuna mtu hata mmoja mwenye kutaka kujua alipo, tokea asubuhi alipofika hapa!?” Akashangazwa sana. Akajikuta ni kama amekwama pale mpaka nesi alipoingia pale. Akamtoa mawazoni.

“Bosi wangu bado upo?!” Akamrushia neno. “Natoka sasahivi. Nimepatwa na wasiwasi naye. Angeweza kunifia pale ofisini!” “Kila mtu anasema ni bora ulipomuwahi. Ila sasahivi anaonekana kuendelea vizuri. Usiwe na wasiwasi.” “Nawashukuru sana.” Ndio akawa kama amemfukuza kurudi nyumbani. Ila bado alijisikia anawajibika kubaki.

Mwana Kulitafuta!

Alirudi nyumbani akiwa na mawazo kibao. Wasiwasi juu ya Kamila na kukumbushwa mapenzi. Hapo ndipo akili yake ikagomea hapo. Usiku huo akazidi kujisikia mpweke na kushindwa kulala kwa haraka. Mawazo yakamrudisha kwa Love, ndipo akamkumbuka Chris.

Akaanza kazi ya kupekua simu ya Chris akimchunguza kama ana siri yeyote anayoweza itumia kumpunguza makali. Alikuwa kwenye kompyuta yake. Akaangalia huo mwezi. Akapita pote, hakuona cha siri sana. Akaendelea kusaka mpaka miezi 6 nyuma, ndipo akakutana na jumbe za mapenzi alizokuwa amefuta! Ila kwa utundu wake akapekenyua mpaka akapata na jumbe alizokuwa amefuta.

Akaanza kuzisoma na kugundua hazikuwa zikitoka kwa mkewe. Akaanza kumtafuta mtumaji. Alikuwa mwanafunzi wa shule ya sekondari Jangwani, lakini anaishi hosteli na wenzie maeneo ya Mwananyamala. Akaendelea kusoma.

Ikaonekana ni kama alimuacha huyo binti akiwa mgonjwa. Baadhi ya jumbe ni huyo binti alikuwa akimlalamikia kutomjali. Sasa moja iliyomfurahisha Colins ni ile aliyomwambia, anamuacha akiwa mgonjwa, wakati ni yeye mwenyewe ndiye aliyemlazimisha kutoa mimba! Tena kwa ahadi ya kuendeleza mapenzi yao baada ya hapo! Colins akajikuta akicheka peke yake mpaka kupiga makofi kabisa.

Katika hizo jumbe za mwisho, hakuonekana kumjibu huyo mrembo. Mwishoe akaona alimfungia simu zake. Alivyo shabiki, akahamia kwenye simu ya huyo mrembo alikuwa akiitwa Zulfa. Akaona alihangaika kumsaka Chris kwa jumbe na simu kwa muda wakutosha tu, mwishoe ni kama alikata tamaa, akaona jumbe zimekoma.

Kwa hiyo furaha tu, Colins akapatwa usingizi mzito na mzuri akijiambia, “Nimekukamata Chris. Na huu ni mwanzo tu. Utajuta kuingilia mambo yangu.” Usiku huo akawa la Chris ameshalipatia ufumbuzi, akalala.

~~~~~~~~~~~~~~~

INAENDELEA.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment